1

1 Mnamo mwaka wa kwanza wa utawala wa Koreshi, mfalme wa Persia, ili neno la Mwenyezi-Mungu alilolinena kwa njia ya nabii Yeremia litimie, Mwenyezi-Mungu alimfanya Koreshi, mfalme wa Persia, atangaze amri ifuatayo katika ufalme wake na kuiweka katika maandishi:

2 “Hivi ndivyo anavyosema Koreshi mfalme wa Persia: Mwenyezi-Mungu, Mungu wa mbingu, amenipatia falme zote za ulimwenguni na ameniagiza nimjengee nyumba Yerusalemu, huko Yuda.

3 Basi sasa, kila mtu katika nyinyi nyote mlio watu wake, Mungu wake awe naye na aende Yerusalemu huko Yuda, na kuijenga upya nyumba ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, Mungu anayeabudiwa huko Yerusalemu.

4 Kila mmoja aliyebaki hai uhamishoni akitaka kurudi, jirani zake na wamsaidie kwa kumpa fedha, dhahabu, mali na wanyama, pamoja na matoleo ya hiari kwa ajili ya nyumba ya Mungu huko Yerusalemu.”

5 Basi, wakaondoka viongozi wa koo za makabila ya Yuda na Benyamini, makuhani na Walawi, na kila mtu ambaye Mungu alimpa moyo wa kwenda kujenga upya nyumba ya Mwenyezi-Mungu, iliyoko Yerusalemu.

6 Majirani waliwasaidia watu hao kwa kuwapa vyombo vya fedha, dhahabu, mali, wanyama na vitu vingine vya thamani, mbali na vile vilivyotolewa kwa hiari.

7 Mfalme Koreshi aliwarudishia vyombo ambavyo mfalme Nebukadneza alikuwa amevichukua kutoka katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu na kuviweka katika nyumba ya miungu yake.

8 Alimkabidhi Mithredathi, mtunza hazina, vyombo hivyo, naye akamhesabia Sheshbaza, mtawala wa Yuda.

9 Ifuatayo ndiyo hesabu yake: Bakuli 30 za dhahabu; bakuli 1,000 za fedha; vyetezo 29;

10 bakuli ndogo za dhahabu 30; bakuli ndogo za fedha 410; vyombo vinginevyo 1,000.

11 Vyombo vyote vya dhahabu na fedha, pamoja na vitu vinginevyo vilikuwa jumla yake 5,400. Vyote hivi, Sheshbaza alivichukua hadi Yerusalemu wakati yeye pamoja na watu wengine alipotolewa uhamishoni Babuloni kwenda Yerusalemu.

2

1 Wafuatao ni watu wa mkoani waliotoka utumwani ambao Nebukadneza mfalme wa Babuloni aliwapeleka mateka Babuloni, wakarudi mjini Yerusalemu na nchini Yuda. Kila mtu alirudi mjini kwake.

2 Viongozi wao walikuwa Zerubabeli, Yeshua, Nehemia, Seraya, Reelaya, Mordekai, Bilshani, Mispari, Bigwai, Rehumu na Baana. Ifuatayo ni idadi ya watu wote wa koo za Israeli waliorudi kutoka uhamishoni:

3 Wa ukoo wa Paroshi: 2,172;

4 wa ukoo wa Shefatia: 372;

5 wa ukoo wa Ara: 775;

6 wa ukoo wa Pahath-moabu, yaani wazawa wa Yeshua na Yoabu: 2,812;

7 wa ukoo wa Elamu: 1,254;

8 wa ukoo wa Zatu: 945;

9 wa ukoo wa Zakai: 760;

10 wa ukoo wa Bani: 842;

11 wa ukoo wa Bebai: 623;

12 wa ukoo wa Azgadi: 1,222;

13 wa ukoo wa Adonikamu: 666;

14 wa ukoo wa Bigwai: 2,056;

15 wa ukoo wa Adini: 454;

16 wa ukoo wa Ateri, yaani Hezekia: 98;

17 wa ukoo wa Besai: 323;

18 wa ukoo wa Yora: 112;

19 wa ukoo wa Hashumu: 223;

20 wa ukoo wa Gibari: 95.

21 Watu wa mji wa Bethlehemu: 123;

22 wa mji wa Netofa: 56;

23 wa mji wa Anathothi: 128;

24 wa mji wa Azmawethi: 42;

25 wa mji wa Kiriath-yearimu, wa Kefira na wa Beerothi: 743;

26 wa mji wa Rama na wa Geba: 621;

27 wa mji wa Mikmashi: 122;

28 wa mji wa Betheli na Ai: 223;

29 wa mji wa Nebo: 52;

30 wa mji wa Magbishi: 156;

31 wa mji wa Elamu wa pili: 1,254;

32 wa mji wa Harimu: 320;

33 wa mji wa Lodi, Hadidi na wa Ono: 725;

34 wa mji wa Yeriko: 345;

35 wa mji wa Senaa: 3,630.

36 Ifuatayo ni idadi ya makuhani waliorudi kutoka uhamishoni: Makuhani wa ukoo wa Yedaya, waliokuwa wazawa wa Yeshua: 673;

37 wa ukoo wa Imeri: 1,052;

38 wa ukoo wa Pashuri: 1,247;

39 wa ukoo wa Harimu: 1,017.

40 Walawi wa ukoo wa Yeshua na wa Kadmieli, wazawa wa Hodavia waliorudi kutoka uhamishoni walikuwa 74.

41 Waimbaji (wazawa wa Asafu), walikuwa 128.

42 Walinzi (wazawa wa Shalumu, wa Ateri, wa Talmoni, wa Akubu, wa Hatita na wa Shobai), walikuwa 139.

43 Koo za watumishi wa hekalu waliorudi kutoka uhamishoni zilikuwa: Ukoo wa Siha, wa Hasufa, wa Tabaothi,

44 ukoo wa Kerosi, wa Siaha, wa Padoni,

45 ukoo wa Lebana, wa Hagaba, wa Akubu,

46 ukoo wa Hagabu, wa Shamlai, wa Hanani,

47 ukoo wa Gideli, wa Gahari, wa Reaya,

48 ukoo wa Resini, wa Nekoda, wa Gazamu,

49 ukoo wa Uza, wa Pasea, wa Besai,

50 ukoo wa Asna, wa Meunimu, wa Nefisimu,

51 ukoo wa Bakbuki, wa Hakufa, wa Harhuri,

52 ukoo wa Basluthi, wa Mehida, wa Harsha,

53 ukoo wa Barkosi, wa Sisera, wa Tema,

54 ukoo wa Nezia na wa Hatifa.

