1 Baada ya kifo cha Shauli, Daudi alirudi baada ya kuwashinda Waamaleki, akakaa Siklagi kwa muda wa siku mbili.
2 Siku iliyofuata, mtu mmoja kutoka kambi ya Shauli, mavazi yake yakiwa yamechanwa kwa huzuni na akiwa na mavumbi kichwani alimwendea Daudi. Alipomfikia Daudi, alijitupa chini mbele yake akamsujudia.
3 Daudi akamwambia, “Unatoka wapi?” Naye akamwambia, “Nimetoroka kutoka kambi ya Waisraeli.”
4 Daudi akamwambia, “Niambie mambo yalivyokuwa huko.” Yule mtu akamjibu, “Watu wetu wameyakimbia mapigano na wengi wetu wameuawa. Zaidi ya hayo, Shauli na mwanawe Yonathani pia wameuawa.”
5 Daudi akamwuliza yule kijana, “Unajuaje kuwa Shauli na Yonathani mwanawe wamekufa?”
6 Yule kijana akamjibu, “Kwa bahati, nilikuwapo mlimani Gilboa. Nilimwona Shauli ameegemea mkuki wake na magari ya wapandafarasi ya adui zake yalikuwa yanamsonga sana.
7 Shauli alipotazama nyuma, aliniona, akaniita. Nilipoitika,
8 yeye aliniuliza mimi ni nani, nami nikamwambia kuwa mimi ni Mmaleki.
9 Hapo, akaniambia, ‘Karibia uniue maana nimejeruhiwa vibaya na maumivu ni makali. Lakini bado ningali hai’.
10 Hivyo, nilikwenda karibu naye na kumuua, kwa sababu nilikuwa na uhakika kuwa akianguka chini, hataweza kuishi zaidi. Lakini taji iliyokuwa kichwani pake na kikuku kilichokuwa mkononi mwake, vyote nimekuletea wewe, bwana wangu.”
11 Daudi akayashika mavazi yake na kuyararua kwa huzuni. Hata watu waliokuwa pamoja na Daudi wakafanya vivyo hivyo.
12 Wakaomboleza, wakalia na kufunga mpaka jioni kwa ajili ya Shauli, Yonathani mwanawe, na nchi ya Waisraeli, watu wa Mwenyezi-Mungu, kwa kuwa wengi wao waliuawa vitani.
13 Daudi akamwuliza yule kijana aliyempasha habari, “Unatoka wapi?” Yeye akajibu, “Mimi ni Mmaleki, lakini ninaishi katika nchi yako kama mgeni.”
14 Daudi akamwuliza, “Ilikuwaje wewe hukuogopa kuunyosha mkono wako na kumuua mtu aliyeteuliwa na Mwenyezi-Mungu kwa kupakwa mafuta?”
15 Kisha, Daudi akamwita mmoja wa vijana wake akamwambia, “Muue mtu huyu!” Yule kijana alimpiga yule Mmaleki, naye akafa.
16 Daudi akasema, “Uwajibike wewe mwenyewe kwa kifo chako, maana umejishuhudia wewe mwenyewe kwa mdomo wako ukisema, ‘Nimemuua mtu aliyeteuliwa na Mwenyezi-Mungu kwa kupakwa mafuta.’”
17 Daudi aliimba ombolezo lifuatalo kwa ajili ya Shauli na mwanawe Yonathani.
18 Daudi alisema watu wa Yuda wafundishwe ombolezo hilo, nalo limeandikwa katika kitabu cha Yashari. Daudi aliimba,
19 “Walio fahari yako, ee Israeli, wameuawa milimani pako. Jinsi gani mashujaa walivyoanguka!
20 Jambo hilo msiuambie mji wa Gathi wala katika mitaa ya Ashkeloni. La sivyo, wanawake Wafilisti watashangilia, binti za wasiotahiriwa, watafurahi.
21 “Enyi milima ya Gilboa, msiwe na umande au mvua juu yenu. Wala mashamba yenu daima yasitoe chochote. Maana huko ngao za shujaa zilitiwa najisi, ngao ya Shauli haikupakwa mafuta.
22 “Upinde wa Yonathani kamwe haukurudi nyuma, upanga wa Shauli kamwe haukurudi bure, daima ziliua wengi. Naam, ziliua mashujaa.
23 “Shauli na Yonathani, watu wa ajabu na wakupendeza. Maishani na kifoni hawakutengana. Walikuwa wepesi kuliko tai, naam, wenye nguvu kuliko simba.
24 “Wanawake wa Israeli, mlilieni Shauli! Aliwavika mavazi mekundu ya fahari, aliyatarizi mavazi yenu kwa dhahabu.
25 “Jinsi gani mashujaa walivyoanguka! Wamekufa wakiwa katika mapambano. Yonathani analala, akiwa ameuawa milimani.
26 Nasikitika kwa ajili yako, ndugu yangu Yonathani. Umekuwa kwangu daima mtu wa kupendeza, pendo lako kwangu limekuwa la ajabu, la ajabu kuliko la mwanamke.
27 “Jinsi gani mashujaa wameanguka, na silaha zao zimeachwa, hazina kazi.”
1 Baada ya mambo haya, Daudi alimwomba Mwenyezi-Mungu shauri, akasema, “Je, niende kwenye mji mmojawapo wa miji ya Yuda?” Mwenyezi-Mungu akamwambia, “Nenda!” Daudi akamwuliza, “Niende mji upi?” Mwenyezi-Mungu akamjibu, “Nenda kwenye mji wa Hebroni.”
2 Hivyo, Daudi alikwenda Hebroni, pamoja na wake zake wawili, Ahinoamu wa Yezreeli, na Abigaili, mjane wa Nabali, kutoka mji wa Karmeli.
3 Aliwachukua watu wake, kila mtu akiwa pamoja na jamaa yake; nao wakafanya makao yao katika miji iliyokuwa kandokando ya Hebroni.
4 Watu wa Yuda walimwendea Daudi huko Hebroni wakampaka mafuta awe mfalme wao. Daudi aliposikia kuwa watu wa Yabesh-gileadi ndio waliomzika Shauli,
5 aliwatuma watu huko Yabesh-gileadi na ujumbe: “Mwenyezi-Mungu na awabariki kwa maana mlionesha utii wenu kwa Shauli, bwana wenu, kwa kumzika.
6 Sasa, Mwenyezi-Mungu awafadhili na kuwa mwaminifu kwenu. Nami nitawatendea mema kutokana na jambo mlilolitenda.
7 Lakini muwe imara na mashujaa. Shauli, bwana wenu, amekufa, na watu wa Yuda wamenipaka mafuta niwe mfalme wao.”
8 Abneri mwana wa Neri, kamanda wa jeshi la Shauli alikuwa amemchukua Ishboshethi mwana wa Shauli na kumpeleka huko Mahanaimu.
9 Huko, Abneri akamtawaza Ishboshethi kuwa mfalme wa nchi ya Gileadi, Ashuru, Yezreeli, Efraimu na Benyamini na Israeli yote.
10 Ishboshethi alikuwa na umri wa miaka arubaini alipoanza kuitawala Israeli, naye alitawala kwa muda wa miaka miwili. Lakini kabila la Yuda lilimfuata Daudi.
11 Daudi alikuwa mfalme wa kabila la Yuda kwa muda wa miaka saba na nusu, makao yake yalikuwa huko Hebroni.
12 Abneri mwana wa Neri, pamoja na maofisa wa Ishboshethi, mwana wa Shauli, waliondoka Mahanaimu na kwenda Gibeoni.
13 Yoabu mwana wa Seruya na watumishi wengine wa Daudi, nao walitoka na kukutana na Abneri na watu aliokuwa nao kwenye bwawa lililoko huko Gibeoni. Kikosi kimoja upande mmoja wa bwawa na kingine upande mwingine.
14 Abneri akamwambia Yoabu, “Waruhusu vijana wapambane mbele yetu!” Yoabu akamjibu, “Sawa.”
15 Ndipo vijana ishirini na wanne wakatolewa: Upande wa kabila la Benyamini na Ishboshethi mwana wa Shauli, vijana kumi na wawili; na upande wa Daudi vijana kumi na wawili.
16 Kila mmoja alimkamata adui yake kichwani, akamchoma mpinzani wake upanga, hivyo wote wawili wakaanguka chini, wamekufa. Hivyo, mahali hapo pakaitwa Helkath-hazurimu. Mahali hapo pako huko Gibeoni.
17 Vita vya siku hiyo vilikuwa vikali. Abneri na watu wa Israeli walipigwa vibaya na watu wa Daudi.
18 Wana watatu wa Seruya: Yoabu, Abishai na Asaheli walikuwapo hapo. Asaheli alikuwa na mbio kama paa.
19 Asaheli alimfuatia Abneri moja kwa moja bila kugeuka kulia wala kushoto.
20 Abneri alipoangalia nyuma na kumwona Asaheli, alimwambia, “Je, ni wewe Asaheli?” Yeye akamjibu, “Naam, ni mimi.”
21 Abneri akamwambia, “Geukia kulia au kushoto, umkamate kijana mmoja na kuchukua nyara zake.” Lakini Asaheli hakuacha kumfuatia.
22 Abneri akamwambia Asaheli mara ya pili, “Acha kunifuatia. Kwa nini nikuue? Nitawezaje kuonana na kaka yako Yoabu?”
23 Lakini Asaheli alikataa. Hivyo Abneri akampiga mkuki tumboni kinyumenyume, na mkuki huo ukatokeza mgongoni kwa Asaheli. Asaheli akaanguka chini, na kufa papo hapo. Watu wote waliofika mahali alipofia Asaheli, walisimama kimya.
24 Lakini Yoabu na Abishai walimfuatia Abneri. Jua lilipokuwa linatua, wakafika kwenye mlima wa Ama, ulioko mashariki ya Gia, katika barabara iendayo jangwa la Gibeoni.
25 Watu wa kabila la Benyamini wakajikusanya pamoja wakawa nyuma ya Abneri, hivyo wakaunda kikosi chao; nao wakasimama juu ya mlima.
26 Kisha Abneri akamwita Yoabu, “Je, tutapigana siku zote? Je, huoni kwamba mwisho utakuwa mchungu? Je, utaendelea kwa muda gani bila kuwashawishi watu wako waache kuwaandama ndugu zao?”
27 Yoabu akamwambia, “Naapa kwa Mungu aliye hai, kwamba kama hungesema jambo hilo, hakika watu wangu wangeendelea kuwaandama ndugu zao hadi kesho asubuhi.”
28 Hivyo, Yoabu akapiga tarumbeta na watu wakaacha kuwafuatia watu wa Israeli, wala hawakupigana zaidi.
29 Abneri na watu wake walipita bonde la Araba usiku kucha. Wakavuka mto Yordani, wakatembea mchana kutwa hadi Mahanaimu.
30 Yoabu aliporudi kutoka kumfuatia Abneri, aliwakusanya watu wake wote, akagundua kuwa watumishi kumi na tisa wa Daudi walikosekana, licha ya Asaheli.
31 Lakini watumishi wa Daudi walikuwa wamewaua watu 360 kutoka kabila la Benyamini pamoja na watu wa Abneri.
32 Yoabu na watu wake waliuchukua mwili wa Asaheli, wakauzika kwenye kaburi la baba yake, lililoko huko Bethlehemu. Yoabu na watu wake walitembea usiku kucha, na kulipokucha wakafika mjini Hebroni.
1 Kulikuwa na vita vya muda mrefu kati ya watu walioiunga mkono jamaa ya Shauli, na wale walioiunga mkono jamaa ya Daudi. Lakini Daudi alizidi kupata nguvu zaidi na zaidi, ambapo upande wa Shauli ulizidi kudhoofika zaidi na zaidi.
2 Watoto wa kiume aliozaliwa Daudi huko Hebroni walikuwa: Amnoni, mzaliwa wake wa kwanza, mama yake alikuwa Ahinoamu kutoka Yezreeli;
3 Kileabu, mzaliwa wake wa pili, mama yake alikuwa Abigaili, mjane wa Nabali kutoka Karmeli; Absalomu, mzaliwa wake wa tatu, mama yake alikuwa Maaka, bintiye Talmai mfalme wa Geshuri;
4 Adoniya, mzaliwa wake wa nne, mama yake alikuwa Hagithi; Shefatia, mzaliwa wake wa tano, mama yake alikuwa Abitali,
5 na Ithreamu, mzaliwa wake wa sita, mama yake alikuwa Egla, mke wake Daudi. Daudi alizaliwa wana hawa wote alipokuwa huko Hebroni.
6 Kadiri vita vilivyoendelea kati ya jamaa ya Daudi na ile ya Shauli, Abneri alizidi kujiimarisha katika jamaa ya Shauli.
7 Shauli alikuwa na suria mmoja aitwaye Rispa, binti Aya. Basi, wakati mmoja, Ishboshethi akamwuliza Abneri, “Kwa nini umelala na suria wa baba yangu?”
8 Abneri alikasirika sana kutokana na maneno ya Ishboshethi, akasema: “Je, unafikiri mimi naweza kumsaliti Shauli? Je, unafikiri kuwa mimi naitumikia jamaa ya Yuda? Tazama, mimi nimekuwa mtiifu kwa jamaa ya baba yako Shauli, ndugu zake, rafiki zake na sijakutia mikononi mwa Daudi hadi leo. Hata hivyo, leo hii unaniona kuwa mwenye hatia kwa ajili ya mwanamke.
9 Mungu aniue ikiwa sitatekeleza yote ambayo Mwenyezi-Mungu alimwapia Daudi.
10 Mwenyezi-Mungu alimwapia Daudi kuwa atauhamisha ufalme kutoka jamaa ya Shauli na kumpa yeye. Naye atatawala Israeli na Yuda kutoka Dani hadi Beer-sheba.”
11 Ishboshethi hakuweza kusema neno, kwa kuwa alikuwa anamwogopa Abneri.
12 Basi, Abneri akatuma wajumbe kwa Daudi, huko Hebroni wakamwambie, “Je, nchi hii ni mali ya nani? Fanya agano na mimi, nami nitakusaidia kuifanya Israeli yote iwe chini yako.”
13 Daudi akamjibu, “Vema, nitafanya agano nawe. Lakini ninakutaka jambo moja kwamba kabla hujaniona sharti kwanza uniletee Mikali binti wa Shauli. Hapo utaniona.”
14 Daudi pia alituma wajumbe kwa Ishboshethi mwana wa Shauli akisema, “Nirudishie mke wangu Mikali ambaye nilimwoa kwa magovi 100 ya Wafilisti.”
15 Basi, Ishboshethi alituma watu wakamchukue Mikali kutoka kwa mumewe, Paltieli mwana wa Laishi.
16 Lakini Paltieli akaenda pamoja na mkewe huku analia njia nzima mpaka huko Bahurimu. Abneri akamwambia Paltieli, “Rudi nyumbani.” Naye akarudi.
17 Abneri alifanya mashauri na wazee wa Israeli, akawaambia, “Kwa muda fulani uliopita mmekuwa mkitaka Daudi awe mfalme wenu.
18 Sasa, lileteni jambo hilo hadharani kwa sababu Mwenyezi-Mungu alimwahidi hivi Daudi, ‘Kwa mkono wako wewe Daudi mtumishi wangu, nitawaokoa watu wangu wa Israeli kutoka kwa Wafilisti na kutoka kwa adui zao wengine.’”
19 Abneri pia akazungumza na Wabenyamini, kisha akaenda mpaka Hebroni kumwambia Daudi kuhusu yale ambayo watu wote wa Israeli na kabila lote la Benyamini walipatana kutenda.
20 Abneri alipomwendea Daudi, alikuwa na watu ishirini, Daudi aliwafanyia karamu.
21 Abneri akamwambia Daudi, “Mimi sasa nitakwenda na kukuletea watu wote wa Israeli, wewe bwana wangu mfalme. Watakuja na kufanya agano nawe, ili uwe mfalme wao, nawe utawatawala wote kama upendavyo.” Daudi akamuaga Abneri aende zake, naye akaondoka kwa amani.
22 Baadaye, Yoabu na baadhi ya watu wa Daudi walirudi kutoka mashambulio, wakaleta nyara nyingi. Lakini Abneri hakuwa pamoja na Daudi huko Hebroni kwani Daudi alikuwa amemuaga aende zake, naye akaondoka kwa amani.
23 Yoabu aliporudi akiwa na jeshi lake lote alilokuwa nalo, aliambiwa kwamba Abneri mwana wa Neri, alikuwa amekuja kumwona mfalme Daudi, naye amemuaga aende zake, naye ameondoka kwa amani.
24 Yoabu alimwendea mfalme na kumwambia, “Sasa umefanya nini? Tazama Abneri alikuja kwako, kwa nini umemwacha aende?
25 Je, unajua kuwa Abneri mwana wa Neri alikuja kukudanganya? Alikuja ili ajue mienendo yako na yale unayoyafanya.”
26 Yoabu alipotoka kuzungumza na Daudi, alituma wajumbe wakamlete Abneri, nao wakamkuta kwenye kisima cha Sira na kumrudisha, lakini Daudi hakujua jambo hilo.
27 Abneri aliporudi Hebroni, Yoabu alimchukua kando kwenye lango kana kwamba anataka kuzungumza naye kwa faragha. Hapo Yoabu akamkata Abneri tumboni kwa sababu Abneri alikuwa amemuua Asaheli ndugu yake, na Abneri akafa.
28 Baadaye Daudi aliposikia habari hizo alisema, “Mimi na ufalme wangu hatuna hatia mbele ya Mwenyezi-Mungu kuhusu damu ya Abneri mwana wa Neri.
29 Lawama ya mauaji hayo yawe juu ya kichwa cha Yoabu na jamaa yote ya baba yake! Jamaa ya Yoabu daima isikose mtu mwenye ugonjwa wa kisonono, au ugonjwa wa ukoma, au anayetembea kwa magogo au kuuawa kwa upanga, au mwenye kukosa chakula!”
30 Yoabu na ndugu yake Abishai walimuua Abneri kwa kuwa alikuwa amemuua ndugu yao Asaheli wakati wa vita huko Gibeoni.
31 Kisha, mfalme Daudi akamwambia Yoabu na wale wote waliokuwa pamoja naye, wararue mavazi yao, wavae mavazi ya gunia ili wamwombolezee Abneri. Wakati wa mazishi hayo, mfalme Daudi alitembea nyuma ya jeneza.
32 Abneri alizikwa huko Hebroni na mfalme aliomboleza kwa sauti akiwa kando ya kaburi, pia watu wengine wote walifanya vivyo hivyo.
