1

1 Heri mtu asiyefuata shauri la waovu, asiyeshiriki njia za wenye dhambi, wala kujumuika na wenye dharau;

2 bali huifurahia sheria ya Mwenyezi-Mungu, na kuitafakari mchana na usiku.

3 Huyo ni kama mti uliopandwa kando ya vijito, unaozaa matunda kwa wakati wake, na majani yake hayanyauki. Kila afanyalo hufanikiwa.

4 Lakini waovu sivyo walivyo; wao ni kama makapi yapeperushwayo na upepo.

5 Kwa hiyo watu waovu wataanguka wakati wa hukumu, wenye dhambi hawatakaa na kusanyiko la waadilifu.

6 Maana Mwenyezi-Mungu huziongoza njia za waadilifu; lakini njia za waovu zitaishia katika maangamizi.

2

1 Kwa nini mataifa yanafanya ghasia? Mbona watu wanafanya njama za bure?

2 Wafalme wa dunia wanajitayarisha; watawala wanashauriana pamoja, dhidi ya Mwenyezi-Mungu na mteule wake.

3 Wanasema: “Tujiondoe katika utawala wao; tutupilie mbali minyororo yao!”

4 Mwenyezi-Mungu atawalaye juu mbinguni, anawacheka na kuwadhihaki.

5 Kisha, anawakaripia kwa ghadhabu, na kuwatisha kwa hasira, akisema:

6 “Nimemtawaza mfalme niliyemteua, anatawala Siyoni, mlima wangu mtakatifu!”

7 Mfalme asema: “Nitatangaza azimio la Mwenyezi-Mungu. Mungu aliniambia: ‘Wewe ni mwanangu, mimi leo nimekuwa baba yako.

8 Niombe nami nitakupa mataifa yawe urithi wako, na dunia nzima kuwa mali yako.

9 Utawaponda kwa fimbo ya chuma; utawavunja kama chungu cha mfinyanzi!’”

10 Sasa enyi wafalme, tumieni busara; sikilizeni onyo hili, enyi watawala wa dunia.

11 Mtumikieni Mwenyezi-Mungu kwa uchaji;

12 msujudieni na kutetemeka; asije akakasirika, mkaangamia ghafla; kwani hasira yake huwaka haraka. Heri yao wote wanaokimbilia usalama kwake!

3

1 Ee Mwenyezi-Mungu, tazama walivyo wengi adui zangu, ni wengi mno hao wanaonishambulia.

2 Wengi wanasema juu yangu, “Hatapata msaada kwa Mungu.”

3 Lakini wewe ee Mwenyezi-Mungu u ngao yangu kila upande; kwako napata fahari na ushindi wangu.

4 Nakulilia kwa sauti, ee Mungu, nawe wanisikiliza kutoka mlima wako mtakatifu.

5 Nalala na kupata usingizi, naamka tena maana wewe ee Mwenyezi-Mungu wanitegemeza.

6 Sitayaogopa maelfu ya watu, wanaonizingira kila upande.

7 Uje ee Mwenyezi-Mungu! Niokoe ee Mungu wangu! Wewe wawavunja mataya maadui zangu wote; wawavunja meno waovu wasinidhuru.

8 Mwenyezi-Mungu ndiwe uokoaye; uwape baraka watu wako.

4

1 Ee Mungu mtetezi wa haki yangu, unijibu niombapo. Nilipokuwa katika shida, wewe ulinisaidia; unionee huruma na kusikia sala yangu.

2 Jamani, mtaniharibia jina langu mpaka lini? Mpaka lini mtapenda upuuzi na kusema uongo?

3 Jueni kuwa Mwenyezi-Mungu amejiteulia mwaminifu wake. Mwenyezi-Mungu husikia kila ninapomwomba.

4 Tetemekeni kwa hofu na msitende dhambi; tafakarini vitandani mwenu na kunyamaza.

5 Toeni tambiko zilizo sawa, na kumtumainia Mwenyezi-Mungu.

6 Wengi husema: “Laiti tungepata tena fanaka! Utuangalie kwa wema, ee Mwenyezi-Mungu!”

7 Lakini mimi umenijalia furaha kubwa moyoni, kuliko ya hao walio na divai na ngano kwa wingi.

8 Nalala na kupata usingizi kwa amani; ee Mwenyezi-Mungu, wewe peke yako waniweka salama.

5

1 Usikilize maneno yangu, ee Mwenyezi-Mungu, usikie ninavyopiga kite.

2 Usikilize kilio changu, Mfalme wangu na Mungu wangu, maana wewe ndiwe nikuombaye.

3 Ee Mwenyezi-Mungu, alfajiri waisikia sauti yangu, asubuhi nakutolea tambiko yangu, kisha nangojea unijibu.

4 Wewe si Mungu apendaye ubaya; kwako uovu hauwezi kuwako.

5 Wenye majivuno hawastahimili mbele yako; wewe wawachukia wote watendao maovu.

6 Wawaangamiza wote wasemao uongo; wawachukia wauaji na wadanganyifu.

7 Lakini, kwa wingi wa fadhili zako, mimi nitaingia nyumbani mwako; nitakuabudu kuelekea hekalu lako takatifu, nitakusujudia kwa uchaji.

8 Uniongoze, ee Mwenyezi-Mungu, katika uadilifu wako, maana maadui zangu ni wengi; uiweke njia yako wazi mbele yangu.

9 Vinywani mwao hamna ukweli; mioyoni mwao wamejaa maangamizi, wasemacho ni udanganyifu wa kifo, ndimi zao zimejaa hila.

10 Uwaadhibu kwa hatia yao ee Mungu; waanguke kwa njama zao wenyewe; wafukuze nje kwa sababu ya dhambi zao nyingi, kwa sababu wamekuasi wewe.

11 Lakini wafurahi wote wanaokimbilia usalama kwako, waimbe kwa shangwe daima. Uwalinde wanaolipenda jina lako, wapate kushangilia kwa sababu yako.

12 Maana wewe Mwenyezi-Mungu wawabariki waadilifu; wawakinga kwa fadhili zako kama kwa ngao.

6

1 Ee Mwenyezi-Mungu, usinikemee kwa hasira yako; usiniadhibu kwa ghadhabu yako.

2 Unihurumie, ee Mwenyezi-Mungu, nimeishiwa nguvu; uniponye, ee Mwenyezi-Mungu, nataabika mpaka mifupani.

3 Ninahangaika sana rohoni mwangu. Ee Mwenyezi-Mungu, utakawia mpaka lini?

4 Unigeukie, ee Mwenyezi-Mungu, uniokoe; unisalimishe kwa sababu ya fadhili zako.

5 Huko kwa wafu hakuna anayekukumbuka; huko kuzimu ni nani awezaye kukusifu?

6 Niko hoi kwa kilio cha uchungu; kila usiku nalowesha kitanda changu kwa machozi; kwa kulia kwangu naulowesha mto wangu.

7 Macho yangu yamechoka kwa huzuni; yamefifia kwa kutaabishwa na adui.

8 Ondokeni kwangu enyi nyote watenda maovu! Maana Mwenyezi-Mungu amesikia kilio changu.

9 Mwenyezi-Mungu amesikia ombi langu; Mwenyezi-Mungu amekubali sala yangu.

10 Maadui zangu wote wataaibika na kufadhaika; watarudi nyuma na kuaibishwa ghafla.

7

1 Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu, nakimbilia usalama kwako; uniokoe na wote wanaonidhulumu, unisalimishe.

2 La sivyo, watakuja kunirarua kama simba, wakanivutia mbali, pasiwe na wa kuniokoa.

3 Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu! Kama nimetenda moja ya mambo haya: Kama nimechafua mikono yangu kwa ubaya,

4 kama nimemlipa rafiki yangu mabaya badala ya mema, au nimemshambulia adui yangu bila sababu,

5 basi, adui na anifuatie na kunikamata; ayakanyage maisha yangu; na kuniulia mbali.

6 Inuka ee Mwenyezi-Mungu, kwa hasira yako, uikabili ghadhabu ya maadui zangu. Inuka, ee Mungu wangu, wewe umeamuru haki ifanyike.

7 Uyakusanye mataifa kandokando yako, nawe uyatawale kutoka juu.

8 Wewe, ee Mwenyezi-Mungu, wayahukumu mataifa; unihukumu kadiri ya uadilifu wangu, kulingana na huo unyofu wangu.

9 Uukomeshe uovu wa watu wabaya, uwaimarishe watu walio wema, ee Mungu uliye mwadilifu, uzijuaye siri za mioyo na fikira za watu.

10 Mungu ndiye ngao yangu; yeye huwaokoa wanyofu wa moyo.

11 Mungu ni hakimu wa haki; kila siku hulaumu maovu.

12 Watu wasipoongoka, Mungu atanoa upanga wake; atavuta upinde wake na kulenga shabaha.

13 Atatayarisha silaha zake za hatari, na kuipasha moto mishale yake.

14 Tazama! Mtu mbaya hutunga uovu, hujaa uharibifu na kuzaa udanganyifu.

15 Huchimba shimo, akalifukua, kisha hutumbukia humo yeye mwenyewe.

16 Uharibifu wake utamrudia yeye mwenyewe; ukatili wake utamwangukia yeye binafsi.

17 Nitamshukuru Mwenyezi-Mungu kwani ni mwema; nitaimba sifa za jina la Mwenyezi-Mungu, Mungu Mkuu.

8

1 Ee Mwenyezi-Mungu, Bwana wetu, kweli jina lako latukuka duniani kote! Utukufu wako waenea mpaka juu ya mbingu!

2 Kwa sifa za watoto wadogo na wanyonyao, umejiwekea ngome dhidi ya adui zako, uwakomeshe waasi na wapinzani wako.

3 Nikiangalia mbingu, kazi ya vidole vyako, mwezi na nyota ulizozisimika huko,

4 mtu ni nini, ee Mungu, hata umfikirie, binadamu ni nini hata umjali?

5 Umemfanya awe karibu kama Mungu, umemvika fahari na heshima.

6 Ulimpa madaraka juu ya kazi zako zote; uliviweka viumbe vyote chini ya mamlaka yake:

7 Kondoo, ng'ombe, na wanyama wa porini;

8 ndege, samaki, na viumbe vyote vya baharini.

9 Ee Mwenyezi-Mungu, Bwana wetu, kweli jina lako latukuka duniani kote!

9

1 Nitakushukuru Mungu kwa moyo wangu wote; nitayasimulia matendo yako yote ya ajabu.

2 Nitafurahi na kushangilia kwa sababu yako; nitaliimbia sifa jina lako, ewe Mungu Mkuu.

3 Wakati ulipotokea, maadui zangu walirudi nyuma, walijikwaa na kuangamia.

4 Umenitetea kuhusu kisa changu cha haki; umeketi katika kiti chako cha enzi, ukatoa hukumu iliyo sawa.

5 Umeyakemea mataifa, umewaangamiza waovu; majina yao umeyafutilia mbali milele.

6 Maadui wameangamia milele; umeingolea mbali miji yao, kumbukumbu lao limetoweka.

7 Lakini Mwenyezi-Mungu anatawala milele; ameweka kiti chake cha enzi apate kuhukumu.

8 Anauhukumu ulimwengu kwa haki; anayaamua mataifa kwa unyofu.

9 Mwenyezi-Mungu ni ngome ya watu wanaoonewa; yeye ni ngome nyakati za taabu.

10 Wanaokujua wewe, ee Mungu hukutegemea, wewe Mwenyezi-Mungu huwatupi wakutafutao.

11 Mwimbieni sifa Mwenyezi-Mungu akaaye Siyoni. Yatangazieni mataifa mambo aliyotenda!

12 Mungu hulipiza kisasi kwa umwagaji damu; kamwe hasahau kilio cha wanaoonewa.

13 Unirehemu, ee Mwenyezi-Mungu! Ona mateso ninayoteswa na wanaonichukia; wewe waninyakua kutoka nguvu za kifo,

14 nisimulie sifa zako mbele ya watu wa Siyoni, nipate kushangilia kwa sababu umeniokoa.

15 Watu wa mataifa wametumbukia katika shimo walilochimba, wamenaswa miguu katika wavu waliouficha.

16 Mwenyezi-Mungu amejionesha alivyo; ametekeleza hukumu. Watu waovu wamenaswa kwa matendo yao wenyewe.

17 Waovu wataishia kuzimu; naam, mataifa yote yanayomsahau Mungu.

18 Lakini fukara hawatasahauliwa daima; tumaini la maskini halitapotea milele.

19 Inuka, ee Mwenyezi-Mungu! Usimwache binadamu ashinde. Uyakusanye mataifa mbele yako, uyahukumu.

20 Uyatie hofu, ee Mwenyezi-Mungu, watu wa mataifa watambue kuwa wao ni watu tu!

10

1 Ee Mwenyezi-Mungu, mbona wasimama mbali? Kwa nini wajificha wakati tumo taabuni?

2 Kwa kiburi waovu wanawatesa maskini; njama zao ziwanase wao wenyewe.

3 Mwovu hujisifia tamaa zake mbaya, mtu wa tamaa hulaani na kumkataa Mwenyezi-Mungu.

4 Katika majivuno yake husema: “Mungu hatagundua.” Mawazo yake yote ni: “Hakuna Mungu.”

5 Njia za mwovu hufanikiwa daima; kwake hukumu zako ziko mbali na mawazo yake, na huwadharau maadui zake wote.

6 Huwaza moyoni: “Sitakuwa na wasiwasi; sitapatwa na dhiki maishani.”

7 Kinywa chake kimejaa laana, udanganyifu na dhuluma; mwepesi kusema maneno ya kuchukiza na maovu.

8 Hujificha vijijini huku anaotea, amuue kwa siri mtu asiye na hatia. Yuko macho kumvizia mnyonge;

9 huotea mafichoni mwake kama simba. Huvizia apate kuwakamata maskini; huwanasa kwa mtego wake na kuwachukua.

10 Mnyonge huvamiwa na kuangushwa chini; huangushwa kwa ukatili wa mtu mwovu.

11 Mwovu huwaza moyoni mwake: “Mungu amesahau; ameficha uso wake, haoni kitu!”

12 Inuka, ee Mwenyezi-Mungu, uwaadhibu; usiwasahau wanaodhulumiwa.

13 Ee Mungu, kwa nini mwovu anakudharau, na kusema ati hutamfanya awajibike?

14 Lakini wewe wawaona wenye dhiki na shida; nawe daima uko tayari kuwasaidia. Mnyonge anakutegemea wewe, ee Mungu, wewe umekuwa daima msaada wa yatima.

15 Uzivunje nguvu za mtu mwovu; ukomeshe uovu wake wote, usiwepo tena.

16 Mwenyezi-Mungu ni mfalme milele na milele! Mataifa yasiyomjua yatatoweka nchini mwake.

17 Ee Mwenyezi-Mungu, wapokea dua za mnyonge; wampa moyo na kumtegea sikio.

18 Utawatendea haki yatima na wanaodhulumiwa, binadamu aliye udongo asiweze tena kuleta hofu.

11

1 Kwake Mwenyezi-Mungu nakimbilia usalama; mnawezaje basi kuniambia: “Ruka kama ndege, mpaka milimani,

2 maana waovu wanavuta pinde; wameweka mishale tayari juu ya uta, wawapige mshale watu wema gizani!

3 Kama misingi ikiharibiwa, mtu mwadilifu atafanya nini?”

4 Mwenyezi-Mungu yumo katika hekalu lake takatifu; kiti cha enzi cha Mwenyezi-Mungu kiko mbinguni. Kwa macho yake huwachungulia wanadamu, na kujua kila kitu wanachofanya.

5 Mwenyezi-Mungu huwapima waadilifu na waovu; huwachukia kabisa watu wakatili.

6 Atawanyeshea waovu makaa ya moto na madini ya kiberiti; upepo wa hari utakuwa ndio adhabu yao.

7 Mwenyezi-Mungu ni mwadilifu na apenda uadilifu; watu wanyofu watakaa pamoja naye.

12

1 Fanya haraka, ee Mwenyezi-Mungu! Watu wema wamekwisha; waaminifu wametoweka miongoni mwa watu.

2 Kila mmoja humdanganya mwenzake, husema kwa kudanganya na kwa moyo wa unafiki.

3 Ee Mwenyezi-Mungu uikomeshe hiyo midomo ya udanganyifu, na ndimi hizo zinazojigamba kupindukia.

4 Wao husema: “Kwa ndimi zetu tutashinda; midomo tunayo, nani awezaye kututawala?”

5 Lakini Mwenyezi-Mungu asema: “Kwa sababu maskini wanadhulumiwa, na wahitaji wanapiga kite, sasa naja, nami nitawapa usalama wanaoutazamia.”

6 Neno la Mwenyezi-Mungu ni safi, safi kama fedha iliyosafishwa katika tanuri, naam, kama fedha iliyosafishwa mara saba.

7 Utulinde, ee Mwenyezi-Mungu, utukinge daima na kizazi hiki kiovu.

8 Waovu wanazunguka kila mahali; upotovu unatukuzwa kati ya watu.

13

1 Mpaka lini ee Mwenyezi-Mungu, utanisahau? Je, utanisahau mpaka milele? Mpaka lini utanificha uso wako?

2 Nitakuwa na wasiwasi rohoni hadi lini, na sikitiko moyoni siku hata siku? Hadi lini adui zangu watafurahia taabu zangu?

3 Uniangalie na kunijibu, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu. Uyaangazie macho yangu, nisipatwe na usingizi wa kifo.

4 Usiwaache maadui zangu waseme: “Tumemweza huyu!” Watesi wangu wasije wakafurahia kuanguka kwangu.

5 Lakini mimi nazitumainia fadhili zako; moyo wangu na ufurahie wokovu wako.

6 Nitakuimbia wewe, ee Mwenyezi-Mungu, kwa ukarimu mwingi ulionitendea!

14

1 Wapumbavu hujisemea moyoni: “Hakuna Mungu.” Wote wamepotoka kabisa, wametenda mambo ya kuchukiza; hakuna hata mmoja atendaye jema!

2 Mwenyezi-Mungu anawaangalia wanadamu kutoka mbinguni, aone kama kuna yeyote mwenye busara, kama kuna yeyote anayemtafuta Mungu.

3 Lakini wote wamekosa, wote wamepotoka pamoja; hakuna atendaye mema, hakuna hata mmoja.

4 “Je, hao watendao maovu hawana akili? Wanawatafuna watu wangu kama mikate; wala hawanijali mimi Mwenyezi-Mungu.”

5 Hapo watashikwa na hofu kubwa, maana Mungu yu pamoja na waadilifu.

6 Unaweza kuvuruga mipango ya maskini, lakini Mwenyezi-Mungu ndiye kimbilio lake.

7 Laiti ukombozi wa Israeli ungefika kutoka Siyoni! Mwenyezi-Mungu atakaporekebisha hali ya watu wake, wazawa wa Yakobo watashangilia; Waisraeli watafurahi.

15

1 Nani ee Mwenyezi-Mungu atakayekaa hemani mwako? Nani atakayeishi juu ya mlima wako mtakatifu?

2 Ni mtu aishiye bila lawama, atendaye daima yaliyo mema, asemaye ukweli kutoka moyoni;

3 ni mtu asiyesengenya watu, asiyemtendea uovu rafiki yake, wala kumfitini jirani yake;

4 ni mtu anayewadharau wafisadi, lakini huwaheshimu wamchao Mwenyezi-Mungu; ni mtu asiyegeuza kiapo chake hata kikimtia hasara;

5 asiyekopesha fedha yake kwa riba, wala kupokea rushwa kumdhulumu asiye na hatia. Mtu atendaye hayo, kamwe hatatikisika.

16

1 Unilinde ee Mungu; maana kwako nakimbilia usalama.

2 Namwambia Mungu: “Wewe u Bwana wangu; sina jema lolote ila wewe.”

3 Ni bora sana hao watakatifu walioko nchini, kukaa nao ndiyo furaha yangu.

4 Lakini wanaoabudu miungu mingine, watapata mateso mengi. Tambiko ya damu sitaitolea kamwe, na majina ya miungu hiyo sitayataja.

5 Wewe ee Mwenyezi-Mungu ndiwe riziki yangu kuu, majaliwa yangu yamo mikononi mwako.

6 Umenipimia sehemu nzuri sana; naam, urithi wangu ni wa kupendeza.

7 Namsifu Mwenyezi-Mungu kwa kuniongoza, usiku dhamiri yangu yanionya.

8 Namweka Mwenyezi-Mungu mbele yangu daima; yuko pamoja nami, wala sitatikisika.

9 Kwa hiyo nitafurahi kwa moyo wote na kushangilia, nami nitakaa salama salimini.

10 Naam wewe hutaiacha nafsi yangu kuzimu, hutaniacha mimi mwaminifu wako nipate kuoza.

11 Wanionesha njia ya kufikia uhai; kuwako kwako kwanijaza furaha kamili, katika mkono wako wa nguvu mna mema ya milele.

17

1 Ee Mwenyezi-Mungu usikie kisa changu cha haki, usikilize kilio changu, uitegee sikio sala yangu isiyo na hila.

2 Haki yangu na ije kutoka kwako, kwani wewe wajua jambo lililo la haki.

3 Wewe wajua kabisa moyo wangu; umenijia usiku, kunichunguza, umenitia katika jaribio; hukuona uovu ndani yangu, sikutamka kitu kisichofaa.

4 Kuhusu matendo watendayo watu; mimi nimeitii amri yako, nimeepa njia ya wadhalimu.

5 Nimefuata daima njia yako; wala sijateleza kamwe.

6 Nakuita, ee Mungu, kwani wewe wanijibu; unitegee sikio, uyasikie maneno yangu.

7 Onesha fadhili zako za ajabu, uwaokoe kutoka kwa adui zao, wale wanaokimbilia usalama kwako.

8 Unilinde kama mboni ya jicho; unifiche kivulini mwa mabawa yako,

9 mbali na mashambulio ya waovu, mbali na maadui zangu hatari wanaonizunguka.

10 Hao hawana huruma yoyote moyoni; wamejaa maneno ya kujigamba.

11 Wananifuatia na kunizunguka; wananivizia waniangushe chini.

12 Wako tayari kunirarua kama simba: Kama mwanasimba aviziavyo mawindo.

13 Inuka, ee Mwenyezi-Mungu, uwakabili na kuwaporomosha. Kwa upanga uiokoe nafsi yangu kutoka kwa waovu.

14 Kwa mkono wako, ee Mwenyezi-Mungu, uniokoe mikononi mwa watu hao, watu ambao riziki yao ni dunia hii tu. Uwajaze adhabu uliyowawekea, wapate ya kuwatosha na watoto wao, wawaachie hata na wajukuu zao.

15 Lakini mimi nitauona uso wako, kwani ni mwadilifu; niamkapo nitajaa furaha kwa kukuona.

18

1 Nakupenda, ee Mwenyezi-Mungu, nguvu yangu!

2 Mwenyezi-Mungu ni mwamba wangu, ngome yangu na mkombozi wangu; Mungu wangu, mwamba wangu ninayemkimbilia usalama; ngao yangu, nguvu za wokovu wangu na ngome yangu.

3 Namwita Mwenyezi-Mungu astahiliye sifa anisaidie, nami naokolewa kutoka kwa maadui zangu.

4 Kamba za kifo zilinizingira, mawimbi ya maangamizi yalinivamia;

5 kamba za kuzimu zilinizinga, mitego ya kifo ilinikabili.

6 Katika taabu yangu nilimwita Mwenyezi-Mungu, nilimlilia Mungu wangu anisaidie. Aliisikia sauti yangu hekaluni mwake; kilio changu kilimfikia masikioni mwake.

7 Hapo dunia ikatetemeka na kutikisika; misingi ya milima ikayumbayumba, kwani Mungu alikuwa amekasirika.

8 Moshi ulifuka kutoka puani mwake, moto uunguzao ukatoka kinywani mwake; makaa ya moto yalilipuka kutoka kwake.

9 Aliinamisha anga, akashuka chini; na wingu jeusi chini ya miguu yake.

10 Alipanda kiumbe chenye mabawa akaruka; akapaa kasi juu ya mabawa ya upepo.

11 Alijifunika giza pande zote, mawingu mazito yaliyojaa maji yalimzunguka.

12 Umeme ulimulika mbele yake; kukatokea mawinguni mvua ya mawe na makaa ya moto.

13 Mwenyezi-Mungu alinguruma kutoka mbinguni; Mungu Mkuu akatoa sauti yake, kukatokea mvua ya mawe na makaa ya moto.

14 Aliwapiga maadui mishale yake, akawatawanya, alirusha umeme, akawatimua.

15 Ulipowakemea maadui zako ee Mwenyezi-Mungu, ulipowatisha kwa ghadhabu yako, vilindi vya bahari vilifunuliwa, misingi ya dunia ikaonekana.

16 Mungu alinyosha mkono kutoka juu akanichukua, kutoka katika maji mengi alininyanyua.

17 Aliniokoa kutoka kwa maadui zangu wenye nguvu nyingi, aliniokoa kutoka kwa hao walionichukia, maana walikuwa na nguvu kunishinda.

18 Walinivamia nilipokuwa taabuni, lakini Mwenyezi-Mungu alikuwa kinga yangu.

19 Alinileta, akaniweka mahali pa usalama; alinisalimisha, kwani alipendezwa nami.

20 Mwenyezi-Mungu alinipa tuzo kadiri ya uadilifu wangu; alinituza kwa vile mikono yangu haina hatia.

21 Maana nimefuata njia za Mwenyezi-Mungu, wala sikujitenga na Mungu wangu kwa uovu.

22 Nimeshika maagizo yake yote, sikuacha kufuata masharti yake.

23 Mbele yake sikuwa na hatia; nimejikinga nisiwe na hatia.

24 Mwenyezi-Mungu amenituza kadiri ya uadilifu wangu; yeye ajua kwamba mikono yangu haina hatia.

25 Wewe ni mwaminifu kwa walio waaminifu; mwema kwa wale walio wema.

26 Wewe ni mkamilifu kwa walio wakamilifu; lakini mkatili kwa watu walio waovu.

27 Wewe wawaokoa walio wanyenyekevu, lakini wenye majivuno huwaporomosha.

28 Wewe ee Mwenyezi-Mungu, waniangazia; walifukuza giza langu, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu.

29 Kwa msaada wako nakishambulia kikosi; wewe wanipa nguvu ya kuruka ukuta.

30 Huyu Mungu matendo yake hayana dosari! Ahadi ya Mwenyezi-Mungu ni ya kuaminika; yeye ni ngao kwa wote wanaomkimbilia usalama.

31 Nani aliye Mungu isipokuwa Mwenyezi-Mungu? Nani aliye mwamba wa usalama ila Mungu wetu?

32 Mungu ndiye anijaliaye nguvu kila upande; ndiye anayeifanya salama njia yangu.

33 Ameiimarisha miguu yangu kama ya paa, na kuniweka salama juu ya vilele.

34 Hunifunza kupigana vita, mikono yangu iweze kuvuta upinde wa shaba.

35 Umenipa ngao yako ya kuniokoa; mkono wako wa kulia umenitegemeza; wema wako umenifanikisha.

36 Umenirahisishia njia yangu; wala miguu yangu haikuteleza.

37 Niliwafuatia adui zangu na kuwakamata; sikurudi nyuma mpaka nimewaangamiza.

38 Niliwaangusha chini wasiweze kuinuka tena; walianguka chini ya miguu yangu.

39 Wewe ulinijalia nguvu ya kupigana vita; uliwaporomosha maadui chini yangu.

40 Uliwafanya maadui zangu wakimbie, na wale walionichukia niliwaangamiza.

41 Walipiga yowe lakini hapakuwa na wa kuwaokoa; walimlilia Mwenyezi-Mungu lakini hakuwajibu.

42 Niliwatwanga wakawa kama vumbi inayopeperushwa na upepo; niliwakanyaga kama tope la njiani.

43 Wewe uliniokoa na mashambulizi ya watu, ukanifanya mtawala wa mataifa. Watu nisiowajua walinitumikia.

44 Mara waliposikia habari zangu walinitii. Wageni walinijia wakinyenyekea.

45 Wageni walikufa moyo; wakaja kutoka ngome zao wakitetemeka.

46 Mwenyezi-Mungu yu hai! Asifiwe mwamba wa usalama wangu; atukuzwe Mungu wa wokovu wangu.

47 Yeye ameniwezesha kulipiza kisasi; na kuyashinda mataifa chini yangu.

48 Ameniokoa kutoka kwa maadui zangu, akanikuza juu ya wapinzani wangu, na kunisalimisha mbali na watu wakatili.

49 Kwa hiyo nitakutukuza kati ya mataifa, ee Mwenyezi-Mungu nitaliimbia sifa jina lako.

50 Mungu humjalia mfalme wake ushindi mkubwa; humwonesha fadhili zake huyo mteule wake, naam, humfadhili Daudi na wazawa wake milele.

19

1 Mbingu zatangaza utukufu wa Mungu; anga ladhihirisha kazi ya mikono yake.

2 Mchana waupasha habari mchana ufuatao, usiku waufahamisha usiku ufuatao.

3 Hamna msemo au maneno yanayotumika; wala hakuna sauti inayosikika;

4 hata hivyo, sauti yao yaenea duniani kote, na maneno yao yafika kingo za ulimwengu. Mungu ameliwekea jua makao yake angani;

5 nalo hutoka kama bwana arusi chumbani mwake, lafurahi kama shujaa aliye tayari kushindana.

6 Lachomoza toka upande mmoja, na kuzunguka hadi upande mwingine; hakuna kiwezacho kuliepa joto lake.

7 Sheria ya Mwenyezi-Mungu ni kamilifu, humpa mtu uhai mpya; masharti ya Mwenyezi-Mungu ni thabiti, huwapa hekima wasio na makuu.

8 Kanuni za Mwenyezi-Mungu ni sawa, huufurahisha moyo; amri ya Mwenyezi-Mungu ni safi, humwelimisha mtu.

9 Kumcha Mwenyezi-Mungu ni jambo jema, na la kudumu milele; maagizo ya Mwenyezi-Mungu ni sawa, yote ni ya haki kabisa.

10 Yatamanika kuliko dhahabu; kuliko dhahabu safi kabisa. Ni matamu kuliko asali; kuliko asali safi kabisa.

11 Yanifunza mimi mtumishi wako; kuyafuata kwaniletea tuzo kubwa.

12 Lakini nani aonaye makosa yake mwenyewe? Ee Mungu, niepushe na makosa nisiyoyajua.

13 Unikinge mimi mtumishi wako na makosa ya makusudi, usikubali hayo yanitawale. Hapo nitakuwa mkamilifu, wala sitakuwa na hatia ya kosa kubwa.

14 Maneno ya kinywa changu, na mawazo ya moyo wangu, yakubalike mbele yako, ee Mwenyezi-Mungu, mwamba wangu na mkombozi wangu!

20

1 Mwenyezi-Mungu akujibu uwapo taabuni; jina la Mungu wa Yakobo likulinde.

2 Akupelekee msaada kutoka hekaluni mwake; akutegemeze kutoka mlima Siyoni.

3 Azikumbuke sadaka zako zote; azikubali tambiko zako za kuteketezwa.

4 Akujalie unayotamani moyoni mwako, aifanikishe mipango yako yote.

5 Tutashangilia kwa ajili ya ushindi wako; tutatweka bendera kulitukuza jina la Mungu wetu. Mwenyezi-Mungu akutimizie maombi yako yote!

6 Najua Mwenyezi-Mungu atamsaidia mfalme aliyemteua, atamjibu kutoka patakatifu pake mbinguni; kwa mkono wake wa kulia atamjalia ushindi mkubwa.

7 Wengine hujigamba kwa magari ya vita; wengine hujigamba kwa farasi wao. Lakini sisi twajivunia Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu.

8 Hao watajikwaa na kuanguka; lakini sisi tutainuka na kusimama imara.

9 Umjalie mfalme ushindi, ee Mwenyezi-Mungu; utujibu wakati tunapokuomba.

21

1 Mfalme ashangilia, ee Mwenyezi-Mungu, kwa nguvu yako, anafurahi mno kwa msaada uliompa.

2 Umemtimizia matakwa ya moyo wake; wala hukumkatalia ombi lake.

3 Umemjia, ukampa baraka nzurinzuri; umemvika taji ya dhahabu safi kichwani mwake.

4 Alikuomba maisha nawe ukampa; ulimpa maisha marefu milele na milele.

5 Kwa msaada wako ametukuka sana; wewe umemjalia fahari na heshima.

6 Wamjalia baraka zako daima; wamfurahisha kwa kuwako kwako.

7 Mfalme anamtumainia Mwenyezi-Mungu; kwa fadhili za Mungu Mkuu atakuwa salama.

8 Mkono wako ewe mfalme utawakamata maadui zako wote; mkono wako wa kulia utawakamata wanaokuchukia.

9 Utakapotokea utawaangamiza kama kwa tanuri ya moto. Mwenyezi-Mungu atawamaliza kwa hasira yake, moto utawateketeza kabisa.

10 Utawaangamiza wazawa wao kutoka duniani; watoto wao hawatasalia kati ya binadamu.

11 Hata kama wakipanga maovu dhidi yako, kama wakitunga mipango ya hila, kamwe hawataweza kufaulu.

12 Kwa maana wewe utawatimua mbio, utawalenga usoni kwa mishale yako.

13 Utukuzwe ee Mwenyezi-Mungu kwa sababu ya nguvu yako! Tutaimba na kuusifu uwezo wako.

22

1 Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha? Mbona uko mbali sana kunisaidia, mbali na maneno ya kilio changu?

2 Ee Mungu wangu, nalia mchana lakini hujibu; napiga yowe usiku, lakini nafuu sipati.

3 Hata hivyo, wewe ni mtakatifu; wewe watawala na kusifiwa na Waisraeli.

4 Wazee wetu walikutegemea; walikutegemea, nawe ukawaokoa.

5 Walikulilia wewe, wakaokolewa; walikutegemea, nao hawakuaibika.

6 Lakini mimi ni mdudu tu, wala si mtu; nimepuuzwa na kudharauliwa na watu.

7 Wote wanionao hunidhihaki; hunifyonya na kutikisa vichwa vyao.

8 Husema: “Alimtegemea Mwenyezi-Mungu, basi, Mungu na amkomboe! Kama Mungu anapendezwa naye, basi, na amwokoe!”

9 Lakini ndiwe uliyenitoa tumboni mwa mama yangu, uliniweka salama kifuani pa mama yangu.

10 Nimekutegemea tangu kuzaliwa kwangu. Tangu nilipozaliwa wewe umekuwa Mungu wangu.

11 Usikae mbali nami, kwani taabu imekaribia; wala hakuna wa kunisaidia.

12 Maadui wengi wanizunguka kama fahali; wamenisonga kama fahali wakali wa Bashani!

13 Wanafunua vinywa vyao kama simba, tayari kushambulia na kurarua.

14 Nimekwisha kama maji yaliyomwagika; mifupa yangu yote imeteguka; moyo wangu ni kama nta, unayeyuka ndani mwangu.

15 Koo langu limekauka kama kigae; ulimi wangu wanata kinywani mwangu. Umeniacha kwenye mavumbi ya kifo.

16 Genge la waovu limenizunguka; wananizingira kama kundi la mbwa; wamenitoboa mikono na miguu.

17 Nimebaki mifupa mitupu; maadui zangu waniangalia na kunisimanga.

18 Wanagawana nguo zangu, na kulipigia kura vazi langu.

19 Lakini wewe ee Mwenyezi-Mungu, usikae mbali nami; ewe msaada wangu, uje haraka kunisaidia.

20 Iokoe nafsi yangu mbali na upanga, yaokoe maisha yangu makuchani mwa mbwa hao!

21 Uniokoe kinywani mwa simba; iokoe nafsi yangu dhaifu toka pembe za nyati hao.

22 Nitawasimulia ndugu zangu matendo yako; nitakusifu kati ya kusanyiko lao:

23 Enyi mnaomcha Mwenyezi-Mungu, msifuni! Mtukuzeni enyi wazawa wote wa Yakobo! Mcheni Mungu enyi wazawa wote wa Israeli!

