1 Yafuatayo ni maneno ya Yeremia mwana wa Hilkia, mmoja wa makuhani wa mji wa Anathothi, katika nchi ya Benyamini.
2 Neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Yeremia mnamo mwaka wa kumi na tatu wa utawala wa Yosia mwana wa Amoni, mfalme wa Yuda.
3 Lilimjia tena wakati Yehoyakimu mwana wa Yosia, alipokuwa mfalme wa Yuda. Yeremia aliendelea kupata neno la Mwenyezi-Mungu hadi mwishoni mwa mwaka wa kumi na moja wa utawala wa Sedekia mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda. Mnamo mwezi wa tano wa mwaka huo, watu wa Yerusalemu walipelekwa uhamishoni.
4 Mwenyezi-Mungu aliniambia neno lake:
5 “Kabla hujachukuliwa mimba, mimi nilikujua, kabla hujazaliwa, mimi nilikuweka wakfu; nilikuteua uwe nabii kwa mataifa.”
6 Nami nikajibu, Aa! Bwana Mwenyezi-Mungu, mimi sijui kusema, kwa kuwa bado ningali kijana.
7 Lakini Mwenyezi-Mungu akaniambia, “Usiseme kwamba wewe ni kijana bado. Utakwenda kwa watu wote nitakaokutuma kwao, na yote nitakayokuamuru utayasema.
8 Wewe usiwaogope watu hao, kwa maana niko pamoja nawe kukulinda. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
9 Kisha Mwenyezi-Mungu akaunyosha mkono wake, akagusa kinywa changu, akaniambia, “Tazama nimeyatia maneno yangu kinywani mwako.
10 Leo nimekupa mamlaka juu ya mataifa na falme, uwe na mamlaka ya kungoa na kubomoa, mamlaka ya kuharibu na kuangamiza, mamlaka ya kujenga na ya kupanda.”
11 Neno la Mwenyezi-Mungu lilinijia: “Yeremia, unaona nini?” Nami nikasema, “Ninaona tawi la mlozi unaochanua.”
12 Mwenyezi-Mungu akaniambia, “Umeona vizuri, maana niko macho kulitekeleza neno langu.”
13 Neno la Mwenyezi-Mungu likanijia mara ya pili: “Unaona nini?” Nami nikasema, “Ninaona chungu kinatokota kimeinama upande wangu kutoka kaskazini.”
14 Mwenyezi-Mungu akaniambia, “Maangamizi yataanzia kutoka kaskazini na kuwapata wakazi wote wa nchi hii.
15 Maana naziita falme zote za kaskazini na makabila yote. Wafalme wake wote watakuja na kila mmoja wao ataweka kiti chake cha enzi mbele ya malango ya Yerusalemu na kandokando ya kuta zake zote, na kuizunguka miji yote ya Yuda.
16 Nami nitawahukumu Waisraeli kwa ajili ya uovu wao wote wa kuniacha mimi, wakafukizia ubani miungu mingine na kuabudu sanamu walizojitengenezea wenyewe.
17 Sasa basi, wewe Yeremia jiweke tayari. Haya! Nenda ukawaambie mambo yote ninayokuamuru. Usiwaogope, nisije nikakufanya mwoga mbele yao.
18 Leo hii nakufanya kuwa imara kama mji uliozungukwa na ngome, kama mnara wa chuma na kama ukuta wa shaba nyeusi, dhidi ya nchi yote, dhidi ya wafalme wa Yuda, wakuu wake, makuhani wake na watu wake wote.
19 Watapigana nawe, lakini hawatashinda kwa sababu mimi niko pamoja nawe kukuokoa. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
1 Neno la Mwenyezi-Mungu likanijia:
2 “Nenda ukawatangazie waziwazi wakazi wote wa Yerusalemu kuwa mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Naukumbuka uaminifu wako ulipokuwa kijana, jinsi ulivyonipenda kama mchumba wako, ulivyonifuata jangwani kwenye nchi ambayo haikupandwa kitu.
3 Israeli, wewe ulikuwa mtakatifu kwangu, ulikuwa matunda ya kwanza ya mavuno yangu. Wote waliokudhuru walikuwa na hatia, wakapatwa na maafa. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
4 Sikilizeni neno la Mwenyezi-Mungu, enyi wazawa wa Yakobo. Sikilizeni enyi jamaa zote za wazawa wa Israeli.
5 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Wazee wenu waliona kosa gani kwangu hata wakanigeuka na kuniacha, wakakimbilia miungu duni, hata nao wakawa watu duni?
6 Hawakujiuliza: ‘Yuko wapi Mwenyezi-Mungu aliyetutoa nchini Misri, aliyetuongoza nyikani katika nchi ya jangwa na makorongo, nchi kame na yenye giza nene, nchi isiyopitiwa na mtu yeyote, wala kukaliwa na binadamu?’
7 Niliwaleta katika nchi yenye rutuba, muyafurahie mazao yake na mema yake mengine. Lakini mlipofika tu mliichafua nchi yangu, mkaifanya chukizo nchi niliyowapa iwe yenu.
8 Nao makuhani hawakujiuliza: ‘Yuko wapi Mwenyezi-Mungu?’ Wataalamu wa sheria hawakunijua, viongozi wa watu waliniasi; manabii nao walitabiri kwa jina la Baali na kuabudu sanamu zisizo na faida yoyote.”
