1 Ajabu mji uliokuwa umejaa watu, sasa wenyewe umebaki tupu! Ulikuwa maarufu kati ya mataifa; sasa umekuwa kama mama mjane. Miongoni mwa miji ulikuwa kama binti mfalme; sasa umekuwa mtumwa wa wengine.
2 Walia usiku kucha; machozi yautiririka. Hakuna hata mmoja wa wapenzi wake wa kuufariji. Rafiki zake wote wameuhadaa; wote wamekuwa adui zake.
3 Watu wa Yuda wamekwenda uhamishoni pamoja na mateso na utumwa mkali. Sasa wanakaa miongoni mwa watu wa mataifa, wala hawapati mahali pa kupumzika. Waliowafuatia wamewakamata wakiwa taabuni.
4 Barabara za kwenda Siyoni zinasikitisha; hakuna wapitao kwenda kwenye sikukuu. Malango ya mji wa Siyoni ni tupu; makuhani wake wanapiga kite, wasichana wake wana huzuni, na mji wenyewe uko taabuni.
5 Adui zake ndio wanaoutawala na wanafanikiwa, kwani Mwenyezi-Mungu ameutesa kwa sababu ya makosa mengi. Watoto wake wametekwa na kupelekwa mbali.
6 Fahari yote ya watu wa Siyoni imewatoweka; wakuu wake wamekuwa kama kulungu wasio na malisho. Bila nguvu waliwakimbia watesi wao.
7 Ukiwa sasa magofu matupu, Yerusalemu wakumbuka fahari yake. Ulipoangukia mikononi mwa maadui zake, hakuna aliyekuwako kuusaidia. Washindi wake walichekelea kuanguka kwake.
8 Yerusalemu ulitenda dhambi mbaya, ukawa mchafu kwa dhambi zake. Wote waliousifia wanaudharau, maana wameuona uchi wake. Wenyewe wapiga kite na kujificha kwa aibu.
9 Uchafu wake ulionekana waziwazi, lakini wenyewe haukujali mwisho wake. Anguko lake lilikuwa kubwa mno; hakuna awezaye kuufariji. Wasema: “Tazama ee Mwenyezi-Mungu mateso yangu, maana adui yangu ameshinda.”
10 Maadui wamenyosha mikono yao, wanyakue vitu vyake vyote vya thamani. Naam umeona watu wa mataifa wakiingia hekaluni, watu ambao Mwenyezi-Mungu aliwakataza kujumuika na jumuiya ya watu wake.
11 Watu wa Yerusalemu wote wanahangaika kutafuta chakula; hazina zao wanazitoa kupata chakula, wajirudishie nguvu zao. Nao mji unalia, “Hebu niangalie, ee Mwenyezi-Mungu, ona jinsi nilivyogeuka kuwa duni.
12 “Enyi wapita njia, hivi hamjali kitu? Tazameni! Hakuna aliyepatwa na uchungu kama mimi, uchungu alioniletea Mwenyezi-Mungu, siku ya hasira yake kali.
13 “Aliteremsha moto kutoka juu, ukanichoma hata mifupani mwangu. Alinitegea wavu akaninasa, kisha akanirudisha nyuma, akaniacha nimeduwaa na kuzirai mchana kutwa.
14 “Aliyahesabu makosa yangu yote akayakusanya mahali pamoja; aliyafunga shingoni mwangu kama nira, nikafyonzwa nguvu zangu kwa uzito wake. Mwenyezi-Mungu aliniweka mikononi mwao watu ambao siwezi kuwapinga.
15 “Mwenyezi-Mungu aliwakataa askari walionilinda, alitangaza wakati maalumu wa kuniadhibu kuwaponda vijana wangu wa kiume. Aliwaponda kama katika shinikizo watu wangu wa Yuda.
16 “Kwa sababu ya hayo ninalia, machozi yanitiririka, sina mtu yeyote wa kunifariji; hakuna yeyote wa kunitia moyo. Watoto wangu wameachwa wakiwa, maana adui yangu amenishinda.
