1

1 Mwenyezi-Mungu alimwita Mose na kuongea naye katika hema la mkutano, akamwambia,

2 “Waambie Waisraeli kwamba kama mtu anapenda kumtolea Mwenyezi-Mungu sadaka ya mnyama, mnyama huyo atamchagua kutoka kundi lake la ng'ombe, kondoo au mbuzi.

3 “Kama sadaka anayotoa mtu ni ya kuteketezwa, atamchagua mnyama dume asiye na dosari kutoka kundi lake, atamtolea mbele ya mlango wa hema la mkutano ili apate fadhili ya Mwenyezi-Mungu;

4 ataweka mkono wake juu ya kichwa cha mnyama wa sadaka ya kuteketezwa, ambayo itakubaliwa kwa ajili ya kumfanyia huyo mtu upatanisho.

5 Kisha, atamchinja huyo ng'ombe mbele ya Mwenyezi-Mungu. Nao makuhani, wazawa wa Aroni, wataichukua damu na kuinyunyizia madhabahu mlangoni mwa hema la mkutano, pande zake zote.

6 Huyo mtu atamchuna huyo mnyama wa sadaka ya kuteketezwa na kumkata vipandevipande.

7 Hao makuhani wazawa wa Aroni watazipanga kuni juu ya madhabahu na kuwasha moto.

8 Kisha makuhani hao watachukua vile vipande vya nyama, kichwa na mafuta, na kuviweka juu ya kuni juu ya madhabahu.

9 Lakini matumbo na miguu ya mnyama huyo mtu ataviosha kwa maji. Kuhani ataiteketeza sadaka yote juu ya madhabahu. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu.

10 “Kama sadaka yake ya kuteketezwa ataitoa katika kundi la kondoo au mbuzi, basi, atachagua dume asiye na dosari.

11 Atamchinjia upande wa kaskazini wa madhabahu, mbele ya Mwenyezi-Mungu, hao makuhani, wazawa wa Aroni watainyunyizia madhabahu damu pande zake zote.

12 Kisha huyo mtu atamkata vipandevipande, akivitenga kichwa pamoja na mafuta yake, na kuhani ataviweka kwenye moto juu ya madhabahu.

13 Lakini matumbo na miguu yake ataviosha kwa maji. Kuhani ataiteketeza yote juu ya madhabahu. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu.

14 “Ikiwa anamtolea Mwenyezi-Mungu sadaka ya kuteketezwa ya ndege, basi, ataleta sadaka yake ya hua au kinda la njiwa.

15 Kuhani atamleta ndege huyo kwenye madhabahu, atamkongonyoa kichwa chake na kukiteketeza juu ya madhabahu. Damu yake itanyunyiziwa ubavuni mwa madhabahu.

16 Kibofu chake pamoja na uchafu wake ataviondoa na kutupa upande wa mashariki wa madhabahu ambako majivu huwekwa.

17 Atamshika mabawa na kumpasua, lakini asimkate vipande viwili. Kisha, kuhani atamteketeza kwenye madhabahu, juu ya kuni. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu.”

2

1 “Mtu yeyote akileta sadaka ya nafaka kwa Mwenyezi-Mungu, sadaka hiyo iwe ya unga laini. Atautia mafuta na ubani.

2 Kisha, atawaletea hao makuhani wa ukoo wa Aroni. Atachukua konzi moja ya unga huo laini wenye mafuta na ubani na kumpelekea kuhani mmojawapo ambaye atauteketeza juu ya madhabahu uwe sadaka ya ukumbusho kwa Mwenyezi-Mungu. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu.

3 Sehemu inayobaki ya sadaka hiyo ni ya makuhani. Hiyo ni sehemu takatifu kabisa ya sadaka anayotolewa Mwenyezi-Mungu kwa moto.

4 “Kama mtu anamtolea Mungu sadaka ya nafaka iliyookwa jikoni, hiyo itakuwa ya mikate isiyotiwa chachu ya unga laini uliochanganywa na mafuta ya zeituni, au ya mikate myembamba isiyo na chachu na isiyopakwa mafuta.

5 Iwapo sadaka unayotoa ni ya mkate uliookwa kwenye kikaango, hiyo itakuwa ya unga laini uliochanganywa na mafuta ya zeituni lakini bila chachu.

6 Mikate hiyo itakatwakatwa na kumiminiwa mafuta; hiyo ni sadaka ya nafaka.

7 Kama sadaka unayotoa ni ya mikate iliyopikwa katika sufuria, hiyo itakuwa ya unga laini na imetiwa mafuta.

8 Utaleta sadaka ya nafaka iliyotengenezwa kwa vitu hivyo mbele ya Mwenyezi-Mungu; na kuhani ataipeleka kwenye madhabahu.

9 Kuhani atachukua sehemu ya sadaka hiyo ikiwa ni sadaka ya ukumbusho na kuiteketeza juu ya madhabahu. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu.

10 Sehemu inayobaki ya sadaka ya nafaka, ni ya makuhani. Hiyo ni sehemu takatifu kabisa ya sadaka inayotolewa Mwenyezi-Mungu kwa moto.

11 “Sadaka yoyote ya nafaka utakayomletea Mwenyezi-Mungu ni lazima iwe imetengenezwa bila chachu; kwani hakuna ruhusa kamwe kutumia chachu wala asali katika sadaka anazotolewa Mwenyezi-Mungu kwa moto.

12 Unaweza kumletea Mwenyezi-Mungu mazao yako ya kwanza kama sadaka. Lakini hayo hayatatolewa madhabahuni kama harufu ya kumpendeza.

13 Utakoleza sadaka zako zote za nafaka kwa chumvi. Kamwe usiache kuweka chumvi katika sadaka yako ya nafaka, kwani chumvi ni ishara ya agano alilofanya Mungu pamoja nanyi.

14 “Ukimtolea Mwenyezi-Mungu sadaka ya mazao yako ya kwanza utaitoa hiyo ikiwa imechomwa katika masuke yake, au utaitoa katika mikate ya kuokwa iliyotengenezwa kwa ngano iliyosagwa.

15 Utaitia mafuta na kuweka ubani; hiyo ni sadaka ya nafaka.

16 Kuhani ataiteketeza sehemu ya sadaka hiyo ya nafaka iliyopondwa na mafuta pamoja na ubani wake wote, iwe sadaka ya ukumbusho; hiyo ni sadaka anayotolewa Mwenyezi-Mungu kwa moto.

3

1 “Kama mtu anatoa sadaka ya amani, na sadaka yake ni ng'ombe dume au jike basi, mnyama huyo asiwe na dosari mbele yangu.

2 Ataweka mkono wake juu ya kichwa cha mnyama huyo na kumchinja mlangoni mwa hema la mkutano. Hao makuhani wazawa wa Aroni watainyunyizia madhabahu damu yake pande zake zote.

3 Mafuta yote yanayofunika na yaliyo juu ya matumbo ya mnyama wa sadaka hiyo ya amani atayateketeza kama sadaka anayotolewa Mwenyezi-Mungu kwa moto.

4 Atatoa pia zile figo mbili na mafuta yake pamoja na ile sehemu bora ya ini.

5 Wazawa wa Aroni wataiteketeza madhabahuni pamoja na sadaka ya kuteketezwa iliyoko juu ya kuni; hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu.

6 “Kama sadaka hiyo ya kufanya amani unayomtolea Mwenyezi-Mungu ni kutoka kundi la kondoo au mbuzi, basi achaguliwe dume au jike asiye na dosari.

7 Kama mtu atatoa mwanakondoo kuwa sadaka yake, basi, atamtolea mbele ya Mwenyezi-Mungu,

8 akiweka mkono wake juu ya kichwa cha mnyama huyo na kumchinja mbele ya hema la mkutano. Makuhani wazawa wa Aroni watainyunyizia madhabahu damu yake pande zake zote.

9 Kisha, kutoka katika sadaka hiyo ya amani anayotolewa Mwenyezi-Mungu kwa moto, atamtolea sehemu zifuatazo: Mafuta yake, mkia wenye mafuta mzima uliokatwa karibu kabisa na uti wa mgongo pamoja na mafuta yote yanayofunika matumbo na mafuta yote yaliyo kwenye matumbo,

10 zile figo mbili na mafuta yake pamoja na sehemu bora ya ini.

11 Kuhani ataviteketeza hivyo vyote juu ya madhabahu kama chakula anachotolewa Mwenyezi-Mungu kwa moto.

12 “Kama sadaka yake ni mbuzi, basi, atamtolea mbele ya Mwenyezi-Mungu

13 akiweka mkono wake juu ya kichwa cha mnyama huyo na kumchinja mbele ya hema la mkutano. Wazawa wa Aroni watainyunyizia madhabahu damu yake pande zake zote.

14 Kisha, mafuta yote yanayofunika matumbo

15 na zile figo mbili na mafuta yake pamoja na sehemu bora ya ini, atamtolea Mwenyezi-Mungu sadaka ya kuteketezwa kwa moto.

16 Kuhani ataviteketeza juu ya madhabahu kama chakula kinachotolewa kwa Mwenyezi-Mungu kwa moto kutoa harufu ya kumpendeza Mungu. Mafuta yote ni ya Mwenyezi-Mungu.

17 Ndiyo maana siku zote na mahali popote mtakapokaa ni lazima kushika kanuni hii. Kamwe msile mafuta wala damu.”

4

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

2 “Waambie watu wa Israeli hivi: Kama mtu ametenda dhambi bila kukusudia, akafanya kitu kilichokatazwa na amri ya Mwenyezi-Mungu, atafanya kama ifuatavyo:

3 Ikiwa kuhani ambaye amepakwa mafuta ndiye aliyetenda dhambi hata akawatia watu hatiani, basi huyo atamtolea Mwenyezi-Mungu fahali mchanga asiye na dosari awe sadaka ya kuondoa dhambi.

4 Atamleta huyo fahali mchanga kwenye mlango wa hema la mkutano, mbele ya Mwenyezi-Mungu; naye ataweka mkono wake juu ya kichwa cha fahali huyo na kumchinja mbele ya Mwenyezi-Mungu.

5 Huyo kuhani, aliyepakwa mafuta atachukua kiasi cha damu na kuingia nayo ndani ya hema la mkutano.

6 Atachovya kidole chake katika damu hiyo na kuirashia mara saba mbele ya Mwenyezi-Mungu upande wa mbele wa pazia la mahali patakatifu.

7 Kuhani atachukua sehemu ya damu na kuzipaka pembe za madhabahu ya kufukizia ubani wa harufu nzuri, mbele ya Mwenyezi-Mungu katika hema la mkutano. Damu inayobaki ataimwaga chini kwenye tako la madhabahu ya kuteketezea sadaka iliyoko karibu na mlango wa hema la mkutano.

8 Kisha atayaondoa mafuta yote ya ng'ombe huyo: Mafuta yanayofunika matumbo,

9 figo mbili na mafuta yaliyo juu yake na yale yaliyo kiunoni, na yale yaliyoshikamana na figo na ini; hizi ni sehemu zilezile zinazoondolewa kwa mnyama wa sadaka ya amani.

10 Kuhani atazichukua na kuziteketeza juu ya madhabahu ya kuteketezea sadaka.

11 Lakini ngozi ya huyo ng'ombe, nyama, kichwa, miguu, matumbo na mavi yake,

12 yaani ng'ombe mzima aliyesalia atampeleka na kumteketeza nje ya kambi mahali safi ambapo majivu hutupwa, naye atamchoma kwa moto juu ya kuni; atachomwa moto hapo mahali pa kumwagia majivu.

13 “Iwapo jumuiya yote nzima ya Israeli imetenda dhambi bila ya kukusudia kwa kufanya kitu kilichokatazwa na amri ya Mwenyezi-Mungu

14 mara dhambi hiyo itakapojulikana, jumuiya yote itatoa fahali mchanga awe sadaka ya kuondoa dhambi. Watamleta kwenye hema la mkutano.

15 Wazee wa jumuiya ya watu wataweka mikono yao juu ya kichwa cha huyo fahali, kisha atachinjwa mbele ya Mwenyezi-Mungu.

16 Yule kuhani aliyeteuliwa rasmi kwa kupakwa mafuta ataleta sehemu ya damu ya huyo fahali ndani ya hema la mkutano.

17 Atachovya kidole chake katika hiyo damu na kuinyunyiza mbele ya pazia mara saba, mbele ya Mwenyezi-Mungu.

18 Kisha, sehemu ya damu atazipaka pembe za madhabahu iliyoko katika hema la mkutano mbele ya Mwenyezi-Mungu. Damu inayobaki ataimwaga chini kwenye tako la madhabahu ya kuteketezea sadaka iliyo karibu na mlango wa hema la mkutano.

19 Mafuta yote ya mnyama huyo atayachukua na kuyateketeza kwenye madhabahu.

20 Kwa hiyo atamfanya fahali huyu kama alivyomfanya yule mwingine wa sadaka ya kuondoa dhambi. Basi, huyo kuhani atawafanyia watu ibada hiyo ya upatanisho kwa ajili ya dhambi, nao watasamehewa.

21 Kisha atamchukua fahali huyu na kumpeleka nje ya kambi na kumteketeza kwa moto kama alivyomfanya yule mwingine. Hiyo ni sadaka ya kuondoa dhambi ya jumuiya.

22 “Ikiwa mtawala ametenda dhambi bila kukusudia kwa kufanya kitu kilichokatazwa na amri ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wake, na hivyo akawa na hatia,

23 mara akijulishwa dhambi hiyo aliyotenda, ataleta sadaka yake ya beberu asiye na dosari.

24 Ataweka mkono wake juu ya kichwa cha beberu na kumchinjia mahali wanapochinjia sadaka za kuteketezwa mbele ya Mwenyezi-Mungu; hiyo ni sadaka ya kuondoa dhambi.

25 Kuhani atachovya kidole chake katika damu ya sadaka ya kuondoa dhambi na kuzipaka pembe za madhabahu ya kuteketezea sadaka. Damu inayobaki ataimwaga chini kwenye tako la madhabahu ya kuteketezea sadaka.

26 Mafuta yote ya beberu huyo atayateketeza madhabahuni, kama afanyavyo na mafuta ya mnyama wa sadaka ya amani. Kwa hiyo kuhani atamfanyia mtawala ibada hiyo ya upatanisho kwa ajili ya dhambi yake, naye atasamehewa.

27 “Kama mtu wa kawaida ametenda dhambi bila kukusudia, kwa kufanya kitu kilichokatazwa na amri ya Mwenyezi-Mungu na hivyo akawa na hatia,

28 mara atakapojulishwa kuwa ametenda dhambi, ataleta sadaka ya mbuzi jike asiye na dosari kwa ajili ya kuondoa dhambi aliyotenda.

29 Ataweka mkono wake juu ya kichwa cha mbuzi huyo wa sadaka ya kuondoa dhambi, na kumchinjia mahali wanapochinjia wanyama wa sadaka za kuteketezwa.

30 Kuhani atachovya kidole chake katika damu ya sadaka ya kuondoa dhambi na kuzipaka pembe za madhabahu ya kuteketezea sadaka. Damu iliyobaki ataimwaga chini kwenye tako la madhabahu.

31 Mafuta yote ya mbuzi huyo atayaondoa kama aondoavyo mafuta ya wanyama wa sadaka za amani, naye kuhani atayateketeza madhabahuni, na harufu yake nzuri itampendeza Mwenyezi-Mungu. Basi, kuhani atamfanyia huyo mtu hiyo ibada ya upatanisho, naye atasamehewa.

32 “Ikiwa mtu huyo ataleta mwanakondoo kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi, basi, ataleta mwanakondoo jike asiye na dosari.

33 Ataweka mkono wake juu ya kichwa cha mwanakondoo huyo wa sadaka ya kuondoa dhambi, na kumchinjia mahali pale wanapochinjia wanyama wa sadaka za kuteketezwa.

34 Kisha kuhani atachovya kidole chake katika damu ya sadaka ya kuondoa dhambi na kuzipaka pembe za madhabahu ya kuteketezea sadaka. Damu inayobaki ataimwaga chini kwenye tako la madhabahu.

35 Kisha atayaondoa mafuta yote kama aondoavyo mafuta ya mwanakondoo wa sadaka ya amani, na kuhani atayateketeza juu ya madhabahu, pamoja na sadaka zitolewazo kwa Mwenyezi-Mungu kwa moto. Naye kuhani atamfanyia ibada ya upatanisho kwa ajili ya dhambi yake, naye atasamehewa.”

5

1 “Kama mtu yeyote akitakiwa kutoa ushahidi kwenye baraza juu ya jambo aliloona au kulisikia naye akakataa kusema kitu, basi, huo ni uovu na atauwajibikia.

2 Au kama mtu yeyote miongoni mwenu amekuwa najisi bila kukusudia kwa kugusa kitu chochote najisi, iwe ni mzoga wa mnyama wa porini au wa kufugwa au wadudu, atakuwa na hatia.

3 Au mtu akigusa chochote kilicho najisi cha binadamu, kiwe kiwacho, ambacho humfanya mtu kuwa najisi, naye hana habari, basi, atakapojua atakuwa na hatia.

4 Au, kama mtu akiapa kufanya chochote kile, chema au kibaya, kama wafanyavyo watu bila kufikiri, atakapojua atakuwa na hatia.

5 Basi, mtu akiwa na hatia kuhusu mambo hayo lazima akiri dhambi yake aliyotenda

6 na kumletea Mwenyezi-Mungu sadaka yake ya kuondoa hatia. Kwa ajili ya dhambi aliyotenda ataleta kondoo jike au mbuzi jike kutoka kundi lake amtoe sadaka kwa ajili ya kuondoa dhambi. Naye kuhani atamfanyia upatanisho kwa ajili ya dhambi yake.

7 “Lakini kama hawezi kutoa mwanakondoo wa sadaka ya kuondoa hatia kwa ajili ya dhambi aliyotenda, basi atamletea Mwenyezi-Mungu hua wawili au makinda mawili ya njiwa: Mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi, na mwingine kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa.

8 Atawaleta kwa kuhani, naye kuhani atamtoa mmoja awe sadaka ya kuondoa dhambi kwa kumkongonyoa shingo yake bila kukichopoa kichwa chake.

9 Sehemu ya damu yake ataipaka pembeni mwa madhabahu na ile nyingine ataimimina chini kwenye tako la madhabahu. Hiyo ni sadaka ya kuondoa dhambi.

10 Kisha atamtoa yule wa pili kuwa sadaka ya kuteketezwa kulingana na maagizo. Kuhani atamfanyia huyo mtu upatanisho kwa ajili ya dhambi yake, naye atasamehewa.

11 “Ikiwa hawezi kutoa hua wawili au makinda mawili ya njiwa kama sadaka yake ya kuondoa dhambi aliyotenda, basi, ataleta unga kilo moja. Lakini hatautia mafuta wala ubani kwani ni sadaka ya kuondoa dhambi.

12 Atamletea kuhani, naye atachukua unga huo konzi moja na kuuteketeza juu ya madhabahu kama sehemu ya ukumbusho, pamoja na sadaka anazotolewa Mwenyezi-Mungu kwa moto. Hiyo ni sadaka ya kuondoa dhambi.

13 Basi, kuhani atamfanyia huyo mtu ibada ya upatanisho kwa ajili ya dhambi, naye atasamehewa. Unga unaobaki utakuwa wake kuhani kama ifanyikavyo kuhusu sadaka ya nafaka.”

