1

1 Lifuatalo ni simulizi la Nehemia, mwana wa Hakalia. Ikawa, nilipokuwa katika mji mkuu wa Susa, katika mwezi wa Kislevu wa mwaka wa ishirini,

2 Hanani, mmoja wa ndugu zangu, akaja pamoja na baadhi ya watu toka nchini Yuda. Nikawauliza kuhusu Wayahudi wenzetu waliosalimika, yaani ambao hawakuhamishiwa Babuloni na kuhusu mji wa Yerusalemu.

3 Wao wakaniambia, “Wayahudi waliosalimika na kubaki katika mkoa ule, wako katika taabu na aibu. Ukuta wa mji wa Yerusalemu umebomolewa na malango yake yameteketea.”

4 Niliposikia hayo nilikaa chini na kulia, nikaomboleza kwa siku kadhaa. Nikafunga na kumwomba Mungu wa mbinguni,

5 nikisema, “Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wa mbinguni, wewe u Mungu aliye mkuu na wa kutisha, unalishika agano lako na unawafadhili wale wakupendao na kuzishika amri zako.

6 Yasikilize kwa makini maombi yangu, na uniangalie mimi mtumishi wako, ninapokuomba kwa ajili ya watumishi wako, watu wa Israeli, usiku na mchana. Ninaungama dhambi za watu wa Israeli, tulizofanya mbele yako. Mimi pamoja na watu wa jamaa yangu tumefanya dhambi.

7 Tumetenda mabaya mbele yako, hatujazishika amri zako, kanuni na maagizo yako uliyomwagiza mtumishi wako Mose.

8 Kumbuka sasa lile ulilomwambia mtumishi wako Mose, uliposema, ‘Kama hamtakuwa waaminifu, nitawatawanya miongoni mwa mataifa.

9 Lakini mkinirudia, mkazishika amri zangu na kuzifuata hata ingawa nitakuwa nimewatawanya mbali kabisa, nitawarudisha mahali nilipochagua kuwa mahali pangu pa kuabudiwa.’

10 Watu wa Israeli ni watumishi wako na watu wako uliwakomboa kwa uwezo wako na mkono wako wenye nguvu.

11 Ee Bwana, yasikie maombi yangu mimi mtumishi wako na ya watumishi wako wanaofurahia kukutii wewe. Nakuomba unifanikishe leo, mimi mtumishi wako, na kunijalia kuhurumiwa na mfalme.” Basi, mimi nilikuwa na jukumu la kumpa mfalme kinywaji.

2

1 Katika mwezi wa Nisani, katika mwaka wa ishirini wa utawala wa mfalme Artashasta, wakati divai ilipokuwa mbele yake, nilichukua divai na kumpelekea mkononi mwake. Kamwe sikuwahi kuwa mwenye huzuni mbele yake.

2 Mfalme Artashasta akaniuliza, “Je, mbona unaonekana kuwa mwenye huzuni, ingawa huonekani kuwa mgonjwa? Naona una huzuni sana moyoni mwako!” Ndipo nilipoogopa sana.

3 Nikamjibu, “Ee mfalme, udumu milele! Kwa nini nisiwe mwenye huzuni wakati mji wa Yerusalemu yalimo makaburi ya babu zangu uko tupu na malango yake yameteketezwa kwa moto?”

4 Ndipo mfalme Artashasta akanijibu, “Sasa unaomba nini?” Nikamwomba Mungu wa mbinguni.

5 Halafu nikamwambia mfalme, “Ee mfalme, ikiwa unapendezwa nami na ikiwa nimepata upendeleo mbele yako, nakuomba unitume Yuda ili niende kuujenga upya mji ambamo yamo makaburi ya babu zangu.”

6 Mfalme akaniuliza (malkia akiwa karibu naye), “Utakuwa huko kwa muda gani na utarudi lini hapa?” Ombi langu akalikubali nami nikamjulisha wakati nitakaporudi.

7 Nikamjibu, “Ee mfalme ikiwa unapendezwa nami, naomba nipewe barua ili nizipeleke kwa watawala wa mkoa wa magharibi ya mto Eufrate ili waniruhusu nipite hadi nchini Yuda.

8 Pia nakuomba barua iandikwe kwa Asafu mtunzaji wa msitu wa kifalme ili anipatie mbao za kutengenezea miimo ya malango ya ngome ya hekalu, ukuta wa mji na nyumba yangu nitakamokaa.” Mfalme akakubali ombi langu kwa kuwa Mungu, kwa wema wake, alikuwa pamoja nami.

9 Nilipowafikia wakuu wa mkoa wa magharibi ya mto Eufrate, niliwapa barua za mfalme. Mfalme alikuwa amenituma pamoja na maofisa wa jeshi na wapandafarasi.

10 Lakini Sanbalati, Mhoroni, na Tobia, Mwamoni, mtumishi wake, waliposikia kuwa nimekuja ili kushughulikia hali njema ya watu wa Israeli, hawakufurahia kabisa jambo hilo.

11 Hivyo nikafika Yerusalemu, nikakaa huko kwa siku tatu.

12 Kisha niliondoka usiku, mimi pamoja na watu wachache; sikumwambia mtu yeyote yale ambayo Mungu alikuwa ameyaweka moyoni mwangu kwa ajili ya mji wa Yerusalemu. Lakini siku moja usiku, niliondoka na kuwachukua watu wachache tu. Sikuchukua mnyama yeyote isipokuwa punda niliyempanda mimi mwenyewe.

13 Nikatoka nikipitia Lango la Bondeni katika njia ielekeayo kwenye Kisima cha Joka na Lango la Mavi; nikazikagua kuta za mji wa Yerusalemu ambazo zilikuwa zimebomolewa pamoja na malango yake ambayo yalikuwa yameteketezwa kwa moto.

14 Halafu, nikaenda kwenye Lango la Chemchemi na kwenye Bwawa la Mfalme. Lakini yule punda niliyempanda hakuweza kupita.

15 Wakati huo wa usiku, nikapitia bondeni na kukagua ukuta wa mji. Nilirudi nikapitia Lango la Bondeni.

16 Maofisa hawakujua mahali nilipokuwa nimekwenda wala nimefanya nini. Tena nilikuwa sijawaambia Wayahudi, makuhani, viongozi, wakuu wala wale watu ambao wangeifanya kazi ya kuujenga upya mji.

17 Kisha nikawaambia, “Bila shaka mnaliona tatizo letu kuwa mji wa Yerusalemu ni magofu na malango yake yameteketezwa kwa moto. Basi, na tuujenge tena ukuta wa Yerusalemu ili tusiaibishwe zaidi.”

18 Nikawaeleza jinsi Mungu alivyokuwa pamoja nami akinitendea kwa wema wake. Nikawaeleza pia maneno ambayo mfalme alikuwa ameniambia. Wao walipoyasikia hayo, wakasema, “Haya, na tuanze kazi ya ujenzi.” Hivyo wakajiandaa kwa kazi hiyo njema.

19 Lakini Sanbalati, Mhoroni, Tobia, Mwamoni mtumishi wake, na Geshemu, Mwarabu, waliposikia, wakatucheka na kutuzomea wakisema, “Ni kitu gani hiki mnachotenda? Je, mnataka kumwasi mfalme?”

20 Nikawajibu, “Mungu wa mbinguni atatufanikisha katika kazi hii, nasi tulio watumishi wake tutaanza ujenzi. Lakini nyinyi hamna fungu wala haki wala kumbukumbu katika mji wa Yerusalemu.”

3

1 Basi Lango la Kondoo lilijengwa upya na Eliashibu, kuhani mkuu, pamoja na ndugu zake waliokuwa makuhani. Waliliweka wakfu na kutia milango yake; wakaliweka wakfu tangu Mnara wa Mia Moja hadi Mnara wa Hananeli.

2 Sehemu iliyofuata ilijengwa upya na watu wa mji wa Yeriko. Baada ya hayo akafuata Zakuri mwana wa Imri kujenga ukuta.

3 Lango la Samaki lilijengwa upya na ukoo wa Hasena, wakatia miimo yake, milango, bawaba na makomeo yake.

4 Sehemu inayofuata ilijengwa upya na Meremothi, mwana wa Uria, mwana wa Hakosi. Sehemu inayofuata ilijengwa upya na Meshulamu, mwana wa Berekia, mwana wa Meshezabeli. Sehemu inayofuata ilijengwa upya na Sadoki, mwana wa Baana.

5 Sehemu inayofuata ilijengwa na watu kutoka mji wa Tekoa. Lakini viongozi wa mji wakakataa kufanya kazi ya mikono waliyoagizwa kufanya na wasimamizi.

6 Lango la Zamani lilijengwa upya na Yoyada, mwana wa Pasea, pamoja na Meshulamu, mwana wa Besodeya, wakatia miimo yake, milango, bawaba na makomeo yake.

7 Waliowafuata hao katika kazi hiyo ya kujenga upya walikuwa Melatia, Mgibeoni; Yadoni, Mmeronothi pamoja na watu wa mji wa Gibeoni na Mizpa waliokuwa chini ya uongozi wa mtawala wa mkoa wa magharibi ya mto Eufrate.

8 Sehemu inayofuata, ilijengwa upya na Uzieli, mwana wa Harkaya, mfua dhahabu. Sehemu inayofuata hadi Ukuta Mpana ilijengwa upya na Hanania, mtengenezaji wa marashi.