17 “Nainyosha mikono yangu lakini hakuna wa kunifariji. Mwenyezi-Mungu ametoa amri dhidi yangu mimi Yakobo, jirani zangu wawe maadui zangu. Naam, mimi Yerusalemu nimekuwa kinyaa kwao.
18 “Lakini Mwenyezi-Mungu amefanya sawa kwa maana nimeliasi neno lake. Nisikilizeni enyi watu wote, yatazameni mateso yangu. Wasichana wangu na wavulana wangu, wamechukuliwa mateka.
19 “Niliwaita wapenzi wangu, lakini wao wakanihadaa. Makuhani na wazee wangu wamefia mjini wakijitafutia chakula, ili wajirudishie nguvu zao.
20 “Ona, ee Mwenyezi-Mungu nilivyo taabuni. Roho yangu imechafuka, moyo wangu unasononeka kwani nimekuasi vibaya. Huko nje kumejaa mauaji, ndani nako ni kama kifo tu.
21 “Sikiliza ninavyopiga kite; hakuna wa kunifariji. Maadui zangu wote wamesikia juu ya taabu yangu: Wanafurahi kwamba umeniletea maafa. Uifanye ile siku uliyoahidi ifike, uwafanye nao wateseke kama mimi.
22 “Uwapatilize kwa ajili ya uovu wao wote. Uwatende kama ulivyonitenda mimi kwa sababu ya makosa yangu yote. Nasononeka sana kwa maumivu na moyo wangu unazimia.”
1 Mwenyezi-Mungu, kwa hasira yake, amewaweka watu wa Siyoni gizani. Fahari ya Israeli ameibwaga chini. Siku ya hasira yake alilitupilia mbali hata hekalu lake.
2 Mwenyezi-Mungu ameharibu bila huruma makazi yote ya wazawa wa Yakobo. Kwa ghadhabu yake amezibomoa ngome za watu wa Yuda. Ufalme wao na watawala wake ameuporomosha chini kwa aibu.
3 Nguvu yote ya Israeli ameivunja kwa hasira. Hakunyosha mkono kuwasaidia walipokutana na adui; amewawakia watu wa Yakobo kama moto, akateketeza kila kitu.
4 Amevuta upinde wake kama adui, na kuuweka mkono wake wa kulia tayari, amewaua wote tuliowaonea fahari katika maskani yetu watu wa Siyoni. Ametumiminia hasira yake kama moto.
5 Mwenyezi-Mungu amekuwa kama adui, ameangamiza watu wa Israeli; majumba yake yote ameyaharibu, ngome zake amezibomoa. Amewazidishia watu wa Yuda matanga na maombolezo.
6 Hekalu lake amelibomoa kama kitalu bustanini, maskani yake ameiharibu. Amefutilia mbali sikukuu na Sabato huko Siyoni, kwa hasira yake kuu amewakataa mfalme na makuhani.
7 Mwenyezi-Mungu ameipuuza madhabahu yake na hekalu lake amelikataa. Kuta za majumba mjini amewaachia maadui wazibomoe, wakapiga kelele humo nyumbani kwa Mwenyezi-Mungu kama kelele za wakati wa sikukuu.
8 Mwenyezi-Mungu alipania kuubomoa ukuta wa mji wa Siyoni; aliupima na kuhakikisha kila kitu kimeharibiwa; minara na kuta za nje ya mji akazifanya ukiwa, zote kwa pamoja zikaangamia.
9 Malango yake yameanguka chini, makomeo yake ameyaharibu na kuyavunjavunja. Mfalme na wakuu wake wako uhamishoni kati ya mataifa. Mwongozo wa sheria umetoweka kabisa, manabii wake hawapati tena maono kutoka kwake Mwenyezi-Mungu.
10 Wazee wa Siyoni wameketi chini kimya, wamejitia mavumbi vichwani na kuvaa mavazi ya gunia. Wasichana wa Yerusalemu wameinamisha vichwa.