14 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

15 “Kama mtu yeyote akikosa kwa kutenda dhambi bila kujua kuhusu kutotoa vitu vitakatifu anavyotolewa Mwenyezi-Mungu, atamletea kondoo dume asiye na dosari kutoka kundi lake. Wewe utapima thamani yake kulingana na kipimo rasmi cha mahali patakatifu. Hiyo ni sadaka ya kuondoa hatia.

16 Zaidi ya hayo, huyo mtu atalipa madhara yote aliyosababisha kuhusu vitu vitakatifu kwa kuongeza sehemu ya tano ya thamani yake na kumpatia kuhani yote. Basi, kuhani atamfanyia ibada ya upatanisho kwa ajili ya dhambi kwa huyo kondoo dume aliye sadaka ya kuondoa hatia, naye atasamehewa.

17 “Mtu yeyote akitenda dhambi bila kujua, kwa kuvunja amri yoyote ya Mwenyezi-Mungu, yeye ana hatia, na atalipa adhabu ya hatia yake.

18 Atamletea kuhani kondoo dume asiye na dosari kutoka kundi lake akiwa na thamani sawa na ile ya sadaka ya hatia. Na kuhani atamfanyia upatanisho kwa kosa alilofanya, naye atasamehewa.

19 Hiyo ni sadaka ya hatia; yeye ana hatia mbele ya Mwenyezi-Mungu.”

6

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

2 “Ikiwa mtu yeyote ametenda dhambi na kumwasi Mwenyezi-Mungu kwa kumdanganya jirani yake juu ya amana au dhamana aliyowekewa, au kumnyanganya au amemdhulumu mwenzake,

3 au amepata kitu cha jirani yake kilichopotea, akasema kwamba hakukiona, au ameapa uongo juu ya chochote ambacho watu hufanya wakawa na hatia,

4 mtu huyo anapokuwa ametenda dhambi na amekuwa na hatia, ni lazima arudishe alichoiba au alichopata kwa dhuluma, au amana aliyopewa, au kitu cha jirani yake kilichopotea akakipata,

5 au chochote alichoapa kwa uongo. Atalipa kila kitu kikamilifu na kuongeza sehemu ya tano ya thamani yake. Mara atakapojua kosa lake atamrudishia mwenyewe.

6 Kisha atamletea kuhani kondoo dume au mbuzi dume asiye na dosari amtolee Mwenyezi-Mungu sadaka ya kuondoa hatia; thamani ya mnyama huyo itakuwa ile ya kawaida ya kuondoa hatia.

7 Kuhani atamfanyia ibada ya upatanisho mbele ya Mwenyezi-Mungu, naye atasamehewa kosa ambalo alikuwa amelifanya.”

8 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

9 “Mpe Aroni na wanawe maagizo haya: Ufuatao ni mwongozo wa ibada kuhusu sadaka ya kuteketezwa. Sadaka ya kuteketezwa itakuwa motoni juu ya madhabahu usiku kucha hadi asubuhi na moto wake uchochewe, usizimike.

10 Kisha kuhani akiwa amevaa vazi lake rasmi la kitani na kaptura yake ya kitani, atachukua majivu ya ile sadaka kutoka madhabahuni na kuyaweka kando ya madhabahu.

11 Halafu baada ya kubadilisha mavazi yake atayapeleka yale majivu nje ya kambi mahali palipo safi.

12 Moto wa madhabahu lazima uendelee kuwaka, na wala usizimwe. Kila siku asubuhi kuhani ataweka kuni kwenye moto huo na juu yake atapanga sadaka ya kuteketezwa, kabla ya kuteketeza mafuta ya sadaka ya amani.

13 Moto utaendelea kuwaka daima juu ya madhabahu bila kuzimishwa kamwe.

14 “Ufuatao ni mwongozo wa ibada kuhusu sadaka ya nafaka. Wazawa wa Aroni ndio walio na uwezo wa kumtolea Mwenyezi-Mungu sadaka hiyo juu ya madhabahu.

15 Mmoja wa makuhani atachukua konzi moja ya unga wa sadaka ya nafaka pamoja na mafuta na ubani wote na kuviteketeza juu ya madhabahu kama sehemu ya ukumbusho; harufu yake itampendeza Mwenyezi-Mungu.

16 Unga uliosalia atakula Aroni na wazawa wake makuhani bila kutiwa chachu. Wataula kwenye mahali patakatifu uani mwa hema la mkutano.

17 Kamwe usiokwe pamoja na chachu. Nimewapa wao sehemu hiyo kutoka sadaka wanazonitolea kwa moto. Ni sadaka takatifu kabisa kama zilivyo sadaka za kuondoa dhambi na za kuondoa hatia.

18 Wazawa wa kiume wa Aroni ndio peke yao wanaoruhusiwa kula sehemu hiyo maana hiyo imetengwa daima kwa ajili yao kutoka sadaka anazotolewa Mwenyezi-Mungu kwa moto. Yeyote atakayezigusa atakuwa mtakatifu.”

19 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

20 “Tangu wakati wa kuwekwa wakfu kwa Aroni na wazawa wake wanapaswa kumtolea Mwenyezi-Mungu kilo moja ya unga laini kwa siku, nusu moja ya unga huo ataitoa asubuhi na nusu nyingine jioni.

21 Unga huo utachanganywa na mafuta na kuokwa; kisha utauleta ukiwa vipandevipande na kumtolea Mwenyezi-Mungu; na harufu ya sadaka yake itampendeza Mungu.

22 Kuhani aliye mzawa wa Aroni ambaye amepakwa mafuta kushika nafasi yake atamtolea Mwenyezi-Mungu sadaka hiyo; hilo ni agizo la milele. Sadaka yote itateketezwa.

23 Sadaka yoyote ya nafaka iliyotolewa na kuhani itateketezwa yote; haitaliwa kamwe.”

24 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

25 “Mwambie Aroni na wanawe kuwa ufuatao ni mwongozo wa ibada kuhusu sadaka ya kuondoa dhambi, mahali pale ambapo mnyama wa sadaka ya kuteketezwa huchinjiwa ndipo atakapochinjiwa mnyama wa sadaka ya kuondoa dhambi, mbele ya Mwenyezi-Mungu; hiyo ni sadaka takatifu kabisa.

26 Kuhani anayetolea sadaka hiyo ndiye atakayeila. Italiwa mahali patakatifu, uani mwa hema la mkutano.

27 Chochote kitakachogusa nyama hiyo kitakuwa kitakatifu; vazi lolote likidondokewa na damu ya sadaka hiyo, basi, vazi hilo litaoshewa mahali patakatifu.

28 Sadaka hiyo ikichemshiwa katika vyombo vya udongo, vyombo hivyo vitavunjwa. Lakini ikiwa vyombo hivyo ni vya shaba, basi, vitasafishwa na kusuzwa kwa maji.

29 Wanaoruhusiwa kuila ni wanaume wa ukoo wa makuhani peke yao kwa vile hiyo ni sadaka takatifu kabisa.

30 Lakini kama damu ya sadaka yoyote ya kuondoa dhambi imeletwa ndani ya hema la mkutano ili kufanyia ibada ya upatanisho katika mahali patakatifu, sadaka hiyo itateketezwa kwa moto.”

7

1 “Ufuatao ni mwongozo wa ibada kuhusu sadaka ya kuondoa hatia. Sadaka hiyo ni takatifu kabisa.

2 Mnyama wa sadaka ya kuondoa hatia atachinjiwa mahali wanapochinjiwa wanyama wa sadaka za kuteketezwa, na damu yake itarashiwa madhabahu pande zake zote.

3 Mafuta yake yote: Mafuta ya mkia na yale yanayofunika matumbo yatatolewa na kuteketezwa

4 pamoja na zile figo mbili pamoja na mafuta yake na ile sehemu bora ya ini.

5 Kuhani ataviteketeza juu ya madhabahu kama sadaka anayotolewa Mwenyezi-Mungu kwa moto. Hiyo ni sadaka ya kuondoa hatia.

6 Wanaoruhusiwa kula sadaka hiyo ni wanaume wa ukoo wa makuhani peke yao; ni sadaka takatifu kabisa. Italiwa katika mahali patakatifu.

7 Sheria ni moja kuhusu sadaka ya kuondoa hatia na sadaka ya kuondoa dhambi: Kuhani anayefanya ibada ya upatanisho ndiye atakayeichukua.

8 Kuhani anayetoa sadaka ya kuteketezwa ya mtu yeyote, atachukua ngozi ya mnyama aliyetolewa.

9 Sadaka yoyote ya nafaka iliyookwa jikoni au katika sufuria au katika kikaango itakuwa mali ya kuhani anayeitoa.

10 Kila sadaka ya nafaka, iwe imechanganywa na mafuta au kavu, itakuwa ya wazawa wa Aroni, na wote wagawiwe kwa sawa.

11 “Ufuatao ni mwongozo wa ibada kuhusu sadaka za amani ambazo mtu aweza kumtolea Mwenyezi-Mungu.

12 Ikiwa mtu anatoa sadaka hiyo ya kumshukuru Mungu, basi, ataitoa pamoja na maandazi yasiyotiwa chachu yaliyopakwa mafuta, mikate myembamba iliyopakwa mafuta na maandazi ya unga laini uliochanganywa na mafuta.

13 Pamoja na sadaka hiyo yake ya amani ya kumshukuru Mungu, ataleta maandazi yaliyotiwa chachu.

14 Kutokana na maandazi hayo, atamtolea Mwenyezi-Mungu andazi moja kutoka kila sadaka; maandazi hayo yatakuwa yake kuhani anayeirashia madhabahu damu ya sadaka za amani.

15 Nyama ya sadaka hiyo ya amani ya kumshukuru Mungu italiwa siku hiyohiyo inapotolewa; hataacha hata sehemu yake hadi asubuhi.

16 Lakini kama sadaka hiyo ya amani ni ya nadhiri au ya hiari, italiwa siku hiyohiyo inapotolewa na sehemu nyingine yaweza kuliwa kesho yake.

17 Lakini nyama yoyote ya sadaka hiyo inayobaki hadi siku ya tatu itateketezwa.

18 Tena nyama yoyote ya sadaka ya amani ikiliwa siku ya tatu, haitakubaliwa, wala haitapokelewa kwa faida yake mtu aliyeitoa. Nyama hiyo ni chukizo na mtu atakayeila atawajibika kwa uovu wake.

19 “Nyama yoyote inayogusa kitu najisi isiliwe. Nyama hiyo itateketezwa kwa moto. Wote walio safi wanaweza kula nyama

20 iliyotolewa sadaka ya amani kwa Mwenyezi-Mungu. Lakini mtu yeyote aliye najisi, akila nyama hiyo, atatengwa na watu wake.

21 Mtu yeyote anayegusa kitu chochote kilicho najisi, au kitu najisi cha mtu, au mnyama aliye najisi, au kitu chochote najisi ambacho ni chukizo, akila nyama ya sadaka ya amani aliyotolewa Mwenyezi-Mungu, mtu huyo atatengwa na watu wake.”

22 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

23 “Waambie Waisraeli hivi: Msile mafuta ya ng'ombe au ya kondoo au ya mbuzi.

24 Mafuta ya mnyama yoyote aliyekufa mwenyewe au ya mnyama aliyeuawa na mnyama wa porini yaweza kuwekwa kwa matumizi mengine, lakini kamwe msiyale.

25 Mtu yeyote akila mafuta ya mnyama aliyetolewa kwa Mwenyezi-Mungu kwa moto, atatengwa na watu wake.

26 Tena, kamwe msile damu yoyote ile, iwe ya ndege au ya mnyama mahali popote mnapoishi.

27 Mtu yeyote akila damu yoyote, atatengwa na watu wake.”

28 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

29 “Waambie watu wa Israeli hivi: Mtu yeyote akitoa sadaka ya amani, atampa Mwenyezi-Mungu sehemu ya sadaka hiyo.

30 Atamletea kwa mikono yake mwenyewe kama sadaka ya kuteketezwa kwa moto. Ataleta mafuta yake pamoja na kidari ambacho atafanya nacho ishara ya kumtolea Mwenyezi-Mungu.

31 Kuhani atayateketeza mafuta yote juu ya madhabahu, lakini kidari kitakuwa cha Aroni na wanawe makuhani.

32 Mguu wa kulia wa nyuma wa mnyama wa sadaka zenu za amani mtampa kuhani.

33 Mguu huo utakuwa mali ya kuhani aliye mzawa wa Aroni anayetoa damu ya sadaka za amani na mafuta yake.

34 Mwenyezi-Mungu amewaagiza watu wa Israeli watenge kidari hicho na mguu huo wa mnyama wa sadaka zao za amani, wampe kuhani Aroni na wazawa wake, maana sehemu hiyo wamewekewa hao makuhani milele.

35 Hiyo ndiyo sehemu iliyotengwa kwa ajili ya Aroni na wanawe kutoka katika sadaka anazotolewa Mwenyezi-Mungu kwa moto, tangu siku walipotawazwa kuwa makuhani wa Mwenyezi-Mungu.

36 Walipowekwa wakfu kwa kupakwa mafuta, Mwenyezi-Mungu aliamuru Waisraeli wawape sehemu hiyo ya sadaka; hiyo itakuwa daima haki yao.”

37 Basi, hayo ndiyo maagizo kuhusu sadaka ya kuteketezwa, sadaka ya nafaka, sadaka ya kuondoa dhambi, sadaka ya kuondoa hatia, kuhusu kuwekwa wakfu na kuhusu sadaka ya amani.

38 Mwenyezi-Mungu alimpa Mose amri hizi mlimani Sinai siku ile alipowaamuru Waisraeli wamletee sadaka zao, kule jangwani Sinai.

8

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

2 “Mwite Aroni na wanawe wakutane mbele ya mlango wa hema la mkutano; chukua mavazi matakatifu, mafuta ya kupaka, ng'ombe wa sadaka ya kuondolea dhambi, kondoo madume wawili, na kikapu cha mikate isiyotiwa chachu.

3 Kisha, ikusanye jumuiya yote ya Waisraeli mbele ya mlango wa hema la mkutano.”

4 Mose akafanya kama alivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu, akaikusanya jumuiya yote mbele ya mlango wa hema la mkutano.

5 Mose akaiambia jumuiya yote hivi: “Lifuatalo ni jambo ambalo Mwenyezi-Mungu ameamuru lifanywe.”

6 Hapo Mose akawaleta Aroni na wanawe na kuwatawadha.

7 Kisha akamvika Aroni joho na kuifunga kwa mkanda, akamvika kanzu, akamvalisha kizibao na kukifunga kiunoni mwake kwa mkanda uliofumwa kwa ustadi.

8 Kisha akaweka kifuko kifuani pa Aroni na ndani ya kifuko hicho akatia mawe ya kauli.

9 Halafu akamvika Aroni kilemba na upande wa mbele wa kilemba hicho akaweka pambo la dhahabu, taji takatifu, kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru.

10 Kisha Mose akachukua mafuta ya kupaka, akaipaka ile maskani na vitu vyote vilivyokuwa ndani yake akaviweka wakfu.

11 Alinyunyiza sehemu ya mafuta hayo juu ya madhabahu mara saba, akaipaka mafuta na vyombo vyake vyote, birika na tako lake, kuviweka wakfu.

12 Vilevile Mose akampaka Aroni mafuta kichwani ili kumweka wakfu.

13 Kisha Mose akawaleta wana wa Aroni akawavika joho na kuwafunga mikanda viunoni, na kuwavisha kofia kama alivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu.

14 Kisha Mose akamleta ng'ombe wa sadaka ya kuondoa dhambi, naye Aroni na wanawe wakaweka mikono yao juu ya kichwa cha ng'ombe huyo.

15 Mose akamchinja huyo ng'ombe, akachukua damu akazipaka pembe za madhabahu pande zote kwa kidole chake kuitakasa. Kisha akachukua damu iliyobaki akaimwaga chini kwenye tako la madhabahu ambayo aliweka wakfu kwa kuifanyia ibada ya upatanisho.

16 Kisha, akachukua mafuta yote yaliyokuwa kwenye matumbo yake, sehemu bora ya ini pamoja na figo zote mbili na mafuta yake na kuviteketeza juu ya madhabahu.

17 Lakini nyama ya ng'ombe huyo, ngozi yake na mavi yake, akaviteketeza kwa moto nje ya kambi kama alivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu.

18 Kisha, Mose akamleta kondoo dume wa sadaka ya kuteketezwa. Aroni na wanawe wakaweka mikono yao juu ya kichwa cha kondoo huyo.

19 Mose akamchinja na damu ya kondoo huyo akairashia madhabahu pande zake zote.

20 Alimkata huyo kondoo vipandevipande, akaviteketeza pamoja na kichwa chake na mafuta yake.

21 Baada ya matumbo na miguu kuoshwa kwa maji, Mose aliviteketeza vyote juu ya madhabahu pamoja na sehemu nyingine za huyo kondoo kama sadaka ya kuteketezwa. Hiyo ni sadaka itolewayo kwa moto, yenye harufu ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu. Mose alifanya kama alivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu.

22 Kisha akamleta kondoo dume mwingine, kwa ajili ya kuweka wakfu. Aroni na wanawe wakaweka mikono yao juu ya kichwa cha kondoo huyo.

23 Mose akamchinja. Akachukua damu ya kondoo huyo na kumpaka Aroni kwenye ncha ya sikio lake la kulia, kidole gumba cha mkono wake wa kulia na cha mguu wake wa kulia.

24 Wanawe Aroni nao wakaja, naye Mose akawapaka kiasi cha damu kwenye ncha za masikio yao ya kulia, vidole gumba vya mikono yao ya kulia na kwenye vidole gumba vya miguu yao ya kulia. Damu nyingine akainyunyizia madhabahu pande zake zote.

25 Kisha, akachukua mafuta yote, mkia pamoja na mafuta yake, mafuta yote yanayofunika matumbo, sehemu bora ya ini, pamoja na figo zote mbili, mafuta yake na paja la mguu wa kulia wa nyuma wa huyo kondoo dume.

26 Kisha, kwenye kile kikapu cha mikate iliyowekwa mbele ya Mwenyezi-Mungu akatoa mkate mmoja usiotiwa chachu, mkate mmoja wenye mafuta na mkate mmoja mdogo, akaviweka vyote juu ya vipande vya mafuta na ule mguu.

27 Mose akaviweka mikononi mwao Aroni na wanawe, nao wakafanya ishara ya kumtolea Mwenyezi-Mungu.

28 Kisha Mose akavichukua vitu hivyo vyote kutoka mikononi mwao na kuviteketeza juu ya madhabahu pamoja na sadaka ya kuteketezwa. Hii ni sadaka ya kuwekwa wakfu, yenye harufu ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu; ni sadaka itolewayo kwa moto.

29 Kisha Mose akachukua kile kidari na kufanya ishara ya kumtolea Mwenyezi-Mungu. Sehemu hiyo ya yule kondoo dume wa kuweka wakfu ni mali yake Mose kama alivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu.

30 Halafu Mose akachukua mafuta ya kupaka na damu kutoka madhabahu akamnyunyizia Aroni na wanawe hata na pia mavazi yao. Hivyo Mose akamweka wakfu Aroni na wanawe pamoja na mavazi yao.

31 Mose akamwambia Aroni na wanawe, “Chemsheni ile nyama mbele ya mlango wa hema la mkutano, muile hapo mlangoni pamoja na mkate kutoka katika kikapu chenye sadaka za kuwekea wakfu. Fanyeni kama nilivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu, kwamba sehemu hiyo italiwa na Aroni na wanawe.

