1

1 Maono aliyoyaona Isaya, mwana wa Amozi, kuhusu Yuda na mji wa Yerusalemu, nyakati za utawala wa Uzia, Yothamu, Ahazi na Hezekia, wafalme wa Yuda.

2 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Sikilizeni enyi mbingu, tega sikio ee dunia. Mimi nimewalea wanangu wakakua, lakini sasa wameniasi!

3 Ngombe humfahamu mwenyewe, punda hujua kibanda cha bwana wake; lakini Waisraeli hawajui, watu wangu, hawaelewi!”

4 Ole wako wewe taifa lenye dhambi, watu waliolemewa na uovu, wazawa wa wenye kutenda maovu, watu waishio kwa udanganyifu! Nyinyi mmemwacha Mwenyezi-Mungu, mmemdharau Mtakatifu wa Israeli, mmefarakana naye na kurudi nyuma.

5 Kwa nini huachi uasi wako? Mbona wataka kuadhibiwa bado? Kichwa chote ni majeraha matupu, na moyo wote unaugua!

6 Toka wayo hadi kichwa hamna penye nafuu, umejaa majeraha na vidonda vitoavyo damu, navyo havikuoshwa, kufungwa wala kutiwa mafuta.

7 Nchi yenu imeharibiwa kabisa; miji yenu imeteketezwa kwa moto. Wageni wananyakua nchi yenu mkiona kwa macho, imeharibiwa kama uharibifu wa Sodoma.

8 Mji Siyoni umeachwa kama kibanda shambani, kama kitalu katika shamba la matango, kama mji uliozingirwa.

9 Mwenyezi-Mungu wa majeshi asingalituachia wachache, tungalikwisha kuwa kama watu wa Sodoma, tungalikuwa hali ileile ya Gomora.

10 Sikilizeni neno la Mwenyezi-Mungu enyi watawala waovu kama wa Sodoma! Sikilizeni mafunzo ya Mungu wetu enyi watu waovu kama wa Gomora!

11 Mwenyezi-Mungu asema hivi; “Wingi wa tambiko zenu ni kitu gani kwangu? Nimezichoka sadaka zenu za kondoo wa kuteketezwa na mafuta ya wanyama wenu wanono. Sipendezwi na damu ya fahali, wala ya wanakondoo, wala ya beberu.

12 Mnapokuja mbele yangu kuniabudu nani aliyewataka mkanyagekanyage nyua zangu?

13 Msiniletee tena matoleo yenu yasiyo na maana; ubani ni chukizo kwangu. Acheni kufanya sikukuu za mwezi mpya, Sabato na mikutano mikubwa ya ibada; sikubali ibada zilizochanganyika na dhambi.

14 Sikukuu zenu za mwezi mpya na nyinginezo moyo wangu wazichukia. Zimekuwa mzigo mzito kwangu, nami nimechoka kuzivumilia.

15 “Mnapoinua mikono yenu kuomba nitauficha uso wangu nisiwaone. Hata mkiomba kwa wingi sitawasikia, maana mikono yenu imejaa damu.

16 Jiosheni, jitakaseni; ondoeni uovu wa matendo yenu mbele yangu. Acheni kutenda maovu,

17 jifunzeni kutenda mema. Tendeni haki, ondoeni udhalimu, walindeni yatima, teteeni haki za wajane.”

18 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Njoni, basi, tuhojiane. Ingawa mna madoa mekundu ya dhambi, mtatakaswa na kuwa weupe kama theluji; madoa yenu yajapokuwa mekundu kama damu, mtakuwa weupe kama sufu.

19 Mkiwa tayari kunitii, mtakula mazao mema ya nchi.

20 Lakini mkikaidi na kuniasi, mtaangamizwa kwa upanga. Mimi, Mwenyezi-Mungu, nimesema.”

21 Jinsi gani mji uliokuwa mwaminifu sasa umegeuka kuwa kahaba! Wakati mmoja haki ilitawala humo, lakini sasa umejaa wauaji.

22 Fedha yenu imekuwa takataka; divai yenu imechanganyika na maji.

23 Viongozi wako ni waasi; wanashirikiana na wezi. Kila mmoja anapenda hongo, na kukimbilia zawadi. Hawawatetei yatima, haki za wajane si kitu kwao.

24 Kwa hiyo asema Bwana Mwenyezi-Mungu, Mwenye Nguvu wa Israeli: “Nitawamwagia maadui zangu hasira yangu, nitawalipiza kisasi wapinzani wangu.

25 Nitanyosha mkono wangu dhidi yenu; nitayeyusha uchafu wenu kabisa, na kuondoa takataka yenu yote.

26 Nitawapeni waamuzi wenu kama kwanza na washauri wenu kama pale awali. Ndipo Yerusalemu utakapoitwa ‘Mji wa Uadilifu’ utaitwa ‘Mji Mwaminifu’”

27 Mji Siyoni utakombolewa kwa haki, uadilifu utawaokoa watakaotubu humo.

28 Lakini waasi na wenye dhambi wote wataangamizwa pamoja; wanaomwacha Mwenyezi-Mungu watateketezwa.

29 Mtaionea aibu hiyo mialoni mliyoipenda sana; mtafadhaika kwa sababu ya bustani mlizofurahia.

30 Mtakuwa kama mwaloni unaonyauka majani; kama shamba lisilo na maji.

31 Wenye nguvu watakuwa kama majani makavu, matendo yao yatakuwa kama cheche za moto. Watateketea pamoja na matendo yao, wala hapatakuwa na mtu wa kuwaokoa.

2

1 Neno alilopewa Isaya, mwana wa Amozi, kuhusu Yuda na Yerusalemu.

2 Siku zijazo mlima wa nyumba ya Mwenyezi-Mungu utaimarishwa kupita milima yote, utainuliwa juu ya vilima vyote. Mataifa yote yatamiminika huko,

3 watu wengi wataujia na kusema, “Njoni tupande mlima wa Mwenyezi-Mungu, twende nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, apate kutufundisha njia zake, nasi tuishi kadiri ya mwongozo wake. Maana sheria itakuja kutoka Siyoni; neno la Mwenyezi-Mungu kutoka Yerusalemu.”

4 Mungu atasuluhisha mizozo ya mataifa atakata mashauri ya watu wengi. Watu watafua panga za vita kuwa majembe na mikuki yao kuwa miundu ya kupogolea. Taifa halitapigana na taifa lingine wala hayatafanya tena mazoezi ya vita.

5 Sasa, enyi wazawa wa Yakobo, njoni, tutembee katika mwanga wa Mwenyezi-Mungu.

6 Sasa, ee Mungu, umewatupa watu wako, wazawa wa Yakobo. Maana kweli wachawi wa mashariki wamejaa kati yao, wapo na wapiga ramli kama kwa Wafilisti. Wanashirikiana na watu wageni.

7 Nchi yao imejaa fedha na dhahabu, hazina yao ni kubwa kupindukia. Nchi yao imejaa farasi, magari yao ya kukokotwa hayana idadi.

8 Nchi yao imejaa vinyago vya miungu, huabudu kazi ya mikono yao, vitu walivyotengeneza wao wenyewe.

9 Kwa hiyo, kila mtu ataaibishwa na kufedheheshwa. Usiwasamehe hata kidogo, ee Mungu!

10 Ingieni katika mwamba, mkajifiche mavumbini, kuiepa hasira ya Mwenyezi-Mungu, mbali na utukufu wa enzi yake.

11 Siku yaja ambapo kiburi cha watu kitashushwa, majivuno ya kila mtu yatavunjwa; na Mwenyezi-Mungu peke yake atatukuzwa siku hiyo.

12 Naam, yaja siku ya Mwenyezi-Mungu wa majeshi dhidi ya wenye kiburi na majivuno, dhidi ya wote wanaojikweza;

13 dhidi ya mierezi yote ya Lebanoni, ambayo ni mirefu na mizuri, dhidi ya mialoni yote nchini Bashani;

14 dhidi ya milima yote mirefu, dhidi ya vilima vyote vya juu;

15 dhidi ya minara yote mirefu, dhidi ya kuta zote za ngome;

16 dhidi ya meli zote za Tarshishi, na dhidi ya meli zote nzuri.

17 Kiburi chote cha watu kitakomeshwa, majivuno ya kila mtu yatavunjwa. Na Mwenyezi-Mungu peke yake atatukuzwa siku hiyo.

18 Vinyago vyote vya miungu vitatoweka kabisa.

19 Ingieni katika mapango miambani, katika mashimo ardhini, kuiepa hasira ya Mwenyezi-Mungu, mbali na utukufu wa enzi yake, atakapokuja kuitia hofu dunia.

20 Siku hiyo, watu watawatupia panya na popo vinyago vyao vya fedha na dhahabu walivyojitengenezea ili kuviabudu.

21 Nao wataingia katika mapango miambani na kwenye nyufa za miamba, kuiepa hasira ya Mwenyezi-Mungu, mbali na utukufu wa enzi yake, atakapokuja kuitia hofu dunia.

22 Usimwamini binadamu, uhai wake haudumu kama pumzi. Yeye anafaa kitu gani?

3

1 Sasa, Bwana Mwenyezi-Mungu wa majeshi ataondoa kutoka Yerusalemu na Yuda kila tegemeo: Tegemeo lote la chakula, na tegemeo lote la kinywaji.

2 Ataondoa mashujaa na askari, waamuzi na manabii, waaguzi na wazee,

3 majemadari wa vikosi vya watu hamsini, na watu wenye vyeo, washauri, wachawi stadi na walozi hodari.

4 Mungu ataweka watoto wawatawale; naam, watoto wachanga watawatawala.

5 Watu watadhulumiana, kila mtu na jirani yake; vijana watawadharau wazee wao, na watu duni watapuuza wakuu wao.

6 Wakati huo ndugu atamwambia ndugu yake wakiwa bado nyumbani kwa baba yao: “Wewe unalo koti; utakuwa kiongozi wetu. Chukua hatamu juu ya uharibifu huu!”

7 Lakini siku hiyo atasema, “Mimi siwezi kuwa mwuguzi, nyumbani mwangu hamna chakula wala mavazi. Msinifanye mimi kuwa kiongozi wenu.”

8 Watu wa Yerusalemu wamejikwaa, watu wa Yuda wameanguka, kwa kuwa wanampinga Mwenyezi-Mungu kwa maneno na matendo, wakipuuza utukufu wake miongoni mwao.

9 Ubaguzi wao unashuhudia dhidi yao; wanatangaza dhambi yao kama ya Sodoma, wala hawaifichi. Ole wao watu hao, kwani wamejiletea maangamizi wenyewe.

10 Waambieni waadilifu jinsi walivyo na bahati: Kwani watakula matunda ya matendo yao.

11 Lakini ole wao watu waovu! Mambo yatawaendea vibaya, kwani waliyotenda yatawapata wao wenyewe.

12 Watu wangu watadhulumiwa na watoto; wanawake ndio watakaowatawala. Enyi watu wangu, viongozi wenu wanawapotosha, wanavuruga njia mnayopaswa kufuata.

13 Mwenyezi-Mungu yu tayari kuanza mashtaka, anasimama kuwahukumu watu wake.

14 Mwenyezi-Mungu anawashtaki wazee na wakuu wa watu wake: “Nyinyi ndio mlioliharibu shamba la mizabibu; mali walizowanyanganywa maskini zimo nyumbani kwenu.

15 Mnamaanisha nini kuwakandamiza watu wangu, kuwatendea ukatili watu maskini? Nauliza mimi Bwana, Mwenyezi-Mungu wa majeshi.”

16 Mwenyezi-Mungu asema: “Wanawake wa Siyoni wana kiburi; wanatembea wameinua shingo juu, wakipepesa macho yao kwa tamaa. Hatua zao ni za maringo, na miguuni njuga zinalia.

17 Basi, mimi Mwenyezi-Mungu nitawaadhibu; nitawanyoa nywele hao wanawake wa Siyoni, na kuwavua nguo za kufunika uchi wao.”

18 Siku yaja ambapo Mwenyezi-Mungu atawanyanganya wanawake wa Yerusalemu vitu vyote wanavyoringia: Njuga, kaya, mikufu,

19 vipuli, vikuku, shungi,

20 vitambaa vya kichwani, bangili, vibwebwe, vibweta vya marashi, hirizi,

21 pete, hazama,

22 mavazi ya sikukuu, mitandio, majoho, mikoba,

23 mavazi yaoneshayo, mavazi ya kitani, vilemba na shela.

24 Badala ya kunukia marashi watatoa uvundo; badala ya mishipi mizuri watatumia kamba; badala ya nywele nzuri watakuwa na upara; badala ya mavazi mazuri watavaa matambara; uzuri wao wote utageuka kuwa aibu.

25 Wanaume wenu wataangamia kwa upanga, watu wenu wenye nguvu watakufa vitani.

26 Malango ya mji yatalia na kuomboleza; nao mji utakuwa kama mwanamke aliyepokonywa kila kitu, ameketi mavumbini.

4

1 Wakati huo wanawake saba watamvamia mwanamume mmoja na kumwambia, “Chakula na mavazi tutajitafutia wenyewe, lakini wewe utuondolee aibu yetu, uturuhusu tuitwe kwa jina lako.”

2 Siku ile, tawi atakalochipusha Mwenyezi-Mungu litakuwa zuri na tukufu, nayo matunda ya nchi yatakuwa ya fahari na utukufu kwa wale Waisraeli watakaosalia. Waisraeli watakaobaki watayaonea fahari na kujivunia mazao ya nchi yao.

3 Wale watakaosalia hai mjini Yerusalemu, naam, wale watakaobaki huko Siyoni, wataitwa “Wateule wa Mungu;” hao ndio wale wote watakaokuwa wameandikwa kitabuni mwake waishi huko Yerusalemu.

4 Kwa roho yake, Bwana atawaweka sawa na kuwatakasa. Na atakapokwisha kuwatakasa wanawake wa Siyoni uchafu wao na kufuta madoa ya damu yaliyomo humo Yerusalemu,

5 hapo atafanya kila mahali juu ya mlima Siyoni na juu ya mikutano ya watu kuwe na wingu wakati wa mchana, na moshi na moto uwakao vizuri wakati wa usiku. Zaidi ya hayo utukufu wa Mungu utaufunika na kuulinda mji wote.

6 Utukufu wake utakuwa kwao kivuli kuwakinga na joto la mchana; na kimbilio na kinga yao wakati wa dhoruba na mvua.

5

1 Nitaimba juu ya rafiki yangu, wimbo wa rafiki yangu na shamba lake la mizabibu: Rafiki yangu alikuwa na shamba la mizabibu juu ya kilima chenye rutuba nyingi.

2 Alililima vizuri na kuondoa mawe yote, akaotesha humo mizabibu iliyochaguliwa; alijenga mnara wa ulinzi katikati yake, akachimba kisima cha kusindikia divai. Kisha akangojea lizae zabibu, lakini likazaa zabibu chungu.

3 Kwa hiyo rafiki yangu anasema hivi: “Enyi wakazi wa Yerusalemu na watu wa Yuda, amueni tafadhali kati yangu na shamba langu.

4 Ni kitu gani nilichokosa kulifanyia shamba langu? Na nilipotazamia lizae zabibu nzuri, mbona basi, likazaa zabibu chungu?

5 “Na sasa nitawaambieni nitakavyolifanya hilo shamba langu. Nitauondoa ua wake, nalo litaharibiwa. Nitaubomoa ukuta wake, nalo litakanyagwakanyagwa.

6 Nitaliacha liharibiwe kabisa, mizabibu yake haitapogolewa wala kupaliliwa. Litaota mbigili na miiba. Tena nitayaamuru mawingu yasinyeshe mvua juu yake.”

7 Naam! Shamba la mizabibu la Mwenyezi-Mungu wa majeshi ni jumuiya ya Waisraeli, na mizabibu mizuri aliyoipanda ni watu wa Yuda. Yeye alitazamia watende haki, badala yake wakafanya mauaji; alitazamia uadilifu, badala yake wakasababisha kilio!

8 Ole wao wanaonunua nyumba baada ya nyumba, wanaoongeza mashamba juu ya mashamba yao, mpaka kila sehemu inakuwa mali yao, na hamna nafasi kwa wengine nchini.

9 Nimemsikia Mwenyezi-Mungu wa majeshi akitamka hivi: “Hakika nyumba nyingi zitabaki tupu, majumba makubwa mazuri bila wakazi.

10 Shamba la mizabibu la eka kumi litatoa lita nane tu za divai; anayepanda kilo 100 za mbegu atavuna kilo 10 tu za nafaka.”

11 Ole wao wanaoamka asubuhi na mapema wapate kukimbilia kunywa kileo; wanaokesha hata usiku, mpaka divai iwaleweshe!

12 Katika karamu zao, hapakosekani vinubi, zeze, matari, filimbi na divai. Lakini hawajali matendo ya Mwenyezi-Mungu, wala kuzitambua kazi za mikono yake.

13 Kwa hiyo, watu wangu watapelekwa uhamishoni kwa sababu ya utovu wao wa akili. Watu wenu mashuhuri watakufa njaa, watu wengi watakufa kwa kiu.

14 Kuzimu inawangoja kwa hamu kubwa, imepanua kinywa chake mpaka mwisho. Waheshimiwa pamoja na raia wa Yerusalemu wanaingia humo makundi kwa makundi, kadhalika na wote wanaousherehekea.

15 Kila mtu atafedheheshwa, na wenye kiburi wote wataaibishwa.

16 Lakini Mwenyezi-Mungu wa majeshi atatukuzwa. Yeye huonesha ukuu wake kwa matendo yake ya haki, kwa kuwahukumu watu wake.

17 Wanakondoo, wanambuzi na ndama, watapata malisho yao kwenye magofu ya miji yao, kana kwamba hizo ni sehemu za malisho yao.

18 Ole wao wanaoburuta uovu kama kwa kamba; wanaokokota dhambi kama kwa kamba za mkokoteni.

19 Wanasema: “Mwache Mwenyezi-Mungu afanye haraka, tunataka kuyaona aliyosema atayafanya! Mtakatifu wa Israeli na atimize kusudi lake. Hebu na tuone ana mipango gani!”

20 Ole wao wanaosema uovu ni wema na wema ni uovu. Giza wanasema ni mwanga na mwanga wanasema ni giza. Kichungu wanasema ni kitamu na kitamu wanakiona kuwa kichungu.

21 Ole wao wanaojiona kuwa wenye hekima ambao wanajiona kuwa wenye akili.

22 Ole wao mabingwa wa kunywa divai, hodari sana wa kuchanganya vileo.

23 Kwa hongo kidogo wanawaachilia wenye hatia na kuwanyima wasio na hatia haki yao.

24 Kwa hiyo, kama moto uteketezavyo nyasi, kama majani yateketeavyo katika mwali wa moto ndivyo na mizizi yao itakavyooza, na maua yao yatakavyopeperushwa juu kama vumbi. Maana wameiacha sheria ya Mwenyezi-Mungu wa majeshi, wamedharau neno la yule Mtakatifu wa Israeli.

25 Kwa hiyo hasira ya Mwenyezi-Mungu iliwawakia watu wake, akaunyosha mkono wake dhidi yao, akawachapa, hata milima ikatetemeka, maiti zao zikawa kama takataka katika barabara za mji. Hata hivyo, hasira yake haikutulia, mkono wake bado ameunyosha kuwaadhibu.

26 Mwenyezi-Mungu analiashiria taifa la mbali; anawapigia mruzi watu kutoka miisho ya dunia; nao waja mbio na kuwasili haraka!

27 Hawachoki wala hawajikwai; hawasinzii wala hawalali; hakuna mshipi wao uliolegea wala kamba ya kiatu iliyokatika.

28 Mishale yao ni mikali sana, pinde zao zimevutwa tayari. Kwato za farasi wao ni ngumu kama mawe; mwendo wa magurudumu ya magari ni kimbunga.

29 Askari wao wananguruma kama simba; wananguruma kama wanasimba ambao wamekamata mawindo yao na kuwapeleka mahali mbali ambapo hakuna awezaye kuwanyanganya.

30 Siku hiyo, watanguruma juu ya Israeli kama mvumo wa bahari iliyochafuka. Atakayeiangalia nchi kavu ataona giza tupu na dhiki, mwanga utafunikwa na mawingu.

6

1 Mnamo mwaka aliofariki mfalme Uzia, nilimwona Bwana ameketi katika kiti cha enzi kilicho juu na cha fahari. Pindo la vazi lake lilienea hekaluni mote,

2 na juu yake walikuwa wamekaa malaika. Kila mmoja alikuwa na mabawa sita: Mawili ya kufunika uso, mawili ya kufunika mwili na mawili ya kurukia.

3 Waliitana kila mmoja na mwenzake hivi: “Mtakatifu, mtakatifu, mtakatifu, ni Mwenyezi-Mungu wa majeshi! Dunia yote imejaa utukufu wake.”

4 Sauti yao iliitikisa misingi ya milango ya hekalu, nalo likajaa moshi.

5 Basi, mimi nikasema, “Ole wangu! Mimi nimeangamia, maana, midomo yangu ni najisi, na watu ninaoishi nao ni najisi kama mimi. Hata hivyo, kwa macho yangu mwenyewe, nimemwona Mfalme, Mwenyezi-Mungu wa majeshi.”

6 Basi, mmoja wa hao malaika akaruka kunijia, akiwa ameshika mkononi koleo lililokuwa na kaa la moto alilolitwaa madhabahuni.

7 Naye akinigusa nalo mdomoni, akasema: “Tazama, kaa hili limekugusa mdomo; umeondolewa hatia yako, umesamehewa dhambi yako.”

8 Kisha nikamsikia Mwenyezi-Mungu akisema, “Nimtume nani? Ni nani atakayekuwa mjumbe wetu?” Nami nikajibu, “Niko hapa! Nitume mimi.”

9 Naye akaniambia, “Nenda ukawaambie watu hawa: ‘Mtasikiliza sana, lakini hamtaelewa; mtatazama sana, lakini hamtaona.’”

10 Kisha akaniambia, “Zipumbaze akili za watu hawa, masikio yao yasisikie, macho yao yasione; ili wasije wakaona kwa macho yao, wakasikia kwa masikio yao, wakaelewa kwa akili zao, na kunigeukia, nao wakaponywa.”

11 Mimi nikauliza, “Bwana, mpaka lini?” Naye akanijibu, “Mpaka hapo miji itakapobaki tupu bila wakazi, nyumba bila watu, na nchi itakapoharibiwa kabisa.

12 Nami Mwenyezi-Mungu nitawapeleka watu mbali, na kuifanya nchi yote kuwa mahame.

13 Hata wakibaki watu asilimia kumi, nao pia watateketezwa. Hao watakuwa kama mvinje au mwaloni ambao kisiki chake kimebaki baada ya kukatwa.” (Kisiki hicho ni mbegu takatifu ya chanzo kipya.)

7

1 Wakati mfalme Ahazi mwana wa Yothamu na mjukuu wa Uzia, alipokuwa anatawala Yuda, Resini, mfalme wa Aramu, na Peka mwana wa Remalia, mfalme wa Israeli, waliushambulia mji wa Yerusalemu, lakini hawakuweza kuuteka.

2 Mfalme wa Yuda alipopata habari kwamba Waashuru wanashirikiana na Waisraeli, yeye pamoja na watu wote wa Yuda waliogopa na kutetemeka kama miti inayotikiswa na upepo.

3 Mwenyezi-Mungu akamwambia Isaya, “Mchukue mwanao, Shearyashubu, uende kukutana na mfalme Ahazi. Utamkuta barabarani mahali wanapofanyia kazi watengenezaji nguo, mwisho wa mfereji uletao maji kutoka bwawa la juu.

4 Mwambie awe macho, atulie na asiogope wala asife moyo, kwa sababu ya hasira kali ya mfalme Resini wa Ashuru, na ya mwana wa Remalia. Hao wawili ni kama tu moshi wa kuni zinazozimika.

5 Waashuru, kadhalika na Peka pamoja na jeshi la Efraimu wamefanya mpango mbaya dhidi yako. Wamesema,

6 ‘Twende kuivamia nchi ya Yuda, tuwatie watu hofu, tuitwae nchi na kumtawaza mwana wa Tabeeli awe mfalme wao.’

7 “Lakini mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Jambo hilo halitafaulu kamwe.

8 Kwani mji mkuu wa Aramu ni Damasko, na huyo Resini ni mkuu wa Damasko tu. Mji mkuu wa Efraimu ni Samaria, na mwana wa Remalia ni mkuu wa Samaria tu. Mnamo miaka sitini na mitano utawala wa Efraimu utavunjwa; Efraimu halitakuwa taifa tena. Kama hutaamini hutaimarika.”

9

10 Tena Mwenyezi-Mungu akamwambia Ahazi,

11 “Mwombe Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, akupe ishara; iwe ni kutoka chini kuzimu au juu mbinguni.”

12 Ahazi akajibu, “Sitaomba ishara! Sitaki kumjaribu Mwenyezi-Mungu.”

13 Basi, Isaya akamjibu, “Sikiliza basi, enyi watu wa ukoo wa Daudi! Je, haitoshi kuwachosha watu hata sasa mnataka kumchosha Mungu wangu pia?

14 Haya basi, Bwana mwenyewe atawapa ishara: Msichana atachukua mimba, atajifungua mtoto wa kiume na kumwita jina lake Emanueli.

15 Atakula siagi na asali mpaka atakapojua kukataa mabaya na kuchagua mema.

16 Maana, kabla mtoto huyo hajajua kukataa maovu na kuchagua mema, nchi za wafalme hao wawili unaowaogopa zitakuwa mahame.

17 Mwenyezi-Mungu atakuletea wewe pamoja na watu wako na jamii yote ya kifalme siku za taabu kuliko zile zote zilizowahi kutokea tangu wakati watu wa Efraimu walipojitenga na Yuda; yaani, atawaleteeni mfalme wa Ashuru.”

18 Wakati huo, Mwenyezi-Mungu atawapigia mruzi watu wa Misri waje kama nzi toka vijito vya mto Nili; na watu wa Ashuru waje kama nyuki kutoka nchi yao.

19 Watakuja makundi kwa makundi na kuyajaza mabonde yaliyopasukapasuka, mapango miambani, miiba, vichaka vyote na malisho yote.

20 Wakati huo, Bwana atakopa wembe kutoka ngambo ya mto Eufrate, yaani mfalme wa Ashuru. Atawanyoa vichwa vyenu, miili yenu na kukatilia mbali pia ndevu zenu.

21 Wakati huo, mtu atafuga ng'ombe mmoja mchanga na kondoo wawili;

22 nao watatoa maziwa kwa wingi hata aweze kula siagi. Watu watakaosalia katika nchi watakula siagi na asali.

23 Wakati huo, kila mahali palipokuwa na mashamba ya mizabibu kwa maelfu ya thamani ya fedha 1,000 kwa kipimo cha hekalu yatakuwa mbigili na miiba mitupu.

24 Watu watakwenda huko kuwinda kwa pinde na mishale, maana nchi yote itakuwa imejaa mbigili na miiba.

25 Nayo milima yote iliyokuwa ikilimwa itakuwa imejaa mbigili na miiba, hata hakuna mtu atakayejaribu kwenda huko, badala yake itakuwa malisho ya ng'ombe na kondoo.

8

1 Mwenyezi-Mungu aliniambia hivi: “Chukua ubao mkubwa, uandike juu yake maneno yanayosomeka kwa urahisi: ‘TEKA-HARAKA-POKONYA-UPESI.’”

2 Basi, nikajipatia mashahidi wawili waaminifu ambao wangenishuhudia: Kuhani Uria na Zekaria, mwana wa Yeberekia.

3 Nililala na mke wangu ambaye pia ni nabii, akapata mimba, akajifungua mtoto wa kiume. Mwenyezi-Mungu akaniambia, “Mpe mtoto huyo jina ‘Teka-haraka-pokonya-upesi.’

4 Maana kabla mtoto huyu hajafikia umri wa kuweza kutamka: ‘Baba’ au ‘Mama,’ utajiri wa Damasko na nyara walizoteka huko Samaria zitapelekwa kwa mfalme wa Ashuru.”

5 Mwenyezi-Mungu aliongea nami tena, akaniambia,

6 “Kwa kuwa watu hawa wameyakataa maji ya Shiloa yatiririkayo polepole, wakafa moyo mbele ya mfalme Resini na mfalme Peka mwana wa Remalia,

7 basi, mimi Bwana nitawaletea mafuriko makuu ya maji ya mto Eufrate yaani mfalme wa Ashuru na nguvu zake zote; yatafurika na kupita kingo zake.

8 Utaingia nchini Yuda kwa nguvu na kufurika na kupanda mpaka shingoni; utaenea juu ya nchi yako yote, ee Emanueli!”

9 Unganeni enyi watu wa mataifa nanyi mtafedheheshwa! Sikilizeni enyi nchi za mbali duniani! Jiwekeni tayari na kufedheheshwa; naam, kaeni tayari na kufedheheshwa.

10 Shaurianeni pamoja lakini itakuwa bure; fanyeni mipango lakini haitafaulu, maana Mungu yu pamoja nasi.

11 Mwenyezi-Mungu alinionya kwa nguvu nisifuate njia za watu hawa, akaniambia,

12 “Usijumuike nao katika njama zao, wala usiogope yale wanayoyaogopa wala kuwa na hofu.

13 Nitambue mimi peke yangu, Mwenyezi-Mungu wa majeshi, kuwa mtakatifu; utaniogopa na kunicha mimi peke yangu.

14 Mimi nitakuwa kimbilio, nitakuwa pia kama jiwe la kujikwaa, mwamba wa kuziangusha falme za Israeli na Yuda; nitakuwa mtego wa kuwatega na kuwanasa wakazi wa Yerusalemu.

15 Watu wengi watajikwaa, wataanguka na kupondeka; watanaswa katika mtego huo na kuchukuliwa mateka.”

16 Nitalihifadhi agizo hilo na kulifunga fundisho hilo miongoni mwa wafuasi wangu.

17 Nitamngojea Mwenyezi-Mungu ambaye amejificha mbali na wazawa wa Yakobo; nitamtumainia.

18 Mimi pamoja na watoto alionipa Mwenyezi-Mungu ni ishara na alama katika Israeli kwa jina la Mwenyezi-Mungu wa majeshi akaaye mlimani Siyoni.

19 Baadhi watawaambieni: “Nendeni mkatake shauri kwa mizimu na mizuka iliayo kama ndege; kwani ni kawaida watu kutaka shauri kwa miungu yao, na kutaka shauri kwa wafu kwa ajili ya walio hai.”

20 Hakika anayesema hivyo hajapata kuona mwanga. Lakini nyinyi shikilieni lile agizo na fundisho la Mungu.

21 Watu watatangatanga nchini wamefadhaika sana na wenye njaa. Na wakiwa na njaa, hasira zitawawaka na kumlaani mfalme wao kadhalika na Mungu wao. Watatazama juu mbinguni

22 na kuiangalia dunia, lakini wataona tu taabu, giza na mauzauza ya shida. Hakuna atakayeliepa giza hilo kuu.