55 Koo za wazawa wa watumishi wa Solomoni waliorudi kutoka uhamishoni zilikuwa, ukoo wa Sotai, wa Hasoferethi, wa Perudha,

56 ukoo wa Yaala, wa Darkoni, wa Gideli,

57 ukoo wa Shefatia, wa Hatili, wa Pokereth-hasebaimu na wa Ami.

58 Nao watumishi wote wa hekalu na wazawa wa watumishi wa Solomoni waliorudi kutoka uhamishoni walikuwa watu 392.

59 Watu wa miji ifuatayo, pia walirudi: Wa mji wa Tel-mela, wa Tel-harsha, wa Kerubu, wa Adani na wa Imeri, ila hawakuweza kuthibitisha kuwa walikuwa wazawa wa Waisraeli.

60 Wao walikuwa watu wa ukoo wa Delaya wa Tobia na wa Nekoda, jumla watu 652.

61 Watu wa koo zifuatazo za makuhani pia walirudi: Ukoo wa Habaya, wa Hakosi na wa Barzilai. Huyo Barzilai alikuwa ameoa binti Barzilai wa Gileadi, naye pia akaitwa Barzilai.

62 Hao walitafuta orodha yao katika kumbukumbu za koo, lakini hawakuonekana humo. Kwa hiyo hawakuruhusiwa kushika ukuhani kwani walihesabiwa kuwa najisi.

63 Mtawala akawaambia kuwa hawaruhusiwi kushiriki chakula kitakatifu sana, mpaka awepo kuhani atakayeweza kutoa kauli ya Urimu na Thumimu.

64 Watu wote waliorudi kutoka uhamishoni jumla yao ilikuwa 42,360;

65 mbali na hao, kulikuwa na watumishi wanaume na wanawake 7337; na walikuwa na waimbaji wanaume na wanawake, wote 200.

66 Walikuwa na farasi 736, nyumbu 245,

67 ngamia 435, na punda 6,720.

68 Watu hao waliotoka uhamishoni, walipofika kwenye nyumba ya Mwenyezi-Mungu mjini Yerusalemu, baadhi ya viongozi wa koo hizo walitoa matoleo ya hiari ili kusaidia ujenzi wa nyumba ya Mungu katika Yerusalemu.

69 Walitoa kila mtu kadiri ya uwezo wake kwa ajili ya kazi hii. Jumla ya matoleo hayo ilikuwa kilo 500 za dhahabu, kilo 2,800 za fedha na mavazi 100 kwa ajili ya makuhani.

70 Basi, makuhani, Walawi na baadhi ya watu wengine wakaanza kuishi mjini Yerusalemu na katika vitongoji vyake. Nao waimbaji, walinzi wa hekalu na watumishi wa hekalu wakaanza kuishi katika miji yao; Waisraeli wote waliishi katika miji yao.

3

1 Baadaye mwezi wa saba ulipofika, na watu wa Israeli wakiwa wamekwisha kaa katika miji yao, wote walikusanyika pamoja mjini Yerusalemu.

2 Yeshua, mwana wa Yosadaki, pamoja na makuhani wenzake, na Zerubabeli, mwana wa Shealtieli, pamoja na jamaa zake, waliijenga upya madhabahu ya Mungu wa Israeli, ili waweze kumtolea sadaka za kuteketezwa kama ilivyoandikwa katika sheria ya Mose, mtu wa Mungu.

3 Waliijenga madhabahu hiyo mahali palepale ilipokuwa hapo zamani, kwa kuwa waliwaogopa watu waliokuwa wanaishi katika nchi hiyo. Kisha wakawa wanamtolea Mwenyezi-Mungu sadaka za kuteketezwa juu yake kila siku asubuhi na jioni.

4 Waliiadhimisha sikukuu ya vibanda kama ilivyoandikwa katika sheria; kila siku walitoa sadaka za kuteketezwa zilizohitajika kwa ajili ya siku hiyo.

5 Walitoa pia sadaka za kawaida ambazo ziliteketezwa nzima, sadaka zilizotolewa wakati wa sikukuu ya mwezi mpya na katika sikukuu nyingine zote alizoagiza Mwenyezi-Mungu. Pia, walitoa tambiko zote zilizotolewa kwa hiari.

6 Ingawa msingi wa hekalu la Mwenyezi-Mungu ulikuwa bado kuwekwa, watu walianza kutoa sadaka za kuteketezwa tangu siku ya kwanza ya mwezi wa saba.

7 Watu walitoa fedha za kuwalipa maseremala na waashi, walitoa pia chakula, vinywaji na mafuta, ili vipelekwe katika miji ya Tiro na Sidoni kupata miti ya mierezi kutoka Lebanoni. Miti hiyo ililetwa kwa njia ya bahari hadi Yopa. Haya yote yalifanyika kwa msaada wa mfalme Koreshi wa Persia.

8 Basi, watu walianza kazi mnamo mwezi wa pili wa mwaka wa pili baada ya kufikia nyumba ya Mungu mjini Yerusalemu. Zerubabeli, mwana wa Shealtieli, Yeshua mwana wa Yosadaki, ndugu zao wengine, makuhani, Walawi na watu wengine wote waliorudi Yerusalemu kutoka uhamishoni, walijiunga nao katika kazi hiyo. Walawi wote waliokuwa na umri wa miaka ishirini au zaidi, waliteuliwa ili kusimamia kazi ya kuijenga upya nyumba ya Mwenyezi-Mungu.

9 Yeshua, wanawe na jamaa yake, pamoja na Kadmieli na wanawe, (wa ukoo wa Yuda) walishirikiana kusimamia ujenzi wa nyumba ya Mungu. Walisaidiwa na wazawa wa Henadadi na ndugu zao Walawi.

10 Wajenzi walipoanza kuweka msingi wa hekalu la Mwenyezi-Mungu, makuhani wakiwa wamevalia mavazi yao rasmi, walisimama mahali pao na tarumbeta mikononi, nao Walawi wa ukoo wa Asafu wakisimama na matoazi yao; basi, walimtukuza Mwenyezi-Mungu kufuatana na maagizo ya mfalme Daudi wa Israeli.

11 Waliimba kwa kupokezana, wakimsifu na kumtukuza Mwenyezi-Mungu: “Kwa kuwa yu mwema, fadhili zake kwa Israeli zadumu milele.” Watu wote walipaza sauti kwa nguvu zao zote, wakamsifu Mwenyezi-Mungu kwa sababu ya kuanza kujengwa msingi wa nyumba ya Mwenyezi-Mungu.