24 Maana yeye hapuuzi au kudharau unyonge wa mnyonge; wala hajifichi mbali naye, ila humsikia anapomwomba msaada.

25 Kwa sababu yako ninakusifu katika kusanyiko kubwa la watu; nitatimiza ahadi zangu mbele yao wakuchao.

26 Maskini watakula na kushiba; wanaomtafuta Mwenyezi-Mungu watamsifu. Mungu awajalie kuishi milele!

27 Ulimwengu wote utakumbuka na kumrudia Mwenyezi-Mungu; jamaa zote za mataifa zitamwabudu.

28 Maana Mwenyezi-Mungu ni mfalme; yeye anayatawala mataifa.

29 Wenye kiburi wote duniani watasujudu mbele yake; wote ambao hufa watainama mbele yake, wote ambao hawawezi kudumisha uhai wao.

30 Vizazi vijavyo vitamtumikia; watu watavisimulia habari za Mwenyezi-Mungu,

31 watatangaza matendo yake ya wokovu. Watu wasiozaliwa bado wataambiwa: “Mwenyezi-Mungu ndiye aliyefanya hayo!”

23

1 Mwenyezi-Mungu ni mchungaji wangu, sitapungukiwa na kitu.

2 Hunipumzisha kwenye malisho mabichi; huniongoza kando ya maji matulivu,

3 na kuirudishia nafsi yangu nguvu mpya. Huniongoza katika njia sawa kwa hisani yake.

4 Nijapopita katika bonde la giza kuu la kifo, sitaogopa hatari yoyote, maana wewe ee Mwenyezi-Mungu u pamoja nami; gongo lako na fimbo yako vyanilinda.

5 Umeniandalia karamu mbele ya maadui zangu; umenipaka mafuta kichwani pangu; kikombe changu umekijaza mpaka kufurika.

6 Kweli wema wako na fadhili zako zitakuwa pamoja nami, siku zote za maisha yangu; nami nitakaa nyumbani mwa Mwenyezi-Mungu milele.

24

1 Dunia na vyote vilivyomo ni vyake Mwenyezi-Mungu; ulimwengu na wote waishio humo ni mali yake.

2 Maana yeye aliweka misingi ya dunia juu ya bahari; aliisimika imara juu ya mito ya maji.

3 Nani atakayepanda mlima wa Mwenyezi-Mungu? Nani atakayekaa katika hekalu lake takatifu?

4 Ni mtu wa matendo mema na moyo safi, asiyeuelekeza moyo wake katika upuuzi, wala kuapa kwa uongo.

5 Mtu huyo atapokea baraka kwa Mwenyezi-Mungu, na haki yake kwa Mungu mwokozi wake.

6 Ndio hali ya kizazi cha watu wamtafutao yeye; naam, watu wamtafutao Mungu wa Yakobo.

7 Fungukeni enyi milango; fungukeni enyi milango ya kale, ili Mfalme mtukufu aingie.

8 Ni nani huyo Mfalme mtukufu? Ni Mwenyezi-Mungu, mwenye nguvu na uwezo; Mwenyezi-Mungu, mwenye uwezo vitani.

9 Fungukeni enyi malango, fungukeni enyi milango ya kale, ili Mfalme mtukufu aingie.

10 Ni nani huyo Mfalme mtukufu? Ni Mwenyezi-Mungu, wa majeshi, yeye ndiye Mfalme mtukufu.

25

1 Ee Mwenyezi-Mungu, kwako naielekeza nafsi yangu!

2 Nakutumainia wewe, ee Mungu wangu, usiniache niaibike; adui zangu wasifurahie kushindwa kwangu.

3 Usimwache anayekutumainia apate aibu; lakini waaibike wote wanaokuasi kwa makusudi.

4 Unijulishe njia zako, ee Mwenyezi-Mungu; unifundishe nifuate unayotaka.

5 Uniongoze katika ukweli wako na kunifundisha, kwani wewe ni Mungu, mwokozi wangu; ninakutegemea wewe kila siku.

6 Uikumbuke huruma yako ee Mwenyezi-Mungu; uzikumbuke na fadhili zako kuu, ambazo zimekuwako tangu kale.

7 Usikumbuke dhambi na makosa ya ujana wangu; unikumbuke kadiri ya fadhili zako, kwa ajili ya wema wako, ee Mwenyezi-Mungu.

8 Mwenyezi-Mungu ni mwema na mnyofu, kwa hiyo huwafundisha wenye dhambi njia.

9 Huwaongoza wanyenyekevu katika uadilifu; naam, huwafundisha hao njia yake.

10 Mwenyezi-Mungu hutenda kwa fadhili na uaminifu, kwa wale wanaoshika agano lake na maamuzi yake.

11 Kwa ajili ya jina lako, ee Mwenyezi-Mungu, unisamehe kosa langu kwani ni kubwa.

12 Kila mtu anayemcha Mwenyezi-Mungu, Mwenyezi-Mungu atamfunza njia ya kufuata.

13 Mtu wa namna hiyo atafanikiwa daima, na wazawa wake watamiliki nchi.

14 Mwenyezi-Mungu ni rafiki ya wale wamchao; yeye huwajulisha hao agano lake.

15 Namwangalia Mwenyezi-Mungu daima; yeye atainasua miguu yangu mtegoni.

16 Unielekee, ee Mungu, unionee huruma, maana mimi ni mpweke na mnyonge.

17 Uniondolee mahangaiko ya moyoni mwangu; unitoe katika mashaka yangu.

18 Uangalie mateso yangu na dhiki yangu; unisamehe dhambi zangu zote.

19 Angalia jinsi walivyo wengi maadui zangu; ona jinsi wanavyonichukia kwa ukatili.

20 Uyalinde maisha yangu, uniokoe; nakimbilia usalama kwako, usikubali niaibike.

21 Wema na uadilifu vinihifadhi, maana ninakutumainia wewe.

22 Ee Mungu, uwaokoe watu wako, Israeli; uwaokoe katika taabu zao zote.

26

1 Ee Mwenyezi-Mungu, unitetee, maana nimeishi bila hatia, nimekutumainia wewe bila kusita.

2 Unijaribu, ee Mwenyezi-Mungu, na kunipima; uchunguze moyo wangu na akili zangu.

3 Fadhili zako ziko mbele ya macho yangu, ninaishi kutokana na uaminifu wako.

4 Sijumuiki na watu wapotovu; sishirikiani na watu wanafiki.

5 Nachukia mikutano ya wabaya; wala sitajumuika na waovu.

6 Nanawa mikono yangu kuonesha sina hatia, na kuizunguka madhabahu yako, ee Mwenyezi-Mungu,

7 nikiimba wimbo wa shukrani, na kusimulia matendo yako yote ya ajabu.

8 Ee Mwenyezi-Mungu, napenda makao yako, mahali unapokaa utukufu wako.

9 Usiniangamize pamoja na wenye dhambi, wala usinitupe pamoja na wauaji,

10 watu ambao matendo yao ni maovu daima, watu ambao wamejaa rushwa.

11 Lakini mimi ninaishi kwa unyofu; unihurumie na kunikomboa.

12 Mimi nimesimama mahali palipo imara; nitamsifu Mwenyezi-Mungu katika kusanyiko kubwa.

27

1 Mwenyezi-Mungu ni mwanga wangu na wokovu wangu, ni nani nitakayemwogopa? Mwenyezi-Mungu ni ngome ya maisha yangu, sitamwogopa mtu yeyote.

2 Waovu wakinishambulia, na kutaka kuniangamiza, hao wapinzani wangu watajikwaa na kuanguka.

3 Hata jeshi likinizunguka, moyo wangu hautaogopa kitu; hata nikikabiliwa na vita, bado nitakuwa na tumaini.

4 Jambo moja nimemwomba Mwenyezi-Mungu, nalo ndilo ninalolitafuta: Nikae nyumbani mwa Mwenyezi-Mungu siku zote za maisha yangu; niuone uzuri wake Mwenyezi-Mungu, na kutafuta maongozi yake hekaluni mwake.

5 Siku ya taabu atanificha bandani mwake; atanificha katika hema lake, na kunisalimisha juu ya mwamba.

6 Nami kwa fahari nitaangalia juu ya maadui zangu wanaonizunguka. Nitamtolea tambiko kwa shangwe hekaluni mwake, nitaimba na kumshangilia Mwenyezi-Mungu.

7 Usikie, ee Mwenyezi-Mungu, ninapokulilia, unionee huruma na kunijibu.

8 Moyo wangu waniambia: “Njoo umtafute Mungu!” Basi, naja kwako, ee Mwenyezi-Mungu.

9 Usiache kuniangalia kwa wema. Usinikatae kwa hasira mimi mtumishi wako; wewe umekuwa daima msaada wangu. Usinitupe wala usiniache, ee Mungu Mwokozi wangu.

10 Hata kama wazazi wangu wakinitupa, Mwenyezi-Mungu atanipokea kwake.

11 Unifundishe njia yako, ee Mwenyezi-Mungu; uniongoze katika njia iliyo sawa, kwa sababu ya maadui zangu.

12 Usiniache maadui wanitende wapendavyo; maana mashahidi wa uongo wananikabili, nao wanatoa vitisho vya ukatili.

13 Naamini nitauona wema wake Mwenyezi-Mungu katika makao ya walio hai.

14 Mtegemee Mwenyezi-Mungu! Uwe na moyo, usikate tamaa! Naam, mtegemee Mwenyezi-Mungu!

28

1 Nakulilia, ee Mwenyezi-Mungu! Ewe mwamba wa usalama wangu usiniwie kama kiziwi, la sivyo kama usiponisikiliza, nitakuwa kama wale washukao shimoni kwa wafu.

2 Sikiliza sauti ya ombi langu, ninapokulilia unisaidie, ninapoinua mikono yangu kuelekea maskani yako takatifu.

3 Usinipatilize pamoja na watu wabaya, pamoja na watu watendao maovu: Watu wasemao na wenzao maneno ya amani, kumbe wamejaa uhasama moyoni.

4 Uwaadhibu kadiri ya matendo yao, kufuatana na maovu waliyotenda. Waadhibu kadiri ya matendo yao wenyewe; uwatendee yale wanayostahili.

5 Hawajali matendo ya Mwenyezi-Mungu; hawatambui mambo aliyoyafanya. Kwa sababu hiyo atawabomoa, wala hatawajenga tena upya.

6 Atukuzwe Mwenyezi-Mungu, maana amesikiliza ombi langu.

7 Mwenyezi-Mungu ndiye nguvu yangu na ngao yangu; tegemeo la moyo wangu limo kwake. Amenisaidia nami nikashangilia kwa moyo; kwa wimbo wangu ninamshukuru.

8 Mwenyezi-Mungu ni nguvu ya watu wake; yeye ni kimbilio la wokovu kwa mfalme wake mteule.

9 Ee Mungu, uwaokoe watu wako; uwabariki watu hao walio mali yako. Uwe mchungaji wao na kuwategemeza milele.

29

1 Mpeni Mwenyezi-Mungu heshima enyi viumbe vya mbinguni, semeni Mwenyezi-Mungu ni mtukufu na mwenye nguvu.

2 Semeni jina la Mwenyezi-Mungu ni tukufu. Mwabuduni katika mahali pake patakatifu.

3 Sauti ya Mwenyezi-Mungu yasikika juu ya maji; Mungu mtukufu angurumisha radi, sauti ya Mwenyezi-Mungu yasikika juu ya bahari!

4 Sauti ya Mwenyezi-Mungu ina nguvu, sauti ya Mwenyezi-Mungu imejaa fahari.

5 Sauti ya Mwenyezi-Mungu huvunja mierezi; Mwenyezi-Mungu avunja mierezi ya Lebanoni.

6 Huirusha milima ya Lebanoni kama ndama, milima ya Sirioni kama mwananyati.

7 Sauti ya Mwenyezi-Mungu hutoa miali ya moto.

8 Sauti ya Mwenyezi-Mungu hutetemesha jangwa, Mwenyezi-Mungu hutetemesha jangwa la Kadeshi.

9 Sauti ya Mwenyezi-Mungu huitikisa mivule, hukwanyua majani ya miti msituni, na hekaluni mwake wote wasema: “Utukufu kwa Mungu!”

10 Mwenyezi-Mungu ameketi juu ya gharika; Mwenyezi-Mungu ni mfalme atawalaye milele.

11 Mwenyezi-Mungu na awape watu wake nguvu! Mwenyezi-Mungu na awabariki watu wake kwa amani!

30

1 Ee Mwenyezi-Mungu, nakutukuza maana umeniokoa, wala hukuwaacha maadui zangu wanisimange.

2 Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu, nilikulilia msaada, nawe ukaniponya.

3 Ee Mwenyezi-Mungu, umeniokoa kutoka kuzimu; umenipa tena uhai, umenitoa miongoni mwa waendao kuzimu.

4 Mwimbieni Mwenyezi-Mungu sifa, enyi waaminifu wake; kumbukeni utakatifu wake na kumshukuru.

5 Hasira yake hudumu kitambo kidogo, wema wake hudumu milele. Kilio chaweza kuwapo hata usiku, lakini asubuhi huja furaha.

6 Mimi nilipofanikiwa, nilisema: “Kamwe sitashindwa!”

7 Kwa wema wako, ee Mwenyezi-Mungu, umeniimarisha kama mlima mkubwa. Lakini ukajificha mbali nami, nami nikafadhaika.

8 Nilikulilia wewe, ee Mwenyezi-Mungu; naam niliomba dua kwako ee Mwenyezi-Mungu:

9 “Je, utapata faida gani nikifa na kushuka hadi kwa wafu? Je, mavumbi ya wafu yanaweza kukusifu? Je, yanaweza kusimulia uaminifu wako?

10 Usikie, ee Mwenyezi-Mungu, unihurumie; ee Mwenyezi-Mungu, unisaidie!”

11 Wewe umegeuza maombolezo langu kuwa ngoma ya furaha; umeniondolea huzuni yangu, ukanizungushia furaha.

12 Mimi nitakusifu wala sitakaa kimya. Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu nitakushukuru milele.

31

1 Kwako, ee Mwenyezi-Mungu, nakimbilia usalama, usiniache niaibike kamwe; kwa uadilifu wako uniokoe.

2 Unitegee sikio, uniokoe haraka! Uwe kwangu mwamba wa usalama, ngome imara ya kuniokoa.

3 Naam, wewe ni mwamba wangu na ngome yangu; kwa hisani yako uniongoze na kunielekeza.

4 Unitoe katika mtego walionitegea mafichoni; maana wewe ni kimbilio la usalama wangu.

5 Mikononi mwako naiweka roho yangu; umenikomboa, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu mwaminifu.

6 Wawachukia wanaoabudu sanamu batili; lakini mimi nakutumainia wewe, ee Mwenyezi-Mungu.

7 Nitashangilia na kufurahia fadhili zako, maana wewe waiona dhiki yangu, wajua na taabu ya nafsi yangu.

8 Wewe hukuniacha nitiwe mikononi mwa maadui zangu; umenisimamisha mahali pa usalama.

9 Unionee huruma, ee Mwenyezi-Mungu, niko taabuni; macho yangu yamechoka kwa huzuni, nimeishiwa nguvu mwilini na rohoni.

10 Maisha yangu yamekwisha kwa majonzi; naam, miaka yangu kwa kulalamika. Nguvu zangu zimeniishia kwa kutaabika; hata mifupa yangu imekauka.

11 Nimekuwa dharau kwa maadui zangu wote; kioja kwa majirani zangu. Rafiki zangu waniona kuwa kitisho; wanionapo njiani hunikimbia.

12 Nimesahaulika kama mtu aliyekufa; nimekuwa kama chungu kilichovunjikavunjika.

13 Nasikia watu wakinongonezana, vitisho kila upande; wanakula njama dhidi yangu, wanafanya mipango ya kuniua.

14 Lakini mimi nakutumainia wewe, ee Mwenyezi-Mungu. Nasema: “Wewe ni Mungu wangu!”

15 Maisha yangu yamo mikononi mwako; uniokoe na maadui zangu, niokoe na hao wanaonidhulumu.

16 Uniangalie kwa wema mimi mtumishi wako; uniokoe kwa fadhili zako.

17 Usiniache niaibike ee Mwenyezi-Mungu, maana mimi ninakuomba; lakini waache waovu waaibike, waache wapotelee kwa mshangao huko kuzimu.

18 Izibe midomo ya hao watu waongo, watu walio na kiburi na majivuno, ambao huwadharau watu waadilifu.

19 Jinsi gani ulivyo mwingi wema wako, uliowawekea wale wanaokucha! Wanaokimbilia usalama kwako wawapa mema binadamu wote wakiona.

20 Wawaficha mahali salama hapo ulipo, mbali na mipango mibaya ya watu; wawaweka salama katika ulinzi wako, mbali na ubishi wa maadui zao.

21 Asifiwe Mwenyezi-Mungu, maana amenionesha fadhili zake kwa namna ya ajabu, nilipozingirwa kama mji unaoshambuliwa.

22 Nami niliogopa na kudhani kwamba ulikuwa umenitupa; kumbe, ulisikia kilio changu nilipokuita unisaidie.

23 Mpendeni Mwenyezi-Mungu, enyi watakatifu wake wote. Mwenyezi-Mungu huwalinda watu waaminifu; lakini huwaadhibu kabisa wenye kiburi wanavyostahili.

24 Muwe hodari na kupiga moyo konde, enyi nyote mnaomtumainia Mwenyezi-Mungu.

32

1 Heri yake mtu aliyesamehewa kosa lake, mtu ambaye dhambi yake imeondolewa kabisa.

2 Heri mtu ambaye Mwenyezi-Mungu hamwekei hatia, mtu ambaye hana hila moyoni mwake.

3 Wakati nilipokuwa sijakiri dhambi yangu, nilikuwa nimedhoofika kwa kulia mchana kutwa.

4 Mchana na usiku mkono wako ulinilemea; nikafyonzwa nguvu zangu, kama maji wakati wa kiangazi.

5 Kisha nilikiri makosa yangu kwako; wala sikuuficha uovu wangu. Nilisema ninakuungamia makosa yangu ee Mwenyezi-Mungu, ndipo nawe ukanisamehe dhambi zangu zote.

6 Kwa hiyo, kila mwaminifu na akuletee maombi; jeshi likaribiapo au mafuriko, hayo hayatamfikia yeye.

7 Wewe ndiwe kinga yangu; wewe wanilinda katika taabu. Umenijalia shangwe za kukombolewa.

8 Mungu asema: “Nitakufunza na kukuonesha njia unayopaswa kufuata. Nitakushauri kwa uangalifu mkubwa.

9 Usiwe mpumbavu kama farasi au nyumbu, ambao lazima wafungwe lijamu na hatamu, la sivyo hawatakukaribia.”

10 Watu waovu watapata mateso mengi, bali wanaomtumainia Mwenyezi-Mungu wazungukwa na fadhili zake.

11 Furahini na kushangilia kwa sababu ya Mwenyezi-Mungu enyi waadilifu; pigeni vigelegele vya shangwe enyi wanyofu wa moyo.

33

1 Shangilieni kwa sababu ya Mwenyezi-Mungu enyi waadilifu! Kumsifu Mungu ni wajibu wa watu wanyofu.

2 Msifuni Mwenyezi-Mungu kwa zeze; mwimbieni kwa kinubi cha nyuzi kumi.

3 Mwimbieni wimbo mpya; pigeni kinubi vizuri na kushangilia.

4 Neno la Mwenyezi-Mungu ni la kweli; na matendo yake yote ni ya kuaminika.

5 Mungu apenda uadilifu na haki, dunia imejaa fadhili za Mwenyezi-Mungu.

6 Mbingu ziliumbwa kwa neno la Mwenyezi-Mungu, na vyote vilivyomo kwa pumzi ya mdomo wake.

7 Alikusanya maji ya bahari kama katika chupa, vilindi vya bahari akavifunga ghalani.

8 Dunia yote na imwogope Mwenyezi-Mungu! Wakazi wote duniani, wamche!

9 Maana alisema na ulimwengu ukawako; alitoa amri nao ukajitokeza.

10 Mwenyezi-Mungu hupangua mipango ya mataifa, na kuyatangua mawazo yao.

11 Mpango wa Mwenyezi-Mungu hudumu milele; maazimio yake yadumu vizazi vyote.

12 Heri taifa ambalo Mungu wake ni Mwenyezi-Mungu; heri wale aliowachagua kuwa watu wake mwenyewe!

13 Mwenyezi-Mungu huangalia chini kutoka mbinguni, na kuwaona wanadamu wote.

14 Kutoka kwenye kiti chake cha enzi, huwaangalia wakazi wote wa dunia.

15 Yeye huunda mioyo ya watu wote, yeye ajua kila kitu wanachofanya.

16 Mfalme hawezi kuokolewa kwa kuwa na jeshi kubwa; wala shujaa hapati ushindi kwa nguvu zake kubwa.

17 Farasi wa vita hafai kitu kwa kupata ushindi; nguvu zake nyingi haziwezi kumwokoa mtu.

18 Mwenyezi-Mungu huwaangalia wale wamchao, watu ambao wanatumainia fadhili zake.

19 Yeye huwaokoa katika kifo, huwaweka hai wakati wa njaa.

20 Mioyo yetu yamtumainia Mwenyezi-Mungu. Yeye ni msaada wetu na ngao yetu.

21 Naam twafurahi kwa sababu yake; tuna matumaini katika jina lake takatifu.

22 Fadhili zako zikae nasi, ee Mwenyezi-Mungu, kwani sisi tumekuwekea tumaini letu.

34

1 Nitamtukuza Mwenyezi-Mungu nyakati zote, sitaacha kamwe kuzitamka sifa zake.

2 Mimi nitaona fahari juu ya Mwenyezi-Mungu, wanyonge wasikie na kufurahi.

3 Mtukuzeni Mwenyezi-Mungu pamoja nami, sote pamoja tulisifu jina lake.

4 Nilimwomba Mwenyezi-Mungu naye akanijibu, na kuniondoa katika hofu zangu zote.

5 Mgeukieni Mungu mpate kufurahi; nanyi hamtaaibishwa kamwe.

6 Maskini alimlilia Mwenyezi-Mungu, naye akamsikia, na kumwokoa katika taabu zake zote.

7 Malaika wa Mwenyezi-Mungu huwalinda wote wamchao, na kuwaokoa katika hatari.

8 Jaribuni mwone Mwenyezi-Mungu alivyo mwema. Heri mtu anayekimbilia usalama kwake.

9 Mcheni Mwenyezi-Mungu enyi watakatifu wake; maana wenye kumcha hawatindikiwi na kitu.

10 Hata wanasimba hutindikiwa na kuona njaa; lakini wanaomtafuta Mwenyezi-Mungu hawakosi chochote chema.

11 Njoni enyi vijana mkanisikilize, nami nitawafundisha kumcha Mwenyezi-Mungu.

12 Je, watamani kufurahia maisha, kuishi maisha marefu na kufurahia mema?

13 Basi, acha kusema mabaya, na kuepa kusema uongo.

14 Jiepushe na uovu, utende mema; utafute amani na kuizingatia.

15 Mwenyezi-Mungu huwaangalia waadilifu, na kusikiliza malalamiko yao;

16 lakini huwapinga watu watendao maovu, awafutilie mbali kutoka duniani.

17 Waadilifu wakimlilia Mwenyezi-Mungu yeye huwasikia, na kuwaokoa katika taabu zao zote.

18 Mwenyezi-Mungu yu karibu na waliokufa moyo; huwaokoa wote waliokata tamaa kabisa.

19 Mateso ya mwadilifu ni mengi, lakini Mwenyezi-Mungu humwokoa kutoka yote.

20 Huvilinda viungo vya mwili wake wote, hakuna hata mfupa wake mmoja utakaovunjwa.

21 Ubaya huwaletea waovu kifo; wanaowachukia waadilifu wataadhibiwa.

22 Mwenyezi-Mungu huokoa maisha ya watumishi wake, wote wanaomkimbilia hawataadhibiwa.

35

1 Ee Mwenyezi-Mungu, uwapinge hao wanaonipinga; uwashambulie hao wanaonishambulia.

2 Utwae ngao yako na kingio lako, uinuke uje ukanisaidie!

3 Chukua mkuki na sime yako dhidi ya wanaonifuatia. Niambie mimi kwamba utaniokoa.

4 Waone haya na kuaibika, hao wanaoyanyemelea maisha yangu! Warudishwe nyuma kwa aibu, hao wanaozua mabaya dhidi yangu.

5 Wawe kama makapi yapeperushwayo na upepo, wakikimbizwa na malaika wa Mwenyezi-Mungu!

6 Njia yao iwe ya giza na utelezi, wakifukuzwa na malaika wa Mwenyezi-Mungu!

7 Maana walinitegea mitego bila sababu; walinichimbia shimo bila kisa chochote.

8 Maangamizi yawapate wao kwa ghafla, wanaswe katika mtego wao wenyewe, watumbukie humo na kuangamia!

9 Hapo mimi nitafurahi kwa sababu ya Mwenyezi-Mungu; nitashangilia kwa kuwa yeye ameniokoa.

10 Nitamwambia Mwenyezi-Mungu kwa moyo wangu wote: “Wewe ee Mwenyezi-Mungu, hakuna aliye kama wewe! Wewe wawaokoa wanyonge makuchani mwa wenye nguvu, maskini na fukara mikononi mwa wanyanganyi.”

11 Mashahidi wakorofi wanajitokeza; wananiuliza mambo nisiyoyajua.

12 Wananilipa mema yangu kwa mabaya; nami binafsi nimebaki katika ukiwa.

13 Lakini wao walipokuwa wagonjwa, mimi nilivaa magunia kuonesha huzuni; nilijitesa kwa kujinyima chakula. Nilisali nikiwa nimeinamisha kichwa,

14 kana kwamba namlilia rafiki au ndugu yangu. Nilikwenda huko na huko kwa huzuni, kama mtu anayeomboleza kifo cha mama yake.

15 Lakini mimi nilipoanguka walikusanyika kunisimanga. Walikusanyika pamoja dhidi yangu. Watu nisiowajua walinirarua bila kukoma, wala hakuna aliyewazuia.

16 Watu ambao huwadhihaki vilema, walinisagia meno yao kwa chuki.

17 Ee Mwenyezi-Mungu, utatazama tu mpaka lini? Uniokoe kutoka kwenye mashambulio yao; uyaokoe maisha yangu na simba hao.

18 Hapo nitakushukuru kati ya kusanyiko kubwa la watu; nitakutukuza kati ya jumuiya kubwa ya watu.

19 Usiwaache maadui hao wabaya wanisimange, hao wanichukiao bure wafurahie mateso yangu.

20 Maneno wasemayo si ya amani, wanazua maneno ya hila dhidi ya wananchi watulivu.

21 Wananishtaki kwa sauti: “Haya! Haya! Tumeona wenyewe uliyotenda!”

22 Lakini wewe Mwenyezi-Mungu waona jambo hilo, usinyamaze, ee Mwenyezi-Mungu, usikae mbali nami.

23 Uinuke, ee Mwenyezi-Mungu, ukanitetee; uje, ee Mungu wangu, uangalie kisa changu.

24 Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu, unitetee, ufanye kulingana na uadilifu wako; usiwaache maadui zangu wanisimange.

25 Usiwaache wajisemee: “Tumefanikiwa tulivyotaka!” Au waseme: “Tumemmaliza huyu!”

26 Waache hao wanaofurahia maafa yangu, washindwe wote na kufedheheka. Hao wote wanaojiona wema kuliko mimi, waone haya na kuaibika.

27 Lakini wanaotaka kuona kuwa sina hatia, wapaaze sauti kwa furaha waseme daima: “Mwenyezi-Mungu ni mkuu mno! Hupendezwa na fanaka ya mtumishi wake.”

28 Hapo nami nitatangaza uadilifu wako; nitasema sifa zako mchana kutwa.

36

1 Dhambi huongea na mtu mwovu, ndani kabisa moyoni mwake; jambo la kumcha Mungu halimo kabisa kwake.

2 Mwovu hujipendelea mwenyewe, hufikiri uovu wake hautagunduliwa na kulaaniwa.

3 Kila asemacho ni uovu na uongo; ameacha kutumia hekima na kutenda mema.

4 Alalapo huwaza kutenda maovu, hujiweka katika njia isiyo njema, wala haachani na uovu.

5 Fadhili zako ee Mwenyezi-Mungu zaenea hata mbinguni; uaminifu wako wafika mawinguni.

6 Uadilifu wako ni kama milima mikubwa, hukumu zako ni kama vilindi vya bahari. Wewe, ee Mwenyezi-Mungu, wawalinda wanadamu na wanyama

7 Jinsi gani zilivyo bora fadhili zako! Wanadamu hukimbilia kivulini mwa mabawa yako.

8 Wawashibisha kwa utajiri wa nyumba yako; wawanywesha kutoka mto wa wema wako.

9 Wewe ndiwe asili ya uhai; kwa mwanga wako twaona mwanga.

10 Uendelee kuwafadhili wale wanaokutambua; uzidi kuwa mwema kwa wanyofu wa moyo.

11 Usikubali wenye majivuno wanivamie, wala watu waovu wanikimbize.

12 Kumbe watendao maovu wameanguka; wameangushwa chini, hawawezi kuinuka.

37

1 Usihangaike kwa sababu ya waovu; usiwaonee wivu watendao mabaya.

2 Maana hao watatoweka mara kama nyasi; watanyauka kama mimea mibichi.

3 Mtumainie Mwenyezi-Mungu na kutenda mema, upate kuishi katika nchi na kuwa salama.

4 Uitafute furaha yako kwa Mwenyezi-Mungu, naye atakujalia unayotamani moyoni.

5 Mkabidhi Mwenyezi-Mungu maisha yako; mtumainie yeye naye atafanya kitu.

6 Ataufanya wema wako ungae kama mwanga, na uadilifu wako kama jua la adhuhuri.

7 Tulia mbele ya Mwenyezi-Mungu, mngojee kwa saburi; usihangaike juu ya wale wanaofanikiwa, watu wanaofaulu katika mipango yao mibaya.

8 Epuka hasira wala usiwe na ghadhabu; usihangaike maana hiyo huzidisha ubaya.

9 Watu watendao mabaya wataangamizwa, bali wanaomtumaini Mwenyezi-Mungu wataimiliki nchi.

10 Bado kitambo kidogo, naye mwovu atatoweka; utamtafuta pale alipokuwa, wala hutamwona.

11 Lakini wapole wataimiliki nchi, hao watafurahia wingi wa fanaka.

12 Mwovu hula njama dhidi ya mwadilifu, na kumsagia meno kwa chuki.

13 Lakini Mwenyezi-Mungu humcheka mwovu, kwani ajua mwisho wake u karibu.

14 Waovu huchomoa panga na kuvuta pinde zao, wapate kuwaua maskini na fukara; wawachinje watu waishio kwa unyofu.

15 Lakini panga zao zitawapenya wao wenyewe, na pinde zao zitavunjwavunjwa.

16 Afadhali mali kidogo ya mtu mwadilifu kuliko utajiri wa watu waovu wengi.

17 Maana nguvu za waovu zitavunjwa, lakini Mwenyezi-Mungu huwategemeza waadilifu.

18 Mwenyezi-Mungu hutunza maisha ya watu waaminifu, na urithi wao utadumu milele.

19 Hawataaibika zikifika nyakati mbaya; siku za njaa watakuwa na chakula tele.

20 Lakini waovu wataangamia, maadui za Mwenyezi-Mungu watanyauka kama maua nyikani; naam, watatoweka kama moshi.

21 Mtu mwovu hukopa bila kurudisha; lakini mwadilifu hutoa kwa ukarimu.

22 Waliobarikiwa na Mwenyezi-Mungu wataimiliki nchi, lakini waliolaaniwa naye watafutiliwa mbali.

23 Mwenyezi-Mungu huziongoza nyayo za mtu, humlinda yule ampendezaye.

24 Ajapoanguka, haanguki akabaki chini, kwa sababu Mwenyezi-Mungu humtegemeza.

25 Nilikuwa kijana na sasa ni mzee; kamwe sijaona mwadilifu ameachwa na Mungu, au watoto wake wakiombaomba chakula.

26 Daima huwapa wengine kwa furaha na kukopesha, na watoto wake ni baraka.

27 Achana na uovu, utende mema, nawe utaishi nchini daima;

28 maana Mwenyezi-Mungu hupenda uadilifu, wala hawaachi waaminifu wake. Huwalinda hao milele; lakini wazawa wa waovu wataangamizwa.

29 Waadilifu wataimiliki nchi, na wataishi humo milele.

30 Mtu mwadilifu husema maneno ya hekima, kwa ulimi wake hunena yaliyo ya haki.

31 Huizingatia moyoni mwake sheria ya Mungu wake; naye hatetereki katika mwenendo wake.

32 Mtu mwovu humvizia mtu mwema na kujaribu kumuua;

33 lakini Mwenyezi-Mungu hatamtia mtu mwema makuchani mwake, wala kumwacha apatilizwe akishtakiwa.

34 Mtumainie Mwenyezi-Mungu na kushika njia yake, naye atakukuza uimiliki nchi, na kuwaona waovu wakiangamizwa.

35 Nilimwona mwovu mdhalimu sana, alijiweka juu ya wote kama mierezi ya Lebanoni!

36 Baadaye nikapita hapo, naye hakuwapo tena; nikamtafuta, lakini hakuonekana tena.

37 Mwangalie mtu mwema, mtu mwadilifu; mtu anayependa amani hujaliwa wazawa.

38 Lakini wakosefu wote wataangamizwa; na wazawa wao watafutiliwa mbali.

39 Mwenyezi-Mungu huwaokoa waadilifu, na kuwalinda wakati wa taabu.

40 Mwenyezi-Mungu huwasaidia na kuwaokoa; huwatoa makuchani mwa waovu na kuwaokoa, maana wanakimbilia usalama kwake.

38

1 Ee Mwenyezi-Mungu, usinikemee kwa hasira yako; usiniadhibu kwa ghadhabu yako.

2 Mishale yako imenichoma; mkono wako umenigandamiza.

3 Hamna mahali nafuu mwilini mwangu, kwa sababu umenikasirikia; hamna penye afya hata mifupani mwangu, kwa sababu ya dhambi yangu.

4 Nimefunikwa kabisa na dhambi zangu, zinanilemea kama mzigo mzito mno kwangu.

5 Madonda yangu yameoza na kunuka, na hayo ni matokeo ya ujinga wangu.

6 Nimepindika mpaka chini na kupondeka; mchana kutwa nazunguka nikiomboleza.

7 Viungo vyangu vimeshambuliwa na homa; mwilini mwangu hamna nafuu yoyote.

8 Nimelegea na kupondekapondeka; nasononeka kwa kusongwa moyoni.

9 Ee Bwana, wewe wajua tazamio langu lote; kwako hakikufichika kilio changu.

10 Moyo wanidunda, nguvu zimeniishia; hata macho yangu nayo yamekwisha fifia.

11 Rafiki na wenzangu wanaepa kuona mateso yangu, na jamaa zangu wanakaa mbali nami.

12 Wanaotaka kuniua wanatega mitego yao; wanaonitakia niumie wanatishia kuniangamiza. Mchana kutwa wanafanya mipango dhidi yangu.

13 Lakini mimi nimekuwa kama kiziwi, sisikii; nimekuwa kama bubu asiyeweza kusema kitu.

14 Naam, nimekuwa kama mtu asiyesikia, kama mtu asiye na chochote cha kujitetea.

15 Lakini ninakutumainia wewe, ee Mwenyezi-Mungu; wewe, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu, ndiwe utakayenijibu.

16 Nakuomba tu maadui wasinisimange, wasione fahari juu ya kuanguka kwangu.

17 Karibu sana nitaanguka; nakabiliwa na maumivu ya daima.

18 Naungama uovu wangu; dhambi zangu zanisikitisha.

19 Maadui zangu hawajambo, wana nguvu; ni wengi mno hao wanaonichukia bure.

20 Hao wanaonilipa maovu kwa wema wangu, wananipinga kwa sababu natenda mema.

21 Usinitupe, ee Mwenyezi-Mungu; ee Mungu wangu, usikae mbali nami.

22 Uje haraka kunisaidia; ewe Mwenyezi-Mungu, uliye wokovu wangu.

39

1 Nilisema: “Nitayachunga maisha yangu, nisije nikatenda dhambi kwa usemi wangu. Nitafunga mdomo wangu waovu wawapo karibu nami.”