11 Macho yangu yamevimba kwa kulia, roho yangu imechafuka. Moyo wangu una huzuni nyingi kwa sababu ya kuangamizwa kwa watu wangu kwa sababu watoto wachanga wanazirai katika barabara za mji.
12 Wanawalilia mama zao: “Wapi chakula, wapi kinywaji?” Huku wanazirai kama majeruhi katika barabara za mjini, na kukata roho mikononi mwa mama zao.
13 Nikuambie nini ee Yerusalemu? Nikulinganishe na nini? Nikufananishe na kitu gani ili niweze kukufariji, ee Siyoni uliye mzuri? Maafa yako ni mengi kama bahari. Ni nani awezaye kukuponya?
14 Manabii wako wamekuonea maono madanganyifu, hawakufichua wazi uovu wako ili wapate kukurekebisha, bali walikuonea kauli ya uongo na ya kupotosha.
15 Wapita njia wote wanakudhihaki; wanakuzomea, ee Yerusalemu, wakitikisa vichwa vyao kwa dharau na kusema: “Je, huu ndio ule mji uliofikia upeo wa uzuri, mji uliokuwa furaha ya dunia nzima?”
16 Maadui zako wote wanakuzomea, wanakufyonya na kukusagia meno, huku wakisema, “Tumemwangamiza! Kweli, siku ile tuliyoingojea kwa hamu sasa imefika na tumeiona!”
17 Mwenyezi-Mungu amefanya yale aliyokusudia, ametekeleza yale aliyotishia; kama alivyopanga tangu kale ameangamiza bila huruma yoyote; amewafanya maadui wafurahie adhabu yako, amewakuza mashujaa wa maadui zako.
18 Kuta zako, ee mji wa Siyoni, zimlilie Mwenyezi-Mungu! Machozi na yatiririke kama mto mchana na usiku! Lia na kuomboleza bila kupumzika!
19 Usiku kucha uamkeamke ukalie. Mfungulie Mwenyezi-Mungu yaliyo moyoni mwako. Mwinulie mikono yako kuwaombea watoto wako, watoto wanaozirai kwa njaa popote barabarani.
20 Tazama ee Mwenyezi-Mungu uone! Je, kuna yeyote uliyemtendea ulivyotutendea sisi? Je, hata kina mama wawale watoto wao? Je, nao makuhani wauawe hekaluni mwako?
21 Maiti za vijana na wazee zimelala vumbini barabarani, wasichana na wavulana wangu wameuawa kwa upanga; umewaua bila huruma siku ya hasira yako.
22 Umewaalika kama kwenye sikukuu maadui zangu walionitisha kila upande. Katika siku ya hasira yako ee Mwenyezi-Mungu, hakuna aliyetoroka au kunusurika. Wale niliowazaa na kuwalea adui zangu wamewaangamiza.
