1

1 Mnamo siku ya kwanza ya mwezi wa pili, mwaka wa pili baada ya wana wa Israeli kutoka Misri, Mwenyezi-Mungu aliongea na Mose ndani ya hema la mkutano jangwani Sinai, akamwambia hivi:

2 “Wewe na Aroni fanyeni sensa ya jumuiya yote ya Waisraeli, familia mojamoja kwa kufuata koo zao na idadi ya majina yao kila mwanamume mmojammoja;

3 wale wote katika Israeli wanaoweza kwenda vitani, wenye umri kuanzia miaka ishirini na zaidi, mtawaweka katika orodha ya vikosi vikosi.

4 Tena mwanamume mmoja wa kila kabila atakuwa pamoja nanyi, kila mmoja aliye kiongozi wa jamaa za kabila lake.

5 Haya ndiyo majina ya watu watakaokusaidia: Kabila la Reubeni: Elisuri, mwana wa Shedeuri;

6 Kabila la Simeoni: Shelumieli mwana wa Suri-shadai;

7 Kabila la Yuda: Nashoni mwana wa Aminadabu;

8 Kabila la Isakari: Nethaneli mwana wa Suari;

9 Kabila la Zebuluni: Eliabu mwana wa Heloni;

10 Kabila la Efraimu: Elishama mwana wa Amihudi; Kabila la Manase: Gamalieli mwana wa Pedasuri;

11 Kabila la Benyamini: Abidani mwana wa Gideoni;

12 Kabila la Dani: Ahiezeri mwana wa Amishadai;

13 Kabila la Asheri: Pagieli mwana wa Okrani;

14 Kabila la Gadi: Eliasafu mwana wa Deueli;

15 Kabila la Naftali: Ahira mwana wa Enani.”

16 Hawa ndio viongozi waliochaguliwa miongoni mwa jumuiya yote ya watu wa Israeli, kama viongozi wakuu wa makabila yao na viongozi wa koo za Israeli.

17 Basi, Mose na Aroni wakawachukua watu hawa waliotajwa,

18 na mnamo siku ya kwanza ya mwezi wa pili, wakaikusanya jumuiya yote ya watu waliokuwa wamehesabiwa kila mmoja kulingana na familia yake na ukoo wake. Kufuatana na majina ya watu waliokuwa na umri wa miaka ishirini na zaidi, mmojammoja,

19 kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose. Mose akawahesabu watu hawa kule jangwani Sinai.

20 Watu waliotoka katika kabila la Reubeni aliyekuwa mzaliwa wa kwanza wa Israeli, kwa kufuata vizazi vyao, kulingana na familia zao na jamaa zao, kadiri ya jumla ya majina yao mmojammoja, kila mwanamume aliyekuwa na umri wa miaka ishirini na zaidi, aliyefaa kuingia jeshini,

21 walikuwa watu 46,500.

22 Kutoka kabila la Simeoni kwa kufuata vizazi vyao kulingana na familia zao na jamaa zao kadiri ya jumla ya majina yao mmojammoja, wenye umri kuanzia miaka ishirini na zaidi, waliofaa kuingia jeshini,

23 walikuwa watu 59,300.

24 Kutoka kabila la Gadi kwa kufuata vizazi vyao kulingana na familia zao na jamaa zao kadiri ya jumla ya majina yao mmojammoja, wenye umri kuanzia miaka ishirini na zaidi, waliofaa kuingia jeshini,

25 walikuwa watu 45,650.

26 Kutoka kabila la Yuda kwa kufuata vizazi vyao kulingana na familia zao na jamaa zao kadiri ya jumla ya majina yao mmojammoja, wenye umri kuanzia miaka ishirini na zaidi, waliofaa kuingia jeshini,

27 walikuwa watu 74,600.

28 Kutoka kabila la Isakari kwa kufuata vizazi vyao kulingana na familia zao na jamaa zao kadiri ya jumla ya majina yao mmojammoja, wenye umri kuanzia miaka ishirini na zaidi, waliofaa kuingia jeshini,

29 walikuwa watu 54,400.

30 Kutoka kabila la Zebuluni kwa kufuata vizazi vyao kulingana na familia zao na jamaa zao kadiri ya jumla ya majina yao mmojammoja, wenye umri kuanzia miaka ishirini na zaidi, waliofaa kuingia jeshini,

31 walikuwa watu 57,400.

32 Kutoka kabila la Efraimu, mwanawe Yosefu, kwa kufuata vizazi vyao kulingana na familia zao na jamaa zao kadiri ya jumla ya majina yao mmojammoja, wenye umri kuanzia miaka ishirini na zaidi, waliofaa kuingia jeshini,

33 walikuwa watu 40,500.

34 Kutoka kabila la Manase, mwanawe Yosefu, kwa kufuata vizazi vyao kulingana na familia zao na jamaa zao kadiri ya jumla yao mmojammoja, wenye umri kuanzia miaka ishirini na zaidi waliofaa kuingia jeshini,

35 walikuwa watu 32,200.

36 Kutoka kabila la Benyamini, kwa kufuata vizazi vyao kulingana na familia zao na jamaa zao kadiri ya jumla ya majina yao mmojammoja, wenye umri kuanzia miaka ishirini na zaidi, waliofaa kuingia jeshini,

37 walikuwa watu 35,400.

38 Kutoka kabila la Dani kwa kufuata vizazi vyao kulingana na familia zao na jamaa zao kadiri ya jumla ya majina yao mmojammoja, wenye umri kuanzia miaka ishirini na zaidi, waliofaa kuingia jeshini,

39 walikuwa watu 62,700.

40 Kutoka kabila la Asheri, kwa kufuata vizazi vyao kulingana na familia zao na jamaa zao kadiri ya jumla ya majina yao mmojammoja, wenye umri kuanzia miaka ishirini na zaidi, waliofaa kuingia jeshini,

41 walikuwa watu 41,500.

42 Kutoka kabila la Naftali, kwa kufuata vizazi vyao kulingana na familia zao na jamaa zao kadiri ya jumla ya majina ya mmojammoja, wenye umri kuanzia miaka ishirini na zaidi, waliofaa kuingia jeshini,

43 walikuwa watu 53,400.

44 Hawa ndio watu waliokuwa wamehesabiwa ambao Mose na Aroni waliwahesabu wakisaidiwa na wale viongozi kumi na wawili wa Israeli, kila kiongozi akiwakilisha ukoo wake.

45 Hivyo jumla ya wanaume wote wa Israeli wenye umri kuanzia miaka ishirini na zaidi, waliofaa kuingia jeshini nchini Israeli

46 ilikuwa watu 603,550.

47 Lakini Walawi hawakuhesabiwa pamoja na yale makabila mengine,

48 kwa sababu Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

49 “Usihesabu kabila la Lawi wala usiwafanyie sensa kati ya watu wa Israeli;

50 bali utawateua wawe waangalizi wa hema la ushuhuda, vyombo vyake vyote na kila kitu kilichomo ndani yake; watakuwa wakilibeba pamoja na vyombo vyake vyote. Watahudumu humo ndani na kupiga kambi yao kwa kulizunguka.

51 Tena wakati wa hema kungolewa Walawi ndio watakaolingoa na wakati wa hema kusimikwa Walawi ndio watakaolisimamisha.

52 Waisraeli wengine wote watapiga kambi zao makundimakundi, kila mtu katika kundi lake na chini ya bendera yake.

53 Lakini Walawi watapiga kambi zao kulizunguka hema la maamuzi, wakililinda ili mtu yeyote asije akalikaribia na kusababisha ghadhabu yangu kuwaka dhidi ya jumuiya ya watu wa Israeli; basi Walawi watalitunza hema la maamuzi.”

54 Kwa hiyo Waisraeli wakafanya kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.

2

1 Mwenyezi-Mungu aliwapa Mose na Aroni, maagizo yafuatayo:

2 “Waisraeli watapiga kambi zao, kila mmoja akikaa mahali penye bendera yake, penye alama za ukoo wake. Watapiga kambi zao kulizunguka hema la mkutano.

3 “Wale watakaopiga kambi upande wa mashariki kuelekea mawio ya jua watakuwa kikundi cha watu walio chini ya bendera ya Yuda na kiongozi wao atakuwa Nashoni mwana wa Aminadabu,

4 kikosi chake kulingana na hesabu ni wanaume 74600.

5 Wale watakaofuata kupiga kambi baada ya watu wa Yuda watakuwa kabila la Isakari, kiongozi wao akiwa Nethaneli mwana wa Suari,

6 kikosi chake kulingana na hesabu ni wanaume 54,400.

7 Kisha kabila la Zebuluni, kiongozi wao akiwa Eliabu mwana wa Heloni,

8 kikosi chake kulingana na hesabu ni wanaume 57,400.

9 Jumla yote ya watu watakaokuwa katika kambi ya Yuda kulingana na makundi yao ni watu 186,400. Hao ndio watakaotangulia kusafiri.

10 “Kwa upande wa kusini, wale walio chini ya bendera ya kundi la Reubeni kulingana na makundi yao, kiongozi wao akiwa Elisuri mwana wa Shedeuri,

11 kikosi chake kulingana na hesabu kitakuwa na watu 46,500.

12 Kisha wale watakaopiga kambi kando ya watu wa Reubeni watakuwa ni watu wa kabila la Simeoni, kiongozi wao akiwa Shelumieli mwana wa Suri-shadai,

13 kikosi chake kulingana na hesabu kitakuwa na watu 59,300.

14 Hatimaye kabila la Gadi, kiongozi wao akiwa Eliasafu mwana wa Reueli,

15 kikosi chake kulingana na hesabu kitakuwa na watu 45,650.

16 Jumla ya wanaume watakaokuwa katika kambi ya Reubeni kulingana na makundi yao ni watu 151,450. Hawa ndio watakaokuwa katika msafara wa pili.

17 “Halafu, kambi ya kabila la Walawi, ikiwa katikati ya kambi zote, na wakiwa wamebeba hilo hema la mkutano, wataondoka; kila kundi litasafiri kwa kufuata nafasi yake chini ya bendera yao.

18 “Kwa upande wa magharibi, wale walio chini ya bendera ya kundi la Efraimu watapiga kambi kulingana na makundi yao, kiongozi wao akiwa Elishama mwana wa Amihudi,

19 kikosi chake kulingana na hesabu kitakuwa na watu 32,200.

20 Mara tu baada ya Waefraimu litafuata kabila la Manase: Kiongozi wake akiwa Gamalieli, mwana wa Pedasuri,

21 kikosi chake kulingana na hesabu kitakuwa watu 32,000.

22 Hatimaye kabila la Benyamini: Kiongozi wake ni Abidani, mwana wa Gideoni,

23 kikosi chake kulingana na hesabu kitakuwa na watu 35,400.

24 Jumla ya watu watakaokuwa katika kambi ya Efraimu kulingana na makundi yao ni watu 108,100. Kundi hili la Efraimu litakuwa katika msafara wa tatu.

25 “Kwa upande wa kaskazini, watapiga kambi katika makundi yao wale walio chini ya bendera ya Dani, kiongozi wao atakuwa Ahiezeri, mwana wa Amishadai,

26 kikosi chake kulingana na hesabu kitakuwa na watu 62,700.

27 Kisha wale watakaopiga kambi baada yao watakuwa watu wa kabila la Asheri, kiongozi wao akiwa Pagieli mwana wa Okrani,

28 kikosi chake kulingana na hesabu kitakuwa na watu 41,500.

29 “Hatimaye watu wa kabila la Naftali, kiongozi wake akiwa Ahira mwana wa Enani,

30 kikosi chake kulingana na hesabu, kitakuwa na watu 53,400.

31 Jumla ya watu watakaokuwa katika kambi ya Dani kulingana na makundi yao ni watu 157,600. Kundi hili la Dani litakuwa katika msafara wa mwisho, bendera baada ya bendera.”

32 Hao ndio Waisraeli waliohesabiwa kulingana na koo zao, katika kambi na vikosi vyao; wote walikuwa 603,550.

33 Lakini Walawi hawakuhesabiwa miongoni mwa watu wa Israeli kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.

34 Hivyo ndivyo, Waisraeli walivyofanya kila kitu kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose. Walipiga kambi zao, kufuata bendera zao na walisafiri kila mmoja akiandamana na jamaa yake kwa kufuata ukoo wake.

3

1 Wafuatao ndio wazawa wa Aroni na Mose wakati Mwenyezi-Mungu alipozungumza na Mose mlimani Sinai.

2 Haya ndiyo majina ya wana wa Aroni: Nadabu, mzaliwa wake wa kwanza, Abihu, Eleazari na Ithamari.

3 Hawa waliwekwa wakfu kwa kupakwa mafuta wawe makuhani.

4 Lakini Nadabu na Abihu walikufa mbele ya Mwenyezi-Mungu, wakati walipomtolea Mwenyezi-Mungu moto usio mtakatifu katika jangwa la Sinai. Wao hawakuwa na watoto kwa hiyo Eleazari na Ithamari wakawa wanahudumu kama makuhani wakati wa uhai wa Aroni baba yao.

5 Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,

6 “Walete karibu watu wa kabila la Lawi, uwaweke mbele ya kuhani Aroni ili uwape jukumu la kumtumikia.

7 Watafanya kazi kwa niaba yake na ya jumuiya yote kwenye hema la mkutano wanapohudumu mahali patakatifu,

8 wataangalia na kutunza vyombo vyote vya hema la mkutano na kuwasaidia Waisraeli wanapotoa huduma zao kwenye mahali patakatifu.

9 Walawi utampa Aroni na wazawa wake makuhani; hao wametolewa kati ya Waisraeli wawahudumie kabisa.

10 Utawateua Aroni na wanawe ili waweze kutekeleza huduma zao za ukuhani; lakini kama mtu yeyote mwingine atakaribia, atauawa.”

11 Mwenyezi-Mungu akaendelea kumwambia Mose,

12 “Angalia, sasa nimewateua Walawi miongoni mwa Waisraeli wote, badala ya kila mzaliwa wa kwanza wa kiume kifunguamimba katika kila familia ya Israeli. Walawi ni wangu,

13 kwani kila mzaliwa wa kwanza katika Israeli ni wangu. Wakati nilipowaua wazaliwa wa kwanza wote wa Wamisri nilijiwekea wakfu kila mzaliwa wa kwanza katika Israeli; kila mzaliwa wa kwanza wa binadamu hata wa mnyama; wao watakuwa wangu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.”

14 Baadaye Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose katika jangwa la Sinai,

15 “Wahesabu wana wa Lawi wote kulingana na koo zao na familia zao, kila mwanamume kuanzia watoto wenye umri wa mwezi mmoja na zaidi.”

16 Basi, Mose akawahesabu kufuatana na neno la Mwenyezi-Mungu, kama alivyomwamuru.

17 Wafuatao ndio waliokuwa wana wa Lawi: Gershoni, Kohathi na Merari.

18 Na haya ndiyo majina ya wana wa Gershoni kwa kufuata familia zao: Libni na Shimei.

19 Wana wa Kohathi kwa kufuata familia zao: Amramu, Ishari, Hebroni na Uzieli.

20 Wana wa Merari kwa kufuata familia zao: Mahli na Mushi. Hizi zilikuwa jamaa za Walawi kulingana na koo zao.

21 Familia za Walibni na Washimei zilitokana na Gershoni; hizi ndizo zilizokuwa jamaa za Wagershoni.

22 Idadi yao kwa kadiri ya hesabu ya wanaume wote kuanzia waliokuwa na mwezi mmoja na zaidi ni 7,500.

23 Familia za Wagershoni, iliwapasa kupiga kambi yao upande wa magharibi, nyuma ya hema takatifu

24 naye Eliasafu mwana wa Laeli akiwa mkuu wa ukoo wa Wagershoni.

25 Kazi ya wana wa Gershoni ilikuwa kulitunza hema takatifu, hema pamoja na kifuniko chake, pazia la mlango wa hema la mkutano,

26 mapazia ya ua ulioko kati ya hema takatifu na madhabahu, na pazia la mlango wa ua, na kamba zake. Huduma zote zilizohusu vitu hivi zilikuwa zao.

27 Familia za Waamrami, Waishari, Wahebroni na Wauzieli zilitokana na Kohathi; hizi ndizo zilizokuwa jamaa za Wakohathi.

28 Kadiri ya hesabu ya wanaume wote kuanzia wenye umri wa mwezi mmoja na zaidi ilikuwa 8,600, waliohusika na huduma za mahali patakatifu.

29 Familia za wana wa Kohathi zilitakiwa kupiga kambi yao upande wa kusini wa mahali patakatifu,

30 naye Elisafani, akiwa mkuu wa ukoo huo wa familia za Wakohathi.

31 Wajibu wao ulikuwa kulitunza sanduku la agano, meza, kinara cha taa, madhabahu, vyombo wanavyotumia makuhani mahali patakatifu na pazia; huduma zote zilizohusu vitu hivi zilikuwa zao.

32 Naye Eleazari mwana wa kuhani Aroni aliwekwa kuwa mkuu wa wakuu wa Walawi, na msimamizi wa wahudumu wote wa mahali patakatifu.

33 Familia za Wamahli na Wamushi zilitokana na Merari.

34 Hizi ndizo familia za Merari. Idadi yao kadiri ya hesabu ya wanaume wote kuanzia wenye umri wa mwezi mmoja na zaidi ilikuwa watu 6,200.

35 Mkuu wa ukoo wa familia za Merari alikuwa Surieli mwana wa Abihaili; hawa walitakiwa kupiga kambi yao upande wa kaskazini wa hema takatifu.

36 Wao walipewa kazi ya kutunza mbao za hema takatifu, mataruma, nguzo, vitako na vifaa vyote vya kushikilia hema; huduma zote zilizohusu vitu hivi zilikuwa juu yao.

37 Pia walihitajika kutunza nguzo za ua zilizouzunguka na vitako vyake, vigingi na kamba zake.

38 Mose na Aroni na wana wao walitakiwa kupiga kambi yao mbele ya hema takatifu upande wa mashariki kuelekea mawio ya jua. Wajibu wao ulikuwa kutoa huduma kwenye mahali patakatifu kwa lolote lililohitajika kufanyika kwa ajili ya Waisraeli. Mtu mwingine yeyote aliyesogea karibu ilibidi auawe.

39 Idadi ya Walawi kulingana na familia zao, wanaume wote kuanzia watoto wenye umri wa mwezi mmoja na zaidi ambao Mose na Aroni waliwahesabu kwa amri ya Mwenyezi-Mungu, ilikuwa watu 22,000.

40 Kisha Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose, “Wahesabu kwa majina wazaliwa wa kwanza wa kiume wote wa Waisraeli kuanzia wenye umri wa mwezi mmoja na zaidi.

41 Nawe utatenga Walawi kwa ajili yangu mimi Mwenyezi-Mungu; pia utatenga kwa ajili yangu mifugo yote ya Walawi badala ya wazaliwa wa kwanza wa mifugo ya watu wa Israeli.”

42 Basi, Mose akawahesabu wazaliwa wa kwanza wote wa watu wa Israeli kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru.

43 Wazaliwa wote wa kwanza wa kiume kadiri ya hesabu ya majina, kuanzia wenye umri wa mwezi mmoja na zaidi, kufuata walivyohesabiwa, walikuwa 22,273.

44 Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,

45 “Sasa, watenge Walawi wote kuwa wangu badala ya wazaliwa wa kwanza wa Waisraeli. Kadhalika, watenge ng'ombe wa Walawi wote badala ya wazaliwa wa kwanza wa ng'ombe wa Waisraeli. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

46 Kwa ajili ya fidia ya wazaliwa wa kwanza wa kiume wa watu wa Israeli 273, wanaozidi idadi ya wanaume Walawi,

47 utapokea kwa kila mwanamume fedha shekeli tano, kulingana na kipimo cha mahali patakatifu, ambayo ni sawa na gera ishirini,

48 na fedha hizo kwa ajili ya fidia ya hao waliozidi idadi yao utampa Aroni na wanawe.”

49 Mose akatii, akachukua fedha hizo za fidia ya hao waliozidi idadi ya waliofidiwa na Walawi;

50 alipokea kutoka wazaliwa wa kwanza wa Waisraeli fedha kiasi cha shekeli 1,365, kulingana na kipimo cha mahali patakatifu,

51 akawapa Aroni na wanawe fedha hizo za fidia sawa na neno la Mwenyezi-Mungu kama alivyomwamuru.

4

1 Mwenyezi-Mungu akawaambia Mose na Aroni,

2 “Wahesabu watu wa ukoo wa Kohathi, mmoja wa koo za Lawi, kufuatana na jamaa zao na koo zao;

3 utawaorodhesha wanaume wote wenye umri kati ya miaka thelathini na hamsini wanaofaa kujiunga na huduma ya hema la mkutano.

4 Hii ndio itakayokuwa huduma ya wana wa Kohathi, kuhusu vitu vitakatifu kabisa.

5 “Wakati wa kuvunja kambi, Aroni na wanawe wataingia katika hema, na kulishusha pazia lililoko mbele ya sanduku la agano, kisha walifunike kwa pazia hilo.

6 Juu yake wataweka kifuniko cha ngozi laini ya mbuzi, kisha watatandaza kitambaa cha rangi ya buluu safi. Halafu wataingiza mipiko ya kulichukulia sanduku hilo.

7 “Juu ya meza ya kutolea mikate inayowekwa mbele ya Mwenyezi-Mungu watatandaza kitambaa cha buluu ambacho juu yake wataweka sahani, visahani vya ubani, bakuli na bilauri, kwa ajili ya kutolea tambiko za kinywaji. Daima kutakuwa na mkate juu ya meza.

8 Kisha, watavifunika vyombo hivi vyote kwa kitambaa chekundu, na juu yake wataweka kifuniko cha ngozi laini ya mbuzi. Halafu wataingiza mipiko yake ya kulibeba.

9 “Watachukua kitambaa cha buluu ambacho watafunikia kinara cha taa na taa zake, makasi zake, sinia zake na vyombo vyote vinavyotumiwa kukiwekea mafuta.

10 Watakiweka pamoja na vyombo vyake vyote ndani ya ngozi laini ya mbuzi na kukiweka juu ya mipiko ya kuchukulia.

11 “Halafu watatandaza kitambaa cha buluu juu ya madhabahu ya dhahabu na kuifunika kwa ngozi laini ya mbuzi juu yake. Halafu wataingiza mipiko yake ya kuichukulia.

12 Watavichukua vyombo vyote vinavyotumika mahali patakatifu, watavifunga kwa kitambaa cha buluu na kuvifunika kwa ngozi laini ya mbuzi, kisha wataviweka juu ya mipiko yake ya kuchukulia.

13 Watayaondoa majivu kutoka madhabahuni na juu yake watatandaza kitambaa cha zambarau.

14 Juu yake wataviweka vyombo vyote vitumikavyo katika ibada kwenye madhabahu: Vyetezo, nyuma, miiko na mabakuli. Kisha, juu yake watatandaza kifuniko cha ngozi laini ya mbuzi na kuiingiza mipiko yake ya kulibebea.

15 Baada ya Aroni na wanawe kupafunika mahali patakatifu pamoja na vyombo na vifaa vyake vyote, wakiwa tayari kuanza safari, watu wa ukoo wa Kohathi watakuja na kuvibeba. Lakini wao, hawaruhusiwi kabisa kuvigusa vyombo hivyo vitakatifu, wasije wakafa. Hiyo ndiyo kazi ya ukoo wa Kohathi kila wakati hema la mkutano linapohamishwa.

16 Eleazari mwana wa kuhani Aroni itampasa kuyatunza mafuta ya taa, ubani wa kunukia, tambiko za nafaka za kila siku, mafuta ya kupaka ili kuweka wakfu na kila kitu kilichowekwa wakfu katika hema hilo.”

17 Kisha Mwenyezi-Mungu akawaambia Mose na Aroni,

18 “Msiache ukoo wa familia za Kohathi miongoni mwa Walawi uangamizwe.

19 Basi, ili kuwaepusha wasije wakauawa kwa kuvikaribia vyombo hivyo vitakatifu sana utafanya hivi: Aroni na wanawe wataingia na kumpangia kila mmoja wao wajibu wake na kazi yake.

20 Lakini wazawa wa Kohathi hawataingia kamwe kuvitazama vitu hivyo vitakatifu sana; wakifanya hivyo watakufa.”

21 Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,

22 “Wahesabu watu wa ukoo wa Gershoni, kufuatana na familia na koo zao;

23 utawahesabu wanaume wote wenye umri kati ya miaka thelathini na hamsini wanaofaa kujiunga na huduma ya hema la mkutano.

24 Wajibu wao utakuwa huu: Watabeba mapazia ya hema takatifu na hema la mkutano pamoja na

25 kifuniko chake, kifuniko cha ngozi laini ya mbuzi kilicho juu yake, pazia la lango,

26 mapazia na kamba za ua ulio kandokando ya hema na madhabahu, mapazia ya lango la kitalu, na vifaa vyote vinavyotumika pamoja na vitu hivi. Wao watashughulika na mambo yote yanayohusika na vitu hivi.

27 Aroni na wanawe makuhani ndio watakaoamrisha huduma zote za Wagershoni kuhusu vitu watakavyobeba na kazi watakazofanya. Utawapangia vitu vyote vile ambavyo wanapaswa kubeba.

28 Hii ndiyo huduma ya jamaa za Gershoni kwenye hema la mkutano; watafanya kazi chini ya uongozi wa Ithamari mwana wa kuhani Aroni.

29 “Kadhalika, utawahesabu wana wa Merari, kufuatana na jamaa zao na koo zao.

30 Utawahesabu wanaume wote wenye umri kati ya miaka thelathini na hamsini, wanaofaa kujiunga na huduma ya hema la mkutano.

31 Wao, watakuwa na wajibu na kubeba mbao, mataruma, nguzo na misingi ya hema la mkutano.

32 Kadhalika na nguzo za ua za kuzunguka pande zote, vikalio, vigingi na kamba pamoja na vifaa vyake vyote na vyombo vyake vingine vyote. Nawe utawapangia kufuata majina yao vitu watakavyopaswa kubeba.

33 Hii ndiyo itakayokuwa kazi ya wana wa ukoo wa Merari katika huduma yao yote ndani ya hema la mkutano, chini ya uongozi wa Ithamari mwana wa kuhani Aroni.”