32 Nyama yoyote au mkate wowote utakaosalia ni lazima kuteketezwa.

33 Hamtatoka nje ya mlango wa hema la mkutano kwa muda wote wa siku saba, yaani mpaka muda wenu wa kuwekwa wakfu umekwisha, muda ambao utachukua siku saba.

34 Mwenyezi-Mungu ameamuru tufanye kama tulivyofanya leo ili tuwafanyieni ibada ya upatanisho.

35 Mtabaki mlangoni mwa hema la mkutano usiku na mchana kwa muda wa siku saba, mkifanya mambo aliyoamuru Mwenyezi-Mungu, la sivyo mtakufa. Ndivyo nilivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu.”

36 Basi, Aroni na wanawe wakafanya mambo yote aliyoamuru Mwenyezi-Mungu kwa njia ya Mose.

9

1 Siku ya nane baada ya siku saba za kuwekwa wakfu, Mose akamwita Aroni na wanawe pamoja na wazee wa Israeli.

2 Mose akamwambia Aroni, “Chukua ndama dume kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi na kondoo dume kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa; wanyama wote wasiwe na dosari. Kisha watoe sadaka mbele ya Mwenyezi-Mungu.

3 Waambie Waisraeli wachukue beberu mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi, na ndama mmoja na mwanakondoo mmoja wote wa umri wa mwaka mmoja na wasio na dosari kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa,

4 fahali mmoja na kondoo dume mmoja kwa ajili ya sadaka za amani, wakamtolee Mwenyezi-Mungu pamoja na sadaka ya nafaka iliyochanganywa na mafuta kwa maana leo Mwenyezi-Mungu atawatokea.”

5 Waisraeli wakaleta vyote hivyo mbele ya hema la mkutano kama Mose alivyowaamuru na jumuiya yote ikaenda kusimama mbele ya Mwenyezi-Mungu.

6 Mose akawaambia, “Hili ndilo jambo ambalo Mwenyezi-Mungu aliwaamuru mlifanye ili utukufu wake uonekane kwenu.”

7 Hapo Mose akamwambia Aroni, “Nenda kwenye madhabahu, utolee hapo sadaka yako ya kuondoa dhambi na sadaka ya kuteketezwa na kufanya ibada ya upatanisho kwa ajili yako na kwa ajili ya watu wa Israeli. Kisha tolea hapo sadaka za watu na kuwafanyia ibada ya upatanisho kama alivyoamuru Mwenyezi-Mungu.”

8 Basi, Aroni akaikaribia madhabahu, akamchinja yule ndama aliyemtoa awe sadaka ya kuondoa dhambi yake mwenyewe.

9 Wanawe wakamletea damu, naye akachovya kidole chake katika damu hiyo na kuzipaka pembe za madhabahu. Damu iliyosalia akaimwaga kwenye tako la madhabahu.

10 Lakini mafuta na figo akaviteketeza vyote juu ya madhabahu kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.

11 Lakini ile ngozi akaiteketeza kwa moto nje ya kambi.

12 Kisha Aroni akamchinja mnyama wa sadaka ya kuteketezwa. Wanawe wakamletea damu, naye akainyunyizia madhabahu pande zote.

13 Kisha wakamletea sadaka ya kuteketezwa, kipande kimojakimoja, na kichwa; naye akaviteketeza juu ya madhabahu.

14 Akaosha matumbo na miguu na kuiteketeza pamoja na ile sadaka ya kuteketezwa kwenye madhabahu.

15 Kisha, Aroni akaweka mbele sadaka ya watu. Alimchukua mbuzi wa sadaka ya watu ya kuondoa dhambi, akamchinja na kumtoa sadaka ya kuondoa dhambi, kama alivyofanya kwa yule wa kwanza.

16 Kisha akaweka mbele ile sadaka ya kuteketezwa akatolea sadaka hiyo kulingana na agizo.

17 Kisha akaweka mbele sadaka ya nafaka akijaza konzi moja na kuiteketeza juu ya madhabahu pamoja na sadaka ya kuteketezwa ya kila asubuhi.

18 Halafu Aroni akamchinja pia fahali na yule kondoo dume wa sadaka za amani kwa ajili ya watu. Wanawe wakamletea damu ambayo aliinyunyizia madhabahu pande zote.

19 Mafuta ya fahali huyo na kondoo dume, mkia wa kondoo, mafuta yaliyofunika matumbo, figo na sehemu bora ya ini

20 wakayaweka juu ya vidari, naye akaviteketeza kwenye madhabahu.

21 Lakini vile vidari na ule mguu wa nyuma wa kulia, Aroni alifanya navyo ishara ya kumtolea Mwenyezi-Mungu, kama Mose alivyoamuru.

22 Aroni alipomaliza kutolea sadaka zote: Sadaka za kuondoa dhambi, sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani, aliwainulia watu mikono, akawabariki, kisha akashuka chini.

23 Ndipo Mose na Aroni wakaingia ndani ya hema la mkutano; walipotoka waliwabariki watu, nao utukufu wa Mwenyezi-Mungu ukaonekana kwa watu wote.

24 Mwenyezi-Mungu akawasha moto ukaiteketeza sadaka ya kuteketezwa na mafuta yaliyokuwa juu ya madhabahu. Watu wote walipouona huo moto walipaza sauti na kusujudu.

10

1 Nao Nadabu na Abihu, wanawe Aroni, walichukua kila mmoja chetezo chake, wakaweka moto na ubani, wakamtolea Mwenyezi-Mungu moto najisi, ambao haukulingana na agizo lake Mwenyezi-Mungu.

2 Basi, moto ukatokea mbele ya Mwenyezi-Mungu, ukawateketeza hao vijana, wakafa mbele yake.

3 Hapo, Mose akamwambia Aroni, “Kwa tukio hili Mwenyezi-Mungu amekuonesha maana ya kile alichosema: ‘Nitajionesha kuwa mtakatifu miongoni mwa wale walio karibu nami; nitatukuzwa mbele ya watu wote!’” Aroni akanyamaza kimya.

4 Basi, Mose akawaita Mishaeli na Elsafani, wanawe Uzieli, baba mdogo wa Aroni, akawaambia waje kuondoa maiti za ndugu zao maskani na kuzipeleka nje ya kambi.

5 Wakachukua maiti za ndugu zao na kuzipeleka nje ya kambi wakiwa wamevaa mavazi yao, kama Mose alivyoamuru.

6 Kisha Mose akamwambia Aroni na wanawe, Eleazari na Ithamari, “Msivuruge nywele zenu na wala msirarue mavazi yenu kuomboleza, la sivyo mtakufa na kuiletea jumuiya yote ghadhabu ya Mwenyezi-Mungu. Lakini ndugu zenu yaani jumuiya yote ya Israeli, wanaweza kuomboleza kwa sababu ya moto huo aliouleta Mwenyezi-Mungu.

7 Msitoke nje ya mlango wa hema la mkutano, la sivyo mtakufa; kwani mafuta ya kupaka ya Mwenyezi-Mungu yangali juu yenu.” Aroni na wanawe wakafanya kama Mose alivyosema.

8 Mwenyezi-Mungu aliongea na Aroni, akasema,

9 “Mnapoingia ndani ya hema la mkutano, wewe na wanao msinywe divai wala kileo chochote, la sivyo mtakufa. Hii itakuwa sheria ya kudumu katika vizazi vyenu vyote.

10 Ni lazima mtofautishe kati ya mambo matakatifu na mambo yasiyo matakatifu, kati ya mambo najisi na yasiyo najisi.

11 Mtawafundisha Waisraeli masharti yote ambayo nimewaambia kwa njia ya Mose.”

12 Mose akamwambia Aroni na wanawe waliosalia: Eleazari na Ithamari, “Chukueni ile sehemu ya sadaka ya nafaka iliyosalia kutoka sadaka anazotolewa Mwenyezi-Mungu kwa moto; muile karibu na madhabahu bila kutiwa chachu kwa sababu ni takatifu kabisa.

13 Mtaila katika mahali patakatifu kwa sababu hiyo ni haki yako na wazawa wako kutoka katika sadaka anazotolewa Mwenyezi-Mungu kwa moto. Hivyo ndivyo nilivyoamriwa.

14 Lakini kidari ambacho hufanywa nacho ishara ya kumtolea Mwenyezi-Mungu na mguu unaotolewa sadaka kama ishara, mnaweza kula mahali popote pasipo najisi. Utakula wewe, na watoto wako wa kiume na wa kike. Vitu hivyo umepewa kama haki yako na ya wazawa wako kutoka sadaka za amani za watu wa Israeli.

15 Ule mguu uliotolewa na kidari cha sadaka ya kufanyia ishara ya kumtolea Mwenyezi-Mungu watavileta pamoja na sadaka za mafuta zitolewazo kwa moto, ili kufanya ishara ya kuvitolea mbele ya Mwenyezi-Mungu, viwe sadaka ya kutolewa kwa ishara. Hivyo vitakuwa vyako pamoja na wanao; ni haki yenu milele kama Mwenyezi-Mungu alivyoamuru.”

16 Basi, Mose alichunguza kwa makini kuhusu mbuzi mmoja aliyetolewa sadaka ya kuondoa dhambi, kumbe akagundua kuwa alikwisha teketezwa. Hivyo akawakasirikia sana Eleazari na Ithamari, wana wa Aroni waliosalia, akawauliza,

17 “Kwa nini hamkumla katika mahali patakatifu kwa vile huyo ni kitu kitakatifu kabisa na mlikuwa mmepewa huyo ili kuondoa hatia ya jumuiya na kuwafanyia ibada ya upatanisho mbele ya Mwenyezi-Mungu?

18 Tena, kwa vile damu yake haikuletwa ndani ya mahali patakatifu, ni dhahiri iliwapasa kumla ndani ya mahali patakatifu kama nilivyoamuru.”

19 Aroni akamwambia Mose, “Tazama, leo wametolea sadaka yao ya kuondoa dhambi na sadaka ya kuteketezwa mbele ya Mwenyezi-Mungu; hata hivyo mambo haya yamenipata! Tena kama ningekula ile sadaka ya kuondoa dhambi hivi leo, je, ingekubalika mbele ya Mwenyezi-Mungu?”

20 Mose aliposikia hayo, akaridhika.

11

1 Mwenyezi-Mungu aliwaambia Mose na Aroni,

2 “Wawaambie Waisraeli hivi:

3 Kati ya wanyama wote duniani, mmeruhusiwa kula mnyama yeyote mwenye kwato zilizogawanyika sehemu mbili na ambaye hucheua.

4 Lakini msile mnyama yeyote ambaye hucheua lakini kwato zake hazikugawanyika sehemu mbili, au ambaye kwato zake zimegawanyika lakini hacheui. Msile ngamia, kwani hucheua lakini kwato zake hazikugawanyika sehemu mbili. Kwenu huyo ni najisi.

5 Pelele msimle; yeye hucheua lakini kwato zake hazikugawanyika; kwenu huyo ni najisi.

6 Sungura msimle; yeye hucheua lakini kwato zake hazikugawanyika; kwenu huyo ni najisi.

7 Nguruwe msimle; ana kwato zilizogawanyika lakini hacheui; kwenu huyo ni najisi.

8 Kwa sababu wanyama hao ni najisi msile nyama yao wala msiguse mizoga yao.

9 “Samaki yeyote wa baharini au mtoni mwenye mapezi na magamba, mnaweza kumla.

10 Lakini chochote kinachoishi baharini au mitoni, ambacho hakina mapezi wala magamba, yaani viumbe vyote viendavyo majini na viumbe vingine vyote viishivyo majini ni najisi kwenu.

11 Viumbe hivyo vitakuwa daima najisi kwenu. Msile nyama yao, wala msiiguse mizoga yao kwani ni najisi.

12 Chochote kinachoishi majini ambacho hakina mapezi na magamba ni najisi kwenu.

13 “Ndege wote wafuatao ni najisi kwenu; hivyo msile: Tai, furukombe, kipungu,

14 mwewe, aina zote za kozi,

15 aina zote za kunguru,

16 mbuni, kirukanjia, dudumizi, aina zote za kipanga,

17 bundi, mnandi, bundi kubwa,

18 mumbi, mwari, mderi,

19 korongo, aina zote za koikoi, hudihudi na popo.

20 “Wadudu wote wenye mabawa na waendao kwa miguu minne, hao ni najisi kwenu.

21 Lakini, baadhi ya wadudu wenye mabawa na wanakwenda kwa miguu minne ya kurukia ardhini mnaweza kula.

22 Hao ni: Kila aina ya nzige, kila aina ya senene, kila aina ya panzi na kila aina ya parare.

23 Lakini wadudu wengine wote wenye mabawa na miguu minne ni najisi kwenu.

24 “Kugusa wanyama fulanifulani humfanya mtu kuwa najisi; yeyote atakayegusa mizoga yao atakuwa najisi mpaka jioni.

25 Mtu akichukua sehemu ya mizoga yake atakuwa najisi mpaka jioni, na mavazi yake ni lazima yafuliwe.

26 Mtu yeyote akigusa mnyama mwenye kwato zilizogawanyika lakini hacheui, mtu huyo atakuwa najisi.

27 Wanyama wote waendao kwa vitanga vyao ingawa wana miguu minne, ni najisi kwenu; na yeyote atakayegusa mzoga wa mnyama kama huyo atakuwa najisi mpaka jioni.

28 Mtu yeyote anayebeba mzoga atakuwa najisi, naye atasafisha mavazi yake. Hao ni najisi kwenu.

29 “Viumbe vifuatavyo ni najisi kwenu: Kicheche, panya, kila aina ya mjombakaka,

30 guruguru, kenge, mijusi, goromwe, na kinyonga.

31 Hao wote ni najisi kwenu na yeyote atakayegusa mizoga yao, atakuwa najisi mpaka jioni.

32 Ikiwa mzoga wa viumbe hao unakiangukia kitu chochote, kiwe ni kifaa cha mbao au vazi au ngozi au gunia au chombo chochote kitumiwacho kwa kusudi lolote lile, chombo hicho kitakuwa najisi mpaka jioni. Ili kukifanya kiwe safi ni lazima kukiosha kwa maji.

33 Ikiwa mzoga wake umeangukia chombo cha udongo, basi, chochote kilicho ndani ya chombo hicho ni najisi na lazima chombo hicho kivunjwe.

34 Chakula au kinywaji chochote kilichokuwa ndani ya chombo hicho kitakuwa najisi.

35 Kila kitu ambacho sehemu ya mzoga imekiangukia, kitakuwa najisi. Ikiwa ni tanuri au jiko, ni lazima kivunjwe. Vitakuwa najisi navyo ni najisi kwenu.

36 Hata hivyo, kisima au chemchemi ya maji vitakuwa safi. Lakini chochote kinachogusa mzoga kitakuwa najisi.

37 Iwapo sehemu ya mzoga inaziangukia mbegu za kupanda, mbegu hizo hazitakuwa najisi.

38 Lakini ikiwa mbegu zimetiwa katika maji ili kuota na sehemu yoyote ya mzoga ikaziangukia, basi, mbegu hizo ni najisi kwenu.

39 “Iwapo mnyama yeyote mnayeruhusiwa kula, anakufa mwenyewe, yeyote atakayegusa mzoga wake, atakuwa najisi mpaka jioni.

40 Mtu yeyote akila nyama ya mzoga huo atafua mavazi yake na atakuwa najisi mpaka jioni. Na yeyote atakayebeba mzoga huo, atafua mavazi yake, naye atakuwa najisi mpaka jioni.

41 “Kiumbe chochote kitambaacho duniani ni najisi kwenu, kamwe msikile.

42 Chochote kiendacho kwa tumbo lake, chochote kiendacho kwa miguu yote minne au nyayo nyingi, naam, chochote kitambaacho, kamwe msikile kwa maana ni najisi kwenu.

43 Hivyo msije mkawa najisi kwa kula viumbe vitambaavyo na hivyo mkawa najisi.

44 Kwa kuwa mimi Mwenyezi-Mungu ndimi Mungu wenu, jiwekeni wakfu na kuwa watakatifu kwa maana mimi ni mtakatifu.

45 Kwa kuwa mimi Mwenyezi-Mungu ndimi niliyewatoa nchini Misri ili niwe Mungu wenu; kwa hiyo muwe watakatifu kwa maana mimi ni mtakatifu.”

46 Hiyo basi, ndiyo sheria kuhusu wanyama, ndege na viumbe vyote hai ambavyo huishi majini na nchi kavu,

47 ili kupambanua kati ya kisicho najisi na kilicho najisi; kinachoweza kuliwa na kisichoweza kuliwa.

12

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

2 “Waambie watu wa Israeli hivi: Mwanamke akipata mimba, akajifungua mtoto wa kiume, atakuwa najisi kwa muda wa siku saba kulingana na siku zake zihusikanazo na hali ya wanawake.

3 Mtoto huyo atatahiriwa katika siku yake ya nane.

4 Kisha mama mtoto ataendelea kuwa najisi kwa muda wa siku thelathini na tatu. Wakati huo, kamwe asiguse chochote kilichowekwa wakfu wala kuingia mahali patakatifu mpaka siku za kutakasika kwake zitakapotimia.

5 Lakini, kama amejifungua mtoto wa kike, basi, atakuwa najisi kwa muda wa majuma mawili kama ilivyo anapokuwa katika siku zake. Ataendelea katika kutakasika kwake kwa muda wa siku sitini na sita.

6 “Siku za kutakaswa kwake zitakapotimia, iwe amepata mtoto wa kiume au wa kike, atamletea kuhani mlangoni mwa hema la mkutano mwanakondoo wa mwaka mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa na kinda la njiwa au hua, kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi.

7 Kuhani atamtolea mbele ya Mwenyezi-Mungu na kumfanyia huyo mama ibada ya upatanisho mbele ya Mwenyezi-Mungu. Hivyo huyo mwanamke atakuwa safi kutokana na damu yake. Huo ni mwongozo kuhusu mwanamke yeyote anayejifungua mtoto wa kiume au wa kike.

8 “Kama hawezi kutoa mwanakondoo, basi, ataleta hua wawili au makinda mawili ya njiwa; mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa na mwingine kwa ajili ya sadaka ya kuondolea dhambi. Kuhani atamfanyia mama huyo ibada ya upatanisho, naye atakuwa safi.”

13

1 Mwenyezi-Mungu aliwaambia Mose na Aroni,

2 “Iwapo mtu yeyote atakuwa na uvimbe au upele au kipaku mwilini mwake, ikadhihirika kwamba ni ukoma, basi, ataletwa kwa kuhani Aroni au mmoja wa wanawe aliye kuhani.

3 Kuhani atapakagua mahali palipo na ugonjwa na ikiwa nywele za mahali hapo zimebadilika kuwa nyeupe na ugonjwa wenyewe ukionekana kuwa uko ndani zaidi ya ngozi ya mwili wake, basi, huo ni ukoma. Kuhani akimaliza kumkagua, hivyo atatangaza kuwa mtu huyo ni najisi.

4 Lakini ikiwa kipele hicho, ingawa cheupe hakikuingia ndani sana ya ngozi na wala nywele za mahali hapo hazikubadilika kuwa nyeupe, basi, kuhani atamtenga mtu huyo kwa muda wa siku saba.

