1

1 Wimbo wa Solomoni ulio bora kuliko nyimbo zote.

2 Heri midomo yako inibusu, maana pendo lako ni bora kuliko divai.

3 Manukato yako yanukia vizuri, na jina lako ni kama marashi yaliyomiminwa. Kwa hiyo wanawake hukupenda!

4 Nichukue, twende zetu haraka, mfalme amenileta katika chumba chake. Tutafurahi na kushangilia kwa sababu yako, tutasifu mapenzi yako kuliko divai. Wanawake wana haki kukupenda!

5 Enyi wanawake wa Yerusalemu, mimi ni mweusi na ninapendeza, kama mahema ya Kedari, kama mapazia ya Solomoni.

6 Msinishangae kwa sababu ni mweusi, maana jua limenichoma. Ndugu zangu walinikasirikia, wakanifanya mlinzi wa mashamba ya mizabibu. Lakini sikutunza shamba langu la mizabibu.

7 Hebu niambie ee wangu wa moyo, utawalisha wapi kondoo wako? Ni wapi watakapopumzikia adhuhuri? Kwa nini mimi nikutafute kati ya makundi ya wenzako?

8 Ewe upendezaye kuliko wanawake wote; kama hujui, fanya hivi: Zifuate nyayo za kondoo; basi, walishe mbuzi wako karibu na hema za wachungaji.

9 Wewe ee mpenzi wangu, nakulinganisha na farasi dume wa magari ya Farao.

10 Mashavu yako yavutia kwa vipuli, na shingo yako kwa mikufu ya johari.

11 Lakini tutakufanyizia mikufu ya dhahabu, iliyopambwa barabara kwa fedha.

12 Mfalme alipokuwa kwenye kochi lake, marashi yangu ya nardo yalisambaa kila mahali.

13 Mpenzi wangu ni kama mfuko wa manemane kwangu, kati ya matiti yangu.

14 Mpenzi wangu ni kama maua ya hina yachanuayo, kwenye mashamba ya mizabibu huko Engedi.

15 Hakika u mzuri, ee mpenzi wangu, hakika u mzuri! Macho yako ni kama ya hua!

16 Hakika u mzuri ewe nikupendaye, u mzuri kweli! Majani mabichi yatakuwa kitanda chetu;

17 mierezi itakuwa nguzo za nyumba yetu, na miberoshi itakuwa dari yake.

2

1 Mimi ni ua la Sharoni, ni yungiyungi ya bondeni.

2 Kama yungiyungi kati ya michongoma, ndivyo alivyo mpenzi wangu kati ya wasichana.

3 Kama mtofaa kati ya miti ya msituni, ndivyo alivyo mpenzi wangu kati ya wavulana. Nafurahia kuketi chini ya kivuli chake, na tunda lake tamu sana kwangu.

4 Alinichukua hadi ukumbi wa karamu, akatweka bendera ya mapenzi juu yangu.

5 Nishibishe na zabibu kavu, niburudishe kwa matofaa, maana naugua kwa mapenzi!

6 Mkono wake wa kushoto chini ya kichwa changu, mkono wake wa kulia wanikumbatia.

7 Nawasihi enyi wanawake wa Yerusalemu, kama walivyo paa au swala wa porini, msiyachochee wala kuyaamsha mapenzi, hadi hapo wakati wake utakapofika.

8 Hiyo ni sauti ya mpenzi wangu, yuaja mbio, anaruka milima, vilima anavipita kasi!

9 Mpenzi wangu ni kama paa, ni kama swala mchanga. Amesimama karibu na ukuta wetu, achungulia dirishani, atazama kimiani.

10 Mpenzi wangu aniambia: “Inuka basi, ewe mpenzi wangu, unipendezaye, njoo twende zetu.

11 Tazama, majira ya baridi yamepita, nazo mvua zimekwisha koma;

12 maua yamechanua kila mahali. Wakati wa kuimba umefika; sauti ya hua yasikika mashambani mwetu.

13 Mitini imeanza kuzaa; na mizabibu imechanua; inatoa harufu nzuri. Njoo, basi, ewe mpenzi wangu unipendezaye, njoo twende.

14 Ee hua wangu, uliyejificha miambani. Hebu niuone uso wako, hebu niisikie sauti yako, maana sauti yako yapendeza na uso wako wavutia.

15 “Tukamatieni mbweha, wale mbweha wadogowadogo, wanaoiharibu mizabibu yetu inayochanua.”

16 Mpenzi wangu ni wangu, nami ni wake. Yeye hulisha kondoo wake penye yungiyungi,

17 hadi hapo jua linapochomoza na vivuli kutoweka. Rudi kama paa mpenzi wangu, kama swala mdogo juu ya milima ya Betheri.