9

1 Lakini nchi ile iliyokuwa imekumbwa na huzuni haitabaki daima katika giza hilo kuu. Hapo awali Mungu alizifedhehesha nchi za Zebuluni na Naftali, lakini siku za usoni ataifanikisha sehemu hii ya baharini na nchi iliyo ngambo ya Yordani na hata Galilaya wanamoishi watu wa mataifa.

2 Watu waliotembea gizani wameona mwanga mkubwa. Watu walioishi katika nchi ya giza kuu, sasa mwanga umewaangazia.

3 Wewe, ee Mungu, umelikuza taifa, umeiongeza furaha yake. Watu wanafurahi mbele yako, wana furaha kama wakati wa mavuno, kama wafurahivyo wanaogawana nyara.

4 Maana nira nzito walizobeba, nira walizokuwa wamefungwa, na fimbo ya wanyapara wao, umezivunjavunja kama wakati wa Wamidiani.

5 Viatu vyote vya washambulizi vitani na mavazi yote yenye madoa ya damu yatateketezwa kama kuni za kuwasha moto.

6 Maana mtoto amezaliwa kwa ajili yetu, tumepewa mtoto wa kiume. Naye atapewa mamlaka ya kutawala. Ataitwa: “Mshauri wa Ajabu”. “Mungu Mwenye Nguvu”, “Baba wa Milele”, “Mfalme wa Amani”.

7 Utawala wake utastawi daima, amani ya ufalme wake haitakoma. Atachukua wadhifa wa mfalme Daudi na kutawala juu ya ufalme wake; ataustawisha na kuuimarisha, kwa haki na uadilifu, tangu sasa na hata milele. Hayo atayafanya Mwenyezi-Mungu wa majeshi.

8 Mwenyezi-Mungu ametoa tamko dhidi ya Yakobo nalo litampata Israeli.

9 Watu wote watatambua, ukoo wote wa Efraimu na wakazi wa Samaria. Kwa kiburi na majivuno wanasema:

10 “Kuta za matofali zimeanguka lakini sisi tutazijenga kwa mawe yaliyochongwa! Nyumba za boriti za mikuyu zimeharibiwa lakini mahali pake tutajenga za mierezi.”

11 Basi, Mwenyezi-Mungu atawaletea wapinzani na kuwachochea maadui zao.

12 Waaramu upande wa mashariki, Wafilisti upande wa magharibi, wamepanua vinywa vyao kuimeza Israeli. Hata hivyo, hasira yake haijatulia, bado ameunyosha mkono wake.

13 Ingawa aliwaadhibu watu, hawakumrudia Mwenyezi-Mungu wa majeshi.

14 Basi kwa muda wa siku moja tu, Mwenyezi-Mungu atakata katika Israeli vichwa na mikia, tawi la mtende na nyasi:

15 Vichwa ndio wazee na waheshimiwa, mikia ndio manabii wafundishao uongo.

16 Wale wanaoongoza watu hawa wamewapotosha, na hao wanaoongozwa nao wamepotoka.

17 Kwa hiyo, Mwenyezi-Mungu hawahurumii vijana wao, hana huruma juu ya yatima na wajane wao; kwani hakuna hata mmoja amchaye Mungu, kila mtu husema uongo. Hata hivyo, hasira yake haijatulia, bado ameunyosha mkono wake.

18 Uovu huwaka kama moto uteketezao mbigili na miiba; huwaka kama moto msituni, na kutoa moshi mzito upandao angani juu.

19 Kwa ghadhabu ya Mwenyezi-Mungu wa majeshi nchi imechomwa moto, na watu ni kama kuni za kuuwasha. Hakuna mtu anayemhurumia ndugu yake;

20 wananyanganya upande mmoja na hawatosheki; wanakula upande mwingine lakini hawashibi. Kila mmoja anamshambulia mwenzake.

21 Manase dhidi ya Efraimu, Efraimu dhidi ya Manase na wote wawili dhidi ya Yuda. Hata hivyo, hasira ya Mwenyezi-Mungu haijatulia, bado ameunyosha mkono wake.

10

1 Ole wao wanaotunga sheria zisizo za haki, watu wanaopitisha sheria za kukandamiza.

2 Huwanyima maskini haki zao, na kuwaibia maskini wa watu wangu maslahi yao. Wajane wamekuwa nyara kwao; yatima wamekuwa mawindo yao.

3 Je, mtafanya nini siku ya adhabu, siku dhoruba itakapowajieni kutoka mbali? Mtamkimbilia nani kuomba msaada? Mtakwenda wapi kuweka mali yenu?

4 Litakalowabakia ni kujikunyata kati ya wafungwa na kuangamia pamoja na wanaouawa vitani. Hata hivyo, hasira ya Mwenyezi-Mungu haijatulia, bado ameunyosha mkono wake.

5 Ole wake Ashuru, fimbo ya hasira yangu, yeye ashikaye kiboko cha hasira yangu!

6 Nilimtuma kuliadhibu taifa ovu, nilimwamuru kuwaadhibu watu niliowakasirikia, kuwapora na kuteka nyara, na kuwakanyaga chini kama tope njiani.

7 Lakini Ashuru hakudhamiria hivyo, yeye alikuwa na nia nyingine; alikusudia kuharibu kabisa, kuangamiza mataifa mengi iwezekanavyo.

8 Maana alisema: “Je, si kweli majemadari wangu ni wafalme?

9 Je, si kweli kwamba Kalno nitautenda kama Karkemishi, mji wa Hamathi kama mji wa Arpadi, Samaria kama Damasko?

10 Kama nimefaulu kuunyosha mkono wangu dhidi ya falme zenye sanamu za miungu kubwa kuliko sanamu za Yerusalemu na Samaria;

11 je, nitashindwa kuutenda Yerusalemu na sanamu zake, kama nilivyoutenda Samaria na sanamu zake?”

12 Wakati Mwenyezi-Mungu atakapomaliza kazi zake zote mlimani Siyoni na mjini Yerusalemu, atamwadhibu mfalme wa Ashuru, kwa sababu ya majivuno na kiburi chake.

13 Maana mfalme wa Ashuru alisema: “Kwa nguvu zangu mwenyewe nimetenda hayo, na kwa hekima yangu, maana mimi ni mwerevu! Nimeondoa mipaka kati ya mataifa, nikazipora hazina zao; kama fahali nimewaporomosha walioketia viti vya enzi.

14 Kama mtu anyoshaye mkono kwenye kiota, ndivyo nilivyochukua mali yao; kama mtu aokotavyo mayai yaliyoachwa kiotani, ndivyo nilivyowaokota duniani kote, wala hakuna mtu aliyeweza kupiga bawa, au aliyefungua kinywa kunipigia kelele.” Lakini Mwenyezi-Mungu asema hivi:

15 “Je, shoka litajigamba dhidi ya anayelitumia? Msumeno waweza kujivuna dhidi ya mwenye kukata nao? Ni kana kwamba fimbo ingeweza kumwinua anayeishika, au mkongojo kumwinua mwenye kuutumia!”

16 Kwa hiyo, Bwana Mwenyezi-Mungu wa majeshi, atawaletea askari wao ugonjwa wa kuwakondesha, na fahari yao itateketezwa kama kwa moto.

17 Mungu aliye mwanga wa Israeli atakuwa kama moto, Mtakatifu wa Israeli atakuwa mwali wa moto ambao kwa siku moja utateketeza kila kitu: Miiba yake na mbigili zake pamoja.

18 Misitu yake ya fahari na mashamba yake mazuri, Mwenyezi-Mungu atayaangamiza yote; itakuwa kama mtu aliyemalizwa na ugonjwa.

19 Miti itakayobaki msituni mwake itakuwa michache sana hata mtoto mdogo ataweza kuihesabu.

20 Siku ile wazawa wa Yakobo watakaobaki, naam, Waisraeli watakaosalia hawatalitegemea tena taifa lililowaadhibu, bali watamtegemea kabisa Mwenyezi-Mungu, Mtakatifu wa Israeli.

21 Wazawa wa Yakobo wachache watakaobaki watamrudia Mungu Mkuu.

22 Maana, hata kama sasa Waisraeli ni wengi kama mchanga wa pwani, ni wachache tu watakaorudi. Maangamizi yamepangwa yafanyike, nayo yatafanyika kwa haki tupu.

23 Naam! Bwana, Mwenyezi-Mungu wa majeshi, atakamilisha kabisa katika nchi yote jambo aliloamua kutenda.

24 Kwa hiyo, Bwana Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi: “Enyi watu wangu mnaokaa Siyoni msiwaogope Waashuru ambao wanawapiga kwa fimbo, wakiinua mikongojo yao dhidi yenu kama walivyofanya Wamisri.

25 Maana bado kitambo, nayo hasira yangu itapita na ghadhabu yangu itawageukia Waashuru.

26 Mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi na nitawachapa kama nilivyowachapa Wamidiani kwenye jabali la Orebu. Nitanyosha fimbo yangu juu ya bahari kuwachapa kama nilivyowafanya Wamisri.

27 Wakati huo, mzigo waliowabebesha nitauondoa na nira waliyowatia shingoni mwenu itavunjwa.” Adui amepanda kutoka Rimoni,

28 amefika mjini Ayathi. Amepitia huko Migroni, mizigo yake ameiacha Mikmashi.

29 Amekwisha pita kivukoni, usiku huu analala Geba. Watu wa Rama wanatetemeka kwa hofu, wakazi wa Gibea, mji wa Shauli, wamekimbia.

30 Pazeni sauti enyi watu wa Galimu! Tegeni sikio enyi watu wa Laisha! Jibuni enyi wenyeji wa Anathothi!

31 Watu wa Madmena wako mbioni, wakazi wa Gebimu wanakimbilia usalama.

32 Leo hii, adui atatua Nobu, atatikisa ngumi yake dhidi ya mlima Siyoni; naam, atautikisia ngumi mji wa Yerusalemu.

33 Bwana Mwenyezi-Mungu wa majeshi atakata matawi yake kwa ukatili; miti mirefu itaangushwa chini, walio juu wataaibishwa.

34 Atakata vichaka vya msituni kwa shoka, Lebanoni na mierezi yake maarufu itaanguka.

11

1 Kutatokea chipukizi katika kisiki cha Yese, tawi litachipua mizizini mwake.

2 Roho ya Mwenyezi-Mungu itakaa kwake, roho ya hekima na maarifa, roho ya shauri jema na nguvu, roho ya ujuzi na ya kumcha Mwenyezi-Mungu.

3 Atafurahia kumcha Mwenyezi-Mungu. Hatahukumu kadiri ya mambo ya njenje, wala kuamua kufuatana na yale anayosikia.

4 Atawapatia haki watu maskini, atawaamulia sawasawa wanyonge nchini. Kwa neno lake ataiadhibu dunia, kwa tamko lake atawaua waovu.

5 Haki itakuwa kama mkanda wa kujifunga, uaminifu utakaa naye kama mkanda kiunoni.

6 Mbwamwitu ataishi pamoja na mwanakondoo, chui watapumzika pamoja na mwanambuzi. Ndama na wanasimba watakula pamoja, na mtoto mdogo atawaongoza.

7 Ngombe na dubu watakula pamoja, ndama wao watapumzika pamoja; na simba atakula majani kama ng'ombe.

8 Mtoto mchanga atacheza kwenye shimo la nyoka mtoto ataweza kutia mkono shimoni mwa nyoka wa sumu.

9 Katika mlima mtakatifu wa Mungu hakutakuwa na madhara wala uharibifu. Maana kumjua Mwenyezi-Mungu kutaenea pote nchini, kama vile maji yajaavyo baharini.

10 Siku ile chipukizi wa Yese atakuwa ishara kwa mataifa; mataifa yatamtafuta na makazi yake yatatukuka.

11 Siku hiyo, Bwana ataunyosha mkono wake tena kuwarejesha watu wake waliosalia huko Ashuru, Misri, Pathrosi, Kushi, Elamu, Shinari, Hamathi na sehemu za pwani.

12 Naye atatweka bendera kuwaashiria mataifa, kuwakusanya Waisraeli waliodharauliwa, kuwaleta pamoja watu wa Yuda waliotawanywa, na kuwarudisha toka pembe nne za dunia.

13 Wivu wa Efraimu juu ya Yuda utakoma, hakutakuwa tena na uadui kati ya Yuda na Efraimu.

14 Wote pamoja watawavamia Wafilisti walio magharibi, pamoja watawapora watu wakaao mashariki. Watawashinda Waedomu na Wamoabu, nao Waamoni watawatii.

15 Mwenyezi-Mungu atakausha ghuba ya bahari ya Shamu, kwa pumzi yake ichomayo atakausha mto Eufrate, nao utagawanyika katika vijito saba, watu wavuke humo miguu mikavu.

16 Tena, kutakuwa na barabara kuu toka Ashuru kwa ajili ya watu wake waliobaki humo kama ilivyokuwa kwa Waisraeli wakati walipotoka nchini Misri.

12

1 Siku hiyo mtasema: “Nakushukuru, ee Mwenyezi-Mungu, maana ingawa ulinikasirikia, hasira yako imetulia, nawe umenifariji.

2 Mungu ndiye mwenye kuniokoa, nitamtegemea yeye, wala sitaogopa; Mwenyezi-Mungu hunijalia nguvu; yeye mwenyewe ndiye aniokoaye.”

3 Mtachota maji kwa furaha kutoka visima vya wokovu.

4 Siku hiyo mtasema: “Mshukuruni Mwenyezi-Mungu mwombeni kwa jina lake. Yajulisheni mataifa matendo yake, tangazeni kuwa jina lake limetukuka.

5 Mwimbieni Mwenyezi-Mungu sifa kwa kuwa ametenda mambo makuu; haya na yajulikane duniani kote.

6 Pazeni sauti na kuimba kwa furaha, enyi wakazi wa Siyoni, maana aliye mkuu miongoni mwenu ndiye Mungu, Mtakatifu wa Israeli.”

13

1 Kauli ya Mungu dhidi ya Babuloni ambayo Isaya, mwana wa Amozi, alipewa katika maono:

2 Mungu asema: “Twekeni bendera juu ya mlima usio na miti. Wapaazieni sauti askari wapungieni watu mkono waingie malango ya mji wa wakuu.

3 Mimi nimewaamuru wateule wangu, nimewaita mashujaa wangu, hao wenye kunitukuza wakishangilia, waje kutekeleza lengo la hasira yangu.”

4 Sikilizeni kelele milimani kama za kundi kubwa la watu! Sikilizeni kelele za falme, na mataifa yanayokusanyika! Mwenyezi-Mungu wa majeshi analikagua jeshi linalokwenda vitani.

5 Wanakuja kutoka nchi za mbali, wanatoka hata miisho ya dunia: Mwenyezi-Mungu na silaha za hasira yake anakuja kuiangamiza dunia.

6 Lieni maana siku ya Mwenyezi-Mungu imekaribia; inakuja kama maafa kutoka kwa Mungu Mwenye Nguvu.

7 Kwa hiyo mikono ya kila mtu italegea, kila mtu atakufa moyo.

8 Watu watafadhaika, watashikwa na hofu na maumivu, watakuwa na uchungu kama mama anayejifungua. Watatazamana kwa mashaka, nyuso zao zitawaiva kwa haya.

9 Siku ya Mwenyezi-Mungu inakuja, siku kali, ya ghadhabu na hasira kali. Itaifanya nchi kuwa uharibifu, itawaangamiza wenye dhambi wake.

10 Nyota na vilimia vyake angani hazitaangaza; jua linapochomoza litakuwa giza, na mwezi hautatoa mwanga wake.

11 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Nitauadhibu ulimwengu kwa uovu wake, waovu kwa sababu ya makosa yao. Nitakikomesha kiburi cha wenye majivuno, na kuporomosha ubaradhuli wa watu katili.

12 Nitawafanya watu kuwa wachache kuliko dhahabu safi; binadamu watakuwa wachache kuliko dhahabu ya Ofiri.

13 Nitazitetemesha mbingu nayo nchi itatikisika katika misingi yake kwa sababu ya ghadhabu yangu Mwenyezi-Mungu siku ile ya hasira yangu kali.

14 “Kama swala anayewindwa, kama kondoo wasio na mchungaji, kila mmoja atajiunga na watu wake kila mtu atakimbilia nchini mwake.

15 Yeyote atakayeonekana atatumbuliwa, atakayekamatwa atauawa kwa upanga.

16 Watoto wao wachanga watapondwapondwa mbele yao, watanyanganywa nyumba zao, na wake zao watanajisiwa.

17 “Ninawachochea Wamedi dhidi yao; watu ambao hawajali fedha wala hawavutiwi na dhahabu.

18 Mishale yao itawaua vijana, hawatakuwa na huruma kwa watoto, wala kuwahurumia watoto wachanga.

19 Babuloni johari ya falme zote na umaarufu wa kiburi cha Wakaldayo utakuwa kama Sodoma na Gomora, wakati Mungu alipoiangamiza.

20 Kamwe hautakaliwa tena na watu, watu hawataishi humo katika vizazi vyote. Hakuna Mwarabu atakayepiga hema lake humo, wala mchungaji atakayechunga wanyama wake humo.

21 Badala yake watakuwamo wanyama wakali wa porini, bundi watajaa katika nyumba zake. Mbuni wataishi humo, na majini yatachezea humo.

22 Mbwamwitu watalia ndani ya ngome zake, mbweha wataonekana ndani ya nyumba zao za anasa. Wakati wa Babuloni umekaribia, wala siku zake hazitaongezwa.”

14

1 Mwenyezi-Mungu atawahurumia tena watu wa Yakobo, atawateua tena Waisraeli. Atawarudisha katika nchi yao wenyewe, na wageni watakuja na kukaa pamoja na watu wa Yakobo.

2 Watu wa mataifa watawasaidia Waisraeli kurudi katika nchi waliyopewa na Mwenyezi-Mungu. Na hapo watawatumikia Waisraeli kama watumwa. Wale waliowateka sasa watatekwa na Waisraeli, na watawatawala wale waliowadhulumu.

3 Ewe Israeli, wakati Mwenyezi-Mungu atakapokufariji baada ya mateso, misukosuko na utumwa uliofanyiwa,

4 utaimba utenzi huu wa kumdhihaki mfalme wa Babuloni: “Jinsi gani mdhalimu alivyokomeshwa! Ujeuri wake umekomeshwa!

5 Mwenyezi-Mungu amelivunja gongo la waovu, ameivunja fimbo ya kifalme ya watawala,

6 ambao walipiga nayo watu kwa hasira bila kukoma, na kuwatawala kwa udhalimu bila huruma.

7 Sasa dunia yote ina utulivu na amani, kila mtu anaimba kwa furaha.

8 Misonobari inafurahia kuanguka kwako, nayo mierezi ya Lebanoni pamoja yasema: ‘Kwa vile sasa umeangushwa, hakuna mkata miti atakayekuja dhidi yetu!’

9 “Kuzimu nako kumechangamka, ili kukulaki wakati utakapokuja. Kunaiamsha mizimu ije kukusalimu na wote waliokuwa wakuu wa dunia; huwaamsha kutoka viti vyao vya enzi wote waliokuwa wafalme wa mataifa.

10 Wote kwa pamoja watakuambia: ‘Nawe pia umedhoofika kama sisi! Umekuwa kama sisi wenyewe!

11 Fahari yako imeteremshwa kuzimu pamoja na muziki wa vinubi vyako. Chini mabuu ndio kitanda chako, na wadudu ndio blanketi lako!’

12 “Jinsi gani ulivyoporomoshwa toka mbinguni, wewe uliyekuwa nyota angavu ya alfajiri. Jinsi gani ulivyoangushwa chini, wewe uliyeyashinda mataifa!

13 Wewe ulijisemea moyoni mwako: ‘Nitapanda mpaka mbinguni; nitaweka kiti changu juu ya nyota za Mungu, nitaketi juu ya mlima wakutanapo miungu, huko mbali pande za kaskazini.

14 Nitapanda vilele vya mawingu nitajifanya kuwa sawa na Mungu Mkuu.’

15 Lakini umeporomoshwa hadi kuzimu; umeshushwa chini kabisa shimoni.

16 “Watakaokuona watakukodolea macho, watakushangaa wakisema: ‘Je, huyu ndiye aliyetetemesha dunia na kuzitikisa falme,

17 aliyegeuza dunia kuwa kama jangwa, akaangamiza miji yake, na kuwanyima wafungwa wake kurudi kwao?’

18 Wafalme wote wa mataifa wamezikwa kwa heshima kila mmoja ndani ya kaburi lake.

19 Lakini wewe umetupwa nje ya kaburi lako; kama mtoto wa kuchukiza aliyezaliwa mfu maiti yako imekanyagwakanyagwa, umerundikiwa maiti za waliouawa kwa upanga, waliotupwa mashimoni penye mawe.

20 Lakini wewe hutaunganishwa nao katika mazishi, maana uliiharibu nchi yako, wewe uliwaua watu wako. Wazawa wa waovu na wasahaulike kabisa!

21 Kaeni tayari kuwachinja watoto wake kwa sababu ya makosa ya baba zao, wasije wakaamka na kuimiliki nchi, na kuijaza dunia yote miji yao.”

22 Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi: “Nitaushambulia mji wa Babuloni na kuuangamiza kabisa. Nitaharibu kila kitu, mji wote, watoto na yeyote aliyebaki hai. Mimi Mwenyezi-Mungu nimenena.

23 Nitaufanya kuwa makao ya nungunungu, na utakuwa madimbwi ya maji. Nami nitaufagilia mbali kwa ufagio wa maangamizi. Mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi nimenena.”

24 Mwenyezi-Mungu wa majeshi ameapa: “Kama nilivyopanga, ndivyo itakavyokuwa; kama nilivyokusudia, ndivyo itakavyokamilika.

25 Nitauvunja uwezo wa Waashuru nchini mwangu; nitawakanyagakanyaga katika milima yangu. Nitawaondolea watu wangu nira ya dhuluma yao, na mzigo wa mateso yao.”

26 Huu ndio uamuzi wake Mwenyezi-Mungu kuhusu dunia yote; hii ndiyo adhabu atakayotoa juu ya mataifa yote.

27 Kama Mwenyezi-Mungu wa majeshi ameamua, nani atakayeweza kubatilisha uamuzi wake? Kama amepania kutoa adhabu, ni nani atakayempinga?

28 Mwaka alipofariki mfalme Ahazi, Mungu alitoa kauli hii:

29 “Msishangilie enyi Wafilisti wote, kwamba Ashuru, fimbo iliyowapiga, imevunjika; maana, nyoka wa kawaida atazaa nyoka mwenye sumu, na nyoka mwenye sumu atazaa joka lirukalo.

30 Wazaliwa wa kwanza wa maskini watashiba, na fukara watakaa kwa usalama. Lakini chipukizi wenu nitawaua kwa njaa; na yeyote wenu atakayebaki nitamuua.

31 Piga yowe ewe lango; lia ewe mji; yeyuka kwa hofu ewe nchi yote ya Filistia. Maana moshi wa askari waja kutoka kaskazini, wala hakuna atakayechelewa katika majeshi yake.”

32 Basi watapewa jibu gani wajumbe wa taifa hilo? Wataambiwa: Mwenyezi-Mungu ameijenga imara Siyoni, na maskini wa watu wake watakimbilia usalama huko.

15

1 Kauli ya Mungu dhidi ya nchi ya Moabu. Mji wa Ari nchini Moabu umeangamizwa usiku; mji wa Kiri nchini Moabu umeteketezwa usiku.

2 Watu wa Diboni wamepanda hekaluni, hadi mahali pa juu kuomboleza, watu wa Moabu wanalia kwa ajili ya Nebo na Medeba; vichwa vyote vimenyolewa upara, ndevu zao zote zimekatwa kabisa.

3 Wanapita njiani wamevaa mavazi ya gunia. Kwenye paa za nyumba na viwanja vya mji watu wanalia na kukauka kwa machozi.

4 Watu wa Heshboni na Eleale wanalia, sauti zao zinasikika hadi Yahazi. Hata askari wa Moabu wanalia kwa sauti; mioyo yao inatetemeka.

5 Moyo wangu unasononeka juu ya nchi ya Moabu; wakimbizi wake wanakimbilia Soari, wanakimbia mpaka Eglath-shelishiya. Wanapanda njia ya kwenda Luhithi wakilia, njiani kwenda Horonaimu wanatoa kilio cha maangamizi.

6 Kijito cha Nimrimu kimekauka; nyasi zimekauka, majani mabichi yamenyauka, hakuna chochote kinachoota hapo.

7 Watu wanavuka kijito cha Mierebi wamebeba mali yao yote waliyochuma, na kila walichojiwekea kama akiba.

8 Kilio kimezuka pote nchini Moabu, maombolezo yao yamefika Eglaimu, naam, yamefika mpaka Beer-elimu.

9 Maji ya Diboni yamejaa damu, lakini Mungu ataongeza msiba wa Diboni. Hao wachache watakaobaki hai na kukimbia kutoka nchini Moabu, watapelekewa simba wa kuwaua.

16

1 Pelekeni wanakondoo kwa mtawala wa nchi, pelekeni kutoka Sela jangwani mpaka mlimani Siyoni.

2 Kama ndege wanavyohangaika na kurukaruka, wakiwa wamefukuzwa kutoka viota vyao, ndivyo walivyo mabinti wa Moabu kwenye vivuko vya Arnoni.

3 Wamoabu wanawaambia watu wa Yuda, “Tupeni mwongozo, tuamulieni. Enezeni ulinzi wenu juu yetu, kama vile usiku uenezavyo kivuli chake. Tuficheni sisi wakimbizi; msitusaliti sisi tuliofukuzwa.

4 Wakimbizi wa Moabu waishi kwenu, muwe kimbilio lao mbali na mwangamizi.” Mdhalimu atakapokuwa ametoweka, udhalimu utakapokuwa umekoma, na wavamizi kutoweka nchini,

5 utawala adili utazinduliwa katika maskani ya Daudi, mtawala apendaye kutenda haki, na mwepesi wa kufanya yaliyo sawa; atatawala humo kwa uaminifu.

6 Watu wa Yuda wanasema hivi: “Tumesikia juu ya kiburi cha Moabu, tunajua jinsi alivyojivuna mno; tumesikia juu ya majivuno, kiburi na ufidhuli wake; lakini majivuno yake hayo ni bure.”

7 Sasa Wamoabu wanalia; wote wanaomboleza juu ya nchi yao. Ombolezeni kwa pigo hilo kubwa, na juu ya maandazi ya zabibu za Kir-haresethi.

8 Mashamba ya Heshboni yamefifia. Kadhalika na zabibu za Sibma ambazo ziliwalevya wakuu wa mataifa zikafika Yazeri na kusambaa hata jangwani, chipukizi zake zikafika hata ngambo ya bahari.

9 Kwa hiyo ninalia pamoja na Yazeri kwa ajili ya mizabibu ya Sibma. Machozi yananitoka kwa ajili yenu, enyi miji ya Heshboni na Eleale; maana vigelegele vya mavuno ya matunda, vigelegele vya mavuno ya nafaka vimetoweka.

10 Furaha na shangwe zimetoweka katika shamba la rutuba. Kwenye mizabibu hakuna kuimba tena, wala kupiga vigelegele. Hakuna tena kukamua zabibu shinikizoni, sauti za furaha za mavuno zimekomeshwa.

11 Hivyo, nafsi yangu yalilia Moabu kama kinubi, na moyo wangu kwa ajili ya mji wa Kir-heresi.

12 Watu wa Moabu wanapojitokeza kuabudu mungu wao, wanapojichosha huko juu mahali pa ibada, wanapokwenda mahali pao patakatifu kusali, hawatakubaliwa.

13 Hili ndilo jambo alilosema Mwenyezi-Mungu wakati uliopita kuhusu Moabu.

14 Lakini sasa Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Baada ya miaka mitatu kamili, ikihesabiwa kama mfanyakazi anavyohesabu siku zake, fahari ya Moabu itakwisha. Ingawa watu wake ni wengi, watakaobaki hai watakuwa wachache na wanyonge.”

17

1 Kauli ya Mungu dhidi ya Damasko. “Damasko utakoma kuwa mji; utakuwa rundo la magofu.

2 Mitaa yake imeachwa mahame milele. Itakuwa makao ya makundi ya wanyama, wala hakuna mtu atakayewatisha.

3 Ngome za kujihami za Efraimu zitatoweka, na utawala wa Damasko utakwisha. Waashuru ambao watabaki hai, watakuwa na fedheha kama wazawa wa Israeli. Mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi nimenena.

4 “Siku hiyo, fahari ya Yakobo itaporomoshwa, na unono wake ataupoteza.

5 Atakwisha kama shamba lililovunwa, atafanyiwa kama mvunaji avunavyo nafaka, atakuwa kama shamba lililovunwa bondeni Refaimu.

6 Atabakiziwa wachache kama vile baada ya zeituni: Zeituni mbili, tatu katika tawi la juu; nne, tano katika matawi ya mti uzaao sana. Mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, nimenena.”

7 Siku hiyo, watu watamwangalia Muumba wao, na kuelekeza macho yao kwa huyo Mtakatifu wa Israeli.

8 Hawatazielekea tena madhabahu ambazo ni kazi za mikono yao wenyewe, wala kuzitazamia tena kazi za mikono yao wenyewe, yaani sanamu za mungu Ashera na madhabahu za kufukizia ubani.

9 Siku hiyo miji yao imara itaachwa mahame, kama miji ambayo Wahivi na Waamori waliihama walipokuwa wakiwakimbia wazawa wa Israeli. Kila kitu kitakuwa uharibifu.

10 Maana wewe Israeli umemsahau Mungu aliyekuokoa, hukumkumbuka Mwamba wa usalama wako. Kwa hiyo, hata mkipanda mimea ya Baali, na kuiweka wakfu kwa mungu wa kigeni;

11 hata mkiifanya ikue siku hiyohiyo mliyoipanda na kuifanya ichanue asubuhi hiyohiyo, mavuno yenu yatatoweka siku hiyo ya balaa na maumivu yasiyoponyeka.

12 Lo! Ngurumo ya watu wengi! Wananguruma kama bahari. Lo! Mlio wa watu wa mataifa! Yanatoa mlio kama wa maji mengi.

13 Mataifa yananguruma kama ngurumo ya maji mengi, lakini Mungu atayakemea, nayo yatakimbilia mbali. Yatafukuzwa kama makapi mlimani mbele ya upepo; kama vumbi litimuliwalo na kimbunga.

14 Wakati wa jioni yanaleta hofu kuu, lakini kabla ya asubuhi yametoweka! Hilo ndilo litakalowapata wanaonyakua mali yetu, ndilo litakalowapata wanaotupora.

18

1 Ole, wake nchi iliyojaa mvumo wa mabawa, nchi iliyoko ngambo ya mito ya Kushi!

2 Inatuma wajumbe ambao wanasafiri mtoni Nili, wamepanda mashua za mafunjo. Nendeni, enyi wajumbe wepesi, kwa taifa kubwa na hodari, la watu warefu na wa ngozi laini. Watu hao wanaoogopwa kila mahali na nchi yao imegawanywa na mito.

3 Enyi wakazi wote ulimwenguni, nanyi mkaao duniani! Ishara itakapotolewa mlimani, tazameni! Tarumbeta itakapopigwa, sikilizeni.