5 Siku ya saba, kuhani atamwangalia tena mtu huyo, na ikiwa, kulingana na uchunguzi wa kuhani, ugonjwa huo haujaenea kwenye ngozi yake, basi, kuhani atamtenga mtu huyo kwa siku nyingine saba.

6 “Kuhani atamkagua tena mtu huyo siku ya saba. Kama kulingana na uchunguzi wake, ile sehemu ya ugonjwa imefifia na ugonjwa haujaenea, basi, kuhani atamtangaza mtu huyo kuwa safi; huo ni upele tu. Mtu huyo atafua mavazi yake, naye atakuwa safi.

7 Lakini upele huo ukiwa umeenea kwenye ngozi, baada ya mtu huyo kujionesha kwa kuhani kwa ajili ya kutakaswa kwake, basi, atakuja tena kwa kuhani.

8 Kuhani atamwangalia tena, na kama ule upele umeenea kwenye ngozi, basi, kuhani atamtangaza mtu huyo kuwa najisi; huo ni ukoma.

9 “Kama mtu ameshikwa na ukoma, ataletwa kwa kuhani.

10 Kuhani atamwangalia na kama kuna uvimbe mweupe ambao umezifanya nywele zake ziwe nyeupe na uvimbe huo umegeuka kuwa kidonda kibichi,

11 huo ni ukoma wa muda mrefu. Kuhani atamtangaza mtu huyo kuwa najisi. Hakuna haja ya kumweka mtu huyo kwa uchunguzi kwani yu najisi tayari.

12 Kama ukoma umemshika na umeenea mwili mzima, toka utosini hadi nyayoni kama atakavyoona kuhani,

13 hapo kuhani atamwangalia. Kuhani akiona kuwa ukoma umemwenea mwili mzima, basi, atamtangaza mtu huyo kuwa safi kwa sababu mwili umegeuka kuwa mweupe na hivyo mtu huyo yu safi.

14 Lakini kukionekana mwilini mwa mtu huyo kidonda kibichi, basi, mtu huyo atakuwa najisi.

15 Kuhani ataangalia hicho kidonda kibichi na kumtangaza kuwa ni najisi kwa sababu huo ni ukoma.

16 Lakini hicho kidonda kikigeuka tena kuwa cheupe, mtu huyo atarudi kwa kuhani.

17 Kuhani atamwangalia na akiona kuwa kimegeuka kuwa cheupe, basi, atamtangaza mtu huyo kuwa safi.

18 “Kama mtu ameshikwa na jipu, nalo limepona,

19 lakini mahali pale lilipokuwa jipu pamegeuka kuwa uvimbe mweupe au kuwa pekundu lakini peupe kiasi, ni lazima kumwonesha kuhani.

20 Kuhani atamwangalia huyo mtu. Kuhani akiona pamegeuka kuwa na shimo na nywele za mahali hapo zimegeuka kuwa nyeupe, basi, kuhani atamtangaza mtu huyo kuwa najisi; huo ni ugonjwa wa ukoma ambao umetokana na jipu.

21 Lakini kama kuhani atamwangalia huyo mtu na kuona kuwa nywele za mahali hapo si nyeupe na wala hakuna shimo, ila pamefifia, basi, atamtenga huyo mtu kwa muda wa siku saba.

22 Kama ugonjwa huo utaenea kwenye ngozi, basi, kuhani atamtangaza mtu huyo kuwa najisi; sehemu hiyo ina ugonjwa.

23 Lakini, kama ile sehemu haijaenea, basi, lile ni kovu la jipu tu. Kuhani atamtangaza mtu huyo kuwa safi.

24 “Au, Iwapo kuna mahali palipoungua na ile nyama mbichi imegeuka kuwa nyekundu-nyeupe au ni nyeupe,

25 kuhani atapaangalia. Kama akiona kuwa nywele zimegeuka kuwa nyeupe na pana shimo, basi, huo ni ukoma. Ukoma huo umejitokeza kwa njia ya mahali hapo palipoungua. Kuhani atamtangaza mtu huyo kuwa najisi; kwani anao ugonjwa wa ukoma.

26 Lakini kama kuhani akiona kuwa nywele za mahali hapo si nyeupe na hakuna shimo ila pamefifia, basi, kuhani atamtenga mtu huyo kwa muda wa siku saba.

27 Siku ya saba kuhani atamwangalia. Kama umeenea kwenye ngozi, basi, kuhani atamtangaza mtu huyo kuwa najisi; kwani anao ugonjwa wa ukoma.

28 Lakini, kama ile alama haijaenea, ila imefifia, huo ni uvimbe uliotokana na kuungua; basi, kuhani atamtangaza mtu huyo kuwa safi; kwani hilo ni kovu la kuungua.

29 “Kama mtu yeyote mwanamume au mwanamke, ana kidonda kichwani au kidevuni,

30 kuhani atauangalia ugonjwa huo. Iwapo kuhani ataona kuwa kuna shimo na nywele ni manjano na nyembamba, basi, atamtangaza mtu huyo kuwa najisi; kwani huo ni upele na ni ukoma wa kichwa au wa kidevu.

31 Kama kuhani ataona kuwa hakuna shimo na nywele si nyeusi, basi kuhani atamtenga mtu huyo kwa muda wa siku saba.

32 Siku ya saba kuhani atakiangalia kile kidonda. Kama kidonda hicho hakijaenea na hakuna nywele zenye rangi ya manjano wala hakuna vipele vyovyote mahali hapo, basi,

33 mtu huyo atanyoa nywele au ndevu zake. Lakini mahali pale penye vipele hatapanyoa. Kisha kuhani atamtenga mtu huyo kwa muda mwingine wa siku saba.

34 Siku ya saba, kuhani ataviangalia vile vipele. Iwapo kuhani ataona kuwa vipele hivyo havikuenea kwenye ngozi na wala havikwenda ndani ya ngozi, basi, atamtangaza mtu huyo kuwa safi. Mtu huyo atafua mavazi yake, naye atakuwa safi.

35 Lakini iwapo vipele hivyo vimeenea baada ya kutakaswa,

36 mtu huyo ataangaliwa na kuhani na ikiwa vimeenea kwenye ngozi, kuhani hatahitaji kutafuta nywele zenye rangi manjano; mtu huyo atakuwa najisi.

37 Lakini iwapo kuhani ataona kuwa vile vipele vimepona na nywele nyeusi zimeota mahali hapo, basi, vidonda hivyo vimepona, basi, mtu huyo ni safi. Kuhani atamtangaza mtu huyo kuwa safi.

38 “Kama mtu yeyote, awe mwanamume au mwanamke, ana alama nyeupe mwilini mwake,

39 kuhani atamwangalia mtu huyo. Iwapo kuhani ataona kuwa alama hizo ni nyeupe kiasi, huo ni upele wa kawaida; mtu huyo ni safi.

40 “Kama mwanamume amepata upara, yeye ni safi kwani ana upara tu.

41 Iwapo upara huo umetanda tangu nyuma mpaka mbele mtu huyo ana upara tu na yu safi.

42 Lakini kama kwenye kichwa penye upara au kwenye paji la uso penye upara kuna alama nyekundu-nyeupe, huo ni ukoma unaotokea kwenye upara wake kichwani au kwenye paji lake.

43 Kuhani atamwangalia. Iwapo kuhani ataona kuwa huo uvimbe ni mwekundu-mweupe kwenye upara au kwenye paji lake na unaonekana kama ukoma kwenye ngozi yake,

44 basi, mtu huyo ana ukoma; yeye ni najisi. Kuhani atamtangaza mtu huyo kuwa najisi. Ugonjwa wake upo kwenye kichwa chake.

45 “Mwenye ukoma yeyote atavaa nguo zilizochanika, nywele zake hatazichana, na mdomo wake wa juu ataufunika na atapaza sauti akisema, ‘Mimi ni najisi, mimi ni najisi.’

46 Ataendelea kuwa najisi kwa muda wote alio na ugonjwa huo. Yeye ni najisi; naye atakaa peke yake nje ya kambi.”

47 “Kama kuna namna ya upele wa ukoma kwenye vazi, liwe la sufu au kitani,

48 vazi hilo liwe limefumwa au limesokotwa kwa kitani au sufu au ni vazi la ngozi ya aina yoyote ile,

49 iwapo upele huo una rangi ya kijani au nyekundu katika vazi hilo, basi, vazi hilo lina upele. Kwa hiyo ni lazima kumwonesha kuhani.

50 Kuhani atauangalia upele huo na kuliweka vazi hilo kando kwa muda wa siku saba.

51 Siku ya saba atauangalia upele huo. Ikiwa upele huo umeenea katika vazi hilo, liwe ni la kufuma au kusokotwa au la ngozi au la ngozi ya aina yoyote ile, vazi hilo lina upele. Hivyo vazi hilo ni najisi.

52 Kuhani atalichoma moto vazi hilo kwani lina namna ya upele wa ukoma.

53 “Kama kuhani ataona kuwa upele haukuenea katika vazi, basi,

54 ataamuru vazi hilo lifuliwe na kuwekwa kando kwa muda mwingine wa siku saba.

55 Kuhani ataliangalia hilo vazi baada ya kuoshwa. Ikiwa ile alama haijabadilika rangi yake hata ingawa upele haukuenea, basi, vazi hilo ni najisi. Vazi hilo utalichoma moto, iwe alama ya upele ipo nyuma au mbele ya vazi hilo.

56 “Kama kuhani ataona kuwa ile alama imefifia baada ya kufuliwa, basi atararua ile sehemu iliyo na namna ya upele wa ukoma.

57 Kisha, ikiwa hiyo alama inaonekana tena baadaye katika vazi lililofumwa au lililosokotwa au katika kitu chochote cha ngozi, basi upele umeenea. Hapo vazi hilo utalichoma moto.

58 Lakini vazi ambalo upele umetokea baada ya kulifua itabidi lifuliwe mara ya pili na hivyo lipate kuwa safi.”

59 Hiyo ni sheria kuhusu namna ya upele wa ukoma unaotokea katika vazi la sufu au kitani au lililofumwa au lililosokotwa au la ngozi. Kwa njia hiyo mtaweza kupambanua kati ya vazi lisilo najisi na lile lililo najisi.

14

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

2 “Ifuatayo ni sheria kumhusu mwenye ukoma katika siku ya kutakaswa kwake. Baada ya kupona ataletwa kwa kuhani.

3 Kuhani atakwenda kumwangalia huyo mtu nje ya kambi. Ikiwa ukoma huo umepona,

4 basi, kuhani ataamuru watu walete ndege wawili safi walio hai, kipande cha mwerezi, sufu ya rangi nyekundu na tawi la husopo kwa ajili ya huyo mtu atakayetakaswa.

5 Kuhani atawaamuru wamchinje ndege mmoja katika chungu chenye maji safi ya chemchemi.

6 Kuhani atamchukua yule ndege mwingine hai, kipande kile cha mwerezi, sufu ya rangi nyekundu na lile tawi la husopo na kuvitumbukiza vyote katika damu ya yule ndege aliyechinjwa.

7 Kisha, atamnyunyizia huyo mwenye kutakaswa ile damu mara saba, halafu atamtangaza mtu huyo kuwa safi. Yule ndege hai atamwacha aende zake mashambani nje ya mji.

8 Huyo mtu atayafua mavazi yake, atanyoa nywele zake, na kuoga; naye atakuwa safi. Baada ya hayo atarudi kambini, lakini atakaa nje ya hema lake kwa muda wa siku saba.

9 Siku ya saba atanyoa nywele zake zote, ndevu na kope za macho yake. Kisha atafua mavazi yake na kuoga, ataoga kwa maji; naye atakuwa safi.

10 “Siku ya nane ataleta wanakondoo madume wawili wasio na dosari, kondoo jike wa mwaka mmoja asiye na dosari, kilo tatu za unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya sadaka ya nafaka pamoja na mafuta theluthi moja ya lita.

11 Kuhani atakayemtakasa mtu huyo atamleta mbele ya Mwenyezi-Mungu karibu na mlango wa hema la mkutano pamoja na vitu alivyoleta.

12 Kuhani atachukua mwanakondoo dume mmoja na kumtolea sadaka ya kuondoa hatia pamoja na yale mafuta theluthi moja ya lita. Atafanya ishara ya kuvitolea mbele ya Mwenyezi-Mungu.

13 Kisha atamchinja huyo mwanakondoo katika mahali patakatifu, wanapochinjia wanyama wa sadaka ya kuondoa dhambi na sadaka ya kuteketezwa. Sadaka hii ya kuondoa hatia, kama ilivyo sadaka ya kuondoa dhambi, ni mali yake kuhani; ni sadaka takatifu kabisa.

14 Kuhani atachukua kiasi cha damu ya sadaka ya kuondoa hatia na kumpaka mtu anayetakaswa katika ncha ya sikio lake la kulia na kidole gumba cha mkono wake wa kulia na kidole gumba cha mguu wake wa kulia.

15 Kisha, kuhani atachukua kiasi cha ile theluthi moja ya mafuta na kuyatia katika kiganja cha mkono wake wa kushoto.

16 Atachovya kidole cha mkono wake wa kulia katika mafuta hayo na kumnyunyizia huyo mtu anayetakaswa mara saba mbele ya Mwenyezi-Mungu.

17 Kiasi cha mafuta yanayobaki katika kiganja chake atampaka huyo mtu anayetakaswa katika ncha ya sikio lake la kulia na kidole gumba cha mkono wake wa kulia na kidole gumba cha mguu wake wa kulia, mahali palepale alipompaka damu ya sadaka ya kuondoa hatia.

18 Yale mafuta yaliyobaki atampaka huyo mtu kichwani. Hivyo kuhani atamfanyia ibada ya upatanisho mbele ya Mwenyezi-Mungu.

19 Kuhani atatolea sadaka ya kuondoa dhambi na kumfanyia huyo mtu anayetakaswa ibada ya upatanisho ili kumwondolea unajisi wake. Kisha atamchinja mwanakondoo wa sadaka ya kuteketezwa.

20 Kuhani atatolea ile sadaka ya kuteketezwa na sadaka ya nafaka juu ya madhabahu. Hivyo kuhani atamfanyia huyo mtu ibada ya upatanisho, naye atakuwa safi.

21 “Lakini ikiwa mtu huyo ni maskini, hana uwezo wa kutoa vitu hivyo, basi ataleta mwanakondoo dume mmoja kuwa fidia ya sadaka ya kuondoa hatia ambaye atafanyiwa ishara ya kutoa sadaka ili kumfanyia huyo mtu ibada ya upatanisho. Ataleta pia kilo moja ya unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya sadaka ya nafaka na mafuta theluthi moja ya lita.

22 Ataleta pia hua wawili au makinda mawili ya njiwa kadiri anavyoweza mmoja atakuwa kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi na mwingine kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa.

23 Siku ya nane atamletea kuhani vitu hivyo mbele ya mlango wa hema la mkutano kwa ajili ya utakaso wake mbele ya Mwenyezi-Mungu.

24 Kuhani atamchukua huyo mwanakondoo dume wa sadaka ya kuondoa hatia pamoja na yale mafuta theluthi moja ya lita na kufanya ishara ya kuvitolea mbele ya Mwenyezi-Mungu.

25 Atamchinja huyo mwanakondoo dume wa sadaka ya kuondoa hatia. Kuhani atachukua kiasi cha damu na kumpaka huyo mtu anayetakaswa katika ncha ya sikio lake la kulia, katika kidole gumba cha mkono wake wa kulia na kidole gumba cha mguu wake wa kulia.

26 Kuhani atatia kiasi cha mafuta hayo katika kiganja cha mkono wake wa kushoto.

27 Kisha atamnyunyizia huyo mtu kwa kidole chake cha kulia kiasi cha hayo mafuta yaliyomo katika kiganja chake cha kushoto mara saba mbele ya Mwenyezi-Mungu.

28 Kuhani atampaka huyo mtu anayetakaswa mafuta katika ncha ya sikio lake la kulia, katika kidole gumba cha mkono wake wa kulia, na kidole gumba cha mguu wake wa kulia. Atampaka mahali pale ambapo alimpaka ile damu ya sadaka ya kuondoa hatia.

29 Mafuta yanayosalia mkononi mwake atampaka huyo mtu kichwani, ili kumfanyia ibada ya upatanisho mbele ya Mwenyezi-Mungu.

30 Kisha kuhani atamchukua mmoja wa wale hua au njiwa wawili kadiri mtu huyo anavyoweza kuleta.

31 Hua atakuwa kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi na mwingine kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa. Pamoja na hao, atatoa sadaka ya nafaka; naye kuhani atamfanyia huyo mtu ibada ya upatanisho mbele ya Mwenyezi-Mungu.

32 Huo ndio mwongozo kuhusu mtu mwenye ukoma asiyeweza kutoa sadaka za kumtakasa.”

33 Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose na Aroni,

34 “Mtakapoingia katika nchi ya Kanaani ambayo ninawapa kuwa milki yenu, nami nikafanya namna ya upele wa ukoma uote katika ukuta wa nyumba fulani katika nchi mtakayoimiliki,

35 basi, mwenye nyumba hiyo ni lazima amwambie kuhani kwamba namna ya upele wa ukoma umeonekana katika nyumba yake.

36 Kuhani ataamuru vitu vyote ndani ya nyumba hiyo vitolewe kabla yeye mwenyewe hajaanza uchunguzi wake; visije vyote kutangazwa kuwa najisi. Kisha kuhani ataingia kuiangalia nyumba hiyo.

37 Atauchunguza upele huo; kama upele huo umeonekana ukutani na umesababisha madoa ya rangi ya kijani kibichi au nyekundu na kuonekana kuwa yamepenya ndani ya kuta,

38 basi, kuhani atatoka nje mlangoni na kuifunga nyumba hiyo kwa muda wa siku saba.

39 Siku ya saba kuhani atarudi na kuiangalia tena nyumba hiyo. Ikiwa upele huo umeenea katika kuta za nyumba hiyo,

40 kuhani ataamuru mawe yaliyoko kwenye sehemu zenye upele yatolewe na kutupwa mahali najisi nje ya mji.

41 Lipu ya nyumba hiyo itabanduliwa na kifusi chake kutupwa mahali najisi nje ya mji.

42 Kisha watachukua mawe mapya na kujenga mahali walipobomoa; nao wataipiga nyumba hiyo lipu upya.

43 “Ikiwa upele huo utatokea tena baada ya kutoa mawe hayo na kukwangua lipu na kuipiga lipu upya,

44 yapasa kuhani aje kuichunguza. Ikiwa upele umeenea katika nyumba hiyo, basi huo ni upele wa kufisha; nyumba hiyo ni najisi.

45 Nyumba hiyo ni lazima ibomolewe na mawe yake, miti yake na lipu vipelekwe mahali najisi nje ya mji.

46 Zaidi ya hayo, yeyote atakayeingia ndani ya nyumba hiyo wakati itakapokuwa imefungwa, atakuwa najisi mpaka jioni.

47 Yeyote anayelala katika nyumba hiyo au kulia chakula ndani yake, lazima ayafue mavazi yake.

48 “Lakini ikiwa baada ya kuikagua nyumba hiyo, kuhani ataona kuwa upele haujaenea baada ya kupigwa lipu, basi, kuhani atatangaza kuwa nyumba hiyo ni safi kwani upele umekwisha.

49 Ili kuitakasa nyumba hiyo, mwenye nyumba ataleta ndege wawili pamoja na kipande cha mwerezi, sufu nyekundu na tawi la husopo.