33 Mfalme alimwombolezea Abneri akisema, “Je, ilikuwaje Abneri akafa kama mpumbavu?
34 Mikono yako haikufungwa na miguu yako haikutiwa pingu. Amekufa kama mtu aliyeuawa na waovu!” Na watu wote walimlilia tena.
35 Kisha, watu wote walikwenda kumshawishi Daudi ale mkate wakati ulipokuwa bado mchana. Lakini Daudi aliapa akawaambia, “Mungu na aniue ikiwa nitaonja mkate au kitu chochote hadi jua litakapotua.”
36 Watu wote waliyaona mambo hayo, nao walipendezwa; kama vile kila kitu alichofanya mfalme kilivyowapendeza.
37 Hivyo, siku ile, Waisraeli wote walielewa kwamba haikuwa nia ya mfalme Daudi kumuua Abneri mwana wa Neri.
38 Mfalme Daudi aliwaambia watumishi wake, “Je, hamjui kuwa leo mtu mkuu na mashuhuri amefariki katika Israeli?
39 Ijapokuwa mmenipaka mafuta ili niwe mfalme, lakini leo mimi ni mnyonge. Hawa wana wa Seruya ni wakatili kupita kiasi. Mwenyezi-Mungu na awaadhibu waovu hawa sawasawa na uovu wao.”
1 Ishboshethi mwana wa Shauli, aliposikia kwamba Abneri ameuawa huko Hebroni, alivunjika moyo na watu wote wa Israeli walifadhaika.
2 Ishboshethi mwana wa Shauli, alikuwa na watu wawili waliokuwa viongozi wa kikosi cha uvamizi; mmoja aliitwa Baana na mwingine Rekabu. Hao walikuwa wana wa Rimoni, mtu wa kabila la Benyamini kutoka mji wa Be-erothi, (kwa maana Be-erothi pia ulikuwa mali ya kabila la Benyamini).
3 Wakazi wa Be-erothi walikimbilia Gitaimu, na wameishi huko kama wageni hadi leo.
4 Yonathani mwana wa Shauli, alikuwa na mtoto aliyelemaa miguu yake yote miwili. Mtoto huyo aliitwa Mefiboshethi. Mefiboshethi alikuwa na umri wa miaka mitano habari za kifo cha Shauli na Yonathani ziliposikika kutoka Yezreeli. Yaya aliyekuwa anamtunza aliposikia kuwa Shauli na Yonathani wameuawa huko Yezreeli, alimchukua Mefiboshethi akakimbia naye. Lakini alipokuwa anakimbia kwa haraka mtoto huyo alianguka, naye akalemaa.
5 Rekabu na Baana wana wa Rimoni Mbeerothi, wakaenda nyumbani kwa Ishboshethi. Walifika huko adhuhuri, Ishboshethi alipokuwa anapumzika nyumbani kwake.
6 Waliingia nyumbani wakijifanya kana kwamba wanataka kuchukua ngano, wakamkuta Ishboshethi amelala kitandani mwake ndani ya chumba chake cha kulala, wakamchoma mkuki tumboni. Baada ya kumwua hivyo hao ndugu wawili walimkata kichwa wakatoroka wakiwa wamekichukua. Walipitia njia ya Araba, wakasafiri usiku kucha.
7
8 Halafu walichukua kichwa cha Ishboshethi na kumpelekea Daudi huko Hebroni. Nao wakamwambia mfalme Daudi, “Hiki ni kichwa cha Ishboshethi mwana wa Shauli ambaye ni adui yako, aliyekuwa anataka kuyaangamiza maisha yako. Mwenyezi-Mungu leo amekulipizia kisasi dhidi ya Shauli na wazawa wake.”
9 Lakini Daudi akamjibu Rekabu na Baana, nduguye, wana wa Rimoni, Mbeerothi,. “Naapa kwa Mwenyezi-Mungu aliye hai, kwamba yeye ameyakomboa maisha yangu kutokana na kila adui.
10 Yule mtu aliyekuja kuniambia kuwa Shauli amekufa, akidhani kuwa ananiletea habari njema, nilimkamata na kumwua huko. Hivyo ikawa ndiyo zawadi niliyompa kutokana na taarifa yake.
11 Je, mtu mwovu anapomuua mtu mwadilifu akiwa kitandani, nyumbani kwake, je, si haki kwangu kumlipiza kwa sababu ya kumwaga damu kwa kumwulia mbali toka duniani?”
12 Daudi akawaamuru vijana wake, nao wakawaua. Wakawakata mikono yao na miguu yao. Halafu wakawatundika mtini kando ya bwawa huko Hebroni. Lakini walikichukua kichwa cha Ishboshethi na kukizika katika kaburi la Abneri huko Hebroni.
1 Kisha makabila yote ya Israeli yalimwendea Daudi huko Hebroni, na kumwambia, “Tazama, sisi ni mwili na damu yako.
2 Hapo awali, Shauli alipokuwa mfalme wetu wewe ndiwe uliyewaongoza Waisraeli vitani, na Mwenyezi-Mungu alikuambia ‘Utakuwa mchungaji wa watu wangu Israeli na utakuwa mkuu juu ya Israeli.’”
3 Basi, wazee wote wa Israeli wakamwendea mfalme Daudi huko Hebroni; naye akafanya agano nao mbele ya Mwenyezi-Mungu, halafu wakampaka Daudi mafuta awe mfalme wa Israeli.
4 Daudi alikuwa na umri wa miaka thelathini alipoanza kutawala, na alitawala kwa muda wa miaka arubaini.
5 Huko Hebroni, alitawala watu wa Yuda kwa muda wa miaka saba na miezi sita, na huko Yerusalemu alitawala watu wa Israeli pamoja na Yuda kwa muda wa miaka thelathini na mitatu.
6 Baadaye mfalme na watu wake walikwenda Yerusalemu kuwashambulia Wayebusi waliokuwa wenyeji wa nchi hiyo. Lakini wao wakamwambia, “Hutaingia mjini humu, kwani vipofu na vilema watakufukuzia mbali.” Walimwambia hivyo kwani walifikiri kuwa Daudi asingeweza kuingia mjini humo.
7 Hata hivyo, mfalme Daudi aliiteka ngome ya Siyoni, yaani mji wa Daudi.
8 Siku hiyo, Daudi alisema, “Mtu yeyote atakayewapiga Wayebusi na apitie kwenye mfereji wa maji ili kuwashambulia vilema na vipofu ambao roho yangu inawachukia.” Ndio maana watu husema, “Vipofu na vilema hawataingia nyumbani.”
9 Daudi alikaa kwenye ngome hiyo, nao mji akauita, “Mji wa Daudi.” Daudi aliujenga mji kuuzunguka, akianzia Milo kuelekea ndani.
10 Naye Daudi akazidi kuwa maarufu zaidi kwa sababu Mwenyezi-Mungu, Mungu wa majeshi, alikuwa pamoja naye.
11 Kisha, mfalme Hiramu wa Tiro alituma wajumbe kwa Daudi; alimpelekea pia mierezi, maseremala na waashi ambao walimjengea Daudi ikulu.
12 Hivyo, Daudi akatambua kwamba Mwenyezi-Mungu amemwimarisha awe mfalme wa Israeli, na kwamba ameukuza ufalme wake kwa ajili ya watu wake wa Israeli.
13 Daudi alijitwalia masuria na wake zaidi wa huko mjini Yerusalemu baada ya kutoka Hebroni. Hao, wakamzalia watoto zaidi wa kiume na wa kike.
14 Yafuatayo ndiyo majina ya watoto wa kiume, wake zake waliomzalia huko Yerusalemu: Shamua, Shobabu, Nathani, Solomoni,
15 Ibhari, Elishua, Nefegi, Yafia,
16 Elishama, Eliada na Elifeleti.
17 Wafilisti waliposikia kwamba Daudi amepakwa mafuta kuwa mfalme wa Israeli, wote walitoka kwenda kumtafuta, lakini yeye alipata habari, akaingia ndani ya ngome.
18 Wafilisti walifika na kujitawanya kwenye Bonde la Refaimu.
19 Basi, Daudi alimwuliza Mwenyezi-Mungu shauri, “Je, niende kuwashambulia Wafilisti? Je, utawatia mikononi mwangu?” Naye Mwenyezi-Mungu akamwambia Daudi, “Nenda, maana hakika nitawatia Wafilisti mikononi mwako.”
20 Basi, Daudi akafika Baal-perasimu, na kuwashinda Wafilisti; halafu akasema, “Mwenyezi-Mungu amepita katikati ya adui zangu kama mafuriko ya maji yaendayo kasi.” Kwa hiyo mahali hapo pakaitwa Baal-perasimu.
21 Wafilisti waliziacha sanamu zao za miungu mahali hapo, naye Daudi na watu wake wakazichukua.
22 Kwa mara ya pili, Wafilisti walifika tena na kujitawanya kwenye bonde la Refaimu.
23 Daudi alipomwomba Mwenyezi-Mungu shauri, Mwenyezi-Mungu alimwambia, “Usiwashambulie kutoka hapa ulipo, bali zunguka na kuwashambulia kutoka mkabala wa miti na miforosadi.
24 Na mara mtakaposikia vishindo vya gwaride kwenye vilele vya miforosadi hiyo, hapo jipe moyo kwani nitakuwa nimetoka ili kukutangulia kulipiga jeshi la Wafilisti.”
25 Daudi alifanya kama alivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu, naye akawapiga Wafilisti kutoka Geba hadi Gezeri.
1 Kwa mara nyingine, Daudi aliwakusanya wale askari bora wa Israeli, jumla yao 30,000.
2 Daudi aliondoka akaenda pamoja na watu wake wote aliokuwa nao kutoka Baala-yuda, kwenda kulichukua toka huko sanduku la Mungu linaloitwa kwa jina lake Mwenyezi-Mungu wa Majeshi, akaaye kwenye kiti chake cha enzi juu ya viumbe wenye mabawa.
3 Basi, wakalichukua sanduku la Mungu kutoka katika nyumba ya Abinadabu iliyokuwa mlimani, wakalibeba juu ya gari jipya. Uza na Ahio wana wa Abinadabu wakawa wanaliendesha gari hilo jipya,
4 likiwa na sanduku hilo la Mungu, naye Ahio akiwa anatangulia mbele ya sanduku hilo.
5 Daudi na watu wote wa Israeli, wakawa wanaimba nyimbo na kucheza kwa nguvu zao zote, mbele ya Mwenyezi-Mungu. Walipiga ala za muziki zilizotengenezwa kwa mvinje: Vinubi, vinanda, matari, kayamba na matoazi.
6 Walipofika kwenye uwanja wa kupuria nafaka wa Nakoni, Uza aliunyosha mkono wake na kulishika sanduku la Mungu kwa sababu wale ng'ombe walijikwaa.
7 Hapo, hasira ya Mwenyezi-Mungu ikawaka dhidi ya Uza. Mungu akamuua palepale. Uza akafa papo hapo kando ya sanduku la Mungu.
8 Naye Daudi alikasirika kwa kuwa Mwenyezi-Mungu alimwadhibu Uza kwa hasira. Hivyo, mahali hapo pakaitwa Peres-uza mpaka hivi leo.
9 Siku hiyo Daudi alimwogopa Mwenyezi-Mungu akasema, “Sasa litanijiaje sanduku la Mwenyezi-Mungu?”
10 Kwa hiyo, Daudi hakuwa tayari kulipeleka sanduku la Mwenyezi-Mungu ndani ya mji wa Daudi, bali Daudi alilipeleka nyumbani kwa Obed-edomu, Mgiti.
11 Sanduku hilo la Mwenyezi-Mungu lilikaa nyumbani kwa Obed-edomu kwa muda wa miezi mitatu; naye Mwenyezi-Mungu akambariki Obed-edomu pamoja na jamaa yake.
12 Mfalme Daudi aliposikia kuwa Mwenyezi-Mungu ameibariki jamaa ya Obed-edomu na vitu vyote alivyokuwa navyo kwa sababu ya sanduku la Mungu, akaenda kulichukua sanduku la agano kutoka nyumbani kwa Obed-edomu na kulipeleka kwenye mji wa Daudi kwa shangwe.
13 Watu wale waliolibeba sanduku la Mwenyezi-Mungu kila walipopiga hatua sita, Daudi alitoa tambiko: Fahali na ndama mmoja mnono.
14 Daudi akiwa amejifunga kizibao cha kuhani kiunoni mwake alicheza kwa nguvu zake zote mbele ya Mwenyezi-Mungu.
15 Hivyo, yeye na Waisraeli wote walilipeleka sanduku la Mwenyezi-Mungu hadi mjini mwa Daudi kwa shangwe na sauti kubwa ya tarumbeta.
16 Sanduku la Mwenyezi-Mungu lilipokuwa linaingia katika mji wa Daudi, Mikali binti Shauli alichungulia dirishani akamwona mfalme Daudi akirukaruka na kucheza mbele ya Mwenyezi-Mungu; basi, akamdharau moyoni mwake.
17 Kisha waliliingiza sanduku la Mwenyezi-Mungu ndani ya hema ambalo Daudi alikuwa amelipiga hapo na kuliweka mahali pake. Naye Daudi akatoa tambiko za kuteketezwa na tambiko za amani mbele ya Mwenyezi-Mungu.
18 Daudi alipomaliza kutoa tambiko za kuteketezwa na za amani, aliwabariki watu kwa jina la Mwenyezi-Mungu wa majeshi,
19 na akawagawia watu wote, kundi lote la Waisraeli, wanaume na wanawake, kila mmoja, mkate, kipande cha nyama na mkate wa zabibu. Baadaye, watu wote waliondoka, kila mtu akarudi nyumbani kwake.
20 Daudi aliporudi nyumbani kwake ili kuibariki jamaa yake, Mikali, binti Shauli, alikwenda kumlaki, akasema, “Ajabu ya mfalme wa Israeli kujiheshimu leo, kwa kujifunua uchi wake mbele ya watumishi wake wa kiume na wa kike kama mshenzi avuavyo mavazi yake mbele ya watu bila aibu!”
21 Daudi akamwambia Mikali, “Nilikuwa mbele ya Mwenyezi-Mungu ambaye alinichagua mimi badala ya baba yako, na jamaa yake, ili kuniteua kuwa mkuu juu ya Israeli, watu wake Mwenyezi-Mungu, kwa hiyo mimi nitacheza tu mbele ya Mwenyezi-Mungu.
22 Nitajishusha mwenyewe zaidi kuliko sasa. Wewe utaniona kuwa si kitu, lakini hao watumishi wa kike uliowasema wataniheshimu.”
23 Basi Mikali binti Shauli hakuwa na mtoto mpaka kufa kwake.
1 Wakati mfalme Daudi alipokuwa akikaa katika ikulu, naye Mwenyezi-Mungu amemuwezesha kuwa na amani na adui zake kila upande,
2 mfalme Daudi akamwambia nabii Nathani, “Hebu tazama; mimi ninakaa katika nyumba iliyojengwa kwa mierezi, lakini sanduku la Mungu linakaa hemani.”
3 Nathani akamwambia mfalme, “Nenda ufanye chochote unachofikiria moyoni mwako, kwa kuwa Mwenyezi-Mungu yu pamoja nawe.”
4 Lakini usiku uleule neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Nathani,
5 “Nenda ukamwambie mtumishi wangu Daudi, ‘Mwenyezi-Mungu asema hivi: Je, wewe utanijengea nyumba ya kukaa?
6 Tangu siku ile nilipowatoa Waisraeli nchini Misri mpaka hivi leo sijaishi kwenye nyumba. Nimetembea kila mahali nikiwa ninakaa hemani.
7 Je, kila mahali ambako nimekwenda na Waisraeli wote nimemwuliza mtu yeyote wa Israeli ambaye nilimwamuru awachunge watu wa Israeli: Kwa nini hajanijengea nyumba ya mierezi?
8 Kwa hiyo basi, mwambie mtumishi wangu Daudi: Mwenyezi-Mungu wa majeshi anasema hivi: Nilikutoa malishoni ulikokuwa unawachunga kondoo, ili uwe mkuu wa watu wangu Israeli.
9 Tangu wakati huo nimekuwa pamoja nawe kokote ulikokwenda na nimewaangamiza adui zako wote mbele yako. Nitakufanya kuwa maarufu kama wakuu wengine duniani.
10 Nami nitawachagulia watu wangu wa Israeli mahali pa kuishi, niwapandikize, ili waishi mahali pao wenyewe, wasisumbuliwe tena. Nao watu wakatili wanaotumia nguvu hawatawatesa tena kama hapo awali,
11 tangu wakati nilipowateua waamuzi juu ya watu wangu Israeli, nami nitakulinda kutokana na adui zako wote. Zaidi ya yote, mimi Mwenyezi-Mungu nakutangazia kuwa nitakujengea nyumba.
12 Siku zako zitakapotimia na utakapofariki na kujiunga na babu zako, nitamfanya mmoja wa watoto wako wewe mwenyewe awe mfalme, nami nitauimarisha ufalme wake.
13 Yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa ajili ya jina langu na kiti chake cha enzi cha ufalme wake nitakiimarisha milele.
14 Mimi nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwanangu. Akifanya maovu, nitamrudi kama wanadamu wanavyowarudi wana wao kwa fimbo.
15 Lakini sitamwondolea fadhili zangu kama vile nilivyoziondoa kwa Shauli, niliyemwondoa mbele yako.
16 Ukoo wako na ufalme wako vitadumu imara daima. Kiti chako cha enzi kitakuwa imara milele.’”
17 Nathani alimweleza Daudi kila kitu ambacho alioneshwa katika maono hayo na Mungu.
18 Kisha mfalme Daudi akaingia ndani na kuketi mbele ya Mwenyezi-Mungu; halafu akaomba, “Mimi ni nani ee Bwana Mungu, na jamaa yangu ni nini hata ukaniinua mpaka hapa nilipo leo!
19 Tena jambo hili lilikuwa dogo machoni pako, Bwana Mungu; zaidi ya hayo umeiahidi jamaa yangu mambo makubwa katika miaka mingi ijayo; na kwamba umenijalia kuona hayo, Ee Bwana Mungu.