2 Nilikuwa kama bubu, bila kusema kitu, nilinyamaza lakini sikupata nafuu. Mateso yangu yalizidi kuwa makali,

3 mahangaiko yangu yakaniunguza moyoni. Kadiri nilivyowaza ndivyo nilivyotaabika, kisha maneno haya yakanitoka:

4 “Ee Mwenyezi-Mungu, unijulishe mwisho wangu, siku zangu za kuishi zimenibakia ngapi, nijue yapitavyo kasi maisha yangu!”

5 Kumbe umenipimia maisha mafupi sana! Maisha yangu si kitu mbele yako. Hakika, kila binadamu ni kama pumzi tu!

6 Kweli, kila mtu anapita kama kivuli; jitihada zake zote ni bure tu; anakusanya mali, asijue atakayeipata!

7 Na sasa, ee Bwana, ninatazamia nini? Tumaini langu ni kwako wewe!

8 Uniokoe katika makosa yangu yote; usikubali wapumbavu wanidhihaki.

9 Niko kama bubu, sisemi kitu, kwani wewe ndiwe uliyetenda hayo.

10 Usiniadhibu tena; namalizika kwa mapigo yako.

11 Unapomwadhibu mtu dhambi zake kwa kumkemea, unaharibu kama nondo kile akipendacho. Hakika, kila binadamu ni kama pumzi tu!

12 Usikie sala yangu, ee Mwenyezi-Mungu; usikilize kilio changu, usikae kimya ninapolia. Maana, mimi ni kama mgeni tu apitaye, ni msafiri kama walivyokuwa wazee wangu wote.

13 Uache kunitazama nipate kufurahi kidogo, kabla sijaaga dunia, na kutoweka kabisa.

40

1 Nilimngojea Mwenyezi-Mungu kwa uvumilivu, akanielekea na kukisikia kilio changu.

2 Aliniondoa katika shimo la hatari, alinitoa katika matope ya dimbwi, akanisimamisha salama juu ya mwamba, na kuziimarisha hatua zangu.

3 Alinifundisha wimbo mpya, wimbo wa sifa kwa Mungu wetu. Wengi wataona na kuogopa, na kumtumainia Mwenyezi-Mungu.

4 Heri mtu anayemtumainia Mwenyezi-Mungu; mtu asiyejiunga na watu wenye majivuno, watu waliopotoka kwa kuabudu miungu ya uongo.

5 Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu, umetufanyia mengi ya ajabu, na mipango yako juu yetu haihesabiki; hakuna yeyote aliye kama wewe. Kama ningeweza kusimulia hayo yote, idadi yake ingenishinda.

6 Wewe hutaki tambiko wala sadaka, tambiko za kuteketeza wala za kuondoa dhambi; lakini umenipa masikio nikusikie.

7 Ndipo niliposema: “Niko tayari; ninayotakiwa kufanya yameandikwa katika kitabu cha sheria;

8 kutimiza matakwa yako, ee Mungu wangu ni furaha yangu, sheria yako naishika kwa moyo wangu wote!”

9 Nimesimulia habari njema za ukombozi, mbele ya kusanyiko kubwa la watu. Kama ujuavyo ee Mwenyezi-Mungu, mimi sikujizuia kuitangaza.

10 Sikuuficha moyoni mwangu ukombozi ulionijalia, nimetangaza daima kuwa wewe ni mwokozi mwaminifu; sikulificha kusanyiko kubwa la watu fadhili zako na uaminifu wako.

11 Ee Mwenyezi-Mungu, usininyime huruma yako! Fadhili zako na uaminifu wako vinihifadhi daima.

12 Maafa yasiyohesabika yanizunguka, maovu yangu yanikaba hata siwezi kuona; ni mengi kuliko nywele kichwani mwangu, nami nimevunjika moyo.

13 Upende ee Mwenyezi-Mungu kuniokoa; ee Mwenyezi-Mungu, uje haraka kunisaidia.

14 Wanaonuia kuniangamiza, na waaibike na kufedheheka! Hao wanaotamani niumie, na warudi nyuma na kuaibika!

15 Hao wanaonisimanga, na wapumbazike kwa kushindwa kwao!

16 Lakini wote wale wanaokutafuta wafurahi na kushangilia kwa sababu yako. Wapendao wokovu wako, waseme daima: “Mwenyezi-Mungu ni Mkuu!”

17 Mimi ni maskini na fukara, ee Bwana; lakini ee Bwana wewe wanikumbuka. Ndiwe msaada wangu na mwokozi wangu; uje, ee Mungu wangu, usikawie!

41

1 Heri mtu anayewajali maskini; Mwenyezi-Mungu atamwokoa wakati wa shida.

2 Mwenyezi-Mungu atamlinda na kumweka hai, naye atafanikiwa katika nchi; Mungu hatamwacha makuchani mwa maadui zake.

3 Mwenyezi-Mungu atamsaidia awapo mgonjwa, atamponya maradhi yake yote.

4 Nami nilisema: “Unifadhili, ee Mwenyezi-Mungu, unihurumie maana nimekukosea wewe.”

5 Madui zangu husema vibaya juu yangu: “Atakufa lini na jina lake litoweke!”

6 Wanitembeleapo husema maneno matupu; wanakusanya mabaya juu yangu, na wafikapo nje huwatangazia wengine.

7 Wote wanichukiao hunongonezana juu yangu; wananiwazia mabaya ya kunidhuru.

8 Husema: “Maradhi haya yatamuua; hatatoka tena kitandani mwake!”

9 Hata rafiki yangu wa moyoni niliyemwamini, rafiki ambaye alishiriki chakula changu, amegeuka kunishambulia!

10 Ee Mwenyezi-Mungu, unionee huruma! Unipe nafuu, nami nitawalipiza.

11 Hivyo nitajua kwamba unapendezwa nami, maadui zangu wasipopata fahari juu yangu.

12 Wewe umenitegemeza kwani natenda mema; waniweka mbele yako milele.

13 Asifiwe Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, tangu milele na hata milele! Amina! Amina!

42

1 Kama paa atamanivyo maji ya kijito, ndivyo ninavyokutamani, ee Mungu wangu!

2 Naona kiu ya Mungu, kiu ya Mungu aliye hai. Nitafika lini kwake na kuuona uso wake?

3 Machozi yamekuwa chakula changu mchana na usiku, waliponiambia kila siku: “Yuko wapi Mungu Wako!”

4 Nakumbuka tena mambo haya kwa majonzi moyoni mwangu: Jinsi nilivyokwenda na umati wa watu, nikawaongoza kwenda nyumbani kwa Mungu wakipiga vigelegele vya shukrani; umati wa watu wakifanya sherehe!

5 Mbona nasononeka hivyo moyoni? Kwa nini nahangaika hivyo ndani mwangu? Nitamtumainia Mungu, maana nitamsifu tena yeye aliye msaada wangu na Mungu wangu.

6 Nimesongwa na huzuni moyoni mwangu, kwa hiyo ninakukumbuka wewe, ee Mungu, kutoka katika eneo la Yordani, kutoka mlima Hermoni na Mizari.

7 Nimeporomoshewa mafuriko ya maji mafuriko ya maji yaja karibu nayo yaita maporomoko mapya. Mawimbi na mapigo yako yamenikumba.

8 Mwenyezi-Mungu atanijalia fadhili zake mchana; nami nimwimbie wimbo wa sifa usiku, nimwombe Mungu anipaye uhai.

9 Namwambia Mungu, mwamba wangu: “Kwa nini umenisahau? Yanini niende huko na huko nikiomboleza kwa kudhulumiwa na adui yangu?”

10 Nimepondwa kwa matukano yao, wanaponiuliza kila siku: “Yuko wapi, Mungu wako!”

11 Mbona nasononeka hivyo moyoni? Kwa nini nahangaika hivyo? Nitamtumainia Mungu, maana nitamsifu tena Mungu, aliye msaada wangu na Mungu wangu.

43

1 Onesha kuwa sina hatia ee Mungu; utetee kisa changu dhidi ya watu wabaya; uniokoe na watu waongo na waovu.

2 Nakimbilia usalama kwako ee Mungu; kwa nini umenitupilia mbali? Yanini niende huko na huko nikiomboleza kwa kudhulumiwa na adui yangu?

3 Upeleke mwanga na ukweli wako viniongoze, vinipeleke kwenye mlima wako mtakatifu, kwenye makao yako.

4 Hapo, ee Mungu, nitakwenda madhabahuni pako; nitakuja kwako, ee Mungu, furaha yangu kuu. Nitakusifu kwa zeze, ee Mungu, Mungu wangu.

5 Mbona ninahuzunika hivyo moyoni? Kwa nini nahangaika hivyo ndani mwangu? Nitamtumainia Mungu, nitamsifu tena yeye aliye msaada wangu na Mungu wangu.

44

1 Ee Mungu, sisi tumesikia kwa masikio yetu, wazee wetu wametusimulia mambo uliyotenda nyakati zao, naam, mambo uliyotenda hapo kale:

2 Kwa mkono wako mwenyewe uliyafukuza mataifa mengine, na mahali pao ukawakalisha watu wako; uliyaadhibu mataifa mengine, na kuwafanikisha watu wako.

3 Watu wako hawakuitwaa nchi kwa silaha zao, wala hawakupata ushindi kwa nguvu zao; ila uliwasalimisha kwa mkono wako mwenyewe, kwa kuwaangazia uso wako, kwani wewe uliwapenda.

4 Wewe ni mfalme wangu na Mungu wangu! Wawajalia ushindi wazawa wa Yakobo.

5 Kwa nguvu yako twawashinda maadui zetu, kwa jina lako twawakanyaga wanaotushambulia.

6 Mimi siutegemei upinde wangu, wala upanga wangu hauwezi kuniokoa.

7 Wewe ndiwe uliyetuokoa na maadui zetu; uliwavuruga wale waliotuchukia.

8 Daima tutaona fahari juu yako, ee Mungu; tutakutolea shukrani milele.

9 Lakini sasa umetuacha na kutufedhehesha; huandamani tena na majeshi yetu.

10 Umetufanya tuwakimbie maadui zetu, nao wakaziteka nyara mali zetu.

11 Umetufanya kama kondoo wanaopelekwa kuchinjwa; umetutawanya kati ya mataifa mengine.

12 Umewauza watu wako kwa bei ya chini; wala hukupata faida yoyote.

13 Umetufanya kuwa kioja kwa jirani zetu, nao wanatudhihaki na kutucheka.

14 Umetufanya tudharauliwe na watu wa mataifa; wanatutikisia vichwa vyao kwa kutupuuza.

15 Mchana kutwa fedheha yaniandama, na uso wangu umejaa aibu tele

16 kwa maneno na madharau ya wenye kunitukana, kwa kukabiliwa na maadui zangu na walipiza kisasi.

17 Hayo yote yametupata sisi ijapokuwa hatujakusahau, wala hatujavunja agano lako.

18 Hatujakuasi wewe, wala hatujaziacha njia zako.

19 Hata hivyo umetuacha hoi kati ya wanyama wakali; umetuacha katika giza kuu.

20 Tungalikuwa tumekusahau wewe Mungu wetu, tukamkimbilia mungu wa uongo,

21 ee Mungu, ungalikwisha jua jambo hilo, kwa maana wewe wazijua siri za moyoni.

22 Lakini kwa ajili yako twakikabili kifo kila siku; tunatendewa kama kondoo wanaopelekwa kuchinjwa.

23 Amka, ee Bwana! Mbona umelala? Inuka! Tafadhali usitutupe milele!

24 Mbona wajificha mbali nasi, na kusahau dhiki na mateso yetu?

25 Tumedidimia hata mavumbini, tumegandamana na ardhi.

26 Uinuke, uje kutusaidia! Utukomboe kwa sababu ya fadhili zako.

45

1 Moyo wangu umejaa mawazo mema: Namtungia mfalme shairi langu, ulimi wangu ni kama kalamu ya mwandishi stadi.

2 Wewe u mzuri kuliko wanadamu wote, maneno yako ni fadhili tupu. Kwa hiyo Mungu amekubariki milele.

3 Jifunge upanga wako, ewe shujaa! Wewe ni mtukufu na mwenye fahari.

4 Songa mbele kwa utukufu upate ushindi, utetee ukweli na kulinda haki. Mkono wako utende mambo makuu.

5 Mishale yako ni mikali, hupenya mioyo ya maadui za mfalme; nayo mataifa huanguka chini yako.

6 Kiti chako cha enzi ni imara, chadumu milele kama cha Mungu. Wewe watawala watu wako kwa haki.

7 Wapenda uadilifu na kuchukia uovu. Kwa hiyo Mungu, Mungu wako, amekuteua, na kukupa furaha kuliko wenzako.

8 Mavazi yako yanukia marashi na udi, wanamuziki wakuimbia katika majumba ya pembe za ndovu.

9 Binti za wafalme ni baadhi ya wanaokulaki, naye malkia amesimama kulia kwako, amevaa mapambo ya dhahabu safi ya Ofiri.

10 Sikiliza binti, ufikirie! Tega sikio lako: Sahau sasa watu wako na jamaa zako.

11 Uzuri wako wamvutia mfalme; yeye ni bwana wako, lazima umtii.

12 Watu wa Tiro watakuletea zawadi; matajiri watataka upendeleo wako.

13 Binti mfalme anaingia mzuri kabisa! Vazi lake limefumwa kwa nyuzi za dhahabu.

14 Akiwa amevalia vazi la rangi nyingi, anaongozwa kwa mfalme, akisindikizwa na wasichana wenzake; nao pia wanapelekwa kwa mfalme.

15 Kwa furaha na shangwe wanafika huko, na kuingia katika jumba la mfalme.

16 Ee mfalme, utapata watoto wengi watakaotawala mahali pa wazee wako; utawafanya watawale duniani kote.

17 Nitalifanya jina lako litukuzwe katika vizazi vyote, nayo mataifa yatakusifu daima na milele.

46

1 Mungu ni kimbilio letu na nguvu yetu; yeye ni msaada wetu daima wakati wa taabu.

2 Kwa hiyo hatutaogopa chochote, dunia ijapoyeyuka na milima kutikisika kutoka baharini;

3 hata kama bahari ikichafuka na kutisha, na milima ikatetemeka kwa machafuko yake.

4 Kuna mto ambao maji yake hufurahisha mji wa Mungu, makao matakatifu ya Mungu Mkuu.

5 Mungu yumo mjini humo, nao hauwezi kutikiswa; Mungu ataupa msaada alfajiri na mapema.

6 Mataifa yaghadhibika na tawala zatikisika; Mungu anguruma nayo dunia yayeyuka.

7 Mwenyezi-Mungu wa majeshi yu pamoja nasi, Mungu wa Yakobo ni kimbilio letu.

8 Njoni mwone matendo ya Mwenyezi-Mungu; oneni maajabu aliyoyafanya duniani.

9 Hukomesha vita popote duniani, huvunjavunja pinde na mikuki, nazo ngao huziteketeza.

10 Asema: “Nyamazeni na kujua kuwa mimi ni Mungu! Mimi natukuka katika mataifa yote; mimi natukuzwa ulimwenguni kote!”

11 Mwenyezi-Mungu wa majeshi yu pamoja nasi, Mungu wa Yakobo ni kimbilio letu.

47

1 Enyi watu wote, pigeni makofi! Msifuni Mungu kwa sauti za shangwe!

2 Maana Mwenyezi-Mungu, Mungu Mkuu, anatisha. Yeye ni Mfalme mkuu wa ulimwengu wote.

3 Ametuwezesha kuwashinda watu wa mataifa, ameyaweka mataifa chini ya mamlaka yetu.

4 Ametuchagulia nchi hii iwe urithi wetu, ambayo ni fahari ya Yakobo anayempenda.

5 Mungu amepanda juu na vigelegele, Mwenyezi-Mungu na sauti ya tarumbeta.

6 Mwimbieni Mungu sifa, mwimbieni! Mwimbieni mfalme wetu sifa, mwimbieni!

7 Mwimbieni Mungu sifa kwa tenzi; maana yeye ni mfalme wa ulimwengu wote.

8 Mungu anayatawala mataifa yote; amekaa katika kiti chake cha enzi kitakatifu.

9 Viongozi wa watu wa mataifa wanakusanyika, wanajiunga na watu wa Mungu wa Abrahamu, maana nguvu zote duniani ni zake Mungu, yeye ametukuka sana.

48

1 Mwenyezi-Mungu, ni mkuu; astahili kusifiwa sana katika mji wake na mlima wake mtakatifu.

2 Mlima Siyoni huko kaskazini, wapendeza kwa urefu; mji wa Mfalme mkuu ni furaha ya ulimwengu.

3 Mungu anazilinda ngome zake; yeye amejionesha kuwa ngome ya usalama.

4 Wafalme walikusanyika, wakaenda pamoja kushambulia.

5 Lakini walipouona mji wa Siyoni, wakashangaa; wakashikwa na hofu, wakatimua mbio.

6 Hofu kuu iliwashika, wakasikia uchungu kama mama anayejifungua,

7 kama waliokumbwa na kimbunga cha mashariki ambacho huzivunjavunja meli za Tarshishi.

8 Yote tuliyosikia tumejionea wenyewe katika mji wa Mwenyezi-Mungu wa majeshi, naam, katika mji wa Mungu wetu; Mungu atauimarisha milele.

9 Ee Mungu, twazitafakari fadhili zako, tukiwa hekaluni mwako.

10 Jina lako lasifika kila mahali, sifa zako zaenea popote duniani. Kwa mkono wako umetenda kwa haki;

11 watu wa Siyoni na wafurahi! Watu wa Yuda na washangilie, kwa sababu ya maamuzi yako ya haki!

12 Tembeeni huko Siyoni mkauzunguke, mkaihesabu minara yake.

13 Zitazameni kuta zake na kuchunguza ngome zake; mpate kuvisimulia vizazi vijavyo, kwamba:

14 “Huyu ni Mungu, Mungu wetu milele! Atakuwa kiongozi wetu milele!”

49

1 Sikieni jambo hili enyi watu wote! Tegeni sikio enyi wakazi wote wa dunia;

2 sikilizeni nyote, wakubwa kwa wadogo, matajiri na maskini kwa pamoja.

3 Maneno yangu yatakuwa mazitomazito; mimi nitasema maneno ya hekima.

4 Nitatega sikio nisikilize methali, nitafafanua kitendawili kwa muziki wa zeze.

5 Ya nini niogope siku mbaya, wakati nizungukwapo na uovu wa adui?

6 Watu waovu hutegemea mali zao, hujisifia wingi wa utajiri wao.

7 Lakini binadamu hawezi kamwe kujikomboa mwenyewe; hawezi kumlipa Mungu bei ya maisha yake,

8 maana fidia ya maisha ni kubwa mno. Hawezi kutoa kitu chochote kinachotosha,

9 kimwezeshe aendelee kuishi daima, asipate kuonja kaburi.

10 Yeye afahamu kuwa hata wenye hekima hufa, wapumbavu hali kadhalika na watu wajinga. Wote hao huwaachia wengine mali zao.

11 Makaburi ni makao yao hata milele; ni makao yao vizazi hata vizazi, ingawa hapo awali walimiliki ardhi.

12 Binadamu hatadumu katika fahari yake; atakufa tu kama mnyama.

13 Hayo ndiyo yawapatao wanaojiamini kipumbavu, ndio mwisho wa wale wanaojivunia mali zao.

14 Wataongozwa kama kondoo hadi kuzimu, kifo kitakuwa mchungaji wao. Watashuka moja kwa moja kaburini. Miili yao itaozea huko, Kuzimu kutakuwa makao yao.

15 Lakini Mungu ataniokoa na kuzimu. Atanisalimisha kutoka huko.

16 Usihangaike ukiona mtu anatajirika, wala mali yake ikiongezeka zaidi na zaidi.

17 Maana atakapokufa hatachukua chochote, mali yake haitashuka huko chini pamoja naye.

18 Ajapojikuza katika maisha haya, na kusifiwa kwa sababu ya kufanikiwa,

19 atajiunga na wazee waliomtangulia kufa, ambao hawawezi kuona tena mwanga.

20 Binadamu hatadumu milele katika fahari yake, atakufa tu kama mnyama.

50

1 Mungu wa nguvu Mwenyezi-Mungu, amenena, amewaita wakazi wa dunia, tokea mawio ya jua hadi machweo yake.

2 Kutoka Siyoni, mji mzuri mno, Mungu anajitokeza, akiangaza.

3 Mungu wetu anakuja, na sio kimyakimya: Moto uunguzao wamtangulia, na dhoruba kali yamzunguka.

4 Kutoka juu anaziita mbingu na dunia; zishuhudie akiwahukumu watu wake:

5 “Nikusanyieni waaminifu wangu, waliofanya agano nami kwa tambiko!”

6 Mbingu zatangaza uadilifu wa Mungu; kwamba Mungu mwenyewe ni hakimu.

7 “Sikilizeni watu wangu, ninachosema! Israeli, natoa ushahidi dhidi yako. Mimi ni Mungu! Mimi ni Mungu wako!

8 Sikukaripii kwa sababu ya tambiko zako; hujaacha kunitolea tambiko za kuteketeza.

9 Kwa kweli sina haja na fahali wa zizi lako, wala beberu wa mifugo yako;

10 maana wanyama wote porini ni mali yangu, na maelfu ya wanyama milimani ni wangu.

11 Ndege wote wa mwitu ni mali yangu, na viumbe vyote hai mashambani ni vyangu.

12 Kama ningeona njaa singekuambia wewe, maana ulimwengu na vyote vilivyomo ni vyangu.

13 Je, wadhani nala nyama ya fahali, au Kunywa damu ya mbuzi?

14 Shukrani iwe ndio tambiko yako kwa Mungu mtimizie Mungu Aliye Juu ahadi zako.

15 Uniite wakati wa taabu, nami nitakuokoa, nawe utaniheshimu.”

16 Lakini Mungu amwambia mtu mwovu: “Ya nini kuzitajataja tu sheria zangu? Kwa nini unasemasema juu ya agano langu?

17 Wewe wachukia kuwa na nidhamu, na maneno yangu hupendi kuyafuata.

18 Ukimwona mwizi unaandamana naye, na wazinzi unashirikiana nao.

19 Uko tayari daima kunena mabaya; kazi ya ulimi wako ni kutunga uongo.

20 Wakaa kitako kumsengenya binadamu mwenzako, naam, kumchongea ndugu yako mwenyewe.

21 Umefanya hayo yote nami nimenyamaa. Je, wadhani kweli mimi ni kama wewe? Lakini sasa ninakukaripia, ninakugombeza waziwazi.

22 “Fikirini vizuri jambo hili, enyi msionijali, la sivyo nitawaangamizeni, wala hapatakuwa na wa kuwaokoeni.

23 Anayenipa shukrani kama tambiko yake, huyo ndiye anayeniheshimu; yeyote anayedumu katika njia yangu, huyo ndiye nitakayemwokoa.”

51

1 Nihurumie, Ee Mungu, kadiri ya fadhili zako; ufutilie mbali makosa yangu, kadiri ya wingi wa huruma yako.

2 Unioshe kabisa hatia yangu; unisafishe dhambi yangu.

3 Nakiri kabisa makosa yangu, daima naiona waziwazi dhambi yangu.

4 Nimekukosea wewe peke yako, nimetenda yaliyo mabaya mbele yako. Uamuzi wako ni wa haki hukumu yako haina lawama.

5 Mimi ni mkosefu tangu kuzaliwa kwangu, mwenye dhambi tangu tumboni mwa mama yangu.

6 Wewe wataka unyofu wa ndani; hivyo nifundishe hekima moyoni.

7 Unitakase kwa husopo, nitakate; unioshe niwe mweupe pe.

8 Nijaze furaha na shangwe, nifurahishe tena, mimi ambaye uliniponda.

9 Ugeuke, usiziangalie dhambi zangu; uzifute hatia zangu zote.

10 Uniumbie moyo safi, ee Mungu, uweke ndani yangu roho mpya na thabiti.

11 Usinitupe mbali nawe; usiniondolee roho yako takatifu.

12 Unifanye nifurahi tena kwa kuniokoa, utegemeze ndani yangu moyo wa utii.

13 Hapo nitawafunza wakosefu njia yako, nao wenye dhambi watarudi kwako.

14 Uniokoe na hatia ya umwagaji damu, ee Mungu, Mungu mwokozi wangu, nami nitaimba kwa sauti kuwa umeniokoa.

15 Uniwezeshe kusema, ee Bwana, midomo yangu itangaze sifa zako.

16 Kwa kweli wewe hupendezwi na tambiko, ama sivyo mimi ningalikutolea. Wewe huna haja na tambiko za kuteketezwa.

17 tambiko yangu kwako ee Mungu, ni moyo mnyofu; wewe, ee Mungu, hukatai moyo mnyofu na mtiifu.

18 Ee Mungu, upende kuutendea mema mji wa Siyoni; uzijenge tena upya kuta za mji wa Yerusalemu.

19 Hapo utapendezwa na tambiko za kweli: Sadaka za kuteketezwa na za kuteketezwa nzima; mafahali watatolewa tambiko madhabahuni pako.

52

1 Mbona, ewe jitu, wajivunia ubaya wako dhidi ya wenye kumcha Mungu?

2 Kila wakati unawaza maangamizi; ulimi wako ni kama wembe mkali! Unafikiria tu kutenda mabaya.

3 Wewe wapenda uovu kuliko wema, wapenda uongo kuliko ukweli.

4 Ewe mdanganyifu mkuu, wapenda mambo ya kuangamiza wengine.

5 Kwa hivyo Mungu atakuangamiza milele, atakunyakua na kukuondoa nyumbani mwako; atakungoa katika nchi ya walio hai.

6 Waadilifu wataona hayo na kuogopa, kisha watakucheka na kusema:

7 “Tazameni yaliyompata mtu huyu! Yeye hakutaka Mungu awe kimbilio lake; bali alitegemea wingi wa mali yake, na kutafuta humo usalama wake!”

8 Lakini mimi ni kama mzeituni mbichi, unaostawi katika nyumba ya Mungu. Nazitegemea fadhili zake milele na milele.

9 Ee Mungu, nitakushukuru daima, kwa ajili ya mambo uliyofanya. Nitatangaza kwamba wewe ni mwema, mbele ya watu wako waaminifu.

53

1 Wapumbavu hujisemea moyoni: “Hakuna Mungu!” Wote wamepotoka kabisa, wametenda mambo ya kuchukiza; hakuna hata mmoja atendaye jema.

2 Mungu anawaangalia wanadamu kutoka mbinguni, aone kama kuna yeyote mwenye busara, kama kuna yeyote anayemtafuta Mungu.

3 Lakini wote wamekosa, wote wamepotoka pamoja, hakuna atendaye mema, hakuna hata mmoja.

4 “Je, hao watendao maovu hawana akili? Wanawatafuna watu wangu kama mikate; wala hawanijali mimi Mungu!”

5 Hapo watashikwa na hofu kubwa, hofu ambayo hawajapata kuiona; maana Mungu ataitawanya mifupa ya adui, hao wataaibika maana Mungu amewakataa.

6 Laiti ukombozi wa Israeli ungefika kutoka Siyoni! Mungu atakaporekebisha hali ya watu wake, wazawa wa Yakobo watashangilia; Waisraeli watafurahi.

54

1 Uniokoe, ee Mungu, kwa jina lako; unitetee kwa nguvu yako.

2 Uisikie, ee Mungu, sala yangu; uyategee sikio maneno ya kinywa changu.

3 Watu wenye kiburi wananishambulia; wakatili wanayawinda maisha yangu, watu ambao hawamjali Mungu.

4 Najua Mungu ni msaada wangu, Mwenyezi-Mungu hutegemeza maisha yangu.

5 Yeye atawaadhibu maadui zangu kwa uovu wao wenyewe; kwa uaminifu wako, ee Mungu, uwaangamize.

6 Nitakutolea tambiko kwa moyo mkunjufu; nitakushukuru kwa kuwa ni vema.

7 Maana umeniokoa katika taabu zangu zote, nami nimewaona maadui zangu wameshindwa.

55

1 Ee Mungu, tega sikio usikie sala yangu; usiangalie pembeni ninapokuomba.

2 Unisikilize na kunijibu; nimechoshwa na lalamiko langu.

3 Nina hofu kwa vitisho vya maadui zangu, na kwa kudhulumiwa na watu waovu. Watu waovu wananitaabisha, kwa hasira wananifanyia uhasama.

4 Moyo wangu umejaa hofu, vitisho vya kifo vimenisonga.

5 Natetemeka kwa hofu kubwa, nimevamiwa na vitisho vikubwa.

6 Laiti ningekuwa na mabawa kama njiwa! Ningeruka mbali na kupata pumziko;

7 naam, ningesafiri mbali sana, na kupata makao jangwani.

8 Ningekimbilia mahali pa usalama, mbali na upepo mkali na dhoruba.

9 Ee Bwana, uwaangamize na kuvuruga lugha yao; maana naona ukatili na ugomvi mjini,

10 vikiuzunguka usiku na mchana, na kuujaza maafa na jinai.

11 Uharibifu umeenea pote mjini, uhasama na udhalimu kila mahali.

12 Kama adui yangu angenitukana, ningeweza kustahimili hayo; kama mpinzani wangu angenidharau, ningeweza kujificha mbali naye.

13 Kumbe, lakini, ni wewe mwenzangu; ni wewe rafiki yangu na msiri wangu!

14 Sisi tulizoea kuzungumza kirafiki; pamoja tulikwenda nyumbani kwa Mungu.

15 Acha kifo kiwafumanie maadui zangu; washuke chini Kuzimu wangali hai; maana uovu umewajaa moyoni mwao.

16 Lakini mimi namlilia Mungu, naye Mwenyezi-Mungu ataniokoa.

17 Jioni, asubuhi na adhuhuri, nalalama na kulia, naye ataisikia sauti yangu.

18 Atanikomboa salama katika vita ninayoikabili, kwa maana maadui zangu ni wengi.

19 Mungu atawalaye tangu milele, atanisikia na kuwaaibisha maadui zangu, maana hawapendi kujirekebisha, wala hawamwogopi Mungu.

20 Mwenzangu amewashambulia rafiki yake, amevunja mapatano yake.

21 Maneno yake ni laini kuliko siagi, lakini mawazo yake ni ya kufanya vita. Maneno yake ni mororo kama mafuta, lakini yanakata kama upanga mkali.

22 Mwachie Mwenyezi-Mungu mzigo wako, naye atakutegemeza; kamwe hamwachi mwadilifu ashindwe.

23 Wewe, ee Mungu, utawaporomosha shimoni chini kabisa, watu hao wauaji na wadanganyifu; hao hawatafikia nusu ya maisha yao. Lakini mimi nitakutumainia wewe ee Mungu!

56

1 Ee Mungu, unionee huruma, maana watu wananishambulia. Mchana kutwa maadui wananidhulumu.

2 Mchana kutwa maadui zangu wananishambulia; ni wengi mno hao wanaonipiga vita.

3 Ee Mungu Mkuu, hofu inaponishika, mimi nakutumainia wewe.

4 Namtumainia Mungu na kusifu neno lake; namtumainia Mungu, wala siogopi. Binadamu dhaifu atanifanya nini?

5 Mchana kutwa wanapotosha kisa changu; mawazo yao yote ni ya kunidhuru.

6 Wanakutana kupanga na kunivizia; wanachunguza yote nifanyayo; wananiotea kwa shabaha ya kuniua.

7 Ee Mungu, uwalipe kwa kadiri ya uovu wao, uwaangushe hao waovu kwa hasira yako.

8 Wewe wakujua kusukwasukwa kwangu; waweka kumbukumbu ya machozi yangu yote. Je, yote si yamo kitabuni mwako?

9 Kila mara ninapokuomba msaada wako, maadui zangu wanarudishwa nyuma. Najua kweli Mungu yuko upande wangu.

10 Namtumaini Mungu na kusifu neno lake; namtumainia Mwenyezi-Mungu na kusifu neno lake.

11 Namtumainia Mungu, wala siogopi. Binadamu atanifanya nini?

12 Ee Mungu, nitatimiza ahadi zangu kwako; nitakutolea tambiko za shukrani,

13 Maana umeniokoa katika kifo, naam, umenilinda nisianguke chini; nipate kuishi mbele yako, ee Mungu, katika mwanga wa uhai.

57

1 Unihurumie, ee Mungu, unihurumie, maana kwako nakimbilia usalama. Kivulini mwa mabawa yako nitakimbilia usalama, hata hapo dhoruba ya maangamizi itakapopita.

2 Namlilia Mungu Mkuu, Mungu anikamilishiaye nia yake.

3 Atanipelekea msaada toka mbinguni na kuniokoa; atawaaibisha hao wanaonishambulia. Mungu atanionesha fadhili zake na uaminifu wake!

4 Mimi nimezungukwa na maadui, wenye uchu wa damu kama simba; meno yao ni kama mikuki na mishale, ndimi zao ni kama panga kali.

5 Utukuzwe, ee Mungu, juu ya mbingu! Utukufu wako uenee duniani kote!

6 Maadui wamenitegea wavu waninase, nami nasononeka kwa huzuni. Wamenichimbia shimo njiani mwangu, lakini wao wenyewe wametumbukia humo.

7 Niko thabiti moyoni, ee Mungu, naam, niko thabiti moyoni; nitaimba na kukushangilia!

8 Amka, ee nafsi yangu! Amkeni, enyi kinubi na zeze! Nitayaamsha mapambazuko!

9 Ee Bwana, nitakushukuru kati ya mataifa; nitakuimbia sifa kati ya mataifa.

10 Fadhili zako zaenea hata juu ya mbingu, uaminifu wako wafika hata mawinguni.

11 Utukuzwe, ee Mungu, juu ya mbingu! Utukufu wako uenee duniani kote!

58

1 Enyi watawala, je, mwahukumu kwa haki kweli? Je, mnawahukumu watu kwa adili?

2 La! Nyinyi mwafikiria tu kutenda maovu; nyinyi wenyewe mwaeneza dhuluma nchini.

3 Waovu wamepotoka tangu kuzaliwa kwao, waongo hao, wamekosa tangu walipozaliwa.

4 Wana sumu kama sumu ya nyoka; viziwi kama joka lizibalo masikio,

5 ambalo halisikii hata sauti ya mlozi, au utenzi wa mganga stadi wa uchawi.

6 Ee Mungu, wavunje meno yao, yangoe, ee Mwenyezi-Mungu, meno ya simba hao.

7 Watoweke kama maji yanayodidimia mchangani, kama nyasi wakanyagwe na kunyauka,

8 watoweke kama konokono ayeyukavyo, kama mimba iliyoharibika isiyoona kamwe jua!

9 Kabla hawajatambua, wangolewe kama miiba, michongoma au magugu. Kwa hasira ya Mungu, wapeperushwe mbali, wakiwa bado hai.

10 Waadilifu watafurahi waonapo waovu wanaadhibiwa; watatembea katika damu ya watu wabaya.

11 Watu wote watasema: “Naam, waadilifu hupata tuzo! Hakika yuko Mungu anayeihukumu dunia!”

59

1 Ee Mungu wangu, uniokoe na maadui zangu; unikinge na hao wanaonishambulia.

2 Uniokoe na hao wanaotenda maovu; unisalimishe kutoka kwa hao wauaji!

3 Tazama! Wananivizia waniue; watu wakatili wanachochea ugomvi dhidi yangu.

4 Bila ya kosa, hatia au dhambi yangu, wanakimbia, ee Mwenyezi-Mungu, kujiweka tayari. Uinuke, ee Mwenyezi-Mungu, ukatazame na kunisaidia!

5 Uinuke, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu Mwenye Nguvu, Mungu wa Israeli. Uamke, uwaadhibu hao watu wasiokujua; usiwaache hao wanaopanga ubaya.

6 Kila jioni maadui hao hurudi wakibweka kama mbwa, na kuzungukazunguka mjini.

7 Tazama, ni matusi tu yatokayo mdomoni mwao, maneno yao yanakata kama upanga mkali; tena wanafikiri hakuna anayewasikia.

