1

1 Palikuwa na mtu mmoja nchini Usi, aitwaye Yobu. Mtu huyo alikuwa mwema na mnyofu; mtu mcha Mungu na mwenye kuepukana na uovu.

2 Yobu alikuwa na watoto saba wa kiume na watatu wa kike;

3 alikuwa na kondoo 7,000, ngamia 3,000, jozi 500 za ng'ombe na punda majike 500; na watumishi wengi sana; yeye alikuwa mashuhuri kuliko watu wote huko mashariki.

4 Mara kwa mara, wanawe Yobu walifanya karamu nyumbani kwa kila mmoja wao kwa zamu; waliwaalika dada zao kula na kunywa pamoja nao.

5 Kila baada ya karamu, Yobu aliwaita wanawe ili awatakase. Aliamka asubuhi na mapema baada ya karamu, akatoa tambiko za kuteketezwa kwa ajili ya kila mmoja wao kwani aliwaza, “Huenda wanangu wametenda dhambi na kumtukana Mungu mioyoni mwao.”

6 Basi, ikatokia siku moja malaika wa Mungu walikwenda kukutana mbele ya Mwenyezi-Mungu, naye Shetani, akajitokeza pia pamoja nao.

7 Mwenyezi-Mungu akamwuliza Shetani, “Umetoka wapi wewe?” Naye Shetani akamjibu Mwenyezi-Mungu, “Nimetoka kutembeatembea na kuzungukazunguka duniani.”

8 Mwenyezi-Mungu akamwambia Shetani, “Bila shaka umemtambua mtumishi wangu Yobu. Duniani kote hamna mwingine aliye kama yeye. Yeye ni mtu mnyofu, mcha Mungu na mwenye kujiepusha na uovu.”

9 Shetani akamjibu Mwenyezi-Mungu, “Je, Yobu anamcha Mwenyezi-Mungu bure?

10 Je, si dhahiri kwamba wewe unamlinda pande zote pamoja na jamaa yake na kila kitu alicho nacho? Wewe umembariki na mali yake imeongezeka katika nchi.

11 Lakini sasa, hebu nyosha tu mkono wako uiguse mali yake kama hutaona akikutukana waziwazi!”

12 Mwenyezi-Mungu akamwambia Shetani, “Haya, waweza kufanya chochote uwezacho juu ya mali yake; ila tu yeye mwenyewe usimguse.” Basi, Shetani akaondoka mbele ya Mwenyezi-Mungu.

13 Ikawa siku moja, watoto wa kiume na wa kike wa Yobu walikuwa wanakula na kunywa pamoja nyumbani kwa kaka yao mkubwa.

14 Basi, mtumishi akafika kwa Yobu, akamwambia, “Tulikuwa tunalima kwa majembe ya kukokotwa na ng'ombe. Punda nao walikuwa wanakula hapo karibu.

15 Basi Wasabea wakatuvamia na kuwachukua wanyama na kuwaua watumishi kwa upanga. Mimi peke yangu nimenusurika ili kuja kukuarifu.”

16 Kabla hajamaliza kusema, mwingine akawasili, akasema, “Umeme wa radi umewachoma na kuwateketeza kondoo na watumishi, mimi tu peke yangu nimenusurika ili kuja kukuarifu.”

17 Huyo naye kabla hajamaliza kusema, mwingine akawasili, akasema, “Wakaldayo walijipanga makundi matatu wakashambulia ngamia, wakawachukua, na kuwaua watumishi wako kwa upanga! Mimi peke yangu nimenusurika ili kuja kukuarifu.”

18 Kabla hajamaliza kusema, akaja mwingine, akasema, “Watoto wako wa kiume na wa kike walikuwa wanakula na kunywa divai nyumbani kwa kaka yao mkubwa.

19 Mara kimbunga kikavuma kutoka jangwani, kikaipiga nyumba hiyo kila upande nayo ikawaangukia, na vijana wote wamekufa, mimi peke yangu nimenusurika ili kuja kukuarifu.”

20 Kisha Yobu akasimama, akararua mavazi yake, akanyoa nywele zake, akajitupa chini na kumwabudu Mungu.

21 Akasema, “Uchi nilikuja duniani, uchi nitaondoka duniani; Mwenyezi-Mungu amenipa, Mwenyezi-Mungu amechukua; litukuzwe jina lake Mwenyezi-Mungu.”

22 Katika mambo haya yote Yobu hakutenda dhambi wala hakumfikiria Mungu kuwa ana kosa.

2

1 Ikatokea tena siku nyingine, malaika wa Mungu walikwenda kukutana mbele ya Mwenyezi-Mungu, naye Shetani akajitokeza pia pamoja nao.

2 Mwenyezi-Mungu akamwuliza Shetani, “Umetoka wapi wewe?” Naye Shetani akamjibu Mwenyezi-Mungu, “Nimetoka kutembeatembea na kuzungukazunguka duniani.”

3 Mwenyezi-Mungu akamwambia Shetani, “Je, umemwangalia mtumishi wangu Yobu? Duniani hakuna mwingine aliye kama yeye. Yeye ni mtu mnyofu, mcha Mungu na mwenye kujiepusha na uovu. Yeye yuko imara katika unyofu wake, ingawa wewe umenichochea nimwangamize bure.”

4 Shetani akamjibu Mwenyezi-Mungu, “Ngozi kwa ngozi! Mtu hutoa kila kitu alicho nacho ili aokoe uhai wake.

5 Lakini sasa hebu nyosha mkono wako umguse mwili wake; nakuambia atakutukana waziwazi.”

6 Basi, Mwenyezi-Mungu akamwambia Shetani, “Haya! Waweza kumfanya utakavyo, walakini usimuue.”

7 Hapo Shetani akaondoka mbele ya Mwenyezi-Mungu, akamtesa Yobu kwa madonda mabaya tangu wayo wa mguu wake mpaka utosini mwake.

8 Yobu akatwaa kigae, akajikuna nacho na kuketi kwenye majivu.

9 Mkewe akamwambia, “Bado tu ungali ukishikilia unyofu wako? Mtukane Mungu, ufe.”

10 Yobu akamjibu mkewe, “Wewe unaongea kama wanawake wapumbavu. Tukipokea mema kutoka kwa Mungu, kwa nini tukatae kupokea pia mabaya kutoka kwake?” Katika mambo hayo yote, Yobu hakutamka neno lolote la kumkosea Mungu.

11 Marafiki watatu wa Yobu: Elifazi kutoka Temani, Bildadi kutoka Shua na Sofari kutoka Naamathi, walisikia juu ya maafa yote yaliyompata Yobu. Basi, wakaamua kwa pamoja waende kumpa pole na kumfariji.

12 Walipomwona kwa mbali hawakumtambua. Basi, wakaanza kupaza sauti na kulia; waliyararua mavazi yao, wakarusha mavumbi angani na juu ya vichwa vyao.

13 Kisha wakaketi udongoni pamoja na Yobu kwa siku saba, mchana na usiku, bila kumwambia neno lolote kwani waliyaona mateso yake kuwa makubwa mno.

3

1 Hatimaye Yobu aliamua kuongea, akailaani siku aliyozaliwa.

2 Yobu akasema:

3 “Ilaaniwe siku ile niliyozaliwa; usiku ule iliposemwa, ‘Mwana amechukuliwa mimba’

4 Siku hiyo na iwe giza! Mungu juu asijishughulishe nayo! Wala nuru yoyote isiiangaze!

5 Mauzauza na giza nene yaikumbe, mawingu mazito yaifunike. Giza la mchana liitishe!

6 Usiku huo giza nene liukumbe! Usihesabiwe katika siku za mwaka, wala usitiwe katika idadi ya siku za mwezi.

7 Naam, usiku huo uwe tasa, sauti ya furaha isiingie humo.

8 Walozi wa siku waulaani, watu stadi wa kuligutua dude Lewiyathani waulaani!

9 Nyota zake za pambazuko zififie, utamani kupata mwanga, lakini usipate, wala usione nuru ya pambazuko.

10 Maana usiku huo haukulifunga tumbo la mama, wala kuficha taabu nisizione.

11 Mbona sikufa nilipozaliwa, nikatoka tumboni na kutoweka?

12 Kwa nini mama yangu alinizaa? Kwa nini nikapata kunyonya?

13 Maana ningekuwa nimezikwa, kimya; ningekuwa nimelazwa na kupumzika,

14 pamoja na wafalme na watawala wa dunia, waliojijengea upya magofu yao;

15 ningekuwa pamoja na wakuu waliokuwa na dhahabu, waliojaza nyumba zao fedha tele.

16 Au, mbona sikuwa kama mimba iliyoharibika, naam, kama mtoto aliyezaliwa mfu?

17 Huko kwa wafu waovu hawamsumbui mtu, huko wachovu hupumzika.

18 Huko wafungwa hustarehe pamoja, hawaisikii kamwe sauti ya mnyapara.

19 Wakubwa na wadogo wako huko, nao watumwa wamepata uhuru mbali na bwana zao.

20 Ya nini kumjalia nuru yule aliye taabuni; na uhai yule aliye na huzuni moyoni?

21 Mtu atamaniye kifo lakini hafi; hutafuta kifo kuliko hazina iliyofichika.

22 Mtu kama huyo atashangilia mno na kufurahi, atafurahi atakapokufa na kuzikwa!

23 Ya nini kumjalia uhai mtu ambaye njia zake zimefungwa, mtu ambaye Mungu amemwekea kizuizi?

24 Kwa maana kusononeka ndio mkate wangu, kupiga kite kwangu kunatiririka mithili ya maji.

25 Kile ninachokiogopa kimenipata, ninachokihofia ndicho kilichonikumba.

26 Sina amani wala utulivu; sipumziki, taabu imenijia.”

4

1 Kisha Elifazi yule Mtemani akamjibu Yobu:

2 “Je, mtu akijaribu kukuambia neno utakasirika? Lakini nani awezaye kujizuia kusema?

3 Sikiliza! Wewe umewafundisha wengi, na kuiimarisha mikono ya wanyonge.

4 Maneno yako yamewainua waliokufa moyo, umewaimarisha waliokosa nguvu.

5 Lakini sasa yamekupata, nawe ukakosa subira, yamekugusa, nawe ukafadhaika.

6 Je, kumcha Mungu si ndilo tegemeo lako? Na unyofu wako si ndilo tumaini lako?

7 Fikiri sasa: Nani asiye na hatia ambaye amepata kuangamia? Au, je, waadilifu wamepata kutupwa?

8 Nijuavyo mimi, wapandao uovu na ubaya huvuna hayohayo,

9 Mungu huwaangamiza hao kwa pumzi yake, hao huteketezwa kwa pigo la hasira yake.

10 Waovu hunguruma kama simba mkali, lakini meno yao huvunjwa.

11 Simba mwenye nguvu hufa kwa kukosa mawindo, na watoto wa simba jike hutawanywa!

12 “Siku moja, niliambiwa neno kwa siri, sikio langu lilisikia mnongono wake.

13 Nikiwa katika mawazo ya njozi za usiku, wakati usingizi mzito huwashika watu,

14 nilishikwa na hofu na kutetemeka, mifupa yangu yote ikagonganagongana.

15 Upepo ukapita mbele ya uso wangu, nywele za mwilini mwangu zikajisimamisha.

16 Kitu kilisimama tuli mbele yangu, nilipokitazama sikukitambua kabisa. Kulikuwa na umbo fulani mbele yangu; kulikuwa kimya, kisha nikasikia sauti.

17 Binadamu afaye aweza kuwa mwadilifu mbele ya Mungu? Mtu aweza kuwa safi mbele ya Muumba wake?

18 Hata watumishi wake, Mungu hana imani nao; na malaika wake huwaona wana kosa;

19 sembuse binadamu viumbe vya udongo, watu ambao chanzo chao ni mavumbi, ambao waweza kupondwapondwa kama nondo!

20 Binadamu kwa masaa machache tu waweza kuangamia; huangamia milele bila kuacha hata alama yao!

21 Iwapo uzi unaoshikilia uhai wao ukikatwa wao hufa tena bila kuwa na hekima.

5

1 “Ita sasa, uone kama kuna wa kukuitikia. Ni yupi kati ya watakatifu utakayemwita?

2 Ama kweli hangaiko humuua mpumbavu, na wivu humwangamiza mjinga.

3 Nimepata kuona mpumbavu akifana, lakini ghafla nikayalaani makao yake.

4 Watoto wake hawana usalama; hudhulumiwa mahakamani, na hakuna mtu wa kuwatetea.

5 Mazao yake huliwa na wenye njaa, hata nafaka iliyoota kati ya miiba; wenye tamaa huuonea shauku utajiri wake.

6 Kwa kawaida mateso hayatoki mavumbini wala matatizo hayachipui udongoni.

7 Bali binadamu huzaliwa apate taabu, kama cheche za moto zirukavyo juu.

8 “Kama ningekuwa wewe ningemgeukia Mungu, ningemwekea yeye Mungu kisa changu,

9 yeye atendaye makuu yasiyochunguzika, atendaye maajabu yasiyohesabika.

10 Huinyeshea nchi mvua, hupeleka maji mashambani.

11 Huwainua juu walio wanyonge, wenye kuomboleza huwapa usalama.

12 Huvunja mipango ya wenye hila, matendo yao yasipate mafanikio.

13 Huwanasa wenye hekima kwa werevu wao, mipango ya wajanja huikomesha mara moja.

14 Hao huona giza wakati wa mchana, adhuhuri hupapasapapasa kama vile usiku.

15 Lakini Mungu huwaokoa yatima wasiuawe, huwanyakua fukara mikononi mwa wenye nguvu.

16 Hivyo maskini wanalo tumaini, nao udhalimu hukomeshwa.

17 “Heri mtu yule ambaye Mungu anamrudi! Hivyo usidharau Mungu Mwenye Nguvu anapokuadhibu.

18 Kwani yeye huumiza na pia huuguza; hujeruhi, na kwa mkono wake huponya.

19 Atakuokoa katika maafa zaidi ya mara moja; katika balaa la mwisho, uovu hautakugusa.

20 Wakati wa njaa atakuokoa na kifo, katika mapigano makali atakuokoa.

21 Utakingwa salama na mashambulio ya ulimi, wala hutaogopa maangamizi yajapo.

22 Maangamizi na njaa vijapo, utacheka, wala hutawaogopa wanyama wakali wa nchi.

23 Nawe utaafikiana na mawe ya shambani, na wanyama wakali watakuwa na amani nawe.

24 Utaona nyumbani mwako mna usalama; utakagua mifugo yako utaiona yote ipo.

25 Utaona pia wazawa wako watakuwa wengi, wengi kama nyasi mashambani.

26 Utafariki ukiwa mkongwe mtimilifu, kama mganda wa ngano ya kupurwa iliyoiva vizuri.

27 Basi huu ndio utafiti wetu; tena ni ukweli; uusikie na kuuelewa kwa faida yako.”

6

1 Yobu akamjibu Elifazi:

2 “Laiti mahangaiko yangu yangepimwa uzani wake, mateso yangu yote yakawekwa katika mizani!