4 Maana, Mwenyezi-Mungu ameniambia hivi: “Toka makao yangu juu nitatazama yanayotukia, nimetulia kama joto katika mwanga wa jua, kama wingu la umande wakati wa mavuno.

5 Maana, kabla ya mavuno, wakati wa kuchanua umekwisha, maua yamepukutika na kuwa zabibu mbivu, Mungu atakata chipukizi kwa kisu cha kupogolea, na kuyakwanyua matawi yanayotanda.

6 Yote yataachiwa ndege milimani, na wanyama wengine wa porini. Ndege walao nyama watakaa humo wakati wa majira ya kiangazi, na wanyama wa porini watafanya makao humo wakati wa majira ya baridi.”

7 Wakati huo, Mwenyezi-Mungu wa majeshi ataletewa tambiko kutoka kwa watu warefu wenye ngozi laini, watu watishao karibu na mbali, taifa la watu wenye nguvu na ushindi, ambalo ardhi yake imegawanywa na mito. Ataletewa tambiko hizo mlimani Siyoni anapoabudiwa yeye Mwenyezi-Mungu wa majeshi.

19

1 Kauli ya Mungu dhidi ya nchi ya Misri. “Mwenyezi-Mungu amepanda juu ya wingu liendalo kasi na kuja mpaka nchi ya Misri. Sanamu za miungu ya Wamisri zitatetemeka mbele yake, mioyo ya Wamisri itayeyuka kwa hofu.

2 Mimi nitawachochea Wamisri wagongane: Ndugu na ndugu yake, jirani na jirani yake, mji mmoja na mji mwingine, mfalme mmoja na mfalme mwingine.

3 Nitawaondolea Wamisri uhodari wao, nitaivuruga mipango yao; watatafuta maoni kwa sanamu na mizimu, wachawi, mizuka na pepo.

4 Nitawatia Wamisri mikononi mwa bwana katili, mfalme mkali ambaye atawatawala. Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu wa majeshi, nimenena.”

5 Maji ya mto Nili yatakaushwa, nao utakauka kabisa.

6 Mifereji yake itatoa uvundo, vijito vyake vitapunguka na kukauka. Nyasi na mafunjo yake yataoza.

7 Sehemu za kandokando ya Nili zitakuwa tupu. Mimea yote iliyopandwa humo itakauka na kupeperushiwa mbali na kutoweka.

8 Wavuvi watalia na kuomboleza, wote watumiao ndoana watalalama; wote wanaotanda nyavu majini watakufa moyo.

9 Wafuma nguo za kitani watakata tamaa, wote kwa pamoja watakufa moyo.

10 Wafuma nguo watafedheheshwa, na vibarua watahuzunika.

11 Viongozi wa mji wa Soani ni wapumbavu kabisa, washauri wa Farao wanatoa shauri la kijinga! Awezaje kila mmoja kumwambia Farao, “Mimi ni mzawa wa mtaalamu stadi; mzawa wa wafalme wa hapo kale!”

12 Wako wapi, ewe Farao, wataalamu wako? Waache basi wakuambie na kukujulisha aliyopanga Mwenyezi-Mungu wa majeshi dhidi ya Misri!

13 Lakini viongozi wa Soani ni wapumbavu, wakuu wa Memfisi wamedanganyika. Hao walio msingi wa makabila yao wamelipotosha taifa la Misri.

14 Mwenyezi-Mungu amewamwagia hali ya vurugu, wakawapotosha Wamisri katika mipango yao yote, wakawa kama mlevi anayeyumbayumba akitapika.

15 Hakuna mtu yeyote nchini Misri, kiongozi au raia, mashuhuri au duni, awezaye kufanya lolote la maana.

16 Siku ile watu wa Misri wataogopa kama wanawake. Watatetemeka kwa hofu watakapomwona Mwenyezi-Mungu wa majeshi ameunyosha mkono wake dhidi yao.

17 Yuda atakuwa tishio kubwa kwa Wamisri. Wote watakaoambiwa habari za Yuda wataingiwa na woga kwa sababu ya jambo aliloamua Mwenyezi-Mungu wa majeshi kuwatenda.

18 Siku hiyo lugha ya Kiebrania itatumika katika miji mitano ya Misri, na watu wa miji hiyo wataapa kuwa waaminifu kwa Mwenyezi-Mungu wa majeshi. Mji mmojawapo utaitwa “Mji wa Jua.”

19 Siku hiyo, kutakuwa na madhabahu kwa ajili ya Mwenyezi-Mungu katikati ya nchi ya Misri, na nguzo iliyowekwa wakfu kwa Mungu kwenye mpaka wa Misri.

20 Madhabahu hiyo itakuwa ishara na ushuhuda kwake Mwenyezi-Mungu wa majeshi katika nchi ya Misri. Watu wakimlilia Mwenyezi-Mungu humo kwa sababu ya kukandamizwa, yeye atawapelekea mkombozi atakayewatetea na kuwakomboa.

21 Mwenyezi-Mungu atajijulisha kwa Wamisri na hapo ndipo Wamisri watakapomkiri na kumwabudu kwa kumtolea tambiko na sadaka za kuteketezwa. Hali kadhalika, watamwekea Mwenyezi-Mungu nadhiri ambazo watazitimiza.

22 Mwenyezi-Mungu atawaadhibu Wamisri na kuwaponya. Nao watamrudia, naye atayasikiliza maombi yao na kuwaponya.

23 Wakati huo, kutakuwa na barabara kuu kutoka nchi ya Misri hadi nchi ya Ashuru. Waashuru watawatembelea Wamisri, na Wamisri watawatembelea Waashuru; nao wote watamwabudu Mungu pamoja.

24 Wakati huo, Israeli itahesabiwa pamoja na Misri na Ashuru; mataifa haya matatu yatakuwa baraka kwa dunia yote.

25 Mwenyezi-Mungu wa majeshi atawabariki na kusema, “Wabarikiwe Wamisri watu wangu, kadhalika na Waashuru ambao ni ishara ya kazi yangu na Waisraeli walio mali yangu.”

20

1 Sargoni mfalme wa Ashuru, alimtuma jemadari wake mkuu kuuvamia mji wa Ashdodi. Naye akaushambulia na kuuteka.

2 Miaka mitatu kabla ya hapo, Mwenyezi-Mungu alikuwa amemwambia Isaya, mwana wa Amozi hivi: “Nenda ukavue vazi la gunia unalovaa kiunoni, na viatu miguuni mwako.” Isaya akafanya hivyo; akawa anatembea uchi na bila viatu.

3 Basi, mnamo mwaka huo mji wa Ashdodi ulipotekwa, Mwenyezi-Mungu alisema: “Mtumishi wangu Isaya amekuwa akitembea uchi na bila viatu kwa muda wa miaka mitatu sasa, kama ishara na alama dhidi ya nchi ya Misri na Kushi.

4 Basi, mfalme wa Ashuru atawachukua mateka Wamisri na Wakushi, wakubwa kwa wadogo. Watachukuliwa, nao watatembea uchi na bila viatu; matako wazi, kwa aibu ya Misri.

5 Kisha wote waliotegemea Kushi na kujivunia Misri watajuta na kufadhaika.

6 Wakati huo, wakazi wa pwani ya Filistia watasema, ‘Tazameni yaliyowapata watu tuliowategemea na kuwakimbilia kuomba msaada watuokoe na mfalme wa Ashuru! Na sasa, sisi tutawezaje kusalimika?’”

21

1 Kauli ya Mungu dhidi ya jangwa kando ya bahari. Kama vimbunga vinavyovuma kutoka kusini, wavamizi wanakuja kutoka jangwani, kutoka katika nchi ya kutisha.

2 Nimeoneshwa maono ya kutisha, maono ya watu wa hila watendao hila, maono ya watu waangamizi wafanyao maangamizi. Pandeni juu vitani enyi Waelamu; shambulieni enyi Wamedi! Mungu atakomesha mateso yote yaliyoletwa na Babuloni.

3 Kwa maono hayo nimeingiwa na hofu kubwa, uchungu mwingi umenikumba; kama uchungu wa mama anayejifungua. Maumivu yamenizidi hata siwezi kusikia; nimefadhaika hata siwezi kuona.

4 Moyo unanidunda na woga umenikumba. Nilitamani jioni ifike lakini ilipofika ikawa ya kutetemesha.

5 Chakula kimetayarishwa, shuka zimetandikwa, sasa watu wanakula na kunywa. Ghafla, sauti inasikika: “Inukeni enyi watawala! Wekeni silaha tayari!”

6 Maana Bwana aliniambia, “Nenda ukaweke mlinzi; mwambie atangaze atakachoona.

7 Akiona kikosi, wapandafarasi wawiliwawili, wapandangamia na wapandapunda, na awe macho; naam, akae macho!”

8 Kisha huyo mlinzi akapaza sauti: “Bwana, nimesimama juu ya mnara wa ulinzi mchana kutwa, nimeshika zamu usiku kucha!”

9 Tazama, kikosi kinakuja, wapandafarasi wawiliwawili. Wanasema: “Babuloni umeanguka! Umeanguka! Sanamu zote za miungu yake zimetupwa chini na kuvunjwavunjwa!”

10 Ewe Israeli, watu wangu, enyi mliotwangwa na kupurwa kama nafaka. Sasa nimewaambieni mambo niliyoyasikia kwa Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli.

11 Kauli ya Mungu dhidi ya Duma. Ninasikia mtu ananiita kutoka Seiri: “Mlinzi, nini kipya leo usiku? Kuna kipya chochote leo usiku?”

12 Nami mlinzi nikajibu: “Asubuhi inakuja, kadhalika na usiku; ukitaka kuuliza, uliza tu; nenda urudi tena.”

13 Kauli ya Mungu dhidi ya Arabia. Enyi misafara ya Dedani, pigeni kambi leo usiku kwenye nyika za Arabia.

14 Enyi wakazi wa nchi ya Tema, wapeni maji hao wenye kiu; wapelekeeni chakula hao wakimbizi.

15 Maana wamekimbia mapanga, mapanga yaliyochomolewa, pinde zilizovutwa na ukali wa mapigano.

16 Maana Bwana aliniambia hivi: “Katika muda wa mwaka mmoja, bila kuzidi wala kupungua, fahari yote ya Kedari itakwisha.

17 Wapiga upinde wachache kati ya mashujaa wa watu wa Kedari ndio watakaosalia. Mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, nimenena.”

22

1 Kauli ya Mungu dhidi ya Bonde la Maono. Kuna nini ee Yerusalemu? Mbona watu wote mmepanda juu ya nyumba?

2 Kwa nini mnapiga kelele za shangwe, na mji wote umechangamka na kujaa vigelegele? Watu wenu waliokufa hawakuuawa vitani, wala hawakuuawa katika mapigano.

3 Maofisa wenu wote walikimbia, wakakamatwa hata kabla ya kufyatua mshale mmoja. Watu wako wote waliopatikana walitekwa, ingawa walikuwa wamekimbilia mbali.

4 Ndiyo maana nawaambieni: Msijali chochote juu yangu niacheni nilie machozi ya uchungu. Msijisumbue kunifariji kwa ajili ya balaa walilopata watu wangu.

5 Maana leo Mwenyezi-Mungu wa majeshi ametuletea mchafuko: Kushindwa na wasiwasi katika Bonde la Maono. Kuta za mji zimebomolewa, mayowe ya wakazi wake yasikika mpaka milimani.

6 Majeshi ya Elamu, pinde na mishale mikononi, walikuja wamepanda farasi na magari ya vita; nalo jeshi la Kiri lilitayarisha ngao zake.

7 Mabonde yako mazuri ewe Yerusalemu, yalijaa magari ya vita na farasi; wapandafarasi walijipanga tayari langoni mwako.

8 Ulinzi wote wa Yuda uliporomoka. Siku hiyo mlikwenda kutafuta silaha zilizokuwa zimehifadhiwa katika Nyumba ya Msitu,

9 mkaona kwamba nyufa za kuta za mji wa Daudi ni nyingi, mkajaza maji bwawa la chini.

10 Mlizikagua nyumba za mji wa Yerusalemu, mkabomoa baadhi yake ili kupata mawe ya kuimarisha kuta za mji.

11 Katikati ya kuta hizo mlijijengea birika la kuhifadhia maji yanapotiririka kutoka bwawa la zamani. Lakini hamkumtafuta Mungu aliyepanga mambo haya yote; hamkumjali yeye aliyepanga hayo yote tangu zamani.

12 Siku hiyo, Mwenyezi-Mungu, wa majeshi aliwataka mlie na kuomboleza, mnyoe nywele na kuvaa mavazi ya gunia.

13 Lakini nyinyi mkafurahi na kusherehekea. Mlichinja ng'ombe na kondoo, mkala nyama na kunywa divai. Nyinyi mlisema: “Acha tule na kunywa maana kesho tutakufa.”

14 Mwenyezi-Mungu wa majeshi alinifunulia haya akisema: “Hakika hawatasamehewa uovu huu, watakufa bila kusamehewa. Mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi nimesema.”

15 Mwenyezi-Mungu wa majeshi aliniambia niende kwa Shebna, msimamizi wa jamaa ya kifalme, nikamwambie hivi:

16 “Una haki gani kuwa huku? Je, una ndugu yeyote hapa, hata ukajichongea kaburi mwambani juu ya mlima?

17 Wewe ni mwenye nguvu, lakini Mwenyezi-Mungu atakutupilia mbali kwa nguvu.

18 Atakubana kabisa na kukuzungushazungusha, kisha atakutupa kama mpira mpaka katika nchi pana. Huko utafia karibu na magari yako ya vita unayojivunia. Wewe ni aibu kwa nyumba ya bwana wako.

19 Mwenyezi-Mungu atakungoa madarakani mwako na kukuporomosha kutoka mahali ulipo.

20 “Siku hiyo, nitamleta mtumishi wangu Eliakimu mwana wa Hilkia.

21 Nitamvisha vazi lako rasmi, nitamfunga mshipi wako na kumpa madaraka yako. Yeye atakuwa baba kwa watu wa Yerusalemu na kwa ukoo wa Yuda.

22 Nitamwekea begani mwake ufunguo wa nyumba ya Daudi. Akifungua, hakuna atakayeweza kufunga na akifunga, hakuna atakayeweza kufungua.

23 Nitamwimarisha Eliakimu kama kigingi kilichofungiwa mahali salama, naye atapata heshima tukufu katika ukoo wa wazee wake.

24 “Watu wote na jamaa yake, wadogo kwa wakubwa watajitegemeza kwake kama chungu na vikombe vilivyotundikwa kwenye kigingi.

25 Lakini siku moja, kama vile kile kigingi kilichofungwa mahali salama kitalegea kwa uzito, Eliakimu naye atapoteza madaraka yake na jamaa zake wote watabaki bila msaada. Mimi Mwenyezi-Mungu nimenena.”

23

1 Kauli ya Mungu dhidi ya Tiro. Ombolezeni, enyi mabaharia wa mbali baharini, maana Tiro mji wenu umeharibiwa, humo hamna tena makao wala bandari. Mtazipokea habari hizo mtakaporejea kutoka Kupro.

2 Nyamazeni kwa mshangao enyi wakazi wa pwani, naam, tulieni enyi wafanyabiashara wa Sidoni, ambao wajumbe wenu wanapita baharini,

3 wakasafiri katika bahari nyingi. Mapato yenu yalikuwa nafaka ya Misri, mkaweza kufanya biashara na mataifa.

4 Aibu kwako ewe Sidoni, mji wa ngome kando ya bahari! Bahari yenyewe yatangaza: “Sijapata kuwa na uchungu wa kuzaa, wala sijawahi kuzaa; sijawahi kulea wavulana, wala kutunza wasichana!”

5 Habari zitakapoifikia Misri kwamba Tiro imeangamizwa, Wamisri watafadhaika sana.

6 Ombolezeni enyi wenyeji wa Foinike! Jaribuni kukimbilia Tarshishi.

7 Je, huu ndio mji wa furaha wa Tiro, mji ambao ulijengwa zamani za kale, ambao wakazi wake walikwenda kumiliki nchi za mbali?

8 Ni nani aliyepanga mambo haya dhidi ya Tiro, mji uliowatawaza wafalme, wafanyabiashara wake walikuwa wakuu, wakaheshimiwa duniani kote?

9 Ni Mwenyezi-Mungu wa majeshi! Yeye ndiye aliyeyapanga haya yote. Alifanya hivyo akiharibu kiburi chao na kuwaaibisha waheshimiwa wake.

10 Limeni sasa ardhi yenu enyi wakazi wa Tarshishi; maana hamna tena bandari kwa ajili ya meli kubwa.

11 Mwenyezi-Mungu ameunyosha mkono wake juu ya bahari, amezitetemesha falme; ametoa amri kuziharibu ngome za Kanaani.

12 Alisema: “Ewe binti Sidoni hutaweza kufanya sherehe tena; hata ukikimbilia Kupro, huko nako hutapata pumziko!”

13 (Ni Wakaldayo, wala si Waashuru, waliowaacha wanyama wa porini wauvamie mji wa Tiro. Wao ndio waliouzungushia mji huo minara ya kuushambulia, wakayabomoa majumba yake na kuufanya magofu.)

14 Pigeni yowe enyi meli za Tarshishi, maana kimbilio lenu limeharibiwa.

15 Hapo mji wa Tiro utasahaulika kwa muda wa miaka sabini, muda wa maisha ya mfalme. Baada ya miaka hiyo sabini, mji wa Tiro utakumbwa na kile watu wanachoimba juu ya malaya:

16 “Twaa kinubi chako uzungukezunguke mjini, ewe malaya uliyesahaulika! Imba nyimbo tamutamu. Imba nyimbo nyinginyingi ili upate kukumbukwa tena.”

17 Baada ya miaka hiyo sabini, Mwenyezi-Mungu atauadhibu mji wa Tiro, nao utarudia kufanya uzinzi kwa kujiuza kwa mataifa yote ya dunia.

18 Fedha utakayopata itawekwa wakfu kwa Mwenyezi-Mungu. Mji wenyewe hautafaidika kwa fedha hiyo ila wale wanaomwabudu Mwenyezi-Mungu wataitumia kununulia chakula kingi na mavazi mazuri.

24

1 Sasa Mwenyezi-Mungu anaiharibu dunia na kuifanya tupu. Atausokota uso wa dunia na kuwatawanya wakazi wake.

2 Kila mtu atapatwa na mambo yaleyale: Mtu wa kawaida na kuhani; mtumwa na bwana wake; mjakazi na bibi yake; mnunuzi na mwuzaji; mkopeshaji na mkopaji; mdai na mdaiwa.

3 Dunia itaharibiwa kabisa na kuangamizwa; Mwenyezi-Mungu ametamka hayo.

4 Dunia inakauka na kunyauka; ulimwengu unafadhaika na kunyauka; mbingu zinafadhaika pamoja na dunia.

5 Watu wameitia najisi dunia maana wamezivunja sheria za Mungu, wamezikiuka kanuni zake, wamelivunja agano lake la milele.

6 Kwa sababu hiyo laana inaitokomeza dunia, wakazi wake wanateseka kwa makosa yao. Wakazi wa dunia wamepungua, ni watu wachache tu waliosalia.

7 Mizabibu inanyauka, divai inakosekana. Wote waliokuwa wenye furaha sasa wanasononeka kwa huzuni.

8 Mdundo wa vigoma umekoma, nderemo na vifijo vimetoweka; midundo ya vinubi imekomeshwa.

9 Hakuna tena kunywa divai na kuimba; mvinyo umekuwa mchungu kwa wanywaji.

10 Mji uliohamwa umejaa uharibifu; kila nyumba imefungwa asiingie mtu.

11 Kuna kilio barabarani kwa kukosa divai; shangwe yote imekoma, furaha imetoweka duniani.

12 Mji ni magofu matupu; malango yake yamevunjwavunjwa.

13 Kama vile zeituni chache tu juu ya mzeituni au tini chache tu juu ya mtini baada ya kumaliza mavuno, ndivyo itakavyokuwa katika nchi zote: Watu wachache watabakia hai.

14 Watakaosalia watapaza sauti, wataimba kwa shangwe. Kutoka magharibi watatangaza ukuu wa Mwenyezi-Mungu,

15 nao wakazi wa mashariki watamsifu. Watu wa mbali watalisifu jina la Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli.

16 Tunasikia nyimbo za sifa kutoka miisho ya dunia, nyimbo za kumsifu Mungu aliye mwadilifu. Lakini mimi ninanyongonyea, naam, ninanyongonyea. Ole wangu mimi! Wasaliti wanaendelea kuwa wasaliti, usaliti wao unazidi kuwa mbaya zaidi.

17 Hofu, mashimo na mitego, hivi ndivyo vinavyowangojeni enyi wakazi wa dunia.

18 Atakayeikimbia hofu atatumbukia shimoni; atakayetoka shimoni atanaswa mtegoni. Madirisha ya mbinguni yamefunguliwa, misingi ya dunia inatikisika.

19 Dunia inavunjikavunjika, inapasuka na kutikiswatikiswa.

20 Inapepesuka kama mlevi, inayumbayumba kama kibanda. Imelemewa na mzigo wa dhambi zake nayo itaanguka wala haitainuka tena.

21 Siku ile Mwenyezi-Mungu ataliadhibu jeshi la angani kadhalika na wafalme wa duniani.

22 Wote watakusanywa kama wafungwa shimoni; watafungwa gerezani pamoja kwa miaka mingi, na baada ya muda huo atawaadhibu.

23 Kisha mwezi utaaibishwa, nalo jua litaona aibu kuangaza, kwa kuwa Mwenyezi-Mungu wa majeshi atatawala huko Yerusalemu katika mlima Siyoni; ataonesha wazee wa watu wake utukufu wake.

25

1 Wewe, ee Mwenyezi-Mungu, ndiwe Mungu wangu; nitakutukuza na kulisifu jina lako, kwa maana umetenda mambo ya ajabu; waitekeleza kwa uaminifu na kweli mipango uliyoipanga tangu zamani.

2 Umeufanya mji ule kuwa rundo la mawe, mji wenye ngome kuwa uharibifu. Majumba ya watu wageni yametoweka, wala hayatajengwa tena upya.

3 Kwa hiyo watu wenye nguvu watakutukuza, miji ya mataifa katili itakuogopa.

4 Maana wewe umekuwa ngome kwa maskini, ngome kwa fukara katika taabu zao. Wewe ni kimbilio wakati wa tufani, kivuli wakati wa joto kali. Kweli pigo la watu wakatili ni kali kama tufani inayopiga ukuta;

5 ni kama joto la jua juu ya nchi kavu. Lakini wewe wakomesha fujo ya wageni. Kama wingu lizimavyo joto la jua ndivyo ukomeshavyo nyumba za ushindi za wakatili.

6 Juu ya mlima Siyoni, Mwenyezi-Mungu wa majeshi atawafanyia watu wote karamu ya vinono na divai nzuri, nyama tamu na mafuta, pamoja na divai safi.

7 Katika mlima huuhuu, Mwenyezi-Mungu ataliondoa wingu la huzuni lililowafunika watu wote, kifuniko cha uchungu juu ya mataifa yote.

8 Bwana Mungu atakiangamiza kifo milele! Atayafuta machozi katika nyuso za watu wote na kuwaondolea watu wake aibu duniani kote. Bwana Mwenyezi-Mungu ametamka.

9 Siku ile, watu wote watasema, “Huyu ndiye Mungu wetu! Tumemngojea atuokoe. Huyu ndiye Mwenyezi-Mungu tuliyemtazamia. Njoni tufurahi na kushangilia kwa kuwa ametuokoa.”

10 Mwenyezi-Mungu ataulinda mlima wa Siyoni, lakini watu wa Moabu watakanyagwakanyagwa nchini mwao kama nyasi katika shimo la mbolea.

11 Watainyosha mikono yao kama mtu anayejaribu kuogelea, lakini pamoja na ustadi wao, Mwenyezi-Mungu ataporomosha kiburi chao.

12 Atayabomoa maboma ya miji ya Moabu yenye kuta ndefu na kuyabwaga chini mavumbini.

26

1 Siku ile watu wataimba wimbo huu katika nchi ya Yuda: Sisi tuna mji imara: Mungu anatulinda kwa kuta na ngome.

2 Fungueni malango ya mji, taifa aminifu liingie; taifa litendalo mambo ya haki.

3 Ee Mungu, wawaweka katika amani walio thabiti, wawaweka katika amani kwa kuwa wanakutegemea.

4 Mtumaini Mwenyezi-Mungu siku zote kwa maana yeye ni mwamba wa usalama milele.

5 Amewaporomosha waliokaa pande za juu, mji maarufu ameuangusha mpaka chini, ameutupa mpaka mavumbini.

6 Sasa mji huo unakanyagwakanyagwa kwa miguu ya watu maskini na fukara.

7 Njia ya watu wanyofu ni rahisi; ewe Mungu mwadilifu, wasawazisha njia yao.

8 Katika njia ya maamuzi yako tunakungojea ee Mwenyezi-Mungu; kulikumbuka jina lako ndiyo tamaa yetu.

9 Moyo wangu wakutamani usiku kucha, nafsi yangu yakutafuta kwa moyo. Utakapoihukumu dunia, watu wote ulimwenguni watajifunza haki.

10 Lakini waovu hata wakipewa fadhili, hawawezi kujifunza kutenda haki. Hata katika nchi ya wanyofu, wao bado wanatenda maovu, wala hawajali ukuu wako wewe Mwenyezi-Mungu.

11 Ee Mwenyezi-Mungu umeinua mkono kuwaadhibu, lakini maadui zako hawauoni. Waoneshe uwapendavyo watu wako nao wataaibika. Moto wa hasira yako uwateketeze maadui zako!

12 Wewe, ee Mwenyezi-Mungu, umetupatia amani; umefanikisha shughuli zetu zote.

13 Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, tulipata kutawaliwa na watu wengine na miungu yao, lakini twakiri wewe pekee kuwa Mungu wetu.

14 Watu hao wamekufa, wala hawataishi tena; wamekuwa mizimu, wala hawatafufuka. Maana wewe umewaadhibu na kuwaangamiza, hakuna atakayeweza kuwakumbuka tena.

15 Umelikuza taifa letu, ee Mwenyezi-Mungu, naam, umelizidisha taifa letu. Umeipanua mipaka yote ya nchi, kwa hiyo wewe watukuka.

16 Ee Mwenyezi-Mungu, walipotaabika walikutafuta, walikuomba msaada ulipowaadhibu.

17 Kama vile mama mjamzito anayejifungua hulia na kugaagaa kwa uchungu, ndivyo tulivyokuwa kwa sababu yako, ee Mwenyezi-Mungu.

18 Sisi tulipata maumivu ya kujifungua lakini tukajifungua tu upepo! Hatukupata ushindi wowote kwa ajili ya nchi yetu, hatukuweza kuongeza idadi ya watu katika nchi.

19 Wafu wako wataishi tena, miili yao itafufuka. Wanaolala mavumbini wataamka na kuimba kwa furaha! Mungu atapeleka umande wake wa uhai, nao walio kwa wafu watatoka hai.

20 Njoni watu wangu, ingieni majumbani mwenu, mkajifungie humo ndani. Jificheni kwa muda mfupi, mpaka ifike ghadhabu ya Mwenyezi-Mungu.

21 Maana Mwenyezi-Mungu aja kutoka kwake juu, kutoka makao yake huko mbinguni; kuwaadhibu wakazi wa dunia kwa uovu wao. Nayo dunia haitaficha tena wale waliouawa, ila itaufichua umwagaji damu wote.

27

1 Siku hiyo, Mwenyezi-Mungu atautwaa upanga wake mkubwa, mkali na imara, na kuliadhibu dude Lewiyathani joka lirukalo na danganyifu; Mwenyezi-Mungu ataliua joka liishilo baharini.

2 Siku hiyo, Mwenyezi-Mungu atasema hivi: “Imbeni utenzi wa shamba langu zuri la mizabibu!

3 Mimi, Mwenyezi-Mungu, ni mkulima wake; nalimwagilia maji kila wakati, ninalilinda usiku na mchana, lisije likaharibiwa na mtu yeyote.

4 Silikasirikii tena shamba hili; kama miiba na mbigili ingelilivamia, mimi ningepambana nayo na kuichoma moto.

5 Maadui za watu wangu wakitaka ulinzi wangu, basi, na wafanye amani nami; naam, wafanye amani nami.”

6 Itakuja siku wazawa wa Yakobo watashika mizizi; naam, watu wa Israeli watachanua na kuchipua, na kuijaza dunia yote kwa matunda.

7 Mungu hakuwaadhibu Waisraeli vikali kama alivyowaadhibu maadui wake; Waisraeli waliopotea vitani, ni wachache kuliko wale wa maadui zake.

8 Aliwaadhibu watu wake kwa kuwapeleka uhamishoni. Wakati wa upepo mkali wa mashariki, aliwaondoa kwa kipigo kikali.

9 Hivi ndivyo uovu wa wazawa wa Yakobo utakavyoondolewa, hivi ndivyo dhambi yake itakavyofutwa kabisa: Ataziharibu madhabahu za miungu; mawe yake yatasagwasagwa kama chokaa; Ashera, wala madhabahu za kufukizia ubani hazitabaki.

10 Mji ule wa ngome sasa umekuwa mtupu, umeachwa na kuhamwa kama jangwa, humo ndama wanalisha na kupumzika.

11 Matawi ya miti yamekauka na kuvunjika; kina mama huyaokota wakawashia moto. Watu hawa hawajaelewa kitu, kwa hiyo Mungu, Muumba wao, hatawahurumia, yeye aliyewafanya, hatawafadhili.

12 Siku hiyo, kutoka mto Eufrate hadi mpakani mwa Misri, Mwenyezi-Mungu ataipura nafaka yake, nanyi Waisraeli mtakusanywa mmojammoja.

13 Siku hiyo, tarumbeta kubwa itapigwa na watu wote wa Israeli waliopotea nchini Ashuru au waliotawanywa nchini Misri watarudi na kumwabudu Mwenyezi-Mungu juu ya mlima mtakatifu huko Yerusalemu.

28

1 Ole wenye majivuno na walevi wa Efraimu, fahari yake inatoweka kama ua linalonyauka! Naam, fahari iliyotawala bondeni kwenye rutubarutuba; na vichwani kwao walio watu walevi kupindukia!

2 Bwana amejichagulia mtu wake shujaa na mwenye nguvu, ambaye ni kama mvua ya mawe na dhoruba kali, kama tufani ya mafuriko makubwa; kwa mkono wake atawatupa chini ardhini.

3 Majivuno na fahari ya walevi wa Efraimu yatakanyagwakanyagwa ardhini,

4 fahari yake inatoweka kama ua linalonyauka; fahari iliyotawala bondeni kwenye rutuba itakuwa kama tini za mwanzo kabla ya kiangazi; mtu akiziona huzichuma na kuzila mara moja.