8 Lakini wewe, ee Mwenyezi-Mungu, wawacheka; unawapuuza hao watu wote wasiokujua.

9 Nitakungoja, ewe uliye nguvu yangu; maana wewe, ee Mungu, u ngome yangu.

10 Mungu wangu utanijia na fadhili zako, utaniwezesha kuwaona maadui zangu wameshindwa.

11 Usiwaue mara moja, watu wangu wasije wakasahau; ila uwayumbishe kwa nguvu yako, uwaporomoshe chini. Ee Bwana, wewe ndiwe ngao yetu!

12 Wao hutenda dhambi kwa yote wasemayo, kwa hiyo na wanaswe katika kiburi chao! Kwa sababu ya laana na uongo wao,

13 uwateketeze kwa hasira yako, uwateketeze wasiwepo tena; ili watu wote wajue kuwa wewe ee Mungu watawala wazawa wa Yakobo hata mpaka miisho ya dunia.

14 Kila jioni maadui hao hurudi wakibweka kama mbwa, na kuzungukazunguka mjini.

15 Hupitapita huko na huko wakitafuta mlo, na wasipotoshelezwa hunguruma.

16 Lakini mimi nitaimba sifa za nguvu yako; nitashangilia asubuhi juu ya fadhili zako; maana wewe umekuwa ngome yangu na kimbilio langu wakati wa taabu.

17 Ewe uliye nguvu yangu, nitakuimbia sifa; ee Mungu, wewe u ngome yangu; Mungu mwenye kunifadhili!

60

1 Ee Mungu, umetutupa na kutuponda, umewaka hasira, tafadhali uturudishie nguvu.

2 Umeitetemesha nchi na kuipasua; uzibe nyufa zake kwani inabomoka.

3 Umewatwika watu wako mateso; tunayumbayumba kama waliolewa divai.

4 Uwape ishara wale wanaokuheshimu, wapate kuuepa mshale.

5 Uwasalimishe hao watu uwapendao; utuokoe kwa mkono wako, na kutusikiliza.

6 Mungu amesema kutoka patakatifu pake “Sasa nitaigawa Shekemu kwa shangwe, Bonde la Sukothi nitalipima sehemusehemu.

7 Gileadi ni yangu, na Manase ni yangu; Efraimu ni kofia yangu ya chuma, na Yuda ni fimbo yangu ya enzi.

8 Moabu ni kama bakuli langu la kunawia, kiatu changu nitaitupia Edomu kuimiliki. Nitapiga kelele ya ushindi juu ya Filistia.”

9 Ni nani atakayenipeleka kwenye mji wa ngome? Ni nani atakayeniongoza mpaka Edomu?

10 Je, umetuacha kabisa, ee Mungu? Wewe huendi tena na majeshi yetu!

11 Utupatie msaada dhidi ya maadui zetu, maana msaada wa binadamu haufai kitu.

12 Mungu akiwa upande wetu tutashinda, yeye atawaponda maadui zetu.

61

1 Ee Mungu, usikie kilio changu, usikilize sala yangu.

2 Ninakulilia kutoka miisho ya dunia, nikiwa nimevunjika moyo. Uniongoze juu kwenye mwamba mkubwa

3 maana wewe ndiwe kimbilio langu, kinga yangu imara dhidi ya adui.

4 Naomba nikae nyumbani mwako milele nipate usalama chini ya mabawa yako.

5 Ee Mungu, umezisikia ahadi zangu, umenijalia sehemu yangu unayowapa wale wakuchao.

6 Umjalie mfalme maisha marefu, miaka yake iwe ya vizazi vingi.

7 Atawale milele mbele yako, ee Mungu; fadhili na uaminifu wako vimlinde.

8 Hivyo nitakuimbia nyimbo za sifa, nikizitekeleza ahadi zangu kila siku.

62

1 Namngojea Mungu peke yake kwa utulivu, kwake watoka wokovu wangu.

2 Yeye peke yake ndiye mwamba na wokovu wangu, yeye ni ngome yangu, sitatikisika.

3 Hata lini mtanishambulia mimi? Hata lini nyinyi nyote mtanipiga, mimi niliye kama kiambaza kilichoinama, kama ukuta unaoanza kubomoka?

4 Mmepanga kuniangusha toka mahali pangu pa heshima; furaha yenu ni kusema uongo. Kwa maneno, mnabariki, lakini moyoni mnalaani.

5 Namngojea Mungu peke yake kwa utulivu; kwake naliweka tumaini langu.

6 Yeye peke yake ndiye mwamba na wokovu wangu, yeye ni ngome yangu, sitatikisika.

7 Wokovu na fahari yangu vyatoka kwa Mungu; mwamba wangu mkuu na kimbilio langu ni Mungu.

8 Enyi watu, mtumainieni Mungu daima; mfungulieni Bwana yaliyo moyoni mwenu. Mungu ndiye kimbilio la usalama wetu.

9 Binadamu wote ni kama pumzi tu; wote, wakubwa kwa wadogo, hawafai kitu. Tena ukiwapima uzito hawafikii kilo, wote pamoja ni wepesi kuliko pumzi.

10 Msitegemee dhuluma, msijisifie mali ya wizi; kama mali zikiongezeka, msizitegemee.

11 Mungu ametamka mara moja, nami nimesikia tena na tena: Kwamba enzi ni mali yake Mungu;

12 naam, nazo fadhili ni zake Bwana; humlipa kila mtu kadiri ya matendo yake.

63

1 Ee Mungu, wewe u Mungu wangu, nami nakutafuta kwa moyo; roho yangu inakutamani kama mtu mwenye kiu; nina kiu kama nchi kavu isiyo na maji.

2 Nimetaka kukuona patakatifuni pako, niione nguvu yako na utukufu wako.

3 Fadhili zako ni bora kuliko maisha, nami nitakusifu kwa mdomo wangu.

4 Nitakushukuru maisha yangu yote; nitainua mikono yangu na kukuomba.

5 Roho yangu inafurahi kama kwa karamu na vinono; kwa shangwe nitaimba sifa zako.

6 Niwapo kitandani ninakukumbuka, usiku kucha ninakufikiria;

7 maana wewe umenisaidia daima. Kivulini mwa mabawa yako nitashangilia.

8 Roho yangu inaambatana nawe kabisa, mkono wako wa kulia wanitegemeza.

9 Lakini hao wanaotaka kuyaangamiza maisha yangu, watatumbukia chini kwenye makao ya wafu.

10 Watauawa kwa upanga, watakuwa chakula cha mbweha.

11 Lakini mfalme atafurahi kwa sababu ya Mungu; wanaoahidi kwa jina la Mungu watamsifu, lakini vinywa vya waongo vitafumbwa.

64

1 Usikie, ee Mungu, lalamiko langu; yalinde maisha yangu na vitisho vya maadui.

2 Unikinge na njama za waovu, na ghasia za watu wabaya.

3 Wananoa ndimi zao kama upanga, wanafyatua maneno ya ukatili kama mishale.

4 Toka mafichoni wamshambulia mtu mnyofu, wanamshambulia ghafla bila kuogopa.

5 Wanashirikiana katika nia yao mbaya; wanapatana mahali pa kuficha mitego yao. Wanafikiri: “Hakuna atakayeweza kuiona.”

6 Hufanya njama zao na kusema: “Sasa tumekamilisha mpango! Nani atagundua hila zetu?” Mipango ya siri imefichika moyoni mwa mtu!

7 Lakini Mungu atawapiga mishale, na kuwajeruhi ghafla.

8 Atawaangamiza kwa sababu ya maneno yao; kila atakayewaona atatikisa kichwa.

9 Hapo watu wote wataogopa; watatangaza aliyotenda Mungu, na kufikiri juu ya matendo yake.

10 Waadilifu watafurahi kwa sababu ya Mwenyezi-Mungu, na kukimbilia usalama kwake; watu wote wanyofu wataona fahari.

65

1 Wastahili sifa, ee Mungu, huko Siyoni, watu watakutimizia wewe ahadi zao,

2 maana wewe wajibu sala zetu. Binadamu wote watakujia wewe.

3 Tunapolemewa na makosa yetu, wewe mwenyewe watusamehe.

4 Heri wale unaowachagua na kuwaleta karibu, waishi katika maskani yako. Sisi tutatoshelezwa na mema ya nyumba yako; mema ya hekalu lako takatifu.

5 Kwa matendo yako makuu watuitikia na kutuokoa, ewe Mungu wa wokovu wetu; wewe ndiwe tumaini la viumbe vyote, duniani kote na mbali baharini.

6 Kwa nguvu yako uliisimika milima mahali pake. Wewe una nguvu mno!

7 Watuliza mshindo wa bahari na wa mawimbi yake, wakomesha ghasia za watu.

8 Ulimwengu wote washangazwa na matendo yako. Wasababisha furaha kila mahali, toka mashariki hata magharibi.

9 Wewe waitunza nchi kwa kuinyeshea mvua, waijalia rutuba na kuistawisha; mto wako umejaa maji tele, waifanikisha nchi na kuipatia mavuno. Hivi ndivyo uitengenezavyo nchi:

10 Mashamba wayanyeshea mvua kwa wingi, na kuyalowanisha kwa maji; ardhi wailainisha kwa manyunyu, na kuibariki mimea ichipue.

11 Wautunukia mwaka wote mema yako, kila ulipopitia pamejaa fanaka.

12 Mbuga za majani zimejaa mifugo, milima nayo imejaa furaha.

13 Malisho yamejaa kondoo, mabonde yamefunikwa kwa ngano. Kila kitu kinashangilia kwa furaha.

66

1 Enyi watu wote duniani mshangilieni Mungu!

2 Imbeni juu ya utukufu wa jina lake, mtoleeni sifa tukufu!

3 Mwambieni Mungu: “Matendo yako ni ya ajabu mno! Nguvu zako ni kubwa mno hata maadui zako wanajikunyata kwa hofu.

4 Dunia yote inakuabudu; watu wote wanakuimbia sifa!”

5 Njoni mkaone mambo aliyotenda Mungu; ametenda mambo ya kutisha kati ya watu:

6 Aligeuza bahari kuwa nchi kavu, watu wakapita humo kwa miguu; hapo nasi tukashangilia kwa sababu yake.

7 Anatawala milele kwa nguvu yake kuu; macho yake huchungulia mataifa yote. Mwasi yeyote asithubutu kumpinga.

8 Msifuni Mungu wetu, enyi mataifa yote; tangazeni sifa zake zipate kusikika.

9 Yeye ametujalia maisha, wala hakutuacha tuanguke.

10 Umetupima, ee Mungu, umetujaribu kama madini motoni.

11 Umetuacha tunaswe wavuni; umetubebesha taabu nzito.

12 Umewaacha watu watukanyage; tumepitia motoni na majini. Lakini sasa umetuleta kwenye usalama.

13 Nitakuja nyumbani kwako na sadaka za kuteketezwa, nitakutimizia nadhiri zangu,

14 nilizotamka na kukuahidi mimi mwenyewe nilipokuwa taabuni.

15 Nitakutolea sadaka za kuteketezwa nononono, tambiko za kuteketezwa za kondoo madume; nitatoa sadaka za ng'ombe na mbuzi.

16 Enyi mnaomcha Mungu, njoni nyote mkasikilize, nami nitawasimulieni aliyonitendea.

17 Mimi nilimlilia msaada kwa sauti, sifa zake nikazitamka.

18 Kama ningalinuia maovu moyoni, Mwenyezi-Mungu hangalinisikiliza.

19 Lakini kweli Mungu amenisikiliza; naam, amesikiliza maneno ya sala yangu.

20 Asifiwe Mungu, maana hakuikataa sala yangu, wala kuondoa fadhili zake kwangu.

67

1 Utuonee huruma, ee Mungu, utubariki; utuelekezee uso wako kwa wema;

2 dunia yote ipate kutambua njia yako, mataifa yote yajue nguvu yako ya kuokoa.

3 Watu wote wakutukuze, ee Mungu; watu wote na wakusifu!

4 Mataifa yote yafurahi na kuimba kwa furaha; maana wawahukumu watu kwa haki, na kuyaongoza mataifa duniani.

5 Watu wote wakutukuze, ee Mungu; watu wote na wakusifu!

6 Nchi imetoa mazao yake; Mungu, Mungu wetu, ametubariki.

7 Mungu aendelee kutubariki. Watu wote duniani na wamche.

68

1 Mungu ainuka, na maadui zake watawanyika; wanaomchukia wakimbia mbali naye!

2 Kama moshi unavyopeperushwa na upepo, ndivyo anavyowapeperusha; kama nta inavyoyeyuka karibu na moto, ndivyo waovu wanavyoangamia mbele ya Mungu!

3 Lakini waadilifu hufurahi ajapo Mungu, hushangilia na kuimba kwa furaha.

4 Mwimbieni Mungu, lisifuni jina lake; mtengenezeeni njia yake apandaye mawinguni. Jina lake ni Mwenyezi-Mungu; furahini mbele yake.

5 Mungu akaaye mahali pake patakatifu, ni Baba wa yatima na mlinzi wa wajane.

6 Mungu huwapa fukara makao ya kudumu, huwafungua wafungwa na kuwapa fanaka. Lakini waasi wataishi katika nchi kame.

7 Ee Mungu, ulipowaongoza watu wako, uliposafiri kule jangwani,

8 dunia ilitetemeka, mbingu zilitiririsha mvua; kwa kuweko kwako, Mungu wa Sinai, naam, kwa kuweko kwako, Mungu wa Israeli!

9 Ee Mungu, uliinyeshea nchi mvua nyingi, uliiburudisha nchi yako ilipokuwa imechakaa.

10 Watu wako wakapata humo makao; ukawaruzuku maskini kwa wema wako.

11 Bwana alitoa amri, nao wanawake wengi wakatangaza habari:

12 “Wafalme na majeshi yao wanakimbia ovyo!” Kina mama majumbani waligawana nyara,

13 ingawa walibaki mazizini: Sanamu za njiwa wa madini ya fedha, na mabawa yao yanangaa kwa dhahabu.

14 Mungu Mwenye Nguvu alipowatawanya wafalme huko, theluji ilianguka juu ya mlima Salmoni.

15 Ewe mlima mrefu, mlima wa Bashani, ewe mlima wa vilele vingi, mlima wa Bashani!

16 Mbona unauonea kijicho mlima aliochagua Mungu akae juu yake? Mwenyezi-Mungu atakaa huko milele!

17 Akiwa na msafara mkubwa, maelfu na maelfu ya magari ya kukokotwa, Bwana anakuja patakatifuni pake kutoka Sinai.

18 Anapanda juu akichukua mateka; anapokea zawadi kutoka kwa watu, hata kutoka kwa watu walioasi; Mwenyezi-Mungu apate kukaa huko.

19 Mwenyezi-Mungu asifiwe siku kwa siku! Yeye hutubebea mizigo yetu; yeye ndiye Mungu wa wokovu wetu.

20 Mungu wetu ni Mungu mwenye kutuokoa; Bwana Mungu pekee ndiye aokoaye katika kifo.

21 Mungu ataviponda vichwa vya maadui zake, naam, vichwa vya wanaoshikilia njia mbaya.

22 Bwana alisema: “Nitawarudisha maadui kutoka Bashani; nitawarudisha kutoka vilindi vya bahari,

23 uoshe miguu katika damu ya maadui zako, nao mbwa wako wale shibe yao.”

24 Ee Mungu, misafara yako ya ushindi yaonekana; misafara ya Mungu wangu, mfalme wangu, hadi patakatifu pake!

25 Mbele waimbaji, nyuma wanamuziki, katikati wasichana wanavumisha vigoma.

26 “Msifuni Mungu katika jumuiya kubwa ya watu. Msifuni Mwenyezi-Mungu, enyi wazawa wa Israeli!”

27 Kwanza ni Benyamini, mdogo wa wote; kisha viongozi wa Yuda na kundi lao, halafu wakuu wa Zebuluni na Naftali.

28 Onesha, ee Mungu, nguvu yako kuu; enzi yako uliyotumia kwa ajili yetu,

29 kutoka hekaluni mwako, Yerusalemu, ambapo wafalme watakujia na zawadi zao.

30 Uwakemee wale wanyama wakaao bwawani, kundi la mabeberu na fahali, mpaka mataifa hayo yakupe heshima na kodi. Uwatawanye hao watu wenye kupenda vita!

31 Mabalozi watakuja kutoka Misri, Waethiopia watamletea Mungu mali zao.

32 Enyi falme za dunia, mwimbieni Mungu, mwimbieni Bwana nyimbo za sifa;

33 mwimbieni yeye apitaye katika mbingu, mbingu za kale na kale. Msikilizeni akinguruma kwa kishindo.

34 Itambueni nguvu kuu ya Mungu; yeye atawala juu ya Israeli, enzi yake yafika katika mbingu.

35 Mungu ni wa kutisha patakatifuni pake, naam, yeye ni Mungu wa Israeli! Huwapa watu wake nguvu na enzi. Asifiwe Mungu!

69

1 Uniokoe, ee Mungu; maji yamenifika shingoni.

2 Ninazama ndani ya matope makuu, hamna hata mahali pa kuweka miguu. Nimetumbukia kwenye kilindi cha maji, nachukuliwa na mawimbi.

3 Niko hoi kwa kupiga yowe, na koo langu limekauka. Macho yangu yamefifia, nikikungojea ewe Mungu wangu.

4 Watu wengi kuliko nywele zangu ndio wanichukiao bure. Wana nguvu sana hao wanaotaka kuniua, hao wanaonishambulia kwa mambo ya uongo. Je, nirudishe kitu ambacho sikuiba?

5 Ee Mungu, waujua upumbavu wangu; makosa yangu hayakufichika kwako.

6 Wanaokutumainia wasiaibishwe kwa sababu yangu, ee Bwana Mwenyezi-Mungu wa majeshi; wanaokutafuta, wasione fedheha kwa sababu yangu ee Mungu wa Israeli.

7 Kwa ajili yako nimefedheheshwa, aibu imefunika uso wangu.

8 Nimekuwa mgeni kwa ndugu zangu, kaka na dada zangu hawanitambui.

9 Upendo wangu kwa nyumba yako unanimaliza. Kashfa zote wanazokutolea wewe zimenipata mimi.

10 Nilipojinyenyekesha kwa kufunga, watu walinilaumu.

11 Nilipovaa vazi la gunia kuomboleza, wao walinidharau.

12 Watu wananisengenya mabarabarani; walevi wanatunga nyimbo juu yangu.

13 Lakini mimi nakuomba wewe, ee Mwenyezi-Mungu; nikubalie ombi langu wakati unaopenda, ee Mungu. Kwa wingi wa fadhili zako unijibu. Wewe ni mkombozi wa kuaminika.

14 Kwa msaada wako amini uniokoe nisizame katika matope; uniokoe na hao wanaonichukia, unisalimishe kutoka vilindi vya maji.

15 Usiniache nikumbwe na mkondo wa maji, au nizame kwenye kilindi au nimezwe na kifo.

16 Unijibu, ee Mwenyezi-Mungu, kwa wema na fadhili zako; unielekee kwa wingi wa huruma yako.

17 Usimfiche mtumishi wako uso wako; unijibu haraka, maana niko hatarini.

18 Unijie karibu na kunikomboa, uniokoe na maadui zangu wengi.

19 Wewe wajua ninavyotukanwa, wajua aibu na kashfa ninazopata; na maadui zangu wote wewe wawajua.

20 Kashfa zimeuvunja moyo wangu, nami nimekata tamaa. Nimetafuta kitulizo lakini sikupata, wa kunifariji lakini sikumpata.

21 Walinipa sumu kuwa chakula, na nilipokuwa na kiu wakanipa siki.

22 Karamu zao na ziwe mtego kwao, na sikukuu zao za sadaka ziwanase.

23 Macho yao yatiwe giza wasiweze kuona, uitetemeshe daima migongo yao.

24 Uwamwagie hasira yako, ghadhabu yako iwakumbe.

25 Kambi zao ziachwe mahame, asiishi yeyote katika mahema yao.

26 Maana wanawatesa wale uliowaadhibu, wanawaongezea majeraha wale uliowajeruhi.

27 Uwaadhibu kwa kila uovu wao; uwakatalie kabisa msamaha wako.

28 Uwafute katika kitabu cha walio hai, wasiwemo katika orodha ya waadilifu.

29 Lakini mimi mnyonge na mgonjwa; uniinue juu, ee Mungu, uniokoe.

30 Kwa wimbo nitalisifu jina la Mungu, nitamtukuza kwa shukrani.

31 Jambo hili litampendeza Mwenyezi-Mungu zaidi, kuliko kumtolea tambiko ya ng'ombe, kuliko kumtolea fahali mzimamzima.

32 Wanyonge wataona hayo na kufurahi; wanaomheshimu Mungu watapata moyo.

33 Mwenyezi-Mungu huwasikiliza fukara; hatawasahau kamwe watu wake wafungwa.

34 Enyi mbingu na dunia msifuni Mungu; bahari na vyote vilivyomo, msifuni.

35 Maana Mungu atauokoa mji Siyoni, na kuijenga tena miji ya Yuda. Watu wake wataishi humo na kuimiliki;

36 wazawa wa watumishi wake watairithi, wale wanaopenda jina lake wataishi humo.

70

1 Upende kuniokoa ee Mungu! Ee Mwenyezi-Mungu, uje haraka kunisaidia.

2 Wanaonuia kuniangamiza, na waaibike na kufedheheka! Hao wanaotamani niumie, na warudi nyuma na kuaibika.

3 Hao wanaonisimanga, na wapumbazike kwa kushindwa kwao.

4 Lakini wote wale wanaokutafuta, wafurahi na kushangilia kwa sababu yako. Wapendao wokovu wako, waseme daima: “Mungu ni mkuu!”

5 Nami niliye maskini na fukara, unijie haraka, ee Mungu! Ndiwe msaada wangu na mkombozi wangu; ee Mwenyezi-Mungu, usikawie!

71

1 Kwako ee Mwenyezi-Mungu, nakimbilia usalama; kamwe usiniache niaibike!

2 Kwa uadilifu wako uniokoe na kunisalimisha; unitegee sikio lako na kuniokoa!

3 Uwe mwamba wangu wa kukimbilia usalama, ngome imara ya kuniokoa, kwani wewe ni mwamba na ngome yangu.

4 Niokoe, ee Mungu wangu, mikononi mwa waovu, kutoka makuchani mwa wabaya na wakatili.

5 Maana wewe Bwana u tumaini langu; tegemeo langu ee Mwenyezi-Mungu, tangu ujana wangu;

6 nimekutegemea tangu kuzaliwa kwangu, ndiwe uliyenitoa tumboni mwa mama yangu. Mimi nitakusifu wewe daima.

7 Kwa wengi nimekuwa kioja, lakini wewe u kimbilio langu imara.

8 Kinywa changu kimejaa sifa zako, na utukufu wako mchana kutwa.

9 Wakati wa uzee usinitupe; niishiwapo na nguvu usiniache.

10 Maana maadui zangu wanasema vibaya juu yangu; wanaovizia uhai wangu wanafanya mipango,

11 na kusema: “Mungu amemwacha; mfuateni na kumkamata, kwani hakuna wa kumwokoa!”

12 Usikae mbali nami, ee Mungu; uje haraka kunisaidia, ee Mungu wangu.

13 Wapinzani wangu wote waaibishwe na kuangamizwa; wenye kutaka kuniumiza wapate aibu na fedheha.

14 Lakini mimi nitakuwa na matumaini daima; tena nitakusifu zaidi na zaidi.

15 Kinywa changu kitatamka matendo yako ya haki, nitatangaza mchana kutwa matendo yako ya wokovu ijapokuwa hayo yanapita akili zangu.

16 Nitataja matendo yako makuu, ee Bwana Mwenyezi-Mungu; nitatangaza kuwa ndiwe mwadilifu peke yako.

17 Ee Mungu, wewe umenifunza tangu ujana wangu; tena na tena, natangaza matendo yako ya ajabu.

18 Usiniache, ee Mungu, niwapo mzee mwenye mvi, hata nivitangazie vizazi vijavyo nguvu yako.

19 Nguvu na uadilifu wako, ee Mungu, vyafika mpaka mbingu za juu. Wewe umefanya mambo makuu mno. Ee Mungu, ni nani aliye kama wewe?

20 Umenifanya nione taabu nyingi ngumu, lakini utanirudishia tena uhai, wewe utaniinua tena kutoka huko chini.

21 Utaniongezea heshima yangu, na kunifariji tena.

22 Nitakusifu pia kwa kinubi, kwa sababu ya uaminifu wako, ee Mungu wangu; nitakuimbia sifa kwa zeze, ewe Mtakatifu wa Israeli.

23 Nitapaza sauti kwa furaha, ninapokuimbia wewe sifa zako, na roho yangu itakusifu maana umeniokoa.

24 Nitatamka uadilifu wako mchana kutwa, maana waliotaka kuniumiza wameaibishwa na kufedheheshwa.

72

1 Ee Mungu, umjalie mfalme uamuzi wako, umpe mwanamfalme uadilifu wako;

2 atawale taifa lako kwa haki, na maskini wako kwa uadilifu.

3 Milima ilete fanaka kwa watu wako, vilima vijae uadilifu.

4 Mfalme awatetee wanyonge wa taifa, awasaidie watoto wa fukara, na kuwaangamiza watu wadhalimu.

5 Mfalme aishi muda mrefu kama jua, na kama mwezi, kwa vizazi vyote.

6 Awe kama manyunyu yaburudishayo mashamba, kama mvua iinyweshayo ardhi.

7 Uadilifu ustawi maisha yake yote, na amani kwa wingi mpaka mwezi ukome.

8 Atawale kutoka bahari hata bahari, kutoka mto Eufrate hata mipaka ya dunia.

9 Maadui zake wakaao nyikani wanyenyekee mbele yake, washindani wake walambe vumbi.

10 Wafalme wa Tarshishi na visiwa wamlipe kodi, wafalme wa Sheba na Seba wamletee zawadi.

11 Wafalme wote wa dunia wamheshimu, watu wa mataifa yote wamtumikie.

12 Anamkomboa fukara anayemwomba, na maskini asiye na wa kumsaidia.

13 Anawahurumia watu dhaifu na fukara, anayaokoa maisha yao wenye shida.

14 Anawatoa katika udhalimu na ukatili, maana maisha yao ni ya thamani kubwa kwake.

15 Mfalme na aishi maisha marefu; apokee zawadi ya dhahabu kutoka Sheba; watu wamwombee kwa Mungu daima, na kumtakia baraka mchana kutwa.

16 Nchi na izae nafaka kwa wingi, vilima vijae mavuno kama ya Lebanoni, na watu mijini wastawi kama nyasi.

17 Jina la mfalme litukuke daima; fahari yake idumu pindi liangazapo jua. Kwake mataifa yote yabarikiwe; watu wote wamwite mbarikiwa!

18 Atukuzwe Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, ambaye peke yake hufanya miujiza.

19 Jina lake tukufu na litukuzwe milele; utukufu wake ujae ulimwenguni kote! Amina, Amina!

20 Mwisho wa sala za Daudi, mwana wa Yese.

73

1 Hakika, Mungu ni mwema kwa watu wanyofu; ni mwema kwa walio safi moyoni.

2 Karibu sana ningejikwaa, kidogo tu ningeteleza;

3 maana niliwaonea wivu wenye kiburi, nilipoona wakosefu wakifanikiwa.

4 Maana hao hawapatwi na mateso; miili yao ina afya na wana nguvu.

5 Taabu za binadamu haziwapati hao; hawapati mateso kama watu wengine.

6 Kiburi kimekuwa mkufu wao shingoni, uhasama ni kama nguo yao.

7 Macho yao hufura kwa uovu; mioyo yao hububujika mipango mibaya.

8 Huwadhihaki wengine na kusema mabaya; hujivuna na kupanga kufanya uhasama.

9 Kwa vinywa vyao hutukana mbingu; kwa ndimi zao hujitapa duniani.

10 Hata watu wa Mungu wanawafuata, hawaoni kwao chochote kibaya na kusadiki kila wanachosema.

11 Wanasema: “Mungu hawezi kujua! Mungu Mkuu hataweza kugundua!”

12 Hivi ndivyo watu waovu walivyo; wana kila kitu na wanapata mali zaidi.

13 Je, nimetunza bure usafi moyoni, na kujilinda nisitende dhambi?

14 Mchana kutwa nimepata mapigo, kila asubuhi nimepata mateso.

15 Kama ningalisema hayo kama wao, ningalikuwa mhaini miongoni mwa watu wako.

16 Basi, nilijaribu kufikiria jambo hili, lakini lilikuwa gumu mno kwangu,

17 mpaka nilipoingia patakatifu pako. Ndipo nikatambua yatakayowapata waovu.

18 Kweli wewe wawaweka mahali penye utelezi; wawafanya waanguke na kuangamia.

19 Wanaangamizwa ghafla, na kufutiliwa mbali kwa vitisho.

20 Ee Bwana, uinukapo, wao hutoweka mara, kama ndoto wakati mtu anapoamka asubuhi.

21 Nilipoona uchungu moyoni na kuchomwa rohoni,

22 nilikuwa mpumbavu na mjinga, nilikuwa kama mnyama mbele yako.

23 Hata hivyo niko daima nawe, ee Mungu! Wanishika mkono na kunitegemeza.

24 Wewe waniongoza kwa mashauri yako; mwishowe utanipokea kwenye utukufu.

25 Mbinguni, nani awezaye kunisaidia ila wewe? Na duniani hamna ninachotamani ila wewe!

26 Hata nikikosa nguvu mwilini na rohoni, wewe, ee Mungu, u mwamba wangu; riziki yangu kuu ni wewe milele.

27 Anayejitenga nawe, hakika ataangamia. Anayekukana, utamwangamiza.

28 Lakini, kwangu ni vema kuwa karibu na Mungu, wewe Bwana Mwenyezi-Mungu ndiwe usalama wangu. Nitatangaza mambo yote uliyotenda!

74

1 Kwa nini, ee Mungu, umetutupa kabisa? Mbona hasira yako inawaka dhidi ya kondoo wako!

2 Kumbuka jumuiya yako uliyojipatia tangu kale, kabila ulilolikomboa liwe mali yako, kumbuka mlima Siyoni mahali unapokaa.

3 Pita juu ya magofu haya ya kudumu! Adui wameharibu kila kitu hekaluni.

4 Maadui zako wamenguruma ushindi hekaluni mwako! Wameweka humo bendera zao za ushindi!

5 Wanafanana na mtema kuni, anayekata miti kwa shoka lake.

6 Waliivunjavunja milango ya hekalu, kwa mashoka na nyundo zao.

7 Walichoma moto patakatifu pako; walikufuru mahali pale unapoheshimiwa.

8 Walipania kutuangamiza sote pamoja; walichoma kila mahali tulipokutania kukuabudu nchini.

9 Hatuzioni tena ishara zetu takatifu, hatuna tena nabii yeyote! Hata hatujui yatakuwa hivi hadi lini!

10 Mpaka lini, ee Mungu, adui atakucheka? Je, watalikufuru jina lako milele?

11 Mbona umeuficha mkono wako? Kwa nini hunyoshi mkono wako?

12 Hata hivyo wewe Mungu ni mfalme wetu tangu kale; umefanya makuu ya wokovu katika nchi.

13 Kwa enzi yako kuu uliigawa bahari; uliviponda vichwa vya majoka ya bahari.

14 Wewe uliviponda vichwa vya dude Lewiyathani; ukawapa wanyama wa jangwani mzoga wake.

15 Wewe umefanya chemchemi na vijito; na kuikausha mito mikubwa.

16 Mchana ni wako na usiku ni wako; umeweka mwezi na jua mahali pao.

17 Wewe umeweka mipaka yote ya dunia; umepanga majira ya kiangazi na ya baridi.

18 Kumbuka, ee Mwenyezi-Mungu, madharau ya maadui zako; taifa pumbavu linalikashifu jina lako. Sisi ni dhaifu kama njiwa.

19 Usiwatupie wanyama wakali uhai wa wapenzi wako; usiyasahau maisha ya maskini wako.

20 Ulikumbuke agano ulilofanya nasi! Nchi imejaa uharamia kila mahali pa giza.

21 Usiwaache wanaokandamizwa waaibishwe, uwajalie maskini na wahitaji walisifu jina lako.

22 Inuka, ee Mungu, ukajitetee; ukumbuke wanavyokudharau kila siku watu wasiokujua.

23 Usisahau makelele za maadui zako; na ghasia za daima za wapinzani wako.

75

1 Tunakushukuru, ee Mungu, tunakushukuru! Tunatangaza ukuu wa jina lako na kusimulia juu ya matendo yako makuu.

2 Mungu asema: “Mimi nimeweka wakati maalumu! Wakati huo nitahukumu kwa haki.

3 Nchi ikitetemeka na vyote vilivyomo, mimi ndiye ninayeitegemeza misingi yake.

4 Nawaambia wenye kiburi: ‘Acheni kujigamba’; na waovu: ‘Msioteshe pembe za kiburi!

5 Msijione kuwa watu wa maana sana, wala kusema maneno ya majivuno.’”

6 Hukumu haitoki mashariki au magharibi; wala haitoki nyikani au mlimani.

7 Mungu mwenyewe ndiye hakimu; humshusha mmoja na kumkweza mwingine.

8 Mwenyezi-Mungu, anashika kikombe mkononi, kimejaa divai kali ya hasira yake; anaimimina na waovu wote wanainywa; naam, wanainywa mpaka tone la mwisho.

9 Lakini mimi nitafurahi milele, nitamwimbia sifa Mungu wa Yakobo.

10 Atavunja nguvu zote za watu waovu; lakini nguvu za waadilifu ataziimarisha.

76

1 Mungu anajulikana katika Yuda; jina lake ni kuu katika Israeli.

2 Makao yake yamo huko Salemu; maskani yake huko Siyoni.

3 Huko alivunja mishale ya adui; alivunja ngao, panga na silaha za vita.

4 Wewe, ee Mungu, watukuka mno; umejaa fahari kuliko milima ya milele.

5 Wenye nguvu walipokonywa nyara zao, sasa wamelala usingizi wa kifo, mashujaa wa vita hawakuweza kutumia mikono yao.

6 Ulipowakemea, ee Mungu wa Yakobo, farasi na wapandafarasi walikufa ganzi.

7 Wewe, ee Mungu, ni wa kutisha mno! Nani awezaye kustahimili mbele yako ukikasirika?

8 Ulijulisha hukumu yako toka mbinguni; dunia iliogopa na kunyamaza;

9 wakati ulipoinuka kutekeleza hukumu, kuwaokoa wote wanaodhulumiwa duniani.

10 Ghadhabu ya watu husababisha tu sifa kwako; na waliookoka vitani watafanya sikukuu zako.

11 Mtimizieni Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu ahadi zenu; enyi mlio karibu mpeni zawadi Mungu wa kutisha.

12 Yeye huzitoa roho za wakuu; huwatisha wafalme wa dunia.

77

1 Namlilia Mungu kwa sauti, kwa sauti namlilia Mungu anisikie.

2 Wakati wa taabu namwomba Bwana; namnyoshea mikono yangu usiku bila kuchoka, lakini sipati faraja yoyote kwa mtu.

3 Ninamfikiria Mungu na kusononeka; ninatafakari na kufa moyo.

4 Wanizuia hata kupata lepe la usingizi, nina mahangaiko hata kusema siwezi.

5 Nafikiria siku za zamani; nakumbuka miaka ya hapo kale.

6 Usiku nawaza na kuwazua moyoni; natafakari na kujiuliza rohoni:

7 “Je, Bwana ametuacha kabisa? Je, hatatuonesha tena hisani yake?

8 Je fadhili zake zimekoma kabisa? Je, hatatimiza tena ahadi zake?

9 Je, Mungu amesahau kuwa na huruma? Je, hasira yake imeuondoa upole wake?”

10 Kisha nikasema, “Kinachonichoma zaidi ni kwamba, Mungu Mkuu hatendi tena kitu kwa ajili yetu!”

11 Nitayakumbuka matendo yako, ee Mwenyezi-Mungu, naam, nitayafikiria maajabu yako ya hapo kale.

12 Nitatafakari juu ya kazi zako, na kuwaza juu ya matendo yako makuu.

13 Kila ufanyacho ee Mungu, ni kitakatifu. Ni mungu gani aliye mkuu kama Mungu wetu?

14 Wewe ni Mungu unayetenda maajabu; wewe umeyaonesha mataifa uwezo wako.

15 Kwa mkono wako wa nguvu uliwakomboa watu wako; uliwakomboa wazawa wa Yakobo na Yosefu.

16 Maji yalipokuona, ee Mungu, maji yalipokuona, yaliogopa mno; naam, bahari ilitetemeka hata vilindini.

17 Mawingu yalichuruzika maji, ngurumo zikavuma angani, mishale ya umeme ikaangaza kila upande.

18 Kishindo cha ngurumo yako kilitokea katika kimbunga, umeme wako ukauangaza ulimwengu; dunia ikatikisika na kutetemeka.

