1 Neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Mika, mwenyeji wa Moreshethi, wakati Yothamu, Ahazi na Hezekia walipokuwa wafalme wa Yuda. Mika aliona mambo yote haya kuhusu Samaria na Yerusalemu.
2 Sikilizeni enyi watu wote; sikiliza ewe dunia na vyote vilivyomo. Mwenyezi-Mungu anakuja kuwashtaki, Bwana anena kutoka hekalu lake takatifu.
3 Naam! Mwenyezi-Mungu yuaja kutoka makao yake; atashuka na kutembea juu ya vilele vya dunia.
4 Milima itayeyuka chini ya nyayo zake, kama nta karibu na moto; mabonde yatapasuka, kama maji yaporomokayo kwenye mteremko.
5 Haya yote yatatukia kwa sababu ya makosa ya wazawa wa Yakobo, kwa sababu ya dhambi za wazawa wa Israeli. Je, uhalifu wa Yakobo waonekana wapi? Katika mji wake mkuu Samaria! Je, uhalifu wa Yuda waonekana wapi? Katika Yerusalemu kwenyewe!
6 Kwa hiyo, Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Mji wa Samaria nitaufanya magofu nyikani, shamba ambalo watu watapanda mizabibu. Mawe yaliyoujenga nitayatupa bondeni, na misingi yake nitaichimbuachimbua.
7 Sanamu zake zote zitavunjwavunjwa, kila kilichochumwa kitateketezwa kwa moto. Vinyago vyake vyote nitaviharibu. Vilirundikwa kutokana na ujira wa malaya, navyo vitatumiwa tena kulipia umalaya.”
8 Kwa sababu hiyo, mimi nitalia na kuomboleza; nitatembea uchi na bila viatu. Nitaomboleza na kulia kama mbweha, nitasikitika na kulia kama mbuni.
9 Majeraha ya Samaria hayaponyeki, nayo yameipata pia Yuda; yamefikia lango la Yerusalemu, mahali wanapokaa watu wangu.
10 Msiitangaze habari hii huko Gathi, wala msilie machozi! Huko Beth-leafra mgaegae mavumbini kwa huzuni.
11 Nendeni enyi wakazi wa Shafiri, mkiwa uchi na wenye haya. Wakazi wa Zaanani msitoke nje ya mji wenu. Watu wa Beth-ezeli wanalia; msaada wao kwenu umeondolewa.
12 Wakazi wa Marothi wanangojea msaada kwa hamu kubwa, lakini maangamizi yaja kutoka kwa Mwenyezi-Mungu karibu kabisa na lango la Yerusalemu.
13 Enyi wakazi wa Lakishi, fungeni farasi wepesi na magari ya vita. Nyinyi mlikuwa mmeiga dhambi ya watu wa Siyoni, makosa ya Waisraeli yalikuwa kwenu.
14 Hivyo, mnapaswa kuagana na kuwaacha wakazi wa Morasheth-gathi. Nao mji wa Akzibu hautawasaidia wafalme wa Israeli,
15 Enyi wakazi wa Maresha, Mungu atawaleteeni tena adui atakayewateka. Viongozi waheshimiwa wa Israeli watakimbilia pangoni huko Adulamu.
16 Enyi watu wa Yuda, nyoeni upara kuwaombolezea watoto wenu wapenzi; panueni upara wenu uwe mpana kama wa tai, maana watoto wenu watawaacha kwenda uhamishoni.
1 Ole wao wanaopanga kutenda maovu wanaolala usiku wakiazimia uovu! Mara tu kunapopambazuka, wanayatekeleza kwani wanao uwezo.
2 Hutamani mashamba na kuyatwaa; wakitaka nyumba, wananyakua. Huwadhulumu wenye nyumba na jamaa zao, huwanyang'anya watu mali zao.
3 Kwa hiyo, Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Ninapanga kuwaleteeni nyinyi maafa, ambayo kamwe hamtaweza kuyakwepa. Utakuwa wakati mbaya kwenu, wala hamtaweza kwenda kwa maringo.
4 Siku hiyo watu watawasimanga kwa wimbo, watalia na kuomboleza kwa uchungu, wakisema: ‘Tumeangamia kabisa; Mwenyezi-Mungu amechukua nchi yetu, naam, ameiondoa mikononi mwetu. Mashamba yetu amewagawia waliotuteka.’”
5 Kwa hiyo hamtagawiwa sehemu yoyote ya ardhi miongoni mwa watu wake Mwenyezi-Mungu.
6 “Usituhubirie sisi. Mambo kama hayo si ya kuhubiriwa. Sisi hatutakumbwa na maafa!