34 Basi, Mose, Aroni na viongozi wa jumuiya yote wakafanya sensa ya watu wa ukoo wa Kohathi, kufuatana na familia zao,

35 wakawaorodhesha watu wote wenye umri kati ya miaka thelathini na hamsini, kila aliyefaa kuingia katika huduma ya hema la mkutano.

36 Idadi yao kufuatana na jamaa zao ilikuwa watu 2,750.

37 Hii ndiyo idadi ya watu wa jamaa ya Kohathi, ambao walihudumu katika hema la mkutano, ambao Mose na Aroni waliwahesabu kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.

38 Idadi ya watu wa ukoo wa Gershoni kufuatana na familia zao,

39 wenye umri kati ya miaka thelathini na hamsini, waliofaa kuhudumu katika hema la mkutano,

40 ilikuwa watu 2,630.

41 Hii ndiyo iliyokuwa idadi ya watu wa familia za wana wa Gershoni wote waliohudumu katika hema la mkutano, ambao Mose na Aroni waliwahesabu kama Mwenyezi-Mungu alivyowaagiza.

42 Idadi ya watu wa ukoo wa Merari kufuatana na jamaa zao na familia zao,

43 wenye umri kati ya miaka thelathini na hamsini, waliofaa kuhudumu katika hema la mkutano,

44 ilikuwa watu 3,200.

45 Hii ndiyo idadi ya watu wa ukoo wa Merari ambao Mose na Aroni waliwahesabu kama Mwenyezi-Mungu alivyomwagiza Mose.

46 Hivyo, Walawi wote walioandikishwa na Mose, Aroni na viongozi wa watu, kwa kufuata jamaa zao na koo zao,

47 wenye umri kati ya miaka thelathini na hamsini, na ambao walifaa kwa huduma na uchukuzi katika hema la mkutano,

48 jumla walikuwa watu 8,580.

49 Kila mmoja alipewa kazi yake ya kufanya kuhusu kubeba hema la mkutano, kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.

5

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

2 “Waamuru Waisraeli wamtoe nje ya kambi kila mtu mwenye ukoma, kila mtu anayetokwa usaha, na kila aliye najisi kwa kugusa maiti.

3 Mtawatoa nje ya kambi watu wote hawa, wanaume kwa wanawake, ili wasije wakaitia najisi kambi yangu ninamokaa.”

4 Waisraeli walifanya hivyo, wakawafukuza nje ya kambi. Kama Mwenyezi-Mungu alivyomwambia Mose, ndivyo Waisraeli walivyofanya.

5 Kisha Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

6 “Waambie Waisraeli kuwa: Mtu yeyote, mwanamume au mwanamke akitenda dhambi dhidi ya mtu, akakosa uaminifu kwa Mwenyezi-Mungu, mtu huyo ana hatia;

7 itambidi aungame dhambi yake aliyotenda. Lazima atoe fidia kamilifu kwa kosa lake, akiongeza asilimia ishirini ya fidia hiyo; atampa fidia hiyo yule aliyemkosea.

8 Lakini ikiwa mtu huyo amefariki na hana jamaa wa karibu ambaye anaweza kupokea fidia hiyo, basi, fidia ya kosa itatolewa kwa Mwenyezi-Mungu kwa ajili ya makuhani; malipo haya ni pamoja na kondoo dume wa upatanisho ambaye atatumiwa kumfanyia upatanisho kwa ajili ya dhambi yake.

9 Michango yote na matoleo yote ambayo Waisraeli wataweka wakfu kwa Mungu na kumletea kuhani itakuwa yake huyo kuhani.

10 Kila kitu kilichowekwa wakfu kwa Mungu na kupelekwa kwa kuhani kitakuwa chake.”

11 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

12 “Waambie Waisraeli: Kama mke wa mtu yeyote amepotoka akakosa uaminifu kwa mumewe,

13 akalala na mtu mwingine bila ya mumewe au mtu mwingine yeyote kujua; amejitia najisi lakini hakuna mtu aliyeshuhudia kitendo chake kwa kuwa hakufumaniwa.

14 Basi, mumewe akiingiwa na shaka na kuwa na wivu juu ya mkewe aliyejitia najisi; au kama amekuwa na wivu juu ya mke wake ingawa mkewe hakujitia najisi,

15 basi wote wawili watakwenda kwa kuhani na kupeleka sadaka inayotakiwa, yaani sehemu ya kumi ya unga wa shayiri; lakini bila kuitia mafuta au ubani, kwa kuwa ni sadaka ya nafaka ya mume anayemshuku mkewe, sadaka inayotolewa kuhusu kosa ambalo linabainishwa.

16 “Kuhani atampeleka huyo mwanamke karibu, na kumsimamisha mbele ya Mwenyezi-Mungu.

17 Kisha, atamimina maji matakatifu katika chombo cha udongo na kutwaa vumbi kutoka sakafuni mwa hema takatifu na kuitia katika maji hayo ili kuyafanya machungu.

18 Kuhani atamweka mbele ya Mwenyezi-Mungu na kumfunua nywele na kumpa sadaka hiyo ya nafaka itolewayo kwa sababu ya shuku ya mumewe. Kuhani mwenyewe atashikilia kile chombo chenye maji machungu yaletayo laana.

19 Halafu kuhani atamwapisha mwanamke huyo akisema: ‘Ikiwa hukulala na mwanamume mwingine, ukajitia najisi hali uko chini ya mamlaka ya mumeo, basi, hutapatwa na laana iletwayo na maji haya machungu.

20 Lakini kama umepotoka hali uko chini ya mamlaka ya mumeo, ukajitia najisi kwa kulala na mwanamume mwingine asiye mume wako,

21 Mwenyezi-Mungu na akuadhibu hata uwe laana na apizo miongoni mwa watu wako, uwe tasa na tumbo lako livimbe.

22 Maji haya yaletayo laana na yaingie tumboni mwako na kukufanya tasa na tumbo lako livimbe.’ Naye mwanamke ataitikia, ‘Amina, Amina.’

23 “Kisha kuhani ataandika laana hizi kitabuni na kuzioshea katika maji machungu;

24 naye atamnywesha mwanamke hayo maji machungu yaletayo laana nayo yataingia ndani yake na kumletea maumivu makali;

25 kisha kuhani atachukua ile sadaka ya nafaka ya wivu mikononi mwa mwanamke huyo na kuitikisa mbele ya Mwenyezi-Mungu, na kuipeleka madhabahuni.

26 Halafu, atatwaa konzi moja ya sadaka hiyo ya nafaka kwa ukumbusho na kuiteketeza madhabahuni. Hatimaye atamnywesha mwanamke maji hayo.

27 Akisha kunywa, kama amejitia najisi na hakuwa mwaminifu kwa mume wake, maji hayo yaletayo laana yatamletea maumivu makali sana; mwili wake utavimba na tumbo lake la uzazi litaharibika. Mwanamke huyo atakuwa laana miongoni mwa watu wake.

28 Lakini kama mwanamke huyo hajajitia unajisi na hana hatia, basi hatadhurika na ataweza kupata watoto.

29 “Basi, hii ndiyo sheria kuhusu kesi za wivu iwapo mwanamke, ingawa yu chini ya mamlaka ya mumewe, atapotoka na kujitia unajisi,

30 au wakati mwanamume ashikwapo na wivu na kumshuku mkewe. Atamsimamisha mwanamke huyo mbele ya Mwenyezi-Mungu, na kuhani atatekeleza masharti yote ya sheria hii.

31 Mumewe hatakuwa na hatia yoyote, lakini mwanamke atawajibika kwa uovu wake.”

6

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

2 “Wape Waisraeli maagizo yafuatayo: Iwapo mwanamume au mwanamke ataweka nadhiri maalumu, nadhiri ya kujiweka wakfu, akajitenga kwa ajili ya Mwenyezi-Mungu,

3 basi, asinywe divai au kileo, asinywe siki ya divai au ya namna nyingine, asinywe maji ya zabibu wala kula zabibu zilizoiva au kavu.

4 Muda wote atakaokuwa mnadhiri asile kitu chochote kinachotokana na mzabibu, tangu kokwa hata maganda yake.

5 “Siku zote za nadhiri yake ya kujitenga, hatanyoa nywele zake; mpaka muda wa nadhiri yake ya kujiweka wakfu kwa Mwenyezi-Mungu utakapomalizika, atakuwa mtakatifu, ataziacha nywele zake ziwe ndefu.

6 Siku zote atakazokuwa amejiweka wakfu kwa Mwenyezi-Mungu, mtu huyo asikaribie maiti,

7 hata kama ni ya baba, mama, ndugu au dada yake, asije akajitia unajisi kwa maana amejiweka wakfu kwa Mwenyezi-Mungu kwa kiapo.

8 Muda wote atakaokuwa mnadhiri atakuwa wakfu kwa Mwenyezi-Mungu.

9 “Endapo nywele za mnadhiri zitatiwa unajisi mtu afapo ghafla karibu naye, atakinyoa kichwa chake wakati wa siku ya kutakaswa kwake; atakinyoa katika siku ya saba.

10 Katika siku ya nane atapeleka hua wawili au makinda mawili ya njiwa kwa kuhani penye lango la hema la mkutano.

11 Kuhani atamtoa mmoja kuwa sadaka ya kuondoa dhambi na mwingine kuwa sadaka ya kuteketezwa, naye atamfanyia upatanisho, kwa sababu alitenda dhambi kwa ajili ya maiti. Siku hiyohiyo, atakiweka wakfu kichwa chake

12 na kujiweka wakfu kwa Mwenyezi-Mungu kwa siku zake za kujitenga. Hizo siku za kwanza hazitahesabiwa kwa sababu nywele zake zilizokuwa zimewekwa wakfu zimetiwa unajisi. Atatoa mwanakondoo dume wa mwaka mmoja kuwa sadaka ya hatia.

13 “Hii ndiyo sheria ya mnadhiri wakati akisha kamilisha muda wake wa kujiweka wakfu: Ataletwa penye lango la hema la mkutano,

14 na kumtolea Mwenyezi-Mungu zawadi zake: Mwanakondoo dume mmoja wa mwaka mmoja asiye na dosari kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa; mwanakondoo jike mmoja wa mwaka mmoja asiye na dosari kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi; na kondoo dume mmoja asiye na dosari kwa ajili ya sadaka ya amani.

15 Pia atatoa kikapu cha mikate isiyotiwa chachu: Maandazi ya unga laini na mafuta, na mikate myembamba iliyopakwa mafuta pamoja na sadaka za nafaka na za kinywaji.

16 “Kuhani atamtolea Mwenyezi-Mungu vitu vyote hivi pamoja na sadaka yake ya dhambi na sadaka yake ya kuteketezwa.

17 Atamtolea Mwenyezi-Mungu huyo kondoo kama tambiko ya amani, atamtoa pamoja na kikapu cha mikate isiyotiwa chachu, sadaka ya nafaka na ya kinywaji.

18 Hapo penye mlango wa hema la mkutano, mnadhiri huyo atanyoa nywele zake na kuzitia katika moto ulio chini ya tambiko ya sadaka ya amani.

19 “Kisha kuhani atachukua bega la yule kondoo dume likiwa limechemshwa pamoja na andazi moja lililotiwa chachu kutoka kikapuni na mikate myembamba pia isiyotiwa chachu na kumpa mnadhiri mikononi akisha maliza kunyoa nywele zake alizokuwa nazo wakati wa kuwekwa wakfu.

20 Halafu kuhani atavitikisa vitu hivyo kama sadaka ya kutikisa mbele ya Mwenyezi-Mungu; vyote hivi ni sehemu takatifu kwa kuhani, pamoja na kidari kilichotikiswa na paja lililotolewa kama sadaka. Baada ya hayo yote, mnadhiri anaweza kunywa divai.

21 “Hiyo ndizo sheria inayomhusu mnadhiri anayeahidi kwa kiapo. Sadaka yake kwa Mwenyezi-Mungu ilingane na nadhiri yake, licha ya chochote kingine anachoweza kutoa; atafanya kulingana na nadhiri aliyoweka, kadiri ya sheria ya kujiweka wakfu kwake.”

22 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

23 “Mwambie Aroni na wanawe kwamba hivi ndivyo mtakavyowabariki Waisraeli: Mtawaambia,

24 ‘Mwenyezi-Mungu awabariki na kuwalinda;

25 Mwenyezi-Mungu awaangalie kwa wema, na kuwafadhili;

26 Mwenyezi-Mungu awaoneshe wema wake na kuwapa amani.’

27 “Ndivyo watakavyotamka jina langu juu ya Waisraeli, nami nitawabariki.”

7

1 Siku Mose alipomaliza kulisimamisha hema takatifu, kulimiminia mafuta na kuliweka wakfu pamoja na vyombo vyake vyote, kuimiminia mafuta na kuiweka wakfu madhabahu na vyombo vyake vyote,

2 viongozi wa Israeli na wakuu wa koo na viongozi wa makabila ambao walisimamia watu wale waliohesabiwa,

3 walimletea Mwenyezi-Mungu matoleo yao: Magari yaliyofunikwa sita na mafahali kumi na wawili, gari moja kwa kila viongozi wawili na fahali mmoja kwa kila kiongozi. Baada ya kuvitoa mbele ya hema takatifu,

4 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

5 “Pokea matoleo haya ili yatumiwe katika huduma itakayofanywa kwa ajili ya hema la mkutano, uwape Walawi, kila mmoja kwa kadiri ya kazi yake.”

6 Basi, Mose akachukua magari na mafahali akawapa Walawi.

7 Wagershoni wakapewa magari mawili na mafahali wanne, kwa kadiri ya huduma yao,

8 na Wamerari wakapewa magari manne na mafahali wanane, kuwasaidia katika kazi zao zote chini ya uongozi wa Ithamari mwana wa kuhani Aroni.

9 Lakini Mose hakuwapa chochote Wakohathi kwa kuwa wao walikuwa na jukumu la kutunza vitu vitakatifu ambavyo vilipaswa kubebwa mabegani.

10 Viongozi hao wakatoa sadaka kwa ajili ya kuiweka wakfu madhabahu siku ile ilipopakwa mafuta; walitoa sadaka zao mbele ya madhabahu.

11 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose, “Kila siku kiongozi mmoja atatoa sadaka yake kwa ajili ya kuiweka wakfu madhabahu.”

12 Basi, yule aliyetoa sadaka siku ya kwanza, alikuwa Nashoni mwana wa Aminadabu, wa kabila la Yuda.

13 Sadaka yake ilikuwa: Sahani moja ya fedha yenye uzito wa kilo moja u nusu na birika moja la fedha lenye uzito wa gramu 800 kulingana na vipimo vya hema takatifu; sahani na birika hilo vikiwa vimejazwa unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya sadaka ya nafaka;

14 kisahani kimoja cha dhahabu chenye uzito wa gramu 110 kikiwa kimejazwa ubani;

15 fahali mmoja mchanga; kondoo dume mmoja, na mwanakondoo dume mmoja wa mwaka mmoja, kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa;

16 beberu mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi;

17 na fahali wawili, kondoo madume watano, beberu watano na wanakondoo madume watano wa mwaka mmoja kwa ajili ya tambiko ya sadaka za amani. Hiyo ndiyo iliyokuwa sadaka ya Nashoni mwana wa Aminadabu.

18 Siku ya pili, Nethaneli mwana wa Suari, kiongozi wa kabila la Isakari alitoa sadaka.

19 Nethaneli alitoa: Sahani moja ya fedha ya kilo moja u nusu na bakuli moja la fedha la gramu 800 kulingana na vipimo vya hema takatifu, sahani na bakuli hilo vikiwa vimejazwa unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya tambiko ya nafaka;

20 kisahani kimoja cha dhahabu cha gramu 110 kikiwa kimejazwa ubani;

21 fahali mmoja mchanga, kondoo dume mmoja, na mwanakondoo dume mmoja wa mwaka mmoja, kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa;

22 beberu mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi;

23 fahali wawili, kondoo madume watano, beberu watano na wanakondoo madume watano wa mwaka mmoja kwa ajili ya tambiko ya sadaka za amani. Hiyo ndiyo iliyokuwa sadaka ya Nethaneli mwana wa Suari.

24 Siku ya tatu ikawa zamu ya Eliabu mwana wa Heloni, kiongozi wa kabila la Zebuluni.

25 Sadaka yake ilikuwa: Sahani moja ya fedha ya kilo moja u nusu na bakuli moja la fedha la gramu 800, kulingana na vipimo vya hema takatifu, sahani na bakuli hilo vikiwa vimejazwa unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya sadaka ya nafaka;

26 kisahani kimoja cha dhahabu cha gramu 110 kikiwa kimejazwa ubani;

27 fahali mmoja mchanga, kondoo dume mmoja, na mwanakondoo dume wa mwaka mmoja, kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa;

28 beberu mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi;

29 fahali wawili, kondoo madume watano, beberu watano na wanakondoo madume watano wa mwaka mmoja kwa ajili ya tambiko ya sadaka za amani. Hiyo ndiyo iliyokuwa sadaka ya Eliabu mwana wa Heloni.

30 Siku ya nne ikawa zamu ya Elisuri mwana wa Shedeuri, kiongozi wa kabila la Reubeni.

31 Sadaka yake ilikuwa: Sahani moja ya fedha ya kilo moja u nusu na bakuli moja la fedha la gramu 800, kulingana na vipimo vya hema takatifu, sahani na bakuli hili vikiwa vimejazwa unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya sadaka ya nafaka;

32 kisahani kimoja cha dhahabu cha gramu 110 kikiwa kimejazwa ubani;

33 fahali mmoja mchanga, kondoo dume mmoja, na mwanakondoo dume wa mwaka mmoja, kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa;

34 beberu mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi;

35 fahali wawili, kondoo madume watano, beberu watano na wanakondoo madume watano wa mwaka mmoja kwa ajili ya tambiko ya sadaka za amani. Hiyo ndiyo iliyokuwa sadaka ya Elisuri mwana wa Shedeuri.

36 Siku ya tano ikawa zamu ya Shelumieli mwana wa Suri-shadai, kiongozi wa kabila la Simeoni.

37 Sadaka yake ilikuwa: Sahani moja ya fedha ya kilo moja u nusu na bakuli moja la fedha la gramu 800, kulingana na vipimo vya hema takatifu, sahani na bakuli vikiwa vimejazwa unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya sadaka ya nafaka;

38 kisahani kimoja cha fedha cha gramu 110 kikiwa kimejazwa ubani;

39 fahali mmoja mchanga, kondoo dume mmoja, na mwanakondoo dume mmoja wa mwaka mmoja, kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa;

40 beberu mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi;

41 na fahali wawili, kondoo madume watano, beberu watano na wanakondoo madume watano wa mwaka mmoja kwa ajili tambiko ya sadaka za amani. Hiyo ndiyo iliyokuwa sadaka ya Shelumieli mwana wa Suri-shadai.

42 Siku ya sita ikawa zamu ya Eliasafu mwana wa Deuli, kiongozi wa kabila la Gadi.

43 Sadaka yake ilikuwa: Sahani moja ya fedha ya kilo moja u nusu na bakuli moja la fedha la gramu 800, kulingana na vipimo vya hema takatifu, sahani na bakuli vikiwa vimejazwa unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya sadaka ya nafaka;

44 kisahani kimoja cha dhahabu cha gramu 110 kikiwa kimejazwa ubani;

45 fahali mmoja mchanga, kondoo dume mmoja wa mwaka mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa;

46 beberu mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi;

47 na mafahali wawili, beberu watano, na wanakondoo madume watano wa mwaka mmoja kwa ajili ya tambiko ya sadaka za amani. Hiyo ndiyo iliyokuwa sadaka ya Eliasafu mwana wa Deuli.

48 Siku ya saba ikawa zamu ya Elishama mwana wa Amihudi, kiongozi wa kabila la Efraimu.

49 Sadaka yake ilikuwa: Sahani moja ya fedha ya kilo moja u nusu na bakuli moja la fedha la gramu 800, kulingana na vipimo vya hema takatifu, sahani na bakuli vikiwa vimejazwa unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya sadaka ya nafaka;

50 kisahani kimoja cha dhahabu cha gramu 110 kikiwa kimejazwa ubani;

51 fahali mmoja mchanga, kondoo dume mmoja wa mwaka mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa;

52 beberu mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi;

53 mafahali wawili, kondoo madume watano, beberu watano na wanakondoo madume watano wa mwaka mmoja kwa ajili ya tambiko ya sadaka za amani. Hiyo ndiyo iliyokuwa sadaka ya Elishama mwana wa Amihudi.

54 Siku ya nane ikawa zamu ya Gamalieli mwana wa Pedasuri, kiongozi wa kabila la Manase.

55 Sadaka yake ilikuwa: Sahani moja ya fedha ya kilo moja u nusu, na bakuli la fedha la gramu 800, kulingana na vipimo vya hema takatifu, vikiwa vimejazwa unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya sadaka ya nafaka;

56 kisahani kimoja cha dhahabu cha gramu 110 kilichokuwa kimejazwa ubani;

57 fahali mmoja mchanga, kondoo dume mmoja wa mwaka mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa;

58 beberu mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi;

59 mafahali wawili, kondoo madume watano, beberu watano na wanakondoo madume watano wa mwaka mmoja kwa ajili ya sadaka za amani. Hiyo ndiyo iliyokuwa sadaka ya Gamalieli mwana wa Padasuri.

60 Siku ya tisa ikawa zamu ya Abidani mwana wa Gideoni, kiongozi wa kabila la Benyamini.

61 Sadaka yake ilikuwa: Sahani moja ya fedha ya kilo moja u nusu na bakuli moja la fedha la gramu 800, kulingana na vipimo vya hema takatifu, sahani na bakuli vilikuwa vimejazwa unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya sadaka ya nafaka;

62 kisahani kimoja cha dhahabu cha gramu 110 kilichokuwa kimejazwa ubani;

63 fahali mmoja mchanga, kondoo dume mmoja wa mwaka mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa;

64 beberu mmoja kwa ajili ya sadaka kuondoa dhambi;

65 fahali wawili, kondoo madume watano, beberu watano na wanakondoo madume watano wa mwaka mmoja kwa ajili ya tambiko ya sadaka ya amani. Hiyo ndiyo iliyokuwa sadaka ya Abidani mwana wa Gideoni.

66 Siku ya kumi ikawa zamu ya Ahiezeri mwana wa Amishadai, kiongozi wa kabila la Dani.

67 Sadaka yake ilikuwa: Sahani moja ya fedha ya kilo moja u nusu na bakuli moja la fedha la gramu 800, kadiri ya vipimo vya hema takatifu; sahani na bakuli vilikuwa vimejazwa unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya sadaka ya nafaka;

68 kisahani kimoja cha dhahabu cha gramu 110 kilichokuwa kimejazwa ubani;

69 fahali mmoja wa mwaka mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa;

70 beberu mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi;

71 fahali wawili, kondoo madume watano, beberu watano na wanakondoo madume watano wa mwaka mmoja kwa ajili ya sadaka ya amani. Hiyo ndiyo iliyokuwa sadaka ya Ahiezeri mwana wa Amishadai.

72 Siku ya kumi na moja ikawa zamu ya Pagieli mwana wa Okrani, kiongozi wa kabila la Asheri.

73 Sadaka yake ilikuwa: Sahani ya fedha ya kilo moja u nusu na bakuli moja la fedha la gramu 800 kadiri ya vipimo vya hema takatifu vikiwa vimejazwa unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya sadaka ya nafaka;

74 kisahani kimoja cha dhahabu cha gramu 110 kilichokuwa kimejazwa ubani;

75 fahali mmoja mchanga, kondoo dume mmoja wa mwaka mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa;

76 beberu mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi;

77 fahali wawili, kondoo madume watano, beberu watano na wanakondoo wa mwaka mmoja watano kwa ajili ya kutoa tambiko ya sadaka ya amani. Hiyo ndiyo iliyokuwa sadaka ya Pagieli mwana wa Okrani.

78 Na siku ya kumi na mbili ilikuwa zamu ya Ahira mwana wa Enani, kiongozi wa kabila la Naftali.

79 Sadaka yake ilikuwa: Sahani moja ya fedha ya kilo moja u nusu na bakuli la fedha la gramu 800 kadiri ya vipimo vya hema takatifu; sahani na bakuli vikiwa vimejazwa unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya sadaka ya nafaka;

80 kisahani kimoja cha dhahabu cha gramu 110 ambacho kilikuwa kimejazwa ubani;

81 fahali mmoja mchanga, kondoo dume mmoja wa mwaka mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa;

82 beberu mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi;

83 fahali wawili, kondoo madume watano, beberu watano na wanakondoo madume wa mwaka mmoja watano kwa ajili ya tambiko ya sadaka ya amani. Hiyo ndiyo iliyokuwa sadaka ya Ahira mwana wa Enani.

84 Jumla ya matoleo ya sadaka za viongozi wa Israeli kwa ajili ya madhabahu siku ilipowekwa wakfu ilikuwa: Sahani za fedha kumi na mbili, birika za fedha kumi na mbili, na visahani vya dhahabu kumi na viwili.

85 Kila sahani ya fedha, ilikuwa yenye uzito wa kilo moja u nusu na kila kisahani kilikuwa chenye uzito wa gramu 800. Hivyo vyombo vyote vilikuwa na uzito wa kilo ishirini na saba na gramu 600 kadiri ya vipimo vya hema takatifu.

86 Vile visahani vya dhahabu kumi na viwili vyenye kujaa ubani, kila kimoja kikiwa na uzito wa gramu 110 kadiri ya vipimo vya hema takatifu vilikuwa na jumla ya uzito wa kilo moja na gramu 320.

87 Jumla ya wanyama wote wa sadaka ya kuteketezwa ilikuwa mafahali kumi na wawili, kondoo madume kumi na wawili, na wanakondoo madume wa mwaka mmoja kumi na wawili, pamoja na sadaka ya nafaka na beberu kumi na wawili kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi,

88 na kwa ajili ya tambiko ya sadaka ya amani, jumla ya wanyama waliotolewa ilikuwa mafahali ishirini na wanne, kondoo madume sitini, beberu sitini, na wanakondoo madume wa mwaka mmoja sitini. Hiyo ndiyo iliyokuwa sadaka iliyotolewa kwa ajili ya madhabahu, baada ya madhabahu hiyo kupakwa mafuta.

89 Wakati Mose alipoingia ndani ya hema la mkutano ili kuongea na Mwenyezi-Mungu, alisikia sauti kutoka upande wa juu wa kiti cha rehema, kilichokuwa juu ya sanduku la agano, kutoka kati ya wale viumbe wawili wenye mabawa.