1 Mimi ni mtu niliyepata mateso kwa fimbo ya ghadhabu yake Mungu.
2 Amenichukua akanipeleka mpaka gizani kusiko na mwanga.
3 Amenyosha mkono wake dhidi yangu mimi tu, akanichapa tena na tena mchana kutwa.
4 Amenichakaza ngozi na nyama, mifupa yangu ameivunja.
5 Amenizingira na kunizungushia uchungu na mateso.
6 Amenikalisha gizani kama watu waliokufa zamani.
7 Amenizungushia ukuta nisitoroke, amenifunga kwa minyororo mizito.
8 Ingawa naita na kulilia msaada anaizuia sala yangu isimfikie.
9 Njia zangu ameziziba kwa mawe makubwa amevipotosha vichochoro vyangu.
10 Yeye ni kama dubu anayenivizia; ni kama simba aliyejificha.
11 Alinifukuza njiani mwangu, akanilemaza na kuniacha mkiwa.
12 Aliuvuta upinde wake, akanilenga mshale wake.
13 Alinichoma moyoni kwa mishale, kutoka katika podo lake.
14 Nimekuwa kitu cha dhihaka kwa watu wote, mchana kutwa nimekuwa mtu wa kuzomewa.
15 Amenijaza taabu, akanishibisha uchungu.
16 Amenisagisha meno katika mawe, akanifanya nigaegae majivuni.
17 Moyo wangu haujui tena amani, kwangu furaha ni kitu kigeni.
18 Nimewaza “Nimekata tamaa kabisa, tumaini langu kwa Mwenyezi-Mungu limetoweka.”
19 Kukumbuka taabu na kutangatanga kwangu kwanipa uchungu kama wa nyongo.
20 Nayafikiria hayo daima, nayo roho yangu imejaa majonzi.
21 Lakini nakumbuka jambo hili moja, nami ninalo tumaini:
22 Kwamba fadhili za Mwenyezi-Mungu hazikomi, huruma zake hazina mwisho.
23 Kila kunapokucha ni mpya kabisa, uaminifu wake ni mkuu mno.
24 Mwenyezi-Mungu ndiye hazina yangu hivyo nitamwekea tumaini langu.
25 Mwenyezi-Mungu ni mwema kwa wanaomtegemea, ni mwema kwa wote wanaomtafuta.
26 Ni vema mtu kungojea kwa saburi ukombozi utokao kwa Mwenyezi-Mungu.
27 Ni vema mtu kujifunza uvumilivu tangu wakati wa ujana wake.
28 Heri kukaa peke na kimya, mazito yanapompata kutoka kwa Mungu.
29 Yampasa kuinama na kujinyenyekesha, huenda ikawa tumaini bado lipo.
30 Yampasa kumgeuzia shavu mwenye kumpiga, na kuwa tayari kupokea matusi yake.
31 Mwenyezi-Mungu hatatutupa milele.
32 Ingawa atufanya tuhuzunike, atakuwa na huruma tena kadiri ya wingi wa fadhili zake.
33 Yeye hapendelei kuwatesa wala kuwahuzunisha wanadamu.
34 Wafungwa wote nchini wanapodhulumiwa na kupondwa;
35 haki za binadamu zinapopotoshwa mbele yake Mungu Mkuu,
36 kesi ya mtu inapopotoshwa mahakamani, je, Mwenyezi-Mungu haoni hayo?
37 Nani awezaye kuamuru kitu kifanyike Mwenyezi-Mungu asipopanga iwe hivyo?
38 Maafa na mema hutokea tu kwa amri yake Mungu Mkuu.
39 Kwa nini mtu anung'unike, ikiwa ameadhibiwa kwa dhambi zake?
40 Na tupime na kuchunguza mwenendo wetu, tupate kumrudia Mwenyezi-Mungu.
41 Tumfungulie Mungu huko mbinguni mioyo yetu na kumwomba:
42 “Sisi tulikukosea na kukuasi nawe bado hujatusamehe.
43 “Umejizungushia hasira yako ukatufuatia, ukatuua bila huruma.
44 Umejizungushia wingu zito, sala yeyote isiweze kupenya humo.
45 Umetufanya kuwa takataka na uchafu miongoni mwa watu wa mataifa.
46 “Maadui zetu wote wanatuzomea.
47 Kitisho na hofu vimetuandama, tumepatwa na maafa na maangamizi.
48 Macho yangu yabubujika mito ya machozi kwa sababu ya kuangamizwa kwa watu wangu.
49 “Machozi yatanitoka bila kikomo,
50 mpaka Mwenyezi-Mungu kutoka huko mbinguni aangalie chini na kuona.
51 Nalia na kujaa majonzi, kuona yaliyowapata kina mama wa mji wangu.
52 “Nimewindwa kama ndege na hao wanichukiao bila sababu.
53 Walinitupa shimoni nikiwa hai na juu yangu wakarundika mawe.
54 Maji yalianza kunifunika kichwa, nami nikafikiri, ‘Huu ni mwisho wangu.’
55 “Kutoka chini shimoni nilikulilia ee Mwenyezi-Mungu.