7 Je, yafaa kusema hivyo, wazawa wa Yakobo? Je, Mwenyezi-Mungu ameacha uvumilivu wake? Je, yeye hufanya mambo kama haya?” Sivyo! Maneno yangu huwafaa watendao mambo mema.
8 Lakini Mwenyezi-Mungu awaambia hivi: “Nyinyi mnawavamia watu wangu kama adui. Mnawanyang'anya mavazi yao watu watulivu; watu wanaopita kwenda zao bila wasiwasi, na wasio na fikira zozote za vita.
9 Mnawafukuza wake za watu wangu kutoka nyumba zao nzuri; watoto wao mmewaondolea fahari yangu milele.
10 Inukeni mwende zenu! Hapa hamna tena pa kupumzika! Kwa utovu wenu wa uaminifu maangamizi makubwa yanawangojea!
11 Kama mtu angetokea akatamka maneno matupu ya uongo na kusema: ‘Nawatabirieni divai na pombe kwa wingi’, mhubiri wa namna hiyo angependwa na watu hawa!
12 “Lakini kweli nitawakusanya nyote enyi watu wa Yakobo, naam, nitawakusanya enyi Waisraeli mliobaki, niwalete pamoja kama kondoo katika zizi, kama kundi kubwa la kondoo malishoni; nanyi mtakuwa kundi la watu wengi.”
13 Yule atakayetoboa njia atawatangulia, nao watalivunja lango la mji na kutoka nje, watapita na kutoka nje. Mfalme wao atawatangulia; Mwenyezi-Mungu mwenyewe atawatangulia.
1 Sasa sikilizeni enyi wakuu wa wazawa wa Yakobo, sikilizeni, enyi watawala wa wazawa wa Israeli! Nyinyi ndio mnaopaswa kujua mambo ya haki.
2 Lakini nyinyi mnachukia mema na kupenda maovu. Mnawachuna ngozi watu wangu, na kubambua nyama mifupani mwao.
3 Mnajilisha kwa nyama ya watu wangu mnawachuna ngozi yao, mnaivunjavunja mifupa yao, na kuwakatakata kama nyama ya kupika, kama nyama ya kutia ndani ya chungu.
4 Wakati unakuja ambapo mtamlilia Mwenyezi-Mungu, lakini yeye hatawajibu. Atauficha uso wake wakati huo, kwa sababu mmetenda mambo maovu.
5 Mwenyezi-Mungu asema hivi kuhusu manabii wanaowapotosha watu wake; manabii ambao hutabiri amani wakipewa kitu, lakini huwatishia watu kwa vita wasipopewa kitu:
6 “Kwenu manabii kutakuwa usiku bila maono, kutakuwa giza kwenu bila ufunuo. Kwenu manabii kutakuchwa, mchana utakuwa giza kwenu.”
7 Mabingwa wa maono watafedheheka, mafundi wa kubashiri wataaibishwa; wote watafunga midomo yao, maana hawatapata jibu lolote kutoka kwa Mungu.
8 Lakini kwa upande wangu, nimejazwa nguvu na roho ya Mwenyezi-Mungu; nimejaliwa kujua haki na kuwa na uwezo niwatangazie wazawa wa Yakobo kosa lao, niwaambie Waisraeli dhambi yao.
9 Sikieni jambo hili enyi viongozi wa wazawa wa Yakobo, sikilizeni, enyi watawala wa Waisraeli: Nyinyi mnachukia mambo ya haki na kupotosha mambo ya adili.
10 Nyinyi mnajenga mji wa Siyoni kwa damu, naam, mji wa Yerusalemu kwa dhuluma.
11 Waamuzi hufanya kazi yao kwa rushwa, makuhani wake hufundisha kwa malipo, manabii hutabiri kwa fedha. Hata hivyo hujidai kumtegemea Mwenyezi-Mungu, wakisema, “Mwenyezi-Mungu, si yupo pamoja nasi? Hatutapatwa na madhara yoyote!”
12 Haya! Kwa sababu yenu, Siyoni utalimwa kama shamba, Yerusalemu utakuwa magofu, nao mlima wa hekalu utakuwa msitu.
1 Utakuja wakati ambapo mlima wa nyumba ya Mwenyezi-Mungu utakuwa mkubwa kuliko milima yote. Naam, utakwezwa juu ya vilima vyote. Watu wengi watamiminika huko,
2 mataifa mengi yataujia na kusema: “Twendeni juu kwenye mlima wa Mwenyezi-Mungu, twende katika nyumba ya Mungu wa Yakobo, ili atufundishe njia zake, nasi tufuate nyayo zake. Maana mwongozo utatoka huko Siyoni; neno la Mwenyezi-Mungu huko Yerusalemu.”