8

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

2 “Mwambie Aroni kwamba wakati atakapoziweka zile taa saba kwenye kinara, azipange ili ziangaze upande wa mbele wa kinara hicho.”

3 Aroni akatii maagizo hayo, akaziweka taa hizo ili ziangaze upande wa mbele wa kinara, kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.

4 Toka sehemu za juu mpaka chini kinara hicho cha taa kilikuwa kimetengenezwa kwa ustadi mkubwa kwa dhahabu iliyofuliwa kufuatana na mfano ambao Mwenyezi-Mungu alikuwa amemwonesha Mose.

5 Tena Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

6 “Watenge Walawi kutoka Waisraeli, uwatakase.

7 Hivi ndivyo utakavyowatakasa: Wanyunyizie maji ya kutakasia kisha uwaambie wajinyoe mwili mzima, wafue nguo zao na kujitakasa.

8 Kisha watatwaa fahali mmoja mchanga pamoja na sadaka yake ya nafaka, yaani unga laini uliochanganywa na mafuta; nawe utatwaa fahali mwingine mchanga kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi.

9 Kisha utawakusanya watu wote wa Israeli na kuwaleta Walawi mbele ya hema la mkutano.

10 Utakapowaleta Walawi mbele yangu, Waisraeli watawawekea Walawi mikono,

11 halafu Aroni atawaweka hao mbele yangu kama sadaka ya kutikiswa kutoka kwa Waisraeli wanihudumie.

12 Kisha Walawi wataweka mikono yao juu ya vichwa vya fahali hao; mmoja wao utamtoa kuwa sadaka ya kuondoa dhambi, na huyo mwingine utamtoa kuwa sadaka ya kuteketezwa inayotolewa kwangu, ili kuwafanyia upatanisho Walawi.

13 “Kisha utawasimamisha Walawi mbele ya Aroni na wanawe na kuwaweka mbele yangu kama sadaka ya kutikiswa.

14 Hivi ndivyo utakavyowatenga Walawi miongoni mwa Waisraeli wengine ili wawe wangu.

15 Baada ya kuwatakasa Walawi na kuwatoa kama sadaka ya kutikiswa wataingia ili kuhudumu katika hema la mkutano.

16 Hao wametolewa wawe wangu kabisa, badala ya wazaliwa wa kwanza wa Waisraeli.

17 Maana wazaliwa wote wa kwanza miongoni mwa Waisraeli ni wangu, wanadamu na wanyama; kwa sababu katika siku nilipowaua wazaliwa wote wa kwanza nchini Misri, niliwaweka wakfu kwangu.

18 Sasa ninawachukua Walawi badala ya wazaliwa wa kwanza wa Waisraeli,

19 na nimempa hao Aroni na wanawe, kama zawadi kutoka kwa Waisraeli, ili wafanye kazi katika hema la mkutano kwa ajili ya Waisraeli na kuwafanyia upatanisho ili pasitokee pigo miongoni mwa Waisraeli wakikaribia mahali patakatifu.”

20 Kwa hiyo Mose, Aroni na jumuiya yote ya Waisraeli wakawaweka wakfu Walawi, kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.

21 Walawi wakajitakasa dhambi na kuzifua nguo zao, naye Aroni akawatoa kama sadaka ya kutikiswa mbele ya Mwenyezi-Mungu. Pia, Aroni alifanya upatanisho kwa ajili yao ili kuwatakasa.

22 Baada ya hayo Walawi waliingia na kufanya huduma yao katika hema la mkutano chini ya usimamizi wa Aroni na wanawe, kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.

23 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

24 “Kila Mlawi mwenye umri wa miaka ishirini na mitano na zaidi, atahudumu katika hema langu la mkutano;

25 na kustaafu afikishapo umri wa miaka hamsini.

26 Baada ya hapo, anaweza kuwasaidia Walawi wenzake wanapohudumu katika hema, lakini haruhusiwi kutoa huduma yoyote peke yake. Ndivyo utakavyowapangia kazi Walawi.”

9

1 Kisha mnamo mwezi wa kwanza wa mwaka wa pili baada ya Waisraeli kutoka Misri, Mwenyezi-Mungu aliongea na Mose katika jangwa la Sinai. Alimwambia:

2 “Waisraeli sharti waiadhimishe sikukuu ya Pasaka wakati uliopangwa.

3 Hii itakuwa siku ya kumi na nne ya mwezi huu; wakati wa jioni watafanya hivyo kufuatana na masharti na maagizo yake yote.”

4 Kwa hiyo, Mose akawaambia watu kwamba wanapaswa kuiadhimisha sikukuu ya Pasaka.

5 Basi, wakaiadhimisha Pasaka jioni, siku ya kumi na nne ya mwezi wa kwanza, katika jangwa la Sinai. Waisraeli walifanya yote kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.

6 Lakini, baadhi ya watu waliokuwapo walikuwa hawawezi kuiadhimisha sikukuu hiyo ya Pasaka kwa sababu walikuwa wamegusa maiti, wakawa najisi. Hao waliwaendea Mose na Aroni,

7 wakawaambia, “Sisi tu najisi kwa kuwa tumegusa maiti, lakini kwa nini tukatazwe kumtolea Mwenyezi-Mungu sadaka zake kwa wakati uliopangwa pamoja na Waisraeli wengine?”

8 Mose akawajibu, “Ngojeni mpaka hapo nitakapopata maagizo juu yenu kutoka kwa Mwenyezi-Mungu.”

9 Naye Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,

10 “Mmoja wenu au mmoja wa wazawa wenu akiwa najisi kwa sababu amegusa maiti au akiwa mbali safarini, lakini akiwa anataka kuiadhimisha sikukuu ya Pasaka,

11 mtu kama huyo anaruhusiwa kufanya hivyo mwezi mmoja baadaye, jioni ya siku ya kumi na nne ya mwezi wa pili. Ataiadhimisha kwa kula mikate isiyotiwa chachu na mboga chungu.

12 Wasibakize chakula chochote hadi asubuhi, wala wasivunje hata mfupa mmoja wa wanyama wa Pasaka. Wataiadhimisha sikukuu hii ya Pasaka kulingana na kanuni zake zote.

13 Lakini mtu yeyote ambaye ni safi au hayumo safarini, asipoiadhimisha sikukuu ya Pasaka, atatengwa na watu wake kwa kuwa hakunitolea sadaka kwa wakati uliopangwa. Ni lazima aadhibiwe kwa ajili ya dhambi yake.

14 “Ikiwa kuna mgeni anayeishi pamoja nanyi na anapenda kuiadhimisha sikukuu ya Pasaka, mtu huyo sharti afanye hivyo kulingana na masharti na maagizo yote ya Pasaka. Kila mtu atafuata masharti yaleyale, akiwa mgeni au mwenyeji.”

15 Siku ambayo hema takatifu lilisimikwa, wingu lilishuka na kulifunika hema la maamuzi. Wakati wa usiku wingu hilo lilionekana kama moto mpaka asubuhi.

16 Hivyo ndivyo ilivyokuwa kila siku; wingu lililifunika hema mchana, na usiku lilionekana kama moto.

17 Kila mara wingu hilo lilipoinuliwa juu ya hema, Waisraeli walivunja kambi na kupiga kambi tena mahali wingu hilo lilipotua.

18 Walisafiri kwa amri ya Mwenyezi-Mungu, na kupiga kambi tena kwa amri yake. Muda wote wingu hilo lilipokuwa juu ya hema, watu walikaa katika kambi hiyo.

19 Hata kama wingu hilo lilikaa juu ya hema kwa muda wa siku nyingi, Waisraeli walimtii Mwenyezi-Mungu, nao hawakuondoka.

20 Wakati mwingine wingu hilo lilikaa juu ya hema kwa muda wa siku chache tu; lakini kila wakati Waisraeli walibaki kambini; walihama kama Mwenyezi-Mungu alivyowaamuru.

21 Wakati mwingine wingu lilikaa juu ya hema tangu jioni mpaka asubuhi tu; na mara tu lilipoinuliwa, hao watu pia walifunga safari. Na ikiwa lilikaa juu ya hema mchana kutwa na usiku kucha, wao waliondoka tu wingu lilipoinuliwa.

22 Ikiwa ni siku mbili, mwezi, mwaka au zaidi, muda wote wingu hilo lilipokuwa juu ya hema, Waisraeli hawakuhama; lakini lilipoinuliwa, nao pia walihama.

23 Kwa agizo la Mwenyezi-Mungu walipiga kambi na kwa agizo la Mwenyezi-Mungu walisafiri. Walishika agizo la Mwenyezi-Mungu kama alivyotoa amri yake kwa njia ya Mose.

10

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

2 “Tengeneza tarumbeta mbili kwa fedha iliyofuliwa. Utazitumia tarumbeta hizo wakati wa kuwaita watu na wakati wa kuvunja kambi.

3 Tarumbeta zote mbili zikipigwa pamoja, watu wote watakusanyika karibu nawe mbele ya lango la hema la mkutano.

4 Lakini kama ikipigwa tarumbeta moja tu, basi ni viongozi tu wa makabila ya Israeli watakaokusanyika karibu nawe.

5 Ishara hiyo ikitolewa kwa kupiga tarumbeta, wakazi wa kambi za mashariki wataanza safari.

6 Ishara hiyo ikipigwa mara ya pili, wale wa kambi za upande wa kusini wataanza kuondoka. Ishara hiyo ya tarumbeta itatolewa kila wakati wa kuanza safari.

7 Lakini wakati wa kuwaita watu wakusanyike pamoja, tarumbeta zitapigwa kwa njia ya kawaida.

8 Wazawa wa Aroni, makuhani, ndio watakaopiga tarumbeta hizo. Utaratibu huo utafuatwa daima katika vizazi vyenu vyote.

9 “Wakati wa vita nchini mwenu dhidi ya adui wanaowashambulia, mtatoa ishara ya vita kwa kupiga tarumbeta hizi ili Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu apate kuwakumbuka na kuwaokoa na adui zenu.

10 Hali kadhalika katika siku zenu za furaha, kama vile sikukuu za mwandamo wa mwezi na sikukuu nyinginezo, mtazipiga tarumbeta hizi wakati mnapotoa sadaka zenu za kuteketezwa na tambiko za sadaka zenu za amani. Hapo mimi Mungu wenu nitawakumbukeni. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.”

11 Mnamo siku ya ishirini ya mwezi wa pili, mwaka wa pili tangu wana wa Israeli walipoondoka Misri, wingu lililokuwa juu ya hema la maamuzi liliinuliwa,

12 nao Waisraeli wakaanza safari yao kutoka jangwa la Sinai. Wingu hilo lilipaa na hatimaye likatua katika jangwa la Parani.

13 Kwa mara ya kwanza Waisraeli walifunga safari hiyo kwa amri ya Mwenyezi-Mungu kama ilivyotolewa na Mose.

14 Wale waliokuwa chini ya bendera ya kikosi cha kabila la Yuda, walitangulia, kundi moja baada ya jingine. Kiongozi wao alikuwa Nashoni mwana wa Aminadabu.

15 Nethaneli mwana wa Suari, alikuwa kiongozi wa kikosi cha kabila la Isakari.

16 Naye Eliabu mwana wa Heloni, alikuwa kiongozi wa kikosi cha kabila la Zebuluni.

17 Kisha, hema lilishushwa, na watu wa ukoo wa Gershoni na wa Merari ambao walilibeba, walianza kuondoka.

18 Halafu, watu waliokuwa chini ya bendera ya kikosi kilichoongozwa na kabila la Reubeni, walifuata kundi moja baada ya jingine. Kiongozi wao alikuwa Elisuri mwana wa Shedeuri.

19 Shelumieli mwana wa Suri-shadai, aliliongoza kabila la Simeoni.

20 Naye Eliasafu mwana wa Deueli, aliliongoza kabila la Gadi.

21 Kisha walifuata watu wa ukoo wa Kohathi, wakiwa wamebeba vyombo vitakatifu. Walipowasili, hema lilikuwa limekwisha simikwa.

22 Baada ya hao, walifuata watu waliokuwa chini ya bendera ya kikosi kilichoongozwa na kabila la Efraimu, kundi moja baada ya jingine. Kiongozi wao alikuwa Elishama mwana wa Amihudi.

23 Gamalieli mwana wa Pedasuri aliliongoza kabila la Manase,

24 naye Abidani mwana wa Gideoni, aliliongoza kabila la Benyamini.

25 Mwisho, wale waliokuwa chini ya bendera ya kikosi kilichoongozwa na kabila la Dani, waliokuwa kama walinzi nyuma ya vikosi vyote, walisafiri, kundi moja baada ya jingine. Hawa waliongozwa na Ahiezeri mwana wa Amishadai.

26 Pagieli, mwana wa Okrani, aliliongoza kabila la Asheri.

27 Naye Ahira mwana wa Enani, aliliongoza kabila la Naftali.

28 Huu basi, ndio utaratibu walioufuata Waisraeli kulingana na makundi yao, kila wakati walipovunja kambi na kuanza kusafiri tena.

29 Mose alimwambia shemeji yake, Hobabu mwana wa Reueli, Mmidiani, mkwe wake, “Sisi tunasafiri kwenda mahali ambapo Mwenyezi-Mungu amesema ‘Nitawapa nyinyi mahali hapo’. Basi, twende pamoja, nasi tutakutendea mema; maana Mwenyezi-Mungu ameahidi kutupa sisi Waisraeli fanaka.”

30 Lakini Hobabu akajibu, “Mimi sitafuatana nanyi; ila nitarudi katika nchi yangu na kwa jamaa zangu.”

31 Mose akamwambia, “Tafadhali usituache, maana wewe unajua mahali tunapoweza kupiga kambi jangwani, na unaweza kuwa kiongozi wetu.

32 Tena ukiandamana nasi chochote chema atakachotutendea Mwenyezi-Mungu, ndicho utakachotendewa nawe pia.”

33 Basi, watu wakasafiri toka Sinai, Mlima wa Mwenyezi-Mungu, mwendo wa siku tatu. Sanduku la agano la Mwenyezi-Mungu liliwatangulia mwendo wa siku tatu, ili kuwatafutia mahali pa kupiga kambi.

34 Kila waliposafiri kutoka kambi moja hadi nyingine, wingu la Mwenyezi-Mungu lilikuwa juu yao mchana.

35 Kila wakati sanduku liliposafiri kwenda mbele, Mose alisema, “Inuka, ee Mwenyezi-Mungu, uwatawanye adui zako, na hao wanaokuchukia uwafanye wakimbie kutoka mbele yako.”

36 Na kila wakati liliposimama, Mose alisema, “Warudie, ee Mwenyezi-Mungu, hawa maelfu na maelfu ya Israeli.”

11

1 Watu walianza kumlalamikia Mwenyezi-Mungu juu ya taabu zao. Mwenyezi-Mungu aliposikia, alishikwa na hasira, akawapelekea moto. Moto huo uliwaka kati yao na kuchoma upande mmoja wa kambi.

2 Watu wakamlilia Mose, naye akamwomba Mwenyezi-Mungu na moto huo ukazimika.

3 Kwa hiyo, mahali hapo pakaitwa Tabera, kwa sababu hapo moto wa Mwenyezi-Mungu uliwaka kati ya watu.

4 Miongoni mwa Waisraeli kulikuwa na kundi fulani lililoandamana nao ambalo lilikuwa na hamu kubwa. Waisraeli kwa mara nyingine walilia, wakisema. “Laiti kama tungeweza kupata nyama ya kula!

5 Tunakumbuka, samaki tuliokula kule Misri bila malipo, matango, matikiti, mboga, vitunguu na vitunguu saumu!

6 Lakini sasa nguvu zimetuishia na hakuna chakula kingine isipokuwa hii mana tu!”

7 Mana ilikuwa kama punje za mtama, rangi yake ilikuwa kama ya bedoza.

8 Watu walizungukazunguka na kuikusanya, kisha waliisaga kwa mawe ya kusagia au waliitwanga kwa vinu, halafu waliitokosa vyunguni na kutengeneza maandazi. Ladha yake ilikuwa kama ya maandazi yaliyokaangwa kwa mafuta.

9 (Umande ulipoanguka kambini wakati wa usiku, mana pia ilianguka pamoja na huo umande).

10 Mose alisikia watu wakilia katika familia zote, kila mtu penye lango la hema lake. Basi, hasira ya Mwenyezi-Mungu iliwaka sana; naye Mose alichukizwa.

11 Ndipo Mose alipomwambia, Mwenyezi-Mungu “Kwa nini unanitendea vibaya mimi mtumishi wako? Mbona hupendezwi nami, kwa nini umenitwika mzigo wa kuwatunza watu wote hawa?

12 Je, ni mimi niliyewazaa, hata ukaniambia niwabebe kifuani pangu kama mlezi abebavyo mtoto mchanga, na kuwapeleka mpaka nchi uliyoapa kuwapa babu zao?

13 Nitapata wapi nyama ya kuwalisha watu hawa wote? Maana wanalia mbele yangu wakisema: ‘Tupe nyama tule!’

14 Siwezi kuwatunza watu wote hawa peke yangu; hilo ni jukumu kubwa mno kwangu!

15 Ikiwa hivi ndivyo utakavyonitenda, afadhali uniue mara moja! Kama ninapata kibali mbele yako, usiniache niikabili taabu yangu.”

16 Basi, Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, “Wakusanyeni wazee sabini wa Israeli, ambao wewe unajua wanaheshimiwa na kukubaliwa na watu kuwa viongozi, uwalete kwenye hema la mkutano, wasimame karibu nawe.

17 Nitashuka huko na kuzungumza nawe; nitachukua sehemu ya roho niliyokupa, niwape watu hao. Nao watabeba jukumu la kuwatunza watu hawa pamoja nawe, usije ukaubeba mzigo huo peke yako.

18 Sasa waambie watu hivi: Jitakaseni kwa ajili ya kesho; mtakula nyama. Mwenyezi-Mungu amesikia mkilia na kusema kuwa hakuna wa kuwapeni nyama, na kwamba hali yenu ilikuwa nzuri zaidi mlipokuwa Misri. Sasa Mwenyezi-Mungu atawapeni nyama, nanyi sharti muile.

19 Mtakula nyama si kwa muda wa siku moja tu, au mbili, au tano, au kumi au ishirini,

20 bali kwa muda wa mwezi mzima! Mtaila hadi iwatoke puani, mpaka muikinai. Yote hayo ni kwa sababu mmemkataa Mwenyezi-Mungu aliye hapahapa miongoni mwenu, na kulia mbele yake mkisema, ‘Kwa nini tulitoka Misri?’”

21 Lakini Mose alimwambia Mwenyezi-Mungu, “Idadi ya watu ninaowaongoza hapa ni 600,000 waendao kwa miguu, nawe wasema, ‘Nitawapa nyama ya kuwatosha mwezi mzima!’

22 Je, panaweza kuchinjwa kondoo na ng'ombe wa kuwatosheleza? Je, samaki wote baharini wavuliwe kwa ajili yao?”

23 Mwenyezi-Mungu akamjibu Mose, “Je, uwezo wangu umepungua? Utaona basi kama neno langu litakuwa la kweli kwako au la.”

24 Basi, Mose akaenda na kuwajulisha watu yale aliyosema Mwenyezi-Mungu. Kisha, akakusanya wazee sabini kutoka miongoni mwa wazee viongozi nao akawaweka kandokando kuizunguka hema.

25 Hapo, Mwenyezi-Mungu akashuka katika wingu na kuzungumza naye. Halafu akatwaa sehemu ya roho aliyokuwa amempa Mose, akawapa kila mmoja wa wale wazee sabini. Walipoingiwa na roho hiyo, wazee hao walianza kutoa unabii, lakini hawakurudia kufanya hivyo.

26 Wazee wawili kati ya wale sabini waliochaguliwa, Eldadi na Medadi, walikuwa wamebaki kambini wenzao walipokwenda kwenye hema. Roho iliwajia humohumo kambini, wakaanza kutoa unabii mahali walipokuwa.

27 Kijana mmoja alitoka mbio na kumwambia Mose, “Eldadi na Medadi wanatoa unabii kambini.”

28 Hapo, Yoshua, mwana wa Nuni, ambaye alikuwa msaidizi wa Mose tangu ujana wake, akamwambia Mose, “Bwana wangu, wakataze!”

29 Lakini Mose akamjibu, “Je, unaona wivu kwa ajili yangu? Laiti Mwenyezi-Mungu angewapa watu wake wote roho yake nao wakawa manabii!”

30 Kisha Mose alirudi kambini pamoja na wale wazee sabini wa Israeli.

31 Baadaye Mwenyezi-Mungu akavumisha upepo kwa ghafla, ukaleta kware kutoka baharini na kuwafanya watue kando ya kambi, mwendo wa siku moja hivi kila upande kuizunguka kambi, wakarundikana chini karibu kimo cha mita moja hivi.

32 Basi, siku hiyo yote, kutwa kucha, na siku iliyofuata watu walishughulika kukusanya kware; hakuna mtu aliyekusanya chini ya kilo 1,000. Wakawaanika kila mahali kandokando ya kambi ili wawakaushe.

33 Kulipokuwa bado kuna nyama kwa wingi na kabla watu hawajawamaliza kuila, Mwenyezi-Mungu aliwakasirikia watu, akawapiga watu kwa pigo kubwa sana.

34 Kwa hiyo mahali hapo palipewa jina Kibroth-hataava; kwa sababu huko ndiko walikowazika watu waliokuwa walafi.

35 Kutoka hapo Kibroth-hataava watu walisafiri mpaka Haserothi, wakapiga kambi yao na kukaa huko.

12

1 Kisha Miriamu na Aroni walianza kumsema vibaya Mose kwa sababu ya mwanamke Mkushi aliyekuwa amemwoa.

2 Wakasema, “Hivi kwani Mwenyezi-Mungu amezungumza kwa kumwagiza Mose peke yake? Je, hajazungumza nasi pia?” Mwenyezi-Mungu aliyasikia maneno hayo.

3 (Mose alikuwa mtu mnyenyekevu kuliko watu wengine wote waliokuwa duniani.)

4 Halafu ghafla, Mwenyezi-Mungu akawaambia Mose, Aroni na Miriamu, “Njoni katika hema la mkutano, nyinyi watatu.” Basi, wote watatu wakaenda kwenye hema la mkutano.

5 Hapo Mwenyezi-Mungu akashuka katika nguzo ya wingu, akasimama kwenye mlango wa hema, akawaita Aroni na Miriamu. Wote wawili wakasogea mbele.

6 Kisha Mwenyezi-Mungu akawaambia, “Sikilizeni maneno yangu: Kama kuna nabii miongoni mwenu, mimi Mwenyezi-Mungu hujifahamisha kwake katika maono na kuongea naye katika ndoto.

7 Lakini kumhusu mtumishi wangu Mose, hali ni tofauti kabisa. Yeye ana jukumu la kuwatunza watu wangu wote.

8 Mimi huongea naye ana kwa ana, waziwazi na si kwa kutumia mafumbo. Yeye huliona umbo langu mimi Mwenyezi-Mungu. Kwa nini, basi, hamkuogopa kusema vibaya dhidi ya mtumishi wangu Mose?”

9 Hapo Mwenyezi-Mungu akawaka hasira dhidi yao, akaondoka, akaenda zake.

10 Wingu lilipoondoka juu ya hema la mkutano, Miriamu alionekana ana ukoma, mweupe kama theluji. Aroni alipogeuka na kumtazama Miriamu, alishangaa kuona kuwa ameshikwa na ukoma.

11 Hapo, Aroni akamwambia Mose, “Ewe bwana wangu, usituadhibu kwa kuwa tumetenda mambo ya kipumbavu na kufanya dhambi.

12 Usimfanye Miriamu awe kama mtu aliyezaliwa mfu, ambaye karibu nusu ya mwili wake umelika.”

13 Mose akamlilia Mwenyezi-Mungu akisema, “Nakusihi, ee Mungu, umponye.”

14 Lakini Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, “Kama baba yake angemtemea mate usoni, je, hangeaibika kwa siku saba? Basi, mtoe nje ya kambi akae huko muda wa siku saba, kisha unaweza kumruhusu arudi kambini.”

15 Kwa hiyo, Miriamu akafukuzwa nje ya kambi kwa muda wa siku saba. Watu hawakuanza tena safari hadi Miriamu aliporudishwa tena kambini.

16 Baada ya hayo, watu walifanya safari kutoka Haserothi, wakapiga kambi katika jangwa la Parani.

13

1 Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,

2 “Tuma watu waende wakaipeleleze nchi ya Kanaani ambayo ninawapa wana wa Israeli. Utatuma mtu mmoja kutoka katika kila kabila, na mtu huyo lazima awe kiongozi katika kabila lake.”

3 Basi, kwa mujibu wa agizo la Mwenyezi-Mungu, Mose akatuma watu kutoka jangwa la Parani. Watu wote waliotumwa walikuwa viongozi wa makabila mbalimbali ya wana wa Israeli.

4 Ifuatayo ndiyo orodha ya majina ya watu hao: Kabila la Reubeni, Shamua mwana wa Zakuri.

5 Kabila la Simeoni, Shafati mwana wa Hori.

6 Kabila la Yuda, Kalebu mwana wa Yefune.

7 Kabila la Isakari, Igali mwana wa Yosefu.

8 Kabila la Efraimu, Hoshea mwana wa Nuni.

9 Kabila la Benyamini, Palti mwana wa Rafu.

10 Kabila la Zebuluni, Gadieli mwana wa Sodi.

11 Kabila la Yosefu (yaani kabila la Manase), Gadi mwana wa Susi.

12 Kabila la Dani, Amieli mwana wa Gemali.

13 Kabila la Asheri, Sethuri mwana wa Mikaeli.

14 Kabila la Naftali, Nabi mwana wa Wofsi.

15 Kabila la Gadi, Geueli mwana wa Maki.

16 Haya ndiyo majina ya watu ambao Mose aliwatuma kwenda kuipeleleza nchi ya Kanaani. Mose alimpa Hoshea mwana wa Nuni jina jipya, akamwita Yoshua.

17 Alipowatuma kwenda kuipeleleza nchi ya Kanaani, Mose aliwaambia: “Nendeni juu kule Negebu, hadi kwenye nchi ya milima,

18 mkaipeleleze nchi ilivyo. Chunguzeni pia kama watu wanaoishi humo ni wenye nguvu au dhaifu, wengi au wachache.

