1 Yafuatayo ni maneno ya Mhubiri mwana wa Daudi, aliyekuwa mfalme huko Yerusalemu.
2 Bure kabisa, bure kabisa, nakuambia mimi Mhubiri! Kila kitu ni bure kabisa!
3 Binadamu hufaidi nini kwa jasho lake lote hapa duniani?
4 Kizazi chapita na kingine chaja, lakini dunia yadumu daima.
5 Jua lachomoza na kutua; laharakisha kwenda machweoni.
6 Upepo wavuma kusini, wazunguka hadi kaskazini. Wavuma na kuvuma tena, warudia mzunguko wake daima.
7 Mito yote hutiririkia baharini, lakini bahari kamwe haijai; huko ambako mito hutiririkia ndiko huko inakotoka tena.
8 Mambo yote husababisha uchovu, uchovu mkubwa usioelezeka. Jicho halichoki kuona, wala sikio kusikia.
9 Yaliyokuwako ndio yatakayokuwako, yaliyotendeka ndio yatakayotendeka; duniani hakuna jambo jipya.
10 Watu husema, “Tazama jambo jipya,” kumbe lilikwisha kuwako zama za kale.
11 Hakuna mtu anayekumbuka ya zamani wala atakayekumbuka yatakayotukia baadaye.
12 Mimi Mhubiri, nilikuwa mfalme wa Israeli, huko Yerusalemu.
13 Nilipania kuchunguza na kutafuta kwa hekima kila kitu kinachotukia duniani. Hiyo ni taabu kubwa ambayo Mungu amewapa wanadamu.
14 Nimeyaona yote yanayofanywa duniani; yote ni bure: Ni sawa na kufukuza upepo!
15 Kilichopindika hakiwezi kunyoshwa, kisichokuwapo hakiwezi kuhesabiwa.
16 Basi, nikatafakari nikisema, “Nimejipatia hekima nyingi zaidi kupita wote waliopata kutawala Yerusalemu kabla yangu. Naam, nina uzoefu wa hekima na maarifa.”
17 Nilipania kubainisha kati ya hekima, wazimu na upumbavu. Lakini niligundua kwamba kufanya hivyo ni sawa na kufukuza upepo.
18 Maana katika kuwa na hekima nyingi mna wasiwasi; na aongezaye maarifa zaidi huongeza huzuni zaidi.
1 Basi, nikawaza; “Ngoja nijitumbukize katika starehe, nijifurahishe.” Lakini, niligundua kwamba kufanya hivyo ni bure kabisa.
2 Nikasema kuhusu kicheko, “Ni wazimu”, na starehe “Mna faida gani?”
3 Nilifikiria sana, namna ya kujichangamsha akili kwa divai, huku nikisukumwa na ari yangu ya kupata hekima; pia namna ya kuandamana na upumbavu ili nione yaliyo bora kabisa ambayo wanadamu wanaweza wakafanya waishipo maisha yao mafupi hapa duniani.
4 Nilifanya mambo makuu: Nilijenga majumba na kujilimia mashamba ya mizabibu.
5 Nilijifanyia bustani na viunga, nikapanda miti ya matunda ya kila aina.
6 Nilijichimbia mabwawa ya maji ya kumwagilia hiyo miti.
7 Nilinunua watumwa, wanawake kwa wanaume, na wengine wakazaliwa nyumbani mwangu. Nilikuwa na mali nyingi, makundi ya ng'ombe na kondoo wengi kuliko mtu yeyote aliyenitangulia kukaa Yerusalemu.
8 Nilijirundikia fedha na dhahabu kutoka hazina za wafalme na toka mikoani, nami nilipata waimbaji wanaume kwa wanawake, na masuria watamaniwao.
9 Naam, nikawa mkuu, mkuu kuwapita wote waliopata kuwako Yerusalemu kabla yangu; na hekima yangu ikakaa ndani mwangu.
10 Kila macho yangu yalichokitamani nilikipata. Moyo wangu sikuunyima raha yoyote ile; kwa kuwa moyo wangu ulifurahia niliyotenda, na hili lilikuwa tuzo la jasho langu.
11 Kisha nikafikiria yote niliyokuwa nimefanya kwa mikono yangu, jinsi nilivyotoa jasho katika kufanya hayo. Nikagundua kwamba yote yalikuwa bure kabisa; ilikuwa ni sawa na kufukuza upepo, hapakuwapo faida yoyote chini ya mbingu.
12 Basi, nikaanza kufikiria maana ya kuwa na hekima, kuwa mwendawazimu, na kuwa mpumbavu. Nilijiuliza, “Mtawala mpya anaweza kufanya kitu gani?”