5 Siku ile Mwenyezi-Mungu wa majeshi atakuwa taji tukufu, kama kilemba kizuri kwa watu wake watakaobaki hai.

6 Waamuzi mahakamani atawaongoza kutenda haki, nao walinzi wa mji atawapa nguvu.

7 Lakini wako wengine waliolewa divai na kuyumbayumba kwa sababu ya pombe; naam, makuhani na manabii wamelewa mvinyo, wamevurugika kwa divai. Wanayumbayumba kwa pombe kali; maono yao yamepotoka, wanapepesuka katika kutoa hukumu.

8 Meza zote zimetapakaa matapishi, hakuna mahali popote palipo safi.

9 Wao wananidhihaki na kuuliza: “Huyu nabii ataka kumfundisha nani? Je, anadhani atatueleza sisi ujumbe wake? Je, sisi ni watoto wachanga walioachishwa kunyonya juzijuzi?

10 Anatufundisha kama watoto wadogo: Sheria baada ya sheria, mstari baada ya mstari; mara hiki, mara kile!”

11 Haya basi! Mwenyezi-Mungu ataongea na watu hawa kwa njia ya watu wa lugha tofauti wanaoongea lugha ngeni.

12 Hata hivyo yeye alikuwa amewaahidi: “Nitawaonesheni pumziko, nitawapeni pumziko enyi mliochoka. Hapa ni mahali pa pumziko.” Lakini wao hawakutaka kunisikiliza.

13 Kwa hiyo kwao neno la Mwenyezi-Mungu litakuwa tu: Sheria sheria, mstari mstari; mara hiki, mara kile! Nao watalazimika kukimbia lakini wataanguka nyuma; watavunjika, watanaswa na kutekwa.

14 Basi, sikilizeni neno la Mwenyezi-Mungu, enyi wenye madharau mnaotawala watu wa Yerusalemu,

15 “Nyinyi mnajidai mmefanya mkataba na kifo, mmefanya mapatano na Kuzimu! Nyinyi mwasema eti balaa lijapo halitawapata, kwa sababu mmefanya uongo kuwa tegemeo lenu, na udanganyifu kuwa kinga yenu!”

16 Basi, hivi ndivyo asemavyo Mwenyezi-Mungu: “Tazama! Naweka mjini Siyoni jiwe la msingi, jiwe ambalo limethibitika. Jiwe la pembeni, la thamani, jiwe ambalo ni la msingi thabiti; jiwe lililo na maandishi haya: ‘Anayeamini hatatishika.’

17 Nitatumia haki kama kipimo changu, nitatumia uadilifu kupimia.” Mvua ya mawe itaufagilia mbali uongo mnaoutegemea, na mafuriko yataharibu kinga yenu.

18 Hapo mkataba wenu na kifo utabatilishwa, na mapatano yenu na Kuzimu yatafutwa. Janga lile kuu litakapokuja litawaangusheni chini.

19 Kila litakapopitia kwenu litawakumba; nalo litapita kila asubuhi, mchana na usiku. Kusikia ujumbe huu tu kutakuwa kitisho.

20 Kwenu itakuwa kama ajinyoshaye juu ya kitanda kifupi mno, au kujifunika kwa blanketi lililo dogo mno!

21 Maana Mwenyezi-Mungu atainuka kama kule mlimani Perazimu; atawaka hasira kama kule bondeni Gibeoni. Atatekeleza mpango wake wa ajabu; atatenda kazi yake ya kustaajabisha.

22 Basi, nyinyi msiwe na madharau vifungo vyenu visije vikakazwa zaidi. Maana nimesikia kuwa Mwenyezi-Mungu wa majeshi ameazimia kuiangamiza nchi yote.

23 Tegeni sikio msikilize ninayowaambieni; sikilizeni kwa makini hotuba yangu.

24 Je, alimaye ili kupanda hulima tu? Je, huendelea kulima na kusawazisha shamba lake?

25 La! Akisha lisawazisha shamba lake, hupanda mbegu za bizari na jira, akapanda ngano na shayiri katika safu, na mipakani mwa shamba mimea mingineyo.

26 Mtu huyo huwa anajua la kufanya, kwa sababu Mungu wake humfundisha.

27 Bizari haipurwi kwa mtarimbo wala jira kwa gari la ng'ombe! Ila bizari hupurwa kwa kijiti na jira kwa fimbo.

28 Mkulima apurapo ngano yake, haendelei kuipura mpaka kuvunja punje zake. Anajua jinsi ya kuipura kwa gurudumu, bila kuziharibu punje za ngano.

29 Ujuzi huu nao watoka kwa Mwenyezi-Mungu wa majeshi. Mipango yake Mungu ni ya ajabu, hekima yake ni kamilifu kabisa.

29

1 Ole wako Yerusalemu, madhabahu ya Mungu; mji ambamo Daudi alipiga kambi yake! Miaka yaja na kupita, na sikukuu zako zaendelea kufanyika;

2 lakini mimi Mungu nitauhuzunisha Yerusalemu, nako kutakuwa na vilio na maombolezo, mji wenyewe utakuwa kama madhabahu iliyolowa damu ya watu waliouawa.

3 Mimi nitapanga jeshi dhidi ya Yerusalemu, nami nitauzingira na kuushambulia.

4 Utaangushwa mbali sana ndani ya ardhi; kutoka huko mbali utatoa sauti; maneno yako yatatoka huko chini mavumbini; sauti yako itatoka ardhini kama ya mzimu.

5 Kundi la maadui zako litakuwa kama vumbi laini, waliokutendea ukatili watakuwa kama makapi. Hayo yatafanyika ghafla.

6 Mwenyezi-Mungu wa majeshi atakuja kukusaidia; atakuja na ngurumo, tetemeko la ardhi na sauti kubwa; atakuja na kimbunga, tufani na moto uunguzao.

7 Hapo, kundi la mataifa yote yanayoshambulia Yerusalemu, wote wanaoshambulia ngome yake na kuutia wasiwasi, watatoweka kama ndoto, kama maono ya usiku.

8 Mataifa yote yanayoushambulia mji wa Yerusalemu yatakuwa kama mtu mwenye njaa anayeota anakula lakini aamkapo bado anaumwa na njaa! Au mtu mwenye kiu anayeota kuwa anakunywa, lakini anaamka mdhaifu, bado ana kiu.

9 Endeleeni kuwa wapumbavu na kuduwaa! Jipofusheni na kuwa vipofu! Leweni lakini si kwa divai; pepesukeni lakini si kwa pombe.

10 Mwenyezi-Mungu amewamiminia hali ya usingizi mzito; ameyafumba macho yenu enyi manabii, amefunika vichwa vyenu enyi waonaji.

11 Basi, kwenu nyinyi maono yote haya ni kama ujumbe ulioandikwa katika kitabu kilichofungwa kwa mhuri. Ukimpelekea mtu yeyote ajuaye kusoma, ukamwambia, “Hebu nisomee kitabu hiki,” atasema, “Siwezi kukisoma kwani kimefungwa kwa mhuri.”

12 Na ukimpa mtu yeyote asiyejua kusoma, ukamwambia, “Hebu nisomee kitabu hiki,” atakuambia, “Sijui kusoma.”

13 Bwana asema, “Watu hawa huja kuniabudu kwa maneno matupu, hali mioyo yao iko mbali nami. Wananiheshimu kulingana na mapokeo ya watu tu, jambo walilojifunza wao wenyewe.

14 Hivyo, nitawatenda tena watu hawa maajabu, mambo ya ajabu na ya kushangaza. Nao wenye hekima wao wataishiwa hekima, na busara ya wenye busara wao itatoweka.

15 “Ole mnaomficha Mwenyezi-Mungu mipango yenu, mnaotenda matendo yenu gizani na kusema: ‘Hamna atakayetuona; nani awezaye kujua tunachofanya?’

16 Nyinyi mnafanya mambo kinyume kabisa! Je, mfinyanzi na udongo ni hali moja? Chombo hakiwezi kumwambia aliyekitengeneza: ‘Wewe hukunitengeneza.’ Kilichofinyangwa hakiwezi kumwambia aliyekiumba, ‘Wewe hujui chochote.’”

17 Bado kidogo tu, msitu wa Lebanoni utageuzwa kuwa shamba lenye rutuba, na shamba lenye rutuba kuwa msitu.

18 Siku hiyo viziwi watasikia ujumbe ukisomwa kitabuni na kutoka gizani vipofu wataanza kuona.

19 Wanyofu watapata furaha mpya kwa Mwenyezi-Mungu, na maskini wa watu watashangilia kwa furaha kwa sababu ya Mungu, Mtakatifu wa Israeli.

20 Majitu makatili yataangamizwa, wenye kumdhihaki Mungu watakwisha, wote wanaootea kutenda maovu watatokomezwa.

21 Watatoweka wale wanaopotosha kesi ya mtu mahakamani, watu wanaowafanyia hila mahakimu na wasemao uongo kuwanyima haki yao wasio na hatia.

22 Kwa hiyo, Mwenyezi-Mungu aliyemkomboa Abrahamu, asema hivi kuhusu wazawa wa Yakobo: “Wazawa wa Yakobo hawataaibishwa tena, hawatainamisha vichwa vyao tena kwa aibu.

23 Watakapowaona watoto wao, watoto niliowajalia mimi mwenyewe, watalitukuza jina langu mimi Mtakatifu wa Yakobo; watakuwa na uchaji kwangu mimi Mungu wa Israeli.

24 Waliopotoka rohoni watapata maarifa na wenye kununa watakubali kufunzwa.”

30

1 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Ole wao watoto wanaoniasi, wanaotekeleza mipango yao na si mipango yangu, wanaofanya mikataba kinyume cha matakwa yangu! Naam, wanarundika dhambi juu ya dhambi.

2 Bila kunitaka shauri, wanafunga safari kwenda Misri, kukimbilia usalama katika ulinzi wa Farao, kupata mahali pa usalama nchini Misri.

3 Lakini ulinzi wa Farao utakuwa aibu yenu, na usalama nchini Misri utakuwa fedheha yenu.

4 Maana ingawa maofisa wao wamefika Soani, na wajumbe wao mpaka Hanesi,

5 wote wataaibishwa na hao wasioweza kuwasaidia, watu ambao hawawezi kuwapa msaada au faida, ila tu kuwapa aibu na fedheha.”

6 Kauli ya Mungu juu ya wanyama wa pande za Negebu: “Wajumbe wanapita katika nchi ya taabu na shida, yenye simba, nyoka wa sumu na majoka. Wamewabebesha wanyama wao mali zao, kuwapelekea watu wasioweza kuwafaa kitu.

7 Maana msaada wa Misri ni bure, haufai kitu; kwa hiyo nimeipanga Misri jina: ‘Joka lisilo na nguvu!’”

8 Mungu aliniambia: “Sasa chukua kibao cha kuandikia, uandike jambo hili mbele yao, liwe ushahidi wa milele:

9 Watu hawa ni waasi, watoto wasioaminika; watu wasiopenda kusikia mafunzo ya Mwenyezi-Mungu.

10 Huwaambia waonaji: ‘Msione maono’, na manabii: ‘Msitutangazie ukweli, bali tuambieni mambo ya kupendeza, toeni unabii wa mambo ya udanganyifu tu.

11 Geukeni na kuiacha njia ya ukweli; msituambie tena juu ya Mungu, Mtakatifu wa Israeli.’”

12 Kwa hiyo Mungu, Mtakatifu wa Israeli asema: “Nyinyi mmeukataa ujumbe wangu; mkapania kufanya dhuluma na udanganyifu.

13 Basi, dhambi hii itawaleteeni maangamizi kama ufa mkubwa katika ukuta mrefu; utabomoka mara na kuanguka chini ghafla.

14 Kuporomoka kwa ukuta huo, ni kama kupasuka kwa chungu ambacho kimepasuliwa vibaya sana, bila kusalia kigae cha kuchukulia moto mekoni, au kuchotea maji kisimani.”

15 Bwana Mungu, Mtakatifu wa Israeli, asema: “Mkinirudia na kutulia mtaokolewa; kwa utulivu na kunitumainia mtapata nguvu.” Lakini nyinyi hamkutaka.

16 Badala yake mlisema, “La! Sisi tutakimbia na farasi wenye mbio.” Sawa, mtakimbia na farasi wenye mbio, lakini farasi wa maadui zenu wana mbio zaidi.

17 Watu wenu elfu moja watamkimbia askari mmoja adui; na askari watano maadui watawakimbizeni nyote. Mwishowe, watakaosalia watakuwa kama mlingoti wa bendera mlimani, kama alama iliyo juu ya kilima.

18 Hata hivyo, Mwenyezi-Mungu anangoja awafadhili, atainuka na kuwaonea huruma. Maana, Mwenyezi-Mungu ni Mungu atendaye haki. Heri wote wale wanaomtumainia.

19 Enyi watu wa Siyoni, enyi watu wa Yerusalemu, hakika nyinyi hamtaomboleza tena. Kweli Mungu atawahurumia; mara tu atakaposikia kilio chenu atawaitikeni.

20 Ingawa Bwana atawalisha taabu na kuwanywesha dhiki, yeye ndiye Mwalimu wenu na hatajificha tena; nanyi mtamwona kwa macho yenu wenyewe.

21 Mkienda kulia au kushoto, mtasikia sauti nyuma yenu ikisema, “Njia ni hii; ifuateni.”

22 Mtavifanya haramu vinyago vyenu vya miungu vilivyopakwa fedha na sanamu zenu zilizopakwa dhahabu. Mtazitupilia mbali kama vitu najisi, mkisema, “Poteleeni mbali!”

23 Mtakapopanda mbegu zenu, Mwenyezi-Mungu atanyesha mvua kwa wakati wake, nazo zitakua na kuwapa mavuno mengi. Mifugo yenu nayo itapata malisho kwa wingi.

24 Mafahali na punda wenu wa kulimia watapata malisho yaliyochambuliwa vizuri na kutiwa chumvi.

25 Wakati utakapofika ambapo maadui watauawa na ngome zao kubomolewa, vijito vya maji vitatiririka kutoka kila mlima na kilima.

26 Tena mwezi utawaka kama jua, nao mwanga wa jua utakuwa mara saba ya mwanga wake wa kawaida, kana kwamba mwanga wa siku saba umeangaza katika siku moja. Mambo haya yote yatatukia wakati Mwenyezi-Mungu atakapoyafunga na kuyaponya majeraha aliyowaletea watu wake.

27 Tazameni, Mwenyezi-Mungu mwenyewe anakuja toka mbali! Amewaka hasira na moshi wafuka; midomo yake yaonesha ghadhabu yake, maneno anayosema ni kama moto uteketezao.

28 Pumzi yake ni kama mafuriko ya mto ambao maji yake yanafika hadi shingoni. Anakuja kuyachekecha mataifa kwa chekecheke ya maangamizi, kuwafunga lijamu na kuwapeleka wasikotaka.

29 Lakini nyinyi watu wa Yerusalemu mtaimba kwa furaha kama mfanyavyo wakati wa mkesha wa sikukuu. Mtajaa furaha kama watu wanaotembea kwa mdundo wa muziki wa filimbi kwenda mlimani kwa Mwenyezi-Mungu, Mwamba wa Israeli.

30 Mwenyezi-Mungu atawafanya watu wote waisikie sauti yake tukufu na pigo la nguvu yake lionekane kwa hasira nyingi. Kutakuwa na ndimi za moto mkali, ngurumo, dhoruba na mvua ya mawe.

31 Waashuru watajaa hofu watakaposikia sauti ya Mwenyezi-Mungu wakati atakapowachapa na fimbo yake.

32 Kila pigo la adhabu ya Mwenyezi-Mungu juu ya Waashuru litaandamana na mdundo wa ngoma na zeze. Yeye mwenyewe binafsi atapigana na Waashuru.

33 Naam, mahali pa kumteketeza mfalme wa Ashuru pamekwisha tayarishwa muda mrefu uliopita. Mahali penyewe ni shimo kubwa na pana. Moto upo na kuni kwa wingi. Mwenyezi-Mungu ataupulizia pumzi yake kama kijito cha madini ya kiberiti na kuuwasha.

31

1 Ole wao wale waendao Misri kuomba msaada, ole wao wanaotegemea farasi, wanaotegemea wingi wa magari yao ya vita, na nguvu za askari wao wapandafarasi, nao hawamtegemei Mtakatifu wa Israeli, wala hawamwombi Mwenyezi-Mungu shauri!

2 Mungu ni mwenye busara na huleta maangamizi. Habadilishi tamko lake; ila yuko tayari kuwakabili watu waovu kadhalika na wasaidizi wa watendao mabaya.

3 Wamisri ni binadamu tu wala si Mungu; farasi wao nao ni wanyama tu, si roho. Mwenyezi-Mungu akiunyosha mkono wake, taifa linalotoa msaada litajikwaa, na lile linalosaidiwa litaanguka; yote mawili yataangamia pamoja.

4 Mwenyezi-Mungu aliniambia: “Kama vile simba au mwanasimba angurumavyo kuyakinga mawindo yake, hata kundi la wachungaji likiitwa kumkabili, yeye hatishiki kwa kelele zao, wala hashtuki kwa sauti zao. Ndivyo atakavyoshuka Mwenyezi-Mungu wa majeshi kupigana juu ya mlima Siyoni na kilima chake.

5 Kama ndege arukavyo juu ya viota vyake, ndivyo Mwenyezi-Mungu atakavyoulinda Yerusalemu, ataulinda na kuukomboa, atauhifadhi na kuuokoa.

6 Enyi Waisraeli, mrudieni huyo mliyemsaliti vibaya.

7 Wakati utafika ambapo nyote mtavitupilia mbali vinyago vyenu vya fedha na dhahabu ambavyo mmejitengenezea kwa mikono yenu, vikawakosesha.

8 Hapo Waashuru watauawa kwa upanga, lakini si kwa upanga wa binadamu; naam, wataangamizwa kwa upanga ambao ni zaidi ya ule wa binadamu. Waashuru watakimbia na vijana wao watafanyizwa kazi za kitumwa.

9 Mfalme wao atatoroka kwa hofu, na maofisa wao wataiacha bendera yao kwa woga. Hayo ameyatamka Mwenyezi-Mungu ambaye moto wake umo mjini Siyoni, naam, tanuri lake limo mjini Yerusalemu.”

32

1 Kutatokea mfalme atakayetawala kwa uadilifu, nao viongozi wataongoza kwa kufuata haki.

2 Kila mmoja atakuwa kama mahali pa kujikinga na upepo, kama mahali pa kujificha wakati wa tufani. Watakuwa kama vijito vya maji katika nchi kame, kama kivuli cha mwamba mkubwa jangwani.

3 Macho hayatafumbwa tena, masikio yatabaki wazi.

4 Wafanyao mambo kwa hamaki wataamua kwa busara, wenye kigugumizi wataongea sawasawa.

5 Wapumbavu hawataitwa tena waungwana, wala walaghai hawataitwa tena waheshimiwa.

6 Wapumbavu hunena upumbavu, na fikira zao hupanga kutenda uovu, kutenda mambo yasiyo mema, kusema mambo ya kumkufuru Mwenyezi-Mungu. Huwaacha wenye njaa bila chakula, na wenye kiu huwanyima kinywaji.

7 Ulaghai wa walaghai ni mbaya; hao huzua visa viovu, na kumwangamiza maskini kwa maneno ya uongo, hata kama madai ya maskini ni halali.

8 Lakini waungwana hutenda kiungwana, nao hutetea mambo ya kiungwana.

9 Inukeni, enyi wanawake mnaostarehe, mnisikilize; sikilizeni ninayosema enyi mabinti mlioridhika.

10 Katika mwaka mmoja hivi mtatetemeka nyinyi mliotosheka; maana hamtapata mavuno yoyote, na mavuno ya zabibu yatatoweka.

11 Tetemekeni kwa woga, enyi mnaojikalia tu; tetemekeni kwa hofu, enyi mnaostarehe! Vueni nguo zenu, mbaki uchi, mjifunge vazi la gunia viunoni mwenu.

12 Jipigeni vifua kwa huzuni, ombolezeni, kwa sababu ya bustani zilizokuwa nzuri, kwa mizabibu iliyokuwa ikizaa sana,

13 kwa ardhi ya watu wangu inayoota miiba na mbigili, kwa nyumba zote zilizojaa watu wenye furaha, kwa mji uliokuwa na shangwe.

14 Maana ikulu ya mfalme itaachwa mahame, mji huo wa watu wengi utahamwa. Mlima na mnara wa ulinzi utakuwa mapango milele, pundamwitu watapitapita huko kwa furaha, kondoo watapata malisho yao humo.

15 Hali itaendelea kuwa hivyo mpaka tumiminiwe roho ya Mungu kutoka juu. Hapo jangwa litakuwa shamba la rutuba tena, na mashamba ya rutuba yatakuwa msitu.

16 Haki itadumu katika nchi iliyokuwa nyika, uadilifu utatawala katika mashamba yenye rutuba.

17 Kutokana na uadilifu watu watapata amani, utulivu na usalama utadumu milele.

18 Watu wangu watakaa katika makao ya amani, katika maskani salama na mazingira matulivu.

19 Msitu wa adui utatoweka kabisa, na mji wake utaangamizwa.

20 Lakini heri yenu nyinyi: Mtapanda mbegu zenu popote penye maji, ng'ombe na punda wenu watatembeatembea watakavyo.

33

1 Ole wako ewe mwangamizi, unayeangamiza bila wewe kuangamizwa! Ole wako wewe mtenda hila, ambaye hakuna aliyekutendea hila! Utakapokwisha kuangamiza wewe utaangamizwa! Utakapomaliza kuwatendea watu hila wewe utatendewa hila.

2 Ee Mwenyezi-Mungu, utuonee huruma, kwako tumeliweka tumaini letu. Uwe kinga yetu kila siku, wokovu wetu wakati wa taabu.

3 Kwa kishindo cha sauti yako watu hukimbia; unapoinuka tu, mataifa hutawanyika.

4 Maadui zao wanakusanya mateka, wanayarukia kama panzi.

5 Mwenyezi-Mungu ametukuka, yeye anaishi juu mbinguni. Ameujaza Siyoni haki na uadilifu.

6 Enyi watu wa Yerusalemu, Mwenyezi-Mungu atawajalieni usalama, atawaokoa na kuwapa hekima na maarifa. Hazina yenu kuu ni kumcha Mwenyezi-Mungu.

7 Haya, mashujaa wao wanalia, wajumbe wa amani wanaomboleza.

8 Barabara kuu zimebaki tupu; hamna anayesafiri kupitia humo. Mikataba inavunjwa ovyo, mashahidi wanadharauliwa. Hamna anayejali tena maisha ya binadamu.

9 Nchi inaomboleza na kunyauka; misitu ya Lebanoni imekauka, bonde zuri la Sharoni limekuwa jangwa, huko Bashani na mlimani Karmeli miti imepukutika majani yake.

10 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Sasa mimi nitainuka; sasa nitajiweka tayari; sasa mimi nitatukuzwa.

11 Mipango yenu yote ni kama makapi, na matokeo yake ni takataka tupu. Pumzi yangu itawaangamiza kama moto.

12 Watu watakuwa kama wamechomwa kuwa majivu, kama miiba iliyokatwa na kuteketezwa motoni.

13 Sikilizeni mambo mliyofanya enyi mlio mbali, nanyi mlio karibu kirini uwezo wangu.”

14 Wenye dhambi katika Siyoni wanaogopa, wasiomcha Mungu wanatetemeka na kusema: “Nani awezaye kuukaribia moto huu mkali? Nani awezaye kustahimili miali ya moto wa milele?”

15 Ni mtu aishiye kwa uadilifu na asemaye ukweli; mtu anayedharau kabisa utajiri wa dhuluma, anayekataa hongo kata kata, asiyekubali kamwe kusikia mipango ya mauaji, wala hakubali macho yake yaone maovu.

16 Mtu wa namna hiyo anaishi juu, mahali salama penye ngome na miamba; chakula chake atapewa daima, na maji yake ya kunywa hayatakosekana.

17 Mtaweza kumwona mfalme katika fahari yake, mtaiona nchi anayotawala, kubwa na pana.

18 Mtafikiria tisho lililopita na kujiuliza, “Wako wapi wale waliokadiria na kukisia kodi? Wako wapi wale waliopeleleza ulinzi wetu?”

19 Hamtawaona tena watu wale wenye kiburi, wanaozungumza lugha isiyoeleweka.

20 Tazameni Siyoni tunamofanya sikukuu zetu; tazameni mji Yerusalemu, makao matulivu, hema imara; vigingi vyake havitangolewa kamwe, kamba zake hazitakatwa hata moja.

21 Humo Mwenyezi-Mungu atatuonesha ukuu wake. Kutakuwa na mito mikubwa na vijito, ambamo meli za vita hazitapita, wala meli kubwa kuingia.

22 Maana Mwenyezi-Mungu ni hakimu wetu, yeye ni mtawala wetu; Mwenyezi-Mungu ni mfalme wetu, yeye ndiye anayetuokoa.

23 Ewe Siyoni, kamba zako zimelegea, haziwezi kushikilia matanga yake, wala kuyatandaza. Lakini nyara nyingi zitagawanywa; hata vilema wataweza kuchukua sehemu yao.

24 Hakuna atakayesema tena ni mgonjwa; watu watasamehewa uovu wao wote.

34

1 Karibieni mkasikilize enyi mataifa, tegeni sikio enyi watu. Sikiliza ee dunia na vyote vilivyomo, ulimwengu na vyote vitokavyo humo!

2 Mwenyezi-Mungu ameyakasirikia mataifa yote, ameghadhabika dhidi ya majeshi yao yote. Ameyapangia mwisho wao, ameyatoa yaangamizwe.

3 Maiti zao zitatupwa nje; harufu ya maiti zao itasambaa; milima itatiririka damu yao.

4 Jeshi lote la angani litaharibika, anga zitakunjamana kama karatasi. Jeshi lake lote litanyauka, kama majani ya mzabibu yanyaukavyo, naam, kama tunda la mtini linyaukavyo.

5 Upanga wa Mungu uko tayari juu mbinguni. Tazama, washuka kuwaadhibu Waedomu, watu ambao ameamua kuwaangamiza.

6 Upanga utalowa damu na kutapakaa mafuta, kama kwa damu ya kondoo na mbuzi, na mafuta ya figo za kondoo dume. Maana Mwenyezi-Mungu atatoa kafara huko Bosra, kutakuwa na mauaji makubwa nchini Edomu.

7 Nyati wataangamia pamoja nao, ndama kadhalika na mafahali. Nchi italoweshwa damu, udongo utarutubika kwa mafuta yao.

8 Maana Mwenyezi-Mungu anayo siku ya kisasi; mwaka wa kulipiza maadui wa Siyoni.

9 Vijito vya Edomu vitatiririka lami, udongo wake utakuwa madini ya kiberiti; ardhi yake itakuwa lami iwakayo.

10 Itawaka usiku na mchana bila kuzimika, moshi wake utafuka juu milele. Nchi itakuwa jangwa siku zote, hakuna atakayepitia huko milele.

11 Itakuwa makao ya kozi na nungunungu, bundi na kunguru wataishi humo. Mwenyezi-Mungu atawaletea ghasia, na timazi la fujo kwa wakuu wake.

12 Nchi itaitwa “Nchi bila Mfalme;” wakuu wake wote wametoweka.

13 Miiba itaota katika ngome zake, viwavi na michongoma mabomani mwao. Itakuwa makao ya mbwamwitu, maskani yao mbuni.

14 Pakamwitu na fisi watakuwa humo, majini yataitana humo; kwao usiku utakuwa mwanga, na humo watapata mahali pa kupumzikia.

15 Humo bundi watataga mayai na kuyaatamia, wataangua vifaranga na kuviweka kivulini mwao. Humo vipanga watakutania, kila mmoja na mwenzake.

16 Someni katika kitabu cha Mwenyezi-Mungu: “Hakuna hata kiumbe kimoja kitakachokosekana, kila kimoja kitakuwako na mwenzake.” Maana Mwenyezi-Mungu mwenyewe ametamka hivyo, roho yake itawakusanya hao wote.

17 Mwenyezi-Mungu amepanga sehemu ya kila mmoja wao, ametumia kamba kuwapimia nchi hiyo; wataimiliki milele na milele, wataishi humo kizazi hata kizazi.

35

1 Nyika na nchi kavu vitachangamka, jangwa litafurahi na kuchanua maua.

2 Litachanua maua kwa wingi kama waridi, litashangilia na kuimba kwa furaha. Mungu atalijalia fahari ya milima ya Lebanoni, uzuri wa mlima Karmeli na wa bonde la Sharoni. Watu watauona utukufu wa Mwenyezi-Mungu, watauona ukuu wa Mungu wetu.

3 Imarisheni mikono yenu dhaifu, kazeni magoti yenu manyonge.

4 Waambieni waliokufa moyo: “Jipeni moyo, msiogope! Tazameni Mungu wenu atakuja kulipiza kisasi, atakuja kuwaadhibu maadui zenu; atakuja yeye mwenyewe kuwaokoeni.”

5 Hapo vipofu wataona tena, na viziwi watasikia tena.

6 Walemavu watarukaruka kama paa, na bubu wataimba kwa furaha. Maji yatabubujika nyikani na vijito vya maji jangwani.

7 Mchanga wa moto jangwani utakuwa bwawa la maji, ardhi kavu itabubujika vijito vya maji. Makao ya mbwamwitu yatajaa maji; nyasi zitamea na kukua kama mianzi.

8 Humo kutakuwa na barabara kuu, nayo itaitwa “Njia Takatifu.” Watu najisi hawatapitia humo, ila tu watu wake Mungu; wapumbavu hawatadiriki kuikanyaga,

9 humo hakutakuwa na simba, mnyama yeyote mkali hatapitia humo, hao hawatapatikana humo. Lakini waliokombolewa ndio watakaopita humo.

10 Waliokombolewa na Mwenyezi-Mungu watarudi, watakuja Siyoni wakipiga vigelegele. Watakuwa wenye furaha ya milele, watajaliwa furaha na shangwe; huzuni na kilio vitatoweka kabisa.

36

1 Mnamo mwaka wa kumi na nne wa utawala wa mfalme Hezekia, mfalme Senakeribu wa Ashuru aliishambulia miji yote yenye ngome ya Yuda na kuiteka.

2 Kisha mfalme wa Ashuru alimtuma jemadari mkuu kutoka Lakishi na jeshi kubwa kumwendea mfalme Hezekia. Jemadari alisimama karibu na mfereji wa bwawa lililoko upande wa juu katika barabara kuu inayoelekea uwanda wa Dobi.

3 Nao walilakiwa na Eliakimu mwana wa Hilkia, aliyekuwa msimamizi wa ikulu, Shebna aliyekuwa katibu, pamoja na mwandishi Yoa mwana wa Asafu.

4 Ndipo mkuu wa matowashi wa Ashuru alipowaambia, “Mwambieni Hezekia kuwa mfalme mkuu wa Ashuru anamwuliza, ‘Je, unategemea nini kwa ukaidi wako huo?

5 Je, unadhani kuwa maneno matupu ndiyo maarifa na nguvu katika vita? Ni nani unayemtegemea hata ukaniasi?

6 Angalia! Sasa unategemea Misri, utete uliovunjika ambao utamchoma mkono yeyote atakayeuegemea. Hivyo ndivyo Farao, mfalme wa Misri alivyo, kwa wote wale wanaomtegemea.’

