1 Neno la Mwenyezi-Mungu lililomjia Sefania mwana wa Kushi, mwana wa Gedalia, mwana wa Amenia, mwana wa Hezekia, wakati wa utawala wa mfalme Yosia mwana wa Amoni, mfalme wa Yuda:
2 Mwenyezi-Mungu asema: “Nitavifagilia mbali viumbe vyote duniani:
3 Wanadamu, wanyama, ndege wa angani na samaki wa baharini; vyote nitaviangamiza. Waovu nitawaangamiza kabisa; wanadamu nitawafagilia mbali duniani.
4 Nitaunyosha mkono wangu dhidi ya nchi ya Yuda, kadhalika na wakazi wote wa mji wa Yerusalemu. Nitaangamiza mabaki yote ya Baali kutoka nchi hii, na hakuna atakayetambua jina lao.
5 Nitawaangamiza wote wanaosujudu juu ya paa, wakiabudu jeshi la mbinguni. Nitawaangamiza wale wanaoniabudu na kuapa kwa jina langu, hali wanaapa pia kwa jina la mungu Milkomu.
6 Nitawaangamiza wote walioniacha mimi Mwenyezi-Mungu wote walioacha kunitafuta na kuniuliza shauri.”
7 Nyamazeni mbele ya Bwana Mwenyezi-Mungu, kwani siku ya Mwenyezi-Mungu iko karibu. Mwenyezi-Mungu ameandaa tambiko, nao aliowaalika amewateua.
8 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Katika siku ile ya karamu yangu, nitawaadhibu viongozi wa watu hao, kadhalika na wana wa mfalme pamoja na wote wanaoiga desturi za kigeni.
9 Siku hiyo nitawaadhibu wote: Wanaoruka kizingiti cha nyumba kama wapagani, wanaojaza nyumba ya bwana wao vitu vya dhuluma na wizi.
10 “Siku hiyo, nasema mimi Mwenyezi-Mungu, Kutasikika kilio kutoka Lango la Samaki, maombolezo kutoka Mtaa wa Pili, na mlio mkubwa kutoka milimani.
11 Lieni enyi wakazi wa Makteshi! Wafanyabiashara wote wameangamia, wote wapimao fedha wamefutiliwa mbali.
12 Wakati huo nitaupekua mji wa Yerusalemu kwa taa, nitawaadhibu wanaoishi wametulia kama machicha ya divai, wote ambao husema mioyoni mwao: ‘Mwenyezi-Mungu hatafanya kitu: Chema au kibaya.’
13 Utajiri wao utanyakuliwa, na nyumba zao zitaachwa tupu! Watajijengea nyumba, lakini hawataishi humo. Watapanda mizabibu, lakini hawatakunywa divai yake.”
14 Ile siku kubwa ya Mwenyezi-Mungu imekaribia, iko karibu na inakuja mbio. Mlio wa siku ya Mwenyezi-Mungu ni wa uchungu; hapo, shujaa atalia kwa sauti.
15 Siku hiyo itakuwa siku ya ghadhabu, ni siku ya dhiki na uchungu, siku ya giza na huzuni; siku ya uharibifu na maangamizi, siku ya mawingu na giza nene.
16 Siku hiyo ni ya mlio wa tarumbeta ya vita, dhidi ya miji yenye ngome na kuta ndefu.
17 Kwa kuwa watu wamemkosea Mwenyezi-Mungu, yeye atawaletea dhiki kubwa, hivyo kwamba watatembea kama vipofu. Damu yao itamwagwa kama vumbi, na miili yao kama mavi.
18 Fedha yao wala dhahabu yao havitaweza kuwaokoa katika siku hiyo ya ghadhabu ya Mwenyezi-Mungu. Kwa moto wa wivu wake dunia yote itateketezwa. Kwa ukamilifu na kwa namna ya kutisha atawafanya wakazi wote duniani watoweke.
1 Kusanyikeni, kusanyikeni enyi taifa la watu wasio na aibu,
2 kabla hamjapeperushwa mbali kama makapi, kabla haijawajia siku ya hasira kali ya Mwenyezi-Mungu, kabla haijawajia siku ya ghadhabu ya Mwenyezi-Mungu.
3 Mtafuteni Mwenyezi-Mungu enyi wanyenyekevu wote nchini, enyi mnaozitii amri zake. Tafuteni uadilifu, tafuteni unyenyekevu; labda mtaiepa siku ya ghadhabu ya Mwenyezi-Mungu.
4 Mji wa Gaza utahamwa, Ashkeloni utakuwa tupu. Wakazi wa Ashdodi watatimuliwa mchana, na wale wa Ekroni watang'olewa.
5 Ole wenu wakazi wa nchi za pwani, watu mnaoishi huko Krete! Mwenyezi-Mungu ametamka dhidi yenu enyi wakazi wa Kanaani, nchi ya Filistia: Mimi nitawaangamiza asibaki hata mkazi mmoja!
6 Nanyi nchi za pwani mtafanywa kuwa malisho; mtakuwa vibanda vya wachungaji na mazizi ya kondoo.
7 Nchi ya pwani itamilikiwa na mabaki ya ukoo wa Yuda. Watachunga mifugo yao huko. Nyumba za mji wa Ashkeloni zitakuwa mahali pao pa kulala. Maana Mwenyezi-Mungu, Mungu wao atawakumbuka na kuwarudishia hali yao njema.
8 “Nimeyasikia masuto ya Moabu na dhihaka za Waamoni; jinsi walivyowasuta watu wangu, na kujigamba kuiteka nchi yao.
