1

1 Solomoni, mwanawe mfalme Daudi, alijiimarisha katika utawala wake, naye Mwenyezi-Mungu, Mungu wake alikuwa pamoja naye, akambariki na kumfanya awe mkuu sana.

2 Mfalme Solomoni aliwaita makamanda wote wa vikosi vya maelfu na vya mamia, waamuzi, na viongozi wote wa koo za Israeli.

3 Kisha akaandamana nao hadi mahali pa ibada huko Gibeoni. Walikwenda huko kwa sababu hapo ndipo mahali lilipokuwa hema la mkutano la Mungu alilolitengeneza Mose mtumishi wa Mwenyezi-Mungu, nyikani.

4 (Lakini, sanduku la Mungu lilikuwa Yerusalemu katika hema ambalo mfalme Daudi alilipigilia alipolileta kutoka Kiriath-yearimu).

5 Tena, madhabahu ya shaba iliyotengenezwa na Bezaleli, mwana wa Uri na mjukuu wa Huri, pia ilikuwa huko Gibeoni mbele ya hema takatifu la Mwenyezi-Mungu. Hapo mfalme Solomoni na watu wote wakamwomba Mwenyezi-Mungu.

6 Solomoni alipanda mbele ya madhabahu ya shaba iliyokuwa kwenye hema la mkutano. Hapo mbele ya Mwenyezi-Mungu, akatoa tambiko 1,000 za kuteketezwa juu ya madhabahu hayo.

7 Usiku huo, Mungu alimtokea Solomoni, akamwambia, “Omba chochote, nami nitakupa.”

8 Solomoni akamwambia Mungu, “Ulimwonesha baba yangu Daudi fadhili nyingi, na umenijalia kuwa mfalme mahali pake.

9 Sasa, ee Mungu, Mwenyezi-Mungu, itimize ahadi uliyompa baba yangu Daudi. Umenitawaza niwe mfalme juu ya watu hawa walio wengi kama mavumbi.

10 Kwa hiyo, nakuomba unipe hekima na maarifa ili niweze kuwatawala watu wako vizuri. La sivyo, nitawezaje kuwatawala hawa watu wako walio wengi hivi?”

11 Mungu akamjibu Solomoni, “Kwa kuwa jambo hili uliloomba limo moyoni mwako, na wala hukuomba mali, wala utajiri, wala heshima wala hukuomba wanaokuchukia waangamizwe, wala maisha marefu, lakini umeomba hekima na maarifa ili uwatawale vizuri watu wangu ambao nimekupa uwe mfalme wao,

12 ninakupa hekima na maarifa. Pia, nitakupa utajiri, mali na heshima zaidi ya mfalme mwingine yeyote aliyekuwako kabla yako na mfalme mwingine yeyote atakayetawala baada yako.”

13 Basi, Solomoni aliondoka mahali hapo pa kuabudia, huko Gibeoni, lilipokuwa hema la mkutano, akarudi Yerusalemu. Akaitawala Israeli.

14 Solomoni alikusanya magari ya farasi na wapandafarasi; alikuwa na magari ya farasi 1,400, na wapandafarasi 12,000, ambao aliwaweka katika miji yenye vituo vya magari ya farasi na kwake katika Yerusalemu.

15 Mfalme Solomoni aliongeza fedha na dhahabu zikawa nyingi kama mawe katika Yerusalemu, na mbao za mierezi zikapatikana kwa wingi kama mikuyu ya Shefela.

16 Farasi wa Solomoni walitoka Misri na Kilikia; wafanyabiashara wake waliwanunua huko.

17 Walinunua gari moja la farasi kutoka Misri kwa bei ya shekeli 600 za fedha, na farasi mmoja kwa shekeli 150 za fedha. Kisha waliwauzia wafalme wa Wahiti na Shamu farasi hao na magari.

2

1 Mfalme Solomoni alikata shauri kujenga nyumba ambamo Mwenyezi-Mungu ataabudiwa, na pia kujijengea yeye mwenyewe jumba la kifalme.

2 Alipanga wanaume 70,000 wawe wachukuzi wa mizigo, 80,000 wawe wachonga mawe milimani na wengine 3,600 wawe wasimamizi wao.

3 Kisha, Solomoni akatuma ujumbe kwa Hiramu, mfalme wa Tiro, akamwambia, “Nitendee na mimi kama ulivyomtendea baba yangu Daudi, ulipompelekea mierezi ya kujengea ikulu.

4 Tazama, karibu nianze kujenga nyumba ya kumwabudia Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu. Nitaiweka wakfu, nayo itakuwa mahali pa kufukiza ubani wa harufu nzuri mbele yake, na mahali pa mikate ya kuwekwa mbele yake daima, na tambiko za kuteketezwa asubuhi na jioni na pia siku za Sabato, mwezi mwandamo, na sikukuu nyinginezo za Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, kama alivyoiagiza Israeli milele.

5 Nyumba ninayokusudia kujenga itakuwa kubwa sana, kwani Mungu wetu ni mkuu zaidi ya miungu yote.

6 Lakini ni nani awezaye kumjengea nyumba ikiwa mbingu zenyewe hazimtoshi, wala mbingu za juu sana? Nami ni nani basi, hata nimjengee nyumba isipokuwa tu kama mahali pa kufukizia ubani mbele yake?

7 Basi, sasa nitumie mtu mwenye ujuzi wa kutengeneza vyombo kwa dhahabu, fedha, shaba, na chuma, na nguo za rangi ya zambarau, za rangi nyekundu na ya samawati, ajuaye pia, kutia nakshi. Yeye atashirikiana katika kazi hiyo na mafundi walioko pamoja nami katika Yuda na Yerusalemu, ambao baba yangu Daudi aliwachagua.

8 Tena nipelekee mierezi, miberoshi na misandali kutoka Lebanoni, kwa maana najua ya kwamba watumishi wako ni hodari sana wa kupasua mbao huko Lebanoni. Nao watumishi wangu watashirikiana na watumishi wako,

9 ili wanipasulie mbao kwa wingi, maana nyumba ninayokusudia kujenga ni kubwa na ya ajabu.

10 Kwa ajili ya watumishi wako, yaani maseremala watakaopasua mbao, nitatoa tani 2,000 za ngano iliyopondwa, tani 2,000 za shayiri, lita 400,000 za divai na lita 400,000 za mafuta.”

11 Naye Hiramu, mfalme wa Tiro, alimjibu Solomoni kwa barua akisema: “Kwa kuwa Mwenyezi-Mungu anawapenda watu wake, amekufanya uwe mfalme wao.

12 Atukuzwe Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, aliyeziumba mbingu na dunia! Amempa mfalme Daudi mwana mwenye hekima, busara na akili, atakayemjengea Mwenyezi-Mungu nyumba, na kujijengea ikulu.

13 Sasa nakupelekea fundi stadi sana na mwenye akili, jina lake Huramu-abi,

14 mwana wa mmoja wa wanawake wa kabila la Dani, na baba yake alikuwa mkazi wa Tiro. Yeye ana ujuzi mwingi wa kutumia dhahabu, fedha, shaba, chuma, mawe, miti, rangi ya zambarau, ya samawati, nyekundu na nguo za kitani safi. Tena ni hodari na anaweza kutia nakshi na kuchora michoro ya kila aina kufuatana na kielelezo chochote ambacho angepewa. Yeye atafanya kazi pamoja na mafundi wako, mafundi wa bwana wangu, Daudi, baba yako.

15 Sasa basi, bwana wangu, vitu hivyo ulivyosema: Ngano, shayiri, mafuta na divai, tafadhali uvitume kwa watumishi wako,

16 nasi tutapasua mbao kadiri ya mahitaji yako kutoka huko Lebanoni; kisha tutazifunga pamoja zielee majini mpaka Yopa. Kutoka huko utazipeleka Yerusalemu.”

17 Mfalme Solomoni aliamuru sensa ifanywe ya wageni wote walioishi katika nchi ya Israeli. Sensa hii ni kama ile aliyoifanya Daudi, baba yake. Kulikuwa na wageni wapatao 153,600.

18 Kati yao, 70,000 aliwapa kazi ya upagazi, 80,000 wakawa wachonga mawe milimani, na 3,600 wakawa wasimamizi ili wawahimize watu kufanya kazi.

3

1 Kisha Solomoni alianza kujenga nyumba ya Mwenyezi-Mungu katika Yerusalemu juu ya mlima Moria ambapo Mwenyezi-Mungu alimtokea Daudi baba yake, mahali ambapo Daudi alikuwa amepachagua, kwenye kiwanja cha kupuria cha Ornani Myebusi.

2 Mfalme Solomoni alianza ujenzi wa hekalu mnamo mwezi wa pili wa mwaka wa nne wa utawala wake.

3 Vipimo alivyotumia Solomoni katika ujenzi wa nyumba ya Mungu, vilikuwa kadiri ya vipimo vya awali, urefu mita 27 na upana mita 9.

4 Chumba cha sehemu ya kuingilia kilikuwa na urefu wa mita 9, sawa na upana wa nyumba hiyo, na kimo chake mita 54. Kuta zake zilifunikwa kwa dhahabu safi upande wa ndani.

5 Ukumbi ulizungushiwa mbao za miberoshi na kufunikwa kwa dhahabu safi na kuchorwa mifano ya miti ya mitende na minyororo.

6 Mfalme Solomoni aliipamba nyumba ya Mwenyezi-Mungu kwa mawe mazuri ya thamani. Dhahabu aliyotumia ilitoka nchi ya Parvaimu.

7 Aliifunika nyumba yote kwa dhahabu: Boriti zake, vizingiti vyake, kuta zake na milango yake. Kutani palichongwa viumbe wenye mabawa.

8 Tena, alipatengeneza mahali patakatifu sana. Urefu wake ulikuwa mita 9, sawasawa na upana wake ambao pia ulikuwa mita 9. Alitumia zaidi ya tani 20 za dhahabu kukifunika chumba hicho.

9 Misumari aliyoitumia ilikuwa ya uzani wa gramu 570 za dhahabu. Pia alivifunika vyumba vyote vya ghorofani kwa dhahabu.

10 Alitengeneza sanamu mbili za viumbe wenye mabawa kwa mbao, akazifunika kwa dhahabu na kuziweka mahali patakatifu sana.

11 Kila kiumbe kilikuwa na mabawa mawili yenye urefu wa mita 4.4 jumla, mita 2.25 kila bawa. Bawa mojawapo liligusa ukuta upande mmoja wa chumba na la pili liligusana na la kiumbe wa pili.

12 Kadhalika bawa moja la kiumbe wa pili liligusa ukuta upande mwingine wa chumba na la pili likagusana na la kiumbe wa kwanza katikati ya chumba.

13 Urefu wa mabawa mawili ya viumbe hawa ni mita 4.5. Yalisimama sambamba, nyuso za viumbe wenye mabawa zikielekea ukumbini.

14 Alitengeneza pazia kwa kitambaa cha kitani safi, cha rangi ya samawati, ya zambarau na nyekundu. Alilinakshi kwa michoro ya viumbe wenye mabawa.

15 Mfalme Solomoni alitengeneza nguzo mbili za shaba, kila moja yenye urefu wa mita 15.5, akaziweka mbele ya nyumba. Kila nguzo ilikuwa na taji juu yake yenye urefu wa mita 2.2.

16 Alitengeneza namna ya mapambo ya mikufu juu ya vichwa vya nguzo hizo, akachonga pia michoro ya makomamaga 100 juu yake.

17 Alizisimamisha nguzo hizo kwenye sebule ya hekalu, moja upande wa kusini, na nyingine upande wa kaskazini; ile ya upande wa kusini aliita Yakini, na ya upande wa kaskazini akaiita Boazi.

4

1 Mfalme Solomoni alitengeneza madhabahu ya shaba ya mraba mita 9 kwa mita 9, na kimo chake mita 4.5.

2 Kisha, alitengeneza tangi la maji la mviringo, lenye upana wa mita 4.5 kutoka ukingo hadi ukingo, kina cha mita 2.25, na mzingo wa mita 13.5.

3 Chini ya ukingo kulizunguka hilo tangi, kulikuwa na safu mbili za mapambo ya mafahali, safu moja juu ya safu nyingine; mapambo hayo yalifyatuliwa pamoja na sehemu nyingine za hilo tangi.

4 Nalo tangi lilikuwa limewekwa juu ya sanamu za mafahali kumi na wawili, tatu zikielekea kaskazini, tatu magharibi, tatu kusini na nyingine tatu mashariki.

5 Unene wa ukingo wake ulikuwa sentimita 7.5. Ukingo wake ulikuwa kama ukingo wa kikombe, na kama ua la yungiyungi. Tangi hilo liliweza kuchukua kiasi cha lita 60,000 za maji.

6 Alitengeneza pia birika kumi za kuoshea vitu vilivyotumika katika tambiko za kuteketezwa. Tano kati ya bakuli hizo aliziweka kusini na tano upande wa kaskazini. Tangi lilitumiwa na makuhani kunawia.

7 Alitengeneza vinara kumi vya dhahabu kama ilivyoagizwa, akaviweka ukumbini mwa hekalu; vitano upande wa kusini, na vitano upande wa kaskazini.

8 Alitengeneza pia meza kumi, nazo akaziweka ukumbini mwa hekalu. Kisha alitengeneza birika 100 za dhahabu.

9 Alitengeneza ua wa ndani wa makuhani na mwingine mkubwa wa nje, na milango ya ua ambayo aliifunika kwa shaba;

10 na lile tangi akaliweka kwenye pembe ya kusini-mashariki ya nyumba.

11 Huramu alitengeneza vyungu, sepetu na mabirika. Basi Huramu akamaliza kazi aliyomfanyia mfalme Solomoni kuhusu nyumba ya Mungu:

12 Nguzo mbili, mabakuli, taji mbili juu ya nguzo, na nyavu mbili kwa ajili ya kufunika mabakuli ya taji zilizowekwa juu ya nguzo;

13 pia mifano ya makomamanga 400 kwa ajili ya nyavu hizo mbili, safu mbilimbili za makomamanga kwa kila wavu, ili kupamba mabakuli yale mawili ya taji zilizokuwa juu ya kila nguzo.

14 Hali kadhalika alitengeneza birika juu ya magari,

15 na tangi lile moja, na sanamu za mafahali kumi na mawili chini ya hilo tangi.

16 Halafu masufuria, sepetu na nyuma na vyombo vingine vyote vya nyumba ya Mwenyezi-Mungu ambavyo Huramu-abi alimtengenezea mfalme Solomoni, vilikuwa vya shaba iliyongarishwa.

17 Vitu hivyo vyote mfalme alivitengeneza katika uwanda wa Yordani, sehemu ya udongo wa mfinyanzi iliyokuwa kati ya Sukothi na Sereda.

18 Uzani wa shaba iliyotumika kutengenezea vyombo hivi haukujulikana kwa maana Solomoni alitengeneza vyombo vingi sana.

19 Solomoni alitengeneza vitu vyote vilivyokuwa katika nyumba ya Mungu: Madhabahu ya dhahabu na meza za mikate ya kuwekwa mbele ya Mungu;

20 vinara na taa za dhahabu safi za kuangazia mahali pale patakatifu sana, kama ilivyoamriwa;

21 maua, taa na koleo, vyote vikiwa vya dhahabu safi kabisa;

22 mikasi na mabirika, visahani vya ubani na vyetezo vya kubebea moto, vyote vya dhahabu safi. Pete za hekalu za milango ya mahali pale patakatifu sana, na za milango mingine ya ukumbi, zote zilitengenezwa kwa dhahabu.

5

1 Hivyo, Solomoni akamaliza kazi zote zilizohusu nyumba ya Mwenyezi-Mungu. Kisha Solomoni akaleta mali yote Daudi baba yake aliyokuwa ameiweka wakfu, yaani: Fedha, dhahabu na vyombo; akaiweka katika hazina za nyumba ya Mungu.

2 Basi mfalme Solomoni akawakutanisha Yerusalemu wazee na viongozi wote wa makabila na wa koo za Israeli ili waliondoe sanduku la agano la Mwenyezi-Mungu kutoka katika mji wa Daudi, yaani Siyoni.

3 Ndipo wote walipokutana mbele ya mfalme katika sikukuu ya mwezi wa saba.

4 Baada ya wazee wote wa Israeli kuwasili, Walawi walilibeba sanduku la agano,

5 Walawi na makuhani walilihamisha sanduku la agano na hema la mkutano na vyombo vitakatifu vyote vilivyokuwa humo hemani.

6 Mfalme Solomoni na mkutano wa Israeli wakakusanyika mbele ya sanduku la agano nao wakatoa sadaka za ng'ombe na kondoo wasiohesabika.

7 Kisha makuhani wakaliingiza sanduku la agano la Mwenyezi-Mungu mahali pake, katika chumba cha ndani cha nyumba, mahali patakatifu sana, chini ya mabawa ya wale viumbe.

8 Hao viumbe wenye mabawa walitandaza mabawa yao juu ya mahali lilipowekwa sanduku, kwa hiyo sanduku na mipiko yake ya kulibebea vilikuwa chini ya mabawa.

9 Kwa kuwa mipiko hiyo ilikuwa mirefu sana, ncha zake ziliweza kuonekana kutoka mahali patakatifu mbele ya chumba cha ndani, lakini haikuweza kuonekana kutoka upande wa nje. Mipiko hiyo ingali mahali hapo hata leo.

10 Hakukuwa na kitu ndani ya sanduku la agano, ila vile vibao viwili vya mawe ambavyo Mose aliviweka humo kule Horebu, mahali Mwenyezi-Mungu alipofanya agano na watu wa Israeli, walipotoka Misri.

11 Ikawa makuhani walipotoka pale mahali patakatifu, (kwa sababu makuhani wote waliokuwapo bila kujali makundi yao, walikuwa wamejitakasa.),

12 Walawi wote waimbaji, wakiwamo Asafu, Hemani, na Yeduthuni, pamoja na Walawi wengine wa koo zao, wakiwa wamejivalia nguo zao za kitani safi huku wamebeba matoazi, vinanda na vinubi, walisimama upande wa mashariki wa madhabahu. Makuhani 120 wapiga tarumbeta walikuwa pamoja nao.

13 Waimbaji, huku wakifuatiwa na sauti linganifu za tarumbeta, matoazi na vyombo vingine vya muziki, walimsifu Mwenyezi-Mungu wakiimba: “Maana yeye ni mwema, na fadhili zake zadumu milele.” Wakati huo nyumba ya Mwenyezi-Mungu ilijazwa wingu.

14 Nao makuhani walishindwa kuhudumu humo kwa sababu ya wingu hilo, maana utukufu wa Mwenyezi-Mungu uliijaza nyumba ya Mungu.

6

1 Ndipo Solomoni akasema, “Mwenyezi-Mungu alisema ya kwamba atakaa katika giza nene.

2 Hakika nimekujengea nyumba tukufu, mahali pa makao yako ya milele.”

3 Kisha Solomoni akaigeukia jumuiya yote ya watu wa Israeli wakiwa wamesimama, akawabariki.

4 Akasema, “Atukuzwe Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, kwani kwa nguvu yake ameitimiza ahadi yake aliyoitoa kwa baba yangu Daudi akisema,

5 ‘Tangu niwaondoe watu wangu kutoka nchi ya Misri, sikuchagua mji wowote katika makabila ya Israeli ili nijengewe nyumba nitakamoabudiwa; na sikumchagua mtu yeyote awe mkuu wa watu wangu Israeli.

6 Nimeuchagua mji wa Yerusalemu uwe mji ambamo nitaabudiwa, na nimemchagua Daudi awatawale watu wangu Israeli.’

7 “Kwa hiyo, baba yangu Daudi alikusudia kujenga nyumba atakamoabudiwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli.

8 Lakini Mwenyezi-Mungu alimwambia baba yangu Daudi, ‘Ni vyema kwamba ulikusudia moyoni mwako kunijengea nyumba.

9 Hata hivyo, si wewe utakayejenga hiyo nyumba, ila mwanao utakayemzaa ndiye atakayenijengea hiyo nyumba.’”

10 “Na sasa Mwenyezi-Mungu ametimiza ahadi yake, kwani nimekuwa mfalme mahali pa baba yangu Daudi, na kukikalia kiti cha enzi cha Israeli kama Mwenyezi-Mungu alivyoahidi; pia nimejenga nyumba ya kumwabudia Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli.

11 Katika nyumba hiyo nimeliweka sanduku la agano, ambalo ndani yake mna agano la Mwenyezi-Mungu alilofanya na watu wa Israeli.”

12 Kisha, Solomoni alisimama mbele ya madhabahu ya Mwenyezi-Mungu halafu mbele ya jumuiya yote ya watu wa Israeli, aliinua mikono yake juu.

13 Solomoni alikuwa ametengeneza jukwaa la shaba ambalo aliliweka katikati ya ua. Urefu na upana wake ulikuwa mita mbili na robo, na kimo chake mita moja na robo. Alipanda jukwaani na kupiga magoti mbele ya jumuiya yote ya Israeli, akainua mikono yake kuelekea mbinguni.

14 Aliomba akisema, “Ee, Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, hakuna Mungu mwingine kama wewe, mbinguni ama duniani. Wewe ni mwaminifu, kwani umetimiza agano lako na kuwaonesha fadhili zako watumishi wako wanaoishi wakikutii kwa moyo wao wote.

15 Umetimiza ahadi uliyotoa kwa mtumishi wako baba yangu Daudi; naam, yale uliyonena umeyatimiza leo kwa uwezo wako mwenyewe.

16 “Kwa hiyo sasa, Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, ninakuomba pia utimize ile ahadi uliyomwahidi mtumishi wako Daudi baba yangu, ukisema, ‘Siku zote utakuwa na mzawa wa kuketi katika kiti cha enzi cha Israeli, iwapo wazawa wako watafuata kwa uangalifu sheria yangu kama wewe ulivyofanya mbele yangu.’

17 Sasa, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, nakusihi utimize yote uliyomwahidi mtumishi wako Daudi.

18 “Lakini, ee Mungu kweli utakaa humu duniani na binadamu? Hata mbingu zenyewe, wala mbingu za mbingu za juu sana hazikutoshi, itakutoshaje nyumba hii ambayo nimeijenga?

19 Hata hivyo, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu, mimi mtumishi wako, nakuomba unisikilize na kunitimizia ombi langu ninalokuomba leo.

20 Ichunge nyumba hii mchana na usiku, mahali ambapo umechagua watu wako waliabudu jina lako. Unisikie mimi mtumishi wako ninapokuja mahali hapa kuomba.

21 Sikia maombi yangu mimi mtumishi wako na ya watu wako Israeli wanapoomba wakielekea mahali hapa. Usikie maombi kutoka huko mbinguni na ukisha sikia, utusamehe.