12 Wengi wa makuhani, Walawi, na viongozi wa koo waliokuwa wazee na ambao walikuwa wameiona nyumba ya kwanza, walilia kwa sauti kubwa walipouona msingi wa nyumba hii mpya unawekwa, ingawa watu wengine wengi walipaza sauti kwa furaha.

13 Watu hawakuweza kutofautisha kati ya sauti za furaha na za kilio kwa sababu zilikuwa nyingi na zilisikika mbali sana.

4

1 Kisha maadui wa watu wa Yuda na Benyamini waliposikia kwamba watu waliorudi kutoka uhamishoni wanalijenga upya hekalu la Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli,

2 walimwendea Zerubabeli na viongozi wa koo, na kumwambia, “Tafadhali tushirikiane katika ujenzi wa hekalu. Sisi kama nyinyi tunamwabudu Mungu wenu, na tumekuwa tukimtolea tambiko tangu zamani za Esar-hadoni, mfalme wa Ashuru aliyetuleta hapa.”

3 Lakini Zerubabeli, Yeshua na viongozi wengine wa koo za Israeli wakawaambia, “Sisi hatuhitaji msaada wowote kutoka kwenu ili kuijenga nyumba ya Mungu wetu. Sisi wenyewe tutamjengea Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, kama mfalme Koreshi wa Persia alivyotuamuru.”

4 Hapo, watu waliokuwa wanaishi mahali hapo wakaanza kuwavunja moyo na kuwatisha Wayahudi ili wasiendelee kama walivyokusudia.

5 Tena waliwahonga maofisa wa serikali ya Persia wawapinge Wayahudi. Waliendelea kufanya hivyo muda wote wa utawala wa Koreshi, mpaka wakati wa utawala wa Dario.

6 Mwanzoni mwa utawala wa mfalme Ahasuero, maadui wa watu waliokaa Yuda na Yerusalemu waliandika mashtaka dhidi yao.

7 Tena wakati wa utawala wa Artashasta, mfalme wa Persia, Bishlamu, Mithredathi, Tabeeli na rafiki zao, walimwandikia barua mfalme Artashasta. Barua hiyo iliandikwa kwa herufi za Kiaramu na kutafsiriwa.

8 Pia mtawala Rehumu na Shimshai, katibu wa mkoa, walimwandikia Artashasta barua ifuatayo dhidi ya Yerusalemu:

9 “Kutoka kwa mtawala Rehumu na Shimshai, katibu wa mkoa pamoja na wenzetu, na mahakimu, maofisa wote ambao hapo awali walitoka Ereki, Babuloni na Susa katika nchi ya Elamu,

10 pamoja na watu wa mataifa mengine ambao Asur-banipali, mtu mkuu na mwenye nguvu aliwahamisha na kuwaweka katika mji wa Samaria na mahali pengine katika mkoa wa magharibi ya Eufrate.”

11 Barua yenyewe ilikuwa hivi: “Kwa mfalme Artashasta: Sisi watumishi wako katika mkoa wa magharibi ya Eufrate, tunakutumia salamu.

12 Tungependa ufahamu, ewe mfalme, kwamba Wayahudi waliokuja hapa kutoka maeneo mengine ya ufalme wako wamekwenda Yerusalemu na wanaujenga upya mji huo mwasi na mwovu. Wanamalizia kujenga kuta zake na kutengeneza msingi.

13 Tungependa ufahamu, ewe mfalme, kuwa mji huu ukijengwa upya na kuta zake zikimalizika, watu hawatalipa kodi, ushuru wala ada, na hazina yako itapungua.

14 Sasa, kwa kuwa ni wajibu wetu, ee mfalme, hatungependa kuona ukivunjiwa heshima, ndiyo maana tumeona ni vizuri tukuarifu

15 ili ufanye uchunguzi katika kumbukumbu za babu zako. Humo utagundua kwamba tangu zamani, mji huu ulikuwa mwasi na umewasumbua sana wafalme na watawala wa mikoa, na kuwa tangu zamani watu wake ni wachochezi sana; ndio sababu mji huo uliangamizwa.

16 Kwa hiyo tunakujulisha kwamba ikiwa mji huu utajengwa upya na kuta zake zikimalizika, hutaweza kuutawala mkoa wa magharibi ya Eufrate.”

17 Kisha mfalme akapeleka jibu lifuatalo: “Kwa mtawala Rehumu, kwa Shishai, katibu wa mkoa, pamoja na wenzenu wote wanaoishi Samaria na mahali penginepo katika mkoa wa magharibi ya Eufrate.

18 “Barua mliyonitumia imetafsiriwa na kusomwa mbele yangu.

19 Nimetoa amri uchunguzi ufanywe na imegunduliwa kuwa ni kweli kwamba tangu zamani mji huu wa Yerusalemu umekuwa ukiwapinga wafalme na kwamba watu wake wamekuwa waasi na wachochezi wakubwa.

20 Wafalme wenye nguvu wamepata kuutawala mji huo pamoja na mkoa wa magharibi ya Eufrate wakitoza kodi, ushuru na ada.

21 Kwa hiyo, toeni amri watu hao waache kuujenga upya mji huo hadi hapo nitakapotoa maagizo mengine.

22 Tena, angalieni sana msichelewe kufanya hivyo, nisije nikapata hasara.”

23 Mara tu waliposomewa barua hii kutoka kwa Artashasta, Rehumu, katibu Shimshai na wenzao waliharakisha kwenda Yerusalemu na kuwalazimisha kwa nguvu Wayahudi waache kuujenga mji.

24 Kazi ya kuijenga upya nyumba ya Mungu mjini Yerusalemu ilisimama, na hali hiyo iliendelea mpaka mwaka wa pili wa utawala wa Dario, mfalme wa Persia.

5

1 Wakati huo, manabii wawili, Hagai na Zekaria, mwana wa Ido, waliwatolea unabii Wayahudi waliokuwa wanakaa Yuda na Yerusalemu, katika jina la Mungu wa Israeli.

2 Nao Zerubabeli, mwana wa Shealtieli, na Yeshua, mwana wa Yosadaki, walipousikia ujumbe huo walianza tena kuijenga nyumba ya Mungu mjini Yerusalemu, wakisaidiwa na manabii wa Mungu.

3 Baadaye Tatenai, mtawala wa mkoa wa magharibi ya Eufrate, Shethar-bozenai na wenzao, walikwenda Yerusalemu na kuuliza, “Nani aliyewaamuru kuijenga nyumba hii mpaka kuimaliza?”