9 Mwenyezi-Mungu asema, “Kwa hiyo, mimi nitawalaumu nyinyi, na nitawalaumu wazawa wenu.
10 Haya, vukeni bahari hadi Kupro mkaone, au tumeni watu huko Kedari wakachunguze, kama jambo kama hili limewahi kutokea:
11 Kwamba kuna taifa lililowahi kubadilisha miungu yake ingawa miungu hiyo si miungu! Lakini watu wangu wameniacha mimi, utukufu wao, wakafuata miungu isiyofaa kitu.
12 Shangaeni enyi mbingu, juu ya jambo hili, mkastaajabu na kufadhaika kabisa. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
13 Maana, watu wangu wametenda maovu mawili; wameniacha mimi niliye chemchemi ya maji ya uhai, wakajichimbia visima vyao wenyewe, visima vyenye nyufa, visivyoweza kuhifadhi maji.
14 “Je, Israeli ni mtumwa, ama amezaliwa utumwani? Mbona basi amekuwa kama mawindo?
15 Simba wanamngurumia, wananguruma kwa sauti kubwa. Nchi yake wameifanya jangwa, miji yake imekuwa magofu, haina watu.
16 Isitoshe, watu wa Memfisi na Tahpanesi, wameuvunja utosi wake.
17 Israeli, je, hayo yote si umejiletea mwenyewe, kwa kuniacha mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, niliyekuwa ninakuongoza njiani?
18 Na sasa itakufaa nini kwenda Misri, kunywa maji ya mto Nili? Au itakufaa nini kwenda Ashuru, kunywa maji ya mto Eufrate?
19 Uovu wako utakuadhibu; na uasi wako utakuhukumu. Ujue na kutambua kuwa ni vibaya mno kuniacha mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, na kuondoa uchaji wangu ndani yako. Mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi nimesema.
20 “Tangu zamani wewe ulivunja nira yako, ukaikatilia mbali minyororo yako, ukasema, ‘Sitakutumikia’. Juu ya kila kilima kirefu na chini ya kila mti wa majani mabichi, uliinamia miungu ya rutuba kama kahaba.
21 Lakini mimi nilikupanda kama mzabibu mteule, mzabibu wenye afya na wa mbegu safi; mbona basi umeharibika, ukageuka kuwa mzabibu mwitu?
22 Hata ukijiosha kwa magadi, na kutumia sabuni nyingi, madoa ya uovu wako bado yatabaki mbele yangu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
23 “Unawezaje kusema, ‘Mimi si najisi; sijawafuata Mabaali?’ Tazama ulivyotenda dhambi kule bondeni; angalia ulivyofanya huko! Wewe ni kama mtamba wa ngamia, akimbiaye huko na huko;
24 kama pundamwitu aliyezoea jangwani. Katika tamaa yake hunusanusa upepo; nani awezaye kuizuia hamu yake? Amtakaye hana haja ya kujisumbua; wakati wake ufikapo watampata tu.
25 Israeli, usiichakaze miguu yako wala usilikaushe koo lako. Lakini wewe wasema: ‘Hakuna tumaini lolote. Nimeipenda miungu ya kigeni, hiyo ndiyo nitakayoifuata.’
26 “Kama vile mwizi aonavyo aibu akishikwa, ndivyo Waisraeli watakavyoona aibu; wao wenyewe, wafalme wao, wakuu wao, makuhani wao na manabii wao.
27 Hao huuambia mti: ‘Wewe u baba yangu,’ na jiwe: ‘Wewe ndiwe uliyenizaa;’ kwa maana wamenipa kisogo, wala hawakunielekezea nyuso zao. Lakini wakati wa shida husema: ‘Inuka utuokoe!’
28 “Lakini iko wapi miungu yako uliyojifanyia? Iinuke basi, kama inaweza kukusaidia, wakati unapokuwa katika shida. Ee Yuda, idadi ya miungu yako ni sawa na idadi ya miji yako!
29 Mbona mnanilalamikia? Nyinyi nyote mmeniasi. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
30 Niliwaadhibu watu wako bila kufanikiwa, wao wenyewe walikataa kukosolewa. Upanga wako uliwamaliza manabii wako kama simba mwenye uchu.
31 Enyi watu! Sikilizeni ninachosema mimi Mwenyezi-Mungu: Je, nimekuwa jangwa kwa Israeli au nchi yenye giza nene? Kwa nini basi watu wangu waseme: ‘Sisi tu watu huru; hatutakuja kwako tena!’
32 Kijana msichana aweza kusahau mapambo yake au bibi arusi mavazi yake? Lakini watu wangu wamenisahau kwa muda wa siku zisizohesabika.
33 Kweli wewe ni bingwa wa kutafuta wapenzi! Hata wanawake wabaya huwafundisha njia zako.
34 Nguo zako zina damu ya maskini wasio na hatia, japo hukuwakuta wakivunja nyumba yako. “Lakini licha ya hayo yote,
35 wewe wasema: ‘Mimi sina hatia; hakika hasira yake imegeuka mbali nami.’ Lakini mimi nitakuhukumu kwa sababu unasema: ‘Sikutenda dhambi.’
36 Kwa nini unajirahisisha hivi, ukibadilibadili mwenendo wako? Utaaibishwa na Misri, kama ulivyoaibishwa na Ashuru.
37 Na huko pia utatoka, mikono kichwani kwa aibu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimewakataa wale uliowategemea, wala hutafanikiwa kwa msaada wao.