19 Wewe uliweka njia yako juu ya bahari; ulitembea juu ya maji yale mengi, lakini nyayo zako hazikuonekana.

20 Uliwaongoza watu wako kama kondoo, chini ya uongozi wa Mose na Aroni.

78

1 Sikieni mafundisho yangu, enyi watu wangu; yategeeni sikio maneno ya kinywa changu.

2 Nitasema nanyi kwa mafumbo, nitasema mambo yaliyofichika tangu kale;

3 mambo tuliyoyasikia na kuyajua, mambo ambayo wazee wetu walitusimulia.

4 Hatutawaficha watoto wetu; ila tutakisimulia kizazi kijacho matendo matukufu ya Mwenyezi-Mungu na uwezo wake; tutawaambia maajabu yake aliyotenda.

5 Aliwapa wazawa wa Yakobo masharti, aliweka sheria katika Israeli, ambayo aliwaamuru wazee wetu wawafundishe watoto wao;

6 ili watu wa kizazi kijacho, watoto watakaozaliwa baadaye, wazijue, nao pia wawajulishe watoto wao,

7 ili wamwekee Mungu tumaini lao, wasije wakasahau matendo ya Mungu, bali wazingatie amri zake.

8 Wasiwe kama walivyokuwa wazee wao, watu wakaidi na waasi; kizazi ambacho hakikuwa na msimamo thabiti, ambacho hakikuwa na uaminifu kwa Mungu.

9 Watu wa Efraimu, pinde na mishale mkononi, walirudi nyuma, wakakimbia siku ile ya vita.

10 Hawakulizingatia agano la Mungu; walikataa kufuata sheria yake.

11 Walisahau mambo aliyokuwa ametenda, miujiza aliyokuwa amewaonesha.

12 Alifanya maajabu mbele ya wazee wao, kondeni Soani, nchini Misri.

13 Aliigawa bahari, akawapitisha humo; aliyafanya maji yasimame kama ukuta.

14 Mchana aliwaongoza kwa wingu; usiku kucha kwa mwanga wa moto.

15 Aliipasua miamba kule jangwani, akawanywesha maji kutoka vilindini.

16 Alibubujisha vijito kutoka mwambani, akatiririsha maji kama mito.

17 Hata hivyo waliendelea kumkosea Mungu; walimwasi Mungu Mkuu kule jangwani.

18 Walimjaribu Mungu kwa makusudi; wakidai wapewe chakula walichotaka.

19 Walimkufuru Mungu wakisema: “Je, Mungu aweza kutupa chakula jangwani?

20 Ni kweli, aliupiga mwamba, maji yakabubujika kama mto; lakini, sasa aweza kweli kutupatia mkate, na kuwapatia watu wake nyama?”

21 Mwenyezi-Mungu, aliposikia hayo, alijawa na ghadhabu, moto ukawawakia wazawa wa Yakobo; hasira yake ikawavamia watu wa Israeli,

22 kwa sababu hawakuwa na imani naye, wala hawakuamini nguvu yake ya kuokoa.

23 Hata hivyo aliyaamuru mawingu ya juu, akaifungua milango ya mbingu;

24 akawanyeshea mana wale, akawapa nafaka kutoka mbinguni.

25 Binadamu, wakala chakula cha malaika; naye aliwapelekea chakula cha kutosha.

26 Alivumisha upepo wa mashariki, kwa nguvu yake akachochea pepo za kusini;

27 akawanyeshea watu wake nyama kama vumbi, ndege wengi kama mchanga wa pwani;

28 ndege hao walianguka kambini mwao, kila mahali kuzunguka makao yao.

29 Watu walikula wakashiba; Mungu aliwapa walichotaka.

30 Lakini hata kabla ya kutosheleza hamu yao, chakula kikiwa bado mdomoni mwao,

31 hasira ya Mungu iliwaka juu yao; akawaua wenye nguvu miongoni mwao, na kuwaangusha vijana wa Israeli.

32 Hata hivyo waliendelea kumkosea Mungu; ijapokuwa alitenda maajabu, hawakuamini.

33 Basi, akazikatisha siku zao kama pumzi, miaka yao kwa maafa ya ghafla.

34 Kila alipowaua, waliobaki walimgeukia; walitubu, wakamgeukia Mungu kwa moyo.

35 Walikumbuka kwamba Mungu alikuwa mwamba wao; Mungu Mkuu alikuwa mkombozi wao.

36 Lakini walimdanganya kwa maneno yao; kila walichomwambia kilikuwa uongo.

37 Hawakuambatana naye kwa moyo, hawakuwa waaminifu kwa agano lake.

38 Lakini Mungu mwenye huruma alisamehe uovu wao, na wala hakuwaangamiza. Mara nyingi aliizuia hasira yake, wala hakuiacha ghadhabu yake yote iwake.

39 Alikumbuka kwamba wao ni watu tu; ni kama upepo upitao na kutoweka.

40 Mara ngapi walimwasi kule jangwani, na kumchukiza hukohuko nyikani!

41 Walimjaribu Mungu tena na tena, wakamkasirisha huyo Mtakatifu wa Israeli.

42 Hawakuikumbuka nguvu yake, wala siku ile alipowaokoa na maadui zao,

43 alipotenda maajabu nchini Misri, na miujiza kondeni Soani!

44 Aliigeuza ile mito kuwa damu, Wamisri wasipate maji ya kunywa.

45 Aliwapelekea makundi ya nzi waliowasumbua, na vyura waliowatia hasara.

46 Alituma nzige, wakala mavuno yao, na kuharibu mashamba yao.

47 Aliiharibu mizabibu yao kwa mvua ya mawe, na mitini yao kwa baridi kali.

48 Ngombe wao aliwaua kwa mvua ya mawe, na kondoo wao kwa radi.

49 Aliacha hasira yake kali iwawakie, ghadhabu, chuki na dhiki, na kundi la malaika waangamizi.

50 Aliachilia hasira yake iendelee, wala hakuwaepusha na kifo, bali aliwaangamiza kwa tauni.

51 Aliwaua wazaliwa wa kwanza wote wa Wamisri; naam, chipukizi wa kwanza kambini mwa Hamu.

52 Kisha aliwahamisha watu wake kama kondoo, akawaongoza jangwani kama kundi la mifugo.

53 Aliwaogoza salama, wala hawakuogopa; lakini bahari iliwafunika maadui zao.

54 Aliwaleta katika nchi yake takatifu, katika mlima aliouteka kwa nguvu yake.

55 Aliyafukuza mataifa mbele yao, akazitoa nchi zao ziwe mali ya Israeli, akayakalisha makabila ya Israeli mahemani mwao.

56 Hata hivyo walimjaribu na kumwasi Mungu Mkuu; wala hawakuzingatia masharti yake.

57 Ila waligeuka na kufanya mabaya kama wazee wao; wakayumbayumba kama upinde usio imara.

58 Walimkasirisha kwa madhabahu zao za miungu; wakamchochea aone wivu kwa sanamu zao za kuchonga.

59 Mungu alipoona hayo, akawaka hasira; akamkataa Israeli katakata.

60 Aliyaacha makao yake kule Shilo, makao ambamo alikaa kati ya watu.

61 Aliiacha ishara ya nguvu yake itekwe, utukufu wake utiwe mikononi mwa maadui.

62 Aliwakasirikia watu wake mwenyewe; akawatoa waangamizwe kwa upanga.

63 Moto ukawateketeza vijana wao wa kiume, na wasichana wao wakakosa wachumba.

64 Makuhani wao walikufa kwa upanga, wala wajane wao hawakuomboleza.

65 Kisha Bwana aliamka kama kutoka usingizini, kama shujaa aliyechangamshwa na divai.

66 Akawatimua maadui zake; akawatia aibu ya kudumu milele.

67 Lakini aliikataa jamaa ya Yosefu, wala hakulichagua kabila la Efraimu.

68 Ila alilichagua kabila la Yuda, mlima Siyoni anaoupenda.

69 Alijenga hapo hekalu lake kubwa kama mbingu, kama dunia aliyoiweka imara milele.

70 Alimchagua Daudi, mtumishi wake, akamtoa katika kazi ya kuchunga kondoo.

71 Alimtoa katika kazi ya kuchunga kondoo na wanakondoo, awe na jukumu la kuchunga watu wa Yakobo taifa lake. Achunge Israeli, watu wake Mungu mwenyewe.

72 Daudi akawafunza kwa moyo wake wote, akawaongoza kwa uhodari mkubwa.

79

1 Ee Mungu, watu wasiokujua wameivamia nchi yako. Wamelitia najisi hekalu lako takatifu, na kuufanya mji wa Yerusalemu kuwa magofu.

2 Wameacha maiti za watumishi wako ziliwe na ndege, miili ya watu wako chakula cha wanyama wa porini.

3 Damu yao imemwagwa kama maji mjini Yerusalemu, wamelazwa humo na hakuna wa kuwazika.

4 Tumekuwa aibu kwa mataifa ya jirani, jirani zetu wanatucheka na kutudhihaki.

5 Ee Mwenyezi-Mungu, je, utakasirika hata milele? Hasira yako ya wivu itawaka kama moto hata lini?

6 Uwamwagie watu wasiokujua hasira yako; naam, tawala zote zisizoheshimu jina lako.

7 Maana wamemmeza Yakobo, taifa lako, wameteketeza kabisa makao yake.

8 Usituadhibu kwa sababu ya makosa ya wazee wetu. Huruma yako itujie haraka, maana tumekandamizwa mno!

9 Utusaidie, ee Mungu, mwokozi wetu; kwa heshima ya jina lako utuokoe na kutusamehe dhambi zetu, kwa ajili ya jina lako.

10 Kwa nini mataifa yatuambie: “Yuko wapi Mungu wenu?” Utujalie tuone ukiwalipiza watu wa mataifa mauaji ya watumishi wako.

11 Kilio cha hao wafungwa kikufikie; kwa nguvu yako kuu uwaokoe waliohukumiwa kufa.

12 Mataifa hayo yaliyokudharau, ee Bwana, yalipizwe mara saba!

13 Nasi watu wako, tulio kondoo wa kundi lako, tutakushukuru milele, na kukusifu nyakati zote.

80

1 Utege sikio, ewe Mchungaji wa Israeli, uwaongozaye wazawa wa Yosefu kama kondoo. Ewe ukaaye juu ya viumbe vyenye mabawa, uangaze,

2 mbele ya Efraimu, Benyamini na Manase. Uoneshe nguvu yako, uje kutuokoa!

3 Uturekebishe, ee Mungu; utuangalie kwa wema, nasi tutaokoka.

4 Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wa majeshi, hata lini utazikasirikia sala za watu wako?

5 Umefanya huzuni iwe chakula chetu; umetunywesha machozi kwa wingi.

6 Umetufanya tuwe dharau kwa jirani zetu; maadui zetu wanatudhihaki.

7 Ee Mungu wa majeshi, uturekebishe, utuangalie kwa wema, nasi tutaokoka.

8 Ulileta mzabibu kutoka Misri; ukawafukuza watu wa mataifa mengine, na kuupanda katika nchi yao.

9 Uliupalilia upate kukua, nao ukatoa mizizi na kuenea kote nchini.

10 Uliifunika milima kwa kivuli chake, na matawi yake yakawa kama mierezi mikubwa.

11 Matawi yake yalienea mpaka baharini; machipukizi yake mpaka kando ya mto Eufrate.

12 Mbona ulibomoa kuta zilizouzunguka? Sasa kila apitaye anachuma zabibu zake;

13 nguruwe mwitu wanauharibu, na wanyama wa porini wanautafuna!

14 Utugeukie tena ee Mungu wa majeshi. Uangalie toka mbinguni, uone; ukautunze mzabibu huo.

15 Uulinde mche ulioupanda kwa mkono wako; hilo chipukizi uliloimarisha wewe mwenyewe.

16 Watu walioukata na kuuteketeza, uwatazame kwa ukali, waangamie.

17 Mkono wako umkinge huyo uliyemfadhili; huyo uliyemteua kwa ajili yako.

18 Hatutakuacha na kukuasi tena; utujalie uhai, nasi tutakusifu.

19 Ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi uturekebishe; utuangalie kwa wema, nasi tutaokoka.

81

1 Mwimbieni kwa sauti Mungu, nguvu yetu, mshangilieni Mungu wa Yakobo;

2 vumisheni wimbo wa shangwe, pigeni ngoma, chezeni zeze na kinubi cha sauti nzuri.

3 Pigeni tarumbeta kutangaza mwezi mwandamo, na pia mwezi mpevu, wakati wa sikukuu yetu.

4 Hiyo ndiyo kanuni katika Israeli; hilo ndilo agizo la Mungu wa Yakobo.

5 Aliwapa watu wa Israeli agizo hilo, alipoishambulia nchi ya Misri. Nasikia sauti nisiyoitambua ikisema:

6 “Mimi nilikutua mizigo yako mabegani, nilikuondolea matofali uliyochukua mikononi.

7 Ukiwa shidani uliniita, nami nikakuokoa. Nilikujibu nikiwa mafichoni katika ngurumo. Nilikujaribu kwenye maji ya Meriba.

8 Enyi watu wangu, sikieni onyo langu. Laiti ungenisikiliza, ee Israeli!

9 Asiwepo kwako mungu wa kigeni; usiabudu kamwe mungu mwingine.

10 Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, niliyekutoa katika nchi ya Misri. Fumbua kinywa chako, nami nitakulisha.

11 “Lakini watu wangu hawakunisikiliza; Israeli hakunitaka kabisa.

12 Hivyo, nikawaacha wabaki na ukaidi wao; wafuate mashauri yao wenyewe.

13 Laiti watu wangu wangenisikiliza! Laiti Israeli angefuata njia yangu!

14 Ningewashinda maadui zao haraka; ningenyosha mkono dhidi ya wadhalimu wao.

15 Wanichukiao wangenipigia magoti kwa hofu, na adhabu yao ingekuwa ya milele.

16 Lakini wewe ningekulisha kwa ngano bora, ningekushibisha kwa asali ya mwambani.”

82

1 Mungu anasimamia baraza lake; anatoa hukumu katika kusanyiko la miungu:

2 “Mpaka lini mtaendelea kuhukumu bila haki na kuwapendelea watu waovu?

3 Wapeni wanyonge na yatima haki zao; tekelezeni haki za wanaoonewa na fukara.

4 Waokoeni wanyonge na maskini, waokoeni makuchani mwa wadhalimu.

5 “Lakini nyinyi hamjui wala hamfahamu! Nyinyi mnatembea katika giza la upotovu! Misingi yote ya haki duniani imetikiswa!

6 Mimi nilisema kuwa nyinyi ni miungu; kwamba nyote ni watoto wa Mungu Mkuu!

7 Hata hivyo, mtakufa kama watu wote; mtaanguka kama mkuu yeyote.”

8 Inuka ee Mungu, uuhukumu ulimwengu; maana mataifa yote ni mali yako.

83

1 Ee Mungu, usikae kimya! Usinyamaze ee Mungu, wala usitulie!

2 Tazama! Maadui zako wanafanya ghasia; wanaokuchukia wanainua vichwa kwa kiburi.

3 Wanapanga kwa hila kuwadhuru watu wako; wanashauriana dhidi ya hao unaowalinda.

4 Wanasema: “Njoni tuliangamize taifa lao, jina la Israeli lisikumbukwe tena.”

5 Naam, wanakubaliana kwa moyo mmoja, wanakula kiapo dhidi yako:

6 Watu wa Edomu na Waishmaeli, Wamoabu na watu wa Hagari;

7 watu wa Gebali, Amoni na Amaleki, watu wa Filistia na wakazi wa Tiro.

8 Hata Ashuru imeshirikiana nao, imewaunga mkono wazawa wa Loti!

9 Uwatende ulivyowatenda watu wa Midiani, ulivyowatenda Sisera na Yabini mtoni Kishoni,

10 watu uliowaangamiza kule Endori, wakawa takataka juu ya nchi.

11 Uwatende wakuu wao kama Orebu na Zeebu; watawala wao wote kama Zeba na Zalmuna,

12 ambao walisema: “Tutajitekea nchi ya Mungu.”

13 Ee Mungu wangu, uwafanye kama vumbi; kama makapi yapeperushwayo na upepo.

14 Kama vile moto unavyoteketeza msitu, na miali ya moto inavyounguza milima,

15 uwakimbize hao kwa tufani yako, na kuwatisha kwa kimbunga chako!

16 Uzijaze nyuso zao fedheha, wapate kukutafuta, ee Mwenyezi-Mungu.

17 Waone fedheha na kuhangaika milele, waangamie kwa aibu kabisa.

18 Wajue kwamba wewe peke yako ambaye jina lako ni Mwenyezi-Mungu, ndiwe Mungu Mkuu juu ya dunia yote.

84

1 Jinsi gani yanavyopendeza makao yako, ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi!

2 Nafsi yangu yatamani mno maskani ya Mwenyezi-Mungu! Moyo na mwili wangu wote wamshangilia Mungu aliye hai.

3 Hata shomoro wamepata makao yao, mbayuwayu wamejenga viota vyao, humo wameweka makinda yao, katika madhabahu zako, ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mfalme wangu na Mungu wangu!

4 Heri wale wanaokaa nyumbani mwako, wakiimba daima sifa zako.

5 Heri watu wanaopata nguvu zao kwako, wanaotamani kwenda kuhiji mlimani kwako.

6 Wapitapo katika bonde kavu la Baka, hulifanya kuwa mahali pa chemchemi, na mvua za vuli hulijaza madimbwi.

7 Wanaendelea kupata nguvu zaidi na zaidi; watamwona Mungu wa miungu huko Siyoni.

8 Usikie sala yangu ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi; unitegee sikio, ee Mungu wa Yakobo.

9 Ee Mungu, umwangalie kwa wema ngao yetu mfalme, umtazame huyo uliyemweka wakfu kwa mafuta.

10 Siku moja tu katika maskani yako, ni bora kuliko siku elfu mahali pengine; afadhali kusimama mlangoni pa nyumba yako, kuliko kuishi nyumbani kwa watu waovu.

11 Mwenyezi-Mungu ni jua letu na ngao yetu; yeye hutuneemesha na kutujalia fahari. Hawanyimi chochote kilicho chema, wale waishio kwa unyofu.

12 Ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi, heri mtu yule anayekutumainia wewe!

85

1 Ee Mwenyezi-Mungu, umeifadhili nchi yako; umemjalia Yakobo bahati nzuri tena.

2 Umewasamehe watu wako kosa lao; umezifuta dhambi zao zote.

3 Umeizuia ghadhabu yako yote; umeiacha hasira yako kali.

4 Uturekebishe tena, ee Mungu mwokozi wetu; uiondoe chuki uliyo nayo juu yetu.

5 Je, utatukasirikia hata milele? Je, utadumisha ghadhabu yako kwa vizazi vyote?

6 Je, hutatujalia tena maisha mapya, ili watu wako wafurahi kwa sababu yako?

7 Utuoneshe, fadhili zako, ee Mwenyezi-Mungu, utujalie wokovu wako.

8 Hebu nisikie anachosema Mwenyezi-Mungu; maana anaahidi kuwapa watu wake amani, watu wake mwenyewe wasiporudia upuuzi wao

9 Hakika yu tayari kuwaokoa wanaomheshimu, na utukufu wake utadumu nchini mwetu.

10 Fadhili zake na uaminifu vitakutana; uadilifu na amani vitaungana.

11 Uaminifu utachipuka katika nchi; uadilifu utashuka toka mbinguni.

12 Naam, Mwenyezi-Mungu atatuletea fanaka, na nchi yetu itatoa mazao yake mengi.

13 Uadilifu utamtangulia Mungu na kumtayarishia njia yake.

86

1 Unitegee sikio, ee Mwenyezi-Mungu, unijibu, maana mimi ni fukara na mnyonge.

2 Uyahifadhi maisha yangu maana mimi ni mchaji wako; uniokoe mimi mtumishi wako ninayekutegemea.

3 Wewe ni Mungu wangu; basi, unionee huruma, maana nakulilia mchana kutwa.

4 Uifurahishe roho yangu mimi mtumishi wako, maana sala zangu nazielekeza kwako ee Bwana.

5 Wewe, ee Bwana, u mwema na mwenye kusamehe; mwingi wa fadhili kwa wote wakuombao.

6 Ee Mwenyezi-Mungu, uitegee sikio sala yangu; ukisikie kilio cha ombi langu.

7 Siku za taabu nakuita, maana wewe waniitikia.

8 Ee Bwana, hakuna Mungu aliye kama wewe; hakuna awezaye kufanya unayofanya wewe.

9 Mataifa yote uliyoyaumba, yatakuja kukuabudu, ee Bwana; yatatangaza ukuu wa jina lako.

10 Wewe ndiwe mkuu, wafanya maajabu; wewe peke yako ndiwe Mungu.

11 Unifundishe njia yako, ee Mwenyezi-Mungu, nipate kuwa mwaminifu kwako; uongoze moyo wangu nikuheshimu.

12 Ee Bwana, Mungu wangu, nitakusifu kwa moyo wote; nitatangaza ukuu wa jina lako milele.

13 Fadhili zako kwangu ni nyingi mno! Umeniokoa kutoka chini kuzimu.

14 Ee Mungu, watu wenye kiburi wamenikabili; kundi la watu wakatili wanataka kuniua, wala hawakujali wewe hata kidogo.

15 Lakini wewe Bwana, ni Mungu wa rehema na huruma; wewe ni mvumilivu, mwingi wa fadhili na uaminifu.

16 Unigeukie, unihurumie; unijalie nguvu yako mimi mtumishi wako, umwokoe mtoto wa mjakazi wako.

17 Unioneshe ishara ya wema wako, ee Mwenyezi-Mungu, ili wale wanaonichukia waaibike, waonapo umenisaidia na kunifariji.

87

1 Mungu amejenga mji wake juu ya mlima wake mtakatifu.

2 Mwenyezi-Mungu anaupenda mji wa Siyoni, kuliko makao mengine ya Yakobo.

3 Mambo ya fahari yanasemwa juu yako, ee mji wa Mungu:

4 “Miongoni mwa wale wanijuao mimi, wapo watu wa Misri na Babuloni. Kadhalika Filistia, Tiro na Kushi, wote walizaliwa kwako!”

5 Na kuhusu Siyoni itasemwa: “Siyoni ni mama wa huyu na huyu; Mungu Mkuu atauthibitisha.”

6 Mwenyezi-Mungu ataandika katika kitabu, atakapoorodhesha watu: “Huyu amezaliwa huko!”

7 Wote wanacheza ngoma na kuimba: “Siyoni, chanzo chetu ni kwako.”

88

1 Ee Mwenyezi-Mungu, mwokozi wangu, ninalia mchana kutwa, na usiku nakulalamikia.

2 Sala yangu ikufikie, usikilize kilio changu.

3 Maafa mengi yamenipata, nami niko karibu kufa.

4 Ninaonekana kama mtu anayekufa, nguvu zangu zote zimeniishia.

5 Nimesahauliwa kati ya wafu, kama waliouawa, walioko kaburini; kama wale ambao huwakumbuki tena, ambao wametengwa na ulinzi wako.

6 Umenitupa katika kina cha kaburi; katika sehemu za giza na kina kikuu.

7 Hasira yako imenilemea; umenisonga kwa mawimbi yako yote.

8 Umewafanya rafiki zangu waniepe, umenifanya kuwa chukizo kwao. Nimefungwa ndani, wala siwezi kutoroka;

9 macho yangu yamefifia kwa huzuni. Kila siku nakulilia, ee Mwenyezi-Mungu; ninakunyoshea mikono yangu.

10 Je, wewe huwatendea wafu maajabu yako? Je, mizimu hufufuka na kukusifu?

11 Je, fadhili zako zinatajwa kaburini, au uaminifu wako kwenye makao ya maangamizi?

12 Je, maajabu yako yanajulikana humo gizani, au wema wako katika nchi ya waliosahauliwa?

13 Lakini mimi nakulilia, ee Mwenyezi-Mungu; kila asubuhi nakuletea ombi langu.

14 Mbona ee Mwenyezi-Mungu wanitupilia mbali? Kwa nini unanificha uso wako?

15 Nimeteseka na kukaribia kifo tangu ujana wangu; nateseka kwa mapigo yako, niko hoi kabisa.

16 Ghadhabu yako imeniwakia; mashambulio yako ya kutisha yananiangamiza.

17 Yananizunguka kama mafuriko mchana kutwa; yananizingira yote kwa pamoja.

18 Umewafanya rafiki na wenzangu wote waniepe; giza ndilo limekuwa mwenzangu.

89

1 Ee Mwenyezi-Mungu, nitaimba fadhili zako milele; nitavitangazia vizazi vyote uaminifu wako.

2 Natamka kuwa fadhili zako zadumu milele; uaminifu wako ni thabiti kama mbingu.

3 Umesema: “Nimefanya agano na mteule wangu, nimemwapia mtumishi wangu Daudi:

4 ‘Daima nitamweka mzawa wako kuwa mfalme, tena nitaudumisha ufalme wako milele.’”

5 Mbingu na zisifu maajabu yako, ee Mwenyezi-Mungu; uaminifu wako usifiwe katika kusanyiko la watakatifu.

6 Nani mbinguni awezaye kulinganishwa nawe ee Mwenyezi-Mungu? Nani aliye sawa nawe kati ya viumbe vya mbinguni?

7 Wewe waogopwa katika baraza la watakatifu; wote wanaokuzunguka wanatiwa hofu kuu.

8 Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wa majeshi, ni nani mwenye nguvu kama wewe, ee Mwenyezi-Mungu? Uaminifu umekuzunguka pande zote.

9 Wewe watawala machafuko ya bahari; mawimbi yake yakiinuka, wayatuliza.

10 Uliliponda joka Rahabu na kuliua; uliwatawanya adui zako kwa nguvu yako.

11 Mbingu ni zako na dunia ni yako pia; ulimwengu na vitu vyote vilivyomo wewe uliviumba.

12 Wewe uliumba kaskazini na kusini; milima Tabori na Hermoni inakusifu kwa furaha.

13 Mkono wako una nguvu, mkono wako una nguvu na umeshinda!

14 Uadilifu na haki ni msingi wa utawala wako; fadhili na uaminifu vyakutangulia!

15 Heri watu wanaojua kukushangilia, wanaoishi katika mwanga wa wema wako, ee Mwenyezi-Mungu.

16 Wanafurahi mchana kutwa kwa sababu yako, na kukusifu kwa ajili ya uadilifu wako.

17 Wewe ndiwe fahari na nguvu yao; kwa wema wako twapata ushindi.

18 Ee Mwenyezi-Mungu, mlinzi wetu ni wako, mfalme wetu ametoka kwako ewe Mtakatifu wa Israeli.

19 Zamani ulinena katika maono, ukawaambia watumishi wako waaminifu: “Nimempa nguvu shujaa mmoja, nimemkuza huyo niliyemteua kati ya watu.

20 Nimempata Daudi, mtumishi wangu; nimemweka wakfu kwa mafuta yangu matakatifu.

21 Mkono wangu wa nguvu utakuwa naye daima; mkono wangu mimi mwenyewe utamwimarisha.

22 Maadui hawataweza kumshinda, wala waovu hawatamnyanyasa.

23 Mimi nitawaponda wapinzani wake; nitawaangamiza wote wanaomchukia.

24 Nitakuwa mwaminifu kwake na kumfadhili, kwa jina langu atapata ushindi mkubwa.

25 Nitaimarisha nguvu na utawala wake, toka bahari hata mito.

26 Yeye ataniita: ‘Wewe ni Baba yangu, Mungu wangu, mwamba wa wokovu wangu.’

27 Nami nitamfanya kuwa mzaliwa wangu wa kwanza, mkuu kuliko wafalme wote duniani.

28 Fadhili zangu nitamwekea milele, na agano langu kwake litadumu daima.

29 Nitaudumisha daima ukoo wake wa kifalme, na ufalme wake kama mbingu.

30 “Lakini wazawa wake wakiiacha sheria yangu, wasipoishi kadiri ya maagizo yangu,

31 kama wakizivunja kanuni zangu, na kuacha kutii amri zangu,

32 hapo nitawaadhibu makosa yao; nitawapiga kwa sababu ya uovu wao.

33 Lakini sitaacha kumfadhili Daudi, wala kuwa mwongo kuhusu uaminifu wangu.

34 Sitavunja agano langu naye, wala kubatili neno nililotamka kwa mdomo wangu.

35 “Nimeapa mara moja tu kwa utakatifu wangu; nami sitamwambia Daudi uongo.

36 Ukoo wake utadumu milele; na ufalme wake kama jua.

37 Utadumu milele kama mwezi utokezavyo angani.”

38 Lakini sasa ee Mungu, umemtupa na kumkataa, umejaa ghadhabu dhidi ya huyo uliyemweka wakfu.

39 Umefuta agano ulilofanya na mtumishi wako; umeitupa taji yake mavumbini.

40 Kuta zote za mji wake umezibomoa; ngome zake umezivunjavunja.

41 Wote wapitao wanampokonya mali zake; amekuwa dharau kwa jirani zake.

42 Maadui zake umewapa ushindi; umewafurahisha maadui zake wote.

43 Silaha zake umezifanya butu; ukamwacha ashindwe vitani.

44 Umemvua madaraka yake ya kifalme ukauangusha chini utawala wake.

45 Umezipunguza siku za ujana wake, ukamfunika fedheha tele.

46 Ee Mwenyezi-Mungu, utajificha hata milele? Hata lini hasira yako itawaka kama moto?

47 Ukumbuke, ee Bwana, ufupi wa maisha yangu; kwamba binadamu uliyemuumba anaishi muda mfupi!

48 Ni mtu gani aishiye asipate kufa? Nani awezaye kujiepusha na kifo?

49 Ee Bwana, ziko wapi basi fadhili zako, ulizomwapia Daudi kwa uaminifu wako?

50 Ee Bwana, ukumbuke anavyotukanwa mtumishi wako, jinsi nivumiliavyo matusi ya wasiokujua.

51 Ona wanavyomzomea, ee Mwenyezi-Mungu; jinsi wanavyomdhihaki mteule wako kila aendako.

52 Asifiwe Mwenyezi-Mungu milele! Amina! Amina!

90

1 Ee Bwana, tangu vizazi vyote, wewe umekuwa usalama wetu.

2 Kabla ya kuwapo milima, kabla hujauumba ulimwengu; wewe ndiwe Mungu, milele na milele.

3 Wamwambia binadamu, “Rudi mavumbini!” Naye binadamu hurudi mavumbini alimotoka!

4 Kwako miaka elfu ni kama siku moja tu, ni kama jana ambayo imekwisha pita; kwako ni kama mkesha mmoja wa usiku!

5 Wawafutilia mbali watu kama ndoto! Binadamu ni kama nyasi zinazochipua asubuhi:

6 Asubuhi huchipua na kuchanua, jioni zimekwisha nyauka na kukauka.

7 Hasira yako inatuangamiza; tunatishwa na ghadhabu yako.

8 Maovu yetu umeyaweka mbele yako; dhambi zetu za siri ziko wazi mbele yako.

9 Kwa hasira yako maisha yetu yatoweka, yanaisha kama pumzi.

10 Miaka ya kuishi ni sabini, au tukiwa wenye afya, themanini; lakini yote ni shida na taabu! Siku zapita mbio, nasi twatoweka mara!

11 Nani anayetambua uzito wa hasira yako? Nani anayejali matokeo ya ghadhabu yako?

12 Utufundishe ufupi wa maisha yetu ili tuweze kuwa na hekima.

13 Urudi, ee Mwenyezi-Mungu! Utakasirika hata lini? Utuonee huruma sisi watumishi wako.

14 Utushibishe fadhili zako asubuhi, tushangilie na kufurahi maisha yetu yote.

15 Utujalie sasa miaka mingi ya furaha, kama ulivyotupa miaka mingi ya shida na taabu.

16 Utuoneshe matendo yako sisi watumishi wako; uwaoneshe wazawa wetu uwezo wako mtukufu.

17 Utufadhili ee Bwana, Mungu wetu; uzitegemeze kazi zetu, uzifanikishe shughuli zetu.

91

1 Anayekaa chini ya ulinzi wa Mungu Mkuu, anayeishi chini ya kivuli cha Mungu Mwenye Nguvu,

2 ataweza kumwambia Mwenyezi-Mungu: “Wewe ni kimbilio langu na ngome yangu; Mungu wangu, ninayekutumainia!”

3 Hakika Mungu atakuokoa katika mtego; atakukinga na maradhi mabaya.

4 Atakufunika kwa mabawa yake, utapata usalama kwake; mkono wake utakulinda na kukukinga.

5 Huna haja ya kuogopa vitisho vya usiku, wala shambulio la ghafla mchana;

6 huna haja ya kuogopa baa lizukalo usiku, wala maafa yanayotokea mchana.

7 Hata watu elfu wakianguka karibu nawe, naam, elfu kumi kuliani mwako, lakini wewe baa halitakukaribia.

8 Kwa macho yako mwenyewe utaangalia, na kuona jinsi watu waovu wanavyoadhibiwa.

9 Wewe umemfanya Mwenyezi-Mungu kuwa kimbilio lako; naam, Mungu aliye juu kuwa kinga yako.

10 Kwa hiyo, hutapatwa na maafa yoyote; nyumba yako haitakaribiwa na baa lolote.

11 Maana Mungu atawaamuru malaika zake, wakulinde popote uendapo.

12 Watakuchukua mikononi mwao, usije ukajikwaa kwenye jiwe.

13 Utakanyaga simba na nyoka, utawaponda wana simba na majoka.

14 Mungu asema: “Nitamwokoa yule anipendaye; nitamlinda anayenitambua!

15 Akiniita, mimi nitamwitikia; akiwa taabuni nitakuwa naye; nitamwokoa na kumpa heshima.

16 Nitamridhisha kwa maisha marefu, nitamjalia wokovu wangu.”

92

1 Ni vema kukushukuru, ee Mwenyezi-Mungu, kuliimbia sifa jina lako, ee Mungu Mkuu.

2 Ni vema kutangaza fadhili zako asubuhi, na uaminifu wako nyakati za usiku,

3 kwa muziki wa zeze na kinubi, kwa sauti tamu ya zeze.

4 Ee Mwenyezi-Mungu, matendo yako yanifurahisha; nitashangilia kwa sababu ya mambo yote uliyotenda.

5 Matendo yako, ee Mwenyezi-Mungu, ni makuu mno! Mawazo yako ni mazito mno!

6 Mtu mpumbavu hawezi kufahamu, wala mjinga hajui jambo hili:

7 Kwamba waovu waweza kustawi kama nyasi, watenda maovu wote waweza kufanikiwa, lakini mwisho wao ni kuangamia milele,

8 bali wewe, ee Mwenyezi-Mungu, u mkuu milele.

9 Hao maadui zako, ee Mwenyezi-Mungu, naam, hao maadui zako, hakika wataangamia; wote watendao maovu, watatawanyika!

10 Wewe umenipa nguvu kama nyati; umenimiminia mafuta ya kuburudisha.

11 Kwa macho nimeona maadui zangu wameshindwa; nimesikia kilio chao watendao maovu.

12 Waadilifu hustawi kama mitende; hukua kama mierezi ya Lebanoni!

13 Kama miti iliyopandwa nyumbani mwa Mwenyezi-Mungu, hustawi katika nyua za Mungu wetu;

14 huendelea kuzaa matunda hata uzeeni; daima wamejaa utomvu na wabichi;

15 wapate kutangaza kwamba Mwenyezi-Mungu ni mnyofu, Mwamba wangu, kwake hamna upotovu.

