1

1 Mnamo mwaka wa tatu wa utawala wa mfalme Yehoyakimu wa Yuda, mfalme Nebukadneza wa Babuloni alikwenda Yerusalemu, akauzingira mji.

2 Bwana akamwacha Yehoyakimu atiwe mikononi mwa mfalme Nebukadneza pamoja na baadhi ya vyombo vya nyumba ya Mungu. Basi mfalme Nebukadneza akachukua mateka na vyombo akavipeleka nchini Shinari, akaviweka katika hazina ya miungu yake.

3 Mfalme Nebukadneza akamwamuru Ashpenazi, towashi wake mkuu, amchagulie baadhi ya vijana wa Israeli wa jamaa ya kifalme na ya watu mashuhuri.

4 Mfalme alitaka vijana wasio na kasoro, wazuri kwa umbo, wenye uzoefu wa kila hekima, wenye akili na maarifa na wanaofaa kutoa huduma katika ikulu. Alitaka pia vijana hao wafundishwe kusoma na kuandika lugha ya Wakaldayo.

5 Mfalme aliagiza vijana hao wapewe chakula bora ambacho yeye mwenyewe alikula na divai ambayo alikunywa. Vijana hao walitakiwa wapewe mafunzo kwa miaka mitatu, kisha wapelekwe kwa mfalme.

6 Miongoni mwa vijana waliochaguliwa walikuwa Danieli, Hanania, Mishaeli na Azaria, wote wa kabila la Yuda.

7 Huyo towashi mkuu akawapa majina mengine; Danieli akamwita Belteshaza, Hanania akamwita Shadraki, Mishaeli akamwita Meshaki na Azaria akamwita Abednego.

8 Lakini Danieli aliamua kutojitia unajisi kwa kula chakula bora cha mfalme na kunywa divai yake. Kwa hiyo, alimwomba towashi mkuu amruhusu asile vitu hivyo na kujitia unajisi.

9 Basi, Mungu akamjalia Danieli kupendelewa na kuhurumiwa na Ashpenazi, towashi mkuu.

10 Lakini, towashi mkuu akamwambia Danieli, “Nina hofu kwamba bwana wangu mfalme ambaye ametoa maagizo kuhusu chakula na vinywaji unavyopaswa kutumia, ataona kuwa afya yako si nzuri kama ya wenzako wa rika lako. Hivyo maisha yangu yatakuwa hatarini.”

11 Hapo Danieli akamwendea mtumishi aliyewekwa na towashi mkuu kumlinda yeye na wenzake kina Hanania, Mishaeli na Azaria, akamwambia,

12 “Tafadhali utujaribu, sisi watumishi wako kwa muda wa siku kumi kwa kutupa mboga za majani na maji.

13 Kisha, tulinganishe sisi na hao vijana wengine wanaokula chakula cha mfalme, halafu utoe uamuzi wako kulingana na jinsi utakavyoona.”

14 Mlinzi akakubaliana nao, akawajaribu kwa muda wa siku kumi.

15 Baada ya siku hizo kumi, aliwaangalia akaona kuwa wale vijana waliokula mboga za majani walionekana wenye afya na nguvu kuliko wale wengine wote waliolishwa chakula cha kifalme.

16 Basi, yule mlinzi akawaacha waendelee kula mboga za majani badala ya chakula cha fahari na divai.

17 Mungu aliwajalia vijana hao wanne maarifa na ujuzi katika elimu na hekima. Zaidi ya hayo, alimjalia Danieli kipawa cha kufasiri maono na ndoto.

18 Muda ulipotimia ambapo hao vijana wangepelekwa kwa mfalme kama alivyokuwa ameagiza, yule towashi mkuu akawapeleka vijana wote mbele ya Nebukadneza.

19 Mfalme alipozungumza nao wote, hakuna walioonekana kuwa bora kama Danieli, Hanania, Mishaeli na Azaria. Basi, wakakubaliwa kumhudumia mfalme.

20 Jambo lolote la hekima au maarifa ambalo mfalme aliwauliza alijionea mwenyewe kwamba vijana hao wanne walikuwa bora mara kumi kuliko waaguzi na wachawi wote katika utawala wake.

21 Danieli alidumu katika huduma ya ikulu mpaka mwaka wa kwanza wa mfalme Koreshi.

2

1 Mnamo mwaka wa pili wa utawala wake, mfalme Nebukadneza aliota ndoto, akawa na wasiwasi sana rohoni hata usingizi ukamtoweka.

2 Basi, mfalme akaamuru waganga, walozi na wachawi wa Wakaldayo waletwe ili wamfasirie ndoto yake. Wote wakaja na kusimama mbele yake.

3 Mfalme Nebukadneza akawaambia, “Niliota ndoto, nayo inanipa wasiwasi, nami nataka nijulishwe tafsiri yake.”

4 Wale Wakaldayo wakamwambia mfalme kwa Kiaramu, “Uishi, ee mfalme! Tusimulie ndoto yako nasi watumishi wako tutakufasiria.”

5 Mfalme akawaambia, “Nimetoa kauli yangu kamili: Ikiwa hamtanijulisha ndoto yenyewe na maana yake, mtangolewa viungo vyenu kimojakimoja, na nyumba zenu zitabomolewa.

6 Lakini mkiniambia hiyo ndoto na maana yake, nitawapa zawadi, tuzo na heshima kubwa. Basi, nijulisheni ndoto hiyo na maana yake!”

7 Wao wakamjibu mara ya pili, “Mfalme, tusimulie ndoto hiyo, nasi watumishi wako tutakufasiria.”

8 Hapo mfalme akawakatiza kwa kusema, “Najua kweli kwamba mnajaribu kupoteza wakati kwa kuwa mnaona kwamba nilikwisha toa kauli yangu kamili,

9 kwamba msiponijulisha ndoto hiyo, adhabu yenu ni moja. Mmepatana kunidanganyadanganya na kunilaghailaghai huku muda unapita. Niambieni ndoto hiyo, nami nitajua kuwa mnaweza kunijulisha maana yake.”

10 Wale Wakaldayo wakamjibu: “Mfalme, hakuna mtu yeyote duniani awezaye kutimiza matakwa yako. Hakuna mfalme yeyote, hata awe mkuu na mwenye nguvu kiasi gani aliyepata kuwauliza waganga au walozi au Wakaldayo jambo kama hilo.

11 Jambo unalouliza, ee mfalme, ni gumu. Hakuna mtu anayeweza kukufunulia isipokuwa miungu peke yake ambayo haikai miongoni mwa wanaadamu.”

12 Kusikia hivyo, mfalme Nebukadneza alikasirika na kughadhibika sana, akaamuru wenye hekima wote wa Babuloni waangamizwe.

13 Basi, tangazo likaenea kuwa wenye hekima wote wauawe; Danieli na wenzake, nao pia wakatafutwa ili wauawe.

14 Basi, Danieli, kwa tahadhari na busara, alimwendea Arioko, mkuu wa kikosi cha walinzi wa mfalme na ambaye alipewa jukumu la kuwaua wenye hekima wa Babuloni,

15 akamwuliza, “Kwa nini amri ya mfalme ni kali hivyo?” Hapo Arioko akamsimulia Danieli kisa chote.

16 Ndipo Danieli alipomwendea mfalme na kumwomba ampe muda ili aweze kumjulisha mfalme maana ya ndoto yake.

17 Kisha, Danieli akarudi nyumbani, akawajulisha wenzake Hanania, Mishaeli na Azaria jambo hilo.

18 Aliwaambia wamwombe Mungu wa mbinguni awaonee huruma kuhusu fumbo hilo, ili wao wasiangamie pamoja na wenye hekima wengine wa Babuloni.

19 Ndipo Danieli alipofunuliwa fumbo hilo usiku katika maono. Naye Danieli akamshukuru Mungu wa mbinguni,

20 akasema, “Na litukuzwe milele na milele jina lake Mungu. Hekima na nguvu ni vyake.

21 Hubadilisha nyakati na majira, huwaondoa na kuwatawaza wafalme. Wenye busara huwapa hekima, wenye maarifa huwaongezea ufahamu.

22 Hufunua siri na mafumbo, ajua kilichoko gizani, mwanga wakaa kwake.

23 Kwako, ee Mungu wa wazee wangu, natoa shukrani na kukusifu, maana umenipa hekima na nguvu, umetujulisha kile tulichokuomba, umetujulisha kile kisa cha mfalme.”

24 Basi, Danieli akamwendea Arioko aliyekuwa ameteuliwa kuwaangamiza wenye hekima wa Babuloni, akamwambia, “Usiwaue wenye hekima wa Babuloni, ila nipeleke mimi mbele ya mfalme, nami nitamweleza maana ya ndoto yake.”

25 Basi, Arioko akampeleka Danieli mbele ya mfalme kwa haraka na kumwambia, “Nimempata mtu fulani miongoni mwa mateka wa Yuda anayeweza kukufasiria ndoto yako, ee mfalme.”

26 Mfalme akamwuliza Danieli, ambaye pia aliitwa Belteshaza, “Je, unaweza kunijulisha ndoto niliyoota na maana yake?”

27 Danieli akamjibu mfalme, “Hakuna wenye hekima, wachawi, waganga wala wanajimu wanaoweza kukujulisha fumbo hilo lako.

28 Lakini, yuko Mungu mbinguni ambaye hufumbua mafumbo, naye amekujulisha, ee mfalme Nebukadneza, mambo yatakayotukia siku zijazo. Ndoto yako na maono yaliyokujia kichwani mwako ulipokuwa umelala ni haya:

29 Kwako ee mfalme, ulipokuwa umelala kitandani mwako, yalikujia mawazo kuhusu mambo yatakayotukia baadaye; naye Mungu afumbuaye mafumbo, alikuonesha yale yatakayotukia.