1 “Mume akimpa talaka mkewe, naye akaondoka kwake, na kuwa mke wa mwanamume mwingine, je mume yule aweza kumrudia mwanamke huyo? Je, kufanya hivyo hakutaitia nchi unajisi mkubwa? Wewe Israeli, umefanya ukahaba na wapenzi wengi, je, sasa unataka kunirudia mimi?
2 Inua macho uvitazame vilele vya vilima! Pako wapi mahali ambapo hawajalala nawe? Uliwangoja wapenzi wako kando ya njia, kama bedui aviziavyo watu jangwani. Umeifanya nchi kuwa najisi, kwa ukahaba wako mbaya kupindukia.
3 Ndiyo maana manyunyu yamezuiliwa, na wala mvua za vuli hazijanyesha. Hata hivyo uko macho makavu kama kahaba, huna haya hata kidogo.
4 “Hivi punde tu si ulinililia ukisema: ‘Wewe u baba yangu, ulinipenda tangu utoto wangu?
5 Je, utanikasirikia daima? Utachukizwa nami milele?’ Israeli, hivyo ndivyo unavyosema; na kumbe umetenda uovu wote ulioweza.”
6 Wakati wa utawala wa mfalme Yosia, Mwenyezi-Mungu aliniambia hivi: “Je, umeona jinsi Israeli asiye mwaminifu alivyofanya? Aliniacha, akapanda juu ya kila kilima kirefu na kwenda chini ya kila mti wenye majani mabichi, akafanya ukahaba wake humo!
7 Mimi nilidhani kuwa baada ya kufanya yote hayo, atanirudia. Lakini wapi; hakunirudia. Yuda, dada yake mdanganyifu, alishuhudia yote hayo.
8 Zaidi ya hayo, Yuda alishuhudia kuwa nilimpa Israeli talaka kwa sababu ya ukahaba wake na kwa kukosa uaminifu kwangu. Lakini hata hivyo, Yuda, dada yake mdanganyifu, hakuogopa; naye pia alikwenda na kufanya ukahaba!
9 Na, kwa kuwa yeye aliona kuwa ukahaba ni jambo dogo sana kwake, aliitia nchi unajisi, na kufanya ukahaba kwa kuabudu mawe na miti.
10 Pamoja na hayo yote, Yuda, dada mdanganyifu wa Israeli, hakunirudia kwa moyo wote, bali kwa unafiki tu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
11 Mwenyezi-Mungu akaniambia, “Mwasi Israeli amedhihirisha kuwa yeye ni afadhali kuliko Yuda mdanganyifu.
12 Basi, nenda ukamtangazie Israeli maneno yafuatayo: Rudi, ewe Israeli, usiye mwaminifu. Nami sitakutazama kwa hasira kwa kuwa mimi ni mwenye huruma. Naam, sitakukasirikia milele.
13 Wewe, kiri tu kosa lako: Kwamba umeniasi mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako; kwamba chini ya kila mti wenye majani, umewapa miungu wengine mapenzi yako wala hukuitii sauti yangu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
14 “Rudini, enyi watoto msio na uaminifu, maana, mimi ndimi Bwana wenu. Nitawachukua mmoja kutoka kila mji, na wawili kutoka katika kila ukoo, niwapeleke hadi mlimani Siyoni. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
15 “Nitawapeni wachungaji wanipendao moyoni, watakaowalisha kwa maarifa na busara.
16 Siku hizo, wakati mtakapokuwa mmeongezeka na kuwa wengi nchini, watu hawatalitajataja tena sanduku langu la agano. Hawatalifikiria kabisa, wala hawatalikumbuka tena; hawatalihitaji, wala hawataunda jingine.
17 Wakati huo, mji wa Yerusalemu utaitwa ‘Kiti cha Enzi cha Mwenyezi-Mungu’, na mataifa yote yatakusanyika humo mbele yangu. Hawatafuata tena ukaidi wa matendo yao.
18 Siku hizo, watu wa Yuda wataungana na watu wa Israeli, na wote kwa pamoja watatoka katika nchi ya kaskazini na kurudi katika nchi niliyowapa wazee wenu iwe mali yao.”
19 Mwenyezi-Mungu asema, “Israeli, mimi niliwaza, laiti ningekuweka miongoni mwa wanangu, na kukupa nchi nzuri ajabu, urithi usio na kifani kati ya mataifa yote. Nilidhani ungeniita, ‘Baba Yangu’, na kamwe usingeacha kunifuata.
20 Lakini kama mke asiye mwaminifu amwachavyo mumewe, ndivyo ulivyokosa uaminifu kwangu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
21 “Kelele zasikika juu ya vilima: Waisraeli wanalia na kuomboleza, kwa kuwa wamepotoka katika njia zao, wamenisahau mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wao.
22 Rudini, enyi watoto msio na uaminifu, mimi nitaponya utovu wenu wa uaminifu. “Nanyi mwasema: ‘Tazama, sisi tunarudi kwako, maana, wewe ndiwe Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu.
23 Kweli tumedanganyika mno kuabudu huko vilimani, hakika wokovu wa Israeli watoka kwake Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu.
24 “ ‘Tangu ujana wetu, tendo hili la aibu limeangamiza kila kitu walichotolea jasho wazee wetu: Makundi yao ya kondoo na ng'ombe, wana wao na binti zao.
25 Hatuna budi kujilaza chini kwa aibu, na kuiacha fedheha yetu itufunike. Tangu ujana wetu hadi leo hii, wazee wetu na sisi wenyewe tumetenda dhambi mbele ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, wala hatukumtii Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu.’”