9 Kwa hiyo, niishivyo mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, mimi Mungu wa Israeli, Moabu itakuwa kama Sodoma na Amoni itakuwa kama Gomora. Nchi zake zitakuwa za viwavi na mashimo ya chumvi, zitakuwa ukiwa milele. Watu wangu watakaobaki wataziteka nyara, watu wa taifa langu waliosalia watazimiliki.”
10 Hayo yatakuwa malipo ya kiburi chao, kwa sababu waliwadhihaki na kujigamba dhidi ya watu wa Mwenyezi-Mungu wa majeshi.
11 Mwenyezi-Mungu atakuwa wa kutisha dhidi yao; miungu yote ya dunia ataikondesha. Mataifa yote duniani yatamsujudia; kila taifa katika mahali pake.
12 Nanyi watu wa Kushi pia mtauawa kwa upanga wake.
13 Mwenyezi-Mungu atanyosha mkono wake kaskazini, na kuiangamiza nchi ya Ashuru. Ataufanya mji wa Ninewi kuwa ukiwa, kuwa mahali pakavu kama jangwa.
14 Makundi ya mifugo yatalala humo, kadhalika kila mnyama wa porini. Tai na yangeyange na korongo wataishi juu ya nguzo zake, bundi watalia kwenye madirisha yake, kunguru watalia kwenye vizingiti, maana nyumba zake za mierezi zitakuwa tupu.
15 Je, huu ndio mji uliojivuna na kuishi kwa usalama, mji uliojisemea, “Ni mimi tu, hakuna mwingine!” Jinsi gani umekuwa mtupu na makao ya wanyama wa mwituni! Kila apitaye karibu atauzomea na kuudharau.
1 Ole wake mji wa Yerusalemu, mji mchafu, najisi na mdhalimu.
2 Hausikilizi onyo lolote, wala haukubali kukosolewa. Haukumtegemea Mwenyezi-Mungu kamwe, wala kumkaribia Mungu wake.
3 Viongozi wake ni simba wangurumao, mahakimu wake ni mbwamwitu wenye njaa jioni wasioacha chochote mpaka asubuhi.
4 Manabii wake ni watu wasiojali na wadanganyifu. Makuhani wake wamevitia unajisi vitu vitakatifu na kuihalifu sheria kwa nguvu.
5 Lakini Mwenyezi-Mungu aliye mjini humo ni mwadilifu, yeye hatendi jambo lolote baya. Kila siku asubuhi hudhihirisha kauli yake, naam, kila kunapopambazuka huitekeleza. Lakini wahalifu hawana aibu hata kidogo.
6 Mwenyezi-Mungu asema: “Nimeyafutilia mbali mataifa; kuta zao za kujikinga ni magofu. Barabara zao nimeziharibu, na hamna apitaye humo. Miji yao imekuwa mitupu, bila watu, na bila wakazi.
7 Nilisema, ‘Hakika mji huu watanicha na kukubali kukosolewa; hautaacha kukumbuka mara hizo zote nilizowaadhibu.’ Lakini watu wake walizidisha tamaa zao za kufanya matendo yao kuwa upotovu.
8 “Kwa hiyo ningojeni mimi Mwenyezi-Mungu, ngoja siku nitakapoinuka kutoa mashtaka. Nimeamua kuyakusanya mataifa na falme, kuyamwagia ghadhabu yangu, kadhalika na ukali wa hasira yangu. Dunia yote itateketezwa kwa moto wa ghadhabu yangu.
9 “Wakati huo nitaibadili lugha ya watu, nitawawezesha kusema lugha adili ili waniite mimi Mwenyezi-Mungu, na kuniabudu kwa moyo mmoja.
10 Kutoka ng'ambo ya mito ya Kushi watu wangu wanaoniomba ambao wametawanyika, wataniletea sadaka yangu.
11 “Siku hiyo, haitakulazimu kuona aibu, kutokana na matendo yako ya kuniasi, maana nitawaondoa miongoni mwako wale wanaojigamba na kujitukuza nawe hutakuwa na kiburi tena katika mlima wangu mtakatifu.
12 Nitakuachia watu wapole na wanyenyekevu ambao watakimbilia usalama kwangu mimi Mwenyezi-Mungu.
13 Waisraeli watakaobaki, hawatatenda mabaya wala hawatasema uongo; wala kwao hatapatikana mdanganyifu yeyote. Watapata malisho na kulala wala hakuna mtu atakayewatisha.”
14 Imba kwa sauti, ewe Siyoni, paza sauti ee Israeli. Furahi na kushangilia kwa moyo wote, ewe Yerusalemu!
15 Mwenyezi-Mungu amekuondolea hukumu iliyokukabili, amewageuzia mbali adui zako. Mwenyezi-Mungu, mfalme wa Israeli yuko pamoja nawe hutaogopa tena maafa.
16 Siku hiyo, mji wa Yerusalemu utaambiwa: “Usiogope, ee Siyoni, usilegee mikono.
17 Mwenyezi-Mungu, Mungu wako yu pamoja nawe yeye ni shujaa anayekuletea ushindi. Yeye atakufurahia kwa furaha kuu, kwa upendo wake atakujalia uhai mpya. Atakufurahia kwa wimbo wa sauti kubwa,
18 kama vile katika siku ya sikukuu.” Mwenyezi-Mungu asema: “Nitakuondolea maafa yako, nawe hutahitaji kuona aibu kwa ajili yake.
19 Wakati huo, nitawaadhibu wote wanaokukandamiza. Nitawaokoa vilema na kuwakusanya waliotupwa, na kubadili aibu yao kuwa sifa na fahari duniani kote.
20 Wakati huo nitawakusanya, na kuwafanya mjulikane na kusifiwa, miongoni mwa watu wote duniani nitakapowarudishia hali yenu njema nanyi muone kwa macho yenu wenyewe. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”