3 Yangekuwa mazito kuliko mchanga wa pwani. Ndio maana maneno yangu ni ya kuropoka!

4 Naam, mishale ya Mungu Mwenye Nguvu imenichoma; nafsi yangu imekunywa sumu yake. Vitisho vya Mungu vimenikabili.

5 Je, pundamwitu hulia akiwa na majani, au ng'ombe akiwa na malisho?

6 Je, kitu kisicho na ladha chaweza kuliwa bila chumvi? Je ute wa yai una utamu wowote?

7 Sina hamu ya kuvigusa vyakula hivyo, hivyo ni vyakula vyangu vichukizavyo.”

8 “Laiti ningejaliwa ombi langu, Mungu akanipatia kile ninachotamani:

9 Kwamba angekuwa radhi kunipondaponda, angenyosha mkono wake anikatilie mbali!

10 Hiyo ingekuwa faraja yangu, ningefurahi katika maumivu yasiyo na huruma.

11 Lakini sina nguvu ya kuweza kuendelea; sijui mwisho wangu utakuwaje, nipate kuvumilia.

12 Je, nguvu zangu ni kama za mawe? Au mwili wangu kama shaba?

13 Kweli kwangu hamna cha kunisaidia; msaada wowote umeondolewa kwangu.

14 “Anayekataa kumhurumia rafiki yake, anakataa kumcha Mungu mwenye nguvu.

15 Rafiki zangu wamenidanganya kama kijito, wamenihadaa kama mitaro isiyo na maji.

16 Ambayo imejaa barafu, na theluji imejificha ndani yake.

17 Lakini wakati wa joto hutoweka, wakati wa hari hubaki mito mikavu.

18 Misafara hupotea njia wakitafuta maji, hupanda nyikani na kufia huko.

19 Misafara ya Tema hutafuta tafuta, wasafiri wa Sheba hutumaini.

20 Huchukizwa kwa kutumaini bure, hufika kwenye vijito hivyo na kuudhika.

21 Nyinyi mmekuwa kama vijito hivyo, mwaona balaa yangu na kuogopa.

22 Je, nimesema mnipe zawadi? Au mnitolee rushwa kwa mali zenu?

23 Au mniokoe makuchani mwa adui? Au mnikomboe mkononi mwa wadhalimu?

24 “Nifundisheni, nami nitanyamaza. Nielewesheni jinsi nilivyokosea.

25 Maneno ya kweli yana nguvu kubwa! Lakini makaripio yenu yananikosoa nini?

26 Je, mnadhani kwamba mwaweza kuyakosoa maneno? Maneno ya mtu aliyekata tamaa ni upepo tu.

27 Nyinyi mnathubutu hata kuwapigia yatima kura; mnawapigia bei hata marafiki zenu!

28 Lakini sasa niangalieni tafadhali. Mimi sitasema uongo mbele yenu.

29 Acheni tafadhali, kusiwe na uovu; acheni sasa, kwani mimi ni mnyofu.

30 Je, mnadhani kwamba nimesema uovu? Je, mnafikiri mimi siyatambui machungu?

7

1 “Binadamu anayo magumu duniani, na siku zake ni kama siku za kibarua!

2 Yeye ni kama mtumwa atamaniye kivuli, kama mwajiriwa angojaye kwa hamu mshahara wake.

3 Basi nimepangiwa miezi na miezi ya ubatili, yangu ni majonzi usiku hata usiku.

4 Nilalapo nasema, ‘Nitaamka lini?’ Kwani saa za usiku huwa ndefu sana; nagaagaa kitandani mpaka kuche!

5 Mwili wangu umejaa mabuu na uchafu; ngozi yangu imekauka na kutokwa na usaha wa jipu.

6 Siku zangu zapita kasi kuliko gurudumu la mshonaji, nazo zafikia mwisho wake bila matumaini.

7 “Kumbuka, maisha yangu ni pumzi tu; jicho langu halitaona jema lolote tena.

8 Anayeniona sasa, hataniona tena, punde tu ukinitazama nitakuwa nimetoweka.

9 Kama wingu lififiavyo na kutoweka ndivyo nao watu washukavyo kuzimu bila kurudi.

10 Anayeondoka harudi tena kwa jamaa yake, na pale alipokuwa anaishi husahaulika mara.

11 “Kwa hiyo sitakizuia kinywa changu kuongea; nitasema kwa msongo wa roho yangu, nitalalamika kwa uchungu wa nafsi yangu.

12 Je, mimi ni bahari au dude la baharini hata uniwekee mlinzi?

13 Nikisema, ‘Kitanda kitanipumzisha, malazi yangu yatanipunguzia malalamiko yangu,’

14 wewe waja kunitia hofu kwa ndoto, wanitisha kwa kuniletea maono;

15 hata naona afadhali kujinyonga, naona heri kufa kuliko kupata mateso haya.

16 Nayachukia maisha yangu; sitaishi milele. Niacheni, maana siku zangu ni pumzi tu!

17 Binadamu ni nini hata umjali? Kwa nini hata unajishughulisha naye?

18 Wewe waja kumchunguza kila asubuhi, kila wakati wafika kumjaribu!

19 Utaendelea kuniangalia hata lini, bila kuniacha hata nimeze mate?

20 Kama nikitenda dhambi, yakudhuru nini ewe mkaguzi wa binadamu? Mbona umeniweka kuwa shabaha ya mapigo yako? Je, mimi nimekuwa mzigo kwako?

21 Mbona hunisamehi kosa langu na kuniondolea uovu wangu? Hivi punde nitalazwa chini kaburini, utanitafuta, lakini sitakuwapo tena!”

8

1 Ndipo Bildadi, Mshuhi, akamjibu Yobu:

2 “Utasema mambo haya mpaka lini? Mpaka lini maneno yako yatakuwa matupu kama upepo?

3 Kwani, wadhani Mungu hupotosha haki? Au, je, Mungu Mwenye Nguvu hupotosha ukweli?

4 Kama watoto wako wamemkosea Mungu, yeye amewalipiza matokeo ya uhalifu wao.

5 Kama utamtafuta Mungu ukamsihi huyo Mungu mwenye nguvu,

6 kama wewe u safi moyoni na mnyofu, kweli Mungu atakuja kukusaidia, na kukujalia makao unayostahili.

7 Na ingawa ulianza kuishi kwa unyonge maisha yako ya baadaye yatakuwa ya fahari zaidi.

8 Jifunze tafadhali kwa wale waliotutangulia, zingatia mambo waliyogundua hao wazee.

9 Sisi ni watu wa juzijuzi tu, hatujui kitu; siku zetu duniani ni kivuli kipitacho.

10 Lakini wao watakufunza na kukuambia, mambo waliyopata kuyatoa katika maarifa yao:

11 Mafunjo huota tu penye majimaji, matete hustawi mahali palipo na maji.

12 Hata kama yamechanua na bila kukatwa, yakikosa maji hunyauka kabla ya mimea mingine.

13 Ndivyo walivyo wote wanaomsahau Mungu. Tumaini la wasiomwamini Mungu litapotea.

14 Tegemeo lao huvunjikavunjika, tumaini lao ni utando wa buibui.

15 Wanaegemea nyumba yao lakini haitasimama, huishikilia lakini haidumu.

16 Jua litokapo yeye hustawi; hueneza matawi yake bustanini mwake.

17 Mizizi yake hujisokotasokota kwenye mawe naye aenda kuchunguza ndani ya mwamba.

18 Lakini akiangamizwa kutoka makao yake, hayo yatamkana yakisema: ‘Sijapata kukuona.’

19 Tazama, huo ndio mwisho wa furaha ya mtu huyo, na mahali pao patachipua wengine.

20 “Tazama! Mungu hatamkataa mtu asiye na hatia, wala kuwasaidia waovu.

21 Ila atakijaza kinywa chako kicheko, na midomo yako sauti ya furaha.

22 Wale wakuchukiao wataingiwa na aibu, makao ya waovu yatatoweka kabisa.”

9

1 Kisha Yobu akajibu:

2 “Kweli najua hivyo ndivyo ilivyo. Lakini mtu awezaje kuwa mwema mbele ya Mungu?

3 Kama mtu angethubutu kushindana naye, hataweza kufika mbali; hata kujibu swali moja kati ya elfu.

4 Yeye ni mwenye hekima mno na nguvu nyingi, nani aliyepingana naye, akashinda?

5 Yeye huiondoa milima bila yenyewe kutambua, huibomolea mbali kwa hasira yake.

6 Yeye huitikisa dunia kutoka mahali pake, na nguzo zake zikatetemeka.

7 Huliamuru jua lisichomoze huziziba nyota zisiangaze.

8 Yeye peke yake alizitandaza mbingu, na kuyakanyaga mawimbi ya bahari.

9 Ndiye aliyezifanya nyota angani: Dubu, Orioni, Kilimia, na nyota za kusini.

10 Ndiye atendaye makuu yasiyoeleweka, mambo ya ajabu yasiyo na idadi.

11 Loo! Hupita karibu nami nisimwone, kisha huenda zake bila ya mimi kumtambua.

12 Tazama! Yeye huchukua anachotaka; nani awezaye kumzuia? Nani awezaye kumwuliza: ‘Unafanya nini?’

13 “Mungu hatazuia hasira yake; chini yake wainama kwa hofu Rahabu na wasaidizi wake.

14 Nitawezaje basi kumjibu Mungu? Nitachagua wapi maneno ya kumwambia?

15 Ingawa sina hatia, siwezi kumjibu. Lazima kumwomba anihurumie huyo mshtaki wangu.

16 Hata kama ningemwita naye akajibu, nisingeweza kuamini kuwa ananisikiliza.

17 Yeye huniponda kwa dhoruba; huongeza majeraha yangu bila sababu.

18 Haniachi hata nipumue; maisha yangu huyajaza uchungu.

19 Kama ni kushindana, yeye ana nguvu mno! Na kama ni kutafuta juu ya haki, nani atakayemleta mahakamani?

20 Ingawa sina hatia, maneno yangu yenyewe yangenihukumu; ingawa sina lawama, angenithibitisha kuwa mpotovu.

21 Sina lawama, lakini sijithamini. Nayachukia maisha yangu.

22 Yote ni mamoja, kwa hiyo nasema; Mungu huwaangamiza wema na waovu.

23 Maafa yaletapo kifo cha ghafla, huchekelea balaa la wasio na hatia.

24 Nchi ikitiwa watu waovu katika utawala wa mwovu, Mungu huyafumba macho ya mahakimu wake! Kama si yeye afanyaye hivyo, ni nani basi?

25 “Siku zangu zaenda mbio kuliko mpiga mbio; zinakimbia bila kuona faida.

26 Zapita kasi kama mashua ya matete; kama tai anayerukia mawindo yake.

27 Nasema: ‘Nitasahau lalamiko langu, niondoe uso wangu wa huzuni na kuwa na furaha!’

28 Lakini nayaogopa maumivu yangu yote, kwani najua Mungu hataniona kuwa sina hatia.

29 Ikiwa nitahukumiwa kuwa na hatia, ya nini basi nijisumbue bure?

30 Hata kama nikitawadha kwa theluji, na kujitakasa mikono kwa sabuni,

31 hata hivyo, atanitumbukiza shimoni kwenye uchafu, na mavazi yangu yataniona kuwa kinyaa.

32 Mungu si mtu kama mimi niweze kumjibu, hata tuweze kwenda mahakamani pamoja.

33 Hakuna msuluhishi kati yetu, ambaye angeamua kati yetu sisi wawili.

34 Mungu na aniondolee hiyo fimbo ya kunipiga, na kitisho chake kisinitie hofu!

35 Hapo ningeweza kusema bila kumwogopa; kwani sivyo nilivyo nafsini mwangu.

10

1 “Nayachukia maisha yangu! Malalamiko yangu nitayasema bila kizuizi. Nitasema kwa uchungu wa moyo wangu.

2 Nitamwambia Mungu: Usinihukumu. Nijulishe kisa cha kupingana nami.

3 Je, ni sawa kwako kunionea, kuidharau kazi ya mikono yako na kuipendelea mipango ya waovu?

4 Je, una macho kama ya binadamu? Je, waona kama binadamu aonavyo?

5 Je, siku zako ni kama za binadamu? Au miaka yako kama ya binadamu,

6 hata uuchunguze uovu wangu, na kuitafuta dhambi yangu?

7 Wewe wajua kwamba mimi sina hatia, na hakuna wa kuniokoa mikononi mwako.

8 Mikono yako iliniunda na kuniumba, lakini sasa wageuka kuniangamiza.

9 Kumbuka kwamba uliniumba kwa udongo. Je, utanirudisha tena mavumbini?

10 Je, si wewe uliyenimimina kama maziwa, na kunigandisha kama jibini?

11 Uliuumba mwili wangu kwa mifupa na mishipa, ukaifunika mifupa yangu kwa nyama na ngozi.

12 Umenijalia uhai na fadhili, uangalifu wako umeisalimisha nafsi yangu.

13 Hata hivyo mambo haya uliyaficha moyoni. Lakini najua kuwa hiyo ilikuwa nia yako.

14 Ulikuwa unangojea uone kama nitatenda dhambi, ili ukatae kunisamehe uovu wangu.

15 Kama mimi ni mwovu, ole wangu! Kama mimi ni mwadilifu, siwezi kujisifu; kwani nimejaa fedheha, nikiyatazama mateso yangu.

16 Nikiinua kichwa tu waniwinda kama simba na kuniponda tena kwa maajabu yako.

17 Kila mara unao ushahidi dhidi yangu; waiongeza hasira yako dhidi yangu, waniletea maadui wapya wanishambulie.

18 “Ee Mungu, kwa nini ulinitoa tumboni mwa mama? Afadhali ningekufa kabla ya watu kuniona.

19 Ningepelekwa moja kwa moja kaburini, nikawa kama mtu asiyepata kuwako.

20 Je, siku za maisha yangu si chache? Niachie nipate faraja kidogo,

21 kabla ya kwenda huko ambako sitarudi, huko kwenye nchi ya huzuni na giza nene;

22 nchi ya huzuni na fujo, ambako mwanga wake ni kama giza.”

11

1 Kisha Sofari, Mnaamathi, akamjibu Yobu:

2 “Je, wingi huu wa maneno uachwe tu bila kujibiwa? Je, mtu wa maneno mengi aonesha kuwa hana hatia?

3 Je, kuropoka kwako kutanyamazisha watu? Na kama ukidhihaki, je, hamna atakayekuaibisha?

4 Wewe wadai: ‘Ninachosema ni kweli, naam, sina lawama mbele ya Mungu.’

5 Laiti Mungu angefungua kinywa chake akatoa sauti yake kukujibu!

6 Angekueleza siri za hekima, maana yeye ni mwingi wa maarifa. Jua kwamba Mungu hakuhesabu makosa yako yote.

7 “Je, unaweza kugundua siri zake Mungu na kujua ukomo wake yeye Mungu mwenye nguvu?

8 Ukuu wake wapita mbingu, wewe waweza nini? Kimo chake chapita Kuzimu, wewe waweza kujua nini?

9 Ukuu huo wapita marefu ya dunia, wapita mapana ya bahari.

10 Kama Mungu akipita, akamfunga mtu na kumhukumu, nani awezaye kumzuia?

11 Mungu anajua watu wasiofaa; akiona maovu yeye huchukua hatua.

12 “Mpumbavu hawezi kuwa na maarifa, pundamwitu ni pundamwitu tu.

13 “Yobu, ukiufanya moyo wako mnyofu, utainua mikono yako kumwomba Mungu!