19 Pelelezeni kama nchi hiyo ni nzuri au mbaya, na kama miji wanamoishi ni kambi au ni nyumba zilizozungukwa na ngome.

20 Chunguzeni pia kama nchi yenyewe ni tajiri au maskini, ina miti au haina. Muwe na mioyo ya ujasiri na mnaporudi chukueni baadhi ya matunda ya nchi hiyo.” Hayo yalikuwa majira ya zabibu zianzapo kuiva.

21 Basi, watu hao wakaenda na kuipeleleza nchi toka jangwa la Sini hadi Rehobu, karibu na njia ya kuingilia Hamathi.

22 Walikwenda hadi Negebu wakapita mpaka mji wa Hebroni. Humo waliwakuta Waahimani, Washeshai na Watalmai, wazawa wa Anaki. (Mji wa Hebroni ulikuwa umejengwa miaka saba kabla ya mji wa Soani ulioko nchini Misri).

23 Walipofika katika Bonde la Eshkoli, watu hao walikata shada la mzabibu lililokuwa na matunda mengi nalo lilibebwa na watu wawili juu ya mti. Walichukua pia makomamanga kadhaa na tini.

24 Mahali hapo paliitwa Bonde la Eshkoli kwa sababu ya shada ambalo watu hao wa Israeli walikata kutoka mahali hapo.

25 Baada ya kuipeleleza nchi kwa muda wa siku arubaini, watu hao walirudi.

26 Waliwaendea Mose, Aroni na jumuiya ya Waisraeli huko Kadeshi, katika jangwa la Parani, wakatoa taarifa ya mambo waliyoyaona na kuwaonesha matunda ya nchi.

27 Walimwambia Mose, “Tuliifikia nchi uliyotutuma tuipeleleze; hiyo ni nchi inayotiririka maziwa na asali, na hili ni tunda lake.

28 Lakini wenyeji wake ni wenye nguvu sana, na miji yao ni imara na mikubwa sana. Zaidi ya hayo, huko tuliona wazawa wa Anaki.

29 Waamaleki wanakaa katika eneo la Negebu; Wahiti, Wayebusi na Waamori wanakaa katika eneo la milima, na Wakanaani wanakaa karibu na bahari ya Mediteranea na karibu na kingo za mto Yordani.”

30 Lakini Kalebu aliwanyamazisha watu mbele ya Mose, akasema, “Twende mara moja tukaimiliki nchi hiyo. Kwa kuwa tunao uwezo sana wa kushinda.”

31 Lakini watu walioandamana naye kuipeleleza nchi wakasema, “Hatutaweza kupigana na watu hao; wao wana nguvu kuliko sisi.”

32 Kwa hiyo wakaeneza mambo ya uongo kati ya wana wa Israeli kuhusu nchi waliyoipeleleza, wakisema, “Nchi hiyo inawaua watu wake. Pia watu wote tuliowaona huko ni wakubwa sana.

33 Tuliona majitu huko, wazawa wa Anaki. Sisi tulijiona kuwa kama panzi mbele yao, na ndivyo walivyotuona sisi.”

14

1 Jumuiya yote ya Waisraeli ikaangua kilio kikubwa, watu wakalia usiku ule.

2 Waliwalalamikia Mose na Aroni wakisema, “Afadhali tungefia Misri! Afadhali tungefia papa hapa jangwani!

3 Kwa nini Mwenyezi-Mungu anatupeleka katika nchi hiyo? Tutauawa vitani, na wake zetu na watoto wetu watachukuliwa mateka! Si afadhali turudi Misri?”

4 Basi wakaanza kuambiana, “Na tuchague kiongozi, turudi Misri.”

5 Hapo, Mose na Aroni wakaanguka kifudifudi mbele ya jumuiya yote ya Waisraeli.

6 Yoshua, mwana wa Nuni, na Kalebu, mwana wa Yefune, ambao walikuwa miongoni mwa wale watu waliokwenda kuipeleleza hiyo nchi, wakazirarua nguo zao

7 na kuiambia jumuiya yote ya Waisraeli, “Nchi tuliyokwenda kuipeleleza ni nzuri kupita kiasi.

8 Ikiwa Mwenyezi-Mungu amependezwa nasi, atatupeleka huko na kutupa nchi inayotiririka maziwa na asali.

9 Mradi tu msimwasi Mwenyezi-Mungu, wala msiwaogope wenyeji wa nchi hiyo. Maana wao ni mboga tu kwetu; kinga yao imekwisha ondolewa kwao, naye Mwenyezi-Mungu yu pamoja nasi; msiwaogope!”

10 Lakini jumuiya yote ikatishia kuwapiga mawe. Ghafla, utukufu wa Mwenyezi-Mungu ukatokea juu ya hema la mkutano, mbele ya Waisraeli wote.

11 Kisha Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose, “Watu hawa watanidharau mpaka lini? Na, mpaka lini wataendelea kutoniamini, hata pamoja na miujiza yote niliyotenda kati yao?

12 Nitawapiga kwa maradhi mabaya na kuwatupilia mbali; lakini, kutokana nawe, nitaunda taifa lingine kubwa, lenye nguvu kuliko wao.”

13 Lakini Mose akamwambia Mwenyezi-Mungu, “Uliwatoa watu hawa nchini Misri kwa nguvu yako. Wamisri watakaposikia kwamba umewatenda hivyo watu wako,

14 watawapasha habari wakazi wa nchi hii. Maana watu hawa wamekwisha pata habari kwamba wewe, ee Mwenyezi-Mungu, u pamoja nasi; maana wewe, ee Mwenyezi-Mungu, unaonekana waziwazi wingu lako linaposimama juu yetu, na kwamba wewe hututangulia mchana kwa nguzo ya wingu na usiku kwa nguzo ya moto.

15 Sasa basi, ukiwaua watu wako wote kwa mara moja, mataifa ambayo yamekwisha sikia sifa zako yatasema,

16 ‘Mwenyezi-Mungu aliwaua watu wake jangwani kwa sababu alishindwa kuwapeleka katika nchi aliyoahidi kuwapa.’

17 Basi, sasa nakusihi, ee Mwenyezi-Mungu, utuoneshe uwezo wako kwa kufanya kama ulivyotuahidi uliposema,

18 ‘Mimi Mwenyezi-Mungu si mwepesi wa hasira, ni mwenye fadhili nyingi, na ni mwenye kusamehe uovu na makosa. Lakini kwa vyovyote vile sitakosa kuwaadhibu watoto na wajukuu hadi kizazi cha tatu na cha nne kwa dhambi za wazazi wao.’

19 Nakusihi uwasamehe watu hawa dhambi zao, kadiri ya fadhili zako nyingi kama vile ulivyowasamehe tangu watoke Misri hadi sasa.”

20 Mwenyezi-Mungu akajibu, “Nimewasamehe kama ulivyoomba.

21 Lakini kwa kweli, kama niishivyo na kadiri dunia itakavyojaa utukufu wangu,

22 hakuna hata mmoja wao ambaye amewahi kuuona utukufu wangu na miujiza yangu niliyoifanya Misri na jangwani kisha akazidi kunijaribu mara hizi zote bila ya kutii sauti yangu,

23 ataiona nchi ile niliyoapa kuwapatia babu zao; kadhalika hata wale wanaonidharau pia hawataiona.

24 Bali kwa sababu mtumishi wangu Kalebu ni tofauti, na amenitii kikamilifu, nitamfikisha kwenye nchi hiyo aliyoingia na wazawa wake wataimiliki.

25 Kwa kuwa Waamaleki na Wakanaani wanakaa katika mabonde ya nchi hiyo, kesho geukeni nyuma mwende jangwani kuelekea bahari ya Shamu.”

26 Kisha Mwenyezi-Mungu akamwuliza Mose na Aroni,

27 “Kundi hili la watu waovu litaendelea kuninungunikia mpaka lini? Nimechoka na haya manunguniko ya Waisraeli juu yangu!

28 Sasa wajibu hivi: Kama niishivyo, nasema mimi Mwenyezi-Mungu, nitawatendeeni yaleyale niliyosikia mkiyasema:

29 Mtakufa na miili yenu itatupwa humuhumu jangwani, kwa sababu mmenungunika dhidi yangu, hakuna hata mmoja wenu mwenye umri wa kuanzia miaka ishirini na zaidi,

30 atakayeingia katika nchi hiyo ambayo niliapa kuwapa iwe yenu, isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune, na Yoshua mwana wa Nuni.

31 Nyinyi mlisema kuwa watoto wenu watatekwa nyara, lakini mimi nitawafikisha watoto wenu kwenye nchi mliyoidharau, ili waijue na iwe makao yao.

32 Lakini nyinyi, mtafia humuhumu jangwani.

33 Watoto wenu watatangatanga na kutaabika humu jangwani kwa muda wa miaka arubaini kwa ajili ya ukosefu wenu wa imani mpaka mtu wenu wa mwisho atakapofia jangwani.

34 Kutokana na makosa yenu, mtataabika kwa muda wa miaka arubaini, sawa na zile siku arubaini mlizopeleleza ile nchi, mwaka mmoja kwa kila siku moja; mtatambua kwamba mimi nimechukizwa.

35 Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema: Hakika nitawatenda hivyo nyinyi nyote mliokusanyika hapa kunipinga. Wote wataishia humuhumu jangwani na ni humu watakamofia.”

36 Wale watu ambao Mose aliwatuma kwenda kuipeleleza ile nchi waliorudi na kusababisha watu wamnungunikie Mwenyezi-Mungu kwa kuleta taarifa mbaya dhidi ya nchi,

37 watu hao waliotoa taarifa ya uovu kuhusu hiyo nchi, walikufa kwa pigo mbele ya Mwenyezi-Mungu.

38 Lakini Yoshua mwana wa Nuni, na Kalebu mwana wa Yefune, walibaki hai miongoni mwa wale watu waliokwenda kuipeleleza nchi.

39 Naye Mose aliwaambia Waisraeli wote nao walilia kwa uchungu mwingi.

40 Kesho yake, waliamka alfajiri na mapema wakaenda sehemu za milimani, wakisema, “Sasa tuko tayari kabisa kwenda mahali ambapo Mwenyezi-Mungu alituahidi. Tunakiri kwamba tulitenda dhambi.”

41 Lakini Mose akasema, “Sasa mbona mnavunja agizo la Mwenyezi-Mungu? Hivyo hamtafaulu!

42 Msiende huko milimani msije mkapigwa bure na adui zenu, maana, Mwenyezi-Mungu hayuko pamoja nanyi.

43 Mkiwakabili Waamaleki na Wakanaani, mtafia vitani; kwa kuwa mmeacha kumfuata Mwenyezi-Mungu, yeye hatakuwa pamoja nanyi.”

44 Hata hivyo, wao walisisitiza kwenda juu milimani, ingawa sanduku la agano la Mwenyezi-Mungu, wala Mose hakuondoka kambini.

45 Ndipo Waamaleki na Wakanaani, waliokuwa wakiishi katika nchi hiyo ya milima, wakashuka, wakawashambulia na kuwashinda. Wakawafukuza mpaka mji wa Horma.

15

1 Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,

2 “Waambie Waisraeli kwamba mtakapofika katika nchi ninayowapeni ambamo mtaishi,

3 mkanitolea mimi Mwenyezi-Mungu sadaka kutoka katika mifugo yenu, sadaka ya kuteketezwa au tambiko, ili mtu atimize nadhiri aliyoweka au kutoa sadaka ya hiari au sadaka ya wakati wa sikukuu zenu zilizowekwa, na kufanya harufu nzuri ya kunipendeza mimi Mwenyezi-Mungu,

4 basi, yule atoaye sadaka yake, atamletea pia Mwenyezi-Mungu sadaka ya nafaka ya kilo moja ya unga laini uliokandwa na kuchanganywa na lita moja ya mafuta;

5 pamoja na divai ya sadaka ya kinywaji, lita moja, vitu hivyo vitaandamana na kila mnyama wa tambiko ya kuteketezwa: Kondoo au mbuzi.

6 Wakati wa kutoa sadaka ya kondoo dume, kilo mbili za unga uliokandwa na lita moja u nusu ya mafuta vitatolewa kama sadaka ya nafaka,

7 pamoja na sadaka ya kinywaji ya lita moja u nusu ya divai, na kufanya harufu nzuri ya sadaka haya kumpendeza Mwenyezi-Mungu.

8 Wakati mtakapomtolea Mwenyezi-Mungu fahali kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa au tambiko ili kutimiza nadhiri au kwa ajili ya sadaka za amani,

9 mtu atamtoa kama sadaka pamoja na sadaka ya nafaka ya unga wa kilo tatu ulio mzuri na lita 2 za mafuta,

10 pamoja na sadaka ya kinywaji ya lita 2 za divai, na kufanya harufu nzuri ya sadaka ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu.

11 “Hivyo ndivyo vitu vitakavyotolewa pamoja na kila fahali, kondoo dume au mbuzi.

12 Hesabu ya vitu hivyo itaongezwa kulingana na hesabu ya wanyama watakaotolewa.

13 Kila mwananchi Mwisraeli atafuata maagizo hayo wakati anapotoa tambiko, harufu impendezayo Mwenyezi-Mungu.

14 Na kama kuna mgeni anayeishi pamoja nanyi kwa muda au daima, akitaka kutoa sadaka yake kwa kuiteketeza, harufu impendezayo Mwenyezi-Mungu, mtu huyo atafanya kama mnavyofanya nyinyi.

15 Katika vizazi vyote vijavyo, kanuni zilezile mtakazofuata nyinyi ndizo atakazofuata mgeni yeyote atakayeishi pamoja nanyi; mbele ya Mwenyezi-Mungu mtakuwa sawa;

16 nyinyi na yeye mtakuwa chini ya sheria ileile moja na maagizo yaleyale.”

17 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose, “Waeleze

18 Waisraeli kwamba wakati watakapoingia katika nchi ninayowapeleka

19 kila mtakapokula mazao ya nchi hiyo, mtatenga kiasi fulani na kunipa mimi Mwenyezi-Mungu.

20 Mtakapooka mikate, mkate wa kwanza wa mazao ya kwanza ya nafaka yenu utatolewa kama sadaka kutoka mahali pa kupuria nafaka.

21 Mtanitolea mimi Mwenyezi-Mungu sadaka hii maalumu katika vizazi vyenu vyote vijavyo.

22 “Lakini ikiwa mtakosa kuzifuata amri zote ambazo mimi Mwenyezi-Mungu nimewapa kwa njia ya Mose,

23 kama siku zijazo watu hawatafuata yote ambayo mimi Mwenyezi-Mungu nimemwamuru Mose,

24 basi, ikiwa kosa hilo limefanyika bila kukusudia, bila jumuiya kujua, jumuiya yote itatoa fahali mmoja mchanga kuwa sadaka ya kuteketezwa, harufu nzuri ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu, pamoja na sadaka yake ya nafaka na ya divai kufuatana na maagizo yake. Kadhalika watu watatoa beberu mmoja kuwa sadaka ya kuondoa dhambi.

25 Kuhani atafanya upatanisho kwa ajili ya jumuiya yote ya Waisraeli, nao watasamehewa kwa sababu si kosa lililokusudiwa, na wameleta sadaka yao, sadaka ya kuteketeza kwa Mwenyezi-Mungu kama tambiko na sadaka ya kuondoa dhambi kwa ajili ya kosa lao.

26 Jumuiya yote ya Waisraeli, pamoja na wageni wanaoishi nao, watasamehewa kwa sababu wote walihusika na kosa hilo.

27 “Mtu mmoja akifanya dhambi bila kujua, atatoa mbuzi jike wa mwaka mmoja kuwa sadaka ya kuondoa dhambi.

28 Kuhani atafanya upatanisho mbele ya Mwenyezi-Mungu, kwa ajili ya huyo mtu aliyekosa bila kujua, naye atasamehewa.

29 Mtafuata sheria moja kila mtu atakayekosea bila kukusudia, awe ni mwananchi Mwisraeli au ni mgeni anayeishi pamoja nanyi.

30 “Lakini mtu yeyote atakayekosa kwa makusudi, awe mwananchi au mgeni, atakuwa anamdhihaki Mwenyezi-Mungu, na ni lazima akatiliwe mbali miongoni mwa watu wake.

31 Maana amekataa yale aliyosema Mwenyezi-Mungu na kuvunja mojawapo ya amri zake. Mtu huyo atakatiliwa mbali kabisa; na lawama ya kifo chake itakuwa juu yake mwenyewe.”

32 Siku moja, wakati Waisraeli walipokuwa jangwani, walimwona mtu mmoja akiokota kuni siku ya Sabato.

33 Basi, mtu huyo akapelekwa mbele ya Mose, Aroni na jumuiya yote.

34 Wao wakamweka kifungoni kwa sababu haikuwa bado imesemwa wazi namna ya kumfanya mtu wa namna hiyo.

35 Ndipo Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, “Mtu huyo lazima auawe; jumuiya yote itampiga mawe nje ya kambi.”

36 Basi, watu wakamtoa nje ya kambi, wakampiga mawe mpaka akafa, kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.

37 Kisha Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose:

38 “Waambie watu wa Israeli, uwaagize wajifanyie vishada katika ncha za mavazi yao, na kutia nyuzi za buluu juu ya kila kishada. Waambie wafanye hivyo katika vizazi vyao vyote vijavyo.

39 Vishada hivyo vitakuwa kumbukumbu kwenu. Kila mtakapoviona, mtazikumbuka amri zangu zote na kuzifuata, ili msije mkafuata matakwa yenu na yale mnayoyaona kwa macho yenu wenyewe.

40 Vishada hivyo vitawakumbusha amri zangu zote na mtazifuata zote kikamilifu, nanyi mtakuwa watakatifu wangu.

41 Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, niliyewatoa nchini Misri ili niwe Mungu wenu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.”

16

1 Baadaye Kora mwana wa Ishari, mwana wa Kohathi, mwana wa Lawi, akatwaa watu pamoja na watu watatu wa ukoo wa Reubeni: Dathani na Abiramu, wana wa Eliabu, na Oni, mwana wa Pelethi,

2 hao wote waliungwa mkono na viongozi mashuhuri 250 waliochaguliwa na jumuiya yote, wakamwasi Mose.

3 Walikusanyika mbele ya Mose na Aroni, wakawaambia, “Nyinyi mmepita kikomo! Jumuiya yote ni takatifu na kila mtu katika jumuiya hii ni mtakatifu, na Mwenyezi-Mungu yu pamoja nasi sote. Mbona sasa nyinyi mnajifanya wakuu wa jumuiya ya Mwenyezi-Mungu?”

4 Mose aliposikia hayo, alijitupa chini kifudifudi.

5 Kisha akamwambia Kora na wafuasi wake, “Kesho asubuhi, Mwenyezi-Mungu ataonesha ni nani aliye wake na ni nani aliye mtakatifu, naye atakayemchagua, atamwezesha kukaribia madhabahuni.

6 Basi, fanyeni hivi: Asubuhi, wewe pamoja na wafuasi wako, mtachukua vyetezo,

7 mweke makaa ya moto ndani na kutia ubani juu yake, kisha mtavipeleka mbele ya Mwenyezi-Mungu. Halafu tutaona ni nani aliyechaguliwa na Mwenyezi-Mungu. Nyinyi Walawi mmepita kikomo!”

8 Mose akaendelea kumwambia Kora, “Sikilizeni, enyi Walawi!

9 Je, mnaona ni jambo dogo kwenu kwamba Mungu wa Israeli amewateua nyinyi miongoni mwa jumuiya ya Israeli, ili muweze kumkaribia, mhudumie katika hema la Mwenyezi-Mungu na kuihudumia na kuitumikia jamii yote?

10 Amewatunukia heshima ya kuwa karibu naye, nyinyi pamoja na Walawi wenzenu wote. Sasa mnataka kunyakua hata ukuhani?

11 Kwa hiyo wewe na kundi lako mnamshambulia Mwenyezi-Mungu. Nyinyi mnamnungunikia Aroni, lakini ukweli ni kwamba mnanungunika dhidi ya Mungu.”

12 Mose alituma ujumbe kwa Dathani na Abiramu wana wa Eliabu ili waitwe, lakini wao wakasema, “Hatutakuja!

13 Je, ni jambo dogo kwamba umetutoa Misri, nchi inayotiririka maziwa na asali, ili uje kutuua humu jangwani? Tena, unajifanya mkuu wetu!

14 Zaidi ya hayo, hukutuleta kwenye nchi inayotiririka maziwa na asali, wala kutupatia urithi wa mashamba na mashamba ya mizabibu. Unafikiri utawafanya hawa watu kuwa vipofu? Hatutakuja!”

15 Mose alikasirika mno, akamwambia Mwenyezi-Mungu “Usizikubali sadaka za watu hawa. Mimi sijachukua punda wa mtu yeyote, wala sijamdhuru mtu!”

16 Mose akamwambia Kora, “Kesho usikose kuja pamoja na wafuasi wako mbele ya Mwenyezi-Mungu. Aroni pia atakuwapo.

17 Kila mmoja wenu achukue chetezo chake, na kutia ubani, kisha atakipeleka mbele ya Mwenyezi-Mungu; kwa jumla vitakuwa vyetezo 250; wewe pia na Aroni, kila mmoja atakuwa na chetezo chake.”

18 Basi, kila mmoja wao akachukua chetezo chake, akatia makaa ya moto na ubani, kisha wakaenda na kusimama mlangoni mwa hema la mkutano, pamoja na Mose na Aroni.

19 Naye Kora akawakusanya watu wote pamoja, wakasimama mbele ya Mose na Aroni ambao walikuwa mlangoni mwa hema la mkutano. Ndipo utukufu wa Mwenyezi-Mungu ukawatokea watu wote!

20 Hapo Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose na Aroni,

21 “Jitengeni na watu hawa, niwaangamize sasa hivi.”

22 Lakini Mose na Aroni wakajitupa chini kifudifudi na kusema, “Ee Mwenyezi-Mungu uliye asili ya uhai wa binadamu wote. Je, mtu mmoja akikukosea, utaikasirikia jumuiya nzima?”

23 Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,

24 “Waambie watu waondoke karibu na makao ya hema ya Kora, Dathani na Abiramu.”

25 Basi, Mose akaenda kwa Dathani na Abiramu, akifuatwa na wazee wa Israeli.

26 Alipofika, akawaambia watu, “Tafadhalini ondokeni kwenye hema za watu hawa waovu na msiguse kitu chao chochote, msije mkaangamizwa pamoja nao kwa sababu ya dhambi zao zote.”

27 Watu wakaondoka kwenye makao ya Kora, Dathani na Abiramu. Dathani na Abiramu wakatoka mahemani mwao na kusimama mlangoni wakiandamana na wake zao na watoto wao wote hata wale wanaonyonya.

28 Hapo Mose akawaambia watu, “Hivi ndivyo mtakavyotambua kuwa Mwenyezi-Mungu ndiye aliyenituma kufanya mambo haya yote, wala siyo kwa matakwa yangu mwenyewe.

29 Watu hawa wakifa kifo cha kawaida, au wakipatwa na maafa kama watu wengine, basi jueni kuwa Mwenyezi-Mungu hakunituma.

30 Lakini Mwenyezi-Mungu akifanya jambo ambalo halijapata kutendeka, ardhi ikafunuka na kuwameza watu hawa pamoja na kila kitu chao, wakaenda kuzimu wakiwa hai, basi mtajua kuwa watu hawa wamemdharau Mwenyezi-Mungu.”

31 Mara tu alipomaliza kusema maneno hayo yote, ardhi chini ya Dathani na Abiramu ikafunuka

32 kuwameza watu hao, jamaa zao, pamoja na wafuasi wote wa Kora na mali zao zote.

33 Basi, wao, pamoja na vyote vilivyokuwa vyao wakashuka kuzimu hali wangali hai. Ardhi ikawafunika, wote wakatoweka.

34 Waisraeli wote wengine waliokuwa karibu waliposikia vilio vyao walikimbia wakisema, “Tukimbie, ardhi isije ikatumeza na sisi pia.”

35 Kisha Mwenyezi-Mungu akapeleka moto ukawateketeza wale watu 250 waliokwenda kufukiza ubani.

36 Baada ya hayo, Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,

37 “Mwambie Eleazari mwana wa kuhani Aroni avitoe hivyo vyetezo penye moto, akautapanye mbali moto uliomo ndani, maana vyetezo hivyo ni vitakatifu.

38 Vimekuwa vitakatifu kwa sababu watu hawa walivileta madhabahuni pa Mwenyezi-Mungu. Basi, vichukue vyetezo vya watu hao waliouawa kwa sababu ya dhambi zao, vifuliwe kuwa vyembamba ili viwe kifuniko cha madhabahu. Hili litakuwa onyo kwa Waisraeli wote.”

39 Basi, kuhani Eleazari alivichukua vyetezo hivyo vya shaba ambavyo vililetwa mbele ya Mwenyezi-Mungu na wale watu walioteketezwa vikafuliwa kuwa kifuniko cha madhabahu.

40 Hili lilikuwa onyo kwa Waisraeli kwamba mtu yeyote ambaye si kuhani, yaani asiye wa ukoo wa Aroni asiende madhabahuni kumfukizia Mwenyezi-Mungu ubani. La sivyo ataangamizwa kama Kora na wafuasi wake. Haya yote yalitendeka kama Mwenyezi-Mungu alivyomwambia Eleazari kwa njia ya Mose.

41 Kesho yake, Waisraeli wote walimnungunikia Mose na Aroni wakisema, “Mmewaua watu wa Mwenyezi-Mungu.”

42 Walipokusanyika mbele ya Mose na Aroni ili kutoa malalamiko yao, waligeuka kuelekea hema la mkutano, wakaona kuwa wingu limeifunika hema na utukufu wa Mwenyezi-Mungu ulikuwa umetokea hapo.

43 Mose na Aroni walikwenda, wakasimama mbele ya hema la mkutano,

44 na Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,

45 “Jitenge na watu hawa, niwaangamize mara moja!” Lakini wao wakajitupa chini kifudifudi.

46 Mose akamwambia Aroni, “Chukua chetezo chako, kitie moto na kukiweka kando ya madhabahu, kisha ukitie ubani halafu uende nacho haraka kwa watu na kuwafanyia upatanisho. Fanya haraka! Ghadhabu ya Mwenyezi-Mungu imekwisha wafikia na pigo limeanza kuwashambulia.”