20 Nikuambie nini zaidi, mimi Daudi, mtumishi wako? Kwani wewe unanijua mimi mtumishi wako, ee Bwana Mungu!
21 Kutokana na ahadi yako na kulingana na moyo wako, umetenda makuu hayo yote ili unijulishe mimi mtumishi wako.
22 Kutokana na yale tuliyosikia, wewe Mwenyezi-Mungu ni mkuu; hakuna aliye kama wewe, na hakuna Mungu mwingine ila wewe.
23 Tena ni watu gani duniani ambao wanaweza kufananishwa na watu wako wa Israeli, ambao Mungu wake alikwenda kuwakomboa ili wawe watu wake? Wewe ee Mungu ulijifanyia jina na kujitendea mambo makubwa na ya ajabu kwa ajili ya nchi yako mbele ya watu wako ambao kwa ajili yako mwenyewe uliwaokoa kutoka Misri, ukayafukuza mataifa na miungu yake mbele yao?
24 Hata umewaimarisha watu wako wa Israeli kwa ajili yako mwenyewe, ili wawe watu wako milele; nawe ee Mwenyezi-Mungu umekuwa Mungu wao.
25 Basi, sasa, ee Mwenyezi-Mungu, ikamilishe ile ahadi uliyosema kuhusu mimi mtumishi wako na kuhusu jamaa yangu kama ulivyoahidi.
26 Nalo jina lako litatukuzwa milele, nao watu watasema, ‘Mwenyezi-Mungu wa majeshi ni Mungu juu ya Israeli!’ Na jamaa yangu, mimi Daudi mtumishi wako, itaimarika mbele yako.
27 Maana wewe, ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, umenifunulia mimi mtumishi wako, ukisema ‘Nitakujengea nyumba;’ ndio maana nina ujasiri kutoa ombi hili mbele yako.
28 Sasa, ee Bwana Mungu, wewe ndiwe Mungu, na maneno yako ni kweli na umeniahidi mimi mtumishi wako jambo hili jema;
29 kwa hiyo, nakuomba nyumba yangu mimi mtumishi wako ipate kudumu milele mbele yako; kwani wewe umesema hivyo, pia kwa baraka zako nyumba yangu itabarikiwa milele.”
1 Baada ya hayo, Daudi aliwapiga, akawashinda Wafilisti. Akauteka mji wa Metheg-ama kutoka utawala wa Wafilisti.
2 Kisha aliwashinda Wamoabu. Aliwapanga katika mistari mateka hao, na kuwalaza chini. Aliamuru wale waliokuwa katika mistari miwili wauawe na wale wa mstari wa tatu waachwe hai. Hivyo, Wamoabu wakawa watumishi wake Daudi na wakawa wanamlipa kodi.
3 Daudi pia alimshinda Hadadezeri mwana wa Rehobu, mfalme wa Soba. Daudi alipata ushindi huu wakati Hadadezeri alipokuwa njiani kwenda kulirudisha eneo la mto Eufrate kuwa chini ya utawala wake.
4 Daudi aliteka wapandafarasi 1,700, na askari wa miguu 20,000. Kisha Daudi alikata mishipa ya miguu ya nyuma ya farasi wote wa magari, ila alibakiza farasi wa kutosheleza magari 100.
5 Nao Waaramu wa Damasko walipokwenda kumsaidia Hadadezeri, mfalme wa Soba, Daudi aliwashambulia na kuwaua watu 22,000.
6 Halafu Daudi aliweka kambi za kijeshi katika mji wa Waaramu wa Damasko. Basi, Waaramu wakawa watumishi wake na wakawa wanamlipa kodi. Mwenyezi-Mungu alimpa Daudi ushindi kokote alikokwenda.
7 Daudi alizichukua ngao za dhahabu walizobeba wanajeshi wa Hadadezeri na kuzipeleka Yerusalemu.
8 Pia alichukua shaba nyingi sana kutoka miji ya Beta na Berothai, iliyokuwa miji ya Hadadezeri.
9 Wakati Toi, mfalme wa Hamathi, aliposikia kwamba Daudi amelishinda jeshi lote la Hadadezeri,
10 alimtuma mwanawe Yoramu kwa mfalme Daudi kumpelekea salamu na pongezi kwa sababu alikuwa amepigana na Hadadezeri na kumshinda. Maana Hadadezeri alipigana na Toi mara nyingi. Yoramu alimpelekea Daudi zawadi za vyombo vya fedha, dhahabu na shaba.
11 Zawadi hizo, pamoja na fedha na dhahabu alizokuwa ameziteka kwa mataifa yote aliyoyashinda, aliziweka wakfu kwa Mwenyezi-Mungu,
12 yaani kutoka Edomu, Moabu, Amoni, Filistia, Amaleki, pamoja na nyara alizoteka kwa mfalme Hadadezeri, mwana wa Rehobu mfalme wa Soba.
13 Daudi alijiongezea umaarufu wake. Alipokuwa anarudi baada ya kumshinda Hadadezeri, aliwaua Waedomu 18,000, katika Bonde la Chumvi.
14 Akaweka kambi za kijeshi katika Edomu yote. Nao Waedomu wote wa huko wakawa watumishi wake. Mwenyezi-Mungu alimpa Daudi ushindi kokote alikokwenda.
15 Hivyo, Daudi akatawala juu ya Israeli yote, akahakikisha watu wake wote wanatendewa haki ipasavyo.
16 Yoabu mwana wa Seruya, alikuwa mkuu wa majeshi. Yehoshafati mwana wa Ahiludi, alikuwa mweka kumbukumbu.
17 Sadoki mwana wa Ahitubu na Ahimeleki mwana wa Abiathari, walikuwa makuhani. Seraya alikuwa katibu.
18 Benaya mwana wa Yehoyada alikuwa kiongozi wa Wakerethi na Wapelethi, nao wana wa Daudi wakawa makuhani.
1 Siku moja, Daudi aliuliza, “Je, kuna mtu yeyote aliyesalia katika jamaa ya Shauli? Kama yuko, ningependa kumtendea wema kwa ajili ya Yonathani.”
2 Kulikuwa na mtumishi wa jamaa ya Shauli aliyeitwa Siba. Siba aliitwa kwenda kwa Daudi. Mfalme Daudi alimwuliza, “Je wewe ndiye Siba?” Naye akamjibu, “Naam, mimi mtumishi wako ndiye.”
3 Mfalme akamwuliza, “Je, hakuna mtu yeyote aliyesalia katika jamaa ya Shauli? Kama yuko, ningependa kumtendea wema wa Mungu.” Siba akamjibu, “Yuko mwana wa Yonathani, lakini yeye amelemaa miguu.”
4 Mfalme akamwuliza, “Yuko wapi?” Siba akamjibu, “Yuko nyumbani kwa Makiri mwana wa Amieli huko Lo-debari.”
5 Basi, mfalme Daudi akatuma watu, naye akaletwa kutoka nyumbani kwa Makiri mwana wa Amieli huko Lo-debari.
6 Basi, Mefiboshethi mwana wa Yonathani, na mjukuu wa Shauli akaenda kwa mfalme Daudi, akaanguka kifudifudi mbele ya mfalme Daudi, akasujudu. Daudi akamwita, “Mefiboshethi.” Naye akamjibu, “Naam! Mimi hapa mtumishi wako.”
7 Daudi akamwambia, “Usiogope. Mimi nitakutendea wema kwa ajili ya baba yako Yonathani. Ile ardhi yote iliyokuwa ya babu yako Shauli nitakurudishia. Nawe, daima utakula mezani pangu.”
8 Mefiboshethi akasujudu, na kusema, “Mimi ni sawa na mbwa mfu; kwa nini unishughulikie hivyo?”
9 Kisha, mfalme Daudi akamwita Siba mtumishi wa Shauli, akamwambia, “Ile mali yote iliyokuwa ya Shauli na jamaa yake nimempa mjukuu wa bwana wako.
10 Wewe, watoto wako na watumishi wako mtakuwa mnamlimia Mefiboshethi na mtamletea mavuno ili mjukuu wa bwana wako awe daima na chakula. Lakini yeye atakula mezani pangu.” Wakati huo, Siba alikuwa na watoto wa kiume kumi na watano na watumishi ishirini.
11 Kisha, Siba akamwambia mfalme, “Mimi mtumishi wako, nitafanya yote kulingana na amri yako.” Basi, Mefiboshethi akawa anapata chakula chake mezani pa Daudi, kama mmojawapo wa watoto wa mfalme.
12 Mefiboshethi alikuwa na mtoto mdogo wa kiume aliyeitwa Mika. Watu wote wa jamaa ya Siba wakawa watumishi wa Mefiboshethi.
13 Hivyo, Mefiboshethi aliyekuwa amelemaa miguu yake yote akawa anaishi mjini Yerusalemu, na kupata chakula chake mezani pa mfalme daima.
1 Baada ya hayo mfalme Nahashi wa Waamori akafa, na mwanawe aliyeitwa Hanuni akawa mfalme badala ya baba yake.
2 Mfalme Daudi akasema, “Nitamtendea wema Hanuni, mwana wa Nahashi kama baba yake alivyonitendea.” Hivyo, Daudi alituma wajumbe kumpelekea salamu za rambirambi. Nao wajumbe wa Daudi walipofika katika nchi ya Waamori,
3 wakuu wa Waamori walimwambia bwana wao, Hanuni, “Je, unadhani kwamba Daudi kwa kukutumia watu wa kukufariji anamheshimu baba yako? Je, Daudi hakuwatuma watu hawa kwako ili kuuchunguza na kuupeleleza mji halafu wauteke?”
4 Basi, Hanuni aliwachukua wajumbe hao wa Daudi akamnyoa kila mmoja nusu ya ndevu zake, akayapasua mavazi yao katikati mpaka matakoni, kisha akawaacha waende zao.
5 Waliona aibu mno kurudi nyumbani. Daudi alipopashwa habari alituma watu kuwalaki kwani hao wajumbe waliona aibu sana. Naye mfalme aliwaambia, “Kaeni mjini Yeriko, hata mtakapoota ndevu, kisha mrudi nyumbani.”
6 Waamoni walipoona kuwa wamemchukiza Daudi, walikodi wanajeshi Waaramu 20,000 waendao kwa miguu, kutoka Beth-rehobu na Soba; wanajeshi 12,000, kutoka Tobu, na mfalme Maaka akiwa na wanajeshi 1,000.
7 Naye Daudi aliposikia habari hizo, alimtuma Yoabu kwenda na jeshi lote la mashujaa.
8 Waamoni walitoka na kujipanga tayari kwa vita kwenye lango la mji wa Raba, mji wao mkuu; nao Waaramu kutoka Soba na Rehobu na watu kutoka Tobu na Maaka walijipanga nyikani.
9 Yoabu alipoona kuwa vita ni vikali dhidi yake, mbele na nyuma, aliwateua baadhi ya wanajeshi Waisraeli hodari zaidi akawapanga kukabiliana na Waaramu.
10 Wale wanajeshi wengine waliobaki aliwaweka chini ya uongozi wa ndugu yake Abishai, naye akawapanga ili wakabiliane na Waamoni.
11 Yoabu akamwambia Abishai, “Ikiwa Waaramu wananizidi nguvu, utanisaidia lakini kama Waamoni wanakuzidi nguvu, nitakuja kukusaidia.
12 Lakini jipe moyo! Tupigane kiume kwa ajili ya watu wetu na kwa ajili ya miji ya Mungu wetu; naye Mwenyezi-Mungu atutendee lile analoona ni jema kwake.”
13 Basi, Yoabu na watu wake walisonga mbele kwenda kupigana na Waaramu, nao Waaramu walikimbia.
14 Waamoni walipoona kuwa Waaramu wamekimbia, nao pia walimkimbia Abishai na kuingia mjini. Yoabu akaacha kupigana na Waamoni, akarudi Yerusalemu.
15 Lakini Waaramu walipoona kwamba wameshindwa na Waisraeli, walijikusanya pamoja.
16 Hadadezeri aliagiza Waaramu waliokuwa ngambo ya mto Eufrate waletwe, wapelekwe huko Helamu wakiongozwa na Shobaki kamanda wa jeshi la Hadadezeri.
17 Daudi alipopata habari, aliwakusanya pamoja Waisraeli wote, akavuka mto Yordani na kwenda mpaka Helamu. Nao Waaramu walijipanga tayari kwa vita dhidi ya Daudi, wakaanza kupigana naye.
18 Lakini Waaramu walikimbia mbele ya Waisraeli. Daudi aliwaua Waaramu 700 waliokuwa madereva wa magari ya vita, wapandafarasi 40,000. Pia alimwumiza Shobaki kamanda wa jeshi lao, naye akafia papo hapo.
19 Kisha wafalme wote waliokuwa watumishi wa Hadadezeri walipoona kuwa wameshindwa na Waisraeli, walifanya mapatano ya amani na Israeli, nao wakawa watumishi wa Israeli. Hivyo Waaramu hawakuthubutu kuwasaidia Waamoni tena.
1 Hata ikawa katika mwanzo wa mwaka mpya, wakati ambapo wafalme huenda vitani, Daudi alimtuma Yoabu na maofisa wake pamoja na Waisraeli wote kupigana; nao waliteka nyara Waamoni na kuuzingira mji wa Raba. Lakini Daudi alibaki Yerusalemu.
2 Siku moja, wakati wa jioni, Daudi aliamka kitandani akaenda kwenye paa ya ikulu. Alipokuwa anatembea huko juu, alimwona mwanamke mmoja akioga na mwanamke huyo alikuwa mzuri sana.
3 Daudi akatuma mtu kuuliza mwanamke huyo ni nani. Mtu huyo akamwambia Daudi “Mwanamke huyo ni Bathsheba binti wa Eliabu, na ni mke wa Uria Mhiti.”
4 Basi, Daudi alituma wajumbe wamlete. Basi Bathsheba akaja kwa Daudi, naye Daudi akalala naye; (mwanamke huyo alikuwa ndio tu amejitakasa baada ya hedhi yake); kisha akarudi nyumbani kwake.
5 Mwanamke huyo akapata mimba, naye akatuma habari kwa Daudi kuwa ana mimba yake.
6 Basi, Daudi akamtumia Yoabu ujumbe, “Mtume Uria, Mhiti kwangu.” Naye Yoabu akamtuma Uria kwa Daudi.
7 Uria alipofika kwake, Daudi alimwuliza habari za Yoabu, watu wote, na hali ya vita.
8 Halafu Daudi alimwambia Uria, “Rudi nyumbani kwako ukanawe miguu yako.” Uria alitoka nyumbani kwa mfalme, na mara mfalme akampelekea zawadi.
9 Lakini Uria hakurudi nyumbani kwake, bali alilala pamoja na watumishi wote wa bwana wake kwenye lango la ikulu.
10 Daudi alipoambiwa kwamba Uria hakwenda nyumbani kwake, Daudi alimwuliza Uria, “Wewe umetoka safari, kwa nini hukuenda nyumbani kwako?”
11 Uria alimjibu Daudi “Sanduku la agano, pamoja na majeshi yote ya Israeli na Yuda yanakaa kwenye vibanda vitani. Bwana wangu Yoabu na watumishi wake wote wamepiga kambi mbugani; je ni sawa mimi niende nyumbani nikale na kunywa na kulala na mke wangu? Kama uishivyo na roho yako inavyoishi, sitafanya kitu cha namna hiyo.”
12 Kisha, Daudi akamwambia Uria, “Basi, kaa hapa leo pia, na kesho nitakuacha urudi.” Hivyo Uria akabaki mjini Yerusalemu siku hiyo. Siku iliyofuata,
13 Daudi alimwalika Uria kula na kunywa huko kwake, akamfanya Uria alewe. Hata hivyo, usiku ule Uria hakwenda nyumbani kwake, ila alilala kwenye kochi lake pamoja na watumishi wa bwana wake.
14 Asubuhi yake, Daudi alimwandikia Yoabu barua akampa Uria aipeleke kwa Yoabu.
15 Katika barua hiyo Daudi aliandika hivi: “Mweke Uria kwenye mstari wa mbele, mahali ambako mapigano ni makali kabisa, kisha umwache huko na kurudi nyuma ili apigwe, afe.”
16 Basi, Yoabu alipokuwa anauzingira mji alimweka Uria mahali ambapo alijua wazi wanajeshi wa adui walikuwa hodari sana.
17 Wakazi wa mji huo walitoka katika mji wao na kupigana na Yoabu. Baadhi ya watumishi wa Daudi, waliuawa. Uria Mhiti naye aliuawa pia.
18 Kisha, Yoabu alipeleka habari zote kwa Daudi akimweleza juu ya vita.
19 Yoabu akamwamuru huyo mtumishi aliyemtuma hivi, “Baada ya kumweleza mfalme mambo yote kuhusu vita,
20 akikasirika na kukuuliza, ‘Kwa nini mlikwenda karibu na mji mlipokuwa mnapigana? Hamkujua kwamba wangewapiga mishale kutoka kwenye kuta za mji wao?
21 Nani alimuua Abimeleki mwana wa Yerubeshethi? Si alikuwa mwanamke mmoja mjini Thebesi ambaye alitupa jiwe la kusagia kutoka kwenye ukuta nalo likamuua Abimeleki? Kwa nini basi, mlikwenda karibu na ukuta?’ Basi, wewe utamwambia hivi, ‘Hata mtumishi wako Uria Mhiti, naye amekufa.’”
22 Yule mjumbe alikwenda kwa Daudi na kumwambia yote aliyotumwa na Yoabu ayaseme.
23 Yule mjumbe akamwambia Daudi, “Adui zetu walituzidi nguvu, wakatoka nje ya miji na kutushambulia nyikani. Hata hivyo sisi tuliwarudisha mpaka kwenye lango la mji.
24 Halafu wakatupiga mishale sisi watumishi wako kutoka ukutani. Baadhi ya watumishi wako waliuawa. Hata mtumishi wako Uria, Mhiti, naye amekufa.”
25 Daudi akamwambia yule mjumbe, “Utamwambia hivi Yoabu, ‘Jambo hili lisikusumbue kwani upanga hauna macho, vita huua yeyote yule. Bali, imarisha mashambulizi dhidi ya mji, hadi umeuangamiza mji huo’. Ndivyo utakavyomtia moyo Yoabu.”
26 Bathsheba mke wa Uria aliposikia kwamba mumewe Uria amekufa, alimwombolezea mumewe.
27 Muda wa matanga ulipokwisha, Daudi aliagiza Bathsheba achukuliwe na kupelekwa nyumbani kwake. Bathsheba akawa mke wa Daudi, naye akamzalia Daudi mtoto wa kiume. Lakini jambo hilo alilofanya Daudi lilimchukiza Mwenyezi-Mungu.