14 Kama una uovu, utupilie mbali. Usikubali ubaya uwemo nyumbani mwako.

15 Hapo utajitokeza mbele ya watu bila lawama, utakuwa thabiti bila kuwa na hofu.

16 Utazisahau taabu zako zote; utazikumbuka tu kama mafuriko yaliyopita.

17 Maisha yako yatangaa kuliko jua la adhuhuri, giza lake litabadilika kuwa mngao wa pambazuko.

18 Utakuwa na ujasiri maana lipo tumaini; utalindwa na kupumzika salama.

19 Utalala bila kuogopeshwa na mtu; watu wengi watakuomba msaada.

20 Lakini waovu macho yao yatafifia, njia zote za kutorokea zitawapotea; tumaini lao la mwisho ni kukata roho!”

12

1 Ndipo Yobu akajibu:

2 “Sawa! Nyinyi ni watu wa hekima. Hekima itakufa wakati ule mtakapokufa.

3 Mimi nami ni mwelewa kama nyinyi. Mimi si mtu duni kuliko nyinyi. Yote mliyosema kila mtu anajua.

4 Nimekuwa kichekesho kwa rafiki zangu: Mimi niliyemwomba Mungu na akanijibu; mimi niliye mwadilifu na bila lawama, nimekuwa kichekesho kwa watu.

5 Mtu anayestarehe hudharau msiba; kwake, msiba huwajia wale wanaoteleza.

6 Makao ya wanyanganyi yana amani; wenye kumchokoza Mungu wako salama, nguvu yao ni mungu wao.

7 Lakini waulize wanyama nao watakufunza; waulize ndege nao watakuambia.

8 Au iulize mimea nayo itakufundisha; sema na samaki nao watakuarifu.

9 Nani kati ya viumbe hivyo, asiyejua kwamba Mwenyezi-Mungu ametenda hayo?

10 Uhai wa kila kiumbe hai umo mikononi mwake; kadhalika na pumzi ya uhai wa binadamu.

11 Je, sikio haliyapimi maneno kama ulimi uonjavyo chakula?

12 Hekima iko kwa watu wazee, maarifa kwao walioishi muda mrefu.

13 Lakini hekima na uwezo ni vyake Mungu, yeye ana maarifa na ujuzi.

14 Akibomoa, hakuna awezaye kujenga upya; akimfunga mtu, hakuna awezaye kumfungua.

15 Akizuia mvua, twapata ukame; akiifungulia, nchi hupata mafuriko.

16 Yeye ana nguvu na hekima; wanaodanganywa na wanaodanganya ni wake.

17 Huwaacha washauri waende zao uchi, huwafanya waamuzi kuwa wapumbavu.

18 Huwavua wafalme vilemba vyao; na kuwafunga viunoni kamba za wafungwa;

19 Huwaacha makuhani waende uchi; na kuwaangusha wenye nguvu.

20 Huwanyanganya washauri kipawa chao cha kuongea, huwapokonya wazee hekima yao.

21 Huwamwagia wakuu aibu, huwaondolea wenye uwezo nguvu zao.

22 Huvifunua vilindi vya giza, na kuleta mwangani yaliyokuwa gizani.

23 Huyakuza mataifa kisha huyaangamiza, huyafanya yapanuke kisha huyatawanya.

24 Huwaondolea viongozi wa watu ujuzi wao, huwafanya watangetange nyikani kusiko na njia,

25 wakapapasapapasa gizani kusiko na mwanga; na kuwafanya wapepesuke kama walevi.

13

1 “Tazama, hayo yote nimeyaona kwa macho yangu; nimeyasikia kwa masikio yangu mwenyewe na kuelewa.

2 Yote mnayoyajua, mimi pia nayajua. Mimi si mtu duni kuliko nyinyi.

3 Lakini ningependa kusema na Mungu mwenye nguvu, natamani kujitetea mbele zake Mungu.

4 Lakini nyinyi mnaupakaa uongo chokaa; nyinyi nyote ni waganga wasiofaa kitu.

5 Laiti mngekaa kimya kabisa, ikafikiriwa kwamba mna hekima!

6 Sikilizeni basi hoja yangu, nisikilizeni ninapojitetea.

7 Je, mnadhani mwamtumikia Mungu kwa kusema uongo? Mnafikiri kusema kwa hila kunamfaa yeye?

8 Je, mnajaribu kumpendelea Mungu? Je, mtamtetea Mungu mahakamani?

9 Je, akiwakagua nyinyi mtapona? Au mnadhani mnaweza kumdanganya Mungu kama watu?

10 Hakika yeye atawakemea kama mkionesha upendeleo kwa siri.

11 Je, fahari yake haiwatishi? Je, hampatwi na hofu juu yake?

12 Misemo yenu ni methali za majivu, hoja zenu ni ngome za udongo.

13 “Nyamazeni, nami niongee. Yanipate yatakayonipata.

14 Niko tayari hata kuhatarisha maisha yangu;

15 Mungu aniue akitaka, sina la kupoteza, hata hivyo nitautetea mwenendo wangu mbele yake.

16 Kama nikifaulu hapo nitakuwa nimeshinda, maana mtu mwovu hawezi kwenda mbele yake.

17 Sikilizeni kwa makini maneno yangu, maelezo yangu na yatue masikioni mwenu.

18 Kesi yangu nimeiandaa vilivyo, nina hakika mimi sina hatia.

19 “Nani atakayeipinga hoja yangu? Niko tayari kunyamaza na kufa.

20 Mungu wangu, nijalie tu haya mawili, nami sitajificha mbali na wewe:

21 Kwanza uniondolee mkono wako unaonipiga, na usiniangamize kwa kitisho chako.

22 “Uanze kutoa hoja yako nami nikujibu. Au mimi nianze, nawe unijibu.

23 Makosa na dhambi zangu ni ngapi? Nijulishe hatia na dhambi yangu.

24 “Mbona unaugeuza uso wako mbali nami? Kwa nini unanitendea kama adui yako?

25 Je, utalitisha jani linalopeperushwa, au kuyakimbiza makapi?

26 Wewe umetoa mashtaka makali dhidi yangu, na kunibebesha dhambi za ujana wangu.

27 Wanifunga minyororo miguuni, wazichungulia hatua zangu zote, na nyayo zangu umeziwekea kikomo.

28 Nami naishia kama mti uliooza, mithili ya vazi lililoliwa na nondo.

14

1 “Mtu ni mtoto tu wa mwanamke; huishi siku chache tena zilizojaa taabu.

2 Huchanua kama ua, kisha hunyauka. Hukimbia kama kivuli na kutoweka.

3 Ee Mungu, kwa nini unajali hata kumwangalia na kuanza kuhojiana naye?

4 Nani awezaye kutoa kitu kisafi kutoka kitu kichafu? Hakuna anayeweza.

5 Siku za kuishi binadamu zimepimwa; ee, Mungu umeipanga idadi ya miezi yake; hawezi kupita kikomo ulichomwekea.

6 Angalia pembeni basi, umwache; ili apate kufurahia siku zake kama kibarua.

7 Maana mti ukikatwa lipo tumaini la kuota, waweza kuchipua tena.

8 Japo mizizi yake itazeeka udongoni, na shina lake kufia ardhini,

9 lakini kwa harufu tu ya maji utachipua; utatoa matawi kama chipukizi.

10 Lakini mtu hufa na huo ndio mwisho wake. Akisha toa roho anabakiwa na nini tena?

11 “Kama vile maji yakaukavyo ziwani, na mto unavyokoma kutiririka,

12 ndivyo anavyokufa mtu, wala haamki tena; hataamka tena wala kugutuka, hata hapo mbingu zitakapotoweka.

13 “Laiti ungenificha kuzimu; ungenificha hadi ghadhabu yako ipoe; nao muda ulionipimia ukiisha ungenikumbuka.

14 Je, mtu akifa anaweza kuishi tena? Siku zangu zote za kazi ningekungoja hadi wakati wa kufunguliwa ufike.

15 Hapo ungeniita, nami ningeitika, wakati ungetaka kuniona mimi kiumbe chako.

16 Ndipo ungeweza kuzihesabu hatua zangu, ungeacha kuzichunguza dhambi zangu.

17 Makosa yangu yangefungiwa katika mfuko, nawe ungeufunika uovu wangu.

18 “Lakini milima huanguka majabali hungoka mahali pake.

19 Mtiririko wa maji hula miamba, mvua kubwa hufanya mmomonyoko wa ardhi. Ndivyo nawe unavyoharibu tumaini la binadamu.

20 Wewe wamwangusha binadamu, naye akatoweka milele; waubadilisha uso wake na kumtupilia mbali.

21 Watoto wake wakiheshimika, yeye hana habari. Wakiporomoshwa, yeye haoni kabisa.

22 Huhisi tu maumivu ya mwili wake, na kuomboleza tu hali yake mbaya.”

15

1 Kisha Elifazi, Mtemani, akajibu:

2 “Je, mtu wa hekima hujibu kwa maneno ya upuuzi? Je, mtu huyo amejaa maneno matupu?

3 Je, mwenye hekima hujitetea kwa maneno yasiyofaa, au kwa maneno yasiyo na maana?

4 Lakini wewe unapuuza uchaji wa Mungu; na kuzuia kutafakari mbele ya Mungu.

5 Uovu wako ndio unaokifundisha kinywa chako, nawe wachagua kusema kama wadanganyifu.

6 Maneno yako mwenyewe yanakuhukumu, sio mimi; matamshi yako yashuhudia dhidi yako.

7 Je, wewe ni mtu wa kwanza kuzaliwa? Je, wewe ulizaliwa kabla ya kuweko vilima?

8 Je, ulipata kuweko katika halmashauri ya Mungu? au, wewe ndiwe peke yako mwenye hekima?

9 Unajua kitu gani tusichokijua sisi? Unafahamu kitu gani tusichokifahamu sisi?

10 Miongoni mwetu wapo wazee wenye hekima, wenye miaka mingi kuliko baba yako.

11 Je, faraja anazokupa Mungu ni ndogo mno? Au je, neno lake la upole kwako si kitu?

12 Mbona moyo unakusukuma kukasirika na kutoa macho makali,

13 hata kumwasi Mungu na kusema maneno mabaya kama hayo?

14 Mtu ni nini hata aweze kuwa mwadilifu? au yule aliyezaliwa na mwanamke hata aweze kuwa mwema?

15 Ikiwa Mungu hawaamini hata watakatifu wake, nazo mbingu si safi mbele yake,

16 sembuse binadamu aliye kinyaa na mpotovu binadamu atendaye uovu kama kunywa maji!

17 “Sasa nisikilize, nami nitakuonesha, nitakuambia yale niliyoyaona,

18 mafundisho ya wenye hekima, mambo ambayo wazee wao hawakuyaficha,

19 ambao Mungu aliwapa hiyo nchi peke yao, wala hakuna mgeni aliyepita miongoni mwao.

20 Mwovu atateseka kwa maumivu siku zote, miaka yote waliyopangiwa wakatili.

21 Sauti za vitisho zitampigia kelele masikioni, anapodhani amestawi mwangamizi atamvamia.

22 Mwovu hana tumaini la kutoka gizani; mwisho wake ni kufa kwa upanga.

23 Hutangatanga kutafuta chakula, akisema, ‘Kiko wapi?’ Ajua kwamba siku ya giza inamkaribia.

24 Taabu na uchungu, vyamtisha; vyamkabili kama jeshi la mfalme anayeshambulia.

25 Kwa sababu amenyosha mkono wake dhidi ya Mungu; akadiriki kumpinga huyo Mungu mwenye nguvu;

26 alikimbia kwa kiburi kumshambulia, huku ana ngao yenye mafundo makubwa.

27 Uso wake ameunenepesha kwa mafuta, na kiuno chake kimejaa mafuta.

28 Ameishi katika miji iliyoachwa tupu, katika nyumba zisizokaliwa na mtu; nyumba zilizotakiwa ziwe lundo la uharibifu.

29 Mtu huyo kamwe hatakuwa tajiri; wala utajiri wake hautadumu duniani.

30 Hatalikwepa giza la kifo. Ndimi za moto zitakausha chipukizi zake, maua yake yatapeperushwa na upepo.

31 Heri aache kutumainia upuuzi na kujidanganya, maana upuuzi ndio utakaokuwa tuzo lake.

32 Atalipwa kikamilifu kabla ya kufa kwake, na wazawa wake hawatadumu.

33 Atakuwa kama mzabibu unaopukutisha zabibu mbichi, kama mzeituni unaoangusha maua yake.

34 Wote wasiomcha Mungu hawatapata watoto, moto utateketeza mahema ya wala rushwa.

35 Wanatunga udanganyifu na kuzaa uovu. Mioyo yao hupanga udanganyifu.”

16

1 Hapo Yobu akajibu:

2 “Mambo kama hayo nimeyasikia mengi; nyinyi ni wafariji duni kabisa!

3 Mwisho wa maneno haya matupu ni lini? Au ni kitu gani kinachowachochea kujibu?

4 Kama nyinyi mngekuwa mimi, na mimi nyinyi, ningeweza kusema kama nyinyi ningeweza kubuni maneno dhidi yenu, na kutikisa kichwa changu.

5 Ningeweza kuwatia moyo kwa maneno yangu, na maneno yangu ya faraja yangewatuliza.

6 “Lakini nikisema maumivu yangu hayatulii, na nikikaa kimya hayaondoki.

7 Kweli Mungu amenichakaza ameharibu kila kitu karibu nami.

8 Amenifanya ninyauke, na huo ni ushindi dhidi yangu. Kukonda kwangu kumenikabili na kushuhudia dhidi yangu.

9 Amenirarua kwa hasira na kunichukia; amenisagia meno; na adui yangu ananikodolea macho.

10 Watu wananidhihaki na kunicheka; makundi kwa makundi hunizunguka, na kunipiga makofi mashavuni.

11 Mungu amenitia mikononi mwa wajeuri, na kunitupa mikononi mwa waovu.

12 Nilikuwa nimestarehe, lakini akanivunjavunja, alinikaba shingo na kunipasua vipandevipande; alinifanya shabaha ya mishale yake,

13 akanipiga mishale kutoka kila upande. Amenipasua figo bila huruma, na nyongo yangu akaimwaga chini.

14 Hunivunja na kunipiga tena na tena; hunishambulia kama askari.

15 “Nimejishonea mavazi ya gunia, fahari yangu nimeibwaga mavumbini.

16 Uso wangu ni mwekundu kwa kulia, kope zangu zimekuwa nyeusi ti;

17 ingawa sijafanya dhuluma kwa mkono wangu, na sala zangu kwa Mungu ni safi.

18 “Ewe dunia, usiifunike damu yangu iliyomwagika; kilio changu kienee kila mahali.

19 Nina hakika ninaye shahidi wangu mbinguni, mwenye kunitetea yuko huko juu.

20 Rafiki zangu wanidharau; nabubujika machozi kumwomba Mungu.

21 Laiti mtu angenitetea mbele ya Mungu, kama ifanyikavyo duniani kati za watu wawili.

22 Naam, miaka yangu ni michache, nami nitakwenda huko ambako sitarudi.

17

1 “Nimevunjika moyo, siku zangu zimekwisha, kaburi langu liko tayari.

