1 Neno la Bwana lililomjia Hosea mwana wa Beeri, nyakati za Uzia, Yothamu, Ahazi na Hezekia, wafalme wa Yuda, na Yeroboamu mwana wa Yoashi, mfalme wa Israeli.
2 Mwenyezi-Mungu alipoanza kuongea na Waisraeli kwa njia ya Hosea, alimwambia hivi: “Nenda ukaoe mwanamke mzinzi, uzae naye watoto wa uzinzi, maana watu wa nchi hii wanafanya uzinzi mwingi kwa kuniacha mimi.”
3 Basi, Hosea akaenda, akamwoa Gomeri, binti Diblaimu. Gomeri akapata mimba, akamzalia Hosea mtoto wa kiume.
4 Mwenyezi-Mungu akamwambia Hosea, “Mpe mtoto huyo jina ‘Yezreeli’, maana bado kitambo kidogo tu, nami nitaiadhibu jamaa ya Yehu kwa mauaji aliyoyafanya bondeni Yezreeli. Nitaufutilia mbali ufalme katika taifa la Israeli.
5 Siku hiyo, nitazivunja nguvu za kijeshi za Israeli huko bondeni Yezreeli.”
6 Gomeri alipata mimba tena, akazaa mtoto wa kike. Mwenyezi-Mungu akamwambia Hosea, “Mpe mtoto huyo jina ‘Asiyehurumiwa’, maana sitawahurumia tena Waisraeli wala sitawasamehe.
7 Lakini nitawahurumia watu wa Yuda na kuwaokoa. Mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wao, nitawaokoa, lakini si kwa nguvu za kijeshi, au pinde, au panga, au farasi au wapandafarasi.”
8 Gomeri alipomwachisha kunyonya “Asiyehurumiwa,” alipata mimba tena, akamzalia Hosea mtoto mwingine wa kiume.
9 Mwenyezi-Mungu akamwambia Hosea, “Mpe mtoto huyo jina ‘Siwangu,’ maana nyinyi si watu wangu, wala mimi si wenu.”
10 Lakini idadi ya Waisraeli itakuwa kubwa kama mchanga wa pwani ambao haupimiki wala hauhesabiki. Pale ambapo Mungu aliwaambia, “Nyinyi si watu wangu,” sasa atawaambia, “Nyinyi ni watoto wa Mungu aliye hai.”
11 Watu wa Yuda na wa Israeli wataungana pamoja na kumchagua kiongozi wao mmoja; nao watastawi katika nchi yao. Hiyo itakuwa siku maarufu ya Yezreeli.
1 Basi, waiteni kaka zenu, “Watu wangu,” na dada zenu, “Waliohurumiwa.”
2 Mlaumuni mama yenu mlaumuni, maana sasa yeye si mke wangu wala mimi si mume wake. Mlaumuni aondokane na uasherati wake, ajiepushe na uzinzi wake.
3 La sivyo, nitamvua nguo abaki uchi, nitamfanya awe kama alivyozaliwa. Nitamfanya awe kama jangwa, nitamweka akauke kama nchi kavu. Nitamuua kwa kiu.
4 Na watoto wake sitawahurumia, maana ni watoto wa uzinzi.
5 Mama yao amefanya uzinzi, aliyewachukua mimba amefanya mambo ya aibu. Alisema; “Nitaambatana na wapenzi wangu, ambao hunipa chakula na maji, sufu na kitani, mafuta na divai.”
6 Basi, nitaiziba njia yake kwa miiba, nitamzungushia ukuta, asipate njia ya kutokea nje.
7 Atawafuata wapenzi wake, lakini hatawapata; naam, atawatafuta, lakini hatawaona. Hapo ndipo atakaposema, “Nitarudi kwa mume wangu wa kwanza; maana hapo kwanza nilikuwa nafuu kuliko sasa.”
8 Hakujua kwamba ni mimi niliyempa nafaka, divai na mafuta, niliyemjalia fedha na dhahabu kwa wingi, ambazo alimpelekea Baali.
9 Kwa hiyo wakati wa mavuno nitaichukua nafaka yangu, nitaiondoa divai yangu wakati wake. Nitamnyang'anya nguo zangu za sufu na kitani, ambazo zilitumika kuufunika uchi wake.
10 Nitamvua abaki uchi mbele ya wapenzi wake, wala hakuna mtu atakayeweza kunizuia.
11 Nitazikomesha starehe zake zote, sikukuu zake za mwezi mwandamo na za Sabato, na sikukuu zote zilizoamriwa.
12 Nitaiharibu mizabibu yake na mitini, anayosema ni malipo kutoka kwa wapenzi wake. Nitaifanya iwe misitu, nao wanyama wa porini wataila.
