1 Hizi ni methali za Solomoni mfalme wa Israeli, mwana wa Daudi.
2 Methali hizi zawapatia watu hekima na nidhamu; zawafanya waelewe maneno ya busara,
3 zawafanya kuwa na nidhamu, utaratibu, uadilifu, haki na kutenda kwa usawa.
4 Huwapatia wajinga werevu na vijana maarifa na hadhari.
5 Mwenye hekima azisikie na kuongeza elimu yake, naye mwenye busara apate mwongozo.
6 Mtu aelewe methali na mifano, maneno ya wenye hekima na vitendawili vyao.
7 Kumcha Mwenyezi-Mungu ni msingi wa maarifa, lakini wapumbavu hudharau hekima na adabu.
8 Mwanangu, sikiliza mwongozo wa baba yako, wala usiyapuuze mafundisho ya mama yako;
9 hayo yatakupamba kilemba kichwani pako, kama mkufu shingoni mwako.
10 Mwanangu, usikubali kushawishiwa na wenye dhambi.
11 Wakisema: “Twende tukamvizie mtu na kumuua; njoo tukawashambulie wasio na hatia!
12 Tutawameza kama Kuzimu wakiwa hai, watakuwa kama wale washukao Shimoni.
13 Tutajitwalia mali zote za thamani, nyumba zetu tutazijaza nyara.
14 Njoo ushirikiane nasi, vyote tutakavyopata tutagawana.”
15 Wewe mwanangu usiandamane nao, uzuie mguu wako usifuatane nao.
16 Maana wao wako mbioni kutenda maovu, haraka zao zote ni za kumwaga damu.
17 Mtego utegwao huku ndege anaona, mtego huo wategwa bure.
18 Wao huvizia na kujiangamiza wao wenyewe, hutega mtego wa kujinasa wao wenyewe.
19 Ndivyo zilivyo njia za waishio kwa ukatili; ukatili huyaangamiza maisha ya wakatili.
20 Hekima huita kwa sauti barabarani, hupaza sauti yake sokoni;
21 huita juu ya kuta, hutangaza penye malango ya mji:
22 “Enyi wajinga! Mpaka lini mtapenda kuwa wajinga? Mpaka lini wenye dharau watafurahia dharau zao, na wapumbavu kuchukia maarifa?
23 Sikilizeni maonyo yangu; nitawamiminia mawazo yangu, nitawajulisha maneno yangu.
24 Kwa kuwa nimewaita mkakataa kusikiliza, nimewapungia mkono mje mkakataa,
25 mkapuuza mashauri yangu yote, wala hamkuyajali maonyo yangu,
26 nami pia nitayachekelea maafa yenu, nitawadhihaki mnapokumbwa na hofu,
27 hofu itakapowakumba kama tufani, maafa yenu yatakapowavamia kama kimbunga, wakati udhia na dhiki vitakapowapata.
28 Hapo ndipo mtakaponiita lakini sitaitika; mtanitafuta kwa bidii lakini hamtanipata.
29 Kwa kuwa mliyachukia maarifa, wala hamkuchagua kumcha Mwenyezi-Mungu;
30 maadamu mlikataa shauri langu, mkayapuuza maonyo yangu yote;
31 basi, mtakula matunda ya mienendo yenu, mtavimbiwa kwa hila zenu wenyewe.
32 Maana wajinga hujiua kwa ukaidi wao, wapumbavu hujiangamiza kwa kujiamini kwao.
33 Lakini kila anisikilizaye atakaa salama, atatulia bila kuogopa mabaya.”
1 Mwanangu, ukiyakubali maneno yangu, na kuyathamini maagizo yangu;
2 ukitega sikio lako kusikiliza hekima, na kuuelekeza moyo wako upate ufahamu;
3 naam, ukiomba upewe busara, ukisihi upewe ufahamu;
4 ukiitafuta hekima kama fedha, na kuitaka kama hazina iliyofichika;
5 hapo utaelewa ni nini kumcha Mwenyezi-Mungu, utafahamu maana ya kumjua Mungu.
6 Maana Mwenyezi-Mungu huwapa watu hekima; kinywani mwake hutoka maarifa na ufahamu.
7 Huwawekea wanyofu akiba ya hekima safi, yeye ni ngao kwa watu waishio kwa uaminifu.
8 Huilinda mienendo ya watu watendao haki, na kuzihifadhi njia za waaminifu wake.
9 Ukinisikiliza utafahamu uadilifu na haki, utajua jambo lililo sawa na jema.
10 Maana hekima itaingia moyoni mwako, na maarifa yataipendeza nafsi yako.
11 Busara itakulinda, ufahamu utakuhifadhi;
12 vitakuepusha na njia ya uovu, na watu wa maneno mapotovu;
13 watu waziachao njia nyofu, ili kuziendea njia za giza;
14 watu wafurahiao kutenda maovu, na kupendezwa na upotovu wa maovu;
15 watu ambao mienendo yao imepotoka, nazo njia zao haziaminiki.
16 Hekima itakuwezesha kumkwepa mwanamke mwasherati, mwanamke malaya wa maneno matamu;
17 mwanamke amwachaye mwenzi wa ujana wake, na kulisahau agano la Mungu wake.
18 Nyumba yake yaelekea kuzimu, njia zake zinakwenda ahera.
19 Yeyote amwendeaye kamwe harudi, wala hairudii tena njia ya uhai.
20 Kwa hiyo utafuata mfano wa watu wema, na kuzingatia mienendo ya waadilifu.
21 Maana wanyofu wataipata nchi, na waaminifu watadumu ndani yake.
22 Lakini waovu wataondolewa nchini, na wenye hila watangolewa humo.
1 Mwanangu, usiyasahau mafundisho yangu, bali kwa moyo wako uzishike amri zangu.
2 Maana yatakupa wingi wa siku, maisha marefu na fanaka kwa wingi.
3 Utii na uaminifu visitengane nawe. Vifunge shingoni mwako; viandike moyoni mwako.
4 Hivyo utakubalika na kusifika, mbele ya Mungu na mbele ya wanadamu.
5 Mtumaini Mwenyezi-Mungu kwa moyo wako wote, wala usitegemee akili zako mwenyewe.
6 Umtambue Mungu katika kila ufanyalo, naye atazinyosha njia zako.
7 Usijione wewe mwenyewe kuwa mwenye hekima; mche Mwenyezi-Mungu na kujiepusha na uovu.
8 Hiyo itakuwa dawa mwilini mwako, na kiburudisho mifupani mwako.
9 Mheshimu Mwenyezi-Mungu kwa mali yako, na kwa malimbuko ya mazao yako yote.
10 Hapo ghala zako zitajaa nafaka, na mapipa yako yatafurika divai mpya.
11 Mwanangu, usidharau adhabu ya Mwenyezi-Mungu, wala usiudhike kwa maonyo yake;
12 maana Mwenyezi-Mungu humwonya yule ampendaye, kama baba amwonyavyo mwanawe mpenzi.
13 Heri mtu anayegundua hekima, mtu yule anayepata ufahamu.
14 Hekima ni bora kuliko fedha, ina faida kuliko dhahabu.
15 Hekima ina thamani kuliko johari, hamna unachotamani kiwezacho kulingana nayo.
16 Kwa mkono wake wa kulia Hekima atakupa maisha marefu; kwa mkono wake wa kushoto atakupa mali na heshima.
17 Njia zake ni za kupendeza, zote zaelekea kwenye amani.
18 Hekima ni mti wa uhai kwa wote wampatao; wana heri wote wanaoshikamana naye.
19 Kwa hekima Mwenyezi-Mungu aliweka misingi ya dunia, kwa akili aliziimarisha mbingu.
20 Kwa maarifa yake vilindi vilipasuka, na mawingu yakadondosha umande.
21 Mwanangu, zingatia hekima safi na busara; usiviache vitoweke machoni pako,
22 navyo vitakuwa uhai nafsini mwako, na pambo zuri shingoni mwako.
23 Hapo utaweza kwenda zako kwa usalama, wala mguu wako hautajikwaa.
24 Ukiketi hutakuwa na hofu; ukilala utapata usingizi mtamu.
25 Usiogope juu ya tishio la ghafla, wala shambulio kutoka kwa waovu,
26 Maana Mwenyezi-Mungu ndiye atakayekutegemeza; atakuepusha usije ukanaswa mtegoni.
27 Usimnyime mtu anayehitaji msaada, ikiwa unao uwezo wa kufanya hivyo.
28 Usimwambie jirani yako aende zake hadi kesho, hali wewe waweza kumpa anachohitaji leo.
29 Usipange maovu dhidi ya jirani yako, anayeishi karibu nawe bila wasiwasi.
30 Usigombane na mtu bila sababu ikiwa hajakudhuru kwa lolote.
31 Usimwonee wivu mtu mkatili, wala usiige mwenendo wake.
32 Maana waovu ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu; lakini yeye huwafanya marafiki zake wale walio wanyofu.
33 Mwenyezi-Mungu huapiza nyumba za waovu, lakini huyabariki makao ya waadilifu.
34 Yeye huwadharau wenye dharau, lakini huwafadhili wanyenyekevu.
35 Wenye hekima watavuna heshima, lakini wapumbavu watapata fedheha.
1 Wanangu, sikilizeni mwongozo wa baba yenu, tegeni sikio mpate kuwa na akili.
2 Maana ninawapa maagizo mema, msiyakatae mafundisho yangu.
3 Mimi pia nilikuwa mtoto mwenye baba, nilikuwa mpole, kipenzi cha mama yangu.
4 Baba yangu alinifundisha hiki: “Zingatia kwa moyo maneno yangu, shika amri zangu nawe utaishi.
5 Jipatie hekima, jipatie ufahamu; usisahau wala kupuuza maneno yangu.
6 Usimwache Hekima, naye atakutunza; umpende, naye atakulinda.
7 Jambo la msingi ni kujipatia hekima; toa vyote ulivyonavyo ujipatie akili.
8 Mthamini sana Hekima, naye atakutukuza; ukimshikilia atakupa heshima.
9 Atakuvika kilemba kizuri kichwani pako, atakupa taji maridadi.”
10 Mwanangu, sikia na kuyapokea maneno yangu, ili upate kuwa na miaka mingi ya kuishi.
11 Nimekufundisha njia ya hekima, nimekuongoza katika njia nyofu.
12 Ukitembea hatua zako hazitazuiwa, wala ukikimbia hutajikwaa.
13 Zingatia mafundisho ya Hekima na usimwache aponyoke, mshike kwa makini maana yeye ni uhai wako.
14 Usijiingize katika njia ya waovu, wala usifuate mwenendo wa watu wabaya.
15 Iepe njia hiyo wala usiikaribie; jiepushe nayo, uende zako.
16 Waovu kamwe hawalali wasipotenda uovu; hawapati usingizi wasipomkwaza mtu.
17 Maana uovu ndicho chakula chao, ukatili ndiyo divai yao.
18 Njia ya watu wema ni kama nuru ya alfajiri, ambayo hungaa zaidi na zaidi hata mchana kamili.
19 Lakini njia ya waovu ni kama giza nene, hawajui kinachowafanya wajikwae.
20 Mwanangu, sikiliza kwa makini maneno yangu, itegee sikio misemo yangu.
21 Usiyaache yatoweke machoni pako, yahifadhi ndani ya moyo wako.
22 Maana hayo ni uhai kwa mtu anayeyapata, ni dawa kwa mwili wake wote.
23 Linda moyo wako kwa uangalifu wote, maana humo zatoka chemchemi za uhai.
24 Tenga mbali nawe lugha potovu; wala midomo yako isitamke maneno madanganyifu.
25 Uyaelekeze macho yako mbele kwa ujasiri, mtazamo wako uwe mbele moja kwa moja.
26 Fikiria njia utakayochukua, na hatua zako zote zitakuwa kamili.
27 Usigeukie kulia wala kushoto; epusha mguu wako mbali na uovu.
1 Mwanangu, sikia hekima yangu, tega sikio usikilize elimu yangu.
2 Ndipo utakapoweza kuhifadhi busara, na midomo yako izingatie maarifa.
3 Mdomo wa mwanamke mpotovu ni mtamu kama asali, maneno yake ni laini kuliko mafuta;
4 lakini hatimaye ni mchungu kama pakanga, ni mkali kama upanga wenye makali kuwili.
5 Nyayo zake zaelekea chini mautini, hatua zake zaenda kuzimu.
6 Yeye haijali njia ya uhai, njia zake ni za kutangatanga, wala hajui.
7 Sasa enyi wanangu, nisikilizeni, wala msisahau maneno ya kinywa changu.
8 Iepushe njia yako mbali naye, wala usiukaribie mlango wa nyumba yake.
9 Usije ukawapa wengine heshima yako, na wakatili miaka yako;
10 wageni wasije wakajishibisha kwa mali yako, na jasho lako likaishia nyumbani kwa mgeni.