1 Basi Mwenyezi-Mungu akamtuma nabii Nathani kwa Daudi. Nathani alimwendea Daudi, akamwambia, “Kulikuwa na wanaume wawili katika mji mmoja; mmoja alikuwa tajiri na mwingine alikuwa maskini.
2 Yule tajiri alikuwa na kondoo wengi na ng'ombe wengi.
3 Lakini yule maskini alikuwa na mwanakondoo mdogo mmoja jike, ambaye alikuwa amemnunua. Alimtunza, naye akakua nyumbani mwake pamoja na watoto wake. Alimlisha mwanakondoo huyo chakula kilekile kama chake na kunywea kikombe chake naye pia alikuwa akimpakata kifuani. Mwanakondoo huyo alikuwa kama binti kwa yule mtu maskini.
4 Siku moja, yule tajiri alifikiwa na mgeni. Basi, tajiri huyo hakutaka kuchukua mmoja wa kondoo wake mwenyewe au ng'ombe wake, amchinjie mgeni wake, ila alikwenda na kumnyanganya yule maskini mwanakondoo wake, akamchinjia mgeni wake.”
5 Daudi aliposikia hayo, akawaka hasira dhidi ya yule tajiri. Akamwambia nabii Nathani, “Naapa kwa Mwenyezi-Mungu aliye hai kwamba mtu aliyefanya jambo hilo anastahili kufa!
6 Ni lazima amlipe yule maskini mwanakondoo huyo, tena mara nne, kwani ametenda jambo baya na hakuwa na huruma!”
7 Nathani akamwambia Daudi, “Wewe ndiwe huyo mtu! Sasa, Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Mimi nilikupaka mafuta uwe mfalme juu ya Israeli na kukuokoa mikononi mwa Shauli.
8 Nilikupa nyumba ya bwana wako na wake zake wawe wako, tena nikakupa watu wa Israeli na wa Yuda uwatawale. Na kama haya yangekuwa kidogo mno kwako ningekuongezea mara mbili zaidi ya hayo.
9 Kwa nini basi, umedharau neno langu mimi Mwenyezi-Mungu ukafanya uovu huu mbele yangu? Umemuua Uria Mhiti, kwa upanga, ukamchukua mke wake kuwa mkeo. Umewatumia Waamoni kumwua Uria vitani!
10 Kwa hiyo basi, kwa kuwa umenidharau na umemchukua mke wa Uria Mhiti, kuwa mkeo, mauaji hayataondoka katika jamaa yako’.
11 Sikiliza, Mwenyezi-Mungu asema, ‘Tazama, nitazusha maafa katika jamaa yako mwenyewe. Nitawachukua wake zako ukiona kwa macho yako mwenyewe na kumpa jirani yako, naye atalala nao hadharani.
12 Wewe ulifanya jambo hilo kwa siri, lakini mimi nitayafanya haya mbele ya Waisraeli wote hadharani.’”
13 Basi, Daudi akamwambia Nathani, “Nimetenda dhambi dhidi ya Mwenyezi-Mungu.” Nathani akamwambia, “Mwenyezi-Mungu amekusamehe dhambi yako, nawe hutakufa.
14 Hata hivyo, kwa kuwa kwa tendo lako umemdharau kabisa Mwenyezi-Mungu, mtoto wako atakufa.”
15 Kisha Nathani akarudi nyumbani kwake. Mwenyezi-Mungu alimpiga mtoto ambaye Bathsheba mkewe Uria alimzalia Daudi, naye akawa mgonjwa.
16 Daudi alimwomba Mungu mtoto apate nafuu. Alikwenda chumbani kwake, na usiku kucha akalala sakafuni.
17 Wazee waliokuwa wanamwangalia katika jumba hilo walimfuata na kumsihi aamke, lakini yeye alikataa, na hakula chakula chochote pamoja nao.
18 Juma moja baadaye, mtoto huyo akafa. Watumishi wa Daudi waliogopa kumwambia kuwa mtoto amekufa, kwani walifikiri, “Mtoto huyo alipokuwa hai, tulizungumza naye, lakini hakutusikiliza. Sasa, tutamwambiaje kuwa mtoto wake amekufa? Huenda akajidhuru.”
19 Daudi alipowaona watumishi wake wananongonezana, akagundua kuwa mtoto wake amekufa. Hivyo, akawauliza, “Je, mtoto amekufa?” Nao wakamjibu, “Naam! Amekufa.”
20 Kisha, Daudi aliinuka kutoka sakafuni, akaoga, akajipaka mafuta na kubadilisha mavazi yake. Halafu akaenda katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu na kuabudu. Kisha akarudi nyumbani na alipotaka chakula, akapewa, naye akala.
21 Ndipo watumishi wake wakamwuliza, “Ni jambo gani hili ulilofanya? Mtoto alipokuwa hai, wewe ulifunga na kumlilia. Lakini alipokufa, umeinuka, ukala chakula.”
22 Daudi akawajibu, “Ni kweli mtoto alipokuwa hai, nilifunga na kulia. Nilifanya hivyo kwani nilifikiri, ‘Nani anajua? Huenda Mwenyezi-Mungu akanirehemu ili mtoto aishi’.
23 Lakini sasa amekufa, ya nini nifunge? Je, mimi naweza kumrudisha duniani? Siku moja, nitakwenda huko alikokwenda, lakini yeye hawezi kurudi kwangu.”
24 Halafu Daudi akamfariji Bathsheba mkewe. Akalala naye, naye akapata mimba na kujifungua mtoto wa kiume, ambaye Daudi alimwita Solomoni. Mwenyezi-Mungu alimpenda mtoto huyo,
25 naye akamtuma nabii Nathani kwa Daudi kuwa amwite mtoto huyo Yedidia kwa ajili ya Mwenyezi-Mungu.
26 Wakati huo, Yoabu aliushambulia Raba mji wa Waamoni, naye akauteka huo mji wa kifalme.
27 Yoabu akatuma ujumbe kwa Daudi, “Nimeushambulia mji wa Raba, nami nimelikamata bwawa lao la maji.
28 Sasa wakusanye watu wote waliosalia, upige kambi kuuzunguka na kuuteka. La sivyo, nikiuteka, utaitwa kwa jina langu.”
29 Hivyo, Daudi akakusanya watu wote akaenda Raba, akaushambulia na kuuteka mji huo.
30 Kisha akachukua taji ya mfalme wao kutoka kichwani pake. Uzito wa taji hiyo ya dhahabu ulikuwa kilo thelathini na tano; na ndani yake mlikuwamo jiwe la thamani. Naye Daudi akavikwa taji hiyo kichwani pake. Pia aliteka idadi kubwa sana ya nyara katika mji huo.
31 Halafu aliwachukua watu wa mji huo, akawaweka wafanye kazi wakitumia misumeno, sururu za chuma, mashoka ya chuma na kuwatumia kufanya kazi katika tanuri ya matofali; hivyo ndivyo alivyoitenda miji yote ya Waamoni. Hatimaye Daudi na watu wote walirudi Yerusalemu.
1 Absalomu, alikuwa na dada yake mzuri aliyeitwa Tamari. Muda si muda, Amnoni, mtoto mwingine wa kiume wa Daudi, akampenda sana Tamari.
2 Amnoni aliteseka sana hata akajifanya mgonjwa kwa sababu ya dada yake Tamari hasa kwa vile Tamari alikuwa bikira, na ilionekana jambo lisilowezekana kwa Amnoni kufanya chochote naye.
3 Lakini Amnoni alikuwa na rafiki aliyeitwa Yonadabu, mtoto wa Shama, ndugu ya Daudi. Yonadabu alikuwa mtu mwerevu sana.
4 Yonadabu akamwambia Amnoni, “Wewe ni mtoto wa mfalme, kwa nini unakonda na unaonekana huna furaha kila siku? Mbona hutaki kuniambia.” Amnoni akamwambia, “Nampenda Tamari, dada ya ndugu yangu Absalomu.”
5 Yonadabu akamwambia, “Wewe jilaze kitandani ukidai kuwa u mgonjwa. Baba yako atakapokuja kukuona, wewe msihi ukisema, ‘Mruhusu dada yangu, Tamari, aje aniletee mkate nipate kula na aniandalie chakula mbele yangu ili nikione naye mwenyewe anilishe.’”
6 Hivyo, Amnoni akaendelea kulala kitandani, akijifanya mgonjwa. Mfalme alipokwenda kumwona, Amnoni alimwambia, “Nakuomba, Tamari aje hapa anitengenezee mikate michache huku nikimwangalia. Halafu yeye mwenyewe anilishe.”
7 Hivyo, Daudi alipeleka ujumbe kwa Tamari kwamba aende nyumbani kwa kaka yake Amnoni, akamtengenezee chakula.
8 Tamari alikwenda huko, akamkuta Amnoni amelala. Akachukua unga, akaukanda, na kuoka mikate mbele ya Amnoni.
9 Mikate hiyo ilipokuwa tayari, Tamari akaiopoa kutoka kikaangoni. Akampelekea Amnoni, lakini Amnoni alikataa kula, akasema kila mmoja na atolewe nje, na wote wakaondoka.
10 Kisha, Amnoni akamwambia Tamari, “Sasa niletee mikate hiyo chumbani kwangu, halafu unilishe.” Tamari aliichukua mikate aliyoiandaa na kuipeleka chumbani kwa kaka yake Amnoni.
11 Hapo, alipokuwa anampatia mikate hiyo, Amnoni alimkamata na kumwambia, “Njoo ulale nami.”
12 Tamari akamwambia, “Sivyo, kaka yangu, usinilazimishe. Kitendo hiki hakifanyiki katika Israeli. Usifanye kitendo hiki cha kipumbavu.
13 Kwa upande wangu, siwezi kuvumilia aibu hiyo. Na kwa upande wako, utakuwa mmoja wa wapumbavu wa Israeli. Basi, mimi nakusihi uzungumze na mfalme kwani hatakukataza kunioa.”
14 Lakini Amnoni hakutaka kumsikiliza na kwa kuwa alimzidi nguvu, alimlazimisha, akalala naye.
15 Kisha, Amnoni akamchukia Tamari kupita kiasi. Akamchukia Tamari kuliko alivyompenda hapo awali. Akamwambia Tamari, “Ondoka mara moja.”
16 Tamari akamjibu, “Sivyo kaka yangu; ovu hili kubwa la kunifukuza ni baya zaidi kuliko lile ulilonitendea.” Lakini Amnoni hakutaka kumsikiliza.
17 Akamwita kijana wake aliyemtumikia, akamwambia, “Mtoe mwanamke huyu mbele yangu. Na mlango uufunge kwa komeo.”
18 Amnoni na yule kijana wakamtoa nje na kuufunga mlango kwa komeo. Tamari alikuwa amevaa vazi refu lenye mikono mirefu kwani hivyo ndivyo walivyovaa mabikira wa mfalme zamani hizo.
19 Basi, Tamari alijipaka majivu kichwani, akalipasua vazi lake, akaweka mikono yake kichwani, halafu akaondoka huku analia kwa sauti.
20 Kaka yake, Absalomu, alipomwona, alimwuliza, “Je, Amnoni kaka yako amelala nawe? Tulia dada yangu. Yeye ni kaka yako. Usilitie jambo hilo moyoni mwako.” Hivyo, Tamari aliishi katika nyumba ya Absalomu akiwa na huzuni na mpweke.
21 Mfalme Daudi aliposikia jambo hilo alikasirika sana.
22 Absalomu alimchukia Amnoni sana hata hakusema naye, kwa sababu alimshika kwa nguvu dada yake Tamari akalala naye.
23 Baada ya miaka miwili mizima, Absalomu alikuwa na shughuli ya kuwakata kondoo wake manyoya mjini Baal-hasori, karibu na Efraimu. Akawaalika watoto wote wa kiume wa mfalme.
24 Absalomu alimwendea mfalme Daudi, akamwambia, “Tazama, mimi mtumishi wako ninao wakata-kondoo manyoya. Nakuomba wewe mfalme pamoja na watumishi wako, mwende pamoja nami, mtumishi wako.”
25 Mfalme akamjibu, “Sivyo, mwanangu, tusiende wote; tusije tukawa mzigo kwako.” Ingawa Absalomu alizidi kumsihi baba yake aende, lakini mfalme alikataa, ila alimpa baraka zake.
26 Halafu, Absalomu akamwambia, “Kama huendi, basi, mruhusu ndugu yangu Amnoni twende naye.” Mfalme akamjibu, “Lakini kwa nini aende pamoja nanyi?”
27 Lakini Absalomu alizidi kumsihi, na mwishowe mfalme akamruhusu Amnoni na wanawe wengine waende kwenye sherehe hiyo.
28 Absalomu akawaambia watumishi wake, “Mwangalieni Amnoni atakapokuwa amekunywa divai na kufurahi. Nitakapowaambia, ‘Mpigeni Amnoni,’ muueni. Hiyo ni amri yangu kwenu. Jipeni moyo na muwe hodari.”
29 Hivyo, watumishi wa Absalomu walimtendea Amnoni kama walivyoamriwa na Absalomu, kisha wana wa kiume wengine wa mfalme wakaondoka kila mmoja akapanda nyumbu wake na kukimbia.
30 Walipokuwa bado njiani, Daudi alipata habari kuwa Absalomu amewaua watoto wake wote hakuna hata mmoja aliyesalia.
31 Mfalme Daudi aliinuka, akararua mavazi yake kwa huzuni akalala chini. Hata na watumishi wake wote waliokuwa wamesimama karibu naye walirarua mavazi yao.
32 Lakini Yonadabu, mwana wa Shimea, ndugu ya Daudi akamwambia, “Bwana wangu, usifikiri kuwa wanao wote wameuawa. Amnoni pekee ndiye aliyeuawa. Haya Absalomu aliyakusudia kuyafanya tangu wakati ule Amnoni alipomshika kwa nguvu dada yake Tamari na kulala naye.
33 Hivyo, bwana wangu, usifikiri moyoni mwako kwamba watoto wako wote wamekufa. Ni Amnoni pekee ndiye aliyeuawa.”
34 Lakini Absalomu alikuwa amekwisha kimbia. Naye kijana aliyekuwa na zamu ya ulinzi, mara akaona kundi kubwa la watu wanakuja kutokea mlimani katika barabara ya kutoka Horonaimu.
35 Yonadabu akamwambia Daudi, “Tazama mfalme, wanao wanakuja kama nilivyokuambia mimi mtumishi wako.”
36 Mara tu yule mtumishi alipomaliza kusema, wana wa kiume wa mfalme wakaingia, wakaanza kulia kwa sauti. Mfalme na watumishi wake wote, wakalia kwa uchungu.
37 Lakini Absalomu alikimbilia kwa Talmai mwana wa Amihudi, mfalme wa mji wa Geshuri. Mfalme Daudi akamwombolezea mwanawe Amnoni kwa siku nyingi.
38 Absalomu alikimbilia mjini Geshuri, akakaa huko kwa muda wa miaka mitatu.
39 Baada ya mfalme Daudi kutulia kutokana na kifo cha Amnoni, alianza kutamani kumwona mwanawe Absalomu.
1 Yoabu mwana wa Seruya, alitambua kwamba maelekeo ya moyo wa Daudi yalikuwa kwa Absalomu tu.
2 Hivyo alituma watu huko Tekoa ili wamtafutie mwanamke mwenye hekima. Walipomleta, akamwambia, “Jisingizie unafanya matanga. Vaa nguo za kuomboleza, usijipake mafuta, ila ujifanye kama mwanamke ambaye amekuwa katika maombolezo ya wafu kwa muda mrefu.
3 Halafu nenda kwa mfalme ukamwambie yale ninayokuambia.” Kisha Yoabu akamwambia maneno ya kumwambia mfalme.
4 Huyo mwanamke kutoka Tekoa akaenda kwa mfalme, akaanguka kifudifudi, mbele ya mfalme, akasujudu, akamwambia, “Ee mfalme, nisaidie.”
5 Mfalme akamwambia, “Una shida gani?” Yule mwanamke akajibu, “Nasikitika, mimi ni mjane, mume wangu amekufa.
6 Nilikuwa na watoto wa kiume wawili. Siku moja, walipokuwa mbugani, walianza kugombana. Kwa vile hapakuwa na mtu yeyote wa kuwaamua, mmoja akampiga mwenzake, akamuua.
7 Sasa ndugu zangu wote wamenigeuka mimi mtumishi wako; wanataka nimtoe kwao mtoto aliyemuua mwenzake ili wamuue kwa kuyaangamiza maisha ya ndugu yake. Hivyo, watamuua huyu ambaye sasa ndiye mrithi. Wakifanya hivyo, watazima kabisa tumaini langu lililobakia, na mume wangu hataachiwa jina wala mzawa duniani.”
8 Mfalme akamwambia yule mwanamke, “Rudi nyumbani nitaamuru jambo lako liangaliwe.”
9 Yule mwanamke kutoka Tekoa akasema, “Bwana wangu mfalme, hatia yote na iwe juu yangu na juu ya jamaa ya baba yangu. Hivyo, wewe na ufalme wako msiwe na hatia.”
10 Mfalme akamwambia, “Mtu yeyote akikutishia mlete kwangu na hatakuja kukugusa tena.”
11 Yule mwanamke akamwambia, “Tafadhali, mfalme, niombee kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, ili yule ndugu yangu ambaye angelipiza kisasi cha mauaji ya mwanangu asifanye hatia nyingine kubwa ya kumwua yule mtoto wangu mwingine.” Mfalme Daudi akamwambia, “Kama Mwenyezi-Mungu aishivyo, hakuna hata unywele mmoja wa mwanao utakaoanguka chini.”
12 Yule mwanamke akamwambia, “Nakuomba, mimi mtumishi wako, uniruhusu niseme neno moja kwako mfalme.” Mfalme akamwambia, “Sema”.
13 Yule mwanamke akamwambia, “Kwa nini basi, umepanga uovu huu dhidi ya watu wa Mungu? Kulingana na uamuzi wako juu ya jambo hilo wewe mwenyewe umejihukumu kuwa na hatia kwa sababu humruhusu mwanao arudi nyumbani kutoka alikokimbilia.
14 Sisi sote lazima tutakufa. Sisi ni kama maji yaliyomwagika chini ambayo hayazoleki. Hata Mungu hafanyi tofauti kwa mtu huyu na tofauti kwa mwingine; yeye hutafuta njia ili waliopigwa marufuku, wakakimbia, wapate kurudi.
15 Mimi nimekuja kuzungumza nawe, bwana wangu mfalme, kwani wamenitisha. Basi, mimi mtumishi wako, niliwaza kuwa, ‘Afadhali nikazungumze na mfalme, huenda akanitimizia mahitaji yangu mimi mtumishi wake.