30 Lakini mimi sikufumbuliwa fumbo hili kwa sababu nina hekima kuliko wanaadamu wengine, bali ili wewe mfalme, upate kujulishwa maana ya ndoto yako na kujua mawazo yako.

31 “Katika ndoto yako, ee mfalme, uliona sanamu kubwa, yenye nguvu na iliyongaa sana, imesimama mbele yako. Sanamu hiyo ilikuwa ya kutisha mno.

32 Kichwa cha sanamu hiyo kilikuwa cha dhahabu safi, kifua chake na mikono yake vilikuwa vya fedha na tumbo lake na mapaja yake vilikuwa vya shaba.

33 Miguu yake ilikuwa ya chuma na nyayo zake zilikuwa za mchanganyiko wa chuma na udongo wa mfinyanzi.

34 Ukiwa bado unaangalia, jiwe lilingoka lenyewe, bila kuguswa, na kuipondaponda miguu ya shaba na udongo wa mfinyanzi ya ile sanamu, na kuivunja vipandevipande.

35 Mara kile chuma, udongo wa mfinyanzi, shaba, fedha na dhahabu, vyote vikavunjika vipandevipande na kuwa kama makapi ya mahali pa kupuria nafaka wakati wa kiangazi. Upepo ukavipeperushia mbali kisibakie hata kipande kimoja. Lakini lile jiwe lililoivunja ile sanamu likageuka kuwa mlima mkubwa na kuijaza dunia yote.

36 “Hiyo ndiyo ndoto yako, ee mfalme. Na sasa tutakupa maana yake.

37 Wewe, ee mfalme, mfalme wa wafalme! Mungu amekupa ufalme, uwezo, nguvu na utukufu!

38 Amekupa mamlaka juu ya wanaadamu wote, wanyama wa porini na ndege wote wa angani, kokote kule waliko. Wewe ndiwe kile kichwa cha dhahabu!

39 Baada yako utafuata ufalme mwingine, lakini ufalme huo utakuwa dhaifu. Huu utafuatwa na ufalme wa tatu unaofananishwa na shaba; huo utaitawala dunia yote.

40 Baada ya falme hizo, utafuata ufalme mwingine imara kama chuma. Na kama vile chuma kivunjavyo na kupondaponda vitu vyote, ndivyo ufalme huo utakavyovunjavunja na kusagilia mbali falme zilizotangulia.

41 Uliona pia kuwa nyayo na vidole vya sanamu hiyo vilikuwa nusu udongo wa mfinyanzi na nusu chuma. Hii ina maana kwamba ufalme huo utagawanyika; lakini utakuwa na kiasi fulani cha nguvu za chuma kwa sababu kulikuwa na chuma kilichochanganyikana na udongo wa mfinyanzi.

42 Kama ulivyoona, vidole vyake vya miguu vilikuwa nusu chuma na nusu udongo wa mfinyanzi, na hii inamaanisha kwamba ufalme huo utakuwa na nguvu kiasi fulani na udhaifu kiasi fulani.

43 Hii inamaanisha kwamba watawala wa ufalme huo watachanganyikana kwa kuoana na watu wasio wa taifa lao, lakini hawatafaulu kuchanganyikana kama vile chuma kisivyoweza kuchanganyikana na udongo wa mfinyanzi.

44 Wakati wa wafalme hao, Mungu wa mbinguni ataanzisha ufalme ambao kamwe hautaangamizwa. Watu wengine hawataushinda na kuutawala ufalme huo, bali ufalme huo utaziponda na kuzikomesha falme zilizotangulia, nao utadumu milele.

45 Uliliona jiwe lililongoka lenyewe toka mlimani, bila kuguswa, na jinsi lilivyoivunja vipandevipande ile sanamu iliyotengenezwa kwa chuma, shaba, udongo wa mfinyanzi, fedha na dhahabu. Ee mfalme, Mungu Mkuu amekufunulia mambo yatakayotukia baadaye. Mimi nimekusimulia. Ndoto yako ni ya kweli na maana yake ni halisi.”

46 Ndipo mfalme Nebukadneza alipoanguka kifudifudi na kumsujudia Danieli na kuamuru wamtolee Danieli tambiko na ubani.

47 Mfalme akamwambia Danieli, “Hakika, Mungu wako ni Mungu wa miungu na Bwana wa wafalme, na ndiye afumbuaye mafumbo kwa sababu umefaulu kunifumbulia fumbo hili.”

48 Kisha mfalme Nebukadneza akamtunukia Danieli heshima kubwa, akampa zawadi nyingi kubwakubwa, na kumfanya mtawala wa mkoa wote wa Babuloni, na mkuu wa wenye hekima wote wa Babuloni.

49 Danieli akamwomba mfalme, naye mfalme akawaweka Shadraki, Meshaki na Abednego kuwa wasimamizi wa mambo ya utawala ya mkoa wa Babuloni. Lakini Danieli akabakia katika jumba la mfalme.

3

1 Mfalme Nebukadneza alitengeneza sanamu ya dhahabu, yenye kimo mita ishirini na nane na upana mita tatu. Aliisimamisha katika sehemu tambarare ya Dura, mkoani Babuloni.

2 Kisha mfalme akaamuru maliwali, wasimamizi, wakuu wa mikoa, washauri, watunza hazina, majaji, mahakimu na maofisa wote wa mikoa wahudhurie sherehe ya kuzindua rasmi sanamu aliyoisimamisha.

3 Basi, maliwali, wasimamizi, wakuu wa mikoa, washauri, watunza hazina, majaji, mahakimu na maofisa wote wa mikoa wakakusanyika tayari kwa uzinduzi wa sanamu aliyosimamisha mfalme Nebukadneza.

4 Mpiga mbiu akatangaza kwa sauti kubwa, “Enyi watu wa makabila yote, mataifa yote na lugha zote, mnaamriwa kwamba

5 mkisikia sauti ya baragumu, filimbi, kinubi, zeze, santuri, zumari na sauti za ala nyingine za muziki, lazima mwiname chini na kuiabudu sanamu ya dhahabu aliyosimamisha mfalme Nebukadneza.

6 Na yeyote ambaye hatainama chini na kuiabudu, atatupwa mara moja katika tanuri ya moto mkali.”

7 Kwa hiyo, watu wote, mara waliposikia sauti za baragumu, filimbi, kinubi, zeze, santuri, zumari na sauti za ala nyingine za muziki, walianguka kifudifudi na kuiabudu ile sanamu ya dhahabu ambayo mfalme Nebukadneza aliisimamisha.

8 Wakati huo, baadhi ya Wakaldayo wakajitokeza na kuwashtaki Wayahudi. Walimwambia mfalme Nebukadneza,

9 “Uishi, ee mfalme!

10 Wewe, ee mfalme, ulitoa amri kuwa kila mtu anaposikia sauti ya baragumu, filimbi, kinubi, zeze, santuri, zumari na kila aina ya muziki, ainame chini na kuiabudu ile sanamu ya dhahabu.

11 Na kwamba mtu yeyote asiyeinama chini na kuiabudu sanamu hiyo, atupwe ndani ya tanuri ya moto mkali.

12 Sasa, kuna Wayahudi fulani uliowateua kushughulikia mambo ya utawala wa mkoa wa Babuloni, yaani Shadraki, Meshaki na Abednego; watu hawa, ee mfalme, hawakuitii amri yako. Wanakataa kuitumikia miungu yako na kuiabudu ile sanamu ya dhahabu uliyoisimamisha.”

13 Hapo mfalme Nebukadneza, huku akiwaka hasira, akaamuru Shadraki, Meshaki na Abednego waletwe mbele yake. Nao wakawaleta mbele ya mfalme.

14 Mfalme Nebukadneza akawauliza, “Je, ni kweli kwamba wewe Shadraki, wewe Meshaki na wewe Abednego, hamuitumikii miungu yangu wala kuiabudu ile sanamu ya dhahabu niliyoisimamisha?

15 Basi, mtakaposikia tena sauti ya baragumu, filimbi, kinubi, zeze, santuri, zumari na sauti za ala nyingine za muziki, je, mko tayari kuinama chini na kuiabudu sanamu niliyotengeneza? Kama mkikataa, mtatupwa mara moja katika tanuri ya moto mkali. Je, ni mungu gani anayeweza kuwaokoa mikononi mwangu?”

16 Shadraki, Meshaki na Abednego wakamjibu mfalme, “Ee Nebukadneza, sisi hatuhitaji kukujibu kuhusu jambo hilo.

17 Ikiwa ndivyo, Mungu wetu ambaye tunamtumikia aweza kutuokoa katika tanuri ya moto mkali; tena atatuokoa mikononi mwako, ee mfalme.

18 Lakini, hata kama haitafanyika hivyo, ujue wazi, ee mfalme, kwamba sisi hatutaitumikia miungu yako wala kuiabudu sanamu ya dhahabu uliyosimamisha.”

19 Hapo, mfalme Nebukadneza akawaka hasira, sura yake ikabadilika kwa chuki dhidi ya Shadraki, Meshaki na Abednego. Akaamuru mwako wa moto wa tanuri uongezwe mara saba kuliko kawaida yake.

20 Akaamuru watu fulani wenye nguvu kabisa katika jeshi lake wawafunge Shadraki, Meshaki na Abednego na kuwatupa katika ile tanuri ya moto mkali.

21 Basi, vijana hao wakafungwa hali wamevaa makoti yao, kanzu zao, kofia na mavazi yao mengine, wakatupwa katikati ya ile tanuri ya moto mkali.

22 Kwa vile amri ya mfalme ilikuwa kali, ule moto ulikuwa umewashwa ukawa mkali sana, hata ndimi za moto zikawateketeza wale watu waliowapeleka Shadraki, Meshaki na Abednego.

23 Ndipo Shadraki, Meshaki na Abednego, wakiwa wamefungwa, wakatumbukia katika ile tanuri ya moto mkali.

24 Basi, mfalme Nebukadneza akashangaa, akainuka kwa haraka na kuwauliza washauri wake, “Je, hatukuwafunga watu watatu na kuwatupa motoni?” Nao wakamjibu mfalme, “Naam, mfalme! Ndivyo!”