47 Basi, Aroni akafanya kama alivyoambiwa na Mose. Alichukua chetezo chake na kukimbia hadi katikati ya watu waliokuwa wamekusanyika pamoja. Alipoona kwamba pigo limekwisha anza, alitia ubani katika chetezo na kuwafanyia watu upatanisho.

48 Alipofanya hivyo, pigo hilo lilikoma, naye akabaki katikati ya waliokufa na walio hai.

49 Idadi ya watu waliokufa kwa pigo ilikuwa 14,700, bila kuhesabu wale waliokufa kutokana na uasi wa Kora.

50 Pigo lilipokoma, Aroni alirudi kwa Mose mlangoni mwa hema la mkutano.

17

1 Kisha Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,

2 “Waambie Waisraeli wakuletee fimbo kumi na mbili, kila kiongozi wa kabila fimbo moja. Liandike jina la kila mmoja wao kwenye fimbo yake,

3 na jina la Aroni liandike juu ya fimbo inayowakilisha kabila la Lawi. Patakuwa na fimbo moja kwa kila kiongozi wa kabila.

4 Zichukue fimbo hizo katika hema la mkutano na kuziweka mbele ya sanduku la agano, mahali ambapo mimi hukutana nawe.

5 Fimbo ya mtu nitakayemchagua itachipua. Kwa njia hii nitayakomesha manunguniko ya Waisraeli juu yenu.”

6 Mose akaongea na watu wa Israeli. Viongozi wao wote wakampa kila mmoja fimbo yake kulingana na kabila lake jumla zikawa fimbo kumi na mbili. Fimbo ya Aroni iliwekwa pamoja na fimbo hizo.

7 Mose akaziweka fimbo hizo zote mbele ya Mwenyezi-Mungu katika hema la mkutano.

8 Kesho yake asubuhi, Mose alikwenda katika hema la mkutano. Humo, aliikuta fimbo ya Aroni wa kabila la Lawi, imechipua na kutoa vichipukizi vilivyochanua maua na kuzaa matunda mabivu ya mlozi.

9 Kisha Mose akazitoa fimbo zote hapo mbele ya Mwenyezi-Mungu, akawaonesha Waisraeli wote, na kila kiongozi akachukua fimbo yake.

10 Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, “Irudishe fimbo ya Aroni mbele ya sanduku la agano. Hiyo itatunzwa mahali hapo, na ni onyo kwa waasi hao kwamba wasipoacha kuninungunikia, watakufa.”

11 Mose akafanya kama alivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu.

12 Waisraeli wakamwambia Mose, “Angalia sasa! Tunaangamia! Tumekwisha! Sote tumekwisha.

13 Kila mtu atakayekaribia, hema la Mwenyezi-Mungu atakufa. Je, tutaangamia sote?”

18

1 Basi, Mwenyezi-Mungu akamwambia Aroni, “Lawama zote kuhusu huduma ya hema takatifu, zitakuwa juu yako, wanao na ukoo wako; kadhalika makosa yanayoambatana na ukuhani wako wewe mwenyewe na wanao mtahusika.

2 Wewe, wanao na wazawa wako wote mtahudumu kama makuhani; jamaa zako wengine wa kabila lako watafanya kazi pamoja nawe mbele ya hema la maamuzi.

3 Wao watafanya kazi utakazowapa na kutimiza wajibu wao kuhusu hema. Lakini hawana ruhusa kuvigusa vyombo vya hema, wala kuikaribia madhabahu, wasije wakafa, nawe pia ukafa.

4 Wao watajiunga nawe kazini na kutimiza wajibu wao kikamilifu kuhusu huduma zote za hema, na wala pasiwe na mtu mwingine atakayekukaribia humo.

5 Nyinyi mtafanya huduma za mahali patakatifu na madhabahu, ili ghadhabu yangu isije ikawatokea tena Waisraeli.

6 Ni mimi niliyewachagua ndugu zenu Walawi miongoni mwa Waisraeli kama toleo kwenu. Wao wametengwa kwa ajili yangu mimi Mwenyezi-Mungu, ili watoe huduma katika hema la mkutano.

7 Lakini wewe peke yako na wanao mtatoa huduma zote za kikuhani kwa ajili ya madhabahu na vyote vilivyomo katika mahali patakatifu. Huo ni wajibu wenu, kwa sababu ninawapeni kipawa cha ukuhani. Mtu yeyote asiyestahili atakayevikaribia vyombo vya hema, atauawa.”

8 Mwenyezi-Mungu akamwambia Aroni, “Ninakukabidhi matoleo waliyonipa Waisraeli, vitu vyote vitakatifu walivyonipa: Vitu vyote vilivyowekwa wakfu na Waisraeli. Ninakupa vitu vyote wewe na wazawa wako kuwa fungu lenu, na hiyo ni haki yenu milele.

9 Kati ya vitu vitakatifu kabisa ambavyo haviteketezwi motoni, hivi vitakuwa vyenu: Sadaka za nafaka, sadaka za kuondoa dhambi na sadaka za hatia. Kila kitu watu watakachonitolea kama tambiko takatifu kitakuwa chako na wanao.

10 Mtavila vitu hivyo kama vitu vitakatifu kabisa, na ni wanaume tu ndio watakaovila; vitu hivyo ni vitakatifu kwenu.

11 “Pia, vitu vingine vyote watakavyonitolea Waisraeli kama sadaka za kutikisa, vitakuwa vyako. Ninakupa wewe, wanao na binti zako kuwa haki yenu milele. Mtu yeyote katika jamaa yako asiye najisi anaweza kula vitu hivyo.

12 “Ninakupa vitu vyote vizuri vinavyotokana na malimbuko ambayo Waisraeli hunitolea: Mafuta safi, divai na nafaka.

13 Mazao yote ya kwanza ya matunda mabivu ya mashamba yao ambayo wataniletea mimi, yatakuwa yako. Kila mtu asiye najisi katika jamaa yako anaweza kula.

14 Kila kitu kilichowekwa wakfu nchini Israeli kitakuwa chenu.

15 “Kila mzaliwa wa kwanza ambaye Waisraeli watanitolea, akiwa mzaliwa wa kwanza wa binadamu, au wa mnyama, atakuwa wako. Walakini huna budi kuwakomboa wazaliwa wa kwanza wote wa binadamu, na kila mzaliwa wa kwanza wa mnyama aliye najisi ni lazima akombolewe.

16 Wazaliwa hao wa kwanza watakombolewa wakiwa wenye umri wa mwezi mmoja kwa kulipiwa fedha shekeli tano, kulingana na vipimo vya hema takatifu.

17 Lakini wazaliwa wa kwanza wa ng'ombe, kondoo au mbuzi wasikombolewe; hao ni watakatifu. Damu yao utainyunyizia madhabahu na mafuta yao utayateketeza kuwa sadaka ya kuteketezwa ambayo ni harufu nzuri inipendezayo mimi Mwenyezi-Mungu.

18 Nyama yao unaweza kuila, kama vile kidari na mguu wa nyuma wa kulia vinavyotolewa kama sadaka ya kutikisa.

19 “Ninakupa wewe, wanao na binti zako, vitu vyote ambavyo watu wa Israeli hunitolea; hivyo ni haki yenu daima. Hili ni agano la milele mbele yangu ambalo ni kwa ajili yako na wazawa wako.”

20 Mwenyezi-Mungu akamwambia Aroni, “Wewe hutakuwa na urithi wowote katika nchi yao, wala kuwa na fungu lako miongoni mwao; mimi ndimi fungu lako na urithi wako kati ya Waisraeli.”

21 “Kuhusu Walawi, hao nimewapa zaka zote ambazo Waisraeli hunitolea kuwa urithi wao. Haya yatakuwa malipo yao kwa huduma wanayotoa katika kulitunza hema langu la mkutano.

22 Na tangu sasa, watu wengine wa Israeli wasilikaribie hema la mkutano wasije wakatenda dhambi na kujiletea kifo.

23 Lakini Walawi peke yao ndio watakaohudumu katika hema la mkutano; na kuwajibika kikamilifu juu yake. Hili ni sharti la kudumu katika vizazi vyenu vyote. Walawi hawatakuwa na mali ya kurithi nchini Israeli,

24 kwa sababu zaka wanazonitolea Waisraeli nimewapa kuwa urithi wao. Ndio maana nimesema kwamba wao hawatakuwa na urithi kati ya Waisraeli.”

25 Kisha, Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

26 “Tena utawaambia Walawi maagizo yafuatayo: Wakati mtakapopokea zaka ambayo Mwenyezi-Mungu amewapa kutoka kwa Waisraeli iwe urithi wenu, mtanitolea mimi Mwenyezi-Mungu sehemu moja ya kumi ya zaka hiyo.

27 Sadaka hii yenu itakubaliwa kuwa kama malimbuko ya nafaka au kama zabibu anazonitolea mkulima.

28 Basi, ndivyo mtakavyonitolea mimi Mwenyezi-Mungu sadaka za zaka mtakazopokea kutoka kwa Waisraeli. Zaka hiyo mtakayonitolea mimi Mwenyezi-Mungu mtampa kuhani Aroni.

29 Kutokana na matoleo yote mtakayopokea, mtamtolea Mwenyezi-Mungu zaka ya sehemu iliyo bora kuliko zote na takatifu.

30 Kwa hiyo utawaambia: Mkishanitolea sehemu bora kuliko zote, sehemu itakayobakia itakuwa yenu, kama ilivyo kwa mkulima ambaye huchukua kinachobakia baada ya kutoa sadaka zake za mazao ya kwanza ya nafaka na zabibu.

31 Nanyi mtakula kilichotolewa mkiwa mahali popote pale pamoja na jamaa zenu maana ni ujira wenu kwa sababu ya huduma yenu katika hema la mkutano.

32 Hamtakuwa na hatia yoyote mkila vitu hivyo, iwapo kama mmemtolea Mwenyezi-Mungu sehemu bora kuliko zote, nanyi hamtavikufuru vitu vitakatifu vya Waisraeli na kufa.”

19

1 Mwenyezi-Mungu aliendelea kuwaambia Mose na Aroni,

2 “Haya ni masharti ya sheria ambayo mimi Mwenyezi-Mungu ninatoa. Waambieni Waisraeli wawaletee ng'ombe jike mwekundu asiye na dosari wala kasoro yoyote, na ambaye hajapata kufungwa nira.

3 Nyinyi mtampa kuhani Eleazari ng'ombe huyo. Atatolewa nje ya kambi na kuchinjwa mbele ya kuhani huyo.

4 “Kisha kuhani Eleazari atachukua kiasi cha damu na kuinyunyiza kwa kidole mara saba, kuelekea upande wa mbele wa hema la mkutano.

5 Ngombe huyo mzima atateketezwa kwa moto mbele ya kuhani. Kila kitu chake kitateketezwa; ngozi, nyama, damu na utumbo wake.

6 Halafu kuhani atachukua mti wa mwerezi, husopo na sufu nyekundu na kuvitia katika moto huo.

7 Baada ya hayo, kuhani atazifua nguo zake na kuoga mwili kwa maji, halafu anaweza kuingia kambini; atakuwa najisi hadi jioni.

8 Mtu atakayemteketeza ng'ombe huyo pia atazifua nguo zake kwa maji na kuoga mwili kwa maji, lakini naye pia atakuwa najisi hadi jioni.

9 Mtu aliye safi atayazoa majivu ya ng'ombe huyo na kuyapeleka mahali safi nje ya kambi. Yatahifadhiwa na kutumiwa na jumuiya nzima ya Israeli kutengeneza maji ya kuondoa najisi, ili kuondoa dhambi.

10 Mtu atakayeyazoa majivu ya ng'ombe huyo lazima azifue nguo zake, lakini atakuwa najisi hadi jioni. Sharti hili ni la kudumu, na litawahusu Waisraeli na watu wengine watakaoishi pamoja nao.

11 “Mtu akigusa maiti ya mtu yeyote, atakuwa najisi kwa siku saba.

12 Siku ya tatu na ya saba mtu huyo atajiosha kwa yale maji ya utakaso, naye atakuwa safi. Lakini akiacha kujitakasa katika siku ya tatu na ya saba, mtu huyo atabaki kuwa najisi.

13 Agusaye maiti, yaani mwili wa mtu aliyekufa, asipojitakasa, analitia najisi hema la Mwenyezi-Mungu, naye atatengwa na wana wa Israeli. Mtu huyo atabaki najisi kwa sababu hakunyunyiziwa yale maji ya utakaso.

14 “Na hii ndiyo sheria ya kufuatwa kama mtu akifia hemani: Kila mtu atakayeingia ndani ya hema hilo, au aliye ndani ya hema hilo, atakuwa najisi kwa siku saba.

15 Kila chombo kilicho wazi ambacho hakina kifuniko juu yake kitakuwa najisi.

16 Mtu yeyote akigusa mwili wa mtu aliyeuawa au aliyekufa kifo cha kawaida nje ya nyumba, au akigusa mfupa wa mtu au kaburi, atakuwa najisi kwa siku saba.

17 “Kwa ajili ya wale waliojitia najisi watachukua majivu ya sadaka ya kuondoa dhambi iliyoteketezwa, majivu hayo yatachanganywa na maji ya mtoni katika chungu.

18 Mtu aliye safi atachukua husopo, halafu ataichovya katika maji hayo, kisha atainyunyizia hema, vyombo vyote vilivyomo ndani ya hema na watu waliokuwamo ndani. Atamnyunyizia pia mtu aliyegusa mfupa wa mtu, au mwili wa mtu aliyeuawa au aliyekufa kifo cha kawaida, au aliyegusa kaburi.

19 Katika siku ya tatu na ya saba, mtu aliye safi atamnyunyizia mtu aliye najisi maji hayo; hivyo katika siku ya saba, atamtakasa mtu huyo aliye najisi, naye atazifua nguo zake na kuoga, na jioni atakuwa safi.

20 “Lakini mtu akiwa najisi asipojitakasa, mtu huyo atakataliwa mbali na jumuiya, kwa kuwa analitia najisi hema la Mwenyezi-Mungu. Kwa vile hakunyunyiziwa maji ya utakaso, yu unajisi.

21 Watu watalishika sharti hili daima. Mtu atakayenyunyiza maji ya kutakasia ataosha nguo zake; naye anayegusa maji hayo ya najisi atakuwa najisi hadi jioni.

22 Chochote atakachogusa mtu najisi kitakuwa najisi, na yeyote atakayekigusa kitu hicho atakuwa najisi mpaka jioni.”

20

1 Jumuiya nzima ya Waisraeli ilifika katika jangwa la Sinai mnamo mwezi wa kwanza, wakapiga kambi yao huko Kadeshi. Wakiwa huko, Miriamu alifariki, akazikwa.

2 Mahali hapo walipopiga kambi hapakuwa na maji. Kwa hiyo watu jumuiya yote, wakakusanyika kinyume cha Mose na Aroni.

3 Waliwalalamikia wote wakisema, “Afadhali tungekufa pamoja na ndugu zetu mbele ya hema la Mwenyezi-Mungu!

4 Kwa nini mlituleta sisi jumuiya ya Mwenyezi-Mungu huku jangwani? Je, mlituleta ili tufe pamoja na mifugo yetu?

5 Na, kwa nini mlitutoa Misri na kutuleta mahali hapa pabaya hivi? Hapa si mahali pa nafaka, tini, zabibu wala makomamanga. Hata maji ya kunywa hakuna!”

6 Hapo, Mose na Aroni waliondoka kwenye umati wa watu, wakaenda kusimama kwenye mlango wa hema la mkutano, wakasujudu. Basi, utukufu wa Mwenyezi-Mungu ukawatokea,

7 naye Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,

8 “Twaa ile fimbo yako, kisha wewe na Aroni ndugu yako, muikusanye jumuiya yote ya watu. Halafu, mbele ya macho yao, uuambie mwamba ulio mbele ya macho yao utoe maji yake. Naam, utaufanya mwamba utoe maji, ili jumuiya nzima ya watu na mifugo yao waweze kunywa.”

9 Mose akaenda kuichukua ile fimbo mbele ya Mwenyezi-Mungu kama alivyoamriwa.

10 Kisha Mose na Aroni wakaikusanya jumuiya yote ya watu mbele ya mwamba, naye Mose akawaambia, “Sikilizeni sasa, enyi waasi: Je, tuwatoleeni maji kutoka mwamba huu?”

11 Kisha Mose akainua mkono wake, akaupiga ule mwamba mara mbili kwa fimbo yake. Maji yakabubujika kwa wingi, watu wakanywa pamoja na mifugo yao.

12 Lakini Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose na Aroni, “Kwa kuwa nyinyi hamkuniamini mimi, wala kunistahi mbele ya macho ya Waisraeli, basi kwa sababu hiyo hamtaiingiza jumuiya hii katika ile nchi niliyowapa.”

13 Hayo ni maji ya Meriba, mahali ambapo Waisraeli walimnungunikia Mwenyezi-Mungu, naye alijionesha kwa utakatifu kati yao.

14 Mose alipeleka wajumbe kutoka Kadeshi kwa mfalme wa Edomu akamwambia: “Ndugu yako, Israeli, asema hivi: Wewe wazijua taabu zote tulizozipata.

15 Jinsi babu zetu walivyokwenda Misri, ambako tuliishi kwa muda mrefu na jinsi Wamisri walivyowatesa babu zetu, wakatutesa na sisi pia.

16 Tulimlilia Mwenyezi-Mungu, naye akakisikia kilio chetu, akatuletea malaika aliyetuondoa Misri. Sasa tuko hapa Kadeshi, mji unaopakana na nchi yako.

17 Tafadhali uturuhusu tupite nchini mwako. Hatutakanyaga mashamba yenu, wala yale ya mizabibu; wala hatutakunywa maji ya visima vyenu. Tutaifuata barabara kuu ya mfalme na kwenda moja kwa moja bila kugeuka kulia au kushoto, mpaka tutakapotoka katika nchi yako.”

18 Lakini mfalme wa Edomu akamjibu, “La! Hutapita katika nchi yangu, kama ukipita nitatoka na kukushambulia kwa upanga.”

19 Waisraeli wakamwambia, “Sisi tutafuata njia kuu; kama sisi na mifugo yetu tukinywa maji yenu, tutalipa. Tunachoomba tafadhali turuhusu tu, tupite kwa miguu wala hatutaki neno lolote lingine.”

20 Lakini mfalme wa Edomu akasisitiza: “Hatutawaruhusu.” Mara, Waedomu wenye nguvu wakatoka kupigana nao.

21 Basi, Waedomu wakakataa kuwapa ruhusa Waisraeli kupita katika mipaka yao. Waisraeli wakageuka na kushika njia nyingine.

22 Waisraeli wote walisafiri kutoka Kadeshi, wakafika kwenye Mlima Hori.

23 Basi, Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose na Aroni huko kwenye Mlima Hori, mpakani mwa nchi ya Edomu,

24 “Aroni atakufa; hataingia katika nchi ambayo nimewapa watu wa Israeli kwa sababu nyinyi wawili mliiasi amri yangu kule Meriba

25 Mchukue Aroni na Eleazari mwanawe, uwalete juu ya Mlima Hori.

26 Kisha, mvue Aroni mavazi yake rasmi, umvalishe mwanawe Eleazari. Aroni atakufa akiwa huko mlimani.”

27 Mose alifanya kama alivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu. Wote watatu walipanda mlimani mbele ya jumuiya yote ya watu.

28 Kisha Mose alimvua Aroni mavazi yake rasmi, akamvalisha mwanawe, Eleazari. Naye Aroni akafa palepale mlimani. Kisha Mose na Eleazari wakateremka chini.

29 Jumuiya yote ya watu ilipopata habari kwamba Aroni amefariki, ikafanya matanga ya siku thelathini.

21

1 Mfalme mmoja Mkanaani wa Aradi aliyeishi huko Negebu alipopata habari kwamba Waisraeli walikuwa wanakuja kwa njia ya Atharimu, alikwenda kuwashambulia, akawateka baadhi yao.

2 Hapo, Waisraeli wakamwekea Mwenyezi-Mungu nadhiri wakisema: “Kama utawatia watu hawa mikononi mwetu, basi tutaiangamiza kabisa miji yao.”

3 Mwenyezi-Mungu akalisikia ombi lao, akawapa ushindi juu ya Wakanaani. Waisraeli wakawaangamiza kabisa Wakanaani pamoja na miji yao. Kwa hiyo mahali hapo pakaitwa Horma.

4 Waisraeli walifunga safari kutoka Mlima Hori wakapitia njia inayoelekea bahari ya Shamu ili waizunguke nchi ya Edomu. Lakini njiani watu walikufa moyo.

5 Basi, wakaanza kumnungunikia Mungu na Mose, wakisema, “Kwa nini mmetutoa Misri tuje tukafie humu jangwani? Humu hamna chakula wala maji; nasi tumechoshwa na chakula hiki duni.”

6 Hapo Mwenyezi-Mungu akapeleka nyoka wenye sumu miongoni mwa watu, wakawauma hata Waisraeli wengi wakafa.

7 Basi, watu wakamwendea Mose, wakamwambia, “Tumetenda dhambi kwa kumnungunikia Mwenyezi-Mungu na wewe pia. Mwombe Mwenyezi-Mungu atuondolee nyoka hawa.” Kwa hiyo, Mose akawaombea watu.

8 Ndipo Naye Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, “Tengeneza nyoka wa shaba, umtundike juu ya mlingoti. Mtu yeyote atakayeumwa na nyoka, akimtazama nyoka huyo wa shaba, atapona.”

9 Basi, Mose akatengeneza nyoka wa shaba, akamtundika juu ya mlingoti. Kila mtu aliyeumwa na nyoka alipomtazama nyoka huyo wa shaba, alipona.

10 Waisraeli waliendelea na safari yao, wakapiga kambi huko Obothi.

11 Kutoka huko walisafiri mpaka Iye-abarimu, katika jangwa upande wa mashariki, mwa Moabu.

12 Kutoka huko walisafiri wakapiga kambi yao katika bonde la Zeredi.

13 Kutoka huko walisafiri, wakapiga kambi kaskazini ya mto Arnoni, ambao hutiririka kutoka katika nchi ya Waamori na kupitia jangwani. Mto Arnoni ulikuwa mpaka kati ya Wamoabu na Waamori.

14 Kwa sababu hiyo, imeandikwa katika kitabu cha vita vya Mwenyezi-Mungu: “Mji wa Wahebu nchini Sufa, na mabonde ya Arnoni,

15 na mteremko wa mabonde unaofika hadi mji wa Ari, na kuelekea mpakani mwa Moabu!”

16 Kutoka huko Waisraeli walisafiri mpaka Beeri; yaani kisima ambapo Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose, “Wakusanyeni watu pamoja, nami nitawapa maji.”

17 Hapo Waisraeli waliimba wimbo huu: “Bubujika maji ee kisima! – Kiimbieni!

18 Kisima kilichochimbwa na wakuu kilichochimbwa sana na wenye cheo, kwa fimbo zao za enzi na bakora.” Kutoka jangwani walisafiri mpaka Matana,

19 kutoka Matana mpaka Nahalieli, kutoka Nahalieli mpaka Bamothi,

20 na kutoka Bamothi mpaka kwenye bonde linaloingia nchi ya Moabu, kwenye kilele cha Mlima Pisga, kielekeacho chini jangwani.

21 Waisraeli walimpelekea mfalme Sihoni wa Waamori, ujumbe huu:

22 “Turuhusu tupite katika nchi yako; hatutakwenda pembeni na kuingia mashambani au katika mashamba ya mizabibu, wala hatutakunywa maji ya visima vyenu; tutapita moja kwa moja katika barabara kuu ya mfalme mpaka tumeondoka nchini mwako.”

23 Lakini Sihoni hakuwaruhusu watu wa Israeli wapite katika nchi yake. Aliwakusanya watu wake, akaenda Yahasa Jangwani kuwashambulia Waisraeli.

24 Lakini Waisraeli walimuua, wakaitwaa nchi yake tangu mto Arnoni hadi mto Yaboki, yaani hadi mpaka wa nchi ya Waamoni ambao ulikuwa unalindwa sana.

25 Waisraeli waliiteka miji hii yote nao wakaishi katika miji ya Waamori katika Heshboni na vitongoji vyake.

26 Heshboni ulikuwa mji wa Sihoni mfalme wa Waamori, ambaye hapo awali alikuwa amepigana na mfalme wa Moabu na kuiteka nchi yake yote mpaka mto Arnoni.

27 Ndiyo maana washairi wetu huimba: “Njoni Heshboni na kujenga. Mji wa Sihoni na ujengwe na kuimarishwa.

28 Maana moto ulitoka Heshboni, miali ya moto ilitoka mjini kwa Sihoni, uliuteketeza mji wa Ari wa Moabu, ukaiangamiza milima ya mto Arnoni.

29 Ole wenu watu wa Moabu! Mmeangamizwa, enyi watu wa mungu Kemoshi! Umewafanya watoto wenu wa kiume kuwa wakimbizi, binti zako umewaacha wachukuliwe mateka mpaka kwa Sihoni, mfalme wa Amori.

30 Lakini sasa wazawa wao wameangamizwa, kutoka Heshboni mpaka Diboni, kutoka Nashimu mpaka Nofa, karibu na Medeba.”

31 Basi, Waisraeli wakakaa katika nchi ya Waamori.

32 Kisha Mose alituma watu wapeleleze mji wa Yazeri; wakauteka pamoja na vitongoji vyake, wakawafukuza Waamori waliokaa humo.

33 Waisraeli waligeuka wakafuata njia iendayo Bashani. Mfalme Ogu wa Bashani akatoka na jeshi lake kuwashambulia huko Edrei.

34 Lakini Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, “Usimwogope, maana nimemtia mikononi mwako pamoja na watu wake wote na nchi yake yote. Utamtendea kama ulivyomtendea Sihoni, mfalme wa Waamori, aliyekuwa anakaa Heshboni.”

35 Basi, Waisraeli wakamuua Ogu, wanawe na watu wake wote, bila kumwacha hata mtu mmoja, kisha wakaitwaa nchi yake.

22

1 Waisraeli walianza safari tena, wakaenda kupiga kambi yao katika tambarare za Moabu, mashariki ya mto Yordani, kuelekea mji wa Yeriko.