1 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Ukitaka kurudi ee Israeli, nirudie mimi. Ukiviondoa vitu vya kuchukiza mbele yangu, usipotangatanga huko na huko,
2 ukiapa kwa ukweli, unyofu na uadilifu, kwa kusema, ‘Kama Mwenyezi-Mungu aishivyo’, ndipo mataifa yatakapopata baraka kwangu, na kutukuka kwa sababu yangu.”
3 Mwenyezi-Mungu awaambia hivi watu wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu: “Limeni mashamba yenu mapya; msipande mbegu zenu penye miiba.
4 Enyi watu wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu, jitakaseni kwa ajili yangu mimi Mwenyezi-Mungu, wekeni mioyo yenu wazi mbele yangu. La sivyo, ghadhabu yangu itachomoza kama moto, iwake hata pasiwe na mtu wa kuizima, kwa sababu ya uovu wa matendo yenu.
5 “Tangazeni huko Yuda, pazeni sauti huko Yerusalemu! Pigeni tarumbeta kila mahali nchini! Pazeni sauti na kusema: Kusanyikeni pamoja! Kimbilieni miji yenye ngome!
6 Twekeni bendera ya vita kuelekea Siyoni, kimbilieni usalama wenu, msisitesite! Mwenyezi-Mungu analeta maafa na maangamizi makubwa kutoka kaskazini.
7 Kama simba atokavyo mafichoni mwake, mwangamizi wa mataifa ameanza kuja, anakuja kutoka mahali pake, ili kuiharibu nchi yako. Miji yako itakuwa magofu matupu, bila kukaliwa na mtu yeyote.
8 Kwa hiyo, vaa vazi la gunia, omboleza na kulia; maana, hasira kali ya Mwenyezi-Mungu, bado haijaondoka kwetu.
9 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Siku hiyo, mfalme na wakuu watakufa moyo; makuhani watapigwa na bumbuazi, na manabii watashangaa.”
10 Kisha nikasema: “Aa, Mwenyezi-Mungu, hakika umewadanganya kabisa watu hawa na mji wa Yerusalemu! Uliwaambia mambo yatawaendea vema, kumbe maisha yao yamo hatarini kabisa!”
11 Wakati huo, wataambiwa hivi watu hawa pamoja na mji wa Yerusalemu, “Upepo wa hari kutoka vilele vikavu vya jangwani utawavumia watu wangu. Huo si upepo wa kupepeta au kusafisha,
12 bali ni upepo mkali sana utokao kwangu. Ni mimi Mwenyezi-Mungu nitakayetoa hukumu juu yao.”
13 Tazama! Adui anakuja kama mawingu. Magari yake ya vita ni kama kimbunga, na farasi wake waenda kasi kuliko tai. Ole wetu! Tumeangamia!
14 Yerusalemu, yasafishe maovu moyoni mwako, ili upate kuokolewa. Mpaka lini utaendelea kuwaza maovu?
15 Sauti kutoka Dani inatoa taarifa; inatangaza maafa kutoka vilima vya Efraimu.
16 Inayaonya mataifa, inaitangazia Yerusalemu: “Wavamizi waja kutoka nchi ya mbali, wanaitisha miji ya Yuda,
17 wanauzingira Yerusalemu kama walinda mashamba, kwa sababu watu wake wameniasi mimi Mwenyezi-Mungu.
18 Yuda, mwenendo wako na matendo yako yamekuletea hayo. Hayo ndiyo maafa yaliyokupata, tena ni machungu; yamepenya mpaka ndani moyoni mwako.”
19 Uchungu, uchungu! Nagaagaa kwa uchungu! Moyo wangu unanigonga vibaya. Wala siwezi kukaa kimya. Maana naogopa mlio wa tarumbeta, nasikia kingora cha vita.
20 Maafa baada ya maafa, nchi yote imeharibiwa. Ghafla makazi yangu yameharibiwa, na hata mapazia yake kwa dakika moja.
21 Hadi lini nitaona bendera ya vita na kuisikia sauti ya tarumbeta?
22 Mwenyezi-Mungu asema: “Watu wangu ni wapumbavu, hawanijui mimi. Wao ni watoto wajinga; hawaelewi kitu chochote. Ni mabingwa sana wa kutenda maovu, wala hawajui kutenda mema.”
23 Niliiangalia nchi, lo! Imekuwa mahame na tupu; nilizitazama mbingu, nazo hazikuwa na mwanga.
24 Niliiangalia milima, lo, ilikuwa inatetemeka, na vilima vyote vilikuwa vinayumbayumba.
25 Nilikodoa macho wala sikuona mtu; hata ndege angani walikuwa wametoweka.
26 Niliona nchi yenye rutuba imekuwa jangwa, na miji yake yote imekuwa magofu matupu, kwa sababu ya hasira kali ya Mwenyezi-Mungu.
27 Maana Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Nchi nzima itakuwa jangwa tupu; lakini sitaiharibu kabisa.
28 Kwa hiyo, nchi itaomboleza, na mbingu zitakuwa nyeusi. Maana, nimetamka na sitabadili nia yangu; nimeamua, wala sitarudi nyuma.
29 Watakaposikika wapandafarasi na wapiga mishale, kila mmoja atatimua mbio. Baadhi yao watakimbilia msituni, wengine watapanda majabali. Kila mji utaachwa tupu; hakuna mtu atakayekaa ndani.
30 Nawe Yerusalemu uliyeachwa tupu, unavalia nini mavazi mekundu? Ya nini kujipamba kwa dhahabu, na kujipaka wanja machoni? Unajirembesha bure! Wapenzi wako wanakudharau sana; wanachotafuta ni kukuua.