22 “Mtu akimkosea mwenzake, naye akaletwa apate kuapa mbele ya madhabahu yako katika nyumba hii, na akiapa tafadhali

23 wewe usikie kutoka huko mbinguni, uchukue hatua na kuwahukumu watumishi wako. Aliye na hatia umwadhibu kadiri ya makosa yake; asiye na hatia umwachilie na kumpatia tuzo kadiri ya uadilifu wake.

24 “Wakati watu wako Israeli watakaposhindwa na maadui zao, kwa sababu ya dhambi walizotenda dhidi yako, nao wakitubu kwako na kukiri jina lako, wakiomba msamaha wako kwa unyenyekevu katika nyumba hii,

25 basi, usikie kutoka huko mbinguni. Usamehe dhambi zao na uwarudishe katika nchi uliyowapa wao na babu zao.

26 “Mvua isiponyesha kwa sababu wametenda dhambi dhidi yako, wakiomba wakielekea mahali hapa na kulikiri jina lako, pia wakiziacha dhambi zao, tafadhali

27 uwasikie kutoka huko mbinguni, na usamehe dhambi zao watumishi wako watu wako Waisraeli, huku ukiwafundisha kufuata njia nyofu, ukanyeshe mvua katika nchi yako hii ambayo uliwapa watu wako iwe mali yao.

28 “Iwapo kuna njaa nchini au tauni, ukame, ugonjwa wa mimea, nzige au viwavi, au ikiwa watu wako wamezingirwa na maadui zao katika mji wao wowote ule; ikiwa kuna pigo lolote au ugonjwa wowote,

29 tafadhali usikie maombi yoyote yatakayoombwa na mtu yeyote au watu wako wote wa Israeli, kila mtu akijua taabu yake na huzuni yake akikuomba huku akinyosha mikono yake kuelekea nyumba hii.

30 Basi usikie kutoka kwako mbinguni, utoe msamaha, pia umtendee kila mtu kadiri anavyostahili, kwani ni wewe tu ujuaye mawazo ya mioyo ya wanadamu wote.

31 Hivyo watakutii na kuenenda katika njia zako wakati wote wanapoishi katika nchi uliyowapa babu zetu.

32 “Vivyo hivyo wakati mgeni asiye mmoja wa watu wako Israeli atakuja kutoka nchi ya mbali kwa ajili ya jina lako kuu, na kwa sababu ya nguvu na ulinzi wako, kuomba katika nyumba hii,

33 nakusihi umsikie toka huko kwako mbinguni, na umjalie huyo mgeni yote atakayokuomba kusudi watu wote ulimwenguni wapate kujua jina lako na kukutii kama wafanyavyo watu wako Israeli na wapate kufahamu kwamba nyumba hii ambayo nimeijenga inajulikana kwa jina lako.

34 “Watu wako wakienda vitani kupigana na maadui zao kokote kule utakakowapeleka, nao wakikuomba wakielekea mji huu uliouchagua na nyumba ambayo nimeijenga kwa ajili ya jina lako,

35 nakusihi usikie sala yao na maombi yao ukiwa huko mbinguni na uwapatie ushindi vitani.

36 “Ikiwa watatenda dhambi dhidi yako, maana hakuna mtu asiyetenda dhambi, na ukiwakasirikia na kuwaacha washindwe na adui, hata wapelekwe mateka mpaka nchi ya mbali au ya karibu;

37 kama watakapokuwa huko uhamishoni watajirudi kwa roho yao yote na kwa moyo wao wote na kutubu na kukuomba msamaha, wakisema, ‘Tumetenda dhambi; tumepotoka na kufanya maovu’;

38 pia kama watatubu kwa moyo wao wote na kwa roho yao yote wakati watakapokuwa katika nchi ya uhamisho, na kama watakuomba wakielekea nchi yao ambayo uliwapatia babu zao, mji huu ambao uliuchagua na nyumba hii ambayo nimeijenga kwa ajili ya jina lako;

39 basi, nakusihi usikie huko mbinguni uliko sala yao na maombi yao na uwapatie haki zao, uwasamehe watu wako ambao wametenda dhambi dhidi yako.

40 “Sasa ee Mungu wangu, tuangalie na upokee maombi tutakayoomba mahali hapa.

41 Sasa inuka ee Bwana Mungu, uingie mahali pako pa kupumzika wewe pamoja na sanduku la agano la nguvu zako. Makuhani wako ee Bwana Mungu, wapate wokovu, na watakatifu wako wafurahie wema wako.

42 Ee Bwana Mungu, usimpige kisogo masiha wako. Kumbuka fadhili zako kwa mtumishi wako Daudi.”

7

1 Solomoni alipomaliza sala yake, moto ulishuka kutoka mbinguni na kuchoma sadaka na tambiko za kuteketeza zilizotolewa, kisha utukufu wa Mwenyezi-Mungu ukaijaza nyumba.

2 Kwa kuwa utukufu wa Mwenyezi-Mungu ulijaa nyumba ya Mwenyezi-Mungu, makuhani hawakuweza kuingia humo.

3 Waisraeli wote walipoona moto ukishuka kutoka mbinguni na utukufu wa Mwenyezi-Mungu ulijaa katika nyumba walisujudu nyuso zao zikifika mpaka sakafuni, wakamwabudu na kumshukuru Mwenyezi-Mungu wakisema, “Kwa kuwa ni mwema, fadhili zake zadumu milele.”

4 Kisha mfalme Solomoni na watu wote walimtolea Mwenyezi-Mungu tambiko.

5 Naye Solomoni alimtolea Bwana ng'ombe 22,000 na kondoo 120,000. Hivyo ndivyo Solomoni na watu wote walivyoiweka wakfu nyumba ya Mungu.

6 Makuhani walisimama mahali maalumu walipoagizwa kusimama, nao Walawi walisimama wakiwa na vyombo vya Mwenyezi-Mungu vya muziki mfalme Daudi alivyovitengeneza kwa ajili ya kutoa shukrani kwa Mwenyezi-Mungu. Waliimba, “Kwa kuwa fadhili zake zadumu milele,” Daudi alivyowaagiza. Makuhani walipiga tarumbeta hali Waisraeli wote walikuwa wamesimama.

7 Basi, mfalme Solomoni akaiweka wakfu sehemu ya katikati ya ua uliokuwa mbele ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu, kwani hapo ndipo alipotolea sadaka za kuteketezwa na mafuta ya sadaka za amani, kwa sababu ile madhabahu ya shaba haikutosha kwa sadaka hizo zote.

8 Naye Solomoni kwa muda wa siku saba alifanya sikukuu pamoja na kusanyiko kubwa la watu wote wa Israeli waliotoka kiingilio cha Hamathi mpaka mto wa Misri.

9 Siku ya nane, walikusanyika wakafanya ibada maalumu baada ya muda wa siku saba walizotumia kuitakasa meza ya matoleo ya sadaka, na siku saba nyingine za sikukuu.

10 Siku iliyofuata ambayo ilikuwa siku ya ishirini na tatu ya mwezi wa saba, Solomoni aliwaaga watu waende kwao, wakishangilia na kufurahi moyoni kwa sababu ya wema ambao Mwenyezi-Mungu aliowajalia Daudi, Solomoni na watu wake Israeli.

11 Basi, mfalme Solomoni alimaliza kuijenga nyumba ya Mwenyezi-Mungu na ikulu na alifaulu kuyatekeleza yale yote aliyokusudia kuifanyia nyumba ya Mwenyezi-Mungu na ikulu.

12 Kisha Mwenyezi-Mungu alimtokea usiku, akamwambia, “Nimesikia sala yako na nimepachagua mahali hapa pawe nyumba yangu ya kunitolea tambiko.

13 Nikiwanyima mvua ama nikiwaletea nzige wale mimea yao au wakipatwa na maradhi mabaya

14 kama watu hao wangu wakijinyenyekesha, wakasali, wakanitafuta na kuacha njia zao mbaya, basi, mimi nitawasikiliza kutoka juu mbinguni; nitawasamehe dhambi yao na kuistawisha nchi yao.

15 Sasa nitalichunga hekalu hili na kusikiliza maombi yatakayofanyika hapa,

16 kwa maana nimeitakasa nyumba hii ili watu waliabudu jina langu hapa milele. Nitailinda na kuipenda daima.

17 Nawe, kama ukinitumikia kwa uaminifu kama Daudi baba yako alivyofanya, ukitenda yote niliyokuamuru na kutii maongozi yangu na maagizo yangu,

18 basi, mimi nitakiimarisha kiti chako cha ufalme kama nilivyofanya agano na Daudi baba yako nikisema, ‘Hutakosa mtu wa kutawala Israeli.’

19 Lakini mkiacha kunifuata, mkayaasi maongozi yangu na amri nilizowapa, na kwenda kutumikia miungu mingine na kuiabudu,

20 kwa sababu hiyo mimi nitawangoeni kutoka nchi hii ambayo nimewapa. Kadhalika na nyumba hii ambayo nimeiweka wakfu kwa ajili ya jina langu nitaitupilia mbali nami, na kuifanya kitu cha kupuuzwa na kudharauliwa miongoni mwa mataifa yote.

21 Na juu ya nyumba hii ambayo nimetukuka, kila apitaye karibu atashtuka na kuuliza, ‘Kwa nini Mwenyezi-Mungu amefanya hivyo kwa nchi hii na kwa nyumba hii?’

22 Watu wengine watajibu, ‘Ni kwa sababu walimwacha Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zao aliyewatoa nchini Misri; wakashikamana na miungu mingine, wakaiabudu na kuitumikia. Kwa hiyo Mwenyezi-Mungu amewaletea maafa haya yote.’”

8

1 Miaka ishirini, ambayo Solomoni aliijenga nyumba ya Mwenyezi-Mungu na ikulu ilipokwisha kupita,

2 Solomoni aliijenga upya miji aliyopewa na Huramu, halafu akawapa Waisraeli miji hiyo waishi humo.

3 Baadaye Solomoni alielekea Hamath-zoba na kuuteka,

4 na kuujenga mji wa Tadmori nyikani. Aliijenga upya miji ya ghala iliyokuwa huko Hamathi.

5 Kadhalika, Solomoni alijenga miji ifuatayo: Beth-horoni wa juu, na Beth-horoni wa chini, miji yenye ngome, kuta, malango na makomeo,

6 mji wa Baalathi, na miji yake yote ya ghala, magari yake ya kukokotwa na ya wapandafarasi wake, na chochote alichotaka kujenga katika Yerusalemu, Lebanoni au kwingineko katika ufalme wake.

7 Watu wengine wote waliobaki miongoni mwa Wahiti, Waamori, Waperizi, Wahivi na Wayebusi, yaani wote ambao hawakuwa Waisraeli,

8 pia wazawa wao ambao Waisraeli hawakuwaangamiza, Solomoni aliwafanyiza kazi za kulazimishwa, na hivi ndivyo wanavyofanya hata sasa.

9 Lakini kati ya watu wa Israeli, Solomoni hakumfanya mtu yeyote kuwa mtumwa kwa ajili ya kazi yake; wao walikuwa askari, makamanda wa maofisa wake, makamanda wa magari yake ya kukokotwa na wapandafarasi wake.

10 Ifuatayo ndiyo jumla ya maofisa wakuu wa mfalme Solomoni: Walikuwa 250, waliokuwa na mamlaka juu ya watu.

11 Solomoni alimhamisha binti Farao mfalme wa Misri, kutoka mji wa Daudi, akampeleka kwenye nyumba aliyomjengea. Alisema, “Mke wangu hataishi katika nyumba ya Daudi mfalme wa Israeli, kwa maana mahali pote ambapo sanduku la Mwenyezi-Mungu limekuwa, ni patakatifu.”

12 Solomoni alimtolea Mwenyezi-Mungu tambiko za kuteketeza juu ya madhabahu aliyokuwa amemjengea Mwenyezi-Mungu mbele ya ukumbi wa hekalu.

13 Alitoa tambiko hizo kadiri ilivyotakiwa na amri ya Mose kila siku takatifu, yaani siku za Sabato, sikukuu za mwezi mwandamo, na sikukuu tatu za kila mwaka – sikukuu ya mikate isiyotiwa chachu, sikukuu ya majuma na sikukuu ya vibanda.

14 Akifuata maagizo ya Daudi baba yake, alipanga zamu za kila siku za makuhani na za Walawi waliowasaidia makuhani kusifu na kuzitekeleza kazi zao. Kadhalika aliwapanga walinda malango katika makundi aliyoyaweka kulinda kila lango; maana ndivyo alivyoamuru Daudi, mtu wa Mungu.

15 Nao hawakuyaacha maagizo mfalme aliyowaamuru makuhani na Walawi jambo lolote na kuhusu hazina.

16 Basi miradi yote ya Solomoni aliyofanya tangu jiwe la msingi wa nyumba ya Mwenyezi-Mungu lilipowekwa ilikamilika. Hivyo nyumba ya Mwenyezi-Mungu ilimalizika.

17 Kisha Solomoni alikwenda Esion-geberi na Elothi iliyo pwani mwa bahari, katika nchi ya Edomu.

18 Huramu alimpelekea merikebu zilizokuwa chini ya uongozi wa maofisa wake, pamoja na mabaharia stadi. Hao, pamoja na maofisa wa Solomoni, walisafiri hadi Ofiri, na kuchukua kutoka huko dhahabu, wakamletea mfalme Solomoni kiasi cha kilo 15,000.

9

1 Malkia wa Sheba aliposikia sifa za Solomoni, aliwasili Yerusalemu ili kumjaribu Solomoni kwa maswali magumu. Alifuatana na msafara wa watu, pamoja na ngamia waliobeba manukato, dhahabu nyingi sana na vito vya thamani. Na alipofika kwa Solomoni, alimwuliza maswali yote aliyokuwa nayo moyoni mwake.

2 Solomoni aliyajibu maswali yote; hapakuwapo na jambo lolote aliloshindwa kumweleza.

3 Malkia wa Sheba alipoiona hekima ya Solomoni na nyumba aliyokuwa ameijenga,

4 tena alipotazama chakula kilichoandaliwa mezani pwake na kuona jinsi maofisa wake walivyoketi mezani na huduma ya watumishi wake na jinsi walivyovalia; pia wanyweshaji wake na jinsi walivyovalia, tambiko za kuteketeza ambazo alizitoa katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu, alipoona hayo yote akashangaa sana.

5 Basi, akamwambia mfalme, “Yote niliyosikia nchini kwangu kuhusu kazi zako na hekima yako ni ya kweli!

6 Lakini sikuweza kuamini habari zao mpaka nilipofika na kujionea mwenyewe, na kumbe niliambiwa nusu tu; hekima yako na ufanisi wako ni zaidi ya yale niliyosikia.

7 Wana bahati wake zako! Wana bahati hawa watumishi wako ambao daima husimama mbele yako na kusikiliza hekima yako!

8 Na asifiwe Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, ambaye amependezwa nawe, akakuketisha juu ya kiti chake cha enzi, uwe mfalme kwa niaba yake Mwenyezi-Mungu, Mungu wako. Kwa sababu Mungu wako amewapenda Waisraeli na kuwaimarisha milele, amekuweka wewe uwe mfalme juu yao ili udumishe haki na uadilifu.”

9 Kisha akampa mfalme zaidi ya kilo 4,000 za dhahabu, na kiasi kikubwa cha manukato na vito vya thamani. Aina ya manukato ambayo huyo malkia wa Sheba alimpatia mfalme Solomoni, ilikuwa ya pekee.

10 Kadhalika, watumishi wa Huramu pamoja na watumishi wa Solomoni walioleta dhahabu kutoka Ofiri, walileta pia miti ya misandali na mawe ya thamani.

11 Solomoni alitumia miti hiyo kutengeneza madari ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu na ikulu, na pia kutengenezea vinubi na vinanda vya waimbaji. Mambo ya namna hiyo hayakuwa yameonekana kamwe katika nchi ya Yuda.

12 Naye mfalme Solomoni alimpatia malkia wa Sheba kila kitu alichotamani, chochote alichoomba mbali na vitu alivyomletea mfalme. Hatimaye malkia aliondoka akarudi katika nchi yake akiwa pamoja na watumishi wake.

13 Kila mwaka, Solomoni alipelekewa dhahabu kadiri ya kilo 23,000,

14 mbali na dhahabu aliyopokea kutoka kwa wafanyabiashara na wachuuzi. Wafalme wote wa Arabia na wakuu wa mikoa ya Israeli pia walimletea Solomoni fedha na dhahabu.

15 Mfalme Solomoni alitengeneza ngao kubwa 200; kila moja ilipakwa kadiri ya kilo saba za dhahabu iliyofuliwa.

16 Pia alitengeneza ngao ndogondogo 300, kila moja ilipakwa dhahabu ipatayo kilo tatu, halafu mfalme akaziweka katika jengo lililoitwa Nyumba ya Msitu wa Lebanoni.

17 Hali kadhalika mfalme alitengeneza kiti cha enzi kikubwa cha pembe, akakifunikiza dhahabu safi.

18 Kiti hicho kilikuwa na ngazi sita na kiti cha kuegemea miguu cha dhahabu, vyote hivyo vilikuwa vimeshikamanishwa na kiti hicho cha enzi; na kila upande kilikuwa na mahali pa kuegemeza mikono; pia kilikuwa na sanamu mbili za simba karibu na mahali hapo pa kuegemeza mikono.

19 Palikuwa na sanamu kumi na mbili za simba waliosimama mwishoni mwa kila ngazi. Kiti kama hicho kilikuwa hakijawahi kutengenezwa katika ufalme wowote ule.

20 Vikombe vyote vya mfalme Solomoni vilikuwa vya dhahabu, na vyombo vyote vilivyokuwa katika Nyumba ya Msitu wa Lebanoni vilikuwa vya dhahabu safi. Fedha haikuhesabiwa kuwa kitu cha thamani katika siku za Solomoni.

21 Solomoni alikuwa na merikebu zilizosafiri mpaka Tarshishi na watumishi wa Huramu, na kila baada ya miaka mitatu, merikebu hizo zilirudi zikimletea dhahabu, fedha, pembe, nyani na tausi.

22 Mfalme Solomoni aliwapita wafalme wote duniani kwa mali na kwa hekima.

23 Nao wafalme wa nchi zote walikuwa na hamu ya kumwendea Solomoni ili kusikiliza hekima yake ambayo Mungu alikuwa amemjalia.

24 Kila mmoja wao alimletea zawadi: Vyombo vya fedha na vya dhahabu, mavazi na silaha manukato, farasi na nyumbu. Zawadi hizi alizipokea kila mwaka.

25 Mfalme Solomoni akawa na vibanda 4,000 vya kuwekea farasi na magari, na askari wapandafarasi 12,000 ambao aliwaweka katika miji yenye vituo vya magari ya farasi na katika Yerusalemu.

26 Aliwatawala wafalme wote waliokuwako kuanzia mto Eufrate, hadi nchi ya Wafilisti na hadi mpakani na Misri.

27 Basi Solomoni alifanya fedha katika Yerusalemu kuwa kitu cha kawaida kama mawe katika Yerusalemu, na mbao za mierezi zilipatikana kwa wingi kama mikuyu iliyomo Shefela.

28 Solomoni aliletewa farasi walionunuliwa kutoka Misri na nchi nyinginezo.

29 Matendo mengine ya Solomoni, kutoka mwanzo hadi mwisho, yameandikwa katika kitabu cha “Historia ya Nabii Nathani,” katika “Unabii wa Ahiya wa Shilo,” na katika “Maono ya Ido” mwonaji, ambayo yahusu pia Yeroboamu mwana wa Nebati.

30 Solomoni alitawala nchi yote ya Israeli kwa miaka arubaini.

31 Hatimaye Solomoni alifariki dunia na kuzikwa katika mji wa Daudi baba yake. Rehoboamu, mwanawe, akatawala mahali pake.

10

1 Basi, Rehoboamu akaenda Shekemu, ambako Waisraeli wote walikuwa wamekusanyika ili kumtawaza awe mfalme.

2 Naye Yeroboamu mwana wa Nebati alipopata habari kuhusu tendo hilo (wakati huo alikuwa bado anaishi Misri alikokwenda alipomkimbia Solomoni) alitoka Misri.

3 Lakini Waisraeli walituma ujumbe na kumwita. Kisha, yeye pamoja na Waisraeli wote walimwendea Rehoboamu na kumwambia,

4 “Baba yako alitutwika mzigo mzito. Basi, utupunguzie mzigo huo, nasi tutakutumikia.”

5 Rehoboamu akawajibu, “Rudini kwangu baada ya siku tatu.” Basi wakaondoka.

6 Baadaye, Rehoboamu alitaka kujua maoni ya wazee ambao walikuwa washauri wa Solomoni, baba yake, alipokuwa angali hai, akawauliza, “Je, mnanishauri niwape jibu gani watu hawa?”

7 Wazee hao wakamjibu, “Ukiwahurumia watu hawa, ukiwafurahisha na kusema nao maneno mazuri, hapo watakuwa watumishi wako daima.”

8 Lakini Rehoboamu alipuuza shauri la wazee na badala yake akashauriana na vijana wa rika lake ambao walikuwa washauri wake.

9 Basi, akawauliza, “Nyinyi mnatoa shauri gani ili tuweze kuwajibu watu hawa walioniambia, ‘Punguza mzigo ambao baba yako alitutwika?’”

10 Hao vijana wakamjibu, “Watu hao waliokuambia ‘Baba yako alitutwika mzigo mzito, lakini wewe utupunguzie,’ wewe waambie hivi: ‘Kidole changu kidogo cha mwisho ni kinene zaidi kuliko kiuno cha baba yangu.

11 Mzigo wa baba yangu ulikuwa mzito, lakini wangu utakuwa mzito zaidi. Baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, lakini mimi nitawapiga kwa mijeledi yenye miiba.’”

12 Basi katika siku ya tatu Yeroboamu pamoja na watu wote wakarudi kwa Rehoboamu kama alivyokuwa amewaagiza.

13 Naye mfalme Rehoboamu akawajibu kwa ukali, akapuuza shauri la wazee,

14 na kufuata shauri la vijana wenzake. Basi akasema, “Baba yangu aliwatwika mzigo mzito, lakini mimi nitaufanya kuwa mzito zaidi. Baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, lakini mimi nitawapiga kwa mijeledi yenye miiba”

15 Hivyo mfalme hakuwajali watu kwa sababu jambo hili lilisababishwa na Mungu ili Mwenyezi-Mungu atimize neno lake alilomwambia Yeroboamu, mwana wa Nebati kwa njia ya Ahiya wa Shilo.

16 Lakini watu wote wa Israeli walipoona kwamba mfalme hakuwajali walimwambia, “Tuna sehemu gani kwa Daudi? Hatuna urithi katika mwana wa Yese. Kila mmoja na arudi nyumbani kwake, enyi watu wa Israeli. Itunze nyumba yako mwenyewe, ee Daudi.” Hivyo watu wote wa Israeli wakarudi makwao.