11 Mwishoni mwa maisha yako utaomboleza wakati mwili wako utakapoangamizwa.
12 Hapo utasema, “Jinsi gani nilivyochukia nidhamu, na kudharau maonyo moyoni mwangu!
13 Sikuisikiliza sauti ya waalimu wangu, wala kuwategea sikio wakufunzi wangu.
14 Sasa niko karibu kuangamia kabisa mbali na jumuiya ya watu.”
15 Mkeo ni kama kisima cha maji safi: Kunywa maji ya kisima chako mwenyewe.
16 Ya nini chemchemi zako zitawanywe mbali, na vijito vya maji barabarani?
17 Hiyo ni yako wewe mwenyewe, wala usiwashirikishe watu wengine.
18 Chemchemi yako na ibarikiwe, umfurahie mke uliyemwoa ukiwa kijana.
19 Ni mzuri kama ayala, apendeza kama paa. Mahaba yake yakufurahishe kila wakati, umezwe daima na pendo lake.
20 Mwanangu, ya nini kutekwa na mwanamke mwasherati? Ya nini kumkumbatia kifuani mwanamke mgeni?
21 Kumbuka njia za mtu zi wazi mbele ya Mwenyezi-Mungu; yeye anaona kila hatua anayochukua binadamu.
22 Mtu mwovu hunaswa kwa uovu wake mwenyewe; hukamatwa katika tanzi za dhambi yake mwenyewe.
23 Yeye hufa kwa utovu wa nidhamu, huangamia kwa sababu ya upuuzi wake mkuu.
1 Mwanangu, kama umejitolea kumdhamini jirani yako, ikiwa umetoa ahadi yako kwa ajili ya mtu huyo,
2 umejibana kwa maneno yako mwenyewe, umejinasa kwa ahadi uliyofanya.
3 Ujue kwamba uko chini ya mamlaka ya mwenzio, lakini mwanangu, ukitaka kujiokoa, basi fanya hivi: Mwendee mtu huyo mara moja umsihi akupe uhuru wako.
4 Jitahidi usiache macho yako yapate usingizi, wala kope za macho yako zisinzie.
5 Jiokoe kwa kujitoa katika mtego huo, mithili ya paa ama ndege amtorokavyo mwindaji.
6 Ewe mvivu! Hebu ukamchungulie sisimizi, fikiria namna yake ya kuishi ukapate hekima.
7 Sisimizi hana kiongozi, ofisa, wala mtawala;
8 lakini hujiwekea chakula wakati wa kiangazi, hujikusanyia akiba wakati wa mavuno.
9 Ewe mvivu, utalala hapo mpaka lini? Utaamka lini katika usingizi wako?
10 Wasema: “Acha nilale kidogo tu, acha nisinzie kidogo! Niache nikunje mikono nipumzike kidogo!”
11 Wakati huo umaskini utakuvamia kama mnyanganyi, ufukara utakufuata kama jambazi.
12 Mtu mwovu, mtu asiyefaa kitu, huzururazurura akisema maneno mapotovu.
13 Hukonyeza jicho kuwakosesha wengine, huparuza kwa nyayo, na kuashiria watu kwa vidole.
14 Akiwa amejaa ulaghai moyoni hutunga maovu, huzusha ugomvi kila mahali.
15 Kutokana na hayo maafa yatamvamia ghafla, ghafla atadhurika vibaya asiweze kupona tena.
16 Kuna vitu sita anavyochukia Mwenyezi-Mungu; naam, vitu saba ambavyo ni chukizo kwake:
17 Macho ya kiburi, ulimi mdanganyifu, mikono inayoua wasio na hatia,
18 moyo unaopanga mipango miovu, miguu iliyo mbioni kutenda maovu,
19 shahidi wa uongo abubujikaye uongo, na mtu achocheaye fitina kati ya ndugu.
20 Mwanangu, shika maagizo ya baba yako, wala usisahau mafundisho ya mama yako;
21 yaweke daima moyoni mwako, yafunge shingoni mwako.
22 Yatakuongoza njiani mwako, yatakulinda wakati ulalapo, yatakushauri uwapo macho mchana.
23 Maana amri hiyo ni taa, na sheria hiyo ni mwanga. Maonyo hayo na nidhamu yatuweka njiani mwa uhai.
24 Yatakulinda mbali na mwanamke mbaya, yatakuepusha na maneno matamu ya mwanamke mgeni.
25 Usimtamani mwanamke huyo kwa uzuri wake, wala usikubali kunaswa kwa kope za macho yake.
26 Mtu hupoteza kipande cha mkate kwa malaya, lakini kwa mke wa mtu mwingine utapoteza uhai wako wote.
27 Je, waweza kuweka moto kifuani na nguo zako zisiungue?
28 Je, waweza kukanyaga makaa ya moto na nyayo zako zisiungue?
29 Ndivyo alivyo mwanamume alalaye na mke wa mwenzake; yeyote anayemgusa mwanamke huyo hataacha kuadhibiwa.
30 Watu hawambezi sana mtu akiiba kwa sababu ya njaa;
31 lakini akipatikana lazima alipe mara saba; tena atatoa mali yote aliyo nayo.
32 Mwanamume anayezini na mke wa mtu hana akili kabisa; huyo hujiangamiza yeye mwenyewe.
33 Atapata majeraha na madharau; fedheha atakayopata haitamtoka.
34 Maana wivu wa mume humfanya kuwa mkali kabisa; wakati atakapolipiza kisasi hana cha kuhurumia.
35 Hatakubali fidia yoyote; wala kutulizwa na zawadi zako nyingi.
1 Mwanangu, yashike maneno yangu, zihifadhi kwako amri zangu.
2 Zifuate amri zangu nawe utaishi; yalinde mafundisho yangu kama mboni ya jicho lako.
3 Yafunge vidoleni mwako; yaandike moyoni mwako.
4 Iambie Hekima: “Wewe ni dada yangu”, na Busara “Wewe ni rafiki yangu”.
5 Vitakulinda mbali na mwanamke mbaya, vitakuepusha na maneno matamu ya mwanamke mgeni.
6 Siku moja dirishani mwa nyumba yangu, nilichungulia nje kupitia viunzi vya dirisha,
7 nikawaona vijana wengi wajinga, na mmoja hasa aliyekuwa mpumbavu.
8 Huyo alikuwa akitembea kwenye barabara ile, karibu na kona alikoishi mwanamke fulani. Basi akashika njia iendayo nyumbani kwa mwanamke huyo.
9 Ilikuwa yapata wakati wa jioni, giza na usiku vilikuwa vimeanza kuingia.
10 Punde kijana akakutana na huyo mwanamke; amevalia kama malaya, ana mipango yake.
11 Alikuwa mwanamke wa makelele na mkaidi; miguu yake haitulii nyumbani:
12 Mara barabarani, mara sokoni, katika kila kona ya njia hakosekani akivizia.
13 Alimkumbatia kijana huyo na kumbusu, na kwa maneno matamu, akamwambia:
14 “Ilinilazimu kutoa tambiko zangu; leo hii nimekamilisha nadhiri yangu.
15 Ndio maana nimetoka ili nikulaki, nimekutafuta kwa hamu nikakupata.
16 Nimetandika kitanda changu vizuri, kwa shuka za rangi za kitani kutoka Misri.
17 Nimekitia manukato, manemane, udi na mdalasini.
18 Njoo tulale pamoja mpaka asubuhi; njoo tujifurahishe kwa mahaba.
19 Mume wangu hayumo nyumbani, amekwenda safari ya mbali.
20 Amechukua bunda la fedha; hatarejea nyumbani karibuni.”
21 Alimshawishi kwa maneno mengi ya kubembeleza; kijana akashawishika kwa maneno yake matamu.
22 Hapo akamfuata huyo mwanamke moja kwa moja, kama ng'ombe aendaye machinjioni, kama paa arukiaye mtegoni.
23 Hakutambua kwamba hiyo itamgharimu maisha yake, mpaka alipojikuta amekuwa kama amechomwa mshale moyoni, amekuwa kama ndege aliyenaswa wavuni.
24 Sasa wanangu, nisikilizeni; yategeeni sikio maneno ya kinywa changu.
25 Msikubali kuongozwa na mwanamke kama huyo, wala msipitepite katika mapito yake.
26 Maana amewaangusha wanaume wengi; ni wengi mno hao aliowachinja.
27 Nyumba yake ni njia ya kwenda kuzimu, ni mahali pa kuteremkia mautini.
1 Sikilizeni! Hekima anaita! Busara anapaza sauti yake!
2 Juu penye mwinuko karibu na njia, katika njia panda ndipo alipojiweka.
3 Karibu na malango ya kuingilia mjini, mahali wanapoingia watu anaita kwa sauti:
4 “Enyi watu wote, nawaita nyinyi! Wito wangu ni kwa ajili ya binadamu.
5 Enyi wajinga, jifunzeni kuwa na akili; sikilizeni kwa makini enyi wapumbavu.
6 Sikilizeni maana nitakachosema ni jambo muhimu; midomoni mwangu mtatoka mambo ya adili.
7 Kinywa changu kitatamka kweli tupu; uovu ni chukizo midomoni mwangu.
8 Kinywa changu kitatamka maneno ya kweli, udanganyifu ni haramu midomoni mwangu.
9 Kwa mtu mwelewa kila kitu ni wazi, kwa mwenye maarifa yote ni sawa.
10 Chagua mafundisho yangu badala ya fedha; na maarifa badala ya dhahabu safi.
11 “Mimi Hekima nina thamani kuliko johari; chochote unachotamani hakiwezi kulingana nami.
12 Mimi Hekima ninao ujuzi; ninayo maarifa na busara.
13 Kumcha Mwenyezi-Mungu ni kuchukia uovu. Nachukia kiburi, majivuno na maisha mabaya; nachukia na lugha mbaya.
14 Nina uwezo wa kushauri na nina hekima. Ninao ujuzi na nina nguvu.
15 Kwa msaada wangu wafalme hutawala, watawala huamua yaliyo ya haki.
16 Kwa msaada wangu viongozi hutawala, wakuu na watawala halali.
17 Nawapenda wale wanaonipenda; wanaonitafuta kwa bidii hunipata.
18 Utajiri na heshima viko kwangu, mali ya kudumu na fanaka.
19 Matunda yangu ni mazuri kuliko dhahabu safi, faida yangu yashinda ile ya fedha bora.
20 Natembea katika njia ya uadilifu; ninafuata njia za haki.
21 Mimi huwatajirisha wanaonipenda, huzijaza tele hazina zao wanipendao.
22 “Mwenyezi-Mungu aliniumba mwanzoni mwa kazi yake, zama za zama kabla ya kuwako kitu chochote.
23 Nilifanywa mwanzoni mwa nyakati, nilikuwako kabla ya dunia kuanza.
24 Nilizaliwa kabla ya vilindi vya bahari, kabla ya chemchemi zibubujikazo maji.
25 Kabla ya milima haijaumbwa, na vilima kusimamishwa mahali pake, mimi nilikuwako tayari.
26 Kabla Mungu hajaumba dunia na mashamba yake, wala chembe za kwanza za mavumbi ya dunia.
27 Nilikuwako wakati alipoziweka mbingu, wakati alipopiga duara juu ya bahari;
28 wakati alipoimarisha mawingu mbinguni, alipozifanya imara chemchemi za bahari;
29 wakati alipoiwekea bahari mpaka wake, maji yake yasije yakavunja amri yake; wakati alipoiweka misingi ya dunia.
30 Nilikuwa pamoja naye kama fundi stadi, nilikuwa furaha yake kila siku, nikishangilia mbele yake daima,
31 nikifurahia dunia na wakazi wake, na kupendezwa kuwa pamoja na wanadamu.
32 “Sasa basi wanangu, nisikilizeni: Heri wale wanaofuata njia zangu.
33 Sikilizeni mafunzo mpate hekima, wala msiyakatae.
34 Heri mtu anayenisikiliza, anayekaa kila siku mlangoni pangu, anayekesha karibu na milango yangu.
35 Anayenipata mimi amepata uhai, amepata upendeleo kwa Mwenyezi-Mungu.
36 Asiyenipata anajidhuru mwenyewe; wote wanaonichukia wanapenda kifo.”
1 Hekima amejenga nyumba yake, nyumba yenye nguzo saba.
2 Amechinja wanyama wa karamu, divai yake ameitayarisha, ametandika meza yake.
3 Amewatuma watumishi wake wa kike mjini, waite watu kutoka kwenye vilele vya miinuko:
4 “Yeyote aliye mjinga na aje hapa!” Na yeyote aliye mpumbavu humwambia:
5 “Njoo ukale chakula, na unywe divai niliyotengeneza.
