1

1 Kauli ya Mungu aliyoiona nabii Habakuki.

2 “Ee Mwenyezi-Mungu, nitakulilia mpaka lini, nawe usinisikilize na kunisaidia? Kwa nini nalia: ‘Dhuluma’ nawe hutuokoi?

3 Kwa nini wanifanya nishuhudie mabaya na taabu? Uharibifu na ukatili vinanizunguka, ugomvi na mashindano yanazuka.

4 Hivyo sheria haina nguvu, wala haki haitekelezwi. Waovu wanawazunguka waadilifu, hivyo hukumu hutolewa ikiwa imepotoshwa.”

5 Mungu akasema: “Yaangalie mataifa, uone! Utastaajabu na kushangaa. Maana ninatenda kitu ukiwa bado unaishi, kitu ambacho ungeambiwa hungesadiki.

6 Maana ninawachochea Wakaldayo, taifa lile kali na lenye hamaki! Taifa lipitalo katika nchi yote, ili kunyakua makao ya watu wengine.

7 Wao ni watu wa kuchukiza na kutisha; wao hujiamulia wenyewe nini haki na adhama.

8 “Farasi wao ni wepesi kuliko chui; wakali kuliko mbwamwitu wenye njaa. Wapandafarasi wao wanatoka mbali, wanaruka kasi kama tai arukiavyo mawindo.

9 “Wote wanakuja kufanya ukatili; kwa nyuso kakamavu wanasonga mbele, wanakusanya mateka wengi kama mchanga.

10 Wanawadhihaki wafalme, na kuwadharau watawala. Kila ngome kwao ni mzaha, wanairundikia udongo na kuiteka.

11 Kisha wanasonga mbele kama upepo, wafanya makosa na kuwa na hatia, maana, nguvu zao ndizo mungu wao!”

12 “Je, wewe si ndiwe Mwenyezi-Mungu, tangu kale na kale? Wewe ndiwe Mungu wangu, Mtakatifu wangu, usiyekufa Ee Mwenyezi-Mungu, umewateua Wakaldayo watuhukumu; Ewe Mwamba, umewaimarisha ili watuadhibu!

13 Wewe ni mtakatifu kabisa, huwezi kutazama uovu, huwezi kustahimili kamwe kuona mabaya. Mbona basi wawaona wafanya maovu na kunyamaza, kwa nini unanyamaza waovu wanapowamaliza wale watu walio waadilifu kuliko wao?

14 “Umewafanya watu kama samaki baharini, kama viumbe vitambaavyo visivyo na kiongozi!

15 Wakaldayo huwavua watu kwa ndoana, huwavutia nje kwa wavu wao, huwakusanya wote katika jarife lao, kisha hufurahi na kushangilia.

16 Kwa hiyo, wanazitambikia nyavu zao, na kuzifukizia ubani; maana kwa hizo huweza kuishi kwa anasa, na kula chakula cha fahari.

17 “Je, hawataacha kamwe kuvuta upinde wao? Je, wataendelea tu kuwanasa watu, na kuyaangamiza mataifa bila huruma?

2

1 Mimi nitasimama mahali pa kuchungulia, na kukaa juu mnarani; nitakaa macho nione ataniambia nini, atajibu nini kuhusu lalamiko langu.”

2 Kisha, Mwenyezi-Mungu akanijibu hivi: “Yaandike maono haya; yaandike wazi juu ya vibao, anayepitia hapo apate kuyasoma.

3 Maono haya yanangoja wakati wa kufaa; ni maono ya ukweli juu ya mwisho. Kama yaonekana kuchelewa, uyasubiri; hakika yatafika, wala hayatachelewa.

4 Andika: ‘Waangalie wenye kiburi, hao wataangamia; lakini waadilifu wataishi kwa kumwamini Mungu.’”

5 Zaidi ya hayo, divai hupotosha; mtu mwenye kiburi hatadumu. Yuko tayari kuwameza wengine kama Kuzimu; kama vile kifo, hatosheki na kitu. Hujikusanyia mataifa yote, na watu wote kama mali yake.

6 Kila mtu atamdhihaki mtu wa namna hiyo na kumtungia misemo ya dhihaka: “Ole wako unayejirundikia visivyo vyako, na kuchukua rehani mali za watu lakini hulipi! Utaendelea kufanya hivyo hadi lini?

7 Siku moja wadeni wako watainuka ghafla, wale wanaokutetemesha wataamka. Ndipo utakuwa mateka wao.

8 Wewe umeyapora mataifa mengi, lakini wote wanaosalimika watakupora wewe, kwa mauaji na dhuluma uliyoitendea dunia, naam, uliyoifanyia miji na wakazi wake wote.

9 “Ole wako unayejitajirisha kwa hasara ya mwingine, ujengaye nyumba yako juu milimani ukidhani kuwa salama mbali na madhara.