25 Kisha akauliza, “Lakini sasa mbona ninaona watu wanne wakitembeatembea humo motoni bila kufungwa na wala hawadhuriki, na mtu wa nne anaonekana kama mwana wa miungu?”

26 Basi, mfalme Nebukadneza akaukaribia mlango wa tanuri ya moto mkali, akaita, “Shadraki, Meshaki na Abednego, watumishi wa Mungu Mkuu, tokeni mje hapa!” Shadraki, Meshaki na Abednego wakatoka motoni.

27 Maliwali, wasimamizi, wakuu wa mikoa na washauri wa mfalme, wote wakakusanyika pamoja, wakaona ya kuwa ule moto haukuweza kuwaunguza hao watatu. Nywele zao hazikuungua, mavazi yao hayakuungua, wala hawakuwa na harufu yoyote ya moto.

28 Basi, mfalme Nebukadneza akasema, “Na asifiwe Mungu wa Shadraki, Meshaki na Abednego kwa kuwa alimtuma malaika wake na kuwaokoa watumishi wake ambao wanamtegemea. Wao walikataa kutii amri yangu ya kifalme, wakaitoa mhanga miili yao badala ya kuabudu mungu mwingine, ila Mungu wao peke yake.

29 Kwa hiyo, naamuru kwamba watu wa kabila lolote, taifa lolote au lugha yoyote, watakaosema kitu chochote dhidi ya Mungu wa Shadraki, Meshaki na Abednego, watangolewa viungo vyao kimojakimoja na nyumba zao zitabomolewa. Maana hakuna mungu mwingine awezaye kuokoa namna hii.”

30 Basi, mfalme Nebukadneza akawapandisha vyeo Shadraki, Meshaki na Abednego katika mkoa wa Babuloni.

4

1 “Mimi mfalme Nebukadneza, nawaandikia watu wa makabila yote, mataifa yote na lugha zote kote duniani. Nawatakieni amani tele!

2 Nimeona vema kuwajulisha ishara na maajabu ambayo Mungu Mkuu amenionesha.

3 Jinsi gani zilivyo kubwa ishara zake Mungu! Maajabu yake ni makuu mno! Ufalme wake ni ufalme wa milele; enzi yake yadumu kizazi hata kizazi.

4 “Mimi, Nebukadneza, nilikuwa ninaishi raha mstarehe nyumbani kwangu na kufana katika ikulu yangu.

5 Lakini nikaota ndoto iliyonitisha; nikiwa nimelala kitandani, mawazo na maono kichwani mwangu yaliniogopesha.

6 Hivyo, nikaamuru wenye hekima wote wa Babuloni waletwe mbele yangu ili wanieleze maana ya ndoto hiyo.

7 Ndipo waganga, walozi, Wakaldayo na wanajimu wakaletwa. Nikawasimulia ndoto yangu, lakini hawakuweza kunieleza maana yake.

8 Baadaye, akaja Danieli, anayeitwa pia Belteshaza, jina la mungu wangu, ambaye roho ya miungu mitakatifu imo ndani yake. Nami nikamsimulia ndoto yangu, nikasema:

9 Ee Belteshaza, uliye mkuu wa waganga, nafahamu kuwa roho ya miungu mitakatifu imo ndani yako, na kwamba hakuna fumbo lililo gumu kwako. Hii ndiyo ndoto yangu; niambie maana yake.

10 “Nilipokuwa nimelala, niliona maono haya: Niliona mti mrefu sana katikati ya dunia.

11 Mti uliendelea kukua, ukawa imara na kilele chake kikafika mbinguni. Uliweza kuonekana kutoka kila mahali duniani.

12 Majani yake yalikuwa mazuri. Ulikuwa umejaa matunda, kiasi cha kuitosheleza dunia nzima. Wanyama wote wa porini walipata kivuli chini yake, na ndege wa angani walikaa katika matawi yake. Viumbe vyote vilipata chakula kutoka mti huo.

13 “Nilipokuwa nimelala kitandani, niliona maono: Mlinzi mtakatifu alishuka kutoka mbinguni.

14 Akapaaza sauti akisema, ‘Kateni mti huu na kuyakatakata matawi yake. Pukuteni majani yake na kuyatawanya matunda yake. Wanyama na watoroke chini yake na ndege kutoka matawi yake.

15 Lakini acheni kisiki chake na mizizi yake ardhini, kwenye majani mabichi ya kondeni kikiwa kimefungwa hapo kwa mnyororo wa chuma na shaba. Mwacheni mtu huyo aloweshwe kwa umande wa mbinguni; mwacheni aishi pamoja na wanyama wa porini na kula nyasi mbugani.

16 Akili yake ya utu ibadilishwe, awe na akili ya mnyama kwa miaka saba.

17 Hii ni hukumu iliyotangazwa na walinzi; ni uamuzi wa walio watakatifu, ili wanaadamu wote kila mahali wapate kutambua kuwa Mungu Mkuu anayo mamlaka juu ya falme zote za wanaadamu; yeye humpa ufalme mtu yeyote ampendaye, humfanya mfalme hata mtu duni wa mwisho.’

18 “Hii ndiyo ndoto niliyoota mimi Nebukadneza. Sasa, wewe Belteshaza, nieleze maana yake; kwani wenye hekima wote katika ufalme wangu hawawezi kuniambia maana yake; lakini wewe utaweza kwa kuwa roho ya miungu mitakatifu imo ndani yako.”

19 Hapo, Danieli, aliyeitwa pia Belteshaza, akashangaa kwa muda, na fikira zake zikamfadhaisha. Mfalme akamwambia, “Belteshaza, ndoto hii, wala maana yake visikufadhaishe!” Belteshaza akamjibu, “Bwana wangu, laiti ndoto hii na maana yake ingewahusu adui zako!

20 Mti uliouona ukiwa mkubwa na wenye nguvu, ambao matawi yake marefu yalifika mbinguni, nao ukionekana kutoka kila mahali duniani,

21 majani yake yakiwa mazuri, na matunda yake mengi ya kulisha viumbe vyote, wanyama wa porini wakipata kivuli chini yake, na ndege wa angani wakikaa katika matawi yake,

22 basi, ni wewe ee mfalme ambaye umekuwa mkubwa na mwenye nguvu. Ukuu wako umefika mpaka mbinguni, na ufalme wako umeenea mpaka miisho ya dunia.

23 Kisha ukaona tena, ee mfalme, Mlinzi mtakatifu akishuka kutoka mbinguni, akaamuru: ‘Ukateni mti huu, mkauangamize. Lakini acheni kisiki chake na mizizi yake ardhini kwenye majani mabichi ya kondeni, kikiwa kimefungwa hapo kwa mnyororo wa chuma na shaba. Mwacheni mtu huyo aloweshwe kwa umande wa mbinguni; mwacheni aishi pamoja na wanyama wa porini kwa miaka saba.’

24 “Hii basi, bwana wangu, ndiyo maana ya ndoto yako, kadiri ya uamuzi wa Mungu Mkuu juu yako:

25 Wewe utafukuzwa mbali na wanaadamu! Utaishi pamoja na wanyama wa porini, utakula majani kama ng'ombe; utalowa kwa umande wa mbinguni. Utakaa katika hali hiyo kwa miaka saba, na mwishowe utatambua kwamba Mungu Mkuu ndiye mwenye uwezo juu ya falme za wanaadamu, na humpa ufalme mtu yeyote amtakaye.

26 Tena amri ile ya kukiacha kisiki na mizizi ya mti huo ardhini ina maana hii: Wewe utarudishiwa tena ufalme wako hapo utakapotambua kwamba Mungu wa mbinguni ndiye atawalaye.

27 Kwa sababu hiyo, ee mfalme, sikiliza shauri langu. Achana na dhambi zako na maovu yako, utende haki na kuwaonea huruma waliodhulumiwa; huenda muda wako wa fanaka ukarefushwa!”

28 Hayo yote yalimpata mfalme Nebukadneza.

29 Miezi kumi na miwili baadaye, mfalme Nebukadneza alikuwa anatembea juu ya dari ya ikulu ya mji wa Babuloni.

30 Basi, akasema kwa sauti, “Tazama Babuloni, mji mkuu nilioujenga kwa nguvu zangu uwe makao yangu ya kifalme na kwa ajili ya utukufu wangu!”

31 Mara tu alipotamka maneno hayo, sauti kutoka mbinguni ikatamka: “Ewe mfalme Nebukadneza, sikiliza ujumbe huu juu yako! Ufalme umekutoka!

32 Utafukuzwa mbali na wanaadamu! Utaishi pamoja na wanyama wa porini kondeni, na utakula majani kama ng'ombe! Utakaa katika hali hiyo kwa muda wa miaka saba, na mwishowe utatambua kwamba Mungu Mkuu ndiye mwenye uwezo juu ya falme za wanaadamu, na humpa ufalme mtu yeyote amtakaye.”

33 Mara moja jambo hilo juu ya mfalme Nebukadneza likatekelezwa. Alifukuzwa mbali na wanaadamu, akawa anakula majani kama ng'ombe. Alilowa kwa umande wa mbinguni, na nywele zake zikawa ndefu kama manyoya ya tai, na kucha zake kama za ndege.

34 “Mwishoni mwa ile miaka saba, mimi Nebukadneza niliinua macho yangu kutazama juu mbinguni na akili zangu zikanirudia. Nilimshukuru Mungu Mkuu na kumheshimu yeye aishiye milele: Kwa sababu enzi yake ni enzi ya milele, ufalme wake wadumu kizazi hata kizazi.

35 Wakazi wote wa dunia si kitu; hufanya atakavyo na viumbe vya mbinguni, na wakazi wa duniani; hakuna awezaye kumpinga, au kusema ‘Unafanya nini?’