16 Maana mfalme atanisikiliza na kuniokoa mikononi mwa mtu ambaye anataka kuniangamiza mimi pamoja na mwanangu kutoka urithi wa Mungu’.
17 Nami mjakazi wako nilifikiri kuwa, ‘Neno lake bwana wangu mfalme litanipa amani moyoni, kwani wewe bwana wangu mfalme ni kama malaika wa Mungu katika kupambanua mema na mabaya.’ Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, awe pamoja nawe.”
18 Ndipo mfalme alipomjibu yule mwanamke, “Usinifiche jambo lolote nitakalokuuliza.” Yule mwanamke akasema, “Sema bwana wangu mfalme.”
19 Mfalme akamwuliza, “Je, Yoabu anahusika katika jambo hili?” Yule mwanamke akasema, “Kama uishivyo, bwana wangu mfalme, mtu hawezi kukwepa kulia au kushoto kuhusu jambo ulilosema bwana wangu mfalme. Yoabu yule mtumishi wako ndiye aliyenituma. Ni yeye aliyeniambia maneno yote haya niliyokuambia mimi mtumishi wako.
20 Yoabu alifanya hivyo ili kubadilisha mambo. Lakini, wewe bwana wangu, una hekima kama ya malaika wa Mungu hata unaweza kujua mambo yote yaliyoko duniani.”
21 Kisha, mfalme akamwambia Yoabu, “Sasa sikiliza, natoa kibali changu ili umrudishe nyumbani yule kijana Absalomu.”
22 Yoabu alianguka chini kifudifudi, akasujudu na kumtakia mfalme baraka, akasema, “Leo, mimi mtumishi wako, bwana wangu mfalme, ninajua kuwa nimepata kibali mbele yako, kwa kulikubali ombi langu.”
23 Hivyo, Yoabu aliondoka, akaenda Geshuri kumleta Absalomu mjini Yerusalemu.
24 Lakini mfalme akasema, “Absalomu aishi mbali nami; aishi nyumbani kwake. Asije hapa kuniona.” Hivyo, Absalomu akawa anaishi mbali, nyumbani kwake na hakumwona mfalme Daudi.
25 Katika Israeli yote, hakuna yeyote aliyesifiwa kwa uzuri kama Absalomu. Tangu nyayo zake hadi utosini mwake, Absalomu hakuwa na kasoro yoyote.
26 Kila alipokata nywele zake, (na kila mwishoni mwa mwaka alikata nywele zake kwani zilikuwa nzito), alipozipima, zilikuwa na uzito wa kilo mbili kulingana na vipimo vya kifalme.
27 Absalomu alizaa watoto watatu wa kiume pamoja na binti mmoja jina lake Tamari. Tamari alikuwa mwanamke mzuri.
28 Basi, Absalomu aliishi mjini Yerusalemu kwa muda wa miaka miwili mizima bila kumwona mfalme Daudi.
29 Kisha, Absalomu alimtumia ujumbe Yoabu, ili aende kwa mfalme kwa niaba yake, lakini Yoabu akakataa. Absalomu akatuma ujumbe mara ya pili lakini Yoabu akakataa.
30 Basi, Absalomu akawaambia watumishi wake, “Angalieni Yoabu ana shamba la shayiri karibu na langu. Nendeni mkalichome moto.” Kwa hiyo watumishi wa Absalomu wakalichoma moto shamba la Yoabu.
31 Yoabu akaenda nyumbani kwa Absalomu akamwuliza, “Kwa nini watumishi wako wamechoma moto shamba langu?”
32 Absalomu akamjibu, “Tazama, nilikupelekea ujumbe, uje huku ili nikutume kwa mfalme, ukamwulize: ‘Kwa nini niliondoka Geshuri? Ingekuwa bora kwangu kubaki huko’. Sasa nisaidie nipate kumwona mfalme. Kama nina hatia basi, na aniue!”
33 Kwa hiyo Yoabu akaenda na kumweleza mfalme maneno hayo yote, naye akamwita Absalomu, naye akaingia kwa mfalme, akaanguka kifudifudi mbele ya mfalme. Na mfalme akambusu Absalomu.
1 Baada ya tukio hilo, Absalomu alijipatia gari, farasi na watu hamsini wa kumtangulia.
2 Absalomu alizoea kuamka asubuhi na mapema na kwenda kusimama kwenye njia inayoelekea kwenye lango la mji. Mtu yeyote aliyekuwa na madai ambayo alitaka kuyapeleka kwa mfalme ili kupata uamuzi wake, Absalomu humwita mtu huyo kando na kumwuliza, “Unatoka mji gani?” Kama mtu huyo akisema ametoka mji fulani wa kabila la Israeli,
3 Absalomu humwambia, “Madai yako ni ya haki kabisa. Lakini hakuna mtu yeyote aliyeteuliwa na mfalme kukusikiliza.”
4 Tena, Absalomu humwambia, “Laiti mimi ningekuwa mwamuzi wa Israeli! Kila mtu mwenye madai au shauri angekuja kwangu, nami ningempa haki yake!”
5 Zaidi ya hayo, Absalomu alinyosha mkono wake akamkumbatia na kumbusu mtu yeyote aliyekuja kumwinamia na kumsujudu.
6 Basi, hivyo ndivyo Absalomu alivyowatendea Waisraeli wote waliokuja kutafuta uamuzi wa mfalme. Kwa kufanya hivyo, Absalomu aliiteka mioyo ya Waisraeli.
7 Baada ya miaka minne, Absalomu alimwambia mfalme, “Tafadhali uniruhusu niende huko Hebroni ili kutimiza nadhiri yangu ambayo nilimwekea Mwenyezi-Mungu;
8 maana, mimi mtumishi wako, nilipoishi kule Geshuri katika Aramu, nilimwekea Mwenyezi-Mungu nadhiri nikisema kuwa kama Mwenyezi-Mungu atanirudisha mjini Yerusalemu basi, nitamwabudu yeye.”
9 Mfalme akamwambia, “Basi, nenda kwa amani.” Absalomu akaondoka kwenda Hebroni.
10 Lakini Absalomu alituma wajumbe kwa siri katika makabila yote ya Israeli, wakasema, “Mara moja mtakaposikia mlio wa tarumbeta, semeni, ‘Absalomu ni mfalme katika Hebroni!’”
11 Absalomu alipokwenda huko Hebroni, alikwenda na watu 200 aliowaalika kutoka Yerusalemu, nao walikwenda huko kwa nia njema, wala hawakujua chochote kuhusu mpango wa Absalomu.
12 Wakati Absalomu alipokuwa akitoa tambiko, alituma ujumbe mjini Gilo kumwita Ahithofeli, Mgilo, aliyekuwa mshauri wa mfalme Daudi. Uasi wa Absalomu ukazidi kupata nguvu na watu walioandamana naye wakazidi kuongezeka.
13 Mjumbe fulani alipomwendea Daudi na kumwambia, “Watu wa Israeli wamevutwa na Absalomu!”
14 Basi, Daudi akawaambia watumishi wake waliokuwa naye mjini Yerusalemu, “Inukeni tukimbie, la sivyo, hatutaweza kumwepa Absalomu. Tufanye haraka kuondoka asije akatuletea maafa na kuuangamiza mji kwa mapanga.”
15 Lakini watumishi wake wakamwambia, “Sisi watumishi wako, bwana wetu mfalme, tuko tayari kufanya lolote unaloamua.”
16 Basi, mfalme akaondoka pamoja na jamaa yake, lakini akawaacha masuria wake kumi wakishughulika na kazi za nyumbani.
17 Mfalme akaondoka pamoja na watu wake wote. Lakini akatua kidogo walipofikia nyumba ya mwisho mjini.
18 Watumishi wote wa mfalme, Wakerethi wote, Wapelethi wote, pamoja na Wagiti 600 waliomfuata mfalme Daudi kutoka mji wa Gathi, waliondoka pamoja naye wakimtangulia.
19 Kisha, mfalme Daudi alipomwona Itai, Mgiti, alimwambia, “Kwa nini hata wewe umeondoka pamoja nasi? Rudi ukakae na huyo mfalme kijana. Maana wewe ni mgeni huku, tena ni mkimbizi kutoka nyumbani kwenu.
20 Wewe ulikuja huku juzijuzi tu. Je, nikufanye mtu wa kutangatanga pamoja nasi, nikijua kuwa sijui hata kule ninakoenda? Rudi nyumbani pamoja na ndugu zako. Naye Mwenyezi-Mungu akuoneshe fadhili zake na uaminifu.”
21 Lakini Itai akamjibu mfalme, “Kama Mwenyezi-Mungu aishivyo na wewe bwana wangu mfalme uishivyo, popote utakapokuwa, ikiwa ni kwa kufa au ni kwa kuishi, nami mtumishi wako nitakuwapo.”
22 Basi, Daudi akamwambia Itai, “Nenda basi, endelea mbele.” Hivyo, Itai, Mgiti, akapita yeye mwenyewe pamoja na watoto wake.
23 Daudi alipokuwa akipita pamoja na watu wake, watu wote nchini kote walilia kwa sauti. Mfalme Daudi akavuka kijito cha Kidroni pamoja na watu wote, wakapita kuelekea jangwani.
24 Kuhani Abiathari akatoka, hata na kuhani Sadoki akatoka pamoja na Walawi wote huku wamelibeba sanduku la agano la Mungu. Wakaliweka chini lile sanduku la Mungu, mpaka watu wote walipopita kutoka mjini Yerusalemu.
25 Kisha mfalme akamwambia Sadoki, “Lirudishe sanduku la agano la Mungu mjini. Kama ninakubalika mbele ya Mwenyezi-Mungu, bila shaka atanirudisha na kunijalia kuliona tena sanduku lake na kuyaona maskani yake.
26 Lakini ikiwa Mwenyezi-Mungu hapendezwi nami basi, mimi niko tayari; na anitendee lolote analoona jema kwake.”
27 Mfalme Daudi akamwambia tena Sadoki, “Tazama, mchukue mwanao Ahimaasi na Yonathani mwana wa Abiathari mrudi nyumbani kwa amani.
28 Lakini nitakuwa nikingojea penye vivuko huku nyikani, mpaka nitakapopata habari kutoka kwako.”
29 Kwa hiyo Sadoki na Abiathari wakalirudisha sanduku la agano la Mungu mjini Yerusalemu, wakabaki humo.
30 Lakini Daudi aliendelea, akapanda Mlima wa Mizeituni huku analia, bila viatu na kichwa chake kimefunikwa. Hata watu wote waliokuwa pamoja naye walivifunika vichwa vyao wakawa wanapanda mlima huku wanalia.
31 Wakati huo, Daudi aliambiwa kuwa hata Ahithofeli alikuwa mmoja wa waasi waliojiunga na Absalomu. Lakini Daudi akaomba akisema, “Ee Mwenyezi-Mungu nakuomba, uufanye mpango wa Ahithofeli usifanikiwe.”
32 Daudi alipofika kwenye kilele cha mlima, mahali pa kumwabudia Mungu, mtu mmoja jina lake Hushai kutoka Arki alikuja ili kumlaki, mavazi yake yakiwa yameraruka na kichwani pake kuna mavumbi.
33 Daudi akamwambia, “Ukienda pamoja nami, utakuwa mzigo kwangu.
34 Lakini kama utarudi mjini Yerusalemu na kumwambia Absalomu, ‘Nitakuwa mtumishi wako, ee mfalme; kama vile nilivyokuwa mtumishi wa baba yako, hapo awali’; basi utanifanyia mpango wa Ahithofeli usifanikiwe.
35 Makuhani Sadoki na Abiathari wako pamoja nawe mjini! Basi, chochote utakachosikia kutoka nyumbani kwa mfalme, waambie makuhani Sadoki na Abiathari.
36 Tazama, watoto wao wawili wa kiume, Ahimaasi mwana wa Sadoki na Yonathani mwana wa Abiathari, wako pamoja nao. Na chochote mtakachosikia mtanipelekea habari kwa njia yao.”
37 Basi, Hushai rafiki ya mfalme Daudi, akarudi mjini na wakati Absalomu alipokuwa anaingia mjini Yerusalemu.
1 Daudi alipokuwa amekipita kidogo kilele cha mlima, Siba mtumishi wa Mefiboshethi alimlaki Daudi akiwa na punda wawili ambao walikuwa wametandikwa huku wamebeba mikate200, vishada 100 vya zabibu kavu, matunda 100 ya kiangazi na kiriba cha divai.
2 Mfalme akamwuliza Siba, “Kwa nini umeleta vitu hivi?” Siba akamjibu, “Punda ni kwa ajili ya kupanda jamaa yako, mikate na matunda ya kiangazi ni kwa ajili ya vijana wote, nayo divai ni kwa ajili ya watakaozimia jangwani.”
3 Mfalme akamwuliza, “Mwana wa bwana wako yuko wapi?” Siba akamwambia mfalme, “Yeye amebaki mjini Yerusalemu kwa sababu anadhani kwamba watu wa Israeli watamrudishia ufalme wa Shauli babu yake.”
4 Mfalme akamwambia Siba, “Basi, yale yaliyokuwa mali ya Mefiboshethi sasa ni mali yako.” Siba akamwambia, “Nashukuru, bwana wangu mfalme, nami naomba nipate fadhili mbele yako daima.”
5 Wakati Daudi alipowasili kule Bahurimu, alitokea mtu mmoja wa ukoo wa Shauli, jina lake Shimei mwana wa Gera, akaanza kumlaani Daudi kwa mfululizo.
6 Akawa anamtupia mfalme Daudi mawe pamoja na watumishi wake. Watu wengine wote na mashujaa wakawa wanamzunguka Daudi upande wa kulia na kushoto.
7 Shimei alimlaani Daudi akisema, “Nenda zako; nenda zako, wewe mtu mwuaji, mtu asiye na faida!
8 Mwenyezi-Mungu amekulipiza kisasi kutokana na kumwaga damu yote ya jamaa ya Shauli, ambaye sasa wewe umechukua ufalme mahali pake. Sasa, Mwenyezi-Mungu amempa ufalme Absalomu mwanao. Tazama, sasa maangamizi yamekupata kwa sababu wewe ni mwuaji.”
9 Ndipo Abishai mwana wa Seruya, akamwambia mfalme, “Kwa nini huyu mbwa mfu akulaani wewe bwana wangu mfalme? Niruhusu nimwendee, nami nitakikata kichwa chake.”
10 Lakini mfalme akamwambia, “Je, kuna nini kati yangu na nyinyi wana wa Seruya? Ikiwa Mwenyezi-Mungu amemwambia ‘Mlaani Daudi’, nani sasa anaweza kuuliza ‘Kwa nini umefanya hivyo?’”
11 Tena mfalme Daudi akamwambia Abishai na hata watumishi wake wote, “Ikiwa mtoto wangu mwenyewe anayawinda maisha yangu, je si zaidi mtu wa kabila la Benyamini? Nyinyi mwacheni anilaani kwani Mwenyezi-Mungu amemwagiza anilaani.
12 Huenda Mwenyezi-Mungu akaangalia uovu wangu, naye akanilipa wema kwa laana hii ninayopata leo.”
13 Hivyo mfalme Daudi na watu wake wakaendelea na safari huku Shimei akiwa anamfuata akimtupia mawe na kurusha juu vumbi dhidi ya mfalme Daudi. Shimei alikuwa akitembea kileleni mwa mlima, mkabala na mfalme Daudi.
14 Kisha mfalme pamoja na watu wote waliokuwa pamoja naye, wakafika mtoni wakiwa wamechoka. Basi wakapumzika.
15 Wakati huo, Absalomu na watu wote wa Israeli wakaenda mjini Yerusalemu na Ahithofeli pamoja nao.
16 Hushai kutoka Arki, rafiki ya Daudi, akamwendea Absalomu, akamwambia, “Uishi mfalme! Uishi mfalme!”
17 Absalomu akamwuliza Hushai, “Je, huu ndio uaminifu wako kwa rafiki yako Daudi? Mbona hukuenda pamoja na rafiki yako?”
18 Hushai akamjibu, “La! Maana yule ambaye amechaguliwa na Mwenyezi-Mungu, watu hawa na watu wote wa Israeli, huyo ndiye, mimi nitakuwa wake yeye, na nitabaki naye.
19 Zaidi ya hayo, je, nitamtumikia nani? Je, si mwana wa rafiki yangu? Basi, kama nilivyomtumikia baba yako ndivyo nitakavyokutumikia wewe.”
20 Ndipo Absalomu alipomwambia Ahithofeli, “Nishauri; tufanye nini?”
21 Ahithofeli akamwambia Absalomu, “Waingilie masuria wa baba yako ambao aliwaacha kuangalia nyumba yake. Baadaye watu wote wa Israeli watakaposikia kwamba umechukizwa na baba yako, hapo watu wote walio pamoja nawe watatiwa nguvu.”
22 Hivyo, watu wakampigia Absalomu hema kwenye paa, naye akalala na masuria wa baba yake, watu wote wa Israeli wakiwa wanaona.
23 Siku hizo, shauri lolote alilotoa Ahithofeli lilikuwa kama limetolewa na Mungu. Na shauri alilotoa Ahithofeli liliheshimiwa na Daudi na Absalomu.
1 Zaidi ya Hayo, Ahithofeli alimwambia Absalomu, “Niruhusu nichague watu 12,000, niondoke na kumfuatia Daudi leo usiku.
2 Nitamshambulia akiwa amechoka na amevunjika moyo, nami nitamtia wasiwasi. Watu wote walio pamoja naye watakimbia. Nitampiga mfalme peke yake,
3 na kuwarudisha watu wengine wote kwako kama bibiarusi anavyokwenda nyumbani kwa mumewe. Wewe unayatafuta maisha ya mtu mmoja tu; na watu wengine watakuwa na amani.”
4 Shauri hilo la Ahithofeli lilimpendeza Absalomu na wazee wote wa Israeli.
5 Kisha, Absalomu akasema, “Mwiteni Hushai pia, yule mtu wa Arki, tusikie analotaka kusema.”
6 Hushai alipofika kwa Absalomu, Absalomu alimwuliza, “Hivyo ndivyo alivyosema Ahithofeli. Je, tufanye kama alivyotushauri? Kama sivyo, basi, tuambie lako.”