17 Lakini Rehoboamu alitawala watu wa Israeli waliokaa katika miji ya Yuda.

18 Kisha mfalme Rehoboamu alipomtuma Hadoramu aliyekuwa mnyapara mkuu wa kazi za kulazimishwa, watu wa Israeli walimpiga mawe, wakamuua. Ndipo Rehoboamu alipopanda gari lake haraka akakimbilia Yerusalemu.

19 Hivyo, watu wa Israeli wamekuwa katika hali ya maasi dhidi ya utawala wa ukoo wa Daudi mpaka leo.

11

1 Rehoboamu alipofika Yerusalemu, alikusanya askari stadi180,000 wa makabila ya Yuda na Benyamini, apate kupigana na Israeli, ili ajirudishie huo ufalme.

2 Lakini ujumbe wa Mungu ulimjia Shemaya mtu wa Mungu, kusema:

3 “Mwambie Rehoboamu mwana wa Solomoni, mfalme wa Yuda na Waisraeli wote katika Yuda na Benyamini ya kwamba

4 mimi Bwana nasema, ‘Msiende wala msipigane na ndugu zenu. Rudini kila mtu nyumbani kwake, maana hayo yaliyotokea ni kama nilivyopanga.’” Basi wakatii ujumbe wa Mwenyezi-Mungu, wakarudi nyumbani, wala hawakwenda kupigana na Yeroboamu.

5 Rehoboamu alikaa Yerusalemu na akajenga ngome na kuiimarisha miji ifuatayo iliyokuwa nchini Yuda:

6 Bethlehemu, Etamu, Tekoa,

7 Beth-suri, Soko, Adulamu,

8 Gathi, Maresha, Zifu,

9 Adoraimu, Lakishi, Azeka,

10 Sora, Ayaloni na Hebroni. Miji hiyo yenye ngome imo Yuda na Benyamini.

11 Aliziimarisha ngome hizo na humo ndani akaweka makamanda na maghala ya vyakula, mafuta na divai.

12 Ndani ya kila mji, aliweka ngao na mikuki, na kuifanya miji hiyo kuwa imara sana. Yuda na Benyamini zikawa chini ya mamlaka yake.

13 Makuhani na Walawi wote waliokuwa wanaishi kote nchini Israeli, walimwendea kutoka maeneo yao.

14 Walawi waliyaacha malisho yao, na maeneo yao mengine kwa sababu Yeroboamu na wanawe waliwakataza kumtumikia Mwenyezi-Mungu kama makuhani wa Mwenyezi-Mungu.

15 Yeroboamu alijichagulia makuhani wake mwenyewe wa kuhudumu mahali pa juu pa kuabudia miungu na yale majini na sanamu za ndama alizojitengenezea.

16 Watu wote ambao walikuwa wamenuia kwa moyo wa dhati kumwabudu Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, kutoka katika makabila yote ya Israeli, waliandamana na Walawi hadi Yerusalemu ili wapate kumtolea tambiko Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zao.

17 Hivyo, waliuimarisha ufalme wa Yuda, na kwa muda wa miaka mitatu, wakauunga mkono utawala wa Rehoboamu mwanawe Solomoni, nao ukawa imara na wakaishi katika hali ileile waliyoishi wakati walipokuwa chini ya utawala wa mfalme Daudi na mfalme Solomoni.

18 Rehoboamu alioa mke, jina lake Mahalathi binti Yeremothi mwana wa Daudi. Mama yake alikuwa Abihaili binti Eliabu, mwana wa Yese.

19 Naye alimzalia wana watatu: Yeushi, Shemaria na Zahamu.

20 Baadaye, alimwoa Maaka binti Absalomu, naye akamzalia Abiya, Atai, Ziza na Shelomithi.

21 Rehoboamu alioa wake kumi na wanane na masuria sitini, akazaa watoto wa kiume ishirini na wanne na mabinti sitini. Miongoni mwa wake zake wote na masuria wake, alimpenda Maaka binti Absalomu zaidi.

22 Hivyo akamchagua Abiya, mwana wa Maaka, awe mkuu kati ya ndugu zake, kwani alinuia kumfanya awe mfalme.

23 Rehoboamu alifanya jambo la busara, akawatawanya baadhi ya wanawe katika nchi yote ya Yuda na Benyamini akiwaweka katika miji yote yenye ngome. Wakiwa humo, aliwapa vyakula tele na pia akawaoza wake wengi.

12

1 Ikawa utawala wa Rehoboamu ulipokwisha imarika na kuwa na nguvu, yeye pamoja na watu wake wote waliacha kutii sheria ya Mwenyezi-Mungu.

2 Katika mwaka wa tano wa utawala wake, kwa sababu hawakumtii Mwenyezi-Mungu, Shishaki, mfalme wa Misri aliushambulia Yerusalemu,

3 akiwa na magari 1,200, wapandafarasi 60,000, na askari wengi mno wasiohesabika, waliotoka Misri pamoja naye: Walibia, Wasukii na Waethiopia.

4 Aliiteka miji yenye ngome katika Yuda, akafika hadi Yerusalemu.

5 Kisha Nabii Shemaya alimwendea mfalme Rehoboamu na wakuu wa Yuda, waliokusanyika Yerusalemu ambapo walikimbilia ili kumwepuka Shishaki, akamwambia, “Mwenyezi-Mungu asema hivi, ‘Nyinyi mmeniacha mimi, kwa hiyo basi, nami nimewaacha nyinyi na kuwatia mikononi mwa Shishaki.’”

6 Ndipo wakuu wa Israeli na mfalme wakajinyenyekesha, wakasema, “Mwenyezi-Mungu ametenda sawa.”

7 Mwenyezi-Mungu alipoona ya kuwa wamejinyenyekesha, alizungumza tena na nabii Shemaya, akamwambia, “Wamejinyenyekesha, sitawaangamiza, bali nitawaokoa baada ya muda mfupi. Sitaushushia mji wa Yerusalemu ghadhabu yangu kuuharibu kwa mkono wa Shishaki,

8 lakini watamtumikia ili wapate kujua tofauti iliyopo kati ya kunitumikia mimi na kuwatumikia wafalme wa duniani.”

9 Basi, mfalme Shishaki wa Misri aliushambulia Yerusalemu, akaichukua hazina yote ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu na ya ikulu, pamoja na ngao za dhahabu alizozitengeneza mfalme Solomoni.

10 Badala ya ngao hizo, mfalme Rehoboamu alitengeneza ngao za shaba na kuziweka chini ya ulinzi wa wangojamlango wa ikulu.

11 Kila wakati mfalme alipokwenda katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu, walinzi waliiingia wakazibeba ngao hizo na baadaye wakazirudisha katika chumba cha ulinzi.

12 Alipojinyenyekesha, Mwenyezi-Mungu aliacha kumghadhibikia na hakumwangamiza kabisa. Zaidi ya hayo, hali ya nchi ya Yuda ilikuwa nzuri.

13 Hivyo mfalme Rehoboamu alijiimarisha zaidi katika Yerusalemu, akaitawala Yuda. Alikuwa na umri wa miaka arubaini na mmoja alipoanza kutawala Yuda. Naye alitawala kwa muda wa miaka kumi na saba katika Yerusalemu, mji ambao Mwenyezi-Mungu aliuchagua miongoni mwa makabila yote ya Israeli aabudiwe humo. Mama yake Rehoboamu aliitwa Naama, kutoka Amoni.

14 Rehoboamu alitenda maovu, kwa maana hakunuia kumtafuta Mwenyezi-Mungu kwa moyo.

15 Matendo yote ya mfalme Rehoboamu ya mwanzo mpaka ya mwisho na rekodi ya ukoo yameandikwa katika kitabu cha Kumbukumbu za nabii Shemaya, na Kumbukumbu za Ido Mwonaji. Wakati huu wote, kulikuwa na vita vya mfululizo kati ya Rehoboamu na Yeroboamu.

16 Hatimaye Rehoboamu alifariki na kuzikwa katika mji wa Daudi, na Abiya mwanawe, akatawala mahali pake.

13

1 Abiya alianza kutawala Yuda mnamo mwaka wa kumi na nane wa utawala wa mfalme Yeroboamu.

2 Alitawala kwa muda wa miaka mitatu akiwa Yerusalemu. Mama yake alikuwa Maaka binti Urieli wa Gibea. Kulitokea vita kati ya Abiya na Yeroboamu.

3 Abiya alijiandaa kupigana vita akiwa na jeshi la askari hodari 400,000, naye Yeroboamu akamkabili na jeshi lake la askari hodari 800,000.

4 Mfalme Abiya alisimama juu ya mlima Semaraimu, ulioko kati ya milima ya Efraimu, akamwambia Yeroboamu na watu wa Israeli, “Nisikilize ewe Yeroboamu na watu wote wa Israeli!

5 Je, hamjui kwamba Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, alimwahidi Daudi kwa kufanya naye agano lisilovunjika kuwa daima, wafalme wote wa Israeli watatoka katika uzao wake?

6 Lakini Yeroboamu mwana wa Nebati mtumishi wa Solomoni, mwana wa Daudi alimwasi bwana wake.

7 Baadaye, alijikusanyia kikundi cha mabaradhuli, watu wapumbavu wasiofaa kitu, nao wakamshawishi Rehoboamu mwana wa Solomoni, kutenda yale waliyotaka wao, naye hangeweza kuwazuia kwani wakati huo alikuwa bado kijana bila uzoefu mwingi.

8 “Sasa nyinyi mnadhani mnaweza kupinga ufalme wa Mwenyezi-Mungu aliopewa Daudi na uzao wake kwa sababu eti mnalo jeshi kubwa na sanamu za dhahabu za ndama, alizowatengenezea Yeroboamu kuwa miungu yenu!

9 Je, hamkuwafukuza makuhani wa Mwenyezi-Mungu, wana wa Aroni, kadhalika na Walawi, na kujifanyia makuhani wenu wenyewe kama wafanyavyo watu wa mataifa mengine? Yeyote ajaye kwenu kujiweka wakfu na ndama dume ama kondoo madume saba, huwa kuhani wa vitu ambavyo si miungu.

10 “Lakini kuhusu sisi, Mwenyezi-Mungu, ndiye Mungu wetu, wala hatujamwacha. Tena tunao makuhani wa uzao wa Aroni ambao wanamtumikia Mwenyezi-Mungu, nao husaidiwa na Walawi.

11 Kila siku asubuhi na jioni, makuhani humtolea sadaka za kuteketezwa nzima, na kumfukizia ubani wenye harufu nzuri, tena hupanga juu ya meza ya dhahabu safi, mikate ya kuwekwa mbele ya Mungu, na kukitunza kinara cha dhahabu na kuziwasha taa kila siku jioni. Sisi tunayafuata maagizo ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, lakini nyinyi mmemwacha.

12 Hebu tazameni, Mungu mwenyewe ndiye kiongozi wetu na makuhani wake wanazo tarumbeta zao tayari kuzipiga ili kutupa ishara ya kuanza vita dhidi yenu. Enyi watu wa Israeli, acheni kupigana vita dhidi ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zenu. Hamwezi kushinda!”

13 Lakini wakati huo, Yeroboamu alikuwa amekwisha tuma baadhi ya wanajeshi wake kulivamia jeshi la Yuda kutoka upande wa nyuma, hali wale wengine wamewakabili kutoka upande wa mbele.

14 Watu wa Yuda walipotazama nyuma, walishtuka kuona wamezingirwa; basi walimlilia Mwenyezi-Mungu, nao makuhani wakazipiga tarumbeta zao.

15 Ndipo wanajeshi wa Yuda wakapiga kelele ya vita, na walipofanya hivyo, Mungu alimshinda Yeroboamu na jeshi lake la watu wa Israeli mbele ya Abiya na watu wa Yuda.

16 Watu wa Israeli waliwakimbia watu wa Yuda naye Mungu akawatia mikononi mwao.

17 Abiya na jeshi lake aliwashambulia sana, akawashinda; akaua wanajeshi wa Israeli, laki tano waliokuwa baadhi ya wanajeshi hodari sana katika Israeli.

18 Kwa hiyo, watu wa Yuda walipata ushindi dhidi ya watu wa Israeli kwa sababu walimtegemea Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zao.

19 Abiya alimfukuza Yeroboamu, akamnyanganya baadhi ya miji yake: Betheli, Yeshana, Efroni pamoja na vijiji vilivyokuwa kandokando ya miji hiyo.

20 Yeroboamu hakuweza kupata nguvu tena wakati wa Abiya. Mwishowe Mwenyezi-Mungu alimpiga, naye akafa.

21 Lakini Abiya aliendelea kupata nguvu zaidi. Akaoa wanawake kumi na wanne, akapata watoto wa kiume ishirini na wawili na mabinti kumi na sita.

22 Matendo mengine ya Abiya, shughuli zake na maneno yake, yameandikwa katika kitabu cha “Historia ya Nabii Ido.”

14

1 Mwishowe, Abiya alifariki na kuzikwa katika mji wa Daudi na Asa mwanawe akatawala mahali pake. Wakati wa Asa, kulikuwa na amani nchini kwa muda wa miaka kumi.

2 Asa alitenda yaliyokuwa mazuri na mema mbele ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wake.

3 Aliondoa nchini madhabahu za kigeni na mahali pa kuabudia miungu mingine, akabomoa minara na kuzikatakata sanamu za Ashera.

4 Aliwaamuru watu wa Yuda wamtafute Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zao, na kuzitii sheria na amri.

5 Pia aliondoa mahali pote pa kuabudia miungu mingine na meza za kufukizia ubani kutoka katika miji yote ya Yuda; halafu ufalme wake ulikuwa na amani chini ya utawala wake.

6 Alijenga miji yenye ngome katika Yuda wakati huo wa amani, na kwa muda wa miaka kadhaa, hapakutokea vita kwa maana Mwenyezi-Mungu alimpa amani.

7 Naye akawaambia watu wa Yuda, “Na tuiimarishe miji kwa kuizungushia kuta na minara na malango yenye makomeo. Nchi bado imo mikononi mwetu kwa maana tumeyatenda mapenzi yake Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, naye ametupa amani pande zote.” Basi wakajenga, wakafanikiwa.

8 Mfalme Asa alikuwa na jeshi la askari 300,000 kutoka Yuda, wenye ngao na mikuki, na wengine 280,000 kutoka Benyamini, wenye ngao na pinde. Wote walikuwa watu mashujaa sana.

9 Zera, Mwethiopia aliishambulia nchi ya Yuda akiwa na jeshi la askari 1,000,000 na magari 300, akasonga mbele hadi Maresha.

10 Asa alitoka akaenda kupigana naye. Pande zote mbili zilijipanga katika bonde la Sefatha karibu na Maresha.

11 Hapo Asa akamlilia Mwenyezi-Mungu, Mungu wake, akisema, “Ee Mwenyezi-Mungu, hakuna mwingine kama wewe, mwenye uwezo wa kulisaidia jeshi liwe dhaifu au lenye nguvu. Tusaidie, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, kwa kuwa sisi tunakutegemea wewe, na kwa jina lako tumekuja kupigana na jeshi hili kubwa ajabu. Ee Mwenyezi-Mungu, wewe ndiwe Mungu wetu; usimruhusu binadamu yeyote ashindane nawe.”

12 Basi, Mwenyezi-Mungu aliwashinda Waethiopia mbele ya Asa na jeshi lake la watu wa Yuda. Waethiopia wakakimbia.

13 Asa pamoja na wanajeshi wake wakawafuatilia mpaka Gerari, wakawaua Waethiopia wengi sana, asibaki hata mmoja, kwani walikuwa wamekwisha shindwa na Mwenyezi-Mungu pamoja na jeshi lake. Jeshi la Yuda lilichukua nyara nyingi sana.

14 Liliharibu miji yote iliyokuwa kandokando ya Gerari, kwa kuwa watu waliokuwamo katika miji hiyo waliingiwa na hofu ya Mwenyezi-Mungu. Jeshi lilichukua mali nyingi kutoka katika miji hiyo kwa sababu kulikuwamo mali nyingi sana.

15 Lilishambulia pia wachungaji, likachukua kondoo wengi na ngamia. Kisha likarejea Yerusalemu.

15

1 Roho ya Mungu ilimjia Azaria mwana wa Odedi,

2 naye akatoka kwenda kumlaki mfalme Asa, akamwambia, “Nisikilize, ee mfalme Asa na watu wote wa Yuda na Benyamini! Mwenyezi-Mungu yu pamoja nanyi, ikiwa mtakuwa pamoja naye. Mkimtafuta, mtampata, lakini mkimwacha naye atawaacha.

3 Kwa muda mrefu sasa, Waisraeli wameishi bila Mungu wa kweli, wala makuhani wa kuwafundisha, na bila sheria.

4 Lakini walipopatwa na shida, walimgeukia Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, wakamtafuta, wakampata.

5 Zamani hizo, hakuna mtu aliyeweza kuingia wala kutoka kwa usalama kwa sababu hapakuwa na amani; ghasia nyingi mno ziliwasumbua wananchi wa kila nchi.

6 Kulijaa mafarakano mengi, taifa moja lilipigana na taifa lingine na mji mmoja ulipigana na mji mwingine, kwa sababu Mungu aliwafadhaisha kwa taabu za kila aina.

7 Lakini nyinyi jipeni moyo, wala msilegee kwa maana mtapata tuzo kwa kazi mfanyayo.”

8 Asa alipoyasikia maneno haya, yaani unabii wa Azaria mwana wa Odedi, alipata moyo. Akaziondoa sanamu zote za kuchukiza katika nchi yote ya Yuda na Benyamini, na kutoka katika miji yote aliyoiteka katika nchi ya milima ya Efraimu. Pia, akaitengeneza upya madhabahu ya Mwenyezi-Mungu iliyokuwa katika ukumbi wa nyumba ya Mwenyezi-Mungu.

9 Asa aliwaita watu wote wa Yuda na Benyamini, na wengine wote waliokuwa wakikaa nchini mwake kutoka Efraimu, Manase na Simeoni. Hawa walikuja kwake walipoona kuwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wake, alikuwa pamoja naye.

10 Wote walikusanyika Yerusalemu katika mwezi wa tatu wa mwaka wa kumi na tano wa utawala wake Asa.

11 Siku hiyo, walimtolea Mwenyezi-Mungu tambiko za ng'ombe 700 na kondoo 7,000, kutoka katika zile nyara walizoteka.

12 Hapo wakafanya agano, ya kuwa watamtii Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zao, kwa moyo wote na kwa roho yao yote;

13 na kwamba yeyote asiyemtii Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, awe kijana au mzee, mwanamume au mwanamke, sharti auawe.

14 Walimwapia Mwenyezi-Mungu kwa sauti kuu, wakapaza sauti zaidi, wakapiga tarumbeta na baragumu.

15 Watu wote wa Yuda walikuwa na furaha tele kwa kuwa walikuwa wameapa kwa moyo wote. Walikuwa wamemtafuta kwa dhati, wakampata. Naye Mwenyezi-Mungu akawapa amani pande zote.

16 Mfalme Asa alimwondoa hata Maaka, mama yake, katika cheo chake cha mama malkia, kwa sababu alitengeneza sanamu ya kuchukiza ya Ashera, mungu wa kike. Asa alikatilia mbali sanamu hiyo, akaipondaponda na kuiteketeza katika bonde la kijito Kidroni.

17 Lakini hata hivyo mahali pa kutambikia miungu mingine katika Israeli hapakuharibiwa; lakini yeye alikuwa na moyo mwaminifu maisha yake yote.

18 Alivirudisha katika nyumba ya Mungu vifaa vyote vilivyowekwa wakfu na baba yake pamoja na vile alivyoviweka wakfu yeye mwenyewe: Fedha na dhahabu na vyombo vinginevyo.

19 Hapakuwa na vita tena nchini mpaka mwaka wa thelathini na tano wa utawala wake Asa.

16

1 Katika mwaka wa thelathini na sita wa utawala wa mfalme Asa, Baasha, mfalme wa Israeli, aliishambulia nchi ya Yuda na kuanza kuujenga mji wa Rama ili apate kuzuia mtu yeyote asitoke wala kuingia kwa Asa mfalme wa Yuda.

2 Ndipo mfalme Asa akachukua fedha na dhahabu kutoka katika hazina ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu na ikulu, akazituma Damasko kwa Ben-hadadi, mfalme wa Aramu na ujumbe akasema,

3 “Na tufanye mkataba wa ushirikiano kati yangu na wewe kama walivyofanya baba yangu na baba yako; tazama nakupa zawadi ya fedha na dhahabu; nenda ukavunje mkataba wa ushirikiano ulioko kati yako na mfalme Baasha wa Israeli ili aache mashambulizi dhidi yangu.”

4 Hapo mfalme Ben-hadadi alikubali pendekezo la mfalme Asa, akawatuma majemadari wake na majeshi yake kwenda kuishambulia miji ya Israeli. Nao waliiteka miji ya Iyoni, Dani, Abel-maimu, na miji yote ya Naftali iliyokuwa na ghala za vyakula.

5 Mfalme Baasha alipopata habari za mashambulizi hayo, aliacha kuujenga mji wa Rama, akasimamisha kazi yake.

6 Ndipo mfalme Asa alipowapeleka watu wote wa Yuda, wakahamisha mawe ya Rama na mbao, vifaa ambavyo Baasha alivitumia kujengea. Kisha Asa alitumia vifaa hivyo kujengea miji ya Geba na Mizpa.

7 Wakati huo, Hanani mwonaji alimwendea mfalme Asa wa Yuda, akamwambia, “Kwa sababu ulimtegemea mfalme wa Shamu badala ya kumtegemea Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, jeshi la mfalme wa Shamu limekuponyoka.

8 Je, wale Waethiopia na Walibia hawakuwa jeshi kubwa na magari na wapandafarasi wengi? Lakini kwa vile ulimtegemea Mwenyezi-Mungu, yeye aliwatia mikononi mwako.

9 Mwenyezi-Mungu huuchunga kwa makini ulimwengu wote, ili kuwapa nguvu wale walio waaminifu kwake. Umetenda jambo la kipumbavu, kwa hiyo tangu sasa, utakuwa na vita kila mara.”

10 Maneno haya yalimfanya Asa amkasirikie sana Hanani mwonaji, hata akamfunga gerezani. Wakati huohuo, Asa alianza kuwatesa vikali baadhi ya watu.

11 Matendo ya Asa, toka mwanzo hadi mwisho, yameandikwa katika kitabu cha “Wafalme wa Yuda na Israeli.”

12 Katika mwaka wa thelathini na tisa wa ufalme wake, Asa alishikwa na ugonjwa wa miguu, akaugua sana. Lakini hata wakati huo, Asa hakumgeukia Mwenyezi-Mungu amsaidie, bali alijitafutia msaada kutoka kwa waganga.