31 Nilisikia sauti kama ya mwanamke anayejifungua, yowe kama anayejifungua mtoto wa kwanza. Ilikuwa sauti ya Yerusalemu akitweta, na kuinyosha mikono yake akisema, ‘Ole wangu! Wanakuja kuniua!’”
1 Kimbieni huko na huko mjini Yerusalemu; pelelezeni na kujionea wenyewe! Chunguzeni masoko yake mwone kama kuna mtu atendaye haki mtu atafutaye ukweli; akiwako, basi Mwenyezi-Mungu atausamehe Yerusalemu.
2 Ingawa wanaapa: “Kama Mwenyezi-Mungu aishivyo”, viapo vyao ni vya uongo.
3 Ee Mwenyezi-Mungu, wewe watafuta daima uaminifu. Umewatwanga, lakini hawakuona uchungu; umewateketeza, lakini walikataa kukosolewa. Wamezifanya nyuso zao kuwa ngumu kuliko mwamba; wamekataa kabisa kurudi kwako.
4 Ndipo nilipowaza: “Hawa ni watu duni hawana akili; hawajui matakwa ya Mwenyezi-Mungu, hawajui Sheria ya Mungu wao.
5 Nitawaendea wakuu niongee nao; bila shaka, wao wanajua matakwa ya Mwenyezi-Mungu; wanajua sheria ya Mungu wao.” Lakini wote waliivunja nira yao. Waliikatilia mbali minyororo yao.
6 Kwa hiyo simba kutoka msituni atawaua; mbwamwitu kutoka jangwani atawararua. Chui anaivizia miji yao. Kila atokaye humo atararuliwa vipandevipande, kwa sababu dhambi zao ni nyingi, maasi yao ni makubwa.
7 Mwenyezi-Mungu anauliza: “Nitawezaje kukusamehe ee Yerusalemu? Watu wako wameniasi; wameapa kwa miungu ya uongo. Nilipowashibisha kwa chakula, wao walifanya uzinzi, wakajumuika majumbani mwa makahaba.
8 Walikuwa kama farasi walioshiba wenye tamaa, kila mmoja akimtamani mke wa jirani yake.
9 Je, nisiwaadhibu kwa mambo haya yote? Nisilipize kisasi juu ya taifa kama hili?
10 “Pandeni mpite katika mashamba yake ya mizabibu mkaharibu kila kitu bila kumaliza kabisa. Yakateni matawi yake, kwani hayo si yangu mimi Mwenyezi-Mungu.
11 Naam, watu wa Israeli na watu wa Yuda, wamekosa kabisa uaminifu kwangu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
12 Wamesema uongo juu ya Mwenyezi-Mungu wamesema: “Hatafanya kitu; hatutapatwa na uovu wowote; hatutashambuliwa wala kuona njaa.
13 Manabii si kitu, ni upepo tu; maana neno lake Mungu halimo ndani yao.” Basi hayo na yawapate wao wenyewe!
14 Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi: “Kwa kuwa wao wamesema jambo hilo, sasa nitayafanya maneno niliyokupa wewe Yeremia kuwa moto. Watu hawa watakuwa kuni, na moto huo utawateketeza.
15 “Nami Mwenyezi-Mungu nasema juu yenu enyi Waisraeli: Mimi naleta taifa moja kutoka mbali, lije kuwashambulia. Taifa ambalo halishindiki, taifa ambalo ni la zamani, ambalo lugha yake hamuifahamu, wala hamwezi kuelewa wasemacho.
16 Mishale yao husambaza kifo; wote ni mashujaa wa vita.
17 Watayala mazao yenu na chakula chenu; watawamaliza watoto wenu wa kike na wa kiume. Watachinja makundi yenu ya kondoo na ng'ombe; wataiharibu mizabibu yenu na mitini yenu. Miji yenu ya ngome mnayoitegemea, wataiharibu kwa silaha zao.
18 “Lakini, hata katika siku hizo mimi Mwenyezi-Mungu nasema, sitawaangamiza na kuwamaliza kabisa.
19 Na watu wenu watakapouliza ‘Kwa nini Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, ametutendea mambo hayo yote?’ Wewe utawaambia, ‘Nyinyi mlimwacha Mwenyezi-Mungu, mkaitumikia miungu ya kigeni katika nchi yenu. Basi ndivyo mtakavyowatumikia watu wengine katika nchi isiyo yenu.’
20 “Watangazie wazawa wa Yakobo, waambie watu wa Yuda hivi:
21 Sikilizeni enyi wajinga na wapumbavu; watu mlio na macho, lakini hamwoni, mlio na masikio, lakini hamsikii.
22 Mbona hamniogopi? Nauliza mimi Mwenyezi-Mungu! Kwa nini hamtetemeki mbele yangu? Mimi niliweka mchanga uwe mpaka wa bahari, kizuizi cha daima ambacho bahari haiwezi kuvuka. Ingawa mawimbi yanaupiga, hayawezi kuupita; ingawa yananguruma, hayawezi kuuruka.
23 Lakini watu hawa wana moyo wa ukaidi na uasi; wameniacha wakaenda zao.
24 Wala hawasemi mioyoni mwao; ‘Na tumche Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, anayetujalia mvua kwa wakati wake, anayetupatia mvua za masika na mvua za vuli; na kutupa majira maalumu ya mavuno.’