13 Nitamlipiza sikukuu za Baali alizoadhimisha, muda alioutumia kuwafukizia ubani, akajipamba kwa pete zake na johari, na kuwaendea wapenzi wake, akanisahau mimi. Mimi Mwenyezi-Mungu nasema.
14 Kwa hiyo, nitamshawishi, nitampeleka jangwani na kusema naye kwa upole.
15 Huko nitamrudishia mashamba yake ya mizabibu, bonde la Akori nitalifanya lango la tumaini. Atanifuata kwa hiari kama alipokuwa kijana, kama wakati alipotoka katika nchi ya Misri.
16 “Mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Siku hiyo, wewe utaniita ‘Mume wangu,’ na sio tena ‘Baali wangu.’
17 Maana, nitalifanya jina la Baali lisitamkike tena kinywani mwako.
18 Nitafanya agano na wanyama wa porini, ndege wa angani pamoja na vyote vitambaavyo, wasikuumize. Nitatokomeza upinde, upanga na silaha za vita katika nchi, na kukufanya uishi kwa usalama.
19 Nitakufanya mke wangu milele; uwe wangu kwa uaminifu na haki, kwa fadhili na huruma.
20 Naam, nitakuposa kwa uaminifu, nawe utanijua mimi Mwenyezi-Mungu.
21 “Siku hiyo, mimi Mwenyezi-Mungu nasema, nitaikubali haja ya mbingu ya kunyesha mvua, mbingu nazo zitaikubali haja ya ardhi.
22 Ardhi itaikubali haja ya nafaka, divai na mafuta, navyo vitatosheleza mahitaji ya Yezreeli.
23 Nitamwotesha Yezreeli katika nchi; nitamhurumia ‘Asiyehurumiwa’, na wale walioitwa ‘Siwangu’, nitawaambia, ‘Nyinyi ni watu wangu.’ Nao watasema, ‘Wewe ni Mungu wetu.’”
1 Mwenyezi-Mungu aliniambia, “Nenda tena ukampende mwanamke anayependwa na mwanamume mwingine na ambaye ni mzinzi. Mpende kama mimi Mwenyezi-Mungu ninavyowapenda Waisraeli, ingawa wao wanaigeukia miungu mingine na kuwa na uchu wa maandazi ya zabibu kavu.”
2 Basi, nikamnunua huyo mwanamke kwa vipande kumi na vitano vya fedha na magunia mengi ya shayiri.
3 Kisha nikamwambia, “Lazima uwe wangu kwa siku nyingi bila kufanya uzinzi au kuwa mke wa mtu mwingine; nami pia nitakuwa mwaminifu.”
4 Hivyo ndivyo Waisraeli watakavyokuwa: Watakaa kwa muda mrefu bila mfalme au mkuu; bila tambiko, wala mnara wala kizibao cha kifuani wala kinyago.
5 Baadaye, Waisraeli watarudi na kumtafuta Mwenyezi-Mungu, Mungu wao, na kumtafuta mfalme wao, mzawa wa Daudi. Ndipo watakapomcha Mwenyezi-Mungu, na kutazamia wema wake siku za mwisho.
1 Msikilizeni Mwenyezi-Mungu, enyi Waisraeli. Mwenyezi-Mungu anawashutumu wakazi wa nchi hii. “Hamna tena uaminifu wala wema nchini; hamna anayemjua Mungu katika nchi hii.
2 Kuapa, uongo, mauaji, wizi na uzinzi huzuka humo. Umwagaji damu hufuatana mfululizo.
3 Kwa hiyo, nchi yote ni kame, wakazi wake wote wanaangamia pamoja na wanyama wa porini na ndege; hata samaki wa baharini wanaangamizwa.
4 “Lakini watu wasilaumiwe, wasishutumiwe; maana mimi nakushutumu wewe kuhani.
5 Wewe utajikwaa mchana, naye nabii atajikwaa pamoja nawe usiku. Nitamwangamiza mama yako Israeli.
6 Watu wangu wameangamia kwa kutonijua, maana wewe kuhani umekataa mafundisho. Nimekukataa kuwa kuhani wangu. Kwa kuwa umeisahau sheria ya Mungu wako, nami pia nitawasahau watoto wako.
7 “Kadiri makuhani walivyoongezeka, ndivyo wote walivyozidi kuniasi. Basi, nitaigeuza fahari yao kuwa aibu.
8 Wanajishibisha kwa sadaka za watu wangu wenye dhambi. Wana hamu sana ya kuwaona wametenda dhambi.
9 Lakini yatakayowapata watu yatawapata makuhani; nitawaadhibu kwa sababu ya mwenendo wao, nitawalipiza matendo yao wenyewe.
10 Watakula, lakini hawatashiba; watazini, lakini hawatapata watoto, kwa sababu wameniacha mimi Mwenyezi-Mungu, na kufuata miungu mingine.