13 Basi, mimi nikagundua kwamba hekima ni bora kuliko upumbavu, kama mwanga ulivyo bora kuliko giza.
14 Mwenye hekima anayo macho, huona aendako, lakini mpumbavu hutembea gizani. Hata hivyo, nikatambua kwamba mwenye hekima na mpumbavu mwisho wao ni uleule.
15 Basi, nikasema moyoni mwangu, “Yatakayompata mpumbavu yatanipata na mimi pia. Kwa nini, basi, nimekuwa na hekima kiasi chote hiki?” Nikajibu, nikiwaza, “Hayo nayo ni bure kabisa.”
16 Maana hakuna amkumbukaye mwenye hekima, wala amkumbukaye mpumbavu, kwani siku zijazo wote watasahaulika. Jinsi mwenye hekima afavyo ndivyo afavyo mpumbavu!
17 Kwa hiyo, nikayachukia maisha, maana yote yatendekayo duniani yalinisikitisha. Yote yalikuwa bure kabisa; nilikuwa nikifukuza upepo.
18 Nilichukia kazi yangu yote niliyokuwa nimefanya hapa duniani, kuona kwamba ilinipasa nimwachie mtu ambaye atatawala baada yangu.
19 Tena, ni nani ajuaye kwamba atakuwa mwenye hekima au atakuwa mpumbavu? Hata hivyo, yeye atamiliki yote niliyofanya kwa kutumia hekima yangu hapa duniani. Pia hayo yote ni bure kabisa.
20 Basi, nilipofikiria tena juu ya yote niliyofanya duniani, nilikata tamaa.
21 Maana, wakati mwingine mtu ambaye amefanya kazi kwa kutumia hekima, akili na maarifa yake, humwachia mtu mwingine afurahie matunda ya kazi ambayo hakuitolea jasho. Pia hilo nalo ni bure kabisa; ni jambo baya sana.
22 Mtu anafaidi nini kutokana na kazi zake zote, na juhudi anazohangaika nazo duniani?
23 Kwa sababu maisha yake yote yamejaa taabu, na kazi yake ni mahangaiko matupu; hata usiku akili yake haipumziki! Hayo nayo ni bure kabisa.
24 Hakuna chema kimfaacho binadamu, isipokuwa kula na kunywa na kuifurahia kazi yake. Hili nalo nimeliona kuwa latoka kwa Mungu,
25 maana usipojaliwa na Mungu, huwezi kupata chakula wala kujifurahisha.
26 Mungu humjalia mtu apendezwaye naye hekima, akili na furaha; lakini humpa mwenye dhambi kazi ya kuvuna na kurundika, kisha akampa anayempendeza yeye Mungu. Yote hayo pia ni bure kabisa; ni sawa na kufukuza upepo.
1 Kila kitu kina majira yake, kila jambo duniani lina wakati wake:
2 Wakati wa kuzaliwa na wakati wa kufa; wakati wa kupanda na wakati wa kuvuna kilichopandwa;
3 wakati wa kuua na wakati wa kuponya; wakati wa kubomoa na wakati wa kujenga;
4 wakati wa kulia na wakati wa kucheka; wakati wa kuomboleza na wakati wa kucheza;
5 wakati wa kutupa mawe na wakati wa kuyakusanya mawe pamoja; wakati wa kukumbatia na wakati wa kuacha kukumbatia;
6 wakati wa kutafuta na wakati wa kupoteza; wakati wa kuhifadhi na wakati wa kutupa;
7 wakati wa kurarua na wakati wa kushona; wakati wa kukaa kimya na wakati wa kuongea;
8 wakati wa kupenda na wakati wa kuchukia; wakati wa vita na wakati wa amani.
9 Mfanyakazi hufaidi nini kutokana na juhudi zake hizo?
10 Mimi nimeiona kazi ambayo binadamu amepewa na Mungu.
11 Mungu amekifanya kila kitu kiwe kizuri kwa wakati wake. Amempa binadamu hamu ya kujua mambo ya baadaye, lakini hajamjalia fursa ya kuelewa matendo yake Mungu tangu mwanzo mpaka mwisho.
12 Najua kwamba, kwa binadamu, liko jambo moja tu la kumfaa; kufurahi na kujifurahisha muda wote aishipo.
13 Sote inatupasa kula na kunywa na kufurahia matunda ya kazi zetu. Hayo ni majaliwa ya Mungu.
14 Najua kwamba lolote atendalo Mungu linadumu milele. Hakuna kinachoweza kuongezwa wala kupunguzwa; Mungu amefanya mambo yawe hivyo kusudi wanadamu wamche yeye.