36 “Wakati huo huo akili zangu zikanirudia; nilirudishiwa pia heshima yangu, fahari yangu na utukufu wa ufalme wangu. Washauri na maofisa wangu walikuja kunitafuta, nikarudishwa katika ufalme wangu na kupata heshima kama pale awali.

37 “Na sasa, mimi Nebukadneza ninamsifu na kumtukuza na kumheshimu mfalme wa mbinguni. Maana matendo yake yote ni ya haki, naye huwashusha wenye kiburi.”

5

1 Siku moja mfalme Belshaza aliwaandalia karamu kubwa maelfu ya wakuu wake na kunywa divai pamoja nao.

2 Kutokana na kunywa divai, mfalme Belshaza akatoa amri vile vyombo vya dhahabu na fedha ambavyo mfalme Nebukadneza, baba yake, alivichukua kutoka hekalu la Yerusalemu, viletwe ili avitumie kunywea divai pamoja na maofisa wake, wake zake na masuria wake.

3 Basi, vile vyombo vya dhahabu na fedha vilivyochukuliwa hekaluni Yerusalemu vikaletwa. Mfalme, maofisa wake, wake zake na masuria wake wakavitumia kunywea.

4 Walikunywa huku wanaisifu miungu iliyotengenezwa kwa dhahabu, fedha, shaba, chuma, miti na mawe.

5 Mara, vidole vya mkono wa mwanaadamu vikatokea na kuandika kwenye lipu ya ukuta wa ikulu ya mfalme, mahali palipomulikwa vizuri, mkabala na kinara cha taa. Mfalme aliuona mkono huo ukiandika.

6 Basi, mfalme akabadilika rangi na fikira zake zikamfadhaisha, viungo vyake vikalegea na magoti yakaanza kutetemeka.

7 Mfalme Belshaza akapaaza sauti waletwe wachawi, Wakaldayo wenye hekima na wanajimu waletwe. Walipoletwa, mfalme akawaambia wenye hekima hao wa Babuloni, “Yeyote atakayesoma maandishi haya na kunijulisha maana yake, atavishwa mavazi rasmi ya zambarau na mkufu wa dhahabu shingoni mwake, na kupewa nafasi ya tatu katika ufalme.”

8 Basi, wenye hekima wote wa mfalme wakaja, lakini hawakuweza kuyasoma maandishi hayo wala kumjulisha mfalme maana yake.

9 Basi, mfalme Belshaza akazidi kuhangaika na rangi yake ikazidi kugeuka, nao wakuu wake wakawa na wasiwasi.

10 Kutokana na kelele za mfalme na wakuu wake, mama mfalme aliingia ukumbini mwa karamu, akasema, “Uishi, ee mfalme! Si lazima mawazo yako yakufadhaishe na kubadilika rangi yako.

11 Katika ufalme wako yupo mtu ambaye roho ya miungu mitakatifu imo ndani yake. Wakati wa utawala wa baba yako, mtu huyu alidhihirika kuwa mwenye ujuzi, ufahamu na hekima kama ya miungu. Baba yako, mfalme Nebukadneza, alimfanya kuwa mkuu wa waaguzi, wachawi, Wakaldayo wenye hekima, na wanajimu,

12 kwa sababu ana roho njema, maarifa, ujuzi wa kufasiri ndoto, kufumbua mafumbo na kutatua matatizo. Jina la mtu huyo ni Danieli ambaye baba yako alimwita Belteshaza. Basi na aitwe, naye atakueleza maana ya maandishi haya.”

13 Hapo, Danieli akaletwa mbele ya mfalme, naye mfalme akamwuliza: “Je, wewe ndiwe Danieli, mmoja wa mateka aliowaleta baba yangu mfalme, kutoka nchi ya Yuda?

14 Nimesikia kwamba roho ya miungu mitakatifu imo ndani yako, na kwamba una ujuzi, na akili, na hekima ya ajabu.

15 Wenye hekima na wachawi walipoletwa hapa kusoma na kunieleza maana ya maandishi haya, walishindwa.

16 Lakini, nimesikia kwamba wewe unaweza kueleza vitendawili na kutambua mafumbo. Basi, kama ukifaulu kusoma maandishi haya na kunieleza maana yake, utavishwa mavazi rasmi ya zambarau na kuvishwa mkufu wa dhahabu shingoni mwako. Utapewa nafasi ya tatu katika ufalme huu.”

17 Danieli akamjibu mfalme Belshaza, “Waweza kukaa na zawadi zako ee mfalme au kumpa mtu mwingine. Hata hivyo, ee mfalme, nitakusomea maandishi hayo na kukueleza maana yake.

18 Ee mfalme, Mungu Mkuu alimpa baba yako mfalme Nebukadneza, ufalme, ukuu, fahari na utukufu.

19 Kwa sababu ya ukuu aliompa, watu wa makabila yote, mataifa yote na lugha zote walitetemeka na kumwogopa. Nebukadneza aliweza kumuua mtu yeyote aliyetaka na kumwacha hai yeyote aliyetaka. Aliyetaka kumpandisha cheo alimpandisha, aliyetaka kumshusha cheo alimshusha.

20 Lakini alipoanza kuwa na kiburi, akawa na roho ngumu na mwenye majivuno, aliondolewa katika kiti chake cha enzi, akanyanganywa utukufu wake.

21 Alifukuzwa mbali na wanaadamu, akili yake ikafanywa kama ya mnyama, akaishi na pundamwitu, akawa anakula majani kama ng'ombe. Alinyeshewa mvua mwilini mpaka alipotambua kwamba Mungu Mkuu ndiye atawalaye falme za wanaadamu, naye humweka mfalme yeyote amtakaye.

22 Lakini wewe Belshaza, mwanawe, ingawa unayajua haya yote, hukujinyenyekeza!

23 Badala yake umejikuza mwenyewe dhidi ya Bwana wa mbinguni: Umeleta vyombo vya nyumba yake Mungu ukavitumia kunywea divai, wewe, maofisa wako, wake zako na masuria wako, na kuisifu miungu iliyotengenezwa kwa fedha, dhahabu, shaba, chuma, miti na mawe; miungu ambayo haioni, haisikii wala haijui lolote. Lakini Mungu, ambaye uhai wako u mkononi mwake, na njia zako zi wazi mbele yake, hukumheshimu!

24 Basi, Mungu ametuma mkono uandike maandishi haya.

25 “Maandishi yenyewe ni: ‘MENE, MENE, TEKELI, PARSINI.’

26 Na hii ndiyo maana yake: MENE maana yake, Mungu amehesabu siku za ufalme wako na kuukomesha.

27 TEKELI maana yake, wewe umepimwa katika mizani, nawe ukaonekana huna uzito wowote.

28 PERESI maana yake, ufalme wako umegawanywa kati ya Wamedi na Wapersi.”

29 Hapo, mfalme Belshaza akaamuru Danieli avishwe mavazi rasmi ya zambarau na mkufu wa dhahabu shingoni. Ikatangazwa kuwa Danieli atashikilia nafasi ya tatu katika ufalme.

30 Usiku huo huo, mfalme Belshaza wa Wakaldayo, aliuawa;

31 naye mfalme Dario, Mmedi, akashika utawala akiwa na umri wa miaka sitini na miwili.

6

1 Mfalme Dario aliamua kuteua wakuu 120 kusimamia mambo ya utawala.

2 Aliwateua pia wakuu watatu, Danieli akiwa mmojawapo, wawasimamie wale wakuu wengine na maslahi ya mfalme, asije akapata hasara.

3 Muda si muda, Danieli akadhihirika kuwa bora kuliko wale wasimamizi wengine na wakuu wote kwa kuwa alikuwa na roho njema. Hivyo mfalme akanuia kumpa uongozi wa ufalme wote.

4 Wale wakuu pamoja na maliwali wakatafuta kisingizio cha kumshtaki Danieli kuhusu mambo ya ufalme, lakini hawakuweza kupata sababu ya kumlaumu, wala kosa lolote, kwani Danieli alikuwa mwaminifu. Hakupatikana na kosa, wala hatia yoyote.

5 Ndipo wakapatana hivi: “Hatutapata kisingizio chochote cha kumshtaki Danieli isipokuwa kama kisingizio hicho kitakuwa kinahusu sheria ya Mungu wake.”

6 Basi, hao wakuu na maliwali kwa pamoja, wakamwendea mfalme na kumwambia, “Uishi ee mfalme Dario!

7 Sisi wakuu uliotuweka, wasimamizi, maliwali, washauri na wakuu wa mikoa, sote tumepatana kuwa inafaa, ee mfalme, utoe amri na kuhakikisha inafuatwa kikamilifu. Amuru kwamba kwa muda wa siku thelathini kusiwe na mtu yeyote atakayeruhusiwa kuomba kitu chochote kwa mungu yeyote au kwa mtu yeyote, isipokuwa kutoka kwako wewe, ewe mfalme. Mtu yeyote atakayevunja sheria hii na atupwe katika pango la simba.

8 Hivyo, ee mfalme Dario, utoe amri hiyo na kuitia hati sahihi yako ili isibadilishwe. Nayo itakuwa sheria ya Wamedi na Wapersi, sheria ambayo haibatilishwi.”

9 Hivyo, mfalme Dario akaitia sahihi hati ya sheria hiyo.

10 Danieli alipojua kuwa ile hati imetiwa sahihi, alirudi nyumbani kwake ghorofani katika chumba chake kilichokuwa na madirisha yaliyofunguka kuelekea Yerusalemu. Humo, Danieli, kama ilivyokuwa kawaida yake, alipiga magoti mara tatu kila siku akamwomba na kumshukuru Mungu wake.