7 Lakini hata kama mkiniambia, ‘Tunamtegemea Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu,’ je, si huyohuyo ambaye Hezekia aliziharibu madhabahu zake na kuwaambia watu wa Yuda na Yerusalemu, ‘Mnapaswa kuabudu mbele ya madhabahu hii?’

8 Basi, fanyeni mkataba na bwana wangu mfalme wa Ashuru; mimi nitawapatieni farasi 2,000, kama mtaweza kupata wapandafarasi.

9 Mwawezaje kumrudisha nyuma ofisa mmoja kati ya watumishi wa bwana wangu aliye na cheo cha chini sana wakati mnategemea Misri kupata magari ya vita na wapandafarasi!

10 Zaidi ya hayo, je, mnafikiri nimekuja bila amri ya Mwenyezi-Mungu ili kuishambulia na kuiangamiza nchi hii? Mwenyezi-Mungu ndiye aliyeniambia ‘Ishambulie nchi hii na kuiangamiza!’”

11 Kisha Eliakimu, Shebna na Yoa wakamjibu mkuu wa matowashi, “Tafadhali sema nasi kwa lugha ya Kiaramu maana tunaielewa. Usiseme nasi kwa lugha ya Kiebrania kwa kuwa watu walioko ukutani wanasikia.”

12 Yule mkuu wa matowashi akawaambia, “Je unadhani bwana wangu amenituma kutoa ujumbe huu kwa bwana wenu na kwenu wenyewe tu? Maneno yangu ni pia kwa watu wanaokaa ukutani! Muda si muda wao kama vile nyinyi itawabidi kula mavi yao wenyewe na kunywa mikojo yao wenyewe!”

13 Kisha huyo mkuu wa matowashi akasimama, akapaza sauti na kusema kwa Kiebrania, “Sikilizeni maneno ya mfalme mkuu, mfalme wa Ashuru!

14 Hiki ndicho anachosema mfalme: Msikubali Hezekia awadanganye, kwa sababu hataweza kuwaokoa.

15 Msikubali awashawishi ili mumtegemee Mwenyezi-Mungu akisema, ‘Mwenyezi-Mungu hakika atatuokoa na mji huu hautatiwa mkononi mwa mfalme wa Ashuru.’

16 Msimsikilize Hezekia; maana mfalme wa Ashuru anasema: ‘Muwe na amani nami, na kujisalimisha kwangu. Hapo kila mmoja wenu ataweza kula matunda ya mzabibu wake mwenyewe na ya matunda ya mtini wake mwenyewe na kunywa maji ya kisima chake mwenyewe.

17 Mpaka baadaye nitakapokuja na kuwapelekeni katika nchi kama hii yenu; nchi yenye nafaka na divai, nchi yenye mkate na mashamba ya mizabibu.’

18 Angalieni basi Hezekia asiwahadae akisema kwamba Mwenyezi-Mungu atawaokoeni. Je, kuna yoyote kati ya miungu ya mataifa aliyewahi kuokoa nchi yake mkononi mwa mfalme wa Ashuru?

19 Je, iko wapi miungu ya Hamathi na Arpadi? Iko wapi miungu ya Sefarvaimu? Je, imeokoa Samaria mkononi mwangu?

20 Ni nani miongoni mwa miungu ya nchi hizi aliyeokoa nchi zao katika mkono wangu, hata iwe kwamba Mwenyezi-Mungu ataweza kuuokoa mji wa Yerusalemu mkononi mwangu?”

21 Lakini watu walinyamaza, wala hawakumjibu neno kama vile walivyoamriwa na mfalme akisema, “Msimjibu.”

22 Kisha Eliakimu mwana wa Hilkia aliyekuwa mkuu wa ikulu, katibu Shebna, na Yoa mwana wa Asafu mwandishi, wakamwendea mfalme Hezekia huku mavazi yao yakiwa yameraruliwa, wakamweleza maneno ya mkuu wa matowashi.

37

1 Basi, mfalme Hezekia aliposikia habari hiyo alirarua mavazi yake, akavaa vazi la gunia, akaingia katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu.

2 Aliwaamuru Eliakimu, mkuu wa ikulu, Shebna, katibu, na wazee wa makuhani, wamwendee nabii Isaya mwana wa Amozi, wakiwa wamevaa mavazi ya magunia.

3 Nao wakamwambia Isaya, “Hezekia anasema hivi, ‘Leo ni siku ya huzuni, siku ya kukemewa, na ya dharau. Sisi tumekuwa kama mama anayetaka kujifungua mtoto, lakini hana nguvu ya kumzaa.

4 Inawezekana kwamba Mwenyezi-Mungu, Mungu wako alisikia maneno ya mkuu wa matowashi ambaye ametumwa na mfalme wa Ashuru, bwana wake, ili kumtukana Mungu aliye hai, naye Mwenyezi-Mungu, Mungu wako atapinga maneno aliyoyasikia; kwa hiyo waombee watu waliobaki.’”

5 Basi, hao watumishi wa mfalme Hezekia walipokwisha fika kwa Isaya,

6 yeye akawaambia, “Mwambieni bwana wenu kwamba Mwenyezi-Mungu asema hivi: ‘Usiogope kwa sababu ya maneno ya watumishi wa mfalme wa Ashuru uliyoyasikia, maneno ambayo wameyasema kunidharau.

7 Tazama nitamfanya mfalme asikie uvumi halafu atarudi katika nchi yake, na huko nitamfanya auawe kwa upanga.’”

8 Kisha yule mkuu wa matowashi aliposikia kwamba mfalme wa Ashuru alikuwa ameondoka Lakishi, aliondoka na kumkuta akishambulia mji wa Libna.

9 Halafu aliposikia habari kwamba Tirhaka mfalme wa Kushi anakuja kupigana naye, alituma wajumbe kwa Hezekia, akisema,

10 “Mwambieni Hezekia mfalme wa Yuda: ‘Usikubali Mungu wako unayemtegemea akudanganye kwa kukuahidi kwamba Yerusalemu hautatekwa na mfalme wa Ashuru.

11 Wewe umekwisha sikia jinsi wafalme wa Ashuru walivyozitenda nchi nyingine na kuziangamiza kabisa. Je, unadhani wewe utaokoka?

12 Je, miungu ya mataifa iliokoa Gozani, Harani, Resefu na Waedeni waliokaa Telasari, mataifa ambayo wazee wangu waliyaangamiza?

13 Wako wapi wafalme wa Hamathi, Arpadi, Sefarvaimu, Hena na Iva?’”

14 Mfalme Hezekia alipokea barua kutoka kwa wajumbe na kuisoma. Kisha akaenda na kuingia katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu, akaiweka mbele ya Mwenyezi-Mungu.

15 Halafu akamwomba Mwenyezi-Mungu akisema;

16 “Ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, unayeketi katika kiti cha enzi juu ya viumbe wenye mabawa. Wewe ndiwe uliyeumba mbingu na dunia.

17 Ee, Mwenyezi-Mungu, fumbua macho uone, tega sikio lako, uyasikie matusi yote ambayo Senakeribu amepeleka na kukutukana wewe Mungu uliye hai.

18 Ee Mwenyezi-Mungu, ni kweli kwamba wafalme wa Ashuru wameangamiza mataifa yote na nchi zao.

19 Waliweza kuitupa miungu yao motoni, kwa sababu haikuwa miungu kweli bali sanamu za miti au mawe zilizochongwa na mikono ya watu.

20 Sasa ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, utuokoe makuchani mwa Senakeribu, ili falme zote za dunia zijue kwamba wewe peke yako ndiwe uliye Mwenyezi-Mungu.”

21 Kisha Isaya mwana na Amozi, alituma ujumbe kwa Hezekia akisema, “Hivi ndivyo anavyosema Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli: Kwa kuwa umeniomba kuhusu Senakeribu mfalme wa Ashuru,

22 basi huu ndio ujumbe wangu kuhusu huyo mfalme: Mji wa Siyoni, naam, Yerusalemu, unakudharau na kukutukana. Yerusalemu, mji mzuri unakutikisia kichwa kwa dhihaka.

23 Wewe umemtukana nani? Umemkashifu nani? Umethubutu kumbeza nani kwa majivuno? Ni mimi Mungu, Mtakatifu wa Israeli!

24 Umewatumia watumishi wako kunidhihaki mimi Bwana; wewe umesema, ‘Kwa magari yangu mengi ya vita, nimekwea vilele vya milima, mpaka kilele cha Lebanoni. Nimeangusha mierezi yake mirefu, na misonobari mizurimizuri. Nimevifikia vilele vyake na ndani ya misitu yake mikubwa.

25 Nimechimba visima na kunywa maji yake, na nilikausha vijito vya Misri kwa nyayo za miguu yangu.’

26 “Je, hujasikia ewe Senakeribu kwamba nilipanga jambo hili tangu zamani? Ninachotekeleza sasa nilikipanga zamani. Nilikuweka uifanye miji yenye ngome kuwa rundo la magofu.

27 Wakazi wake wakiwa wameishiwa nguvu, wametishika na kufadhaika. Wamekuwa kama mimea shambani, kama nyasi changa shambani, kama majani yaotayo juu ya paa au kama ngano kabla hazijakomaa ambazo hunyauka upepo mkavu uvumapo.

28 Lakini, nakujua wewe Senakeribu; najua kila unachofanya na kuacha kufanya; najua mipango yako dhidi yangu.

29 Kwa vile umefanya mipango dhidi yangu na nimeusikia ufidhuli wako, nitatia ndoana yangu puani mwako, na lijamu yangu kinywani mwako. Nitakurudisha njia ileile uliyojia.”

30 “Na hii ndiyo itakuwa ishara kwako Hezekia: Mwaka huu na mwaka ujao mtakula kinachomea chenyewe bila kupandwa. Lakini katika mwaka wa tatu mtapanda na kuvuna mavuno; mtapanda mizabibu na kula matunda yake.

31 Wale watakaobaki katika ukoo wa Yuda wataongezeka na kuwa wengi kama vile mti unavyotoa mizizi yake udongoni na kuzaa matunda juu.

32 Maana kutakuwa na watu watakaosalia huko Yerusalemu; naam, huko mlimani Siyoni kutakuwako watu wachache watakaosalimika.” Mwenyezi-Mungu wa majeshi amedhamiria kukamilisha hayo.

33 Mwenyezi-Mungu asema hivi juu ya mfalme wa Ashuru: “Hataingia katika mji huu, wala kuupiga mshale wala kuingia kwa ngao wala kuuzingira.

34 Atarudi kwa njia ileile aliyojia na wala hataingia katika mji huu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimetamka hayo.

35 Naam, kwa ajili ya heshima yangu mimi na kwa ajili ya mtumishi wangu Daudi nitaulinda na kuuokoa mji huu.”

36 Basi, wakati wa usiku malaika wa Mwenyezi-Mungu aliingia kambini mwa Waashuru na kuwaua watu 185,000. Halafu kulipopambazuka watu hao wote walionekana wakiwa maiti.

37 Kisha Senakeribu mfalme wa Ashuru akaondoka, akaenda kwake, akakaa Ninewi.

38 Siku moja, wakati Senakeribu alipokuwa akiabudu katika nyumba ya Nisroki mungu wake, wanawe wawili, Adrameleki na Sharezeri, walimuua kwa upanga, halafu wakakimbilia nchini Ararati. Naye Esar-hadoni, mwanawe, akatawala badala yake.

38

1 Wakati huo, mfalme Hezekia aliugua sana karibu kufa. Ndipo nabii Isaya mwana wa Amozi, akamwendea, akamwambia, “Hivi ndivyo anavyosema Mwenyezi-Mungu: Panga mambo yako sawasawa katika nyumba yako kwa kuwa utakufa, hutapona.”

2 Hezekia akageukia upande wa ukuta na kumwomba Mwenyezi-Mungu,

3 akisema, “Ee Mwenyezi-Mungu, nakusihi ukumbuke jinsi nilivyokutumikia kwa uaminifu na kwa moyo wangu wote, na kutenda yaliyo sawa mbele yako.” Hezekia akalia kwa uchungu sana.

4 Kisha neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Isaya:

5 “Nenda ukamwambie Hezekia, Mwenyezi-Mungu, Mungu wa baba yako Daudi, anasema hivi: Nimesikia ombi lako na nimeyaona machozi yako. Basi, nakuongezea miaka kumi na mitano ya kuishi.

6 Nitakuokoa wewe pamoja na mji huu mikononi mwa mfalme wa Ashuru na kuulinda.”

7 Isaya akamjibu, “Hii itakuwa ishara kwako kutoka kwa Mwenyezi-Mungu kwamba Mwenyezi-Mungu atafanya kama alivyoahidi.

8 Nitafanya kivuli kwenye ngazi iliyojengwa na Ahazi, kirudi nyuma hatua kumi.” Nacho kivuli kikarudi nyuma hatua kumi.

9 Kisha mfalme Hezekia alipopona, akatunga wimbo huu wa shukrani:

10 “Nilisema: Nikiwa mbichi kabisa, inanibidi niage dunia. Mimi nimepangiwa kwenda kuzimu siku zote zilizonibakia.

11 Nilisema sitamwona tena Mwenyezi-Mungu, katika nchi ya walio hai; wala sitamwona mtu yeyote tena, miongoni mwa wakazi wa ulimwengu.

12 Makao yangu yamengolewa kwangu, kama hema la mchungaji; kama, mfumanguo nimefungasha maisha yangu; Mungu amenikatilia mbali; kabla hata mwisho wa siku amenikomesha.

13 Usiku kucha nililia kuomba msaada; kama simba, anavunjavunja mifupa yangu; mchana na usiku ananikomesha.

14 “Ninalia kama mbayuwayu, nasononeka kama njiwa. Macho yangu yamefifia kwa kuangalia juu. Ee Bwana, nateseka; uwe wewe usalama wangu!

15 Lakini niseme nini: Yeye mwenyewe aliniambia, naye mwenyewe ametenda hayo. Usingizi wangu wote umenitoroka kwa sababu ya uchungu moyoni mwangu.

16 “Ee Bwana, Sisi twaishi kutokana na yote uliyotenda, kwa hayo yote mimi binafsi pia ninaishi. Nirudishie afya, uniwezeshe kuishi.

17 Nilipata mateso makali kwa faida yangu; lakini umeyaokoa maisha yangu kutoka shimo la uharibifu, maana umezitupa dhambi zangu nyuma yako.

18 Huko kuzimu mtu hawezi kukushukuru wewe; waliokufa hawawezi kukushukuru wewe. Wala washukao huko shimoni hawawezi tena kutumainia uaminifu wako.

19 Walio hai ndio wanaokushukuru, kama na mimi ninavyofanya leo. Kina baba huwajulisha watoto wao uaminifu wako.

20 “Mwenyezi-Mungu ataniokoa. Nasi tutamsifu kwa nyimbo za vinubi siku zote za maisha yetu, nyumbani kwake Mwenyezi-Mungu.”

39

1 Wakati huo, mfalme Merodak-baladani mwana wa Baladani, mfalme wa Babuloni, aliposikia kwamba Hezekia alikuwa ameugua na sasa amepona, alimtumia ujumbe pamoja na zawadi.

2 Basi, Hezekia aliwakaribisha na kuwaonesha nyumba ya hazina: Fedha, dhahabu, viungo vya kukolezea chakula, mafuta ya thamani, vifaa vyake vyote vya kijeshi na vitu vyote vilivyokuwamo katika bohari zake. Hakuna chochote katika ikulu yake au katika nchi yake ambacho hakuwaonesha.

3 Ndipo nabii Isaya alipokwenda kwa mfalme Hezekia na kumwuliza, “Watu hawa wamesema nini? Na, wamekujia kutoka wapi?” Naye Hezekia akamjibu “Wamenijia kutoka nchi ya mbali, huko Babuloni.”

4 Halafu Isaya akamwuliza, “Wameona nini katika ikulu yako?” Hezekia akamjibu, “Wameona yote yaliyomo katika ikulu yangu. Hakuna chochote katika bohari zangu ambacho sikuwaonesha.”

5 Ndipo Isaya akamwambia Hezekia, “Sikia neno la Mwenyezi-Mungu wa majeshi:

6 Tazama, siku zinakuja ambapo vyote vilivyomo nyumbani mwako na vitu vyote walivyokusanya wazee wako hadi leo, vitapelekwa mpaka Babuloni. Hakuna kitu chochote kitakachobaki; ndivyo asemavyo Mwenyezi-Mungu.

7 Tena baadhi ya watoto wako mwenyewe wa kiume watapelekwa mateka nao watakuwa matowashi katika ikulu ya mfalme wa Babuloni.”

8 Naye Hezekia akamwambia Isaya, “Neno la Mwenyezi-Mungu ulilosema ni sawa.” Alisema hivyo kwani alifikiri, “Kutakuwa na amani na usalama muda wote niishipo.”

40

1 Mungu wenu asema: “Wafarijini watu wangu, nendeni mkawafariji.

2 Semeni na wenyeji wa Yerusalemu kwa upole, waambieni kwamba utumwa wao umekwisha, wamesamehewa uovu wao. Mwenyezi-Mungu amewaadhibu maradufu kwa sababu ya dhambi zao zote.”

3 Sauti ya mtu anaita jangwani: “Mtayarishieni Mwenyezi-Mungu njia, nyosheni barabara kuu kwa ajili ya Mungu wetu.

4 Kila bonde litasawazishwa, kila mlima na kilima vitashushwa; ardhi isiyo sawa itafanywa sawa, mahali pa kuparuza patalainishwa.

5 Kisha utukufu wa Mwenyezi-Mungu utafunuliwa, na watu wote pamoja watauona. Mwenyezi-Mungu mwenyewe ametamka hayo.”

6 Sikiliza! Kuna sauti inasema, “Tangaza!” Nami nikauliza, “Nitangaze nini?” Naye: “Tangaza: Binadamu wote ni kama majani; uthabiti wao ni kama ua la shambani.

7 Majani hunyauka na ua hufifia, Mwenyezi-Mungu avumishapo upepo juu yake. Hakika binadamu ni kama majani.

8 Majani hunyauka na ua hufifia, lakini neno la Mungu wetu ladumu milele.”

9 Nenda juu ya mlima mrefu, ewe Siyoni, ukatangaze habari njema. Paza sauti yako kwa nguvu, ewe Yerusalemu, ukatangaze habari njema. paza sauti yako bila kuogopa. Iambie miji ya Yuda: “Mungu wenu anakuja.”

10 Bwana Mungu anakuja na nguvu, kwa mkono wake anatawala. Zawadi yake iko pamoja naye, na tuzo lake analo.

11 Atalilisha kundi lake kama mchungaji, atawakusanya wanakondoo mikononi mwake, atawabeba kifuani pake, na kondoo wanyonyeshao atawaongoza polepole.

12 Nani awezaye kupima maji ya bahari kwa konzi yake, kuzipima mbingu kwa mikono yake? Nani awezaye kuutia udongo wa dunia kikombeni; kuipima milima kwa mizani au vilima kwa kipimo cha uzani?

13 Nani awezaye kuiongoza akili ya Mwenyezi-Mungu, au kuwa mshauri wake na kumfunza?

14 Mwenyezi-Mungu alimtaka nani shauri, ndipo akapata kuwa mwenye ujuzi? Nani aliyemfunza njia za haki? Nani aliyemfundisha maarifa, na kumwonesha namna ya kuwa na akili?

15 Kwake mataifa ni kama tone la maji katika ndoo, ni kama vumbi juu ya mizani. Kwake visiwa ni vyepesi kama vumbi laini.

16 Kuni zote za Lebanoni na wanyama wake wote havitoshi kwa sadaka ya kuteketezwa mbele yake.

17 Mataifa yote si kitu mbele yake; kwake ni vitu duni kabisa na batili.

18 Mtamlinganisha Mungu na nini basi, au ni kitu gani cha kumfananisha naye?

19 Je, anafanana na kinyago? Hicho, fundi hukichonga, mfua dhahabu akakipaka dhahabu, na kukitengenezea minyororo ya fedha!

20 Au ni sanamu ya mti mgumu? Hiyo ni ukuni mtu anaochagua, akamtafuta fundi stadi, naye akamchongea sanamu imara!

21 Je, nyinyi bado hamjui? Je, hamjapata kusikia? Je, hamkuambiwa tangu mwanzo? Je, hamjafahamu mwanzo wa dunia?

22 Dunia iliumbwa na huyo aketiye juu ya mbingu; kutoka huko wakazi wa dunia ni kama panzi! Yeye amezitandaza mbingu kama pazia, na kuzikunjua kama hema la kuishi.

23 Yeye huwaporomosha wakuu wenye nguvu, watawala wa dunia huwafanya kuwa si kitu.

24 Mara tu wanaposimikwa na kuanza kuota, hata kabla hawajatoa mizizi kama miti udongoni, Mwenyezi-Mungu akiwapulizia hunyauka, kimbunga huwapeperusha kama makapi!

25 Mungu Mtakatifu auliza hivi: “Nani basi, mtakayemlinganisha nami? Je, kuna mtu aliye kama mimi?”

26 Inueni macho yenu juu mbinguni! Je, ni nani aliyeziumba nyota hizo? Ni yule aziongozaye kama jeshi lake, anayeijua idadi yake yote, aziitaye kila moja kwa jina lake. Kwa sababu yeye ni mwenye nguvu nyingi, hakuna hata moja inayokosekana.

27 Enyi watu wa Israeli wazawa wa Yakobo, kwa nini mnalalamika na kusema: “Mwenyezi-Mungu hatujali sisi! Mungu wetu hajali haki yetu!”

28 Je, nyinyi bado hamjui? Je, hamjapata kusikia? Mwenyezi-Mungu ndiye Mungu wa milele; yeye ndiye Muumba wa kila kitu duniani. Yeye hafifii kamwe wala kuishiwa nguvu. Maarifa yake hayachunguziki.

29 Yeye huwapa uwezo walio hafifu, wanyonge huwapa nguvu.

30 Hata vijana watafifia na kulegea; naam, wataanguka kwa uchovu.

31 Lakini wote wanaomtumainia Mwenyezi-Mungu, watapata nguvu mpya. Watapanda juu kwa mabawa kama tai; watakimbia bila kuchoka; watatembea bila kulegea.

41

1 Mungu asema hivi: “Enyi wakazi wa mbali nyamazeni mnisikilize! Enyi mataifa jipeni nguvu; jitokezeni mkatoe hoja zenu, na tuje pamoja kwa hukumu.

2 “Nani, ila mimi, aliyemwita shujaa toka mashariki, mtu ambaye hupata ushindi popote aendako? Mimi huyatia mataifa makuchani mwake, naye huwaponda wafalme chini ya miguu yake! Upanga wake huwafanya kuwa kama vumbi, kwa upinde wake huwapeperusha kama makapi.

3 Yeye huwafuatia na kupita salama; huenda kasi kana kwamba hagusi chini.

4 Nani aliyefanya yote haya yatendeke? Ni nani aliyepanga wakati wa kila tukio? Mimi Mwenyezi-Mungu nipo tangu mwanzo, mimi nitakuwapo hata milele.

5 “Wakazi wa mbali wameona niliyotenda, wakaogopa; dunia yote inatetemeka kwa hofu. Watu wote wamekusanyika, wakaja.

6 Kila mmoja anamhimiza mwenzake akisema, ‘Haya! Jipe moyo!’

7 Fundi anamhimiza mfua dhahabu, naye alainishaye sanamu kwa nyundo, anamhimiza anayeiunga kwa misumari. Wote wanasema, ‘Imeungika vizuri sana!’ Kisha wanaifunga kwa misumari isitikisike.

8 “Sikiliza ewe Israeli, mtumishi wangu, wewe, Yakobo ambaye nimekuchagua, wewe mzawa wa Abrahamu, rafiki yangu;

9 wewe niliyekuleta toka miisho ya dunia, wewe niliyekuambia: ‘Wewe u mtumishi wangu; mimi sikukutupa, bali nilikuchagua.’

10 Basi, usiogope, mimi nipo pamoja nawe. Usifadhaike, mimi ni Mungu wako. Nitakuimarisha na kukusaidia; nitakulinda kwa mkono wangu wa ushindi.

11 “Naam! Wote waliokuwakia hasira, wataaibishwa na kupata fedheha. Wote wanaopingana nawe, watakuwa si kitu na kuangamia.

12 Utawatafuta hao wanaopingana nawe, lakini watakuwa wameangamia.

13 Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, ndimi ninayetegemeza mkono wako. Mimi ndimi ninayekuambia: ‘Usiogope, nitakusaidia.’”

14 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Enyi watu wa Yakobo dhaifu kama mdudu, enyi Waisraeli, msiogope! Mimi Mwenyezi-Mungu nasema nitawasaidia. Mimi ni Mkombozi wenu, Mtakatifu wa Israeli.

15 Nitawafanya muwe kama chombo cha kupuria, chenye meno mapya na makali. Mtaipura milima na kuipondaponda; vilima mtavisagasaga kama makapi.

16 Mtaipepeta milima hiyo, nao upepo utaipeperushia mbali, naam, dhoruba itaitawanya huko na huko. Nanyi mtafurahi kwa sababu yangu Mwenyezi-Mungu; mtaona fahari kwa sababu yangu Mungu Mtakatifu wa Israeli.

17 “Maskini na fukara wakitafuta maji wasipate, wakiwa wamekauka koo kwa kiu, mimi Mwenyezi-Mungu nitawajibu; mimi Mungu wa Israeli, sitawaacha.

18 Nitabubujisha mito kwenye milima mikavu, na chemchemi katika mabonde. Nitaigeuza nyika kuwa bwawa la maji, na nchi kame kuwa chemchemi za maji.

19 Nitapanda miti huko nyikani: Mierezi, mikakaya, mijohoro, na mizeituni; nitaweka huko jangwani: Miberoshi, mivinje na misonobari.

20 Watu wataona jambo hilo, nao watatambua na kuelewa kwamba mimi Mwenyezi-Mungu nimetenda hayo, mimi Mtakatifu wa Israeli nimefanya jambo hilo.”

21 Mwenyezi-Mungu, Mfalme wa Yakobo, asema: “Enyi miungu ya mataifa, njoni mtoe hoja zenu!

22 Leteni hoja zenu, mtuambie yatakayotukia. Tuambieni matukio ya kwanza yalikuwa yapi nasi tutayatafakari moyoni. Au tutangazieni yajayo, tujue yatakayokuja.

23 Tuambieni yatakayotokea baadaye, nasi tujue basi kama nyinyi ni miungu. Fanyeni kitu chochote, chema au kibaya, ili tutishike na kuogopa.

24 Hakika, nyinyi si kitu kabisa. hamwezi kufanya chochote kile. Anayechagua kuwaabudu nyinyi ni chukizo.

25 “Nimechochea mtu toka kaskazini, naye amekuja; naam, nimemchagua mtu toka mashariki, naye atalitamka jina langu. Yeye atawakanyaga wafalme kama tope, kama vile mfinyanzi apondavyo udongo wake.

26 Nani aliyebashiri haya tangu mwanzo, hata sisi tupate kuyatambua? Nani aliyetangulia kuyatangaza, ili sasa tuseme, alisema ukweli? Hakuna hata mmoja wenu aliyeyataja, wala hakuna aliyesikia maneno yenu.

27 Mimi ni yule wa kwanza, niliyetangaza kwa Siyoni, nikapeleka Yerusalemu mjumbe wa habari njema.

28 Nimeangalia kwa makini sana, lakini simwoni yeyote yule; hamna yeyote kati ya hao miungu awezaye kushauri; nikiuliza hakuna awezaye kunijibu.

29 La! Miungu hiyo yote ni udanganyifu, haiwezi kufanya chochote; sanamu zao za kusubu ni upuuzi.

42

1 “Tazameni mtumishi wangu ninayemtegemeza; mteule wangu ambaye moyo wangu umependezwa naye. Nimeiweka roho yangu juu yake, naye atayaletea mataifa haki.

2 Hatalia wala hatapiga kelele, wala hatapaza sauti yake barabarani.

3 Mwanzi uliochubuka hatauvunja, utambi ufukao moshi hatauzima; ataleta haki kwa uaminifu.

4 Yeye hatafifia wala kufa moyo, hata atakapoimarisha haki duniani. Watu wa mbali wanangojea mwongozo wake.”

5 Hivi ndivyo asemavyo Mwenyezi-Mungu aliyeziumba mbingu, akazitandaza kama hema, yeye aliyeiunda nchi na vyote vilivyomo, yeye awapaye watu waliomo pumzi, na kuwajalia uhai wote waishio humo:

6 “Mimi Mwenyezi-Mungu nimekuita kutenda haki, nimekushika mkono na kukulinda. Kwa njia yako nitaweka ahadi na watu wote, wewe utakuwa mwanga wa mataifa.

7 Utayafumbua macho ya vipofu, utawatoa wafungwa gerezani, waliokaa gizani utawaletea uhuru.

8 Jina langu mimi ni Mwenyezi-Mungu; utukufu wangu sitampa mwingine, wala sifa zangu sanamu za miungu.

9 Tazama, mambo niliyotabiri yametukia; na sasa natangaza mambo mapya, nakueleza hayo kabla hayajatukia.”

10 Mwimbieni Mwenyezi-Mungu wimbo mpya! Dunia yote iimbe sifa zake: Bahari na vyote vilivyomo, nchi za mbali na wakazi wake;

11 jangwa na miji yake yote ipaaze sauti, vijiji vya wakazi wa Kedari vimsifu, wakazi wa Sela waimbe kwa shangwe; wapaaze sauti kutoka mlimani juu.

12 Wote wakaao nchi za mbali, na wamtukuze na kumsifu Mwenyezi-Mungu.

13 Mwenyezi-Mungu ajitokeza kama shujaa; kama askari vitani ajikakamua kupigana. Anapaza sauti kubwa ya vita, na kujionesha mwenye nguvu dhidi ya maadui zake.

14 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Kwa muda mrefu sasa nimenyamaza, nimekaa kimya na kujizuia; lakini sasa nitalia kama mama anayejifungua, anayetweta pamoja na kuhema.

15 Nitaharibu milima na vilima, na majani yote nitayakausha. Mito ya maji nitaigeuza kuwa nchi kavu, na mabwawa ya maji nitayakausha.

16 “Nitawaongoza vipofu katika njia wasiyoifahamu, nitawaongoza katika njia ambazo hawazijui. Mbele yao giza nitaligeuza kuwa mwanga, na mahali pa kuparuza patakuwa laini. Huo ndio mpango wangu wa kufanya, nami nitautekeleza.

17 Wote wanaotegemea sanamu za miungu, wote wanaoziambia: Nyinyi ni miungu yetu; watakomeshwa na kuaibishwa.

18 “Sikilizeni enyi viziwi! Tazameni enyi vipofu, mpate kuona!

19 Nani aliye kipofu ila mtumishi wangu? Nani aliye kiziwi kama mjumbe ninayemtuma? Ni nani aliye kipofu kama huyu niliyemweka wakfu, au kipofu kama mtumishi wa Mwenyezi-Mungu?