13 Hatimaye Asa alifariki mnamo mwaka wa arubaini na moja wa utawala wake.

14 Alizikwa katika kaburi alilokuwa amejichimbia mwenyewe mwambani, katika mji wa Daudi. Walimlaza ndani ya jeneza lililokuwa limejazwa manukato ya kila aina yaliyotayarishwa na mafundi wa kutengeneza marashi, wakawasha moto mkubwa sana kwa heshima yake.

17

1 Naye Yehoshafati mwanawe alitawala mahali pa baba yake Asa, akajiimarisha dhidi ya Israeli.

2 Aliweka majeshi katika miji yote ya Yuda yenye ngome, na katika maeneo mengine ya Yuda, na katika miji ya Efraimu ambayo Asa baba yake aliiteka akaweka askari walinzi.

3 Mwenyezi-Mungu alikuwa pamoja na Yehoshafati kwa sababu alifuata njia za awali za baba yake, na wala hakumwabudu Baali.

4 Yeye alimtafuta Mungu wa baba yake na kuzitii amri zake, wala hakufuata matendo ya watu wa Israeli.

5 Mwenyezi-Mungu, aliuimarisha ufalme wa Yuda mikononi mwa Yehoshafati, nao watu wote wakamletea zawadi, akatajirika sana na kuheshimika.

6 Alipenda sana moyoni kumtumikia Mwenyezi-Mungu, na zaidi ya hayo, alipaharibu mahali pote pa kuabudia miungu mingine na sanamu za Ashera, mungu wa kike, nchini Yuda.

7 Mnamo mwaka wa tatu wa utawala wake, Yehoshafati aliwatuma maofisa wafuatao wakafundishe katika miji ya Yuda: Ben-haili, Obadia, Zekaria, Nethaneli na Mikaya.

8 Walawi tisa na Makuhani wawili waliandamana nao. Walawi hao walikuwa Shemaya, Nethania, Zebadia, Asaheli, Shemiramothi, Yehonathani, Adoniya, Tobia na Tob-adoniya; na makuhani walikuwa Elishama na Yehoramu.

9 Walikichukua kitabu cha sheria ya Mwenyezi-Mungu, wakazunguka nacho katika miji yote ya Yuda wakifundisha watu.

10 Mwenyezi-Mungu alizitia hofu falme zote jirani na Yuda, zikaogopa kupigana vita na Yehoshafati.

11 Baadhi ya Wafilisti walimletea Yehoshafati zawadi pamoja na fedha nyingi, na Waarabu wengine nao wakamletea kondoo madume 7,700, na mabeberu 7,700.

12 Kwa hiyo Yehoshafati aliendelea kuwa mkuu zaidi. Alijenga ngome na miji yenye ghala,

13 kwa hiyo alikuwa na ghala kubwa katika miji ya Yuda. Huko Yerusalemu, aliweka askari wa jeshi mashujaa.

14 Hii ndiyo orodha yao kulingana na koo za baba zao: Adna alikuwa kamanda wa vikosi vya askari 1,000 wa kabila la Yuda. Chini yake, kulikuwa na askari laki tatu.

15 Wa pili katika cheo alikuwa kamanda Yehohanani, akiwa na askari 280,000,

16 na wa tatu alikuwa Amasia mwana wa Zikri, akiwa na askari mashujaa 200,000. Amasia alijitolea kwa hiari kumtumikia Mwenyezi-Mungu.

17 Kamanda wa vikosi vya askari, waliotoka katika kabila la Benyamini alikuwa Eliada, mtu shupavu, naye alikuwa na askari 200,000, wenye nyuta na ngao.

18 Wa pili alikuwa Yehozabadi, aliyekuwa na askari 180,000 waliojiandaa tayari kwa vita.

19 Watu wote hao walimhudumia mfalme huko Yerusalemu; na zaidi ya hayo, mfalme aliweka askari wengine katika miji ile mingine yenye ngome kote nchini Yuda.

18

1 Wakati mfalme Yehoshafati wa Yuda alipokuwa amekwisha kuwa mtu tajiri na mwenye heshima, alifanya mpango wa ndoa baina ya jamaa yake, na jamaa ya mfalme Ahabu wa Israeli.

2 Baada ya miaka kadhaa Yehoshafati alikwenda Samaria kumtembelea mfalme Ahabu. Ahabu akamchinjia Yehoshafati kondoo na ng'ombe wengi, kwa heshima yake pamoja na watu waliokuwa pamoja naye, kisha akamshawishi aandamane naye kuushambulia mji wa Ramoth-gileadi.

3 Ahabu mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati mfalme wa Yuda, “Je, utaandamana nami kwenda kuushambulia mji wa Ramoth-gileadi?” Naye akajibu, “Naam, mimi niko nawe, pia watu wangu ni watu wako. Tutakuwa pamoja nawe vitani.”

4 Kisha Yehoshafati akaendelea kumwambia mfalme wa Israeli, “Lakini kwanza mwulize Mwenyezi-Mungu shauri.”

5 Basi, Ahabu akaitisha kikao cha manabii wapatao 400, akawauliza, “Je, twende tukaushambulie mji wa Ramoth-gileadi, au nisiende?” Wao wakamjibu, “Nenda! Mungu atakupatia ushindi!”

6 Lakini, Yehoshafati akauliza, “Je, hapa hakuna nabii mwingine wa Mwenyezi-Mungu ambaye twaweza kumwuliza shauri?”

7 Naye mfalme wa Israeli akamjibu Yehoshafati, “Yupo bado mmoja, Mikaya mwana wa Imla. Yeye twaweza kumwuliza shauri la Mwenyezi-Mungu. Lakini namchukia kwa sababu yeye kamwe hatabiri jambo jema juu yangu, ila mabaya tu.” Yehoshafati akamwambia, “Si vizuri mfalme kusema hivyo.”

8 Basi, Ahabu, mfalme wa Israeli akamwita ofisa mmoja na kumwamuru, “Haraka, nenda ukamlete Mikaya mwana wa Imla.”

9 Wakati huo, mfalme wa Israeli pamoja na Yehoshafati, mfalme wa Yuda, walikuwa wameketi katika viti vyao vya enzi wakikaa kwenye kiwanja cha kupuria nafaka kwenye lango la kuingilia mjini Samaria nao walikuwa wamevalia mavazi yao ya kifalme. Wakati huo manabii wote walikuwa wakitoa unabii wao mbele yao.

10 Kisha mmoja wa manabii hao, Sedekia mwana wa Kenaana, akajitengenezea pembe za chuma, akasema, “Mwenyezi-Mungu asema hivi: ‘Kwa pembe hizi, utawarudisha nyuma Washamu hata kuwaangamiza.’”

11 Hata wale manabii wengine wakatabiri vivyo hivyo wakasema, “Nenda ukaushambulie Ramoth-gileadi, Mwenyezi-Mungu atautia mikononi mwako.”

12 Wakati huo, yule mjumbe aliyetumwa kwa Mikaya alimwambia, “Manabii wengine wote kwa pamoja wamemtabiria mfalme ushindi; tafadhali nawe pia ufanye kama wao, umtabirie mema.”

13 Lakini Mikaya akamjibu, “Kama Mwenyezi-Mungu aishivyo, kile atakachoniambia Mungu wangu, ndicho nitakachosema.”

14 Basi, Mikaya alipofika mbele ya mfalme, mfalme akamwuliza, “Je, twende kupigana vitani huko Ramoth-gileadi au nisiende?” Mikaya akajibu, “Nenda ushinde; Mwenyezi-Mungu atawatia mikononi mwako.”

15 Lakini mfalme akamwambia, “Nitakuapisha mara ngapi kwamba kila unaposema nami kwa jina la Mwenyezi-Mungu, ni lazima uniambie ukweli mtupu?”

16 Naye Mikaya akasema, “Niliwaona watu wote wa Israeli wametawanyika milimani kama kondoo wasio na mchungaji. Naye Mwenyezi-Mungu akasema, ‘Watu hawa hawana kiongozi; waache warudi kila mtu nyumbani kwake kwa amani.’”

17 Hapo mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati, “Sikukuambia, kamwe hatatabiri jema juu yangu, ila mabaya tu?”

18 Kisha Mikaya akasema: “Haya, sikia neno la Mwenyezi-Mungu: Nilimwona Mwenyezi-Mungu ameketi katika kiti chake cha enzi na jeshi lake lote la mbinguni limesimama upande wake wa kulia na wa kushoto.

19 Ndipo Mwenyezi-Mungu akauliza, ‘Ni nani atakayemshawishi Ahabu mfalme wa Israeli aende akaangamie huko Ramoth-gileadi?’ Kila mmoja akajibu alivyofikiri.

20 Kisha, pepo mmoja akajitokeza mbele ya Mwenyezi-Mungu, akasema, ‘Mimi nitamshawishi.’ Mwenyezi-Mungu akamwuliza, ‘Kwa mbinu gani?’

21 Naye akajibu, ‘Nitakwenda na kuwafanya manabii wake wote waseme uongo.’ Mwenyezi-Mungu akamwambia, ‘Wewe utamshawishi na utafaulu; haya nenda ukafanye hivyo.’

22 Basi ndivyo ilivyo: Mwenyezi-Mungu amewafanya hawa manabii wako waseme uongo. Lakini Bwana amenena mabaya juu yako!”

23 Hapo nabii Sedekia mwana wa Kenaana akamkaribia Mikaya, akampiga kofi shavuni na kumwuliza, “Kwa njia gani Roho wa Mwenyezi-Mungu ameniacha na akaja kunena nawe?”

24 Mikaya akamjibu, “Siku ile utakapoingia katika chumba cha ndani kujificha ndipo utakapojua.”

25 Naye mfalme wa Israeli akatoa amri, “Mkamateni Mikaya mrudisheni kwa Amoni, mkuu wa mji, na kwa Yoashi, mwana wa mfalme.

26 Waambie wamfunge gerezani na kumlisha mkate kidogo na maji, mpaka nitakaporudi salama.”

27 Ndipo Mikaya aliposema, “Ukirudi salama, basi, utajua Mwenyezi-Mungu hakunena nami.” Kisha akaendelea kusema, “Sikieni, enyi watu wote!”

28 Basi, mfalme wa Israeli akaenda pamoja na Yehoshafati mfalme wa Yuda kuushambulia mji wa Ramoth-gileadi.

29 Mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati, “Mimi nitavaa mavazi yasiyo ya kifalme kuingia vitani, lakini wewe utavaa mavazi yako ya kifalme.” Hivyo mfalme wa Israeli akaenda vitani bila kuvaa mavazi ya kifalme.

30 Mfalme wa Aramu alikuwa amewaamuru makapteni wake waliosimamia magari yake ya kukokotwa akisema, “Msipigane na mtu yeyote yule mkubwa au mdogo, ila tu na mfalme wa Israeli.”

31 Baadaye makapteni hao walipomwona Yehoshafati, walisema, “Huyu mfalme wa Israeli.” Kwa hiyo, walimwelekea kumshambulia; lakini Yehoshafati akapiga kelele, na Mwenyezi-Mungu akamwokoa. Mungu akawaondoa wale waliokuwa karibu kumshambulia.

32 Makapteni walipotambua kwamba hakuwa mfalme wa Israeli, waliacha kumshambulia, wakarudi.

33 Lakini askari mmoja wa Aramu akauvuta upinde wake kwa kubahatisha, mshale ukamchoma mfalme wa Israeli katika nafasi ya kuungana kwa vazi lake la chuma. Hapo Ahabu akamwambia dereva wa gari lake, “Nimejeruhiwa! Geuza gari uniondoe vitani.”

34 Nayo mapigano siku hiyo, yakazidi kuwa makali huku mfalme wa Israeli amejiegemeza mwenyewe garini akiwaelekea Washamu mpaka jioni. Halafu mnamo machweo ya jua, alifariki.

19

1 Mfalme Yehoshafati wa Yuda alirejea salama katika ikulu yake mjini Yerusalemu.

2 Lakini mwonaji Yehu mwana wa Hanani, alikwenda kumlaki mfalme, akamwambia, “Je, unadhani ni vema kuwasaidia waovu na kuwapenda wamchukiao Mwenyezi-Mungu? Mambo uliyofanya yamekuletea ghadhabu ya Mwenyezi-Mungu.

3 Walakini, kuna wema fulani ndani yako. Umekwisha ziondoa sanamu zote za Ashera, mungu wa kike, na umejitahidi sana kumtafuta Mungu kwa moyo wote.”

4 Mfalme Yehoshafati alikaa Yerusalemu, lakini hata hivyo, mara kwa mara aliwatembelea watu wa Beer-sheba kusini, mpaka milima ya Efraimu, upande wa kaskazini. Alifanya hivyo ili kuwavutia watu wamrudie Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zao.

5 Aliteua waamuzi katika miji yote ya Yuda yenye ngome,

6 akawaambia, “Muwe waangalifu sana wakati mnapoamua, kwa maana hukumu mtoayo hamwitoi kwa amri ya binadamu, bali kwa amri itokayo kwa Mwenyezi-Mungu, naye yu pamoja nanyi mnapotoa uamuzi.

7 Basi, sasa mwogopeni Mwenyezi-Mungu, muwe waangalifu katika kila jambo mtakalotenda kwa sababu Mwenyezi-Mungu wetu hatavumilia upotoshaji wa haki, wala upendeleo wala ulaji rushwa.”

8 Mjini Yerusalemu, Yehoshafati aliteua Walawi kadhaa, waamuzi na baadhi ya wakuu wa jamaa za Waisraeli wawe waamuzi wa magomvi yahusuyo uvunjaji wa sheria za Mwenyezi-Mungu, au ugomvi baina ya wakazi wa mji.

9 Akawaamuru akisema; “Tekelezeni wajibu wenu mkimwogopa Mwenyezi-Mungu, kwa uaminifu na kwa moyo wote.

10 Kila mara ndugu zenu kutoka katika mji wowote ule wanapowaletea shtaka lolote kuhusu uuaji, uvunjaji wa sheria, amri, kanuni au maagizo, washaurini vema ili wasije wakamkosea Mwenyezi-Mungu. Msipofanya hivyo, nyinyi pamoja na ndugu zenu mtapatwa na ghadhabu ya Mwenyezi-Mungu. Lakini mkiutekeleza wajibu wenu, hamtakuwa na hatia.

11 Amaria, kuhani mkuu, ndiye atakayesimamia mambo yote yanayomhusu Mwenyezi-Mungu, naye Zebadia mwana wa Ishmaeli, gavana wa Yuda atasimamia mambo yote ya utawala, na Walawi watakuwa maofisa. Jipeni moyo muyatekeleze masharti haya, naye Mwenyezi-Mungu awe pamoja nao walio wema.”

20

1 Baada ya muda, majeshi ya Moabu na Amoni pamoja na baadhi ya Wameuni, waliivamia Yuda.

2 Watu kadhaa walikuja wakamwambia mfalme Yehoshafati, “Jeshi kubwa limekuja kukushambulia kutoka Edomu, ngambo ya Bahari ya Chumvi. Tayari wamekwisha teka Hasason-tamari.” (Hili ni jina lingine la Engedi).

3 Yehoshafati akashikwa na woga, akamwomba Mwenyezi-Mungu amwongoze. Akatangaza watu wote nchini Yuda wafunge.

4 Watu wakaja Yerusalemu kutoka miji yote ya Yuda, wakakusanyika ili kumwomba Mwenyezi-Mungu awasaidie.

5 Yehoshafati akasimama katikati ya kusanyiko la watu wa Yuda na Yerusalemu mbele ya ua mpya wa nyumba ya Mwenyezi-Mungu,

6 akaomba kwa sauti akisema, “Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zetu, wewe ndiwe Mungu uliye mbinguni! Wewe unazitawala falme zote duniani; unao uwezo na nguvu, wala hakuna awezaye kukupinga.

7 Ni wewe ee Mungu wetu, uliyewafukuza wenyeji wa nchi hii wakati watu wako Israeli walipoingia katika nchi hii, ukawapa wazawa wa Abrahamu rafiki yako, iwe yao milele.

8 Nao wamekaa humu, na kukujengea hekalu kwa heshima ya jina lako, wakijua

9 kwamba wakipatwa na maafa yoyote, vita, maradhi mabaya, au njaa, basi watakuja na kusimama mbele ya nyumba hii mbele yako, wakulilie katika shida zao, nawe utawasikiliza na kuwaokoa.

10 Sasa watu wa Amoni, Moabu na wa mlima Seiri, ambao hukuwaruhusu babu zetu washambulie nchi zao walipotoka Misri, wakapitia kandokando wasiwaangamize,

11 tazama, jinsi wanavyotulipa. Wanakuja kututoa katika nchi yako uliyotupa iwe mali yetu.

12 Wewe ndiwe Mungu wetu! Waadhibu, kwani sisi hatuna uwezo wowote mbele ya jeshi kubwa kama hili linalotujia. Hatujui la kufanya ila tunatazamia msaada kutoka kwako.”

13 Wanaume wote wa Yuda, pamoja na wake zao na watoto wao, walikuwa wamesimama hapo mbele ya Mwenyezi-Mungu.

14 Ndipo Roho wa Mwenyezi-Mungu akamjia mmoja wa Walawi aliyekuwa hapo, jina lake Yahazieli mwana wa Zekaria, mwana wa Benaya, mwana wa Yeieli, mwana wa Matania, wa ukoo wa Asafu.

15 Yahazieli akasema, “Sikilizeni watu wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu na mfalme Yehoshafati, Mwenyezi-Mungu awaambia hivi: Msiogope wala msihangaike kwa sababu ya jeshi hili kubwa. Vita hivi si vyenu, bali ni vya Mungu.

16 Kesho washambulieni wakati watakapokuwa wakipanda Bonde la Sisi. Mtawakuta mwisho wa bonde, mashariki mwa jangwa la Yerueli.

17 Hamtahitaji kupigana vita hivi. Nyinyi jipangeni tu halafu mngojee, na mtaona Mwenyezi-Mungu akiwashinda kwa niaba yenu. Enyi watu wa Yuda na Yerusalemu, msiogope wala msifadhaike. Nendeni vitani, naye Mwenyezi-Mungu atakuwa pamoja nanyi!”

18 Hapo mfalme Yehoshafati akasujudu pamoja na watu wote wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu wakamsujudu na kumwabudu Mwenyezi-Mungu.

19 Walawi wa ukoo wa Kohathi na Kora, wakasimama na kumsifu Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, kwa sauti kubwa sana.

20 Kesho yake, wakaamka asubuhi na mapema, wakaenda mpaka katika jangwa la Tekoa. Walipokuwa wanaondoka, Yehoshafati alisimama, akawaambia, “Nisikilizeni, enyi watu wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu! Mwaminini Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, nanyi mtakuwa imara. Muwe na imani na manabii wake, nanyi mtafaulu.”

21 Baada ya kushauriana na watu, mfalme alichagua wanamuziki fulani, akawaagiza wajivike mavazi yao rasmi kisha watangulie mbele ya jeshi, wakiimba: “Mshukuruni Mwenyezi-Mungu, maana fadhili zake zadumu milele!”

22 Wakati walipoanza kuimba na kusifu, Mwenyezi-Mungu aliwavuruga akili wanajeshi wa Amoni, Moabu na wa Mlima Seiri waliokuja kupigana na Yuda. Na wanajeshi hao wakashindwa.

23 Watu wa Amoni na wa Moabu wakawashambulia wenyeji wa mlima Seiri, na kuwaangamiza kabisa. Baada ya kuwaangamiza wakazi wa mlima Seiri wakaanza kushambuliana wao kwa wao, wakaangamizana.

24 Jeshi la Yuda lilipofika penye mnara wa ulinzi huko jangwani, waliangalia upande wa maadui, wakaona maiti zimetapakaa kila mahali. Hakuna mtu yeyote aliyenusurika.

25 Yehoshafati na wanajeshi wake wakaenda kuchukua nyara wakakuta ng'ombe wengi, mali, nguo na vitu vingine vya thamani. Iliwachukua muda wa siku tatu kusomba nyara hizo, na hata hivyo, hawakuzimaliza kwani zilikuwa nyingi mno.

26 Siku ya nne wakakusanyika katika Bonde la Sifa, na kumsifu Mwenyezi-Mungu kwa yote aliyowafanyia. Ndio maana bonde hilo linaitwa Bonde la Sifa hadi hivi leo.

27 Kisha Yehoshafati akawaongoza wanajeshi wake mpaka Yerusalemu kwa shangwe, kwa sababu Mwenyezi-Mungu aliwashinda maadui zao.

28 Walipofika Yerusalemu, walikwenda moja kwa moja hadi nyumba ya Mwenyezi-Mungu, wakipiga vinanda, vinubi na tarumbeta.

29 Falme zote ziliingiwa na hofu ziliposikia jinsi Mwenyezi-Mungu alivyowashinda maadui za Israeli.

30 Basi, Yehoshafati akatawala kwa amani, na Mungu akampa amani pande zote.

31 Yehoshafati alikuwa na umri wa miaka thelathini na mitano alipoanza kutawala Yuda. Alitawala kutoka Yerusalemu kwa muda wa miaka ishirini na mitano. Mama yake alikuwa Azuba binti Shilhi.

32 Alitenda mema mbele ya Mwenyezi-Mungu kama alivyofanya Asa baba yake.

33 Lakini hakupaharibu mahali pa kutolea tambiko kilimani. Watu walikuwa bado hawajamgeukia na kumwabudu Mungu wa babu zao kwa mioyo yao.

34 Matendo mengine ya Yehoshafati, kutoka mwanzo wa utawala wake mpaka mwisho, yameandikwa katika kitabu cha kumbukumbu za Yehu mwana wa Hanani, ambamo zimo katika kitabu cha Wafalme wa Israeli.

35 Baada ya haya, Yehoshafati mfalme wa Yuda, alijiunga na Ahazia mfalme wa Israeli, aliyetenda mambo maovu.

36 Walishirikiana kuunda merikebu za kusafiria mpaka Tarshishi; waliziundia huko Esion-geberi.

37 Lakini Eliezeri mwana wa Dodavahu, kutoka mji wa Maresha, akatoa unabii dhidi ya Yehoshafati, akisema, “Kwa sababu umejiunga na Ahazia, Mwenyezi-Mungu atavunja merikebu zote mlizotengeneza.” Baadaye merikebu hizo zilivunjikavunjika; kwa hiyo hazikuweza kusafiri mpaka Tarshishi.

21

1 Hatimaye Yehoshafati alifariki na kuzikwa pamoja na babu zake katika makaburi ya kifalme katika mji wa Daudi; naye Yehoramu mwanawe akatawala mahali pake.

2 Yehoramu alikuwa na ndugu kadhaa wana wa Yehoshafati: Azaria, Yehieli, Zekaria, Azaria, Mikaeli na Shefatia.

3 Baba yao aliwapa zawadi kubwakubwa za fedha, dhahabu na vitu vingine vya thamani, na pia miji ya Yuda yenye ngome. Lakini kwa sababu Yehoramu ndiye aliyekuwa mzaliwa wake wa kwanza, Yehoshafati akampa ufalme atawale badala yake.

