1

1 Neno la Mwenyezi-Mungu lililomjia Yoeli, mwana wa Pethueli:

2 Sikilizeni kitu hiki enyi wazee; tegeni sikio wakazi wote wa Yuda! Je, jambo kama hili limewahi kutokea maishani mwenu, au nyakati za wazee wenu?

3 Wasimulieni watoto wenu jambo hili, nao wawasimulie watoto wao, na watoto wao wakisimulie kizazi kifuatacho.

4 Nzige, makundi kwa makundi, wameivamia mimea; kilichoachwa na nzige kimeliwa na tunutu, kilichoachwa na tunutu kimeliwa na parare, kilichoachwa na parare kimeliwa na matumatu.

5 Enyi walevi, levukeni na kulia; pigeni yowe, enyi walevi wa divai; zabibu zote za kutengeneza divai mpya zimeharibiwa.

6 Jeshi la nzige limeivamia nchi yetu; lina nguvu na ni kubwa ajabu; meno yake ni kama ya simba, na magego yake ni kama ya simba jike.

7 Limeiharibu mizabibu yetu, na kuitafuna mitini yetu. Limeyabambua magamba yake na kuyatupa chini, na matawi yake yameachwa meupe.

8 Lieni kama msichana aliyevaa vazi la gunia akiombolezea kifo cha mchumba wake.

9 Sadaka za nafaka na kinywaji zimetoweka nyumbani kwa Mwenyezi-Mungu. Makuhani, wahudumu wa Mwenyezi-Mungu, wanaomboleza.

10 Mashamba yamebaki matupu; nchi inaomboleza, maana nafaka imeharibiwa, divai imetoweka, mafuta yamekosekana.

11 Ombolezeni enyi wakulima; pigeni yowe enyi watunza mizabibu. Ngano na shayiri zimeharibika, mavuno yote shambani yameangamia.

12 Mizabibu imenyauka; mitini imedhoofika; mikomamanga, mitende na mitofaa imekauka, naam miti yote shambani imekauka. Furaha imetoweka miongoni mwa watu.

13 Enyi makuhani, jivikeni magunia kuomboleza, lieni enyi wahudumu wa madhabahu. Ingieni hekaluni mkaomboleze usiku kucha! Sadaka za nafaka na kinywaji zimetoweka nyumbani kwa Mungu.

14 Toeni amri watu wafunge; itisheni mkutano wa kidini. Kusanyeni wazee na wakazi wote wa nchi, nyumbani kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, na humo mkamlilie Mwenyezi-Mungu.

15 Ole wetu kwa ile siku ya Mwenyezi-Mungu, siku hiyo ya Mwenyezi-Mungu inakaribia; inakuja pamoja na maangamizi, kutoka kwa Mungu Mkuu.

16 Mazao yetu yameharibiwa huku tunatazama. Furaha na kicheko vimetoweka nyumbani kwa Mungu wetu.

17 Mbegu zinaoza udongoni; ghala za nafaka ni ukiwa mtupu, ghala zimeharibika, kwa kukosa nafaka ya kuhifadhi.

18 Tazama wanyama wanavyolia kwa huzuni! Makundi ya ng'ombe yanahangaika, kwa sababu yamekosa malisho; hata makundi ya kondoo yanateseka.

19 Ninakulilia wewe, ee Mwenyezi-Mungu, moto umemaliza malisho nyikani, miali ya moto imeteketeza miti mashambani.

20 Hata wanyama wa porini wanakulilia wewe, maana, vijito vya maji vimekauka, moto umemaliza malisho nyikani.

2

1 Pigeni tarumbeta huko Siyoni; pigeni baragumu juu ya mlima mtakatifu! Tetemekeni enyi wakazi wa Yuda, maana siku ya Mwenyezi-Mungu inakuja, naam, siku hiyo iko karibu!

2 Hiyo ni siku ya giza na huzuni; siku ya mawingu na giza nene. Jeshi kubwa la nzige linakaribia kama giza linalotanda milimani. Namna hiyo haijapata kuweko kamwe wala haitaonekana tena katika vizazi vyote vijavyo.

3 Kama vile moto uteketezavyo jeshi hilo laharibu kila kitu mbele yake na kuacha nyuma kila kitu kinateketezwa; kabla hawajapita, nchi ni kama bustani ya Edeni, lakini wakisha pita, ni jangwa tupu. Hakuna kiwezacho kuwaepa!

4 Wanaonekana kama farasi, wanashambulia kama farasi wa vita,

5 Wanaporukaruka kwenye vilele vya milima, wanarindima kama magari ya farasi, wanavuma kama mabua makavu motoni. Wamejipanga kama jeshi kubwa tayari kabisa kufanya vita.