3

1 Usiku nikiwa kitandani mwangu, niliota namtafuta nimpendaye moyoni mwangu; nilimtafuta, lakini sikumpata.

2 Niliamka nikazunguka mjini, barabarani na hata vichochoroni, nikimtafuta yule wangu wa moyo. Nilimtafuta, lakini sikumpata.

3 Walinzi wa mji waliniona walipokuwa wanazunguka mjini. Basi nikawauliza, “Je, mmemwona mpenzi wangu wa moyo?”

4 Mara tu nilipoachana nao, nilimwona mpenzi wangu wa moyo; nikamshika wala sikumwachia aondoke, hadi nilipompeleka nyumbani kwa mama yangu, hadi chumbani kwake yule aliyenizaa.

5 Nawasihini, enyi wanawake wa Yerusalemu, kama walivyo paa au swala, msiyachochee wala kuyaamsha mapenzi, hadi hapo wakati wake utakapofika.

6 Ni kitu gani kile kitokacho jangwani kama mnara wa moshi, kinukiacho manemane na ubani, manukato yauzwayo na wafanyabiashara?

7 Tazama! Ni machela ya Solomoni; amebebwa juu ya kiti chake cha enzi; amezungukwa na walinzi sitini, mashujaa bora wa Israeli.

8 Kila mmoja wao ameshika upanga, kila mmoja wao ni hodari wa vita. Kila mmoja ana upanga wake mkononi, tayari kumkabili adui usiku.

9 Mfalme Solomoni alijitengenezea machela, kwa mbao nzuri kutoka Lebanoni.

10 Nguzo zake zilitengenezwa kwa fedha; mgongo wake kwa dhahabu; mahali pa kukalia pamefunikwa vitambaa vya zambarau, walichoshona kwa upendo wanawake wa Yerusalemu, waliokishonea alama za upendo.

11 Njoni basi enyi wanawake wa Siyoni, mkamwone mfalme Solomoni. Amevalia taji aliyovikwa na mama yake, siku alipofanya harusi yake, naam, siku ambayo moyo wake ulijaa furaha.

4

1 Hakika u mzuri ewe mpenzi wangu, hakika u mzuri! Macho yako ni kama ya hua nyuma ya shela lako, nywele zako ni kama kundi la mbuzi washukao katika milima ya Gileadi.

2 Meno yako ni kama kondoo majike waliokatwa manyoya wanaoteremka baada ya kuogeshwa. Kila mmoja amezaa mapacha, na hakuna yeyote aliyefiwa.

3 Midomo yako ni kama utepe mwekundu, kinywa chako chavutia kweli. Nyuma ya shela lako, mashavu yako ni kama nusu mbili za komamanga.

4 Shingo yako ni kama mnara wa Daudi, uliojengwa ili kuhifadhia silaha, ambako zimetundikwa ngao elfu moja zote zikiwa za mashujaa.

5 Matiti yako ni kama paa mapacha, ambao huchungwa penye yungiyungi.

6 Nitakaa kwenye mlima wa manemane, na kwenye kilima cha ubani, hadi hapo kutakapopambazuka, na giza kutoweka.

7 Tazama ulivyo mzuri ee mpenzi wangu, wewe huna kasoro yoyote.

8 Njoo, bibiarusi wangu tuondoke Lebanoni; na tuiachilie mbali Lebanoni. Shuka toka kilele cha mlima Amana, toka kilele cha Seniri na Hermoni, toka mapango ya simba, toka milima ya chui.

9 Umefurahisha moyo wangu, dada yangu, bi arusi, umefurahisha moyo wangu, kwa kunitupia jicho mara moja tu, na kwa huo mkufu wako shingoni.

10 Dada yangu, bi arusi; pendo lako ni tamu ajabu. Ni bora kuliko divai, marashi yako yanukia kuliko viungo vyote.

11 Midomo yako yadondosha asali, ee bibiarusi wangu; ulimi wako una asali na maziwa. Harufu nzuri ya mavazi yako ni kama ya Lebanoni.

12 Dada yangu, naam, bi arusi, ni bustani iliyofichika, bustani iliyosetiriwa; chemchemi iliyotiwa mhuri.

13 Machipukizi yako ni bustani ya mikomamanga pamoja na matunda bora kuliko yote, hina na nardo.

14 Nardo na zafarani, mchai na mdalasini manemane na udi, na mimea mingineyo yenye harufu nzuri.

15 U chemchemi ya bustani, kisima cha maji yaliyo hai, vijito vitiririkavyo kutoka Lebanoni.

16 Vuma, ewe upepo wa kaskazi, njoo, ewe upepo wa kusi; vumeni juu ya bustani yangu, mlijaze anga kwa manukato yake. Mpenzi wangu na aje bustanini mwake, ale matunda yake bora kuliko yote.