11 “Divai mpya na ya zamani huondoa maarifa.
12 Watu wangu huomba shauri kutoka kwa mti; kijiti chao cha ramli ndicho kinachowapa kauli. Nia ya kufanya uzinzi imewapotosha; wamefanya uzinzi kwa kufuata miungu mingine, wakaniacha mimi Mungu wao.
13 Wanatambikia kwenye vilele vya milima; naam, wanatoa tambiko vilimani, chini ya mialoni, migude na mikwaju, maana kivuli chao ni kizuri. “Kwa hiyo binti zenu hufanya uzinzi, na bibiarusi wenu hufanya uasherati.
14 Lakini sitawaadhibu binti zenu wanapofanya uzinzi, wala bibi arusi wenu wanapofanya uasherati, maana, wanaume wenyewe ndio wanaofuatana na wazinzi, na kutambikia pamoja nao katika ibada za uzinzi. Watu hawa watovu wa akili hakika wataangamia!
15 “Ama kweli nyinyi Waisraeli ni wazinzi! Lakini, msiwafanye watu wa Yuda wawe na hatia! Msiende mahali patakatifu huko Gilgali, wala msiende kule Beth-aveni. Wala msiape mkisema, ‘Kama Mwenyezi-Mungu aishivyo!’”
16 Waisraeli ni wakaidi kama punda. Kwa nini basi Mungu ashughulike kuwachunga, kama kondoo kwenye malisho mapana?
17 “Watu wa Efraimu wamejifunga na sanamu. Haya! Waache waendelee tu!
18 Kama vile genge la walevi, wanajitosa wenyewe katika uzinzi; wanapendelea aibu kuliko heshima yao.
19 Basi, kimbunga kitawapeperusha, na watayaonea aibu matambiko yao kwa miungu ya uongo.
1 “Haya! Sikilizeni enyi makuhani! Tegeni sikio, enyi Waisraeli! Sikilizeni enyi ukoo wa kifalme! Nyinyi mlipaswa kuzingatia haki, badala yake mmekuwa mtego huko Mizpa, mmekuwa wavu wa kuwanasa huko Tabori.
2 Mmechimba shimo refu la kuwanasa huko Shitimu. Lakini mimi nitawaadhibuni nyote.
3 Nawajua watu wa Efraimu, Waisraeli hawakufichika kwangu. Nyinyi watu wa Efraimu mmefanya uzinzi, watu wote wa Israeli wamejitia najisi.
4 “Matendo yao yanawazuia wasimrudie Mungu wao. Mioyoni mwao wamejaa uzinzi; hawanijui mimi Mwenyezi-Mungu.
5 Kiburi cha Waisraeli chaonekana wazi; watu wa Efraimu watajikwaa katika hatia yao, nao watu wa Yuda watajikwaa pamoja nao.
6 Watakwenda na makundi yao ya kondoo na ng'ombe, kumtafuta Mwenyezi-Mungu; lakini hawataweza kumpata, kwa sababu amejitenga nao.
7 Wamevunja uaminifu kwa Mwenyezi-Mungu, wamezaa watoto walio haramu. Mwezi mwandamo utawaangamiza, pamoja na mashamba yao.
8 “Pigeni baragumu huko Gibea, na tarumbeta huko Rama. Pigeni king'ora huko Beth-aveni. Enyi watu wa Benyamini, adui yenu yuko nyuma!
9 Siku nitakapotoa adhabu Efraimu itakuwa kama jangwa! Ninachotangaza miongoni mwa makabila ya Israeli, ni jambo litakalotukia kwa hakika.
10 Viongozi wa Yuda wamekuwa wenye kubadili mipaka ya ardhi. Mimi nitawamwagia hasira yangu kama maji.
11 Efraimu ameteswa, haki zake zimetwaliwa; kwani alipania kufuata upuuzi.
12 Hivyo mimi Mungu niko kama nondo kwa Efraimu, kama donda baya kwa watu wa Yuda.
13 Watu wa Efraimu walipogundua ugonjwa wao, naam, watu wa Yuda walipogundua donda lao, watu wa Efraimu walikwenda Ashuru kuomba msaada kwa mfalme mkuu; lakini yeye hakuweza kuwatibu, hakuweza kuponya donda lenu.
14 Maana mimi nitakuwa kama simba kwa Efraimu, kama mwanasimba kwa watu wa Yuda. Mimi mwenyewe nitawararua na kuondoka, nitawachukua na hakuna atakayewaokoa.
15 Nitarudi mahali pangu na kujitenga nao mpaka wakiri kosa lao na kunirudia. Taabu zao zitawafundisha wanitafute, wakisema:
1 “ ‘Twendeni, tukamrudie Mwenyezi-Mungu! Yeye mwenyewe ameturarua, lakini yeye mwenyewe atatuponya. Yeye mwenyewe ametujeruhi, lakini yeye mwenyewe atatibu majeraha yetu.