11 Watu wale waliofanya mpango dhidi ya Danieli waliingia ndani, wakamkuta Danieli akiomba dua na kumsihi Mungu wake.

12 Basi, walikwenda kwa mfalme na kumshtaki Danieli kwa kutumia ile sheria, wakisema, “Mfalme Dario, je, hukutia sahihi hati ya sheria kuwa kwa muda wa siku thelathini hakuna mtu yeyote atakayeruhusiwa kuomba kitu chochote, kwa mungu yeyote, au kwa mtu yeyote isipokuwa kutoka kwako wewe, ee mfalme, na kwamba yeyote atakayevunja sheria hii atatumbukizwa katika pango la simba?” Mfalme akaitikia, “Hivyo ndivyo ilivyo, kulingana na sheria ya Wamedi na Wapersi ambayo haiwezi kubatilishwa.”

13 Wakamwambia mfalme, “Yule Danieli aliye mmoja wa mateka kutoka nchi ya Yuda hakuheshimu wewe mfalme wala haitii amri uliyotia sahihi. Yeye anasali mara tatu kila siku.”

14 Mfalme aliposikia maneno hayo, alisikitika sana. Akajitahidi sana kupata njia ya kumwokoa Danieli. Aliendelea kujaribu mpaka jua likatua.

15 Wale watu wakamwendea mfalme Dario kwa pamoja na kumwambia, “Ee mfalme, ujue kuwa hakuna sheria wala amri yoyote ya Wamedi na Wapersi inayoweza kubatilishwa baada ya kuwekwa na mfalme.”

16 Ndipo mfalme Dario akatoa amri, naye Danieli akaletwa na kutupwa katika pango la simba. Mfalme akamwambia Danieli, “Mungu wako ambaye unamtumikia daima, na akuokoe.”

17 Jiwe likaletwa na kuwekwa mlangoni mwa lile pango. Mfalme akalipiga mhuri wake binafsi na ule wa wakuu wake, ili uamuzi kuhusu Danieli usibatilishwe.

18 Kisha mfalme akarudi katika ikuluni yake ambamo alikesha akifunga; hakufanya tafrija ya aina yoyote, na usingizi ukampaa.

19 Alfajiri na mapema, mfalme Dario aliamka, akaenda kwa haraka kwenye pango la simba.

20 Alipofika karibu akamwita Danieli kwa sauti ya huzuni, “Danieli, mtumishi wa Mungu aliye hai! Je, Mungu wako unayemtumikia daima ameweza kukuokoa na simba hawa?”

21 Danieli akamjibu mfalme, “Uishi, ee mfalme!

22 Mungu wangu alileta malaika wake kuvifumba vinywa vya simba hawa, nao hawakunidhuru. Alifanya hivyo kwa sababu alijua mimi sina lawama yoyote kwake na wala sijafanya lolote baya mbele yako.”

23 Hapo mfalme akafurahi sana; akaamuru Danieli atolewe pangoni. Basi wakamtoa, naye alikuwa hajadhurika hata kidogo, kwa sababu alimtegemea Mungu wake.

24 Mfalme akaamuru wale watu waliomchongea Danieli wakamatwe, nao wakatupwa ndani ya lile pango la simba pamoja na wake zao na watoto wao. Nao, hata kabla hawajagusa chini, simba waliwashambulia na kuivunjavunja mifupa yao.

25 Ndipo mfalme Dario akawaandikia watu wa makabila yote, mataifa yote, na lugha zote duniani: “Nawatakieni amani kwa wingi.

26 Nitatoa amri kwamba watu wote katika ufalme wangu ni lazima wamwogope na kumcha Mungu wa Danieli. “Yeye ni Mungu aliye hai, aishiye milele; ufalme wake kamwe hauwezi kuangamizwa, utawala wake hauna mwisho.

27 Yeye hukomboa na kuokoa, hufanya ishara na maajabu mbinguni na duniani, maana amemwokoa Danieli makuchani mwa simba.”

28 Basi, Danieli akapata fanaka wakati wa utawala wa mfalme Dario na wa mfalme Koreshi, Mpersi.

7

1 Mnamo mwaka wa kwanza wa utawala wa mfalme Belshaza wa Babuloni, Danieli aliota ndoto na kuona maono akiwa amelala kitandani mwake. Aliiandika ndoto yake hii:

2 “Mimi Danieli niliona katika maono usiku, pepo nne toka pande zote za mbinguni zikiichafua bahari kuu.

3 Wanyama wakubwa wanne, wakainuka kutoka humo baharini, kila mmoja tofauti na mwenzake.

4 Mnyama wa kwanza alikuwa kama simba, na alikuwa na mabawa kama ya tai. Nikiwa namwangalia, mabawa yake yalingolewa, naye akainuliwa na kusimama kwa miguu miwili kama binadamu. Kisha, akapewa akili ya binadamu.

5 “Mnyama wa pili alikuwa kama dubu ambaye upande wake mmoja ulikuwa umeinuka. Kinywani mwake alikuwa na mbavu tatu alizozishikilia kwa meno yake. Sauti ikamwambia, ‘Haya, kula nyama nyingi kadiri uwezavyo.’

6 “Baada ya hayo, nilimwona mnyama mwingine. Huyu alikuwa kama chui mwenye mabawa manne ya ndege mgongoni mwake. Alikuwa na vichwa vinne na alipewa mamlaka.

7 “Kisha, katika maono yangu hayo ya usiku nikamwona mnyama wa nne wa ajabu na wa kutisha, mwenye nguvu sana. Huyu alikuwa na meno makubwa ya chuma ambayo aliyatumia kula na kuvunjavunja, na mabaki aliyakanyagakanyaga kwa nyayo zake. Alikuwa tofauti na wale wanyama wengine watatu, kwani alikuwa na pembe kumi.

8 Nilipokuwa naziangalia hizo pembe, niliona upembe mwingine mdogo ukiota miongoni mwa zile kumi. Ili kuupa nafasi upembe huu zile pembe nyingine tatu zilingolewa pamoja na mizizi yake. Ulikuwa na macho ya binadamu na kinywa kilichotamka maneno ya kujigamba.

9 “Nikiwa bado naangalia, viti vya enzi viliwekwa hapo, kisha ‘Mzee wa kale na kale’ akaja, akaketi. Alikuwa amevaa vazi jeupe kama theluji; nywele zake zilikuwa kama sufu safi. Kiti chake cha enzi kilikuwa cha miali ya moto na magurudumu ya kiti chake yalikuwa ya moto uwakao.

10 Kutoka kiti hicho kijito cha moto kilibubujika, kikatiririka. Maelfu walimtumikia, na mamilioni walisimama mbele yake. Mahakama ikawa tayari kwa kikao, na vitabu vikafunguliwa.

11 “Kutokana na maneno ya kujigamba yaliyokuwa yanasemwa na ile pembe, nikatazama. Nikiwa natazama, huyo mnyama wa nne aliuawa, mwili wake ukaharibiwa na kutolewa uchomwe moto.

12 Wale wanyama wengine walinyanganywa mamlaka yao, lakini wao wenyewe wakaachwa waendelee kuishi kwa muda fulani.

13 “Wakati wa maono haya usiku, niliona mmoja kama mwana wa mtu akija katika mawingu, akamwendea yule ‘Mzee wa kale na kale,’ wakanileta mbele yake.

14 Akapewa mamlaka, utukufu na ufalme, ili watu wa makabila yote, mataifa yote na lugha zote wamtumikie. Utawala wake ni wa milele na ufalme wake kamwe hautaangamizwa.

15 “Maono niliyoyaona mimi Danieli yalinishtua, nami nikafadhaika.

16 Nilimkaribia mmojawapo wa wale waliosimama huko na kumwuliza maana halisi ya mambo hayo yote. Naye akanisimulia na kunieleza maana yake:

17 ‘Wanyama hao wanne wakubwa ni wafalme wanne watakaotokea duniani.

18 Lakini watakatifu wa Mungu Mkuu watapewa ufalme, nao wataumiliki ufalme huo milele na milele.’

19 “Kisha nikataka nielezwe juu ya yule mnyama wa nne, ambaye alikuwa tofauti kabisa na wale wengine, wa ajabu na wa kutisha sana, ambaye meno yake yalikuwa ya chuma na makucha yake ya shaba. Aliyatumia meno hayo kula na kuvunjavunja, na mabaki aliyakanyagakanyaga kwa nyayo zake.

20 Aidha nilitaka nielezwe juu ya zile pembe kumi alizokuwa nazo kichwani mwake, na ule upembe mmoja ambao kabla haujaota, zilingoka pembe tatu; upembe uliokuwa na macho na kinywa ambacho kilitamka maneno ya kujigamba, na ambao ulionekana kuwa mkubwa kuliko pembe nyingine.

21 “Nikiwa bado naangalia, pembe hiyo ilipigana vita na watakatifu, nayo ikawashinda.

22 Lakini yule ‘Mzee wa kale na kale’ akainuka, akawapa haki watakatifu wa Mungu na wakati ulipotimia, hao watakatifu wakapewa ufalme.

23 “Nikaelezwa hivi: ‘Yule mnyama wa nne ni ufalme wa nne utakaokuwako duniani. Ufalme huo utakuwa tofauti na falme nyingine, nao utaiangamiza dunia nzima. Utaibwaga chini na kuipasua vipandevipande.

24 Zile pembe kumi ni wafalme kumi watakaotokana na ufalme huo. Halafu watafuatwa na mfalme mwingine ambaye atakuwa tofauti na wale waliomtangulia, na atawaangusha wafalme watatu.

25 Huyo atamkufuru Mungu Mkuu na kuwatesa watakatifu wake. Atajaribu kubadilisha nyakati na sheria zao, na watakatifu watatiwa mikononi mwake kwa muda wa miaka mitatu na nusu.

26 Lakini mahakama itafanya kikao; watamnyanganya utawala wake, nao utafutwa na kuangamizwa kabisa.

27 Ufalme, utawala na ukuu wa falme zote duniani watapewa watu wa watakatifu wa Mungu Mkuu. Ufalme wao utakuwa wa kudumu milele, na tawala zote zitawatumikia na kuwatii.’