3 Mungu atasuluhisha mizozo ya mataifa mengi, atakata mashauri ya mataifa makubwa ya mbali. Nayo yatafua mapanga yao kuwa majembe, na mikuki yao kuwa miundu ya kupogolea. Taifa halitapigana na taifa lingine, wala hayatafanya tena mazoezi ya vita.
4 Kila mtu atakaa kwa amani chini ya mitini na mizabibu yake, bila kutishwa na mtu yeyote. Mwenyezi-Mungu wa majeshi, ametamka yeye mwenyewe.
5 Mataifa mengine hufuata njia zao, kwa kuitegemea miungu yao, lakini sisi twafuata njia zetu kwa kumtegemea Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, milele na milele.
6 Mwenyezi-Mungu asema, “Siku ile nitawakusanya walemavu, naam, nitawakusanya waliochukuliwa uhamishoni, watu wale ambao niliwaadhibu.
7 Hao walemavu ndio watakaobaki hai; hao waliochukuliwa uhamishoni watakuwa taifa lenye nguvu. Nami Mwenyezi-Mungu nitawatawala mlimani Siyoni, tangu wakati huo na hata milele.”
8 Nawe kilima cha Yerusalemu, wewe ngome ya Siyoni, ambamo Mungu anafanya ulinzi juu ya watu wake, kama mchungaji juu ya kondoo wake; wewe utakuwa tena mji maarufu kama hapo awali, Yerusalemu utakuwa tena mji mkuu wa mfalme.
9 Sasa kwa nini mnalia kwa sauti? Je, hamna mfalme tena? Mshauri wenu ametoweka? Mnapaza sauti ya uchungu, kama mama anayejifungua!
10 Enyi watu wa Siyoni, lieni na kugaagaa kama mama anayejifungua! Maana sasa mtaondoka katika mji huu mwende kukaa nyikani, mtakwenda mpaka Babuloni. Lakini huko, mtaokolewa. Huko Mwenyezi-Mungu atawakomboa makuchani mwa adui zenu.
11 Mataifa mengi yamekusanyika kuwashambulia. Yanasema: “Acheni mji wao utiwe najisi, nasi tuyaone magofu ya Siyoni!”
12 Lakini wao hawafahamu mawazo ya Mwenyezi-Mungu wala hawaelewi mpango wake: Kwamba amewakusanya pamoja, kama miganda mahali pa kupuria.
13 Mwenyezi-Mungu asema, “Enyi watu wa Siyoni, inukeni mkawaadhibu adui zenu! Nitawapeni nguvu kama fahali mwenye pembe za chuma na kwato za shaba. Mtawasaga watu wa mataifa mengi; mapato yao mtaniwekea wakfu mimi, mali zao mtanitolea mimi Bwana wa dunia yote.”
1 Jumuikeni mkajikusanye enyi watu wa Yerusalemu; mkisema: “Tumezingirwa, tumesongwa; naye kiongozi wa Israeli wanampiga shavuni kwa fimbo.”
2 Mwenyezi-Mungu asema, “Lakini wewe Bethlehemu katika Efratha, wewe ni mdogo tu kati ya jamii za Yuda, lakini kwako kutatoka mtawala atakayetawala juu ya Israeli kwa niaba yangu. Asili yake ni ya zama za kale.”
3 Hivyo Mungu atawaacha watu wake kwa maadui, mpaka yule mama mjamzito atakapojifungua. Kisha ndugu zake waliobakia, watarudi na kuungana na Waisraeli wenzao.
4 Huyo mtawala atawachunga watu wake kwa nguvu ya Mwenyezi-Mungu, kwa fahari yake Mwenyezi-Mungu, Mungu wake. Watu wake wataishi kwa usalama, maana atakuwa mkuu mpaka miisho ya dunia.
5 Yeye ndiye atakayeleta amani. Waashuru wakivamia nchi yetu, na kuupenya ulinzi wetu, tutapeleka walinzi wawakabili, naam, tutawapeleka viongozi wetu kwa wingi.
6 Kwa silaha zao wataitawala nchi ya Ashuru, na kuimiliki nchi ya Nimrodi. Watatuokoa mikononi mwa Waashuru, watakapowasili mipakani mwa nchi yetu na kuanza kuivamia nchi yetu.