4 Pia waliuliza, “Ni akina nani wanaojenga nyumba hii? Tunataka majina yao.”

5 Lakini Mungu alikuwa anawalinda viongozi wa Wayahudi, kwa hiyo maofisa hao hawakuwakataza mpaka hapo walipomwandikia mfalme Dario na kupata maoni yake.

6 Basi, Tatenai, mtawala wa mkoa wa magharibi ya Eufrate, Shethar-bozenai na wenzao, wakamwandikia mfalme Dario.

7 Ifuatayo ni ripoti waliyompelekea mfalme: “Kwa mfalme Dario; tunakutakia amani.

8 Tungetaka kukufahamisha ee mfalme, kuwa tulikwenda mkoani Yuda ilipo nyumba ya Mungu Mkuu. Nyumba hii inajengwa upya kwa mawe makubwamakubwa na kuta zake zinawekwa boriti za miti. Kazi hiyo inafanywa kwa uangalifu mkubwa na inaendelea vizuri sana.

9 Tuliwauliza viongozi hao watuambie ni nani aliyewapa amri ya kuijenga upya nyumba hii mpaka kuimaliza.

10 Tuliwauliza pia majina yao ili tuweze kukujulisha wale wanaoongoza kazi hiyo.

11 “Wao walitujibu hivi: ‘Sisi ni watumishi wa Mungu wa mbingu na dunia, na tunaijenga upya nyumba ambayo ilikuwa imejengwa na kumalizika hapo awali na mfalme mmoja mkuu wa Israeli.

12 Lakini kwa kuwa babu zetu walimkasirisha Mungu wa mbingu, yeye aliwatia mikononi mwa mfalme Nebukadneza wa Babuloni, Mkaldayo, aliyeiharibu nyumba hii na kuwapeleka watu uhamishoni huko Babuloni.

13 Lakini mnamo mwaka wa kwanza wa utawala wake mfalme Koreshi wa Babuloni alitoa amri nyumba hii ya Mungu ijengwe upya.

14 Pia alivirudisha vyombo vya dhahabu na fedha ambavyo mfalme Nebukadneza alikuwa amevichukua kutoka katika hekalu huko Yerusalemu na kuviweka katika hekalu la Babuloni. Vyombo hivyo Koreshi aliviondoa hekaluni Babuloni na kumkabidhi Sheshbaza ambaye alikuwa amemteua awe mtawala wa Yuda; alimwamuru

15 achukue vyombo hivyo na kuvirudisha katika hekalu la Yerusalemu, na kuijenga upya nyumba ya Mungu mahali pake.

16 Kisha Sheshbaza alikuja na kuweka msingi wa nyumba ya Mungu mjini Yerusalemu, na tangu wakati huo ujenzi umekuwa ukiendelea mpaka sasa, lakini bado haijamalizika.’

17 Basi, ukipenda ewe mfalme, amuru uchunguzi ufanywe katika kumbukumbu za kifalme mjini Babuloni kama mfalme Koreshi alitoa amri nyumba hii ya Mungu ijengwe upya mjini Yerusalemu. Kisha, tunakuomba utujulishe maoni yako kuhusu jambo hili.”

6

1 Mfalme Dario alitoa amri na uchunguzi ulifanywa mjini Babuloni katika nyumba ya kumbukumbu za kifalme.

2 Lakini kitabu kilipatikana mjini Ekbatana katika mkoa wa Media, nacho kilikuwa na maagizo yafuatayo:

3 “Mnamo mwaka wa kwanza wa utawala wake, mfalme Koreshi alitoa amri nyumba ya Mungu ijengwe upya mjini Yerusalemu, na iwe mahali pa kutolea tambiko na sadaka za kuteketezwa. Kimo chake kitakuwa mita 27 na upana wake mita 27.

4 Kuta zake zitajengwa kwa safu moja ya miti juu ya kila safu tatu za mawe makubwa. Gharama zote zilipwe kutoka katika hazina ya mfalme.

5 Pia, vyombo vyote vya dhahabu na fedha ambavyo mfalme Nebukadneza alivileta Babuloni kutoka katika hekalu la Yerusalemu, vitarudishwa na kuwekwa kila kimoja mahali pake katika nyumba ya Mungu.”

6 Ndipo Dario akapeleka ujumbe ufuatao: “Kwa Tatenai, mtawala wa mkoa wa magharibi ya Eufrate, Shethar-bozenai na maofisa wenzako mkoani. ‘Msiende huko kwenye hekalu,

7 na acheni kazi ya ujenzi wa nyumba hii ya Mungu iendelee. Mwacheni mtawala wa Yuda na viongozi wa Wayahudi waijenge nyumba ya Mungu mahali pake.

8 Zaidi ya hayo, natoa amri kwamba nyinyi mtawasaidia katika kazi hiyo. Gharama zao zote zitalipwa bila kuchelewa kutoka katika hazina ya mfalme inayotokana na kodi kutoka katika mkoa wa magharibi wa mto Eufrate.

9 Kila siku, tena bila kukosa, mtawapa makuhani wa Yerusalemu kila kitu watakachohitaji; iwe ni fahali wachanga, kondoo dume au wanakondoo wa sadaka za kuteketezwa kwa Mungu wa mbinguni, au ngano, chumvi, divai au mafuta.

10 Haya yote yatatendeka ili waweze kumtolea Mungu wa mbinguni tambiko zinazompendeza na waombee maisha yangu mimi mfalme na watoto wangu.

11 Naamuru pia kwamba mtu yeyote ambaye hatatii amri hii, boriti ingolewe kutoka katika nyumba yake, na atumbuliwe kwayo. Tena, nyumba yake na ifanywe kuwa rundo la mavi.

12 Mungu aliyeuchagua mji wa Yerusalemu kuwa mahali pake pa kuabudiwa na amwangushe mfalme au taifa lolote litakalopinga amri hii au kutaka kuiharibu nyumba hii ya Mungu iliyoko mjini Yerusalemu. Mimi Dario nimetoa amri hii. Ni lazima ifuatwe.’”

13 Basi, Tatenai, mtawala wa mkoa wa magharibi ya mto Eufrate, Shethar-bozenai, na maofisa wenzao, wakafanya bidii kutekeleza maagizo ya mfalme.

14 Viongozi wa Wayahudi waliendelea vizuri sana na kazi ya ujenzi wa hekalu, wakitiwa moyo kwa mahubiri ya nabii Hagai na Zekaria, mwana wa Ido. Walimaliza ujenzi wa hekalu kama walivyoamriwa na Mungu wa Israeli, na kama walivyoagizwa na mfalme Koreshi, mfalme Dario na mfalme Artashasta, wa Persia.