20 Nyinyi mmeona mambo mengi, lakini hamwelewi kitu. Masikio yenu yako wazi, lakini hamsikii kitu!”

21 Mwenyezi-Mungu, kwa ajili ya uaminifu wake, alipenda kukuza mwongozo wake na kuutukuza.

22 Lakini hawa ni watu walioibiwa mali na kuporwa! Wote wamenaswa mashimoni, wamefungwa gerezani. Wamekuwa kama mawindo bila mtu wa kuwaokoa, wamekuwa nyara na hakuna asemaye, “Waokolewe!”

23 Je, mtatega sikio kusikia kitu hiki? Nani kati yenu atakayesikiliza vizuri yatakayotukia?

24 Ni nani aliyewatia Waisraeli mikononi mwa adui zao? Nani aliyewaacha wanyanganywe mali zao? Ni Mwenyezi-Mungu ambaye tumemkosea! Wazee wetu walikataa kuzifuata njia zake, wala hawakuzitii amri zake.

25 Kwa hiyo aliwamwagia hasira yake kali, akawaacha wakumbane na vita vikali. Hasira yake iliwawakia kila upande, lakini wao hawakuelewa chochote; iliwachoma, lakini hawakutilia jambo hilo maanani.

43

1 Mwenyezi-Mungu aliyewaumba enyi watu wa Yakobo, yeye aliyewafanya enyi watu wa Israeli, asema: “Msiogope, maana mimi nimewakomboa; nimewaita kwa jina nanyi ni wangu.

2 Mkipita katika mafuriko, mimi nitakuwa pamoja nanyi; mkipita katika mito, haitawashinda nguvu. Mkitembea katika moto, hamtaunguzwa; mwali wa moto hautawaunguza.

3 Maana mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, Mungu Mtakatifu wa Israeli, Mwokozi wenu. Nitaitoa nchi ya Misri iwe fidia yenu, nitaitoa Kushi na Seba ili mwachwe huru.

4 Kwa vile mna thamani mbele yangu, kwa kuwa nimewapa hadhi na kuwapenda, mimi nawaacha watu kusudi niwapate nyinyi, nayaachilia mataifa badala ya maisha yenu.

5 Msiogope maana mimi nipo pamoja nanyi. “Nitawarudisha wazawa wenu toka mashariki, nitawakusanyeni kutoka magharibi.

6 Nitaiambia kaskazini, ‘Waache waondoke’, na kusini, ‘Usiwazuie’! Warudisheni watu kutoka mbali, kutoka kila mahali duniani.

7 Kila mmoja hujulikana kwa jina langu, niliwaumba wote na kuwafanya kwa ajili ya utukufu wangu.”

8 Waleteni mbele watu hao, ambao wana macho lakini hawaoni wana masikio lakini hawasikii!

9 Mataifa yote na yakusanyike, watu wote na wakutane pamoja. Nani kati ya miungu yao awezaye kutangaza yatakayotukia? Nani awezaye kutuonesha yanayotukia sasa? Wawalete mashahidi wao kuthibitisha kwamba walifanya hivyo. Waache wasikilize na kusema, “Ilikuwa kweli.”

10 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Nyinyi Waisraeli ni mashahidi wangu; niliwachagua muwe watumishi wangu, mpate kunijua na kuniamini, kwamba ndimi peke yangu Mungu. Kabla yangu hajapata kuwapo mungu mwingine, wala hatakuwapo mungu mwingine.

11 “Mimi peke yangu ndimi Mwenyezi-Mungu, hakuna mkombozi mwingine ila mimi.

12 Nilitangaza yale ambayo yangetukia, kisha nikaja na kuwakomboa. Hakuna mungu mwingine aliyewahi kufanya hivyo, nanyi ni mashahidi wangu.

13 Mimi ni Mungu na nitakuwa Mungu daima. Hakuna awezaye kuiepa nguvu yangu; hakuna awezaye kupinga ninayofanya.”

14 Mwenyezi-Mungu, Mkombozi wenu, Mtakatifu wa Israeli, asema hivi: “Kwa ajili yenu nitatuma jeshi Babuloni. Nitayavunjilia mbali malango ya mji wake, na kelele za hao Wakaldayo zitageuka maombolezo.

15 Mimi ni Mwenyezi-Mungu, Mtakatifu wenu; Mimi ndimi Muumba wa Israeli, Mfalme wenu.”

16 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Wakati mmoja nilifanya barabara baharini nikaweka njia kati ya mawimbi makubwa.

17 Nililipiga jeshi lenye nguvu, jeshi la magari na farasi wa vita, askari na mashujaa wa vita. Niliwaangusha chini wasiweze kuinuka tena, niliwakomesha na kuwazima kama utambi wa taa. Sasa nasema:

18 ‘Msiyanganganie mambo yaliyopita, wala msifikirie vitu vya zamani.

19 Tazameni, mimi ninafanya kitu kipya. Kinafanyika sasa hivi, nanyi mtaweza kukiona. Nitafanya njia nyikani, na kububujisha mito jangwani.

20 Wanyama wa porini wataniheshimu, kina mbweha na kina mbuni, maana nitaweka maji nyikani, na kububujisha mito jangwani, ili kuwanywesha watu wangu wateule,

21 watu niliowaumba kwa ajili yangu mwenyewe, ili wazitangaze sifa zangu!’

22 “Lakini ewe taifa la Yakobo, hukuniabudu mimi; enyi watu wa Israeli, mlinichoka mimi!

23 Hamjaniletea kondoo wenu wa sadaka za kuteketezwa, wala kuniheshimu kwa tambiko zenu. Nami sikuwalemeza kwa kutaka sadaka, wala sikuwachosha kwa kuwadai ubani.

24 Hamkuninunulia manukato kwa faida yenu, wala kuniridhisha kwa nyama nono za tambiko. Badala yake dhambi zenu zimekuwa mzigo kwangu, mmenichosha kabisa kwa makosa yenu.

25 Walakini mimi ndimi niliyefuta makosa yenu kwa heshima yangu, ndimi niyafutaye makosa kwa ajili yangu mwenyewe, na wala sitazikumbuka dhambi zenu.

26 “Niambie kama mna kisa nami, njoo tukahojiane; toeni mashtaka yenu ili tuuone ukweli wenu!

27 Babu yenu wa kwanza alitenda dhambi, wapatanishi wenu waliniasi.

28 Kwa hiyo niliwafanya haramu wakuu wa mahali patakatifu nikawaacha watu wa Yakobo waangamizwe, naam, nikawaacha Waisraeli watukanwe.”

44

1 “Sikiliza ewe taifa Israeli mtumishi wangu; sikiliza ewe kizazi cha Yakobo mteule wangu.

2 Mimi, Mwenyezi-Mungu Muumba wako, niliyekufanya tangu tumboni mwa mama yako, nimekuja kukusaidia wewe. Mimi Mwenyezi-Mungu nasema: Usiogope, ewe taifa la Yakobo, mtumishi wangu, naam, usiogope ewe Yeshuruni mteule wangu.

3 “Nitaimwagilia maji nchi iliyokauka, na kutiririsha mto katika nchi kame. Nitawamiminia roho yangu wazawa wako, nitawamwagia watoto wako baraka yangu.

4 Watachipua kama nyasi penye maji mengi, kama majani kandokando ya vijito.

5 “Mmoja atasema: ‘Mimi ni wa Mwenyezi-Mungu’, mwingine atajiita kwa jina la Yakobo, mwingine ataandika mkononi mwake, ‘Wa Mwenyezi-Mungu’, na kujitambulisha kwa jina la Israeli.”

6 Mwenyezi-Mungu, Mfalme na Mkombozi wa Israeli, naam, Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi: “Mimi ni wa kwanza na wa mwisho; hakuna Mungu mwingine ila mimi.

7 Ni nani Mungu aliye kama mimi? Mwache atangaze na kusema wazi mbele yangu. Nani alitangaza hapo kale mambo ambayo yatatukia? Na watuambie yale ambayo bado kutokea.

8 Enyi watu wangu, msiogope wala msiwe na hofu, Je, sikuwaambia tangu zamani mambo yatakayotokea? Nyinyi ni mashahidi wangu. Je, yuko Mungu mwingine ila mimi? Je, kuna mwenye nguvu mwingine? Huyo simjui!”

9 Watu wote wanaotengeneza sanamu za miungu ni bure kabisa; na vitu hivyo wanavyovifurahia haviwafai chochote. Wanaoshuhudia hiyo miungu ya uongo ni vipofu na wajinga. Kwa hiyo hao wataaibishwa!

10 Ajabu ya mtu kutengeneza sanamu au kinyago cha mungu ambaye hawezi kumsaidia chochote!

11 Hakika wote wanaomheshimu wataaibishwa, tena hao mafundi wa sanamu ni binadamu tu. Basi, wakutane wote, wajitokeze, nao watatishika na kuaibishwa.

12 Mfuachuma huchukua madini, akayayeyusha motoni na kufua sanamu. Huigongagonga kwa nyundo ili kuipa umbo kwa mikono yake yenye nguvu. Wakati wote huo yeye huona njaa na kuchoka; huona kiu na nguvu kumwishia.

13 Kadhalika naye seremala hupima kipande cha mbao, akakitia alama kwa kalamu yake, kisha kwa vifaa vyake hukichonga na kukipa umbo la binadamu na sura ya kupendeza; kisha akaiweka sanamu hiyo ya mungu mahali pake pa pekee.

14 Mtu hukata mti wa mwerezi ili autumie, au huchagua mberoshi au mwaloni. Huuacha ukue kati ya miti ya msituni. Au hupanda mwerezi na mvua huustawisha.

15 Sehemu ya mti huo itatumiwa kama kuni; mtu huota moto wake na kuoka mikate yake juu yake. Sehemu nyingine ya mti huohuo, mtu hujichongea sanamu ya mungu, akainakshi, halafu akaiabudu.

16 Kisha huchukua kuni zake akaoka nazo moto, akachoma nyama juu yake, akala, akashiba. Halafu hukaa hapo akiota moto na kusema, “Naam! Ama kweli nimepata joto! Huo ndio moto!”

17 Sehemu iliyobaki ya mti huohuo, hujichongea sanamu ya mungu, kinyago chake, kisha huisujudia na kuiabudu. Huiomba akisema, “Wewe ni mungu wangu, niokoe!”

18 Watu hao hawajui wala hawaelewi kitu chochote. Wamefumbwa macho wasiweze kuona; kadhalika na akili zao wasiweze kufahamu.

19 Hakuna awezaye kutafakari; au kuwa na akili na kufikiri na kusema: “Nusu ya mti huo niliwashia moto; tena nikaoka mikate juu ya makaa yake, nikachoma nyama, nikala. Je, sehemu iliyobaki nitatengeneza sanamu ambayo ni chukizo na kukisujudia hicho kipande cha mti?”

20 La! Fikira zake zimeambatana na hicho ambacho ni majivu tu! Mtu huyo amepotoka hata hawezi kujiokoa mwenyewe na kusema: “Kweli ninachoshika mkononi ni udanganyifu mtupu!”

21 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Ewe taifa la Yakobo kumbuka; naam, kumbuka ewe Israeli: Wewe ni mtumishi wangu. Nilikuumba ili uwe mtumishi wangu, nami kamwe sitakusahau.

22 Nimeyafagilia mbali makosa yako kama wingu, nimezifanya dhambi zako zitoweke kama ukungu. Rudi kwangu maana mimi nimekukomboa.”

23 Imbeni kwa furaha enyi mbingu, kwa sababu ya hayo aliyotenda Mwenyezi-Mungu. Pazeni sauti enyi vilindi vya dunia! Imbeni kwa furaha enyi milima! Enyi misitu na miti yote iliyomo, imbeni. Maana Mwenyezi-Mungu amewakomboa wazawa wa Yakobo, naye atatukuka katika nchi ya Israeli.

24 Mwenyezi-Mungu, Mkombozi wako, aliyekuumba tangu tumboni mwa mama yako, asema: “Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu niliyeumba vitu vyote. Mimi peke yangu nilizitandaza mbingu, niliiumba dunia kwa nguvu yangu mwenyewe!

25 Mimi huzivuruga ishara za watabiri waongo na kuwapumbaza waaguzi. Mimi huyakanusha maneno ya wenye hekima na kufanya ujuzi wao kuwa upumbavu.

26 Lakini huuthibitisha ujumbe wa mtumishi wangu, na kukamilisha maaguzi ya wajumbe wangu. Mimi ndimi niuambiaye mji wa Yerusalemu: Wewe Yerusalemu, utakaliwa tena na watu. Na miji ya Yuda: Nyinyi mtajengeka tena: Magofu yenu nitayarekebisha tena.

27 Mimi ndimi ninayeviamuru vilindi: Kaukeni.

28 Ndimi nimwambiaye Koreshi: Wewe utawachunga watu kwa niaba yangu. Wewe utatekeleza mipango yangu yote. Ndimi ninayesema kuhusu Yerusalemu: Wewe Yerusalemu utajengwa tena upya; na juu ya hekalu: Msingi wako utawekwa tena.”

45

1 Mwenyezi-Mungu asema hivi juu ya Koreshi: “Wewe ni mfalme wangu niliyekuteua; mimi naitegemeza nguvu yako ili uyashinde mataifa mbele yako, na kuzivunja nguvu za wafalme. Mimi nayafungua malango ya mji mbele yako, na hakuna lango litakalofungwa.

2 Mimi nitakutangulia, na kuisawazisha milima mbele yako. Nitaivunjavunja milango ya shaba, na kuvikatakata vizuizi vyake vya chuma.

3 Nitakupa hazina zilizofichwa gizani, na mali iliyo mahali pa siri, upate kutambua kwamba mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, ninayekuita kwa jina lako.

4 Kwa ajili ya mtumishi wangu Yakobo, naam, kwa ajili ya mteule wangu Israeli, nimekuita kwa jina lako; nimekupa jina la heshima ingawa wewe hunijui.

5 “Mimi ni Mwenyezi-Mungu, wala hakuna mwingine; hakuna Mungu mwingine ila mimi. Ninakuimarisha ingawa wewe hunijui,

6 ili watu wote, toka mashariki hadi magharibi, wajue kwamba hakuna Mungu mwingine ila mimi; mimi ni Mwenyezi-Mungu na hakuna mwingine.

7 Mimi hufanya mwanga na kuumba giza; huleta fanaka na kusababisha balaa. Mimi Mwenyezi-Mungu hutenda vitu hivi vyote.

8 Enyi mbingu, nyesheni kutoka huko juu, mawingu na yadondoshe uadilifu; dunia na ifunuke, ichipushe wokovu, na kuchanusha uadilifu pia! Mimi, Mwenyezi-Mungu nimefanya hayo.”

9 Ole wake mtu ashindanaye na Muumba wake, mtu aliye chombo cha udongo kushindana na mfinyanzi wake! Je, udongo humwuliza anayeufinyanga: “Unatengeneza nini hapa?” Au kumwambia, “Kazi yako si kamili!”

10 Ole wake mtoto amwambiaye baba yake, “Kwa nini umenizaa?” Au amwambiaye mama yake, “Ya nini umenileta duniani?”

11 Mwenyezi-Mungu, Mtakatifu wa Israeli, Mungu, Muumba wa Israeli asema: “Je, mwathubutu kuniuliza juu ya watoto wangu, au kuniamuru juu ya kazi zangu mwenyewe?

12 Ni mimi niliyeifanya dunia, na kuumba binadamu aishiye humo. Mikono yangu ndiyo iliyozitandaza mbingu, na jeshi lote la nyota liko kwa amri yangu.

13 Ni mimi niliyemwamuru Koreshi kuchukua hatua, atekeleze matakwa yangu. Nitazifanikisha njia zake zote; ataujenga upya mji wangu Yerusalemu, na kuwapa uhuru watu wangu walio uhamishoni, bila kutaka malipo wala zawadi.” Mwenyezi-Mungu wa majeshi amesema.

14 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Utajiri wa Misri na bidhaa za Kushi, pamoja na za watu wa Seba, majitu marefu, zitakuja kwako mwenyewe wewe taifa la Israeli, zote zitakuwa mali yako. Watu hao watakutumikia wamefungwa minyororo; watakusujudia na kukiri wakisema: ‘Kwako kuna Mungu wa kweli, wala hakuna Mungu mwingine ila yeye.’”

15 Kweli wewe ni Mungu uliyefichika, Mungu wa Israeli, Mungu Mwokozi.

16 Watengenezaji sanamu wataaibika na kufadhaika, wote kwa pamoja watavurugika.

17 Lakini taifa la Israeli litaokolewa na Mwenyezi-Mungu, litapata wokovu wa milele. Halitaaibishwa wala kufadhaishwa milele.

18 Mwenyezi-Mungu, Mungu pekee, ndiye aliyeiumba dunia, ndiye aliyeiumba na kuitegemeza. Hakuiumba iwe ghasia na tupu, ila aliiumba ikaliwe na viumbe vyake. Yeye asema sasa: “Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, wala hakuna mwingine.

19 Mimi sikunena kwa siri, wala katika nchi yenye giza. Mimi sikuwaambia wazawa wa Yakobo wanitafute katika ghasia. Mimi Mwenyezi-Mungu husema ukweli, maneno yangu ni ya kuaminika.”

20 Enyi watu wa mataifa mliosalia, kusanyikeni pamoja mje! Nyinyi mmekosa akili: Nyinyi mwabeba sanamu za miti na kumwomba mungu asiyeweza kuokoa watu.

21 Semeni wazi na kutoa hoja zenu; shaurianeni pamoja! Ni nani aliyetangaza zamani matukio ya sasa? Ni nani aliyetamka mambo haya zamani? Je, haikuwa mimi Mwenyezi-Mungu? Hakuna Mungu mwingine ila mimi! Mimi ni Mungu wa haki na mwokozi; hakuna mwingine ila mimi.

22 Nigeukieni mimi mpate kuokolewa, popote mlipo duniani. Maana mimi ni Mungu, wala hakuna mwingine.

23 Mimi nimeapa kwa nafsi yangu, ninachotamka ni ukweli, neno langu halitarudi nyuma: Kila binadamu atanipigia magoti, kila mtu ataapa uaminifu.

24 “Watasema juu yangu, ‘Haki na nguvu viko kwa Mwenyezi-Mungu peke yake.’” Wote waliomwakia hasira Mwenyezi-Mungu watamjia yeye na kuaibishwa.

25 Lakini wazawa wa Israeli watapata ushindi kwake Mwenyezi-Mungu na kufurahi.

46

1 “Wewe Beli umeanguka; Nebo umeporomoka. Wakati mmoja watu walibeba sanamu zenu. Sasa wanazibeba mgongoni mwa wanyama, hao wanyama wachovu wamelemewa.

2 Nyinyi mmeanguka na kuvunjika, hamwezi kuviokoa vinyago vyenu; nyinyi wenyewe pia mtapelekwa uhamishoni!

3 “Sikilizeni enyi wazawa wa Yakobo, nisikilizeni enyi mabaki ya watu wangu wa Israeli. Mimi niliwatunzeni tangu mlipozaliwa; niliwabebeni tangu tumboni mwa mama yenu.

4 Mimi ni yuleyule hata katika uzee wenu; hata katika uzee wenu mimi nitawabeba. Nilifanya hivyo kwanza, nitafanya hivyo tena. Nitawabeba nyinyi na kuwaokoa.

5 “Mtanifananisha na nani, tufanane? Je, mwaweza kunilinganisha na nani, tulingane?

6 Watu humimina dhahabu kutoka mifuko yao, hupima fedha kwenye mizani zao, wakamwajiri mfua dhahabu atengeneze sanamu kisha huisujudu na kuiabudu!

7 Hujitwisha sanamu hiyo mabegani, wakaibeba, kisha huiweka mahali pake, ikakaa papo hapo; kamwe haiwezi hata kusogea kutoka hapo ilipo. Mtu akiililia, haiwezi kumwitikia, wala haiwezi kumwokoa mtu katika taabu zake.

8 “Kumbukeni jambo hili na kutafakari, liwazeni akilini mwenu enyi wakosefu.

9 Kumbukeni mambo niliyotenda hapo kale! Mimi ndimi Mungu na hakuna mwingine; naam, mimi ni Mungu, wala hakuna mwingine kama mimi.

10 Nilitangaza mambo ya mwisho tangu mwanzo, tangu kale nilitangaza mambo yatakayotukia. Lengo langu litatimia; mimi nitatekeleza nia yangu yote.

11 Ninamwita tai wangu kutoka mashariki, naam, msiri wangu kutoka nchi ya mbali. Mimi nimenena na nitayafanya; mimi nimepanga nami nitatekeleza.

12 “Nisikilizeni, enyi wenye vichwa vigumu, nisikilizeni enyi mlio mbali na ukombozi.

13 Siku ya kuwakomboa naileta karibu, haiko mbali tena; siku ya kuwaokoeni haitachelewa. Nitauokoa mji wa Siyoni, kwa ajili ya Israeli, fahari yangu.

47

1 “Teremka uketi mavumbini ewe Babuloni binti mzuri! Keti chini pasipo kiti cha enzi ewe binti wa Wakaldayo! Tokea sasa hutaitwa tena mwororo wala nadhifu.

2 Twaa mawe ya kusagia, usage unga kama mtumwa! Vua utaji wako, ukavue na mavazi yako! Pandishia vazi lako miguuni, ukavuke mito.

3 Watu watauona uchi wako; naam, wataiona aibu yako. Mimi nitalipiza kisasi, wala sitamhurumia yeyote.”

4 Mkombozi wetu ndiye Mtakatifu wa Israeli; Mwenyezi-Mungu wa majeshi ndilo jina lake.

5 Mwenyezi-Mungu asema: “Ewe taifa la Wakaldayo lililo kama binti mzuri, keti kimya na kutokomea gizani. Maana umepoteza hadhi yako ya kuwa bimkubwa wa falme.

6 Niliwakasirikia watu wangu Israeli, nikawafanya watu wangu kuwa haramu. Niliwatia mikononi mwako, nawe hukuwaonea huruma; na wazee uliwatwisha nira nzito mno.

7 Ulijisemea moyoni: ‘Nitakuwa malkia milele’, nawe hukuyatafakari mambo yanayotokea, wala kufikiri mwisho wake.

8 “Sasa, basi, sikiliza ewe mpenda anasa, wewe unayedhani kuwa u salama, na kujisemea: ‘Ni mimi tu, na hakuna mwingine isipokuwa mimi. Kamwe sitakuwa mjane, wala sitafiwa na wanangu.’

9 Haya yote mawili yatakupata, ghafla, katika siku moja: Kupoteza watoto wako na kuwa mjane, ijapokuwa una wingi wa uchawi wako, na nguvu nyingi za uganga wako.

10 “Ulijiona salama katika uovu wako; ukajisemea, ‘Hakuna mtu anayeniona.’ Hekima na elimu yako vilikupotosha, ukajisemea moyoni mwako, ‘Mimi ndiye; hakuna mwingine anayenishinda.’

11 Lakini maafa yatakupata ambayo hutaweza kujiepusha nayo. Balaa litakukumba ambalo hutaweza kulipinga; maangamizi yatakujia ghafla ambayo hujapata kamwe kuyaona.

12 Endelea basi na uganga wako, tegemea wingi wa uchawi wako. Wewe uliyapania hayo tangu ujana wako ukitumainia kwamba utafanikiwa au kusababisha kitisho kwa watu!

13 Wewe umejichosha bure na washauri wako. Basi, na wajitokeze hao wanajimu wakuokoe! Wao huzigawa mbingu sehemusehemu, huzichunguza nyota na kubashiri kila mwezi yatakayokupata.

14 “Kumbuka, wao ni kama mabua makavu: Moto utayateketezea mbali! Hawawezi hata kujiokoa wenyewe mbali na ukali wa moto huo. Moto huo si wa kujipatia joto, huo si moto wa kuota!

15 Ndivyo watakavyokuwa hao uliowategemea hivyo, hao uliojishughulisha nao tangu ujana wako. Watatangatanga kila mmoja njia yake; hakuna hata mmoja atakayeweza kukuokoa.”

48

1 Sikilizeni, enyi watu wa Yakobo, enyi mnaojulikana kwa jina la Israeli, nyinyi mlio wa ukoo wa Yuda. Nyinyi huapa kwa jina la Mwenyezi-Mungu, na kudai mnamwabudu Mungu wa Israeli; lakini hayo si ukweli wala sawa.

2 Nyinyi mnaona fahari kujiita watu wa mji mtakatifu, na kujidai kumtegemea Mungu wa Israeli, ambaye jina lake ni Mwenyezi-Mungu wa majeshi.

3 “Nilitangaza zamani matukio ya awali, niliyatamka mimi mwenyewe na kuyafanya yajulikane kwenu. Mara nikaanza kuyatekeleza, nayo yakapata kutukia.

4 Lakini nilikujua wewe kuwa mkaidi; kichwa kigumu kama chuma, uso wako mkavu kama shaba.

5 Kwa hiyo nilikutangazia tangu zamani, kabla hayajatukia mimi nilikutangazia, usije ukasema, ‘Kinyago changu kiliyatenda hayo, sanamu zangu za kuchonga na kusubu ziliyafanya.’

6 “Wewe uliyasikia na sasa unayaona yote. Kwa nini huwezi kuyakiri? Tangu sasa nitakujulisha mambo mapya; mambo yaliyofichika ambayo hukuyajua.

7 Mambo hayo yanatukia sasa; hukupata kuyasikia kabla ya leo, hivyo huwezi kusema, ‘Aa! Nilikwisha yajua.’

8 Hujapata kamwe kuyasikia wala kuyajua; tangu zamani masikio yako hayakuyasikia. Nilijua kuwa wewe ni mwenye hila, na kwamba wewe ni mwasi tangu kuzaliwa.

9 “Kwa heshima ya jina langu, ninaiahirisha hasira yangu; kwa ajili ya heshima yangu, ninaizuia nisije nikakuangamiza.

10 Mimi nitawajaribu lakini si kama fedha katika tanuri. Nitawajaribu katika tanuri ya taabu.

11 Ninafanya hivyo kwa ajili yangu mwenyewe. Kwa nini jina langu lidharauliwe? Utukufu wangu siwezi kumpa mwingine!

12 “Nisikilize ee taifa la Yakobo, nisikilize ee Israeli niliyekuita. Mimi ndiye Mungu; mimi ni wa kwanza na wa mwisho.

13 Kwa mkono wangu niliuweka msingi wa dunia, mimi mwenyewe nilizitandaza mbingu. Nikiziita mbingu na dunia, zinasimama haraka mbele yangu.

14 “Kusanyikeni nyote msikilize! Nani kati ya miungu yenu aliyetabiri vitu hivi? Mimi Mwenyezi-Mungu nampenda Koreshi; yeye atatekeleza lengo langu kuhusu Babuloni, naam, yeye atawashambulia Wakaldayo.

15 Mimi, naam, mimi nimeyasema na kumwita; nimemleta, naye atafaulu katika mpango wake.

16 Njoni karibu nami msikie jambo hili: Tangu mwanzo mimi sikusema kwa siri, tangu mambo hayo yaanze kutendeka, nimekuwapo.” Sasa, Bwana Mungu amenituma, na kunipa nguvu ya roho yake.

17 Mwenyezi-Mungu, Mtakatifu wa Israeli, Mkombozi wako, asema hivi: “Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, ninayekufundisha kwa faida yako, ninayekuongoza katika njia unayotakiwa kwenda.

18 Laiti ungalizitii amri zangu! Hapo baraka zingekutiririkia kama mto, ungepata fanaka kwa wingi kama mawimbi ya bahari.

19 Wazawa wako wangekuwa wengi kama mchanga, naam, wangekuwa wengi kama chembe za mchanga. Jina lao kamwe lisingaliondolewa, kumbukumbu lao halingalitoweka mbele yangu.”

20 Sasa, ondokeni Babuloni! Kimbieni kutoka Kaldayo! Tangazeni jambo hili kwa sauti za shangwe, enezeni habari zake kila mahali duniani. Semeni: “Mwenyezi-Mungu amelikomboa taifa la mtumishi wake Yakobo.”

21 Alipowaongoza jangwani hawakuona kiu, aliwatiririshia maji kutoka mwambani, aliupasua mwamba maji yakabubujika.

22 Lakini Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Watu waovu sitawapa amani.”

49

1 Nisikilizeni, enyi nchi za mbali, tegeni sikio, enyi watu wa mbali! Mwenyezi-Mungu aliniita kabla sijazaliwa, alitaja jina langu nikiwa tumboni mwa mama yangu.

2 Aliyapa ukali maneno yangu kama upanga mkali, alinificha katika kivuli cha mkono wake; aliufanya ujumbe wangu mkali kama ncha ya mshale, akanificha katika podo lake.

3 Aliniambia, “Wewe ni mtumishi wangu; kwako, Israeli, watu watanitukuza.”

4 Lakini mimi nikafikiri, “Nimeshughulika bure, nimetumia nguvu zangu bure kabisa.” Hata hivyo, Mwenyezi-Mungu atanipa haki yangu; tuzo la kazi yangu liko kwa Mungu.

5 Lakini asema sasa Mwenyezi-Mungu, ambaye aliniita tangu tumboni mwa mama yangu ili nipate kuwa mtumishi wake; nilirudishe taifa la Yakobo kwake, niwakusanye wazawa wa Israeli kwake. Mwenyezi-Mungu amenijalia heshima mbele yake. Mungu wangu amekuwa ndiye nguvu yangu.

6 Yeye asema: “Haitoshi tu wewe kuwa mtumishi wangu, uyainue makabila ya Yakobo, na kurekebisha watu wa Israeli waliobaki. Nitakufanya uwe mwanga wa mataifa, niwaletee wokovu watu wote duniani.”

7 Mwenyezi-Mungu, Mkombozi na Mtakatifu wa Israeli, amwambia hivi yule anayedharauliwa mno, yule anayechukiwa na mataifa, na ambaye ni mtumishi wa watawala: “Wafalme watakuona nao watasimama kwa heshima, naam, wakuu watainama na kukusujudia kwa sababu yangu mimi Mwenyezi-Mungu ambaye hutimiza ahadi zangu; kwa sababu yangu mimi Mtakatifu wa Israeli ambaye nimekuteua wewe.”

8 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Wakati wa kufaa nilikujibu ombi lako; wakati wa wokovu nilikusaidia. Nimekuweka na kukufanya uwe kiungo cha agano langu na mataifa yote: Kuirekebisha nchi iliyoharibika, na kuwarudishia wenyewe ardhi hiyo;

9 kuwaambia wafungwa, ‘Tokeni humo gerezani’, na wale walio gizani, ‘Njoni nje mwangani!’ Kila mahali watakapokwenda watapata chakula hata kwenye vilima vitupu watapata malisho.

10 Hawataona tena njaa wala kuwa na kiu. Upepo wa hari wala jua havitawachoma, mimi niliyewahurumia nitawaongoza na kuwapeleka kwenye chemchemi za maji.

11 Milima yote nitaifanya kuwa njia, na barabara zangu kuu nitazitengeneza.

12 Watu wangu watarudi kutoka mbali, wengine kutoka kaskazini na magharibi, wengine kutoka upande wa kusini.”

13 Imbeni kwa furaha, enyi mbingu! Shangilia ewe dunia. Pazeni sauti mwimbe enyi milima, maana Mwenyezi-Mungu amewafariji watu wake, naam, atawaonea huruma watu wake wanaoteseka.