50 Atamchinja ndege mmoja katika chungu chenye maji safi ya chemchemi.

51 Atachukua kipande cha mwerezi, tawi la husopo na ile sufu nyekundu pamoja na yule ndege mwingine aliye hai na kuvitumbukiza vyote katika damu ya yule ndege aliyechinjwa. Kisha atainyunyizia nyumba hiyo damu mara saba.

52 Hivyo ndivyo atakavyoitakasa nyumba hiyo kwa damu ya ndege, maji safi ya chemchemi, ndege hai, kipande cha mwerezi, tawi la husopo na ile sufu nyekundu.

53 Yule ndege hai atamwacha aende zake mashambani nje ya mji. Hivyo ndivyo atakavyoitakasa nyumba hiyo, nayo itakuwa safi.”

54 Hii ndiyo sheria kuhusu aina yoyote ya namna ya upele wa ukoma;

55 upele katika nguo au nyumba,

56 uvimbe, jipu au kipaku,

57 ili kuonesha ni kitu gani kilicho najisi na kisicho najisi. Hiyo ndiyo sheria kuhusu namna ya upele wa ukoma.

15

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose na Aroni,

2 “Waambieni Waisraeli hivi: Mwanamume yeyote akitokwa na usaha, usaha huo wamfanya kuwa najisi.

3 Na ufuatao ni mwongozo kuhusu najisi hiyo: Muda wote anapotokwa na usaha au usaha unapokuwa umezuiwa ndani yake, mtu huyo ni najisi.

4 Kitanda chochote atakacholalia au atakachokalia, kitakuwa najisi.

5 Mtu yeyote atakayegusa kitanda chake mtu huyo ni lazima ayafue mavazi yake, na kuoga; naye atakuwa najisi mpaka jioni.

6 Mtu yeyote atakayekalia kitu chochote alichokalia huyo mtu mwenye kutokwa na usaha, ni lazima ayafue mavazi na kuoga; na atakuwa najisi hadi jioni.

7 Mtu yeyote atakayemgusa mtu atokwaye na usaha, lazima afue mavazi yake na kuoga; naye atakuwa najisi mpaka jioni.

8 Mtu yeyote akitemewa mate na mtu anayetokwa usaha ni lazima mtu huyo aliyetemewa mate ayafue mavazi yake, na kuoga; naye atakuwa najisi mpaka jioni.

9 Tandiko lolote la mnyama aliloketia mtu anayetokwa na usaha litakuwa najisi.

10 Mtu yeyote atakayegusa kitu chochote alichokalia mtu huyo, atakuwa najisi mpaka jioni. Mtu yeyote anayebeba kitu chochote kilichokuwa cha mtu huyo ni lazima ayafue mavazi yake, na kuoga; naye atakuwa najisi mpaka jioni.

11 Mtu yeyote anayetokwa na usaha akimgusa mtu bila kusafisha kwanza mikono yake na kuoga, aliyeguswa atakuwa najisi mpaka jioni.

12 Chombo chochote cha udongo kilichoguswa na mtu anayetokwa na usaha ni lazima kivunjwe. Lakini chombo chochote cha mbao ni lazima kisafishwe kwa maji.

13 “Mwanamume yeyote anayetokwa na usaha akiponywa ugonjwa wake, ni lazima huyo mtu angoje siku saba kabla ya kuondolewa unajisi wake. Atayafua mavazi yake na kuoga kwa maji ya mtoni; naye atakuwa safi.

14 Siku ya nane, ni lazima alete hua wawili au makinda mawili ya njiwa mbele ya Mwenyezi-Mungu mlangoni mwa hema la mkutano na kumkabidhi kuhani.

15 Kuhani atawatoa hao, mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi na mwingine kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa; naye kuhani atamfanyia huyo mtu ibada ya upatanisho mbele ya Mwenyezi-Mungu na kumwondolea unajisi wake wa kutokwa na usaha.

16 “Kama mwanamume yeyote akitokwa na shahawa yake, ni lazima aoge mwili mzima kwa maji, naye atakuwa najisi mpaka jioni.

17 Vazi lolote lililodondokewa shahawa au ngozi yoyote iliyoguswa na shahawa hiyo ni lazima ioshwe kwa maji, na itakuwa najisi mpaka jioni.

18 Kama mwanamume akilala na mwanamke, akatokwa na shahawa, basi, ni lazima wote wawili waoge kwa maji, nao watakuwa najisi mpaka jioni.

19 “Mwanamke yeyote anapokuwa mwezini, atakuwa najisi kwa muda wa siku saba. Mtu yeyote atakayemgusa mwanamke huyo atakuwa najisi mpaka jioni.

20 Kitu chochote anacholalia au kukalia wakati yu najisi, kitakuwa najisi.

21 Mtu yeyote atakayegusa kitanda cha huyo mwanamke ni lazima ayafue mavazi yake na kuoga kwa maji; naye atakuwa najisi mpaka jioni.

22 Mtu yeyote atakayegusa kitu chochote anachokalia mwanamke huyo ni lazima ayafue mavazi yake na kuoga kwa maji, naye atakuwa najisi mpaka jioni.

23 Mwanamume yeyote atakayegusa kitu chochote alicholalia au kukalia huyo mwanamke, atakuwa najisi mpaka jioni.

24 Kama mwanamume akilala na mwanamke huyo na damu ya huyo mwanamke ikamdondokea huyo mwanamume, basi, mwanamume huyo atakuwa najisi kwa muda wa siku saba. Kitanda chochote atakacholalia huyo mwanamume kitakuwa najisi.

25 “Kama mwanamke anatokwa na damu kwa muda wa siku nyingi kuliko ilivyo kawaida au anatokwa damu wakati usio wa majira yake ya kutokwa damu, basi, ataendelea kuwa najisi muda wote damu inapomtoka.

26 Kitanda chochote anacholalia wakati huo au kiti chochote anachokalia, kitakuwa najisi sawa kama wakati wa unajisi wake wa kutokwa damu.

27 Mtu yeyote atakayegusa vitu hivyo, atakuwa najisi na ni lazima ayafue mavazi yake na kuoga; naye atakuwa najisi mpaka jioni.

28 Baada ya kukauka damu yake mwanamke huyo atangoja hadi siku saba ili kuwa safi; na baada ya muda huo atakuwa safi.

29 Siku ya nane atachukua hua wawili au makinda mawili ya njiwa na kumletea kuhani mlangoni mwa hema la mkutano.

30 Kuhani atamtoa mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi na mwingine kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa. Hivyo kuhani atamfanyia huyo mwanamke ibada ya upatanisho mbele ya Mwenyezi-Mungu na kumwondolea unajisi wake wa kutokwa damu.

31 “Ndivyo mtakavyowatahadharisha Waisraeli na unajisi wao, wasije wakaikufuru maskani yangu takatifu iliyo miongoni mwao wakiingia humo na unajisi wao; wakifanya hivyo watauawa.”

32 Hiyo ndiyo sheria kuhusu mwanamume anayetokwa na usaha na anayetokwa na shahawa na kuwa najisi.

33 Sheria hiyo yamhusu pia mwanamke anayetokwa damu na kuwa najisi. Sheria hiyo yamhusu mwanamume au mwanamke yeyote anayetokwa na chochote na pia yahusu mwanamume anayelala na mwanamke ambaye ni najisi.

16

1 Mwenyezi-Mungu alizungumza na Mose, baada ya wana wawili wa Aroni kufa wakati ule walipomkaribia.

2 Alimwambia, “Mwambie ndugu yako Aroni asiingie mahali patakatifu nyuma ya pazia wakati usiokubaliwa. Asiingie mahali hapo kwani ndipo nitakapotokea katika wingu juu ya kiti cha rehema. Asipotii, atakufa.

3 Aroni ataingia mahali patakatifu sana akiwa na fahali mchanga kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi na kondoo dume kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa.

4 Ataoga mwili wote katika maji, kisha atavaa mavazi matakatifu. Ataingia mahali hapo akiwa amevaa mavazi matakatifu: Joho la kitani baada ya nguo ya ndani ya suruali ya kitani na akiwa amevaa kanzu ya kitani na kujifunga mkanda wa kitani.

5 Atatwaa kutoka jumuiya ya watu wa Israeli beberu wawili kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi na kondoo dume mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa.

6 “Aroni atamtoa huyo fahali sadaka ya kuondoa dhambi kwa ajili yake mwenyewe, na kufanya ibada ya upatanisho kwa ajili yake mwenyewe na jamaa yake.

7 Kisha, wale beberu wawili atawaweka kwenye mlango wa hema la mkutano.

8 Atawapigia kura hao beberu wawili, kura moja kwa ajili ya Mwenyezi-Mungu na nyingine kwa ajili ya Azazeli.

9 Atamleta yule beberu ambaye kura ilimtaka kwa ajili ya Mwenyezi-Mungu na kumtolea sadaka ya kuondoa dhambi.

10 Lakini yule beberu aliyetakiwa na kura kwa ajili ya Azazeli atatolewa mbele ya Mwenyezi-Mungu akiwa hai ili kufanya ibada ya upatanisho kuhani atamwacha aende jangwani kwa Azazeli, ili kuondoa dhambi za jumuiya.

11 “Aroni atamtoa fahali wa sadaka ya kuondoa dhambi kwa ajili yake mwenyewe, na kufanya ibada ya upatanisho kwa ajili yake mwenyewe na kwa ajili ya jamaa yake, kisha atamchinja fahali huyo sadaka ya kuondoa dhambi.

12 Halafu atachukua chetezo na kutwaa makaa madhabahuni mbele ya Mwenyezi-Mungu na ubani konzi mbili uliosagwa vizuri sana.

13 Ili asije akafa, atauleta ubani huo mbele ya Mwenyezi-Mungu na kuutia katika moto ili moshi wa ubani huo ukifunike kifuniko cha sanduku la agano.

14 Atachukua kiasi cha damu ya yule fahali na kunyunyiza kwa kidole chake upande wa mashariki juu ya kiti cha rehema kisha atainyunyizia mbele ya sanduku la agano mara saba kwa kidole chake.

15 “Halafu atamchinja yule beberu wa sadaka ya kuondoa dhambi kwa ajili ya watu wote. Damu ya mbuzi huyo ataileta ndani mahali patakatifu sana na kufanya kama alivyofanya na damu ya yule fahali; atainyunyiza juu ya kiti cha rehema, upande wake wa mbele.

16 Hivyo atafanya ibada ya upatanisho kwa ajili ya mahali patakatifu kwa sababu ya unajisi, makosa na dhambi zote za Waisraeli. Ndivyo atakavyofanya pia kwa ajili ya hema la mkutano lililo miongoni mwa watu hao walio najisi.

17 Wakati Aroni anafanya ibada ya upatanisho kwa ajili yake mwenyewe, jamaa yake na jamii nzima ya Israeli, kamwe asiwepo mtu yeyote ndani ya hema la mkutano hadi atakapokuwa amemaliza na kutoka nje.

18 Kisha atatoka na kwenda kwenye madhabahu iliyo mbele ya Mwenyezi-Mungu na kuifanyia ibada ya upatanisho. Atachukua kiasi cha damu ya yule fahali na ya yule mbuzi na kuzipaka pembe za madhabahu pande zote.

19 Atainyunyizia madhabahu hiyo damu kwa kidole chake mara saba na hivyo kuiweka wakfu na kuitakasa unajisi wote wa watu wa Israeli.

20 “Baada ya Aroni kumaliza kupatakasa mahali patakatifu, hema la mkutano na madhabahu, ndipo atamtoa yule beberu kwa ajili ya Azazeli, akiwa hai.

21 Aroni ataweka mikono yake juu ya kichwa cha huyo beberu hai na kuuungama juu yake dhambi zote za watu wa Israeli, makosa yao yote na dhambi zao zote, ili kumwajibisha huyo. Kisha atamwacha huyo beberu aende jangwani akipelekwa huko na mtu yeyote anayejitoa kwa hiari.

22 Atamwacha huyo beberu aende jangwani, mahali pasipokuwa na watu, akiwa ameyachukua maovu yao yote.

23 “Kisha Aroni atarudi ndani ya hema la mkutano, atavua yale mavazi aliyovaa alipoingia mahali patakatifu sana na kuyaacha humo.

24 Ataoga humo ndani katika mahali patakatifu na kuvaa mavazi yake. Atatoka na kutoa sadaka yake ya kuteketezwa, na sadaka ya kuteketezwa ya watu wa Israeli, ili kufanya ibada ya upatanisho kwa ajili yake mwenyewe na kwa ajili ya watu wote.

25 Mafuta ya sadaka ya kuondoa dhambi atayateketeza juu ya madhabahu.

26 Yule mtu aliyempeleka yule beberu kwa Azazeli kwanza atayafua mavazi yake na kuoga ndipo atakapoweza kuingia kambini.

27 Yule fahali na mbuzi waliotolewa sadaka ya kuondoa dhambi ambao damu yao ilipelekwa mahali patakatifu sana ili kufanya ibada ya upatanisho, watapelekwa nje ya kambi na kuteketezwa. Ngozi zao, nyama na mavi yao, vyote vitateketezwa.

28 Yule mtu atakayewateketeza atayafua mavazi yake na kuoga, ndipo atakapoweza kuingia kambini.

29 “Hili ni sharti ambalo mnapaswa kulifuata milele: Siku ya kumi ya mwezi wa saba, nyinyi wenyewe na hata wageni wanaoishi miongoni mwenu, ni lazima mfunge siku hiyo na kuacha kufanya kazi.

30 Mtafanya hivyo kwa sababu siku hiyo ndiyo siku ambayo mtafanyiwa ibada ya upatanisho, msafishwe dhambi zenu, nanyi mtakuwa safi mbele ya Mwenyezi-Mungu.

31 Siku hiyo ni siku ya mapumziko kamili nanyi mtafunga. Kanuni hiyo ni ya kudumu milele.

32 Kuhani aliyepakwa mafuta na kuwekwa wakfu ashike nafasi ya baba yake, ndiye atakayefanya ibada ya upatanisho akiwa amevaa mavazi matakatifu ya kitani.

33 Atafanya ibada ya upatanisho kwa ajili ya mahali patakatifu sana, kwa ajili ya hema la mkutano, madhabahu, makuhani na kwa ajili ya jumuiya nzima ya Israeli.

34 Hili, basi ni sharti la kudumu milele; ni lazima mlifuate ili kufanya ibada ya upatanisho kwa ajili ya watu wa Israeli mara moja kila mwaka na kusamehewa dhambi zao.” Mose akafanya yote kama alivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu.

17

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

2 “Mwambie Aroni, wanawe na watu wote wa Israeli amri zifuatazo:

3 Kama mtu yeyote miongoni mwa Waisraeli akichinja ng'ombe au mwanakondoo au mbuzi ndani au nje ya kambi,

4 badala ya kumleta mnyama huyo kwenye mlango wa hema la mkutano ili kumtolea Mwenyezi-Mungu mbele ya maskani yake takatifu, mtu huyo atakuwa na hatia ya kumwaga damu; amemwaga damu na atatengwa na watu wake.

5 Kusudi la sheria hii ni kwamba Waisraeli wanapaswa kuleta wanyama ambao wangewachinjia mashambani ili wawalete kwa Mwenyezi-Mungu kwa kuhani kwenye mlango wa hema la mkutano, naye atawachinja na kumtolea Mwenyezi-Mungu sadaka za amani.

6 Basi, kuhani atainyunyizia damu madhabahu ya Mwenyezi-Mungu iliyoko mlangoni mwa hema la mkutano na kuyateketeza yale mafuta yawe harufu nzuri ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu.

7 Kwa hiyo Waisraeli watakoma kabisa kutambikia yale majini, jambo ambalo limewafanya wakose uaminifu kwangu. Sharti hili ni la kudumu milele katika vizazi vyao vyote.

8 “Waambie kwamba mtu yeyote miongoni mwa Waisraeli au mgeni anayeishi kati yao, anayetoa sadaka ya kuteketezwa au tambiko,

9 lakini haileti mbele ya mlango wa hema la mkutano ili kumtolea Mwenyezi-Mungu, mtu huyo atatengwa na watu wake.

10 “Kama mtu yeyote wa jumuiya ya Israeli au mgeni anayeishi kati yao anakula damu yoyote, mimi nitamwandama mtu huyo aliyekula damu na kumtenga mbali na watu wake.

11 Itakuwa hivyo kwa sababu uhai wa kiumbe umo katika damu. Nimewaagiza kuitolea damu madhabahuni ili kufanya ibada ya upatanisho kwa ajili ya roho zenu; kwa sababu damu hufanya upatanisho maana uhai umo katika damu.

12 Ndiyo maana nimewaagiza Waisraeli hivi: Mtu yeyote miongoni mwenu wala mgeni anayeishi kati yenu kamwe asile damu.

13 “Mtu yeyote miongoni mwa Waisraeli au mgeni anayekaa miongoni mwao akienda kuwinda mnyama au ndege, ni lazima aimwage damu chini na kuifunika kwa udongo.

14 Maana, uhai wa kila kiumbe umo katika damu. Ndiyo maana nimewaagiza Waisraeli, kamwe wasile damu ya kiumbe chochote kwani uhai wa kiumbe chochote ni damu yake. Yeyote atakayekula damu atatengwa.

15 “Mtu yeyote awe ni mwenyeji au mgeni, anayekula chochote kilichokufa chenyewe au kilichouawa na mnyama wa porini, lazima ayafue mavazi yake na kuoga; naye atakuwa najisi mpaka jioni. Baada ya hapo atakuwa safi.

16 Lakini asipoyafua mavazi yake na kuoga, ni lazima mtu huyo awajibike kwa uovu wake.”

18

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

2 “Waambie watu wa Israeli hivi: Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.

3 Kamwe msifanye kama wafanyavyo watu wa nchi ya Misri ambako mlikaa; wala msifanye kama wafanyavyo watu wa nchi ya Kanaani ambako nawapeleka. Kamwe msifuate mitindo yao.

4 Nyinyi mtafuata maagizo yangu na kuyashika masharti yangu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.

5 Kwa hiyo, ili mtu apate kuyaokoa maisha, mnapaswa kuyashika masharti yangu na maagizo yangu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

6 “Mtu yeyote wa Israeli haruhusiwi kumkaribia mtu wa jamaa yake wa karibu ili kulala naye. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

7 Kamwe usimvunjie heshima baba yako kwa kulala na mama yako aliyekuzaa. Usimwaibishe; yeye ni mama yako.

8 Kamwe usimvunjie heshima baba yako kwa kulala na mmoja wa wake zake. Hao ni mama zako.

9 Kamwe usilale na dada yako, awe ni dada yako halisi au dada yako wa kambo.

10 Kamwe usilale na mjukuu wako, mtoto wa mwanao au binti yako; maana sehemu zao za siri ni kama zako mwenyewe.

11 Kamwe usilale na msichana aliyezaliwa na mama yako wa kambo aliyeolewa na baba yako; msichana huyo ni dada yako.

12 Kamwe usilale na shangazi yako; kwani huyo ni dada wa baba yako.

13 Kamwe usilale na dada wa mama yako; kwani huyo ni mama yako mkubwa au mdogo.

14 Kamwe usilale na mke wa baba yako mkubwa au mdogo; huyo ni mama yako.

15 Kamwe usilale na mke wa mwanao; huyo ni mkewe mwanao. Kamwe usilale naye.

16 Kamwe usilale na mke wa ndugu yako; huyo ni shemeji yako.

17 Ukilala na mwanamke, basi, kamwe usilale naye na binti yake, wala wajukuu zake. Hao ni ndugu. Kuwachanganya ni kufanya uovu.