28 “Huu ndio mwisho wa jambo hilo. Mawazo yangu yalinishtua sana mimi Danieli, hata rangi yangu ikabadilika. Lakini nililiweka jambo hilo moyoni mwangu.

8

1 “Mnamo mwaka wa tatu wa utawala wa mfalme Belshaza, maono mengine yalinijia mimi Danieli, licha ya maono yale ya kwanza.

2 Katika maono haya, nilijikuta niko Susa, mji mkuu wa mkoa wa Elamu. Nilikuwa nimesimama kando ya mto Ulai.

3 Nilipoinua macho yangu, niliona kondoo dume amesimama kando ya mto huo. Kondoo huyo alikuwa na pembe mbili ndefu, lakini moja ilikuwa ndefu zaidi, nayo ilitokea baada ya ile nyingine.

4 Nilimwona huyo kondoo dume akishambulia kuelekea magharibi, kaskazini na kusini. Hakuna mnyama yeyote aliyethubutu kusimama mbele yake, wala kuzikwepa nguvu zake. Alifanya apendavyo na kujikweza mwenyewe.

5 “Nilipokuwa ninawaza juu ya jambo hili, niliona beberu mmoja kutoka upande wa magharibi akija kasi bila kugusa ardhi. Kati ya macho yake alikuwa na pembe moja kubwa sana.

6 Alimwendea yule kondoo dume mwenye pembe mbili niliyemwona akiwa amesimama kando ya mto, akamshambulia kwa nguvu zake zote.

7 Nilimwona akimsogelea yule kondoo dume. Alikuwa amemkasirikia sana yule kondoo dume, hivyo akamshambulia kwa nguvu na kuzivunja zile pembe zake mbili. Yule kondoo dume hakuweza kustahimili. Alibwagwa chini na kukanyagwakanyagwa, wala hapakuwa na yeyote wa kumwokoa katika nguvu zake.

8 Hapo yule beberu alijikweza sana. Lakini alipofikia kilele cha nguvu zake, ile pembe yake kubwa ikavunjika. Badala yake zikaota pembe nne zilizoonekana waziwazi, zikiwa zimeelekea pande nne za pepo.

9 “Katika mojawapo ya pembe hizo nne, paliota upembe mwingine mdogo, ukakua sana kuelekea upande wa kusini-mashariki, na kuelekea nchi ile nzuri mno.

10 Upembe huo ulikua sana kufikia viumbe vya mbinguni; ukaziangusha chini baadhi ya nyota na kuzikanyagakanyaga.

11 Upembe huo ukajikweza juu ya mkuu wa viumbe vya mbinguni. Ukakomesha tambiko za kuteketezwa ambazo mkuu wa viumbe vya mbinguni alitambikiwa kila siku, na kukufuru maskani yake.

12 Viumbe vya mbinguni vikatiwa nguvuni mwake pamoja na tambiko za kuteketezwa kila siku, kwa njia ya upotovu. Nao ukweli ukatupwa chini. Upembe huo ukaibwaga chini ibada ya kweli. Ulifanikiwa katika kila jambo ulilofanya.

13 “Kisha, nikamsikia mtakatifu mmoja akizungumza na mwenzake. Huyo mwenzake alimwuliza, ‘Je, matukio yaliyotangazwa na maono haya yataendelea kwa muda gani? Kwa muda gani sadaka za kuteketezwa za kila siku zitabaki zimebatilishwa? Kwa muda gani upotovu wa kuangamiza kila kitu utaendelea, na mahali patakatifu pamoja na viumbe vya mbingu vitaendelea kukanyagwa?’

14 Yule mtakatifu wa kwanza akamjibu, ‘Kwa muda wa nyakati za jioni na asubuhi 2,300. Kisha maskani ya Mungu itapata tena hali yake halisi.’

15 “Mimi Danieli nilipoyaona hayo maono, na nilipokuwa nikijaribu kujua maana yake, ghafla, mmoja kama mwanaadamu akasimama mbele yangu.

16 Nikasikia sauti ya mwanaadamu kutoka katika mto Ulai ikiita, ‘Gabrieli, mweleze mtu huyu maana ya maono aliyoona.’

17 Gabrieli akaja karibu na mahali niliposimama. Mimi nikaogopa sana, hata nikaanguka kifudifudi. Lakini akaniambia, ‘Wewe mtu, elewa kwamba maono uliyoyaona yanahusu wakati wa mwisho.’

18 “Alipokuwa anazungumza nami, mimi nikashikwa na usingizi mzito huku nimelala kifudifudi. Lakini yeye akanishika na kunisimamisha.

19 Kisha akaniambia, ‘Sikiliza, ninakufahamisha matokeo ya ghadhabu ya Mungu yatakavyokuwa. Maono hayo yanahusu wakati wa mwisho.

20 “ ‘Yule kondoo dume uliyemwona mwenye pembe mbili, ni wafalme wa Media na Persia.

21 Yule beberu ni mfalme wa Ugiriki. Ile pembe kubwa katikati ya macho yake ni mfalme wa kwanza.

22 Ile pembe iliyovunjika na badala yake zikaota pembe nne, ina maana kwamba ufalme huo mmoja utagawanyika kuwa falme nne, lakini falme hizo hazitakuwa na nguvu kama ule ufalme wa kwanza.

23 Wakati falme hizo zitakapofikia kikomo chake na uovu wao kufikia kilele chake, patatokea mfalme mmoja shupavu na mwerevu.

24 Atakuwa mwenye mamlaka makubwa, atasababisha uharibifu mbaya sana, na atafanikiwa katika kila atendalo. Atawaangamiza watu maarufu na watakatifu wa Mungu.

25 Kwa ujanja wake, atafanikiwa katika mipango yake ya hila, naye atajikweza. Atawaangamiza watu wengi bila taarifa, na atataka kupigana na Mkuu wa wakuu, lakini ataangamizwa pasipo kutumia nguvu za kibinadamu.

26 Maono ya hizo nyakati za jioni na za asubuhi ambayo yameelezwa ni ya kweli. Lakini uyafiche, kwani ni siri, na bado utapita muda mrefu kabla hayajatimia.’

27 “Mimi Danieli, nikazimia na kuugua kwa muda. Nilipopona, nikaendelea na shughuli za mfalme. Lakini yale maono yalinistaajabisha, nami sikuweza kuyaelewa.

9

1 “Katika mwaka Dario mwana wa Ahasuero, Mmedi, alipoanza kutawala juu ya milki ya Wakaldayo,

2 mimi Danieli nilikuwa nikivisoma kwa makini vitabu vitakatifu, na humo nikaelewa maana ya jambo lile Mwenyezi-Mungu alilomfahamisha nabii Yeremia kuhusu ile miaka sabini, muda ambao utahusika na kuharibiwa kwa Yerusalemu.

3 Nilimwomba Mwenyezi-Mungu, kwa moyo, nikimtolea dua pamoja na kufunga, nikavaa vazi la gunia na kuketi kwenye majivu.

4 Nilimwomba Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu, na kuungama, nikisema: “Ee Bwana, wewe ni Mungu mkuu na wa kuogofya. Wewe ni mwaminifu kwa agano lako na unawafadhili wakupendao na kuzitii amri zako.

5 Tumetenda dhambi, tumekosa, tumetenda maovu na kukuasi. Tumezikiuka amri zako na kanuni zako.

6 Hatukuwasikiliza watumishi wako manabii, ambao kwa jina lako waliongea na wafalme wetu, wakuu wetu, wazee wetu na taifa letu lote.

7 Kwako, ee Bwana, kuna uadilifu, lakini sisi daima tumejaa aibu. Jambo hili ni kweli kwetu sote tuishio Yudea, wakazi wa mji wa Yerusalemu na Waisraeli wote ambao umewatawanya katika nchi za mbali na za karibu kwa sababu ya kukosa uaminifu kwako.

8 Aibu, ee Bwana, ni juu yetu, wafalme wetu, wakuu wetu na wazee wetu, kwa sababu tumekukosea.

9 Wewe, Bwana Mungu wetu, una huruma na msamaha, ingawa sisi tumekuasi.

10 Tulikataa kukusikiliza, ee Bwana, Mungu wetu; hatukuishi kulingana na sheria zako ulizotupa kwa njia ya watumishi wako manabii.

11 Waisraeli wote wameiasi sheria yako, wamekuacha wakakataa kukutii. Kwa sababu tumekukosea, tumemwagiwa laana na viapo vilivyoandikwa katika sheria ya Mose, mtumishi wako.

12 Umethibitisha yale uliyosema utatutenda sisi pamoja na watawala wetu kwa kuuadhibu mji wa Yerusalemu vikali zaidi ya mji mwingine wowote duniani.

13 Umetuadhibu kama ilivyoandikwa katika sheria ya Mose, lakini mpaka sasa, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, hatukuomba msamaha wako kwa kuziacha dhambi zetu na kutafakari uaminifu wako.

14 Kwa hiyo, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, ulikuwa tayari kutuadhibu, na ukafanya hivyo, kwa kuwa daima unafanya yaliyo ya haki, nasi hatukukusikiliza.

15 “Na sasa ee Bwana, Mungu wetu, uliyewatoa watu wako nchini Misri kwa nguvu yako kuu na kulifanya jina lako litukuke mpaka sasa, tunasema kwamba tumetenda dhambi; tumefanya maovu.

16 Ee Bwana, kwa kadiri ya matendo yako ya haki usiukasirikie wala kuughadhibikia mji wako wa Yerusalemu, mlima wako mtakatifu. Watu wote wa nchi za jirani wanaudharau mji wa Yerusalemu na watu wako, kwa sababu ya dhambi zetu na maovu waliyotenda wazee wetu.

17 Kwa hiyo, ee Mungu, isikilize sala yangu na maombi yangu mimi mtumishi wako. Kwa hisani yako, uifadhili tena maskani yako iliyoharibiwa.