2 Baada ya siku mbili, atatupa uhai tena, naam, siku ya tatu atatufufua ili tuweze kuishi pamoja naye.
3 Basi tumtambue, tujitahidi kumjua Mwenyezi-Mungu. Kuja kwake ni hakika kama alfajiri, yeye atatujia kama manyunyu, kama mvua za masika ziinyweshayo ardhi.’”
4 Lakini Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Nitakutendea nini ee Efraimu? Nikufanyie nini ee Yuda? Upendo wenu kwangu ni kama ukungu wa asubuhi, kama umande unaotoweka upesi.
5 Ndiyo maana nimewavamia kwa njia ya manabii, nimewaangamiza kwa maneno yangu, hukumu yangu huchomoza kama pambazuko.
6 Maana ninachotaka kwenu ni upendo na si tambiko, Kumjua Mungu na si kutoa sadaka za kuteketezwa.
7 “Lakini mlilivunja agano langu kama mlivyofanya mjini Adamu; huko walinikosea uaminifu.
8 Gileadi ni mji wa waovu, umetapakaa damu.
9 Kama wanyang'anyi wamwoteavyo mtu njiani, ndivyo na makuhani walivyojikusanya na kuvizia. Wanaua watu njiani kuelekea Shekemu, naam, wanatenda uovu kupindukia.
10 Nimeona jambo la kuchukiza sana miongoni mwa Waisraeli: Watu wa Efraimu wanakimbilia miungu mingine naam, Waisraeli wamejitia unajisi.
11 Nawe Yuda hali kadhalika, nimekupangia wakati utakapovuna adhabu.
1 Kila nikitaka kuwarekebisha watu wangu, ninapotaka kuwaponya Waisraeli, uovu wa watu wa Efraimu hufunuliwa, matendo mabaya ya Samaria hujitokeza. Wao huongozwa na udanganyifu, kwenye nyumba wezi huvunja nje barabarani wanyang'anyi huvamia.
2 Hawafikiri hata kidogo kwamba mimi nayakumbuka maovu yao yote. Sasa maovu yao yamewabana. Yote waliyotenda yako mbele yangu.
3 “Wanamfurahisha mfalme kwa maovu yao wanawafurahisha wakuu kwa uhaini wao.
4 Wote ni wazinzi; wao ni kama tanuri iliyowashwa moto ambao mwokaji hauchochei tangu akande unga mpaka mkate utakapoumuka.
5 Kwenye sikukuu ya mfalme, waliwalewesha sana maofisa wake; naye mfalme akashirikiana na wahuni.
6 Kama tanuri iwakavyo, mioyo yao huwaka kwa hila; usiku kucha hasira yao hufuka moshi, ifikapo asubuhi, hulipuka kama miali ya moto.
7 Wote wamewaka hasira kama tanuri, na wanawaangamiza watawala wao. Wafalme wao wote wameanguka, wala hakuna anayeniomba msaada.
8 “Efraimu amechanganyika na watu wa mataifa. Anaonekana kama mkate ambao haukugeuzwa.
9 Wageni wamezinyonya nguvu zake, wala yeye mwenyewe hajui; mvi zimetapakaa kichwani mwake, lakini mwenyewe hana habari.
10 Kiburi cha Waisraeli chashuhudia dhidi yao, hawanirudii mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wao; wala hawanitafuti kwa matukio hayo yote.
11 Efraimu ni kama njiwa, mjinga asiye na akili; mara yuko Misri, mara Ashuru kuomba.
12 Watakapokwenda nitatandaza wavu wangu niwanase, nitawaangusha chini kama ndege wa angani; nitamwaadhibu kadiri ya ripoti ya maovu yao.
13 Ole wao kwa kuwa wameniacha! Maangamizi na yawapate, maana wameniasi. Nilitaka kuwakomboa, lakini wanazua uongo dhidi yangu.
14 “Wananililia, lakini si kwa moyo. Wanagaagaa na kujikatakata vitandani mwao, kusudi nisikilize dua zao za nafaka na divai; lakini wanabaki waasi dhidi yangu.
15 Mimi ndimi niliyeiimarisha mikono yao, lakini wanafikiria maovu dhidi yangu.
16 Wanaigeukia miungu batili, wako kama uta uliolegea. Viongozi wao watakufa kwa upanga, kwa sababu ya maneno yao ya kiburi. Kwa hiyo, watadharauliwa nchini Misri.
1 “Pigeni baragumu! Adui anakuja kama tai kuivamia nyumba ya Mwenyezi-Mungu, kwa kuwa wamelivunja agano langu na kuiasi sheria yangu.