25 Makosa yenu yamewazuia msipate baraka hizo, dhambi zenu zimewafanya msipate mema.
26 Naam, kuna walaghai miongoni mwa watu wangu, watu ambao hunyakua mali za wengine. Wako kama wawindaji wa ndege: Hutega mitego yao na kuwanasa watu.
27 Kama vile kapu lililojaa ndege walionaswa, ndivyo nyumba zao zilivyojaa mali za udanganyifu. Ndiyo maana wamekuwa watu wakubwa na matajiri,
28 wamenenepa na kunawiri. Katika kutenda maovu hawana kikomo hawahukumu yatima kwa haki wapate kufanikiwa, wala hawatetei haki za watu maskini.
29 “Je, nisiwaadhibu kwa mambo haya? Je nitaacha kulipiza kisasi taifa kama hili?
30 Jambo la ajabu na la kuchukiza limetokea katika nchi hii:
31 Manabii wanatabiri mambo ya uongo, makuhani nao hutafuta faida yao wenyewe; na watu wangu wanaona jambo hilo kuwa sawa. Lakini mwisho utakapofika mtafanyaje?”
1 Enyi watu wa Benyamini, ondokeni Yerusalemu mkimbilie usalama! Pigeni tarumbeta mjini Tekoa; onesheni ishara huko Beth-hakeremu, maana maafa na maangamizi makubwa yanakuja kutoka upande wa kaskazini.
2 Mji wa Siyoni ni mzuri na mwororo, lakini utaangamizwa.
3 Watu wataujia kama wachungaji na makundi yao, watapiga hema zao kuuzunguka kila mmoja sehemu yake, wapate kuyaongoza makundi yao.
4 Watasema: “Jitayarisheni kuushambulia Siyoni. Haya! Tuanze kushambulia adhuhuri! Bahati mbaya; jua linatua! Kivuli cha jioni kinarefuka.
5 Basi, tutaushambulia usiku; tutayaharibu majumba yake ya kifalme.”
6 Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema: “Kateni miti yake, rundikeni udongo kuuzingira Yerusalemu. Mji huu ni lazima uadhibiwe, maana hamna lolote ndani yake ila dhuluma.
7 Kama kisima kinavyohifadhi maji yake yakabaki safi, ndivyo Yerusalemu unavyohifadhi uovu wako. Ukatili na uharibifu vyasikika ndani yake, magonjwa na majeraha yake nayaona daima.
8 Hilo na liwe onyo kwako ee Yerusalemu, la sivyo nitakutupa kabisa kwa chuki; nikakufanya uwe jangwa, mahali pasipokaliwa na mtu.”
9 Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi: “Kusanyeni watu wote wa Israeli waliobaki kama watu wakusanyavyo zabibu zote; kama afanyavyo mchumazabibu, pitisheni tena mikono yenu katika matawi yake.”
10 Nitaongea na nani nipate kumwonya, ili wapate kunisikia? Tazama, masikio yao yameziba, hawawezi kusikia ujumbe wako. Kwao neno lako, ee Mwenyezi-Mungu, limekuwa jambo la dhihaka, hawalifurahii hata kidogo.
11 Nimejaa hasira ya Mwenyezi-Mungu dhidi yao. Nashindwa kuizuia ndani yangu. Mwenyezi-Mungu akaniambia: “Imwage hasira barabarani juu ya watoto na pia juu ya makundi ya vijana; wote, mume na mke watachukuliwa, kadhalika na wazee na wakongwe.
12 Nyumba zao zitapewa watu wengine, kadhalika na mashamba yao na wake zao; maana nitaunyosha mkono wangu, kuwaadhibu wakazi wa nchi hii. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
13 Wote, tangu mdogo hadi mkubwa kabisa, kila mmoja anatamani kupata faida isiyo halali. Tangu manabii hadi makuhani, kila mmoja wao ni mdanganyifu.
14 Wameliponya jeraha la watu wangu juujuu, wanasema; ‘Amani, amani’, kumbe hakuna amani yoyote!
15 Je, waliona aibu walipofanya machukizo hayo? La! Hawakuona aibu hata kidogo. Hawakujua hata namna ya kuona aibu. Kwa hiyo wataanguka pamoja na wale waangukao; wakati nitakapowaadhibu, wataangamizwa kabisa. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
16 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Simameni katika njia panda, mtazame. Ulizeni mjue juu ya matukio ya zamani. Tafuteni mahali ilipo njia nzuri muifuate nanyi mtapumzisha nafsi zenu. Lakini wao wakasema: ‘Hatutafuata njia hiyo.’
17 Kisha nikawawekea walinzi, nikawaambia: ‘Sikilizeni ishara ya tarumbeta.’ Lakini wao wakasema: ‘Hatutaisikiliza.’
18 “Kwa hiyo, sikilizeni enyi mataifa; enyi jumuiya ya watu jueni yatakayowapata.
19 Sikiliza ee dunia! Mimi nitawaletea maafa watu hawa kulingana na nia zao mbaya. Maana hawakuyajali maneno yangu, na mafundisho yangu nayo wameyakataa.
20 Ya nini kuniletea ubani kutoka Sheba, na udi wa harufu nzuri kutoka nchi ya mbali? Sadaka zenu za kuteketezwa hazikubaliki, wala tambiko zenu hazinipendezi.
21 Kwa hiyo mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Tazama, nitawawekea watu hawa vikwazo ambavyo vitawakwaza na kuwaangusha chini. Akina baba na watoto wao wa kiume wataangamia, kadhalika na majirani na marafiki.”