15 Kinachotukia sasa, kilikwisha tukia; kitakachotukia baadaye kilikwisha tukia; na Mungu hukifanya kitu kilekile kitukie tena na tena.
16 Zaidi ya hayo, nimegundua duniani kwamba, mahali pa haki na uadilifu, uovu unatawala.
17 Basi, nikasema moyoni mwangu, “Haidhuru! Mungu atawahukumu waadilifu, hali kadhalika na waovu, maana amepanga wakati maalumu kwa kila jambo na kwa kila kazi.”
18 Nikasema moyoni mwangu, “Mungu anawajaribu binadamu, ili kuwaonesha kwamba wao ni sawa tu na wanyama.”
19 Mwisho wa binadamu na mwisho wa mnyama ni uleule. Jinsi anavyokufa binadamu ndivyo anavyokufa mnyama. Wote hupumua namna ileile; binadamu si bora kuliko mnyama. Kwao yote ni bure kabisa.
20 Wote hufa na kwenda mahali pamoja. Wote wametoka mavumbini; na wote watarudi mavumbini,
21 Nani ajuaye, basi, kama kweli roho ya mtu hupaa juu, na roho ya mnyama hudidimia chini ardhini?
22 Ndipo nikatambua kwamba hakuna jambo lililo bora zaidi kwa binadamu kufanya kuliko kufurahia kazi yake, kwa sababu amepangiwa hivyo. Nani awezaye kumjulisha binadamu yale yatakayokuwa baada ya kufa kwake?
1 Kisha nikaona udhalimu wote unaofanyika duniani. Watu wanaokandamizwa hulia machozi, lakini hakuna yeyote anayewafariji. Wakandamizaji wao wana nguvu, ndiyo sababu hakuna wa kuwafariji.
2 Basi, nikafikiri moyoni kuwa wafu waliokwenda wasikorudi, wana nafuu zaidi kuliko watu walio hai.
3 Lakini ana heri zaidi kuliko wafu na walio hai, yule ambaye bado hajazaliwa na kuona maovu yote yanayotendwa hapa duniani.
4 Tena niligundua kwamba juhudi zote za mtu na ujuzi wake katika kazi vyatokana na kuoneana wivu. Hayo nayo ni bure kabisa; ni sawa na kufukuza upepo.
5 Mpumbavu hafanyi kazi na mwisho hujiua kwa njaa.
6 Ni afadhali kuwa na kidogo tu, pamoja na amani moyoni, kuliko kuwa na mengi, pamoja na taabu; sawa tu na kufukuza upepo.
7 Tena, niliona jambo moja bure kabisa duniani.
8 Nilimwona mtu mmoja asiye na mwana wala ndugu; hata hivyo, haachi kufanya kazi; hatosheki kamwe na mali yake; wala hatulii na kujiuliza: “Ninamfanyia nani kazi na kujinyima starehe?” Hilo nalo ni bure kabisa; ni shughuli inayosikitisha.
9 Ni afadhali kuwa wawili kuliko mtu kuwa peke yake. Kwa sababu wawili watapata tuzo la kazi yao.
10 Ikijatokea mmoja akaanguka, huyo mwenzake atamwinua. Lakini ole wake aliye peke yake akianguka! Huyo hatakuwa na mtu wa kumwinua!
11 Hali kadhalika, wawili wakilala pamoja watapata joto; lakini mtu akiwa peke yake atajipatiaje joto?
12 Mtu akiwa peke yake aweza kushindwa na adui, lakini wakiwa wawili watamkabili na kumshinda adui. Kamba tatu zikisokotwa pamoja hazikatiki kwa urahisi.
13 Afadhali kijana maskini mwenye hekima kuliko mfalme mzee mpumbavu, ambaye hasikilizi shauri jema;
14 hata ikiwa alikuwa mfungwa na sasa ni mfalme, au alizaliwa maskini na sasa ni mfalme.
15 Niliwaona watu wote waishio duniani, hata yule kijana ambaye angechukua nafasi ya mfalme.
16 Idadi ya watu haikuwa na kikomo, naye aliwatawala wote. Hata hivyo, wale wanaozaliwa baadaye hawatamfurahia. Hakika hayo nayo ni bure kabisa na kufukuza upepo.
1 Uwe mwangalifu uendapo katika nyumba ya Mungu, na kukaribia ili kusikiliza kwa makini kuliko kutambika kama watambikavyo wapumbavu, watu wasiopambanua kati ya jema na ovu.
2 Fikiri kabla ya kusema, wala usiwe mwepesi kusema chochote mbele ya Mungu, kwa maana Mungu yuko mbinguni na wewe uko duniani. Kwa hiyo usiseme mengi.