2 Waisraeli hunililia wakisema: ‘Mungu wetu, sisi tunakujua.’
3 Lakini Israeli amepuuza mambo mema, kwa hiyo, sasa adui watamfuatia.
4 “Walijiwekea wafalme bila kibali changu, walijiteulia viongozi ambao sikuwatambua. Wamejitengenezea miungu ya fedha na dhahabu, jambo ambalo litawaangamiza.
5 Watu wa Samaria, naichukia sanamu yenu ya ndama. Hasira yangu inawaka dhidi yenu. Mtaendelea mpaka lini kuwa na hatia?
6 Nanyi Waisraeli ni hivyohivyo! Na sanamu yenu hiyo fundi ndiye aliyeitengeneza. Yenyewe si Mungu hata kidogo. Naam! Sanamu ya ndama ya Samaria itavunjwavunjwa!
7 “Wanapanda upepo, watavuna kimbunga! Mimea yao ya nafaka iliyo mashambani haitatoa nafaka yoyote. Na hata kama ikizaa, mazao yake yataliwa na wageni.
8 Waisraeli wamemezwa; sasa wamo kati ya mataifa mengine, kama chombo kisicho na faida yoyote;
9 kwa kuwa wamekwenda kuomba msaada Ashuru. Efraimu ni punda anayetangatanga peke yake; Efraimu amekodisha wapenzi wake.
10 Wametafuta wapenzi kati ya watu wa mataifa, lakini mimi nitawakusanya mara. Na hapo watasikia uzito wa mzigo, ambao mfalme wa wakuu aliwatwika.
11 “Watu wa Efraimu wamejijengea madhabahu nyingi, na madhabahu hizo zimewazidishia dhambi.
12 Hata kama ningewaandikia sheria zangu mara nyingi, wao wangeziona kuwa kitu cha kigeni tu.
13 Wanapenda kutoa tambiko, na kula nyama yake; lakini mimi Mwenyezi-Mungu sipendezwi hata kidogo. Mimi nayakumbuka makosa yao; nitawaadhibu kwa dhambi zao; nitawarudisha utumwani Misri.
14 Waisraeli wamemsahau Muumba wao, wakajijengea majumba ya fahari; watu wa Yuda wamejiongezea miji ya ngome, lakini mimi nitaipelekea moto miji hiyo, na kuziteketeza ngome zao.”
1 Msifurahi enyi Waisraeli! Msifanye sherehe kama mataifa mengine; maana, mmekuwa wazinzi kwa kumwacha Mungu wenu. Mmefurahia malipo ya uzinzi, kila mahali pa kupuria nafaka.
2 Lakini ngano na mapipa ya divai haitawalisha, hamtapata divai mpya.
3 Hawatakaa katika nchi ya Mwenyezi-Mungu; naam, watu wa Efraimu watarudi utumwani Misri; watakula vyakula najisi huko Ashuru.
4 Hawatamtolea Mwenyezi-Mungu sadaka ya divai, wala hawatamfurahisha kwa tambiko zao. Chakula chao kitakuwa kama cha matanga, wote watakaokila watatiwa unajisi. Kitakuwa chakula cha kuwashibisha tu, hakitafaa kuletwa nyumbani kwa Mwenyezi-Mungu.
5 Mtafanya nini katika sikukuu ile iliyopangwa, au katika karamu ya Mwenyezi-Mungu?
6 Mtakapoyakimbia maangamizi ya nchi yenu, Misri itawakaribisheni kwake, lakini makaburi yenu yawangoja huko Memfisi. Magugu yatamiliki hazina zenu za fedha, miiba itajaa katika mahema yenu.
7 Siku za adhabu zimewadia, naam, siku za kulipiza kisasi zimefika; Waisraeli lazima wautambue wakati huo! Nyinyi mnasema, “Nabii ni mpumbavu; anayeongozwa na roho ni mwendawazimu.” Mnasema hivyo kwa sababu ya uovu wenu mkubwa, kwa sababu ya chuki yenu kali dhidi yake.
8 Nabii ni mlinzi wa Waefraimu kwa niaba ya Mungu; lakini, kokote aendako anategewa mtego kama ndege. Hata nyumbani mwa Mungu wake anachukiwa.
9 Nyinyi mmezama katika uovu, kama ilivyokuwa kule Gibea. Mungu atayakumbuka makosa yao, na kuwaadhibu kwa dhambi zao.
10 Mwenyezi-Mungu asema: “Nilipowakuta Waisraeli walikuwa kama zabibu jangwani. Nilipowaona wazee wenu walikuwa bora kama tini za kwanza. Lakini mara walipofika huko Baal-peori, walijiweka wakfu kuabudu chukizo Baali, wakawa chukizo kama hicho walichokipenda.