2 Kweli wanaonidhihaki wamenizunguka, dhihaka zao naziona dhahiri.

3 “Ee Mungu, uwe mdhamini wangu mbele yako, maana hakuna mwingine wa kunidhamini.

4 Maadamu umezifumba akili za rafiki zangu; usiwaache basi wanishinde.

5 Mtu anayewasaliti rafiki zake kwa faida watoto wake watakufa macho.

6 “Nimefanywa kuwa kichekesho kwa watu nimekuwa mtu wa kutemewa mate.

7 Macho yangu yamefifia kwa uchungu; viungo vyangu vyote vimekuwa kama kivuli.

8 Wanyofu wanaduwaa waonapo balaa langu, nao wasio na hatia hujichochea dhidi ya mtu wanayedhani hamchi Mungu.

9 Hata hivyo, mnyofu hushikilia msimamo wake, mtu atendaye mema huzidi kuwa na nguvu zaidi.

10 Lakini nyinyi njoni, njoni nyote tena, kwenu sitampata mwenye hekima hata mmoja.

11 “Siku zangu zimekwisha, mipango yangu imevunjwa; matazamio ya moyo wangu yametoweka.

12 Kwa hao rafiki zangu usiku ni mchana; je, ndio kusema mna mwanga gizani humu?

13 Kwa vile Kuzimu ndio nyumba yangu, na makao yangu yamo humo gizani;

14 kama naliita kaburi ‘baba yangu’ na buu, ‘mama yangu’ au ‘dada yangu’,

15 je, nimebakiwa na tumaini gani? Ni nani awezaye kuona tumaini hilo?

16 Tazamio langu litashuka nami kuzimu! Tutateremka sote wawili hadi huko mavumbini!”

18

1 Kisha Bildadi, Mshuhi, akajibu:

2 “Utawinda maneno ya kusema hadi lini? Tafakari vizuri nasi tutasema.

3 Kwa nini unatufanya kama ng'ombe? Mbona unatuona sisi kuwa wapumbavu?

4 Wewe unajirarua mwenyewe kwa hasira zako. Kwani, dunia itaachwa tupu kwa ajili yako au miamba ihamishwe toka mahali pake?

5 “Naam, mwanga wa mtu mwovu utazimishwa; mwali wa moto wake hautangaa.

6 Nyumbani kwake mwanga ni giza, taa inayomwangazia itazimwa.

7 Hatua zake ndefu zitafupishwa; mipango yake itamwangusha chini.

8 Nyayo zake mwenyewe zitamtia mtegoni; kila akitembea anakumbana na shimo.

9 Mtego humkamata kisiginoni, tanzi humbana kabisa.

10 Amefichiwa kitanzi ardhini; ametegewa mtego njiani mwake.

11 Hofu kuu humtisha kila upande, humfuata katika kila hatua yake.

12 Alikuwa na nguvu, lakini sasa njaa imembana; maafa yako tayari kumwangusha.

13 “Ugonjwa mbaya unakula ngozi yake, maradhi ya kifo hula viungo vyake.

14 Anangolewa katika nyumba aliyoitegemea, na kupelekwa kwa mfalme wa vitisho.

15 Nyumba yake tupu, wengine wataishi humo; madini ya kiberiti yametawanywa katika makao yake.

16 Yeye ni kama mti uliokauka mizizi, matawi yake juu yamenyauka.

17 Nchini hakuna atakayemkumbuka; jina lake halitatamkwa tena barabarani.

18 Ameondolewa mwangani akatupwa gizani; amefukuzwa mbali kutoka duniani.

19 Hana watoto wala wajukuu; hakuna aliyesalia katika makao yake.

20 Watu wa magharibi wameshangazwa na yaliyompata, hofu imewakumba watu wa mashariki.

21 Hayo ndio yanayowapata wasiomjali Mungu; hapo ndipo mahali pa wasiomjua Mungu.”

19

1 Kisha Yobu akajibu:

2 “Mtaendelea kunitesa mpaka lini, na kunivunjavunja kwa maneno?

3 Mara hizi zote kumi mmenishutumu. Je, hamwoni aibu kunitendea vibaya?

4 Hata kama ingekuwa nimekosa kweli, kosa langu lanihusu mimi mwenyewe.

5 Mnaishusha hadhi yangu mpate kujikuza; mnanilaumu kwa kunyenyekezwa kwangu.

6 Jueni kwamba Mungu amenitendea vibaya, na kuninasa katika wavu wake.

7 Tazama napiga yowe: ‘Dhuluma!’ Lakini sijibiwi. Naita kwa sauti kubwa, lakini sipati haki yangu.

8 Njia yangu ameiziba kwa ukuta ili nisipite amezitia giza njia zangu.

9 Amenivua fahari yangu; ameiondoa taji yangu kichwani.

10 Amenivunja pande zote, nami nimekwisha; tumaini langu amelingoa kama mti.

11 Ameichochea ghadhabu yake dhidi yangu; ameniona kuwa kama adui yake.

12 Majeshi yake yanijia kwa pamoja; yametengeneza njia ya kuja kwangu, yamepiga kambi kuizunguka nyumba yangu.

13 Mungu amewaweka ndugu zangu mbali nami; rafiki zangu wakuu wamenitoroka kabisa.

14 Jamaa zangu na marafiki hawanisaidii tena.

15 Wageni nyumbani mwangu wamenisahau; watumishi wangu wa kike waniona kuwa mgeni. Mimi nimekuwa kwao mtu wasiyemjua.

16 Namwita mtumishi wangu lakini haitikii, ninalazimika kumsihi sana kwa maneno.

17 Nimekuwa kinyaa kwa mke wangu; chukizo kwa ndugu zangu mwenyewe.

18 Hata watoto wadogo hunidharau, mara ninapojitokeza wao hunizomea.

19 “Rafiki zangu wakuu wanachukizwa nami, wale niliokuwa nikiwapenda wamenipa kisogo.

20 Mwili wangu umebakia tu mifupa na ngozi, nimeponea chupuchupu baada ya kupoteza yote.

21 Nioneeni huruma, nioneeni huruma enyi rafiki zangu; maana mkono wa Mungu umenifinya.

22 Kwa nini mnanifuatia kama Mungu? Mbona hamtosheki na mwili wangu?

23 “Laiti maneno yangu yangeandikwa! Laiti yangeandikwa kitabuni!

24 Laiti yangechorwa kwa chuma na risasi juu ya jiwe ili yadumu!

25 Najua wazi Mkombozi wangu anaishi, mwishowe yeye atanipa haki yangu hapahapa duniani.

26 Na baada ya ngozi yangu kuharibiwa hivyo, nitamwona Mungu kwa macho yangu mwenyewe.

27 Mimi mwenyewe nitakutana naye; mimi mwenyewe na si mwingine nitamwona kwa macho.

28 “Nyinyi mwaweza kujisemea: ‘Tutamfuatia namna gani?

29 Tutapataje kwake kisa cha kumshtaki?’ Lakini tahadharini na adhabu. Chuki yenu yaweza kuwaletea kifo! Mnapaswa kujua: Mungu peke yake ndiye hakimu.”

20

1 Kisha Sofari, Mnaamathi, akajibu:

2 “Fikira zangu zanifanya nikujibu, wala siwezi kujizuia tena.

3 Nasikia maonyo nisiyoweza kuvumilia, lakini akili yangu yanisukuma nijibu.

4 “Wewe labda umesahau jambo hili: Kwamba tangu zamani Mungu alipomuumba mtu duniani,

5 mwovu atajiona ameshinda kwa muda tu, furaha yake asiyemcha Mungu ni ya muda mfupi tu!

6 Mwovu aweza kufana hata kufikia mbingu, kichwa chake kikafika kwenye mawingu,

7 lakini atatupiliwa mbali kama mavi yake. Waliopata kumjua watajiuliza: ‘Yuko wapi?’

8 Atatoweka kama ndoto, asionekane tena, atafutika kama maono ya usiku.

9 Aliyemwona, hatamwona tena, wala pale alipoishi hapatatambuliwa tena.

10 Yeye mwenyewe itambidi kurudisha mali yake yote, watoto wake wataomba huruma kwa maskini.

11 Japo alijisikia amejaa nguvu za ujana, lakini zote zitalala pamoja naye mavumbini.

12 “Mdomoni mwake uovu ni mtamu kama sukari, anauficha chini ya ulimi wake;

13 hataki kabisa kuuachilia, bali anaushikilia kinywani mwake.

14 Lakini ufikapo tumboni huwa mchungu, mkali kama sumu ya nyoka.

15 Mwovu humeza mali haramu na kuitapika; Mungu huitoa tumboni mwake.

16 Anachonyonya mtu mwovu ni sumu ya nyoka; atauawa kwa kuumwa na nyoka.

17 Hataishi kuiona mitiririko ya fanaka, wala vijito vya mafanikio na utajiri.

18 Matunda ya jasho lake atayaachilia, hatakuwa na uwezo wa kuyaonja,

19 kwa sababu amewaangamiza maskini na kuwaacha, amenyakua nyumba ambazo hakuzijenga.

20 “Kwa vile ulafi wake hauna mwisho, hataweza kuokoa chochote anachothamini.

21 Baada ya kula hakuacha hata makombo, kwa hiyo fanaka yake yote haitadumu.

22 Kileleni mwa fanaka dhiki itamvamia, balaa itamkumba kwa nguvu zote.

23 Akiwa anajishughulisha kushibisha tumbo, Mungu atamletea ghadhabu yake imtiririkie kama chakula chake.

24 Labda ataweza kuepa upanga wa chuma, kumbe atachomwa na upanga wa shaba.

25 Mshale utachomolewa kutoka mwilini mwake; ncha yake itatolewa mgongoni mwake ikingaa, vitisho vya kifo vitamvamia.

26 Hazina zake zitaharibiwa, moto wa ajabu utamteketeza; kilichobaki nyumbani mwake kitateketezwa.

27 Mbingu zitaufichua uovu wake, dunia itajitokeza kumshutumu.

28 Mali zake zitanyakuliwa katika siku ya ghadhabu ya Mungu.

29 Hicho ndicho apewacho mtu mwovu kutoka kwa Mungu, ndicho mwovu alichopangiwa na Mungu.”

21

1 Kisha Yobu akajibu:

2 “Sikilizeni kwa makini maneno yangu; na hiyo iwe ndiyo faraja yenu.

3 Nivumilieni, nami nitasema, na nikisha sema endeleeni kunidhihaki.

4 Je, mimi namlalamikia binadamu? Ya nini basi, nikose uvumilivu?

5 Niangalieni, nanyi mshangae, fumbeni mdomo kwa mkono.

6 Nikifikiri yaliyonipata nafadhaika nafa ganzi mwilini kwa hofu.

7 Kwa nini basi waovu wanaishi bado? Mbona nguvu zao zaongezeka hata uzeeni?

8 Huwaona watoto wao wakifanikiwa; na wazawa wao wakipata nguvu.

9 Kwao kila kitu ni salama bila hofu; wala kiboko cha Mungu hakiwafikii.

10 Naam, ng'ombe wao wote huongezeka, huzaa bila matatizo yoyote.

11 Watoto wao wachanga huwatembeza kama kundi; na watoto wao hucheza ngoma;

12 hucheza muziki wa ngoma na vinubi, na kufurahia sauti ya filimbi.

13 Huishi maisha ya fanaka kisha hushuka kwa amani kuzimu.

14 Humwambia Mungu, ‘Usitusumbue! Hatutaki kujua matakwa yako.

15 Mungu Mwenye Nguvu ni nini hata tumtumikie? Tunapata faida gani tukimwomba dua?’

16 Kufanikiwa kwao si kuko mikononi mwao, wakiwa wamemweka Mungu mbali na mipango yao?

17 “Mara ngapi umepata kuona mwanga wa maisha ya mwovu umezimwa, wakapata kukumbwa na maafa, au Mungu amewahi kuwaangamiza kwa hasira yake?

18 Hata hivyo, na wapeperushwe kama majani makavu, wawe kama makapi yanayochukuliwa na dhoruba!

19 “Nyinyi mwasema, ‘Mungu amewawekea watoto wao adhabu ya watu hao waovu.’ Kwa nini hawalipizi wao wenyewe, wapate kutambua!

20 Waone wao wenyewe wakiangamia; waone wenyewe ghadhabu ya Mungu mwenye nguvu.

21 Maana wakifa watajali nini juu ya wazawa wao, wakati siku zao zitakapokuwa zimefika mwisho?

22 Je, binadamu aweza kumfunza Mungu maarifa, Mungu ambaye huwahukumu wakazi wa mbinguni?

23 “Mtu hufa katika kilele cha ufanisi wake, akiwa katika raha mustarehe na salama;

24 amejaa mafuta tele mwilini, na mifupa yake ikiwa bado na nguvu.

25 Mwingine hufa na huzuni kubwa moyoni, akiwa hajawahi kuonja lolote jema.

26 Hata hivyo, wote hufa na kuzikwa, wote hufunikwa na mabuu.

27 “Sikilizeni! Mimi nayajua mawazo yenu yote, na mipango yenu ya kunidharau.

28 Eti mwauliza, ‘Iko wapi nyumba ya mkuu? Iko wapi nyumba alimoishi mwovu?’

29 “Je, hamjawauliza wapita njia, mkakubaliana na ripoti yao?

30 Mwovu husalimishwa siku ya maafa, huokolewa siku ya ghadhabu!

31 Ni nani atakayemshutumu mtu mwovu, au atakayemlipa kwa yote aliyotenda?

32 Anapochukuliwa kupelekwa kaburini, kaburi lake huwekewa ulinzi.

33 Watu wengi humfuata nyuma na wengine wengi sana humtangulia. Anapozikwa, udongo huteremshwa taratibu.

34 Mtawezaje basi, kunifariji kwa maneno matupu? majibu yenu hayana chochote ila uongo.”

22

1 Kisha Elifazi, Mtemani, akajibu Yobu:

2 “Je, binadamu anafaa chochote kwa Mungu? Kwa kweli mwenye hekima anajifaidi mwenyewe tu.

3 Je, unadhani wamfurahisha Mungu kwa kuwa mnyofu? Au anapata faida gani kama huna hatia?

4 Unadhani anakurudi na kukuhukumu kwa sababu wewe unamheshimu?

5 La! Uovu wako ni mkubwa mno! Ubaya wako hauna mwisho!

6 Wewe umemnyanganya ndugu yako nguo ya rehani; umemchukulia nguo hiyo moja aliyokuwa nayo.

7 Umewanyima maji wale waliokuwa wamechoka; umewanyima chakula wale walio na njaa.

8 Umemruhusu mwenye cheo kuchukua ardhi yote; umemwacha anayependelewa aishi humo.

9 Umewaacha wajane waende mikono mitupu; umewanyima yatima uwezo wao.

10 Kwa hiyo mitego imekuzunguka pande zote, hofu ya ghafla imekuvamia.

11 Giza limekuangukia usione kitu; mafuriko ya maji yamekufunika.

12 Twajua Mungu yuko huko juu mbinguni. Tazama nyota za juu kabisa zilivyo mbali!

13 Lakini wewe wasema: ‘Mungu ajua nini? Je, aweza kupenya mawingu akatoa hukumu?

14 Mawingu mazito yamemzunguka asipate kuona yeye hutembea nje ya anga la dunia!’

15 “Je, umeamua kufuata njia za zamani ambazo watu waovu wamezifuata?