22 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Tazameni, watu wanakuja toka nchi ya kaskazini; taifa kubwa linajitayarisha kutoka mbali duniani.
23 Wamezishika pinde zao na mikuki, watu wakatili wasio na huruma. Vishindo vyao ni kama ngurumo ya bahari. Wamepanda farasi, wamejipanga tayari kwa vita, dhidi yako ewe Siyoni!”
24 Waisraeli wanasema, “Tumesikia habari zao, mikono yetu imelegea; tumeshikwa na dhiki na uchungu, kama mwanamke anayejifungua.
25 Hatuwezi kwenda mashambani, wala kutembea barabarani; maadui wameshika silaha mikononi, vitisho vimejaa kila mahali.”
26 Mwenyezi-Mungu asema, “Jivikeni mavazi ya gunia, enyi watu wangu na kugaagaa katika majivu. Ombolezeni kwa uchungu, kama mtu anayemwombolezea mwana wa pekee, maana mwangamizi atakuja, na kuwashambulia ghafla.
27 Yeremia, wewe nimekuweka kuwa mchunguzi na mpimaji wa watu wangu, ili uchunguze na kuzijua njia zao.
28 Wote ni waasi wakaidi, ni watu wanaopitapita wakisengenya wengine, wagumu kama shaba nyeusi au chuma; wote hutenda kwa ufisadi.
29 Mifuo inafukuta kwa nguvu, risasi inayeyukia humohumo motoni; ni bure kuendelea kuwatakasa watu wangu, waovu hawawezi kuondolewa uchafu wao.
30 Wataitwa ‘Takataka za fedha’, maana mimi Mwenyezi-Mungu nimewakataa.”
1 Mwenyezi-Mungu alimwamuru Yeremia aende kusimama
2 kwenye lango la hekalu lake Mwenyezi-Mungu na kutangaza ujumbe huu: “Sikilizeni neno la Mwenyezi-Mungu enyi watu wa Yuda mnaoingia humu kumwabudu Mwenyezi-Mungu.
3 Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi: Rekebisheni mienendo yenu na matendo yenu, nami nitawaacha mwendelee kukaa mahali hapa.
4 Msitumainie maneno haya ya uongo: ‘Hili ni hekalu la Mwenyezi-Mungu, hekalu la Mwenyezi-Mungu, naam hekalu la Mwenyezi-Mungu.’
5 “Ila kama mkibadili mienendo yenu na matendo yenu, mkitendeana haki kwa dhati;
6 kama mkiacha kuwadhulumu wageni, yatima au wajane au kuwaua watu wasio na hatia katika nchi hii; kama mkiacha kuabudu miungu mingine na kujiangamiza wenyewe,
7 basi mimi nitawaacha daima mkae mahali hapa, katika nchi niliyowapa wazee wenu tangu zamani.
8 “Lakini kumbe, mnayaamini maneno ya uongo bure.
9 Mnaiba, mnaua, mnafanya uzinzi, mnaapa uongo, mnamfukizia mungu Baali ubani na kuabudu miungu mingine ambayo hamjapata kuijua.
10 Kisha, mnakuja na kusimama mbele yangu, katika hekalu hili linalojulikana kwa jina langu na kusema; ‘Tuko salama,’ huku mnaendelea kufanya mambo hayo yanayonichukiza.
11 Je, hekalu hili linalojulikana kwa jina langu limekuwa pango la wanyanganyi? Jueni kuwa mimi nimeyaona yote mnayofanya!
12 Nendeni mahali pangu kule Shilo, mahali nilipopachagua niabudiwe hapo awali, mkaone maangamizi niliyoyafanya huko kwa sababu ya uovu wa watu wangu, Israeli.
13 Nyinyi mmefanya mambo hayo yote, na hata niliposema nanyi tena na tena hamkunisikiliza. Nilipowaiteni hamkuitika.
14 Kwa hiyo, kama nilivyoutendea mji wa Shilo, ndivyo nitakavyolitendea hekalu hili linalojulikana kwa jina langu, hekalu ambalo nyinyi mnalitegemea; naam, mahali hapa ambapo niliwapa nyinyi na wazee wenu.
15 Nitawafukuzeni mbali nami kama nilivyowatupilia mbali ndugu zenu, wazawa wote wa Efraimu.
16 “Nawe, Yeremia, usiwaombee watu hawa, usinililie kwa ajili yao, usiwaombee dua wala usinisihi kwa ajili yao, maana sitakusikiliza.
17 Je, wewe huoni mambo wanayofanya katika miji ya Yuda na katika mitaa ya Yerusalemu?
18 Watoto huokota kuni, akina baba huwasha moto na akina mama hukanda unga ili waoke mikate kwa ajili ya mungu wa kike wanayemwita malkia wa mbinguni. Tena wanaimiminia miungu mingine tambiko ya divai ili kuniudhi.
19 Lakini je, wanamwudhi nani? Mimi? Hata kidogo! Wanajiumiza wao wenyewe na kuchanganyikiwa!
20 Kwa hiyo, mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Nitaimwaga hasira yangu na ghadhabu yangu mahali hapa, juu ya wanadamu na wanyama, miti mashambani na mazao ya nchi. Itawaka na wala haitaweza kuzimwa.”
21 Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi: “Haya, ongezeni tambiko zenu za kuteketezwa juu ya sadaka zenu na kula nyama yake!
22 Maana, siku nilipowatoa wazee wenu nchini Misri, sikuwaambia kitu wala kuwapa amri yoyote juu ya tambiko za kuteketezwa na sadaka.