56 Wewe umenisikia nikikulilia: ‘Usiache kusikia kilio changu cha msaada bali unipatie nafuu.’
57 Nilipokuita ulinijia karibu ukaniambia, ‘Usiogope!’
58 “Umenitetea katika kisa changu ee Mwenyezi-Mungu, umeyakomboa maisha yangu.
59 Umeuona uovu niliotendewa ee Mwenyezi-Mungu, uniamulie kwa wema kisa changu.
60 Umeuona uovu wa maadui zangu, na mipango yao yote ya hila dhidi yangu.
61 “Umesikia matukano yao ee Mwenyezi-Mungu, na mipango yao yote ya hila dhidi yangu.
62 Maneno na mawazo ya maadui zangu siku nzima ni juu ya kuniangamiza mimi.
63 Wakati wote, wamekaa au wanakwenda, mimi ndiye wanayemzomea.
64 Uwalipize, ee Mwenyezi-Mungu kadiri ya hayo matendo yao, kadiri ya mambo waliyotenda wenyewe.
65 Uipumbaze mioyo yao, na laana yako iwashukie.
66 Uwafuatie kwa hasira, uwaangamize, uwafanye watoweke ulimwenguni.”
1 Jinsi gani dhahabu yetu ilivyochujuka, dhahabu safi kabisa ilivyobadilika! Mawe ya thamani yametawanywa yamesambaa barabarani kote.
2 Watoto wa Siyoni waliosifika sana, waliothaminiwa kama dhahabu safi, jinsi gani sasa wamekuwa kama vyombo vya udongo, kazi ya mikono ya mfinyanzi!
3 Hata mbwamwitu huwa na hisia za mama na kuwanyonyesha watoto wao; lakini watu wangu wamekuwa wakatili, hufanya kama mbuni nyikani.
4 Midomo ya watoto wachanga imekauka kwa kiu, watoto wanaomba chakula lakini hakuna anayewapa.
5 Watu waliojilisha vyakula vinono sasa wanakufa njaa barabarani. Waliolelewa na kuvikwa kifalme sasa wanafukua kwa mikono kwenye majaa.
6 Watu wangu wamepata adhabu kubwa kuliko watu wa mji wa Sodoma mji ambao uliteketezwa ghafla bila kuwa na muda wa kunyosha mkono.
7 Vijana wa Siyoni walikuwa safi kuliko theluji, walikuwa weupe kuliko maziwa. Miili yao ilikuwa myekundu kama matumbawe, uzuri wa viwiliwili vyao kama johari ya rangi ya samawati.
8 Sasa sura zao ni nyeusi kuliko makaa, wanapita barabarani bila kujulikana; ngozi yao imegandamana na mifupa yao imekauka, imekuwa kama kuni.
9 Afadhali waliouawa kwa upanga kuliko waliokufa kwa njaa, ambao walikufa polepole kwa kukosa chakula.
10 Kina mama ambao huwa na huruma kuu waliwapika watoto wao wenyewe, wakawafanya kuwa chakula chao wakati watu wangu walipoangamizwa.
11 Mwenyezi-Mungu alionesha uzito wa ghadhabu yake, aliimimina hasira yake kali; aliwasha moto huko mjini Siyoni ambao uliteketeza misingi yake.
12 Wafalme duniani hawakuamini wala wakazi wowote wa ulimwenguni, kwamba mvamizi au adui angeweza kuingia malango ya Yerusalemu.
13 Hayo yalisababishwa na dhambi za manabii wake, yalitukia kwa sababu ya uovu wa makuhani wake ambao walimwaga damu ya waadilifu mjini kwake.
14 Walitangatanga barabarani kama vipofu, walikuwa wamekuwa najisi kwa damu, hata asiwepo mtu yeyote wa kuwagusa.
15 Watu waliwapigia kelele wakisema: “Tokeni, nendeni zenu enyi mlio najisi! Tokeni, tokeni, msiguse chochote.” Hivyo wakawa wakimbizi na kutangatanga; watu wa mataifa walitamka: “Hawa hawatakaribishwa kukaa kwetu!”