18 Tega sikio, ee Mungu wangu; angalia uone taabu tulizo nazo na jinsi unavyotaabika huo mji uitwao kwa jina lako. Tunakutolea maombi yetu si kwa sababu tumetenda haki, bali kwa sababu wewe una huruma nyingi.

19 Ee Mwenyezi-Mungu, utusikie; utusamehe ee Mwenyezi-Mungu. Ee Mwenyezi-Mungu, kwa hisani yako utusikie na kuchukua hatua, wala usikawie, ee Mungu wangu, kwa ajili ya mji huu na watu hawa wanaoitwa kwa jina lako!

20 “Basi, nilipokuwa nikiomba, nikiungama dhambi zangu na dhambi za watu wangu wa Israeli, pamoja na kumsihi Mwenyezi-Mungu kwa ajili ya mlima wake mtakatifu,

21 yule mtu Gabrieli, ambaye nilikuwa nimemwona katika maono hapo awali, alishuka kwa haraka mpaka mahali nilipokuwa. Ilikuwa wakati wa kutoa sadaka ya jioni.

22 Basi, akaniambia, ‘Danieli, nimekuja kukupa hekima na uwezo wa kufahamu.

23 Ulipoanza kuomba, Mungu alitoa jibu, nami nimekuja kukueleza jibu hilo kwa kuwa unapendwa sana. Kwa hiyo, usikilize kwa makini jibu hilo na kuelewa maono hayo.

24 “ ‘Muda wa miaka saba mara sabini umewekwa kwa ajili ya watu wako na juu ya mji wako mtakatifu ili kumaliza makosa, kukomesha dhambi, kusamehe uovu, kuleta haki ya milele, kutia mhuri maono na unabii na kupaka mafuta mahali patakatifu kabisa.

25 Basi, ujue na kufahamu jambo hili: Tangu wakati itakapotolewa amri ya kujengwa upya mji wa Yerusalemu hadi kuja kwake aliyepakwa mafuta, yule aliye mkuu, ni muda wa majuma saba. Kwa muda wa majuma sitini na mawili, mji wa Yerusalemu utajengwa upya, wenye barabara kuu na mahandaki, lakini wakati huo utakuwa wa taabu.

26 Baada ya majuma hayo sitini na mawili, yule aliyepakwa mafuta atakatiliwa mbali hatabaki na kitu. Mji na mahali patakatifu kabisa vitaharibiwa na jeshi la mtawala atakayekuja kushambulia. Mwisho wake utafika kama mafuriko, kukiwa na vita na maangamizi kama yalivyopangwa na Mungu.

27 Mtawala huyo atafanya mapatano imara na watu wengi kwa muda wa miaka saba. Baada ya nusu ya muda huo atakomesha tambiko na sadaka. Mahali pa juu hekaluni patasimamishwa chukizo haribifu, nalo litabaki hapo mpaka yule aliyelisimamisha atakapoangamizwa kama ilivyopangwa na Mungu.’”

10

1 Mnamo mwaka wa tatu wa utawala wa mfalme Koreshi wa Persia, Danieli, aliyeitwa pia Belteshaza, alipewa ufunuo. Ufunuo huo ulikuwa wa kweli, lakini ulikuwa mgumu sana, haukueleweka. Hata hivyo alielewa ufunuo huo maana pia alifahamu maono.

2 “Wakati huo, mimi Danieli, nilikuwa nikiomboleza kwa muda wa majuma matatu.

3 Sikula chakula cha fahari, sikugusa nyama wala divai, na sikujipaka mafuta kwa muda wa majuma hayo yote matatu.

4 “Siku ya ishirini na nne ya mwezi wa kwanza, nilikuwa nimesimama kando ya mto Tigri.

5 Nikainua macho, nikamwona mtu amevaa mavazi ya kitani na kiunoni amejifunga mkanda wa dhahabu kutoka Ufazi.

6 Mwili wake ulingaa kama zabarajadi safi. Uso wake ulifanana na umeme, na macho yake yaliwaka kama miali ya moto. Miguu na mikono yake ilingaa kama shaba iliyosuguliwa sana. Sauti yake ilivuma kama sauti ya umati mkubwa wa watu.

7 “Mimi Danieli peke yangu niliona maono hayo. Wale watu waliokuwa pamoja nami hawakuyaona, lakini walishikwa na hofu sana, wakakimbia, wakajificha.

8 Hivyo, niliachwa peke yangu nikiangalia hayo maono ya kushangaza. Nguvu zikaniishia, na rangi yangu ikaharibika, nikabaki bila nguvu.

9 Nilipoisikia sauti yake, nilianguka chini kifudifudi, nikashikwa na usingizi mzito.

10 Hapo, mkono ukanigusa, ukanisimamisha, na kuimarisha miguu na mikono yangu.

11 Akaniambia, ‘Danieli, wewe unayependwa sana, simama wima usikilize kwa makini maneno nitakayosema, maana nimetumwa kwako.’ Alipokuwa akiniambia maneno haya, mimi nilisimama nikitetemeka.

12 Ndipo yeye akaniambia, ‘Danieli, usiogope. Mungu alilisikia ombi lako tangu siku ile ya kwanza ulipoamua kujinyenyekesha mbele yake ili upate ufahamu. Mimi nimekuja kwa ajili ya ombi lako hilo.

13 Mkuu wa ufalme wa Persia alinipinga kwa muda wa siku ishirini na moja. Lakini Mikaeli, mmoja wa wakuu, akaja kunisaidia, kwa hiyo nikamwacha huko pamoja na mkuu wa ufalme wa Persia,

14 nami nimekuja kukusaidia uyafahamu mambo yatakayowapata watu wako wakati ujao, kwani maono uliyoona yanahusu wakati ujao.’

15 “Alipokuwa ananiambia maneno hayo, niliangalia chini bila kuweza kuongea.

16 Kisha, mmoja mwenye umbo la binadamu, aliigusa midomo yangu, nami nilifungua midomo yangu na kumwambia huyo aliyesimama karibu nami, ‘Ee bwana, maono haya yameniletea maumivu makali hata nimeishiwa nguvu.

17 Mimi ni kama mtumwa mbele ya bwana wake. Nawezaje kuzungumza nawe? Sina nguvu na pumzi imeniishia!’

18 “Yule mmoja aliyeonekana kama mwanaadamu akanigusa kwa mara nyingine, akanitia nguvu.

19 Akaniambia, ‘Usiogope wewe unayependwa sana, uko salama. Uwe imara na hodari.’ Aliposema nami, nilipata nguvu, nikamwambia, ‘Bwana, umekwisha niimarisha; sema kile ulichotaka kusema.’

20 Naye akaniambia, ‘Je, unajua kwa nini nimekujia? Sasa ni lazima nirudi kupigana na malaika mlinzi wa Persia. Halafu, nitakapokuwa nimemshinda, malaika mlinzi wa mfalme wa Ugiriki atatokea.

21 Lakini nitakujulisha yale yaliyoandikwa katika kitabu cha ukweli. Sina mwingine wa kunisaidia kuwashinda hawa isipokuwa Mikaeli, malaika mlinzi wenu.

11

1 “ ‘Lakini kwa upande wangu mimi, katika mwaka wa kwanza wa mfalme Dario Mmedi, nilijitoa kumthibitisha na kumtia nguvu.

2 Sasa nitakueleza ule ukweli wa mambo haya. “ ‘Tazama, wafalme wengine watatu wataitawala nchi ya Persia. Hao watafuatwa na mfalme wa nne ambaye atakuwa tajiri kuliko wale waliomtangulia. Wakati wa kilele cha nguvu na utajiri wake, ataanza kuushambulia ufalme wa Ugiriki.

3 Kisha atatokea mfalme hodari atakayetawala eneo kubwa na kufanya atakavyopenda.

4 Hata hivyo, wakati wa kilele cha uwezo wake, ufalme wake utavunjika na kugawanyika katika sehemu nne kuelekea pepo nne za mbingu. Wazawa wake hawatatawala, wala ufalme hautakuwa mikononi mwa milki aliyotawala, kwa sababu ufalme wake utachukuliwa na wengine.

5 “ ‘Mfalme wa kusini atakuwa mwenye nguvu. Lakini mmoja wa majemadari wake atakuwa na nguvu kuliko yeye na utawala wake utakuwa mkubwa zaidi.

6 Baada ya miaka kadhaa, watafanya mkataba; binti mfalme wa kusini ataolewa katika jamaa ya mfalme na kuratibisha huo mkataba; wa kaskazini, lakini hataendelea kuwa na nguvu, pia mfalme na wazawa wake hawatavumilia; na huyo binti, mwanawe na watumwa wa kike aliokwenda nao, wote watauawa.

7 Baadaye, mmojawapo wa ukoo wa huyo binti atakuwa mfalme. Huyo atayashambulia majeshi ya mfalme wa kaskazini na kuingia katika ngome zao na kushinda.

8 Atazibeba sanamu za kusubu za miungu yao na vyombo vya thamani vya fedha na dhahabu mpaka nchini Misri. Kwa muda wa miaka kadhaa, mfalme wa kusini hatamshambulia mfalme wa kaskazini.

9 Lakini baadaye, mfalme huyu wa kaskazini atauvamia ufalme wa kusini, ila atalazimika kurudi katika nchi yake.

10 “ ‘Wana wa mfalme wa kaskazini watakusanya jeshi kubwa na kujiandaa kwa vita. Jeshi hilo litasonga mbele kama mafuriko litapita na kupigana vita mpaka ngome ya adui.

11 Hapo, mfalme wa kusini, kwa hasira yake, atapigana vita na mfalme wa kaskazini ambaye naye atamkabili kwa jeshi kubwa, lakini litashindwa.