9 Sehemu inayofuata ilijengwa upya na Refaya, mwana wa Huri, mkuu wa nusu ya wilaya ya Yerusalemu.

10 Sehemu inayofuata, inayokabiliana na nyumba yake ilijengwa upya na Yedaya, mwana wa Harumafu. Sehemu inayofuata ilijengwa upya na Hatushi, mwana wa Hashabneya.

11 Sehemu inayofuata pamoja na Mnara wa Tanuri vilijengwa upya na Malkiya, mwana wa Harimu akishirikiana na Hashubu, mwana wa Pahath-moabu.

12 Sehemu inayofuata ilijengwa upya na Shalumu, mwana wa Haloheshi, mtawala wa nusu nyingine ya wilaya ya Yerusalemu. Alisaidiana na binti zake katika ujenzi huo.

13 Lango la Bondeni lilijengwa upya na Hanuni pamoja na wakazi wa mji wa Zanoa. Wakayaweka malango mahali pake, wakatia bawaba na makomeo yake. Waliujenga upya ukuta ukiwa na urefu wa mita 400 hivi hadi Lango la Samadi.

14 Lango la Samadi lilijengwa upya na Malkiya, mwana wa Rekabu, mkuu wa wilaya ya Beth-hakeremu. Akaliweka lango mahali pake, akatia bawaba na makomeo yake.

15 Lango la Chemchemi lilijengwa upya na Shalumu, mwana wa Kolhoze, mkuu wa wilaya ya Mizpa. Akalifunika, akaliweka lango mahali pake, akatia bawabu na makomeo yake. Kwenye Bwawa la Shela akajenga ukuta ulio karibu na bustani ya kifalme hadi ngazi zinazoshuka toka mji wa mfalme Daudi.

16 Sehemu inayofuata hadi kwenye makaburi ya Daudi, bwawa na majengo ya jeshi ilijengwa upya na Nehemia, mwana wa Azbuki, mkuu wa nusu ya wilaya ya Beth-suri.

17 Baada ya hao, Walawi waliendeleza ujenzi mpya wa ukuta. Sehemu inayofuata ilijengwa upya na Rehumu, mwana wa Bani, na Hashabia, mkuu wa nusu ya wilaya ya Keila, alijenga upya sehemu inayohusu wilaya yake.

18 Baada ya huyo, sehemu zinazofuata zilijengwa upya na ndugu zao. Sehemu inayofuata ilijengwa upya na Bavai, mwana wa Henadadi, mkuu wa nusu ya wilaya ya Keila.

19 Sehemu inayofuata inayoelekeana na ghala ya silaha kwenye pembe ya ukuta ilijengwa upya na Ezeri, mwana wa Yeshua, mkuu wa Mizpa.

20 Sehemu inayofuata tangu pembeni hadi kwenye mlango wa Eliashibu, kuhani mkuu, ilijengwa upya na Baruku, mwana wa Zabai.

21 Sehemu inayofuata tangu mlangoni mwa nyumba ya Eliashibu, kuhani mkuu, hadi mwisho wa nyumba hiyo, ilijengwa upya na Meremothi, mwana wa Uria, mwana wa Hakosi.

22 Sehemu inayofuata ilijengwa upya na makuhani waliokaa katika sehemu tambarare.

23 Benyamini na Hashubu walijenga upya sehemu inayokabiliana na nyumba yake. Azaria, mwana wa Maaseya, mwana wa Anania, alijenga upya sehemu inayokabiliana na nyumba yao.

24 Kuanzia kwenye nyumba ya Azaria hadi pembeni mwa ukuta ilijengwa upya na Binui, mwana wa Henadadi.

25 Sehemu inayofuata, tokea pembeni mwa ukuta na mnara wa ikulu ya juu karibu na uwanda wa ulinzi ilijengwa upya na Palali, mwana wa Uzai. Pedaia, mwana wa Paroshi,

26 akishirikiana na watumishi wa hekalu waliokaa Ofeli, walijenga upya sehemu inayokabiliana na Lango la Maji, upande wa mashariki na mnara mrefu.

27 Sehemu nyingine inayofuata, ikitokea kwenye mnara mrefu hadi ukuta wa Ofeli ilijengwa upya na wakazi wa mji wa Tekoa.

28 Juu ya Lango la Farasi palijawa na makuhani, kila mmoja alijenga sehemu inayokabiliana na nyumba yake.

29 Sadoki, mwana wa Imeri alijenga upya sehemu inayokabiliana na nyumba yake. Sehemu inayofuata, ilijengwa upya na Shemaya, mwana wa Shekania, mlinzi wa Lango la Mashariki.

30 Sehemu inayofuata ikiwa ni sehemu yao ya pili ilijengwa upya na Hanania mwana wa Shelemia, akishirikiana na Hanuni, mwana wa sita wa Zalafu. Meshulamu, mwana wa Berekia, alijenga upya sehemu inayokabiliana na chumba chake.

31 Sehemu inayofuata, toka nyumba waliyoitumia wafanyakazi wa hekalu na wafanyabiashara iliyokuwa inaelekeana na Lango la Gereza, karibu na chumba cha juu kwenye pembe upande wa kaskazini-mashariki ilijengwa upya na Malkiya, mfua dhahabu.

32 Sehemu ya mwisho kutoka chumba kwenye pembe hadi Lango la Kondoo ilijengwa upya na wafua dhahabu na wafanyabiashara.

4

1 Sanbalati aliposikia kuwa tumeanza kazi ya kuujenga upya ukuta, alikasirika sana, akaanza kutukebehi,

2 mbele ya rafiki zake na majeshi ya Wasamaria, akisema, “Hawa Wayahudi wanyonge wanafanya nini? Je, kusudi lao ni kuujenga upya mji? Je, watatoa tambiko? Wanaweza kumaliza kazi kwa siku moja tu? Je, wataweza kufanya mawe yaliyorundikana kwenye takataka na kuteketea, yafae kujengea?”

3 Tobia, Mwamoni, aliyekuwa akisimama karibu naye, alitilia mkazo akisema, “Wanajenga nini? Mbweha akipanda juu yake, atabomoa huo ukuta wao wa mawe!”

4 Ndipo nikamwomba Mungu nikisema, “Ee Mungu wetu, sikia wanavyotukebehi; urudishe dharau yao juu yao wenyewe na uwaache watekwe na kuchukuliwa mateka katika nchi ya kigeni.

5 Kamwe usiwasamehe hatia yao, wala dhambi yao kamwe usiisamehe; kwani wamekukasirisha mbele ya wajenzi.”

6 Lakini tuliendelea na ujenzi wa ukuta mpaka ukafikia nusu yake kwa sababu watu walikuwa wamedhamiria kwa dhati.

7 Lakini Sanbalati, Tobia, Waarabu, Waamoni na Waashdodi waliposikia kuwa ujenzi mpya wa ukuta wa Yerusalemu ulikuwa unasonga mbele na kwamba mapengo katika ukuta yanazibwa barabara, wao walizidi kukasirika.

8 Wakala njama kwa pamoja kuja Yerusalemu kutushambulia na hivyo kuleta mvurugano katika mji huo.

9 Ndipo tulipomwomba Mungu wetu na kuweka ulinzi dhidi yao, mchana na usiku.

10 Watu wa Yuda wakawa wakilalamika wakisema, “Nguvu za vibarua zinapungua na bado kuna takataka nyingi za kubeba. Hatuwezi kuendelea kujenga ukuta.”

11 Nao adui zetu wakawa wanasema, “Hawataweza kujua wala kuona, hadi tutakapofika kwao na kuwaua na kusimamisha kazi.”

12 Wayahudi waliokaa miongoni mwa adui zetu waliposikia maneno yao, walitujia mara kumi wakisema, “Watakuja toka kila mahali wanapokaa na kutushambulia.”

13 Hivyo, kwenye sehemu za chini za ukuta ambazo zilikuwa bado kumalizika, nyuma ya ukuta, katika mahali pa wazi, niliwapanga watu kulingana na jamaa zao wakiwa na mapanga, mikuki na pinde.

14 Nilipoona kuwa watu walikuwa na hofu nikawaambia wakuu, maofisa na watu wote kwa ujumla, “Msiwaogope hata kidogo. Mkumbukeni Bwana aliye Mkuu na wa kutisha, basi piganeni kwa ajili ya ndugu zenu, wana wenu, binti zenu, wake zenu na nyumba zenu.”

15 Maadui waliposikia kwamba njama zao tumezigundua na kuwa Mungu amevuruga njama hizo, ndipo sisi sote tulipourudia ukuta, kila mmoja akaendelea na kazi yake.

16 Tokea siku hiyo na kuendelea, nusu ya watumishi wangu wakawa wanaendelea na ujenzi ambapo nusu nyingine ikawa inashika ulinzi wakiwa na mikuki, ngao, pinde na mavazi ya kukinga kifua. Viongozi wetu wakawa upande wa watu wa Yuda

17 waliokuwa wanaujenga ukuta. Hata wale waliokuwa wanabeba vifaa vya ujenzi waliendelea na kazi huku mkono mmoja ukiwa na vifaa vya ujenzi na mkono mwingine silaha yake.

18 Kila mwashi alikuwa na panga lake limefungwa kiunoni mwake na huku anaendelea kujenga. Na mtu wa kupiga tarumbeta alikuwa karibu nami.

19 Nikawaambia wakuu, maofisa na watu wote kwa ujumla “Kazi ni kubwa, nayo imeenea sehemu kubwa hivi ya kwamba tumetawanyika mno juu ya ukuta kila mmoja yuko mbali na mwenzake.