7 Hushai akamwambia Absalomu, “Wakati huu, shauri alilolitoa Ahithofeli si jema.”
8 Zaidi ya hayo, Hushai akamwambia, “Wewe unajua kwamba baba yako na watu wake ni mashujaa na kwamba wamekasirishwa kama dubu jike nyikani aliyenyanganywa watoto wake. Mbali na hayo, unajua kwamba baba yako ni bingwa wa vita. Yeye hatakaa usiku kucha pamoja na watu wake.
9 Hata sasa amekwisha jificha kwenye mojawapo ya mapango yaliyoko huko au mahali pengine. Mtu yeyote atakayesikia kuuawa kwa watu katika mashambulizi ya kwanza atasema kuwa mauaji yametokea katika kundi la wafuasi wa Absalomu.
10 Watu wako watakaposikia hivyo, hata wale watu wako walio shupavu, wenye mioyo shupavu kama ya simba, watavunjika moyo kabisa kwa hofu. Maana, Waisraeli wote wanajua kuwa baba yako ni shujaa na wote walio pamoja naye ni watu hodari.
11 Shauri langu ni kwamba, uwakusanye kwako watu wote wa Israeli tangu Dani hadi Beer-sheba, upande wa kusini, wawe wengi kama mchanga wa bahari, na wewe mwenyewe binafsi uende vitani.
12 Nasi tutamwendea Daudi mahali popote anapoweza kupatikana na tutamvamia kama umande unavyoiangukia ardhi. Basi, hakuna atakayesalia hata kama atakuwa yeye mwenyewe au watu wake wote walio pamoja naye.
13 Iwapo atakimbilia mji fulani, basi, watu wote wa Israeli wataleta kamba na kuuburuta mji huo, hadi bondeni, kisibaki chochote hata jiwe dogo la mji huo.”
14 Absalomu pamoja na watu wote wa Israeli wakasema, “Shauri la Hushai ni bora kuliko shauri la Ahithofeli.” Wakakataa shauri la Ahithofeli kwa kuwa Mwenyezi-Mungu alikuwa amepanga kulishinda shauri jema la Ahithofeli ili aweze kumletea Absalomu maafa.
15 Kisha Hushai akawaambia makuhani Sadoki na Abiathari jinsi Ahithofeli na yeye mwenyewe walivyomshauri Absalomu na wazee wa Israeli.
16 Akawaambia wampelekee Daudi habari upesi kwamba asilale usiku kwenye vivuko jangwani, bali, kwa njia yoyote ile, avuke na kuondoka ili asije akakamatwa na kuuawa, yeye pamoja na watu wake wote.
17 Wakati huo, Yonathani na Ahimaasi walikuwa wakimngojea karibu na Enrogeli, ili wasionekane na mtu yeyote wakiingia mjini. Kila mara mtumishi fulani wa kike alikuwa akiwapelekea habari nao wakaipeleka kwa mfalme Daudi.
18 Lakini wakati huu, walionekana na kijana mmoja ambaye alikwenda na kumhabarisha Absalomu. Hivyo, Yonathani na Ahimaasi waliondoka haraka, wakaenda Bahurimu nyumbani kwa mtu fulani aliyekuwa na kisima uani kwake. Wakaingia humo kisimani na kujificha.
19 Mwanamke mwenye nyumba hiyo akachukua kifuniko na kukifunika kisima hicho, halafu akaanika nafaka juu ya kifuniko. Habari hizo hazikujulikana.
20 Watumishi wa Absalomu walipowasili kwa huyo mwanamke, wakamwambia, “Wako wapi Ahimaasi na Yonathani?” Yule mwanamke akawaambia, “Wamekwenda ngambo ya kijito.” Walipowatafuta na kuwakosa, wakarudi mjini Yerusalemu.
21 Baada ya watumishi wa Absalomu kuondoka, Yonathani na Ahimaasi walitoka kisimani, wakaenda kwa mfalme Daudi na kumpasha habari. Wakamwambia, “Ondoka, uende ngambo ya mto, kwa sababu Ahithofeli amemshauri Absalomu dhidi yako.”
22 Kwa hiyo, Daudi akaondoka na watu wote waliokuwa pamoja naye, wakavuka mto Yordani. Ilipofika asubuhi hakuna mtu aliyebaki nyuma bila kuvuka mto Yordani.
23 Ahithofeli alipoona kwamba shauri lake halikufuatwa, alitandika punda wake, akaenda nyumbani, kwenye mji wake. Alipofika huko, alipanga vizuri mambo ya nyumbani kwake, akajinyonga. Akafariki na kuzikwa kwenye kaburi la baba yake.
24 Basi, Daudi akaenda Mahanaimu. Absalomu akavuka mto Yordani na watu wote wa Israeli.
25 Wakati huo, Absalomu alikuwa amemweka Amasa kuwa mkuu wa jeshi badala ya Yoabu. Amasa alikuwa mwana wa Yithra, Mwishmaeli. Mama yake aliitwa Abigali binti wa Nahashi, aliyekuwa dada yake, Seruya, mama yake Yoabu.
26 Absalomu pamoja na watu wa Israeli walipiga kambi yao katika nchi ya Gileadi.
27 Daudi alipowasili Mahanaimu, Shobi mwana wa Nahashi Mwamoni, kutoka mji wa Raba; Makiri mwana wa Amieli kutoka mji wa Lo-debari, pamoja na Barzilai Mgileadi kutoka mji wa Rogelimu,
28 walipeleka vitanda, mabirika, vyombo vya udongo, ngano, shayiri, unga, bisi, kunde na dengu,
29 asali, siagi, kondoo na jibini kutoka mifugo yao kwa ajili ya Daudi pamoja na watu aliokuwa nao. Maana walisema, “Watu hawa wana njaa, wamechoka na wana kiu kwa ajili ya kusafiri jangwani.”
1 Daudi aliwahesabu watu waliokuwa pamoja naye, akawagawanya katika vikosi vya maelfu chini ya makamanda wao; na vikosi vya mamia, navyo chini ya makamanda wao.
2 Daudi akalituma jeshi lake vitani katika vikosi vitatu: Theluthi moja chini ya Yoabu, theluthi ya pili chini ya Abishai mwana wa Seruya, nduguye Yoabu; na theluthi ya tatu chini ya Itai, Mgiti. Kisha mfalme Daudi akawaambia wote, “Mimi mwenyewe binafsi nitakwenda pamoja nanyi.”
3 Lakini watu wakamwambia, “Hutatoka. Maana, ikiwa tutakimbia, hawatajali juu yetu. Ikiwa nusu yetu watakufa, pia hawatajishughulisha juu yetu. Lakini wewe una thamani kuliko watu 10,000 miongoni mwetu. Hivyo inafaa wewe ubaki mjini na kutupelekea msaada ukiwa mjini.”
4 Mfalme akawaambia, “Lolote mnaloona ni bora kwenu, nitalitenda.” Hivyo, mfalme akasimama kando ya lango, huku jeshi lake likipita: Mamia na maelfu.
5 Mfalme akawaamuru Yoabu, Abishai na Itai, “Kwa ajili yangu, mtendeeni yule kijana Absalomu kwa upole.” Watu wote walimsikia mfalme alipoamuru makamanda wake kuhusu Absalomu.
6 Hivyo, jeshi la Daudi likaenda nyikani kupigana na watu wa Israeli. Mapigano hayo yalifanyika katika msitu wa Efraimu.
7 Watumishi wa Daudi waliwashinda watu wa Israeli. Mauaji ya siku hiyo yalikuwa makubwa kwani watu 20,000 waliuawa.
8 Mapigano hayo yalienea nchini kote na watu wengi walikufa msituni kuliko wale waliouawa kwa upanga vitani.
9 Kisha Absalomu, akiwa amepanda nyumbu, alikutana na watumishi wa Daudi. Nyumbu huyo alipokuwa anapita chini ya tawi kubwa la mwaloni, hapo kichwa cha Absalomu kikakwama kwenye mwaloni. Absalomu akaachwa ananinginia juu. Lakini nyumbu wake akaendelea mbele.
10 Mtu fulani aliyeona tukio hilo, akamwambia Yoabu, “Nimemwona Absalomu akininginia kwenye mwaloni.”
11 Yoabu akamwambia mtu huyo, “Nini? Ulimwona Absalomu? Kwa nini, basi, hukumpiga papo hapo hadi ardhini? Ningefurahi kukulipa vipande kumi vya fedha na mkanda.”
12 Lakini yule mtu akamwambia Yoabu, “Hata kama ningeuona uzito wa vipande 1,000 vya fedha mkononi mwangu, nisingeunyosha mkono wangu dhidi ya mwana wa mfalme. Maana, tulimsikia mfalme alipokuamuru wewe Abishai na Itai kwamba, kwa ajili yake, mumlinde kijana Absalomu.
13 Kwa upande mwingine, kama ningemtendea kwa hila (na hakuna lolote linalofichika kwa mfalme) wewe mwenyewe ungeniruka.”
14 Yoabu akamwambia, “Mimi sina wakati wa kupoteza pamoja nawe.” Hapo Yoabu akachukua mikuki midogo mitatu mkononi mwake, akaenda na kumchoma Absalomu moyoni, Absalomu akiwa bado hai kwenye tawi la mwaloni.
15 Kisha, vijana kumi waliombebea silaha Yoabu, wakaja kumzunguka Absalomu, wakampiga na kumwua.
16 Ndipo Yoabu akapiga tarumbeta na wanajeshi wote wakarudi kuwafuatia watu wa Israeli, kwani Yoabu aliwakataza.
17 Wakamchukua Absalomu wakamtupa kwenye shimo kubwa msituni na kurundika rundo kubwa sana la mawe. Watu wote wa Israeli wakakimbia, kila mmoja nyumbani kwake.
18 Absalomu, wakati wa uhai wake, alikuwa amejijengea na kujisimikia nguzo iliyoko kwenye Bonde la Mfalme, kwani alisema, “Mimi sina mtoto wa kiume wa kudumisha jina langu ili nikumbukwe.” Nguzo hiyo aliipa jina lake, na inaitwa “Nguzo ya Absalomu” mpaka leo.
19 Kisha, Ahimaasi mwana wa Sadoki, akasema, “Niruhusu nikimbie kumpelekea mfalme habari hizi kuwa Mwenyezi-Mungu amemkomboa katika nguvu za adui zake.”
20 Yoabu akamwambia, “Leo, hutapeleka habari hizo. Unaweza kupeleka habari hizo siku nyingine. Lakini leo hutapeleka habari zozote kwa kuwa mwana wa mfalme amekufa.”
21 Ndipo Yoabu akamwambia mtu mmoja, Mkushi, “Wewe, nenda ukamweleze mfalme yale uliyoona.” Mkushi akainama kwa heshima mbele ya Yoabu, akaondoka mbio.
22 Kisha Ahimaasi mwana wa Sadoki akamwambia Yoabu tena, “Haidhuru; niruhusu na mimi nimkimbilie yule Mkushi!” Yoabu akamwambia, “Mbona unataka kukimbia mwanangu? Wewe hutatuzwa lolote kwa habari hizi!”
23 Ahimaasi akamwambia, “Haidhuru; nitakimbia.” Basi, Yoabu akamwambia, “Haya, kimbia.” Kisha Ahimaasi akakimbia akifuata njia ya nyikani akawahi kumpita yule Mkushi.
24 Daudi alikuwa ameketi kati ya malango mawili ya mji. Naye mlinzi wa lango akapanda ukutani hadi juu ya lango na alipoinua macho yake aliona mtu anakimbia peke yake.
25 Huyo mlinzi akapaza sauti akamwambia mfalme. Mfalme akasema, “Kama yuko peke yake, lazima ana habari.” Yule mtu akazidi kukaribia.
26 Mlinzi akamwona mtu mwingine anakimbia, akaita tena langoni akisema, “Tazama, mtu mwingine anakimbia peke yake!” Mfalme akasema, “Naye analeta habari.”
27 Yule mlinzi akasema, “Naona kuwa yule anayekimbia zaidi ni Ahimaasi mwana wa Sadoki.” Mfalme akasema, “Huyo ni mtu mwema, anatuletea habari njema.”
28 Ndipo Ahimaasi akamwambia mfalme kwa sauti kubwa, “Mambo yote ni sawa.” Akainama mbele ya mfalme, akasujudu na kusema, “Na atukuzwe Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, ambaye amekukomboa kutoka watu walioinua mikono yao dhidi yako, bwana wangu mfalme.”
29 Mfalme akamwambia, “Je, kijana Absalomu hajambo?” Ahimaasi akasema, “Wakati Yoabu aliponituma mimi mtumishi wako, niliona kulikuwa na kelele nyingi, lakini sikufahamu maana yake.”
30 Mfalme akasema, “Kaa kando, na usimame hapo.” Basi, Ahimaasi akaenda kando na kusimama kimya.
31 Ndipo na yule Mkushi akafika; naye akasema, “Kuna habari njema kwako bwana wangu mfalme! Maana Mwenyezi-Mungu leo hii amekukomboa kutoka nguvu za wale wote walioinuka dhidi yako.”
32 Mfalme akamwuliza, “Je kijana Absalomu hajambo?” Mkushi akasema, “Maadui wako, bwana wangu mfalme, pamoja na wote wanaoinuka dhidi yako wakikutakia mabaya, wawe kama huyo kijana Absalomu.”
33 Hapo mfalme alishikwa na huzuni kuu, akapanda kwenye chumba kilichokuwa juu ya lango na kulia. Alipokuwa anapanda, akawa analia akisema, “Mwanangu Absalomu, mwanangu Absalomu! Laiti ningalikufa badala yako! Ole, Absalomu mwanangu! Mwanangu!”
1 Yoabu aliambiwa kwamba mfalme alikuwa akilia na kuomboleza juu ya kifo cha Absalomu.
2 Kwa hiyo, ushindi wa siku hiyo uligeuzwa kuwa maombolezo kwa watu wote, waliposikia kuwa mfalme anamwombolezea Absalomu.
3 Hivyo, siku hiyo, watu waliingia mjini kimyakimya kama watu wanaorudi mjini wakiona aibu kwa kukimbia vita.
4 Mfalme alijifunika uso wake na kulia kwa sauti kubwa akisema, “Ole mwanangu Absalomu! Ole, Absalomu, mwanangu! Mwanangu!”
5 Ndipo Yoabu alipoingia nyumbani kwa mfalme, akamwambia, “Leo umetuaibisha sisi watumishi wako wote ambao leo tumeyaokoa maisha yako, maisha ya watoto wako wa kiume, na maisha ya watoto wako wa kike, maisha ya wake zako na maisha ya masuria wako.
6 Wewe unawapenda wale wanaokuchukia na unawachukia wale wanaokupenda. Umetuonesha waziwazi leo kwamba makamanda na watumishi wako hawana maana kwako. Naona kuwa leo, kama Absalomu angekuwa hai, na sisi sote tungalikuwa tumekufa, wewe ungefurahi.
7 Sasa, simama uzungumze na watumishi wako kwa upole. Maana, naapa kwa Mwenyezi-Mungu kwamba, kama huendi kuzungumza nao, hakuna hata mmoja atakayebaki pamoja nawe leo jioni. Hili litakuwa jambo baya zaidi kwako kuliko maovu yote yaliyokupata tangu ujana wako hadi leo.”
8 Kisha, mfalme akatoka akaenda, akaketi mahali pake karibu na lango. Watu wote walipoambiwa kuwa mfalme yuko langoni, wote walimwendea. Wakati huo, watu wote wa Israeli walikuwa wamekimbia, kila mmoja nyumbani kwake.
9 Watu wote walikuwa wanashindana wao kwa wao katika makabila yote ya Israeli, wakisema, “Mfalme Daudi alitukomboa mikononi mwa adui zetu, alituokoa mikononi mwa Wafilisti. Lakini sasa ameikimbia nchi, akimkimbia Absalomu.
10 Tena Absalomu ambaye tulimpaka mafuta awe mfalme wetu, sasa ameuawa vitani. Sasa, kwa nini hatuzungumzii juu ya kumrudisha mfalme Daudi?”
11 Mfalme Daudi akatuma ujumbe kwa makuhani Sadoki na Abiathari, “Waambieni wazee wa Yuda: ‘Kwa nini wao wawe ndio wa mwisho kumrudisha mfalme nyumbani kwake? Ujumbe wa Israeli yote umenifikia mimi mfalme.
12 Nyinyi ni ndugu zangu, nyinyi ni damu yangu; kwa nini muwe wa mwisho kunirudisha mimi mfalme nyumbani?
13 Mwulizeni pia Amasa kama yeye si damu yangu. Tena Mungu aniue ikiwa simfanyi yeye kuwa kamanda wa jeshi langu tangu leo badala ya Yoabu.’”
14 Hivyo, Daudi aliivuta mioyo ya watu wote wa Yuda kama mtu mmoja. Hivyo, wakampelekea ujumbe kusema “Rudi nyumbani, wewe na watumishi wako wote.”
15 Basi, mfalme akaja mto Yordani na watu wote wa Yuda wakaja mpaka Gilgali kumlaki mfalme na kumvusha mtoni Yordani.
16 Shimei mwana wa Gera, Mbenyamini, kutoka Bahurimu, alifanya haraka kwenda pamoja na watu wengine ili kumlaki mfalme Daudi.
17 Shimei alikwenda pamoja na Wabenyamini 1,000. Siba mtumishi wa jamaa ya Shauli, pamoja na watoto wake kumi na watumishi ishirini, walikwenda haraka mtoni Yordani kumtangulia mfalme Daudi.
18 Basi, wakavuka kwenye kivuko ili kuisindikiza jamaa ya mfalme na kumfanyia mfalme yote aliyoyapenda. Shimei mwana wa Gera akaja, akajitupa mbele ya mfalme, akasujudu, wakati mfalme alipokuwa karibu kuvuka mto Yordani.
19 Shimei akamwambia mfalme, “Nakuomba, bwana wangu mfalme, usinihesabu kuwa na hatia wala kukumbuka kosa nililofanya siku ile ulipokuwa ukiondoka mjini Yerusalemu. Nakuomba usiyaweke hayo maanani.
20 Maana, mimi mtumishi wako ninajua kwamba nilitenda dhambi. Hii ndiyo sababu nimekuja leo, nikiwa wa kwanza katika kabila la Yosefu, kuja kukulaki wewe bwana wangu, mfalme.”
21 Ndipo Abishai mwana wa Seruya akasema, “Je, si lazima Shimei auawe maana alimlaani mtu ambaye Mwenyezi-Mungu amemteua kwa kumpaka mafuta?”