15 Ujenzi wa nyumba hiyo ulimalizika mnamo siku ya tatu ya mwezi wa Adari, katika mwaka wa sita wa utawala wa mfalme Dario.

16 Basi, watu wa Israeli, makuhani, Walawi na watu wengine waliokuwa wamerudi kutoka uhamishoni waliiweka wakfu nyumba ya Mwenyezi-Mungu kwa shangwe kuu.

17 Wakati wa kuiweka wakfu nyumba ya Mungu, walitoa mafahali 100, kondoo madume 200, wanakondoo 800 na mbuzi madume 12 kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi, mbuzi mmoja kwa kila kabila la Israeli.

18 Pia, kwa ajili ya huduma ya Mungu katika Yerusalemu, waliwapanga makuhani katika makundi yao ya Walawi katika zamu zao kufuatana na maagizo yaliyoandikwa katika kitabu cha Mose.

19 Mnamo siku ya kumi na nne ya mwezi wa kwanza, watu waliokuwa wamerudi kutoka uhamishoni walisherehekea Pasaka.

20 Makuhani na Walawi walikuwa wamejitakasa, wote walikuwa safi kabisa. Walichinja mwanakondoo wa Pasaka kwa ajili ya watu wote waliorudi kutoka uhamishoni, ndugu zao makuhani na kwa ajili yao wenyewe.

21 Waliokula mwanakondoo wa Pasaka walikuwa Waisraeli wote waliorudi kutoka uhamishoni pamoja na watu wengine wote ambao walikuwa wameziacha njia za mataifa mengine ili kumwabudu Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli.

22 Kwa muda wa siku saba watu walisherehekea kwa furaha sikukuu ya mikate isiyotiwa chachu, kwa sababu Mwenyezi-Mungu aliwajalia furaha na kumpa mfalme wa Ashuru moyo wa upendo kwao, akawasaidia katika kazi za ujenzi wa nyumba ya Mungu wa Israeli.

7

1 Baadaye, wakati wa utawala wa mfalme Artashasta wa Persia, palikuwa na mtu mmoja aliyeitwa Ezra. Ezra alikuwa mwana wa Seraya, mwana wa Azaria, mwana wa Hilkia,

2 mwana wa Shalumu, mwana wa Sadoki, mwana wa Ahitubu,

3 mwana wa Amaria, mwana wa Azaria, mwana wa Merayothi,

4 mwana wa Zerahia, mwana wa Uzi, mwana wa Buki,

5 mwana wa Abishua, mwana wa Finehasi, mwana wa Eleazari, mwana wa Aroni, kuhani mkuu.

6 Ezra aliondoka Babuloni, yeye alikuwa mwandishi mwenye ujuzi mwingi sana katika sheria ambayo Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, alikuwa amempatia Mose. Na kwa msaada wa Mwenyezi-Mungu, Mungu wake, mfalme alimpatia Ezra kila kitu alichohitaji.

7 Mnamo mwaka wa saba wa utawala wa mfalme Artashasta, Ezra alifunga safari kutoka Babuloni kwenda Yerusalemu. Baadhi ya watu wa Israeli, makuhani, Walawi, waimbaji, walinda malango na wahudumu wa hekalu walikwenda pamoja naye.

8 Waliwasili mjini Yerusalemu mnamo siku ya kwanza ya mwezi wa tano katika mwaka wa saba wa utawala wa mfalme Artashasta.

9 Mwenyezi-Mungu aliifanikisha sana safari yao waliyokuwa wameianza siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza.

10 Ezra alikuwa amejitoa kwa moyo wote kujifunza sheria ya Mwenyezi-Mungu, kuitii na kuwafundisha watu wa Israeli maagizo na amri zake.

11 Ifuatayo ni barua ambayo Artashasta alimpa Ezra, kuhani na mwandishi, na mwenye ujuzi katika amri na masharti ambayo Mwenyezi-Mungu aliwapa watu wa Israeli.

12 “Kutoka kwa Artashasta, mfalme wa wafalme, kwa Ezra, kuhani na mtu mwenye ujuzi katika sheria ya Mungu wa mbinguni; Wasalaam!”

13 “Ninaamuru kwamba katika utawala wangu, Mwisraeli yeyote, au kuhani wao, au Mlawi, akitaka kurudi Yerusalemu kwa hiari yake, anaweza kwenda pamoja nawe.

14 “Mimi pamoja na washauri wangu saba, tunakutuma uende ufanye uchunguzi huko Yuda na Yerusalemu kuona kama sheria ya Mungu wako ambayo umekabidhiwa inafuatwa kikamilifu.

15 Utachukua fedha na dhahabu ambayo mimi na washauri wangu tumemtolea kwa hiari Mungu wa Israeli ambaye hekalu lake limo mjini Yerusalemu.

16 Utachukua pia fedha na dhahabu yote utakayokusanya katika mkoa wote wa Babuloni, pamoja na matoleo ya hiari waliyotoa Waisraeli na makuhani wao kwa ajili ya nyumba ya Mungu wao iliyoko Yerusalemu.

17 Fedha hiyo utaitumia kwa uangalifu sana kununua mafahali, kondoo dume, wanakondoo na tambiko ya nafaka na divai, na kuvitoa madhabahuni katika nyumba ya Mungu wenu iliyoko Yerusalemu.

18 Fedha na dhahabu itakayobaki unaweza kuitumia pamoja na wananchi wenzako kama mtakavyopenda, kufuatana na mapenzi ya Mungu.

19 Vyombo ambavyo umekabidhiwa kwa ajili ya ibada ya nyumba ya Mungu wako, utamtolea Mungu wa Yerusalemu.

20 Ukihitaji kitu kingine chochote kwa ajili ya nyumba ya Mungu wako unaweza kukipata kutoka katika hazina ya mfalme.

21 Mimi mfalme Artashasta, natoa amri kwa waweka hazina wote katika mkoa wa magharibi ya mto Eufrate kwamba chochote atakachohitaji Ezra, kuhani na mwandishi wa sheria ya Mungu wa mbinguni, mtampa, tena bila kusita,

22 fedha kiasi atakacho mpaka kufikia kilo 3,400, ngano kilo 10,000, divai lita 2,000, mafuta lita 2,000, na chumvi kiasi chochote atakachohitaji.

