1 Kauli ya Mungu juu ya Ninewi. Kitabu cha maono ya Nahumu wa Elkoshi.
2 Mwenyezi-Mungu ni Mungu mwenye wivu, mlipiza kisasi; Mwenyezi-Mungu hulipiza kisasi na ni mwenye ghadhabu; Mwenyezi-Mungu hulipiza kisasi kwa adui zake, huwaka ghadhabu juu ya adui zake.
3 Mwenyezi-Mungu hakasiriki upesi, lakini amejaa nguvu, Mwenyezi-Mungu kamwe hatawaachilia wenye hatia. Apitapo Mwenyezi-Mungu, huzuka kimbunga na dhoruba; mawingu ni vumbi litimuliwalo na nyayo zake.
4 Huikaripia bahari na kuikausha, yeye huikausha mito yote. Mbuga za Bashani na mlima Karmeli hunyauka, maua ya Lebanoni hudhoofika.
5 Milima hutetemeka mbele yake, navyo vilima huyeyuka; dunia hutetemeka mbele yake, ulimwengu na vyote vilivyomo.
6 Nani awezaye kuikabili ghadhabu ya Mwenyezi-Mungu? Nani awezaye kustahimili ukali wa hasira yake? Yeye huimwaga hasira yake iwakayo kama moto, hata miamba huipasua vipandevipande.
7 Mwenyezi-Mungu ni mwema, yeye ni ngome ya usalama wakati wa taabu. Yeye huwalinda wote wanaokimbilia usalama kwake.
8 Adui wakiivamia nchi kama mafuriko, yeye huwaangamiza; huwafuatia na kuwafukuza mpaka gizani.
9 Mbona mnafanya mipango dhidi ya Mwenyezi-Mungu? Yeye atawakomesha na kuwaangamiza, wala mpinzani wake hataweza kuinuka tena.
10 Watateketezwa kama kichaka cha miiba, kama vile nyasi zilizokauka.
11 Kwako kumetoka aliyepanga maovu dhidi ya Mwenyezi-Mungu aliyefanya njama za ulaghai.
12 Mwenyezi-Mungu awaambia hivi watu wake: “Ingawa Waashuru ni wengi na wenye nguvu, wao wataangushwa na kuangamizwa. Ingawa nimewatesa nyinyi watu wangu, sitawateseni tena zaidi.
13 Sasa nitaivunja nira ya Ashuru shingoni mwenu, na minyororo waliyowafungia nitaikatakata.”
14 Mwenyezi-Mungu ameamuru hivi kuhusu Ninewi: “Hutapata wazawa kulidumisha jina lako. Sanamu zako za kuchonga na za kusubu, nitazivunjavunja nyumbani mwa miungu yako. Mimi nitakuchimbia kaburi lako, maana wewe hufai kitu chochote.”
15 Enyi watu wa Yuda tazameni: Anakuja kutoka mlimani mtu anayeleta habari njema, mjumbe ambaye anatangaza amani. Adhimisheni sikukuu zenu, enyi watu wa Yuda, timizeni nadhiri zenu, maana waovu hawatawavamia tena, kwani wameangamizwa kabisa.
1 Mwangamizi amekuja kukushambulia ee Ninewi. Chunga ngome zako! Weka ulinzi barabarani! Jiweke tayari! Kusanya nguvu zako zote!
2 Mwenyezi-Mungu anamrudishia Yakobo fahari yake, naam, anawapa tena Waisraeli fahari yao, ingawa wavamizi hawakuwaachia kitu, hata matawi yao ya mizabibu waliyakata.
3 Ngao za mashujaa wake ni nyekundu, askari wake wamevaa mavazi mekundu sana. Magari yao ya farasi yanamulika kama miali ya moto, yamepangwa tayari kushambulia; farasi hawatulii kwa uchu wa kushambulia.
4 Magari ya farasi yanatimua mbio barabarani, yanakwenda huko na huko uwanjani. Yanamulika kama miali ya moto! Yanakwenda kasi kama umeme.
5 Sasa anawaita maofisa wake, nao wanajikwaa wanapomwendea; wanakwenda ukutani himahima kutayarisha kizuizi.
6 Vizuizi vya mito vimefunguliwa, ikulu imejaa hofu.
7 Mji uko wazi kabisa, watu wamechukuliwa mateka. Wanawake wake wanaomboleza, wanalia kama njiwa, na kujipigapiga vifuani.