3 Kadiri mtu anavyohangaika zaidi, ndivyo atakavyoota ndoto; sauti ya mpumbavu ni maneno mengi.
4 Ukimwekea Mungu nadhiri, usikawie kuitimiza; na Mungu hapendezwi na wapumbavu. Tekeleza ulichoahidi.
5 Ni afadhali kutoweka nadhiri kuliko kuweka nadhiri kisha usiitimize.
6 Angalia mdomo wako usikuingize dhambini, halafu ikupase kumwambia mjumbe wa Mungu kwamba hukunuia kutenda dhambi. Ya nini kumfanya Mungu akukasirikie na kuiharibu kazi yako?
7 Ndoto zikizidi, kuna maangamizi na maneno huwa mengi. Jambo la maana ni kumcha Mungu.
8 Usishangae ukiona katika nchi watu fukara wanakandamizwa, wananyimwa haki zao na maslahi yao. Kila mwenye cheo anayewadhulumu wanyonge yupo chini ya mkuu mwingine, na juu ya hao wote kuna wakuu zaidi.
9 Hata hivyo, mfalme akijishughulisha na kilimo ni manufaa kwa wananchi wote.
10 Apendaye fedha hatatosheka na fedha; wala atamaniye mali hata akiipata hatatosheka. Hilo nalo ni bure kabisa.
11 Ongezeko la mali huleta ongezeko la walaji, naye mwenye mali yamfaa nini isipokuwa kuitazama tu mali yake?
12 Usingizi wa kibarua ni mtamu, awe ameshiba au amekula kidogo tu. Lakini usingizi wa tajiri ni wa wasiwasi daima, maana ziada ya mali yake humsumbua usiku kucha.
13 Tena, nimeona jambo moja ovu sana duniani: Mtu alijirundikia mali ikawa hatari kwake.
14 Kwa bahati mbaya, mali hiyo iliharibiwa katika matumizi mabaya, mwisho, mtu huyo hakuwa na chochote mkononi na alikuwa na mwana.
15 Kama vile binadamu alivyokuja duniani uchi toka tumboni mwa mama yake, ndivyo atakavyorudi uchi huko alikotoka. Hataweza kuchukua hata sehemu ndogo ya mapato ya kazi yake.
16 Hili nalo ni jambo baya sana. Atarudi kama alivyokuja. Amejisumbua kufukuza upepo, akatoka jasho bure.
17 Aliishi maisha yake yote katika giza na huzuni; katika mahangaiko, magonjwa na hasira.
18 Basi, haya ndiyo niliyogundua: Jambo zuri na la kufaa kwa binadamu ni kula, kunywa na kufurahia matunda ya jasho analotoa katika kazi anayoifanya hapa duniani, siku hizo chache za maisha aliyojaliwa na Mungu, maana hivyo ndivyo alivyopangiwa.
19 Kama Mungu anampa mtu utajiri na mali na kumjalia fursa ya kufurahia hayo, basi binadamu ashukuru na avifaidi hivyo alivyojipatia kwa jasho lake. Hiyo ni zawadi kutoka kwa Mungu.
20 Na kwa kuwa Mungu amemruhusu kuwa na furaha, binadamu hatakuwa na wasiwasi mwingi juu ya maisha yake mafupi.
1 Nimeona jambo moja ovu hapa duniani, linalowakandamiza watu:
2 Mungu humjalia mtu utajiri, mali na heshima, asitindikiwe kitu chochote anachotamani, lakini hampi uwezo wa kuvifurahia vitu hivyo; badala yake, mgeni fulani atavifaidi. Hilo nalo ni bure kabisa; ni jambo la mateso makali.
3 Mtu akiweza kuzaa watoto 100, na akaishi maisha marefu, lakini kama mtu huyo hafurahii maisha yake, wala hafanyiwi mazishi basi nasema mtoto aliyezaliwa amekufa ni afadhali kuliko mtu huyo.
4 Mtoto mfu hafaidiki chochote kwa kuzaliwa; yeye hutokomea gizani, akasahaulika.
5 Zaidi ya hayo, mtoto wa namna hiyo hakupata kuuona mwanga wa jua wala kutambua chochote. Hata hivyo, huyo mtoto angalau hupata pumziko ambapo yule mtu hapati.
6 Ingawa mtu huyo ataishi miaka elfu mbili, lakini hafurahii maisha, basi ni kama huyo mtoto wote wawili huenda mahali pamoja.