4 Yehoramu alipokikalia kiti cha enzi na utawala wake ulipokuwa umekwisha imarika, yeye aliwaua ndugu zake wote kwa upanga, na pia baadhi ya wakuu wa Israeli.

5 Yehoramu alianza kutawala akiwa na umri wa miaka thelathini na miwili. Alitawala huko Yerusalemu kwa muda wa miaka minane.

6 Alizifuata njia mbaya za mfalme Ahabu na za wafalme wengine wa Israeli kama jamaa ya Ahabu ilivyofanya kwa sababu mkewe alikuwa binti ya Ahabu. Alitenda maovu mbele ya Mwenyezi-Mungu,

7 lakini Mwenyezi-Mungu hakutaka kuangamiza ukoo wa Daudi kwa ajili ya agano alilokuwa amefanya na Daudi na pia kwa sababu alikuwa ameahidi wazawa wake wataendelea kutawala milele.

8 Wakati wa enzi ya Yehoramu, watu wa Edomu waliasi utawala wa Yuda, wakamtawaza mfalme wao wenyewe.

9 Kwa hiyo, Yehoramu pamoja na makamanda wake na magari yake yote aliondoka akawashambulia Waedomu waliokuwa wamemzunguka yeye pamoja na makamanda wake na magari.

10 Hivyo Edomu imeuasi utawala wa Yuda mpaka sasa. Wakati huohuo pia, wakazi wa Libna nao wakauasi utawala wake kwa sababu Yehoramu alikuwa amemwacha Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zake.

11 Isitoshe, alitengeneza mahali pa kuabudia miungu mingine katika milima ya Yuda na kusababisha wakazi wa Yerusalemu kukosa uaminifu na watu wa Yuda kupotoka.

12 Nabii Elia alimpelekea mfalme Yehoramu barua ifuatayo: “Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Daudi babu yako, anakulaani kwa sababu hukufuata mwenendo wa Yehoshafati baba yako, au wa Asa mfalme wa Yuda.

13 Badala yake umeifuata mienendo ya wafalme wa Israeli na kuwaongoza watu wa Yuda na Yerusalemu katika kukosa uaminifu kama vile Ahabu, na wafalme wa jamaa yake waliomfuata walivyowaongoza watu wa Israeli kukosa uaminifu. Pia umewaua ndugu zako, ndugu za baba mmoja waliokuwa watu wema zaidi kuliko wewe.

14 Kwa sababu hiyo, Mwenyezi-Mungu atawaadhibu vikali watu wako, wanao, wake zako na kuiharibu mali yako yote.

15 Wewe mwenyewe utaugua maradhi mabaya ya tumbo, ambayo yataongezeka siku hata siku, mpaka matumbo yako yatoke nje.”

16 Kulikuwa na Wafilisti na Waarabu wengine waliokuwa wakikaa karibu na Waethiopia. Hawa, Mwenyezi-Mungu aliwapandisha hasira ili wapigane na Yehoramu.

17 Basi, wakaishambulia nchi ya Yuda, wakaiteka mali yote iliyokuwamo katika jumba la mfalme na kuwachukua mateka wanawe wote na wake zake, isipokuwa Ahazia, mwanawe mdogo.

18 Baada ya haya yote, Mwenyezi-Mungu akamletea mfalme ugonjwa wa tumbo usioponyeka.

19 Aliendelea kuugua, na ugonjwa wake ukawa unaongezeka siku hata siku, hata kufikia mwisho wa mwaka wa pili, akafariki dunia katika maumivu makali. Watu hawakuwasha moto kuomboleza kifo chake kama walivyowafanyia babu zake.

20 Yehoramu alianza kutawala akiwa na umri wa miaka thelathini na miwili; akatawala huko Yerusalemu kwa muda wa miaka minane. Wakati alipofariki, hakuna mtu yeyote aliyemsikitikia. Alizikwa katika mji wa Daudi, ila si katika makaburi ya wafalme.

22

1 Wakazi wa Yerusalemu walimpa Ahazia, mwana mdogo wa Yehoramu, ufalme, atawale mahali pa baba yake kwa sababu wakubwa wake wote waliuawa na kikundi fulani kilichokuja kambini pamoja na Waarabu. Hivyo, Ahazia mwana wa Yehoramu, mfalme wa Yuda, akatawala.

2 Ahazia, alianza kutawala akiwa mwenye umri wa miaka arubaini na miwili, akatawala kutoka Yerusalemu kwa muda wa mwaka mmoja. Mama yake aliitwa Athalia, mjukuu wa Omri.

3 Kwa sababu mama yake alikuwa mshauri wake katika kutenda maovu, naye pia alifuata mienendo ya jamaa ya Ahabu.

4 Alitenda maovu mbele ya Mwenyezi-Mungu kama vile jamaa ya Ahabu ilivyofanya kwani hao ndio waliokuwa washauri wake baada ya kifo cha baba yake, hata aangamie.

5 Hata alifuata shauri lao, akaenda pamoja na mfalme Yehoramu mwana wa Ahabu mfalme wa Israeli kupigana na Hazaeli mfalme wa Shamu huko Ramoth-gileadi. Nao Washamu walimjeruhi Yoramu.

6 Kisha akarudi Yezreeli ili apate kutibiwa majeraha aliyoyapata huko Rama, wakati alipopigana na Hazaeli mfalme wa Shamu. Naye Ahazia mwana wa Yehoramu mfalme wa Yuda alimtembelea Yoramu mwana wa Ahabu huko Yezreeli kwa sababu alikuwa mgonjwa.

7 Lakini hiyo ilikuwa imepangwa na Mungu kuwa maangamizi yampate Ahazia kwa njia hiyo ya kumtembelea Yoramu. Maana alipofika huko, alitoka pamoja na Yoramu kwenda kupigana na Yehu mwana wa Nimshi ambaye Mwenyezi-Mungu alimteua kuuangamiza uzao wa Ahabu.

8 Wakati Yehu alipokuwa akiwahukumu jamaa ya Ahabu alikutana na wakuu wa Yuda pamoja na wana wa ndugu zake Ahazia, waliomtumikia Ahazia, akawaua.

9 Alimtafuta Ahazia, naye akakamatwa akiwa amejificha huko Samaria. Walimleta hadi kwa Yehu, akauawa. Waliuzika mwili wake kwani walisema, “Yeye ni mjukuu wa Yehoshafati, ambaye alimtafuta Mwenyezi-Mungu kwa moyo wake wote.” Hapakubaki hata mtu mmoja wa jamaa ya Ahazia ambaye angeweza kuwa falme.

10 Mara Athalia, mamake Ahazia, alipoona kuwa mwanawe ameuawa, alitoka akaangamiza jamii yote ya kifalme ya Yuda.

11 Lakini Yehosheba, binti ya mfalme Yehoramu alimchukua Yoashi, akamtwaa kwa siri kutoka miongoni mwa wana wa mfalme waliokuwa karibu kuuawa. Alimficha yeye pamoja na yaya wake, katika chumba cha kulala. Hivyo Yehosheba, binti ya mfalme Yehoramu, mke wa kuhani Yehoadani, kwa sababu alikuwa dadaye Ahazia, alimficha Yoashi ili Athalia asimuue.

12 Naye alikaa nao kwa muda wa miaka sita akiwa amefichwa ndani ya nyumba ya Mungu wakati Athalia alipokuwa akitawala nchi.

23

1 Baadaye, mnamo mwaka wa saba, kuhani Yehoyada alijipa moyo akafanya mapatano na makapteni: Azaria mwana wa Yehoramu, Ishmaeli mwana wa Yehohanani, Azaria mwana wa Obedi, Maaseya mwana wa Adaya, na Elishafati mwana wa Zikri.

2 Wakazunguka katika miji yote ya Yuda wakiwakusanya Walawi na viongozi wa makabila ya Israeli, wakaenda mpaka Yerusalemu.

3 Mkutano wote ukafanya agano na mfalme katika nyumba ya Mungu. Yehoyada akawaambia, “Mwangalie huyu mwana wa mfalme! Mwacheni atawale kulingana na ahadi aliyoitoa Mwenyezi-Mungu kuhusu uzao wa Daudi.

4 Hivi ndivyo mtakavyofanya: Theluthi moja yenu nyinyi makuhani na Walawi mtakaoshika zamu siku ya Sabato, mtayalinda malango,

5 theluthi nyingine italinda ikulu na theluthi iliyobakia mtalinda Lango la Msingi. Watu wote watakuwa katika nyua za nyumba ya Mwenyezi-Mungu.

6 Asikubaliwe mtu mwingine yeyote kuingia nyumba ya Mwenyezi-Mungu isipokuwa makuhani tu pekee na wale Walawi watakaokuwa wanahudumu. Hao wanaweza kuingia kwa sababu wao ni watakatifu, lakini wale watu wengine wote, watatii amri ya Mwenyezi-Mungu.

7 Walawi watamzunguka mfalme, kila mtu na silaha yake mkononi; na mtu yeyote atakayejaribu kuingia katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu, atauawa. Mkae na mfalme popote aendapo.”

8 Walawi na watu wa Yuda walitii amri zote alizotoa kuhani Yehoyada. Kila ofisa akawachukua watu wake wote, wale waliokuwa wamemaliza zamu na wale waliokuwa wanaingia kushika zamu siku ya Sabato; kwa sababu Yehoyada hakuwaruhusu waondoke.

9 Kisha kuhani Yehoyada akawapa makapteni mikuki na ngao kubwa na ndogo zilizokuwa mali ya mfalme Daudi, na ambazo zilikuwa zimewekwa katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu.

10 Kisha, akawapanga watu wote kuanzia upande wa kusini mpaka upande wa kaskazini wa nyumba na kuzunguka madhabahu na nyumba, kila mmoja silaha yake mkononi, ili kumlinda mfalme.

11 Halafu wakamtoa nje mwana wa mfalme, wakamvika taji kichwani, na kumpa ule ushuhuda; wakamtawaza nao Yehoyada na wanawe wakampaka mafuta awe mfalme, kisha watu wakashangilia wakisema, “Aishi mfalme!”

12 Naye Malkia Athalia aliposikia sauti za watu wakikimbia na kumshangilia mfalme aliwaendea hao watu waliokuwa katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu.

13 Alipochungulia akamwona mfalme mpya amesimama karibu na nguzo kwenye lango, huku makapteni na wapiga tarumbeta wakiwa kando ya mfalme na wakazi wote wakishangilia na kupiga tarumbeta; nao waimbaji wakiwa na ala zao za muziki wakiongoza watu katika sherehe; ndipo aliporarua nguo zake na kusema kwa sauti kubwa “Uhaini! Uhaini!”

14 Kisha kuhani Yehoyada aliwatoa nje makapteni wa jeshi akisema mtoeni nje katikati ya askari; yeyote atakayemfuata na auawe kwa upanga. Kwa sababu alisema “Msimuulie katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu.”

15 Basi, wakamkamata, na akaingia katika njia ya Lango la Farasi la ikulu, wakamuulia huko.

16 Yehoyada akafanya agano kati yake mwenyewe, watu wote, na mfalme kwamba watakuwa watu wa Mwenyezi-Mungu.

17 Halafu watu wote wakaenda kwenye nyumba ya Baali, wakaibomoa na kuzivunja madhabahu pamoja na sanamu zake. Kisha wakamuua Matani, kuhani wa Baali, mbele ya madhabahu.

18 Kuhani Yehoyada akaweka walinzi kulinda nyumba ya Mwenyezi-Mungu. Hao walinzi walisimamiwa na makuhani na Walawi ambao Daudi aliwaweka katika huduma ya kutunza nyumba ya Mwenyezi-Mungu na kutoa sadaka za kuteketezwa kwa Mwenyezi-Mungu kama ilivyoandikwa katika sheria ya Mose, wakishangilia na kuimba kwa kufuata amri ya Daudi.

19 Aliweka mabawabu malangoni mwa nyumba ya Mwenyezi-Mungu ili asije akaingia mtu yeyote aliye najisi kwa namna moja au nyingine.

20 Aliwachukua makapteni wa jeshi, waheshimiwa, watawala wa watu, na wakazi wote; nao wakamsindikiza mfalme kutoka nyumba ya Mwenyezi-Mungu, wakapitia katika lango la juu mpaka ikulu. Kisha wakamkalisha mfalme kwenye kiti cha enzi.

21 Kwa hiyo wakazi wote walishangilia; na mji wote ulikuwa mtulivu baada ya Athalia kuuawa kwa upanga.

24

1 Yoashi alikuwa na umri wa miaka saba alipoanza kutawala. Alitawala kwa muda wa miaka arubaini huko Yerusalemu. Mama yake alikuwa Sibia kutoka Beer-sheba.

2 Wakati wote kuhani Yehoyada alipokuwa hai Yoashi alitenda mema mbele ya Mwenyezi-Mungu.

3 Yehoyada akamwoza wake wawili, nao wakamzalia watoto wa kiume na wa kike.

4 Baadaye Yoashi aliamua kurekebisha nyumba ya Mwenyezi-Mungu.

5 Basi, akawaita makuhani na Walawi na kuwaamuru, “Nendeni katika miji ya Yuda, mkusanye fedha kutoka kwa Waisraeli wote ili kurekebisha nyumba ya Mungu wenu kila mwaka; harakisheni.” Lakini Walawi hawakuharakisha.

6 Basi, mfalme akamwita kiongozi Yehoyada, akamwuliza, “Mbona hujaamrisha Walawi kukusanya kutoka kwa watu wa Yuda na Yerusalemu, kodi ambayo Mose mtumishi wa Mwenyezi-Mungu, aliagiza watu walipe kwa ajili ya Hema Takatifu la Mwenyezi-Mungu?”

7 (Athalia yule mwanamke mwovu na wafuasi wake walivunja nyumba ya Mungu na kuingia ndani; na vyombo vitakatifu vya nyumba ya Mwenyezi-Mungu walivitumia katika ibada za Mabaali.)

8 Basi, mfalme aliwaamuru Walawi, wakatengeneza sanduku la matoleo na kuliweka nje ya lango la nyumba ya Mwenyezi-Mungu.

9 Kisha tangazo likatolewa kote katika Yuda na Yerusalemu, kwamba watu wote wamletee Mwenyezi-Mungu kodi ambayo Mose mtumishi wa Mungu, aliwaamuru Waisraeli walipokuwa jangwani.

10 Wakuu wote na watu wote walifurahi wakaleta kodi yao wakaitumbukiza kwenye sanduku mpaka walipomaliza kufanya hivyo.

11 Walawi walipopeleka sanduku hilo kwa maofisa wa mfalme, nao walipoona kuwa kuna kiasi kikubwa cha fedha ndani, katibu wa mfalme pamoja na mwakilishi wa kuhani mkuu, walizitoa sandukuni, kisha wakalirudisha mahali pake. Waliendelea kufanya hivyo kila siku, wakakusanya fedha nyingi.

12 Mfalme na Yehoyada walizitoa fedha hizo na kuwapa wale waliosimamia kazi ya urekebishaji wa nyumba ya Mwenyezi-Mungu. Nao wakawaajiri waashi, maseremala warekebishe nyumba ya Mwenyezi-Mungu. Waliajiri pia mafundi wa chuma na shaba ili kurekebisha nyumba ya Mwenyezi-Mungu.

13 Hivyo mafundi hao walishughulika na kazi hiyo kwa bidii, wakairudisha nyumba ya Mwenyezi-Mungu katika hali yake ya awali, wakaiimarisha.

14 Walipomaliza kuitengeneza nyumba ya Mwenyezi-Mungu, walimletea mfalme na Yehoyada dhahabu na fedha iliyobaki; halafu vyombo kwa ajili ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu vilitengenezwa kwa fedha hizo, vyombo hivyo vilikuwa vya kutumika katika huduma ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu, matoleo ya sadaka za kuteketeza na mabakuli ya kufukizia ubani, pia vyombo vya dhahabu na vya fedha. Watu waliendelea kutoa sadaka za kuteketezwa katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu wakati wote wa utawala wa Yehoyada.

15 Lakini Yehoyada alizeeka na alipofikisha umri wa miaka 130, alifariki.

16 Wakamzika katika mji wa Daudi, kwenye makaburi ya wafalme ili kuonesha heshima yao kwake kwa sababu alifanya mema katika Israeli kwa ajili ya Mungu na nyumba yake.

17 Baada ya kifo cha Yehoyada, wakuu wa Yuda walimjia mfalme Yoashi wakamsujudia, wakamshawishi, naye akakubaliana nao.

18 Basi, watu wakaacha kuabudu katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zao, wakaanza kuabudu Maashera na sanamu. Ghadhabu ya Mungu iliwaka juu ya Yuda na Yerusalemu kwa sababu ya hatia hii.

19 Hata hivyo, aliwapelekea manabii kuwaonya ili wamrudie Mwenyezi-Mungu, lakini wao hawakuwasikiliza.

20 Ndipo Roho ya Mungu ikamjia Zekaria mwana wa kuhani Yehoyada, naye akasimama mbele ya watu mahali palipokuwa juu kidogo, akawaambia, “Mwenyezi-Mungu aliwaulizeni kwa nini mnazivunja amri zake na sasa hamwezi kufanikiwa! Kwa vile mmemwacha, naye pia amewaacha!”

21 Lakini wakamfanyia njama; na kwa amri ya mfalme, wakampiga mawe kwenye ua wa nyumba ya Mwenyezi-Mungu wakamuua.

22 Mfalme Yoashi aliyasahau mema yote aliyotendewa na Yehoyada, baba yake Zekaria, akamuua mwanawe. Alipokuwa anakufa, alisema, “Mwenyezi-Mungu na ayaone matendo yenu, akalipize kisasi.”

23 Mwishoni mwa mwaka, jeshi la Washamu lilishambulia Yerusalemu na Yuda. Waliwaua wakuu wote, wakateka nyara nyingi na kumpelekea mfalme wa Damasko.

24 Hata ingawa jeshi la Shamu lilikuwa dogo, Mwenyezi-Mungu alilipa ushindi dhidi ya jeshi kubwa la watu wa Yuda kwa sababu hao watu wa Yuda walikuwa wamemwacha Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zao. Hivyo, Washamu wakatekeleza adhabu ya Mungu juu ya mfalme Yoashi.

25 Maadui walipoondoka, walimwacha akiwa amejeruhiwa vibaya sana, maofisa wake wakala njama wakamwulia kitandani mwake, kulipiza kisasi mauaji ya mwana wa kuhani Yehoyada. Alizikwa katika mji wa Daudi, lakini si kwenye makaburi ya wafalme.

26 Watu waliomfanyia njama walikuwa Zabadi mwana wa mwanamke Mwamoni jina lake Shimeathi, na Yehozabadi mwana wa mwanamke Mmoabu jina lake Shimrithi.

27 Habari za wanawe Yoashi za kuirekebisha nyumba ya Mwenyezi-Mungu na unabii wote juu yake, zimeandikwa katika Maelezo ya Kitabu cha Wafalme. Amazia mwanawe alitawala baada yake.

25

1 Amazia alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala, akatawala kwa muda wa miaka ishirini na mitano katika Yerusalemu. Mama yake aliitwa Yehoadani wa Yerusalemu.

2 Alitenda yaliyo mema mbele ya Mwenyezi-Mungu ingawa hakuyatenda kwa moyo mnyofu.

3 Mara tu Amazia alipojiimarisha mamlakani aliwaua watumishi waliomuua mfalme baba yake.

4 Lakini hakuwaua watoto wao, kama ilivyoandikwa katika sheria zilizomo katika kitabu cha Mose, ambapo Mwenyezi-Mungu anasema: “Wazazi hawatauawa kwa ajili ya watoto wao, wala watoto hawatauawa kwa ajili ya wazazi wao; bali kila mtu atauawa kwa ajili ya dhambi zake mwenyewe.”

5 Mfalme Amazia aliwakusanya wanaume wa makabila ya Yuda na Benyamini, akawapanga katika vikosi mbalimbali kulingana na koo zao, akawaweka chini ya makamanda wa maelfu na wa mamia. Alipowakagua wale wenye umri wa miaka ishirini na zaidi, alipata jumla ya watu 300,000. Wote walikuwa watu wateule, tayari kwa vita, hodari wa kutumia mikuki na ngao.

6 Tena, alikodisha askari wengine mashujaa 1,000 kutoka Israeli, kwa gharama ya kilo 3,000 za fedha.

7 Lakini mtu wa Mungu alimwendea, akamwambia, “Ee mfalme, usiende vitani pamoja na hawa askari wa Israeli, maana Mwenyezi-Mungu hayuko pamoja na watu wa Israeli. Hayuko pamoja na hawa Waefraimu wote.

8 Bali, hivyo, hata ukiwa hodari vitani, Mungu atakufanya ushindwe na maadui, kwa kuwa Mungu ana nguvu kumpa binadamu ushindi au kumfanya binadamu ashindwe.”

9 Amazia akamwuliza huyo mtu wa Mungu, “Tutafanyaje na fedha yote ambayo nimekwisha wapa wanajeshi wa Israeli?” Naye akamjibu, “Mwenyezi-Mungu anaweza kukupa zaidi ya hiyo.”

10 Hapo Amazia akawaachia wanajeshi waliotoka Efraimu warudi makwao. Basi wakarejea kwao wakiwa wamewakasirikia sana watu wa Yuda.

11 Amazia alijipa moyo akaliongoza jeshi lake hadi Bonde la Chumvi. Hapo akapigana na kuwaua watu 10,000 wa Seiri.

12 Waliteka watu 10,000, wakawapandisha juu ya jabali na kuwatupa chini miambani, wakapondeka vipandevipande.

13 Wakati huohuo, wale wanajeshi Waisraeli ambao Amazia aliwaachia warudi kwao akiwakataza wasiandamane naye vitani, walikwenda na kuishambulia miji ya Yuda, toka Samaria hadi Beth-horoni, wakaua watu 3,000 na kuteka nyara nyingi.

14 Amazia aliporejea baada ya kuwashinda Waedomu, alileta miungu ya Waedomu akaifanya kuwa miungu yake, akaisujudia na kuifukizia ubani.

15 Haya yalimkasirisha sana Mwenyezi-Mungu, akatuma nabii kwa Amazia. Nabii huyo akamwuliza Amazia, “Kwa nini unategemea miungu ya watu wengine ambayo hata haikuweza kuwaokoa watu wake wenyewe kutoka mikononi mwako?”

16 Lakini hata kabla hajamaliza kusema, Amazia alimkata kauli akamwambia, “Nyamaza! Tulikufanya lini mshauri wa mfalme? Wataka kuuawa?” Nabii akanyamaza, lakini akasema, “Ninafahamu kuwa Mungu ameamua kukuangamiza kwa maana umetenda haya yote, kisha unapuuza shauri langu.”