6 Achana na ujinga upate kuishi; fuata njia ya akili.”
7 Anayemkosoa mwenye dharau hupata matusi, amkaripiaye mwovu huishia kwa kuumizwa.
8 Usimwonye mwenye dharau maana atakuchukia; mwonye mwenye hekima naye atakupenda.
9 Mfunze mwenye hekima naye atazidi kuwa na hekima; mfundishe mwadilifu naye atazidi kuelimika.
10 Kumcha Mwenyezi-Mungu ni msingi wa hekima; na kumjua yule Mtakatifu ni kupata akili.
11 Kwa msaada wangu mimi Hekima siku zako zitaongezwa; utaongezewa miaka mingi maishani mwako.
12 Kama una hekima, itakufaa wewe mwenyewe; kama ukiidharau, mwenyewe utapata hasara.
13 Mwanamke mpumbavu ana kelele, hajui kitu wala hana haya.
14 Hukaa kitako mlangoni mwa nyumba yake, huweka kiti chake mahali pa juu mjini,
15 na kuwaita watu wapitao njiani, watu wanaokwenda kwenye shughuli zao:
16 “Yeyote aliye mjinga na aje hapa!” Na yeyote aliye mpumbavu humwambia:
17 “Maji ya wizi ni matamu sana; mkate unaoliwa kwa siri ni mzuri sana.”
18 Lakini mjinga hajui kwamba humo mna wafu, wageni wa mwanamke huyo wamo chini Kuzimu.
1 Hizi ni methali za Solomoni: Mtoto mwenye hekima ni furaha ya baba yake; lakini mtoto mpumbavu ni huzuni ya mama yake.
2 Mali iliyopatikana kwa njia mbaya haifai, lakini uadilifu huokoa mtu kutoka kifoni.
3 Mwenyezi-Mungu hawaachi waadilifu wapate njaa, lakini huzipinga tamaa za waovu.
4 Uvivu husababisha umaskini, lakini mkono wa mtu wa bidii hutajirisha.
5 Mwenye busara hukusanya wakati wa mavuno, kulala wakati wa kuvuna ni aibu.
6 Mwadilifu hujiletea baraka yeye mwenyewe, lakini kinywa cha mwovu kimesongwa na ukatili.
7 Waadilifu hukumbukwa kwa baraka, lakini waovu watasahaulika kabisa.
8 Mwenye hekima moyoni hutii amri, lakini mpumbavu aropokaye ataangamia.
9 Aishiye kwa unyofu huishi salama, apotoshaye maisha yake atagunduliwa.
10 Akonyezaye kwa nia mbaya huzusha taabu, lakini aonyaye kwa ujasiri huleta amani.
11 Kinywa cha mwadilifu ni chemchemi ya uhai, lakini kinywa cha mwovu kimesongwa na ukatili.
12 Chuki huzusha ugomvi, lakini upendo hufunika makosa yote.
13 Kinywani mwa mwenye ufahamu mna hekima, lakini wasio na akili watachapwa viboko mgongoni.
14 Wenye hekima huhifadhi maarifa, lakini kuropoka kwa mpumbavu huleta maangamizi haraka.
15 Mali ya tajiri ndio ngome yake, umaskini wa maskini humletea maangamizi.
16 Tuzo la mtu mwema ni uhai, lakini mwovu huishia katika dhambi.
17 Anayekubali maonyo anaelekea kwenye uhai, lakini anayekataa kuonywa amepotoka.
18 Amchukiaye mwingine kwa siri ni mnafiki, anayemsingizia mtu ni mpumbavu.
19 Penye maneno mengi hapakosekani makosa, lakini aneyeuzuia ulimi wake ana busara.
20 Maneno ya mwadilifu ni kama fedha bora; akili ya mtu mwovu haina thamani yoyote.
21 Maneno ya mwadilifu huwafaa watu wengi, lakini wapumbavu hufa kwa kukosa akili.
22 Baraka za Mwenyezi-Mungu ndizo ziletazo fanaka, juhudi za mtu haziongezi hapo chochote.
23 Kwa mpumbavu kutenda maovu ni kama mchezo; lakini watu wenye busara hufurahia hekima.
24 Anachoogopa mtu mwovu ndicho kitakachompata, lakini anachotamani mwadilifu ndicho atakachopewa.
25 Kimbunga hupita na mwovu hutoweka, lakini mwadilifu huimarishwa milele.
26 Kama ilivyo siki kwa meno au moshi machoni, ndivyo alivyo mvivu kwa bwana wake.
27 Kumcha Mwenyezi-Mungu hurefusha maisha, lakini miaka ya waovu itakuwa mifupi.
28 Tumaini la mwadilifu huishia kwenye furaha, lakini tazamio la mwovu huishia patupu.
29 Mwenyezi-Mungu ni ngome ya wanyofu, lakini watendao maovu atawaangamiza.
30 Waadilifu kamwe hawataondolewa nchini, lakini waovu hawatakaa katika nchi.
31 Kinywa cha mwadilifu hutoa mambo ya hekima, lakini ulimi wa mtu mbaya utakatiliwa mbali.
32 Midomo ya waadilifu hujua yanayokubalika, lakini vinywa vya waovu husema tu maovu.
1 Mizani ya udanganyifu ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu, lakini matumizi ya kipimo halali ni furaha kwake.