16 Hao walifagiliwa kabla ya wakati wao, misingi yao ilikumbwa mbali na maji.

17 Hao ndio waliomwambia Mungu, ‘Achana nasi!’ Na ‘Wewe Mungu Mwenye Nguvu waweza nini juu yetu?’

18 Lakini Mungu ndiye aliyejaza nyumba zao fanaka, lakini walimweka mbali na mipango yao!

19 Wanyofu huona na kufurahi, wasio na hatia huwacheka na kuwadharau,

20 Wanasema ama kweli maadui zetu wameangamizwa, na walichobakiza kimeteketezwa kwa moto.

21 “Sasa, Yobu, kubaliana na Mungu uwe na amani, na hapo mema yatakujia.

22 Pokea mafundisho kutoka kwake; na yaweke maneno yake moyoni mwako.

23 Ukimrudia Mungu na kunyenyekea, ukiondoa uovu mbali na makao yako,

24 ukitupilia mbali mali yako, ukaitupa dhahabu ya Ofiri ukingoni mwa kijito,

25 Mungu Mwenye Nguvu akawa ndio dhahabu yako, na fedha yako ya thamani;

26 basi, ndipo utakapomfurahia Mungu mwenye nguvu na kutazama kwa matumaini;

27 utamwomba naye atakusikiliza, nawe utazitimiza nadhiri zako.

28 Chochote utakachoamua kitafanikiwa, na mwanga utaziangazia njia zako.

29 Maana, Mungu huwaporomosha wenye majivuno, lakini huwaokoa wanyenyekevu.

30 Yeye humwokoa mtu asiye na hatia; wewe utaokolewa kwa matendo yako mema.”

23

1 Kisha Yobu akajibu:

2 “Leo pia lalamiko langu ni chungu. Napata maumivu na kusononeka.

3 Laiti ningejua mahali nitakapompata Mungu! Ningeweza kwenda hata karibu naye.

4 Ningeleta kesi yangu mbele yake, na kumtolea hoja yangu.

5 Ningeweza kujua atakachonijibu, na kuelewa atakachoniambia.

6 Je, angeshindana nami kwa nguvu zake zote? La! Bila shaka angenisikiliza.

7 Yeye aweza kuzungumza na mtu mnyofu, Mungu, hakimu wangu angeamua kuwa sina hatia milele.

8 “Tazama, nakwenda mbele, lakini simpati, narudi nyuma, lakini siwezi kumwona.

9 Namtafuta upande wa kushoto lakini simwoni; nageukia kulia, lakini siwezi kumwona.

10 Lakini yeye anajua njia ninayofuata; atakapomaliza kunijaribu nitatoka humo safi kama dhahabu.

11 Nafuata nyayo zake kwa uaminifu njia yake nimeishikilia wala sikupinda.

12 Kamwe sijaacha kushika amri yake, maneno yake nimeyatunza moyoni mwangu.

13 Lakini yeye habadiliki, nani awezaye kumgeuza? Analotaka, ndilo analofanya!

14 Atanijulisha yote aliyonipangia; na mengi kama hayo yamo akilini mwake.

15 Hivyo, natetemeka kwa hofu mbele yake; hata nikifikiria tu napatwa na woga.

16 Mungu ameufanya moyo wangu ufifie, Mungu Mwenye Nguvu amenitia hofu.

17 Maana nimekumbwa na giza, na giza nene limetanda usoni mwangu.

24

1 “Mbona Mungu Mwenye Nguvu haweki wakati maalumu wa hukumu; au kwa nini wamjuao hawazijui siku hizo zake?

2 Watu wanaoondoa alama za mipaka ya mashamba, na wengine huiba mifugo na kuilisha.

3 Huwanyanganya yatima punda wao, humweka rehani ng'ombe wa mjane.

4 Huwasukuma maskini kando ya barabara; maskini wa dunia hujificha mbele yao.

5 Kwa hiyo kama pundamwitu maskini hutafuta chakula jangwani wapate chochote cha kuwalisha watoto wao.

6 Maskini wanalazimika kuokota mabaki ya mavuno mashambani, wanaokota katika mashamba ya mizabibu ya waovu.

7 Usiku kucha hulala uchi bila nguo wakati wa baridi hawana cha kujifunikia.

8 Wamelowa kwa mvua ya milimani, hujibanza miambani kujificha wasilowe.

9 Wapo na wanaowanyakua watoto yatima vifuani mwa mama yao. Wengine huwaweka rehani watoto wa maskini.

10 Watoto hao hufanywa waende uchi bila nguo, wakivuna ngano huku njaa imewabana,

11 wakiwatengenezea waovu mafuta yao, au kukamua divai bila hata kuionja.

12 Kutoka mjini kilio cha wanaokufa chasikika, na walioumizwa hupaza sauti kuomba msaada; lakini Mungu hasikilizi kabisa sala zao.

13 “Wapo wengine waovu wasiopenda mwanga, wasiozifahamu njia za mwanga, na hawapendi kuzishika njia zake.

14 Mwuaji huamka mapema alfajiri, ili kwenda kuwaua maskini na fukara, na usiku ukifika, kazi yake ni kuiba.

15 Mzinifu naye hungojea giza liingie; akisema, ‘Hakuna atakayeniona;’ kisha huuficha uso wake kwa nguo.

16 Usiku wezi huvunja nyumba, lakini mchana hujifungia ndani; wala hawajui kabisa mwanga ni nini.

17 Kwao wote giza nene ni mwanga wa asubuhi; wao ni marafiki wa vitisho vya giza nene.

18 “Lakini mwasema: ‘Waovu huchukuliwa haraka na mafuriko ya maji, makao yao hubaki kuwa nchi iliyolaaniwa; hakuna aendaye kwenye mashamba yao ya mizabibu.’

19 Kama theluji inavyoyeyuka katika joto na ukame ndivyo Kuzimu kunavyowanyakua waovu.

20 Maana mzazi wao huwasahau watu hao, hakuna atakayewakumbuka tena. Ndivyo uovu ulivyovunjwa kama mti.

21 “Waovu huwadhulumu wanawake wasiopata watoto. Wala hawawatendei wema wanawake wajane.

22 Mungu, kwa nguvu yake huwaangamiza wenye uwezo, huinuka nao hukata tamaa ya kuishi.

23 Huwaacha waovu wajione salama, lakini macho yake huchunguza mienendo yao.

24 Waovu hufana kwa muda tu, kisha hutoweka, hunyauka na kufifia kama jani, hukatiliwa mbali kama masuke ya ngano.

25 Nani basi, awezaye kuhakikisha kuwa mimi ni mwongo na kuonesha kwamba maneno yangu si kweli?”

25

1 Kisha Bildadi, Mshuhi, akajibu:

2 “Mungu ni mwenye uwezo mkuu, watu wote na wamche. Yeye huweka amani mpaka juu kwake mbinguni.

3 Nani awezaye kuhesabu majeshi yake? Ni nani asiyeangaziwa na mwanga wake?

4 Mtu awezaje basi, kuwa mwadilifu mbele ya Mungu? Binadamu tu awezaje kujidai kuwa safi?

5 Kwake Mungu, hata mwezi haungai vya kutosha; nyota nazo si safi mbele yake;

6 sembuse mtu ambaye ni mdudu, binadamu ambaye ni buu tu!”

26

1 Kisha Yobu akajibu:

2 “Aa! Jinsi gani ulivyomsaidia asiye na uwezo! Jinsi gani ulivyomwokoa asiye na nguvu!

3 Jinsi gani ulivyomshauri asiye na hekima, na kumshirikisha ujuzi wako!

4 Lakini umetamka hayo kwa ajili ya nani? Nani aliyekusukuma kuongea hivyo?” Bildadi akajibu:

5 “Mizimu huko chini yatetemeka, maji ya chini na wakazi wake yaogopa.

6 Kuzimu kuko wazi kabisa mbele ya Mungu. Abadoni haina kifuniko chochote.

7 Mungu hutandaza kaskazini mahali patupu, na hutundika dunia mahali pasipo na kitu,

8 huyafunga maji mawinguni yawe mazito, nayo mawingu hayapasuki kwa uzito wake.

9 Huufunika uso wa mwezi na kutandaza juu yake wingu.

10 Amechora duara juu ya uso wa bahari, penye mpaka kati ya mwanga na giza.

11 Mungu akitoa sauti ya kukemea, nguzo za mbingu hutetemeka na kustaajabu.

12 Kwa nguvu zake aliituliza bahari; kwa maarifa yake alimwangamiza dude Rahabu.

13 Kwa pumzi yake aliisafisha anga; mkono wake ulilichoma joka lirukalo.

14 Yamkini haya ni machache tu ya matendo yake, ni minongono tu tunayosikia juu yake. Nani awezaye kujua ukuu wa nguvu yake?”

27

1 Yobu akaendelea kutoa hoja yake, akasema:

2 “Naapa kwa Mungu aliye hai, aliyeniondolea haki yangu, Mungu Mwenye Nguvu aliyeifanya nafsi yangu iwe na uchungu!

3 Naapa kuwa kadiri ninavyoweza kupumua, roho ya Mungu ikiwa bado ndani yangu;

4 midomo yangu kamwe haitatamka uongo, wala ulimi wangu kusema udanganyifu.

5 Siwezi kabisa kusema kuwa nyinyi mnasema ukweli mpaka kufa kwangu nasema sina hatia.

6 Nashikilia unyofu wangu, wala sitauacha; katika dhamiri yangu sina cha kunihukumu maishani mwangu.

7 “Adui yangu na apate adhabu ya mwovu, anayeinuka kunilaumu aadhibiwe kama mbaya.

8 Asiyemcha Mungu ana tumaini gani, Mungu anapomkatilia mbali, anapomwondolea uhai wake?

9 Je, atakapokumbwa na taabu, Mungu atasikia kilio chake?

10 Mwovu hawezi kufurahi mbele ya Mungu Mwenye Nguvu; hataweza kudumu akimwomba Mungu.

11 Nitawafundisheni kitendo cha Mungu kilivyo, sitawaficheni mipango yake Mungu Mwenye Nguvu.

12 Lakini nyinyi mnajua jambo hilo vizuri sana! Mbona, basi mnaongea upuuzi?

13 “Hiki ndicho Mungu alichomwekea mtu mwovu, alichopangiwa mdhalimu kupata ni hiki:

14 Watoto wake hata wawe wengi watauawa kwa upanga; wazawa wake hawatakuwa na chakula cha kutosha.

15 Wale watakaopona watakufa kwa maradhi mabaya, na wajane wao hawatawaombolezea.

16 Hata akirundika fedha kama mavumbi, na mavazi kama udongo wa mfinyanzi,

17 na arundike tu, lakini mnyofu ndiye atakayeyavaa, na fedha yake watagawana watu wasio na hatia.

18 Nyumba ajengayo mwovu ni kama utando wa buibui, ni kama kibanda cha mlinzi shambani.

19 Huenda kulala tajiri, lakini ni mara ya mwisho; atafungua macho yake, na utajiri wake umetoweka!

20 Vitisho humvamia kama mafuriko; usiku hukumbwa na kimbunga.

21 Upepo wa mashariki humpeperusha akatoweka; humfagilia mbali kutoka makao yake.

22 Upepo huo humvamia bila huruma; atajaribu kuukimbia lakini mbio za bure.

23 Upepo humzomea akimbiapo, na kumfyonya toka mahali pake.

28

1 “Hakika kuna machimbo ya fedha, na mahali ambako dhahabu husafishwa.

2 Watu huchimba chuma ardhini, huyeyusha shaba kutoka mawe ya madini.

3 Wachimba migodi huleta taa gizani, huchunguza vina vya ardhi na kuchimbua mawe yenye madini gizani.

4 Binadamu huchimba mashimo mbali na makazi ya watu, mbali na watu mahali kusipofikika, wachimba madini huninginia wamefungwa kamba.

5 Kutoka udongoni chakula hupatikana, lakini chini yake kila kitu huvurugwa kwa moto.

6 Katika mawe yake ndimo vilimo vito vya rangi ya samawati na udongo wake una vumbi la dhahabu.

7 “Njia za kwenda kwenye migodi hiyo hakuna ndege mla nyama azijuaye; na wala jicho la tai halijaiona.

8 Wanyama waendao kwa madaha hawajazikanyaga wala simba hawajawahi kuzipitia.

9 Binadamu huchimbua miamba migumu kabisa, huichimbua milima na kuiondolea mbali.

10 Hupasua mifereji kati ya majabali, na jicho lake huona vito vya thamani.

11 Huziba chemchemi zisitiririke, na kufichua vitu vilivyofichika.

12 “Lakini hekima itapatikana wapi? Ni mahali gani panapopatikana maarifa?

13 Hakuna mtu ajuaye thamani ya hekima, wala hekima haipatikani nchini mwa walio hai.

14 Vilindi vyasema, ‘Hekima haimo kwetu,’ na bahari yasema, ‘Haiko kwangu.’

15 Hekima haiwezi kupatikana kwa dhahabu, wala kwa kupima kiasi kingi cha fedha.

16 Haiwezi kupimwa kwa dhahabu ya Ofiri, wala kwa vito vya Sardoniki au vya rangi ya samawati,

17 dhahabu au kioo havilingani nayo, wala haiwezi kubadilishwa na vito vya dhahabu safi.

18 Hekima ina thamani kuliko matumbawe na marijani, thamani yake yashinda thamani ya lulu.

19 Topazi ya Kushi haiwezi kulinganishwa nayo, wala haiwezi kupewa bei ya dhahabu safi.

20 “Basi, hekima yatoka wapi? Ni wapi panapopatikana maarifa?

21 Imefichika machoni pa viumbe vyote hai, na ndege wa angani hawawezi kuiona.

22 Abadoni na Kifo wasema, ‘Tumesikia uvumi wake kwa masikio yetu.’

23 “Mungu aijua njia ya hekima, anajua mahali inapopatikana.

24 Maana yeye huona mpaka upeo wa dunia, huona kila kitu chini ya mbingu.

25 Alipoupa upepo uzito wake, na kuyapimia maji mipaka yake;

26 alipoamua mvua inyeshe wapi, umeme na radi vipite wapi;

27 hapo ndipo alipoiona hekima na kuitangaza, aliisimika na kuichunguza.”

28 Kisha Mungu akamwambia mwanadamu: “Tazama! Kumcha Bwana ndio hekima; na kujitenga na uovu ndio maarifa.”

29

1 Kisha Yobu akaendelea na hoja yake, akasema:

2 “Laiti ningekuwa kama zamani, wakati ule ambapo Mungu alinichunga;

3 wakati taa yake iliponiangazia kichwani, na kwa mwanga wake nikatembea gizani.

4 Wakati huo nilifikia ukamilifu wa maisha, wakati urafiki wa Mungu ulikaa nyumbani kwangu.

5 Mungu Mwenye Nguvu alikuwa bado pamoja nami, na watoto wangu walinizunguka.

6 Nyakati hizo niliogelea kwenye ufanisi, miamba ilinitiririshia vijito vya mafuta!

7 Nilipokutana na wazee langoni mwa mji na kuchukua nafasi yangu mkutanoni,

8 vijana waliponiona walisimama kando, na wazee walisimama wima kwa heshima.