8 Ninewi ni kama bwawa lililobomoka, watu wake wanaukimbia ovyo. “Simameni! Simameni!” Sauti inaita, lakini hakuna anayerudi nyuma.
9 “Chukueni nyara za fedha, chukueni nyara za dhahabu! Hazina yake haina mwisho! Kuna wingi wa kila kitu cha thamani!”
10 Mji wa Ninewi ni maangamizi matupu na uharibifu! Watu wamekufa moyo, magoti yanagongana, nguvu zimewaishia, nyuso zimewaiva!
11 Limekuwaje basi hilo pango la simba, hilo lililokuwa maficho ya wanasimba? Pamekuwaje hapo mahali pa simba, mahali pa wanasimba ambapo hakuna aliyeweza kuwashtua?
12 Simba dume amewararulia watoto wake nyama ya kutosha, akawakamatia simba majike mawindo yao; ameyajaza mapango yake mawindo, na makao yake mapande ya nyama.
13 Tazama, mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi nitapambana nawe: Nitayateketeza kwa moto magari yako ya farasi, nitawamaliza kwa upanga hao simba wako vijana, nyara ulizoteka nitazitokomeza kutoka nchini, na sauti ya wajumbe wako haitasikika tena.
1 Ole wako mji wa mauaji! Umejaa udanganyifu mtupu na nyara tele, usiokoma kamwe kuteka nyara.
2 Sikia! Mlio wa mjeledi, mrindimo wa magurudumu, vishindo vya farasi na ngurumo za magari!
3 Wapandafarasi wanashambulia, panga na mikuki inametameta; waliouawa hawana idadi, maiti wengi sana; watu wanajikwaa juu ya maiti!
4 Ninewi! Wewe umekuwa kama malaya. Umewashawishi watu, ewe binti wa uchawi, uliyeyafanya mataifa kuwa watumwa kwa umalaya wako, na watu wa mataifa kwa uchawi wako.
5 Mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi nasema nitapambana nawe; nitalipandisha vazi lako hadi kichwani, niyaache mataifa yauone uchi wako, tawala ziikodolee macho aibu yako.
6 Nitakutupia uchafu, na kukutendea kwa dharau, na kukufanya uwe kioja kwa watu.
7 Kisha wote watakaokuona watakukimbia wakisema, “Ninewi umeangamizwa, ni nani atakayeuombolezea? Nani atakayekufariji?”
8 Je, wewe Ninewi, ni bora kuliko Thebesi, mji uliojengwa kando ya mto Nili? Thebesi ulizungukwa na maji, bahari ilikuwa boma lake, maji yalikuwa ukuta wake!
9 Kushi ilikuwa nguvu yake; nayo Misri pia, tena bila kikomo; watu wa Puti na Libia waliusaidia!
10 Hata hivyo, ulichukuliwa mateka, watu wake wakapelekwa uhamishoni. Hata watoto wake walipondwapondwa katika pembe ya kila barabara; watu wake mashuhuri walinadiwa, wakuu wake wote walifungwa minyororo.
11 Ninewi, nawe pia utalewa; utamkimbia adui na kujaribu kujificha.
12 Ngome zako zote ni za tini za mwanzo; zikitikiswa zinamwangukia mlaji kinywani.
13 Tazama askari wako: Wao ni waoga kama wanawake. Milango ya nchi yako ni wazi mbele ya adui zako; moto umeyateketeza kabisa makomeo yake.
14 Tekeni maji muwe tayari kuzingirwa; imarisheni ngome zenu. Pondeni udongo kwa kuukanyagakanyaga, tayarisheni tanuri ya kuchomea matofali!
15 Lakini huko pia moto utawateketezeni, upanga utawakatilia mbali; utawamaliza kama nzige walavyo. Ongezekeni kama nzige, naam, ongezekeni kama panzi!
16 Wafanyabiashara wako waliongezeka kuliko nyota; lakini sasa wametoweka kama panzi warukavyo.
17 Wakuu wako ni kama panzi, maofisa wako kama kundi la nzige; wakati wa baridi wanakaa kwenye kuta, lakini jua lichomozapo, huruka, wala hakuna ajuaye walikokwenda.
18 Ewe mfalme wa Ashuru, wachungaji wako wamelala, waheshimiwa wako wamesinzia. Watu wako wametawanyika milimani, wala hakuna yeyote wa kuwakusanya.
19 Hakuna wa kuyapa nafuu majeraha yako, vidonda vyako ni vya kifo. Wote wanaosikia habari zako wanashangilia. Maana ni nani aliyeuepa ukatili wako usio na kikomo?