2 Kiburi huandamana na fedheha, lakini kwa watu wanyenyekevu mna hekima.
3 Unyofu wa watu wema huwaongoza, upotovu wa wenye hila huwaangamiza.
4 Utajiri haufai kitu siku ya ghadhabu, lakini uadilifu huokoa kutoka kifo.
5 Uadilifu wa watu wanyofu huinyosha njia yao, lakini waovu huanguka kwa uovu wao wenyewe.
6 Uadilifu wa wanyofu huwaokoa na hatari, lakini wafitini hunaswa kwa tamaa zao wenyewe.
7 Mwovu akifa tumaini lake nalo hutoweka; tazamio la asiyemcha Mungu huishia patupu.
8 Mtu mnyofu huokolewa katika shida, na mwovu huingia humo badala yake.
9 Asiyemcha Mungu huangamiza wengine kwa mdomo wake, lakini mwadilifu huokolewa kwa maarifa yake.
10 Waadilifu wakipata fanaka mji hushangilia, na waovu wakiangamia watu hupiga vigelegele.
11 Mji hufanikishwa kwa baraka za wanyofu, lakini huangamizwa kwa mdomo wa waovu.
12 Anayemdharau jirani yake hana akili, mtu mwenye busara hukaa kimya.
13 Apitapitaye akichongea hutoa siri, lakini anayeaminika rohoni huficha siri.
14 Pasipo na uongozi taifa huanguka, penye washauri wengi pana usalama.
15 Anayemdhamini mgeni atakuja juta, lakini anayechukia mambo ya dhamana yu salama.
16 Mwanamke mwema huheshimiwa, mwanamume mwenye bidii hutajirika.
17 Mtu mkarimu hufaidika yeye mwenyewe, lakini mtu mkatili hujiumiza mwenyewe.
18 Faida anayopata mwovu ni ya uongo, lakini atendaye mema hakika atapata faida ya kweli.
19 Mtu anayepania kuwa mwadilifu ataishi, lakini anayechagua kutenda maovu atakufa.
20 Wenye nia mbaya ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu, lakini wenye mwenendo mwema ni furaha yake.
21 Hakika mwovu hataepa kuadhibiwa, lakini waadilifu wataokolewa.
22 Mwanamke mzuri asiye na akili, ni kama pete ya dhahabu puani mwa nguruwe.
23 Matazamio ya waadilifu yana matokeo mema; tamaa za waovu huishia katika ghadhabu.
24 Atoaye kwa ukarimu huzidi kutajirika; lakini bahili huzidi kudidimia katika umaskini.
25 Mtu mkarimu atafanikishwa, amnyweshaye mwingine maji naye atanyweshwa.
26 Watu humlaani afichaye nafaka, lakini humtakia baraka mwenye kuiuza.
27 Atafutaye kutenda mema hupata fadhili, lakini atafutaye kutenda maovu atapatwa na maovu.
28 Anayetegemea mali zake ataanguka, lakini mwadilifu atastawi kama jani bichi.
29 Anayeivunja nyumba yake ataambua upepo. Mpumbavu atakuwa mtumwa wa wenye hekima.
30 Matendo ya mwadilifu huleta uhai, lakini uhalifu huuondoa uhai.
31 Ikiwa mwadilifu hupata tuzo hapa duniani, hakika mwovu na mwenye dhambi atapatilizwa.
1 Apendaye nidhamu hupenda maarifa, bali asiyependa kuonywa ni mjinga.
2 Mtu mwema hufadhiliwa na Mwenyezi-Mungu, lakini mwenye nia mbaya hulaaniwa na Mungu.
3 Mtu hawi imara kwa kutenda maovu, lakini hakuna kiwezacho kumngoa mtu mwadilifu.
4 Mke mwema ni taji ya fahari kwa mumewe; amwaibishaye mumewe ni kama kidonda mifupani mwake.
5 Mawazo ya mwadilifu ni ya haki; mashauri ya mwovu ni ya udanganyifu.
6 Maneno ya waovu lengo lake ni kuua, lakini maneno ya waadilifu huwaokoa wanaotishwa.
7 Waovu huangamizwa na kutoweka kabisa, lakini jamaa ya waadilifu hudumishwa.
8 Mtu husifiwa kadiri ya hekima yake, lakini mtu wa fikira mbaya hudharauliwa.
9 Afadhali mtu wa chini anayejitegemea, kuliko ajitakiaye makuu na kukosa chakula.
10 Mtu mwadilifu huwajali wanyama wake, lakini huruma ya mwovu ni ukatili.
11 Mkulima mwenye bidii ana chakula tele, lakini afuataye mambo yasiyofaa hana akili.
12 Waovu hutamani faida isiyo halali, lakini mtu mwadilifu husimama imara.
13 Mtu mwovu hunaswa kwa uongo wake mwenyewe, lakini mwadilifu hutoka katika taabu.
14 Mtu hufanikiwa kutokana na maneno yake kama apatavyo matokeo ya kazi za mikono yake.
15 Mpumbavu huiona njia yake kuwa sawa, lakini mwenye hekima husikiliza shauri.
16 Udhia wa mpumbavu hujulikana mara, lakini mwerevu huyapuuza matukano.
17 Msema kweli hutoa ushahidi wa kweli, lakini shahidi wa uongo hutamka udanganyifu.
18 Maneno ya ovyo hujeruhi kama upanga, lakini asemayo mwenye hekima huponesha kidonda.
19 Ukweli hudumu milele, lakini uongo ni wa kitambo tu.
20 Wanaopanga maovu wamejaa udanganyifu moyoni, lakini wanaonuia mema hupata furaha.
21 Waadilifu hawapatwi na jambo lolote baya, lakini waovu wamejaa dhiki.
22 Midomo isemayo uongo ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu, lakini watu waaminifu ni furaha yake.
23 Mwenye busara huficha maarifa yake, lakini wapumbavu hutangaza upumbavu wao.
24 Kuwa na bidii kutampa mtu cheo, lakini uvivu utamfanya mtumwa.
25 Wasiwasi moyoni humkosesha mtu raha, lakini neno jema humchangamsha.
26 Mtu mwadilifu huuepa uovu, lakini njia ya waovu huwapotosha wenyewe.
27 Mwindaji mvivu hatapata anachowinda, lakini mwenye bidii atafanikiwa.
28 Uadilifu ni njia ya uhai, lakini uovu huongoza katika mauti.
1 Mtoto mwenye hekima husikia maagizo ya baba yake, lakini mwenye dharau hasikilizi maonyo.
2 Mtu mwema hupata mema kutokana na maneno yake, lakini wadanganyifu huishi kwa ukatili.
3 Achungaye mdomo wake huyahifadhi maisha yake, anayeropoka ovyo hujiletea maangamizi.
4 Mvivu hutamani lakini hapati chochote, hali mwenye bidii hujaliwa riziki kwa wingi.
5 Mwadilifu huuchukia uongo, lakini mwovu hutenda kwa aibu na fedheha.
6 Uadilifu huwalinda wenye mwenendo mnyofu, lakini dhambi huwaangusha waovu.
7 Baadhi hujidai kuwa matajiri kumbe hawana kitu; wengine hujiona kuwa maskini hali wana mali tele.
8 Fidia ya mtu ni mali yake, lakini maskini hana cha kutishwa.
9 Mwadilifu hungaa kama taa iwakayo vizuri, lakini waovu ni kama taa inayozimika.
10 Kiburi husababisha tu ugomvi, lakini kwa wanaokubali shauri jema mna hekima.
11 Mali ya harakaharaka hutoweka, lakini akusanyaye kidogokidogo ataiongeza.
12 Tumaini la kungojangoja huumiza moyo, lakini tazamio linalotimia ni mti wa uhai.
13 Anayedharau mawaidha anajiletea maangamizi, lakini anayetii amri atapewa tuzo.
14 Mafundisho ya wenye hekima ni chemchemi ya uhai; humwezesha mtu kuiepa mitego ya kifo.
15 Kuwa na akili huleta fadhili, lakini njia ya waovu ni ya taabu
16 Mwenye busara hutenda kila kitu kwa akili, lakini mpumbavu hutembeza upumbavu wake.
17 Mjumbe mbaya huwatumbukiza watu taabuni, lakini mjumbe mwaminifu huleta nafuu.
18 Umaskini na fedheha humpata asiyejali mafundisho, lakini mwenye kusikia maonyo huheshimiwa.
19 Inafurahisha upatapo kile unachotaka, kwa hiyo wapumbavu huchukia kuepa uovu.
20 Anayeandamana na wenye hekima hupata hekima, lakini anayejiunga na wapumbavu atapata madhara.
21 Watendao dhambi huandamwa na balaa, lakini waadilifu watatuzwa mema.
22 Mtu mwema huwaachia urithi uzao wake, lakini mali ya mwenye dhambi imerundikiwa waadilifu.
23 Shamba la maskini hutoa mazao mengi, lakini bila haki hunyakuliwa.
24 Asiyemwadhibu mtoto wake hampendi; lakini ampendaye mwanawe humrudi mapema.
25 Mwadilifu anacho chakula cha kumtosheleza, lakini tumbo la waovu hutaabika kwa njaa.
1 Mwanamke mwenye hekima huijenga nyumba yake, lakini mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe.
2 Mwenye mwenendo mnyofu humcha Mwenyezi-Mungu, lakini mpotovu humdharau Mungu.
3 Mpumbavu hujiadhibu mwenyewe kwa kuropoka kwake, lakini mwenye hekima hulindwa na maneno yake.
4 Bila ng'ombe wa kulima ghala za mtu ni tupu, mavuno mengi hupatikana kwa nguvu ya ng'ombe wa kulima.
5 Shahidi mwaminifu hasemi uongo, lakini asiyeaminika hububujika uongo.
6 Mwenye dharau hutafuta hekima bure, lakini mwenye busara hupata maarifa kwa urahisi.
7 Ondoka mahali alipo mpumbavu, maana hapo alipo hamna maneno ya hekima.
8 Hekima ya mwenye busara humwonesha njia yake, lakini upumbavu wa wapumbavu huwadanganya wenyewe.
9 Wapumbavu huchekelea dhambi, bali wanyofu hupata fadhili kwa Mungu.
10 Moyo waujua uchungu wake wenyewe, wala mgeni hawezi kushiriki furaha yake.
11 Nyumba ya mtu mwovu itabomolewa, lakini hema ya wanyofu itaimarishwa.
12 Njia unayodhani kuwa ni sawa, mwishoni yaweza kukuongoza kwenye kifo.
13 Huzuni yaweza kufichika katika kicheko; baada ya furaha huja majonzi.
14 Mtu mpotovu atavuna matunda ya mwenendo wake, naye mtu mwema atapata tuzo la matendo yake.
15 Mjinga huamini kila kitu anachoambiwa, lakini mwenye busara huwa na tahadhari.
16 Mwenye hekima ni mwangalifu na huepa uovu, lakini mpumbavu hajizuii wala hana uangalifu.
17 Mwenye kuwaka hasira haraka hutenda kipumbavu, lakini mwenye busara ana uvumilivu.
18 Wajinga hurithi upumbavu, lakini wenye busara hutuzwa taji ya maarifa.
19 Waovu watapiga magoti mbele ya watu wema, watu wabaya mlangoni mwa waadilifu.
20 Maskini huchukiwa hata na jirani yake, lakini tajiri ana marafiki wengi.
21 Anayemdharau jirani yake ni mwenye dhambi, bali ana heri aliye mwema kwa maskini.
22 Anayepanga maovu kweli anakosea! Wanaopanga kutenda mema hufadhiliwa.
23 Bidii katika kila kazi huleta faida, lakini maneno matupu huleta umaskini.
24 Mali ni taji ya fahari ya wenye hekima, lakini ujinga ni shada la wapumbavu.
25 Shahidi wa kweli huokoa maisha, lakini msema uongo ni msaliti.
26 Amchaye Mwenyezi-Mungu ana tumaini imara, na watoto wake watapata kimbilio salama.
27 Kumcha Mwenyezi-Mungu ni chemchemi ya uhai; humwezesha mtu kuepa mitego ya kifo.
28 Fahari ya mfalme ni wingi wa watu wake, lakini bila watu mtawala huangamia.
29 Mtu asiye mwepesi wa hasira ana busara kubwa, lakini akasirikaye upesi hukuza upumbavu.
30 Amani rohoni humpa mtu afya, lakini tamaa huozesha mifupa.
31 Anayemdhulumu maskini anamtukana Muumba wake, lakini amwoneaye huruma mhitaji anamtukuza Mungu.
32 Mwovu huangamizwa kwa matendo yake maovu, lakini mwadilifu hupata usalama kwa unyofu wake.
33 Hekima imo moyoni mwa mtu mwenye busara; haipatikani kamwe mioyoni mwa wapumbavu.
34 Uadilifu hukuza taifa, lakini dhambi ni balaa kwa taifa lolote.
35 Mfalme humfadhili mtumishi atendaye kwa hekima, lakini hasira yake huwakumba watendao yasiyofaa.
1 Kujibu kwa upole hutuliza hasira, lakini neno kali huchochea hasira.
2 Ulimi wa mwenye hekima hueneza maarifa, lakini watu wapumbavu hububujika upuuzi.
3 Macho ya Mwenyezi-Mungu huona kila kitu, humchunguza mtu mwema na mtu mbaya.
4 Ulimi mpole ni chanzo cha uhai, lakini uovu wake huvunja moyo.
5 Mpumbavu hudharau mafundisho ya baba yake, lakini anayekubali maonyo ana busara.
6 Nyumbani mwa mwadilifu mna wingi wa mali, lakini mapato ya waovu huishia na balaa.
7 Mdomo wa mwenye hekima hueneza maarifa, lakini sivyo ilivyo mioyo ya wapumbavu.
8 Sadaka ya waovu ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu, lakini sala ya wanyofu humfurahisha Mungu.
9 Mwenendo wa waovu ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu, lakini Mungu huwapenda wale wafuatao mambo adili.
10 Adhabu kali ipo kwa wanaoacha mwenendo mwema; yeyote achukiaye kuonywa atakufa.
11 Ikiwa Mwenyezi-Mungu ajua yaliyo Kuzimu na Abadoni, mawazo ya binadamu yatawezaje kujificha mbele yake?
12 Mwenye madharau hapendi kuonywa, hatafuti kamwe maoni ya wenye busara.
13 Moyo wa furaha hungarisha uso, lakini uchungu huvunja moyo.
14 Mwenye busara hutafuta maarifa, lakini wapumbavu hujilisha upuuzi.
15 Kwa mnyonge kila siku ni mbaya, lakini kwa mwenye moyo mchangamfu ni sikukuu.
16 Afadhali kuwa na kidogo na kumcha Mwenyezi-Mungu, kuliko kuwa na mali nyingi pamoja na taabu.
17 Afadhali mlo wa jioni wa mchicha na upendo, kuliko karamu ya nyama nono pamoja na chuki.
18 Mtu wa hasira mbaya husababisha ugomvi, lakini asiye mwepesi wa hasira hutuliza ugomvi.
19 Njia ya mvivu imesambaa miiba, njia ya mwaminifu ni wazi kama barabara kuu.
20 Mtoto mwenye hekima humfurahisha baba yake, lakini mpumbavu humdharau mama yake.
21 Upumbavu ni furaha kwa mtu asiye na akili, lakini mwenye busara huchagua njia iliyo sawa.
22 Mipango huharibika kwa kukosa shauri, lakini kwa washauri wengi, hufaulu.
23 Kutoa jibu sahihi hufurahisha; neno lifaalo kwa wakati wake ni jema mno!
24 Njia ya mwenye hekima huelekea juu kwenye uhai, ili aepe kuingia chini kuzimu.
25 Mwenyezi-Mungu huyabomoa makao ya wenye kiburi, lakini huilinda mipaka ya makao ya mjane.
26 Mawazo ya mwovu ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu, bali maneno mema humfurahisha.
27 Anayetamani faida ya ulanguzi anaitaabisha jamaa yake, lakini achukiaye hongo ataishi.
28 Moyo wa mwadilifu hufikiri kabla ya kujibu, lakini kinywa cha mwovu hububujika uovu.
29 Mwenyezi-Mungu yuko mbali na watu waovu, lakini yu karibu na watu wema kuwasikiliza.
30 Macho ya huruma hufurahisha moyo, habari njema huuburudisha mwili.
31 Mtu ambaye husikiliza maonyo mema, anayo nafasi yake miongoni mwa wenye hekima.
32 Anayekataa kufundishwa anajidharau mwenyewe, bali anayekubali maonyo hupata busara.
33 Kumcha Mwenyezi-Mungu ni shule ya hekima; kabla ya kuheshimika ni lazima kuwa mnyenyekevu.
1 Binadamu hupanga mipango yake, lakini kauli ya mwisho ni yake Mwenyezi-Mungu.
2 Matendo ya mtu huonekana kwake kuwa sawa, lakini Mwenyezi-Mungu hupima nia ya mtu.
3 Mwekee Mwenyezi-Mungu kazi yako, nayo mipango yako itafanikiwa.
4 Mwenyezi-Mungu ameumba kila kitu kwa kusudi lake; hata waovu kwa ajili ya siku ya maangamizi.
5 Kila mwenye kiburi ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu; hakika mtu wa namna hiyo hataacha kuadhibiwa.