7 Kazi yote ya mtu ni kwa ajili ya kupata chakula, lakini tamaa yake ya kula haitoshelezwi kamwe.
8 Je, mtu mwenye hekima anayo nafuu zaidi kuliko mpumbavu? Na mtu maskini hupata faida gani akijua namna ya kuyakabili maisha?
9 Hayo nayo ni bure kabisa; ni sawa na kufukuza upepo. Afadhali kuridhika na ulicho nacho kuliko kuhangaika kwa kutamani kitu kingine.
10 Kila kitu kinachotukia kilikwisha pangwa hapo awali; hali ya binadamu inajulikana, na tunajua kwamba mnyonge hawezi kubishana na mtu mwenye nguvu zaidi.
11 Maneno mengi hayana faida, hayamwinui binadamu.
12 Nani ajuaye yamfaayo mtu katika maisha haya mafupi yasiyo na faida, maisha ambayo hupita kama kivuli? Nani duniani ajuaye yatakayompata mtu baada ya kufa?
1 Sifa njema ni bora kuliko marashi ya thamani. Siku ya kufa ni bora kuliko siku ya kuzaliwa.
2 Afadhali kwenda kwenye matanga, kuliko kwenda kwenye karamu, kwa sababu walio hai yawapasa kukumbuka kwamba kifo chatungojea sisi sote.
3 Huzuni ni afadhali kuliko kicheko maana, huzuni ya uso ni faida ya moyo.
4 Moyo wa mwenye hekima huthamini matanga, lakini moyo wa mpumbavu hupenda raha.
5 Afadhali kusikia maonyo ya wenye hekima kuliko kusikiliza nyimbo za wapumbavu.
6 Maana, kicheko cha mpumbavu ni kama mlio wa miiba motoni. Hayo nayo ni bure kabisa.
7 Mwenye hekima akimdhulumu mtu; hujifanya mwenyewe kuwa mpumbavu kupokea rushwa hupotosha akili.
8 Mwisho wa jambo ni afadhali kuliko mwanzo wake; mvumilivu rohoni ni bora kuliko mwenye majivuno.
9 Usiwe mwepesi wa hasira, maana, hasira hukaa ndani ya wapumbavu.
10 Usiulize, “Kwa nini nyakati za kale zilikuwa bora kuliko za sasa?” Huulizi hivyo kwa kutumia hekima.
11 Hekima ni ya thamani kubwa kama urithi; ni muhimu kwa wale wote walio hai.
12 Kulindwa na hekima ni kama kulindwa na fedha. Faida ya maarifa ni kwamba hekima hulinda maisha ya mtu aliye nayo.
13 Tafakarini vema kazi yake Mungu; ni nani awezaye kunyosha alichopinda Mungu?
14 Katika siku za fanaka uwe na furaha; katika siku za maafa utafakari jambo hili: Fanaka, pia maafa, Mungu amefanya hiyo ya kwanza iambatane na ya pili ili binadamu asiweze kujua yatakayotukia baada yake.
15 Katika maisha yangu duni, nimeona kila kitu; mtu mwadilifu hufa ingawa ni mwadilifu, ambapo mtu mwovu huendelea kuishi maisha marefu ingawa ni mwovu.
16 Basi, usiwe mwadilifu sana, wala usiwe mwenye hekima mno! Ya nini kujiangamiza wewe mwenyewe?
17 Lakini pia, usiwe mwovu sana wala usiwe mpumbavu! Ya nini kufa kabla ya wakati wako?
18 Inakupasa ushike la kwanza na la pili pia; maana anayemtii Mungu atajengwa kwayo.
19 Hekima humfanya mwenye busara kuwa na nguvu zaidi kuliko watawala kumi mjini.
20 Hakika, hakuna mtu mwadilifu duniani atendaye mema daima bila kutenda dhambi.
21 Usitie maanani maneno yote wasemayo wanadamu, usije ukamsikia mtumishi wako akikutukana.
22 Wewe mwenyewe wajua moyoni kwamba umeapiza wengine mara nyingi.
23 Nimeyapima hayo yote kwa hekima; nikajisemea: “Nataka kuwa mwenye hekima!” Lakini hekima iko mbali sana nami.
24 Jinsi gani binadamu ataweza kugundua maana ya maisha; jambo hilo ni zito na gumu mno kwetu!
25 Hata hivyo, nilipania kujua na kuchunguza na kutafuta hekima na maana ya mambo yaliyoko, na pia kujua uovu ni upuuzi, na upumbavu ni wazimu.
26 Jambo moja nililogundua lililo baya zaidi kuliko kifo, ni mwanamke ambaye moyo wake ni mtego na wavu, na mikono yake ni kama minyororo. Lakini anayempendeza Mungu humkwepa mwanamke huyo, lakini mwenye dhambi hunaswa naye.