23 Kila kitu alichoagiza Mungu wa mbinguni kwa ajili ya nyumba yake, ni lazima kitekelezwe kikamilifu, asije akaukasirikia ufalme wangu au wanangu.

24 Tunawafahamisheni pia kuwa ni marufuku kuwadai kodi ya mapato, ushuru au ada makuhani, Walawi, waimbaji, walinda mlango, wafanyakazi au watumishi wengine wa nyumba hii ya Mungu.

25 Nawe Ezra, kwa kutumia hekima aliyokupa Mungu wako, hiyo uliyonayo, chagua mahakimu, na waamuzi watakaowaongoza wakazi wote wa mkoa wa magharibi ya Eufrate ambao wanaishi kufuatana na sheria ya Mungu wako. Na yule ambaye haijui sheria hiyo, mfundishe.

26 Mtu yeyote ambaye hatatii sheria ya Mungu wako na ya mfalme, na ahukumiwe mara moja: Kufa, kuhamishwa, kunyanganywa mali yake au kufungwa.”

27 Ezra akasema, “Na asifiwe Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zetu; ambaye amempatia mfalme moyo wa kutia mapambo nyumba ya Mwenyezi-Mungu iliyoko Yerusalemu.

28 Kwa fadhili zake Mungu, nimepata msaada wa mfalme na maofisa wake wenye uwezo mkuu. Nilijipa moyo kwa kuwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu, alikuwa pamoja nami, hata niliwakusanya viongozi wa Israeli ili warudi pamoja nami.”

8

1 Ifuatayo ni orodha ya viongozi wa koo za watu waliorudi pamoja nami Ezra kutoka Babuloni, wakati wa utawala wa mfalme Artashasta:

2 Gershomu, wa ukoo wa Finehasi. Danieli, wa ukoo wa Ithamari. Hatushi, wa ukoo wa Daudi,

3 aliyekuwa mwana wa Shekania. Zekaria, wa ukoo wa Paroshi, pamoja na wanaume 150 wa ukoo wake, walioandikishwa pamoja.

4 Eliehoenai, mwana wa Zerahia, wa ukoo wa Pahath-moabu, pamoja na wanaume 200.

5 Shekania, mwana wa Yahazieli, wa ukoo wa Zatu, pamoja na wanaume 300.

6 Ebedi, mwana wa Yonathani, wa ukoo wa Adini, pamoja na wanaume 50.

7 Yeshaya, mwana wa Athalia, wa ukoo wa Elamu, pamoja na wanaume 70.

8 Zebadia, mwana wa Mikaeli, wa ukoo wa Shefatia, pamoja na wanaume 80.

9 Obadia, mwana wa Yehieli, wa ukoo wa Yoabu, pamoja na wanaume 218.

10 Shelomithi, mwana wa Yosifia, wa ukoo wa Bani, pamoja na wanaume 160.

11 Zekaria, mwana wa Bebai, wa ukoo wa Bebai, pamoja na wanaume 28.

12 Yohanani, mwana wa Hakatani, wa ukoo wa Azgadi, pamoja na watu 110.

13 Elifeleti, Yeueli na Shemaya, wa ukoo wa Adonikamu, pamoja na wanaume 60, (hawa walirudi baadaye).

14 Uthai na Zakuri, wa ukoo wa Bigwai, pamoja na wanaume 70.

15 Niliwakusanya pamoja watu wote kando ya mto uelekeao mji wa Ahava. Huko, tulipiga kambi kwa muda wa siku tatu. Niliwakagua watu wote pamoja na makuhani, lakini sikupata Walawi miongoni mwao.

16 Niliita waje kwangu viongozi tisa: Eliezeri, Arieli, Shemaya, Elnathani, Yaribu, Elnathani, Nathani, Zekaria na Meshulamu, pamoja na waalimu wawili, Yoyaribu na Elnathani.

17 Nikawatuma kwa Ido, kiongozi wa jamii ya watu kule Kasifia, nikimwomba yeye pamoja na wenzake wahudumu wa nyumba ya Mungu, watuletee watu watakaohudumu katika nyumba ya Mungu.

18 Kwa neema yake Mungu, walituletea Sherebia, mtu mwenye busara na Mlawi wa ukoo wa Mahli, pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wanane.

19 Walituletea pia Hashabia na Yeshaya, wote wa ukoo wa Merari, pamoja na ndugu zao ishirini.

20 Mbali na hao, kulikuwa na wahudumu wa hekalu 220 ambao babu zao walikuwa wamechaguliwa na mfalme Daudi na maofisa wake kuwasaidia Walawi. Majina ya watu wote hawa yaliorodheshwa.

21 Kisha, nilitoa maagizo kuwa sote tufike karibu na mto Ahava ili tufunge na kujinyenyekeza mbele za Mungu wetu na kumwomba atulinde na kutuongoza katika safari yetu pamoja na watoto wetu.

22 Ingekuwa aibu kubwa kwangu kumwomba mfalme kikosi cha askari na wapandafarasi wa kutulinda na adui njiani maana nilikuwa nimekwisha mwambia kuwa Mungu wetu huwabariki wote wanaomtafuta, lakini huwachukia na kuwaadhibu wote wanaomwacha.

23 Kwa hiyo tulifunga na kumwomba Mungu atulinde, naye aliyasikia maombi yetu.

24 Halafu kati ya makuhani waliokuwa viongozi nilichagua kumi na wawili: Sherebia, Hashabia pamoja na wenzao kumi.

25 Hawa niliwapimia kwa mizani fedha, dhahabu na vyombo ambavyo mfalme, washauri wake, maofisa wake pamoja na watu wa Israeli walivyokuwa wamevitoa kwa ajili ya sadaka ya nyumba ya Mungu wetu.

26 Hivi ndivyo vitu nilivyowapimia: Fedha tani 22, vyombo 100 vya fedha, uzito wake kilo 70, dhahabu kilo 3400,

27 mabakuli 20 ya dhahabu, uzito wake kilo 8, vyombo viwili vya shaba nzuri iliyongaa yenye thamani kama ya dhahabu.

28 Kisha nikawaambia, “Nyinyi ni wakfu kwa Mwenyezi-Mungu. Kadhalika vyombo ni wakfu na fedha na dhahabu ni matoleo ya hiari kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zenu.

29 Tafadhali vilindeni na vitunzeni mpaka mtakapovipima mbele ya makuhani wakuu, Walawi na viongozi wa koo za Israeli, huko Yerusalemu katika vyumba vya nyumba ya Mwenyezi-Mungu.”