20 Ukiwa mahali popote unapofanya kazi, mara utakaposikia tarumbeta, kimbilia kwetu. Mungu wetu atatupigania.”

21 Hivyo, tukaendelea kufanya kazi yetu na nusu ya watu wakishika silaha tangu mapambazuko hadi nyota zinapoonekana mbinguni.

22 Wakati huo nikawaambia watu, “Kila mwanamume na mtumishi wake atakaa mjini Yerusalemu usiku, ili tuwe na ulinzi usiku, na wakati wa mchana wataendelea na kazi.”

23 Hivyo ikawa mimi, ndugu zangu, watumishi wangu hata na walinzi waliofuatana nami, hatukuvua mavazi yetu; kila mmoja wetu akawa daima na silaha yake mkononi.

5

1 Baada ya muda kulitokea malalamiko miongoni mwa watu, wanaume kwa wanawake, wakiwalalamikia ndugu zao Wayahudi.

2 Kulitokea waliosema, “Tafadhali tupatie nafaka tule ili tuweze kuishi kwa kuwa sisi, wana wetu na binti zetu tu wengi.”

3 Na wengine wakalalamika, “Tumeweka rehani mashamba yetu, mizabibu yetu hata na nyumba zetu ili kupata nafaka kwa sababu ya njaa.”

4 Tena kukawa na hata wale, waliolalamika, wakisema, “Ili kulipa kodi ya mfalme juu ya mashamba na mizabibu yetu, ilitubidi tukope fedha.

5 Lakini sisi ni sawa na Wayahudi wengine; watoto wetu ni sawa na watoto wao. Hata hivyo, tunawalazimisha watoto wetu kuwa watumwa. Baadhi ya binti zetu tayari ni watumwa. Hatuna uwezo wa kuzuia jambo hili kwani mashamba yetu na mizabibu yetu yameporwa na watu wengine.”

6 Niliposikia malalamiko yao, nilikasirika sana.

7 Nikaamua kuchukua hatua. Nikawashutumu wakuu na maofisa, nikawaambia, “Mnawatoza riba ndugu zenu.”

8 Nikasema, “Kulingana na uwezo tulio nao, tumekuwa tukiwanunua tena ndugu zetu Wayahudi waliokuwa wameuzwa kwa watu wa mataifa mengine. Lakini sasa hata mnawauza ndugu zenu, nasi tunalazimika kuwanunua!” Basi walinyamaza kimya, bila kuwa na la kujibu.

9 Kisha nikawaambia, “Mnalolifanya ni baya. Je, haiwapasi kumcha Mungu wetu ili kuzuia mataifa mengine yaliyo adui zetu yasitusute?

10 Zaidi ya hayo, mimi mwenyewe, ndugu zangu na watumishi wangu tumewaazima ndugu zetu fedha na nafaka. Na hatutadai riba yoyote.

11 Leo hii na muwarudishie mashamba yao, mashamba ya mizabibu, mashamba ya mizeituni na nyumba zao, hata na riba ya fedha, nafaka, divai, na mafuta ambayo nilikuwa ninawatoza.”

12 Wao wakaitikia na kusema, “Tutawarudishia na hatutawadai chochote. Tutafanya kama ulivyosema.” Nikawaita makuhani mbele, na viongozi wote wakaapa mbele ya makuhani kufanya kama walivyoahidi.

13 Nilikunguta kibindo changu na kusema, “Kila mmoja asiyetimiza ahadi hii Mungu na amkungute, amtoe katika nyumba yake na katika kazi yake. Basi, akungutike na kubaki mikono mitupu.” Mkutano mzima ukaitikia, na kusema, “Amina” wakamsifu Mwenyezi-Mungu. Watu wakafanya kama walivyokuwa wameahidi.

14 Tangu wakati nilipoteuliwa kuwa mtawala wa nchi ya Yuda kwa miaka kumi na miwili yaani tangu mwaka wa ishirini mpaka mwaka wa thelathini na mbili wa kutawala kwa mfalme Artashasta, sikula chakula kinachostahili kuliwa na mtawala, wala ndugu zangu hawakufanya hivyo.

15 Watawala walionitangulia walikuwa mzigo mzito kwa watu wakiwadai chakula na divai, mbali na kuwadai kuwalipa sarafu za uzito wa shekeli arubaini za fedha. Hata watumishi wao waliwadhulumu watu. Bali, mimi sikufanya hivyo, kwani nilimcha Mungu.

16 Nilikuwa na juhudi nyingi katika ujenzi mpya wa ukuta huu na kamwe sikujipatia hata shamba. Hata watumishi wangu wote walifanya kazi hii kwa bidii.

17 Zaidi ya hayo, kila siku niliwalisha watu 150, wakiwamo Wayahudi na maofisa, mbali na wale watu waliotujia toka mataifa jirani.

18 Kila siku, ili kuwalisha watu hao, nilichinjiwa dume mmoja na kondoo safi sita na kuku. Kila baada ya siku kumi nilitoa kwa wingi viriba vya divai. Lakini licha ya haya yote, kwa kuwa watu walikuwa na mzigo mzito wa kubeba kila siku, sikutaka posho ya ziada.

19 Sasa, ee Mungu wangu, kumbuka wema wangu wote niliowatendea watu hawa.

6

1 Kisha Sanbalati, Tobia, Geshemu, Mwarabu na adui zetu wengine, waliposikia kuwa tumemaliza ujenzi wa ukuta na kwamba hakuna mapengo yoyote (ingawa tulikuwa bado hatujaweka milango ya malango),

2 Sanbalati na Geshemu walituma ujumbe kwangu wakisema, “Na tukutane kwenye kijiji kimojawapo cha tambarare ya Ono.” Lakini walikusudia kunidhuru.

3 Basi, nikawapelekea wajumbe, nikisema, “Kazi ninayoifanya ni muhimu sana. Hivyo siwezi kuja kwenu ili kazi isije ikasimama.”

4 Waliendelea kunitaka niende kwao mara nne, lakini nikawapa jibu lilelile.

5 Mara ya tano, Sanbalati akanitumia barua ya hadhara kwa njia ya mjumbe wake.

6 Na barua yenyewe iliandikwa ifuatavyo: “Kuna habari zilizoenezwa miongoni mwa mataifa jirani, na Geshemu anathibitisha habari hizi, kuwa wewe pamoja na Wayahudi wenzako mnakusudia kuasi. Hii ndiyo sababu mnaujenga upya ukuta. Kulingana na habari hizo, wewe unakusudia kuwa mfalme wao.

7 Ili kuthibitisha wazo lako, umejiwekea manabii mjini Yerusalemu ili watangaze kuwa ‘Kuna mfalme katika nchi ya Yuda’. Taarifa hii ataarifiwa mfalme Artashasta. Hivyo nashauri wewe na mimi tukutane na kuzungumzia jambo hili.”

8 Nami nikampelekea ujumbe: “Hakuna jambo kama hilo. Habari hizo umezibuni wewe mwenyewe.”

9 Walifanya hivyo ili kututisha wakifikiri: “Hawataendelea na kazi, kwa hiyo, hakuna litakalotendeka.” Nikamwomba Mungu wangu nikisema, “Lakini sasa, ee Mungu, nakuomba unipe nguvu.”

10 Nilipokwenda nyumbani kwa Shemaya, mwana wa Delaya mwana wa Mehetabeli, ambaye hakuruhusiwa kutoka nyumbani, aliniambia, “Twende tukutane katika nyumba ya Mungu na milango yake tuifunge kwa sababu leo usiku wanakuja kukuua.”

11 Lakini mimi nikajiuliza moyoni, “Je, mtu kama mimi, ana haja ya kukimbia? Mtu kama mimi anahitaji kuingia hekaluni kusudi apate kuishi? Kamwe sitaingia hekaluni.”

12 Kwa bahati nzuri, nilingamua kuwa alikuwa hajatumwa na Mungu, bali alikuwa amekodishwa na Tobia na Sanbalati atangaze mabaya dhidi yangu.

13 Alikuwa amekodishwa kunitishia nami nifanye dhambi. Na kwa njia hii wangepata mwanya wa kuniharibia jina langu ili kushusha hadhi yangu.

14 Nikamwomba Mungu nikisema, “Ee Mungu, kumbuka yote waliyotenda Tobia na Sanbalati, hata yule Noadia, nabii mwanamke, na manabii wengine waliotaka kunifanya niogope.”

15 Basi, ukuta ulikamilika siku ya ishirini na tano ya mwezi wa Eluli; nayo ilichukua muda wa siku hamsini na mbili.

16 Maadui zetu katika mataifa jirani, waliposikia kuwa kazi tumeimaliza, waliogopa na kuona aibu sana; kwani walijua hakika kuwa kazi hii ilikamilika kwa msaada wa Mungu wetu.

17 Wakati huu wote, viongozi wa Wayahudi walikuwa wakiandikiana na Tobia.

18 Wengi miongoni mwa Wayahudi walishirikiana naye kutokana na kiapo chao kwani alikuwa mkwe wa Shekania, mwana wa Ara. Zaidi ya yote, Yehohanani, mwanawe, alikuwa amemwoa binti Meshulamu, mwana wa Berekia.

19 Pia wakanisimulia matendo mema ya Tobia, na habari zangu wakawa wanampelekea. Naye akawa ananiandikia barua ili kunitisha.