27 Haya, nakuambia mimi Mhubiri, ndio niliyogundua nilipofanya uchunguzi wangu kidogokidogo.
28 Nilipania kugundua mambo hayo tena na tena, lakini sikufaulu. Kati ya wanaume elfu moja, nilifaulu kumwona mwanamume mmoja, anayestahili heshima, lakini kati ya wanawake wote kama hao sikumwona hata mmoja anayestahili heshima.
29 Tazama, nimegundua jambo hili moja: Kwamba Mungu aliwaumba wanadamu wanyofu, lakini wao wenyewe wamejitafutia matatizo.
1 Nani aliye kama mwenye hekima? Nani ajuaye hali halisi ya vitu? Hekima humletea mtu tabasamu, huubadilisha uso wake mwenye huzuni.
2 Tii amri ya mfalme, kwa sababu ya kiapo chako kitakatifu.
3 Usifanye haraka kuondoka mbele yake; wala usiwe na kiburi juu ya jambo baya, maana mfalme hufanya apendavyo.
4 Amri ya mfalme ni kauli ya mwisho; nani athubutuye kumwuliza, “Unafanya nini?”
5 Anayetii amri hatapata madhara, na mwenye hekima atajua kuna wakati na njia.
6 Naam, kila kitu kina wakati wake na njia yake, ingawa binadamu anakabiliwa na tatizo kubwa:
7 Hajui ni nini kitakachotukia baadaye, kwani nani awezaye kumjulisha yatakayotukia baadaye?
8 Hakuna mtu aliye na uwezo wa kushikilia roho yake asife; hakuna mtu aliye na uwezo juu ya siku ya kufa. Wakati wa vita hakuna kuponyoka, na uovu hauwezi kumwokoa mwovu.
9 Haya yote nimeyaona katika uchunguzi wangu juu ya yote yanayotendwa hapa duniani, binadamu anapokuwa na uwezo wa kumkandamiza na kumdhuru binadamu mwenzake.
10 Tena, nimewaona waovu wakizikwa, na watu waliporudi kutoka mahali patakatifu wanawasifu humohumo mjini walimotenda maovu yao. Hayo nayo ni bure kabisa.
11 Kwa vile uovu haupatilizwi haraka, mioyo ya wanadamu hupania kutenda mabaya.
12 Wenye dhambi hutenda maovu mara mia, hata hivyo, huendelea kuishi. Walakini, mimi najua kwamba itakuwa heri kwao wamchao Mungu, kwa sababu ya uchaji wao;
13 lakini hakuna furaha kwa waovu. Wao watapita kama kivuli, maisha yao hayatakuwa marefu kwa sababu hawamchi Mungu.
14 Kuna jambo moja, bure kabisa nililoligundua hapa duniani: Watu wema hutendewa wastahilivyo waovu, nao waovu hutendewa wastahilivyo watu wema. Hili nalo nasema ni bure kabisa.
15 Basi, mimi nasisitiza kuwa mtu ni lazima afaidi raha, kwa kuwa hapa duniani hakuna kilicho kizuri zaidi kuliko kula na kunywa na kujifurahisha. Hayo ndio awezayo kufanya mtu anaposhughulika na kazi katika muda wa maisha yake aliyojaliwa na Mungu duniani.
16 Kila nilipojaribu kujua hekima na kuona yanayotendeka hapa duniani, niligundua kwamba unaweza kukaa macho mchana na usiku,
17 halafu niliona kazi yote ya Mungu ya kwamba mwanadamu hawezi kuelewa kazi inayofanyika duniani. Wenye hekima wanaweza kujidai eti wanajua, lakini, kwa kweli, hawajui.
1 Nilitafakari juu ya hayo yote, nikaona kwamba Mungu anaongoza matendo ya watu wenye hekima na waadilifu; ikiwa ni upendo au chuki, binadamu hajui. Kila kitu kwao ni bure kabisa,
2 maana mwisho uleule huwapata waadilifu na waovu, wema na wabaya, walio safi na walio najisi, wenye kutoa sadaka na wasiotoa sadaka. Aliye mwema ni sawa tu na mwenye dhambi, na mwenye kuapa si tofauti na asiyeapa.
3 Hili ni jambo baya zaidi kati ya yote yatukiayo hapa duniani, kwamba mwisho uleule huwapata wote. Tena, wakati wote wa maisha yao, wanadamu huwa wamejaa uovu na wazimu, na kisha hufa.
4 Lakini anayeambatana na walio hai analo bado tumaini, afadhali mbwa hai kuliko simba mfu.
5 Maana, walio hai hujua ya kwamba watakufa, lakini wafu hawajui chochote. Hawana tuzo tena; hata kumbukumbu lao limesahauliwa kabisa.