93

1 Mwenyezi-Mungu anatawala; amejivika fahari kuu! Mwenyezi-Mungu amevaa fahari na nguvu! Ameuimarisha ulimwengu, nao hautatikisika kamwe.

2 Kiti chako cha enzi ni imara tangu kale; wewe umekuwapo kabla ya nyakati zote.

3 Vilindi vimetoa sauti, ee Mwenyezi-Mungu; naam, vimepaza sauti yake, vilindi vyapaza tena mvumo wake.

4 Mwenyezi-Mungu ana enzi kuu juu mbinguni, ana nguvu kuliko mlio wa bahari, ana nguvu kuliko mawimbi ya maji.

5 Ee Mwenyezi-Mungu, maagizo yako ni thabiti; nyumba yako ni takatifu milele na milele.

94

1 Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu mwenye kulipiza kisasi, ewe Mungu mlipiza kisasi, ujitokeze!

2 Usimame, ee hakimu wa watu wote; uwaadhibu wenye kiburi wanavyostahili!

3 Waovu wataona fahari hata lini? Watajisifia mpaka lini, ee Mwenyezi-Mungu?

4 Hata lini waovu watajigamba kwa maneno? Waovu wote watajivuna mpaka lini?

5 Wanawaangamiza watu wako, ee Mwenyezi-Mungu, wanawakandamiza hao walio mali yako.

6 Wanawaua wajane na wageni; wanawachinja yatima!

7 Wanasema: “Mwenyezi-Mungu haoni, Mungu wa Yakobo hajui!”

8 Enyi wajinga wa mwisho, fikirini kidogo! Enyi wapumbavu, mtapata lini maarifa?

9 Aliyefanya sikio, je, hawezi kusikia? Aliyeumba jicho, je, hawezi kuona?

10 Mwenye kutawala mataifa, je, hawezi kuadhibu? Mkufunzi wa wanadamu, je, hana maarifa?

11 Mwenyezi-Mungu ayajua mawazo ya watu; anajua kwamba hayafai kitu.

12 Heri mtu unayemfunza nidhamu, ee Mwenyezi-Mungu, mtu unayemfundisha sheria yako,

13 ili siku ya taabu apate utulivu, hadi waovu wachimbiwe shimo.

14 Mwenyezi-Mungu hatawaacha watu wake; hatawatupa hao walio mali yake.

15 Maana hukumu zitatolewa kwa haki tena, na wanyofu wote wa moyo wataizingatia.

16 Nani aliyenisaidia kumpinga mtu mwovu? Nani aliyekuwa upande wangu dhidi ya wabaya?

17 Mwenyezi-Mungu asingalinisaidia, ningalikwisha kwenda kwenye nchi ya wafu.

18 Nilipohisi kwamba ninateleza, fadhili zako, ee Mwenyezi-Mungu, zilinitegemeza.

19 Mahangaiko ya moyo wangu yanapozidi, wewe wanifariji na kunifurahisha.

20 Wewe huwezi kushirikiana na mahakimu dhalimu, wanaotunga kanuni za kutetea maovu.

21 Wao wanaafikiana kuwaangamiza waadilifu, na kuwahukumu watu wasio na hatia wauawe.

22 Lakini Mwenyezi-Mungu ni ngome yangu; Mungu wangu ni mwamba wa usalama wangu.

23 Uovu wao atawarudishia wao wenyewe, atawafutilia mbali kwa sababu ya ubaya wao. Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, atawafutilia mbali!

95

1 Njoni tumwimbie Mwenyezi-Mungu, tumshangilie mwamba wa wokovu wetu!

2 Twende mbele zake na shukrani; tumshangilie kwa nyimbo za sifa.

3 Maana Mwenyezi-Mungu, ni Mungu mkuu; yeye ni Mfalme mkuu juu ya miungu yote.

4 Vilindi vyote vya dunia vimo mikononi mwake, vilele vya milima ni vyake.

5 Bahari ni yake, ndiye aliyeifanya; kwa mikono yake aliiumba nchi kavu.

6 Njoni tusujudu na kumwabudu; tumpigie magoti Mwenyezi-Mungu, Muumba wetu!

7 Maana yeye ni Mungu wetu, nasi ni watu wa kundi lake, ni kondoo wake anaowachunga. Laiti leo mngesikiliza sauti yake:

8 “Msiwe wakaidi kama kule Meriba, kama walivyokuwa kule Masa jangwani,

9 wazee wenu waliponijaribu na kunipima, ingawa walikuwa wameona mambo niliyowatendea.

10 Kwa miaka arubaini nilichukizwa nao, nikasema: ‘Kweli, hawa ni watu waliopotoka! Hawajali kabisa njia zangu!’

11 Basi, nilikasirika, nikaapa: ‘Hawataingia mahali pangu pa pumziko!’”

96

1 Mwimbieni Mwenyezi-Mungu wimbo mpya! Mwimbieni Mwenyezi-Mungu, ulimwengu wote!

2 Mwimbieni Mwenyezi-Mungu na kulisifu jina lake. Tangazeni kila siku matendo yake ya wokovu.

3 Yatangazieni mataifa utukufu wake, waambieni watu wote matendo yake ya ajabu.

4 Maana Mwenyezi-Mungu ni mkuu, anasifika sana; anastahili kuheshimiwa kuliko miungu yote.

5 Miungu ya mataifa mengine si kitu; lakini Mwenyezi-Mungu aliziumba mbingu.

6 Utukufu na fahari vyamzunguka; nguvu na uzuri vyalijaza hekalu lake.

7 Mpeni Mwenyezi-Mungu heshima, enyi jamii zote za watu; naam, kirini utukufu na nguvu yake.

8 Lisifuni jina lake tukufu; leteni tambiko na kuingia hekaluni mwake.

9 Mwabuduni Mwenyezi-Mungu katika patakatifu pake; tetemekeni mbele yake ee dunia yote!

10 Yaambieni mataifa: “Mwenyezi-Mungu anatawala! Ameuweka ulimwengu imara, hautatikisika. Atawahukumu watu kwa haki!”

11 Furahini enyi mbingu na dunia! Bahari na ivume pamoja na vyote vilivyomo!

12 Furahini enyi mashamba na vyote vilivyomo! Ndipo miti yote misituni itaimba kwa furaha,

13 mbele ya Mwenyezi-Mungu anayekuja; naam, anayekuja kuihukumu dunia. Ataihukumu dunia kwa haki, na mataifa kwa uaminifu wake.

97

1 Mwenyezi-Mungu anatawala! Furahi, ee dunia! Furahini enyi visiwa vingi!

2 Mawingu na giza nene vyamzunguka; uadilifu na haki ni msingi wa utawala wake.

3 Moto watangulia mbele yake, na kuwateketeza maadui zake pande zote.

4 Umeme wake wauangaza ulimwengu; dunia yauona na kutetemeka.

5 Milima yayeyuka kama nta mbele ya Mwenyezi-Mungu; naam, mbele ya Bwana wa dunia yote.

6 Mbingu zatangaza uadilifu wake; na mataifa yote yauona utukufu wake.

7 Wote wanaoabudu sanamu wanaaibishwa, naam, wote wanaojisifia miungu duni; miungu yote husujudu mbele zake.

8 Watu wa Siyoni wanafurahi; watu wa Yuda wanashangilia, kwa sababu ya hukumu zako, ee Mungu.

9 Wewe Mwenyezi-Mungu ni mkuu juu ya dunia yote; wewe watukuka juu ya miungu yote.

10 Mwenyezi-Mungu huwapenda wanaochukia uovu, huyalinda maisha ya watu wake; huwaokoa makuchani mwa waovu.

11 Mwanga humwangazia mtu mwadilifu, na furaha kwa watu wanyofu wa moyo.

12 Furahini kwa sababu ya Mwenyezi-Mungu enyi waadilifu; mshukuruni kwa ajili ya jina lake takatifu.

98

1 Mwimbieni Mwenyezi-Mungu wimbo mpya, kwa maana ametenda mambo ya ajabu! Mkono wake hodari, mkono wake mtakatifu umempatia ushindi.

2 Mwenyezi-Mungu ameonesha ushindi wake; ameyadhihirishia mataifa uwezo wake wa kuokoa.

3 Amekumbuka fadhili na uaminifu wake kwa Waisraeli. Pande zote za dunia zimeuona ushindi wa Mungu wetu.

4 Dunia yote imshangilie Mwenyezi-Mungu; imsifu kwa nyimbo na vigelegele.

5 Msifuni Mwenyezi-Mungu kwa shangwe, msifuni kwa sauti tamu za zeze.

6 Mpigieni vigelegele Mwenyezi-Mungu mfalme wetu, mshangilieni kwa tarumbeta na sauti ya baragumu.

7 Bahari na ivume na vyote vilivyomo; dunia na wote waishio ndani yake.

8 Enyi mito pigeni makofi; enyi vilima imbeni pamoja kwa shangwe.

9 Shangilieni mbele ya Mwenyezi-Mungu, maana anakuja kutawala dunia. Atauhukumu ulimwengu kwa haki, atawatawala watu kwa uadilifu.

99

1 Mwenyezi-Mungu anatawala, mataifa yanatetemeka! Ameketi juu ya viumbe vyenye mabawa, nayo dunia inatikisika!

2 Mwenyezi-Mungu ni mkuu katika Siyoni; ametukuka juu ya mataifa yote.

3 Wote na walisifu jina lake kuu la kutisha. Mtakatifu ndiye yeye!

4 Ee mfalme mkuu, mpenda uadilifu! Umethibitisha haki katika Israeli; umeleta uadilifu na haki.

5 Msifuni Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu; angukeni kifudifudi mbele zake. Mtakatifu ndiye yeye!

6 Mose na Aroni walikuwa makuhani wake; Samueli alikuwa miongoni mwa waliomlilia. Walimlilia Mwenyezi-Mungu naye akawasikiliza.

7 Alisema nao katika mnara wa wingu; waliyazingatia matakwa yake na amri alizowapa.

8 Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, wewe uliwasikiliza; kwao ulikuwa Mungu mwenye kusamehe, ingawa uliwaadhibu kwa makosa yao.

9 Msifuni Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu; abuduni katika mlima wake mtakatifu! Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, ni mtakatifu.

100

1 Mshangilieni Mwenyezi-Mungu, enyi nchi zote!

2 Mwabuduni Mwenyezi-Mungu kwa furaha, nendeni kwake mkiimba kwa shangwe!

3 Jueni kwamba Mwenyezi-Mungu ni Mungu. Yeye ndiye aliyetuumba, nasi ni mali yake; sisi ni watu wake, ni kondoo wa malisho yake.

4 Pitieni milango ya hekalu lake kwa shukrani, ingieni katika nyua zake kwa sifa. Mshukuruni na kulisifu jina lake.

5 Mwenyezi-Mungu ni mwema; fadhili zake zadumu milele, na uaminifu wake katika vizazi vyote.

101

1 Utenzi wangu kuhusu uaminifu na haki; ninauimba kwa heshima yako, ee Mwenyezi-Mungu.

2 Nitazingatia mwenendo usio na hatia. Je, utakuja kwangu lini? Nitaishi kwa unyofu nyumbani kwangu;

3 sitavumilia kamwe upuuzi. Nayachukia matendo ya watu wapotovu, mambo yao hayataambatana nami.

4 Upotovu wowote ule uwe mbali nami; sitahusika kabisa na uovu.

5 Anayemsengenya jirani nitamfutilia mbali; sitamvumilia mwenye majivuno na kiburi.

6 Nitawaangalia kwa wema watu walio waaminifu, wapate kuishi pamoja nami. Watu wanyofu ndio watakaonitumikia.

7 Mwongo yeyote hatakaa nyumbani mwangu; hakuna msema uongo atakayekaa kwangu.

8 Siku kwa siku nitawaangamiza waovu wote nchini; nitawaangamiza wabaya wote mjini mwa Mwenyezi-Mungu.

102

1 Usikie sala yangu, ee Mwenyezi-Mungu, na kilio changu kikufikie.

2 Usijifiche mbali nami wakati wa taabu! Unitegee sikio lako, unijibu upesi wakati ninapokuomba!

3 Siku zangu zapita kama moshi; mifupa yangu yaungua kama katika tanuri.

4 Nimepondwa moyoni kama nyasi na kunyauka; sina hata hamu ya chakula.

5 Kutokana na kusononeka kwangu, nimebaki mifupa na ngozi.

6 Nimekuwa kama ndege wa jangwani; kama bundi kwenye mahame.

7 Ninalala macho wazi, kama ndege mkiwa juu ya paa.

8 Mchana kutwa maadui zangu wananisimanga, wanaonidhihaki hutumia jina langu kulaania.

9 Majivu yamekuwa chakula changu, machozi nayachanganya na kinywaji changu,

10 kwa sababu ya ghadhabu na hasira yako, maana umeniokota na kunitupilia mbali.

11 Maisha yangu ni kama kivuli cha jioni; ninanyauka kama nyasi.

12 Lakini wewe, ee Mwenyezi-Mungu, watawala milele; jina lako lakumbukwa vizazi vyote.

13 Wewe utainuka na kuurehemu mji wa Siyoni; maana wakati umefika wa kuutendea mema; wakati wake uliopangwa umefika.

14 Watumishi wako wanauthamini sana, ujapokuwa magofu sasa; wanauonea huruma, ingawa umeharibika kabisa.

15 Mataifa yataliheshimu jina la Mwenyezi-Mungu; wafalme wote duniani wataogopa utukufu wake.

16 Mwenyezi-Mungu ataijenga upya Siyoni, na kuonekana alivyo mtukufu.

17 Ataikubali sala ya fukara; wala hatayakataa maombi yao.

18 Andika jambo hili kwa ajili ya vizazi vijavyo; watakaozaliwa baadaye wamsifu Mwenyezi-Mungu.

19 Kwamba aliangalia chini kutoka patakatifu pake juu, Mwenyezi-Mungu aliangalia dunia kutoka mbinguni,

20 akasikia lalamiko la wafungwa; akawaachilia huru waliohukumiwa kuuawa.

21 Hivyo watu watatangaza jina la Mwenyezi-Mungu huko Siyoni; sifa zake zitatangazwa huko Yerusalemu,

22 wakati mataifa yatakapokusanyika pamoja na falme zitakutana kumwabudu Mwenyezi-Mungu.

23 Mungu amenipunguzia nguvu ningali kijana; ameyafupisha maisha yangu.

24 Ee Mungu wangu, usinichukue sasa wakati ningali bado kijana. Ee Mwenyezi-Mungu wewe wadumu milele.

25 Wewe uliiumba dunia zamani za kale, mbingu ni kazi ya mikono yako.

26 Hizo zitatoweka, lakini wewe wabaki; hizo zitachakaa kama vazi. Utazitupilia mbali kama nguo, nazo zitapotelea mbali.

27 Lakini wewe ni yuleyule daima, na maisha yako hayana mwisho.

28 Watoto wa watumishi wako watakaa salama; wazawa wao wataimarishwa mbele yako.

103

1 Ee nafsi yangu, umsifu Mwenyezi-Mungu; nafsi yangu yote ilisifu jina lake takatifu!

2 Ee nafsi yangu, umsifu Mwenyezi-Mungu! Usisahau kamwe wema wake wote.

3 Ndiye anayenisamehe uovu wangu wote, na kuniponya magonjwa yote.

4 Ndiye aniokoaye kutoka kifoni, na kunijalia rehema na fadhili zake.

5 Ndiye anayeniridhisha mema maisha yangu yote, hata nabaki kijana mwenye nguvu kama tai.

6 Mwenyezi-Mungu huhukumu kwa haki; huwajalia wanaodhulumiwa haki zao.

7 Alimjulisha Mose mwongozo wake, aliwaonesha watu wa Israeli matendo yake.

8 Mwenyezi-Mungu ni mwenye rehema na huruma; ni mvumilivu na mwingi wa fadhili.

9 Hatukemeikemei daima, wala hasira yake haidumu milele.

10 Yeye hatuadhibu kama tunavyostahili; hatulipizi kadiri ya uovu wetu.

11 Kama vile anga lilivyo juu mbali na dunia, ndivyo ulivyo mwingi wema wake kwa watu wanaomcha.

12 Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, ndivyo azitengavyo dhambi zetu mbali nasi.

13 Kama vile baba amhurumiavyo mwanawe, ndivyo Mwenyezi-Mungu awahurumiavyo wote wamchao.

14 Mungu ajua mfumo wa nafsi zetu; ajua kwamba sisi ni mavumbi.

15 Walakini binadamu, maisha yake ni kama nyasi tu; huchanua kama ua shambani:

16 Upepo huvuma juu yake nalo latoweka; na mahali lilipokuwa hapaonekani tena.

17 Lakini fadhili za Mwenyezi-Mungu hudumu milele, kwa wale wote wanaomheshimu; na wema wake wadumu vizazi vyote,

18 kwa wote wanaozingatia agano lake, wanaokumbuka kutii amri zake.

19 Mwenyezi-Mungu ameweka kiti chake cha enzi mbinguni; yeye anatawala juu ya vitu vyote.

20 Enyi malaika wakuu, msifuni Mwenyezi-Mungu; mnaotimiza amri zake na kutekeleza neno lake!

21 Enyi jeshi lote la mbinguni, msifuni Mwenyezi-Mungu; enyi watumishi wake mnaotekeleza matakwa yake!

22 Msifuni Mwenyezi-Mungu enyi viumbe vyake vyote; msifuni popote mlipo katika milki yake. Ee nafsi yangu, umsifu Mwenyezi-Mungu!

104

1 Umsifu Mwenyezi-Mungu, ee nafsi yangu! Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu, wewe ni mkuu mno! Umejivika utukufu na fahari.

2 Umejizungushia mwanga kama vazi, umezitandaza mbingu kama hema;

3 umejenga makao yako juu ya maji ya mbingu. Umeyafanya mawingu kuwa gari lako; waruka juu ya mabawa ya upepo,

4 waufanya upepo kuwa mjumbe wako, moto na miali yake kuwa watumishi wako.

5 Dunia umeiweka imara juu ya misingi yake, ili isitikisike milele.

6 Uliifunika dunia kwa bahari kama vazi, na maji yakaimeza milima mirefu.

7 Ulipoyakaripia, maji yalikimbia, yaliposikia ngurumo yako yalitimka mbio.

8 Yaliporomoka toka milimani hadi mabondeni, mpaka pale mahali ulipoyatengenezea.

9 Uliyawekea hayo maji mipaka, yasije yakaifunika tena dunia.

10 Umetokeza chemchemi mabondeni, na mikondo yake ipite kati ya vilima.

11 Hizo zawapatia maji wanyama wote porini. Humo pundamwitu huzima kiu zao.

12 Ndege hujenga viota vyao katika miti ya hapo, hutua katika matawi yake na kuimba.

13 Toka juu angani wainyeshea milima mvua, nayo dunia waitosheleza kwa baraka yako.

14 Waotesha nyasi kwa ajili ya mifugo, na mimea kwa matumizi ya binadamu ili naye ajipatie chakula chake ardhini:

15 Divai ya kumchangamsha, mafuta ya zeituni ya kumfurahisha, na mkate wa kumpa nguvu.

16 Miti mikubwa ya Mwenyezi-Mungu yapata maji ya kutosha; naam, mierezi ya Lebanoni aliyoiotesha.

17 Humo, ndege hujenga viota vyao; korongo hufanya maskani yao katika misonobari.

18 Milima mirefu ni makao ya mbuzimwitu; na pelele hupata maficho yao miambani.

19 Umeuumba mwezi utupimie majira; jua nalo lajua wakati wa kutua.

20 Waleta giza, usiku waingia; nao wanyama wote wa porini wanatoka:

21 Wanasimba hunguruma wapate mawindo, humngojea Mungu awape chakula chao.

22 Jua lichomozapo hurudi makwao, na kujipumzisha mapangoni mwao.

23 Hapo naye binadamu huenda kwenye shughuli zake; na kufanya kazi zake mpaka jioni.

24 Ee Mwenyezi-Mungu, umetenda mambo mengi mno! Yote umeyafanya kwa hekima! Dunia imejaa viumbe vyako!

25 Mbali kule iko bahari - kubwa na pana, ambamo kumejaa viumbe visivyohesabika, viumbe hai, vikubwa na vidogo.

26 Ndimo zinamosafiri meli, na lile dude Lewiyathani uliloliumba licheze humo.

27 Wote wanakungojea wewe, uwapatie chakula chao kwa wakati wake.

28 Wanaokota chochote kile unachowapa; ukifumbua mkono wako wanashiba vinono.

29 Ukiwapa kisogo, wanaogopa; ukiondoa pumzi yao, wanakufa, na kurudi mavumbini walimotoka.

30 Ukiwapulizia pumzi yako, wanaishi tena; wewe waipa dunia sura mpya.

31 Utukufu wa Mwenyezi-Mungu udumu milele; Mwenyezi-Mungu apendezwe na matendo yake mwenyewe.

32 Huitazama dunia nayo hutetemeka, huigusa milima nayo hutoa moshi!

33 Nitamwimbia Mwenyezi-Mungu maisha yangu yote; nitamsifu Mungu wangu muda wote niishipo.

34 Upendezwe, ee Mwenyezi-Mungu, na mawazo yangu haya; maana furaha yangu naipata kwako.

35 Wenye dhambi waondolewe duniani, pasiwe na waovu wowote tena! Umsifu Mwenyezi-Mungu, ee nafsi yangu! Msifuni Mwenyezi-Mungu!

105

1 Mshukuruni Mwenyezi-Mungu, tangazeni ukuu wake; yajulisheni mataifa mambo aliyotenda!

2 Mshangilieni, mwimbieni Mungu sifa; simulieni matendo yake ya ajabu!

3 Jisifieni jina lake takatifu; wenye kumcha Mwenyezi-Mungu na wafurahi.

4 Tafuteni msaada kwa Mwenyezi-Mungu mwenye nguvu; mwendeeni Mwenyezi-Mungu daima.

5 Kumbukeni matendo ya ajabu aliyotenda, miujiza yake na hukumu alizotoa,

6 enyi wazawa wa Abrahamu mtumishi wake, enyi wazawa wa Yakobo, wateule wake;

7 Yeye ndiye Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu; hukumu zake zina nguvu duniani kote.

8 Yeye hulishika agano lake milele, hutimiza ahadi zake kwa vizazi elfu.

9 Hushika agano alilofanya na Abrahamu, na ahadi aliyomwapia Isaka.

10 Alimthibitishia Yakobo ahadi yake, alimhakikishia Israeli agano hilo la milele.

11 Alisema: “Nitawapeni nchi ya Kanaani, nayo itakuwa mali yenu wenyewe.”

12 Watu wa Mungu walikuwa wachache; hawakuwa maarufu, tena walikuwa wageni nchini Kanaani.

13 Walitangatanga kutoka taifa hadi taifa; kutoka nchi moja hadi nchi nyingine.

14 Lakini Mungu hakuruhusu mtu awadhulumu; kwa ajili yao aliwaonya wafalme:

15 “Msiwaguse wateule wangu; msiwadhuru manabii wangu!”

16 Mungu alizusha njaa nchini mwao, akaharibu chakula chao chote.

17 Lakini aliwatangulizia mtu mmoja, Yosefu aliyekuwa ameuzwa utumwani.

18 Walimfunga miguu kwa minyororo, na shingoni kwa nira ya chuma,

19 Muda si muda alichotabiri kilitimia. neno la Mwenyezi-Mungu lilimdhibiti.

20 Mfalme wa Misri akaamuru afunguliwe; mtawala wa mataifa akamwachilia huru.

21 Alimweka kuwa mkurugenzi wa serikali yake, na mkuu wa mali yake yote;

22 awaongoze maofisa wake apendavyo, na kuwafundisha wazee wake hekima.

23 Ndipo Israeli akaingia nchini Misri; Yakobo akawa mgeni katika nchi ya Hamu.

24 Mwenyezi-Mungu akawafanya watu wake wazae sana; akawajalia nguvu kuliko maadui zao.

25 Aliwafanya Wamisri wawachukie watu wake, wakawatendea hila watumishi wake.

26 Kisha akamtuma Mose mtumishi wake, akamtuma na Aroni mteule wake.

27 Wakafanya ishara za Mungu kati ya Wamisri, na miujiza katika nchi hiyo ya Hamu.

28 Mungu akaleta giza juu ya nchi; lakini Wamisri wakakataa kutii amri zake.

29 Akageuza mito yao kuwa damu, akawaua samaki wao wote.

30 Vyura wakaivamia nchi yao, hata jumba la mfalme likajawa nao.

31 Mungu akanena, kukazuka makundi ya nzi, na viroboto katika nchi yote.

32 Badala ya mvua akawapa mvua ya mawe, na umeme uliomulika nchi yao yote;

33 akaharibu mizabibu na mitini yao, akaivunja pia miti ya nchi yao.

34 Mungu akanena, kukazuka nzige, na panzi maelfu yasiyohesabika;

35 wakaitafuna mimea yote katika nchi, wakayala mazao yao yote.

36 Aliwaua wazaliwa wa kwanza nchini mwao, chipukizi wa kwanza wa jamaa za Wamisri.

37 Kisha akawatoa watu wa Israeli nchini, wakiwa na fedha na dhahabu; wala hakuna hata mmoja wao aliyejikwaa.

38 Wamisri walifurahia kuondoka kwao, kwani hofu iliwashika kwa sababu yao.

39 Mungu alitandaza wingu juu ya watu wake, na moto ili kuwaangazia usiku.

40 Waliomba naye akawaletea kware, akawapa mkate kutoka mbinguni kwa wingi.

41 Alipasua mwamba maji yakabubujika; yakatiririka jangwani kama mto.

42 Aliikumbuka ahadi yake takatifu, aliyompa Abrahamu mtumishi wake.

43 Basi akawatoa watu wake nchini, wateule wake wakaimba na kushangilia.

44 Aliwapa nchi za mataifa mengine na kuwakabidhi mashamba ya wenyeji;

45 kusudi watu wake watii masharti yake, na kufuata sheria zake. Asifiwe Mwenyezi-Mungu!

106

1 Haleluya! Msifuni Mwenyezi-Mungu! Mshukuruni Mwenyezi-Mungu kwa kuwa ni mwema; kwa maana fadhili zake zadumu milele!

2 Ni nani awezaye kutaja matendo ya Mwenyezi-Mungu? Ni nani awezaye kumsifu kama anavyostahili?

3 Heri wale wanaotekeleza haki, wanaotenda daima mambo yaliyo sawa.

4 Unikumbuke ee Mwenyezi-Mungu unapowafadhili watu wako; unisaidie wakati unapowaokoa;

5 ili niweze kuona fanaka ya wateule wako, nipate kufurahia furaha ya taifa lako, na kuona fahari pamoja na watu wako.

6 Tumetenda dhambi sisi na wazee wetu; tumetenda maovu, tumefanya mabaya.

7 Wazee wetu walipokuwa Misri, hawakujali matendo ya ajabu ya Mungu; hawakukumbuka wingi wa fadhili zake, bali walimwasi kando ya bahari ya Shamu.

8 Hata hivyo Mungu aliwaokoa kama alivyoahidi, ili aoneshe nguvu yake kuu.

9 Aliikemea bahari ya Shamu ikakauka; akawapitisha humo kama katika nchi kavu.

10 Aliwaokoa mikononi mwa waliowachukia; aliwaokoa kutoka kwa nguvu za maadui zao.

11 Maji ya bahari yaliwafunika maadui zao; wala hakusalia hata mmoja wao.

12 Hapo watu wake wakaamini maneno yake, wakamwimbia tenzi za sifa yake.

13 Lakini mara walisahau matendo yake, wakaacha kutegemea shauri lake.

14 Walijawa na tamaa kubwa kule jangwani, wakamjaribu Mungu kule nyikani.

15 Naye akawapa kile walichoomba, lakini akapeleka maradhi mabaya kati yao.

16 Kule kambini walimwonea wivu Mose, na Aroni mtumishi mtakatifu wa Mwenyezi-Mungu.

17 Ndipo ardhi ikafunguka ikammeza Dathani, na kumzika Abiramu na kundi lake lote;

18 moto ukawatokea wafuasi wao, ukawateketeza watu hao waovu.

19 Walitengeneza ndama wa dhahabu kule Horebu, wakaiabudu sanamu hiyo ya kusubu;

20 waliubadilisha utukufu wa Mungu, kwa sanamu ya mnyama ambaye hula nyasi.

21 Walimsahau Mungu aliyewaokoa, aliyetenda mambo makuu nchini Misri,

22 maajabu katika nchi hiyo ya Hamu, na mambo ya kutisha katika bahari ya Shamu.

23 Mungu alisema atawaangamiza watu wake, ila tu Mose mteule wake aliingilia kati, akaizuia hasira yake isiwaangamize.

24 Kisha wakaidharau nchi ile ya kupendeza, kwa sababu hawakuwa na imani na ahadi ya Mungu.

25 Walinungunika mahemani mwao, wala hawakumsikiliza Mwenyezi-Mungu.

26 Hivyo Mungu akainua mkono akaapa kwamba atawaangamizia jangwani;

27 atawatawanya wazawa wao kati ya watu, na kuwasambaza duniani kote.

28 Kisha wakajiunga kumwabudu Baali kule Peori, wakala tambiko zilizotambikiwa mizimu.

29 Waliichochea hasira ya Mwenyezi-Mungu kwa matendo yao, maradhi mabaya yakazuka kati yao.

30 Lakini Finehasi akasimama kufanya malipizi, na yale maradhi yakakoma.

31 Jambo hilo lakumbukwa kwa heshima yake, tangu wakati huo na nyakati zote.

32 Walimkasirisha Mungu penye maji ya Meriba, Mose akapata taabu kwa ajili yao.

33 Walimtia Mose uchungu rohoni, hata akasema maneno bila kufikiri.

34 Hawakuwaua watu wa mataifa mengine kama Mwenyezi-Mungu alivyowaamuru.

35 Bali walijumuika na watu wa mataifa, wakajifunza kutenda mambo yao.

36 Waliabudu sanamu za miungu yao, nazo zikawa mtego wa kuwaangamiza.

37 Waliwaua watoto wao wa kiume na wa kike, wakawatoa tambiko kwa pepo.

38 Walimwaga damu ya wasio na hatia, damu ya watoto wao wa kiume na wa kike ambao waliwatoa tambiko kwa sanamu za Kanaani, nayo nchi ikatiwa unajisi kwa mauaji hayo.

39 Hivyo wakafanywa najisi kwa matendo yao, 2wakakosa uaminifu kwa Mungu kama wazinzi.

40 Hasira ya Mwenyezi-Mungu ikawawakia watu wake, akachukizwa sana na hao waliokuwa mali yake.

41 Akawatia makuchani mwa watu wa mataifa, hao wenye kuwachukia wakawatawala.

42 Maadui zao waliwakandamiza, wakawatumikisha kwa nguvu.

43 Mara nyingi Mungu aliwaokoa watu wake, lakini wao wakachagua kumwasi, wakazidi kuzama katika uovu wao.

44 Hata hivyo Mungu alizijali taabu zao, wakati aliposikia kilio chao;

45 kwa ajili yao alilikumbuka agano lake, akawahurumia kwa wingi wa fadhili zake.

46 Aliwafanya waliowakandamiza wawaonee huruma.

47 Utuokoe, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, utukusanye pamoja kutoka kwa mataifa, tupate kulisifu jina lako takatifu, na kuona fahari juu ya sifa zako.

48 Asifiwe Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, tangu milele na hata milele! Na watu wote waseme: “Amina!” Asifiwe Mwenyezi-Mungu!

107

1 Mshukuruni Mwenyezi-Mungu kwa kuwa ni mwema; kwa maana fadhili zake zadumu milele!

2 Semeni hivyo, enyi mliokombolewa na Mwenyezi-Mungu, watu ambao aliwaokoa katika taabu,

3 akawakusanyeni kutoka nchi za kigeni: Kutoka mashariki na magharibi, kutoka kaskazini na kusini.

4 Baadhi walitangatanga katika jangwa tupu, wasiweze kufikia mji wa kukaa.

5 Waliona njaa na kiu; wakavunjika moyo kabisa.

6 Ndipo katika taabu yao wakamlilia Mwenyezi-Mungu, naye akawaokoa katika mateso yao.

7 Aliwaongoza katika njia iliyonyoka, mpaka wakaufikia mji wa kukaa.

8 Mshukuruni Mwenyezi-Mungu kwa fadhili zake; kwa sababu ya maajabu aliyowatendea binadamu.

9 Yeye huwatosheleza walio na kiu; na wenye njaa huwashibisha mema.

10 Baadhi waliishi katika giza na ukiwa, wafungwa katika mateso na minyororo,

11 kwa sababu waliasi maagizo ya Mungu, na kuyapuuza mashauri yake Mungu Mkuu.

12 Walikuwa hoi kwa kazi ngumu, wakaanguka chini, pasiwe na wa kuwasaidia.

13 Ndipo katika taabu yao wakamlilia Mwenyezi-Mungu, naye akawaokoa katika mateso yao.

14 Aliwatoa katika giza na ukiwa, na minyororo yao akaivunjavunja.

15 Mshukuruni Mwenyezi-Mungu, kwa fadhili zake; kwa sababu ya maajabu aliyowatendea binadamu.

16 Yeye huvunja na kufungua milango ya shaba, na kukatakata fito za chuma.

17 Baadhi walipumbaa kwa sababu ya dhambi zao, waliteseka kwa sababu ya uovu wao;

18 chakula kikawa kinyaa kwao, wakawa nusura wafe.

19 Ndipo katika taabu yao wakamlilia Mwenyezi-Mungu, naye akawaokoa katika mateso yao.

20 Kwa neno lake aliwaponya, akawaokoa wasiangamie.

21 Mshukuruni Mwenyezi-Mungu kwa fadhili zake; kwa sababu ya maajabu aliyowatendea binadamu.

22 Wamtolee tambiko za shukrani; wasimulie matendo yake kwa nyimbo za shangwe.

23 Baadhi walisafiri baharini kwa meli, na kufanya shughuli zao humo baharini.

24 Waliyaona matendo ya Mwenyezi-Mungu, mambo ya ajabu aliyotenda huko.

25 Aliamuru, akazusha dhoruba kali, ikarusha juu mawimbi ya bahari.

26 Walitupwa juu angani, kisha chini vilindini; uhodari wao ukawaishia katika mkasa huo.

27 Waliyumbayumba na kupepesuka kama walevi; maarifa yao ya uanamaji yakawaishia.

28 Ndipo katika taabu zao wakamlilia Mwenyezi-Mungu, naye akawaokoa katika mateso zao.

29 Aliifanya ile dhoruba kali itulie, nayo mawimbi yakanyamaza.

30 Hapo wakafurahi kwa kupata utulivu; akawafikisha kwenye bandari waliyoiendea.

31 Mshukuruni Mwenyezi-Mungu kwa fadhili zake; kwa sababu ya maajabu aliyowatendea binadamu.

32 Mtukuzeni katika kusanyiko la watu, na kumsifu katika baraza la wazee.

33 Mungu aliigeuza mito kuwa jangwa, chemchemi akazikausha kabisa.

34 Ardhi yenye rutuba akaifanya udongo wa chumvi, kwa sababu ya uovu wa wakazi wake.

35 Aligeuza majangwa kuwa mabwawa ya maji, na nchi kame kuwa chemchemi za maji.

36 Akawahamishia huko wenye njaa, nao wakajenga mji wa kukalika.

37 Walilima mashamba na kupanda mizabibu, wakavuna mazao kwa wingi.

38 Aliwabariki watu wake, wakaongezeka; na idadi ya wanyama wao akaizidisha.

39 Kisha walipopungua na kuwa wanyonge, kwa kukandamizwa, kuteswa na huzuni,

40 aliwadharau wakuu waliowatesa, akawazungusha jangwani kusiko na njia.