10 Lakini kwa mipango yako umeiaibisha jamaa yako. Kwa kuyaangamiza mataifa mengi, umeyaangamiza maisha yako mwenyewe.

11 Ndiyo maana hata mawe yatalalamika ukutani, na boriti za nyumba zitayaunga mkono.

12 “Ole wako unayejenga mji kwa mauaji unayesimika jiji kwa maovu!

13 Mwenyezi-Mungu wa majeshi husababisha juhudi za watu zipotelee motoni, na mataifa yajishughulishe bure.

14 Utukufu wa Mwenyezi-Mungu utaenea pote duniani, kama vile maji yaeneavyo baharini.

15 Ole wako unayewalewesha jirani zako, na kutia sumu katika divai yao ili upate kuwaona wamekaa uchi.

16 Utajaa aibu badala ya heshima. Utakunywa wewe mwenyewe na kupepesuka! Mwenyezi-Mungu mwenyewe atakulevya, na aibu itaifunika heshima yako!

17 Maovu uliyoitenda Lebanoni yatakuvamia wewe; uliwaua wanyama, wanyama nao watakutisha. Yote hayo yatakupata wewe, kwa mauaji na dhuluma uliyoitendea dunia, naam, uliyoifanyia miji na wakazi wake wote.

18 “Chafaa nini kinyago alichotengeneza mtu? Sanamu ni madini yaliyoyeyushwa, ni kitu cha kueneza udanganyifu! Mtengeneza sanamu hutumaini alichotengeneza mwenyewe, kinyago ambacho hakiwezi hata kusema!

19 Ole wake mtu aliambiaye gogo: ‘Amka!’ Au jiwe bubu ‘Inuka!’ Je, sanamu yaweza kumfundisha mtu? Tazama imepakwa dhahabu na fedha, lakini haina uhai wowote.”

20 Lakini Mwenyezi-Mungu yumo katika hekalu lake takatifu; dunia yote na ikae kimya mbele yake.

3

1 Sala ya nabii Habakuki:

2 Ee Mwenyezi-Mungu, nimesikia juu ya fahari yako, juu ya matendo yako, nami naogopa. Uyafanye tena mambo hayo wakati wetu; uyafanye yajulikane wakati huu wetu. Ukasirikapo tafadhali ukumbuke huruma yako!

3 Mungu amekuja kutoka Temani, Mungu mtakatifu kutoka mlima Parani. Utukufu wake umetanda pote mbinguni, nayo dunia imejaa sifa zake.

4 Mng'ao wake ni kama wa jua; miali imetoka mkononi mwake ambamo nguvu yake yadhihirishwa.

5 Maradhi yanatangulia mbele yake, nyuma yake yanafuata maafa.

6 Akisimama dunia hutikisika; akiyatupia jicho mataifa, hayo hutetemeka. Milima ya milele inavunjwavunjwa, vilima vya kudumu vinadidimia; humo zimo njia zake za kale na kale.

7 Niliwaona watu wa Kushani wakiteseka, na watu wa Midiani wakitetemeka.

8 Ee Mwenyezi-Mungu, je, umeikasirikia mito? Je, umeyakasirikia maji ya bahari, hata ukaendesha farasi wako, na magari ya vita kupata ushindi?

9 Uliuweka tayari uta wako, ukaweka mishale yako kwenye kamba. Uliipasua ardhi kwa mito.

10 Milima ilikuona, ikanyauka; mafuriko ya maji yakapita humo. Vilindi vya bahari vilinguruma, na kurusha juu mawimbi yake.

11 Jua na mwezi vilikaa kimya katika makazi yao, vilipoona miali ya mishale yako ikienda kasi, naam, vilipouona mkuki wako ukimetameta.

12 Kwa ghadhabu ulipita juu ya nchi, uliyakanyaga mataifa kwa hasira yako.

13 Ulitoka kwenda kuwaokoa watu wako, kumwokoa yule uliyemweka wakfu kwa mafuta. Ulimponda kiongozi wa jamii ya waovu, ukawaangamiza kabisa wafuasi wake.

14 Amiri jeshi ulimchoma mishale yako, jeshi lilipokuja kama kimbunga kututawanya, wakijigamba kuwaangamiza maskini mafichoni mwao.

15 Kwa farasi wako ulitembea juu ya bahari, bahari inayosukwasukwa na mawimbi.

16 Nasikia hayo nami ninashtuka mwilini, midomo yangu inatetemeka kwa hofu; mifupa yangu inateguka, miguu yangu inatetemeka. Ninangojea kwa utulivu siku ile ya maafa, ambayo inawajia wale wanaotushambulia.

17 Hata kama mitini isipochanua maua, wala mizabibu kuzaa zabibu; hata kama mizeituni isipozaa zeituni, na mashamba yasipotoa chakula; hata kama kondoo wakitoweka zizini, na mifugo kukosekana mazizini,

18 mimi nitaendelea kumfurahia Mwenyezi-Mungu nitamshangilia Mungu anayeniokoa.

19 Bwana, Mwenyezi-Mungu ndiye nguvu yangu, huiimarisha miguu yangu kama ya paa, huniwezesha kupita juu milimani.