7

1 Baada ya ukuta kukamilika, malango yote kuwa tayari, na kuteuliwa kwa walinzi, waimbaji na Walawi,

2 nilimteua ndugu yangu Hanani kuwa mwangalizi wa Yerusalemu akishirikiana na Hanania aliyekuwa mkuu wa ngome katika Yerusalemu; kwa sababu alikuwa mtu wa kutegemewa na anayemcha sana Mungu, hapakuwapo mwingine aliyelingana naye,

3 nikawaagiza, “Malango yasifunguliwe usiku kucha hadi jua linapokuwa limepanda. Kabla hawajaondoka walinzi ni lazima kufunga milango yote kwa makomeo yake. Teueni walinzi miongoni mwa wakazi wa mji wa Yerusalemu, kila mmoja awe mahali pake kukabiliana na nyumba yake.”

4 Mji wa Yerusalemu ulikuwa mpana na mkubwa, lakini wakazi wake walikuwa wachache na nyumba zilikuwa hazijajengwa.

5 Mungu akanipa moyo kuwakusanya viongozi na watu ili kujua koo zao. Nikapata kitabu cha koo za watu waliorudi toka uhamishoni mara ya kwanza, na hawa wafuatao ndio waliokuwa wameorodheshwa ndani yake.

6 Wale waliokuwa uhamishoni kule Babuloni, walirudi mjini Yerusalemu na nchini Yuda, kila mmoja akarudi mjini kwake. Jamaa zao walikuwa wamekaa Babuloni tangu mfalme Nebukadneza alipowahamishia huko wakiwa mateka.

7 Waliporudi waliongozwa na Zerubabeli, Yeshua, Nehemia, Azaria, Raamia, Nahamani, Mordekai, Bilshani, Misperethi, Bigwai, Nehumu na Baana. Ifuatayo ni idadi ya watu wa koo za Israeli waliorudi toka uhamishoni:

8 Watu wa ukoo wa Paroshi: 2,172;

9 wa ukoo wa Shefatia: 372;

10 wa ukoo wa Ara: 652;

11 wa ukoo wa Pahath-moabu, yaani wazawa wa Yeshua na Yoabu: 2,818;

12 wa ukoo wa Elamu: 1,254;

13 wa ukoo wa Zatu: 845;

14 wa ukoo wa Zakai: 760;

15 wa ukoo wa Binui: 648;

16 wa ukoo wa Bebai: 624;

17 wa ukoo wa Azgadi: 2,322;

18 wa ukoo wa Adonikamu: 667;

19 wa ukoo wa Bigwai: 2,067;

20 wa ukoo wa Adini: 655;

21 wa ukoo wa Ateri (ambao pia unaitwa Hezekia): 98;

22 wa ukoo wa Hashumu: 328;

23 wa ukoo wa Bezai: 324;

24 wa ukoo wa Harifu: 112;

25 wa ukoo wa Gibeoni: 95;

26 Watu wa miji ifuatayo pia walirudi: Wa mji wa Bethlehemu na Netofa: 188;

27 wa mji wa Anathothi: 128;

28 wa mji wa Beth-azmawethi: 42;

29 wa miji ya Kiriath-yearimu, Kefira na Beerothi: 743;

30 wa miji ya Rama na Geba: 621;

31 wa mji wa Mikmashi: 122;

32 wa miji ya Betheli na Ai: 123;

33 wa mji mwingine wa Nebo: 52;

34 wa mji mwingine wa Elamu: 1,254;

35 wa mji wa Harimu: 320;

36 wa mji wa Yeriko: 345;

37 wa miji ya Lodi, Hadidi na Ono: 721;

38 wa mji wa Senaa: 3,930.

39 Ifuatayo ni idadi ya makuhani waliorudi kutoka uhamishoni: Makuhani wa ukoo wa Yedaya, waliokuwa wazawa wa Yeshua: 973;

40 wa ukoo wa Imeri: 1,052;

41 wa ukoo wa Pashuri: 1247;

42 wa ukoo wa Harimu: 1017.

43 Walawi wa ukoo wa Yeshua, yaani Kadmieli, wazawa wa Hodavia waliorudi kutoka uhamishoni walikuwa 74.

44 Waimbaji: Wazawa wa Asafu walikuwa 148.

45 Walinzi: Wazawa wa Shalumu, wa Ateri, wa Talmoni, wa Akubu, wa Hatita na wa Shobai, walikuwa 138.

46 Koo za wahudumu hekaluni waliorudi kutoka uhamishoni zilikuwa: Ukoo wa Ziha, wa Hasufa, wa Tabaothi;

47 wa Kerosi, wa Siaha, wa Padoni;

48 wa Lebana, wa Hagaba, wa Shalmai;

49 wa Hanani, wa Gideli, wa Gahari;

50 wa Reaya, wa Resini, wa Nekoda;

51 wa Gazamu, wa Uza, wa Pasea;

52 wa Besai, wa Meunimu, wa Nefushesimu;

53 wa Bakbuki, wa Hakufa, wa Harhuri;

54 wa Baslithi, wa Mehida, wa Harsha;

55 wa Barkosi, wa Sisera, wa Tema;

56 wa Nezia na ukoo wa Hatifa.

57 Koo za wazawa wa watumishi wa mfalme Solomoni waliorudi kutoka uhamishoni zilikuwa: Ukoo wa Sotai, wa Soferethi, wa Perida;

58 wa Yaala, wa Darkoni, wa Gideli;

59 ukoo wa Shefatia, wa Hatili, wa Pokereth-hasebaimu na ukoo wa Amoni.

60 Basi wahudumu wote wa hekalu na wazawa wa watumishi wa Solomoni, waliorudi kutoka uhamishoni, walikuwa 392.

61 Watu wa miji ifuatayo, nao walirudi: Wa Tel-mela, wa Tel-harsha, wa Kerubu, wa Adoni na wa Imeri; ila haikuwezekana kuthibitisha kama walikuwa wazawa wa Waisraeli

62 wazawa wa Delaya, Tobia na wa Nekoda; jumla: Watu 642.

63 Wazawa wa koo zifuatazo za makuhani pia walirudi: Ukoo wa Hobaya, wa Hakozi na wa Barzilai (aliyekuwa ameoa binti za Barzilai, Mgileadi, naye akachukua jina la ukoo huo).

64 Hao walitafuta orodha yao kati ya wengine walioorodheshwa katika kumbukumbu za koo, lakini ukoo wao haukuwemo. Kwa hiyo hawakuruhusiwa kutiwa katika huduma ya ukuhani kwani walihesabiwa kuwa najisi.

65 Mtawala akawaambia kuwa hawaruhusiwi kushiriki chakula kitakatifu sana, mpaka afike kuhani mwenye kauli ya Urimu na Thumimu.

66 Watu wote waliorudi kutoka uhamishoni jumla yao ilikuwa 42,360.

67 Tena kulikuwa na watumishi wanaume na wanawake 7,337, nao walikuwa waimbaji wanaume na wanawake, wote 245.

68 Walikuwa na farasi 736, nyumbu 245,

69 ngamia 435, na punda 6,720.

70 Baadhi ya wakuu wa koo walichangia kazi ya ujenzi. Mtawala wa mkoa alitoa kilo 8 za dhahabu, mabirika 50, mavazi 530.

71 Baadhi ya wakuu wa koo walitoa kilo 168 za dhahabu, na kilo 1,250 za fedha.

72 Matoleo ya watu wengine wote yalikuwa kilo 168 za dhahabu, kilo 140 za fedha na mavazi ya makuhani 67.

73 Basi, makuhani, Walawi, walinzi wa hekalu, waimbaji, baadhi ya watu wengine, watumishi wa hekalu na watu wote wa Israeli, wakaishi katika miji yao.

8

1 Kisha watu wote, kwa nia moja, wakakusanyika mjini Yerusalemu kwenye uwanja ulio karibu na Lango la Maji. Wakamwambia Ezra, mwandishi, kukileta kitabu cha sheria ya Mose ambayo Mwenyezi-Mungu aliwapa watu wa Israeli.

2 Ezra, ambaye alikuwa kuhani, akaenda na kukileta kitabu cha sheria ya Mose mbele ya mkutano mzima, wanaume kwa wanawake na yeyote aliyeweza kuielewa hiyo sheria aliposikia. Siku hiyo ilikuwa ni siku ya kwanza ya mwezi wa saba.

3 Kisha watu wote wanaume kwa wanawake na yeyote aliyeweza kuelewa, Ezra aliwasomea sheria ya Mose akiwa mbele ya Lango la Maji tangu asubuhi hadi adhuhuri. Watu wote wakatega masikio yao kusikiliza kwa makini kitabu cha sheria.

4 Ezra, mwandishi, alikuwa amesimama kwenye mimbari ya mbao iliyotengenezwa kwa kusudi hilo; na kwenye mkono wake wa kulia walikuwa wamesimama Matithia, Shema, Anaya, Uria, Hilkia na Maaseya; na kwenye mkono wake wa kushoto walikuwa wamesimama Pedaya, Mishaeli, Malkiya, Hashumu, Hashbadana, Zekaria na Meshulamu.

5 Ezra akasimama kwenye mimbari, mbele ya watu wote, nao wakawa wanamkazia macho yao kwa utulivu mkubwa. Mara tu Ezra alipokifungua kitabu cha sheria, watu wote wakasimama wima.

6 Ezra akamshukuru Mwenyezi-Mungu, Mungu Mkuu na watu wote wakaitikia “Amina! Amina!” Huku wakiwa wameinua mikono yao juu. Kisha wakamsujudia Mungu huku nyuso zao zikigusa ardhi.