6 Kwa utii na uaminifu mtu huondolewa dhambi, kwa kumcha Mwenyezi-Mungu huepuka uovu.
7 Mwenyezi-Mungu akipendezwa na mwenendo wa mtu, huwageuza hata adui zake kuwa marafiki.
8 Afadhali mali kidogo kwa uadilifu, kuliko mapato mengi kwa udhalimu.
9 Mtu aweza kufanya mipango yake, lakini Mwenyezi-Mungu huongoza hatua zake.
10 Mfalme huamua kwa maongozi ya Mungu; anapotoa hukumu hakosei.
11 Mwenyezi-Mungu hutaka kipimo na mizani halali; mawe yote mfukoni ya kupimia ni kazi yake.
12 Ni chukizo kubwa wafalme kutenda uovu, maana msingi wa mamlaka yao ni haki.
13 Mfalme hupendelea mtu asemaye kwa unyofu; humpenda mtu asemaye ukweli.
14 Hasira ya mfalme ni kama mjumbe wa kifo; mtu mwenye busara ataituliza.
15 Uso wa mfalme ukingaa kuna uhai; wema wake ni kama wingu la masika.
16 Kupata hekima ni bora kuliko dhahabu; kupata akili ni chaguo bora kuliko fedha.
17 Njia ya wanyofu huepukana na uovu; anayechunga njia yake huhifadhi maisha yake.
18 Kiburi hutangulia maangamizi; majivuno hutangulia maanguko.
19 Afadhali kuwa mnyenyekevu na kuwa maskini, kuliko kugawana nyara na wenye kiburi.
20 Anayezingatia mafundisho atafanikiwa; heri mtu yule anayemtumainia Mwenyezi-Mungu.
21 Mwenye hekima moyoni huitwa mwenye akili; neno la kupendeza huwavutia watu.
22 Hekima ni chemchemi ya uhai kwake aliye nayo, bali upumbavu ni adhabu ya wapumbavu.
23 Moyo wa mwenye hekima humwezesha kusema kwa busara; huyafanya maneno yake yawe ya kuvutia.
24 Maneno mazuri ni kama asali; ni matamu rohoni na yenye kuupa mwili afya.
25 Mtu aweza kuona njia yake kuwa sawa, lakini mwishowe humwongoza kwenye kifo.
26 Hamu ya chakula humhimiza mfanyakazi, maana njaa yake humsukuma aendelee.
27 Mtu mwovu hupanga uovu; maneno yake ni kama moto mkali.
28 Mtu mpotovu hueneza ugomvi, mfitini hutenganisha marafiki.
29 Mtu mkatili humshawishi jirani yake; humwongoza katika njia mbaya.
30 Anayekonyeza jicho kwa hila amepanga maovu; anayekaza midomo amekwisha nuia mabaya.
31 Kuwa na mvi za uzee ni taji la utukufu; hupatikana kwa maisha ya uadilifu.
32 Asiye mwepesi wa hasira ni bora kuliko mwenye nguvu; aitawalaye nafsi yake ni bora kuliko autekaye mji.
33 Kura hupigwa kujua yatakayotukia, lakini uamuzi ni wake Mwenyezi-Mungu.
1 Afadhali mkate mkavu kwa amani, kuliko karamu katika nyumba ya ugomvi.
2 Mtumwa mwenye busara atachukua nafasi ya mwana mpumbavu, atapata sehemu ya urithi wa jamaa hiyo.
3 Ubora wa dhahabu ama fedha hupimwa kwa moto, lakini Mwenyezi-Mungu ndiye apimaye mioyo ya watu.
4 Mtenda maovu husikiliza maneno mabaya, mwongo hutegea sikio ulimi mdanganyifu.
5 Anayemdhihaki maskini anamtukana Muumba wake; anayefurahia maafa hatakosa kuadhibiwa.
6 Wazee huwaonea fahari wajukuu zao; watoto huwaonea fahari wazazi wao.
7 Maneno mazuri si kawaida kinywani mwa mpumbavu, sembuse maneno ya uongo kinywani mwa kiongozi!
8 Kwa mhongaji, hongo ni kama hirizi; kila afanyacho hufanikiwa.
9 Anayesamehe makosa hujenga urafiki, lakini anayekumbusha makosa hutenga rafiki.
10 Onyo kwa mwenye busara lina maana, kuliko mapigo mia kwa mpumbavu.
11 Afanyalo mtu mwovu ni kuasi tu; mjumbe mkatili atatumwa dhidi yake.
12 Afadhali kukutana na dubu jike aliyenyanganywa watoto wake, kuliko kukutana na mpumbavu katika upumbavu wake.
13 Mwenye kulipiza mema kwa mabaya, mabaya hayataondoka nyumbani mwake.
14 Kuanzisha ugomvi ni kama kufanya ufa kwenye bwawa; achana na ugomvi kabla haujafurika.
15 Kumsamehe mwenye hatia na kumwadhibu asiye na hatia yote mawili ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu.
16 Ya nini mpumbavu kuwa na fedha mkononi kununulia hekima, wakati yeye mwenyewe hana akili?
17 Rafiki wa kweli ni rafiki siku zote, ndugu huzaliwa asaidie wakati wa taabu.
18 Si jambo la akili kuweka rehani, na kuwa mdhamini wa mtu mwingine.
19 Anayependa ugomvi anapenda dhambi; anayejigamba anajitafutia maangamizi.
20 Mwenye moyo mpotovu hafanikiwi, na msema uongo hupatwa na maafa.
21 Mtoto mpumbavu ni huzuni kwa baba yake, na baba wa mpumbavu hana furaha.
22 Moyo mchangamfu ni dawa, bali moyo wenye huzuni hudhoofisha mwili.
23 Mtu mbaya hupokea hongo kwa siri ili apate kupotosha haki.
24 Mtu mwenye busara lengo lake ni hekima, lakini mpumbavu hupania kila kitu duniani.
25 Mtoto mpumbavu ni huzuni kwa baba yake, na uchungu kwa mama yake mzazi.
26 Si vizuri kumtoza faini mtu asiye na hatia; ni kosa kumchapa viboko muungwana.
27 Asiyesema sana ana maarifa; mtu mtulivu ni mwenye busara.
28 Hata mpumbavu akinyamaza huonekana ana hekima; akifunga mdomo wake huonekana kuwa mwenye akili.
1 Anayetafuta yake tu hujitenga na wenzake; hukasirika akipewa shauri lolote jema.
2 Mpumbavu hapendezwi na busara; kwake cha maana ni maoni yake tu.
3 Ajapo mwovu huja pia dharau; pamoja na aibu huja fedheha.
4 Maneno yaweza kuwa chemchemi ya hekima; yenye kilindi kama bahari, kama kijito kinachobubujika.
5 Si vizuri kumpendelea mtu mwovu, na kumnyima haki mtu mwadilifu.
6 Maneno ya mpumbavu huleta ugomvi; kila anachosema husababisha adhabu.
7 Kinywa cha mpumbavu humwangamiza mwenyewe; mdomo wake ni mtego wa kumnasa yeye mwenyewe.
8 Maneno ya msengenyaji ni kama kitoweo kitamu; ambacho hushuka moja kwa moja mpaka tumboni.
9 Mtu mvivu kazini mwake ni ndugu yake mharibifu.
10 Jina la Mwenyezi-Mungu ni mnara imara; mwadilifu huukimbilia akawa salama.
11 Lakini tajiri hudhani mali ni ngome yake; anafikiri hayo ni ukuta mrefu unaomlinda.
12 Majivuno ya moyoni huleta maangamizi, lakini unyenyekevu huleta heshima.
13 Kujibu kabla ya kusikiliza ni upumbavu na jambo la aibu.
14 Roho ya mtu huweza kustahimili ugonjwa, lakini ukiwa umevunjika moyo, utastahimilije?
15 Mtu mwenye akili hujipatia maarifa, sikio la mwenye busara hutafuta maarifa.
16 Zawadi humfungulia mtu milango; huweza kumfikisha mtu mbele ya mkuu.
17 Ajiteteaye kwanza huonekana msema kweli, mpaka hapo mpinzani wake atakapoanza kumhoji.
18 Kura hukomesha ubishi; huamua kati ya wakuu wanaopingana.
19 Ndugu aliyeudhiwa ni mgumu kuliko mji wa ngome; magomvi hubana kama makufuli ya ngome.
20 Maneno ya mtu yaweza kumshibisha; hutosheka kwa matokeo ya maneno yake.
21 Ulimi una nguvu ya kufanya hai na kuua; wanaopenda kuutumia watakula matunda yake.
22 Anayempata mke amepata bahati njema; hiyo ni fadhili kutoka kwa Mwenyezi-Mungu.
23 Maskini huomba kwa unyenyekevu, bali tajiri hujibu kwa ukali.
24 Marafiki wengi waweza kumwangusha mtu, lakini wapo marafiki waaminifu kuliko ndugu.
1 Afadhali maskini aishiye kwa unyofu, kuliko mtu mpotovu wa maneno na mpumbavu.
2 Haifai mtu kuwa bila akili; mwenda harakaharaka hujikwaa.
3 Mtu akijiangamiza kwa upumbavu wake, huielekeza hasira yake dhidi ya Mwenyezi-Mungu.
4 Mali huvuta marafiki wengi wapya, lakini maskini huachwa bila rafiki.
5 Shahidi mwongo hataacha kuadhibiwa; asemaye uongo hataepa adhabu.
6 Watu wengi hujipendekeza kwa wakuu; kila mtu hutaka kuwa rafiki ya mtu mkarimu.
7 Maskini huchukiwa na ndugu zake; marafiki zake ndio zaidi: Humkimbia! Hata awabembeleze namna gani hatawapata.
8 Ajipatiaye hekima anaipenda nafsi yake; anayezingatia busara atastawi.
9 Shahidi mwongo hatakosa kuadhibiwa; asemaye uongo ataangamia.
10 Haifai kwa mpumbavu kuishi kwa anasa, tena ni vibaya zaidi mtumwa kuwatawala wakuu.
11 Mwenye busara hakasiriki upesi; kusamehe makosa ni fahari kwake.
12 Ghadhabu ya mfalme ni kama ngurumo ya simba, lakini wema wake ni kama umande juu ya majani.
13 Mtoto mpumbavu ni balaa kwa baba yake; na ugomvi wa mke ni kama matone ya mvua yasiyoisha.
14 Nyumba na mali ni urithi apatao mtu kwa wazee wake, lakini mke mwenye busara hutoka kwa Mwenyezi-Mungu.
15 Uzembe ni kama usingizi mzito; mtu mvivu atateseka kwa njaa.
16 Anayeshika amri anasalimisha maisha yake; anayepuuza agizo atakufa.
17 Anayemsaidia maskini anamkopesha Mwenyezi-Mungu; Mwenyezi-Mungu atamlipa kwa tendo lake jema.
18 Mrudi mwanao kungali bado na tumaini, lakini usimwadhibu kiasi cha kumwangamiza.
19 Mtu wa hasira kali lazima apate adhabu; ukimwachia mara moja itakubidi kumwachia tena.
20 Sikiliza shauri na kupokea mafundisho, upate hekima ya kukufaa siku zijazo.
21 Kichwani mwa mtu mna mipango mingi, lakini anachokusudia Mwenyezi-Mungu ndicho kitakachofanyika.
22 Kinachotakiwa kwa mtu ni uaminifu; afadhali mtu maskini kuliko mtu mwongo.
23 Kumcha Mwenyezi-Mungu kunaleta uhai; amchaye hujaliwa pumziko la kutosheleza, wala hatapatwa na baa lolote.
24 Mvivu ni kama mtu atiaye mkono katika sahani ya chakula, lakini hana nguvu ya kuuinua hadi mdomoni.
25 Mwadhibu mwenye mzaha naye mjinga atapata akili; mwonye mwenye busara naye atapata maarifa.
26 Anayemdhulumu baba yake na kumfukuza mama yake, ni mtoto asiyefaa na mpotovu.
27 Mwanangu, ukiacha kusikiliza mafundisho, utapotea mara mbali na maneno ya hekima.
28 Shahidi asiyefaa kitu huidhihaki haki; na kinywa cha mwovu hubugia uovu.
29 Adhabu iko tayari kwa wenye mzaha, mijeledi imetayarishwa kuchapa migongo ya wapumbavu.
1 Divai huleta dhihaka na kileo huleta ugomvi; yeyote anayevutiwa navyo hana hekima.
2 Ghadhabu kali ya mfalme ni kama simba angurumaye; anayemkasirisha anayahatarisha maisha yake.
3 Ni jambo la heshima kuepa ugomvi; wapumbavu ndio wanaogombana.
4 Mvivu halimi wakati wa kulima; wakati wa mavuno atatafuta asipate chochote.
5 Fikira za mtu zimefichika kama kilindi cha maji; lakini mtu mwenye busara ajua kuzichota humo.
6 Watu wengi hujivunia kuwa wema, lakini mwaminifu wa kweli apatikana wapi?
7 Mtu mwadilifu akiishi kwa unyofu; watoto wake atakaowaacha watabarikiwa.
8 Mfalme mwema aketipo kutoa hukumu, huupepeta uovu wote kwa macho yake.
9 Nani athubutuye kusema: “Nimeutakasa moyo wangu; mimi nimetakasika dhambi yangu?”
10 Mizani ya udanganyifu na vipimo vya udanganyifu, vyote ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu.
11 Hata mtoto hujulikana kwa matendo yake, kama tabia yake ni njema na aminifu.
12 Sikio lisikialo na jicho lionalo, yote mawili kayafanya Mwenyezi-Mungu.
13 Usipende kulala tu usije ukawa maskini; uwe macho nawe utakuwa na chakula kingi.
14 “Hakifai, hakifai”, mnunuzi hulalamika, lakini akiondoka hujisifu amepunguziwa bei.
15 Kuna dhahabu na wingi wa mawe ya thamani kubwa; lakini cha thamani kubwa zaidi ni maneno ya busara!
16 Mtu akiahidi mbele yako kumdhamini mgeni, chukua nguo yake; mfanye awajibike kwa kuwadhamini wageni.
17 Chakula kipatikanacho kwa udanganyifu ni kitamu, lakini baadaye huwa kama mchanga kinywani.
18 Mipango mizuri hufanyika kwa kushauriana; ukitaka kuanza vita lazima kutafakari kwanza.
19 Mpiga domo hafichi siri, kwa hiyo mwepe mtu wa kuropoka.
20 Anayemlaani baba yake au mama yake, mwanga wa uhai wake utazimwa kama taa gizani.
21 Mali iliyopatikana kwa haraka mwanzoni, haitakuwa ya heri mwishoni.
22 Usiseme, “Nitalipiza ubaya niliotendewa.” Mtegemee Mwenyezi-Mungu naye atakusaidia.
23 Mizani ya udanganyifu ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu, na vipimo visivyo halali ni kitu kibaya.
24 Hatua za mtu huongozwa na Mwenyezi-Mungu; awezaje binadamu kujua njia ya kwenda?
25 Ni hatari kusema kwa mzaha “Usiahidi kumpa Mungu kitu bila kufikiri, la sivyo utaanza kusikitika baada ya nadhiri yako.”