9 Wakuu waliponiona waliacha kuzungumza waliweka mikono juu ya midomo kuwataka watu wakae kimya.

10 Sauti za waheshimiwa zilinyamazishwa, na vinywa vyao vikafumbwa.

11 Kila aliyesikia habari zangu alinitakia heri na aliponiona, alikubali habari hizo kuwa kweli:

12 Nilimwokoa maskini aliyenililia msaada, kadhalika na yatima asiyekuwa na wa kumsaidia.

13 Waliokuwa karibu kuangamia walinitakia baraka, niliwafanya wajane waone tena furaha moyoni.

14 Uadilifu ulikuwa vazi langu; kutenda haki kulikuwa kama joho na kilemba changu.

15 Kwa vipofu nilikuwa macho ya kuwaonesha njia, kwa viwete nilikuwa miguu yao.

16 Kwa maskini nilikuwa baba yao, nilifanya bidii kutetea haki za watu nisiowajua.

17 Nilizivunja nguvu za watu waovu, nikawafanya wawaachilie mateka wao.

18 Kisha nikafikiri: Nitafia kiotani mwangu nimetulia; siku za maisha yangu zitaongezeka kama mchanga.

19 Mimi ni kama mti uliotandaza mizizi majini, umande wa usiku huburudisha matawi yangu.

20 Napata fahari mpya daima, na nguvu zangu tayari kama mshale na upinde.

21 “Wakati huo watu walinisikiliza na kungoja, walikaa kimya kungojea shauri langu.

22 Nilipomaliza kusema hawakuwa na cha kuongeza, maneno yangu yaliwakolea kama matone ya mvua.

23 Watu waliningojea kama wangojeavyo mvua, walikuwa kama watu wanaotazamia msimu wa vuli.

24 Walipokata tamaa niliwaonesha uso wa furaha, uchangamfu wa uso wangu wakaungangania.

25 Niliwatangulia kuwaongoza, nikawaonesha njia; nilikuwa kwao kama mfalme kati ya majeshi yake; kama mtu anayewafariji wenye msiba.

30

1 “Lakini sasa watu wananidhihaki, tena watu walio wadogo kuliko mimi; watu ambao baba zao niliwaona hawafai hata kuwaangalia mbwa wangu wakilinda kondoo.

2 Ningepata faida gani mikononi mwao, watu ambao nguvu zao zilikuwa zimewaishia?

3 Katika ufukara na njaa kali walitafutatafuta cha kutafuna nyikani sehemu tupu zisizokuwa na chakula.

4 Walichuma mimea jangwani na majani msituni wakala, walikula hata mizizi ya mti wa mfagio.

5 Walifukuzwa mbali na watu, watu waliwapigia kelele kama wezi.

6 Iliwapasa kutafuta usalama mapangoni, kwenye mashimo ardhini na miambani.

7 Huko vichakani walilia kama wanyama, walikusanyika pamoja chini ya upupu.

8 Walikuwa wapumbavu wakuu na mabaradhuli ambao walilazimika kufukuzwa nchini kwa kiboko.

9 “Na sasa wamenitungia wimbo wa kunizomea, nimekuwa kitu cha dhihaka kwao.

10 Wananichukia na kuniepa; wakiniona tu wanatema mate.

11 Kwa kuwa Mungu amenidhoofisha na kuniaibisha, wamekuwa huru kunitendea wapendavyo.

12 Genge la watu lainuka kunishtaki likitafuta kuniangusha kwa kunitegea. Linanishambulia ili niangamie.

13 Watu hao hukata njia yangu huchochea balaa yangu, na hapana mtu wa kuwazuia.

14 Wanakuja kama kwenye ufa mkubwa, na baada ya shambulio wanasonga mbele.

15 Hofu kuu imenishika; hadhi yangu imetoweka kama kwa upepo, na ufanisi wangu umepita kama wingu.

16 “Sasa sina nguvu yoyote nafsini mwangu; siku za mateso zimenikumba.

17 Usiku mifupa yangu yote huuma, maumivu yanayonitafuna hayapoi.

18 Mungu amenikaba kwa mavazi yangu, amenibana kama ukosi wa shati langu.

19 Amenibwaga matopeni; nimekuwa kama majivu na mavumbi.

20 Nakulilia, lakini hunijibu, nasimama kuomba lakini hunisikilizi.

21 Umegeuka kuwa mkatili kwangu, wanitesa kwa mkono wako wenye nguvu.

22 Wanitupa katika upepo na kunipeperusha; wanisukasuka huku na huko katika dhoruba kali.

23 Naam! Najua utanipeleka tu kifoni, mahali watakapokutana wote waishio.

24 “Je, mtu akikumbwa na maangamizi hainui mkono? Je, mtu akiwa taabuni haombi msaada

25 Je, sikuwalilia wale waliokuwa na taabu? Je, sikuona uchungu kwa ajili ya maskini?

26 Lakini nilipotazamia mema, mabaya yalinipata, nilipongojea mwanga, giza lilikuja.

27 Moyo wangu wahangaika wala hautulii kamwe; siku za mateso zimekumbana nami.

28 Napitapita nikiomboleza, kwangu hamna jua. Nasimama hadharani kuomba msaada.

29 Kwa kilio nimekuwa ndugu yake mbwamwitu, mimi na mbuni hamna tofauti.

30 Ngozi yangu imebambuka mifupa yangu inaungua kwa homa.

31 Kinubi changu kimekuwa cha kufanya matanga filimbi yangu kwa ajili ya kuomboleza.

31

1 “Nimejifunga rasmi mimi mwenyewe, macho yangu yasimtazame msichana kwa tamaa.

2 Au je, nangojea nini kutoka kwa Mungu aliye juu? Mungu Mwenye Nguvu ameniwekea kitu gani?

3 Je, maafa hayawapati watu waovu na maangamizi wale watendao mabaya?

4 Je, Mungu haoni njia zangu, na kujua hatua zangu zote?

5 “Kama nimeishi kwa kufuata uongo, kama nimekuwa mbioni kudanganya watu,

6 Mungu na anipime katika mizani ya haki, naye ataona kwamba sina hatia.

7 Kama hatua zangu zimepotoka, moyo wangu ukafuata tamaa za macho yangu; kama mikono yangu imechafuliwa na dhambi,

8 jasho langu na liliwe na mtu mwingine, mazao yangu shambani na yangolewe.

9 “Kama moyo wangu umevutwa kwa mke wa mtu, kama nimenyemelea mlangoni kwa jirani yangu,

10 basi, mke wangu na ampikie mume mwingine, na wanaume wengine wamtumie.

11 Jambo hilo ni kosa kuu la jinai, uovu ambao hakimu lazima atoe adhabu.

12 Kosa langu lingekuwa kama moto, wa kuniteketeza na kuangamiza, na kuchoma kabisa mapato yangu yote.

13 Kama nimekataa kesi ya mtumishi wangu wa kiume au wa kike, waliponiletea malalamiko yao,

14 nitafanya nini basi Mungu atakaponikabili? Je, akinichunguza nitamjibu nini?

15 Maana Mungu ndiye aliyeniumba mimi na mtumishi wangu; yeye ndiye aliyetuumba sisi wote.

16 “Je, nimepata kumnyima maskini mahitaji yake au kuwafanya wajane watumaini bure?

17 Je, nimekula chakula changu peke yangu, bila kuwaachia yatima nao wapate chochote?

18 La! Tangu ujana wangu nimekuwa mlezi wao, tangu utoto wangu nimewaongoza wajane.

19 Je, nilimwona mtu anakufa kwa kukosa nguo, au maskini ambaye hana nguo ya kuvaa,

20 bila kumpa joto kwa mavazi ya manyoya ya kondoo wangu naye akanitakia baraka za shukrani ya moyo?

21 Kama nimenyosha mkono mahakamani dhidi ya yatima, nikijua nitapendelewa na mahakimu,

22 basi, bega langu na lingoke, mkono wangu na ukwanyuke kiwikoni mwake.

23 Maana maafa kutoka kwa Mungu ni kitisho kwangu; mimi siwezi kuukabili ukuu wake.

24 “Je, tumaini langu nimeliweka katika dhahabu, au, nimeiambia dhahabu safi, ‘Wewe ni usalama wangu?’

25 Je, nimepata kufurahia wingi wa utajiri wangu au kujivunia mapato ya mikono yangu?

26 Kama nimeliangalia jua likiangaza, na mwezi ukipita katika uzuri wake,

27 na moyo wangu ukashawishika kuviabudu, nami nikaibusu mikono yangu kwa heshima yake,

28 huo pia ungekuwa uovu wa kuadhibiwa na mahakimu maana ningekuwa mwongo mbele ya Mungu aliye juu.

29 “Je, nimefurahia kuangamia kwa adui yangu, au kufurahi alipopatwa na maafa?

30 La! Sikuruhusu kinywa changu kumtakia mabaya, kwa kumlaani ili afe.

31 Watumishi wangu wote wanasema wazi kila mgeni amekaribishwa nyumbani mwangu.

32 Msafiri hakulala nje ya nyumba yangu, nilimfungulia mlango mpita njia.

33 Je nimeficha makosa yangu kama wengine? Je nimekataa kukiri dhambi zangu?

34 Sijaogopa kusimama mbele ya umati wa watu, wala kukaa kimya au kujifungia ndani, eti kwa kuogopa kutishwa na dharau zao.

35 Laiti angekuwapo mtu wa kunisikiliza! Naweza kutia sahihi yangu katika kila nilichosema. Namwambia Mungu Mwenye Nguvu anijibu! Laiti mashtaka wanayonitolea maadui zangu yangeandikwa!

36 Ningeyavaa kwa maringo mabegani na kujivisha kichwani kama taji.

37 Ningemhesabia Mungu kila kitu nilichofanya, ningemwendea kama mwana wa mfalme.

38 Kama nimeiiba ardhi ninayoilima, nikasababisha mifereji yake iomboleze,

39 kwa kufaidika na mazao yake bila kulipa na kusababisha kifo cha wenyewe,

40 basi miiba na iote humo badala ya ngano, na magugu badala ya shayiri.” Mwisho wa hoja za Yobu.

32

1 Basi hawa watu watatu: Elifazi, Bildadi na Sofari, wakaacha kumjibu Yobu kwa vile alijiona kuwa mwema.

2 Ndipo Elihu, mwana wa Barakeli, wa kabila la Buzi wa ukoo wa Rama, akakasirika. Alimkasirikia Yobu kwa sababu Yobu alijiona yeye mwadilifu na sio Mungu.

3 Pia, aliwakasirikia rafiki watatu wa Yobu kwa sababu hawakuwa na la kumjibu Yobu, na hivyo kuonesha kwamba Mungu amekosa.

4 Elihu alikuwa amekaa kimya wakati hao wazee waliposema na Yobu kwa kuwa yeye alikuwa kijana kuliko wao.

5 Lakini alipoona hao watu watatu wameshindwa kumjibu Yobu, aliwaka hasira.

6 Basi, Elihu mwana wa Barakeli, wa kabila la Buzi akaanza kusema: “Mimi ni kijana, nyinyi ni wazee zaidi; kwa hiyo niliogopa kuwaambieni mawazo yangu.

7 Nilisema moyoni: ‘Waache wenye siku nyingi waseme, wenye miaka mingi wafundishe hekima.’

8 Lakini hiyo roho iliyomo ndani ya mtu, hiyo pumzi ya Mungu Mwenye Nguvu, ndio inayomwezesha mwanadamu kufahamu.

9 Si lazima kuwa mzee ili uwe na hekima wala wazee siyo wenye kufahamu lililo sawa.

10 Kwa hiyo nasema, ‘Nisikilizeni, acheni nami nitoe maoni yangu.’

11 “Basi, mimi nilingojea mlichotaka kusema, nilisikiliza misemo yenu ya hekima, mlipokuwa mnajaribu kutafuta la kusema.

12 Niliwasikiliza kwa makini sana, lakini hakuna mmoja wenu aliyemshinda Yobu; nyote mlishindwa kuyajibu maneno yake.

13 Jihadharini msije mkasema, ‘Sasa tumepata hekima. Atakayemshinda ni Mungu, sio binadamu.’

14 Maneno ya Yobu hayakuwa kwa ajili yangu, kwa hiyo sitamjibu kama mlivyomjibu nyinyi.

15 “Nyinyi mmeduwaa; mmeshindwa, nyinyi hamna cha kusema zaidi.

16 Je, ningoje tu kwa vile hamsemi, kwa sababu mnakaa tu bila kujibu kitu?

17 Mimi pia nitatoa jibu langu; mimi nitatoa pia maoni yangu.

18 Ninayo maneno mengi sana, roho yangu yanisukuma kusema.

19 Moyo wangu umefurika kama divai iliyozibwa, kama kiriba cha divai mpya tayari kupasuka.

20 Ni lazima niseme ili nipate nafuu; yanipasa kufungua kinywa changu na kujibu.

21 Sitampendelea mtu yeyote wala kutumia maneno ya kubembeleza mtu.

22 Maana mimi sijui kubembeleza mtu, la sivyo, Muumba wangu angeniangamiza.

33

1 “Sasa, Yobu, sikiliza hoja yangu; sikiliza maneno yangu yote.

2 Tazama, nafumbua kinywa changu, naam, ulimi wangu utasema.

3 Nitasema kadiri ya unyofu wa moyo wangu; ninayoyajua nitayasema kwa uaminifu.

4 Roho ya Mungu iliniumba, nayo pumzi ya Mungu Mwenye Nguvu yanipa uhai.

5 Nijibu, kama unaweza. Panga hoja zako vizuri mbele yangu, ushike msimamo wako.

6 Wewe na mimi ni sawa mbele ya Mungu; mimi pia niliumbwa kwa sehemu ya udongo.

7 Kwa hiyo huna sababu ya kuniogopa; maneno yangu mazito hayatakulemea.

8 Kweli umesema, nami nikasikia; nimeyasikia yote uliyosema.

9 Wewe umesema, u safi na wala huna kosa, u safi kabisa na huna hatia;

10 umesema kwamba Mungu anakutafutia kisa, na kukuona kama adui yake.

11 Anakufunga miguu minyororo, na kuchunguza hatua zako zote.

12 “Lakini Yobu, nakuambia hapo umekosea. Mungu ni mkuu kuliko binadamu.

13 Kwa nini unashindana naye, ukisema hatajibu swali lako moja?

14 Mungu anaposema hutumia njia moja, au njia nyingine lakini mtu hatambui.

15 Mungu huongea na watu katika ndoto na maono, wakati usingizi mzito unapowavamia,

16 wanaposinzia vitandani mwao. Hapo huwafungulia watu masikio yao; huwatia hofu kwa maonyo yake,

17 wapate kuachana na matendo yao mabaya, na kuvunjilia mbali kiburi chao.

18 Hivyo humkinga mtu asiangamie shimoni, maisha yake yasiangamie kwa upanga.

19 “Mungu humrudi mtu kwa maumivu yamwekayo kitandani, maumivu hushika viungo vyake bila kukoma;

20 naye hupoteza hamu yote ya chakula, hata chakula kizuri humtia kinyaa.