7 Walawi wafuatao walisaidia kuwaelewesha watu sheria: Yeshua, Bani, Sherebia, Yamini, Akubu, Shabethai, Hodia, Maaseya, Kelita, Azaria, Yozabadi, Hanani na Pelaya; walifanya hivyo kila mmoja akiwa amesimama mahali pake.

8 Wakasoma vizuri toka kitabu cha sheria ya Mungu na kuifafanua na watu wote waliweza kuielewa.

9 Watu waliposikia sheria, waliguswa mioyoni mwao, ndipo wote walipoanza kulia. Hivyo Nehemia aliyekuwa mtawala na Ezra kuhani na mwandishi, pamoja na Walawi waliowafundisha watu waliwaambia watu wote, “Siku hii ni siku takatifu kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, hivyo msiomboleze wala kulia.

10 Sasa rudini nyumbani mkafanye sherehe, mle vinono na kunywa divai nzuri, lakini kumbukeni kuwapelekea wale ambao hawana cha kutosha; kwani leo ni siku takatifu kwa Bwana wetu. Msihuzunike kwa sababu furaha anayowajalia Mwenyezi-Mungu itawapeni nguvu.”

11 Hivyo, Walawi wakawatuliza watu wote, wakisema, “Tulieni kwani siku ya leo ni takatifu; msihuzunike.”

12 Watu wote wakarudi nyumbani kwao kula na kunywa; wakifurahi na kuwagawia wengine chakula kwa kuwa waliyaelewa yote waliyotangaziwa.

13 Kesho yake, wakuu wa koo pamoja na makuhani na Walawi wakakusanyika kwa Ezra mwandishi, ili kujifunza sheria.

14 Wakagundua kuwa, imeandikwa katika kitabu cha sheria kuwa Mwenyezi-Mungu alimwamuru Mose, kwamba watu wanapaswa kukaa vibandani wakati wa sikukuu ya mwezi wa saba.

15 Hivyo wakatangaza katika miji yao yote na huko Yerusalemu, wakisema, “Nendeni milimani, mkalete matawi ya mizeituni, mizeituni mwitu, mihadasi, mitende na miti mingineyo ili kujengea vibanda, kama ilivyoandikwa.”

16 Basi, watu wakaenda kuleta matawi, wakajijengea vibanda kila mtu kwenye dari na kwenye baraza ya nyumba yake, kwenye baraza za nyumba ya Mungu, kwenye uwanja wa Lango la Maji na uwanja wa Lango la Efraimu.

17 Watu wote waliorudi kutoka uhamishoni wakatengeneza vibanda wakaishi humo. Hii ilikuwa ni mara ya kwanza watu kuishi katika vibanda tangu wakati Yeshua, mwana wa Nuni alipokuwa akiishi. Watu walifurahi sana.

18 Kila siku, tangu siku ya kwanza hadi ya mwisho, Ezra aliwasomea watu kitabu cha sheria ya Mungu. Waliadhimisha sikukuu hiyo kwa muda wa siku saba, na siku ya nane wakafanya mkutano mkubwa wa kufunga sikukuu, kama ilivyoagizwa.

9

1 Siku ya ishirini na nne ya mwezi huo wa saba, watu wa Israeli walikusanyika, wakifunga na kuvaa mavazi ya magunia na kujipaka udongo kichwani kuonesha majuto yao.

2 Wakati huo, walikuwa wamejitenga mbali na watu wa mataifa mengine, wakasimama na kuungama dhambi zao na maovu ya babu zao.

3 Kwa muda wa kama masaa matatu, walisimama huku sheria ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wao, inasomwa. Na kwa masaa matatu yaliyofuata, walikuwa wakitubu na kumwabudu Mwenyezi-Mungu, Mungu wao.

4 Kuliwekwa jukwaa la Walawi; hapo walisimama Yeshua, Bani, Kadmieli, Shebania, Buni, Sherebia, Bani na Kenani. Wakamwomba kwa sauti kubwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wao.

5 Walawi, yaani: Yeshua, Kadmieli, Bani, Hashabuea, Sherebia, Hodia, Shebania na Pethahia wakawaambia watu; “Simameni na kumsifu Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu. Msifuni milele na milele! Na watu walisifu jina lako tukufu, ambalo hutukuka kuliko baraka na sifa zote.”

6 Ezra akaomba kwa sala ifuatayo: “Wewe peke yako ndiwe Mwenyezi-Mungu; ndiwe uliyefanya mbingu na jeshi lake lote, dunia na vyote vilivyomo, bahari na vyote vilivyomo; nawe ndiwe unayevihifadhi hai, na jeshi lote la mbinguni lakuabudu wewe.

7 Wewe ndiwe Mwenyezi-Mungu, Mungu uliyemchagua Abramu, ukamtoa toka Uri ya Wakaldayo na kumpa jina Abrahamu.

8 Ukamwona kuwa yu mwadilifu mbele yako; ukafanya agano naye kuwapa wazawa wake nchi ya Wakanaani, Wahiti, Waamori, Waperizi, Wayebusi na Wagirgashi. Na ahadi yako ukaitimiza; kwani wewe u mwaminifu.

9 “Uliyaona mateso ya babu zetu walipokuwa nchini Misri, na walipokuomba msaada kwenye Bahari ya Shamu uliwasikia.

10 Ulifanya ishara na maajabu dhidi ya Farao, watumishi wake wote na watu wote wa nchi yake; kwani ulijua kuwa waliwakandamiza babu zetu. Ukajipatia umaarufu uliopo mpaka leo.

11 Uliigawa bahari katikati mbele yao, nao wakapita katikati ya bahari, mahali pakavu. Lakini ukawatupa Wamisri waliowafuatia kama jiwe zito ndani ya maji mengi.

12 Mchana uliwaongoza kwa mnara wa wingu, na usiku uliwaongoza kwa mnara wa moto ili kuwamulikia njia ya kuendea.

13 Kule mlimani Sinai ulishuka toka mbinguni na kuzungumza nao. Ukawapa maagizo safi, sheria za kweli, kanuni nzuri na amri.

14 Kwa njia ya Mose, mtumishi wako, ukawajulisha Sabato yako takatifu na ukawaagiza kuzifuata amri, kanuni na sheria ulizowaamrisha.

15 Walipokuwa na njaa, ukawapa chakula kutoka mbinguni. Walipokuwa na kiu ukawapa maji kutoka kwenye mwamba. Ukawaagiza kuichukua nchi uliyokuwa umewaahidi.

16 Lakini wao na babu zetu wakawa na kiburi na wakawa na shingo ngumu wakakataa kufuata maagizo yako.

17 Wakakataa kutii; wasiyakumbuke maajabu uliyofanya miongoni mwao. Wakawa na shingo zao ngumu, wakajichagulia kiongozi wa kuwarudisha utumwani nchini Misri. Bali wewe Mungu u mwepesi kusamehe, mwenye neema na huruma, wewe hukasiriki upesi. U mwenye fadhili nyingi, na hukuwatupa.

18 Hata walipojitengenezea sanamu ya ndama na kusema, ‘Huyu ndiye mungu wetu aliyetutoa kutoka nchi ya Misri,’ wakawa wamefanya kufuru kubwa.

19 Wewe kwa huruma zako nyingi hukuwatupa kule jangwani. Mnara wa wingu uliowaongoza mchana haukuondoka, wala mnara wa moto uliowamulikia njia usiku, haukuondoka.

20 Ukawapa roho yako njema kuwashauri; ukawapa mana kuwa chakula chao na maji ya kunywa ili kutuliza kiu chao.

21 Ukawatunza jangwani kwa miaka arubaini na hawakukosa chochote; mavazi yao hayakuchakaa wala nyayo zao hazikuvimba.

22 “Ukawaruhusu kushinda falme na mataifa, ukawafanyia mengi kila upande. Wakaishinda nchi ya Heshboni alikotawala mfalme Sihoni; na tena wakaishinda nchi ya Bashani alikotawala mfalme Ogu.

23 Wazawa wao ukawafanya wawe wengi kama nyota za mbinguni; ukawaleta katika nchi uliyowaahidi babu zao.

24 Hivyo, hao wazawa wakaja na kuimiliki nchi; uliwashinda wakazi wa nchi hiyo, Wakanaani, ukawatia mikononi mwao, pamoja na wafalme wao, watu wao na nchi yao ili wawatende wapendavyo.

25 Miji yenye ngome wakaiteka, wakachukua nchi yenye utajiri, majumba yenye vitu vingi vizuri, visima vilivyochimbwa, mashamba ya mizabibu na mizeituni pamoja na miti yenye matunda kwa wingi. Hivyo wakala, wakashiba na kunenepa na kuufurahia wema wako.

26 Lakini hawakuwa waaminifu kwako. Wakakuasi, wakaiacha sheria yako na kuwaua manabii waliowaonya ili wakurudie wewe. Wakakufuru sana.

27 Hivyo, ukawatia katika mikono ya adui zao, nao wakawatesa. Lakini wakiwa katika mateso yao, wakakulilia, nawe ukawasikia kutoka mbinguni. Na kwa huruma zako nyingi, ukawapelekea viongozi wa kuwaokoa; nao wakawakomboa toka mikononi mwao.

28 Lakini amani ilipopatikana wakatenda dhambi tena mbele yako, nawe ukawaacha watiwe katika mikono ya adui zao wawatawale. Hata hivyo, walipotubu na kukulilia ukawasikiliza kutoka mbinguni. Na kwa kulingana na huruma zako nyingi, ukawaokoa mara nyingi.