12 Baada ya kulishinda vibaya jeshi la kaskazini na kuua maelfu, ataanza kujisifu, ila hataendelea kuwa mshindi.

13 “ ‘Maana mfalme wa kaskazini baadaye ataandaa jeshi kubwa kuliko lile la awali. Kisha baada ya miaka kadhaa atarudi na jeshi kubwa lenye vifaa vingi.

14 Wakati huo watu wengi watamwasi mfalme wa kusini. Baadhi ya watu wakatili wa taifa lako Danieli, wataasi ili kutekeleza maono haya, lakini hawatafaulu.

15 Ndipo mfalme wa kaskazini atauzingira mji wenye ngome imara na kuuteka. Wanajeshi wa kusini hawatastahimili, hata wale wateule, maana hawatakuwa na nguvu.

16 Mvamizi atawatenda kama apendavyo, hakuna atakeyethubutu kupingana naye. Atasimama katika nchi tukufu, na nchi hiyo yote itakuwa chini ya mamlaka yake.

17 “ ‘Huyo mvamizi atakusudia kuja na jeshi lake lote, naye atafanya mapatano na kuyatekeleza. Atamwoza binti mmoja ili kuuangamiza ufalme wa adui yake; lakini mpango wake hautafaulu, wala kumfaidia lolote.

18 Baadaye, atazigeukia na kuzishambulia nchi nyingi za pwani na kuzishinda. Lakini jemadari mgeni atamshinda na kuyakomesha majivuno yake mwenyewe; naam, atamrudishia mfalme wa kaskazini majivuno yake mwenyewe.

19 Hapo atageuka kurudi katika ngome za nchi yake mwenyewe, lakini atajikwaa na kuanguka vitani na huo ndio utakaokuwa mwisho wake.

20 “ ‘Huyu atafuatwa na mfalme mwingine ambaye atatuma mtozaushuru kupitia katika fahari ya ufalme wake. Mfalme huyo atauawa baada ya siku chache, lakini si kwa hasira wala vitani.

21 “ ‘Mfalme atakayefuata atakuwa baradhuli ambaye hana idhini ya kushika ufalme, naye atakuja bila taarifa na kunyakua ufalme kwa hila.

22 Majeshi pamoja na kuhani wa hekalu, atawafagilia mbali na kuwaua.

23 Kwa kufanya mapatano, atayahadaa mataifa mengine, na ataendelea kupata nguvu ingawa atatawala taifa dogo.

24 Bila taarifa atazivamia sehemu za mkoa zenye utajiri mwingi na kufanya mambo ambayo hayakufanywa hata na mmoja wa wazee wake waliomtangulia. Kisha, atawagawia wafuasi wake mateka, mali na vitu alivyoteka nyara vitani. Atafanya mipango ya kuzishambulia ngome, lakini kwa muda tu.

25 “ ‘Kwa ujasiri mwingi, ataunda jeshi kubwa ili kuushambulia ufalme wa kusini, naye mfalme wa kusini atajibu mashambulizi hayo kwa jeshi kubwa zaidi na lenye nguvu sana. Lakini, mfalme wa kusini hatafaulu kwani mipango ya hila itafanywa dhidi yake.

26 Wale wanaokula pamoja naye, ndio watakaomwangamiza. Watamwangamiza na jeshi lake litafagiliwa mbali na wengi watauawa.

27 Hapo wafalme hao wawili wataketi pamoja mezani kula, lakini kila mmoja anamwazia mwenzake uovu, na kudanganyana. Ila hawatafanikiwa, maana wakati uliopangwa utakuwa bado haujatimia.

28 Mfalme wa kaskazini atarudi nchini mwake akiwa na mali nyingi, lakini nia yake moyoni ni kulitangua agano takatifu. Atafanya apendavyo, kisha atarudi katika nchi yake.

29 “ ‘Katika wakati uliopangwa ataivamia nchi ya kusini kwa mara nyingine, lakini safari hii, mambo yatakuwa tofauti.

30 Meli kutoka Kitimu zitamshambulia, naye atashikwa na hofu. Kisha atarudi nyuma huku amejaa hasira na atalitangua agano takatifu. Hapo atafuata shauri la wale walioasi agano takatifu.

31 Wanajeshi wake watalitia najisi hekalu na ngome zake, watakomesha tambiko za kuteketezwa kila siku na kusimamisha huko hekaluni chukizo haribifu.

32 Atawashawishi kwa hila wale walioasi agano, lakini watu walio waaminifu kwa Mungu wao watasimama imara na kuchukua hatua.

33 Wenye hekima miongoni mwa watu watawafundisha wengi. Hata hivyo, kwa siku kadhaa watauawa kwa upanga au moto, watachukuliwa mateka au kunyanganywa mali zao.

34 Wakati wanapouawa, watapata msaada kidogo, na wengi wanaojiunga nao, watafanya hivyo kwa unafiki.

35 Baadhi ya wenye hekima watauawa, ili wapate kuondolewa uchafu, kutakaswa na kusafishwa, mpaka wakati wa mwisho, ambao sasa bado haujatimia.

36 “ ‘Mfalme atafanya kama apendavyo. Atajitukuza na kujikweza kwamba yeye ni mkuu kuliko miungu yote, na kumkufuru Mungu wa miungu. Ataendelea kufanikiwa mpaka ghadhabu ifikie kikomo chake, kwani yaliyopangwa lazima yatimie.

37 Mfalme huyo hataijali miungu ya wazee wake wala yule anayependwa na wanawake. Ataidharau miungu mingine yote, kwani atajiweka kuwa mkuu kuliko kila mmoja wao.

38 Badala ya miungu hiyo atamheshimu mungu mlinzi wa ngome, ambaye wazee wake kamwe hawakumwabudu, atamtolea dhahabu, fedha na vito vya thamani, na zawadi za thamana kubwa.

39 Atazishughulikia ngome zake kwa msaada wa mungu wa kigeni. Wale wanaomtambua kuwa mfalme, atawatunukia heshima kubwa, atawapa vyeo vikubwa na kuwagawia ardhi kama zawadi.

40 “ ‘Wakati wa mwisho mfalme wa kusini atamshambulia mfalme huyo wa kaskazini. Lakini mfalme wa kaskazini atajibu mashambulio hayo kwa nguvu kama kimbunga, akitumia magari ya farasi, wapandafarasi na meli nyingi. Atazivamia nchi nyingi na kupita katika nchi hizo kama mafuriko ya maji.

41 Ataivamia hata nchi ile tukufu na kuua maelfu ya watu. Lakini nchi za Edomu, Moabu na sehemu kubwa ya Amoni, zitaokoka kutoka mikononi mwake.

42 Wakati atakapozivamia nchi hizo, hata nchi ya Misri haitanusurika.

43 Atamiliki hazina za dhahabu, fedha na vito vyote vya thamani vya nchi ya Misri. Watu wa Libia na watu wa Kushi watafuata nyayo zake.

44 Lakini habari kutoka mashariki na kaskazini zitamtisha. Naye atatoka kwa hasira kubwa ili kukatilia mbali na kuangamiza wengi.

45 Zaidi ya hayo, atapiga mahema yake makubwa kati ya bahari na mlima mtukufu na mtakatifu. Lakini atakuwa amefikia kikomo chake, na hatakuwapo yeyote wa kumsaidia.

12

1 “ ‘Wakati huo, Mikaeli, malaika mkuu, aliye mlinzi wa watu wako, atatokea. Ndipo kutakuwa na wakati wa taabu sana kuliko nyakati nyingine zote tangu mataifa yalipoanza kuwako duniani. Lakini, wakati huo, kila mmoja wa watu wako ambaye jina lake limeandikwa katika kitabu cha uhai, ataokolewa.

2 Wengi wa wale ambao wamekwisha kufa, watafufuka; wengine watapata uhai wa milele, na wengine watapata uhai na kudharauliwa milele.

3 Wale wenye hekima watangaa kama anga angavu, na wale waliowaongoza wengine kutenda mema, watangaa kama nyota milele.

4 Ila sasa, Danieli, weka siri mambo hayo; kifunge kitabu na kukitia mhuri mpaka wakati wa mwisho utakapofika. Wengi watakimbilia huko na huko, na maarifa yataongezeka.’”

5 “Kisha, mimi Danieli nikatazama, nikaona watu wawili wamesimama penye kingo za mto; mmoja upande huu na mwingine upande wa pili.

6 Nikamwuliza yule aliyesimama upande wa juu wa mto, amevaa mavazi ya kitani, mambo haya ya kutisha yatadumu mpaka lini ndipo yaishe?

7 Yule mtu aliyesimama upande wa juu wa mto, amevaa mavazi ya kitani, akainua mikono yake yote miwili kuelekea mbinguni. Kisha nikamsikia akiapa kwa jina la yule aishiye milele: ‘Itakuwa muda wa nyakati tatu na nusu. Wakati mateso ya watu watakatifu yatakapokomeshwa, mambo haya yote yatakuwa yametimia.’

8 Nilisikia lakini sikuelewa. Ndipo, nikamwuliza, ‘Bwana wangu, mwisho wa mambo haya yote utakuwaje?’

9 Akanijibu, ‘Danieli, sasa nenda zako, kwani maneno haya ni siri na yamefungwa kwa kutiwa mhuri mpaka wakati wa mwisho.

10 Watu wengi wataondolewa uchafu, watatakaswa na kusafishwa. Lakini watu waovu wataendelea kutenda uovu. Hakuna hata mmoja wa hao waovu atakayeelewa; wenye hekima ndio watakaoelewa.

11 “ ‘Tangu wakati wa kukomeshwa kwa sadaka za kuteketezwa kila siku, yaani kutoka wakati ule chukizo haribifu litakaposimamishwa itakuwa muda wa siku 1,290.

12 Heri yao watakaostahimili mpaka siku zile 1,335 zitakapotimia.

13 “ ‘Lakini wewe, ee Danieli, jiendee, ukapumzike kaburini, na wakati huo utakapotimia, utafufuka na kupata tuzo lako.’”