30 Basi, makuhani na Walawi wakachukua fedha, dhahabu na vyombo vyote walivyopimiwa, ili kuvipeleka mjini Yerusalemu katika nyumba ya Mungu wetu.

31 Mnamo siku ya kumi na mbili ya mwezi wa kwanza, tulisafiri kutoka mto Ahava, kwenda Yerusalemu. Mungu wetu alikuwa pamoja nasi, akatulinda na maadui na washambuliaji wa njiani.

32 Tulipofika Yerusalemu, tulipumzika kwa muda wa siku tatu.

33 Mnamo siku ya nne, tukiwa ndani ya nyumba ya Mungu wetu, tulipima ile fedha, dhahabu na vile vyombo, kisha tukamkabidhi kuhani Meremothi, mwana wa Uria. Meremothi alikuwa pamoja na Eleazari, mwana wa Finehasi, na Walawi wawili, Yozabadi, mwana wa Yeshua, na Noadia, mwana wa Binui.

34 Kila kitu kilihesabiwa na kupimwa na wakati huo uzito wa kila kitu uliandikwa.

35 Kisha, watu wote waliorudi kutoka uhamishoni walimtolea Mungu wa Israeli sadaka zao za kuteketezwa. Walitoa mafahali 12 kwa ajili ya Israeli yote, kondoo madume 96 na wanakondoo 77; pia walitoa mbuzi 12 kama sadaka ya kuondoa dhambi. Wanyama wote hawa walitolewa kuwa sadaka ya kuteketezwa kwa Mwenyezi-Mungu.

36 Aidha, waliwakabidhi manaibu wa mfalme na watawala wa mkoa wa magharibi ya Eufrate mwongozo waliopewa na mfalme, nao walitoa msaada kwa watu na kwa ajili ya nyumba ya Mungu.

9

1 Baada ya mambo haya yote kutendeka, viongozi walinijia na kunipa taarifa ifuatayo: “Watu wa Israeli, makuhani na Walawi hawajajitenga na wakazi wa nchi ambao wanatenda machukizo: Waamoni, Wamoabu na Wamisri, Wakanaani, Wahiti, Waperizi, Wayebusi na Waamori.

2 Wayahudi wanaoa wanawake wa kigeni na kuwaoza wavulana wao pia. Hivyo, taifa takatifu la Mungu limechanganyika na watu wa mataifa mengine Isitoshe, maofisa na wakuu ndio wa kwanza kutenda maovu hayo.”

3 Nilipoyasikia maelezo hayo, nilizirarua nguo zangu na joho langu, nikazingoa nywele zangu na ndevu zangu kwa huzuni kubwa na kuketi chini kwa hofu.

4 Ndipo watu wote walioshikwa na hofu kwa sababu ya maneno aliyosema Mungu wa Israeli kuhusu makosa ya wale waliorudi kutoka uhamishoni walipoanza kukusanyika karibu nami hali nikikaa katika hofu hadi jioni, wakati wa kutoa tambiko.

5 Jioni, wakati wa kutoa tambiko ulipofika, niliinuka mahali hapo nilipokuwa nimekaa kwa huzuni huku nguo zangu zimeraruka pamoja na joho, nikapiga magoti na kumnyoshea mikono yangu Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu, na kuomba,

6 nikisema, “Ee Mungu wangu, naona aibu kubwa sana kukiinua kichwa changu mbele yako. Dhambi zetu zimerundikana kupita hata vichwa vyetu; naam, makosa yetu yanafika hata mbinguni.

7 Tangu nyakati za babu zetu hadi sasa, sisi watu wako tumekukosea sana. Na kwa sababu ya dhambi zetu, sisi, wafalme wetu na makuhani wetu tumetiwa mikononi mwa wafalme wa nchi za kigeni, tukauawa, tukachukuliwa mateka na kunyanganywa mali zetu. Na hadi hivi leo, tumetiwa haya kupita kiasi.

8 Lakini sasa, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, kwa muda mfupi umetuonesha huruma yako na kuwawezesha baadhi yetu kuponyoka kutoka utumwani na kuishi kwa usalama mahali hapa patakatifu. Badala ya utumwa, umetupa furaha na maisha mapya.

9 Hukutuacha tuishi utumwani ingawa tulikuwa tu watumwa Uliwafanya wafalme wa Persia wawe wema kwetu na kuturuhusu tuishi na kuijenga nyumba yako iliyokuwa imebomoka, ukatufanya tukae salama hapa Yuda na Yerusalemu.

10 “Lakini sasa, ee Mungu wetu, tuseme nini baada ya hayo yote? Maana, tumeziasi amri zako

11 ulizotupa kwa njia ya watumishi wako manabii ukisema: ‘Nchi mnayoiendea na ambayo itakuwa mali yenu ni nchi iliyo najisi yenye uchafu wa wakazi toka nchi mbalimbali, kwa machukizo yao, wameijaza unajisi tele kila mahali.

12 Kwa hiyo, msiwaoze watu hao binti zenu, wala msiwaruhusu wavulana wenu kuwaoa binti zao. Pia, msishughulikie usalama au mafanikio yao, ili nyinyi wenyewe muweze kuwa na nguvu, na mfaidi mema ya nchi hiyo na kuwaachia watoto wenu kama urithi milele.’

13 Hata baada ya yote yaliyotupata kwa sababu ya maovu yetu na makosa yetu mengi, tunajua kwamba adhabu uliyotupa, ee Mungu wetu, ni ndogo ikilinganishwa na makosa yetu, na umewaacha baadhi yetu hai.

14 Je, tutavunja amri zako tena na kuoana na watu hawa watendao maovu haya? Je, hutatukasirikia na kutuangamiza kabisa, asibaki hata mmoja wetu hai wala yeyote wa kutoroka?

15 Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, wewe ni mwenye haki na umetuacha tubaki kama tulivyo hivi leo. Tunaungama makosa yetu mbele yako, tukijua kuwa hakuna aliye na haki yoyote ya kuja mbele yako kwa ajili ya makosa haya.”

10

1 Wakati Ezra alipokuwa anaomba na kuungama huku analia na kujiangusha kifudifudi mbele ya nyumba ya Mungu, umati mkubwa wa watu wa Israeli, wanaume, wanawake na watoto, walikusanyika karibu naye wakilia kwa uchungu mwingi.

2 Ndipo Shekania, mwana wa Yehieli, wa ukoo wa Elamu, akamwambia Ezra, “Tumekosa uaminifu kwa Mungu kwa kuoa wanawake wa kigeni wa nchi hii, lakini hata hivyo bado kuna tumaini kwa ajili ya Israeli.