7 Wazawa wa Yakobo watakaobaki hai wameenea miongoni mwa mataifa mengi, watakuwa kama umande wa Mwenyezi-Mungu uburudishao, kama manyunyu yaangukayo penye nyasi ambayo hayasababishwi na mtu wala kumtegemea binadamu.
8 Wazawa wa Yakobo watakaobaki hai, wameenea miongoni mwa mataifa na watu wengi watakuwa na nguvu kubwa kama simba kati ya wanyama wa porini, kama mwanasimba miongoni mwa makundi ya kondoo, ambaye kila mahali apitapo, huyarukia na kuyararua mawindo yake, asiwepo mtu yeyote wa kuyaokoa.
9 Waisraeli watawashinda adui zao na kuwaangamiza kabisa.
10 Mwenyezi-Mungu asema, “Wakati huo nitawaondoa farasi wenu, na kuyaharibu magari yenu ya farasi.
11 Nitaiharibu miji ya nchi yenu, na kuzibomolea mbali ngome zenu.
12 Nitatokomeza matendo yenu ya uchawi, nanyi hamtakuwa tena na wapiga ramli.
13 Nitaziharibu sanamu zenu, na nguzo zenu za ibada; nanyi mtakoma kuabudu vitu mlivyotengeneza wenyewe.
14 Nitazing'oa sanamu za Ashera kutoka kwenu, na kuiangamiza miji yenu.
15 Kwa hasira na ghadhabu yangu, nitalipiza kisasi mataifa yote yasiyonitii.”
1 Sikilizeni anachosema Mwenyezi-Mungu: “Wewe nabii, nenda ukailalamikie milima, navyo vilima visikie sauti yako.”
2 Sikilizeni kesi ya Mwenyezi-Mungu enyi milima, sikilizeni enyi misingi ya kudumu ya dunia! Mwenyezi-Mungu anayo kesi dhidi ya watu wake. Yeye atatoa mashtaka dhidi ya Waisraeli.
3 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Enyi watu wangu, nimewatendea nini? Nimewachosha kwa kitu gani? Nijibuni!
4 Mimi niliwatoa nchini Misri; niliwakomboa kutoka utumwani; niliwapeni Mose, Aroni na Miriamu kuwaongoza.
5 Enyi watu wangu, kumbukeni njama za Balaki mfalme wa Moabu, na jinsi Balaamu mwana wa Beori alivyomjibu. Kumbukeni yaliyotukia njiani kati ya Shitimu na Gilgali. Kumbukeni mtambue matendo yangu ya kuwaokoa!”
6 Nimwendee Mwenyezi-Mungu na kitu gani, nipate kumwabudu Mungu aliye juu? Je, nimwendee na sadaka za kuteketezwa, nimtolee ndama wa mwaka mmoja?
7 Je, Mwenyezi-Mungu atapendezwa nikimtolea maelfu ya kondoo madume, au mito elfu na elfu ya mafuta? Je, nimtolee mzaliwa wangu wa kwanza kwa ajili ya kosa langu, naam, mtoto wangu kwa ajili ya dhambi yangu?
8 Mungu amekuonesha yaliyo mema, ewe mtu; anachotaka Mwenyezi-Mungu kwako ni hiki: Kutenda mambo ya haki, kupenda kuwa na huruma, na kuishi kwa unyenyekevu na Mungu wako.
9 Mwenyezi-Mungu anawaita wakazi wa mji, na ni jambo la busara sana kumcha yeye: “Sikilizeni, enyi watu wa Yuda; sikilizeni enyi mliokusanyika mjini.
10 “Je, nitavumilia maovu yaliyorundikwa nyumbani mwao, mali zilizopatikana kwa udanganyifu, na matumizi ya mizani danganyifu, jambo ambalo ni chukizo?
11 Je, naweza kusema hawana hatia watu wanaotumia mizani ya danganyifu na mawe ya kupimia yasiyo halali?
12 Matajiri wa miji wamejaa dhuluma, wakazi wake husema uongo, kila wasemacho ni udanganyifu.
13 Kwa hiyo nami, nimeanza kuwaangusha chini, na kuwaangamiza kwa sababu ya dhambi zenu.
14 Mtakula lakini hamtashiba; ndani mwenu njaa itazidi kuwauma. Mkiweka akiba haitahifadhiwa, na mkihifadhi kitu nitakiharibu kwa vita.