26 Mfalme mwenye busara huwapepeta waovu; huwaadhibu bila huruma.
27 Dhamiri ya mtu ni taa ya Mwenyezi-Mungu; huchunguza nafsi yake mtu mpaka ndani kabisa.
28 Wema na uaminifu humkinga mfalme; utawala wake huimarishwa kwa uadilifu.
29 Fahari ya vijana ni nguvu zao, uzuri wa vikongwe ni mvi za uzee.
30 Mapigo yanayoumiza ni dawa ya kuondoa uovu; viboko husafisha nafsi mpaka ndani kabisa.
1 Moyo wa mfalme ni kama maji yanayotiririka; Mwenyezi-Mungu, huuongoza popote apendapo.
2 Matendo yote ya mtu ni sawa machoni pake, lakini Mwenyezi-Mungu hupima mioyo.
3 Kutenda mambo mema na ya haki, humpendeza Mwenyezi-Mungu kuliko tambiko.
4 Macho ya kiburi na moyo wa majivuno huonesha wazi dhambi ya waovu.
5 Mipango ya mtu wa bidii huleta mali kwa wingi, lakini kila aliye na pupa huishia patupu.
6 Mali ipatikanayo kwa udanganyifu, ni mvuke upitao na mtego wa kifo.
7 Ukatili wa wakatili utawafutilia mbali, maana wanakataa kutenda yaliyo ya haki.
8 Njia ya mtu mwenye hatia imepotoka, lakini mwenendo wa mnyofu umenyooka.
9 Afadhali kuishi pembeni juu ya paa, kuliko kuishi nyumbani na mwanamke mgomvi.
10 Anachopania kutenda mtu mbaya ni uovu; hata kwa jirani yake hana huruma.
11 Ukimwadhibu mwenye dhihaka, mjinga hupata hekima; ukimfundisha mwenye hekima, unampatia maarifa.
12 Mungu Mwadilifu anajua wanayotenda waovu nyumbani kwao; naye atawaangusha na kuwaangamiza.
13 Anayekataa kusikiliza kilio cha maskini, naye pia hatasikilizwa atakapolilia msaada.
14 Hasira hutulizwa kwa zawadi ya siri; tunu apewayo mtu imefichwa hupooza ghadhabu.
15 Haki ikitekelezwa watu wema hufurahi, lakini watu waovu hufadhaishwa.
16 Anayetangatanga mbali na njia ya busara, atajikuta ametua miongoni mwa wafu.
17 Anayependa anasa atakuwa maskini; anayefikiria tu kula na kunywa hatatajirika.
18 Mwovu atapata pigo ambalo halitampata mtu mwema, mkosefu ataadhibiwa badala ya mnyofu.
19 Afadhali kuishi jangwani, kuliko kukaa na mwanamke mgomvi na msumbufu.
20 Nyumbani kwa mwenye busara mna hazina za thamani, lakini mpumbavu huponda mali yake yote.
21 Anayepania uadilifu na huruma, ataishi maisha marefu na kuheshimiwa.
22 Mwenye hekima aweza kuteka mji wa wenye nguvu, na kuziporomosha ngome wanazozitegemea.
23 Achungaye mdomo wake na ulimi wake, hujiepusha na matatizo.
24 Mwenye majivuno na kiburi jina lake ni “Madharau;” matendo yake yamejaa majivuno ya ufidhuli wake.
25 Mvivu hufa kwa kutotimizwa tamaa zake, maana mikono yake milegevu haitaki kufanya kazi.
26 Mchana kutwa mwovu hutamani kupata kitu, lakini mwadilifu hutoa, tena kwa ukarimu.
27 Tambiko ya mwovu ni kitu cha kuchukiza, huchukiza zaidi akiitoa kwa nia mbaya.
28 Shahidi mwongo ataangamia, lakini msikivu hawezi kunyamazishwa.
29 Mtu mwovu hujionesha kuwa jasiri, lakini mwadilifu huhakikisha ametenda sawa.
30 Hakuna hekima, maarifa, wala mawaidha yoyote ya mtu, yawezayo kumshinda Mwenyezi-Mungu.
31 Farasi hutayarishwa kwa vita, lakini ushindi wamtegemea Mwenyezi-Mungu.
1 Afadhali kuwa na sifa nzuri kuliko mali nyingi; wema ni bora kuliko fedha au dhahabu.
2 Matajiri na maskini wana hali hii moja: Mwenyezi-Mungu ni Muumba wao wote.
3 Mtu mwangalifu huona hatari akajificha, lakini wajinga hujitokeza mbele wakaumia.
4 Ukinyenyekea na kumcha Mwenyezi-Mungu, utapata tuzo: Fanaka, heshima na uhai.
5 Njia ya waovu imejaa miiba na mitego; anayetaka kuhifadhi maisha yake ataiepa.
6 Mfunze mtoto namna ya kuishi vizuri, naye hatasahau njia hiyo hata uzeeni.
7 Tajiri humtawala maskini; mkopaji ni mtumwa wa mkopeshaji.
8 Apandaye dhuluma atavuna janga; uwezo wake wa kutenda mabaya utavunjwa.
9 Mtu mkarimu atabarikiwa, maana chakula chake humgawia maskini.
10 Mfukuze mwenye dharau na fujo itatoweka, ugomvi na matusi vitakoma.
11 Mwenye nia safi na maneno mazuri, atakuwa rafiki wa mfalme.
12 Mwenyezi-Mungu hulinda elimu ya kweli, lakini huyavuruga maneno ya waovu.
13 Mvivu husema, “Siwezi kutoka nje; kuna simba huko, ataniua!”
14 Kinywa cha mwasherati ni shimo refu; anayechukiwa na Mwenyezi-Mungu atatumbukia humo.
15 Mtoto hupenda mambo ya kijinga moyoni, lakini fimbo ya nidhamu humwondolea hayo.
16 Anayemdhulumu maskini atamfanya afaidike mwishowe, anayewapa matajiri zawadi ataishia kuwa maskini.
17 Tega sikio usikie maneno ya wenye hekima, elekeza moyo wako uzingatie maarifa yangu.
18 Wewe utafurahi endapo utayaweka moyoni, na kuyakariri kila wakati.
19 Ninayependa kumfundisha leo ni wewe, ili tegemeo lako liwe kwa Mwenyezi-Mungu.
20 Nimekuandikia misemo thelathini, misemo ya maonyo na maarifa,
21 ili kukufundisha yaliyo sawa na kweli; na mtu akikuuliza uweze kumpa jibu sahihi.
22 Usimdhulumu maskini kwa kuwa ni maskini, wala usimnyime fukara haki yake mahakamani.
23 Maana Mwenyezi-Mungu atawatetea; atawapokonya maisha yao wale watakaowadhulumu.
24 Usifanye urafiki na mtu wa hasira, wala usiandamane na mwenye ghadhabu,
25 usije ukajifunza mwenendo wake, ukajinasa kabisa katika mtego.
26 Usiwe mmoja wao wenye kuweka ahadi, watu ambao hujiweka wadhamini wa madeni.
27 Ikiwa huna chochote cha kulipa, hata kitanda unacholalia kitachukuliwa!
28 Usiondoe alama ya mipaka ya zamani ambayo iliwekwa na wazee wako.
29 Je, yuko mtu mwenye maarifa kazini mwake? Huyo atawatumikia wafalme; hatawapa huduma yake watu wasiofaa.
1 Ukiketi kula pamoja na mtawala, usisahau hata kidogo uko pamoja na nani.
2 Zuia sana hamu yako, ikiwa wewe wapenda sana kula.
3 Usitamani vyakula vyake vizuri, maana vyaweza kukudanganya.
4 Ikiwa unayo hekima ya kutosha, usijitaabishe kutafuta utajiri.
5 Kufumba na kufumbua utajiri hutoweka, huwa kama umepata mabawa ghafla, ukaruka na kutowekea angani kama tai.
6 Usile chakula cha mtu bahili, wala usitamani mapochopocho yake,
7 maana moyoni mwake anahesabu unachokula. Atakuambia, “Kula, kunywa!” Lakini moyoni mwake hayuko pamoja nawe.
8 Utatapika vipande ulivyokula; shukrani zako zote zitakuwa za bure.
9 Usiseme maneno yako mbele ya mpumbavu, maana atapuuza hekima ya maneno yako.
10 Usiondoe alama ya mpaka wa zamani, wala usiingilie mashamba ya yatima,
11 maana Mungu, Mkombozi, ni mwenye nguvu, naye ataitetea haki yao dhidi yako.
12 Tumia akili zako kufuata mafundisho; tumia masikio yako kusikiliza maarifa.
13 Usiache kumrudi mtoto; ukimchapa kiboko hatakufa.
14 Ukimtandika kiboko, utayaokoa maisha yake na kuzimu.
15 Mwanangu, moyo wako ukiwa wenye busara, moyo wangu pia utakuwa wenye furaha.
16 Moyo wangu utashangilia, mdomo wako utakaposema maneno yaliyo sawa.
17 Moyo wako usiwaonee wivu wenye dhambi, ila endelea kumcha Mwenyezi-Mungu siku zote.
18 Hakika kuna kesho ya milele, na tumaini lako halitakuwa bure.
19 Sikia mwanangu, uwe na hekima; fikiria sana jinsi unavyoishi.
20 Usiwe mmoja wa walevi wa divai, wala walafi wenye kupenda nyama,
21 maana walevi na walafi wataishia kuwa maskini, anayetumia siku yake kusinzia atavaa matambara.
22 Msikilize baba yako aliyekuzaa, wala usimdharau mama yako akizeeka.
23 Nunua ukweli, wala usiuuze; nunua hekima, mafunzo na busara.
24 Baba wa mtoto mwadilifu atajaa furaha; anayemzaa mtoto mwenye hekima atamfurahia.
25 Wafurahishe baba na mama yako; mama aliyekuzaa na afurahi.
26 Mwanangu, nisikilize kwa makini, shikilia mwenendo wa maisha yangu.
27 Malaya ni shimo refu la kutega watu; mwanamke mgeni ni kama kisima chembamba.
28 Yeye hunyemelea kama mnyanganyi, husababisha wanaume wengi kukosa uaminifu.
29 Ni nani wapigao yowe? Ni nani wenye huzuni? Ni nani wenye ugomvi? Ni nani walalamikao? Ni nani wenye majeraha bila sababu? Ni nani wenye macho mekundu?
30 Ni wale ambao hawabanduki penye divai, wale wakaao chonjo kuonja divai iliyokolezwa.
31 Usiitamani divai hata kwa wekundu wake, hata kama inametameta katika bilauri, na kushuka taratibu unapoinywa.
32 Mwishowe huuma kama nyoka; huchoma kama nyoka mwenye sumu.
33 Macho yako yataona mauzauza, moyo wako utatoa mambo yaliyopotoka.
34 Utakuwa kama mtu alalaye katikati ya bahari, kama mtu alalaye juu ya mlingoti wa meli.
35 Utasema, “Walinichapa, lakini sikuumia; walinipiga, lakini sina habari. Nitaamka lini? Ngoja nitafute kinywaji kingine!”
1 Usiwaonee wivu watu waovu, wala usitamani kuwa pamoja nao,
2 maana fikira zao zote ni juu ya ukatili, hamna jema lolote litokalo midomoni mwao.
3 Nyumba hujengwa kwa hekima, na kuimarishwa kwa busara.
4 Kwa maarifa vyumba vyake hujazwa vitu vya thamani na vya kupendeza.
5 Kuwa na hekima ni bora kuliko kuwa na nguvu, naam, maarifa ni bora kuliko nguvu.
6 Maana kwa mwongozo mzuri waweza kupigana vita, na kwa washauri wengi ushindi hupatikana.
7 Kwa mpumbavu hekima ni ngumu kuielewa; penye mkutano wa mashauri hafungui mdomo.
8 Afikiriaye kutenda maovu daima ataitwa mtu mwenye fitina.
9 Mpango anaofikiria mpumbavu ni dhambi; mwenye dharau huchukiwa na kila mtu.
10 Ukifa moyo wakati wa shida, basi wewe ni dhaifu kweli.
11 Mwokoe mtu anayechukuliwa kuuawa bure; usisite kumwokoa anayeuawa bila hatia.
12 Usiseme baadaye: “Hatukujua!” Maana Mungu apimaye mioyo ya watu huona; yeye atakulipa kulingana na matendo yako!
13 Mwanangu, ule asali maana ni nzuri; sega la asali ni tamu mdomoni.
14 Ndivyo ilivyo hekima nafsini mwako; ukiipata utakuwa na matazamio mema, wala tumaini lako halitakuwa la bure.
15 Usivizie kama mwovu kushambulia makao ya mtu mwema, wala usijaribu kuiharibu nyumba yake,
16 maana mtu mwema huanguka mara nyingi lakini huinuka, lakini mtu mwovu huangamizwa na janga.