5

1 Naingia bustanini mwangu, dada yangu, bi arusi. Nakusanya manemane na viungo, nala sega langu la asali, nanywa divai yangu na maziwa yangu. Kuleni enyi marafiki, kunyweni; kunyweni sana wapendwa wangu.

2 Nililala, lakini moyo wangu haukulala. Sauti ya mpenzi wangu anabisha hodi. “Nifungulie, dada yangu mpenzi wangu, bibiarusi wangu, hua wangu, usiye na kasoro. Kichwa changu kimelowa umande na nywele zangu manyunyu ya usiku.”

3 Nimekwisha yavua mavazi yangu, nitayavaaje tena? Nimekwisha nawa miguu yangu, niichafueje tena?

4 Hapo mpenzi wangu akaugusa mlango, moyo wangu ukajaa furaha.

5 Niliinuka kumfungulia mpenzi wangu. Mikono yangu imejaa manemane, na vidole vyangu vyadondosha manemane, nilipolishika komeo kufungua mlango.

6 Nilimfungulia mlango mpenzi wangu, lakini kumbe, alikuwa amekwisha toweka. Moyo wangu ulifurahi alipokuwa akizungumza! Nilimtafuta, lakini sikumpata; nilimwita, lakini hakuniitikia.

7 Walinzi wa mji waliniona, walipokuwa wanazunguka mjini; wakanipiga na kunijeruhi; nao walinzi wa lango wakaninyanganya shela langu.

8 Nawasihini, enyi wanawake wa Yerusalemu, mkimwona mpenzi wangu, mwelezeni kwamba naugua kwa mapenzi!

9 Ewe upendezaye kuliko wanawake wote! Kwani huyo mpenzi wako ana nini cha zaidi ya mpenzi mwingine, hata utusihi kwa moyo kiasi hicho?

10 Mpenzi wangu ni mzuri na mwenye nguvu, mashuhuri miongoni mwa wanaume elfu kumi.

11 Kichwa chake kizuri kama dhahabu safi, nywele zake ni za ukoka, nyeusi ti kama kunguru.

12 Macho yake ni kama ya hua kandokando ya kijito, ni kama njiwa waliooga maziwa kando ya kijito.

13 Mashavu yake ni kama matuta ya rihani kama bustani iliyojaa manukato na manemane. Midomo yake ni kama yungiyungi, imelowa manemane kwa wingi.

14 Mikono yake imewekwa bangili za dhahabu, amevalia johari za Tarshishi. Kiwiliwili chake ni kama pembe za ndovu zilizopambwa kwa vito vya johari ya rangi ya samawati.

15 Miguu yake ni kama nguzo za alabasta zilizosimikwa katika misingi ya dhahabu. Umbo lake ni kama Lebanoni, ni bora kama miti ya mierezi.

16 Kinywa chake kimejaa maneno matamu, kwa ujumla anapendeza. Basi, hivyo ndivyo alivyo mpenzi wangu, naam, ndivyo alivyo rafiki yangu, enyi wanawake wa Yerusalemu.

6

1 Ewe mwanamke uliye mzuri sana; amekwenda wapi huyo mpenzi wako? Ameelekea wapi mpenzi wako ili tupate kushirikiana nawe katika kumtafuta?

2 Mpenzi wangu amekwenda bustanini mwake, mahali ambapo rihani hustawi. Yeye analisha kondoo wake na kukusanya yungiyungi.

3 Mimi ni wake mpenzi wangu, naye ni wangu; yeye huwalisha kondoo wake penye yungiyungi.

4 Mpenzi wangu, wewe u mzuri kama Tirza, wapendeza kama Yerusalemu, unatisha kama jeshi lenye bendera.

5 Hebu tazama kando tafadhali; ukinitazama nahangaika. Nywele zako ni kama kundi la mbuzi, wateremkao chini ya milima ya Gileadi.

6 Meno yako kama kundi la kondoo majike wanaoteremka baada ya kuogeshwa. Kila mmoja amezaa mapacha, na hakuna yeyote aliyefiwa.

7 Mashavu yako ni kama nusu mbili za komamanga, nyuma ya shela lako.

8 Wapo malkia sitini, masuria themanini, na wasichana wasiohesabika!

9 Hua wangu, mzuri wangu, ni mmoja tu, na ni kipenzi cha mama yake; yeye ni wa pekee kwa mama yake. Wasichana humtazama na kumwita heri, nao malkia na masuria huziimba sifa zake.

10 Nani huyu atazamaye kama pambazuko? Mzuri kama mwezi, mwangavu kama jua, na anatisha kama jeshi lenye bendera.

11 Nimeingia katika bustani ya milozi kutazama machipuko ya bondeni, kuona kama mizabibu imechanua, na mikomamanga imechanua maua.

12 Bila kutazamia, mpenzi wangu, akanitia katika gari la mkuu.

13 Rudi, rudi ewe msichana wa Mshulami. Rudi, rudi tupate kukutazama. Mbona mwataka kunitazama miye Mshulami kana kwamba mnatazama ngoma kati ya majeshi mawili?