41 Lakini aliwaokoa wahitaji katika taabu zao, akaongeza jamaa zao kama kundi la kondoo.

42 Waadilifu waonapo jambo hilo wanafurahi, lakini waovu wote wananyamazishwa.

43 Wenye hekima na wayafikirie mambo haya, wazitambue fadhili zake Mwenyezi-Mungu.

108

1 Niko thabiti moyoni, ee Mungu, naam, niko thabiti moyoni; nitaimba na kukushangilia! Amka, ee nafsi yangu!

2 Amkeni enyi kinubi na zeze! Nitayaamsha mapambazuko!

3 Ee Mwenyezi-Mungu, nitakushukuru kati ya mataifa; nitakuimbia sifa kati ya mataifa.

4 Fadhili zako ni kubwa kuliko mbingu; uaminifu wako waenea hata mawinguni.

5 Utukuzwe, ee Mungu juu ya mbingu! Utukufu wako uenee duniani kote!

6 Watu hao uwapendao na wasalimishwe; utusaidie kwa mkono wako na kutusikiliza.

7 Mungu amesema kutoka patakatifu pake: “Sasa nitaigawa Shekemu kwa shangwe, bonde la Sukothi nitalipima sehemusehemu.

8 Gileadi ni yangu, na Manase ni yangu; Efraimu ni kofia yangu ya chuma, na Yuda ni fimbo yangu ya enzi.

9 Moabu ni kama bakuli langu la kunawia; kiatu changu nitaitupia Edomu kuimiliki. Nitapiga kelele ya ushindi juu ya Filistia!”

10 Ni nani, atakayenipeleka kwenye mji wa ngome? Ni nani atakayeniongoza mpaka Edomu?

11 Je, umetuacha kabisa, ee Mungu? Wewe huendi tena na majeshi yetu!

12 Utupatie msaada dhidi ya maadui zetu, maana msaada wa binadamu haufai kitu.

13 Mungu akiwa upande wetu tutashinda, yeye atawaponda maadui zetu.

109

1 Usinyamaze, ee Mungu ninayekusifu!

2 Watu waovu na wadanganyifu wanishambulia, wanasema uongo dhidi yangu.

3 Wanasema maovu juu yangu, na kunishambulia bila kisa.

4 Ingawa niliwapenda, walinishtaki, hata hivyo niliwaombea dua.

5 Wananilipa uovu kwa wema wangu, na chuki kwa mapendo yangu.

6 Umweke hakimu mbaya dhidi ya adui yangu; na mshtaki wake ampeleke mahakamani.

7 Anapohukumiwa apatikane na hatia; lalamiko lake lihesabiwe kuwa kosa jingine.

8 Siku za maisha yake ziwe chache, mtu mwingine na achukue kazi yake!

9 Watoto wake wawe yatima, na mke wake awe mjane!

10 Watoto wake watangetange na kuombaomba; wafukuzwe katika magofu ya nyumba zao!

11 Anayemdai kitu amnyanganye mali yake yote; na wageni wanyakue mapato ya jasho lake!

12 Pasiwe na mtu wa kumwonea huruma, au Kuwatunza watoto wake yatima!

13 Wazawa wake wote wafe; jina lake lisahauliwe katika kizazi kijacho!

14 Mwenyezi-Mungu aukumbuke uovu wa wazee wake, dhambi za mama yake zisifutwe kamwe!

15 Mwenyezi-Mungu azikumbuke dhambi zao daima; lakini wao wenyewe wasahauliwe duniani.

16 Mwovu huyo hakujali kabisa kuwa na huruma, ila aliwadhulumu maskini na fukara, kadhalika na watu wanyonge mpaka kifo.

17 Yeye alipenda kulaani watu, laana na impate yeye mwenyewe. Hakuwatakia wengine baraka, basi, asipate baraka yeye mwenyewe.

18 Kwake kulaani ni kama kuvaa nguo, basi, laana hizo zimloweshe kama maji, zimwingie mifupani mwake kama mafuta.

19 Laana zimfunike kama nguo, zimzunguke daima kama ukanda.

20 Mwenyezi-Mungu awalipe hayo hao watu wanaonishtaki, naam hao wanaosema mabaya dhidi yangu.

21 Lakini ee Mwenyezi-Mungu, Bwana wangu, unitendee kadiri ya hisani yako; uniokoe, kwa sababu ya wema wa fadhili zako!

22 Mimi ni maskini na fukara; nimejeruhiwa mpaka moyoni mwangu.

23 Natoweka kama kivuli cha jioni; nimepeperushwa kama nzige.

24 Magoti yangu yamenyongonyea kwa mfungo; nimebaki mifupa na ngozi.

25 Nimekuwa dhihaka tupu kwa watu; wanionapo hutikisa vichwa vyao kwa dharau.

26 Unisaidie, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu; uniokoe kadiri ya fadhili zako.

27 Waoneshe watu kuwa ndiwe uliyetenda hayo, wewe, ee Mwenyezi-Mungu, ndiwe uliyefanya hivyo.

28 Waache walaani, lakini wewe unibariki; wanaonishambulia waaibike, nami mtumishi wako nifurahi.

29 Maadui zangu na wavishwe fedheha; wajifunike aibu yao kama blanketi.

30 Nitamshukuru sana Mwenyezi-Mungu kwa sauti; nitamsifu kati ya kundi kubwa la watu,

31 kwa maana yeye humtetea maskini, humwokoa wakati anapohukumiwa.

110

1 Mwenyezi-Mungu amwambia bwana wangu: “Keti upande wangu wa kulia, hata niwaweke maadui zako chini ya miguu yako.”

2 Mwenyezi-Mungu ataeneza enzi yako kutoka Siyoni; utatawala juu ya maadui zako wote.

3 Watu wako watakujia kwa hiari, siku utakapokwenda kuwapiga maadui. Juu ya milima mitakatifu watakujia vijana wako, kama umande unaotokeza alfajiri mapema.

4 Mwenyezi-Mungu amekuapia wala hatabadili nia yake: “Wewe ni kuhani milele kwa utaratibu wa ukuhani wa Melkisedeki.”

5 Bwana yuko upande wako wa kulia; atawaponda wafalme atakapokasirika.

6 Atayahukumu mataifa na kuwaua watu wengi; atawaponda viongozi kila mahali duniani.

7 Mfalme atakunywa maji ya kijito njiani; naye atainua kichwa juu kwa ushindi.

111

1 Msifuni Mwenyezi-Mungu! Nitamshukuru Mwenyezi-Mungu kwa moyo wangu wote, nikijumuika na jamii ya watu waadilifu.

2 Matendo ya Mwenyezi-Mungu ni makuu mno! Wote wanaoyafurahia huyatafakari.

3 Kila afanyacho kimejaa utukufu na fahari; uadilifu wake wadumu milele.

4 Amesababisha matendo yake ya ajabu yakumbukwe; Mwenyezi-Mungu ni mwema na mwenye huruma.

5 Huwapa chakula wenye kumcha; hasahau kamwe agano lake.

6 Amewaonesha watu wake nguvu ya matendo yake, amewapa nchi za mataifa mengine ziwe mali yao.

7 Matendo yake ni ya haki na ya kuaminika; kanuni zake zote ni za kutegemewa.

8 Amri zake zadumu daima na milele; zimetolewa kwa haki na uadilifu.

9 Aliwakomboa watu wake na kufanya nao agano la milele. Yeye ni mtakatifu na wa kutisha mno!

10 Kumcha Mwenyezi-Mungu ni msingi wa hekima; wote wanaozitii amri zake hujaliwa busara. Sifa zake zadumu milele.

112

1 Msifuni Mwenyezi-Mungu! Heri mtu anayemcha Mwenyezi-Mungu, anayefurahia sana kutii amri zake.

2 Wazawa wake watakuwa wenye nguvu nchini; watoto wa wanyofu watapata baraka.

3 Nyumbani kwake kutakuwa na mali nyingi; uadilifu wake wadumu milele.

4 Mtu mwema huangaziwa mwanga gizani; mtu mwenye huruma, mpole na mwadilifu.

5 Mtu mkarimu akopeshaye bila faida, hufanikiwa; mtu afanyaye shughuli zake kwa kutumia haki.

6 Mwadilifu hatashindwa kamwe, huyo atakumbukwa milele.

7 Hana haja ya kuogopa akipata habari mbaya; ana moyo thabiti na humtegemea Mwenyezi-Mungu.

8 Yuko imara moyoni, wala hataogopa; naye atawaona maadui zake wanashindwa.

9 Hutoa kwa ukarimu, huwapa maskini; uadilifu wake wadumu milele. Nguvu yake inatukuzwa kwa heshima.

10 Watu waovu huona hayo na kuudhika; husaga meno kwa chuki na kutoweka, matazamio ya mtu mbaya huishia patupu.

113

1 Msifuni Mwenyezi-Mungu! Enyi watumishi wa Mwenyezi-Mungu, lisifuni jina lake!

2 Jina lake litukuzwe, sasa na hata milele.

3 Kutoka mashariki na hata magharibi, litukuzwe jina la Mwenyezi-Mungu!

4 Mwenyezi-Mungu atawala juu ya mataifa yote, utukufu wake wafika juu ya mbingu.

5 Nani aliye kama Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu? Yeye ameketi juu kabisa;

6 lakini anatazama chini, azione mbingu na dunia.

7 Humwinua fukara kutoka mavumbini; humnyanyua maskini kutoka unyonge wake,

8 na kumweka pamoja na wakuu; pamoja na wakuu wa watu wake.

9 Humjalia mwanamke tasa furaha nyumbani kwake; humfurahisha kwa kumjalia watoto. Msifuni Mwenyezi-Mungu!

114

1 Watu wa Israeli walipotoka Misri, wazawa wa Yakobo walipotoka ugenini,

2 Yuda ikawa maskani ya Mungu, Israeli ikawa milki yake.

3 Bahari iliona hayo ikakimbia; mto Yordani ukaacha kutiririka!

4 Milima ilirukaruka kama kondoo dume; vilima vikaruka kama wanakondoo!

5 Ee bahari, imekuwaje hata ukakimbia? Nawe Yordani, kwa nini ukaacha kutiririka?

6 Enyi milima, mbona mliruka kama kondoo dume? Nanyi vilima, mmerukaje kama wanakondoo?

7 Tetemeka, ee dunia mbele yake Mwenyezi-Mungu; tetemeka mbele ya Mungu wa Yakobo,

8 anayeugusa mwamba ukawa bwawa la maji, nayo majabali yakawa chemchemi za maji!

115

1 Sio sisi, ee Mwenyezi-Mungu, sio sisi; bali wewe peke yako utukuzwe, kwa ajili ya fadhili zako na uaminifu wako.

2 Kwa nini mataifa yaseme: “Mungu wenu yuko wapi?”

3 Mungu wetu yuko mbinguni; yeye hufanya yote anayotaka.

4 Miungu yao ni ya fedha na dhahabu; imetengenezwa kwa mikono ya wanadamu.

5 Ina vinywa, lakini haisemi. Ina macho, lakini haioni.

6 Ina masikio, lakini haisikii. Ina pua, lakini hainusi.

7 Ina mikono, lakini haipapasi. Ina miguu, lakini haitembei. Haiwezi kamwe kutoa sauti.

8 Wote wanaoitengeneza wanafanana nayo, kadhalika na wote wanaoitumainia.

9 Enyi Waisraeli, mtumainieni Mwenyezi-Mungu; yeye ndiye msaada wenu na ngao yenu.

10 Enyi wazawa wa Aroni, mtumainieni Mwenyezi-Mungu; yeye ndiye msaada wenu na ngao yenu.

11 Enyi mnaomcha Mwenyezi-Mungu, mtumainini, yeye ndiye msaada wenu na ngao yenu.

12 Mwenyezi-Mungu atukumbuka na atatubariki; atawabariki watu wa Israeli, atawabariki wazawa wa Aroni.

13 Atawabariki wote wamchao, atawabariki wakubwa na wadogo.

14 Mwenyezi-Mungu awajalieni muongezeke; awajalieni muongezeke nyinyi na wazawa wenu!

15 Mbarikiwe na Mwenyezi-Mungu, aliyeziumba mbingu na dunia.

16 Mbingu ni mali yake Mwenyezi-Mungu, bali dunia amewapa binadamu.

17 Wafu hawamsifu Mwenyezi-Mungu, wala wale wanaoshuka katika nchi ya kimya.

18 Lakini sisi tulio hai twamsifu Mwenyezi-Mungu; tutamsifu sasa na hata milele. Msifuni Mwenyezi-Mungu!

116

1 Nampenda Mwenyezi-Mungu, kwa maana anisikia, maana amesikia kilio cha ombi langu.

2 Yeye amenitegea sikio, hivyo nitamwomba muda wote niishio.

3 Hatari ya kifo ilinizunguka, vitisho vya kaburi vilinivamia; nilijawa na mahangaiko na majonzi.

4 Kisha nikamlilia Mwenyezi-Mungu: “Ee Mwenyezi-Mungu, tafadhali unisalimishe!”

5 Mwenyezi-Mungu amejaa wema na uaminifu; Mungu wetu ni mwenye huruma.

6 Mwenyezi-Mungu huwalinda wanyofu; nilipokuwa nimekandamizwa aliniokoa.

7 Uwe na utulivu mkuu, ee nafsi yangu, maana Mwenyezi-Mungu amenitendea mema.

8 Ameniokoa kifoni na kufuta machozi yangu; akanilinda nisije nikaanguka.

9 Nitatembea mbele yake Mwenyezi-Mungu, katika nchi ya watu walio hai.

10 Nilikuwa na imani hata niliposema: “Mimi nimetaabika mno.”

11 Hata nilisema kwa hofu yangu: “Binadamu wote hawaaminiki!”

12 Nimrudishie nini Mwenyezi-Mungu, kwa ukarimu wote alionitendea?

13 Nitamtolea tambiko ya divai kwa kunikomboa, nitaomba kwa jina lake Mwenyezi-Mungu.

14 Nitamtimizia Mwenyezi-Mungu nadhiri zangu, mbele ya watu wake wote.

15 Kifo cha waaminifu wake Mwenyezi-Mungu si jambo dogo mbele yake.

16 Ee Mwenyezi-Mungu, mimi ni mtumishi wako; ni mtumishi wako, mtoto wa mjakazi wako; umenifungulia vifungo vyangu.

17 Nitakutolea tambiko za shukrani, na kukupa heshima zangu.

18 Nitakutimizia ahadi zangu, ee Mwenyezi-Mungu mbele ya watu wako wote,

19 waliokusanyika hekaluni mwako, katikati ya Yerusalemu. Msifuni Mwenyezi-Mungu!

117

1 Enyi mataifa yote, msifuni Mwenyezi-Mungu! Enyi watu wote mhimidini!

2 Maana fadhili zake kwetu sisi ni kuu; uaminifu wake Mwenyezi-Mungu wadumu milele! Msifuni Mwenyezi-Mungu!

118

1 Mshukuruni Mwenyezi-Mungu, kwa kuwa ni mwema, kwa maana fadhili zake zadumu milele.

2 Watu wa Israeli na waseme: “Fadhili zake zadumu milele.”

3 Wazawa wa Aroni na waseme: “Fadhili zake zadumu milele.”

4 Wote wamchao Mwenyezi-Mungu na waseme: “Fadhili zake zadumu milele.”

5 Katika taabu yangu nilimwomba Mwenyezi-Mungu, naye akanisikia na kuniweka huru.

6 Mwenyezi-Mungu yuko nami, siogopi kitu; binadamu ataweza kunifanya nini?

7 Mwenyezi-Mungu yuko nami, kunisaidia; nami nitawaona maadui zangu wameshindwa.

8 Afadhali kukimbilia usalama kwa Mwenyezi-Mungu, kuliko kumtumainia mwanadamu.

9 Afadhali kukimbilia usalama kwa Mwenyezi-Mungu, kuliko kuwatumainia viongozi wa dunia.

10 Mataifa yote yalinizingira, lakini kwa jina la Mwenyezi-Mungu nikayaangamiza!

11 Yalinizunguka kila upande, lakini kwa jina la Mwenyezi-Mungu, nikayaangamiza!

12 Yalinizunguka, mengi kama nyuki, lakini yakateketea kama kichaka motoni; kwa jina la Mwenyezi-Mungu niliyaangamiza!

13 Nilishambuliwa mno karibu nishindwe, lakini Mwenyezi-Mungu alinisaidia.

14 Mwenyezi-Mungu ni nguvu yangu kuu; yeye mwenyewe ndiye wokovu wangu.

15 Sauti za furaha ya ushindi zasikika hemani mwao waadilifu: “Mkono wa Mwenyezi-Mungu umetenda mambo makuu!

16 Mkono wa nguvu wa Mwenyezi-Mungu umeleta ushindi! Mkono wa Mwenyezi-Mungu umetenda mambo makuu!”

17 Sitakufa, bali nitaishi, na kusimulia matendo ya Mwenyezi-Mungu.

18 Mwenyezi-Mungu ameniadhibu sana, lakini hakuniacha nife.

19 Nifungulie milango ya watu waadilifu, niingie na kumshukuru Mwenyezi-Mungu!

20 Huu ndio mlango wa Mwenyezi-Mungu, watu waadilifu watapitia humo.

21 Nakushukuru, ee Mungu kwa kunijibu; kwa sababu wewe ni wokovu wangu.

22 Jiwe walilokataa waashi, limekuwa jiwe kuu la msingi.

23 Hiyo ni kazi yake Mwenyezi-Mungu nayo ni ya ajabu sana kwetu.

24 Hii ndiyo siku aliyoifanya Mwenyezi-Mungu; tushangilie na kufurahi.

25 Tafadhali utuokoe, ee Mwenyezi-Mungu! Tafadhali utufanikishe, ee Mwenyezi-Mungu!

26 Abarikiwe huyo ajaye kwa jina la Mwenyezi-Mungu! Twawabariki kutoka nyumbani mwa Mwenyezi-Mungu

27 Mwenyezi-Mungu ni Mungu; yeye ametujalia mwanga wake Shikeni matawi ya sherehe, mkiandamana mpaka madhabahuni.

28 Wewe ni Mungu wangu, nami ninakushukuru; ninakutukuza, ee Mungu wangu.

29 Mshukuruni Mwenyezi-Mungu kwa kuwa ni mwema, kwa maana fadhili zake zadumu milele.

119

1 Heri watu wanaoishi bila kosa, wanaozingatia sheria ya Mwenyezi-Mungu.

2 Heri wanaozingatia matakwa yake, wanaomtafuta kwa moyo wao wote,

3 watu wasiotenda uovu kamwe, bali daima hufuata njia zake.

4 Ee Mungu, umetupatia kanuni zako ili tuzishike kwa uaminifu.

5 Laiti mwenendo wangu ungeimarika, kwa kuyafuata masharti yako!

6 Nikizingatia amri zako zote, hapo kweli sitaaibishwa.

7 Nitakusifu kwa moyo mnyofu, nikijifunza maagizo yako maadilifu.

8 Nitayafuata masharti yako; usiniache hata kidogo.

9 Kijana atatunzaje maisha yake kuwa safi? Kwa kuyaongoza kadiri ya neno lako.

10 Najitahidi kukutii kwa moyo wote; usiniache nikiuke amri zako.

11 Nimeshika neno lako moyoni mwangu, nisije nikakukosea.

12 Utukuzwe, ee Mwenyezi-Mungu! Unifundishe masharti yako.

13 Nitayarudia kwa sauti maagizo yako yote uliyotoa.

14 Nafurahi kufuata maamuzi yako, kuliko kuwa na utajiri mwingi.

15 Nazitafakari kanuni zako, na kuzizingatia njia zako.

16 Nayafurahia masharti yako; sitalisahau neno lako.

17 Unitendee mimi mtumishi wako kwa ukarimu, nipate kuishi na kushika neno lako.

18 Uyafumbue macho yangu, niyaone maajabu ya sheria yako.

19 Mimi ni mkimbizi tu hapa duniani; usinifiche amri zako.

20 Roho yangu yaugua kwa hamu kubwa ya kutaka kujua daima maagizo yako.

21 Wewe wawakemea wenye kiburi, walaanifu, ambao wanakiuka amri zako.

22 Uniepushe na matusi na madharau yao, maana nimeyazingatia maamuzi yako.

23 Hata kama wakuu wanakula njama dhidi yangu; mimi mtumishi wako nitayatafakari maamuzi yako.

24 Masharti yako ni furaha yangu; hayo ni washauri wangu.

25 Nagaagaa chini mavumbini; unipe tena uhai kama ulivyoahidi.

26 Nimeungama niliyotenda, nawe ukanijibu; unifundishe masharti yako.

27 Unifundishe namna ya kushika kanuni zako, nami nitayatafakari matendo yako ya ajabu.

28 Niko hoi kwa uchungu; unirudishie nguvu kama ulivyoahidi.

29 Uniepushe na njia za upotovu; unifundishe kwa wema sheria yako.

30 Nimechagua njia ya uaminifu; nimezingatia maagizo yako.

31 Nazingatia maamuzi yako, ee Mwenyezi-Mungu; usikubali niaibishwe!

32 Nitafuata maelekezo ya amri zako, maana unanipa maarifa zaidi.

33 Ee Mwenyezi-Mungu, unifundishe kutii masharti yako; nami nitayashika mpaka mwisho.

34 Unieleweshe nipate kuishika sheria yako, niifuate kwa moyo wangu wote.

35 Uniongoze katika njia ya amri zako, maana humo napata furaha yangu.

36 Unipe ari ya kuzingatia maamuzi yako, na si kwa ajili ya kupata faida isiyofaa.

37 Uniepushe, nisifuate mambo ya upuuzi; unioneshe njia yako, unipe uhai.

38 Unitimizie mimi mtumishi wako ahadi yako; ahadi unayowapa wale wanaokuheshimu.

39 Uniokoe na lawama ninazoogopa; maana maagizo yako ni mema.

40 Natamani sana kuzitii kanuni zako; unijalie uhai maana wewe ni mwadilifu.

41 Fadhili zako zinijie, ee Mwenyezi-Mungu; uniokoe kama ulivyoahidi.

42 Hapo nitaweza kuwajibu hao wanaonitukana, maana mimi nina imani sana na neno lako.

43 Unijalie kusema ukweli wako daima, maana tumaini langu liko katika maagizo yako.

44 Nitatii sheria yako daima, nitaishika milele na milele.

45 Nitaishi katika uhuru kamili, maana nazitilia maanani kanuni zako.

46 Nitawatangazia wafalme maamuzi yako, wala sitaona aibu.

47 Furaha yangu ni kuzitii amri zako, ambazo mimi nazipenda.

48 Naziheshimu na kuzipenda amri zako; nitayatafakari masharti yako.

49 Ukumbuke ahadi yako kwangu mimi mtumishi wako, ahadi ambayo imenipa matumaini.

50 Hata niwapo taabuni napata kitulizo, maana ahadi yako yanipa uhai.

51 Wasiomjali Mungu hunidharau daima, lakini mimi sikiuki sheria yako.

52 Ninapoyakumbuka maagizo yako ya tangu kale, nafarijika, ee Mwenyezi-Mungu.

53 Nashikwa na hasira kali, nionapo waovu wakivunja sheria yako.

54 Masharti yako yamekuwa wimbo wangu, nikiwa huku ugenini.

55 Usiku ninakukumbuka, ee Mwenyezi-Mungu, na kushika sheria yako.

56 Hii ni baraka kubwa kwangu, kwamba nazishika kanuni zako.

57 Wewe, ee Mwenyezi-Mungu, ndiwe riziki yangu kuu; naahidi kushika maneno yako.

58 Naomba radhi yako kwa moyo wangu wote; unionee huruma kama ulivyoahidi!

59 Nimeufikiria mwenendo wangu, na nimerudi nifuate maamuzi yako.

60 Bila kukawia nafanya haraka kuzishika amri zako.

61 Waovu wametega mitego waninase, lakini mimi sisahau sheria yako.

62 Usiku wa manane naamka kukusifu, kwa sababu ya maagizo yako maadilifu.

63 Mimi ni rafiki ya wote wakuchao, rafiki yao wanaozitii kanuni zako.

64 Dunia imejaa fadhili zako, ee Mwenyezi-Mungu, unifundishe masharti yako.

65 Umenitendea vema mimi mtumishi wako, kama ulivyoahidi, ee Mwenyezi-Mungu.

66 Unifundishe akili na maarifa, maana nina imani sana na amri zako.

67 Kabla ya kuniadhibu nilikuwa nikikosea, lakini sasa nashika neno lako.

68 Wewe ni mwema na mfadhili; unifundishe masharti yako.

69 Wenye kiburi wanasema uongo juu yangu, lakini mimi nashika kanuni zako kwa moyo wote.

70 Mioyo yao imejaa upumbavu, lakini mimi nafurahia sheria yako.

71 Nimefaidika kutokana na taabu yangu, maana imenifanya nijifunze masharti yako.

72 Sheria uliyoweka ni bora kwangu, kuliko mali zote za dunia.

73 Mikono yako iliniumba na kuniunda; unijalie akili nijifunze amri zako.

74 Wakuchao wataniona na kufurahi, maana tumaini langu liko katika neno lako.

75 Najua hukumu zako ni adili, ee Mwenyezi-Mungu, na kwamba umeniadhibu kwani wewe ni mwaminifu.

76 Fadhili zako na zinipe faraja, kama ulivyoniahidi mimi mtumishi wako.

77 Unionee huruma nipate kuishi, maana sheria yako ni furaha yangu.

78 Wenye kiburi waaibike kwa maana wamenifanyia hila, lakini mimi nitazitafakari kanuni zako.

79 Wote wakuchao na waje kwangu, wapate kuyajua maamuzi yako.

80 Moyo wangu na uzingatie masharti yako, nisije nikaaibishwa.

81 Niko hoi kwa kukungojea uniokoe; naweka tumaini langu katika neno lako.

82 Macho yangu yanafifia nikingojea ulichoahidi. Nauliza: “Utakuja lini kunifariji?”

83 Nimekunjamana kama kiriba katika moshi, hata hivyo sijasahau masharti yako.

84 Mimi mtumishi wako nitasubiri mpaka lini? Utawaadhibu lini wale wanaonidhulumu?

85 Wenye kiburi wamenichimbia mashimo, watu ambao hawafuati sheria yako.

86 Amri zako zote ni za kuaminika; watu wananitesa bila haki; unisaidie!

87 Karibu wangefaulu kuniangamiza, lakini mimi sijavunja kanuni zako.

88 Unisalimishe kadiri ya fadhili zako, nipate kuzingatia maamuzi uliyotamka.

89 Neno lako, ee Mwenyezi-Mungu, ladumu milele; limethibitika juu mbinguni.

90 Uaminifu wako wadumu vizazi vyote, umeiweka dunia mahali pake nayo yadumu.

91 Kwa amri yako viumbe vyote vipo leo, maana vitu vyote ni watumishi wako.

92 Kama sheria yako isingekuwa furaha yangu, ningalikwisha angamia kwa taabu zangu.

93 Sitasahau kamwe kanuni zako, maana kwa hizo umenipa uhai.

94 Mimi ni wako, uniokoe, maana nimejitahidi kuzishika kanuni zako.

95 Waovu wanivizia wapate kuniua; lakini mimi natafakari masharti yako.

96 Nimetambua kila kitu hufikia kikomo, lakini amri yako ni kamilifu.

97 Naipenda sana sheria yako! Naitafakari mchana kutwa!

98 Amri yako iko nami daima, yanipa hekima kuliko maadui zangu.

99 Ninaelewa kuliko waalimu wangu wote, kwa kuwa nayatafakari maamuzi yako.

100 Nawapita wazee kwa busara yangu, kwa sababu nazishika kanuni zako.

101 Najizuia nisifuate njia mbaya, nipate kulizingatia neno lako.

102 Sikukiuka maagizo yako, maana wewe mwenyewe ulinifundisha.

103 Maneno yako ni matamu sana kwangu; naam, ni matamu kuliko asali!

104 Kwa kanuni zako napata hekima, kwa hiyo nachukia kila mwenendo mbaya.

105 Neno lako ni taa ya kuniongoza, na mwanga katika njia yangu.

106 Nimeapa na kuthibitisha kiapo changu, kwamba nitashika maagizo yako adili.

107 Ee Mwenyezi-Mungu, ninateseka mno; unijalie uhai kama ulivyoahidi.

108 Ee Mwenyezi-Mungu, upokee sala yangu ya shukrani; na kunifundisha maagizo yako.

109 Maisha yangu yamo hatarini daima, lakini siisahau sheria yako.

110 Waovu wamenitegea mitego, lakini sikiuki kanuni zako.

111 Maamuzi yako ni riziki kubwa kwangu milele; hayo ni furaha ya moyo wangu.

112 Nimekusudia kwa moyo wote kufuata masharti yako milele.

113 Nawachukia watu wanafiki, lakini naipenda sheria yako.

114 Wewe ni ngao yangu, kwako napata usalama; naweka tumaini langu katika neno lako.

115 Ondokeni kwangu, enyi waovu, ili nipate kushika amri za Mungu wangu.

116 Uniimarishe ulivyoahidi, nami nitaishi; usikubali niaibike katika tumaini langu.

117 Unitegemeze, niwe salama; niwe daima msikivu kwa masharti yako.

118 Unawakataa wote wanaokiuka masharti yako; mawazo yao maovu ni ya bure.

119 Waovu wote wawaona kuwa takataka, kwa hiyo mimi napenda maamuzi yako.

120 Natetemeka kwa kukuogopa wewe; nimejaa hofu kwa sababu ya hukumu zako.

121 Nimefanya mambo mema na adili; usiniache makuchani mwa maadui zangu.

122 Uahidi kunisaidia mimi mtumishi wako; usikubali wenye kiburi wanidhulumu.

123 Macho yangu yanafifia nikingojea uniokoe, nikingojea utimize uliyoahidi.

124 Unitendee mimi mtumishi wako kadiri ya wema wako, unifundishe masharti yako.

125 Mimi ni mtumishi wako, unipe maarifa, nipate kujua maamuzi yako.

126 Ee Mwenyezi-Mungu, sasa ni wakati wa kufanya kitu, kwa maana watu wanavunja sheria yako.

127 Mimi, nazipenda amri zako, kuliko hata dhahabu safi kabisa.

128 Kwa hiyo, nafuata kanuni zako zote; kila njia potovu naichukia.

129 Maamuzi yako ni ya ajabu; kwa hiyo nayashika kwa moyo wote.

130 Maelezo ya mafundisho yako huleta mwanga; huwapa akili watu wasiojua kitu.

131 Nafungua kinywa kwa hamu kubwa, maana ninatamani sana amri zako.

132 Unigeukie na kunionea huruma, kama uwatendeavyo wanaokupenda.

133 Uniimarishie hatua zangu kama ulivyoahidi; usikubali mimi nitawaliwe na uovu.

134 Unikomboe kutoka udhalimu wa binadamu, ili nipate kuzishika kanuni zako.

135 Uniangazie uso wako kwa wema, unifundishe masharti yako.

136 Macho yangu yabubujika machozi kama mto, kwa sababu watu hawaishiki sheria yako.

137 Ee Mwenyezi-Mungu, wewe ni mwadilifu; na hukumu zako ni za haki.

138 Umetoa maamuzi yako, kwa haki na uthabiti.

139 Upendo wangu kwako wanifanya niwake hasira, maana maadui zangu hawajali maneno yako.

140 Ahadi yako ni hakika kabisa, nami mtumishi wako naipenda.

141 Mimi ni mdogo na ninadharauliwa; hata hivyo sisahau kanuni zako.

142 Uadilifu wako ni wa haki milele; sheria yako ni ya kweli.

143 Taabu na huzuni vimenipata, lakini amri zako ndizo furaha yangu.

144 Maamuzi yako ni ya haki daima; unijalie maarifa nipate kuishi.

145 Nakulilia kwa moyo wangu wote; unijibu, ee Mwenyezi-Mungu, nifuate kanuni zako.

146 Nakulilia, unisalimishe; nipate kuyazingatia maamuzi yako.

147 Naamka kabla ya pambazuko na kukuomba msaada; naweka tumaini langu katika maneno yako.

148 Nakaa macho usiku kucha, ili nitafakari juu ya maagizo yako.

149 Kwa fadhili zako, ee Mwenyezi-Mungu, unisikie; unisalimishe kwa uadilifu wako.

150 Wale wanaonidhulumu vibaya wanakaribia, hao wako mbali kabisa na sheria yako.

151 Lakini wewe u karibu nami, ee Mwenyezi-Mungu, na amri zako zote ni za kuaminika.

152 Tangu zamani, nimejifunza maamuzi yako; ambayo umeyaweka hata yadumu milele.

153 Uangalie mateso yangu, uniokoe, kwa maana sikuisahau sheria yako.

154 Unitetee na kunikomboa; unijalie uhai kama ulivyoahidi.

155 Waovu hawataokolewa kamwe, maana hawajali juu ya masharti yako.

156 Huruma yako ni kubwa, ee Mwenyezi-Mungu, unijalie uhai kama ulivyoahidi.

157 Maadui na wadhalimu wangu ni wengi, lakini mimi sikiuki maamuzi yako.

158 Niwaonapo wahaini hao nachukizwa mno, kwa sababu hawazishiki amri zako.

159 Tazama, ee Mungu, ninavyozipenda kanuni zako! Unijalie uhai kadiri ya fadhili zako.

160 Kitovu cha neno lako ni ukweli, maagizo yako yote adili, yadumu milele.

161 Wakuu wanidhulumu bila kisa, lakini mimi naheshimu maneno yako kwa moyo wote.

162 Nafurahi kwa sababu ya neno lako, kama mtu aliyekuta kitu cha thamani kuu.

163 Nachukia kabisa uongo, lakini naipenda sheria yako.

164 Nakusifu mara saba kila siku, kwa sababu ya maagizo yako adili.

165 Wapendao sheria yako wana amani kuu; hakuna kinachoweza kuwaangusha.

166 Ee Mwenyezi-Mungu, nakungojea uniokoe; mimi natimiza amri zako.

167 Nazingatia maamuzi yako; nayapenda kwa moyo wote.

168 Nazingatia kanuni na maamuzi yako; wewe wauona mwenendo wangu wote.

169 Kilio changu kikufikie, ee Mwenyezi-Mungu! Unijalie akili kama ulivyoahidi.

170 Ombi langu likufikie; uniokoe kama ulivyoahidi.

171 Nitasema sifa zako mfululizo, maana wanifundisha masharti yako.

172 Nitaimba juu ya neno lako, maana amri zako zote ni za haki.

173 Uwe daima tayari kunisaidia, maana nimeamua kufuata kanuni zako.

174 Natazamia sana uniokoe, ee Mwenyezi-Mungu; sheria yako ndiyo furaha yangu.

175 Unijalie kuishi nipate kukusifu; na maagizo yako yanisaidie.

176 Natangatanga kama kondoo aliyepotea; uje kunitafuta mimi mtumishi wako, maana sikusahau amri zako.

120

1 Katika taabu yangu nilimwita Mwenyezi-Mungu, naye akanijibu.

2 Uniokoe ee Mwenyezi-Mungu, na watu wadanganyifu na waongo.

3 Enyi watu wadanganyifu, mtapewa kitu gani? Mtaadhibiwa namna gani?

4 Kwa mishale mikali ya askari, kwa makaa ya moto mkali!

5 Ole wangu kwamba naishi kama mgeni huko Mesheki; naishi kama mgeni katika mahema ya Kedari.

6 Nimeishi muda mrefu mno kati ya watu wanaochukia amani!

7 Wakati ninaposema nataka amani, wao wanataka tu vita.

121

1 Natazama juu milimani; msaada wangu utatoka wapi?

2 Msaada wangu watoka kwa Mwenyezi-Mungu, aliyeumba mbingu na dunia.

3 Hatakuacha uanguke; mlinzi wako hasinzii.

4 Kweli mlinzi wa Israeli hasinzii wala halali.

5 Mwenyezi-Mungu ni mlinzi wako; yuko upande wako wa kulia kukukinga.

6 Mchana jua halitakuumiza, wala mwezi wakati wa usiku.

7 Mwenyezi-Mungu atakukinga na baya lolote; atayalinda salama maisha yako.

8 Mwenyezi-Mungu atakulinda katika shughuli zako zote tangu sasa na hata milele.

122

1 Nilifurahi waliponiambia: “Twende nyumbani kwa Mwenyezi-Mungu.”

2 Sasa tuko tumesimama, kwenye malango yako, ee Yerusalemu!

3 Yerusalemu, mji uliojengwa, ili jumuiya ikutane humo.

4 Humo ndimo makabila yanamofika, naam, makabila ya Israeli, kumshukuru Mwenyezi-Mungu kama alivyoagiza.

5 Humo mmewekwa mahakama ya hukumu ya haki, mahakama ya ukoo wa kifalme wa Daudi.

6 Uombeeni Yerusalemu amani: “Wote wakupendao na wafanikiwe!

7 Ndani ya kuta zako kuwe na amani, majumbani mwako kuweko usalama!”

8 Kwa ajili ya jamaa na ndugu zangu, ee Yerusalemu, nakutakia amani!

9 Kwa ajili ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, ninakuombea upate fanaka!

123

1 Nakutazamia kwa hamu, ee Mwenyezi-Mungu, nakuangalia wewe utawalaye huko juu mbinguni!

2 Kama watumishi wamtegemeavyo bwana wao, kama mjakazi amtegemeavyo bibi yake, ndivyo nasi tunavyokutegemea wewe, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, mpaka hapo utakapotuonea huruma.