21 Mwili wake hukonda hata asitambuliwe, na mifupa yake iliyofichika ikatokeza nje.

22 Yuko karibu sana kuingia kaburini, na maisha yake karibu na wale waletao kifo.

23 Lakini malaika akiwapo karibu naye, mmoja kati ya maelfu ya watetezi wa Mungu, ili kumwonesha lililo jema la kufanya,

24 akamwonea huruma na kumwambia Mungu; ‘Mwokoe asiingie Shimoni, ninayo fidia kwa ajili yake.’

25 Hapo mwili wake utaweza kuwa tena kama kijana, ataweza kurudia tena nguvu zake za ujana.

26 Kisha atamwomba Mungu na kukubaliwa, atakuja mbele yake kwa furaha, na Mungu atamrudishia fahari yake.

27 Atashangilia mbele ya watu na kusema: ‘Nilitenda dhambi na kupotosha haki, nami sikuadhibiwa kutokana na hayo.

28 Mungu aliniokoa nisiangamie Shimoni; nimebaki hai na ninaona mwanga.’

29 “Tazama Mungu humfanyia binadamu haya yote, tena mara mbili, mara tatu.

30 Humwokoa binadamu asiangamie Shimoni, aweze kuona mwanga wa maisha.

31 Sikia Yobu, nisikilize kwa makini; kaa kimya, nami nitasema.

32 Kama una la kusema, nijibu; sema, maana nataka kukuona huna hatia.

33 La sivyo, nyamaza unisikilize, kaa kimya nami nikufunze hekima.”

34

1 Kisha Elihu akaendelea kusema:

2 “Sikilizeni maneno yangu enyi wenye hekima, nitegeeni masikio yenu, nyinyi wenye ujuzi.

3 Sikio huyapima maneno, kama vile ulimi uonjavyo chakula.

4 Basi, na tuchague lililo sawa, tuamue miongoni mwetu lililo jema.

5 Basi, Yobu ametamka: ‘Mimi Yobu sina hatia, Mungu ameniondolea haki yangu.

6 Ingawa sina hatia naonekana kuwa mwongo; kidonda changu hakiponyeki ingawa sina kosa.’

7 Ni nani aliye kama Yobu ambaye kwake ubaradhuli ni kama kunywa maji?

8 Huandamana na watenda maovu hutembea na watu waovu.

9 Maana amesema, ‘Mtu hapati faida yoyote, kujisumbua kumpendeza Mungu.’

10 “Kwa hiyo nisikilizeni, enyi wenye ujuzi. Mungu kamwe hawezi kufanya uovu; Mungu Mwenye Nguvu hawezi kufanya kosa.

11 Mungu atamlipa mtu kadiri ya matendo yake, atamlipiza kulingana na mwenendo wake.

12 Ni ukweli mtupu: Mungu hafanyi ovu; Mungu Mwenye Nguvu kamwe hapotoshi haki.

13 Je, kuna aliyemkabidhi mamlaka juu ya dunia? Uwezo wake juu ya ulimwengu ni wake peke yake.

14 Kama Mungu angejifikiria tu yeye mwenyewe, akiondoa pumzi yake ya uhai duniani,

15 viumbe vyote vingeangamia kabisa, naye binadamu angerudi mavumbini.

16 “Kama una akili sikiliza; sikiliza ninachokuambia.

17 Je, anayetawala ulimwengu kwa sheria zake anachukia haki? Je, utathubutu kumhukumu mwadilifu na mwenye nguvu?

18 Amwambiaye mfalme, ‘Wewe ni takataka!’ Na watu mashuhuri, ‘Nyinyi ni waovu!’

19 Yeye hawapendelei wakuu, wala kuwajali matajiri kuliko maskini, maana wote hao ni kazi ya mikono yake.

20 Kufumba na kufumbua hao wamekufa; hutikiswa usiku na kuaga dunia; nao wenye nguvu hufutiliwa mbali bila kutumia nguvu za mtu.

21 “Macho ya Mungu huchunguza mienendo ya watu; yeye huziona hatua zao zote.

22 Hakuna weusi wala giza nene ambamo watenda maovu waweza kujificha.

23 Mungu hahitaji kumjulisha mtu wakati wa kumleta mbele ya mahakama yake.

24 Huwaangamiza wenye nguvu bila uchunguzi, na kuwaweka wengine mahali pao.

25 Kwa kuwa anayajua matendo yao yote, huwaporomosha usiku wakaangamia.

26 Huwachapa hadharani kwa ajili ya uovu wao,

27 kwa sababu wameacha kumfuata yeye, wakazipuuza njia zake zote.

28 Hata wakasababisha kilio cha maskini kimfikie Mungu, Mungu akasikiliza kilio chao hao walioteswa.

29 Kama Mungu akinyamaza, nani awezaye kumlaumu? Kama akificha uso wake, nani awezaye kumwona,

30 liwe ni taifa au mtu mmojammoja? Hufanya hivyo, mtu mbaya asitawale, au wale wahatarishao maisha ya watu.

31 “Tuseme mtu amemwambia Mungu, ‘Nimekosa, sitatenda dhambi tena.

32 Nioneshe makosa nisiyoweza kuyaona kama nimetenda mabaya sitayarudia tena.’

33 Je, Mungu atapaswa kumwadhibu kama uonavyo wewe? Wewe ndiwe unayeamua, sio mimi. Basi, sema unachofikiri wewe.

34 Mtu yeyote mwenye akili, na kila mwenye hekima anayenisikiliza atasema:

35 ‘Yobu anaongea bila kutumia akili, maneno yake hayana maana.’

36 Laiti Yobu angechunguzwa mpaka mwisho, kwa maana anajibu kama watu waovu.

37 Huongeza uasi juu ya dhambi zake; anaeneza mashaka kati yetu, na kuzidisha maneno yake dhidi ya Mungu.”

35

1 Kisha Elihu akaendelea kusema:

2 “Je, Yobu, unaona jambo hili ni sawa na kufikiri kinyume cha Mungu

3 ukiuliza: ‘Nimepata faida gani kama sikutenda dhambi? Nimefaidika kuliko kama ningalitenda dhambi?’

4 Mimi nitakujibu wewe, na rafiki zako pia.

5 Hebu zitazame mbingu! Tazama mawingu yaliyo juu kuliko wewe!

6 Ukitenda dhambi, je, Mungu ndiye unayemdhuru? Na kama ukizidisha makosa yako, wadhani unamwumiza?

7 Kama wewe ni mwema, je, unampatia faida, au yeye anapokea kitu kutoka kwako?

8 Uovu wako utamdhuru binadamu kama wewe, wema wako utamfaa binadamu mwenzako.

9 “Kwa sababu ya udhalimu mwingi watu hulia, huomba msaada kwa sababu ya mapigo ya wenye nguvu.

10 Lakini hakuna asemaye, ‘Yuko wapi Mungu, Muumba wangu, mwenye kunifanya niwe mchangamfu usiku,

11 anayetuelimisha kuliko wanyama, na kutufanya wenye hekima kuliko ndege!’

12 Watu hao huomba msaada lakini Mungu hawajibu, kwa sababu ya majivuno ya watu waovu.

13 Kweli Mungu hasikilizi kilio cha bure; Mungu Mwenye Nguvu hajali kilio hicho.

14 Atakujibu vipi wakati wewe unasema kwamba humwoni na kwamba kesi yako iko mbele yake na wewe unamngojea!

15 Sasa, kwa vile Mungu anazuia hasira yake, wala hajali sana makosa ya watu,

16 Yobu unafungua mdomo kusema maneno matupu, unazidisha maneno bila akili.”

36

1 Kisha Elihu akaendelea kusema:

2 “Nivumilie kidogo, nami nitakuonesha kitu; maana bado ninacho cha kusema kwa niaba ya Mungu.

3 Nitaleta hekima yangu kutoka mbali sana, na kuonesha kwamba Muumba wangu ni mwadilifu.

4 Kweli maneno yangu si ya uongo; mwenye elimu kamili yuko hapa nawe.

5 “Sikiliza Mungu ni mwenye nguvu wala hamdharau mtu yeyote; uwezo wa akili yake ni mkuu mno!

6 Hawaachi waovu waendelee kuishi; lakini huwapatia wanaodhulumiwa haki zao.

7 Haachi kuwalinda watu waadilifu; huwatawaza, wakatawala na kutukuka.

8 Lakini kama watu wamefungwa minyororo, wamenaswa katika kamba za mateso,

9 Mungu huwaonesha matendo yao maovu, na kwamba wao ni watu wenye kiburi.

10 Huwafungua masikio wasikie mafunzo, na kuwaamuru warudi na kuacha uovu.

11 Wakimtii Mungu na kumtumikia, hufanikiwa katika siku zao zote; miaka yao yote huwa ya furaha.

12 Lakini wasipomtii, huangamia kwa upanga, na kufa kwa kukosa akili.

13 “Wasiomcha Mungu hupenda kukasirika, hawamlilii msaada anapowabana.

14 Hufa wangali bado vijana, maisha yao huisha kama ya walawiti.

15 Lakini Mungu huwaokoa wanyonge kwa unyonge wao hutumia shida zao kuwafumbua macho.

16 Mungu alikuvuta akakutoa taabuni, akakuweka mahali pa wasaa pasipo shida, na mezani pako akakuandalia vinono.

17 “Lakini sasa umehukumiwa kama mwovu, hukumu ya haki imekukumba.

18 Jihadhari ghadhabu isije ikakufanya ukadhihaki, au ukubwa wa mali za kukukomboa ukakupotosha.

19 Je, kilio chako kitafaa kukutoa taabuni, au nguvu zako zote zitakusaidia?

20 Usitamani usiku uje, ambapo watu hufanywa watoweke walipo.

21 Jihadhari! Usiuelekee uovu maana umepatiwa mateso kukuepusha na uovu.

22 Kumbuka ukuu wa uwezo wa Mungu; nani awezaye kumfundisha kitu?

23 Nani basi aliyeweza kumpangia njia yake, au awezaye kumwambia: ‘Umekosea?’

24 “Usisahau kuyasifu matendo yake; ambayo watu wameyashangilia.

25 Watu wote wameona aliyofanya Mungu; binadamu huyaona kutoka mbali.

26 Mungu ni mkuu mno hata hatuwezi kumjua; muda wa maisha yake hauchunguziki.

27 Yeye huyavuta kwake maji ya bahari, na kutoka ukungu hufanya matone ya mvua.

28 Huyafanya mawingu yanyeshe mvua, na kuwatiririshia binadamu kwa wingi.

29 Nani ajuaye jinsi mawingu yatandavyo, au jinsi radi ingurumavyo angani kwake?

30 Yeye huutandaza umeme wake kumzunguka, na kuvifunika vilindi vya bahari.

31 Kwa mvua huwalisha watu na kuwapatia chakula kwa wingi.

32 Huukamata umeme kwa mikono yake, kisha hulenga nao shabaha,

33 Radi hutangaza ujio wake Mungu, hata wanyama hujua kwamba anakuja.

37

1 “Kutokana na hayo, moyo wangu unatetemeka, na kuruka kutoka mahali pake.

2 Sikilizeni ngurumo ya sauti ya Mungu, na mvumo wa sauti kutoka kinywani mwake.

3 Huufanya uenee chini ya mbingu yote, umeme wake huueneza pembe zote za dunia.

4 Ndipo sauti yake hunguruma, sauti ya Mungu hunguruma kwa fahari na muda huo wote umeme humulikamulika.

5 Mungu hupiga radi ya ajabu kwa sauti yake, hufanya mambo makuu tusiyoweza kuyaelewa.

6 Huiambia theluji, ‘Anguka juu ya nchi!’ Na manyunyu na mvua, ‘Nyesha kwa nguvu.’

7 Hufunga shughuli za kila mtu; ili watu wote watambue kazi yake.

8 Wanyama wa porini hurudi mafichoni mwao, na hubaki katika mapango yao.

9 Dhoruba huvuma kutoka chumba chake, na baridi kali kutoka ghalani mwake.

10 Kwa pumzi ya Mungu barafu hutokea, uso wa maji huganda kwa haraka.

11 Mungu hulijaza wingu manyunyu mazito; mawingu husambaza umeme wake.

12 Kwa amri yake vyote huzunguka huku na huko, kutekeleza kila kitu anachokiamuru, kufanyika katika ulimwengu wa viumbe.

13 Mungu hutekeleza matakwa yake duniani; iwe ni kwa ajili ya kuwaadhibu watu, au kwa ajili ya kuonesha upendo wake.

14 “Unapaswa kusikiliza Yobu; nyamaza, usikilize maajabu ya Mungu.

15 Je, wajua jinsi Mungu anavyovipa amri yake, na kufanya umeme wa mawingu yake ungae?

16 Je, wajua jinsi mawingu yanavyoelea angani? Ndizo kazi za ajabu za yule aliye mkamilifu wa maarifa!

17 Wewe wajiona umevaa nguo za joto sana, wakati upepo wa kusi unaivamia nchi.

18 Je, waweza, kuzitandaza mbingu kama yeye zikawa ngumu kama kioo cha shaba?

19 Tufundishe tutakachomwambia Mungu; maana hoja zetu si wazi, tumo gizani.

20 Je, nani anathubutu kumwambia: Nataka kuongea? Nani aseme apate balaa?

21 “Ghafla mtu hawezi tena kuona waziwazi: Jua limefichika nyuma ya mawingu, na upepo umefagia anga!

22 Mngao mzuri hutokea kaskazini; Mungu amezungukwa na utukufu wa kutisha.

23 Mungu Mwenye Nguvu asiyeweza kufikiwa na mtu, uwezo na uadilifu wake ni mkuu, amejaa wema wala hapotoshi haki kamwe.

24 Kwa hiyo, watu wote humwogopa; yeye hamjali mtu yeyote mwenye kiburi.”

38

1 Hapo Mwenyezi-Mungu alimjibu Yobu kutoka dhoruba:

2 “Nani wewe unayevuruga mashauri yangu kwa maneno yasiyo na akili?

3 Jikaze kama mwanamume, nami nitakuuliza nawe utanijibu.

4 “Ulikuwa wapi nilipoiweka misingi ya dunia? Niambie, kama una maarifa.

5 Ni nani aliyeweka vipimo vyake, wajua bila shaka! Au nani aliyelaza kamba juu yake kuipima?

6 Je, nguzo za dunia zimesimikwa juu ya nini, au nani aliyeliweka jiwe lake la msingi,

7 nyota za asubuhi zilipokuwa zikiimba pamoja, na wana wa Mungu wakapaza sauti za shangwe?

8 Ni nani aliyeyafunga mafuriko ya bahari wakati yalipozuka na kuvuma kutoka vilindini?

9 Mimi ndiye niliyeifunika bahari kwa mawingu na kuiviringishia giza nene.

10 Niliiwekea bahari mipaka, nikaizuia kwa makomeo na milango,

11 nikaiambia: ‘Mwisho wako ni hapa, si zaidi! Mawimbi yako ya nguvu yatakomea hapa!’

12 “Yobu, tangu uzaliwe umewahi kuamuru kupambazuke? na kulifanya pambazuko lijue mahali pake,

13 ili lipate kuikamata dunia kwa pembe zake na kuwatimulia mbali waovu waliomo?

14 Dunia hugeuka na kupata rangi kama vazi; kama udongo wa mfinyanzi unavyogeuzwa na mhuri.

15 Lakini waovu watanyimwa mwanga wao, mkono wanaonyosha kupiga watu utavunjwa.

16 “Je, umepata kufika kwenye chemchemi za bahari? au kutembea juu ya sakafu ya kilindi cha bahari?