6 Wakaribiapo, watu hujaa hofu, nyuso zao zinawaiva.

7 Wanashambulia kama mashujaa wa vita; kuta wanazipanda kama wanajeshi. Wote wanakwenda mbele moja kwa moja, bila hata mmoja wao kubadilisha njia.

8 Hakuna amsukumaye mwenziwe; kila mmoja anafuata mkondo wake. Wanapita kati ya vizuizi vya silaha, wala hakuna kiwezacho kuwazuia.

9 Wanauvamia mji, wanapiga mbio ukutani; wanaziparamia nyumba na kuingia, wanapenya madirishani kama wezi.

10 Nchi inatetemeka mbele yao, mbingu zinatikisika. Jua na mwezi vyatiwa giza, nazo nyota zinaacha kuangaza.

11 Mwenyezi-Mungu anaamuru jeshi lake kwa sauti; askari wake ni wengi mno, wanaomtii hawahesabiki. 2Siku ya Mwenyezi-Mungu kweli ni kuu na ya kutisha sana! Nani atakayeweza kuistahimili?

12 “Lakini hata sasa,” nasema mimi Mwenyezi-Mungu, “Nirudieni kwa moyo wote, kwa kufunga, kulia na kuomboleza.

13 Msirarue mavazi yenu kuonesha huzuni bali nirudieni kwa moyo wa toba.” Mrudieni Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu; yeye amejaa neema na huruma; hakasiriki upesi, ni mwingi wa fadhili; daima yu tayari kuacha kuadhibu.

14 Huenda Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, atabadili nia na kuwapeni baraka ya mazao, mkamtolea sadaka za nafaka na kinywaji.

15 Pigeni tarumbeta huko Siyoni! Toeni amri watu wafunge; itisheni mkutano wa kidini.

16 Wakusanyeni watu wote, wawekeni watu wakfu. Waleteni wazee, wakusanyeni watoto, hata watoto wanyonyao. Bwana arusi na bibi arusi na watoke vyumbani mwao.

17 Kati ya madhabahu na lango la hekalu, makuhani, wahudumu wa Mwenyezi-Mungu, walie na kuomba wakisema: “Wahurumie watu wako, ee Mwenyezi-Mungu. Usiyaache mataifa mengine yatudharau na kutudhihaki yakisema, ‘Yuko wapi basi Mungu wao?’”

18 Ndipo Mwenyezi-Mungu akaipenda nchi yake akawahurumia watu wake.

19 Alisikiliza, akajibu sala zao; akasema, “Sasa nitawapeni tena nafaka, sitawafanya mdharauliwe tena na mataifa.

20 Nitawaondoa hao adui watokao kaskazini, nitawafukuza mpaka jangwani; askari wa mbele nitawatupa katika Bahari ya Chumvi na wale wa nyuma katika Bahari ya Mediteranea. Watatoa uvundo na harufu mbaya, hao ambao wamefanya maovu makubwa.

21 “Usiogope, ewe nchi, bali furahi na kushangilia, maana Mwenyezi-Mungu ametenda makuu.

22 Msiogope, enyi wanyama. malisho ya nyikani yamekuwa mazuri, miti inazaa matunda yake, mizabibu na mitini zinazaa kwa wingi.

23 “Furahini, enyi watu wa Siyoni, shangilieni kwa sababu ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, maana amewapeni mvua za masika, amewapeni mvua ya kutosha: Mvua za masika na mvua za vuli kama hapo awali.

24 Mahali pa kupuria patajaa nafaka, mashinikizo yatafurika divai na mafuta.

25 Nitawarudishia miaka ile iliyoliwa na nzige, kila kitu kilicholiwa na tunutu, parare na matumatu, hilo jeshi kubwa nililowaletea!

26 Mtapata chakula kingi na kutosheka; mtalisifu jina la Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, aliyewatendea mambo ya ajabu. Watu wangu, kamwe hawatadharauliwa tena.

27 Mtatambua kwamba mimi nimo miongoni mwenu, enyi Waisraeli; kwamba mimi Mwenyezi-Mungu, ndimi Mungu wenu wala hakuna mwingine. Watu wangu, kamwe hawatadharauliwa tena.

28 “Kisha hapo baadaye nitaimimina roho yangu juu ya binadamu wote. Watoto wenu wa kike na wa kiume watatabiri, wazee wenu wataota ndoto, na vijana wenu wataona maono.