3 Kwa hiyo, na tufanye agano na Mungu wetu, tuachane na wanawake hawa pamoja na watoto wao, kwa kufuatana na ushauri wako na wa wengine wanaotii amri za Mungu. Yote yatendeke kwa kufuatana na sheria.

4 Amka uchukue hatua, sisi tutakuunga mkono. Kwa hiyo jipe moyo ufanye hivyo.”

5 Ezra alianza kwa kuwafanya makuhani, viongozi, Walawi na Waisraeli wengine wote waape kwamba watafanya kama ilivyosemwa, nao wakakubali kula kiapo.

6 Kisha, Ezra akaondoka mbele ya nyumba ya Mungu, akaenda nyumbani kwa Yehohanani, mwana wa Eliashibu. Huko, Ezra alilala usiku kucha bila kula wala kunywa maji, kwa huzuni aliyokuwa nayo juu ya ukosefu wa imani ya watu waliotoka uhamishoni.

7 Tangazo lilitolewa kila mahali nchini Yuda na mjini Yerusalemu kwa wote waliotoka uhamishoni kuwa wakusanyike Yerusalemu.

8 Ikiwa mtu yeyote atashindwa kufika katika muda wa siku tatu, kulingana na amri iliyotolewa na viongozi, mali yake yote itachukuliwa, naye binafsi atapigwa marufuku kujiunga na jumuiya ya watu waliorudi kutoka uhamishoni.

9 Katika siku hizo tatu, mnamo siku ya ishirini ya mwezi wa tisa, watu wote walioishi katika Yuda na Benyamini walifika Yerusalemu na kukusanyika katika uwanja wa nyumba ya Mungu. Watu wote walikuwa wakitetemeka kwa sababu ya jambo waliloitiwa na kwa ajili ya mvua nyingi iliyokuwa ikinyesha.

10 Kuhani Ezra alisimama kuzungumza na watu, akawaambia: “Hamkuwa waaminifu kwa kuoa wanawake wa kigeni, na hivyo mmeiongezea Israeli hatia.

11 Sasa, tubuni dhambi zenu mbele ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zenu, na kufanya yale yanayompendeza. Jitengeni na wakazi wa nchi hii na kuwaacha wake zenu wa kigeni.”

12 Watu wote walipaza sauti na kujibu kwa pamoja, “Ni sawa! Ni lazima tufanye kama unavyosema.”

13 Lakini wakaongeza kusema, “Watu ni wengi na mvua inanyesha sana. Hatuwezi kuendelea kusimama hapa uwanjani, na hili si jambo ambalo litamalizika kwa siku moja au mbili! Tumefanya kosa kubwa sana kuhusu jambo hili.

14 Afadhali maofisa wetu wabaki Yerusalemu kushughulikia jambo hili kwa niaba ya watu wote. Kisha, kila mmoja ambaye ameoa mwanamke wa kigeni na aje kwa zamu pamoja na viongozi na mahakimu wa mji wake, mpaka hapo ghadhabu kali ya Mungu wetu itakapoondolewa kwetu.”

15 Hakuna aliyepinga mpango huu, ila Yonathani, mwana wa Asaheli na Yazeya, mwana wa Tikwa, nao wakaungwa mkono na Meshulamu na Mlawi Shabethai.

16 Watu wote waliorudi kutoka uhamishoni walikubali mpango huo, kwa hiyo kuhani Ezra aliwachagua wanaume kati ya viongozi wa koo mbalimbali na kuyaorodhesha majina yao. Mnamo siku ya kwanza ya mwezi wa kumi, watu hao walianza kazi yao ya uchunguzi wa jambo hilo.

17 Siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, walikuwa wamekwisha maliza uchunguzi wao kuhusu wanaume wote waliokuwa wameoa wanawake wa kigeni.

18 Hii ndiyo orodha ya wanaume waliokuwa wameoa wanawake wa kigeni: Makuhani kulingana na koo zao: Ukoo wa Yeshua, mwana wa Yehosadaki na ndugu zake: Maaseya, Eliezeri, Yaribu na Gedalia.

19 Hao waliahidi kuwaacha wake zao, na wakatoa kondoo dume kuwa sadaka kwa ajili ya hatia yao.

20 Ukoo wa Imeri: Hanani na Zebadia.

21 Ukoo wa Harimu: Maaseya, Elia, Shemaya, Yehieli na Uzia.

22 Ukoo wa Pashuri: Eliehoenai, Maaseya, Ishmaeli, Nethaneli, Yozabadi na Elasa.

23 Walawi: Yozabadi, Shimei, Kelaya (aliyejulikana pia kama Kelita), Pethahia, Yuda na Eliezeri.

24 Kati ya waimbaji: Eliashibu. Walinzi wa hekalu: Shalumu, Telemu na Uri.

25 Watu wengineo wa Israeli: Ukoo wa Paroshi: Ramia, Izia, Malkiya, Miyamini, Eleazari, Malkiya na Benaya.

26 Ukoo wa Elamu: Matania, Zekaria, Yehieli, Abdi, Yeremothi na Elia.

27 Ukoo wa Zatu: Eliehoenai, Eliashibu, Matania, Yeremothi, Zabadi na Aziza.

28 Ukoo wa Bebai: Yehohanani, Hanania, Zabai na Athlai.

29 Ukoo wa Bani: Meshulamu, Maluki, Adaya, Yashubu, Sheali na Yeremothi.

30 Ukoo wa Pahath-moabu: Adna, Kelali, Benaya, Maaseya, Matania, Besaleli, Binui na Manase.

31 Ukoo wa Harimu: Eliezeri, Ishiya, Malkiya, Shemaya, Shimeoni,

32 Benyamini, Maluki na Shemaria.

33 Ukoo wa Hashumu: Matenai, Matata, Zabadi, Elifeleti, Yeremai, Manase na Shimei.

34 Ukoo wa Bani: Maadai, Amramu, Ueli,

35 Benaya, Bedeya, Keluhi,

36 Wania, Meremothi, Eliashibu,

37 Matania, Matenai na Yaasu.

38 Ukoo wa Binui: Shimei,

39 Shelemia, Nathani, Adaya,

40 Maknadebai, Shashai, Sharai,

41 Azareli, Shelemia, Shemaria,

42 Shalumu, Amaria na Yosefu.

43 Ukoo wa Nebo: Yeieli, Matithia, Zabadi, Zebina, Yadai, Yoeli na Benaya.

44 Wanaume hawa wote walikuwa wameoa wanawake wa kigeni. Basi wakawaacha wanawake hao pamoja na watoto wao.