17 Basi, Amazia mfalme wa Yuda alifanya shauri, akatuma ujumbe kwa Yehoashi, mwana wa Yehoahazi, mwana wa Yehu mfalme wa Israeli, akamwambia, “Njoo tupambane.”

18 Lakini Yoashi mfalme wa Israeli alimpelekea ujumbe Amazia akisema, “Siku moja, mchongoma wa Lebanoni uliuambia mwerezi wa hukohuko Lebanoni, ‘Mwoze binti yako kwa mwanangu!’ Lakini mnyama mmoja wa mwituni akapita hapo na kuukanyagakanyaga mchongoma huo.

19 Sasa wewe Amazia unasema, ‘Nimewaua Waedomu;’ na moyo unakufanya ujivune. Basi, kaa nyumbani mwako; ya nini kujitafutia taabu zitakazokuangamiza wewe mwenyewe pamoja na watu wako wa Yuda?”

20 Lakini Amazia hakujali kwa kuwa lilikuwa kusudi la Mungu ili awaweke mkononi mwa maadui zao kwa sababu alitegemea miungu ya Edomu.

21 Kwa hiyo, Yehoashi, mfalme wa Israeli alitoka akakabiliana uso kwa uso na Amazia, mfalme wa Yuda, huko vitani Beth-shemeshi, nchini Yuda.

22 Watu wa Yuda walishindwa na watu wa Israeli na kila mmoja alirudi nyumbani kwake.

23 Halafu Yehoashi mfalme wa Israeli alimteka Amazia mfalme wa Yuda, mwana wa Yoashi, mwana wa Ahazia huko Beth-shemeshi, akampeleka hadi Yerusalemu. Huko, aliubomoa ukuta wa mji huo, kuanzia Lango la Efraimu mpaka Lango la Pembeni, umbali wa karibu mita 200.

24 Alichukua dhahabu yote na fedha hata na vifaa vyote vilivyokuwa katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu chini ya ulinzi wa Obed-edomu; pia alichukua hazina ya ikulu na mateka kisha akarudi Samaria.

25 Amazia mfalme wa Yuda aliishi miaka kumi na mitano baada ya kifo cha mfalme Yehoashi mwana wa Yehoahazi mfalme wa Israeli.

26 Matendo mengine yote ya Amazia kutoka mwanzo hadi mwisho yameandikwa katika Kitabu cha Habari za Wafalme wa Yuda na Israeli.

27 Njama za kumuua Amazia zilifanywa Yerusalemu tangu alipomwacha Mwenyezi-Mungu, kwa hiyo alikimbilia Lakishi. Lakini maadui walituma watu Lakishi wakamuua huko.

28 Maiti yake ililetwa juu ya farasi, na kuzikwa kwenye makaburi ya kifalme katika mji wa Daudi.

26

1 Kisha watu wote wa Yuda wakamchukua Uzia mwanawe Amazia akiwa mwenye umri wa miaka kumi na sita, wakamtawaza mahali pa Amazia baba yake.

2 Halafu baada ya kifo cha baba yake aliujenga upya mji wa Elothi na kuurudisha kwa Yuda.

3 Uzia alianza kutawala akiwa na umri wa miaka kumi na sita; akatawala kwa muda wa miaka hamsini na miwili huko Yerusalemu. Mama yake alikuwa Yekolia wa Yerusalemu.

4 Alitenda mema mbele ya Mwenyezi-Mungu kama baba yake.

5 Alimtumikia Mwenyezi-Mungu kwa uaminifu wakati wa kuishi kwa Zekaria, aliyemfundisha kumtii Mungu. Kadiri alivyomtafuta Mungu, Mungu alimfanikisha.

6 Uzia aliondoka akapiga vita dhidi ya Wafilisti, akazibomoa kuta za miji ya Gathi, Yabne na Ashdodi. Akajenga miji katika eneo la Ashdodi na kwingineko nchini Filistia.

7 Mungu alimsaidia kuwashinda Wafilisti, Waarabu waliokaa Gurbaali na Wameuni.

8 Waamoni walimlipa kodi, na sifa zake zikaenea hadi Misri, kwa sababu alipata nguvu.

9 Tena Uzia alijenga minara katika Yerusalemu penye Lango la Pembeni, Lango la Bondeni na Pembeni na kuiimarisha.

10 Hata nyikani pia alijenga minara, akachimba mabwawa mengi, maana alikuwa na mifugo mingi kwenye sehemu za miinuko na tambarare. Alikuwa na wakulima wa watunza mizabibu milimani, na katika ardhi yenye rutuba kwani alipenda kilimo.

11 Zaidi ya hayo, Uzia alikuwa na jeshi lililojiandaa tayari kwa vita. Lilikuwa limegawanywa katika vikosi mbalimbali, na orodha yao iliwekwa na katibu Yeieli, na Maaseya, ofisa, nao wote walikuwa chini ya uongozi wa Hanania, mmoja wa makamanda wake mfalme.

12 Jumla, viongozi wote wa majeshi walikuwa 2,600.

13 Chini yao, kulikuwa na jeshi la askari 307,500, wenye uwezo mkubwa wa kukabiliana na adui yeyote wa mfalme.

14 Uzia aliwapa askari hao ngao, mikuki, kofia za chuma, deraya, pinde na mawe kwa ajili ya kupiga kwa kombeo.

15 Huko Yerusalemu mafundi wake walimtengenezea mitambo ya kurushia mishale na mawe makubwamakubwa. Sifa zake zilienea kila mahali, nguvu zake zikaongezeka zaidi kwa sababu ya msaada mwingi alioupata kutoka kwa Mungu.

16 Wakati mfalme Uzia alipokuwa na nguvu, alijaa kiburi ambacho kilisababisha maangamizi yake. Alimwasi Mwenyezi-Mungu, Mungu wake kwa kuingia hekaluni akikusudia kufukiza ubani madhabahuni.

17 Lakini kuhani Azaria, pamoja na makuhani wengine mashujaa themanini, wakamfuata mfalme

18 na kumzuia. Wakamwambia, “Si wajibu wako hata kidogo Uzia, kumfukizia Mwenyezi-Mungu ubani. Ni makuhani tu wa uzao wa Aroni ambao wamewekwa wakfu kufukiza ubani. Ondoka mahali hapa patakatifu. Umemkosea Mwenyezi-Mungu na hutapata heshima yoyote kutoka kwake.”

19 Wakati huo, Uzia alikuwa amesimama hekaluni karibu na madhabahu, ameshikilia chetezo cha kufukizia ubani mkononi. Aliwakasirikia makuhani; na mara alipofanya hivyo, akashikwa na ukoma katika paji la uso wake mbele ya makuhani hao.

20 Azaria, kuhani mkuu, na wale makuhani wengine, walimtazama, kisha wakaharakisha kumtoa nje; hata yeye mwenyewe akafanya haraka kutoka, kwa maana Mwenyezi-Mungu alikuwa amemwadhibu.

21 Basi, mfalme Uzia akawa na ukoma mpaka siku ya kufa kwake. Alikaa katika nyumba yake ya pekee kwani hakukubaliwa tena kuingia katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu. Naye Yothamu mtoto wake, akatunza jamaa yake huku akitawala wakazi wa nchi.

22 Matendo mengine yote ya mfalme Uzia kutoka mwanzo mpaka mwisho, yaliandikwa na nabii Isaya mwana wa Amozi.

23 Uzia alifariki na kuzikwa katika eneo la kuzikia wafalme, kwa sababu walisema, “Yeye ana ukoma”. Naye Yothamu mwanawe, akatawala mahali pake.

27

1 Yothamu alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala, alitawala kwa muda wa miaka kumi na sita huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Yerusha binti Sadoki.

2 Alitenda mema mbele ya Mwenyezi-Mungu kama alivyofanya Uzia baba yake; isipokuwa yeye hakuingia katika hekalu la Mwenyezi-Mungu nao watu waliendelea kufanya maovu.

3 Yothamu alijenga Lango la Kaskazini la nyumba ya Mwenyezi-Mungu na kushughulika sana na ujenzi wa ukuta sehemu ya Ofeli.

4 Alijenga miji kwenye nchi ya milima ya Yuda, na kwenye misitu, akajenga ngome na minara katika milima yenye misitu.

5 Alipigana vita dhidi ya mfalme wa Amoni na kuwashinda. Katika mwaka huo Waamoni walimtolea ushuru wa kilo 3,400, tani 1,000 za ngano na kilo 1,000 za shayiri; waliendelea kufanya hivyo katika mwaka wa pili na wa tatu.

6 Mfalme Yothamu aliendelea kuwa mwenye nguvu, kwa sababu aliishi kwa kumtii Mwenyezi-Mungu, Mungu wake.

7 Matendo mengine ya Yothamu, vita vyake na maongozi yake, yote yameandikwa katika Kitabu cha Habari za Wafalme wa Israeli na Yuda.

8 Yothamu alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala, akatawala kwa muda wa miaka kumi na sita huko Yerusalemu.

9 Alifariki na kuzikwa katika mji wa Daudi. Naye Ahazi mwanawe akatawala mahali pake.

28

1 Ahazi alianza kutawala akiwa na umri wa miaka ishirini; alitawala kwa muda wa miaka kumi na sita huko Yerusalemu. Yeye, hakufuata mfano mzuri wa Daudi babu yake, bali alitenda maovu mbele ya Mwenyezi-Mungu,

2 na kufuata mienendo ya wafalme wa Israeli. Isitoshe, alitengeneza hata sanamu za kusubu za Mabaali,

3 akafukiza ubani kwenye Bonde la mwana wa Hinomu na kuwateketeza wanawe kama tambiko, akiiga desturi za kuchukiza za watu ambao walifukuzwa na Mwenyezi-Mungu wakati Waisraeli walipokuwa wanaingia nchini.

4 Alitoa tambiko na kufukiza ubani mahali pa kuabudia miungu mingine, vilimani na chini ya kila mti wenye majani mabichi.

5 Mwenyezi-Mungu, Mungu wake, alimwacha mfalme Ahazi ashindwe na mfalme wa Aramu ambaye pia alichukua mateka watu wake wengi, akarudi nao Damasko. Kadhalika, alimfanya ashindwe na Peka, mwana wa Remalia, mfalme wa Israeli, ambaye alimshinda na kuua watu wengi sana.

6 Aliua askari mashujaa wa Yuda 120,000 katika siku moja. Ilitokea hivyo kwa sababu walimwacha Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zao.

7 Zikri, askari mmoja shujaa wa Israeli, alimuua Maaseya, mwana wa mfalme, Azrikamu, kamanda wa Ikulu, na Elkana aliyekuwa mtu wa pili chini ya mfalme.

8 Jeshi la Israeli lilichukua mateka ndugu zao watu laki mbili wakiwemo wanawake na watoto. Waliwachukua hadi Samaria pamoja na mali nyingi waliyoteka nyara.

9 Baadaye kidogo mtu mmoja, jina lake Odedi, nabii wa Mwenyezi-Mungu, alikuwa anakaa Samaria. Yeye alitoka kuwalaki wanajeshi wa Israeli pamoja na mateka wao wa Yuda walipokuwa karibu kuingia Samaria, akawaambia, “Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zenu, alikuwa amewakasirikia watu wa Yuda, ndiyo maana akawatia mikononi mwenu lakini mmewaua kwa hasira. Tendo hilo limefika mbinguni.

10 Sasa mnanuia kuwafanya wanaume na wanawake wa Yuda na Yerusalemu watumwa wenu. Je, hamtambui ya kuwa nyinyi pia mmetenda dhambi dhidi ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu?

11 Sasa sikieni yale nisemayo: Warudisheni ndugu zenu na dada zenu mliowateka, maana ghadhabu kali ya Mwenyezi-Mungu iko juu yenu.”

12 Nao wakuu fulani wa Efraimu, Azaria mwana wa Yohanani, Berekia mwana wa Meshilemothi, Yehizkia mwana wa Shalumu na Amasa mwana wa Hadlai, pia waliwashutumu hao waliotoka vitani.

13 Wakawaambia, “Msiwalete humu mateka hao, kwa sababu mnanuia kutuletea hatia mbele ya Mwenyezi-Mungu; tendo hili huku litakuwa nyongeza ya dhambi yetu na hatia yetu; kwa sababu hatia yetu tayari ni kubwa na kuna ghadhabu kali juu ya Israeli.”

14 Hivyo, wanajeshi waliwaacha mateka wao na nyara zote mbele ya wakuu na mkutano wote.

15 Wale wakuu waliotajwa majina yao waliwachukua mateka na kwa kutumia nyara wakawavika mateka ambao hawakuwa na nguo; waliwapatia ndara, chakula na vinywaji, na kuwapaka mafuta. Wale ambao walikuwa hawajiwezi, wakawabeba kwa punda, wakawachukua mateka wote hadi Yeriko, mji wa mitende, kwa ndugu zao; kisha wao wakarudi Samaria.

16 Wakati huo, mfalme Ahazi alituma wajumbe kwa mfalme wa Ashuru kuomba msaada,

17 kwa sababu Waedomu walikuwa wamekuja tena, wakaivamia nchi ya Yuda, wakawashinda na kuchukua mateka wengi.

18 Wakati huohuo pia, Wafilisti walikuwa wakiishambulia miji ya Shefela na Negebu ya Yuda. Waliiteka miji ya Beth-shemeshi, Ayaloni, Gederothi, Soko na vijiji vyake, Timna na vijiji vyake, Gimzo na vijiji vyake, wakafanya makao yao huko.

19 Kwa sababu mfalme Ahazi wa Israeli alikuwa na ukatili kwa watu wake, na alikosa uaminifu kwa Mwenyezi-Mungu, Mwenyezi-Mungu aliwafanya watu wa Yuda wakose nguvu.

20 Tiglath-pileseri, mfalme wa Ashuru alimshambulia badala ya kumtia nguvu.

21 Ahazi alichukua dhahabu kutoka katika nyumba ya Mungu, kutoka ikulu na nyumba za wakuu, akampa mfalme wa Ashuru kama kodi; lakini hili pia halikumsaidia kitu.

22 Wakati alipokuwa taabuni zaidi, mfalme huyu Ahazi alizidi kumwasi Mwenyezi-Mungu.

23 Maana aliitolea tambiko miungu ya Damasko iliyokuwa imemshinda vitani akisema, “Maadamu miungu ya Shamu iliwasaidia wafalme wa Shamu, nikiitolea tambiko huenda ikanisaidia nami pia.” Lakini hiyo ilisababisha kuangamia kwake na taifa lote la Israeli.

24 Zaidi ya hayo, alivikusanya vifaa vyote vya nyumba ya Mungu, akavikatakata vipandevipande, kisha akaifunga milango ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu na kujijengea madhabahu katika kila pembe ya Yerusalemu.

25 Na katika kila mji wa Yuda, alitengeneza mahali pa kufukizia ubani miungu mingine. Kwa kutenda hivyo, alimkasirisha Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zake.

26 Matendo yake mengine na mienendo yake yote, kutoka mwanzo hadi mwisho, yameandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Yuda na Israeli.

27 Mfalme Ahazi alifariki, akazikwa mjini Yerusalemu, lakini si katika makaburi ya wafalme wa Israeli. Naye Hezekia mwanawe, akatawala mahali pake.

29

1 Hezekia alianza kutawala Yuda akiwa na umri wa miaka ishirini na mitano, akatawala huko Yerusalemu kwa muda wa miaka ishirini na tisa. Mama yake alikuwa Abiya binti Zekaria.

2 Alitenda mema mbele ya Mwenyezi-Mungu, kama vile alivyofanya Daudi, babu yake.

3 Mnamo mwezi wa kwanza wa mwaka wa kwanza wa utawala wake, mfalme Hezekia aliifungua tena milango ya hekalu, akaitengeneza.

4 Aliwaingiza makuhani na Walawi, kisha akawakusanya uani upande wa mashariki,

5 akawaambia, “Nisikieni enyi Walawi! Jitakaseni na itakaseni nyumba ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zenu. Toeni uchafu wote uliomo patakatifu.

6 Kwa maana babu zetu waliasi na kutenda maovu mbele ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu. Wamemwacha, wakageuzia mbali nyuso zao na kupawekea kisogo mahali aishipo Mwenyezi-Mungu.

7 Tena, waliifunga milango ya ukumbi, wakazizima taa, na hawajafukiza ubani wala kutoa tambiko za kuteketeza katika mahali patakatifu pa Mungu wa Israeli.

8 Kwa sababu hii, Mwenyezi-Mungu aliikasirikia sana Yuda na Yerusalemu, na yale aliyowatenda yamewashangaza na kuwaogofya watu wote, wakawazomea. Haya yote mmeyaona wenyewe kwa macho yenu.

9 Baba zetu waliuawa vitani, na wana wetu na binti zetu na wake zetu ni mateka kwa sababu hiihii.

10 Sasa, nimeamua kwa dhati kufanya agano na Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, ili asitukasirikie zaidi.

11 Basi wanangu, muwe na nidhamu. Mwenyezi-Mungu amewachagua nyinyi ili mumtumikie, muwaongoze watu wake katika ibada, na kumfukizia ubani.”

12 Walawi wafuatao wakaanza kazi: Kutoka ukoo wa Kohathi walikuwa Mahathi mwana wa Amasai na Yoeli mwana wa Azaria; ukoo wa Merari: Kishi mwana wa Abdi na Azaria mwana wa Yehaleli; ukoo wa Gershoni: Yoa mwana wa Zima, na Edeni mwana wa Yoa;

13 ukoo wa Elisafani: Shimori na Yeneli,

14 ukoo wa Hemani: Zekaria na Matania; ukoo wa Yeduthuni: Shemaya na Uzieli.

15 Hawa waliwakusanya Walawi wenzao, wakajitakasa. Kisha wakaingia kama walivyotakiwa kufanya na mfalme, wakaanza kusafisha nyumba ya Mwenyezi-Mungu kama Mwenyezi-Mungu alivyoagiza.

16 Makuhani waliingia katika sehemu ya ndani ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu, wakautoa uchafu wote uliokuwemo, wakauweka uani. Kutoka hapo, Walawi waliuchukua uchafu huo mpaka nje kwenye Bonde la Kidroni.

17 Walianza kazi ya kulitakasa hekalu siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, na kufikia siku ya nane, wakawa wamekwisha maliza kazi yote, hata na ukumbini. Kisha, walifanya kazi kwa muda wa siku nane zaidi hadi siku ya kumi na sita ya mwezi huo, kila kitu kilikamilika.

18 Baadaye, Walawi walimwendea mfalme Hezekia wakamwambia, “Tumekwisha litakasa hekalu lote pamoja na madhabahu ya tambiko za kuteketeza na vyombo vyake vyote, na meza ya mikate mitakatifu na vyombo vyake vyote.

19 Tena, vyombo vyote ambavyo mfalme Ahazi alivyoviondoa wakati wa utawala wake, hapo alipoasi, tumevirudisha na kuviweka wakfu. Vyote vipo mbele ya madhabahu ya Mwenyezi-Mungu.”

20 Mapema kesho yake, mfalme Hezekia aliwakusanya wakuu wa mji, akaenda nao katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu.

21 Wakaleta mafahali saba, kondoo madume saba, wanakondoo saba na mbuzi madume saba, wawe sadaka ya kuondoa dhambi, kwa ajili ya jamaa ya kifalme, patakatifu na watu wa Yuda. Hapo, mfalme aliwaambia makuhani waliokuwa wazawa wa Aroni wawateketeze juu ya madhabahu ya Mwenyezi-Mungu.

22 Makuhani walichinja mafahali kwanza, kisha kondoo madume, halafu wanakondoo na kila mara walichukua damu ya wanyama hao na kunyunyiza juu ya madhabahu.

23 Hatimaye, waliwaleta wale mbuzi madume wa sadaka ya kuondoa dhambi karibu na mfalme na watu wote waliokuwamo, nao wakaweka mikono yao juu ya hao mbuzi madume.

24 Basi, wale makuhani wakawachinja, na kunyunyiza damu yao juu ya madhabahu ili iwe tambiko ya upatanisho kwa Waisraeli wote, kwa maana mfalme Hezekia alikuwa ameagiza itolewe sadaka ya kuteketeza na sadaka ya kuondoa dhambi kwa ajili ya Israeli yote.

25 Mfalme Hezekia aliyafuata maagizo ambayo Mwenyezi-Mungu alikuwa amempa mfalme Daudi kwa njia ya Gadi mwonaji wa mfalme na nabii Nathani. Hivyo basi, akaweka Walawi katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu, baadhi yao wakiwa na matoazi, wengine vinanda na wengine vinubi. Hiyo ilikuwa amri ya Mwenyezi-Mungu kwa njia ya manabii wake.

26 Walawi walisimama na vyombo vya muziki vya Daudi, pia makuhani walisimama wakiwa na tarumbeta zao.

27 Basi, Hezekia akaamuru sadaka ya kuteketeza itolewe juu ya madhabahu. Mara tu tambiko hiyo ilipoanza kutolewa, watu walianza kumsifu Mwenyezi-Mungu kwa nyimbo zilizoandamana na mlio wa tarumbeta na vyombo vya muziki vya Daudi mfalme wa Israeli.

28 Watu wote waliokuwamo walishiriki katika ibada. Waimbaji waliendelea kuimba, na tarumbeta zikaendelea kupigwa hadi shughuli za utoaji wa sadaka hiyo ya kuteketeza ilipokamilika.

29 Hatimaye, mfalme Hezekia pamoja na watu wote waliokuwamo waliinama, wakamwabudu Mwenyezi-Mungu.

30 Kisha mfalme Hezekia na viongozi wakawaambia Walawi wamsifu Mwenyezi-Mungu kwa nyimbo alizotunga mfalme Daudi na mwonaji Asafu. Basi, watu wote wakamtukuza Mungu kwa furaha, na kumsujudia.

31 Ndipo Hezekia akawaambia watu, “Maadamu sasa mmekwisha jitakasa, karibieni, leteni sadaka na matoleo ya shukrani katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu.” Basi, watu wakaleta sadaka zao na matoleo yao ya shukrani, na tambiko za kuteketeza.

32 Sadaka za kuteketeza walizoleta jumla zilikuwa mafahali 70, kondoo madume 100 na wanakondoo 200. Zote hizo zilikuwa sadaka za kuteketeza kwa Mwenyezi-Mungu.

33 Matoleo matakatifu yalikuwa mafahali 600 na kondoo 3,000.

34 Kwa vile ambavyo idadi ya makuhani ilikuwa ndogo, hawakuweza kuwachuna wanyama hao wote. Kwa hiyo, ndugu zao Walawi waliwasaidia hadi walipokamilisha kazi hiyo. Wakati huo, makuhani wengine zaidi walikuwa wamekwisha jitakasa. (Walawi walijiweka katika hali ya usafi zaidi kuliko makuhani.)