18 Kamwe usimwoe dada wa mkeo wakati mke wako yungali hai; hiyo itasababisha ushindani.

19 “Kamwe usilale na mwanamke awapo mwezini.

20 Kamwe usilale na mke wa jirani yako na hivyo kujitia mwenyewe najisi naye.

21 “Kamwe usimtoe mtoto wako yeyote kuwa sadaka kwa mungu Moleki maana kufanya hivyo utalikufuru jina langu mimi Mungu wako. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

22 “Kamwe usilale na mwanamume mwenzio kana kwamba ni mwanamke. Hilo ni chukizo.

23 Kamwe usilale na mnyama ili usijitie najisi; mwanamume au mwanamke yeyote kamwe asifanye hivyo; kufanya hivyo ni upotovu.

24 “Msijitie najisi kwa kufanya mambo hayo kwani kwa sababu ya mambo hayo nayafukuza mataifa yaliyo mbele yenu kwa vile wao hufanya hayo na kujitia najisi.

25 Nchi yao ilitiwa unajisi nami nikaiadhibu, nayo ikawakataa wakazi wake.

26 Lakini nyinyi na wageni wanaokaa kati yenu ni lazima kuyashika masharti na maagizo yangu na wala msifanye machukizo hayo.

27 Machukizo hayo waliyafanya watu waliokaa katika nchi ya Kanaani kabla yenu, nao wakaitia nchi unajisi.

28 Basi, nyinyi msifanye mambo hayo, la sivyo nchi hiyo itawatapika kama ilivyolitapika taifa lililokuwa kabla yenu.

29 Watu wote watakaofanya mambo hayo ya kuchukiza ni lazima watengwe mbali na watu wao.

30 Kwa hiyo shikeni kikamilifu yote ninayowaagiza; msifuate mazoea yoyote ya kuchukiza yaliyofanywa na wale walioishi nchini kabla yenu, msije mkajitia unajisi kwayo. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.”

19

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

2 “Iambie jumuiya yote ya watu wa Israeli hivi: Ni lazima muwe watakatifu kwani mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, ni mtakatifu.

3 Kila mmoja wenu ni lazima amheshimu mama yake na baba yake, na kuzishika Sabato zangu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.

4 Msizigeukie sanamu za miungu, wala msijitengenezee sanamu za kusubu za miungu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.

5 “Mnaponitolea mimi Mwenyezi-Mungu sadaka za amani, mtanitolea kama itakiwavyo ili mpate kukubaliwa.

6 Sadaka hiyo ni lazima iliwe siku hiyohiyo inapotolewa au kesho yake. Chochote kinachobaki hadi siku ya tatu ni lazima kiteketezwe kwa moto.

7 Kama sehemu ya nyama yake italiwa siku ya tatu, tendo hilo ni chukizo; na sadaka hiyo haitakubaliwa,

8 naye atakayekula nyama hiyo ni lazima awajibike kwa uovu wake kwa sababu amekitia unajisi kitu kitakatifu cha Mwenyezi-Mungu. Mtu huyo atatengwa na watu wake.

9 “Utakapovuna mavuno ya nchi yako, usivune kabisa hadi mpakani mwa shamba wala usirudi nyuma kukusanya mabaki.

10 Msirudie kukusanya kila kitu katika shamba la mizabibu, wala usiokote zabibu zilizoanguka chini; utawaachia maskini na wageni. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.

11 “Msiibe, msidanganye wala kuambiana uongo.

12 Msiape uongo kwa jina langu hata kulikufuru jina la Mungu wenu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

13 “Usimdhulumu jirani yako wala kumwibia. Mshahara wa mtu aliyeajiriwa usikae kwako usiku kucha hadi asubuhi.

14 Usimlaani kiziwi wala kuweka kizuizi mbele ya kipofu, bali umche Mungu wako. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

15 “Unapotoa hukumu uamue kwa haki; usimpendelee maskini wala kumwogopa mwenye cheo. Bali ni lazima kumwamua jirani kwa haki.

16 Kamwe usipitepite ukiwachongea watu wa jamaa yako. Usiyatie maisha ya jirani yako katika hatari ya kifo kwa maneno yako. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

17 “Usimwekee kisasi ndugu yako moyoni mwako, bali upatane daima na jirani yako ili usije ukatenda dhambi.

18 Usijilipize kisasi au kuwa na kinyongo dhidi ya wazawa wa watu wako bali umpende jirani yako kama unavyojipenda wewe mwenyewe. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

19 “Yakupasa kuyashika masharti yangu. Usiiache mifugo yako ipandwe na wanyama wa aina nyingine. Shambani mwako usipande mbegu za aina mbili. Usivae vazi lililofumwa kwa aina mbili za nguo.

20 “Mwanamume akilala na mwanamke mtumwa ambaye ameposwa na mwanamume mwingine, lakini bado hajakombolewa wala kupewa uhuru, uchunguzi ufanywe. Lakini wasiuawe kwa sababu mwanamke huyo hakuwa bado huru.

21 Mwanamume huyo ataleta mbele ya hema la mkutano sadaka yake ya kondoo dume ya kuondoa hatia na kunitolea mimi Mwenyezi-Mungu.

22 Kuhani atamfanyia ibada ya upatanisho kwa kutumia kondoo huyo mbele ya Mwenyezi-Mungu kwa ajili ya dhambi aliyotenda; naye atasamehewa dhambi hiyo aliyotenda.

23 “Mtakapofika katika nchi ya Kanaani na kupanda aina zote za miti ya matunda, matunda hayo hamtayala; hamtaruhusiwa kuyala kwa muda wa miaka mitatu.

24 Mnamo mwaka wa nne matunda yake yote yatakuwa matakatifu, yatatolewa kuwa sadaka ya sifa, kwa Mwenyezi-Mungu.

25 Lakini matunda ya kuanzia mwaka wa tano hayo mnaweza kula, na mavuno yenu yataongezeka. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.

26 “Msile nyama yoyote yenye damu. Msipige bao wala kufanya uchawi.

27 Nywele zenu msizikate pembeni wala kunyoa ndevu zenu.

28 Msijitie alama zozote mwilini mwenu kwa ajili ya kuomboleza au kujikatakata mwilini au kujichanja chale. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

29 “Usimchafue binti yako kwa kumfanya kahaba, nchi nzima isije ikaangukia katika ukahaba na hivyo kujaa uovu.

30 Mtazishika Sabato zangu na kupaheshimu mahali pangu patakatifu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

31 “Msiwaendee waaguzi wa mizimu wala wachawi ili kuwaomba wawaagulie na hivyo mkajitia najisi. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.

32 “Uwapo mbele ya mzee ni lazima usimame ili kumpa heshima yake; nawe umche Mungu wako. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

33 “Kama kuna mgeni katika nchi yako usimtendee vibaya.

34 Huyo mgeni anayekaa nawe atakuwa kwako kama mwenyeji nawe utampenda kama unavyojipenda mwenyewe, kwa kuwa nawe ulikuwa mgeni katika nchi ya Misri. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.

35 “Usikose kamwe kuamua kwa haki kuhusu vipimo vya urefu, uzito na ujazo.

36 Ni lazima mtumie mizani halali, na vipimo vilivyo halali. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, niliyewatoa katika nchi ya Misri.

37 Ni lazima kuyashika na kuyatekeleza masharti yangu na maagizo yangu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.”

20

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

2 “Waambie Waisraeli hivi: Mtu yeyote miongoni mwa Waisraeli au mgeni anayekaa miongoni mwenu, akimtoa sadaka mtoto wake yeyote kwa mungu Moleki ni lazima mtu huyo auawe. Wananchi wa hapo watamuua kwa kumpiga mawe.

3 Mimi mwenyewe nitamkabili mtu huyo na kumtenga na watu wake kwa sababu alimtoa mmoja wa watoto wake sadaka kwa mungu Moleki na hivyo kupachafua mahali pangu patakatifu na jina langu takatifu.

4 Kama wananchi wa mahali hapo hawatamwadhibu mtu huyo kwa kumuua,

5 mimi mwenyewe nitamkabili mtu huyo na jamaa yake. Nitawatenga kutoka watu wao, yeye mwenyewe pamoja na wote waliokosa uaminifu kwangu kwa kumwendea mungu Moleki.

6 “Kama mtu yeyote anawaendea waaguzi wa mizimu na wachawi na hivyo kukosa uaminifu kwangu, nitamkabili mtu huyo na kumtenga na watu wake.

7 Kwa hiyo, jiwekeni wakfu muwe watakatifu; kwani mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.

8 Shikeni masharti yangu na kuyatekeleza. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu ninayewatakasa.

9 Mtu yeyote amlaaniye baba yake au mama yake, ni lazima auawe. Amemlaani baba au mama yake, kwa hiyo damu yake itakuwa juu yake.

10 “Kama mwanamume akizini na mke wa jirani yake, ni lazima wote wawili wauawe.

11 Mwanamume akilala na mmoja wa wake za baba yake, anamwaibisha baba yake; wote wawili ni lazima wauawe. Damu yao itakuwa juu yao wenyewe.

12 Mwanamume yeyote akilala na mke wa mwanawe, wote wawili ni lazima wauawe. Wamefanya zinaa ya maharimu; wanawajibika kwa umwagaji wa damu yao wenyewe.

13 Kama mwanamume yeyote akilala na mwanamume mwenzake kana kwamba ni mwanamke, basi, wote wawili ni lazima wauawe kwani wamefanya jambo lililo chukizo; watawajibika kwa umwagaji wa damu yao wenyewe.

14 Kama mwanamume akioa mke na pia kumwoa mama yake, huo ni uovu; wote watatu ni lazima wateketezwe kwa moto kwani wamefanya uovu. Mtafanya hivyo ili uovu usiwe miongoni mwenu.

15 Kama mwanamume yeyote akilala na mnyama ni lazima auawe; na mnyama huyo lazima auawe.

16 Kama mwanamke akimkaribia mnyama na kulala naye ni lazima mwanamke huyo auawe na mnyama huyo pia; damu yao itakuwa juu yao wenyewe.

17 “Kama mwanamume yeyote akimwoa dada yake, binti ya baba yake au mama yake, na binti huyo akakubaliana na mwanamume huyo ambaye ni kaka yake, na kulala naye, hilo ni chukizo, ni lazima watengwe na rika lao kwani wamefanya jambo la aibu. Ni lazima mwanamume huyo awajibike kwa uovu wake.

18 Kama mwanamume akilala na mwanamke aliye mwezini, wote wawili ni lazima watengwe na watu wao; huyo mwanamume amelala na mwanamke aliye na hedhi, na huyo mwanamke amelala na mwanamume akiwa na hedhi.

19 Usilale na dada ya mama yako wala na shangazi yako, maana hao ni jamaa yako wa karibu. Wote watendao hayo watawajibika kwa uovu wao.

20 Kama mtu akilala na mke wa baba yake, mkubwa au mdogo, anamwaibisha baba yake mkubwa au mdogo; wote wawili watawajibika kwa dhambi yao; wote wawili watakufa bila watoto.

21 Kama mwanamume akimwoa mke wa ndugu yake, anamwaibisha ndugu yake, huo ni unajisi; wote wawili watakufa bila watoto.

22 “Mnapaswa kushika na kutekeleza masharti na maagizo yangu yote; la sivyo nchi ile ambamo ninawapeleka itawatapika.

23 Msizifuate desturi za taifa ninalolifukuza mbele yenu; kwani waliyafanya hayo yote, nami nikawachukia sana.

24 Lakini, nimekwisha waambia, ‘Mtarithi nchi yao, mimi nawapa nchi hiyo muimiliki, nchi inayotiririka maziwa na asali.’ Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu niliyewatenga na mataifa mengine.

25 Kwa hiyo, ni lazima mtofautishe kati ya mnyama asiye najisi na aliye najisi, kati ya ndege asiye najisi na aliye najisi. Msijifanye kuwa najisi kwa kugusa mnyama au ndege au chochote kitambaacho duniani ambacho nimekitenga kuwa ni najisi.

26 Kwa kuwa mimi Mwenyezi-Mungu ni mtakatifu, nami nimewatenga nyinyi na mataifa mengine ili muwe mali yangu, mtakuwa watakatifu.

27 “Mwanamume au mwanamke yeyote aliye mlozi au mchawi, ni lazima auawe kwa kupigwa mawe. Wote watawajibika kwa umwagaji wa damu yao wenyewe.”

21

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose, “Waambie makuhani, wana wa Aroni, kwamba pasiwe na mtu yeyote miongoni mwao atakayejitia najisi kwa kugusa maiti ya watu wa jamaa yake,

2 isipokuwa kama ni maiti ya ndugu yake wa karibu, yaani mama yake, baba yake, mwanawe, binti yake, ndugu yake

3 au dada yake ambaye (aliye wa jamaa yake ya karibu), naye hajaolewa bado.

4 Yeye, akiwa mwenye madaraka katika jamaa yake, asijitie unajisi.

5 Wazawa wa Aroni kamwe wasijinyoe upara kuomboleza wala wasikate pembe za ndevu zao wala kujichanja chale mwilini.

6 Watakuwa watakatifu kwa Mungu wao wala wasilikufuru jina la Mungu wao. Maana wao ndio wanaotolea zile sadaka anazopewa Mwenyezi-Mungu kwa moto yaani chakula cha Mungu. Basi, ni lazima wawe watakatifu.

7 Kwa kuwa kuhani amewekwa wakfu kwa Mungu wake, kamwe asioe kahaba, wala mwanamke asiye bikira wala aliyepewa talaka.

8 Utamtambua kuhani kuwa aliyewekwa wakfu, maana yeye ndiye anayetoa sadaka ya mkate wa Mungu wako; utamtambua kuwa mtakatifu, maana mimi Mwenyezi-Mungu ninayekuweka wewe wakfu, ni mtakatifu.

9 Binti wa kuhani yeyote akijitia unajisi kwa kufanya ukahaba, atateketezwa kwa moto kwani anamtia baba yake unajisi.

10 “Kuhani mkuu yeyote, kwa kuwa yeye ni mkuu kati ya ndugu zake, naye amemiminiwa mafuta ya kupaka kichwani pake, na kuwekwa wakfu ili ayavae mavazi matakatifu, asiache nywele zake kuwa ovyo wala asirarue mavazi yake kuomboleza.

11 Asikaribie maiti wala kujitia unajisi kwa maiti hata kama ni ya baba yake au ya mama yake.

12 Kwa kuwa amewekwa wakfu kwa kupakwa mafuta ya Mungu wake kichwani, basi asiondoke mahali patakatifu wala asipatie unajisi. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

13 Kuhani mkuu aweza tu kumwoa msichana ambaye ni bikira.

14 Haruhusiwi kuoa mwanamke mjane, mwanamke asiye bikira, wala kahaba. Ni lazima aoe bikira kutoka watu wake mwenyewe

15 asije akawatia unajisi watoto wake mwenyewe. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu niliyemweka wakfu.”

16 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

17 “Mwambie Aroni hivi: Mzawa wako yeyote katika vizazi vyote vijavyo ambaye ana dosari mwilini, haruhusiwi kukaribia na kunitolea mimi Mungu wake sadaka ya mkate.

18 Mtu yeyote mwenye dosari sikaribie kunitolea sadaka: Awe kipofu, aliyelemaa, aliyeharibika uso, mwenye kiungo kirefu kuliko kawaida,

19 mwenye mguu au mkono ulioumia,

20 mwenye kibyongo, mtu mfupi kuliko kawaida, mwenye macho mabovu au ugonjwa wa ngozi, mwenye upele au towashi.

21 Mzawa yeyote wa kuhani Aroni mwenye kilema asikaribie kunitolea sadaka za kuteketezwa kwa moto; kwa vile ana kilema, basi, asikaribie kunitolea mimi Mungu mkate wangu.

22 Mtu huyo anaweza kula mkate wa Mungu wake, vitu vitakatifu na vile vitakatifu kabisa.

23 Lakini asilikaribie lile pazia wala ile madhabahu kwani ana dosari, asije akapatia unajisi mahali patakatifu; kwa kuwa mimi Mwenyezi-Mungu ndiye ninayewaweka wakfu.”

24 Mose akamweleza Aroni na wanawe na Waisraeli wote mambo hayo yote.

22

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

2 “Mwambie Aroni na wanawe makuhani waviheshimu vitu ambavyo Waisraeli wameniwekea wakfu, wasije wakalikufuru jina langu takatifu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

3 Waambie hivi: Kama mmoja wa wazawa wenu katika vizazi vyenu vyote atavikaribia vitu vitakatifu ambavyo Waisraeli wameviweka wakfu kwangu mimi Mwenyezi-Mungu akiwa najisi, mtu huyo atatengwa nami. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

4 Mtu yeyote wa nasaba ya Aroni akiwa na ugonjwa wa ukoma au anatokwa usaha asile vitu vitakatifu mpaka atakapokuwa safi. Mtu yeyote akimgusa mtu aliyetiwa unajisi kwa kugusa maiti au mtu aliyetokwa na shahawa,

5 au akigusa kiumbe chochote chenye kutambaa ambacho husababisha mtu kuwa najisi au mtu ambaye aweza kumtia unajisi wa aina yoyote ile,

6 mtu huyo, atakuwa najisi mpaka jioni na haruhusiwi kula vyakula vitakatifu mpaka hapo atakapokuwa ameoga.

7 Jua litakapotua ndipo atakapokuwa safi. Baada ya hapo ataweza kula vyakula vitakatifu kwani hicho ndicho chakula chake.

8 Kuhani asile nyama yoyote ya mnyama aliyekufa peke yake au kuuawa na mnyama wa porini, asije akajitia unajisi. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

9 Kwa hiyo, ni lazima makuhani walishike agizo langu, wasije wakafanya dhambi na kuuawa. Mimi Mwenyezi-Mungu ndiye ninayewaweka wakfu.

10 “Mtu asiye wa ukoo wa makuhani haruhusiwi kula chakula kitakatifu. Hata mgeni wa kuhani au mwajiriwa wake haruhusiwi kula.

11 Lakini kama kuhani amemnunua mtumwa ili kuwa mali yake, basi, huyo mtumwa anaruhusiwa kula na pia wale waliozaliwa nyumbani kwake.

12 Kama binti yake kuhani ameolewa na mtu asiye kuhani, haruhusiwi kula sadaka ya vitu vitakatifu.

13 Lakini kama binti yake kuhani ni mjane au amepewa talaka na hana mtoto, naye amerudi nyumbani kwa baba yake, akakaa naye kama alipokuwa kijana, basi, anaweza kula chakula cha baba yake. Hata hivyo, mgeni haruhusiwi kula vyakula hivyo.

14 Kama mtu mwingine akila vyakula vitakatifu bila kujua, basi, atalipa asilimia ishirini ya thamani ya alichokula na kumrudishia kuhani.

15 Kuhani asivitie unajisi vitu ambavyo Waisraeli wamemtolea Mwenyezi-Mungu

16 na hivyo kusababisha watu wawajibike uovu na hatia yao kwa kula vitu vyao vitakatifu. Mimi Mwenyezi-Mungu ndiye ninayeviweka wakfu vitu hivyo.”