7

1 Nyayo zako katika viatu zapendeza sana! Ewe mwanamwali wa kifalme. Mapaja yako ya mviringo ni kama johari, kazi ya msanii hodari.

2 Kitovu chako ni kama bakuli lisilokosa divai iliyokolezwa. Tumbo lako ni kama lundo la ngano lililozungushiwa yungiyungi kandokando.

3 Matiti yako ni kama paa mapacha, ni kama swala wawili.

4 Shingo yako ni kama mnara wa pembe za ndovu; macho yako ni kama vidimbwi mjini Heshboni, karibu na mlango wa Beth-rabi. Pua yako ni kama mnara wa Lebanoni, ambao unauelekea mji wa Damasko.

5 Kichwa chako juu yako ni kama mlima Karmeli, nywele zako za ukoka zangaa kama zambarau; uzuri wako waweza kumteka hata mfalme.

6 Tazama ulivyo mzuri na wa kuvutia! Ewe mpenzi, mwali upendezaye!

7 Umbo lako lapendeza kama mtende, matiti yako ni kama shada za tende.

8 Nilisema nitaupanda mtende na kuzichuma shada za tende. Kwangu matiti yako ni kama shada za zabibu, harufu nzuri ya pumzi yako ni kama matofaa;

9 na kinywa chako ni kama divai tamu. Basi divai na itiririke hadi kwa mpenzi wangu, ipite juu ya midomo yake na meno yake!

10 Mimi ni wake mpenzi wangu, naye anionea sana shauku.

11 Njoo ewe mpenzi wangu, twende mashambani, twende zetu tukalale huko vijijini.

12 Tutaamka mapema, twende kwenye mashamba ya mizabibu, tukaone kama imeanza kuchipua, na kama maua ya zabibu yamekwisha kuchanua, pia kama mikomamanga imeanza kutoa maua. Huko ndiko nitakapokupatia pendo langu.

13 Harufu nzuri ya tunguja imejaa hewani karibu na milango yetu kuna kila aina ya matunda bora, yote mapya na ya siku za nyuma, ambayo nimekuwekea wewe mpenzi wangu.

8

1 Laiti ungekuwa kaka yangu, ambaye amenyonyeshwa na mama yangu! Hivyo, hata kama ningekutana nawe nje, ningekubusu na hakuna ambaye angenidharau.

2 Ningekuongoza na kukufikisha nyumbani kwa mama mzazi, mahali ambapo ungenifundisha upendo. Ningekupa divai nzuri iliyokolezwa, ningekupa divai yangu ya makomamanga yangu.

3 Mkono wako wa kushoto u chini ya kichwa changu, na mkono wako wa kulia wanikumbatia.

4 Nawasihini, enyi wanawake wa Yerusalemu, msiyachochee wala kuyaamsha mapenzi, hadi hapo wakati wake utakapofika.

5 Ni nani huyu ajaye kutoka mbugani, huku anamwegemea mpenzi wake? Chini ya mtofaa, mimi nilikuamsha, pale ambapo mama yako aliona uchungu, naam, pale ambapo mama yako alikuzaa.

6 Nipige kama mhuri moyoni mwako, naam, kama mhuri mikononi mwako. Maana pendo lina nguvu kama kifo, wivu nao ni mkatili kama kaburi. Mlipuko wake ni kama mlipuko wa moto, huwaka kama mwali wa moto.

7 Maji mengi hayawezi kamwe kulizima, mafuriko hayawezi kulizamisha. Mtu akijaribu kununua pendo, akalitolea mali yake yote, atakachopata ni dharau tupu.

8 Tunaye dada mdogo, ambaye bado hajaota matiti. Je, tumfanyie nini dada yetu siku atakapoposwa?

9 Kama angalikuwa ukuta, tungalimjengea mnara wa fedha; na kama angalikuwa mlango, tungalimhifadhi kwa mbao za mierezi.

10 Mimi nalikuwa ukuta, na matiti yangu kama minara yake. Machoni pake nalikuwa kama mwenye kuleta amani.

11 Solomoni alikuwa ana shamba la mizabibu, mahali paitwapo Baal-hamoni. Alilikodisha kwa walinzi; kila mmoja wao alilipa vipande elfu vya fedha.

12 Shamba langu la mizabibu ni shamba langu mwenyewe, naam, ni shamba langu binafsi! Basi, Solomoni, wewe ukae na elfu zako za fedha, na kila mlinzi wa matunda akae na mia mbili zake.

13 Ewe uliye shambani, rafiki zangu wanasikiliza sauti yako; hebu nami niisikie tafadhali!

14 Njoo haraka ewe mpenzi wangu, kama paa au mwanapaa dume juu ya milima ya manukato.