14 Wewe Siyoni wasema: “Mwenyezi-Mungu ameniacha; hakika Bwana wangu amenisahau.”

15 Lakini Mwenyezi-Mungu asema: “Je, mama aweza kumsahau mwanawe anayenyonya, asimwonee huruma mtoto wa tumbo lake? Hata kama mama aweza kumsahau mwanawe, mimi kamwe sitakusahau.

16 Nimekuchora katika viganja vyangu; kuta zako naziona daima mbele yangu.

17 Watakaokujenga upya wanakuja haraka, wale waliokuharibu wanaondoka.

18 Inua macho uangalie pande zote; watu wako wote wanakusanyika na kukujia. Naapa kwa nafsi yangu mimi Mwenyezi-Mungu, watu wako watakuwa kwako kama mapambo, utawafurahia kama afanyavyo bibi arusi na utaji wake.

19 “Kweli umekumbana na uharibifu, makao yako yamekuwa matupu, na nchi yako imeteketezwa. Lakini sasa itakuwa ndogo mno kwa wakazi wake; na wale waliokumaliza watakuwa mbali.

20 Wanao waliozaliwa uhamishoni, watakulalamikia wakisema: ‘Nchi hii ni ndogo mno; tupatie nafasi zaidi ya kuishi.’

21 Hapo ndipo utakapojiuliza mwenyewe: ‘Nani aliyenizalia watoto wote hawa? Nilifiwa na wanangu bila kupata wengine. Nilipelekwa uhamishoni na kutupwa mbali; nani basi aliyewalea watoto hawa? Mimi niliachwa peke yangu, sasa, hawa wametoka wapi?’”

22 Bwana Mungu asema hivi: “Nitayapungia mkono mataifa; naam, nitayapa ishara, nayo yatawabeba watoto wenu wa kiume, kadhalika na watoto wenu wa kike na kuwarudisha kwako.

23 Wafalme watakushughulikia, na malkia watakutengenezea chakula. Watakusujudia na kukupa heshima, na kuramba vumbi iliyo miguuni pako. Hapo utatambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu; wote wanaonitegemea hawataaibika.”

24 Watu wa Yerusalemu walalamika: “Je, shujaa aweza kunyanganywa nyara zake? Au mateka wa mtu katili waweza kuokolewa?”

25 Mwenyezi-Mungu ajibu: “Naam! Hata nyara za shujaa zitachukuliwa, mateka wa mtu katili wataokolewa. Mimi mwenyewe nitawakabili maadui zako, mimi mwenyewe nitawaokoa watoto wako.

26 Nitawafanya wanaokukandamiza watafunane; watalewa damu yao wenyewe kama divai. Hapo binadamu wote watatambua kwamba mimi ni Mwenyezi-Mungu, Mwokozi wako, mimi ni Mkombozi wako, Mwenye Nguvu wa Yakobo.”

50

1 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Kama nimempa talaka mama yako Yerusalemu, hati ya talaka iko wapi? Au kama niliwauza utumwani, yuko wapi basi, huyo niliyemwuzia? Kumbukeni mliuzwa utumwani kwa maovu yenu, mama yenu alifukuzwa kwa makosa yenu.

2 “Nilipokuja kwa nini sikukuta mtu? Nilipoita mbona hamkuitikia? Je, mkono wangu ni mfupi nisiweze kuwaokoeni? Je, sina nguvu ya kuwakomboa? Tazama! Kwa kuikemea kidogo bahari hukauka, na mito nikaifanya kuwa jangwa, samaki wake wakafa na kunuka kwa kukosa maji.

3 Mimi hulivika anga giza, na kulivalisha vazi la kuomboleza.”

4 Bwana Mungu amenipa ufasaha wa lugha, niwatie moyo wale waliochoka. Kila asubuhi hunipa hamu ya kusikiliza anayotaka kunifunza.

5 Bwana Mungu amenifanya msikivu, nami sikuwa mkaidi wala kugeuka mbali naye.

6 Mgongo wangu niliwaachia walionipiga, mashavu yangu waliozingoa ndevu zangu; walioniaibisha na kunitemea mate, sikujificha mbali nao.

7 Bwana Mungu hunisaidia, kwa hiyo siwezi kufadhaika. Uso wangu nimeukaza kama jiwe; najua kwamba sitaaibishwa.

8 Mtetezi wangu yuko karibu. Ni nani atakayepingana nami? Na aje tusimame mahakamani. Adui yangu ni nani? Na ajitokeze mbele basi.

9 Tazama Bwana Mungu hunisaidia. Ni nani awezaye kusema nina hatia? Maadui zangu wote watachakaa kama vazi, nondo watawatafuna.

10 Nani kati yenu amchaye Mwenyezi-Mungu? Nani anayetii maneno ya mtumishi wake? Kama yupo atembeaye gizani bila taa, amtumainie Mwenyezi-Mungu, na kumtegemea Mungu wake.

11 Lakini nyinyi mnaowasha moto, na kujifanyia silaha za mienge, tembeeni kwa mwanga wa moto huo, miali ya moto mliowasha nyinyi wenyewe. Mtakachopata kutoka kwa Mwenyezi-Mungu ni hiki: Nyinyi mtalala chini na mateso makali.

51

1 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Nisikilizeni enyi mnaotaka kukombolewa, nyinyi mnaonitafuta mimi Mwenyezi-Mungu. Utazameni mwamba mlimochongwa, chimbo la mawe mlimochimbuliwa.

2 Mkumbukeni Abrahamu babu yenu, na Sara aliyewazaa nyinyi. Abrahamu alikuwa hana mtoto wakati nilipomwita, lakini nilimbariki na kumfanya kuwa na wengi.

3 “Mimi Mwenyezi-Mungu nitaufariji mji wa Siyoni, nitaparekebisha mahali pake pote palipoharibika. Nyika zake nitazifanya kama bustani ya Edeni, majangwa yake kama bustani ya Mwenyezi-Mungu. Kwake kutapatikana furaha na shangwe, na nyimbo za shukrani zitasikika humo.

4 “Nisikilizeni enyi watu wangu, nitegeeni sikio enyi taifa langu. Sheria na haki zitatoka kwangu mimi; nazo zitakuwa mwanga wa mataifa.

5 Nitaleta ukombozi hima; wokovu nitakaoleta waanza kutokea. Mimi mwenyewe nitayatawala mataifa. Wakazi wa nchi za mbali wananingojea, wanaitegemea nguvu yangu.

6 Inueni macho mzitazame mbingu, kisha tazameni dunia huko chini. Mbingu zitatoweka kama moshi, dunia itachakaa kama vazi, na wakazi wake watakufa kama wadudu. Lakini wokovu niuletao wadumu milele; ukombozi wangu kamwe hautakoma.

7 “Nisikilizeni enyi mjuao mambo ya haki, ambao sheria zangu zimo mioyoni mwenu. Msiogope dharau za watu, wala kufadhaishwa na masimango yao.

8 Maana wataliwa na nondo kama vile vazi; viwavi watawala kama walavyo nguo ya sufu. Lakini ukombozi niletao mimi utadumu milele; wokovu wangu hautakuwa na mwisho.”

9 Amka! Amka ee Mwenyezi-Mungu! Jivike nguvu zako utuokoe. Amka kama ulivyofanya hapo zamani, nyakati za vizazi vya hapo kale. Je, si wewe uliyemkatakata Rahabu, ukalitumbua dude hilo la kutisha?

10 Wewe ndiwe uliyeikausha bahari, ndiwe uliyevikausha vilindi vya maji, ukafanya njia katika vilindi vya bahari, ili wale uliowakomboa wavuke humo.

11 Watu wako uliowakomboa, ee Mwenyezi-Mungu, watarudi, watakuja Siyoni wakiimba; watajaa furaha ya milele, watapata furaha na shangwe. Huzuni na maombolezo vitatoweka kabisa.

12 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Mimi, naam mimi, ndimi ninayekufariji. Kwa nini wewe unamwogopa mtu ambaye hufa, binadamu ambaye hutoweka kama nyasi?

13 Wewe umenisahau mimi Mwenyezi-Mungu Muumba wako, niliyezitandaza mbingu, na kuiweka misingi ya dunia! Wewe waendelea kuogopa siku zote, kwa sababu ya ghadhabu ya mdhalimu wako, kwamba yuko tayari kukuangamiza! Lakini hasira yake itafika wapi?

14 Wanaodhulumiwa watafunguliwa hima, hawatakufa na kushuka shimoni, wala hawatatindikiwa chakula.

15 Mimi ni Mwenyezi-Mungu, Mungu wako; nivurugaye bahari, mawimbi yake yakanguruma; Mwenyezi-Mungu wa majeshi, ndilo jina langu!

16 Nimeyaweka maneno yangu mdomoni mwako; nimekuficha katika kivuli cha mkono wangu. Mimi nilizitandaza mbingu, nikaiweka misingi ya dunia. Mimi nawaambieni enyi watu wa Siyoni: ‘Nyinyi ni watu wangu.’”

17 Amka ewe Yerusalemu! Amka usimame wima! Mwenyezi-Mungu amekunywesha kikombe cha ghadhabu yake, nawe umeinywa mpaka tone la mwisho, mpaka ukayumbayumba.

18 Kati ya watoto wote uliowazaa hakuna yeyote wa kukuongoza. Hakuna hata mmoja wa kukushika mkono kati ya watoto wote uliowalea.

19 Majanga haya mawili yamekupata: Uharibifu na maangamizi; njaa na mauaji. Nani atakayekuonea huruma? Nani atakayekufariji?

20 Watoto wako wamezirai, wamelala pembeni mwa kila barabara, wako kama paa aliyenaswa wavuni. Wamepatwa na ghadhabu ya Mwenyezi-Mungu, wamepatwa na adhabu ya Mungu wako.

21 Basi, sikiliza ewe Yerusalemu unayeteseka; sikiliza wewe uliyelewa, lakini sio kwa divai.

22 Bwana, Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, awateteaye watu wake, asema hivi: “Nimekuondolea kikombe cha kuyumbisha, hutakunywa tena kikombe cha ghadhabu yangu.

23 Nitawanywesha watesi wako kikombe hicho waliokuambia ulale chini wapite juu yako; wakaufanya mgongo wako kama ardhi, kama barabara yao ya kupitia.”

52

1 Amka! Amka! Jipe nguvu zako ewe mji wa Siyoni! Jivike mavazi yako mazuri, ewe Yerusalemu, mji mtakatifu. Maana hawataingia tena kwako watu wasiotahiriwa na walio najisi.

2 Jikungute mavumbi, uinuke ewe Yerusalemu uliyetekwa nyara! Jifungue minyororo yako shingoni, ewe binti Siyoni uliyechukuliwa mateka.

3 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Nyinyi mliuzwa utumwani bila malipo yoyote, na mtakombolewa bila kulipa hata senti moja.

4 Tena mwanzoni nyinyi watu wangu mlikimbilia Misri mkakaa huko. Halafu baadaye Waashuru waliwakandamiza bila sababu yoyote.

5 Katika hali ya sasa napata faida gani kuwaona watu wangu wamepelekwa utumwani? Hao wanaowatawala wanajitapa. Nalo jina langu laendelea kudharauliwa kila siku.

6 Kwa hiyo watu wangu watajua mimi ni nani; siku hiyo watajua kwamba ni mimi ninayesema: Niko!”

7 Tazama inavyopendeza kumwona mjumbe akitokea mlimani, ambaye anatangaza amani, ambaye analeta habari njema, na kutangaza ukombozi! Anauambia mji wa Siyoni: “Mungu wako anatawala!”

8 Sikiliza sauti ya walinzi wako; wanaimba pamoja kwa furaha, maana wanaona kwa macho yao wenyewe, kurudi kwa Mwenyezi-Mungu mjini Siyoni.

9 Pazeni sauti za shangwe, enyi magofu ya Yerusalemu! Mwenyezi-Mungu amewafariji watu wake, ameukomboa mji wa Yerusalemu.

10 Mwenyezi-Mungu ameonesha nguvu yake tukufu, mbele ya mataifa yote. Atawaokoa watu wake, na ulimwengu wote utashuhudia.

11 Ondokeni! Ondokeni! Tokeni hapa; msiguse kitu chochote najisi! Ondokeni huku Babuloni! Jitakaseni enyi mbebao vyombo vya Mwenyezi-Mungu.

12 Safari hii hamtatoka kwa haraka, wala hamtaondoka mbiombio! Maana Mwenyezi-Mungu atawatangulieni, Mungu wa Israeli atawalinda kutoka nyuma.

13 Mungu asema hivi: “Mtumishi wangu atafanikiwa; atatukuzwa na kupewa cheo, atapata heshima kuu.

14 Wengi waliomwona walishtuka, kwa vile sura yake ilikuwa imeharibiwa; hakuwa tena na umbo la kibinadamu!

15 Lakini sasa ameyashangaza mataifa mengi. Wafalme wanaduwaa kwa sababu yake, maana wataona mambo ambayo hawajapata kuambiwa, na kufahamu mambo ambayo hawajapata kusikia.”

53

1 Nani aliyeamini mambo tuliyosikia? Nani aliyetambua kuwa mkono wa Mwenyezi-Mungu ulihusika?

2 Maana, mbele yake Mwenyezi-Mungu, mtumishi wake alikua kama mti mchanga, kama mzizi katika nchi kavu. Hakuwa na umbo wala sura ya kutupendeza, wala hakuwa na uzuri wowote wa kutuvutia.

3 Alidharauliwa na kukataliwa na watu, alikuwa mtu wa uchungu na huzuni. Alikuwa kama mtu kinyaa kwa watu; alidharauliwa na tukamwona si kitu.

4 Hata hivyo alivumilia majonzi yetu, na kubeba huzuni zetu. Sisi tulifikiri amepata adhabu, amepigwa na Mungu na kuteswa.

5 Lakini alijeruhiwa kwa sababu ya dhambi zetu, aliumizwa kwa sababu ya maovu yetu. Kwa kuadhibiwa kwake sisi tumepata uhai; kwa kupigwa kwake sisi tumepona.

6 Sisi sote tumepotea kama kondoo, kila mmoja wetu ameelekea njia yake. Lakini Mwenyezi-Mungu alimtwika adhabu, ambayo sisi wenyewe tuliistahili.

7 Alidhulumiwa na kuteswa, lakini alivumilia kwa unyenyekevu, bila kutoa sauti hata kidogo. Alikuwa kama mwanakondoo apelekwaye machinjoni, kama kondoo akaavyo kimya anapokatwa manyoya. Hakutoa sauti hata kidogo.

8 Alidhulumiwa, akahukumiwa na kupelekwa kuuawa; na hakuna mtu aliyejali yanayompata. Alifukuzwa kutoka nchi ya walio hai, kwa sababu ya makosa ya watu wangu.

9 Walimzika pamoja na wahalifu; katika kifo aliwekwa pamoja na matajiri, ingawa hakutenda ukatili wowote, wala hakusema neno lolote la udanganyifu.

10 Mwenyezi-Mungu alipenda kumwumiza na kumweka katika huzuni. Alijitoa mhanga kwa ajili ya kuondoa dhambi. Mtumishi wa Mungu atakuwa na wazawa; ataishi maisha marefu. Yeye ndiye atakayetimiza mpango wa Mwenyezi-Mungu.

11 Mungu asema: “Baada ya kutaabika sana, mtumishi wangu atafurahi. Kwa kuwajibika kwake kikamilifu, atatosheka na matokeo hayo. Kwa maarifa yake mtumishi wangu mwadilifu atawafanya wengi wawe waadilifu Yeye atazibeba dhambi zao.

12 Kwa hiyo, nitamweka katika cheo cha wakuu, atagawa nyara pamoja na wenye nguvu; kwa kuwa alijitolea mwenyewe kufa, akawekwa katika kundi moja na wakosefu, alizibeba dhambi za watu wengi, akawaombea msamaha hao wakosefu.”

54

1 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Imba kwa shangwe ewe uliye tasa, wewe ambaye hujapata kuzaa! Paza sauti na kuimba kwa nguvu, wewe usiyepata kujifungua mtoto. Maana watoto wako wewe uliyeachwa watakuwa wengi kuliko wa aliye na mume.

2 Panua nafasi hemani mwako, tandaza mapazia hapo unapoishi, usijali gharama zake. Zirefushe kamba zake, na kuimarisha vigingi vyake;

3 maana utapanuka kila upande; wazawa wako watamiliki mataifa, miji iliyokuwa mahame itajaa watu.

4 Usiogope maana hutaaibishwa tena; usifadhaike maana hutadharauliwa tena. Utaisahau aibu ya ujana wako, wala hutaikumbuka tena fedheha ya ujane wako.

5 Muumba wako atakuwa mume wako; Mwenyezi-Mungu wa majeshi, ndilo jina lake, Mtakatifu wa Israeli ndiye Mkombozi wako; yeye aitwa ‘Mungu wa ulimwengu wote’.

6 “Yerusalemu, Mwenyezi-Mungu amekuita tena wewe kama vile mke aliyeachwa na kuhuzunika, mke aliyeolewa akiwa kijana akaachwa. Mungu wako anasema:

7 Nilikuacha kwa muda mfupi tu; kwa huruma nyingi, nitakurudisha.

8 Kwa hasira nyingi nilikuficha uso wangu kwa kitambo, lakini kwa fadhili za milele nitakuonea huruma. Mimi Mwenyezi-Mungu Mkombozi wako, nimesema.

9 “Nitafanya kama nilivyofanya wakati wa Noa: Wakati ule niliapa kwamba sitaifunika tena ardhi kwa gharika. Basi sasa naapa kwamba sitakukasirikia tena wala sitakukemea tena.

10 Milima yaweza kutoweka, vilima vyaweza kuondolewa, lakini fadhili zangu hazitakuondoka, agano langu la amani halitaondolewa. Mimi Mwenyezi-Mungu nikuhurumiaye nimesema.

11 “Ewe Yerusalemu uliyeteseka, uliyetaabishwa na kukosa wa kukufariji! Nitakujenga upya kwa mawe ya thamani, misingi yako itakuwa ya johari ya rangi ya samawati.

12 Minara yako nitaijenga kwa mawe ya akiki, malango yako kwa almasi, na ukuta wako kwa mawe ya thamani.

13 “Watu wako watafunzwa nami Mwenyezi-Mungu, wanao watapata ustawi mwingi.

14 Utaimarika katika uadilifu, utakuwa mbali na dhuluma, nawe hutaogopa kitu; utakuwa mbali na hofu, maana haitakukaribia.

15 Mtu yeyote akija kukushambulia, hatakuwa ametumwa nami. Yeyote atakayekushambulia, ataangamia mbele yako.

16 “Tazama, mimi ndiye niliyemuumba mhunzi, afukutaye moto wa makaa na kufua silaha. Ni mimi pia niliyemuumba mwangamizi anayeangamiza.

17 Silaha zote zilizoundwa kukudhuru wewe hazitafaa chochote kile. Mtu akikushtaki mahakamani, utamshinda. Hilo ndilo fungu nililowapangia watumishi wangu. Hizo ndizo haki nilizowathibitishia. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.

55

1 “Haya! Kila mwenye kiu na aje kwenye maji! Njoni, nyote hata msio na fedha; nunueni ngano mkale, nunueni divai na maziwa. Bila fedha, bila gharama!

2 Mbona mnatumia fedha yenu kwa ajili ya kitu kisicho chakula? Ya nini kutoa jasho lenu kwa kitu kisichoshibisha? Nisikilizeni mimi kwa makini, nanyi mtakula vilivyo bora, na kufurahia vinono.

3 “Tegeni sikio enyi watu wangu, mje kwangu; nisikilizeni, ili mpate kuishi. Nami nitafanya nanyi agano la milele; nitawapeni fadhili nilizomwahidi Daudi.

4 Mimi nilimfanya kiongozi na kamanda wa mataifa ili yeye anishuhudie kwa watu wa mataifa.

5 Sasa utayaita mataifa usiyoyajua, watu wa mataifa yasiyokutambua watakujia mbio, kwa sababu yangu mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako; kwa sababu yangu mimi Mtakatifu wa Israeli niliyekufanya wewe utukuke.”

6 Mtafuteni Mwenyezi-Mungu wakati bado anapatikana, mwombeni msaada wakati yupo bado karibu.

7 Waovu na waache njia zao mbaya, watu wabaya waachane na mawazo yao mabaya; wamrudie Mwenyezi-Mungu apate kuwahurumia, wamwendee Mungu wetu maana atawasamehe.

8 Maana, Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Mawazo yangu si kama mawazo yenu, wala njia zangu si kama njia zenu.

9 Kama vile mbingu zilivyo mbali na dunia, ndivyo njia zangu zilivyo mbali na zenu, na mawazo yangu mbali na mawazo yenu.

10 “Kama vile mvua na theluji ishukavyo toka mbinguni, wala hairudi huko bali huinywesha ardhi, ikaifanya ichipue mimea ikakua, ikampatia mpanzi mbegu na kuwapa watu chakula,

11 vivyo hivyo na neno langu mimi: Halitanirudia bila mafanikio, bali litatekeleza matakwa yangu, litafanikiwa lengo nililoliwekea.

12 “Mtatoka Babuloni kwa furaha; mtaongozwa mwende kwa amani. Milima na vilima mbele yenu vitapaza sauti na kuimba, na miti yote mashambani itawapigia makofi.

13 Badala ya michongoma kutamea misonobari, na badala ya mbigili kutamea mihadasi. Hilo litakuwa jambo litakalowakumbusha watu juu ya mambo niliyotenda mimi Mwenyezi-Mungu; ishara ya milele ambayo haitafutwa.”

56

1 Mwenyezi-Mungu asema: “Zingatieni haki na kutenda mema, maana nitawaokoeni hivi karibuni, watu wataona wazi kwamba ninawakomboeni.

2 Heri mtu anayezingatia kikamilifu ninayosema, anayeshika sheria ya Sabato kwa heshima na kuepa kutenda uovu wowote.

3 “Mgeni anayenitambua mimi Mwenyezi-Mungu asifikiri: ‘Hakika Mwenyezi-Mungu atanitenga na watu wake.’ Naye towashi asiseme: ‘Mimi ni mti mkavu tu!’

4 Maana mimi Mwenyezi-Mungu nasema: Towashi ashikaye sheria zangu za Sabato, anayefanya mambo yanayonipendeza, na kulizingatia agano langu,

5 nitampa nafasi maalumu na ya sifa katika nyumba yangu na kuta zake; nafasi bora kuliko kuwa na watoto wa kiume na wa kike: Nitampa jina la kukumbukwa daima, na ambalo halitafutwa kamwe.

6 “Watu wageni watakaonikiri mimi Mwenyezi-Mungu, watakaoniheshimu, wakapenda jina langu na kuwa watumishi wangu, wote watakaoshika Sabato bila kuikufuru, watu watakaozingatia agano langu,

7 hao nitawaleta katika mlima wangu mtakatifu, na kuwafurahisha katika nyumba yangu ya sala; tambiko na sadaka zao zitakubaliwa madhabahuni pangu. Maana nyumba yangu itaitwa: ‘Nyumba ya sala kwa ajili ya watu wote’.

8 “Hii ni kauli yangu mimi Bwana Mwenyezi-Mungu ninayewakusanya Waisraeli waliotawanyika. Licha ya hao niliokwisha kukusanya, nitawakusanya watu wengine wajumuike nao.”

9 Enyi wanyama wote wakali, nanyi wanyama wote wa mwituni, njoni muwatafune watu wangu.

10 Maana viongozi wao wote ni vipofu; wote hawana akili yoyote. Wote ni kama mbwa bubu wasiobweka, hulala tu na kuota ndoto, hupenda sana kusinzia!

11 Hao ni kama mbwa wenye uchu sana, wala hawawezi kamwe kutoshelezwa. Wachungaji hao hawana akili yoyote; kila mmoja hutafuta faida yake mwenyewe.

12 Huambiana, “Njoni, twende kutafuta divai; njoni tunywe tushibe pombe! Kesho itakuwa kama leo, tena itakuwa sikukuu kubwa zaidi.”

57

1 Mtu mwadilifu akifa, hakuna mtu anayejali; mtu mwema akifariki, hakuna mtu anayefikiri na kusema: “Mtu huyo mwema ameondolewa asipatwe na maafa,

2 ili apate kuingia kwenye amani.” Watu wanaofuata njia ya haki, watakuwa na amani na kupumzika.

3 Lakini Mwenyezi-Mungu asema: “Njoni hapa nyinyi wana wa wachawi; nyinyi wazawa wa wachawi, wazinzi na malaya.

4 Je, mnadhani mnamdhihaki nani? Mnamfyonya nani na kumtolea ulimi? Nyinyi wenyewe ni wahalifu tangu mwanzo, nyinyi ni kizazi kidanganyifu.

5 Nyinyi mnawaka tamaa kwenye miti ya mialoni, na katika kila mti wa majani mabichi. Mnawachinja watoto wenu na kuwatambika katika mabonde na nyufa za majabali.

6 Mnachagua mawe laini mabondeni, na kuyafanya kitovu cha maisha yenu. Mnayamiminia tambiko ya kinywaji na kuyapelekea tambiko ya nafaka! Je, mimi nitaridhishwa kwa vitu hivyo?

7 Mmeweka vitanda vyenu juu ya milima mikubwa, na kwenda huko kutoa tambiko.

8 Nyuma ya milango na miimo mmetundika kinyago chenu. Nyinyi mnaniacha mimi na kutandika na kuvipanua vitanda vyenu. Mnafanya mapatano na hao mliopenda vitanda vyao. Humo mnazitosheleza tamaa zenu mbaya, huku mnakodolea macho kinyago chenu.

9 Mnajitia marashi na manukato kwa wingi kisha mnakwenda kumwabudu Moleki. Mnawatuma wajumbe wenu huko na huko, kujitafutia miungu ya kuabudu; hata kuzimu walifika.

10 Mlichoshwa na safari zenu ndefu, hata hivyo hamkukata tamaa; mlijipatia nguvu mpya, ndiyo maana hamkuzimia.

11 “Mlimwogopa na kutishwa na nani hata mkasema uongo, mkaacha kunikumbuka mimi na kuacha kabisa kunifikiria? Mimi sikuwaambia kitu kwa muda mrefu; ndio maana labda mkaacha kuniheshimu!

12 Mnafikiri mnafanya sawa, lakini nitayafichua matendo yenu, nayo miungu yenu haitawafaa kitu.

13 Mtakapolia kuomba msaada, rundo la vinyago vyenu na liwaokoe! Upepo utavipeperushia mbali; naam, pumzi itavitupilia mbali. Lakini watakaokimbilia usalama kwangu, wataimiliki nchi, mlima wangu mtakatifu utakuwa mali yao.”

14 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Jengeni! Jengeni! Tayarisheni njia! Ondoeni vikwazo vyote njiani mwa watu wangu!”

15 Hivi ndivyo asemavyo Mungu aliye juu kabisa, aishiye milele na ambaye jina lake ni “Mtakatifu”: “Mimi nakaa huko juu, mahali patakatifu, nakaa pia na wenye majuto na wanyenyekevu. Mimi nitawatia moyo walio wanyenyekevu na kuwapa nguvu wenye majuto.

16 Maana sitaendelea kuwalaumu wala kuwakasirikia daima. La sivyo hao niliowaumba watadhoofika mbele yangu, nami ndiye niliyewapa pumzi yangu ya uhai.

17 Niliwakasirikia kwa sababu ya uovu na tamaa zao; niliwaadhibu, nikauficha uso wangu na kukasirika. Lakini wao waliendelea kufuata njia zao wenyewe.

18 Niliiona mienendo yao, lakini nitawaponya; nitawaongoza na kuwapa faraja, nitawatuliza hao wanaoomboleza.

19 Mimi nitawapa amani, amani kwa walio mbali na walio karibu! Mimi nitawaponya.

20 Lakini waovu ni kama bahari iliyochafuka, ambayo haiwezi kutulia; mawimbi yake hutupa tope na takataka.”

21 Mungu wangu asema hivi: “Watu waovu sitawapa amani.”

58

1 Mwenyezi-Mungu asema: “Piga kelele, wala usijizuie; paza sauti yako kama tarumbeta. Watangazie watu wangu makosa yao, waambie wazawa wa Yakobo dhambi zao.

2 Siku hata siku wananijia kuniabudu, wanatamani kujua mwongozo wangu, kana kwamba wao ni taifa litendalo haki, taifa lisilosahau sheria za Mungu wao. Wananitaka niamue kwa haki, na kutamani kukaa karibu na Mungu.

3 “Nyinyi mnaniuliza: ‘Mbona tunafunga lakini wewe huoni? Mbona tunajinyenyekesha, lakini wewe hujali?’ “Ukweli ni kwamba wakati mnapofunga, mnatafuta tu furaha yenu wenyewe, na kuwakandamiza wafanyakazi wenu!

4 Mnafunga, na kugombana na kupigana ngumi. Mkifunga namna hiyo maombi yenu hayatafika kwangu juu.

5 Mfungapo, nyinyi mnajitaabisha; mnaviinamisha vichwa vyenu kama unyasi, na kulalia nguo za magunia na majivu. Je, huo ndio mnaouita mfungo? Je, hiyo ni siku inayokubaliwa nami?

6 “La! Mfungo ninaotaka mimi ni huu: Kuwafungulia waliofungwa bila haki, kuziondoa kamba za utumwa, kuwaachia huru wanaokandamizwa, na kuvunjilia mbali udhalimu wote!

7 Mfungo wa kweli ni kuwagawia wenye njaa chakula chako, kuwakaribisha nyumbani kwako maskini wasio na makao, kuwavalisha wasio na nguo, bila kusahau kuwasaidia jamaa zenu.

8 “Mkifanya hivyo mtangara kama pambazuko, mkiwa wagonjwa mtapona haraka. Matendo yenu mema yatawatangulia, nami nitawalindeni kutoka nyuma kwa utukufu wangu.

9 Ndipo mtakapoomba, nami Mwenyezi-Mungu nitawaitikia; mtalia kwa sauti kuomba msaada, nami nitajibu, ‘Niko hapa!’ “Kama mkiiondoa dhuluma kati yenu, mkiacha kudharau wengine na kusema maovu,

10 mkiwapa chakula kwa ukarimu wenye njaa, mkitosheleza mahitaji ya wenye dhiki, mwanga utawaangazia nyakati za giza, giza lenu litakuwa kama mchana.

11 Mimi Mwenyezi-Mungu nitawaongozeni daima, nitatosheleza mahitaji yenu wakati wa shida. Nitawaimarisha mwilini, nanyi mtakuwa kama bustani iliyomwagiliwa maji, kama chemchemi ya maji ambayo maji yake hayakauki kamwe.

12 Magofu yenu ya kale yatajengwa; mtajenga upya juu ya misingi iliyoachwa zamani. Nanyi mtaitwa watu waliotengeneza upya kuta, watu waliozifanya barabara za mji zipitike tena.