15 Mtapanda mbegu, lakini hamtavuna. Mtasindika zeituni, lakini hamtatumia hayo mafuta. Mtasindika zabibu, lakini hamtakunywa hiyo divai.
16 Nyinyi mnafuata mfano mbaya wa mfalme Omri na mfano wa jamaa ya mfalme Ahabu na mfano mbaya wa jamaa ya mwanawe, Ahabu, na mmefuata mashauri yao. Kwa hiyo nitawaleteeni maangamizi, na kila mtu atawadharau. Watu watawadhihaki kila mahali.”
1 Ole wangu! Hali ilivyo ni kama baada ya mavuno; hakuna tini za mwanzoni ninazotamani. Ni kama wakati wa kuchuma zabibu hakuna hata shada moja la zabibu la kula!
2 Hakuna mcha Mungu aliyebaki nchini, hakuna mtu yeyote mnyofu miongoni mwa watu. Kila mmoja anavizia kumwaga damu; kila mmoja anamwinda mwenzake amnase.
3 Wote ni mabingwa wa kutenda maovu; viongozi na mahakimu hutaka rushwa. Wakubwa huonesha wazi nia zao mbaya, na kufanya hila kuzitekeleza.
4 Mwema zaidi kati yao hutaabisha kama mbigili, aliye mnyofu zaidi ni kama ua wa miiba. Siku iliyongojewa ya adhabu yao imefika. Na sasa mahangaiko yamewakumba.
5 Usimwamini mwenzako, wala usimtumainie rafiki yako. Chunga unachosema kwa mdomo wako, hata na mke wako wewe mwenyewe.
6 Maana, mtoto wa kiume anamdharau baba yake; mtoto wa kike anashindana na mama yake, mke wa mwana anapingana na mama mkwe wake. Maadui wa mtu ni watu wa nyumbani mwake.
7 Lakini mimi namtumainia Mwenyezi-Mungu, namtazamia Mungu mwenye kuniokoa; Mungu wangu atanisikiliza.
8 Usifurahie maafa yangu ewe adui yangu! Nikianguka, nitainuka tena; Nikiwa gizani, Mwenyezi-Mungu ni mwanga wangu.
9 Kwa vile nimemkosea Mwenyezi-Mungu, sina budi kuvumilia ghadhabu yake, mpaka atakapotetea kisa changu na kunijalia haki yangu. Atanileta nje kwenye mwanga, nami nitaona akithibitisha haki.
10 Hapo adui yangu ataona hayo naye atajaa aibu; maana aliniambia: “Wapi basi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako?” Mimi mwenyewe nitamwona adui akianguka; atakanyagwakanyagwa chini kama tope la njiani.
11 Siku yaja ambapo kuta za mji wenu zitajengwa upya. Siku hiyo mipaka ya nchi yenu itapanuliwa.
12 Siku hiyo ndugu zenu watawarudia, kutoka Ashuru na vijiji vya Misri, kutoka nchi ya Misri na eneo la Eufrate; kutoka sehemu za maji na sehemu za milima.
13 Lakini nchi yote nyingine itakuwa jangwa, kwa sababu ya uovu wa wakazi wake.
14 Ee Mungu, uwachunge watu wako kwa fimbo yako, uwachunge hao walio kundi lako mwenyewe ambao wanaishi peke yao katika msitu wamezungukwa na ardhi yenye rutuba. Uwachunge kama ulivyofanya pale awali katika malisho ya Bashani na Gileadi.
15 Kama wakati ulipotutoa nchini Misri, utuoneshe tena maajabu yako.
16 Nao watu wa mataifa watakapoona hayo, watajaa fedheha hata kama wana nguvu. Watashikwa na bumbuazi na kukosa cha kusema na kuwa kama viziwi.
17 Watatambaa mavumbini kama nyoka; naam, kama viumbe watambaao. Watatoka katika ngome zao huku wanatetemeka na kujaa hofu. Watakugeukia wewe Mungu wetu kwa hofu, wataogopa kwa sababu yako.
18 Ee Mungu, ni nani aliye kama wewe? Wewe wasamehe dhambi za watu wako waliobaki, wala huyaangalii makosa yao. Hasira yako haidumu milele, ila wapendelea zaidi kutuonesha fadhili zako.
19 Utatuhurumia tena, ee Mwenyezi-Mungu; utafutilia mbali dhambi zetu, utazitupa zote katika vilindi vya bahari.
20 Utaonesha uaminifu wako na rehema zako kwa wazawa wa Abrahamu na wa Yakobo, kama ulivyowaahidi wazee wetu tangu zamani.