11 Fahari ya Efraimu itatoweka kama ndege; watoto hawatazaliwa tena, hakutakuwa na watoto wa kuzaliwa, wala hakutakuwa na kuchukuliwa mimba!
12 Hata kama wakilea watoto, sitamwacha hai hata mmoja wao. Ole wao, nitakapowaacha peke yao!”
13 Kama nilivyokwisha ona hapo kwanza, Efraimu alikuwa kama mtende mchanga penye konde zuri; lakini sasa Efraimu itamlazimu kuwapeleka watoto wake wauawe.
14 Uwaadhibu watu hawa ee Mwenyezi-Mungu! Lakini utawaadhibu namna gani? Uwafanye wanawake wao kuwa tasa; uwafanye wakose maziwa ya kunyonyesha watoto wao!
15 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Uovu wao wote ulianzia Gilgali; huko ndiko nilipoanza kuwachukia. Kwa sababu ya uovu wa matendo yao, nitawafukuza nyumbani kwangu. Sitawapenda tena. Viongozi wao wote ni waasi.
16 Watu wa Efraimu wamepigwa, wamekuwa kama mti wenye mzizi mkavu, hawatazaa watoto wowote. Hata kama wakizaa watoto, nitawaua watoto wao wawapendao.”
17 Kwa vile wamekataa kumsikiliza, Mungu wangu atawatupa; wao watatangatanga kati ya mataifa.
1 Waisraeli walikuwa kama mzabibu mzuri, mzabibu wenye kuzaa matunda. Kadiri matunda yalivyozidi kuongezeka, ndivyo walivyozidi kujijengea madhabahu. Kadiri nchi yao ilivyozidi kustawi, ndivyo walivyozidi kupamba nguzo zao za ibada.
2 Mioyo yao imejaa udanganyifu. Sasa ni lazima wawajibike kwa hatia yao. Mwenyezi-Mungu atazibomoa madhabahu zao na kuziharibu nguzo zao.
3 Wakati huo watasema: “Hatuna tena mfalme, kwa kuwa hatumchi Mwenyezi-Mungu; lakini, naye mfalme atatufanyia nini?”
4 Wanachosema ni maneno matupu; wanaapa na kufanya mikataba ya bure; haki imekuwa si haki tena, inachipua kama magugu ya sumu shambani.
5 Wakazi wa Samaria watatetemeka kwa sababu ya ndama wa huko Betheli. Watu wake watamwombolezea ndama huyo, hata makuhani wanaomwabudu watamlilia; kwani fahari ya ndama huyo imeondolewa.
6 Kinyago hicho kitapelekwa Ashuru, kama ushuru kwa mfalme mkuu. Watu wa Efraimu wataaibishwa, Waisraeli watakionea aibu kinyago chao.
7 Mfalme wa Samaria atachukuliwa, kama kipande cha mti juu ya maji.
8 Mahali pa kuabudia vilimani pa Aweni, dhambi ya Waisraeli, pataharibiwa. Miiba na magugu vitamea katika madhabahu zao. Nao wataiambia milima, “Tufunikeni” na vilima, “Tuangukieni!”
9 Enyi Waisraeli, nyinyi mmetenda dhambi tangu kule Gibea, na bado mnaendelea. Hakika vita vitawaangamiza hukohuko Gibea.
10 Nitawajia watu hawa wapotovu na kuwaadhibu; watu wa mataifa watakusanyika kuwashambulia, watakapoadhibiwa kwa ajili ya dhambi zao nyingi.
11 Efraimu ni ndama aliyefundishwa vizuri, akapenda kupura nafaka. Lakini sasa shingo yake nzuri nitaifunga nira. Yuda atalima kwa jembe yeye mwenyewe, naam, Yakobo atakokota jembe la kupalilia.
12 Pandeni wema kwa faida yenu, nanyi mtavuna upendo; limeni mashamba yaliyoachwa, maana wakati wa kunitafuta mimi Bwana umefika nami nitawanyeshea baraka.
13 Lakini nyinyi mmepanda uovu, nyinyi mmevuna dhuluma; mmekula matunda ya uongo wenu. Wewe Israeli ulitegemea nguvu zako mwenyewe, na wingi wa askari wako.
14 Kwa hiyo msukosuko wa vita utawajia watu wako; ngome zako zote zitaharibiwa, kama Shalmani alivyoharibu Beth-arbeli vitani, kina mama wakapondwa pamoja na watoto wao.
15 Ndivyo itakavyokuwa kwenu enyi watu wa Betheli, kwa sababu ya uovu wenu mkuu. Kutakapopambazuka mfalme wa Israeli atawatokomeza.
1 “Israeli alipokuwa mtoto, nilimpenda, Kutoka Misri nilimwita mwanangu.