13 “Kama ukiacha kufanya kazi siku ya Sabato, ukaacha shughuli zako siku yangu hiyo takatifu; kama ukiifanya siku yangu kuwa ya furaha, ukaiheshimu siku hiyo takatifu ya Mwenyezi-Mungu, ukaacha na shughuli zako na kupiga domo,

14 utapata furaha yako kwangu mimi Mwenyezi-Mungu, nitakupatia ushindi katika kila pingamizi nchini, nitakulisha mali ya Yakobo, babu yako. Mimi, Mwenyezi-Mungu, nimesema.”

59

1 Msifikiri mkono wa Mungu ni mfupi, hata asiweze kuwaokoeni; au masikio yake yamezibika, hata asiweze kuwasikieni.

2 Dhambi zenu ndizo zinazowatenga na Mungu wenu, dhambi zenu zimemfanya ajifiche mbali nanyi hata asiweze kuwasikieni.

3 Maana mikono yenu imetiwa najisi kwa mauaji, na vidole vyenu kwa matendo maovu. Midomo yenu imesema uongo, na ndimi zenu husema uovu.

4 Hakuna atoaye madai yake kwa haki, wala anayeshtaki kwa uaminifu. Mnategemea hoja batili; mnasema uongo. Mnatunga hila na kuzaa uovu.

5 Mnaangua mayai ya joka lenye sumu, mnafuma utando wa buibui. Anayekula mayai yenu hufa, na yakipasuliwa nyoka hutokea.

6 Utando wenu haufai kwa mavazi, watu hawawezi kujifunikia mnachofuma. Kazi zenu ni kazi za uovu, matendo yenu yote ni ukatili mtupu.

7 Mko mbioni kutenda maovu, mnaharakisha kumwaga damu isiyo na hatia. Mawazo yenu ni mawazo ya uovu, popote mwendapo mnaacha ukiwa na uharibifu.

8 Njia ya amani hamwijui kamwe; njia zenu zote ni za dhuluma. Mmejifanyia njia potovu, yeyote anayepitia humo hapati amani.

9 Ndio maana haki iko mbali nasi, maongozi ya uadilifu hayapo kwetu. Tunatazamia kupata mwanga kumbe ni giza tupu, twatazamia mwangaza, lakini twatembea gizani.

10 Kama vipofu twapapasapapasa ukuta; tunasitasita kama watu wasio na macho. Tunajikwaa mchana kana kwamba ni usiku, miongoni mwa wenye nguvu sisi ni kama wafu.

11 Twanguruma kama dubu, twaomboleza tena na tena kama hua. Twatazamia hukumu ya haki, lakini haipo, twatazamia wokovu, lakini uko mbali nasi.

12 Makosa yetu mbele yako ni mengi mno, dhambi zetu zashuhudia dhidi yetu. Naam, makosa yetu tunaandamana nayo, tunayajua maovu yetu.

13 Tumekuasi na kukukana ee Mwenyezi-Mungu, tumekataa kukufuata ewe Mungu wetu. Udhalimu na uasi ndivyo tunavyopania, mioyoni mwetu twatunga na kutoa maneno ya uongo.

14 Haki imewekwa kando, uadilifu uko mbali; ukweli unakanyagwa mahakamani, uaminifu haudiriki kuingia humo.

15 Ukweli umekosekana, naye anayeacha uovu hunyanyaswa. Mungu aliona mambo hayo, akachukizwa, alichukizwa kwamba hakuna haki.

16 Aliona kwamba hakuna mtu aliyejali, akashangaa kwamba hakuna aliyeingilia kati. Basi akaamua kunyosha mkono wake mwenyewe, uadilifu wake ukamhimiza.

17 Alivaa uadilifu kama vazi la kujikinga kifuani, na wokovu kama kofia ya chuma kichwani. Atajivika kisasi kama vazi, na kujifunika wivu kama joho.

18 Atawaadhibu maadui kadiri ya matendo yao, naam, ghadhabu yake na kisasi vitawapata maadui zake; atawaadhibu hata wakazi wa nchi za mbali.

19 Toka magharibi hadi mashariki, kila mtu atamcha Mwenyezi-Mungu na kutambua utukufu wake. Maana atakuja kama mto uendao kasi, mto unaosukumwa kwa upepo wa Mwenyezi-Mungu.

20 Naye atakuja Siyoni kama Mkombozi, Mkombozi wa wazawa wa Yakobo ambao wataachana na makosa yao. Asema Mwenyezi-Mungu.

21 Mwenyezi-Mungu asema: “Mimi nafanya nanyi agano hili: Roho yangu niliyowajazeni, maneno niliyoyaweka mdomoni mwenu, hayataondoka kwenu kamwe, wala kwa watoto na wajukuu zenu, tangu sasa na hata milele.”

60

1 Inuka ee Siyoni uangaze; maana mwanga unachomoza kwa ajili yako, utukufu wa Mwenyezi-Mungu unakuangaza.

2 Tazama, giza litaifunika dunia, giza nene litayafunika mataifa; lakini wewe, Mwenyezi-Mungu atakuangazia, utukufu wake utaonekana kwako.

3 Mataifa yataujia mwanga wako, wafalme waujia mwanga wa pambazuko lako.

4 Inua macho utazame pande zote; wote wanakusanyika waje kwako. Wanao wa kiume watafika toka mbali, wanao wa kike watabebwa mikononi.

5 Utaona na uso wako utangara, moyo wako utasisimka na kushangilia. Maana utajiri wa bahari utakutiririkia, mali za mataifa zitaletwa kwako.

6 Makundi ya ngamia yataifunika nchi yako, naam, ndama wa ngamia kutoka Midiani na Efa; wote kutoka Sheba watakuja. Watakuletea dhahabu na ubani, wakitangaza sifa za Mwenyezi-Mungu.

7 Makundi ya kondoo wa Kedari yatakusanywa kwako, utaweza kuwatumia kondoo madume wa Nebayothi kuwa kafara; utawatoa kuwa tambiko inayokubalika madhabahuni pa Mungu, naye ataitukuza nyumba yake tukufu.

8 Nani hao wanaopepea kama mawingu, kama njiwa wanaoruka kwenda viotani mwao?

9 Ni meli zitokazo nchi za mbali, zikitanguliwa na meli za Tarshishi. Zinawaleta watoto wako, pamoja na fedha na dhahabu yao, kwa sifa ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, kwa sifa ya Mungu, Mtukufu wa Israeli, maana amewafanya mtukuke.

10 Mwenyezi-Mungu asema: “Wageni watazijenga upya kuta zako, wafalme wao watakutumikia. Maana kwa hasira yangu nilikupiga, lakini kwa fadhili yangu nimekuhurumia.

11 Malango yako yatakuwa wazi daima; usiku na mchana hayatafungwa, ili watu wakuletee utajiri wa mataifa, pamoja na wafalme wao katika maandamano.

12 Kila ufalme au taifa lisilokutumikia litaangamia; mataifa hayo yatatokomezwa kabisa.

13 “Utaletewa fahari ya msitu wa Lebanoni: Mbao za miberoshi, mivinje na misonobari, zitumike kupamba mahali pa maskani yangu; nami nitaparembesha hapo ninapokaa.

14 Wazawa wa wale waliokudhulumu, watakuja na kukuinamia kwa heshima. Wote wale waliokudharau, watasujudu mbele ya miguu yako. Watakuita: ‘Mji wa Mwenyezi-Mungu’, ‘Siyoni, Mji wa Mtakatifu wa Israeli’.

15 “Wewe ulikuwa umeachwa na kuchukiwa, hakuna aliyependa hata kupitia kwako. Lakini sasa nitakufanya uwe na fahari milele, utakuwa mji wa furaha kizazi hata kizazi.

16 Utaletewa chakula na watu wa mataifa, naam, wafalme watakupatia chakula bora. Hapo utatambua kuwa mimi Mwenyezi-Mungu ni Mwokozi wako; mimi Mwenye Nguvu wa Yakobo ni Mkombozi wako.

17 “Badala ya shaba nitakuletea dhahabu, badala ya chuma nitakuletea fedha, badala ya miti, nitakuletea shaba, na badala ya mawe nitakuletea chuma. Amani itatawala juu yako, uadilifu utakuongoza.

18 Ukatili hautasikika tena nchini mwako; wala uharibifu na maangamizi ndani ya mipaka yako. Utaweza kuziita kuta zako: ‘Wokovu’, na malango yako: ‘Sifa’.

19 “Hutahitaji tena jua kukuangazia mchana, wala mwezi kukumulikia usiku; maana mimi Mwenyezi-Mungu ni mwanga wako milele; mimi Mungu wako nitakuwa fahari yako.

20 Mwanga wako mchana hautatua kama jua, wala mwangaza wako usiku kufifia kama mbalamwezi; maana Mwenyezi-Mungu ni mwanga wako milele, nazo siku zako za kuomboleza zitakoma.

21 Watu wako wote watakuwa waadilifu, nao wataimiliki nchi milele. Hao ni chipukizi nililopanda mimi, kazi ya mikono yangu kwa ajili ya utukufu wangu.

22 Aliye mdogo kati yenu atakuwa ukoo, aliye mdogo kuliko wote atakuwa taifa kubwa. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu; wakati ufikapo nitayatekeleza hayo haraka.”

61

1 Bwana Mwenyezi-Mungu amenijaza roho yake, maana Mwenyezi-Mungu ameniweka wakfu, akanituma niwaletee wanaokandamizwa habari njema, niwatibu waliovunjika moyo, niwatangazie mateka kwamba watapata uhuru, na wafungwa kwamba watafunguliwa.

2 Amenituma niutangaze mwaka wake wa neema, na siku ya Mungu wetu ya kulipiza kisasi; niwafariji wote wanaoomboleza;

3 niwape wale wanaoomboleza katika Siyoni taji la maua badala ya majivu, mafuta ya furaha badala ya maombolezo, vazi la sifa badala ya moyo mzito. Nao wataitwa mialoni madhubuti, aliyopanda Mwenyezi-Mungu kuonesha utukufu wake.

4 Watayajenga upya magofu ya zamani, wataisimika miji iliyoharibiwa hapo kwanza; wataitengeneza miji iliyobomolewa, uharibifu wa vizazi vingi vilivyopita.

5 Wageni watakuwa hapo kuwachungia mifugo yenu; watawalimia na kuwatunzia mizabibu yenu.

6 Nanyi mtaitwa: “Makuhani wa Mwenyezi-Mungu”, Mtaitwa: “Watumishi wake Mungu wetu”. Mtafaidika kwa utajiri wa mataifa, mtatukuka kwa mali zao.

7 Kwa vile mlipata aibu maradufu, watu wakaona kuwa fedheha ni majaliwa yenu, sasa mtapata eneo maradufu kuwa mali yenu, na furaha yenu itadumu milele.

8 “Mimi Mwenyezi-Mungu napenda haki; nachukia unyanganyi na uhalifu. Nitawatuza watu wangu kwa uaminifu, nitafanya nao agano la milele.

9 Wazawa wao watakuwa maarufu kati ya mataifa; watajulikana kuwa maarufu kati ya watu wengine. Kila atakayewaona atakiri kwamba wao ni watu aliowabariki Mwenyezi-Mungu.”

10 Nitafurahi sana kwa sababu ya Mwenyezi-Mungu, nafsi yangu itashangilia kwa sababu ya Mungu wangu. Maana amenivika vazi la wokovu, amenivalisha vazi la uadilifu, kama bwana arusi ajipambavyo kwa shada la maua, kama bibi arusi ajipambavyo kwa johari zake.

11 Hivyo, kama vile ardhi ioteshavyo mimea, na shamba lichipushavyo mbegu zilizopandwa humo, Mwenyezi-Mungu atasababisha uadilifu na sifa kuchomoza mbele ya mataifa yote.

62

1 Kwa ajili ya Siyoni sitakaa kimya, kwa ajili ya Yerusalemu sitatulia, mpaka kuokolewa kwake kuchomoze kama umeme, wokovu wake utokeze kama mwenge.

2 Mataifa watauona wokovu wako, wafalme wote watauona utukufu wako. Nawe utaitwa kwa jina jipya, jina atakalokupa Mwenyezi-Mungu mwenyewe.

3 Utakuwa taji zuri mkononi mwa Mwenyezi-Mungu; kilemba cha kifalme mkononi mwa Mungu wako.

4 Hutaitwa tena: “Aliyeachwa”, wala nchi yako haitaitwa: “Ukiwa”. Bali utaitwa: “Namfurahia,” na nchi yako itaitwa: “Aliyeolewa.” Maana Mwenyezi-Mungu amependezwa nawe, naye atakuwa kama mume wa nchi yako.

5 Maana kama kijana mwanamume amwoavyo msichana, ndivyo aliyekujenga atakavyokuwa mume wako. Kama bwana arusi afurahivyo juu ya bibi arusi, ndivyo Mungu atakavyofurahi juu yako.

6 “Juu ya kuta zako ee Yerusalemu nimeweka walinzi, usiku na mchana kamwe hawatakaa kimya.” Enyi mnaomkumbusha Mwenyezi-Mungu ahadi yake, msikae kimya;

7 msimpe hata nafasi ya kupumzika, mpaka atakapousimika mji wa Yerusalemu, na kuufanya uwe fahari ulimwenguni kote.

8 Mwenyezi-Mungu ameapa kwa mkono wake wa kulia, naam, ameapa kwa mkono wake wenye nguvu akisema: “Sitawapa tena maadui zako nafaka yako; wala wageni hawatakunywa tena divai yako ambayo umeitolea jasho.

9 Bali nyinyi mliyoivuna nafaka hiyo, mtaila na kunitukuza mimi Mwenyezi-Mungu. Nyinyi mliochuma zabibu hizo, mtakunywa divai yake katika nyua zangu takatifu.”

10 Wakazi wa Yerusalemu, tokeni, tokeni nje ya mji, watayarishieni njia watu wenu wanaorejea! Jengeni! Jengeni barabara na kuondoa mawe yote! Wekeni alama kwa ajili ya watu.

11 Mwenyezi-Mungu ametangaza duniani kote, waambie watu wa Siyoni: “Mkombozi wenu anakuja, zawadi yake iko pamoja naye na tuzo lake liko mbele yake.”

12 Nyinyi mtaitwa: “Watu Watakatifu”, “Watu waliokombolewa na Mwenyezi-Mungu.” Na Yerusalemu utaitwa: “Mji aupendao Mungu”, “Mji ambao Mungu hakuuacha.”

63

1 Ni nani huyu ajaye kutoka Edomu, anayefika kutoka Bosra na mavazi ya madoa mekundu? Ni nani huyo aliyevaa mavazi ya fahari, anatembea kwa nguvu zake kubwa? Ni mimi Mwenyezi-Mungu ninayetangaza ushindi wangu; nami ni mwenye nguvu ya kuokoa.

2 Lakini mbona nguo yako ni nyekundu, nyekundu kama ya mtu anayekamua zabibu?

3 “Naam, nimekamua zabibu peke yangu, wala hakuna mtu aliyekuja kunisaidia. Nimeyakanyaga mataifa kwa hasira yangu, niliyapondaponda kwa ghadhabu yangu. Nguo zangu zimejaa madoa ya damu yao, imeyachafua kabisa mavazi yangu.

4 Niliamua kuwa siku ya kulipiza kisasi imefika; wakati wa kuwakomboa watu wangu umefika.

5 Nilitazama na hapakuwa na wa kunisaidia; nilishangaa hapakuwa na wa kuniunga mkono. Lakini nilijipatia ushindi kwa mkono wangu, ghadhabu yangu ilinihimiza.

6 Kwa hasira yangu niliwaponda watu, niliwalewesha kwa ghadhabu yangu; damu yao niliimwaga chini ardhini.”

7 Nitasimulia fadhili za Mwenyezi-Mungu; nitataja matendo yake yote yastahiliyo sifa, kwa sababu ya yote aliyotutendea, wema wake mkuu aliowapa Waisraeli kwa huruma yake, kadiri ya wingi wa fadhili zake.

8 Maana alisema juu yao: “Hakika, hawa ni watu wangu; watoto wangu ambao hawatanidanganya.” Basi yeye akawa Mwokozi wao.

9 Katika taabu zao zote, hakumtuma mjumbe mwingine kuwasaidia, ila yeye mwenyewe alikuja kuwaokoa. kwa upendo na huruma yake aliwakomboa. Aliwabeba na kuwachukua tangu zamani.

10 Lakini wao walikuwa wakaidi, wakaihuzunisha roho yake takatifu. Basi, Mungu akageuka, akawa adui yao; yeye mwenyewe akapigana nao.

11 Ndipo walipokumbuka siku za zamani, wakati wa Mose mtumishi wa Mwenyezi-Mungu. Wakauliza, “Yuko wapi sasa Mwenyezi-Mungu, aliyewaokoa wachungaji wa kundi lake baharini? Yuko wapi yule aliyeiweka roho yake takatifu kati yao,

12 ambaye kwa mkono wake wenye nguvu alifanya maajabu kwa njia ya Mose, akapasua bahari na kuwaongoza watu wake, na kujipatia jina la milele?

13 Aliwaongoza katikati ya vilindi vya bahari, wakapita humo kama farasi bila kujikwaa.

14 Kama ng'ombe wapelekwavyo malishoni bondeni, ndivyo roho ya Mungu ilivyowapumzisha watu wake. Ndivyo ee Mungu ulivyowaongoza watu wako, nawe ukajipatia jina tukufu.”

15 Ututazame kutoka mbinguni ee Mungu, uone, utuangalie kutoka makao yako matakatifu na matukufu. Iko wapi bidii yako kwa ajili yetu na nguvu yako? Usiache kutuonesha upendo wako.

16 Maana wewe ndiwe Baba yetu; Abrahamu, mzee wetu, hatujali, naye Israeli hatutambui; lakini wewe, ee Mwenyezi-Mungu, ni Baba yetu. Wewe umeitwa tangu kale: “Mkombozi wetu.”

17 Ee Mwenyezi-Mungu, mbona unatukosesha njia zako? Mbona unatufanya kuwa wakaidi hata tusikuogope? Rudi ee Mungu kwa ajili ya watumishi wako, makabila ambayo daima yalikuwa mali yako.

18 Kwa kitambo tu sisi watakatifu wako tulimiliki nchi, lakini maadui zetu wakaja wakaharibu maskani yako.

19 Tumekuwa kama watu ambao hujawatawala kamwe, kama watu ambao hawakujulikana kwa jina lako.

64

1 Laiti ungalizipasua mbingu ukashuka chini, milima ikakuona na kutetemeka kwa hofu!

2 Ingeteketea kama moto uchomavyo kichaka, kama vile moto uchemshavyo maji. Njoo upate kuwajulisha maadui zako jina lako nayo mataifa yatetemeke kwa kuwako kwako!

3 Wakati ulipotenda maajabu ambayo hatukutazamia, ulishuka chini nayo milima ikatetemeka ilipokuona.

4 Tangu kale hakuna aliyepata kuona wala kusikia kwa masikio yake; hakuna aliyepata kumwona Mungu aliye kama wewe atendaye mambo kwa ajili ya wale wanaomtegemea!

5 Wewe waja kuwasaidia watendao haki kwa furaha, wanaokukumbuka na kuzingatia njia zako. Ulitukasirikia tulipokuwa wenye dhambi; sisi tumeasi kwa muda mrefu.

6 Sote tumekuwa kama watu walio najisi; matendo yetu yote mema ni kama nguo chafu. Sote tunanyauka kama majani, uovu wetu watupeperusha kama upepo.

7 Hakuna hata mmoja anayekuja kukuomba; hakuna anayejishughulisha kukutafuta. Wewe unauficha uso wako mbali nasi, umetuacha tukumbwe na maovu yetu.

8 Hata hivyo, ee Mwenyezi-Mungu, wewe ni Baba yetu. Sisi ni kama udongo, wewe ni mfinyanzi. Sisi sote ni kazi ya mikono yako.

9 Usitukasirikie mno, ee Mwenyezi-Mungu, usiukumbuke uovu wetu daima! Ukumbuke kwamba sisi sote ni watu wako!

10 Miji yako mitakatifu imekuwa nyika; Siyoni umekuwa mahame, Yerusalemu umekuwa uharibifu.

11 Nyumba yetu takatifu na nzuri, ambamo wazee wetu walikusifu, imeteketezwa kwa moto. Mahali petu pote pazuri pamekuwa magofu.

12 Je, kwa hayo yote utajizuia usifanye kitu? Je, utaendelea kunyamaza tu, ee Mwenyezi-Mungu, na kututesa kupita kiasi?

65

1 Mwenyezi-Mungu asema; “Nilikuwa tayari kujionesha kwao wasiouliza habari zangu. Nilikuwa tayari kuwapokea wale wasionitafuta. Nililiambia taifa ambalo halikuomba kwa jina langu: ‘Nipo hapa! Nipo hapa!’

2 Mchana kutwa niliwanyoshea mikono watu waasi, watu ambao hufuata njia zisizo sawa, watu ambao hufuata fikira zao wenyewe.

3 Ni watu ambao daima hunichokoza waziwazi; hutambikia miungu yao katika bustani, na kuifukizia ubani juu ya matofali.

4 Huketi makaburini na kukaa mafichoni usiku. Hula nyama ya nguruwe na mchuzi wa wanyama haramu.

5 Huwaambia wale wanaokutana nao: ‘Kaeni mbali nami; msinikaribie kwani mimi ni mtakatifu!’ Watu hao wananikasirisha mno, hasira yangu ni kama moto usiozimika.

6 “Jueni kuwa nimelitia jambo hilo moyoni, sitanyamaza bali nitawafanya walipe; nitawafanya walipe kwa wingi.

7 Mimi Mwenyezi-Mungu, nitawalipiza maovu yao wayalipie na maovu ya wazee wao. Wao waliifukizia ubani miungu yao milimani, wakanitukana mimi huko vilimani. Nitawafanya walipe kwa wingi, watayalipia matendo yao ya awali.”

8 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Mtu akikuta kishada cha zabibu nzuri, watu husema: ‘Tusikiharibu; kina baraka.’ Ndivyo nitakavyofanya kwa ajili ya watumishi wangu; sitawaangamiza wote.

9 Nitawajalia watu wa Yakobo, na Yuda nitamjalia warithi wa milima yangu; watumishi wangu watakaa huko.

10 Nchi tambarare ya Sharoni itakuwa malisho, bonde la Akori litakuwa mapumziko ya mifugo kwa ajili ya watu wangu walionitafuta.

11 “Lakini nitafanya nini na nyinyi mnaoniacha mimi Mwenyezi-Mungu, msioujali Siyoni, mlima wangu mtakatifu, nyinyi mnaoabudu mungu ‘Gadi’, na kumtolea tambiko ya divai mungu ‘Meni’?

12 Nimewapangia kifo kwa upanga, nyote mtaangukia machinjoni! Maana, nilipowaita, hamkuniitikia; niliponena, hamkunisikiliza. Mlitenda yaliyo maovu mbele yangu, mkachagua yale nisiyoyapenda.

13 Basi, mimi Mwenyezi-Mungu nasema, watumishi wangu watakula, lakini nyinyi mtaona njaa; watumishi wangu watakunywa, lakini nyinyi mtaona kiu; watumishi wangu watafurahi, lakini nyinyi mtafedheheka.

14 Watumishi wangu wataimba kwa furaha moyoni, lakini nyinyi mtalia kwa uchungu moyoni na kupiga kelele kwa uchungu mkubwa rohoni.

15 Wale niliowachagua nitawapa jina jipya. Lakini nyinyi jina lenu watalitumia kulaania; ‘Watasema: Bwana Mungu awaue kama hao.’

16 Basi, mwenye kujitakia baraka nchini, atajitakia baraka kwa Mungu wa kweli. Mwenye kuapa katika nchi hii, ataapa kwa Mungu wa kweli. Maana taabu za zamani zimepita zimetoweka kabisa mbele yangu.

17 “Sasa, naumba mbingu mpya na dunia mpya. mambo ya zamani hayatakumbukwa tena.

18 Furahini, mkashangilie milele, kwa ajili ya vitu hivi ninavyoumba. Yerusalemu nitaufanya mji wa shangwe, na watu wake watu wenye furaha.

19 Nami nitaufurahia mji wa Yerusalemu, nitawafurahia watu wangu. Sauti ya kilio haitasikika tena, kilio cha taabu hakitakuwako.

20 Hakutakuwa tena na vifo vya watoto wachanga, wazee nao hawatakufa kabla ya wakati wao. Akifa mtu wa miaka 100 amekufa akiwa kijana; na akifa kabla ya miaka 100 ni balaa.

21 Watu watajenga nyumba na kuishi humo; watalima mizabibu na kula matunda yake.

22 Hawatajenga nyumba zikaliwe na watu wengine, wala kulima chakula kiliwe na watu wengine. Maana watu wangu niliowachagua wataishi maisha marefu kama miti; wateule wangu watafurahia matunda ya jasho lao.

23 Kazi zao hazitakuwa bure, wala hawatazaa watoto wa kupata maafa; maana watakuwa waliobarikiwa na Mwenyezi-Mungu, wamebarikiwa wao pamoja na wazawa wao.

24 Hata kabla hawajaniita, mimi nitawaitikia; kabla hawajamaliza kusema, nitakuwa nimewajibu.

25 Mbwamwitu na kondoo watakula pamoja, simba watakula nyasi kama ng'ombe, nao nyoka chakula chao kitakuwa vumbi. Katika mlima wangu wote mtakatifu, hakuna atakayeumiza au kuharibu kitu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”

66

1 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Mbingu ni kiti changu cha enzi, dunia ni kiti cha kuwekea miguu yangu. Mtanijengea nyumba ya namna gani basi, Mahali nitakapoweza kupumzika?

2 Mimi mwenyewe nilivifanya vitu hivi vyote, na hivi vyote ni mali yangu. Lakini ninachojali mimi ni mtu mnyenyekevu na mwenye majuto, mtu anayetetemeka asikiapo neno langu.

3 “Lakini watu hawa wanafanya wanavyotaka: Wananitolea tambiko ya ng'ombe na mara wanaua watu kutambikia. Wananitolea sadaka ya mwanakondoo na pia wanamvunja mbwa shingo. Wananitolea tambiko ya nafaka na pia kupeleka damu ya nguruwe. Wanachoma ubani mbele yangu na kwenda kuabudu miungu ya uongo. Hao wamechagua kufuata njia zao wenyewe.

4 Basi, nitawaletea taabu; yatawapata yaleyale wanayoyahofia; maana nilipoita hakuna aliyeitika, niliponena hawakusikiliza. Bali walifanya yaliyo maovu mbele yangu, walichagua yale ambayo hayanipendezi.”

5 Sikilizeni neno la Mwenyezi-Mungu, enyi msikiao neno lake mkatetemeka: “Ndugu zenu ambao wanawachukia, na kuwapiga marufuku kwa sababu yangu, wamesema kwa dharau ‘Mungu na aoneshe utukufu wake, nasi tuwaone nyinyi mkishinda!’ Lakini wao wenyewe ndio watakaoaibishwa!

6 Sikilizeni, ghasia kutoka mjini, sauti kutoka hekaluni! Hiyo ni sauti ya Mwenyezi-Mungu akiwaadhibu maadui zake!

7 “Mji wangu mtakatifu, ni kama mama ajifunguaye bila kuona uchungu; kabla uchungu kuanza, amekwisha zaa mtoto.

8 Ni nani aliyepata kusikia jambo kama hilo? Ni nani aliyewahi kuona jambo kama hilo? Je, nchi nzima yaweza kuzaliwa siku moja? Je, taifa zima laweza kuzaliwa mara moja? Maana Siyoni, mara tu alipoanza kuona uchungu, alijifungua watoto wake.

9 Je, nitawatunza watu wangu mpaka karibu wazaliwe, halafu niwazuie wasizaliwe? Au mimi mwenye kuwajalia watoto, nitafunga kizazi chao? Mimi Mungu wenu nimesema.”

10 Shangilieni na kufurahi pamoja na Yerusalemu enyi mnaoupenda! Shangilieni pamoja nao enyi nyote mlioulilia!

11 Kama mama, Yerusalemu utawanyonyesha, nanyi mtashiba kwa riziki zake; mtakunywa shibe yenu na kufurahi, kutokana na wingi wa fahari yake.

12 Maana Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Nitakuletea fanaka nyingi kama mto, utajiri wa mataifa kama mto uliofurika. Nanyi mtanyonya na kubebwa kama mtoto mchanga, mtabembelezwa kama mtoto magotini mwa mama yake.

13 Kama mama amtulizavyo mwanawe, kadhalika nami nitawatuliza; mtatulizwa mjini Yerusalemu.

14 Mtayaona hayo na mioyo yenu itafurahi; mifupa yenu itapata nguvu kama majani mabichi. Hapo itajulikana kuwa mimi Mwenyezi-Mungu huwalinda watumishi wangu, lakini nikikasirika huwaadhibu maadui zangu.”

15 Mwenyezi-Mungu atakuja kama moto, na magari yake ya vita ni kimbunga. Ataiacha hasira yake ifanye kazi yake kwa ukali, na onyo lake litekelezwe kwa miali ya moto.

16 Mwenyezi-Mungu atatoa hukumu kwa moto, atawaadhibu watu wote kwa upanga; nao atakaowaangamiza watakuwa wengi.

17 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Wapo watu wanaojitakasa na kutawadha wapate kuingia kwenye bustani za ibada za sanamu; wanafanya maandamano na kuhani akiwa kati yao. Watu hao hula nguruwe, panya na vyakula vingine haramu. Watu hao hakika watakufa wote pamoja.

18 Nayajua matendo yao na mawazo yao. Naja kuwakusanya watu wa mataifa yote na lugha zote, wajumuike pamoja na kuuona utukufu wangu.

19 Nitaweka kati yao alama ya uwezo wangu. Watakaosalimika kati yao nitawapeleka kwa watu wa mataifa huko Tarshishi, Puti, Ludi, nchi zenye wapiga upinde stadi; watakwenda pia Tubali na Yowani na nchi ambapo watu hawajapata kusikia umaarufu wangu wala kuuona utukufu wangu. Hao wajumbe wangu watautangaza utukufu wangu katika mataifa hayo.

20 Watawarejesha ndugu zenu wote kutoka katika mataifa yote kama matoleo yangu mimi Mwenyezi-Mungu. Watawaleta wamepanda farasi, nyumbu, ngamia na magari ya farasi mpaka Yerusalemu, kwenye mlima wangu mtakatifu. Watawaleta kama Waisraeli waletavyo sadaka ya nafaka katika chombo safi hadi nyumbani kwangu mimi Mwenyezi-Mungu.

21 Pia nitawachagua baadhi yao kuwa makuhani na baadhi yao kuwa Walawi. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.

22 “Kama vile mbingu mpya na dunia mpya nitakazoumba zitakavyodumu milele kwa uwezo wangu, ndivyo wazawa wako na jina lako litakavyodumu.

23 Katika kila sikukuu ya mwezi mpya, na katika kila siku ya Sabato, binadamu wote watakuja kuniabudu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.

24 “Kisha watakwenda kuziona maiti za wale walioniasi. Wadudu watakaowala hawatakufa, na moto utakaowachoma hautazimika kamwe. Watakuwa chukizo kwa watu wote.”