29 Ukawaonya ili wairudie sheria yako. Hata hivyo, kwa kiburi chao, wakaacha kuzitii amri zako. Wakayaasi maagizo yako, ambayo kwayo mtu akiyatii, ataishi. Wakawa wajeuri pia wakafanya shingo zao ngumu, na wakakataa kuwa watiifu.

30 Ukawavumilia kwa miaka mingi, na kuwaonya kwa njia ya roho yako kwa kupitia manabii wako; hata hivyo hawakusikiliza. Basi ukawaacha ukawatia mikononi mwa mataifa mengine.

31 Hata hivyo, kutokana na huruma zako nyingi, hukuwaacha waangamie kabisa au kuwatupa, kwani wewe u Mungu mwenye neema na huruma.

32 Kwa hiyo, ee Mungu wetu, Mungu Mkuu, mwenye nguvu na wa kutisha, wewe unalishika agano lako na una fadhili nyingi. Mateso yaliyotupata, sisi, wafalme wetu, wakuu wetu, makuhani wetu, manabii wetu, babu zetu na watu wako wote tangu wakati wa wafalme wa Ashuru mpaka leo, usiyaone kuwa ni madogo.

33 Hata hivyo, unayo haki kwa kutuadhibu hivyo; kwani wewe umekuwa mwaminifu ambapo sisi tumekuwa watenda maovu.

34 Wafalme wetu, wakuu wetu, makuhani wetu na babu zetu hawajaishika sheria yako wala kujali amri yako na maonyo yako uliyowapa.

35 Hawakukutumikia katika ufalme wao, wala walipoyafurahia mema yako mengi uliyowajalia kwa wingi, katika nchi kubwa na yenye rutuba uliyowapa hawakuyaacha matendo yao maovu.

36 Na leo tumekuwa watumwa; tu watumwa katika nchi uliyowapa babu zetu wafurahie matunda na vipawa vyake vyema.

37 Kwa sababu ya dhambi zetu, utajiri wa nchi hii unawaendea wafalme uliowaleta kututawala. Wanatutawala wapendavyo hata na mifugo yetu wanaitendea wapendavyo, tumo katika dhiki kuu.”

38 Kutokana na haya yote yaliyotokea, sisi tunaweka agano imara na wakuu wetu kwa maandishi; Walawi na makuhani wanatia sahihi zao na mhuri wao.

10

1 Kwenye hati yenye mhuri kulikuwapo majina ya Nehemia, mtawala wa mkoa, mwana wa Hakalia, na Sedekia;

2 Seraya, Azaria, Yeremia,

3 Pashuri, Amaria, Malkiya,

4 Hatushi, Shebania, Maluki,

5 Harimu, Meremothi, Obadia,

6 Danieli, Ginethoni, Baruku,

7 Meshulamu, Abiya, Miyamini,

8 Maazia, Bilgai na Shemaya.

9 Pia majina ya Walawi: Yeshua, mwana wa Azania, Binui, wazawa wa Henadadi, Kadmieli.

10 Na ndugu zao waliotia sahihi ni: Shebania, Hodia, Kelita, Pelaya, Hanani,

11 Mika, Rehobu, Hashabia,

12 Zakuri, Sherebia, Shebania,

13 Hodia, Bani na Beninu.

14 Majina ya viongozi wa watu: Paroshi, Pahath-moabu, Elamu, Zatu, Bani,

15 Buni, Azgadi, Bebai,

16 Adoniya, Bigwai, Adini,

17 Ateri, Hezekia, Azuri,

18 Hodia, Hashumu, Bezai,

19 Harifu, Anathothi, Nebai,

20 Magpiashi, Meshulamu, Heziri,

21 Meshezabeli, Sadoki, Yadua,

22 Pelatia, Hanani, Anaya,

23 Hoshea, Hanania, Hashubu,

24 Haloheshi, Pilha, Shobeki,

25 Rehumu, Hashabna, Maaseya,

26 Ahia, Hanani, Anani,

27 Maluki, Harimu na Baana.

28 Sisi sote watu wa Israeli, makuhani, Walawi, wangoja malango, waimbaji, watumishi wa hekalu na watu wote waliojitenga na mataifa jirani kufuata sheria ya Mungu pamoja na wake zao, wana wao na binti zao, wote wenye maarifa na fahamu,

29 tunaungana na ndugu zetu, wakuu wetu, katika kula kiapo na kwamba tukivunja kiapo hiki tutaapizwa, na twaapa kuwa tutaishi kwa kufuata sheria ya Mungu ambayo aliitoa kwa njia ya Mose, mtumishi wake. Tena tutatii yote ambayo Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, anatuamuru, na kuwa tutashika maagizo yake na kufuata masharti yake.

30 Binti zetu hatutawaoza kwa watu wa nchi hii na wala wana wetu hawataoa kwao.

31 Ikiwa watu hao wanaleta bidhaa au nafaka kuuza siku ya Sabato, sisi hatutanunua siku hiyo wala siku nyingine yoyote iliyo takatifu. Mwaka wa saba hatutailima ardhi na madeni yote tutayafuta.

32 Tunajiwekea sheria kwamba kwa mwaka tutatoa theluthi moja ya shekeli kwa ajili ya gharama za huduma ya nyumba ya Mungu:

33 Mikate mitakatifu, sadaka za nafaka za kawaida, sadaka za kuteketezwa za kawaida, sadaka za siku za Sabato, sikukuu za mwandamo wa mwezi, sikukuu nyingine zilizowekwa, vitu vingine vitakatifu, sadaka za kuondoa dhambi, ili kuwafanyia upatanisho watu wa Israeli na kazi nyingine zozote za nyumba ya Mungu wetu.

34 Sisi sote, watu wote, makuhani na Walawi tutapiga kura kila mwaka ili kuchagua ukoo utakaoleta kuni za kuteketeza tambiko madhabahuni pa Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, kama sheria ilivyo.

35 Tunaahidi kuleta kila mwaka malimbuko yetu ya mazao na ya matunda ya kila mti kwenye nyumba ya Mwenyezi-Mungu.

36 Kwa kufuata ilivyoandikwa katika sheria kila mzaliwa wa kwanza wa kiume, katika nyumba zetu, atapelekwa katika nyumba ya Mungu wetu kwa makuhani wanaohudumu humo, pia tutapeleka kila mtoto wa kwanza wa kiume wa ng'ombe wetu, mbuzi wetu na kondoo wetu.

37 Kila unga wetu wa kwanza, matoleo yetu, matunda ya miti, divai na mafuta tutavileta kwa kuhani kwenye vyumba vya nyumba ya Mungu wetu. Tena tutaleta zaka zetu za mazao yetu kwa Walawi, kwani ndio wanaohusika na ukusanyaji wa zaka hizo katika vijiji vyetu.

38 Kuhani, mzawa wa Aroni, atakuwa na Walawi wanapopokea zaka. Halafu Walawi watapeleka sehemu ya kumi ya zaka zote zilizotolewa katika nyumba ya Mungu kwenye vyumba na ghala.

39 Watu wa Israeli na Walawi watayapeleka matoleo ya nafaka, divai na mafuta ya zeituni kwenye vyumba ambamo vyombo vya patakatifu vinatunzwa na ambamo makuhani, wangoja malango na waimbaji wana vyumba vyao. Na daima tutaijali nyumba ya Mungu wetu.

11

1 Kisha, viongozi wa watu wakakaa mjini Yerusalemu; watu wengine wote, wakapiga kura kati ya kila jamaa kumi ili kuchagua jamaa moja itakayokaa mjini Yerusalemu, mji mtakatifu. Jamaa nyingine tisa zikakaa katika miji yao mingine.

2 Watu wakawasifu wale wote waliokubali kukaa mjini Yerusalemu.

3 Na katika miji mingine, watu wa Israeli, makuhani, Walawi, walinzi wa malango na wazawa wa watumishi wa Solomoni, walikaa katika maeneo yao wenyewe, katika miji yao.

4 Baadhi ya watu wa kabila la Yuda na wa kabila la Benyamini walikaa katika mji wa Yerusalemu. Wafuatao ndio watu wa ukoo wa Yuda waliokaa mjini Yerusalemu: Athaya, mwana wa Uzia, mwana wa Zekaria, mwana wa Amaria, mwana wa Shefatia, mwana wa Mahalaleli. Wote hao ni wazawa wa Peresi.

5 Pia Maaseya, mwana wa Baruku, mwana wa Kolhoze, mwana wa Hazaya, mwana wa Adaya, mwana wa Yoyaribu, mwana wa Zekaria, Mshilo.

6 Wazawa wote wa Peresi waliokaa mjini Yerusalemu walikuwa wanaume mashujaa 468.

7 Watu wa ukoo wa Benyamini waliokaa mjini Yerusalemu ni: Salu, mwana wa Meshulamu, mwana wa Yoedi, mwana wa Pedaya, mwana wa Kolaya, mwana wa Maaseya, mwana wa Ithieli na mwana wa Yeshaya.