17 Usishangilie kuanguka kwa adui yako; usifurahie moyoni mwako kujikwaa kwake,
18 maana Mwenyezi-Mungu aonaye hayo hatapendezwa; huenda akaacha kumwadhibu.
19 Usihangaike kwa sababu ya watenda mabaya, wala usiwaonee wivu watu waovu,
20 maana mwovu hatakuwa na mema baadaye; taa ya uhai wake itazimwa.
21 Mwanangu, umche Mwenyezi-Mungu na kumheshimu mfalme, wala usishirikiane na wale wasio na msimamo,
22 maana maangamizi yao huwapata ghafla. Hakuna ajuaye maafa watakayozusha.
23 Ifuatayo pia ni misemo ya wenye hekima: Kupendelea watu katika hukumu si vizuri.
24 Anayemwachilia mtu mwenye hatia, hulaaniwa na watu na kuchukiwa na mataifa.
25 Lakini wanaowaadhibu waovu watapata furaha, na baraka njema zitawajia.
26 Jibu lililo la haki, ni kama busu la rafiki.
27 Kwanza fanya kazi zako nje, tayarisha kila kitu shambani, kisha jenga nyumba yako.
28 Usishuhudie bure dhidi ya jirani yako, wala usiseme uongo juu yake.
29 Usiseme, “Nitamtenda kama alivyonitenda! Ni lazima nilipize kisasi!”
30 Nilipitia karibu na shamba la mvivu; shamba la mzabibu la mtu mpumbavu.
31 Nilishangaa kuona limemea miiba, magugu yamefunika eneo lake lote, na ukuta wake wa mawe umebomoka.
32 Nilitazama, nikawaza, mwishowe nikapata funzo:
33 Lala tu kidogo; sinzia tu kidogo! Kunja mikono yako tu upumzike!
34 Lakini kumbuka kwamba uwapo usingizini, umaskini utakuvamia kama mnyanganyi, ufukara kama mtu mwenye silaha.
1 Hizi nazo ni methali nyingine za mfalme Solomoni walizonakili watu wa Hezekia, mfalme wa Yuda.
2 Mungu hutukuzwa kwa kuficha mambo, lakini mfalme hutukuzwa kwa yale anayoeleza.
3 Kama zilivyo mbali mbingu na kirefu kina cha ardhi ndivyo zisivyochunguzika akili za mfalme.
4 Toa takataka katika fedha, na mhunzi atakutengenezea chombo kizuri.
5 Waondoe waovu mbele ya mfalme, na utawala wake utaimarika katika haki.
6 Usijipendekeze kwa mfalme, wala usijifanye mtu mkubwa,
7 maana ni heri kuambiwa, “Njoo huku mbele”, kuliko kuporomoshwa mbele ya mkuu. Mambo uliyoyaona kwa macho yako,
8 usiharakishe kuyapeleka mahakamani; maana utafanya nini hapo baadaye, shahidi mwingine akibatilisha hayo usemayo?
9 Suluhisha ugomvi na mwenzako peke yake, na kila mmoja wenu asitoe siri ya mwenzake;
10 watu wasije wakajua kuna siri, ukajiharibia jina lako daima.
11 Neno lisemwalo wakati unaofaa, ni kama nakshi za dhahabu juu ya madini ya fedha.
12 Onyo la mwenye hekima kwa mtu msikivu, ni bora kuliko pete au vito vya dhahabu safi.
13 Mjumbe mwaminifu humfurahisha yule aliyemtuma, kama maji baridi wakati wa joto la mavuno.
14 Kama vile mawingu na upepo bila mvua, ndivyo alivyo mtu anayejigamba kutoa zawadi asiitoe.
15 Kwa uvumilivu mtawala huweza kushawishika; ulimi laini huvunja mifupa.
16 Upatapo asali kula kiasi cha kukutosha, usije ukaikinai na kuitapika.
17 Usimtembelee jirani yako mara kwa mara, usije ukamchosha naye akakuchukia.
18 Mtu atoaye ushahidi wa uongo dhidi ya mwenziwe, ni hatari kama rungu, upanga au mshale mkali.
19 Kumtegemea mtu asiyeaminika wakati wa taabu, ni kama jino bovu au mguu ulioteguka.
20 Kumwimbia mtu mwenye huzuni, ni kama kuvua nguo wakati wa baridi, au kutia siki katika kidonda.
21 Adui yako akiwa na njaa, mpe chakula; akiwa na kiu, mpe maji ya kunywa.
22 Hivyo utafanya apate aibu kali, kama makaa ya moto kichwani pake, naye Mwenyezi-Mungu atakutuza.
23 Upepo wa kusi huleta mvua, hali kadhalika masengenyo huleta chuki.
24 Afadhali kuishi pembeni juu ya paa, kuliko kuishi nyumbani pamoja na mwanamke mgomvi.
25 Kama vile maji baridi kwa mwenye kiu, ndivyo habari njema kutoka mbali.
26 Mwadilifu akubaliye kufuata mambo ya mwovu, ni chemchemi iliyochafuliwa au kisima kilichotibuliwa.
27 Si vizuri kula asali nyingi mno; kadhalika haifai kujipendekeza mno.
28 Mtu asiyeweza kuzuia hasira yake, ni kama mji usio na ulinzi unaposhambuliwa.
1 Heshima apewayo mpumbavu haimfai; ni kama theluji ya kiangazi, au mvua ya wakati wa mavuno.
2 Kama shomoro au mbayuwayu wasiotua, kadhalika laana asiyostahili mtu haimtui.
3 Mjeledi kwa farasi, lijamu kwa punda, na fimbo kwa mgongo wa mpumbavu.
4 Usimjibu mpumbavu kipumbavu, usije ukafanana naye.
5 Mjibu mpumbavu kama ustahilivyo upumbavu wake, asije akajiona kuwa mwenye hekima zaidi.
6 Kumtuma mpumbavu ujumbe, ni kama kujikata miguu au kujitafutia shida.
7 Methali mdomoni mwa mpumbavu, ni kama miguu ya kiwete inayoninginia.
8 Kumpa mpumbavu heshima, ni kama kufunga jiwe kwenye kombeo.
9 Mpumbavu anayejaribu kutumia methali, ni kama mlevi anayejaribu kungoa mwiba mkononi.
10 Mtu amwajiriye mpumbavu au mlevi, ni kama mpiga upinde anayejeruhi kila mtu.
11 Mpumbavu anayerudiarudia upumbavu wake, ni kama mbwa anayekula matapishi yake.
12 Wamwona mtu ajionaye kuwa mwenye hekima? Nakuambia mpumbavu ni nafuu kuliko huyo.
13 Mvivu husema: “Huko nje kuna simba; siwezi kwenda huko.”
14 Kama vile mlango uzungukiapo bawaba zake, ndivyo mvivu juu ya kitanda chake.
15 Mvivu huutia mkono wake katika sahani ya chakula, lakini hawezi kuuinua hadi mdomoni.
16 Mvivu hujiona kuwa mwenye hekima kuliko watu saba wawezao kujibu kwa busara.
17 Ajiingizaye katika ugomvi usiomhusu, ni kama mtu amshikaye masikio mbwa anayepita.
18 Kama mwendawazimu achezeavyo mienge, au mishale ya kifo,
19 ndivyo alivyo mtu ampotoshaye jirani, kisha aseme, “Nilikuwa natania tu!”
20 Bila kuni, moto huzimika; bila mchochezi, ugomvi humalizika.
21 Kama vile makaa au kuni huchochea moto, ndivyo mgomvi achocheavyo ugomvi.
22 Maneno ya msengenyaji ni kama kitoweo; hushuka mpaka ndani kabisa tumboni.
23 Kama rangi angavu iliyopakwa kigae, ndivyo yalivyo maneno matamu yenye nia mbaya.
24 Mwenye chuki huficha chuki yake kwa maneno mazuri, lakini huwa ana hila moyoni mwake.
25 Akiongea vizuri usimwamini, moyoni mwake mna chuki chungu nzima.
26 Huenda akaficha chuki yake, lakini nia zake mbaya zitajulikana kwa wote.
27 Amchimbiaye mwenzake shimo, hutumbukia mwenyewe; abingirishaye jiwe litamrudia mwenyewe.
28 Asemaye uongo huwachukia hao anaowaumiza, naye abembelezaye huleta maangamizi.
1 Usijisifie ya kesho, hujui nini kitatokea leo mpaka kesho.
2 Acha watu wengine wakusifu, kuliko mdomo wako wewe mwenyewe.
3 Jiwe ni zito na mchanga kadhalika, lakini usumbufu wa mpumbavu ni mzito zaidi.
4 Ghadhabu ni katili na hasira huangamiza; lakini ni nani awezaye kuukabili wivu?
5 Afadhali mtu anayekuonya waziwazi, kuliko yule afichaye upendo.
6 Makaripio ya rafiki yaonesha uaminifu, lakini busu la adui ni udanganyifu.
7 Aliyeshiba hata asali huikataa, lakini kwa mwenye njaa kila kichungu ni kitamu.
8 Mtu aliyepotea mbali na kwake, ni kama ndege aliyepotea mbali na kiota chake.
9 Mafuta na manukato huufurahisha moyo, lakini taabu hurarua roho.
10 Usisahau rafiki zako wala wa baba yako. Ukipatwa na janga usikimbilie kwa nduguyo; afadhali jirani aliye karibu kuliko ndugu aliye mbali.
11 Uwe na hekima mwanangu upate kunifurahisha moyo, nami sitakosa la kumjibu yeyote anayenilaumu.
12 Mwenye busara huona hatari akajificha, lakini mjinga hujitokeza mbele akaumia.
13 Mtu akiahidi mbele yako kumdhamini mgeni, chukua nguo yake; mfanye awajibike kwa kuwadhamini wageni.
14 Amwamkiaye jirani kwa kelele alfajiri, itaeleweka kwamba amemtakia laana.
15 Mke mgomvi daima, ni sawa na tonatona ya maji siku ya mvua.
16 Kumzuia ni sawa na kuzuia upepo, au kukamata mafuta kwa mkono.
17 Chuma hunoa chuma, kadhalika mtu hufundishwa na wenzake.
18 Anayeutunza mtini hula tini, anayemhudumia bwana wake ataheshimiwa.
19 Kama uso ujionavyo wenyewe majini, ndivyo ujijuavyo mwenyewe moyoni.
20 Kuzimu na Uharibifu kamwe havishibi, kadhalika na macho ya watu hayashibi.
21 Ubora wa fedha au dhahabu hupimwa kwa moto, na mtu hupimwa kutokana na sifa zake.
22 Mtwange mpumbavu katika kinu pamoja na nafaka, lakini hutafaulu kumtenganisha na upumbavu wake.
23 Angalia vizuri hali ya mifugo yako; tunza vizuri wanyama wako.
24 Maana utajiri haudumu milele, wala taji haidumu vizazi vyote.
25 Baada ya kukata nyasi na kuzihifadhi, kata majani toka milimani, huku nyasi zinachipua upya.
26 Kondoo watakupatia sufu kwa mavazi, mbuzi nao utauza na kujinunulia mashamba;
27 watakupa maziwa ya kukutosha wewe na jamaa yako, na kwa ajili ya watumishi wako wa kike.