35 Mbali na wingi wa sadaka za kuteketeza, kulikuwako pia mafuta ya sadaka ya amani, hata kulikuwapo sadaka ya kinywaji kwa sadaka za kuteketeza. Hivyo basi, huduma za ibada zikaanzishwa tena hekaluni.

36 Mfalme Hezekia na watu wote wakajawa na furaha tele kwa sababu ya yote Mungu aliyowatendea watu; maana tukio hili lilitokea ghafla.

30

1 Mfalme Hezekia aliwatumia ujumbe watu wote wa Israeli na Yuda, na pia akawaandikia barua wenyeji wa Efraimu na Manase, akiwaalika wote waje katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu Yerusalemu, ili kuiadhimisha sikukuu ya Pasaka kwa heshima yake Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli.

2 Mfalme, viongozi na watu wote wa mji wa Yerusalemu waliafikiana kuiadhimisha sikukuu hiyo ya Pasaka mnamo mwezi wa pili

3 badala ya mwezi wa kwanza kama ilivyokuwa kawaida, kwa sababu idadi ya makuhani waliokuwa wamekwisha kujiweka wakfu ilikuwa ndogo, nao watu walikuwa bado hawajakusanyika Yerusalemu.

4 Aidha, mpango huu ulimridhisha mfalme pamoja na watu wote waliokuwa wamekusanyika.

5 Kwa hiyo waliamua kutoa tangazo kote nchini Israeli, kutoka Beer-sheba hadi Dani, kwamba watu waje Yerusalemu kuiadhimisha sikukuu ya Pasaka ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli. Ulikuwa umepita muda mrefu kabla watu hawajaiadhimisha Pasaka kulingana na sheria zake.

6 Matarishi, kwa amri yake mfalme na maofisa wake, walipeleka barua kote nchini Israeli na Yuda. Barua hizo zilikuwa na ujumbe ufuatao: “Enyi watu wa Israeli mlionusurika baada ya mashambulizi ya wafalme wa Ashuru. Mrudieni Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Abrahamu, Isaka na Israeli, ili naye apate kuwarudieni.

7 Msiwe kama babu zenu na ndugu zenu ambao hawakuwa waaminifu kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zao, ambaye kama mnavyoona aliwaadhibu vikali.

8 Msiwe wakaidi kama babu zenu, ila mtiini Mwenyezi-Mungu. Njoni katika hekalu lake ambalo amelitakasa milele, mumwabudu Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, ili asiwakasirikie.

9 Mkimrudia Mwenyezi-Mungu, wale ambao waliwateka ndugu zenu na watoto wenu, watawahurumia na kuwaacha warudi katika nchi hii. Kwa maana Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, ni mwenye rehema na huruma, naye atawapokea ikiwa mtamrudia.”

10 Basi, matarishi hao wakaenda toka mji mmoja hadi mwingine kote nchini Efraimu na Manase, wakafika hata Zebuluni. Lakini watu waliwacheka na kuwadhihaki.

11 Hata hivyo, watu wachache miongoni mwa makabila ya Asheri, Manase na Zebuluni, walijinyenyekesha wakaja Yerusalemu.

12 Nguvu ya Mungu ilikuwa ikifanya kazi katika Yuda, akawapa moyo kutii amri za mfalme na maofisa wake kadiri ya maagizo ya Mwenyezi-Mungu.

13 Watu wengi sana walijumuika mjini Yerusalemu mnamo mwezi wa pili, kuiadhimisha sikukuu ya mikate isiyotiwa chachu.

14 Walianza kazi, wakaziondoa madhabahu zote zilizokuwa Yerusalemu, na nyingine zote zilizotumiwa kufukizia ubani, wakazibeba na kuzitupa katika Bonde la Kidroni.

15 Siku ya kumi na nne ya mwezi huo walichinja mwanakondoo wa Pasaka. Makuhani na Walawi waliona aibu, wakajitakasa na kuleta sadaka za kuteketeza katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu.

16 Walichukua nafasi zao hekaluni kulingana na maagizo yaliyokuwamo katika sheria za Mose, mtu wa Mungu. Walawi waliwapa makuhani damu ya tambiko, nao wakainyunyiza madhabahuni.

17 Kwa vile wengi wa wale waliokusanyika hapo hawakuwa wamejitakasa, iliwabidi Walawi kuwachinjia wanakondoo wa Pasaka na kuwaweka wakfu kwa Mwenyezi-Mungu.

18 Aidha miongoni mwa kusanyiko hilo la watu, wengi wa wale waliotoka Efraimu, Manase, Isakari na Zebuluni, walikuwa wakiiadhimisha Pasaka kinyume cha maagizo. Hii ni kwa kuwa mfalme Hezekia aliwaombea akisema, “Mwenyezi-Mungu uliye mwema, msamehe yeyote yule

19 atakayekuomba kwa moyo wake wote wewe Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zake, hata ingawa si msafi kulingana na sheria za utakaso.”

20 Mwenyezi-Mungu alikubali ombi la Hezekia, akawasamehe watu hao.

21 Waisraeli wote waliokuwa wamekusanyika mjini Yerusalemu waliiadhimisha sikukuu ya mikate isiyotiwa chachu kwa muda wa siku saba, wakiwa na furaha kubwa. Walawi na makuhani walimsifu Mwenyezi-Mungu kila siku, walimwimbia kwa nguvu zao zote.

22 Mfalme Hezekia aliwasifu na kuwatia moyo makuhani kwa kuwa waliendesha ibada kwa ujuzi mwingi. Baada ya kumaliza siku saba wakati ambao watu walikula, wakatoa sadaka za amani na kumtukuza Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zao,

23 watu waliamua kwa kauli moja kuziendeleza sherehe kwa muda wa siku saba zaidi. Basi, wakaendelea kusherehekea kwa furaha kuu kwa muda wa siku saba zaidi.

24 Mfalme Hezekia wa Yuda aliwapa watu waliokusanyika jumla ya mafahali 1,000 na kondoo 7,000. Hali kadhalika, wakuu wakawapa mafahali 1,000 na kondoo 10,000. Idadi kubwa ya makuhani walijitakasa.

25 Kila mtu aliyehudhuria alifurahi sana. Watu wote wa Yuda, makuhani na Walawi, wakazi wa Yerusalemu waliohudhuria, wageni waliotoka nje ya Yerusalemu na wale walioishi Yuda, wote walifurahi sana.

26 Kukawa na furaha kuu mno Yerusalemu, maana tangu enzi ya mfalme Solomoni mwana wa Daudi, mfalme wa Israeli, jambo kama hilo lilikuwa halijatokea Yerusalemu.

27 Kisha, makuhani na Walawi wakawaombea watu baraka zake Mwenyezi-Mungu, naye katika makao yake matakatifu huko mbinguni akayasikia maombi yao na kuyakubali.

31

1 Baada ya sherehe kumalizika, watu wote wa Israeli walikwenda katika kila mji wa Yuda, wakavunjavunja nguzo za mawe na kuzikatakata sanamu za Ashera, mungu wa kike, na pia wakaziharibu madhabahu na mahali pa kuabudia miungu mingine. Walifanya vivyo hivyo kote katika Yuda, Benyamini, Efraimu na Manase, mpaka walipokwisha kuharibu vyote. Kisha wakarudi mjini mwao, kila mtu kwenye milki yake.

2 Mfalme Hezekia aliwapanga tena makuhani na Walawi katika makundi, akampa kila mmoja wao wajibu maalumu, kuhudumu katika sehemu mbalimbali za hekalu la Mwenyezi-Mungu. Wajibu huo ni pamoja na utoaji wa sadaka za kuteketeza na za amani, kushukuru na kusifu.

3 Kutokana na mali yake mwenyewe, mfalme alitoa sehemu kwa ajili ya sadaka za kuteketezwa asubuhi na jioni, sadaka za siku ya Sabato na wakati wa sherehe za kuadhimisha mwezi mwandamo na zile sikukuu nyingine zilizoamriwa kulingana na sheria ya Mwenyezi-Mungu.

4 Zaidi ya hayo, mfalme aliwaambia wenyeji wa Yerusalemu watoe sehemu waliyostahili kupewa makuhani na Walawi, ili wao wajitolee kikamilifu katika shughuli za sheria za Mwenyezi-Mungu.

5 Mara tu amri hii ilipotolewa, watu wa Israeli walitoa kwa wingi, malimbuko ya nafaka, divai, mafuta, asali na mazao mengine mbalimbali ya shambani, na pia zaka nyingi za kila kitu.

6 Watu wa Israeli na Yuda walioishi katika miji ya Yuda, pia wakaleta zaka zao za ng'ombe na kondoo na vitu vingine, wakaviweka wakfu kwa Mwenyezi-Mungu. Waliviweka vitu hivyo katika mafungu.

7 Katika mwezi wa tatu walianza kuvipanga katika mafungu, wakamaliza mnamo mwezi wa saba.

8 Mfalme Hezekia na maofisa wake walipokuja kuyaona mafungu hayo, walimtukuza Mwenyezi-Mungu na watu wake wa Israeli.

9 Mfalme Hezekia aliwauliza makuhani na Walawi kuhusu mafungu hayo.

10 Azaria, kuhani mkuu aliyekuwa wa uzao wa Sadoki akamjibu, “Tangu watu waanze kuleta matoleo yao hekaluni, tumekuwa na vyakula vya kutosha na hata tunayo akiba kubwa. Mwenyezi-Mungu amewabariki watu wake, ndiyo maana tumepata vitu hivi vyote.”

11 Kisha mfalme Hezekia akawaamuru watengeneze ghala katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu. Wakatengeneza;

12 na humo wakaweka matoleo, zaka na vyote vilivyowekwa wakfu, kwa uaminifu. Wakamweka Konania, Mlawi, awe ofisa mkuu mtunzaji wa vitu hivyo, na Shimei nduguye, awe msaidizi wake.

13 Nao Yehieli, Azazia, Nahathi, Asaheli, Yeremothi, Yozabadi, Elieli, Ismakia, Mahathi na Benaya, waliwekwa wawe wasimamizi chini ya uongozi wa Konania na Shimei nduguye. Hawa wote walichaguliwa na mfalme Hezekia na Azaria, ofisa mkuu wa nyumba ya Mungu.

14 Kore mwana wa Imna, Mlawi, aliyekuwa bawabu wa Lango la Mashariki la hekalu, alisimamia matoleo yote ya hiari kwa Mungu, na ugawaji wa matoleo kwa ajili ya Mwenyezi-Mungu na sadaka zilizo takatifu kabisa.

15 Nao Edeni, Miniamini, Yeshua, Shemaya, Amaria na Shekania, walimsaidia kufanya kazi hiyo kwa uaminifu katika ile miji mingine walimoishi makuhani. Waliwagawia ndugu zao Walawi vyakula, wakubwa kwa wadogo.

16 Tena, bila kujali koo walimoandikishwa, waliwapa sehemu wale watoto wa kiume waliokuwa wametimiza umri wa miaka mitatu na zaidi, na ambao waliingia katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu kila siku kutekeleza wajibu wao. Kila mmoja wao alipata sehemu yake kulingana na huduma aliyotoa kwa zamu yake.

17 Makuhani waliandikishwa kulingana na jamaa zao, hali Walawi waliotimiza miaka ishirini na zaidi waliandikishwa kulingana na kazi zao na zamu zao.

18 Waliandikishwa wote pamoja na watoto wao wadogo, wake zao, wana wao na binti zao kwa kuwa, kwa mujibu wa kazi zao, walihitajika kujiweka katika hali ya utakaso kila mara.

19 Vilevile, miongoni mwa wazawa wa Aroni, makuhani waliokuwa wanakaa katika mashamba waliyomiliki kwa pamoja nje ya miji yao, mlikuwa watu maalumu kwenye miji hiyo ambao waliwagawia sehemu zao za vyakula. Waliwapa sehemu kila mwanamume katika jamaa za makuhani, na kila mmoja aliyekuwa ameandikishwa kati ya Walawi.

20 Hivyo ndivyo mfalme Hezekia alivyotenda yaliyo mema, ya haki na ya uaminifu mbele ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wake, kote nchini Yuda.

21 Kila kazi aliyoifanya katika utumishi wa nyumba ya Mungu au katika utekelezaji wa sheria na amri za Mungu ili kufuata uongozi kutoka kwake, alizifanya kwa moyo wake wote, naye akafanikiwa.

32

1 Baada ya mambo yote hayo ya uaminifu ya mfalme Hezekia, mfalme Senakeribu wa Ashuru aliivamia Yuda. Alikuja akapiga makambi kwenye miji yenye ngome akitumaini kwamba ataishinda iwe mali yake.

2 Mfalme Hezekia alipoona kwamba mfalme Senakeribu amekuja kwa kusudi la kuishambulia Yerusalemu,

3 aliamua, yeye pamoja na maofisa wake wakuu wa majeshi kuyafunga maji ya chemchemi zilizokuwa nje ya miji; nao wakamuunga mkono, wakamsaidia.

4 Wakawakusanya watu wengi pamoja wakazifunga chemchemi zote pamoja na kijito kilichopitia kati ya sehemu hiyo wakisema, “Ya nini kuwaachia wafalme wa Ashuru wakija wakute maji tele?”

5 Ili kuuhami mji, mfalme Hezekia alipiga moyo konde, akajenga upya ukuta wote uliokuwa umebomoka, na juu yake akajenga minara. Upande wa nje, akajenga ukuta mwingine wa pili, na akaiimarisha sehemu iliyoitwa Milo katika mji wa Daudi. Zaidi ya hayo alitengeneza silaha na ngao kwa wingi.

6 Aliwaweka watu wote mjini chini ya makamanda, kisha akawaamuru wakusanyike uwanjani penye Lango la Mji. Hapo akawatia moyo akisema,

7 “Muwe imara na hodari. Msiogope wala msifadhaike mbele ya mfalme wa Ashuru au majeshi yake maana tuliye naye ni mkuu kuliko aliye naye Senakeribu.

8 Yeye anazo nguvu za kibinadamu tu, hali sisi tunaye Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, kutusaidia na kutupigania vita vyetu.” Maneno haya ya mfalme Hezekia yaliwatia moyo sana watu hao.

9 Baada ya hayo, Senakeribu mfalme wa Ashuru, ambaye bado alikuwa ameuzingira mji wa Lakishi akiwa na majeshi yake yote, aliwatuma watumishi wake Yerusalemu kwa Hezekia mfalme wa Yuda na kwa watu wote wa Yuda waliokuwa Yerusalemu, akisema

10 “Hivi ndivyo anavyosema Senakeribu mfalme wa Ashuru: Je, mnategemea nini hata mnakaa Yerusalemu, mji ambao umezingirwa?

11 Je, si kana kwamba Hezekia anawadanganya ili awafanye mfe kwa njaa au kiu anapowaambia, ‘Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu atawaokoa mikononi mwa mfalme wa Ashuru?’

12 Je, siye huyu Hezekia aliyepaharibu mahali pake pa kuabudia na madhabahu zake na kuwaamuru watu wote wa Yuda na Yerusalemu akisema: ‘Mtaabudu mbele ya madhabahu moja, na juu yake mtateketeza sadaka zenu?’

13 Je, kwani hamjui yale yote ambayo mimi na babu zangu tumewatenda watu wote wa mataifa mengine? Je, miungu ya mataifa ya nchi hizo iliweza kuzikomboa nchi zao mkononi mwangu?

14 Ni mungu gani kati ya miungu ya mataifa hayo iliyoharibiwa kabisa na babu zangu aliyeweza kuwakomboa watu wake kutoka mikononi mwangu ndio nanyi muwe na tumaini ya kwamba Mungu wenu atawaokoeni mikononi mwangu?

15 Msidanganywe na Hezekia wala msishawishike kwa hayo. Msimwamini mtu huyu, kwa maana hapajatokea mungu wa taifa au mfalme yeyote aliyefaulu kuwakomboa watu wake kutoka mikononi mwa mfalme wa Ashuru, sembuse huyu Mungu wenu!”

16 Watumishi wa mfalme wa Ashuru walisema maneno mengine mengi mabaya dhidi ya Mwenyezi-Mungu, na dhidi ya Hezekia mtumishi wake.

17 Mfalme mwenyewe aliandika barua akamtukana na kumdharau Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, akisema, “Kama vile ambavyo miungu ya mataifa mengine haikuweza kuwaokoa watu wao kutoka mikononi mwangu, vivyo hivyo Mungu wa Hezekia hataweza kuwaokoa watu wake.”

18 Maofisa hao waliwaambia kwa sauti kubwa kwa lugha ya Kiebrania watu wa Yerusalemu waliokuwa ukutani, wakikusudia kuwatia hofu na woga ili wauteke mji kwa urahisi.

19 Wakazungumza juu ya Mungu wa Yerusalemu kana kwamba ni miungu ya mataifa mengine; sanamu tu zilizotengenezwa kwa mikono ya wanadamu!

20 Hapo mfalme Hezekia na nabii Isaya, mwana wa Amozi, wakamwomba Mungu na kumlilia awasaidie kwa ajili ya mambo haya.

21 Naye Mwenyezi-Mungu akatuma malaika, akaenda na kuwakatilia mbali mashujaa, wanajeshi, makamanda na maofisa katika kambi ya mfalme wa Ashuru. Basi, mfalme wa Ashuru akarejea nchini mwake amejawa aibu. Mara alipoingia ndani ya nyumba ya mungu wake, baadhi ya wanawe mwenyewe wakamuua papo hapo kwa upanga.

22 Kwa njia hii basi, Mwenyezi-Mungu akamwokoa mfalme Hezekia na wakazi wa Yerusalemu kutoka mkono wa Senakeribu mfalme wa Ashuru, na kutoka mkono wa maadui wake wote. Akawapa maisha ya amani na jirani zake wote.

23 Watu wengi sana walikuja wakamletea Mwenyezi-Mungu tambiko huko Yerusalemu, pia wakamletea Hezekia, mfalme wa Yuda zawadi za thamani. Hivyo kutoka wakati huo, akasifiwa sana na mataifa mengine yote.

24 Wakati huo, Hezekia aliugua sana, karibu na kufa. Akamwomba Mwenyezi-Mungu, naye akamjibu na kumpa ishara.

25 Lakini Hezekia hakumtolea Mwenyezi-Mungu shukrani kwa hayo yote aliyomtendea kwa kuwa moyo wake ulikuwa umejaa majivuno. Hii ilisababisha kutaabika kwa Yuda na Yerusalemu.

26 Kwa hiyo ghadhabu ikawa juu yake, juu ya Yuda na juu ya Yerusalemu. Hatimaye Hezekia alinyenyekea akaacha kuwa na moyo uliojaa majivuno; yeye na wakazi wa Yerusalemu walijinyenyekesha kwa hiyo ghadhabu ya Mwenyezi-Mungu haikuwajia wakati Hezekia alipokuwa hai.

27 Mfalme Hezekia alitajirika sana, akaheshimiwa. Alijitengenezea hazina za fedha, za dhahabu, za vito, za viungo, ngao na za aina zote za vyombo vya thamani kubwa.

28 Aidha, alijijengea mabohari ya kuhifadhia mazao ya nafaka, divai na mafuta, na mazizi kwa ajili ya ng'ombe na mengine kwa ajili ya kondoo.

29 Vivyo hivyo alijiongezea miji kwa ajili yake mwenyewe, makundi mengi ya ng'ombe na kondoo kwa sababu Mwenyezi-Mungu alimkirimia mali nyingi.

30 Mfalme Hezekia ndiye aliyeyafunga maji ya chemchemi ya Gihoni, akayachimbia mfereji wa chini kwa chini hadi upande wa magharibi wa mji wa Daudi. Hezekia alifaulu katika kila jambo alilofanya,

31 na hata wakati ambapo mabalozi wa wakuu wa Babuloni waliotumwa kwake kuuliza juu ya mambo ya ajabu yaliyotokea humo, Mungu, alimwacha ajiamulie mwenyewe, ili amjaribu na kujua yote yaliyokuwa moyoni mwake.

32 Matendo mengine ya mfalme Hezekia na wema wake, yameandikwa katika Maono ya nabii Isaya mwana wa Amozi, katika Kitabu cha Wafalme wa Yuda na Israeli.

33 Hezekia alifariki dunia na kuzikwa kwenye sehemu ya juu ya makaburi ya wafalme. Watu wote wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu walimtolea heshima kuu wakati wa kifo chake, naye Manase, mwanawe, akatawala mahali pake.

33

1 Manase alikuwa na umri wa miaka kumi na miwili alipoanza kutawala, akatawala kutoka Yerusalemu kwa muda wa miaka hamsini na mitano.

2 Alitenda maovu mbele ya Mwenyezi-Mungu kwa kuiga mienendo miovu ya mataifa ambayo Mwenyezi-Mungu aliyafukuza wakati watu wake wa Israeli walipokuwa wanaingia nchini.

3 Kwa maana alirekebisha mahali pa kuabudia miungu mingine palipokuwa pamebomolewa na Hezekia baba yake; akajenga madhabahu za kuabudia Mabaali, akatengeneza na sanamu za Maashera. Isitoshe, aliabudu vitu vyote vya mbinguni na kuvitumikia.

4 Alijenga madhabahu katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu mahali ambapo Mwenyezi-Mungu alikuwa amesema, “Jina langu litaabudiwa milele katika Yerusalemu.”

5 Alijenga madhabahu za kuabudia vitu vyote mbinguni kwenye nyua mbili za nyumba ya Mwenyezi-Mungu.

6 Pia aliwatoa wanawe kama sadaka ya kuteketeza katika bonde la mwana wa Hinomu. Alipiga ramli, alibashiri na alitumia hirizi; hata alishirikiana na waaguzi wa mizimu na wachawi. Alitenda maovu mengi mbele ya Mwenyezi-Mungu, akamkasirisha.

7 Nayo sanamu aliyoitengeneza, aliiweka katika nyumba ya Mungu mahali alipopazungumzia, mbele ya Daudi na Solomoni mwanawe: “Katika nyumba hii na katika Yerusalemu kati ya makabila kumi na mawili ya Israeli, ndipo mahali nitakapoabudiwa milele.

8 Na iwapo watu wa Israeli watajali kutenda yote niliyowaamuru, wakatii sheria zote, masharti, na maagizo yaliyotolewa kwa mkono wa Mose, basi kamwe sitawaacha wafukuzwe kutoka katika nchi hii ambayo niliwapa babu zao.”

9 Lakini Manase aliwapotosha watu wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu, wakatenda maovu zaidi kuliko mataifa ambayo Mwenyezi-Mungu aliyaangamiza mbele ya watu wa Israeli.

10 Mwenyezi-Mungu alimwonya Manase na watu wake, lakini hawakumsikia.

11 Kwa hiyo, Mwenyezi-Mungu akawaleta makamanda wa jeshi la mfalme wa Ashuru. Hao makamanda walimkamata Manase kwa kulabu wakamfunga pingu za shaba, wakampeleka hadi Babuloni.