3 Utuhurumie, ee Mwenyezi-Mungu, utuhurumie, maana tumedharauliwa kupita kiasi.

4 Tumeshiba muda mrefu dharau za matajiri, tumepuuzwa mno na wenye kiburi.

124

1 “Kama Mwenyezi-Mungu asingalikuwa upande wetu Semeni nyote mlio katika Israeli:

2 “Kama Mwenyezi-Mungu asingalikuwa upande wetu, wakati ule tuliposhambuliwa na maadui,

3 hakika tungalimezwa tukiwa hai, wakati hasira zao zilipotuwakia.

4 Tungalikumbwa na gharika, tungalifunikwa na mto wa maji,

5 mkondo wa maji ungalituchukua!”

6 Atukuzwe Mwenyezi-Mungu, ambaye hakutuacha makuchani mwao.

7 Tumeponyoka kama ndege mtegoni; mtego umeteguliwa, nasi tukaokoka.

8 Msaada wetu watoka kwa Mwenyezi-Mungu, aliyeumba mbingu na dunia.

125

1 Wanaomtegemea Mwenyezi-Mungu, wako kama mlima Siyoni, ambao hautikisiki bali wabaki imara daima.

2 Kama Yerusalemu inavyozungukwa na milima, ndivyo Mwenyezi-Mungu awazungukavyo watu wake, tangu sasa na hata milele.

3 Waovu hawataendelea kutawala nchi ya waadilifu; wasije waadilifu nao wakafanya maovu.

4 Ee Mwenyezi-Mungu, uwe mwema kwa watu wema, kwa wale wanaozitii amri zako.

5 Lakini wanaogeuka na kufuata njia zao mbaya uwakumbe pamoja na watenda maovu. Amani iwe na Israeli!

126

1 Mwenyezi-Mungu alipoturekebisha na kuturudisha Siyoni, tulikuwa kama watu wanaoota ndoto!

2 Hapo tuliangua kicheko; tulishangilia kwa furaha. Nao watu wa mataifa mengine walisema: “Mwenyezi-Mungu amewatendea mambo makubwa!”

3 Kweli Mwenyezi-Mungu alitutendea mambo makubwa, tulifurahi kwelikweli!

4 Ee Mwenyezi-Mungu, urekebishe tena hali yetu, kama mvua inavyotiririsha maji katika mabonde makavu.

5 Wanaopanda kwa machozi, watavuna kwa shangwe.

6 Wanaokwenda kupanda mbegu wakilia, watarudi kwa furaha wakichukua mavuno.

127

1 Mwenyezi-Mungu asipoijenga nyumba, waijengao wanajisumbua bure. Mwenyezi-Mungu asipoulinda mji, waulindao wanakesha bure.

2 Mnajisumbua bure kuamka mapema asubuhi na kuchelewa kwenda kupumzika jioni, mjipatie chakula kwa jasho lenu. Mungu huwaruzuku walio wake hata walalapo.

3 Watoto ni riziki kutoka kwa Mwenyezi-Mungu; watoto ni tuzo lake kwetu sisi.

4 Watoto waliozaliwa wazazi wakiwa bado vijana, ni kama mishale mikononi mwa askari.

5 Heri mtu aliye na mishale hiyo kwa wingi. Hatashindwa atakapokabiliana na adui mahakamani.

128

1 Heri wote wamchao Mwenyezi-Mungu, wanaoishi kufuatana na amri zake.

2 Utapata matunda ya jasho lako, utafurahi na kupata fanaka.

3 Mkeo atakuwa kama mzabibu wa matunda mengi nyumbani mwako; watoto wako kama chipukizi za mzeituni kuzunguka meza yako.

4 Naam, ndivyo atakavyobarikiwa mtu amchaye Mwenyezi-Mungu.

5 Mwenyezi-Mungu akubariki kutoka Siyoni! Uione fanaka ya Yerusalemu, siku zote za maisha yako.

6 Uishi na hata uwaone wajukuu zako! Amani iwe na Israeli!

129

1 “Nimesumbuliwa vibaya tangu ujana wangu Kila mtu katika Israeli na aseme:

2 “Nimesumbuliwa vibaya tangu ujana wangu, lakini hawakufaulu kunishinda.

3 Walinijeruhi vibaya mgongoni mwangu, wakafanya kama mkulima anayelima shamba.

4 Lakini Mwenyezi-Mungu ni mwadilifu; amezikata kamba za hao watu waovu.”

5 Na waaibishwe na kurudishwa nyuma, wote wale wanaouchukia mji wa Siyoni.

6 Wawe kama nyasi juu ya paa la nyumba, ambazo hunyauka kabla hazijakua,

7 hakuna anayejishughulisha kuzikusanya, wala kuzichukua kama matita.

8 Hakuna apitaye karibu atakayewaambia: “Mwenyezi-Mungu awabariki! Twawabariki kwa jina la Mwenyezi-Mungu!”

130

1 Toka upeo wa unyonge wangu, nakulilia, ee Mwenyezi-Mungu.

2 Ee Bwana, sikia sauti yangu, uitegee sikio sauti ya ombi langu.

3 Kama, ee Mwenyezi-Mungu ungekumbuka maovu yetu nani, ee Bwana, angeweza kusalimika?

4 Lakini kwako twapata msamaha, ili sisi tukuheshimu.

5 Namtumainia Mwenyezi-Mungu kwa moyo wangu wote; nina imani sana na neno lake.

6 Ninamtumainia Mwenyezi-Mungu kuliko walinzi wanavyongojea pambazuko; kuliko walinzi wanavyongojea kuche asubuhi.

7 Ee Israeli, umtumainie Mwenyezi-Mungu, maana kwake Mwenyezi-Mungu kuna fadhili, kwake kuna nguvu kubwa ya kutukomboa.

8 Yeye atawakomboa watu wa Israeli kutoka katika maovu yao yote.

131

1 Ee Mwenyezi-Mungu, sina moyo wa kiburi; mimi si mtu wa majivuno. Sijishughulishi na mambo makuu, au yaliyo ya ajabu mno kwangu.

2 Ila nafsi yangu imetulia na kuwa na amani, kama mtoto mchanga alivyotulia na mama yake; ndivyo nafsi yangu ilivyo tulivu.

3 Ee Israeli, umtumainie Mwenyezi-Mungu, tangu sasa na hata milele.

132

1 Ee Mwenyezi-Mungu, mkumbuke Daudi, kumbuka taabu zote alizopata.

2 Ukumbuke ahadi aliyokupa, ee Mwenyezi-Mungu, kiapo alichokuapia, ewe Mwenye Nguvu wa Yakobo:

3 “Sitaingia ndani ya nyumba yangu, wala kulala kitandani mwangu;

4 sitakubali kulala usingizi, wala kusinzia;

5 mpaka nikupatie wewe Mwenyezi-Mungu mahali pa kukaa, makao yako, ewe Mwenye Nguvu wa Yakobo!”

6 Huko Efratha tulisikia habari za sanduku la agano, tukalikuta katika mashamba ya Yearimu.

7 “Haya! Twende nyumbani kwa Mungu, tuabudu mbele ya kiti chake cha enzi!”

8 Inuka ee Mwenyezi-Mungu, nenda kwenye maskani yako; inuka pamoja na sanduku la agano la uwezo wako!

9 Makuhani wako wawe waadilifu daima; na waaminifu wako wapige vigelegele vya furaha!

10 Kwa ajili ya Daudi, mtumishi wako, usimkatae huyo mfalme uliyemweka wakfu.

11 Mwenyezi-Mungu alimwapia Daudi kiapo thabiti, kiapo ambacho hatakibatilisha: “Nitamtawaza mmoja wa wazawa wako mwenyewe, kuwa mfalme baada yako.

12 Watoto wako wakishika agano langu, na kuzingatia mafundisho nitakayowapa, watoto wao pia watakuwa wafalme kama wewe.”

13 Mwenyezi-Mungu ameuchagua mji wa Siyoni, ametaka uwe makao yake:

14 “Hapa ndipo nitakapokaa milele, ndipo maskani yangu maana nimepachagua.

15 Nitaubariki sana mji wa Siyoni kwa mahitaji yake; nitawashibisha chakula maskini wake.

16 Nitawafanikisha makuhani wake kwa wokovu; waaminifu wake watapiga vigelegele vya furaha.

17 Humo nitamchipusha mfalme shujaa wa ukoo wa Daudi: Kama taa iwakayo nitamtegemeza mfalme niliyemteua.

18 Maadui zake nitawavika aibu; lakini yeye nitamvika fahari ya kifalme.”

133

1 Ni jambo zuri na la kupendeza sana ndugu kuishi pamoja kwa umoja.

2 Ni kama mafuta mazuri yatiririkayo kichwani, mpaka kwenye ndevu zake Aroni, mpaka upindoni mwa vazi lake shingoni.

3 Ni kama umande wa mlima Hermoni, uangukao juu ya vilima vya Siyoni! Huko Mwenyezi-Mungu ameahidi kuwabariki watu wake, kuwapa uhai usio na mwisho.

134

1 Njoni kumsifu Mwenyezi-Mungu enyi watumishi wake wote, enyi nyote mnaotumikia usiku nyumbani mwake.

2 Inueni mikono kuelekea mahali patakatifu, na kumtukuza Mwenyezi-Mungu!

3 Mwenyezi-Mungu awabariki kutoka Siyoni; yeye aliyeumba mbingu na dunia.

135

1 Msifuni Mwenyezi-Mungu! Lisifuni jina la Mwenyezi-Mungu, msifuni enyi watumishi wake.

2 Msifuni enyi mkaao katika nyumba yake, ukumbini mwa nyumba ya Mungu wetu!

3 Msifuni Mwenyezi-Mungu kwa kuwa ni mwema; mtukuzeni kwa nyimbo maana inafaa.

4 Mwenyezi-Mungu amemchagua Yakobo kuwa wake, nyinyi watu wa Israeli kuwa mali yake mwenyewe.

5 Najua hakika kuwa Mwenyezi-Mungu ni mkuu; Bwana wetu ni mkuu juu ya miungu yote.

6 Mwenyezi-Mungu hufanya chochote anachotaka, mbinguni, duniani, baharini na vilindini.

7 Ndiye aletaye mawingu kutoka mipaka ya dunia; afanyaye gharika kuu kwa umeme, na kuvumisha upepo kutoka ghala zake.

8 Ndiye aliyewaua wazaliwa wa kwanza huko Misri, wazaliwa wa watu na wanyama kadhalika.

9 Ndiye aliyefanya ishara na maajabu kwako, ee Misri, dhidi ya Farao na maofisa wake wote.

10 Ndiye aliyeyaangamiza mataifa mengi, akawaua wafalme wenye nguvu:

11 Kina Sihoni mfalme wa Waamori, Ogu mfalme wa Bashani, na wafalme wote wa Kanaani.

12 Alichukua nchi zao na kuwapa watu wake; naam, ziwe riziki ya watu wake Israeli.

13 Jina lako, ee Mwenyezi-Mungu, ladumu milele, utakumbukwa kwa fahari nyakati zote.

14 Mwenyezi-Mungu atawatetea watu wake; na kuwaonea huruma watumishi wake.

15 Miungu ya uongo ya mataifa ni fedha na dhahabu, imetengenezwa kwa mikono ya binadamu.

16 Ina vinywa, lakini haisemi; ina macho, lakini haioni.

17 Ina masikio, lakini haisikii; wala haiwezi hata kuvuta pumzi.

18 Wote walioifanya wafanane nayo, naam, kila mmoja anayeitegemea!

19 Enyi watu wa Israeli, mtukuzeni Mwenyezi-Mungu! Enyi makuhani, mtukuzeni Mwenyezi-Mungu!

20 Enyi Walawi, mtukuzeni Mwenyezi-Mungu! Enyi wachaji wa Mwenyezi-Mungu, mtukuzeni!

21 Atukuzwe Mwenyezi-Mungu katika Siyoni, atukuzwe katika makao yake Yerusalemu. Msifuni Mwenyezi-Mungu!

136

1 Mshukuruni Mwenyezi-Mungu kwa kuwa ni mwema; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

2 Mshukuruni Mungu wa miungu; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

3 Mshukuruni Bwana wa mabwana; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

4 Ndiye peke yake atendaye makuu ya ajabu; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

5 Ndiye aliyeziumba mbingu kwa hekima; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

6 Ndiye aliyeitengeneza nchi juu ya vilindi vya maji; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

7 Ndiye aliyeumba jua, mwezi na nyota; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

8 Jua liutawale mchana; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

9 Mwezi na nyota vitawale usiku; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

10 Ndiye aliyewaua wazaliwa wa kwanza wa Misri; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

11 Akawaondoa watu wa Israeli kutoka huko; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

12 Kwa mkono wake wenye nguvu na enzi; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

13 Ndiye aliyeigawa Bahari ya Shamu sehemu mbili; kwa maana fadhili zake zadumu milele,

14 akawapitisha watu wa Israeli humo; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

15 Lakini akawazamisha humo Farao na jeshi lake; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

16 Ndiye aliyewaongoza watu wake jangwani; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

17 Ndiye aliyewapiga wafalme wenye nguvu; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

18 Akawaua wafalme maarufu; kwa maana fadhili zake zadumu milele;

19 akamuua Sihoni, mfalme wa Waamori, kwa maana fadhili zake zadumu milele;

20 na Ogu, mfalme wa Bashani; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

21 Akachukua nchi zao akawapa watu wake; kwa maana fadhili zake zadumu milele;

22 ziwe riziki ya Israeli, mtumishi wake; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

23 Ndiye aliyetukumbuka wakati wa unyonge wetu; kwa maana fadhili zake zadumu milele;

24 akatuokoa kutoka maadui zetu; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

25 Ndiye akipaye kila kiumbe chenye uhai chakula; kwa maana fadhili zake zadumu milele.

26 Mshukuruni Mungu wa mbinguni; kwa maana fadhili zake zadumu milele!

137

1 Kando ya mito ya Babuloni, tulikaa, tukawa tunalia tulipokumbuka Siyoni.

2 Katika miti ya nchi ile, tulitundika zeze zetu.

3 Waliotuteka walitutaka tuwaimbie; watesi wetu walitutaka tuwafurahishe: “Tuimbieni mojawapo ya nyimbo za Siyoni!”

4 Twawezaje kuimba wimbo wa Mwenyezi-Mungu katika nchi ya kigeni?

5 Ee Yerusalemu, kama nikikusahau, mkono wangu wa kulia na ukauke!

6 Ulimi wangu na uwe mzito, kama nisipokukumbuka wewe, ee Yerusalemu; naam, nisipokuthamini kuliko furaha yangu kubwa!

7 Ee Mwenyezi-Mungu, usisahau waliyotenda Waedomu, siku ile Yerusalemu ilipotekwa; kumbuka waliyosema: “Bomoeni mji wa Yerusalemu! Ngoeni hata na misingi yake!”

8 Ee Babuloni, utaangamizwa! Heri yule atakayekulipiza mabaya uliyotutenda!

9 Heri yule atakayewatwaa watoto wako na kuwapondaponda mwambani!

138

1 Nakushukuru, ee Mwenyezi-Mungu, kwa moyo wangu wote, naimba sifa zako mbele ya miungu.

2 Ninasujudu kuelekea hekalu lako takatifu; nalisifu jina lako, kwa sababu ya fadhili zako na uaminifu wako; kwa sababu umeweka jina lako na neno lako juu ya kila kitu.

3 Nilipokulilia, wewe ulinijibu; umeniongezea nguvu zangu.

4 Wafalme wote duniani watakusifu, ee Mwenyezi-Mungu, kwa sababu wameyasikia maneno yako.

5 Wataimba sifa za matendo yako, ee Mwenyezi-Mungu, kwa maana utukufu wako ni mkuu.

6 Ingawa wewe ee Mwenyezi-Mungu, uko juu ya wote, unawaangalia kwa wema walio wanyonge; nao wenye kiburi huwaona kutoka mbali.

7 Hata nikikumbana na taabu, wewe wanilinda; waunyosha mkono wako dhidi ya hasira ya maadui zangu wakali; kwa nguvu yako kuu wanisalimisha.

8 Ee Mwenyezi-Mungu, utatimiza yote uliyoniahidi. Fadhili zako, ee Mwenyezi-Mungu, zadumu milele. Usisahau kazi ya mkono wako mwenyewe.

139

1 Ee Mwenyezi-Mungu, wewe umenichunguza; wewe wanijua mpaka ndani.

2 Nikiketi au nikisimama, wewe wajua; wajua kutoka mbali kila kitu ninachofikiria.

3 Watambua nikienda au nikipumzika; wewe wazijua shughuli zangu zote.

4 Kabla sijasema neno lolote, wewe, ee Mwenyezi-Mungu, walijua kabisa.

5 Uko kila upande wangu, mbele na nyuma; waniwekea mkono wako kunilinda.

6 Maarifa yako yapita akili yangu; ni makuu mno, siwezi kuyaelewa.

7 Nikimbilie wapi ambako roho yako haiko? Niende wapi ambako wewe huko?

8 Nikipanda juu mbinguni, wewe upo; nikijilaza chini kuzimu, wewe upo.

9 Nikiruka hadi mawio ya jua, au hata mipakani mwa bahari,

10 hata huko upo kuniongoza; mkono wako wa kulia utanitegemeza.

11 Kama ningeliomba giza linifunike, giza linizunguke badala ya mwanga,

12 kwako giza si giza hata kidogo, na usiku wangaa kama mchana; kwako giza na mwanga ni mamoja.

13 Wewe umeniumba, mwili wangu wote; ulinitengeneza tumboni mwa mama yangu.

14 Nakusifu maana nimefanywa kwa namna ya ajabu, matendo yako ni ya ajabu; wewe wanijua kabisakabisa.

15 Umbo langu halikufichika kwako nilipotungwa kwa siri na ustadi ndani ya dunia.

16 Wewe uliniona hata kabla sijazaliwa, uliandika kila kitu kitabuni mwako; siku zangu zote ulizipanga, hata kabla ya kuweko ile ya kwanza.

17 Ee Mungu, mawazo yako ni makuu mno; hayawezi kabisa kuhesabika.

18 Ningeyahesabu yangekuwa mengi kuliko mchanga. Niamkapo, bado nipo pamoja nawe.

19 Laiti, ee Mungu, ungewaua watu waovu! Laiti watu wauaji wangeondoka kwangu!

20 Wanasema vibaya juu yako; wanasema maovu juu ya jina lako!

21 Ee Mwenyezi-Mungu, nawachukia wanaokuchukia; nawadharau sana wale wanaokuasi!

22 Maadui zako ni maadui zangu; ninawachukia kabisakabisa.

23 Unichunguze, ee Mungu, unijue moyo wangu, unipime, uyajue mawazo yangu.

24 Uangalie kama mwenendo wangu ni mbaya, uniongoze katika njia ya milele.

140

1 Ee Mwenyezi-Mungu, uniokoe na watu wabaya, unikinge na watu wakatili.

2 Watu hao huwaza mabaya daima, huzusha magomvi kila mara.

3 Ndimi zao hatari kama za nyoka; midomoni mwao mna maneno ya sumu kama ya joka.

4 Ee Mwenyezi-Mungu, unilinde na makucha ya wabaya; unikinge na watu wakatili ambao wamepanga kuniangusha.

5 Wenye kiburi wamenitegea mitego, wametandaza kamba kama wavu, wameficha mitego njiani wanikamate.

6 Namwambia Mwenyezi-Mungu, “Wewe ndiwe Mungu wangu.” Usikilize, ee Mwenyezi-Mungu, sauti ya ombi langu.

7 Ee Mwenyezi-Mungu, Bwana wangu, mkombozi wangu mkuu, umenikinga salama wakati wa vita.

8 Ee Mwenyezi-Mungu, usiwape waovu wanayotaka; wala mipango yao mibaya usiifanikishe.

9 Hao wanaonizingira wanainua vichwa; uovu wa maneno yao uwapate wao wenyewe!

10 Makaa ya moto yawaangukie; watumbukizwe mashimoni, wasiinuke tena.

11 Wanaowasengenya wengine wasifanikiwe katika nchi; uovu uwapate wakatili na kuwaangamiza mara!

12 Najua Mwenyezi-Mungu hutetea kisa cha wanaoteswa, na kuwapatia haki maskini.

13 Hakika waadilifu watalisifu jina lako; wanyofu watakaa kwako.

141

1 Nakuita, ee Mwenyezi-Mungu, uje haraka kunisaidia! Uisikilize sauti yangu wakati ninapokuita!

2 Sala yangu uipokee kama ubani; niinuapo mikono yangu kwako unikubali kama tambiko ya jioni.

3 Ee Mwenyezi-Mungu ukilinde kinywa changu, uweke ulinzi mlangoni mwa mdomo wangu.

4 Unikinge nisielekee kufanya mabaya, nisijishughulishe na matendo maovu; nisijiunge na watu watendao mabaya, wala nisishiriki kamwe karamu zao.

5 Afadhali mtu mwema anipige kunionya; lakini sikubali kamwe kusifiwa na wabaya, maana nasali daima dhidi ya maovu yao.

6 Wakuu wao watakapopondwa miambani, ndipo watatambua maneno yangu yalikuwa sawa.

7 Mifupa yao itatawanywa mdomoni pa Kuzimu kama kuni zilizopasuliwa vipandevipande!

8 Bali mimi nakutegemea, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu; ninakimbilia usalama kwako, usiniache hatarini.

9 Unikinge na mitego waliyonitegea, uniepushe na matanzi ya hao watu waovu.

10 Waovu wanaswe katika mitego yao wenyewe, wakati mimi najiendea zangu salama.

142

1 Namlilia Mwenyezi-Mungu kwa sauti, namsihi Mwenyezi-Mungu kwa sauti yangu.

2 Namwekea malalamiko yangu, namweleza taabu zangu.

3 Ninapokaribia kukata tamaa kabisa, yeye yupo, anajua mwenendo wangu. Maadui wamenitegea mitego njiani mwangu.

4 Nikiangalia upande wa kulia na kungojea, naona hakuna mtu wa kunisaidia; sina tena mahali pa kukimbilia, hakuna mtu anayenijali.

5 Nakulilia wewe, ee Mwenyezi-Mungu! Wewe ni kimbilio langu la usalama; wewe ni riziki yangu kuu katika nchi ya walio hai.

6 Usikilize kilio changu, maana nimekuwa hoi; uniokoe na watesi wangu, maana wamenizidi nguvu.

7 Unitoe humu kifungoni, ili nipate kukushukuru. Watu waadilifu watajiunga nami kwa sababu umenitendea mema mengi.

143

1 Usikie sala yangu, ee Mwenyezi-Mungu! Ulitegee sikio ombi langu maana wewe ni mwaminifu; unijibu kwa sababu ya uadilifu wako.

2 Usinitie hukumuni mimi mtumishi wako, maana hakuna yeyote aliye mwadilifu mbele yako.

3 Maadui zangu wamenifuatia; wameniangusha chini kabisa wameniketisha gizani kama mtu aliyekufa zamani.

4 Nimevunjika moyo kabisa; nimekufa ganzi kwa ajili ya woga.

5 Nakumbuka siku zilizopita; natafakari juu ya yote uliyotenda, nawaza na kuwazua juu ya matendo yako.

6 Nakunyoshea mikono yangu kuomba; nina kiu yako kama nchi kavu isiyo na maji.

7 Ee Mwenyezi-Mungu, unijibu haraka; maana nimekata tamaa kabisa! Usijifiche mbali nami, nisije nikawa kama wale washukao kwa wafu.

8 Asubuhi unioneshe fadhili zako, maana nimekuwekea tumaini langu. Unifundishe mwenendo wa kufuata, maana nakuelekezea ombi la moyo wangu.

9 Uniokoe, ee Mwenyezi-Mungu, kutoka maadui zangu, maana kwako nakimbilia usalama.

10 Unifundishe kutimiza matakwa yako, maana wewe ni Mungu wangu! Roho yako nzuri iniongoze katika njia sawa.

11 Unifadhili, ee Mwenyezi-Mungu, kwa hisani yako, uniondoe katika taabu kwa sababu ya uadilifu wako.

12 Kwa sababu ya fadhili zako uwakomeshe maadui zangu, uwaangamize wote wanaonidhulumu; maana mimi ni mtumishi wako.

144

1 Atukuzwe Mwenyezi-Mungu, mwamba wangu, anayeipa mikono yangu mazoezi ya vita, na kuvifunza vidole vyangu kupigana.

2 Yeye ni rafiki yangu amini na ngome yangu, kinga yangu na mkombozi wangu; yeye ni ngao yangu, kwake napata usalama; huyashinda mataifa na kuyaweka chini yangu.

3 Ee Mwenyezi-Mungu, mtu ni nini hata umjali? Mwanadamu ni nini hata umfikirie?

4 Binadamu ni kama pumzi tu; siku zake ni kama kivuli kipitacho.

5 Uinamishe mbingu zako, ee Mwenyezi-Mungu, ushuke chini! Uiguse milima nayo itoe moshi!

6 Lipusha umeme, uwatawanye maadui; upige mishale yako, uwakimbize!

7 Unyoshe mkono wako kutoka juu, uniokoe na kuniondoa katika maji haya mengi; uniondoe makuchani mwa wageni,

8 ambao husema maneno ya uongo, hunyosha mkono kushuhudia uongo.

9 Nitakuimbia wimbo mpya, ee Mungu; nitakupigia kinubi cha nyuzi kumi,

10 wewe uwapaye wafalme ushindi, umwokoaye Daudi mtumishi wako!

11 Uniokoe na upanga wa adui katili, uniondoe makuchani mwa wageni, ambao husema maneno ya uongo, hunyosha mkono kushuhudia uongo.

12 Wavulana wetu wakue kikamilifu kama mimea bustanini; binti zetu wawe kama nguzo zilizochongwa kupambia ikulu.

13 Ghala zetu zijae mazao ya kila aina. Kondoo wetu mashambani wazae maelfu kwa maelfu.

14 Mifugo yetu iwe na afya na nguvu; isitupe mimba wala kuzaa kabla ya wakati. Kusiwepo tena udhalimu mitaani mwetu.

15 Heri taifa ambalo limejaliwa hayo! Heri taifa ambalo Mungu wao ni Mwenyezi-Mungu!

145

1 Nitakutukuza, ee Mungu wangu na mfalme wangu; nitalitukuza jina lako daima na milele.

2 Nitakutukuza kila siku; nitalisifu jina lako daima na milele.

3 Mwenyezi-Mungu ni mkuu, astahili sifa nyingi; ukuu wake hauwezi kuchunguzika.

4 Kizazi hata kizazi, sifa za matendo yako zitasimuliwa, watu watatangaza matendo yako makuu.

5 Nitanena juu ya utukufu na fahari yako, nitayatafakari matendo yako ya ajabu.

6 Watu watatangaza ukuu wa matendo yako ya ajabu, nami nitatangaza ukuu wako.

7 Watatangaza sifa za wema wako mwingi, na kuimba juu ya uadilifu wako.

8 Mwenyezi-Mungu ni mwenye huruma na rehema; hakasiriki ovyo, amejaa fadhili.

9 Mwenyezi-Mungu ni mwema kwa wote, ni mwenye huruma kwa viumbe vyake vyote.

10 Viumbe vyako vyote vitakushukuru, ee Mwenyezi-Mungu, nao waaminifu wako watakutukuza.

11 Watasema juu ya utukufu wa ufalme wako, na kutangaza juu ya nguvu yako kuu,

12 ili kila mtu ajue matendo yako makuu, na fahari tukufu ya ufalme wako.

13 Ufalme wako ni ufalme wa milele; mamlaka yako yadumu vizazi vyote. Mwenyezi-Mungu ni mwaminifu katika ahadi zake zote, ni mwema katika matendo yake yote.

14 Mwenyezi-Mungu huwategemeza wote wanaoanguka; huwainua wote waliokandamizwa.

15 Viumbe vyote vinakutazama kwa hamu, nawe wavipa chakula chao kwa wakati wake.

16 Waufumbua mkono wako kwa ukarimu, watosheleza mahitaji ya kila kiumbe hai.

17 Mwenyezi-Mungu ni mwadilifu katika njia zake zote; ni mwema katika matendo yake yote.

18 Mwenyezi-Mungu yuko karibu na wote wanaomwomba, wote wanaomwomba kwa moyo mnyofu.

19 Huwapatia mahitaji yao wote wanaomcha; husikia kilio chao na kuwaokoa.

20 Mwenyezi-Mungu huwalinda wote wanaompenda; lakini atawaangamiza waovu wote.

21 Nitatangaza sifa za Mwenyezi-Mungu; viumbe vyote vilisifu jina lake takatifu, milele na milele.

146

1 Msifuni Mwenyezi-Mungu! Umsifu Mwenyezi-Mungu, ee nafsi yangu!

2 Nitamsifu Mwenyezi-Mungu maisha yangu yote; nitamwimbia Mungu wangu muda wote niishipo.

3 Msiwategemee wakuu wa dunia; hao ni binadamu tu, hawawezi kuokoa.

4 Binadamu akitoa pumzi yake ya mwisho, anarudi mavumbini alimotoka; na hapo mipango yake yote hutoweka.

5 Heri mtu anayesaidiwa na Mungu wa Yakobo, mtu aliyeweka tumaini lake kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wake,

6 aliyeumba mbingu na dunia, bahari na vyote vilivyomo. Yeye hushika ahadi yake milele.

7 Yeye huwapatia wanaoonewa haki zao, huwapa wenye njaa chakula. Mwenyezi-Mungu huwapa wafungwa uhuru,

8 huwafungua macho vipofu. Mwenyezi-Mungu huwainua waliokandamizwa; huwapenda watu walio waadilifu.

9 Mwenyezi-Mungu huwalinda wageni, huwategemeza wajane na yatima; lakini huipotosha njia ya waovu.

10 Mwenyezi-Mungu atawala milele, Mungu wako, ee Siyoni, ni mfalme vizazi vyote! Msifuni Mwenyezi-Mungu!

147

1 Msifuni Mwenyezi-Mungu! Jinsi gani ilivyo vizuri kumwimbia sifa Mungu wetu! Yeye ni mwema na astahili kuimbiwa sifa.

2 Mwenyezi-Mungu anajenga tena mji wa Yerusalemu; anawarudisha Waisraeli waliokuwa uhamishoni.

3 Anawaponya waliovunjika moyo; na kuwatibu majeraha yao.

4 Anaamua idadi itakayokuwako ya nyota, na kuzipa zote majina yao.

5 Bwana wetu ni mkuu, ana nguvu nyingi; maarifa yake hayana kipimo.

6 Mwenyezi-Mungu huwakweza wanyenyekevu, lakini huwatupa waovu mavumbini.

7 Mwimbieni Mwenyezi-Mungu nyimbo za shukrani, mpigieni kinubi Mungu wetu!

8 Yeye hulifunika anga kwa mawingu, huitengenezea nchi mvua, na kuchipusha nyasi vilimani.

9 Huwapa wanyama chakula chao, na kuwalisha makinda ya kunguru yanapolia.

10 Yeye hataki nguvu za farasi, wala hapendezwi na ushujaa wa askari;

11 lakini hupendezwa na watu wamchao, watu wanaotegemea fadhili zake.

12 Umsifu Mwenyezi-Mungu, ee Yerusalemu! Umsifu Mungu wako, ee Siyoni!

13 Maana yeye huimarisha milango yako, huwabariki watu waliomo ndani yako.

14 Huweka amani mipakani mwako; hukushibisha kwa ngano safi kabisa.

15 Yeye hupeleka amri yake duniani, na neno lake hufikia lengo lake haraka.

16 Hutandaza theluji kama pamba, hutawanya umande kama majivu.

17 Huleta mvua ya mawe kama kokoto na kwa ubaridi wake maji huganda.

18 Kisha hutoa amri, maji hayo yakayeyuka; huvumisha upepo wake, nayo yakatiririka.

19 Humjulisha Yakobo ujumbe wake, na Israeli masharti na maagizo yake.

20 Lakini hakuyatendea hivyo mataifa mengine; watu wengine hawayajui maagizo yake. Msifuni Mwenyezi-Mungu!

148

1 Msifuni Mwenyezi-Mungu! Msifuni Mwenyezi-Mungu kutoka mbinguni, msifuni kutoka huko juu mbinguni.

2 Msifuni, enyi malaika wake wote, msifuni, enyi majeshi yake yote.

3 Msifuni, enyi jua na mwezi, msifuni, enyi nyota zote zingaazo.

4 Msifuni, enyi mbingu za juu, na maji yaliyo juu ya mbingu.

5 Vyote vilisifu jina la Mwenyezi-Mungu, maana yeye aliamuru, na vyote vikawa.

6 Yeye aliviweka mahali pao daima, kwa amri ambayo haiwezi kubatilishwa.

7 Msifuni Mwenyezi-Mungu kutoka duniani; enyi majoka ya baharini na vilindini, msifuni.

8 Msifuni enyi moto, mvua ya mawe na theluji, upepo wa tufani unaotimiza amri yake!

9 Msifuni enyi milima na vilima, miti ya matunda na misitu!

10 Msifuni enyi wanyama wa porini na wafugwao, viumbe vitambaavyo na ndege wote!

11 Msifuni enyi wafalme na mataifa yote; viongozi na watawala wote duniani!

12 Msifuni enyi wavulana na wasichana; wazee wote na watoto pia!

13 Nyote lisifuni jina la Mwenyezi-Mungu, maana jina lake peke yake latukuka; utukufu wake wapita dunia na mbingu.

14 Amewapa watu wake nguvu; heshima kwa watu wote waaminifu, watu wa Israeli wapenzi wake. Msifuni Mwenyezi-Mungu!

149

1 Msifuni Mwenyezi-Mungu! Mwimbieni Mwenyezi-Mungu wimbo mpya; msifuni katika kusanyiko la waaminifu!

2 Furahi ee Israeli kwa sababu ya Muumba wako, wakazi wa Siyoni shangilieni kwa sababu ya Mfalme wenu.

3 Lisifuni jina lake kwa ngoma, mwimbieni kwa ngoma na zeze.

4 Maana Mwenyezi-Mungu hupendezwa na watu wake; yeye huwapamba wanyonge kwa ushindi.

5 Watu waaminifu wafurahi kwa fahari; washangilie hata walalapo.

6 Wabubujike sifa kuu za Mungu, na panga zenye makali kuwili mikononi mwao,

7 wawalipe kisasi watu wa mataifa, wawaadhibu watu wasiomjua Mungu;

8 wawafunge wafalme wao kwa minyororo, na viongozi wao kwa pingu za chuma,

9 kusudi watekeleze adhabu iliyoamriwa! Hiyo ndiyo fahari ya waaminifu wa Mungu. Msifuni Mwenyezi-Mungu!

150

1 Msifuni Mwenyezi-Mungu! Msifuni Mungu katika patakatifu pake; msifuni katika mbingu zake kuu.

2 Msifuni kwa sababu ya matendo yake makuu; msifuni kwa ajili ya utukufu wake mkuu.

3 Msifuni kwa mlio wa tarumbeta; msifuni kwa zeze na kinubi!

4 Msifuni kwa ngoma na kucheza; msifuni kwa filimbi na banjo!

5 Msifuni kwa kupiga matoazi. Msifuni kwa matoazi ya sauti kubwa.

6 Kila kiumbe hai kimsifu Mwenyezi-Mungu! Msifuni Mwenyezi-Mungu!