2 Lakini kadiri nilivyozidi kuwaita, ndivyo walivyozidi kwenda mbali nami; waliendelea kuyatambikia Mabaali, na kuvifukizia ubani vinyago vya miungu.
3 Mimi ndiye niliyemfundisha Efraimu kutembea! Mimi mwenyewe niliwachukua mikononi mwangu; lakini hawakutambua kuwa mimi ndiye niliyewatunza.
4 Niliwaongoza kwa kamba za huruma naam, kwa kamba za upendo; kama baba amwinuaye mtoto mpaka shavuni mwake, ndivyo nami nilivyokuwa kwao. Mimi niliinama chini na kuwalisha.
5 Basi, watarudi nchini Misri; watatawaliwa na mfalme wa Ashuru, kwa sababu wamekataa kunirudia.
6 “Upanga utavuma katika miji yao, utavunjavunja miimo ya malango yake na kuwaangamiza katika ngome zao.
7 Watu wangu wamepania kuniacha mimi, wakiitwa waje juu, hakuna hata mmoja anayeweza.
8 Ewe Efraimu, nawezaje kukuacha? Nawezaje kukutupa ewe Israeli? Nitawezaje kukufanya kama mji wa Adma? Nitawezaje kukutenda kama Seboimu! Nazuiwa na moyo wangu; huruma yangu imezidi kuwa motomoto.
9 Nitaizuia hasira yangu kali; sitamwangamiza tena Efraimu, maana mimi ni Mungu, wala si binadamu. “Mimi ndimi Mtakatifu miongoni mwenu, nami sitakuja kuwaangamiza.
10 “Watanifuata mimi Mwenyezi-Mungu ningurumaye kama simba; nitakaponguruma watanijia toka magharibi wakitetemeka.
11 Watakuja kutoka Misri wakitetemeka kama ndege, wataruka kutoka Ashuru kama hua nami nitawarudisha makwao; mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
12 Watu wa Efraimu wananirundikia uongo, na Waisraeli udanganyifu. Watu wa Yuda, wananiasi mimi Mungu Mtakatifu.
1 Watu wa Efraimu wananirundikia uongo, na Waisraeli udanganyifu. Watu wa Yuda, wananiasi mimi Mungu Mtakatifu.
2 “Watu wa Efraimu wanachunga upepo kutwa nzima wanafukuza upepo wa mashariki. Wanazidisha uongo na ukatili, wanafanya mkataba na Ashuru na kupeleka mafuta Misri.”
3 Mwenyezi-Mungu ana mashtaka dhidi ya Yuda; atawaadhibu wazawa wa Yakobo kadiri ya makosa yao, na kuwalipa kadiri ya matendo yao.
4 Yakobo akiwa bado tumboni mwa mama yake, alimshika kisigino kaka yake. Na alipokuwa mtu mzima alishindana na Mungu.
5 Alipambana na malaika, akamshinda; alilia machozi na kuomba ahurumiwe. Huko Betheli, alikutana na Mungu, huko Mungu aliongea naye.
6 Mwenyezi-Mungu, wa majeshi, Mwenyezi-Mungu, ndilo jina lake. Lakini nyinyi mrudieni Mungu wenu. Zingatieni upendo na haki, mtumainieni Mungu wenu daima.
7 “Efraimu ni sawa na mfanyabiashara atumiaye mizani danganyifu, apendaye kudhulumu watu.
8 Efraimu amesema, ‘Mimi ni tajiri! Mimi nimejitajirisha! Hamna ubaya kupata faida. Hata hivyo, hilo si kosa!’”
9 Mwenyezi-Mungu asema, “Mimi ni Mwenyezi-Mungu, Mungu wako; mimi ndimi niliyekutoa nchini Misri! Mimi nitakukalisha tena katika mahema, kama ufanyavyo sasa kwa siku chache tu, wakati wa sikukuu ya vibanda.
10 Mimi niliongea na manabii; ni mimi niliyewapa maono mengi, na kwa njia yao natangaza mpango wangu.
11 Huko Gileadi ni mahali pa dhambi; huko Gilgali walitambika fahali, kwa hiyo madhabahu zao zitakuwa marundo ya mawe kwenye mitaro shambani.”
12 Yakobo alikimbia nchi ya Aramu akiwa huko alifanya kazi apate mke, akachunga kondoo ili apate mke.
13 Kwa nabii Mwenyezi-Mungu aliwatoa Waisraeli nchini Misri, na kwa nabii Mungu aliwahifadhi.
14 Waefraimu wamemchukiza Mwenyezi-Mungu sana. Lakini Mwenyezi-Mungu atawalipiza makosa yao, atawaadhibu kwa mambo maovu waliyotenda.