2 Mfalme Balaki mwana wa Sipori, alijua mambo yote Waisraeli waliyowatendea Waamori.

3 Yeye pamoja na Wamoabu wakashikwa na hofu kubwa juu ya Waisraeli. Waliwaogopa hasa kwa sababu ya wingi wao.

4 Basi Wamoabu wakawaambia viongozi wa Midiani, “Umati huu punde si punde utaharibu kila kitu kandokando yetu kama fahali alavyo majani shambani.” Kwa hiyo, Balaki mwana wa Sipori, aliyekuwa mfalme wa Moabu wakati huo,

5 akapeleka ujumbe kwa Balaamu, mwana wa Beori, huko Pethori, karibu na mto Eufrate, nchini Amawi. Alimwambia Balaamu hivi: “Kuna taifa ambalo limetoka Misri, nalo limeenea kila mahali nchini, tena linatishia kuchukua ardhi yangu.

6 Njoo sasa uwalaani watu hawa kwa ajili yangu maana wana nguvu kuliko mimi. Labda nitaweza kuwashinda na kuwafukuza wasiingie katika nchi yangu, kwa maana najua kuwa wewe ukimbariki mtu hubarikiwa, ukimlaani mtu hulaaniwa.”

7 Basi, maofisa wa Moabu na Midiani wakachukua ada ya mwaguzi, wakaondoka kwenda kwa Balaamu. Walipowasili, walimpa Balaamu ujumbe wa Balaki.

8 Balaamu akawaambia, “Laleni huku usiku huu, nami nitawajulisheni atakayoniambia Mwenyezi-Mungu.” Basi, wazee hao wa Moabu wakakaa na Balaamu.

9 Kisha Mungu alimjia Balaamu, akamwuliza, “Ni nani hawa wanaokaa nawe?”

10 Balaamu akamjibu Mungu, “Balaki mwana wa Sipori amenipelekea ujumbe kwamba

11 kuna watu wa taifa fulani waliotoka Misri, nao wameenea kila mahali nchini. Ameniomba niende kuwalaani watu hao ili pengine afaulu kupigana nao na kuwafukuza.”

12 Mungu akamwambia Balaamu, “Usiende pamoja na watu hawa, wala usiwalaani watu hao maana wamebarikiwa.”

13 Basi, asubuhi yake Balaamu aliamka, akawaambia maofisa wa Balaki, “Rudini nchini mwenu, kwa maana Mwenyezi-Mungu hapendi kuniruhusu kwenda pamoja nanyi.”

14 Kwa hiyo maofisa wa Moabu wakaondoka, wakarudi kwa Balaki, wakamwambia, “Balaamu amekataa kuja pamoja nasi.”

15 Kisha, Balaki akatuma maofisa wengine, wengi zaidi na wa vyeo vya juu kuliko wale wa kwanza.

16 Hao walifika kwa Balaamu, wakamwambia, “Balaki mwana wa Sipori asema hivi: ‘Usikubali kuzuiwa na chochote hata uache kuja kwangu.

17 Nitakutunukia heshima kubwa, na chochote utakachoniomba nitakutimizia. Njoo uwalaani watu hawa.’”

18 Lakini Balaamu akawajibu watumishi wa Balaki, “Hata kama Balaki atanipa nyumba yake imejaa fedha na dhahabu, mimi sitaweza kuvunja amri ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu, kuhusu jambo lolote, dogo au kubwa.

19 Lakini tafadhalini laleni hapa usiku huu kama wale wenzenu, nami nipate kujua atakachoniambia Mwenyezi-Mungu tena.”

20 Basi, Mungu akamjia Balaamu usiku huo, akamwambia, “Kama watu hawa wamekuja kukuita, nenda pamoja nao, lakini fanya tu kile nitakachokuambia.”

21 Balaamu akaamka asubuhi, akatandika punda wake, akaenda pamoja na hao maofisa.

22 Hasira ya Mungu iliwaka kwa sababu Balaamu alikuwa anakwenda; hivyo malaika wa Mwenyezi-Mungu akakabiliana naye njiani. Wakati huo Balaamu alikuwa amepanda punda wake akiwa na watumishi wake.

23 Basi, punda alimwona malaika huyo wa Mwenyezi-Mungu amesimama njiani, ameshika upanga uliochomolewa alani mwake. Kwa hiyo aliiacha njia, akaenda pembeni. Balaamu akampiga huyo punda, akamrudisha njiani.

24 Kisha malaika huyo wa Mwenyezi-Mungu akatangulia mbele, akasimama mahali penye njia nyembamba, kati ya mashamba ya mizabibu na kuta pande zote mbili.

25 Punda alipomwona malaika huyo wa Mwenyezi-Mungu, akajisukumiza ukutani na kuubana mguu wa Balaamu hapo. Kwa hiyo Balaamu akampiga tena huyo punda.

26 Kisha malaika akatangulia tena, akasimama mahali pembamba pasipo na nafasi ya kupita kulia wala kushoto.

27 Punda alipomwona huyo malaika wa Mwenyezi-Mungu, akalala chini. Balaamu akawaka hasira, akampiga kwa fimbo yake.

28 Hapo Mwenyezi-Mungu akakifunua kinywa cha huyo punda, akamwambia Balaamu, “Nimekutendea nini hata ukanipiga mara hizi tatu?”

29 Balaamu akamwambia punda, “Wewe umenidhihaki! Kama ningekuwa na upanga ningalikuulia mbali sasa hivi!”

30 Punda akamwambia Balaamu, “Je, mimi si yuleyule punda wako aliyekubeba maisha yako yote hadi siku hii ya leo? Je, nimewahi kukutendea namna hii?” Balaamu akajibu, “La.”

31 Hapo, Mwenyezi-Mungu akayafungua macho ya Balaamu, naye akamwona malaika wa Mwenyezi-Mungu amesimama njiani, ameshika upanga uliochomolewa alani mwake. Balaamu akajitupa chini kifudifudi.

32 Malaika wa Mwenyezi-Mungu akamwambia Balaamu, “Mbona umempiga punda wako mara hizi tatu? Nimekuja kukuzuia, kwa sababu njia yako ni mbaya.

33 Punda wako ameniona akaniepa mara hizi tatu. Kama asingaligeuka mbali nami hakika ningalikuua wewe na kumwacha hai punda huyu.”

34 Balaamu akamwambia malaika wa Mwenyezi-Mungu “Nimetenda dhambi maana sikujua kwamba umesimama njiani kunizuia. Sasa, kama haikupendezi niendelee na safari hii, basi nitarudi nyumbani.”

35 Lakini malaika wa Mwenyezi-Mungu akamwambia Balaamu, “Nenda na watu hawa, lakini utasema tu kile nitakachokuambia.” Basi, Balaamu akaendelea na safari pamoja na viongozi wa Balaki.

36 Balaki alipopata habari kwamba Balaamu anakuja, alitoka kwenda kumlaki mjini Ari, mji uliokuwa ukingoni mwa mto Arnoni kwenye mpaka wa Moabu.

37 Balaki akamwambia Balaamu, “Kwa nini hukuja kwangu mara moja nilipokuita? Je, ulifikiri sitaweza kukutunukia heshima ya kutosha?”

38 Balaamu akamjibu Balaki, “Sasa nimekuja! Lakini, je, nina mamlaka ya kusema chochote tu? Jambo atakaloniambia Mungu ndilo ninalopaswa kusema.”

39 Basi, Balaamu akaenda pamoja na Balaki wakafika mjini Kiriath-husothi.

40 Huko Balaki alitoa kafara ya ng'ombe na kondoo, akawagawia nyama Balaamu na maofisa waliokuwa pamoja naye.

41 Kesho yake, Balaki alimchukua Balaamu, akapanda naye mpaka Bamoth-baali; kutoka huko, Balaamu aliweza kuwaona baadhi ya Waisraeli.

23

1 Balaamu akamwambia Balaki, “Nijengee madhabahu saba hapa kisha uniletee fahali saba na kondoo madume saba.”

2 Balaki akafanya kama Balaamu alivyosema. Basi, wakatoa juu ya kila madhabahu kafara fahali mmoja na kondoo dume mmoja.

3 Halafu Balaamu akamwambia Balaki, “Baki hapa karibu na sadaka yako ya kuteketezwa, nami niende. Labda Mwenyezi-Mungu atakutana nami. Chochote atakachonionesha nitakuja kukuambia.” Basi, Balaamu akaenda peke yake juu ya kilele cha mlima.

4 Mungu akakutana naye. Balaamu akamwambia, “Nimetayarisha madhabahu saba na kutoa kafara fahali mmoja na kondoo dume mmoja juu ya kila madhabahu.”

5 Mwenyezi-Mungu akampa Balaamu maneno atakayosema na kumwambia arudi kwa Balaki.

6 Balaamu akarudi, akamkuta Balaki amesimama palepale karibu na sadaka yake ya kuteketezwa, pamoja na maofisa wote wa Moabu.

7 Balaamu akamtolea Balaki kauli yake, akasema, “Balaki amenileta hapa kutoka Aramu, naam, mfalme wa Moabu amenileta kutoka milima ya mashariki. ‘Njoo uwalaani watu wa Yakobo kwa ajili yangu, naam, njoo uwalaumu Waisraeli!’

8 Nitamlaanije mtu ambaye Mungu hakumlaani? Nitawalaumuje watu ambao Mwenyezi-Mungu hakuwalaumu?

9 Kutoka vilele vya majabali nawaona; kutoka juu ya milima nawachungulia. Hilo taifa likaalo peke yake, lisilojiona kuwa sawa na mataifa mengine.

10 Nani awezaye kuwahesabu wingi wa watu wa Yakobo, au kukisia umati wa Waisraeli? Nife kifo cha waadilifu, mwisho wangu na uwe kama wao.”

11 Hapo, Balaki akamwambia Balaamu, “Umenifanyia nini? Nimekuleta hapa uwalaani adui zangu, lakini badala yake umewabariki!”

12 Balaamu akamwambia Balaki, “Sina budi kusema maneno aliyonipa Mwenyezi-Mungu.”

13 Baadaye, Balaki akamwambia Balaamu, “Twende mahali pengine ambapo utaweza kuwaona; hata hivyo utaona tu sehemu yao, hutaweza kuwaona wote. Kisha uwalaani kutoka huko kwa niaba yangu.”

14 Basi, Balaki akamchukua Balaamu kwenye shamba la Sofimu, juu ya kilele cha Mlima Pisga. Hapo akajenga madhabahu saba na kutoa juu ya kila madhabahu kafara ya fahali mmoja na kondoo dume mmoja.

15 Balaamu akamwambia Balaki, “Baki hapa karibu na sadaka yako ya kuteketezwa, nami niende kule ngambo kukutana na Mwenyezi-Mungu.”

16 Mwenyezi-Mungu akakutana na Balaamu, akampa maneno atakayosema, na kumwambia arudi kwa Balaki.

17 Basi, Balaamu akarudi, akamkuta Balaki amesimama karibu na sadaka ya kuteketezwa pamoja na maofisa wote wa Moabu. Balaki akamwuliza, “Mwenyezi-Mungu amekuambia nini?”

18 Hapo, Balaamu akamtolea Balaki kauli yake: “Inuka, Balaki, usikie, nisikilize ewe mwana wa Sipori.

19 Mungu si mtu, aseme uongo, wala si binadamu, abadili nia yake! Je, ataahidi kitu na asikifanye, au kusema kitu asikitimize?

20 Tazama, nimepewa amri ya kubariki, naye amebariki wala siwezi kuitangua.

21 Mwenyezi-Mungu hajaona ubaya kwa wana wa Yakobo, wala udhia kwa hao wana wa Israeli. Mwenyezi-Mungu Mungu wao yuko pamoja nao, Yeye husifiwa kwa vifijo miongoni mwao, yeye huzipokea sifa zao za kifalme.

22 Mungu aliyewachukua kutoka Misri, huwapigania kwa nguvu kama za nyati.

23 Hakika ulozi hauwezi kuwapinga watu wa Yakobo, wala uchawi dhidi ya watu wa Israeli. Sasa kuhusu Israeli, watu watasema, ‘Tazameni maajabu aliyotenda Mungu!’

24 Tazama! Waisraeli wameinuka kama simba jike, wanasimama kama simba dume. Ni kama simba asiyelala mpaka amalize mawindo yake, na kunywa damu ya mawindo.”

25 Ndipo Balaki akamwambia Balaamu, “Basi, usiwalaani wala usiwabariki kabisa!”

26 Lakini Balaamu akamjibu Balaki, “Je, sikukuambia kwamba anachosema Mwenyezi-Mungu ndicho ninachopaswa kufanya?”

27 Balaki akamwambia Balaamu, “Njoo; nitakupeleka mahali pengine. Labda Mungu atakubali uwalaani watu hao kutoka huko kwa ajili yangu.”

28 Basi, Balaki akamchukua Balaamu mpaka kwenye kilele cha Mlima Peori, ambapo mtu akisimama anaona jangwani.

29 Balaamu akamwambia Balaki, “Nijengee madhabahu saba hapa, unitayarishie fahali saba na kondoo madume saba.”

30 Balaki akafanya kama alivyoambiwa na Balaamu, kisha akatoa juu ya kila madhabahu kafara fahali mmoja na kondoo dume mmoja.

24

1 Sasa Balaamu alitambua kwamba Mwenyezi-Mungu alipenda kuwabariki Waisraeli, kwa hiyo hakwenda kupiga bao tena, akawa anaangalia jangwani.

2 Alitazama juu akawaona Waisraeli wamepiga kambi, kila kabila mahali pake. Kisha roho ya Mungu ikamjia,

3 naye akatamka kauli hii ya kinabii: Kauli yangu mimi Balaamu mwana wa Peori kauli ya mtu aliyefumbuliwa macho;

4 kauli ya mtu aliyesikia maneno ya Mungu mtu aliyeona maono ya Mungu Mwenye Nguvu, mtu anayesujudu na kuona wazi.

5 Hema zako zapendeza namna gani enyi watu wa Yakobo; naam, kambi zenu enyi watu wa Israeli!

6 Ni kama mabonde yanayotiririka maji, kama bustani kandokando ya mto, kama mishubiri aliyopanda Mwenyezi-Mungu, kama mierezi kandokando ya maji.

7 Watakuwa na hazina ya kutosha ya maji, mbegu yao itapata maji mengi, mfalme wao atakuwa mkuu kuliko Agagi, na ufalme wake utatukuka sana.

8 Mungu aliwachukua kutoka Misri, naye huwapigania kwa nguvu kama nyati. Atayateketeza mataifa yaliyo adui zao, atavunjavunja mifupa yao, atawachoma kwa mishale yake.

9 Ataotea na kulala chini kama simba, nani atathubutu kumwamsha? Abarikiwe yeyote atakayewabariki nyinyi Waisraeli, alaaniwe yeyote atakayewalaani.

10 Balaki akawaka hasira dhidi ya Balaamu, akakunja mikono kwa ghadhabu na kumwambia, “Nilikuita uwalaani adui zangu, lakini mara hizi zote tatu umewabariki!

11 Sasa! Nenda zako. Nilikuwa nimekuahidi kukupa zawadi nyingi, lakini Mwenyezi-Mungu hakukujalia kupata zawadi hizo, amekunyima!”

12 Balaamu akamjibu Balaki, “Je, sikuwaambia wajumbe uliowatuma kwangu

13 kwamba hata kama ungenipa nyumba yako imejaa fedha na dhahabu, mimi sitaweza kukiuka agizo la Mwenyezi-Mungu, kwa kufanya jambo lolote, jema au baya kwa hiari yangu mwenyewe? Nilisema, atakachosema Mwenyezi-Mungu ndicho nitakachokisema.

14 “Sasa ninarudi kwa watu wangu, lakini kabla sijaondoka, acha nikuambie mambo ambayo watu hao watawatendea watu wako siku zijazo.”

15 Basi, Balaamu akatamka kauli hii: “Kauli yangu mimi Balaamu mwana wa Beori, kauli ya mtu aliyefumbuliwa macho,

16 kauli ya mtu aliyesikia maneno ya Mungu, na mtu ajuaye maarifa ya Mungu Mkuu, mtu aonaye maono ya Mungu Mwenye Nguvu, mtu anayesujudu, macho wazi.

17 Ninamwona, atakayekuja, lakini baadaye, namwona, lakini hayuko karibu. Nyota itatokea kwa wazawa wa Yakobo, atatokea mfalme miongoni mwa Waisraeli. Kwa fimbo yake atawachapa viongozi wa Wamoabu atawaangamiza wazawa wote wa Sethi.

18 Edomu itamilikiwa naye, Seiri itakuwa mali yake, Israeli itapata ushindi mkubwa.

19 Mmoja wa wazawa wa Yakobo atatawala naye atawaangamiza watakaonusurika wa Ari.”

20 Kisha Balaamu akawaangalia Waamaleki, akatoa kauli hii: “Amaleki ni taifa lenye nguvu kuliko yote, lakini mwishoni litaangamia kabisa.”

21 Kisha Balaamu akawaangalia Wakeni, akatoa kauli hii: “Makao yenu ni salama, enyi Wakeni, kama kiota juu kabisa mwambani.

22 Lakini mtateketezwa, enyi Wakeni. Mtachukuliwa mateka na Ashuru mpaka lini?”

23 Tena Balaamu akatoa kauli hii: “Lo! Nani ataishi, Mungu atakapofanya hayo?

24 Meli zitafika kutoka Kitimu, wataishambulia Ashuru na Eberi, lakini nao pia wataangamia milele.”

25 Basi, Balaamu akaondoka, akarudi nyumbani; Balaki pia akaenda zake.

25

1 Waisraeli walipokuwa huko Shitimu, wanaume walianza kuzini na wanawake wa Moabu.

2 Wanawake hao waliwaalika Waisraeli washiriki matambiko waliyotambikia miungu yao, nao Waisraeli wakala chakula na kuiabudu miungu yao.

3 Ndivyo Waisraeli walivyojiunga na mungu Baali wa Peori, nayo hasira ya Mwenyezi-Mungu ikawaka dhidi yao.

4 Basi, Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, “Wachukue viongozi wote wa Israeli, uwanyonge mbele yangu juani, ili ghadhabu yangu dhidi yenu ipite.”

5 Mose akawaambia waamuzi wa Israeli, “Kila mmoja wenu amuue mtu yeyote miongoni mwenu ambaye amejiunga na mungu Baali wa Peori.”

6 Wakati huohuo mtu mmoja akamleta mwanamke mmoja Mmidiani nyumbani kwake, Mose na jumuiya yote ya watu wa Israeli wakiwa wanaomboleza penye lango la hema la mkutano.

7 Basi, Finehasi mwana wa Eleazari mwana wa kuhani Aroni alipoona hayo, aliinuka akatoka katika hiyo jumuiya, akachukua mkuki

8 na kumfuatia yule Mwisraeli mpaka hemani, akawachoma mkuki wote wawili tumboni. Maradhi mabaya yaliyokuwa yamewaangamiza Waisraeli yakakomeshwa.

9 Waliokufa kutokana na maradhi yale mabaya walikuwa watu 24,000.

10 Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,

11 “Finehasi mwana wa Eleazari, mwana wa kuhani Aroni, ameizuia hasira yangu dhidi ya Waisraeli; miongoni mwenu ni yeye tu aliyeona wivu kama nilio nao mimi. Ndio maana sikuwaangamiza Waisraeli wote kwa hasira yangu.

12 Kwa hiyo mwambie kwamba ninafanya naye agano la amani.

13 Naagana naye kwamba yeye na wazawa wake watakuwa makuhani milele kwa sababu aliona wivu kwa ajili yangu, Mungu wake, akawafanyia upatanisho Waisraeli.”

14 Huyo Mwisraeli aliyeuawa pamoja na mwanamke wa Kimidiani aliitwa Zimri mwana wa Salu, kiongozi wa jamaa mojawapo katika kabila la Simeoni.

15 Na huyo mwanamke Mmidiani aliyeuawa aliitwa Kozbi binti Suri, aliyekuwa kiongozi wa ukoo fulani huko Midiani.

16 Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,

17 “Wachokoze Wamidiani na kuwaangamiza,

18 kwa sababu waliwachokoza nyinyi kwa hila zao, wakawadanganya kuhusu jambo la Peori, na kwa sababu ya Kozbi, binti yao, aliyeuawa wakati maradhi mabaya yalipozuka kule Peori.”

26

1 Baada ya yale maradhi, Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose na Eleazari mwana wa kuhani Aroni,

2 “Hesabuni jumuiya yote ya Waisraeli, kila mtu kufuatana na jamaa yake. Wahesabuni watu wote wenye umri wa miaka ishirini na zaidi wanaofaa kwenda jeshini.”

3 Mose na kuhani Eleazari wakazungumza na watu kwenye nchi tambarare za Moabu, ngambo ya mto Yordani, karibu na Yeriko, wakawaambia,

4 “Hesabuni watu kuanzia na wenye umri wa miaka ishirini na zaidi, kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.” Idadi ya Waisraeli waliotoka Misri ni hii:

5 Kwanza ni kabila la Reubeni, mzaliwa wa kwanza wa Yakobo. Henoki, Palu,

6 Hesroni na Karmi.

7 Hizo ndizo koo za kabila la Reubeni. Idadi ya wanaume waliohesabiwa ni 43,730.

8 Wazawa wa Palu walikuwa Eliabu,

9 na wanawe Nemueli, Dathani na Abiramu. (Hawa wawili: Dathani na Abiramu, ndio waliokuwa wamechaguliwa miongoni mwa jumuiya, lakini wakampinga Mose na Aroni, na kujiunga na wafuasi wa Kora wakati walipomwasi Mwenyezi-Mungu.

10 Wakati huo ardhi ilifunguka ikawameza, wakafa pamoja na Kora na wafuasi wake moto ulipoangamiza watu 250; wakawa onyo kwa watu.

11 Pamoja na hayo wana wa Kora hawakufa.)

12 Kabila la Simeoni. Nemueli, Yamini, Yakini,

13 Zera na Shauli.

14 Hizo ndizo koo za kabila la Simeoni, jumla yao wanaume 22,000.

15 Kabila la Gadi lilikuwa na jamaa za Sefoni, Hagi, Shuni,

16 Ozni, Eri,

17 Arodi na Areli.

18 Hizo ndizo koo za kabila la Gadi, jumla wanaume 40,500.

19 Kabila la Yuda lilikuwa na wanawe wa Yuda Eri na Onani. Hawa walifia nchini Kanaani.

20 Kabila la Yuda lilikuwa na jamaa za Shela, Peresi, na Zera.

21 Kutoka kwa Peresi, familia ya Hesroni na Hamuli.

22 Hizo ndizo koo za Yuda, jumla wanaume 76,500.

23 Kabila la Isakari lilikuwa na jamaa za Tola, Puva,

24 Yashubu na wa Shimroni.

25 Hizo ndizo koo za Isakari, jumla wanaume 64,300.

26 Kabila la Zebuluni lilikuwa na jamaa za Seredi, wa Eloni na wa Yaleeli.

27 Hizo ndizo koo za Zebuluni, jumla wanaume 60,500.

28 Kabila la Yosefu baba yao Manase na Efraimu.

29 Kabila la Manase lilikuwa na jamaa ya: Makiri, Gileadi.

30 Yezeri, Heleki,

31 Asrieli, Shekemu,

32 Shemida na Heferi.

33 Selofehadi, mwana wa Heferi hakupata watoto wa kiume bali wa kike tu, nao ni Mala, Noa, Hogla, Milka na Tirza.

34 Hizo ndizo koo za Manase, jumla wanaume 52,700.

35 Kabila la Efraimu lilikuwa na jamaa za Shuthela, Bekeri na Tahani.

36 Ukoo wa Erani ulikuwa na jamaa ya Shuthela.

37 Hizo ndizo koo za Efraimu, jumla wanaume 32,500. Zote hizo zilitokana na Yosefu.

38 Kabila la Benyamini lilikuwa na jamaa za Bela, Ashbeli, Ahiramu,

39 Shufamu na Hufamu.

40 Koo za Ardi na Naamani, zilitokana na Bela.

41 Hizo ndizo koo za Benyamini, jumla wanaume 45,600.

42 Kabila la Dani lilikuwa na jamaa ya Shuhamu;

43 ukoo ulikuwa na wanaume 64,400.

44 Kabila la Asheri lilikuwa na jamaa za Imna, Ishvi na Beria.

45 Koo za Heberi na Malkieli zilitokana na Beria.

46 Asheri alikuwa na binti aliyeitwa Sera.

47 Hizo ndizo koo za kabila la Asheri, jumla wanaume 53,400.

48 Kabila la Naftali lilikuwa na jamaa za Yaseeli, Guni,

49 Yeseri na Shilemu.

50 Hizi ndizo koo za kabila la Naftali, jumla wanaume 45,400.

51 Idadi ya wanaume Waisraeli waliohesabiwa ilikuwa 601,730.

52 Kisha Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

53 “Makabila haya yatagawiwa nchi iwe urithi wao, kulingana na idadi ya majina yao.

54 Kabila kubwa litapewa sehemu yao kubwa na dogo litapewa sehemu yao ndogo. Kila kabila litapewa urithi wake kulingana na idadi ya watu wake.

55 Hata hivyo ugawaji wa nchi utafanywa kwa kura. Kila kabila litarithi kulingana na majina ya ukoo wao.

56 Urithi wa kila kabila utagawanywa kwa kura, kila kabila litapata kulingana na ukubwa au udogo wake.”

57 Hizi ndizo koo za Walawi zilizoorodheshwa na jamaa zao: Gershoni, Kohathi na Merari,

58 Pamoja na jamaa za Libni, Hebroni, Mahli, Mushi na Kora. Kohathi alikuwa baba yake Amramu.

59 Mkewe Amramu aliitwa Yokebedi binti yake Lawi, aliyezaliwa Misri. Huyu alimzalia Amramu watoto wawili wa kiume, Aroni na Mose, na binti mmoja, Miriamu.

60 Aroni alikuwa na watoto wa kiume wanne: Nadabu, Abihu, Eleazari na Ithamari.

61 Nadabu na Abihu walikufa walipomtolea Mwenyezi-Mungu sadaka ya moto usiofaa.

62 Idadi ya Walawi wanaume wenye umri wa mwezi mmoja na zaidi ilikuwa 23,000. Hawa hawakuhesabiwa pamoja na Waisraeli wengine kwa sababu wao hawakupewa urithi wowote miongoni mwao.

63 Hao ndio wanaume Waisraeli walioorodheshwa na Mose na kuhani Eleazari katika nchi tambarare za Moabu, ngambo ya mto Yordani, karibu na Yeriko.

64 Miongoni mwao hakuwamo hata mtu mmoja aliyesalia kati ya wale waliohesabiwa na Mose na kuhani Aroni ambao walifanya sensa ya kwanza jangwani Sinai.