16 Mwenyezi-Mungu mwenyewe aliwatawanya, wala hatawajali tena. Makuhani hawatapata tena heshima, wazee hawatapendelewa tena.
17 Tulichoka kukaa macho kungojea msaada; tulikesha na kungojea kwa hamu taifa ambalo halikuweza kutuokoa.
18 Watu walifuatilia hatua zetu, tukashindwa kupita katika barabara zetu. Siku zetu zikawa zimetimia; mwisho wetu ukawa umefika.
19 Waliotufuatia walikuwa wepesi kuliko tai, walitukimbiza milimani, walituvizia huko nyikani.
20 Walimnasa yule ambaye maisha yetu yalimtegemea, yule mfalme aliyewekwa wakfu wa Mwenyezi-Mungu, yule ambaye tulisema: “Chini ya ulinzi wake tutaishi miongoni mwa mataifa.”
21 Wakazi wa Edomu, mwaweza kushangilia kwa sasa, mwaweza kwa sasa kufurahi enyi wakazi wa Uzi; lakini kikombe hiki cha adhabu kitawajia pia, nanyi pia mtakinywa na kulewa, hata mtayavua mavazi yenu!
22 Adhabu ya uovu wako ewe Siyoni imekamilika; Mwenyezi-Mungu hatawaacha zaidi uhamishoni. Lakini nyinyi Waedomu atawaadhibu kwa uovu wenu, atazifichua dhambi zenu.
1 Ukumbuke ee Mwenyezi-Mungu, mambo yaliyotupata! Utuangalie, uone jinsi tulivyoaibishwa!
2 Nchi yetu imekabidhiwa wageni, nyumba zetu watu wengine.
3 Tumekuwa yatima, bila baba, mama zetu wameachwa kama wajane.
4 Maji yetu tunayapata kwa fedha, kuni zetu kwa kuzinunua.
5 Tunalazimishwa kufanya kazi kama punda, tumechoka lakini haturuhusiwi kupumzika.
6 Wamisri na Waashuru tumewanyoshea mikono, ili tupate chakula cha kutosha.
7 Wazee wetu walitenda dhambi na hawapo tena; nasi tunateseka kwa sababu ya makosa yao.
8 Watumwa ndio wanaotutawala, wala hakuna wa kutuokoa mikononi mwao.
9 Chakula chetu twapata kwa kuhatarisha maisha yetu, maana wauaji wanazurura huko mashambani.
10 Ngozi zetu zawaka moto kama tanuri kwa sababu ya njaa inayotuchoma.
11 Wanawake wetu wanashikwa kwa nguvu mjini Siyoni, binti zetu katika vijiji vya Yuda.
12 Wakuu wetu wametungikwa kwa mikono yao; wazee wetu hawapewi heshima yoyote.
13 Vijana wanalazimishwa kusaga nafaka kwa mawe, wavulana wanayumbayumba kwa mizigo ya kuni.
14 Wazee wameacha kutoa mashauri yao, vijana wameacha kuimba.
15 Furaha ya mioyo yetu imetoweka, ngoma zetu zimegeuzwa kuwa ombolezo.
16 Fahari tuliyojivunia imetokomea. Ole wetu kwa kuwa tumetenda dhambi!
17 Kwa ajili hiyo tumeugua moyoni, kwa mambo hayo macho yetu yamefifia.
18 Maana mlima Siyoni umeachwa tupu, mbweha wanazurura humo.
19 Lakini wewe Mwenyezi-Mungu watawala milele, utawala wako wadumu vizazi vyote.
20 Mbona umetuacha muda mrefu hivyo? Mbona umetutupa siku nyingi hivyo?
21 Uturekebishe ee Mwenyezi-Mungu, nasi tukurudie, uturudishie fahari yetu kama zamani.
22 Au, je, umetukataa kabisa? Je, umetukasirikia mno?