22 Lakini Daudi akasema, “Wana wa Seruya, sina lolote nanyi; kwa nini mjifanye kama maadui zangu leo? Je, auawe mtu yeyote katika Israeli siku ya leo? Je, sijui kuwa mimi ni mfalme wa Israeli siku ya leo?”
23 Kisha, mfalme akamwambia Shimei, “Wewe hutauawa.” Mfalme akamwapia Shimei.
24 Mefiboshethi mjukuu wa Shauli, alikwenda pia kumlaki mfalme Daudi. Tangu siku ile mfalme alipoondoka Yerusalemu mpaka aliporudi salama, Mefiboshethi alikuwa hajapata kuosha miguu yake, kukata ndevu zake na hakujali kufua nguo zake.
25 Basi, ikawa alipofika Yerusalemu kumlaki mfalme, Daudi alimwuliza, “Je, Mefiboshethi, kwa nini hukuandamana pamoja nami?”
26 Mefiboshethi akasema, “Ee bwana wangu mfalme, mtumishi wangu alinidanganya. Maana, mimi mtumishi wako, nilimwambia, ‘Nitandikie punda nipate kumpanda kwenda pamoja na mfalme,’ maana mimi mtumishi wako ni kilema.
27 Sasa, amenisingizia kwako, ee bwana wangu mfalme. Lakini wewe, bwana wangu mfalme, uko kama malaika wa Mungu. Fanya lolote unaloona ni jema kwako.
28 Maana, jamaa yote ya babu yangu walikuwa watu ambao wamestahili kuuawa mbele yako, bwana wangu mfalme. Lakini uliniweka mimi mtumishi wako miongoni mwa wale wanaokula mezani pako. Je, nina haki yoyote zaidi hata nikulilie mfalme?”
29 Mfalme akamwambia, “Usiniambie zaidi juu ya mambo yako ya binafsi. Mimi nimekwisha amua kuwa wewe pamoja na Siba mtagawana nchi ya Shauli.”
30 Lakini Mefiboshethi akamwambia mfalme, “Mruhusu Siba aichukue nchi yote peke yake. Mimi nimetosheka kwamba wewe bwana wangu mfalme umerudi nyumbani salama.”
31 Barzilai Mgileadi alikuwa amefika kutoka Rogelimu. Alikuwa amekwenda pamoja na mfalme kwenye mto Yordani ili kumsindikiza hadi ngambo ya mto.
32 Barzilai alikuwa mzee sana, mwenye umri wa miaka themanini. Naye Barzilai alikuwa amemtunza mfalme alipokaa huko Mahanaimu, kwa kuwa alikuwa tajiri sana.
33 Basi, mfalme Daudi akamwambia Barzilai, “Twende wote huko Yerusalemu nami nitakutunza.”
34 Lakini Barzilai akamwambia mfalme, “Je, nina miaka mingi ya kuishi ndipo niende nawe mfalme mpaka Yerusalemu?
35 Mimi leo nina umri wa miaka themanini. Je, nina uwezo wa kubainisha yaliyo mazuri na yale yasiyo mazuri? Je, mimi mtumishi wako, naweza kutambua ladha ya kile ninachokula au kunywa? Je, nitaweza kutambua uzuri wa sauti za waimbaji wanaume au wanawake? Kwa nini mimi mtumishi wako niwe mzigo wa ziada kwako, bwana wangu mfalme?
36 Mimi mtumishi wako nitakwenda nawe mwendo mfupi ngambo ya Yordani. Kwa nini, mfalme anilipe zawadi kubwa hivyo?
37 Nakuomba, uniruhusu mimi mtumishi wako, nifie katika mji wangu, karibu na kaburi la baba yangu na mama yangu. Lakini huyu mtumishi wako Kimhamu, mruhusu aende pamoja nawe bwana wangu mfalme, na mtendee yeye lolote unaloona ni jema.”
38 Mfalme akamwambia, “Kimhamu atakwenda nami, na nitamtendea lolote lililo jema kwako. Na lolote utakalotaka nikutendee, nitakutendea.”
39 Ndipo watu wote wakavuka mtoni Yordani na mfalme naye akavuka. Mfalme akambusu na kumbariki Barzilai, na Barzilai akarudi nyumbani kwake.
40 Mfalme aliendelea mpaka Gileadi, Kimhamu akawa anafuatana naye. Watu wote wa Yuda na nusu ya watu wa Israeli walikuwa wakimsindikiza mfalme.
41 Kisha, watu wote wa Israeli wakaja kwa mfalme na kumwambia, “Kwa nini ndugu zetu watu wa Yuda walikuwa wamekuiba ukiwa njiani, wakakuvusha mto Yordani, wewe na jamaa yako, pamoja na watu wako?”
42 Watu wa Yuda wakawaambia watu wa Israeli, “Kwa sababu mfalme ni ndugu yetu wa karibu. Kwa nini mnakasirika kuhusu jambo hili? Je, tumekula chochote wakati wowote kwa gharama ya mfalme? Au je, yeye ametupa zawadi yoyote?”
43 Watu wa Israeli wakawajibu watu wa Yuda, “Tuna haki mara kumi juu ya mfalme, kuliko mlizo nazo nyinyi, na hata juu ya Daudi mwenyewe. Kwa nini, basi, mlitudharau? Je, sisi hatukuwa wa kwanza kusema kuwa mfalme wetu arudishwe?” Maneno ya watu wa Yuda yalikuwa makali kuliko maneno ya watu wa Israeli.
1 Sasa ikawa kwamba huko Gilgali kulikuwa na mtu mmoja mlaghai aitwaye Sheba mwana wa Bikri, Mbenyamini. Basi Sheba alipiga tarumbeta, na kusema, “Hatuna fungu lolote kwa Daudi, hatuna sehemu yetu katika huyo mwana wa Yese. Enyi watu wa Israeli, kila mmoja na ajiendee hemani kwake!”
2 Hivyo, watu wote wa Israeli wakamwacha Daudi, wakamfuata Sheba mwana wa Bikri. Lakini watu wa Yuda walimfuata mfalme Daudi kwa uaminifu toka mto Yordani mpaka mjini Yerusalemu.
3 Hatimaye, Daudi aliwasili nyumbani kwake mjini Yerusalemu. Mfalme aliwachukua masuria wake kumi ambao alikuwa amewaacha kuangalia nyumba yake, akawaweka kwenye nyumba moja chini ya ulinzi, akawatunza vizuri, lakini hakulala nao. Hivyo, masuria hao wakawa wametiwa ndani hadi siku za kufa kwao, wakaishi kana kwamba, walikuwa wajane.
4 Kisha, mfalme akamwambia Amasa, “Nikusanyie watu wote wa Yuda katika siku tatu, na wewe mwenyewe uwepo.”
5 Basi, Amasa akaenda kuwaita watu wa Yuda. Lakini akachelewa kurudi katika wakati ule aliopangiwa na mfalme.
6 Daudi akamwambia Abishai, “Sasa, Sheba mwana wa Bikri, atatuletea madhara kuliko Absalomu. Chukua watumishi wangu, umfuatie Sheba asije akaingia kwenye miji yenye ngome akaponyoka, tusimwone tena.”
7 Abishai akatoka akiwa pamoja na Yoabu, Wakerethi na Wapelethi pamoja na mashujaa wote. Hao wote waliondoka Yerusalemu kwenda kumfuatia Sheba mwana wa Bikri.
8 Walipofika kwenye jiwe kubwa lililoko huko Gibeoni, Amasa akatoka kuwalaki. Yoabu alikuwa amevaa vazi la kijeshi, na ndani ya vazi hilo kulikuwa na mkanda ulioshikilia upanga kiunoni mwake ukiwa kwenye ala yake. Yoabu alipokuwa anakaribia, upanga wake ulichomoka alani ukaanguka chini.
9 Yoabu akamwambia Amasa, “Je, hujambo ndugu yangu?” Yoabu akamshika Amasa kidevuni kwa mkono wa kulia kana kwamba anataka kumbusu.
10 Lakini Amasa hakuona upanga uliokuwa mkononi mwa Yoabu. Basi, Yoabu akamchoma Amasa upanga tumboni, matumbo yake yakatoka nje, akafa. Yoabu hakumchoma upanga mara mbili. Kisha, Yoabu na nduguye Abishai wakaendelea kumfuatilia Sheba mwana wa Bikri.
11 Mtu mmoja wa Yoabu akaja akasimama karibu na mwili wa Amasa, akasema, “Yeyote anayempenda Yoabu na yeyote anayempenda Daudi, na amfuate Yoabu!”
12 Amasa alikuwa bado anagagaa kwenye damu yake katikati ya barabara kuu. Kwa hiyo, kila mtu aliyepita hapo, alipomwona, alisimama. Lakini yule mtu alipoona kwamba watu wote walikuja na kusimama hapo, aliuondoa mwili wa Amasa barabarani, akaupeleka shambani na kuufunika kwa nguo.
13 Amasa alipoondolewa kwenye barabara kuu, watu wote sasa waliendelea kumfuata Yoabu kumfuatia Sheba mwana wa Bikri.
14 Sheba alipitia katika makabila yote ya Israeli mpaka mji wa Abeli wa Beth-maaka. Watu wote wa ukoo wa Bikri wakakusanyika na kumfuata.
15 Watu wote waliokuwa pamoja na Yoabu wakaenda kumzingira Sheba akiwa katika mji huo wa Abeli wa Beth-maaka. Walirundika kuuzingira mji, na ngome; halafu wakaanza kuubomoa ukuta ili kuuangusha chini.
16 Kisha, mwanamke fulani mwenye hekima alisikika kutoka mjini akisema, “Sikieni! Sikieni! Mwambieni Yoabu aje nizungumze naye.”
17 Yoabu akaenda karibu naye, huyo mwanamke akamwambia, “Je, wewe ni Yoabu?” Yoabu akasema, “Naam! Ni mimi.” Yule mwanamke akamwambia, “Nisikilize mimi mtumishi wako.” Yoabu akamwambia, “Nasikiliza.”
18 Huyo mwanamke akamwambia, “Hapo kale watu walikuwa wakisema, ‘Waacheni watake shauri kutoka mji wa Abeli’. Ndivyo watu walivyoweza kutatua matatizo.
19 Mimi ni mmojawapo wa wale wanaopenda amani na uaminifu katika Israeli. Sasa wewe unakusudia kuuharibu mji ambao ni kama mama katika Israeli. Kwa nini sasa unataka kuuangamiza mji ulio mali yake Mwenyezi-Mungu?”
20 Yoabu akamjibu, “Kamwe maishani mwangu! Sina nia kuangamiza wala kuharibu.
21 Ulivyosema si kweli! Lakini mtu mmoja kutoka sehemu ya milima ya Efraimu aitwaye Sheba mwana wa Bikri anataka kumwasi mfalme Daudi. Mtoeni huyo kwangu nami nitaondoka mjini kwenu.” Yule mwanamke akamwambia Yoabu, “Kichwa chake kitarushwa kwako kupitia ukutani.”
22 Kisha, huyo mwanamke akaenda kwa watu wote mjini kwa busara yake. Wakamkata kichwa Sheba mwana wa Bikri, wakakitupa nje kwa Yoabu. Kwa hiyo, Yoabu akapiga tarumbeta, na kuwatawanya watu wake kutoka mji huo wa Abeli; kila mtu akaenda nyumbani kwake. Kisha Yoabu akarudi kwa mfalme Daudi, mjini Yerusalemu.
23 Sasa Yoabu alikuwa mkuu wa jeshi lote la Israeli. Benaya, mwana wa Yehoyada, alikuwa mkuu wa Wakerethi na Wapelethi.
24 Adoramu alikuwa msimamizi wa kazi za kulazimishwa; Yehoshafati alikuwa mwandishi wa kumbukumbu.
25 Shausha alikuwa katibu; Sadoki na Abiathari walikuwa makuhani.
26 Ira, Myairi alikuwa pia kuhani wa Daudi.
1 Wakati mmoja kulitokea njaa kali nchini Daudi akiwa mfalme. Njaa hiyo ilidumu miaka mitatu mfululizo. Daudi alimwomba Mwenyezi-Mungu shauri. Mwenyezi-Mungu akamwambia, “Shauli na jamaa yake wana hatia ya kumwaga damu kwa sababu aliwaua Wagibeoni.”
2 Hivyo, mfalme Daudi akawaita Wagibeoni (Wagibeoni hawakuwa Waisraeli ila walikuwa mabaki ya Waamori. Ingawa watu wa Israeli walikuwa wameapa kuwaacha hai, lakini Shauli alijaribu kuwaua wote kwani alikuwa na bidii ya upendeleo kwa watu wa Israeli na wa Yuda).
3 Daudi akawauliza Wagibeoni, “Niwatendee nini? Nitalipaje kwa maovu mliyotendewa ili mpate kuibariki nchi hii na watu wake Mwenyezi-Mungu?”
4 Wagibeoni wakamwambia, “Kisa chetu na Shauli pamoja na jamaa yake si jambo la fedha au dhahabu. Wala si juu yetu kumwua yeyote katika nchi ya Israeli.” Mfalme akawauliza tena, “Sasa mnasema niwatendee nini?”
5 Wao wakamwambia mfalme, “Shauli alikusudia kutuua sisi na kutuangamiza, asiache mtu wetu yeyote katika eneo lote la Israeli.
6 Basi, tukabidhi watu saba kati ya wanawe wa kiume, nasi tuwanyonge mbele ya Mwenyezi-Mungu mlimani Gibea, kwa Shauli aliyeteuliwa na Mwenyezi-Mungu.” Mfalme akasema, “Nitawakabidhi kwenu.”
7 Lakini mfalme alimnusuru Mefiboshethi mwana wa Yonathani kwa sababu ya kiapo ambacho Daudi na Yonathani mwana wa Shauli walikuwa wamekula kati yao kwa jina la Mwenyezi-Mungu.
8 Lakini mfalme aliwachukua wana wawili ambao Rispa binti Ahiya alimzalia Shauli, Armoni na Mefiboshethi, pamoja na watoto wote watano wa kiume wa Mikali, binti Shauli ambao alimzalia Adrieli mwana wa Barzilai Mmeholathi.
9 Watoto hao saba wa kiume Daudi aliwakabidhi kwa Wagibeoni, nao wakawatundika mlimani mbele ya Mwenyezi-Mungu, wote saba wakafa pamoja. Watoto hao waliuawa mwanzoni mwa mavuno ya shayiri.
10 Kisha, Rispa binti Aya alichukua nguo ya gunia, akajitandikia mwambani. Alikaa hapo tangu mwanzo wa mavuno mpaka wakati wa mvua ulipowadia na kuinyeshea maiti. Wakati huo wote, aliwafukuza ndege wa angani na wanyama wa porini, usiku na mchana, ili wasifikie maiti hizo.
11 Daudi aliposikia yale aliyofanya Rispa binti Aya, suria wa Shauli,
12 alikwenda na kuichukua mifupa ya Shauli na Yonathani mwanawe kutoka wakazi wa Yabesh-gileadi, waliokuwa wameiiba kutoka mtaani huko Beth-sheani, ambako Wafilisti walikuwa wamemtundika Shauli na Yonathani siku ile Wafilisti walipomuua Shauli mlimani Gilboa.
13 Basi, Daudi akairudisha mifupa ya Shauli na Yonathani mwanawe kutoka huko; halafu wakakusanya mifupa ya vijana saba waliotundikwa.
14 Basi, watu wa Daudi wakaizika mifupa ya Shauli na Yonathani mwanawe katika nchi ya Benyamini, huko Sela katika kaburi la Kishi baba yake Shauli. Walifanya kila kitu ambacho mfalme aliamuru. Baada ya hayo, Mungu akayasikiliza maombi kuhusu nchi yao.
15 Kisha Wafilisti walifanya vita tena na Waisraeli. Naye Daudi na watu wake wakaenda kupigana na Wafilisti. Daudi alichoka sana siku hiyo.
16 Ishbi-benobu, mmojawapo wa wazawa wa majitu ambaye mkuki wake wa shaba ulikuwa na uzito wa karibu kilo tatu na nusu na aliyekuwa amejifunga upanga mpya alisema atamuua Daudi.
17 Lakini Abishai mwana wa Seruya, alikwenda kumsaidia Daudi. Abishai alimshambulia yule Mfilisti na kumwua. Hivyo, watu wakamwapia Daudi wakisema, “Hutakwenda tena nasi vitani, la sivyo utaizima taa ya ufalme katika Israeli.”
18 Baada ya hayo, kulitokea tena mapigano na Wafilisti huko Gobu. Huko Sibekai, Mhushathi, alimuua Safu aliyekuwa mmojawapo wa wazawa wa Warefai.
19 Kulitokea tena mapigano na Wafilisti huko Gobu. Naye Elhanani mwana wa Yaareo-regimu, Mbethlehemu, alimuua Goliathi Mgiti, ambaye mpini wa mkuki wake ulikuwa kama mti wa mfumanguo.
20 Baadaye kulitokea tena vita huko Gathi ambako kulikuwa na mtu mmoja alikuwa mkubwa kwa kimo, na mwenye vidole sita katika kila mkono, na vidole sita katika kila mguu, jumla yake vidole ishirini na vinne. Yeye pia alikuwa mzawa wa majitu.
21 Alipowadhihaki Waisraeli, Yonathani mwana wa Shimei, nduguye Daudi, alimuua.
22 Hao wanne walikuwa wazawa wa majitu huko Gathi, nao waliuawa na Daudi pamoja na watumishi wake.
1 Daudi alimwimbia Mwenyezi-Mungu maneno ya wimbo ufuatao siku ile Mwenyezi-Mungu alipomkomboa mikononi mwa adui zake, na mkononi mwa Shauli.
2 Alisema, “Mwenyezi-Mungu ni mwamba wangu, ngome yangu, na mkombozi wangu.
3 Mungu wangu, mwamba wangu, ninayemkimbilia usalama; ngao yangu, nguvu ya wokovu wangu, ngome yangu na kimbilio langu. Mwokozi wangu; unaniokoa kutoka kwa watu wakatili.
4 Namwita Mwenyezi-Mungu astahiliye sifa anisaidie, nami naokolewa kutoka kwa adui zangu.
5 “Maana mawimbi ya kifo yalinizingira, mafuriko ya maangamizi yalinivamia;
6 kamba za kuzimu zilinizinga, mitego ya kifo ilinikabili.
7 “Katika taabu yangu, nilimwita Mwenyezi-Mungu; nilimwita Mungu wangu. Toka hekaluni mwake aliisikia sauti yangu, kilio changu kilimfikia masikioni mwake.