1 Waefraimu waliponena, watu walitetemeka; Waefraimu walikuwa na uwezo mkubwa huko Israeli, lakini walianza kumwabudu Baali, wakajiletea kifo.
2 Waefraimu wameendelea kutenda dhambi, wakajitengenezea sanamu za kusubu, sanamu zilizotengenezwa kwa ustadi wao, zote zikiwa kazi ya mafundi. Wanasema, “Haya zitambikieni!” Wanaume wanabusu ndama!
3 Basi, watatoweka kama ukungu wa asubuhi, kama umande utowekao upesi; kama makapi yanayopeperushwa mahali pa kupuria, kama moshi unaotoka katika bomba.
4 Mwenyezi-Mungu asema: “Lakini mimi, Mwenyezi-Mungu, ni Mungu wenu, ambaye niliwatoa nchini Misri; hamna mungu mwingine ila mimi, wala hakuna awezaye kuwaokoeni.
5 Ni mimi niliyewatunza mlipokuwa jangwani, katika nchi iliyokuwa ya ukame.
6 Lakini mlipokwisha kula na kushiba, mlianza kuwa na kiburi, mpaka mkanisahau.
7 Basi, nitakuwa kama simba kwenu nyote; nitawavizieni kama chui njiani.
8 Nitawarukieni kama dubu aliyenyang'anywa watoto wake. Nitawararua vifua vyenu na kuwala papo hapo kama simba; nitawararua vipandevipande kama mnyama wa porini.
9 “Nitawaangamiza, enyi Waisraeli. Nani ataweza kuwasaidia?
10 Yuko wapi sasa mfalme wenu awaokoe? Wako wapi wale wakuu wenu wawalinde? Nyinyi ndio mlioomba: ‘Tupatie mfalme na wakuu watutawale.’
11 Kwa hasira yangu mimi nikawapa mfalme, kisha nikamwondoa kwa ghadhabu yangu.
12 “Uovu wa Efraimu uko umeandikwa, dhambi yake imehifadhiwa ghalani.
13 Maumivu kama ya kujifungua mtoto yanamfikia. Lakini yeye ni mtoto mpumbavu; wakati ufikapo wa kuzaliwa yeye hukataa kutoka tumboni kwa mama!
14 Yanibidi kuwakomboa hawa watu kutoka kuzimu; sharti niwaokoe kutoka kifoni! Ewe Kifo, yako wapi maafa yako? Ewe Kuzimu, yako wapi maangamizi yako? Mimi sitawaonea tena huruma!
15 “Hata kama Efraimu atastawi kama nyasi, mimi Mwenyezi-Mungu nitavumisha upepo wa mashariki, upepo utakaozuka huko jangwani, navyo visima vyake vitakwisha maji, chemchemi zake zitakauka. Hazina zake zote za thamani zitanyakuliwa.”
16 Watu wa Samaria wataadhibiwa kwa kosa lao. Kwa sababu wamemwasi Mungu wao. Watauawa kwa upanga, vitoto vyao vitapondwapondwa, na kina mama wajawazito watatumbuliwa.
1 Enyi Waisraeli, mrudieni Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu. Mmejikwaa kwa sababu ya uovu wenu.
2 Ombeni toba kwake, mrudieni na kumwambia: “Utusamehe uovu wote, upokee zawadi zetu, nasi tutakusifu kwa moyo.
3 Ashuru haitatuokoa, hatutategemea tena farasi wa vita. Hatutaviita tena: ‘Mungu wetu’ hivyo vinyago tulivyochonga wenyewe. Kwako ee Mungu yatima hupata huruma.”
4 Mwenyezi-Mungu asema, “Nitaponya utovu wao wa uaminifu; nitawapenda tena kwa hiari yangu, maana sitawakasirikia tena.
5 Nitakuwa kama umande kwa Waisraeli nao watachanua kama yungiyungi, watakuwa na mizizi kama mwerezi wa Lebanoni.
6 Chipukizi zao zitatanda na kuenea, uzuri wao utakuwa kama mizeituni, harufu yao nzuri kama maua ya Lebanoni.
7 Watarudi na kuishi chini ya ulinzi wangu, watastawi kama bustani nzuri. Watachanua kama mzabibu, harufu yao nzuri kama ya divai ya Lebanoni.
8 Enyi watu wa Efraimu, mna haja gani tena na sanamu? Mimi ndiye ninayesikiliza sala zenu, mimi ndiye ninayewatunzeni. Mimi nitawapa kivuli kama mberoshi, kutoka kwangu mtapata matunda yenu.
9 Yeyote aliye na hekima ayaelewe mambo haya, mtu aliye na busara ayatambue. Maana njia za Mwenyezi-Mungu ni nyofu; watu wanyofu huzifuata, lakini wakosefu hujikwaa humo.”