65 Mwenyezi-Mungu alikuwa amesema kwamba wote watafia jangwani, na kweli hakuna hata mmoja wao aliyebaki hai, isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune, na Yoshua mwana wa Nuni.

27

1 Mala, Noa, Hogla, Milka na Tirza walikuwa binti zake Selofehadi. Naye Selofehadi alikuwa mwana wa Heferi, mwana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase mwanawe Yosefu.

2 Basi, hao binti wanne walimwendea Mose, wakasimama mbele yake na kuhani Eleazari na viongozi wote wa jumuiya ya Waisraeli, kwenye mlango wa hema la mkutano, wakasema,

3 “Baba yetu alifia jangwani nyikani na bila mtoto yeyote wa kiume.

4 Yeye hakuwa miongoni mwa wafuasi wa Kora waliokusanyika dhidi ya Mwenyezi-Mungu, bali alikufa kutokana na dhambi yake mwenyewe. Kwa nini basi jina la baba yetu lifutwe katika ukoo wake kwa sababu hakuwa na mtoto wa kiume? Tupe urithi pamoja na ndugu zake baba yetu.”

5 Mose akaleta lalamiko lao mbele ya Mwenyezi-Mungu.

6 Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,

7 “Wanachosema binti za Selofehadi ni kweli; wape urithi pamoja na ndugu za baba yao, wachukue urithi wake.

8 Kisha waambie Waisraeli kwamba mtu yeyote akifa bila kuacha mtoto wa kiume, urithi wake atapewa binti yake.

9 Ikiwa hana binti, basi urithi huo watapewa ndugu zake wa kiume.

10 Na ikiwa hana ndugu wa kiume, basi urithi wake utawaendea baba zake, wakubwa na wadogo.

11 Na ikiwa baba yake hana ndugu wa kiume, basi urithi wake utakuwa wa jamaa yake wa karibu, naye ataumiliki kama mali yake. Hii itakuwa kanuni na sheria kwa Waisraeli, kama vile mimi Mwenyezi-Mungu nilivyokuamuru.”

12 Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, “Panda juu ya Mlima huu wa miinuko ya Abarimu uitazame nchi ambayo nimewapa Waisraeli.

13 Ukisha iona, nawe pia utafariki kama ndugu yako Aroni alivyofariki,

14 kwa sababu hamkuitii amri yangu kule jangwani Sini. Wakati jumuiya yote ya watu walipolalamika juu yangu kule Meriba, hamkuacha utukufu wangu uonekane mbele yao walipotaka wapewe maji.” (Meriba ni chemchemi ya maji ya Kadeshi katika jangwa la Sini).

15 Naye Mose akamwomba Mwenyezi-Mungu,

16 “Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu uliye asili ya uhai wote, nakuomba umteue mtu wa kuisimamia jumuiya hii,

17 ambaye atawatangulia na kuwaongoza katika shughuli zao zote, ili wasije wakawa kama kondoo wasio na mchungaji.”

18 Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, “Mtwae Yoshua mwana wa Nuni, mtu mwenye roho nzuri, kisha umwekee mikono,

19 na kumsimamisha mbele ya kuhani Eleazari na jumuiya yote, umkabidhi jukumu hilo.

20 Mpe sehemu ya mamlaka yako ili jumuiya yote ya Waisraeli imtii.

21 Yeye atamtegemea kuhani Eleazari ambaye atamjulisha matakwa yangu kwa kutumia jiwe la kauli. Kwa njia hii, Eleazari atamwongoza Yoshua na jumuiya yote ya Waisraeli wanapotoka na wanapoingia.”

22 Mose akafanya kama alivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu. Alimtwaa Yoshua na kumsimamisha mbele ya kuhani Eleazari na jumuiya yote ya Waisraeli.

23 Kisha akamwekea mikono kichwani na kumpa mamlaka kama alivyoagizwa na Mwenyezi-Mungu.

28

1 Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

2 “Waamuru Waisraeli ifuatavyo: Nyinyi mtanitolea kwa wakati wake tambiko zitakiwazo: Vyakula vya kuteketezwa kwa moto, vyenye harufu nzuri ya kupendeza.

3 Waambie kwamba sadaka watakayonitolea ya kuteketezwa kwa moto, itakuwa ifuatavyo: Wanakondoo wawili wa mwaka mmoja wasio na dosari yoyote, kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa ya kila siku.

4 Mwanakondoo mmoja atatolewa asubuhi na wa pili jioni;

5 kila mmoja atatolewa pamoja na sadaka ya nafaka ya kilo moja ya unga uliochanganywa pamoja na lita moja ya mafuta bora yaliyopondwa.

6 Hii ni sadaka ya kutolewa kila siku inayoteketezwa kabisa motoni, ambayo ilitolewa kwa mara ya kwanza mlimani Sinai kama sadaka ya chakula, harufu nzuri ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu.

7 Sadaka ya kinywaji itakayotolewa na kila mwanakondoo ni lita moja ya divai. Utaimimina sadaka hii ya kinywaji kikali mahali patakatifu.

8 Wakati wa jioni utamtoa yule mwanakondoo mwingine kama sadaka ya nafaka na kama sadaka ya kinywaji utaitoa kama sadaka ya kuteketezwa kwa moto, sadaka yenye harufu nzuri ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu.

9 “Siku ya Sabato, mtatoa sadaka ya wanakondoo wawili wa kiume wa mwaka mmoja wasio na dosari, sadaka ya nafaka ya kilo mbili za unga laini uliochanganywa na mafuta, na sadaka yake ya kinywaji.

10 Sadaka hii ya kuteketezwa itatolewa kila siku ya Sabato licha ya ile sadaka ya kila siku pamoja na sadaka yake ya kinywaji.

11 “Mwanzoni mwa kila mwezi, mtamtolea Mwenyezi-Mungu sadaka ya kuteketezwa: Fahali wadogo wawili, kondoo dume mmoja na, wanakondoo saba madume wa mwaka mmoja, wasio na dosari.

12 Mtatoa sadaka ya nafaka ya unga laini kilo tatu, uliochanganywa na mafuta kwa kila fahali mmoja; mtatoa kilo mbili za unga kwa kila kondoo dume,

13 na kilo moja ya unga kwa kila mwanakondoo. Sadaka hizi za kuteketezwa ni sadaka za chakula zenye harufu ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu.

14 Kipimo cha sadaka ya kinywaji kinachohitajika ni lita 2 za divai kwa kila fahali; lita moja u nusu kwa kila kondoo dume, na lita moja kwa kila mwanakondoo. Hii ndiyo sadaka ya kuteketezwa ya kila mwezi katika mwaka mzima.

15 Tena mtamtolea Mwenyezi-Mungu sadaka ya kuondoa dhambi, beberu mmoja, licha ya ile sadaka ya kuteketezwa ya kila siku na sadaka yake ya kinywaji.

16 “Siku ya kumi na nne ya mwezi wa kwanza ni Pasaka ya Mwenyezi-Mungu.

17 Siku ya kumi na tano ya mwezi huohuo ni sikukuu. Kwa muda wa siku saba mtakula mikate isiyotiwa chachu.

18 Katika siku ya kwanza kutakuwa na mkutano mtakatifu. Siku hiyo hamtafanya kazi.

19 Mtatoa sadaka ya kuteketezwa kama sadaka ya chakula kwa Mwenyezi-Mungu: Fahali wachanga wawili, kondoo dume mmoja, wanakondoo madume saba wa mwaka mmoja, wote wawe bila dosari.

20 Sadaka ya nafaka itakayoandamana nazo itakuwa ya unga safi uliochanganywa na mafuta, kilo tatu kwa kila fahali, kilo mbili kwa kila kondoo dume,

21 na kilo moja kwa kila mmoja wa wale wanakondoo saba.

22 Mtatoa pia beberu mmoja kuwa sadaka ya kuondoa dhambi ili kuwafanyia upatanisho.

23 Mtatoa vitu hivi licha ya ile sadaka ya kuteketezwa ya kawaida inayotolewa kila siku asubuhi.

24 Vivyo hivyo, kwa muda wa siku saba, mtatoa sadaka ya kuteketezwa ya kawaida ya chakula kwa kuteketezwa, ambayo ni harufu nzuri ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu. Hii mtaitoa licha ya ile sadaka ya kuteketezwa ya kila siku na sadaka yake ya kinywaji.

25 Katika siku ya saba mtafanya mkutano mtakatifu; msifanye kazi.

26 “Mnamo siku ya kwanza ya sikukuu ya majuma wakati mnapomtolea Mwenyezi-Mungu malimbuko ya nafaka zenu, mtafanya mkutano mtakatifu; msifanye kazi.

27 Mtatoa sadaka ya kuteketezwa, harufu nzuri ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu: Fahali wachanga wawili, kondoo dume mmoja, na wanakondoo saba madume wa mwaka mmoja, wote hao wawe hawana dosari.

28 Sadaka ya nafaka itakayoandamana nazo itakuwa ya unga safi uliochanganywa na mafuta kilo tatu kwa kila fahali, kilo mbili kwa kila kondoo dume,

29 na kilo moja kwa kila mwanakondoo.

30 Mtatoa pia beberu mmoja kuwa sadaka ya kuondoa dhambi ili kuwafanyia upatanisho.

31 Mtatoa vitu hivi licha ya ile sadaka ya kuteketezwa ya kawaida pamoja na sadaka yake ya kinywaji.

29

1 “Siku ya kwanza ya mwezi wa saba, mtafanya mkutano mtakatifu. Msifanye kazi. Hiyo ni siku ya kupiga tarumbeta.

2 Mtatoa sadaka ya kuteketezwa, harufu nzuri ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu: Fahali wachanga wawili, kondoo madume wawili, na wanakondoo wa kiume saba wa mwaka mmoja, wote wawe wasio na dosari yoyote.

3 Mtatoa pia sadaka yake ya nafaka ya unga safi uliochanganywa na mafuta: Kilo tatu kwa kila fahali, kilo mbili kwa kila kondoo dume,

4 na kilo moja kwa kila mwanakondoo.

5 Tena mtatoa beberu mmoja kuwa sadaka ya kuondoa dhambi ili kuwafanyia upatanisho.

6 Mtatoa vitu hivi licha ya ile sadaka ya kuteketezwa ya mwezi mpya na sadaka yake ya nafaka, na sadaka ya kila siku ya kuteketezwa pamoja na sadaka yake ya nafaka na sadaka zake za kinywaji kama inavyotakiwa kuwa harufu nzuri ipendezayo, ni sadaka kwa Mwenyezi-Mungu iliyoteketezwa kwa moto.

7 “Siku ya kumi ya mwezi wa saba mtafanya mkutano mtakatifu. Siku hiyo ni lazima mfunge na msifanye kazi.

8 Mtamtolea Mwenyezi-Mungu sadaka ya kuteketezwa kwa moto, harufu ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu: Fahali mmoja mchanga, kondoo dume mmoja, wanakondoo saba wa mwaka mmoja. Wote wasiwe na dosari.

9 Licha ya vitu hivi mtatoa sadaka ya unga safi uliochanganywa na mafuta kilo tatu pamoja na huyo fahali, kilo mbili pamoja na yule kondoo dume,

10 na kilo moja kwa kila mwanakondoo.

11 Mtatoa pia beberu mmoja kwa sadaka ya kuondoa dhambi licha ya sadaka ya kufanyiwa upatanisho, pamoja na sadaka ya kawaida ya kuteketezwa na sadaka yake ya nafaka na sadaka zake za kinywaji.

12 “Siku ya kumi na tano ya mwezi wa saba, mtafanya mkutano mtakatifu. Hamtafanya kazi siku hiyo. Mtaadhimisha sikukuu kwa ajili ya Mwenyezi-Mungu kwa siku saba.

13 Mtatoa sadaka ya kuteketezwa kwa moto, iliyo harufu nzuri inayompendeza Mwenyezi-Mungu: Fahali wachanga kumi na watatu, kondoo madume wawili, wanakondoo kumi na wanne wa mwaka mmoja. Wote wawe bila dosari.

14 Sadaka itakayoandamana nazo itakuwa unga safi uliochanganywa na mafuta: Kilo tatu kwa kila fahali, kilo mbili kwa kila kondoo,

15 na kilo moja kwa kila mwanakondoo.

16 Mtatoa pia beberu mmoja kuwa sadaka ya kuondoa dhambi, licha ya ile sadaka ya kawaida ya kuteketezwa, pamoja na sadaka yake ya nafaka na sadaka yake ya kinywaji.

17 “Siku ya pili mtatoa: Fahali wachanga kumi na wawili, kondoo madume wawili, wanakondoo wa kiume kumi na wanne, wa mwaka mmoja wasio na dosari.

18 Mtatoa pia sadaka ya nafaka na sadaka za vinywaji pamoja na wale fahali, kondoo na wanakondoo, kulingana na idadi yao.

19 Mtatoa pia beberu mmoja kuwa sadaka ya kuondoa dhambi, licha ya sadaka ya kuteketezwa ya kawaida pamoja na sadaka yake ya nafaka na sadaka yake ya kinywaji.

20 “Siku ya tatu mtatoa: Fahali kumi na mmoja, kondoo wawili, wanakondoo kumi na wanne wa mwaka mmoja, wasio na dosari.

21 Mtawatolea pamoja na sadaka ya nafaka na sadaka za kinywaji kama ilivyotakiwa kulingana na idadi yao.

22 Vilevile mtatoa beberu mmoja kwa sadaka ya kuondoa dhambi, licha ya ile sadaka ya kawaida ya kuteketezwa pamoja na sadaka yake ya nafaka na sadaka yake ya kinywaji.

23 “Siku ya nne mtatoa: Fahali kumi, kondoo madume wawili, wanakondoo kumi na wanne, wasio na dosari.

24 Mtatoa pia sadaka ya nafaka na sadaka za kinywaji pamoja na hao fahali na kondoo na wanakondoo kulingana na idadi yao, kama inavyotakiwa.

25 Mtatoa pia beberu mmoja kwa sadaka ya kuondoa dhambi licha ya sadaka ya kawaida ya kuteketezwa, pamoja na sadaka yake ya nafaka na sadaka yake ya kinywaji.

26 “Siku ya tano, mtatoa fahali tisa, kondoo wawili, wanakondoo madume kumi na wanne wa mwaka mmoja wasio na dosari.

27 Mtatoa pia sadaka ya nafaka na sadaka za kinywaji pamoja na hao fahali na kondoo na wanakondoo kulingana na idadi yao kama inavyotakiwa.

28 Mtatoa pia beberu mmoja kwa sadaka ya kuondoa dhambi, licha ya sadaka ya kawaida ya kuteketezwa, pamoja na sadaka yake ya nafaka na sadaka yake ya kinywaji.

29 “Siku ya sita mtatoa fahali wanane, kondoo madume wawili, wanakondoo madume kumi na wanne wa mwaka mmoja wasio na dosari.

30 Mtatoa pia sadaka ya nafaka na sadaka za kinywaji pamoja na hao fahali, kondoo dume na wanakondoo kulingana na idadi yao, kama inavyotakiwa.

31 Mtatoa pia beberu mmoja kuwa sadaka ya kuondoa dhambi, pamoja na sadaka yake ya nafaka na sadaka zake za kinywaji.

32 “Siku ya saba mtatoa fahali saba, kondoo madume watatu, wanakondoo madume kumi na wanne wa mwaka mmoja, wasio na dosari.

33 Mtatoa pia sadaka ya nafaka na sadaka za kinywaji pamoja na hao fahali, kondoo dume, na wanakondoo, kulingana na idadi yao, kama wanavyotakiwa.

34 Mtatoa pia beberu mmoja kuwa sadaka ya kuondoa dhambi, licha ya ile sadaka ya kawaida ya kuteketezwa, pamoja na sadaka yake ya nafaka na sadaka yake ya kinywaji.

35 “Siku ya nane mtakuwa na mkutano mkubwa. Msifanye kazi siku hiyo.

36 Mtatoa sadaka ya kuteketezwa iliyo harufu nzuri inayompendeza Mwenyezi-Mungu: Fahali mmoja, kondoo dume mmoja, na wanakondoo madume saba wa mwaka mmoja wasio na dosari.

37 Mtatoa pia sadaka ya nafaka na sadaka za kinywaji pamoja na huyo fahali, huyo kondoo dume, na wale wanakondoo kulingana na idadi yao kama inavyotakiwa.

38 Pia mtatoa beberu mmoja kuwa sadaka ya kuondoa dhambi, licha ya ile sadaka ya kawaida ya kuteketezwa pamoja na sadaka yake ya nafaka na sadaka ya kinywaji.

39 “Haya ndiyo maagizo kuhusu sadaka za kuteketezwa, sadaka za nafaka, na sadaka za amani mtakazomtolea Mwenyezi-Mungu wakati wa sikukuu zenu zilizopangwa. Licha ya hizi zote, zipo pia sadaka za kuteketezwa, za nafaka na za kinywaji, ambazo mnamtolea Mwenyezi-Mungu kutimiza nadhiri zenu na sadaka zenu za hiari.”

40 Basi, Mose akawaambia Waisraeli kila kitu kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru.

30

1 Kisha Mose alizungumza na viongozi wa makabila ya Israeli, akawaambia, “Hili ndilo neno lililoamriwa na Mwenyezi-Mungu:

2 “Mtu akiweka nadhiri kwa Mwenyezi-Mungu au akiahidi kwa kiapo na kujifunga nafsi yake kwa ahadi, ni lazima atimize ahadi yake; ni lazima atekeleze yote yale aliyotamka kwa kauli yake.

3 “Msichana ambaye bado anaishi nyumbani kwa baba yake akiweka nadhiri kwa Mwenyezi-Mungu na kujifunga mwenyewe kwa ahadi,

4 na baba yake akawa amesikia ahadi hiyo, asimpinge, basi, nadhiri zake alizoweka zitambana na kila ahadi aliyotoa itambana.

5 Lakini kama baba yake akisikia juu ya nadhiri hiyo, akampinga, basi nadhiri zake na ahadi yake havitambana. Mwenyezi-Mungu atamsamehe kwa sababu baba yake amelipinga jambo hilo.

6 “Ikiwa msichana ataolewa baada ya kuweka nadhiri, au kuahidi bila ya kufikiri vizuri kwanza, na akajifunga mwenyewe,

7 halafu mumewe akasikia jambo hilo asimpinge, basi nadhiri zake zitambana na ahadi zake zitambana.

8 Lakini kama mume wake akisikia jambo hilo akampinga, basi huyo mumewe atabatilisha nadhiri ya mkewe na tamko lake alilotoa bila kufikiri; naye Mwenyezi-Mungu atamsamehe.

9 “Lakini nadhiri au ahadi yoyote aliyoiweka mama mjane au mwanamke aliyepewa talaka ambayo kwayo amejifunga, ni lazima imbane.

10 “Mwanamke aliyeolewa akiweka nadhiri au akiahidi kwa kiapo akiwa nyumbani kwa mumewe,

11 kisha mume wake akasikia jambo hilo lakini asimpinge, wala kumwambia kitu, basi, nadhiri zake zote zitambana; kadhalika na ahadi zake zote zitambana.

12 Lakini kama mumewe atakaposikia habari zake, akizitangua na kuzibatilisha, basi, hata kama alitaka kutimiza nadhiri au ahadi zake, hatawajibika kuzitimiza; mumewe atakuwa amezitangua na Mwenyezi-Mungu atamsamehe.

13 Mumewe anaweza kuthibitisha au kutangua nadhiri au ahadi yoyote inayomfunga.

14 Lakini ikiwa mumewe hatasema neno lolote tangu siku atakaposikia habari za nadhiri au ahadi za mkewe, basi atakuwa amezithibitisha siku hiyo alipopata habari zake kwa sababu hakusema chochote.

15 Lakini akizibatilisha na kuzitangua muda fulani baada ya kusikia habari zake, basi yeye atakuwa na lawama kwa kosa la mkewe.”

16 Hizi ndizo kanuni ambazo Mwenyezi-Mungu alimwagiza Mose juu ya mume na mkewe; baba na binti yake, huyo binti akiwa bado kijana na anakaa nyumbani kwa baba yake.

31

1 Mwenyezi-Mungu aliongea na Mose, akamwambia,

2 “Walipize kisasi Wamidiani mambo waliyowatenda Waisraeli; kisha wewe utafariki.”

3 Basi Mose akazungumza na watu akawaambia, “Watayarisheni watu kwa vita waende kuwashambulia Wamidiani kumlipizia Mwenyezi-Mungu kisasi.

4 Kutoka kila kabila la Israeli, mtapeleka watu 1.000 vitani.”

5 Basi, watu 1,000 walitolewa kutoka kila kabila miongoni mwa maelfu ya Waisraeli, jumla wanaume 12,000 wenye silaha.

6 Mose aliwapeleka vitani chini ya uongozi wa Finehasi mwana wa kuhani Eleazari, akiwa na vyombo vya mahali patakatifu na tarumbeta za kutoa ishara.

7 Waliishambulia nchi ya Midiani, kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose, wakawaua wanaume wote.

8 Miongoni mwa watu hao waliouawa, kulikuwako wafalme watano wa Midiani: Evi, Rekemu, Suri, Huri na Reba. Vilevile walimuua Balaamu mwana wa Beori.

9 Waisraeli waliteka nyara: Ng'ombe, kondoo na mali yao yote.

10 Miji yao yote, makazi yao na kambi zao zote waliziteketeza kwa moto.

11 Walichukua nyara zote na mateka yote, ya watu na ya wanyama,

12 wakampelekea Mose na Eleazari, na jumuiya yote ya Waisraeli iliyokuwa kambini katika nchi tambarare za Moabu, ngambo ya Yordani karibu na Yeriko.

13 Mose, kuhani Eleazari, na viongozi wote wa jumuiya ya Waisraeli walitoka kambini, wakaenda kuwalaki wanajeshi.

14 Mose alikasirishwa na maofisa wa jeshi na makamanda waliosimamia makundi ya majeshi 1,000 na makundi ya wanajeshi mamia waliorudi kutoka vitani.

15 Mose akawauliza, “Kwa nini mmewaacha wanawake hawa wote hai?

16 Kumbukeni kwamba wanawake ndio waliofuata shauri la Balaamu, wakasababisha Waisraeli wamwasi Mwenyezi-Mungu kule Peori hata maradhi mabaya yakawajia watu wake Mwenyezi-Mungu.

17 Kwa hiyo basi, waueni watoto wote wa kiume na kila mwanamke aliyewahi kulala na mwanamume.

18 Lakini msiwaue wasichana wote ambao hawajapata kulala na mwanamume; waacheni hai kwa ajili yenu wenyewe.

19 Wote wale walio miongoni mwenu ambao wameua mtu au kugusa maiti ni lazima wakae nje ya kambi kwa muda wa siku saba; jitakaseni pamoja na mateka wenu katika siku ya tatu na ya saba.

20 Ni lazima mtakase pia kila vazi, kila kitu kilichotengenezwa kwa ngozi, kwa manyoya ya kondoo au kwa mti.”

21 Kuhani Eleazari akawaambia wanaume waliorudi vitani, “Hii ndiyo sheria ambayo Mwenyezi-Mungu amempa Mose.

22 Dhahabu, fedha, shaba, chuma, bati na madini ya risasi,

23 yaani vitu vyote ambavyo vinastahimili moto, vitatakaswa kwa kupitishwa motoni. Hata hivyo, ni lazima vitakaswe kwa maji ya utakaso. Vitu vingine vyote ambavyo haviwezi kustahimili moto vitatakaswa kwa maji ya utakaso.

24 Siku ya saba ni lazima muyafue mavazi yenu; ndipo mtakapokuwa safi na kuruhusiwa kuingia kambini.”

25 Mwenyezi-Mungu akaongea na Mose, akamwambia,

26 “Wewe na kuhani Eleazari, pamoja na viongozi wa koo za jumuiya ya Waisraeli, fanyeni hesabu ya nyara ya vitu, watu na wanyama.

27 Gaweni nyara katika mafungu mawili, fungu moja la wanajeshi waliokwenda vitani na fungu lingine kwa ajili ya jumuiya nzima.

28 Kisha kutokana na lile fungu la wanajeshi waliokwenda vitani, tenga zaka kwa ajili ya Mwenyezi-Mungu: Kitu kimoja kutoka kila vitu 500, iwe ni watu, ng'ombe, punda, kondoo au mbuzi,

29 umpe kuhani Eleazari kuwa sadaka kwa Mwenyezi-Mungu.

30 Kutoka lile fungu la jumuiya nzima, chukua sehemu moja ya kila hamsini, iwe ni watu, ng'ombe, punda, kondoo na mbuzi. Hivyo utawapa Walawi ambao wana wajibu wa kuhudumu katika hema la Mwenyezi-Mungu.”

31 Mose na kuhani Eleazari walifanya kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.

32 Nyara walizoteka wanajeshi zilikuwa: Kondoo 675,000,

33 ng'ombe 72,000,

34 punda 61,000,

35 na wasichana ambao hawakuwa wamelala na mwanamume 32,000.

36 Nusu yake, sehemu ambayo iligawiwa wanajeshi waliokwenda vitani, ilikuwa kondoo 337,500,

37 katika hao 675 walitolewa kwa Mwenyezi-Mungu.

38 Ngombe wa wanajeshi walikuwa 36,000, na katika hao 72 walitolewa zaka kwa Mwenyezi-Mungu.

39 Punda wao walikuwa 30,500, na katika hao 61 walitolewa zaka kwa Mwenyezi-Mungu.

40 Watu walikuwa 16,000, na katika hao sehemu ya Mwenyezi-Mungu ilikuwa ni watu thelathini na wawili.

41 Basi, Mose akampa kuhani Eleazari zaka hiyo iliyotolewa kwa Mwenyezi-Mungu, kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.

42 Ile nusu waliopewa Waisraeli, ambayo Mose aliitenga na ile nusu waliyopewa wanajeshi waliokwenda vitani,

43 ilikuwa kondoo 337,500,

44 ng'ombe 36,000,

45 punda 30,500,

46 na watu 16,000.

47 Kutoka nusu hii waliyopewa Waisraeli, Mose alitwaa mmoja kati ya kila mateka hamsini na wanyama hamsini, kama alivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu, akawapa Walawi ambao walihudumu katika hema la Mwenyezi-Mungu.

48 Kisha maofisa wa majeshi, makapteni na makamanda wa askari wakamwendea Mose,

49 wakamwambia “Watumishi wako tumewahesabu askari wote walio chini yetu na tumeona kwamba hakuna hata mmoja wao anayekosekana.