17 Je, umewahi kuoneshwa malango ya kifo, au kuyaona malango ya makazi ya giza nene?

18 Je, wajua ukubwa wa dunia? Niambie kama unajua haya yote.

19 “Je, makao ya mwanga yako wapi? Nyumbani kwa giza ni wapi,

20 ili upate kulipeleka kwenye makao yake, na kuifahamu njia ya kwenda huko kwake.

21 Wewe unapaswa kujua, wewe ambaye umekwisha ishi miaka mingi!

22 “Je, umewahi kuingia katika bohari za theluji, au kuona bohari za mvua ya mawe

23 ambavyo nimevihifadhi kwa ajili ya wakati wa fujo, kwa ajili ya siku ya mapigano na vita?

24 Ipi njia ya kwenda mahali mwanga unapogawanywa, au huko kunakotoka upepo wa mashariki ukasambazwa duniani?

25 “Nani aliyechora angani njia kwa ajili ya mvua? Nani aliyeionesha radi njia yake mawinguni,

26 ikasababisha mvua kunyesha nchini kusikoishi mtu na jangwani ambako hakuna mtu,

27 ili kuiburudisha nchi kavu na kame na kuifanya iote nyasi?

28 “Je, mvua ina baba? Au nani ameyazaa matone ya umande?

29 Je, barafu ilitoka tumboni kwa nani? Nani aliyeizaa theluji?

30 Maji hugeuka kuwa magumu kama jiwe, na uso wa bahari ukaganda.

31 “Angalia makundi ya nyota: Je, unaweza kuifunga minyororo Kilimia, au kuvilegeza vifungo vya Orioni?

32 Je, waweza kuziongoza nyota katika majira yake, au kumwongoza Dubu pamoja na watoto wake?

33 Je, wazijua kanuni zinazotawala mbingu; Je, waweza kuzipangia taratibu zao duniani?

34 “Je, waweza kupaza sauti na kuyaamuru mawingu yakufunike kwa mtiririko wa mvua?

35 Je, wewe ukiamuru umeme umulike, utakujia na kusema: ‘Nipo hapa?’

36 Ni nani aliyemjulisha kwarara kujaa kwa mto Nili au aliyemwambia jogoo kwamba mvua inakuja?

37 Nani mwenye akili ya kuweza kuhesabu mawingu, au kuinamisha viriba vya maji huko mbinguni?

38 ili vumbi duniani igandamane na udongo ushikamane na kuwa matope?

39 “Je, waweza kumwindia simba mawindo yake au kuishibisha hamu ya wana simba;

40 wanapojificha mapangoni mwao, au kulala mafichoni wakiotea?

41 Ni nani awapaye kunguru chakula chao, makinda yao yanaponililia mimi Mungu, na kurukaruka huku na huko kwa njaa?

39

1 “Je, wajua mbuzi wa milimani huzaa lini, au umewahi kuona kulungu akizaa?

2 Je, wajua huchukua mimba kwa muda gani, au siku yenyewe ya kuzaa waijua?

3 “Wajua wakati watakapochuchumaa kuzaa, wakati wa kuzaa watoto wao?

4 Watoto wao hupata nguvu, hukua hukohuko porini, kisha huwaacha mama zao na kwenda zao.

5 “Nani aliyemwacha huru pundamwitu? Nani aliyewaacha waende kwa kuwafungua?

6 Mimi niliwapa jangwa liwe makao yao, mbuga zenye chumvi kuwa makazi yao.

7 Hujitenga kabisa na makelele ya miji, hasikilizi kelele ya kumfanyisha kazi.

8 Hutembeatembea milimani kupata malisho, na kutafuta chochote kilicho kibichi.

9 “Je, nyati atakubali kukutumikia? Au je, atakubali kulala zizini mwako?

10 Je, waweza kumfunga nyati kamba kulima shamba, au avute jembe la kulimia?

11 Je, utamtegemea kwa kuwa ana nguvu nyingi na kumwacha akufanyie kazi zako nzito?

12 Je, wamtazamia nyati akuvunie mavuno yako, na kuleta nafaka mahali pa kupuria?

13 “Mbuni hupigapiga mabawa yake kwa madaha, lakini hawezi kuruka kama korongo.

14 Mbuni huyaacha mayai yake juu ya ardhi ili yapate joto mchangani;

15 lakini hajui kama yanaweza kukanyagwa, au kuvunjwa na mnyama wa porini.

16 Mbuni huwatendea wanawe ukatili kama si wake, hata kazi yake ikiharibika yeye hana wasiwasi;

17 kwa sababu nilimfanya asahau hekima yake, wala sikumpa sehemu yoyote ya akili.

18 Lakini akianza kukimbia, humcheka hata farasi na mpandafarasi.

19 “Je, Yobu, ndiwe uliyewapa farasi nguvu, ukawavika shingoni manyoya marefu?

20 Je, ni wewe unayemfanya farasi aruke kama nzige? Mlio wake wa maringo ni wa ajabu!

21 Huparapara ardhi mabondeni kwa pupa; hukimbilia kwenye mapigano kwa nguvu zake zote.

22 Farasi huicheka hofu, na hatishiki; wala upanga hauwezi kumrudisha nyuma.

23 Silaha wachukuazo wapandafarasi, hugongana kwa sauti na kungaa juani.

24 Farasi husonga mbele, akitetemeka kwa hasira; tarumbeta iliapo, yeye hasimami.

25 Kila ipigwapo tarumbeta, yeye hutoa sauti; huisikia harufu ya vita toka mbali, huusikia mshindo wa makamanda wakitoa amri kwa makelele.

26 “Je, mwewe amejifunza kwako jinsi ya kuruka, na kunyosha mabawa yake kuelekea kusini?

27 Je, tai hupaa juu kwa amri yako, na kuweka kiota chake juu milimani?

28 Tai hufanya makazi yake juu ya miamba mirefu, na ncha kali za majabali ndizo ngome zake.

29 Kutoka huko huotea mawindo, macho yake huyaona kutoka mbali.

30 Makinda yake hufyonza damu; pale ulipo mzoga ndipo alipo tai.”

40

1 Mwenyezi-Mungu akaendelea kumwambia Yobu:

2 “Je, wewe mwenye kuchunguza makosa utashindana na Mungu Mwenye Nguvu? Wewe unayebishana nami Mungu, basi jibu mambo hayo!”

3 Kisha Yobu akamjibu Mwenyezi-Mungu:

4 “Mimi sifai kitu nitakujibu nini? Naufunga mdomo wangu.

5 Nilithubutu kusema na sitasema tena. Nilisisitiza lakini sitaendelea kusema zaidi.”

6 Hapo Mwenyezi-Mungu akamjibu kutoka kimbunga:

7 “Jikaze kama mwanamume. Nitakuuliza, nawe utanijibu.

8 Je, unataka kweli kubatilisha hukumu yangu, kuniona nina hatia ili wewe usiwe na hatia?

9 Je, una nguvu kama mimi Mungu? Waweza kunguruma kwa sauti kama yangu?

10 “Basi, jioneshe kuwa na fahari na ukuu, ujipambe kwa utukufu na fahari.

11 Wamwagie watu hasira yako kuu; mwangalie kila mwenye kiburi na kumwangusha.

12 Mwangalie kila mwenye kiburi na kumporomosha, uwakanyage waovu mahali walipo.

13 Wazike wote pamoja ardhini; mfunge kila mmoja kwa kifungo cha kifo.

14 Hapo nitakutambua, kwamba nguvu yako mwenyewe imekupa ushindi.

15 “Liangalie lile dude Behemothi, nililoliumba kama nilivyokuumba wewe. Hilo hula nyasi kama ng'ombe,

16 lakini mwilini lina nguvu ajabu, na misuli ya tumbo lake ni imara.

17 Huufanya mkia wake mgumu kama mwerezi, mishipa ya mapaja yake imeshonwa pamoja.

18 Mifupa yake ni mabomba ya shaba, viungo vyake ni kama pao za chuma.

19 “Hilo ni la kwanza la ajabu kati ya viumbe vyangu! Ni mimi Muumba wake niwezaye kulishinda.

20 Milima wanamocheza wanyama wote wa porini hutoa chakula chake.

21 Hujilaza chini ya vichaka vya miiba, na kujificha kati ya matete mabwawani.

22 Hujisitiri katika vivuli vya vichaka vya miiba na vya miti iotayo kando ya vijito.

23 Mto ukifurika haliogopi, halitishiki hata mto Yordani ukilifurikia kinywani.

24 Nani awezaye kuliziba macho na kuliteka? Nani awezaye kulitoboa pua kwa mtego?

25 Je, waweza kuvua dude Lewiyathani kwa ndoana, au kuufunga ulimi wake kwa kamba?

26 Je, unaweza kulitia kamba puani mwake, au kulitoboa taya kwa kulabu?

27 Je, wadhani litakusihi uliachilie? Je, litazungumza nawe kwa upole?

28 Je, litafanya mapatano nawe, ulichukue kuwa mtumishi wako milele?

29 Je, utacheza nalo kama ndege, au kulifunga kamba licheze na wajakazi wako?

30 Wadhani wavuvi watashindania bei yake? Je, wafanyabiashara watathubutu kulikata na kugawana?

31 Je, waweza kuichoma ngozi yake kwa mikuki, au kichwa chake kwa mfumo wa kuvua samaki?

32 Jaribu tu kuligusa, uone cha mtema kuni; Kamwe hutarudia tena kufanya hivyo!

41

1 “Yeyote anayeliona hilo dude, hufa moyo na kuzirai.

2 Hakuna mtu yeyote mkali athubutuye kulishtua. Nani, basi awezaye kusimama mbele yangu?

3 Nani aliyenipa kitu, ili nitakiwe kumrudishia? Chochote kilicho chini ya mbingu ni changu.

4 “Sitaacha kukueleza juu ya viungo vya hilo dude au juu ya nguvu zake na umbo lake zuri.

5 Nani awezaye kumbambua vazi lake la nje? Nani awezaye kutoboa deraya lililovaa?

6 Nani awezaye kufungua kinywa chake? Meno yake pande zote ni kitisho!

7 Mgongo wake umefanywa kwa safu za ngao zilizoshikamana pamoja kama kwa mhuri,

8 Kila moja imeshikamana na nyingine, hata hewa haiwezi kupenya katikati yake.

9 Yameunganishwa pamoja, hata haiwezekani kuyatenganisha.

10 Likipiga chafya, mwanga huchomoza, macho yake humetameta kama jua lichomozapo.

11 Kinywani mwake hutoka mienge iwakayo, cheche za moto huruka nje.

12 Puani mwake hufuka moshi, kama vile chungu kinachochemka; kama vile magugu yawakayo.

13 Pumzi yake huwasha makaa; mwali wa moto hutoka kinywani mwake.

14 Shingo yake ina nguvu ajabu, litokeapo watu hukumbwa na hofu.

15 Misuli yake imeshikamana pamoja, imara kama chuma wala haitikisiki.

16 Moyo wake ni mgumu kama jiwe, mgumu kama jiwe la kusagia.

17 Linapoinuka, mashujaa hushikwa na woga, kwa pigo moja huwa wamezirai.

18 Hakuna upanga uwezao kulijeruhi, wala mkuki, mshale au fumo.

19 Kwake chuma ni laini kama unyasi, na shaba kama mti uliooza.

20 Mshale hauwezi kulifanya likimbie; akitupiwa mawe ya teo huyaona kama makapi.

21 Kwake, rungu ni kama kipande cha bua, hucheka likitupiwa fumo kwa wingi.

22 Tumbo lake ni kama limefunikwa na vigae vikali; hukwaruza na kurarua udongo kama chombo cha kupuria.

23 Bahari huisukasuka kama maji yachemkayo, huifanya itoe povu kama chupa ya mafuta.

24 Lipitapo huacha nyuma alama inayongaa; povu jeupe huonekana limeelea baharini.

25 Duniani hakuna kinachofanana nalo; hilo ni kiumbe kisicho na hofu.

26 Huwaona kuwa si kitu wote wenye kiburi; hilo ni mfalme wa wanyama wote wakali.”

42

1 Kisha Yobu akamjibu Mwenyezi-Mungu:

2 “Najua kwamba waweza kila kitu, lolote unalokusudia haliwezi kuzuiliwa.

3 Ulisema kuwa nilithubutu kutatiza mpango wako kijinga. Kweli nilitamka kitu ambacho sikuelewa mambo ya ajabu mno kwangu ambayo sikuwa ninayajua.

4 Uliniambia nisikilize nawe utaniambia; kwamba utaniuliza nami nikujibu.

5 Kweli nilikuwa nimesikia habari zako kwa masikio tu, lakini sasa nakuona kwa macho yangu mwenyewe.

6 Kwa hiyo natubu pamoja na kujipaka mavumbi na majivu, najiona mimi mwenyewe kuwa si kitu kabisa.”

7 Mwenyezi-Mungu alipomaliza kuongea na Yobu, alimwambia Elifazi, Mtemani, “Ghadhabu yangu imewaka dhidi yako na marafiki zako wawili kwani hamkusema ukweli juu yangu kama mtumishi wangu Yobu alivyofanya.

8 Kwa hiyo chukueni mafahali saba na kondoo madume saba, mwende kwa mtumishi wangu Yobu, mkawatoe sadaka ya kuteketezwa kwa ajili yenu. Naye mtumishi wangu Yobu atawaombeeni, nami nitaisikiliza sala yake na kuacha kuwatenda kulingana na upumbavu wenu; maana hamkusema ukweli juu yangu kama mtumishi wangu Yobu alivyofanya.”

9 Basi, Elifazi Mtemani, Bildadi, Mshua na Sofari Mnaamathi, wakafanya kama Mwenyezi-Mungu alivyowaambia. Mwenyezi-Mungu akaipokea sala ya Yobu.

10 Baada ya Yobu kuwaombea rafiki zake, Mwenyezi-Mungu akamrudishia Yobu hali yake ya kwanza. Alimpa maradufu ya yote aliyokuwa nayo hapo awali.

11 Kisha ndugu zake, dada zake na rafiki wote waliomfahamu hapo awali wakamwendea nyumbani kwake, wakala chakula pamoja naye. Wakampa pole na kumfariji kwa ajili ya mateso yote ambayo Mwenyezi-Mungu alikuwa amemletea. Kila mmoja wao akampa Yobu fedha na pete ya dhahabu.

12 Katika miaka ya Yobu iliyofuata Mwenyezi-Mungu alimbariki zaidi kuliko hata alivyokuwa amembariki pale awali. Basi Yobu akawa na kondoo 14,000, ngamia 6,000, ng'ombe 2,000 na punda majike 1,000.

13 Alikuwa pia na watoto wa kiume saba na wa kike watatu.

14 Binti yake wa kwanza alimpa jina Yemima, wa pili Kezia, na wa mwisho Keren-hapuki.

15 Katika nchi yote hiyo hapakuwa na wanawake waliokuwa wazuri kama mabinti wa Yobu. Baba yao akawaachia urithi kama alivyowaachia kaka zao.

16 Baada ya hapo, Yobu aliishi miaka 140, akawaona wajukuu na vitukuu vyake vyote hadi kizazi cha nne.

17 Basi, Yobu akafariki akiwa mzee wa miaka mingi.