8 “Hapo, dunia ikatetemeka na kutikisika, misingi ya mbinguni ikayumbayumba na kuruka, kwani Mungu alikuwa amekasirika.
9 Moshi ulifuka kutoka puani mwake, moto uunguzao ukatoka kinywani mwake, makaa ya moto yalilipuka kutoka kwake.
10 Aliinamisha anga, akashuka chini; na wingu jeusi chini ya miguu yake.
11 Alipanda kiumbe chenye mabawa na kuruka, alionekana juu ya mabawa ya upepo.
12 Alijizungushia giza pande zote, kifuniko chake kilikuwa mawingu mazito na mkusanyiko wa maji.
13 Umeme ulimulika mbele yake, kulilipuka makaa ya moto.
14 Mwenyezi-Mungu alinguruma kutoka mbinguni, Mungu Mkuu akatoa sauti yake.
15 Aliwalenga adui mishale, akawatawanya, alirusha umeme, akawatimua.
16 Mwenyezi-Mungu alipowakemea, kutokana na pumzi ya puani mwake, vilindi vya bahari vilifunuliwa, misingi ya dunia ikaonekana.
17 “Mungu alinyosha mkono wake toka juu, akanichukua, kutoka kwenye maji mengi alininyanyua.
18 Aliniokoa kutoka kwa adui yangu mwenye nguvu, aliniokoa kutoka kwa hao walionichukia maana walikuwa na nguvu nyingi kunishinda.
19 Walinivamia nilipokuwa taabuni, lakini Mwenyezi-Mungu alikuwa kinga yangu.
20 Alinileta, akaniweka mahali pa usalama, alinisalimisha, kwani alipendezwa nami.
21 “Mwenyezi-Mungu alinipa tuzo kadiri ya uadilifu wangu; alinituza kwa vile mikono yangu haina hatia.
22 Maana, nimefuata njia za Mwenyezi-Mungu, wala sikujitenga na Mungu wangu kwa uovu.
23 Nimeshika maagizo yake yote, sikuacha kufuata masharti yake.
24 Mbele yake sikuwa na hatia, nimejikinga nisiwe na hatia.
25 Mwenyezi-Mungu amenituza kadiri ya uadilifu wangu, yeye anajua usafi wangu.
26 “Wewe ni mwaminifu kwa walio waaminifu, mwema kwa wale walio wema.
27 Wewe ni mkamilifu kwa walio wakamilifu, lakini mkatili kwa watu walio waovu.
28 Wewe wawaokoa walio wanyenyekevu, lakini wawaangalia wenye majivuno kuwaporomosha.
29 Ee Mwenyezi-Mungu, wewe u taa yangu, Mungu wangu, unayefukuza giza langu.
30 Kwa msaada wako, wakishambulia kikosi; wewe wanipa nguvu ya kuruka kuta zake.
31 Anachofanya Mungu hakina dosari! Ahadi ya Mwenyezi-Mungu ni ya kuaminika; yeye ni ngao kwa wote wanaomkimbilia.
32 “Nani aliye Mungu isipokuwa Mwenyezi-Mungu? Nani aliye mwamba wa usalama ila Mungu wetu?
33 Mungu huyu ndiye kimbilio langu imara, na ameifanya njia yangu iwe salama.
34 Ameiimarisha miguu yangu kama ya paa, na kuniweka salama juu ya vilele.
35 Hunifunza kupigana vita, mikono yangu iweze kuvuta upinde wa shaba.
36 Umenipa ngao yako ya kuniokoa; msaada wako umenifanya mkuu.
37 Umenirahisishia njia yangu; wala miguu yangu haikuteleza.
38 Niliwafuatia adui zangu na kuwaangamiza, sikurudi nyuma mpaka wameangamizwa.
39 Niliwaangamiza, nikawaangusha chini wasiweze kuinuka tena; walianguka chini ya miguu yangu.
40 Wewe ulinijalia nguvu ya kupigana vita; uliwaporomosha adui chini yangu.
41 Uliwafanya adui zangu wakimbie, na wale walionichukia niliwaangamiza.
42 Walitafuta msaada, lakini hapakuwa na wa kuwaokoa, walimlilia Mwenyezi-Mungu, lakini hakuwajibu.
43 Niliwatwanga na kuwaponda kama mavumbi ya nchi, nikawaponda na kuwakanyaga kama matope barabarani.
44 “Wewe uliniokoa na mashambulizi ya watu wangu, umenifanya mtawala wa mataifa. Watu nisiowajua walinitumikia.
45 Wageni walinijia wakinyenyekea, mara waliposikia habari zangu walinitii.
46 Wageni walikufa moyo; wakaja kutoka ngome zao wakitetemeka.
47 “Mwenyezi-Mungu yu hai! Asifiwe mwamba wangu! Atukuzwe Mungu wangu, mwamba wa wokovu wangu.
48 Yeye ameniwezesha kulipiza kisasi na kuyatiisha mataifa chini yangu.
49 Ameniokoa kutoka adui zangu. Ee Mwenyezi-Mungu, ulinikuza juu ya wapinzani wangu na kunisalimisha mbali na watu wakatili.
50 “Kwa hiyo, nitakutukuza kati ya mataifa, ee Mwenyezi-Mungu, nitaliimbia sifa jina lako.
51 Mungu humjalia mfalme wake ushindi mkubwa; humwonesha fadhili zake huyo aliyemweka wakfu, naam, humfadhili Daudi na wazawa wake milele.”
1 Yafuatayo ni maneno ya mwisho ya Daudi. Ni ujumbe wa Daudi mwana wa Yese; ujumbe wa mtu ambaye Mungu alimfanya awe mkuu. Mungu wa Yakobo alimteua Daudi kuwa mfalme na maneno yake Waisraeli walifurahi kuyaimba.
2 “Roho ya Mwenyezi-Mungu imesema kwa njia yangu, aliyaweka maneno yake kinywani mwangu.
3 Mungu wa Israeli amesema, Mwamba wa Israeli ameniambia, ‘Mtu anapowatawala watu kwa haki, atawalaye kwa kumcha Mungu,
4 yeye ni kama mwanga wa asubuhi, jua linapochomoza asubuhi isiyo na mawingu; naam, kama mvua inayootesha majani ardhini’.
5 Hivyo ndivyo Mungu alivyoujalia ukoo wangu. Maana amefanya nami agano la kudumu milele; agano kamili na thabiti. Naye atanifanikisha katika matakwa yangu yote.
6 Lakini wasiomcha Mungu wote ni kama miiba inayotupwa tu, maana haiwezi kuchukuliwa kwa mkono;
7 kuishika, lazima kutumia chuma au mpini wa mkuki. Watu hao wataangamizwa kabisa kwa moto.”
8 Yafuatayo ni majina ya mashujaa aliokuwa nao Daudi: Yosheb-bashebethi, Mtakmoni, aliyekuwa kiongozi wa wale watatu, yeye alipigana kwa mkuki wake, akaua watu 800 wakati mmoja.
9 Halafu aliyefuata miongoni mwa wale mashujaa watatu alikuwa Eleazari mwana wa Dodo, wa ukoo wa Mwahohi. Siku moja, Eleazari alikuwa pamoja na Daudi walipowatukana Wafilisti waliokuwa wamekusanyika kupigana vita. Waisraeli waliwakimbia Wafilisti.
10 Lakini Eleazari alisimama imara na kupigana na Wafilisti mpaka mkono wake uliposhindwa kupinda, ukabaki umeshikilia upanga wake. Siku hiyo, Mwenyezi-Mungu alijipatia ushindi mkubwa. Baada ya ushindi huo, Waisraeli walirudi mahali alipokuwa Eleazari na kujipatia nyara za bure kutoka kwa Wafilisti waliouawa.
11 Shujaa wa tatu alikuwa Shama mwana wa Agee, Mharari. Wafilisti walikusanyika huko Lehi, mahali palipokuwa na shamba la dengu nyingi, nao Waisraeli waliwakimbia Wafilisti.
12 Lakini alisimama imara katikati ya shamba hilo ili kulitetea, naye akawaua Wafilisti. Mwenyezi-Mungu alijipatia ushindi mkubwa.
13 Kisha, mashujaa watatu kati ya wakuu thelathini waliteremka wakati wa mavuno wakamfikia Daudi kwenye pango huko Adulamu. Wakati huo jeshi la Wafilisti lilikuwa limepiga kambi katika bonde la Refaimu.
14 Naye Daudi wakati huo alikuwa katika ngome, nalo jeshi la Wafilisti lilikuwa mjini Bethlehemu.
15 Daudi akasema kwa hamu kubwa, “Laiti mtu angeweza kunipa maji ya kunywa kutoka katika kisima cha Bethlehemu, kilicho karibu na lango la mji!”
16 Wale mashujaa wake watatu walitoka, wakapenya katikati ya kambi ya jeshi la Wafilisti, wakaenda na kuchota maji katika kisima cha Bethlehemu, karibu na lango la mji, wakamletea Daudi. Lakini Daudi alikataa kuyanywa, na badala yake, akayamwaga chini kama tambiko kwa Mwenyezi-Mungu,
17 akisema, “Kamwe, sina haki ya kunywa maji haya, ee Mwenyezi-Mungu; je, haya si kama damu ya wale walioyahatarisha maisha yao kuyaleta maji haya?” Kwa hiyo, Daudi hakuyanywa maji hayo. Hayo ndiyo mambo waliyotenda wale mashujaa watatu.
18 Abishai nduguye Yoabu, mwana wa Seruya, alikuwa mkuu wa mashujaa thelathini. Yeye alipigana kwa mkuki wake dhidi ya watu 300, akawaua, akajipatia jina miongoni mwa wale mashujaa watatu.
19 Je, huyo hakuwa mashuhuri zaidi miongoni mwa mashujaa watatu? Kwa hiyo akawa kamanda wao, lakini hakuwa shujaa kama wale mashujaa watatu.
20 Naye Benaya mwana wa Yehoyada, kutoka Kabzeeli, alikuwa askari shujaa ambaye alifanya mambo mengi ya ajabu. Aliwaua mashujaa wawili kutoka Moabu, na siku moja wakati wa theluji, alishuka shimoni na kuua simba.
21 Vilevile, aliliua jitu la Misri. Mmisri huyo alikuwa na mkuki, lakini Benaya alimwendea akiwa na fimbo tu, akamnyanganya mkuki huo, na kumwua Mmisri huyo kwa mkuki wake mwenyewe.
22 Benaya, mwana wa Yehoyada alifanya mambo haya, akajipatia jina miongoni mwa wale mashujaa watatu.
23 Basi, akawa mashuhuri kati ya wale mashujaa thelathini, ingawa hakuwa kama wale mashujaa watatu. Na Daudi akampa cheo cha mkuu wa walinzi wake binafsi.
24 Asaheli, nduguye Yoabu, alikuwa mmoja wa mashujaa thelathini. Mashujaa wengine wa Daudi walikuwa: Elhanani, mwana wa Dodo wa Bethlehemu;
25 Shama, Mharodi; Elika, Mharodi;
26 Helesi, Mpalti; Ira, mwana wa Ikeshi, Mtekoa;
27 Abiezeri, Mwanathothi; Mebunai, Mhushathi;
28 Salmoni, Mwahohi; Maharai, Mnetofathi;
29 Helebu mwana wa Baana, Mnetofathi; Itai mwana wa Ribai, toka Gibea katika Benyamini;
30 Benaya, Mpirathoni; Hidai, wa vijito vya Gaashi;
31 Abialboni, Mwarbathi; Azmawethi, Mbahurimu;
32 Eliaba, Mshaalboni; wana wa Yasheni; Yonathani;
33 Shama, Mharari; Ahimu mwana wa Sharari, Mharari;
34 Elifeleti mwana wa Ahasbai, Mmaaka; Eliamu mwana wa Ahithofeli, Mgiloni;
35 Hesrawi, Mkarmeli; Paarai, Mwarbi;
36 Igali mwana wa Nathani, Msoba; Bani, Mgadi;
37 Seleki, Mwamoni; Naharai, Mbeerothi aliyekuwa mbeba silaha wa Yoabu mwana wa Seruya;
38 Ira na Garebu, Waithri;
39 na Uria, Mhiti. Wote pamoja walikuwa mashujaa thelathini na saba.
1 Kwa mara nyingine, Mwenyezi-Mungu aliwakasirikia Waisraeli, akamchochea Daudi dhidi yao, akamwambia awahesabu watu wa Israeli na watu wa Yuda.
2 Hivyo, mfalme akamwambia Yoabu, na makamanda wa jeshi waliokuwa pamoja naye, “Nendeni katika makabila yote ya Israeli kutoka Dani mpaka Beer-sheba, mkawahesabu watu ili nipate kujua idadi yao.”
3 Lakini Yoabu akamwambia mfalme, “Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, na awaongeze Waisraeli mara mia kuliko walivyo sasa, nawe bwana wangu mfalme upate kuona ongezeko hilo kwa macho yako mwenyewe. Lakini, kwa nini wewe bwana wangu mfalme unapendezwa na jambo hili?”
4 Lakini tamko la mfalme lilikuwa na nguvu zaidi dhidi ya Yoabu na makamanda wa jeshi! Basi, Yoabu na makamanda wa jeshi wakaondoka mbele ya mfalme, wakaenda kuwahesabu Waisraeli.
5 Walivuka mto Yordani wakianzia kuhesabu watu tangu Aroeri na mto ulioko bondeni kuelekea Gadi hadi Yazeri.
6 Kisha, wakaenda Gileadi halafu Kadeshi katika nchi ya Wahiti, halafu wakawasili Dani na kutoka Dani wakazunguka kwenda Sidoni,
7 na kufika kwenye ngome ya mji wa Tiro, wakaingia kwenye miji yote ya Wahivi na Wakanaani. Kisha, walitoka wakaenda Negebu ya Yuda huko Beer-sheba.
8 Walipokwisha pitia katika nchi yote, walirejea Yerusalemu baada ya miezi tisa na siku ishirini.
9 Halafu Yoabu alimpelekea mfalme idadi ya watu. Katika Israeli kulikuwamo wanaume mashujaa 800,000 wenye ujuzi wa kutumia mapanga; na katika Yuda, kulikuwa na wanaume 500,000.
10 Lakini Daudi alisumbuliwa sana rohoni mwake baada ya kuwahesabu watu. Kwa hiyo, Daudi akamwambia Mwenyezi-Mungu, “Nimetenda dhambi kubwa kwa tendo nililolifanya. Lakini sasa, ee Mwenyezi-Mungu, nakusihi unisamehe mimi mtumishi wako, kwani nimefanya jambo la kipumbavu kabisa.”
11 Daudi alipoamka kesho yake asubuhi, wakati huo Mwenyezi-Mungu alimpa ujumbe nabii Gadi mwonaji wa mfalme Daudi, akisema,
12 “Nenda ukamwambie hivi Daudi: ‘Mwenyezi-Mungu asema hivi: Ninakupa mambo matatu, nawe ujichagulie mojawapo, nami nitakutendea.’”
13 Hivyo, Gadi akamwendea Daudi na kumweleza, akisema, “Je, wapendelea njaa ya miaka saba iijie nchi yako? Au je, wewe uwakimbie adui zako kwa miezi mitatu wanapokufuatia? Au kuwe na siku tatu ambapo nchi yako itakuwa na maradhi mabaya? Fikiri unipe jibu nitakalompa yeye aliyenituma.”
14 Daudi akamjibu Gadi, “Nina mashaka makubwa! Lakini afadhali niadhibiwe na Mwenyezi-Mungu, kuliko kutiwa mikononi mwa watu, maana yeye ana huruma sana.”
15 Basi, Mwenyezi-Mungu akawaletea Waisraeli maradhi, tangu asubuhi hadi wakati uliopangwa. Watu 70,000 walikufa nchini kote kutoka Dani mpaka Beer-sheba.
16 Lakini wakati malaika aliponyosha mkono wake kuelekea mji wa Yerusalemu ili kuuangamiza, Mwenyezi-Mungu alibadilisha nia yake. Mwenyezi-Mungu akamwambia huyo malaika aliyetekeleza maangamizi kwa watu, “Basi! Yatosha; rudisha mkono wako.” Malaika wa Mwenyezi-Mungu alikuwa amesimama karibu na uwanja wa kupuria nafaka wa Arauna, Myebusi.
17 Daudi alipomwona huyo malaika aliyekuwa anawaua watu, alimwambia Mwenyezi-Mungu, “Tazama, Mimi ndiye niliye na hatia! Mimi mwenyewe nimekosa! Hawa watu wapole hawakufanya uovu. Nakusihi sana uniadhibu mimi na jamaa ya baba yangu.”
18 Siku hiyohiyo Gadi akamwendea Daudi, akamwambia, “Panda juu, ukamjengee Mwenyezi-Mungu madhabahu, katika kiwanja cha kupuria nafaka cha Arauna, Myebusi.”
19 Basi, Daudi akapanda juu kufuatana na neno la Gadi kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru.
20 Arauna alipoangalia upande wa chini alimwona mfalme akimkaribia pamoja na watumishi wake, naye akatoka, akaenda na kumsujudia mfalme, akainama mpaka chini ardhini.
21 Kisha Arauna akamwuliza mfalme, “Kwa nini bwana wangu mfalme amenijia mimi mtumishi wake?” Daudi akamjibu, “Nimekuja kununua uwanja wako wa kupuria nafaka ili nimjengee Mwenyezi-Mungu madhabahu ili tauni iliyowakumba watu ikome.”
22 Naye Arauna akamwambia Daudi, “Bwana wangu mfalme, chukua chochote unachoona kinafaa na utolee sadaka. Mimi nawatoa fahali hawa kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa na vifaa hivi vya kupuria na nira za ng'ombe kuwa kuni.
23 Hivi vyote, ee mfalme, nakupa. Natumaini Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, atapokea sadaka yako kwa wema.”
24 Lakini mfalme akamwambia Arauna, “La! Wewe hutanipa chochote. Mimi nitavinunua kwako kwa thamani yake. Sitamtolea Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu, sadaka za kuteketezwa ambazo hazijanigharimu kitu.” Hivyo, mfalme Daudi alinunua uwanja wa kupuria na fahali kwa fedha shekeli hamsini.
25 Kisha Daudi akamjengea Mwenyezi-Mungu madhabahu mahali hapo na kumtolea sadaka za kuteketezwa na za amani. Basi, Mwenyezi-Mungu akayakubali maombi kwa ajili ya nchi, na ile tauni iliyowakumba Waisraeli ikakoma.