17 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

18 “Mwambie Aroni na wanawe makuhani na Waisraeli wote hivi: Kama mtu yeyote miongoni mwenu au mgeni yeyote aishiye katika Israeli akitoa sadaka yake, iwe ni ya kutimiza nadhiri au sadaka ya hiari ya kumtolea Mwenyezi-Mungu kwa kuteketezwa,

19 ili apate kukubalika, atatoa katika ng'ombe dume au katika kondoo dume asiye na dosari.

20 Ni marufuku kutoa chochote kilicho na dosari kwani hakitakubaliwa kwa faida yenu.

21 Mtu yeyote anapomtolea Mwenyezi-Mungu sadaka ya amani ili kutimiza nadhiri au sadaka ya hiari kutoka katika kundi lake la mifugo, ili akubaliwe ni lazima awe ni mnyama mkamilifu; mnyama huyo asiwe na dosari yoyote.

22 Usimtolee Mwenyezi-Mungu mnyama yeyote aliye kipofu, kilema, aliyevunjika mahali, anayetokwa na usaha, mwenye upele au ukurutu, wala usiwatoe kuwa sadaka ya kuteketezwa kwa moto juu ya madhabahu ya Mwenyezi-Mungu.

23 Fahali au mwanakondoo aliye na kiungo kimoja kirefu au kifupi kuliko kawaida waweza kumtoa sadaka ya hiari; lakini huyo usimtoe kuwa sadaka ya kutimiza nadhiri.

24 Mnyama ambaye kiungo chake cha kiume kimejeruhiwa, kimepondwa, kimevunjwa au kimekatwa, kamwe usimtolee Mwenyezi-Mungu; usifanye kitu cha namna hiyo nchini mwako.

25 Wala usipokee kutoka kwa wageni wanyama wa namna hiyo na kunitolea mimi Mungu wako kama chakula. Wanyama hao wana dosari kwa vile wamekatwa na hawatakubaliwa kwa faida yenu.”

26 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

27 “Fahali, kondoo dume au beberu akizaliwa atabaki na mama yake kwa siku saba. Lakini tangu siku ya nane anaweza kutolewa kwa Mwenyezi-Mungu kama sadaka ya kuteketezwa kwa moto.

28 Lakini usimchinje ng'ombe au kondoo siku moja pamoja na ndama wake.

29 Utakaponitolea mimi Mwenyezi-Mungu sadaka ya shukrani utaitoa kwa namna ambayo itakufanya ukubaliwe.

30 Mnyama huyo ni lazima aliwe siku hiyohiyo; msimbakize mpaka kesho yake asubuhi. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

31 “Kwa hiyo mtazishika na kuzitekeleza amri zangu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

32 Msilikufuru jina langu takatifu, kwani ni lazima niheshimiwe miongoni mwa watu wa Israeli. Mimi Mwenyezi-Mungu ndiye ninayewaweka wakfu.

33 Mimi ndimi niliyewatoa nchini Misri ili niwe Mungu wenu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.”

23

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

2 “Waambie Waisraeli hivi: Katika sikukuu zangu mimi Mwenyezi-Mungu ambazo zimepangwa mtakuwa na mkutano mtakatifu. Sikukuu ambazo nimepanga ni hizi:

3 Kutakuwa na siku sita za kufanya kazi. Lakini siku ya saba ni Sabato; siku hiyo ni ya mapumziko rasmi, hamtafanya kazi na mtakuwa na mkutano mtakatifu. Siku hiyo ya saba hamtafanya kazi; hiyo ni Sabato ambayo ni wakfu kwangu mimi Mwenyezi-Mungu katika makao yenu yote.

4 “Sikukuu zangu nyingine mimi Mwenyezi-Mungu ambazo mtakuwa na mkutano mtakatifu zitafanyika katika nyakati zifuatazo zilizopangwa.

5 “Jioni ya siku ya kumi na nne ya mwezi wa kwanza mtaadhimisha kwa heshima yangu mimi Mwenyezi-Mungu sikukuu ya Pasaka.

6 Siku ya kumi na tano ya mwezi huohuo, sikukuu ya mikate isiyotiwa chachu itaanza. Kwa muda wa siku saba, mtakula mikate isiyotiwa chachu.

7 Katika siku ya kwanza mtakuwa na mkutano mtakatifu. Siku hiyo msifanye kazi.

8 Kwa muda wa siku hizo zote saba mtanitolea mimi Mwenyezi-Mungu sadaka za kuteketezwa kwa moto. Katika siku ya saba mtafanya mkutano mtakatifu. Msifanye kazi.”

9 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

10 “Waambie Waisraeli hivi: Mtakapoingia katika nchi ambayo ninawapeni mkavuna mazao yake, mtamletea kuhani mganda wa mavuno ya kwanza.

11 Kuhani atafanya nayo ishara ya kunitolea siku inayofuata siku ya Sabato ili mpate kukubaliwa.

12 Siku hiyo mnapofanya ishara ya kutoa huo mganda mbele yangu mtanitolea mimi Mwenyezi-Mungu sadaka ya kuteketezwa ya mwanakondoo dume wa mwaka mmoja asiye na dosari.

13 Pamoja na sadaka hiyo, mtatoa sadaka ya nafaka ya kilo mbili za unga laini uliochanganywa na mafuta ambayo mtanitolea mimi Mwenyezi-Mungu kwa moto, na harufu yake itanipendeza. Sadaka yake ya kinywaji ni lita moja ya divai.

14 Kabla ya siku hiyo ya kuniletea mimi Mungu wenu sadaka hiyo, hamruhusiwi kula mazao ya kwanza ya mavuno yenu, yawe mabichi, yamekaangwa au yemeokwa kuwa mikate. Hili ni sharti la kufuata milele katika vizazi vyenu mahali popote mtakapoishi.

15 “Mtahesabu majuma saba kamili tangu siku ile inayofuata Sabato ile ambapo mtaleta mganda wa sadaka ya kunitolea kwa ishara mimi Mwenyezi-Mungu.

16 Mnamo siku ya hamsini, siku ya pili ya Sabato ya saba, mtanitolea mimi Mwenyezi-Mungu sadaka ya nafaka mpya.

17 Kila jamaa italeta mikate miwili ya sadaka ya kutoa kwa ishara mbele yangu mimi Mwenyezi-Mungu. Kila mkate ni lazima uwe umetengenezwa kwa kilo mbili za unga laini uliotiwa chachu; na huo mtanitolea mimi Mwenyezi-Mungu ukiwa ni matoleo ya malimbuko yenu.

18 Pamoja na hayo, mtatoa wanakondoo saba wa mwaka mmoja, fahali mchanga mmoja, na kondoo madume wawili. Wanyama hao watakuwa sadaka ya kuteketezwa pamoja na sadaka ya nafaka na sadaka za kinywaji. Harufu ya sadaka hizi itanipendeza mimi Mwenyezi-Mungu.

19 Mtatoa beberu mmoja wa sadaka ya kuondoa dhambi na wanakondoo madume wawili wa mwaka mmoja kwa ajili ya sadaka za amani.

20 Kuhani atavipitisha mbele yangu mimi Mwenyezi-Mungu viwe sadaka ya kutoa kwa ishara pamoja na mkate wa mavuno ya kwanza na wale wanakondoo wawili. Vitu hivyo ni vitakatifu kwa Mwenyezi-Mungu navyo vitakuwa kwa matumizi ya kuhani tu.

21 Siku hiyohiyo mtatoa ilani ya mkutano mtakatifu; msifanye kazi. Hili ni sharti la kufuata milele katika vizazi vyenu vyote, katika makazi yenu.

22 “Unapovuna mavuno yako shambani, kamwe usivune kabisa hadi mpakani mwa shamba lako wala usirudi nyuma kukusanya masalio. Utawaachia hayo maskini na wageni. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.”

23 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

24 “Waambie watu wa Israeli hivi: Siku ya kwanza ya mwezi wa saba mtaadhimisha siku ya mapumziko rasmi, siku ya ukumbusho itakayotangazwa kwa mlio wa tarumbeta na kufanya mkutano mtakatifu.

25 Msifanye kazi siku hiyo na ni lazima mnitolee mimi Mwenyezi-Mungu sadaka ya kuteketezwa kwa moto.”

26 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

27 “Siku ya kumi ya mwezi huu wa saba ni siku ya upatanisho. Siku hiyo ni siku ya kuwa na mkutano mtakatifu. Mtafunga na kutoa sadaka anazotolewa Mwenyezi-Mungu kwa moto.

28 Msifanye kazi zenu zozote za kawaida siku hiyo. Siku hiyo ni siku ya upatanisho, siku ya kuwafanyieni upatanisho mbele ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.

29 Mtu yeyote asiyefunga siku hiyo ni lazima atengwe mbali na watu wake.

30 Mtu yeyote atakayefanya kazi yoyote siku hiyo nitamwangamiza miongoni mwa watu wake.

31 Msifanye kazi: Hili ni sharti la kufuata milele katika vizazi vyenu, na katika makao yenu yote.

32 Siku hiyo, itakuwa kwenu Sabato ya mapumziko rasmi na mtafunga. Siku ya Sabato ni siku ya kumi ya mwezi huo tangu jioni hadi jioni inayofuata.”

33 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

34 “Waambie Waisraeli hivi: Tangu siku ya kumi na tano ya mwezi huo wa saba mtamfanyia Mwenyezi-Mungu sikukuu ya vibanda kwa muda wa siku saba. Hiyo ni sikukuu ya Mwenyezi-Mungu.

35 Siku ya kwanza ya siku hizo saba, mtakuwa na mkutano mtakatifu na msifanye kazi.

36 Kwa muda wa siku saba mtatoa sadaka anazopewa Mwenyezi-Mungu kwa moto. Siku ya nane mtakuwa na mkutano mkubwa na kumtolea Mwenyezi-Mungu sadaka ya kuteketezwa. Mkutano huo ni mtakatifu. Siku hiyo msifanye kazi.

37 “Hizo ndizo sikukuu za Mwenyezi-Mungu zilizopangwa ambazo mtatoa ilani kuwe na mkutano mtakatifu wa kumtolea Mwenyezi-Mungu sadaka zitolewazo kwa moto, sadaka za kuteketezwa, sadaka za nafaka na sadaka za kinywaji, kila moja katika siku yake maalumu.

38 Sadaka hizo ni pamoja na zile mnazonitolea mimi Mwenyezi-Mungu siku ya Sabato kama vile pia sadaka zenu za kawaida, sadaka za kutimiza nadhiri zenu, na sadaka zenu za hiari mnazonitolea mimi Mwenyezi-Mungu.

39 “Baada ya kuvuna mashamba yenu mtafanya sikukuu kwa muda wa siku saba, tangu siku ya kumi na tano ya mwezi wa saba. Siku ya kwanza itakuwa siku ya mapumziko na hata siku ya nane.

40 Katika siku ya kwanza mtachukua matunda ya miti yenu mizuri, matawi ya mitende, matawi yenye majani mengi na matawi ya miti iotayo kandokando ya mto, nanyi mtafanya sherehe mbele ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu kwa siku saba.

41 Kila mwaka ni lazima kuadhimisha sikukuu hii kwa muda wa siku saba kwa heshima ya Mwenyezi-Mungu. Hili ni sharti la kufuata milele katika vizazi vyenu. Mtaifanya katika mwezi wa saba.

42 Kwa muda wa siku saba mtaishi katika vibanda. Wakazi wote wa Israeli wataishi katika vibanda wakati huo.

43 Jambo hilo litavijulisha vizazi vyenu kuwa nilipowatoa babu zenu nchini Misri, niliwafanya waishi katika vibanda. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.”

44 Mose akawatangazia Waisraeli sikukuu za Mwenyezi-Mungu zilizopangwa.

24

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

2 “Waamuru watu wa Israeli wakuletee mafuta safi kwa ajili ya taa ili taa hiyo iendelee kuwaka daima.

3 Aroni ataiweka taa hiyo ndani ya hema la mkutano, nje ya pazia la sanduku la maamuzi ili ipate kuwaka mbele yangu tangu usiku mpaka asubuhi. Hili ni sharti la kufuata milele katika vizazi vyenu.

4 Ataziweka hizo taa katika kinara cha taa cha dhahabu safi ziwake daima mbele ya Mwenyezi-Mungu.

5 “Chukua unga laini, kilo kumi na mbili na kuoka mikate kumi na miwili.

6 Mikate hiyo itapangwa safu mbili juu ya meza ya dhahabu safi, kila safu mikate sita.

7 Kila safu utaitia ubani safi ili iambatane na mikate hiyo, na kuwa sehemu ya sadaka ya kuteketezwa ya ukumbusho kwa Mwenyezi-Mungu.

8 Kila siku ya Sabato Aroni ataipanga sawasawa katika safu mbele yangu mimi Mwenyezi-Mungu kwa niaba ya watu wa Israeli kama agano la milele.

9 Aroni na wazawa wake peke yao ndio wanaoruhusiwa kula mikate hiyo kwani ni mitakatifu kabisa kwa sababu ni sehemu ya sadaka ninazotolewa mimi Mwenyezi-Mungu kwa moto. Hiyo ni haki yao milele.”

10 Siku moja kukatokea mzozo huko kambini kati ya Mwisraeli mmoja na kijana mmoja wa mama Mwisraeli aitwaye Shelomithi lakini baba Mmisri.

11 Siku moja yule kijana ambaye mama yake aliitwa Shelomithi binti Dibri wa kabila la Dani, alilikufuru na kulilaani jina la Mungu. Basi watu walimpeleka kijana kwa Mose,

12 wakamtia ndani mpaka hapo watakapofunuliwa matakwa ya Mwenyezi-Mungu.

13 Basi, Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,

14 “Mtoe kijana aliyekufuru nje ya kambi, na wale wote waliomsikia akikufuru waweke mikono yao juu ya kichwa chake, na jumuiya yote imuue kwa kumpiga mawe.

15 Nawe uwaambie Waisraeli kwamba mtu yeyote atakayemlaani Mungu wake ni lazima awajibike kwa dhambi yake.

16 Mtu yeyote awe ni mwenyeji au mgeni anayemkufuru Mwenyezi-Mungu, jumuiya nzima itamuua kwa kumpiga mawe.

17 Mtu yeyote anayeua mtu mwingine ni lazima naye auawe.

18 Mtu yeyote anayeua mnyama ni lazima atoe fidia: Uhai kwa uhai.

19 Mtu yeyote anayemwumiza jirani, ni lazima naye aumizwe kulingana na kiasi alichomwumiza jirani yake,

20 amemvunja mfupa naye atavunjwa mfupa, jicho kwa jicho, jino kwa jino. Kila mtu anayemwumiza mwenzake ni lazima naye aumizwe kulingana na tendo lake.

21 Anayemuua mnyama ni lazima atoe fidia; lakini mtu yeyote akimuua mtu mwingine ni lazima naye auawe.

22 Sheria hii yamhusu mgeni na mwenyeji. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.”

23 Basi, Mose akawaambia Waisraeli hayo yote. Wakampeleka yule mtu aliyemlaani Mwenyezi-Mungu nje ya kambi, wakamuua kwa kumpiga mawe. Ndivyo Waisraeli walivyofanya kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.

25

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose huko mlimani Sinai,

2 “Waambie Waisraeli hivi: Mtakapofika katika nchi ninayowapeni mimi Mwenyezi-Mungu kila mwaka wa saba nchi itapumzishwa isilimwe kwa heshima ya Mwenyezi-Mungu.

3 Kwa muda wa miaka sita mtailima nchi, mtapanda, mtapogoa mizabibu yenu na kuvuna mazao yenu.

4 Lakini mwaka wa saba utakuwa ni sabato ya mapumziko rasmi; ni sabato ya Mwenyezi-Mungu. Msipande chochote wala kuipogoa mizabibu yenu.

5 Chochote kinachoota peke yake msikivune wala kuchuma zabibu kutoka miti isiyopogolewa. Huo utakuwa mwaka wa kuipumzisha ardhi rasmi.

6 Hata hivyo mwaka huo wa pumziko rasmi kwa nchi utawapa chakula nyinyi wenyewe, watumwa wenu wa kiume na wa kike, watu mliowaajiri na wageni wanaokaa miongoni mwenu.

7 Nchi itailisha mifugo yenu na wanyama wa porini wanaokaa miongoni mwenu.

8 “Mtahesabu miaka saba mara saba na jumla yake ni miaka arubaini na tisa.

9 Kisha, katika siku ya kumi ya mwezi wa saba ambayo ni siku ya kufanyiwa upatanisho mtamtuma mtu kupiga tarumbeta katika nchi yote.

10 Mwaka wa hamsini mtauheshimu kwa kutangaza uhuru kwa watumwa wote nchini. Mwaka huo utakuwa ni sikukuu ya ukumbusho wa miaka hamsini. Kila mmoja wenu atairudia mali yake na jamaa yake.

11 Kwa kuwa mwaka huo, ni wa sikukuu ya ukumbusho wa miaka hamsini, msipande mbegu au kuvuna chochote kiotacho chenyewe wala kuchuma zabibu kutoka miti msiyoipogoa.

12 Mwaka huo ni wa sikukuu kwenu; utakuwa mwaka mtakatifu. Hivyo mtakula yale yanayoota yenyewe mashambani.

13 “Katika mwaka huo chochote ambacho kiliuzwa ni lazima kirudishwe kwa mwenyewe.

14 Unaponunua au kuuza ardhi kwa jirani usimpunje.

15 Bei ya ardhi ni lazima ilingane na miaka kabla ya kurudishwa kwa mwenyewe.

16 Kama miaka inayohusika ni mingi utaongeza bei na kama miaka hiyo ni michache utapunguza bei, kwani bei yake itapimwa kulingana na mazao anayokuuzia.

17 Msipunjane, bali, mtamcha Mungu wenu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.

18 “Kwa hiyo, mtafuata masharti yangu na kutekeleza maagizo yangu, ili mpate kuendelea kuishi kwa usalama katika nchi.

19 Nchi itatoa mazao yake nanyi mtakula na kushiba na kuishi humo kwa usalama.

20 Lakini labda mtafikiri, ‘Tutakula nini katika mwaka wa saba iwapo haturuhusiwi kupanda wala kuvuna mazao yetu?’

21 Haya! Mimi nitaibariki nchi katika mwaka wa sita nayo itawapeni mazao ya kuwatosha kwa miaka mitatu.

22 Mtakapopanda katika mwaka wa nane mtakuwa mnakula mazao ya zamani na mtaendelea kula tu hata mwaka wa tisa mtakapoanza tena kuvuna.

23 “Kamwe ardhi isiuzwe kabisa, kwani hiyo ni mali yangu na nyinyi ni wageni na wasafiri nchini mwangu.

24 Ndiyo maana katika nchi yote mtakuwa na utaratibu wa kuikomboa ardhi.

25 “Kama ndugu yako anakuwa maskini, akauza ardhi yake, basi, ndugu yake wa karibu mwenye jukumu la kuikomboa, ataikomboa.

26 Ikiwa mtu huyo hana ndugu mwenye jukumu la kuikomboa, lakini baadaye akawa tajiri na kupata uwezo wa kuikomboa ardhi yake,

27 basi, atahesabu miaka inayohusika tangu alipoiuza na kulipa gharama zake; na yule mtu aliyeinunua ni lazima amrudishie.

28 Lakini ikiwa hana uwezo wa kuikomboa, basi, itabaki mikononi mwa yule aliyeinunua mpaka mwaka wa sikukuu ya ukumbusho wa miaka hamsini. Katika mwaka huo, ni lazima mali hiyo iachiliwe na kurudishiwa yule mtu aliyeiuza.