29 Hata juu ya watumishi wa kiume na wa kike, nitaimimina roho yangu wakati huo.

30 “Nitatoa ishara mbinguni na duniani; kutakuwa na damu, moto na minara ya moshi.

31 Jua litatiwa giza, na mwezi utakuwa mwekundu kama damu, kabla ya kufika siku ya Mwenyezi-Mungu, siku iliyo kuu na ya kutisha.

32 Hapo watu wote watakaoomba kwa jina la Mwenyezi-Mungu wataokolewa. Maana katika mlima Siyoni na Yerusalemu, watakuwako watu watakaosalimika, kama nilivyosema mimi Mwenyezi-Mungu.

3

1 “Wakati huo na siku hizo nitakapoirekebisha hali ya Yuda na Yerusalemu,

2 nitayakusanya mataifa yote, niyapeleke katika bonde liitwalo, ‘Mwenyezi-Mungu Ahukumu. Huko nitayahukumu mataifa hayo, kwa mambo yaliyowatendea watu wangu Israeli, hao walio mali yangu mimi mwenyewe. Maana waliwatawanya miongoni mwa mataifa, waligawa nchi yangu

3 na kugawana watu wangu kwa kura. Waliwauza wavulana ili kulipia malaya, na wasichana ili kulipia divai.

4 “Mnataka kunifanya nini enyi Tiro na Sidoni na maeneo yote ya Filistia? Je, mna kisasi nami mnachotaka kulipiza? Kama mnalipiza kisasi, mimi nitawalipizeni mara moja!

5 Mmechukua fedha na dhahabu yangu, na kuvibeba vitu vyangu vya thamani hadi kwenye mahekalu yenu.

6 Mmewapeleka watu wa Yuda na Yerusalemu mbali na nchi yao, mkawauza kwa Wagiriki.

7 Sasa, nitawarudisha watu wangu kutoka huko mlikowauza. Nitawalipizeni kisasi kwa yote mliyowatendea.

8 Watoto wenu wa kiume na wa kike nitawafanya wauzwe kwa watu wa Yuda, nao watawauzia Washeba, watu wa taifa la mbali kabisa. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.

9 “Watangazieni watu wa mataifa jambo hili: Jitayarisheni kwa vita, waiteni mashujaa wenu; askari wote na wakusanyike, waende mbele.

10 Majembe yenu yafueni yawe mapanga, miundu yenu ya kupogolea iwe mikuki. Hata aliye dhaifu na aseme: ‘Mimi pia ni shujaa’.

11 Njoni haraka, enyi mataifa yote jirani, kusanyikeni huko bondeni.” Ee Mwenyezi-Mungu! Teremsha askari wako dhidi yao!

12 “Haya mataifa na yajiweke tayari; yaje kwenye bonde liitwalo: ‘Mwenyezi-Mungu Ahukumu’. Huko, mimi Mwenyezi-Mungu, nitaketi kuyahukumu mataifa yote ya jirani.

13 Haya! Chukueni mundu wa kuvuna, kwani sasa ni wakati wa mavuno. Ingieni! Wapondeni kama zabibu ambazo zimejaza shinikizo. Uovu wao umepita kiasi kama mapipa yanayofurika.”

14 Wanafika makundi kwa makundi kwenye bonde la Hukumu, maana siku ya Mwenyezi-Mungu imekaribia.

15 Jua na mwezi vinatiwa giza, na nyota zimeacha kuangaza.

16 Mwenyezi-Mungu ananguruma huko Siyoni; sauti yake inavuma kutoka Yerusalemu; mbingu na dunia vinatetemeka. Lakini Mwenyezi-Mungu ni kimbilio la watu wake, ni ngome ya usalama kwa Waisraeli.

17 “Hapo, ewe Israeli, utajua kwamba mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, nakaa Siyoni, mlima wangu mtakatifu, Yerusalemu utakuwa mji mtakatifu; na wageni hawatapita tena humo.

18 “Wakati huo, milima itatiririka divai mpya, na vilima vitatiririka maziwa. Vijito vyote vya Yuda vitajaa maji; chemchemi itatokea nyumbani mwa Mwenyezi-Mungu, na kulinywesha bonde la Shitimu.

19 “Misri itakuwa mahame, Edomu itakuwa jangwa tupu, kwa sababu waliwashambulia watu wa Yuda wakawaua watu wasio na hatia.

20 Bali Yuda itakaliwa milele, na Yerusalemu kizazi hata kizazi.

21 Nitawaadhibu waliomwaga damu ya watu wa Yuda wala sitawaachia wenye hatia. Mimi, Mwenyezi-Mungu nakaa Siyoni.”