6 Upendo wao, chuki zao na tamaa zao, vyote vimetoweka pamoja nao, na wala hawatashiriki chochote hapa duniani.
7 Nenda ukale chakula chako kwa furaha, ukanywe na divai yako kwa moyo mchangamfu, maana Mungu amekwisha ikubali kazi yako.
8 Vaa vizuri, jipake mafuta kichwani.
9 Furahia maisha pamoja na mke wako umpendaye muda wote wa maisha yako ya bure ambayo Mungu amekujalia hapa duniani; maana hilo ndilo ulilopangiwa maishani, katika kazi zako hapa duniani.
10 Kila unachotaka kufanya kifanye kwa nguvu zako zote, maana, hakuna kazi, wala wazo, wala maarifa, wala hekima huko kuzimu unakokwenda.
11 Tena, nimeona kitu kimoja hapa duniani, kwamba wenye mbio hawafaulu katika riadha, wala wenye nguvu hawashindi vita; wenye busara hawapati chakula, wenye akili hawatajiriki, wala wenye ujuzi hawapandi vyeo; lakini wakati wa bahati huwapata wote pamoja.
12 Mtu hajui saa yake itafika lini. Kama vile samaki wanavyonaswa katika wavu kwa bahati mbaya, na kama vile ndege wanavyonaswa katika mtego kwa ghafla, ndivyo wanadamu wanavyonaswa na balaa inapowaangukia bila ya kutazamia.
13 Pia hapa duniani nimeona mfano wa hekima, na ulionekana kwangu kuwa wenye maana sana.
14 Palikuwa na mji mmoja mdogo wenye wakazi wachache. Mfalme mmoja mwenye nguvu akafika, akauzingira na kujiandaa kuushambulia.
15 Katika mji huo, alikuwapo maskini mmoja mwenye hekima, ambaye, kwa hekima yake aliuokoa mji huo. Lakini hakuna mtu aliyemkumbuka huyo maskini baadaye.
16 Basi, mimi nasema, hekima ni bora kuliko nguvu, ingawa hekima ya maskini haithaminiwi, na maneno yake hayasikilizwi.
17 Afadhali kusikiliza maneno matulivu ya mwenye hekima, kuliko kusikiliza kelele za mfalme katika kikao cha wapumbavu.
18 Kuwa na hekima ni bora kuliko kutegemea silaha, lakini mwenye dhambi mmoja huharibu mazuri mengi.
1 Nzi waliokufa husababisha marashi kunuka; upumbavu kidogo hubatilisha hekima na heshima.
2 Moyo wa mwenye hekima humwongoza kutenda yaliyo sawa; lakini mtu mpumbavu moyo wake humpotosha.
3 Hata apitapo njiani, mpumbavu hutambulikana hivyo, humjulisha kila mtu kwamba yeye ni mpumbavu.
4 Mtawala akikuwakia hasira, usijiuzulu; makosa makubwa huweza kufutwa ukiwa mnyenyekevu.
5 Kuna uovu niliogundua hapa duniani, uovu unaosababishwa na watawala:
6 Kwamba wapumbavu wanapewa kazi za madaraka ya juu, na matajiri wanachukua nafasi za mwisho.
7 Nimeona watumwa wanapanda farasi, na wakuu wanatembea kwa miguu kama watumwa.
8 Mchimba shimo hutumbukia mwenyewe, abomoaye ukuta huumwa na nyoka.
9 Mchonga mawe huumizwa nayo, mkata kuni hukabiliwa na hatari.
10 Nguvu nyingi zaidi zahitajika kwa mtumiaji shoka butu lisilonolewa, lakini kutumia hekima humfanya mtu afanikiwe.
11 Nyoka akiuma kabla hajachochewa, mchochezi hahitajiki tena.
12 Maneno ya mwenye hekima humnufaisha asemaye; lakini midomo ya mpumbavu humwangamiza.
13 Mpumbavu huanza kusema kwa maneno ya kijinga, na kumaliza kauli yake kwa wazimu mbaya.
14 Mpumbavu hububujika maneno. Binadamu hajui yatakayokuwako, wala yale yatakayotukia baada yake.
15 Mpumbavu huchoshwa na kazi yake hata asijue njia ya kurudia nyumbani.
16 Ole wako, ewe nchi, mtawala wako akiwa kijana, na viongozi wako wakifanya sherehe asubuhi.
17 Heri yako, ewe nchi, mtawala wako akiwa mtu wa heshima, na viongozi wako wakifanya sherehe wakati wa kufaa, ili kujipatia nguvu na si kujilewesha.