29 “Kama mtu akiuza nyumba yake ya kuishi iliyo ndani ya mji uliojengewa ukuta, ataweza kuikomboa katika kipindi cha mwaka mmoja tangu alipoiuza. Kwa mwaka huo mzima atakuwa na haki ya kuikomboa.

30 Kama nyumba iliyo katika mji uliojengewa ukuta haikukombolewa kwa muda wa mwaka mmoja, basi, itakuwa mali ya yule aliyeinunua milele katika vizazi vyao vyote; wala haitarudishwa katika mwaka wa sikukuu ya kukumbuka miaka hamsini.

31 Lakini nyumba za vijiji ambavyo havikuzungushiwa ukuta zitakuwa chini ya sheria ileile ya ardhi; nyumba hizo zinaweza kukombolewa katika mwaka mmoja lakini ni lazima zirudishwe kwa wenyewe katika mwaka wa kukumbuka miaka hamsini.

32 Hata hivyo, nyumba zilizomo katika miji wanayomiliki Walawi zinaweza kukombolewa wakati wowote.

33 Ikiwa mmoja wa Walawi haitumii haki yake ya kukomboa, basi, nyumba iliyouzwa ni lazima irudishwe kwa mwenyewe katika mwaka wa kukumbuka miaka hamsini, kwani nyumba zilizomo katika miji wanayomiliki Walawi wamepewa kama sehemu yao kutoka kwa watu wa Israeli.

34 Lakini mashamba wanayomiliki Walawi kwa pamoja, yasiuzwe, kwani huo ni urithi wao wa kudumu.”

35 “Kama ndugu yako amekuwa maskini hata asiweze kujitunza mwenyewe akiwa pamoja nawe, ni lazima umtunze aendelee kuishi nawe; mtendee kama mgeni au msafiri aliye kwako.

36 Usimtake akulipe riba ya namna yoyote ile. Ila mche Mungu, naye ndugu yako apate kuishi pamoja nawe.

37 Usimkopeshe fedha kwa riba au kumpa chakula ili akulipe faida.

38 Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, niliyekutoa nchini Misri ili kukupa nchi ya Kanaani, na ili nami niwe Mungu wako.

39 “Kama ndugu yako anayeishi karibu nawe amekuwa maskini, akijiuza kwako, usimfanye akutumikie kama mtumwa.

40 Atakaa nawe kama mtumishi aliyeajiriwa au kama msafiri. Atakutumikia hadi mwaka wa kuadhimisha miaka hamsini.

41 Mwaka huo ni lazima umpe uhuru wake arudi kwa jamaa yake na urithi wa wazee wake; mwachie pamoja na jamaa yake.

42 Kwa kuwa Waisraeli ni watumishi wangu ambao niliwatoa nchini Misri, basi, wasiuzwe kama watumwa.

43 Usimtawale ndugu yako kwa ukatili, ila utamcha Mungu wako.

44 Kuhusu watumwa, wa kike na wa kiume, unaweza kuwanunua kutoka kwa watu wa mataifa mengine ya jirani.

45 Unaweza pia kununua watumwa kutoka kwa wageni wanaokaa pamoja nawe na jamaa zao waliozaliwa nchini mwenu; nao watakuwa mali yako.

46 Hao watumwa unaweza kuwakabidhi kwa watoto wako wawe mali yao milele. Hao unaweza kuwafanya watumwa wako, lakini kuhusu ndugu yako Mwisraeli, usimtawale kwa ukatili.

47 “Kama mgeni au msafiri anayekaa miongoni mwenu amekuwa tajiri na ndugu yako akawa maskini na kujiuza kwa huyo mgeni au huyo msafiri au kwa mmoja wa jamaa zao,

48 anaweza kukombolewa baada ya kujiuza; mmojawapo wa ndugu zake anaweza kumkomboa.

49 Mjomba wake anaweza pia kumkomboa, au binamu yake au ndugu wa karibu katika ukoo wake; anaweza pia kujikomboa yeye mwenyewe kama akiwa tajiri.

50 Yeye akishirikiana na yule aliyemnunua, atahesabu idadi ya miaka tangu alipojiuza mpaka mwaka wa kuadhimisha kukumbuka miaka hamsini. Gharama ya kuachiliwa huru kwake italingana na miaka aliyomtumikia. Muda ambao amekuwa mtumwa wa bwana wake utapimwa kama muda wa mtumishi wa kuajiriwa.

51 Kama idadi ya miaka mpaka mwaka wa ukumbusho wa miaka hamsini ni kubwa zaidi, basi atarudisha kiasi kikubwa cha bei aliyolipiwa.

52 Kama miaka michache imepungua kabla ya kufikia sikukuu ya ukumbusho wa miaka hamsini, atahesabu kiasi cha bei iliyobaki kulingana na miaka hiyo na kumlipa hiyo fidia.

53 Muda wote atakaokuwa kwa bwana wake ni lazima atendewe kama mtumishi aliyeajiriwa kila mwaka. Huyo aliyemnunua asimtendee kwa ukatili.

54 Lakini ikiwa mtu huyo na jamaa yake hakukombolewa kwa njia hizo, basi apewe uhuru wake katika mwaka wa ukumbusho wa miaka hamsini.

55 Waisraeli ni watumishi wangu, kwani niliwatoa katika nchi ya Misri. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.

26

1 “Msijitengenezee sanamu za miungu ya uongo, msishike sanamu zao za kuchonga wala nguzo wala sanamu za mawe yaliyochongwa nchini mwenu na kuvisujudu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.

2 Shikeni sabato zangu na kuheshimu mahali pangu patakatifu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

3 “Kama mkifuata masharti yangu na kuzishika amri zangu,

4 nitawanyeshea mvua wakati ufaao, nchi ipate kuzaa mavuno kwa wingi, nayo miti ya mashambani matunda yake.

5 Kupura nafaka kutaendelea mpaka wakati wa kuvuna zabibu, na uvunaji zabibu mpaka wakati wa kupanda mbegu. Mtakuwa na chakula tele na kuishi kwa usalama nchini mwenu.

6 Nitawapeni amani nchini hata muweze kulala bila ya kuogopeshwa na chochote. Nitawaondoa wanyama wakali katika nchi na nchi yenu haitakumbwa na vita.

7 Mtawafukuza adui zenu na kuwaua kwa upanga.

8 Watano wenu watawafukuza adui 100 na 100 wenu watawafukuza adui 10,000. Adui zenu wataangamia mbele yenu kwa upanga.

9 Nitawafadhili na kuwajalia mpate watoto wengi na kuongezeka; nami nitaliimarisha agano langu nanyi.

10 Wakati wa mavuno mtakuwa bado mnakula mazao ya zamani; tena itawalazimu kuondoa yaliyobaki kupata nafasi ya kuhifadhi mavuno mapya.

11 Nitaweka maskani yangu miongoni mwenu, wala sitawaacheni.

12 Nitatembea kati yenu na kuwa Mungu wenu nanyi mtakuwa watu wangu.

13 Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, niliyewatoa nchini Misri ili msiwe watumwa wa Wamisri. Mimi nimevunja nira mliyofungiwa shingoni mwenu na kuwafanya mtembee wima.

14 “Lakini kama hamtanisikiliza wala kufuata amri zangu,

15 kama mkidharau masharti yangu na kuchukia kwa roho maagizo yangu mkaacha kuzitii amri zangu zote na kuvunja agano langu,

16 basi, mimi nitafanya hivi: Nitawapiga kwa kuwaletea hofu kuu ya ghafla, kifua kikuu na homa itakayowapofusha macho na kuwadhoofisha. Mtapanda mbegu zenu bila mafanikio kwani adui zenu ndio watakaokula.

17 Mimi nitawakabili, nanyi mtapigwa na adui zenu; mtatawaliwa na wale wanaowachukia. Mtatishwa na kukimbia hata kama hakuna mtu yeyote anayewafukuza.

18 Na Kama hata baada ya kuadhibiwa hivyo, hamtanisikiliza, basi, nitawaadhibu mara saba zaidi kwa ajili ya dhambi zenu.

19 Kiburi chenu nitakivunjilia mbali kwa kuzifanya mbingu huko juu kuwa ngumu kama chuma, na nchi yenu bila mvua iwe ngumu kama shaba.

20 Mtatumia nguvu zenu bure maana mashamba yenu hayatatoa mavuno na nchi yenu haitazaa matunda.

21 “Kama mkiendelea kunipinga na kukataa kunisikiliza, nitazidisha tena adhabu yenu mara saba kadiri ya wingi wa dhambi zenu.

22 Nitawapeleka wanyama wakali kati yenu ambao watawanyakulieni watoto wenu na kula mifugo yenu; na kukata idadi yenu hata njia zenu zigeuke kama jangwa.

23 “Kama hata baada ya adhabu hiyo bado hamnigeukii mimi, ila mnazidi kupingana nami,

24 basi, nami nitapingana nanyi na kuwaadhibu mara saba zaidi kwa ajili ya dhambi zenu.

25 Nitawaleteeni upanga ambao utalipiza kisasi juu ya agano mlilovunja. Nyinyi mtakimbilia katika miji yenu, lakini nitawapelekea maradhi mabaya na kuwatia mikononi mwa adui zenu.

26 Chakula chenu nitakipunguza hata wanawake kumi watumie jiko moja tu kuoka mikate. Watawagawia kwa kipimo. Na hata baada ya kula bado mtakuwa na njaa tu.

27 “Na kama hata baada ya hayo yote bado hamtanisikiliza mkaendelea kunipinga,

28 basi nami nitapingana nanyi kwa hasira kali, na kuwaadhibu mimi mwenyewe mara saba zaidi kwa ajili ya dhambi zenu.

29 Ndipo mtakula watoto wenu, wa kiume na kike.

30 Nitapaharibu mahali penu pa ibada milimani, nitazibomoa madhabahu zenu za kufukizia ubani, na kuzitupa maiti zenu juu ya sanamu za miungu yenu. Roho yangu itawachukia kabisa.

31 Miji yenu nitaiteketeza mahali penu patakatifu nitapafanya jangwa na harufu zenu nzuri za sadaka kamwe sitazikubali.

32 Nitaiteketeza nchi yenu hivyo kwamba hata adui wanaohamia humo watashangaa.

33 Nitawatawanya nyinyi miongoni mwa watu wa mataifa na kuchomoa upanga dhidi yenu. Nchi yenu itakuwa ni ukiwa na miji yenu uharibifu.

34 “Nyinyi mtakapokuwa mikononi mwa adui zenu, hapo ndipo nchi itakapozifurahia sabato zake wakati itakapokuwa hali ya ukiwa. Nchi itapumzika na kufurahia sabato zake.

35 Kadiri itakapokuwa hali ya ukiwa itapata kiasi ambacho haikupata katika sabato zenu mlipokuwa mkiishi humo.

36 Na kwa baadhi yenu watakaosalimika nitawaletea woga mioyoni mwao, katika nchi ya adui zao hata jani linalopeperushwa litawakimbiza. Watakimbia kama mtu anayekimbia vita. Watakimbia na kuanguka hata kama hamna mtu anayewafukuza.

37 Wataangukiana ovyo kama mtu anayekimbia vita hata kama hamna anayewafukuza. Hamtakuwa na nguvu yoyote kuwakabili adui zenu.

38 Mtaangamia kati ya mataifa na nchi za adui zenu zitawameza.

39 Kama baadhi yenu wakisalimika katika nchi za adui zenu watadhoofika kwa sababu ya uovu wao; na kwa sababu ya uovu wa wazee wao.

40 “Lakini kama wakitubu uovu wao na uovu wa wazee wao juu ya uasi waliotenda dhidi yangu na pia juu ya kupingana kwao nami,

41 wakatambua kwa nini nilipingana nao na kuwapeleka katika nchi ya adui zao; kama kweli moyo wao mkaidi ukinyenyekea na kutubu uovu wao,

42 basi, hapo nami nitalikumbuka agano langu na Abrahamu, Isaka na Yakobo; na kuikumbuka ile nchi niliyowaahidia.

43 “Wakati watakapokuwa nje ya nchi yao, nchi hiyo itafurahia sabato zake hapo itakapokuwa hali ya ukiwa. Wakati huo wao watatubu uovu wao wa kupuuza maagizo yangu na kuyachukia maagizo yangu.

44 Lakini, kwa hayo yote, wawapo katika nchi ya adui zao; mimi sitawatupa wala kuwachukia hata kuwaangamiza kabisa na kulivunjilia mbali agano langu.

45 La! Kwa ajili yao nitalikumbuka agano nililofanya na wazee wao ambao niliwatoa katika nchi ya Misri, mataifa yakishuhudia, ili mimi niwe Mungu wao. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.”

46 Hayo ndiyo masharti, maagizo na sheria ambazo Mwenyezi-Mungu aliwapa watu wa Israeli kule mlimani Sinai kwa njia ya Mose.

27

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

2 “Waambie Waisraeli hivi: Mtu akiweka nadhiri ya kumtolea Mwenyezi-Mungu binadamu, mtu huyo anaweza kuondoa nadhiri yake kwa kulipa kiasi cha fedha kinachokadiriwa kama ifuatavyo:

3 Mwanamume wa miaka ishirini hadi miaka sitini atakombolewa kwa fedha shekeli 50 kulingana na kipimo cha mahali patakatifu.

4 Kama ni mwanamke, atakombolewa kwa fedha shekeli 30.

5 Kama mtu huyo ni wa miaka kati ya mitano na 20 atakombolewa kwa fedha shekeli 20 kama ni mvulana na shekeli 10 za fedha kama ni msichana.

6 Ikiwa ni mtoto wa umri wa kati ya mwezi mmoja na miaka mitano atakombolewa kwa shekeli 5 za fedha kama ni mvulana na shekeli 3 za fedha kama ni msichana.

7 Ikiwa mtu huyo umri wake ni zaidi ya miaka sitini, thamani yake itakuwa ni shekeli 15 za fedha kama ni mwanamume na shekeli 10 za fedha kama ni mwanamke.

8 Lakini ikiwa mtu huyo ni maskini na hawezi kulipa gharama yake, basi, mtu huyo atapelekwa kwa kuhani. Kuhani atampima thamani yake kulingana na uwezo wa huyo aliyeweka nadhiri.

9 “Ikiwa nadhiri yenyewe inahusu mnyama wa namna ambayo watu humtolea Mwenyezi-Mungu sadaka, basi mnyama huyo huwa kitu kitakatifu.

10 Hairuhusiwi kumbadilisha mnyama huyo kwa mwingine awaye yeyote, mzuri kwa mbaya au mbaya kwa mzuri. Kama akimbadilisha kwa mnyama mwingine, wote wawili watakuwa watakatifu.

11 “Kama nadhiri hiyo yahusu mnyama najisi, wa aina ambayo si halali kumtolea Mwenyezi-Mungu, basi, mtu aliyemtoa, atamleta kwa kuhani,

12 naye kuhani ataamua thamani yake kulingana na uzuri au ubaya wake. Jinsi atakavyoamua kuhani, ndivyo itakavyokuwa.

13 Lakini ikiwa mwenyewe anataka kumkomboa, basi, ataongeza asilimia ishirini ya thamani ya mnyama huyo.

14 “Mtu akiiweka wakfu nyumba yake kuwa takatifu kwa Mwenyezi-Mungu, kuhani ataamua thamani yake kulingana na uzuri au ubaya wake. Jinsi atakavyoamua, ndivyo itakavyokuwa.

15 Kama huyo mtu aliyeiweka wakfu akitaka kuikomboa hiyo nyumba, basi, ataongeza asilimia ishirini ya thamani yake, nayo itakuwa mali yake.

16 “Mtu akiiweka ardhi yake, ambayo ni urithi wake, wakfu kwa Mwenyezi-Mungu basi, thamani yake itapimwa kulingana na mbegu zinazotumika kulipanda shamba hilo; kwa kila kilo ishirini za shayiri thamani yake itakuwa shekeli hamsini za fedha.

17 Kama akiliweka wakfu shamba lake katika mwaka wa kuadhimisha miaka hamsini, thamani yake ni lazima ilingane na vipimo vyenu.

18 Lakini kama akiliweka wakfu baada ya mwaka huo, basi, kuhani ataamua thamani yake kulingana na miaka iliyobaki kufikia mwaka wa ukumbusho wa miaka hamsini na thamani yake ipunguzwe.

19 Kama mwenyewe akitaka kulikomboa, basi, ni lazima aongeze asilimia ishirini ya thamani ya shamba hilo, na kisha litakuwa mali yake.

20 Lakini kama hataki kulikomboa au amemwuzia mtu mwingine, basi, shamba hilo lisikombolewe tena.

21 Katika mwaka wa ukumbusho wa miaka hamsini shamba hilo litaachiliwa na kuwa lake Mwenyezi-Mungu milele. Kuhani ndiye atakayelimiliki.

22 “Kama mtu akiweka wakfu shamba alilonunua, yaani sio lake kwa urithi,

23 kuhani ataamua thamani ya shamba hilo kwa kulingana na miaka iliyobaki kufikia mwaka wa ukumbusho wa miaka hamsini na mtu huyo atalazimika kulipa thamani yake kama ni kitu kitakatifu kwa Mwenyezi-Mungu.

24 Lakini katika mwaka wa ukumbusho wa miaka hamsini, shamba hilo ni lazima arudishiwe yule mtu aliyeliuza.

25 Kila thamani itapimwa kwa kipimo cha uzito cha shekeli kulingana na kipimo cha mahali patakatifu: Uzito wa gera 20 ni sawa na uzito wa shekeli moja.

26 “Hairuhusiwi kumweka wakfu mzaliwa wa kwanza wa wanyama; kisheria huyo ni wake Mwenyezi-Mungu; awe ni ng'ombe au kondoo.

27 Kama anayehusika ni mnyama najisi, mwenyewe atamnunua kwa kulingana na mnavyompima na ataongeza asilimia ishirini ya thamani ya mnyama huyo. Kama hakombolewi, basi, atauzwa kulingana na vipimo vyenu.

28 “Lakini kitu chochote kilichowekwa wakfu kwa Mwenyezi-Mungu, kiwe ni mtu au mnyama au kitu kilichopatikana kwa urithi, hakitauzwa wala kukombolewa. Chochote kilichowekwa wakfu kwa Mwenyezi-Mungu ni kitakatifu kabisa.

29 Mtu yeyote aliyewekwa wakfu kwa Mwenyezi-Mungu ili aangamizwe, asikombolewe; sharti auawe.

30 “Zaka za mazao iwe ni nafaka au matunda ya miti, yote ni mali ya Mwenyezi-Mungu; ni takatifu kwa Mwenyezi-Mungu.

31 Kama mtu akitaka kuikomboa zaka yake, atalipa thamani yake na kuongeza asilimia ishirini ya thamani ya zaka hiyo.

32 Kuhusu mifugo, inapohesabiwa, kila mnyama wa kumi ni mtakatifu kwa Mwenyezi-Mungu.

33 Mtu yeyote hana ruhusa kuuliza kama mnyama huyo ni mzuri au mbaya wala mnyama huyo kamwe hatabadilishwa kwa mwingine. Kama akibadilishwa kwa mwingine, wanyama wote wawili watakuwa watakatifu; hawatakombolewa.”

34 Hizo ndizo amri ambazo Mwenyezi-Mungu alimwamuru Mose ili awaambie Waisraeli, mlimani Sinai.