50 Basi, tumeleta vyombo vya dhahabu, vikuku, bangili, pete za mhuri, vipuli na shanga ambavyo kila mtu alipata. Tumevitoa ili nafsi zetu zifanyiwe upatanisho mbele ya Mwenyezi-Mungu.”

51 Mose na kuhani Eleazari wakapokea vitu vyote vilivyonakshiwa kwa dhahabu.

52 Jumla ya dhahabu yote waliyomtolea Mwenyezi-Mungu ilikuwa karibu kilo 200.

53 (Kila askari alijichukulia nyara zake binafsi).

54 Basi, Mose na kuhani Eleazari wakaipokea dhahabu hiyo kutoka kwa makamanda wakaipeleka katika hema la mkutano, iwe ukumbusho wa Waisraeli mbele ya Mwenyezi-Mungu.

32

1 Makabila ya Reubeni na Gadi yalikuwa na mifugo mingi sana. Basi, walipoona kwamba eneo la Yazeri na Gadi lilifaa kwa mifugo,

2 waliwaendea Mose, kuhani Eleazari na viongozi wa jumuiya, wakawaambia,

3 “Miji ya Atarothi, Diboni, Yazeri, Nimra, Heshboni, Eleale, Sebamu, Nebo na Beoni,

4 nchi ambayo Mwenyezi-Mungu alishinda kwa ajili ya jumuiya ya Israeli, ni nchi nzuri kwa mifugo, nasi tunayo mifugo mingi sana.

5 Basi, kama mkitukubalia tunawaomba mtupe nchi hii iwe mali yetu; msituvushe ngambo ya mto Yordani.”

6 Mose akawajibu watu wa makabila ya Gadi na Reubeni, “Je, mnataka kubaki hapa huku ndugu zenu Waisraeli wanakwenda vitani?

7 Mbona mnawavunja moyo Waisraeli wasiende katika nchi ambayo Mwenyezi-Mungu amewapa?

8 Hivyo ndivyo walivyofanya babu zenu nilipowatuma kutoka Kadesh-barnea kuipeleleza nchi.

9 Wao walikwenda hadi bonde la Eshkoli, wakaiona nchi, lakini waliporudi, waliwavunja moyo Waisraeli ili wasiingie katika nchi aliyowapa Mwenyezi-Mungu.

10 Mwenyezi-Mungu aliwaka hasira siku hiyo, akaapa akisema,

11 ‘Hakika hakuna mtu yeyote kati ya watu waliotoka Misri mwenye umri wa miaka ishirini na zaidi atakayeiona nchi niliyoapa kuwapa Abrahamu, Isaka na Yakobo, kwa sababu hawakunitii kikamilifu.’

12 Wote hawataiona, isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune, Mkenizi, na Yoshua mwana wa Nuni, maana wao wamenitii kikamilifu.

13 Mwenyezi-Mungu aliwaka hasira dhidi ya Waisraeli, akawafanya watangetange jangwani kwa muda wa miaka arubaini; kizazi kizima kilichokuwa kimefanya maovu mbele yake kikafariki.

14 Na sasa, enyi kizazi cha wenye dhambi, mmezuka mahali pa wazee wenu, kuongeza tena hasira kali ya Mwenyezi-Mungu dhidi ya Waisraeli.

15 Kama nyinyi mkikataa kumfuata, yeye atawaacheni tena jangwani, nanyi mtasababisha watu hawa wote waangamie.”

16 Basi, wakamwendea Mose, wakamwambia, “Kwanza turuhusu tuwajengee kondoo wetu mazizi, na watoto wetu miji hapa.

17 Lakini sisi wenyewe tutachukua silaha zetu tayari kwenda vitani pamoja na ndugu zetu Waisraeli, na tutakuwa mstari wa mbele vitani hadi tuwafikishe mahali watakapokaa. Wakati huo watoto wetu watakaa kwenye miji yenye ngome, ili kujilinda na wenyeji wa nchi hii.

18 Hatutarudi nyumbani hadi hapo Waisraeli wengine wote watakapomiliki maeneo yao waliyogawiwa.

19 Hatutamiliki mali yoyote miongoni mwao ngambo ya mto Yordani, kwa sababu sisi tumepata maeneo yetu ngambo hii, mashariki ya mto Yordani.”

20 Mose akawaambia, “Kama kweli mtafanya kama mlivyosema, basi papa hapa mbele ya Mwenyezi-Mungu, chukueni silaha zenu kwenda vitani.

21 Kila mpiganaji wenu atavuka mto Yordani na mkiwa chini ya uongozi wa Mwenyezi-Mungu, mtawashambulia adui zetu mpaka Mwenyezi-Mungu awashinde,

22 na kuimiliki nchi. Mkisha fanya hayo, mtarudi, maana mtakuwa mmetimiza wajibu wenu kwa Mwenyezi-Mungu na ndugu zenu Waisraeli. Kisha Mwenyezi-Mungu atakubali nchi hii ya mashariki ya Yordani kuwa mali yenu.

23 Lakini nawaonyeni kwamba msipotimiza ahadi yenu, mtakuwa mnamtendea Mwenyezi-Mungu dhambi; jueni kwa hakika kwamba mtaadhibiwa.

24 Wajengeeni watoto wenu miji na kondoo wenu mazizi; lakini fanyeni kama mlivyoahidi.”

25 Kisha, watu wa Gadi na wa Reubeni wakamwambia Mose, “Sisi watumishi wako tutafanya kama ulivyotuamuru.

26 Wake zetu, watoto wetu na kondoo na ng'ombe, watabaki hapa katika miji ya Gileadi.

27 Lakini sisi watumishi wako tuko tayari kwenda vitani chini ya uongozi wa Mwenyezi-Mungu. Tutavuka mto Yordani na kupigana, kama ulivyosema.”

28 Basi, Mose akatoa amri zifuatazo kwa kuhani Eleazari, kwa Yoshua mwana wa Nuni, na kwa viongozi wa jamaa za makabila ya Waisraeli:

29 “Ikiwa watu wa Gadi na wa Reubeni watavuka mto Yordani pamoja nanyi wakiwa na silaha zao chini ya uongozi wa Mwenyezi-Mungu, mkashinda na kuichukua nchi hiyo, basi mtawapa nchi ya Gileadi iwe mali yao.

30 Lakini kama hawatavuka mto Yordani pamoja nanyi na silaha zao, basi watamiliki sehemu ya nchi ya Kanaani pamoja nanyi.”

31 Watu wa Gadi na wa Reubeni wakajibu, “Bwana, sisi tutafanya kama Mwenyezi-Mungu alivyotuambia sisi watumishi wako.

32 Chini ya uongozi wake Mwenyezi-Mungu, tutavuka na silaha zetu mpaka nchini Kanaani, lakini nchi tuliyopewa hapa mashariki ya Yordani itakuwa mali yetu.”

33 Basi, Mose akawapa watu wa makabila ya Gadi na Reubeni na nusu ya kabila la Manase mwana wa Yosefu, nchi yote ya mfalme Sihoni wa Waamori na nchi ya mfalme Ogu wa Bashani pamoja na miji na maeneo yaliyokuwa kandokando ya miji hiyo.

34 Kabila la Reubeni likaijenga miji ya Diboni, Atarothi, Aroeri,

35 Atroth-shofani, Yazeri, Yogbeha,

36 Beth-nimra na Beth-harani, miji yenye ngome na mazizi ya kondoo.

37 Kabila la Gadi lilijenga miji ya Heshboni, Eleale, Kiriathaimu,

38 Nebo na Baal-meoni (majina ya hiyo miji yalibadilishwa), na Sibma. Miji waliyoijenga waliipa majina mengine.

39 Wazawa wa Makiri, mwana wa Manase, waliishambulia nchi ya Gileadi, wakaiteka na kuwafukuza Waamori waliokuwa wanakaa humo.

40 Kwa hiyo, Mose akawapa watu wa ukoo wa Makiri mwana wa Manase, nchi ya Gileadi, nao wakakaa humo.

41 Yairi, wa kabila la Manase, alishambulia vijiji kadhaa vya Gileadi na kuviteka, akavipa jina Hawoth-yairi.

42 Naye Noba aliishambulia na kuiteka Kenathi na vijiji vyake, akauita Noba, jina lake mwenyewe.

33

1 Vifuatavyo ni vituo ambavyo Waisraeli walipiga kambi walipotoka Misri wakiwa katika makundi ya makabila yao chini ya uongozi wa Mose na Aroni.

2 Mose aliandika jina la kila mahali walipopiga kambi, kituo baada ya kituo, kwa agizo la Mwenyezi-Mungu.

3 Waisraeli waliondoka mjini Ramesesi mnamo siku ya kumi na tano ya mwezi wa kwanza, siku moja baada ya Pasaka ya kwanza. Waliondoka kwa uhodari mkubwa mbele ya Wamisri wote,

4 ambao walikuwa wanawazika wazaliwa wao wa kwanza wa kiume aliowaua Mwenyezi-Mungu; kwani Mwenyezi-Mungu alikuwa ameiadhibu hata miungu yao.

5 Basi, Waisraeli waliondoka Ramesesi, wakapiga kambi yao huko Sukothi.

6 Kutoka Sukothi, walipiga kambi yao huko Ethamu, ukingoni mwa jangwa.

7 Kutoka Ethamu, waligeuka na kurudi hadi Pi-hahirothi, mashariki ya Baal-sefoni, wakapiga kambi yao karibu na Migdoli.

8 Waliondoka Pi-hahirothi, wakapita bahari ya Shamu mpaka jangwa la Ethamu; walisafiri jangwani mwendo wa siku tatu, wakapiga kambi yao Mara.

9 Kutoka Mara, walisafiri hadi Elimu; huko Elimu kulikuwa na chemchemi kumi na mbili za maji na mitende sabini, wakapiga kambi yao mahali hapo.

10 Walisafiri kutoka Elimu, wakapiga kambi yao karibu na bahari ya Shamu.

11 Kutoka Bahari ya Shamu walipiga kambi yao katika jangwa la Sini.

12 Kutoka jangwa la Sini, walipiga kambi yao Dofka.

13 Kutoka Dofka walipiga kambi yao huko Alushi.

14 Kutoka Alushi walipiga kambi yao huko Refidimu, ambapo hapakuwa na maji ya kunywa.

15 Waliondoka Refidimu wakapiga kambi yao katika jangwa la Sinai.

16 Kutoka Sinai walipiga kambi yao huko Kibroth-hataava.

17 Kutoka Kibroth-hataava, walipiga kambi yao huko Haserothi.

18 Kutoka Haserothi, walipiga kambi yao huko Rithma.

19 Kutoka Rithma, walipiga kambi yao huko Rimon-perezi.

20 Kutoka Rimon-perezi, walipiga kambi yao huko Libna.

21 Kutoka Libna walipiga kambi yao Risa.

22 Waliondoka Risa, wakapiga kambi yao huko Kehelatha.

23 Kutoka Kehelatha, walipiga kambi yao kwenye Mlima Sheferi.

24 Kutoka Mlima Sheferi walipiga kambi yao huko Harada.

25 Kutoka Harada, walipiga kambi yao huko Makelothi.

26 Kutoka Makelothi, walipiga kambi yao huko Tahathi.

27 Kutoka Tahathi walipiga kambi yao Tera.

28 Kutoka Tera walipiga kambi yao Mithka.

29 Kutoka Mithka, walipiga kambi yao Hashmona.

30 Kutoka Hashmona, walipiga kambi yao Moserothi.

31 Kutoka Moserothi, walipiga kambi yao Bene-yaakani.

32 Kutoka Bene-yaakani, walipiga kambi yao Hor-hagidgadi.

33 Kutoka Hor-hagidgadi, walipiga kambi yao Yot-batha.

34 Kutoka Yot-batha, walipiga kambi yao Abrona.

35 Kutoka Abrona, walipiga kambi yao Esion-geberi.

36 Waliondoka Esion-geberi, wakasafiri na kupiga kambi yao katika jangwa la Sini, (yaani Kadeshi).

37 Kutoka Kadeshi, walipiga kambi yao mlimani Hori, mpakani mwa nchi ya Edomu.

38 Kwa agizo la Mwenyezi-Mungu kuhani Aroni alipanda juu ya Mlima Hori, na huko, akafariki mnamo siku ya kwanza ya mwezi wa tano, mwaka wa arubaini tangu Waisraeli walipotoka nchini Misri.

39 Aroni alikuwa na umri wa miaka 123 alipofariki juu ya Mlima Hori.

40 Mfalme wa Aradi, Mkanaani, aliyekaa Negebu katika nchi ya Kanaani, alipata habari kwamba Waisraeli walikuwa wanakuja.

41 Kutoka Mlima Hori, Waisraeli walipiga kambi yao Salmona.

42 Kutoka Salmona, walipiga kambi yao Punoni.

43 Kutoka Punoni, walipiga kambi yao Obothi.

44 Kutoka Obothi, walipiga kambi yao Iye-abarimu, katika eneo la Moabu.

45 Kutoka Iye-abarimu, walipiga kambi yao Dibon-gadi.

46 Kutoka Dibon-gadi, walisafiri na kupiga kambi yao Almon-diblathaimu.

47 Kutoka Almon-diblathaimu, walisafiri na kupiga kambi yao katika milima ya Abarimu, karibu na Mlima Nebo.

48 Kutoka milima ya Abarimu, walisafiri na kupiga kambi yao katika tambarare za Moabu ngambo ya mto Yordani karibu na Yeriko.

49 Walipiga kambi hiyo karibu na mto Yordani kati ya Beth-yeshimothi na bonde la Abel-shitimu kwenye tambarare za Moabu.

50 Katika tambarare za Moabu, ngambo ya mto Yordani karibu na Yeriko, Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose,

51 “Waambie Waisraeli kwamba mtakapovuka mto Yordani na kuingia katika nchi ya Kanaani,

52 wafukuzeni wenyeji wote wa nchi hiyo mbele yenu. Mtaziharibu sanamu zao zote za mawe na za kusubu na kupabomoa kila mahali pao pa juu pa ibada.

53 Mtaichukua nchi hiyo na kukaa humo kwa sababu nimewapeni muimiliki.

54 Mtaigawanya nchi hiyo kwa kura kufuata familia zenu; eneo kubwa kwa kabila kubwa na eneo dogo kwa kabila dogo.

55 Lakini kama msipowafukuza wenyeji wa nchi hiyo kwanza, basi wale mtakaowaacha watakuwa kama vibanzi machoni mwenu au miiba kila upande, na watawasumbua.

56 Nami nitawafanyeni nyinyi kama nilivyokusudia kuwafanya wao.”

34

1 Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,

2 “Waamuru Waisraeli ukisema: Mtakapoingia Kanaani, nchi ambayo ninawapa iwe nchi yenu, mipaka ya eneo lenu lote itakuwa kama ifuatavyo.

3 Upande wa kusini mpaka wenu utakuwa kutoka jangwa la Sini kupitia upande wa Edomu. Utaanzia mashariki upande wa kusini mwisho wa Bahari ya Chumvi.

4 Kisha utapinda kusini kuelekea pito la Akrabimu na kupitia Sini hadi Kadesh-barnea, upande wa kusini. Kutoka hapo, mpaka utapinda kuelekea kaskazini-magharibi hadi Hasar-adari na kupita hadi Azmoni.

5 Kutoka Azmoni utapinda kuelekea kijito cha Misri kwenye mpaka wa Misri na kuishia bahari ya Mediteranea.

6 “Mpaka wenu wa upande wa magharibi utakuwa bahari ya Mediteranea.

7 “Mpaka wenu wa upande wa kaskazini utakuwa kama ifuatavyo: Kutoka bahari ya Mediteranea, mtatia alama hadi Mlima Hori.

8 Kutoka Mlima Hori mtatia alama hadi pito la Hamathi, na kuendelea hadi Sedadi,

9 na kupita hadi Zifroni na kuishia Hazar-enani; huo utakuwa mpaka wenu wa kaskazini.

10 “Mpaka wenu wa upande wa mashariki mtauweka kutoka Hazar-enani hadi Shefamu.

11 Kutoka Shefamu utaelekea kusini hadi Ribla, mashariki mwa Aini; kisha mpaka huo utakwenda chini hadi mteremko wa mashariki wa ziwa Kinerethi,

12 halafu utateremka kufuata mto Yordani hadi Bahari ya Chumvi; hii ndiyo itakuwa nchi yako kama mpaka ulivyo.”

13 Basi, Mose akawaambia Waisraeli, “Hii ndiyo nchi mtakayoirithi kwa kupiga kura, nchi ambayo Mwenyezi-Mungu ameagiza yapewe makabila tisa na nusu.

14 Kabila la Reubeni na la Gadi, na nusu ya kabila la Manase yamepata urithi wao kulingana na koo zao.

15 Makabila hayo mawili na nusu yamepata urithi wao ngambo ya mto Yordani upande wa mashariki, mkabala wa Yeriko, mawioni.”

16 Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,

17 “Kuhani Eleazari na Yoshua mwana wa Nuni ndio watakaowagawia watu nchi kuwa mali yao.

18 Utachukua pia kiongozi mmoja kutoka kila kabila kusaidia katika ugawaji wa nchi.

19 Haya ndiyo majina yao: Kabila la Yuda, Kalebu mwana wa Yefune.

20 Kabila la Simeoni, Shemueli mwana wa Amihudi.

21 Kabila la Benyamini, Elidadi mwana wa Kisloni.

22 Kabila la Dani, Buki mwana wa Yogli.

23 Kabila la Manase mwanawe Yosefu, Hanieli mwana wa Efodi.

24 Kabila la Efraimu, mwanawe Yosefu, Kemueli mwana wa Shiftani.

25 Kabila la Zebuluni, Elisafani mwana wa Parnaki.

26 Kabila la Isakari, Paltieli mwana wa Azani.

27 Kabila la Asheri, Ahihudi mwana wa Shelomi

28 Kabila la Naftali, Pedaheli mwana wa Amihudi.

29 Hawa ndio watu ambao Mwenyezi-Mungu aliwaamuru wawagawie Waisraeli nchi ya Kanaani kuwa mali yao.”

35

1 Mwenyezi-Mungu aliongea na Mose katika tambarare za Moabu, ngambo ya mto Yordani karibu na Yeriko, akamwambia,

2 “Waamuru Waisraeli kwamba kutokana na urithi watakaomiliki, wawape Walawi miji ya kukaa na sehemu za malisho kandokando ya miji hiyo.

3 Miji hiyo itakuwa yao, nao watakaa humo na malisho yake yatakuwa kwa ajili ya ng'ombe na mifugo yao pamoja na wanyama wao wengine.

4 Malisho ya maeneo mtakayowapa Walawi kandokando ya miji yataenea kila upande umbali wa mita 450 kutoka kwenye kuta za miji hiyo.

5 Kwa hiyo, eneo hilo la malisho litakuwa la mita 900, na litaenea kila upande wa mji, mji wenyewe ukiwa katikati. Eneo hilo litakuwa malisho yao kandokando ya miji yao.

6 Mtawapa Walawi miji sita ya makimbilio ambapo mtu akimuua mwenzake bila kukusudia ataruhusiwa kukimbilia. Pamoja na hiyo, mtawapa miji mingine arubaini na miwili.

7 Jumla ya miji mtakayowapa Walawi itakuwa arubaini na minane; mtawapa miji hiyo pamoja na sehemu za malisho yake.

8 Idadi ya miji mtakayowapa Walawi katika urithi wa Waisraeli itategemea ukubwa wa kabila; kabila kubwa litatoa miji mingi na kabila dogo litatoa michache. Kila kabila litatoa miji yake kwa ajili ya Walawi kulingana na eneo litakalorithi.”

9 Mwenyezi-Mungu akaongea na Mose, akamwambia,

10 Waambie Waisraeli kwamba wakati mtakapovuka mto Yordani na kuingia nchini Kanaani,

11 mtachagua miji itakayokuwa miji ya makimbilio ambamo kama mtu akimuua mwenzake bila kukusudia ataweza kukimbilia.

12 Miji hiyo itakuwa mahali pa kukimbilia usalama ili huyo mwuaji asiuawe na mwenye kulipiza kisasi kabla ya kuhukumiwa na jumuiya.

13 Mtajitengea miji sita kwa ajili ya makimbilio.

14 Kati ya miji hiyo sita mtakayoitenga, mitatu iwe mashariki ya Yordani, na mitatu iwe katika nchi ya Kanaani.

15 Miji hii itakuwa ya makimbilio kwa ajili ya Waisraeli na wageni wa kudumu au wa muda wanaokaa pamoja nao. Mtu yeyote akimuua mwingine bila kukusudia anaweza kukimbilia huko.

16 “Lakini mtu akimpiga mwenzake kwa kitu cha chuma, akafa, mtu huyo ni mwuaji na ni lazima auawe.

17 Mtu yeyote akimpiga mwenzake kwa jiwe, akifa, mtu huyo ni mwuaji, na lazima auawe.

18 Kama akimpiga mwenzake kwa silaha ya mti ambayo yaweza kusababisha kifo, akafa, mtu huyo ni mwuaji, na ni lazima auawe.

19 Jamaa wa karibu wa mtu aliyeuawa atalipiza kisasi. Huyu atakapokutana na huyo mwuaji, atatekeleza hukumu ya kifo.

20 “Hali kadhalika, kama mtu anamchukia mwenzake halafu, akamsukuma au kumtupia kitu kwa kumvizia,

21 au kwa kumpiga ngumi akafa, basi mtu huyo aliyempiga mwenzake ni mwuaji na ni lazima auawe. Jamaa wa karibu wa mtu aliyeuawa atalipiza kisasi atakapokutana naye.

22 “Lakini kama mtu akimsukuma mwenzake kwa ghafla bila chuki au kumtupia kitu bila kumvizia

23 au mtu akirusha jiwe linaloweza kusababisha kifo, akamuua mtu bila kukusudia, ingawa hakuwa adui yake wala hakutaka kumdhuru,

24 basi, jumuiya itaamua kati ya huyo mwuaji na jamaa ya mtu aliyeuawa anayetaka kulipiza kisasi, kulingana na sheria hizi.

25 Jumuiya itamwokoa mtu huyo aliyeua mikononi mwa jamaa ya mtu aliyeuawa, na kumrudisha katika mji wa makimbilio alimokuwa amekimbilia. Atakaa huko mpaka kifo cha kuhani mkuu wa wakati huo aliyeteuliwa kwa kupakwa mafuta matakatifu.

26 Lakini huyo aliyeua akitoka nje ya mji aliokimbilia wakati wowote ule,

27 halafu jamaa ya mtu aliyeuawa akampata nje ya mipaka ya mji huo wa makimbilio akamuua, huyo hatakuwa na hatia ya kuua.

28 Maana huyo aliyeua ni lazima akae ndani ya mji wa makimbilio mpaka kuhani mkuu atakapofariki; lakini baada ya kifo cha kuhani mkuu anaweza kurudi nyumbani.

29 “Sheria hizi zitatumika katika vizazi vyenu vyote, mahali popote mtakapokaa.

30 “Mtu yeyote atakayeua mtu, atahukumiwa kifo kutokana na ushahidi wa mashahidi wawili au zaidi; mtu yeyote hawezi kuhukumiwa kifo kutokana na ushahidi wa mtu mmoja.

31 “Msipokee fidia yoyote kuokoa maisha ya mwuaji aliyepatikana na hatia, akahukumiwa kifo; mtu huyo lazima auawe.

32 Msipokee wala msikubali fidia yoyote kutoka kwa mtu aliyekimbilia mji wa makimbilio ili kumruhusu arudi kukaa nyumbani kwake kabla ya kifo cha kuhani mkuu.

33 Mkifanya hivyo mtakuwa mnaitia unajisi nchi ambayo mnakaa. Umwagaji damu huitia nchi unajisi, na hakuna sadaka iwezayo kuitakasa nchi iliyofanyiwa mauaji isipokuwa kwa kumuua mwuaji huyo.

34 Msiitie unajisi nchi ambayo mnakaa, nchi ambayo mimi ninakaa; maana mimi Mwenyezi-Mungu ninakaa miongoni mwenu Waisraeli.”

36

1 Viongozi wa jamaa katika ukoo wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, mwana wa Yosefu, walikwenda kuzungumza na Mose na viongozi wengine wa koo za Waisraeli.

2 Wakasema, “Bwana wetu, Mwenyezi-Mungu alikuamuru kuwagawia watu wa Israeli nchi kwa kura, kuwa urithi wao; alikuamuru pia uwape binti za Selofehadi ndugu yetu urithi wa baba yao.

3 Lakini wao wakiolewa na Waisraeli wa makabila mengine, urithi wao utatoka kwetu na kuwaendea watu wa kabila watakamoolewa; kwa hiyo urithi wetu sisi utapungua.

4 Katika sikukuu ya ukumbusho urithi wao utahesabiwa pamoja na ule wa kabila watakamoolewa na hivyo kabila letu halitapata urithi huo tena.”

5 Basi, Mose akawapa Waisraeli agizo lifuatalo kutoka kwa Mwenyezi-Mungu, akawaambia, “Watu wa ukoo wa kabila la Yosefu, wamesema ukweli.

6 Na hivi ndivyo anavyoamuru Mwenyezi-Mungu kuhusu binti za Selofehadi; wako huru kuolewa na mtu yeyote wampendaye, lakini waolewe katika kabila lao,

7 ili urithi wa Waisraeli usihamishiwe kwa kabila lingine; kila Mwisraeli atazingatia urithi wa kabila lake.

8 Mwanamke yeyote mwenye urithi katika kabila mojawapo la Israeli ni lazima aolewe na mtu wa kabila lake, ili kila Mwisraeli achukue urithi wa babu zake.

9 Hivyo hapatakuwa na urithi wowote utakaohamishwa kutoka kabila moja hadi jingine. Kila kabila la Waisraeli litashikilia urithi wake.”

10 Binti za Selofehadi walifanya kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.

11 Wote: Mala, Tirza, Hogla, Milka na Noa wakaolewa na binamu zao.

12 Waliolewa katika jamaa za ukoo wa Manase mwana wa Yosefu, na urithi wao ukabaki katika kabila la baba yao.

13 Hizo ndizo amri na maagizo ambayo Mwenyezi-Mungu aliwapa Waisraeli kwa njia ya Mose katika tambarare za Moabu, ngambo ya Mto Yordani karibu na mji wa Yeriko.