12 Wakati alipokuwa taabuni, alimwomba Mwenyezi-Mungu, Mungu wake, akajinyenyekesha sana mbele ya Mungu wa babu zake.

13 Alimsihi, naye Mungu akapokea ombi lake na sala yake akamrudisha Yerusalemu katika ufalme wake. Ndipo Manase akatambua kuwa Mwenyezi-Mungu ndiye Mungu.

14 Baada ya haya, Manase alijenga ukuta mwingine upande wa nje wa mji wa Daudi, magharibi mwa Gihoni, bondeni, akauendeleza hadi Lango la Samaki, akauzungusha hadi Ofeli; akauinua juu sana. Pamoja na hayo, aliweka makamanda wa majeshi katika miji yote ya Yuda yenye ngome.

15 Alitoa katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu miungu yote ya kigeni na sanamu pamoja na madhabahu zote alizokuwa amezijenga kwenye mlima wa nyumba ya Mwenyezi-Mungu na katika Yerusalemu; alivitupa nje ya mji.

16 Alirudisha madhabahu ya kumwabudia Mwenyezi-Mungu, na juu yake akatoa tambiko za amani na za shukrani, akawaamuru watu wa Yuda wamwabudu Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli.

17 Hata hivyo watu waliendelea kutoa sadaka mahali pa kufanyia ibada, lakini kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wao tu.

18 Matendo mengine ya Manase, sala yake kwa Mungu wake na maneno ya waonaji waliozungumza naye kwa jina la Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, hayo, yote yameandikwa katika Mambo ya Nyakati za Wafalme wa Israeli.

19 Nalo ombi lake na jinsi Mungu alivyompokea, dhambi zake zote na ukosefu wa uaminifu wake, mahali alipojenga pa kuabudia na jinsi alivyotengeneza Ashera na sanamu kabla ya kujinyenyekesha, hayo yameandikwa katika Kumbukumbu za Waonaji.

20 Manase alifariki na kuzikwa katika ikulu yake, naye Amoni, mwanawe, akatawala mahali pake.

21 Amoni alikuwa na umri wa miaka ishirini na miwili alipoanza kutawala Yuda; alitawala miaka miwili huko Yerusalemu.

22 Alitenda maovu mbele ya Mwenyezi-Mungu, kama vile Manase baba yake alivyofanya. Pia alitoa sadaka na kutumikia sanamu ambazo Manase baba yake alichonga.

23 Naye hakujinyenyekesha mbele za Mwenyezi-Mungu, kama alivyofanya Manase, lakini yeye aliongeza kutenda makosa zaidi.

24 Baadaye watumishi wake walikula njama na kumuua katika ikulu yake.

25 Lakini watu wa Yuda wakawaua hao wote waliokula njama dhidi ya Amoni; kisha wakamfanya Yosia, mwanawe kuwa mfalme badala yake.

34

1 Yosia alikuwa na umri wa miaka minane alipoanza kutawala; alitawala miaka thelathini na mmoja huko Yerusalemu.

2 Alitenda mema mbele ya Mwenyezi-Mungu. Alifuata njia zake Daudi babu yake, na kushika amri za Mwenyezi-Mungu kwa dhati.

3 Katika mwaka wa nne wa utawala wake, mfalme Yosia, akiwa bado kijana, alianza kumwabudu Mungu wa Daudi, baba yake. Baadaye alipokuwa na umri wa miaka kumi na miwili alianza kuisafisha Yuda na Yerusalemu kwa kuharibu mahali pa kuabudia miungu mingine, sanamu za Ashera, na sanamu nyinginezo za kuchonga na za kusubu.

4 Watu wake walizibomoa madhabahu za ibada za Mabaali mbele yake na alizikatakata madhabahu za kufukizia ubani zilizoinuliwa juu ya madhabahu hizo; pia alizipondaponda sanamu za Ashera na nyinginezo za kuchonga na za kusubu; alizifanya kuwa mavumbi, nayo mavumbi akayamwaga juu ya makaburi ya wale ambao hapo awali walizitolea sadaka.

5 Aidha, aliiteketeza mifupa ya makuhani wa miungu hiyo kwenye madhabahu zao, hivyo akatakasa Yuda na Yerusalemu.

6 Alifanya vivyo hivyo katika miji ya Manase, Efraimu, Simeoni mpaka Naftali na kwenye magofu yaliyokuwa kandokando ya miji hiyo.

7 Alizibomoa madhabahu na kupondaponda Maashera na sanamu za kuchongwa zikawa mavumbi. Kadhalika alizikatakata madhabahu za kufukizia ubani katika nchi yote ya Israeli. Hatimaye alirudi Yerusalemu.

8 Katika mwaka wa kumi na nane wa utawala wake, wakati ambapo alikuwa amekwisha takasa nchi na nyumba, alituma watu watatu: Shafani mwana wa Azalia, Maaseya gavana wa mji na Yoa mwana wa Yoahazi, Katibu, ili waende kuirekebisha nyumba ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wake.

9 Walimwendea Hilkia, kuhani mkuu, wakamkabidhi fedha zilizokuwa zimeletwa katika nyumba ya Mungu ambazo zilikusanywa na Walawi wangojamlango, kutoka Manase, Efraimu na kutoka pande nyingine zote za Israeli, nchi yote ya Yuda na Benyamini, na pia kutoka kwa wenyeji wa Yerusalemu.

10 Zilikabidhiwa wale mafundi waliosimamia marekebisho ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu; na mafundi waliofanya kazi katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu walizitoa ili kutengeneza na kurekebisha nyumba.

11 Waliwapatia maseremala na wajenzi kwa ajili ya kununulia mawe yaliyochongwa, mbao za kuunganishia na mihimili ya kutumia katika kurekebisha yale majengo ambayo wafalme wa Yuda waliyaacha yakabomokabomoka.

12 Watu hao waliifanya kazi hiyo kwa uaminifu, wakiwa chini ya uongozi wa Walawi Yahathi na Obadia, chini ya wana wa Merari na Zekaria na Meshulamu na chini ya wazawa wa Kohathi. Walawi wote waliokuwa na ujuzi sana katika upigaji wa vyombo vya muziki,

13 waliwasimamia wachukuzi wa mizigo na kuwaongoza wote waliofanya kazi mbalimbali; baadhi ya Walawi walikuwa waandishi, maofisa na hata walinda mlango.

14 Wakati walipokuwa wanashughulika na utoaji wa fedha zilizokuwa zimeletwa katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu, kuhani Hilkia alipata Kitabu cha Sheria ya Mwenyezi-Mungu iliyotolewa kwa mkono wa Mose.

15 Kisha Hilkia alimwambia Shafani mwandishi, “Nimekipata Kitabu cha Sheria katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu.” Halafu Hilkia akampatia Shafani kitabu.

16 Naye Shafani akampelekea mfalme na kumpasha habari, akisema, “Yote watumishi wako waliyokabidhiwa wanayafanya.

17 Wametoa fedha zilizopatikana katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu, halafu wamezikabidhi kwa wasimamizi na mafundi.”

18 Kisha Katibu Shafani akamwambia mfalme, “Kuhani Hilkia amenipa kitabu.” Naye Shafani akakisoma mbele ya mfalme.

19 Mfalme aliposikia maneno ya sheria alirarua mavazi yake.

20 Ndipo alipomwamuru Hilkia, Ahikamu mwana wa Shafani, Abdoni mwana wa Mika, katibu Shafani na Asaya, mtumishi wa mfalme, akisema,

21 “Nendeni mkatafute shauri kutoka kwa Mwenyezi-Mungu kwa niaba yangu na watu ambao wamebaki katika Israeli na Yuda, kuhusu maneno yaliyomo katika kitabu kilichopatikana. Kwa sababu ghadhabu ya Mwenyezi-Mungu imetuangukia, maana babu zetu hawakushika neno la Mwenyezi-Mungu, wala kufanya yaliyoandikwa humo.”

22 Kwa hiyo Hilkia pamoja na wale wengine mfalme aliowatuma walimwendea nabii Hulda, mkewe Shalumu, mwana wa Tokathi, mwana wa Hasra, mtunza mavazi yaliyotumika hekaluni (alikuwa anaishi Yerusalemu katika mtaa wa pili); nao walizungumza naye juu ya mambo yaliyotokea.

23 Basi akawaambia, “Hivi ndivyo anavyosema Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli: Mwambie huyo aliyewatuma kwangu,

24 Mwenyezi-Mungu anasema hivi, ‘Tazama nitaleta uovu juu ya Yerusalemu na juu ya wakazi wake, laana zote zilizoandikwa katika kitabu kilichosomwa mbele ya mfalme wa Yuda.

25 Kwa sababu wameniacha mimi na kufukizia miungu mingine ubani ili wanikasirishe sana kwa kazi zote za mikono yao, basi ghadhabu yangu itamwagika juu ya mahali hapa wala haitatulizwa.

26 Lakini kumhusu mfalme wa Yuda, aliyewatuma kutafuta shauri la Mwenyezi-Mungu mwambie kwamba, hivi ndivyo anavyosema Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli juu ya maneno uliyoyasikia:

27 Kwa kuwa umetubu na kunyenyekea mbele yangu, hata umerarua mavazi yako na kulia uliposikia maneno yangu dhidi ya mahali hapa, na dhidi ya wakazi wake, na umejinyenyekesha mbele yangu, nami pia nimekusikia.

28 Adhabu ambayo nitailetea Yerusalemu, sitaileta wakati wa uhai wako. Utawala wako utakuwa wa amani.’” Basi, wajumbe wakamletea mfalme Yosia habari hizi.

29 Kisha mfalme Yosia aliita na kukusanya viongozi wote wa Yuda na Yerusalemu.

30 Naye mfalme akaenda katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu pamoja na wanaume wote wa Yuda, na wakazi wa Yerusalemu wakifuatana na makuhani, Walawi na watu wengine wote wakubwa kwa wadogo. Ndipo alipowasomea maneno ya kitabu cha agano kilichopatikana katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu.

31 Halafu mfalme alisimama mahali pake akafanya agano mbele ya Mwenyezi-Mungu, kumfuata Mwenyezi-Mungu, kushika amri, maamuzi na masharti yake kwa moyo wake wote na kwa roho yake yote, kutenda maneno yote ya agano yaliyoandikwa katika kitabu hicho.

32 Tena aliwafanya wote waliokuwa katika Yerusalemu na katika Benyamini kuzingatia agano. Nao wakazi wa Yerusalemu waliishi kwa kufuata agano la Mungu, Mungu wa babu zao.

33 Kisha Yosia aliondoa sanamu zote za kuchukiza zilizokuwa katika eneo lote la watu wa Israeli, na kuwahimiza watu wote wa Israeli kumtumikia Mwenyezi-Mungu, Mungu wao. Katika maisha yake yote hawakumwacha Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zao.

35

1 Mfalme Yosia aliadhimisha Pasaka mjini Yerusalemu, wakachinja wanakondoo wa Pasaka siku ya kumi na nne ya mwezi wa kwanza.

2 Aliwateua makuhani kwa kazi zao ambazo walihitajika kufanya katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu na kuwatia moyo wazifanye kikamilifu.

3 Pamoja na hayo, aliwapa Walawi waliowafundisha watu wa Israeli na ambao walikuwa wakfu kwa Mwenyezi-Mungu, maagizo yafuatayo: “Liwekeni sanduku takatifu ndani ya nyumba ambayo Solomoni mwana wa Daudi, mfalme wa Israeli alijenga; hamhitaji kulibebabeba tena mabegani. Sasa mtumikieni Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu na watu wake Waisraeli.

4 Timizeni wajibu wenu kulingana na koo zenu, kufuatana na maagizo ya Daudi mfalme wa Israeli na Solomoni mwanawe.

5 Simameni pia mahali patakatifu kama wawakilishi wa jamaa za koo zenu wasiofanya kazi za ukuhani, na kila mmoja aiwakilishe jamaa moja ya Walawi.

6 Mchinjeni mwanakondoo wa Pasaka, mjitakase, halafu itayarisheni kwa ajili ya ndugu zenu, ili waweze kutimiza agizo la Mwenyezi-Mungu lililosemwa na Mose.”

7 Kisha Yosia aliwapa watu, wanambuzi wapatao 30,000, na mafahali 3,000, wote hawa walitolewa kwenye mifugo ya mfalme.

8 Nao maofisa wake, kwa hiari yao, walitoa mchango wao wakawapa watu, makuhani na Walawi. Hilkia, Zekaria na Yehieli, maofisa wa nyumba ya Mungu, waliwapa makuhani wanakondoo na wanambuzi 2,600 na mafahali 300 kwa ajili ya sadaka za Pasaka.

9 Naye Konania na nduguze wawili, Shemaya na Nethaneli, pamoja na Hashabia, Yeieli na Yozabadi, waliokuwa viongozi wa Walawi, nao pia waliwapa wanakondoo na wanambuzi 5,000 na mafahali 500, kwa ajili ya sadaka za Pasaka.

10 Baada ya matayarisho yote ya Pasaka kumalizika, makuhani walisimama mahali pao, na Walawi katika makundi yao; sawasawa na amri ya mfalme.

11 Walimchinja mwanakondoo wa Pasaka, nao makuhani walinyunyiza damu, waliyopokea kutoka kwao nao Walawi waliwachuna wanyama.

12 Halafu walitenga sadaka za kuteketeza ili waweze kuzigawa kulingana na jamaa zao walio makuhani ili wamtolee Mwenyezi-Mungu kama ilivyoandikwa katika kitabu cha Mose. Nayo mafahali waliwafanya vivyo hivyo.

13 Walimchoma mwanakondoo wa Pasaka juu ya moto kama ilivyoagizwa, na pia walizitokosa sadaka takatifu katika vyungu, masufuria na kwenye vikaango, na kuwagawia upesiupesi watu wasiofanya kazi ya ukuhani.

14 Baadaye, Walawi wakajiandalia sehemu zao na za makuhani kwa maana makuhani wa uzao wa Aroni walikuwa wanashughulika na utoaji wa sadaka za kuteketeza, na vipande vya mafuta, mpaka usiku; kwa hiyo Walawi waliandaa kwa ajili yao wenyewe na kwa ajili ya makuhani wa uzao wa Aroni.

15 Nao waimbaji wazawa wa Asafu walishika nafasi zao, kwa mujibu wa maagizo ya mfalme Daudi, Asafu, Hemani na Yeduthuni, mwonaji wa mfalme. Nao mabawabu walikuwa kwenye malango; hawakuhitajika kuziacha nafasi zao za kazi kwa kuwa ndugu zao Walawi waliwaandalia Pasaka.

16 Hivyo basi, huduma yote ya Mwenyezi-Mungu ilitayarishwa siku hiyo, ili kuiadhimisha Pasaka na kutoa sadaka za kuteketeza kwenye madhabahu ya Mwenyezi-Mungu kama alivyoamuru mfalme Yosia.

17 Wakati huo watu wote wa Israeli waliohudhuria waliiadhimisha sikukuu hiyo ya Pasaka na sikukuu ya mikate isiyotiwa chachu, kwa muda wa siku saba.

18 Pasaka kama hiyo ilikuwa haijasherehekewa katika Israeli yote tangu siku za nabii Samueli. Hapajatokea mfalme hata mmoja wa Israeli aliyeadhimisha Pasaka kama hii iliyoadhimishwa na mfalme Yosia pamoja na makuhani, Walawi na watu wote wa Yuda, watu wa Israeli na wakazi wa Yerusalemu.

19 Pasaka hiyo iliadhimishwa katika mwaka wa kumi na nane wa utawala wake mfalme Yosia.

20 Baada ya haya yote aliyofanya mfalme Yosia kwa ajili ya hekalu, Neko, mfalme wa Misri, aliongoza jeshi lake kwenda kushambulia Karkemishi kwenye mto Eufrate. Naye mfalme Yosia alitoka kumkabili,

21 lakini mfalme Neko akamtumia ujumbe usemao: “Vita hivi havikuhusu wewe hata kidogo ewe mfalme wa Yuda. Sikuja kupigana nawe bali dhidi ya maadui zangu, na Mungu ameniamuru niharakishe. Acha basi kumpinga Mungu, ambaye yu upande wangu, la sivyo atakuangamiza.”

22 Lakini Yosia hakukubali kumwachia. Alikataa kuyasikiliza maneno aliyonena Mungu kwa njia ya Neko, kwa hiyo akajibadilisha ili asitambulike, kisha akaingia vitani katika tambarare ya Megido.

23 Nao wapiga upinde walimpiga mshale mfalme Yosia; basi ndipo mfalme alipowaambia watumishi wake: “Niondoeni! Nimejeruhiwa vibaya sana.”

24 Watumishi wake walimtoa katika gari lake la farasi, wakambeba na gari lake la pili hadi Yerusalemu. Hapo akafariki dunia na kuzikwa katika makaburi ya kifalme. Watu wote wa Yuda na Yerusalemu waliomboleza kifo cha Yosia.

25 Nabii Yeremia pia alitunga shairi la maombolezo kwa ajili ya kifo chake; nao waimbaji wote, wanaume kwa wanawake, humtaja Yosia katika maombolezo yao, mpaka leo. Imekuwa desturi kufanya maombolezo haya katika Israeli. Hayo yameandikwa katika Maombolezo.

26 Matendo mengine ya Yosia na matendo yake mema kama yalivyoandikwa katika sheria ya Mwenyezi-Mungu,

27 na matendo yake tangu mwanzo hadi mwisho, hayo yameandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Israeli na Yuda.

36

1 Watu wa Yuda walimtwaa Yehoahazi, mwana wa Yosia, wakamtawaza awe mfalme mahali pa baba yake.

2 Yehoahazi alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitatu alipoanza kutawala; akatawala kwa muda wa miezi mitatu huko Yerusalemu.

3 Baadaye mfalme wa Misri alimwondoa huko Yerusalemu na akaitoza nchi kodi ya kilo 3,400 za fedha na kilo 34 za dhahabu.

4 Kisha mfalme wa Misri akamweka Eliakimu, nduguye Yehoahazi, kuwa mfalme wa Yuda na Yerusalemu, akabadilisha jina lake kuwa Yehoyakimu; lakini Neko akamtwaa Yehoahazi nduguye mpaka Misri.

5 Yehoyakimu alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala, akatawala kwa muda wa miaka kumi na mmoja huko Yerusalemu. Alitenda maovu mbele ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wake.

6 Nebukadneza mfalme wa Babuloni, alimshambulia, akamfunga kwa pingu ili kumpeleka mateka Babuloni.

7 Nebukadneza pia alitwaa baadhi ya vyombo vya nyumba ya Mwenyezi-Mungu akavipeleka Babuloni na kuviweka katika ikulu yake huko Babuloni.

8 Basi, matendo mengine ya Yehoyakimu, pamoja na machukizo aliyotenda na mengine yaliyoonekana dhidi yake tazama yameandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Israeli na Yuda. Yehoyakini mwanawe alitawala badala yake.

9 Yehoyakini alikuwa na umri wa miaka minane alipoanza kutawala. Alitawala huko Yerusalemu kwa muda wa miezi mitatu na siku kumi. Alitenda maovu mbele ya Mwenyezi-Mungu.

10 Mwaka ulipokwisha, mfalme Nebukadneza alituma wajumbe, wakamchukua Yehoyakini mateka hadi Babuloni, pamoja na vyombo vya thamani vya nyumba ya Mwenyezi-Mungu. Akamtawaza Sedekia, nduguye, kuwa mfalme wa Yuda na Yerusalemu.

11 Sedekia alikuwa na umri wa miaka ishirini na mmoja alipoanza kutawala, akatawala huko Yerusalemu kwa muda wa miaka kumi na mmoja.

12 Alitenda maovu mbele ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wake, wala hakunyenyekea mbele ya nabii Yeremia ambaye alisema maneno yaliyotoka kwa Mwenyezi-Mungu.

13 Sedekia alimwasi pia mfalme Nebukadneza aliyekuwa amemfanya aape kwa jina la Mungu kwamba hatamwasi. Alikuwa mkaidi sana na mwenye kiburi akakataa kumgeukia Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli.

14 Hata makuhani, viongozi wa Yuda pamoja na watu walikosa uaminifu kabisa wakiiga matendo yote ya kuchukiza ya watu wa mataifa mengine; waliichafua nyumba ya Mwenyezi-Mungu ambayo yeye mwenyewe alikuwa ameitakasa huko Yerusalemu.

15 Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zao, mara kwa mara alituma kwao wajumbe wake maana alikuwa na huruma kwa watu wake na makao yake.

16 Lakini wao waliendelea kuwadhihaki wajumbe wa Mungu, wakayapuuza maneno yake na kuwacheka manabii wake mpaka hatimaye ghadhabu ya Mwenyezi-Mungu ikawaka dhidi ya watu wake hata kusiwe na namna yoyote ya kutoroka.

17 Kwa hiyo, Mwenyezi-Mungu alimleta mfalme wa Wakaldayo ambaye aliwaangamiza vijana wao kwa upanga hata ndani ya mahali patakatifu; wala hakumhurumia mtu yeyote awe mvulana au msichana, mzee au mnyonge. Wote Mwenyezi-Mungu aliwatia mikononi mwake.

18 Alitwaa vyombo vyote vya nyumba ya Mungu vikubwa na vidogo na hazina ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu na ya mfalme na maofisa wake. Alivipeleka vyote mpaka Babuloni.

19 Aliichoma moto nyumba ya Mungu, akaubomoa ukuta wa Yerusalemu, akayachoma moto majumba yote ya kifalme na kuharibu vyombo vyake vyote vya thamani.

20 Watu walionusurika vitani aliwachukua uhamishoni Babuloni. Huko wakawa watumwa wake na wa wazawa wake mpaka mwanzo wa ufalme wa Persia.

21 Hivyo likatimia neno la Mwenyezi-Mungu alilosema nabii Yeremia: “Nchi itabaki tupu bila kulimwa miaka sabini kulingana na muda wa pumziko ambao haukuadhimishwa.”

22 Mnamo mwaka wa kwanza wa utawala wa Koreshi, mfalme wa Persia, ili litimie neno la Mwenyezi-Mungu alilolinena kwa njia ya nabii Yeremia, Mwenyezi-Mungu alimfanya Koreshi, mfalme wa Persia, atangaze amri ifuatayo katika ufalme wake wote na kuiweka katika maandishi:

23 “Hivi ndivyo anavyosema Koreshi mfalme wa Persia: Mwenyezi-Mungu, Mungu wa mbingu, amenipatia falme zote za ulimwenguni, na ameniagiza nimjengee nyumba katika Yerusalemu, nchini Yuda. Basi, sasa kila mtu katika nyinyi nyote mlio watu wake Mwenyezi-Mungu, Mungu wake na awe pamoja naye, na aende.”