18 Kutokana na uvivu wa mtu, paa hubonyea; kwa sababu ya uzembe, nyumba huvuja.
19 Chakula ni kwa ajili ya kujifurahisha, divai huchangamsha maisha; na fedha husababisha hayo yote.
20 Usimwapize mtawala hata moyoni mwako, wala usimwapize tajiri hata chumbani mwako unakolala, kwa kuwa ndege ataisikia sauti yako, au kiumbe arukaye atatangaza maneno yako.
1 Jishughulishe na biashara hata kama kwa kubahatisha; yawezekana baadaye ukapata chochote kile.
2 Wagawie watu saba hata wanane sehemu yako, maana, hujui balaa litakalofika duniani.
3 Mawingu yakijaa maji, mvua hunyesha; mti ukiangukia kusini au kaskazini, hapo uangukiapo ndipo ulalapo.
4 Anayengoja upepo hatapanda mbegu, anayesubiri mawingu yatoweke, hatavuna kitu.
5 Usivyojua jinsi uhai unavyoingia katika mifupa ya mtoto tumboni mwa mamake, kadhalika huwezi kuelewa matendo ya Mungu, ambayo hufanya kila kitu.
6 Panda mbegu asubuhi na jioni usiache kupanda, maana, hujui zipi zitaota; za asubuhi, za jioni, au zote zitakuwa nzuri.
7 Mwanga wafaa, na kuliona jua kwapendeza macho.
8 Mtu akiishi miaka mingi, na aifurahie miaka hiyo yote; lakini akumbuke kuwa siku za giza zitakuwa nyingi, na kwamba yote yatakayofuata ni bure.
9 Ewe kijana, furahia ujana wako, moyo wako, uchangamke wakati ungali kijana. Fuata mapenzi ya moyo wako na upeo wa macho yako. Lakini kumbuka kwamba Mungu atakuhukumu kadiri ya hayo yote.
10 Ondoa mahangaiko moyoni mwako, jikinge, usipate maumivu mwilini kwa sababu ujana na mwisho wa maisha ni bure kabisa.
1 Umkumbuke Muumba wako siku za ujana wako, kabla hazijaja siku na miaka ambapo utasema: “Sifurahii tena vitu hivyo!”
2 Umkumbuke kabla ya wakati ambapo kwako mwanga wa jua utafifia; mwezi na nyota haviangazi tena, nayo mawingu yametanda tena baada ya mvua.
3 Wakati ambapo mikono inayokulinda inatetemeka, miguu yako imara imepindika, meno yako ya kusagia hayafai kwa uchache, na macho ya kuchungulia dirishani yamefifia.
4 Wakati ambapo milango ya masikio yako imezibika, na sauti za visagio ni hafifu; lakini usiku hata kwa sauti ya ndege utagutuka.
5 Wakati huo utaogopa kupanda mahali pa juu na kutembea barabarani ni kitisho; wakati miti ya mlozi inachanua na panzi wanashiba, lakini wewe hutakuwa na hamu tena. Wakati huo binadamu anapaswa kwenda katika makao yake ya milele, nao waombolezaji watapitapita barabarani.
6 Wakati huo uzi wa dhahabu utakatika, bakuli la dhahabu litapasuka, mtungi wa maji utavunjikia kisimani, kadhalika na gurudumu la kuvutia maji.
7 Nawe vumbi utarudia udongoni ulimotolewa na roho yako itamrudia Mungu aliyeiumba.
8 Mimi Mhubiri nasema: Yote ni bure kabisa! Yote ni bure.
9 Basi, zaidi ya kuwa na hekima yake, Mhubiri aliwafundisha watu ujuzi. Alizipima, akazichunguza na kuzirekebisha methali kwa ustadi mwingi.
10 Mhubiri alijitahidi kupata maneno ya kupendeza, akaandika kwa ufasaha maneno ya kweli.
11 Misemo ya wenye hekima ni kama michokoo na methali zilizokusanywa pamoja na mchungaji mmoja ni kama vigingi vilivyopigiliwa imara ardhini.
12 Zaidi ya hayo, mwanangu, jihadhari! Kuandika vitabu hakuna mwisho na kusoma kwingi huchokesha mwili.
13 Baada ya hayo yote yaliyokwisha semwa bado kuna hili linalotakiwa: Mche Mungu, na uzishike amri zake; kwa sababu hilo ndilo jukumu aliloumbiwa binadamu.
14 Maana, Mungu atahukumu matendo yetu yote, hata yale yanayotendwa kwa siri, yawe mema au mabaya.