8 Baada ya huyo walikuwako Gabai na Salai. Jumla yao 928.

9 Yoeli, mwana wa Zikri, alikuwa ndiye mkuu wao; naye Yuda mwana wa Hasenua alikuwa mkuu wa pili wa mji.

10 Makuhani waliokaa mjini Yerusalemu walikuwa: Yedaya, mwana wa Yoaribu, Yakini,

11 Seraya, mwana wa Hilkia, mwana wa Meshulamu, mwana wa Sadoki, mwana wa Merayothi, mwana wa Ahitubu aliyekuwa msimamizi wa nyumba ya Mungu;

12 hao pamoja na ndugu zao waliofanya kazi hekaluni; walikuwa watu 822. Pamoja na hao, kulikuwa na Adaya, mwana wa Yerohamu, mwana wa Pelalia, mwana wa Amsi, mwana wa Zekaria, mwana wa Pashuri, mwana wa Malkiya;

13 pia kulikuwa ndugu zake waliokuwa wakuu wa jamaa za baba zao; wote pamoja walikuwa watu 242. Pia walikuwako Amaasai, mwana wa Azareli, mwana wa Ahzai, mwana wa Meshilemothi, mwana wa Imeri,

14 pamoja na ndugu zao; wote wakiwa 128, watu mashujaa. Na mkuu wao alikuwa Zabdieli mwana wa Hagedolimu.

15 Nao Walawi waliokaa mjini Yerusalemu walikuwa: Shemaya, mwana wa Hashubu, mwana wa Azrikamu, mwana wa Hashabia, na mwana wa Buni.

16 Shabethai na Yozabadi, wakuu wa ukoo wa Walawi, walikuwa wasimamizi wa kazi za nje ya nyumba ya Mungu,

17 na Matania, mwana wa Mika, mwana wa Zabdi, mzawa wa Asafu, aliyekuwa kiongozi wakati wa kuomba sala za shukrani. Bakbukia alikuwa msaidizi wake. Pamoja nao alikuwako Abda, mwana wa Shamua, mwana wa Galali na mzawa wa Yeduthuni.

18 Walawi wote waliokaa mjini Yerusalemu, mji mtakatifu, walikuwa 284.

19 Wangoja malango waliokaa mjini Yerusalemu walikuwa: Akubu na Talmoni pamoja na ndugu zao waliokuwa wakilinda malango, walikuwa 172.

20 Watu wengine wa Israeli, makuhani na Walawi walikaa katika miji ya Yuda, kila mmoja katika urithi wake.

21 Lakini watumishi wa hekalu walikaa mjini Yerusalemu katika eneo la Ofeli wakiwa chini ya usimamizi wa Ziha na Gishpa.

22 Kiongozi wa Walawi waliokaa mjini Yerusalemu alikuwa, Uzi, mwana wa Bani, mwana wa Hashabia, mwana wa Matania, mwana wa Mika wa ukoo wa Asafu, waliokuwa waimbaji, viongozi waangalizi wa shughuli za nyumba ya Mungu.

23 Mfalme alikuwa ametoa amri kuhusu zamu zao na mahitaji yao ya kila siku.

24 Pethahia, mwana wa Meshezabeli, wa ukoo wa Zera katika kabila la Yuda, alikuwa mwakilishi kwa mfalme kuhusu mambo yote ya watu wa Yuda.

25 Watu wengine walikaa katika miji karibu na mashamba yao. Baadhi ya watu wa kabila la Yuda walikaa Kiriath-arba, Diboni na Yekabzeeli pamoja na vijiji vilivyoizunguka.

26 Wengine pia walikaa katika miji ya Yeshua, Molada, Beth-peleti,

27 Hasar-shuali na Beer-sheba pamoja na vijiji vilivyoizunguka.

28 Wengine walikaa katika mji wa Ziklagi, Mekona na vijiji vilivyoizunguka.

29 Wengine walikaa katika miji ya Enrimoni, Sora, Yarmuthi,

30 Zanoa na Adulamu pamoja na vijiji vilivyoizunguka, Lakishi na mashamba yaliyouzunguka, na katika Azeka pamoja na vijiji vilivyouzunguka. Hii ina maana kwamba watu wa Yuda walikaa katika eneo lililoko kati ya Beer-sheba upande wa kusini na Bonde la Hinomu upande wa kaskazini.

31 Watu wa kabila la Benyamini walikaa Geba, Mikmashi, Ai, Betheli na vijiji vinavyoizunguka.

32 Wengine walikaa Anathothi, Nobu, Anania,

33 Hazori, Rama, Gitaimu,

34 Hadidi, Seboimu, Nebalati,

35 Lodi na Ono lililokuwa Bonde la Mafundi.

36 Baadhi ya Walawi wa Yuda walichanganyikana na watu wa Benyamini.

12

1 Ifuatayo ni orodha ya makuhani na Walawi waliorudi kutoka uhamishoni pamoja na Zerubabeli, mwana wa Shealtieli, na kuhani mkuu Yeshua. Makuhani: Seraya, Yeremia, Ezra,

2 Amaria, Maluki, Hatushi,

3 Shekania, Rehumu, Meremothi,

4 Ido, Ginethoni, Abiya,

5 Miyamini, Maadia, Bilga,

6 Shemaya, Yoyaribu, Yedaya,

7 Salu, Amoki, Hilkia na Yedaya. Hao walikuwa ni wakuu wa makuhani na ndugu zao wakati wa Yeshua.

8 Walawi: Yeshua, Binui, Kadmieli, Sherebia, Yuda na Matania, ambaye alihusika na usimamizi wa nyimbo za shukrani akishirikiana na ndugu zake.

9 Nao Bakbukia na Uno rafiki zao, walisimama ibadani mkabala nao.

10 Yeshua alimzaa Yoyakimu, Yoyakimu alimzaa Eliashibu, Eliashibu alimzaa Yoyada,

11 Yoyada alimzaa Yonathani na Yonathani akamzaa Yadua.

12 Yoyakimu alipokuwa kuhani mkuu, makuhani wafuatao walikuwa wakuu wa koo zao: Wa Seraya, Meraya; wa Yeremia, Hanania;

13 wa Ezra, Mehulamu; wa Amaria, Yehohanani;

14 wa Maluki, Yonathani; wa Shebania, Yosefu;

15 wa Harimu, Adna; wa Merayothi, Helkai;

16 wa Ido, Zekaria; wa Ginethoni, Meshulamu;

17 wa Abiya, Zikri; ukoo wa Miniamini; wa Moadia, Piltai;

18 wa Bilga, Shamua; wa Shemaya, Yehonathani;

19 wa Yoaribu, Matenai; wa Yedaya, Uzi;

20 wa Salai, Kalai; wa Amoki, Eberi;

21 wa Hilkia, Heshabia; na wa ukoo wa Yedaya, Nethaneli.

22 Wakati wa Eliashibu, Yoyada, Yohanani na Yadua wakuu wa jamaa za Walawi, waliorodheshwa; vilevile wakati wa utawala wa mfalme Dario wakuu wa jamaa za makuhani waliorodheshwa.

23 Wakuu wa jamaa za ukoo wa Lawi waliorodheshwa katika kitabu cha Kumbukumbu mpaka wakati wa Yohanani mjukuu wa Eliashibu.

24 Viongozi wa Walawi: Hashabia, Sherebia, Yeshua mwana wa Kadmieli walisimama mkabala na ndugu zao; walipangwa kuimba nyimbo za kusifu na kushukuru, kufuatana na amri ya mfalme Daudi, mtu wa Mungu.

25 Mabawabu walikuwa: Matania, Bakbukia, Obadia, Meshulamu, Talmoni na Akubu; pia hao walikuwa walinzi wa ghala.

26 Watu hao waliishi wakati wa Yoyakimu, mwana wa Yeshua mwana wa Yosadaki na pia wakati wa Nehemia aliyekuwa mtawala wa mkoa; na hata wakati wa Ezra kuhani na mwandishi.

27 Kisha wakati wa kuweka wakfu ukuta wa Yerusalemu Walawi walitafutwa kila mahali walipokaa ili kuja Yerusalemu kusherehekea kwa furaha pamoja na shukrani na nyimbo, wakitumia matoazi, vinubi na zeze.

28 Wazawa wa waimbaji wakakusanyika kutoka viunga vya Yerusalemu na vijiji vya Wanetofathi,

29 pia kutoka Beth-gilgali, eneo la Geba na Azmawethi, kwa sababu waimbaji walikuwa wamejijengea vijiji kandokando ya Yerusalemu.

30 Makuhani na Walawi walijitakasa, pia waliwatakasa watu, malango na ukuta.

31 Niliwakusanya viongozi wote wa Yuda kwenye ukuta na kutenga waimbaji katika makundi mawili makubwa yaliyoimba nyimbo za shukrani wakiwa katika maandamano. Kundi moja lilielekea upande wa kulia wa ukuta hadi kwenye Lango la Takataka.

32 Waimbaji hao walifuatiwa na Hoshaya akiwa pamoja na nusu ya viongozi wa Yuda.

33 Pamoja naye walikwenda Azaria, Ezra, Meshulamu,

34 Yuda, Benyamini, Shemaya na Yeremia.

35 Wazawa wafuatao wa makuhani walikuwa na tarumbeta: Zekaria, mwana wa Yonathani, mwana wa Shemaya aliyekuwa mwana wa Matania, mwana wa Mikaya, mwana wa Zakuri, mwana wa Asafu.

36 Ndugu zake wafuatao waliimba kwa ala za muziki za mfalme Daudi, mtu wa Mungu, yaani Shemaya, Azareli, Milalai, Gilalai, Maai, Nethaneli, Yuda na Hanani, walitanguliwa na Ezra mwandishi.