1 Waovu hukimbia japo hawafukuzwi na mtu, lakini waadilifu ni hodari kama simba.
2 Taifa la fujo huzusha viongozi wengi, lakini kwa kiongozi mmoja mwenye akili na maarifa huwa na utengemano
3 Mtu mhitaji anayewadhulumu maskini, amefanana na mvua kubwa inayoharibu mimea.
4 Watu wanaovunja sheria huwasifu waovu, lakini wanaoishika sheria hupingana nao.
5 Waovu hawajui maana ya haki, lakini wamchao Mwenyezi-Mungu wanaielewa kabisa.
6 Afadhali maskini aishiye kwa unyofu, kuliko tajiri aishiye kwa upotovu.
7 Mtoto ashikaye sheria ni mwenye hekima, lakini rafiki wa walafi humwaibisha baba yake.
8 Aongezaye mali yake kwa riba na kutoza faida anamkusanyia mwingine mwenye kuwahurumia maskini.
9 Anayekataa kuisikia sheria, huyo hata sala yake ni chukizo kwa Mungu.
10 Anayemshawishi mtu mwema kutenda mabaya, ataanguka katika shimo lake mwenyewe. Wasio na hatia wamewekewa mema yao.
11 Tajiri hujiona mwenyewe kuwa mwenye hekima, lakini maskini mwenye busara atamfichua.
12 Watu wema wakipata madaraka maisha hufana, lakini waovu wakitawala watu hujificha.
13 Afichaye makosa yake hatafanikiwa; lakini anayeungama na kuyaacha atapata rehema.
14 Heri mtu amchaye Mwenyezi-Mungu daima; lakini mkaidi wa moyo ataangukia maafa.
15 Mtawala mwovu anayewatawala maskini, ni kama simba angurumaye au dubu anayeshambulia.
16 Mtawala asiye na akili ni mdhalimu mkatili; lakini achukiaye mali ya udanganyifu atatawala muda mrefu.
17 Mtu anayelemewa na hatia ya kuua mtu, atakuwa mkimbizi mpaka kaburini; mtu yeyote na asijaribu kumzuia.
18 Aishiye kwa unyofu atasalimishwa, lakini mdanganyifu ataanguka kabisa.
19 Anayelima shamba lake atapata chakula kingi, bali anayefuata yasiyofaa atapata umaskini tele.
20 Mtu mwaminifu atapata baraka tele, lakini mwenye pupa ya kuwa tajiri hataepa adhabu.
21 Si vizuri kumbagua mtu; watu hufanya mabaya hata kwa kipande cha mkate.
22 Mtu bahili hukimbilia mali, wala hajui kwamba ufukara utamjia.
23 Amwonyaye mwenzake hatimaye hupata mema zaidi, kuliko yule anayembembeleza kwa maneno matamu.
24 Anayeiba mali ya baba yake au mama yake, akasema si kosa, hana tofauti yoyote na wezi wengine.
25 Mchoyo huchochea ugomvi, lakini anayemtegemea Mwenyezi-Mungu atafanikiwa.
26 Anayetegemea akili yake mwenyewe ni mpumbavu; lakini anayeishi kwa hekima atakuwa salama.
27 Aliye mkarimu kwa maskini hatatindikiwa kitu, lakini anayekataa kuwaangalia atalaaniwa kwa wingi.
28 Waovu wakitawala watu hujificha, lakini wakiangamia, waadilifu huongezeka.
1 Anayeonywa mara nyingi akawa mkaidi, ataangamia ghafla asipone tena.
2 Waadilifu wakitawala watu hufurahi, lakini waovu wakitawala watu hulalamika.
3 Apendaye hekima humfurahisha baba yake; lakini aandamanaye na malaya hufuja mali yake.
4 Mfalme akitumia haki huipatia nchi uthabiti, lakini akipenda hongo taifa huangamia.
5 Mwenye kumbembeleza jirani yake, anatega mtego wa kujinasa mwenyewe.
6 Mtu mbaya hunaswa kwa kosa lake, lakini mtu mwadilifu huimba na kufurahi.
7 Mwadilifu anajua haki za maskini, lakini mtu mwovu hajui mambo hayo.
8 Wenye dharau huutia vurugu mji mzima, lakini wenye hekima hutuliza ghadhabu.
9 Mwenye hekima akibishana na mpumbavu, mpumbavu huwaka hasira na kucheka bila kutulia.
10 Wapendao kumwaga damu humchukia mtu asiye na hatia, lakini watu wema huyalinda maisha yake.
11 Mpumbavu huonesha hasira yake wazi, lakini mwenye hekima huizuia na kuituliza.
12 Mtawala akisikiliza mambo ya uongo, maofisa wake wote watakuwa waovu.
13 Maskini na mkandamizaji wanafanana kwa kitu kimoja: Wote wawili wamepewa macho na Mwenyezi-Mungu.
14 Mfalme anayewaamua maskini kwa haki, atauona utawala wake umeimarika milele.
15 Adhabu na maonyo huleta hekima, lakini mtoto aliyeachwa afanye apendavyo humwaibisha mama yake.
16 Waovu wakitawala maovu huongezeka, lakini waadilifu watashuhudia kuanguka kwao.
17 Mpe nidhamu mwanao naye hatakupa wasiwasi; yeye ataufurahisha moyo wako.
18 Pasipo maono ya kinabii watu hukosa nidhamu; heri mtu yule anayeshika sheria.
19 Mtumwa haonyeki kwa maneno matupu, maana ingawa anayaelewa yeye hatayatii.
20 Wamwona mtu apayukaye bila kufikiri? Mtu mpumbavu ni afadhali kuliko yeye.
21 Ambembelezaye mtumwa wake tangu utoto, mwishowe mtumwa huyo atamrithi.
22 Mwenye ghadhabu huchochea ugomvi, mtu wa hasira husababisha makosa mengi.
23 Kiburi cha mtu humporomosha mwenyewe, lakini mnyenyekevu wa roho atapata heshima.
24 Anayeshirikiana na mwizi anajidhuru mwenyewe; husikia laana ya aliyeonewa bila kusema neno.
25 Kuwaogopa watu ni kujitega mwenyewe, lakini anayemtumaini Mwenyezi-Mungu yu salama.
26 Wengi hupenda kujipendekeza kwa mtawala, hali mtu hupata haki yake kwa Mwenyezi-Mungu.
27 Mdhalimu ni chukizo kwa mnyofu, naye mnyofu ni chukizo kwa mwovu.
1 Maneno ya Aguri, mwana wa Yake. Mawaidha ambayo mtu huyu alimwambia Ithieli, naam, Ithieli na Ukali.
2 Mimi ni mpumbavu mno, wala si mtu; nayo akili ya binadamu sina.
3 Sijajifunza hekima, wala sijui kitu juu ya Mungu Mtakatifu.
4 Ni nani aliyepanda juu mbinguni akashuka chini? Ni nani aliyekamata upepo mkononi? Ni nani aliyefunga maji katika kitambaa? Ni nani aliyeiweka mipaka yote ya dunia? Jina lake ni nani? Na ni nani jina la mwanawe? Niambie kama wajua!
5 Maneno yote ya Mungu ni ya kuaminika; yeye ni ngao yao wote wanaomkimbilia.
6 Usiongeze neno katika maneno yake, asije akakukemea, nawe ukaonekana mwongo.
7 Mambo haya mawili nakuomba ee Mungu, wala usinikatalie kabla sijafa:
8 Uniondolee uongo na udanganyifu; usinipe umaskini wala utajiri; unipatie chakula ninachohitaji,
9 nisije nikashiba nikakukana; nikasema, “Mwenyezi-Mungu ni nani?” Au nisije nikawa maskini nikaiba, na kulikufuru jina lako ee Mungu wangu.
10 Usimchongee mtumwa kwa bwana wake, asije akakulaani, ukaonekana una hatia.
11 Kuna watu ambao huwalaani baba zao, wala hawana shukrani kwa mama zao.
12 Kuna watu ambao hujiona kuwa wema, kumbe bado hawajatakaswa uchafu wao.
13 Kuna na wengine – kiburi ajabu! Hudharau kila kitu wanachokiona.
14 Kuna watu ambao meno yao ni kama upanga, na magego yao ni kama visu. Wako tayari kuwatafuna maskini wa nchi, na wanyonge walio miongoni mwa watu!
15 Mruba anao binti wawili wasemao, “Nipe, nipe!” Kuna vitu vitatu ambavyo kamwe havishibi, naam, vitu vinne visivyosema, “Imetosha!”
16 Kuzimu, tumbo la mwanamke lisilozaa, ardhi isiyoshiba maji, na moto usiosema, “Imetosha!”
17 Kama mtu akimdhihaki baba yake, na kudharau utii kwa mama yake, kunguru wa bondeni watamdonoa macho, na kuliwa na tai.
18 Kuna mambo matatu yaliyo ya ajabu kwangu, naam, mambo manne nisiyoyaelewa:
19 Njia ya tai angani, njia ya nyoka mwambani, njia ya meli baharini, na kinachomvuta mwanamume kwa mwanamke.
20 Mwenendo wa mwanamke mwasherati ni hivi: Yeye hula, akajipangusa mdomo, na kusema, “Sijafanya kosa lolote!”
21 Kuna mambo matatu ambayo huitetemesha dunia, naam, mambo manne ambayo haiwezi kuyastahimili:
22 Mtumwa anayekuwa mfalme; mpumbavu anayeshiba chakula;
23 mwanamke asiyependwa anayeolewa; na mjakazi achukuapo nafasi ya bibi yake.
24 Kuna viumbe vinne vidogo sana duniani, lakini vina akili sana:
25 Sisimizi: Wadudu wasio na nguvu, lakini hujihifadhia chakula wakati wa kiangazi;
26 pelele: Wanyama wasio na uwezo, lakini hujitengenezea makao miambani;
27 nzige: Hawana mfalme, lakini wote huenda pamoja kwa vikosi;
28 mjusi: Waweza kumshika mkononi, lakini huingia katika ikulu.
29 Kuna viumbe vitatu vyenye mwendo wa kupendeza, naam, kuna viumbe vinne vyenye mwendo mzuri;
30 simba: Mnyama mwenye nguvu kuliko wote, wala hamwogopi mnyama mwingine yeyote;
31 jogoo aendaye kwa maringo; tena beberu; na mfalme mbele ya watu wake.
32 Kama umekuwa mpumbavu hata ukajisifu, au kama umekuwa unapanga maovu, chunga mdomo wako.
33 Maana ukisukasuka maziwa utapata siagi, ukimpiga mtu pua atatoka damu; kadhalika kuchochea hasira huleta ugomvi.
1 Maneno ya mfalme Lemueli. Mawaidha aliyofundishwa na mama yake:
2 Nikuambie nini mwanangu? Nikuambie nini mwanangu niliyekuzaa? Nikuambie nini wewe niliyekuomba kwa Mungu?
3 Usimalize nguvu zako kwa wanawake, usiwape mali yako hao wanaoangamiza wafalme.
4 Haifai ee Lemueli, haifai wafalme kunywa divai, wala wakuu kutamani vileo.
5 Wakinywa watasahau maagizo ya sheria, na kuwanyima haki wenye taabu.
6 Mpe kileo mtu anayekufa, wape divai wale wenye huzuni tele;
7 wanywe na kusahau umaskini wao, wasikumbuke tena taabu yao.
8 Lakini wewe, lazima useme kwa ajili ya wote walio bubu; na kutetea haki za wote wasiojiweza.
9 Sema kwa ajili yao na kuamua kwa haki, linda haki za maskini na fukara.
10 Mke mwema kweli, apatikana wapi? Huyo ana thamani kuliko johari!
11 Mumewe humwamini kwa moyo, kwake atapata faida daima.
12 Kamwe hamtendei mumewe mabaya, bali humtendea mema maisha yake yote.
13 Hutafuta sufu na kitani, na kufanya kazi kwa mikono yake kwa bidii.
14 Yeye ni kama meli za biashara: Huleta chakula chake kutoka mbali.
15 Huamka kabla ya mapambazuko, akaitayarishia jamaa yake chakula, na kuwagawia kazi watumishi wake.
16 Hufikiria kununua shamba, kisha hulinunua, na kulima zabibu kwa faida ya jasho lake.
17 Huwa tayari kufanya kazi kwa nguvu na kuiimarisha mikono yake.
18 Hutambua kwamba shughuli zake zina faida; hufanya kazi hata usiku kwa mwanga wa taa yake.
19 Husokota nyuzi kwa mikono yake mwenyewe, kwa vidole vyake mwenyewe husuka nguo zake.
20 Huufungua mkono wake kuwapa maskini, hunyosha mkono kuwasaidia fukara.
21 Hawahofii watu wake ijapo baridi ya kipupwe, maana kila mmoja anazo nguo za kutosha.
22 Hujitengenezea matandiko, mavazi yake ni ya zambarau ya kitani safi.
23 Mume wake ni mtu mashuhuri barazani, anakoshiriki vikao vya wazee wa nchi.
24 Mwanamke huyo hutengeneza nguo na kuziuza, huwauzia wafanyabiashara mishipi.
25 Nguvu na heshima ndizo sifa zake, hucheka afikiriapo wakati ujao.
26 Hufungua kinywa kunena kwa hekima, huwashauri wengine kwa wema.
27 Huchunguza yote yanayofanyika nyumbani mwake, kamwe hakai bure hata kidogo.
28 Watoto wake huamka na kumshukuru, mumewe huimba sifa zake.
29 Husema, “Wanawake wengi wametenda mambo ya ajabu, lakini wewe umewashinda wote.”
30 Madaha huhadaa na uzuri haufai, bali mwanamke amchaye Mwenyezi-Mungu atasifiwa.
31 Jasho lake lastahili kulipwa, shughuli zake hazina budi kuheshimiwa popote.