37 Kwenye Lango la Chemchemi walipanda ngazi kuelekea mji wa Daudi, wakaipita Ikulu ya Daudi, na kuelekea nyuma kwenye ukuta hadi kwenye Lango la Maji, mashariki ya mji.

38 Kundi lingine lililoimba nyimbo za shukrani lilielekea upande wa kushoto juu ya ukuta. Mimi nilifuatana na kundi hili pamoja na nusu ya watu. Tulipitia Mnara wa Tanuri hadi kwenye Ukuta Mpana.

39 Na kutoka hapo, tulipitia Lango la Efraimu, Lango la Yeshana, Lango la Samaki, Mnara wa Hananeli, Mnara wa Mia Moja mpaka kwenye Lango la Kondoo. Tulimalizia maandamano yetu kwenye Lango la Gereza.

40 Hivyo, makundi yote mawili yaliyokuwa yanaimba nyimbo za shukrani yalisimama katika nyumba ya Mungu, pamoja nami na nusu ya viongozi;

41 hata na makuhani waliokuwa na tarumbeta: Eliakimu, Maaseya, Miniamini, Mikaya, Eliehoenai, Zekaria na Hanania.

42 Hao walifuatwa na Maaseya, Shemaya, Eleazari, Uzi, Yehohanani, Malkiya, Elamu na Ezeri. Waimbaji waliimba wakiongozwa na Yezrahia.

43 Siku hiyo, watu walitoa tambiko nyingi na kufurahi kwani Mungu aliwafanya wawe na furaha kubwa. Pia wanawake na watoto, wote walifurahi. Vigelegele vya furaha toka mjini Yerusalemu vilisikika mbali.

44 Wakati huo walichaguliwa watu wa kutunza vyumba vya ghala ambamo matoleo kwa ajili ya hekalu yalitunzwa, malimbuko ya kwanza, zaka na kuyakusanya kutoka mashamba ya miji, kwa ajili ya makuhani na Walawi kama ilivyotakiwa na sheria. Watu wote waliwafurahia makuhani na Walawi waliohudumu,

45 kwa sababu walifanya ibada ya Mungu wao na ibada ya utakaso, kama waimbaji walivyoimba hata walinzi wa malango kulingana na agizo la mfalme Daudi na Mfalme Solomoni mwanawe.

46 Tangu wakati wa mfalme Daudi na Asafu kulikuweko kiongozi wa waimbaji, na kulikuwako nyimbo za sifa na shukrani kwa Mungu.

47 Watu wote wa Israeli, tangu wakati wa Zerubabeli na Nehemia, walitoa matoleo ya kila siku ambayo yaliwatunza waimbaji walinda malango. Zaidi ya yote, watu wa Israeli walitoa matoleo kwa ajili ya Walawi, nao Walawi wakatenga sehemu kwa ajili ya wazawa wa Aroni.

13

1 Katika siku hiyo ya sherehe, kitabu cha Mose kilisomwa na ilifahamika kuwa Waamoni na Wamoabu kamwe wasiingie katika mkutano wa watu wa Mungu.

2 Maana watu wa Israeli, walipokuwa wanasafiri toka Misri, hawakuwapa chakula wala maji ya kunywa, badala yake walimkodisha Balaamu kuwalaani watu wa Israeli, lakini Mungu wetu aligeuza laana yao kuwa baraka.

3 Watu wa Israeli waliposikia sheria hiyo waliwatenga watu wa mataifa mengine.

4 Kabla ya siku ya sherehe, kuhani Eliashibu aliyekuwa ameteuliwa kuangalia vyumba vya nyumba ya Mungu wetu, na mwenye uhusiano mwema na Tobia,

5 alimruhusu Tobia kutumia chumba kikubwa ambamo hapo awali walikuwa wameweka tambiko za nafaka, ubani, vyombo, zaka za nafaka, divai, mafuta; vitu hivyo vyote Waisraeli walivyoagizwa kuwapa Walawi, waimbaji, walinda malango, na matoleo kwa makuhani.

6 Wakati mambo haya yalipokuwa yanatendeka mimi sikuwako Yerusalemu; kwani katika mwaka wa thelathini na mbili wa utawala wa mfalme Artashasta wa Babuloni, nilikuwa nimeomba likizo; nami nikaenda kutoa ripoti kwake.

7 Niliporudi Yerusalemu ndipo nikagundua uovu wa Eliashibu wa kumpa Tobia chumba katika ua wa nyumba ya Mungu.

8 Nilikasirika sana na nikavitupa nje vyombo vyote vya Tobia.

9 Niliamuru watu, nao wakatakasa vyombo hivyo, ndipo nikarudisha humo vifaa vya nyumba ya Mungu, pamoja na tambiko za nafaka na ubani.

10 Tena nikagundua kuwa Walawi hawakupewa haki zao; na matokeo yake ni kwamba Walawi na waimbaji waliokuwa wakifanya kazi hapo awali, sasa walikwisha rudia mashamba yao.

11 Nikawakemea viongozi, nikasema, “Kwa nini nyumba ya Mungu imeachwa?” Niliwakusanya pamoja na kuwarudisha kazini.

12 Kisha, watu wote wa Israeli, wakaanza tena kuleta zaka zao za nafaka, divai na mafuta kwenye ghala.

13 Nikawateua watu wafuatao kuwa watunzaji wa ghala: Kuhani Shelemia, mwandishi Sadoki na Pedaia Mlawi. Hanani, mwana wa Zakuri, mwana wa Matania akawa msaidizi wao. Walikuwa waaminifu na kazi yao ilikuwa kuwagawia ndugu zao mahitaji yao.

14 Ee, Mungu wangu, nikumbuke kwa ajili ya haya yote na usiyasahau matendo yangu mema niliyofanya kwa ajili ya nyumba yako na kwa ajili ya huduma yako.

15 Wakati huohuo, nikawaona watu wa Yuda wakisindika na kukamua zabibu siku za Sabato. Tena wengine walikuwa wakiwabebesha punda wao nafaka, divai, zabibu, tini na vitu vingine wakivipeleka mjini Yerusalemu. Nikawaonya kuwa hawana ruhusa kuuza vitu siku hiyo.

16 Watu wengine toka mji wa Tiro walileta samaki na bidhaa nyingine mjini Yerusalemu na kuwauzia watu wetu siku ya Sabato.

17 Nikawakemea viongozi wa watu wa Yuda, nikisema, “Uovu gani huu mnaofanya, kuikufuru Sabato?

18 Je, babu zetu hawakufanya uovu wa namna hii hii na kumfanya Mungu wetu kutuletea maafa pamoja na mji huu? Na bado mnaleta ghadhabu yake juu ya watu wa Israeli kwa kuikufuru Sabato.”

19 Hivyo, niliamuru kuwa malango ya mji wa Yerusalemu yafungwe mara Sabato inapoanza jioni, wakati giza linapoanza kuingia, na yasifunguliwe mpaka Sabato imekwisha. Niliweka baadhi ya watumishi wangu kwenye malango na kuwaagiza kuwa kitu chochote kisiletwe mjini siku ya Sabato.

20 Mara mbili au tatu hivi wafanyabiashara waliokuwa wakiuza bidhaa za aina mbalimbali iliwabidi kulala nje ya mji.

21 Niliwaonya na kuwaambia: “Hakuna maana kulala nje ya mji. Mkijaribu tena nitatumia nguvu.” Hivyo tangu wakati huo hawakurudi tena siku ya Sabato.

22 Niliagiza Walawi kujitakasa na kwenda kuyalinda malango ili kutunza Sabato iwe takatifu. Ee, Mungu wangu, nikumbuke hata na kwa hili pia na unihurumie kutokana na fadhili zako kuu.

23 Tena wakati huo niliona Wayahudi waliooa wanawake kutoka Ashdodi, Amoni na Moabu;

24 na nusu ya watoto wao walizungumza Kiashdodi au lugha nyingine na hawakuweza kuzungumza lugha ya Yuda.

25 Niliwakemea na kuwaapiza, hata nikawapiga baadhi yao na kuwavuta nywele zao. Niliwalazimisha kuapa kwa jina la Mungu, nikisema, “Binti zenu msiwaoze kwa vijana wao, wala binti zao wasiolewe na vijana wenu au na nyinyi wenyewe.

26 Je, Solomoni hakutenda dhambi kwa sababu ya wanawake wa namna hiyo? Yeye alikuwa mfalme mkuu kuliko wafalme wa mataifa mengine. Mungu alimpenda na akamfanya kuwa mfalme juu ya watu wote wa Israeli, hata hivyo wanawake wa mataifa mengine, walimfanya hata yeye atende dhambi.

27 Je, sasa tufuate mfano wenu na tutende dhambi hii kubwa ya kutomtii Mungu wetu kwa kuoa wanawake wa kigeni?”

28 Mmoja kati ya wana wa Yoyada, mwana wa kuhani mkuu Eliashibu, alioa binti Sanbalati kutoka mji wa Beth-horoni; kwa sababu hiyo nilimfukuza kutoka mbele yangu.

29 Ee Mungu, kumbuka jinsi watu walivyochafua ukuhani na agano la kikuhani na la Walawi.

30 Niliwatakasa watu kutokana na chochote kilichokuwa cha kigeni. Nikatayarisha mwongozo kwa ajili ya makuhani na Walawi kuhusu kazi ya kila mmoja wao.

31 Niliagiza matoleo ya kuni kufanyika katika wakati unaopaswa na malimbuko wakati wake. Ee Mungu wangu, nikumbuke kwa ajili ya haya yote na unijalie mema.