23 Lakini niliwapa amri hii: Waitii sauti yangu ili niwe Mungu wao, nao wawe watu wangu. Niliwaamuru pia waishi kama nilivyowaagiza, ili mambo yao yawaendee vema.
24 Lakini wao hawakunitii wala kunitegea sikio. Badala yake wakafuata fikira zao wenyewe na ukaidi wa mioyo yao, wakarudi nyuma badala ya kusonga mbele.
25 Tangu siku ile wazee wenu walipotoka nchini Misri hadi leo, sijakoma kuwatuma kwenu watumishi wangu, manabii.
26 Lakini hamkunisikiliza wala kunitegea sikio, ila mlizidi kuwa wakaidi, mkawa waasi kuliko hata wazee wenu.
27 “Basi, wewe Yeremia utawaambia maneno haya yote, lakini wao hawatakusikiliza. Utawaita, lakini hawatakuitikia.
28 Utawaambia; ‘Nyinyi ni taifa ambalo halikutii sauti ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, wala kukubali kuwa na nidhamu. Kwenu uaminifu umekufa; umetoweka kabisa katika maneno yenu.’
29 “Nyoeni nywele zenu enyi wakazi wa Yerusalemu, mzitupe; fanyeni maombolezo juu ya vilele vya milima, maana, mimi Mwenyezi-Mungu nimewakataa nyinyi, mlio kizazi kilichosababisha hasira yangu!
30 “Watu wa Yuda wametenda uovu mbele yangu. Wameweka vinyago vyao vya kuchukiza ndani ya nyumba hii ijulikanayo kwa jina langu, wakaitia unajisi.
31 Wamejenga madhabahu iitwayo ‘Tofethi’ huko kwenye bonde la mwana wa Hinomu, wapate kuwachoma sadaka watoto wao wa kiume na wa kike humo motoni. Mimi sikuwa nimewaamuru kamwe kufanya jambo hilo, wala halikunijia akilini mwangu.
32 Kwa sababu hiyo, siku zaja ambapo hawataliita tena ‘Tofethi,’ au ‘Bonde la Mwana wa Hinomu,’ bali wataliita ‘Bonde la Mauaji.’ Huko ndiko watakakozika watu, kwa sababu hapatakuwa na mahali pengine pa kuzikia.
33 Maiti za watu hao zitakuwa chakula cha ndege wa angani na wanyama wa porini, na hapatakuwa na mtu atakayewafukuza.
34 Nchi itakuwa jangwa na katika miji ya Yuda na mitaa ya Yerusalemu nitakomesha sauti zote za vicheko na furaha, sauti za bwana arusi na bibi arusi, kwa sababu nchi itakuwa ukiwa.
1 “Wakati huo, nasema mimi Mwenyezi-Mungu, mifupa ya wafalme wa Yuda, mifupa ya wakuu wao, mifupa ya makuhani, mifupa ya manabii na mifupa ya wakazi wote wa Yerusalemu itachimbuliwa makaburini mwao.
2 Itaachwa imetandazwa mbele ya jua na mwezi na sayari zote za mbinguni, vitu ambavyo walivipenda na kuvitumikia, wakavitaka shauri na kuviabudu. Mifupa hiyo haitakusanywa wala kuzikwa, bali itakuwa kama mavi juu ya ardhi.
3 Watu wote waliobaki wa jamaa hii mbovu, mahali popote pale nilipowatawanya, wataona heri kufa kuliko kuishi. Ndivyo nisemavyo mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi.
4 “Wewe Yeremia utawaambia kuwa mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Mtu akianguka, je hainuki tena? Mtu akipotea, je, hairudii tena njia yake?
5 Mbona basi, watu hawa wameacha njia iliyo sawa na kuendelea katika upotovu wao? Wanashikilia miungu yao ya uongo, na kukataa kunirudia mimi!
6 Mimi nilisikiliza kwa makini, lakini wao hawakusema ukweli wowote. Hakuna mtu anayetubu uovu wake, wala kujiuliza; ‘Nimefanya nini?’ Kila mmoja wao anashika njia yake, kama farasi akimbiliavyo moja kwa moja vitani.
7 Hata korongo anajua wakati wa kuhama; njiwa, mbayuwayu na koikoi, hufuata majira yao ya kurudi. Lakini watu wangu hawa hawajui kitu juu ya amri zangu mimi Mwenyezi-Mungu.
8 Mnawezaje kusema: ‘Sisi tuna hekima, sisi tunayo sheria ya Mwenyezi-Mungu,’ hali waandishi wa sheria, wameipotosha sheria yangu?
9 Wenye hekima wenu wataaibishwa; watafadhaishwa na kunaswa. Wamelikataa neno la Mwenyezi-Mungu; je, ni hekima gani hiyo waliyo nayo?
10 Kwa hiyo, wake zao nitawapa watu wengine, mashamba yao nitawapa wengine. Maana, tangu mdogo hadi mkubwa, kila mmoja ana tamaa ya faida haramu. Tangu manabii hadi makuhani, kila mmoja anatenda kwa udanganyifu.
11 Wameliponya jeraha la watu wangu juujuu, wakisema, ‘Kuna amani, kuna amani’, kumbe hakuna amani yoyote!
12 Je, waliona aibu walipotenda machukizo hayo? La hasha! Hawakuona aibu hata kidogo. Hata hawajui kuona haya. Kwa hiyo, wataanguka pamoja na wale walioanguka; nitakapowaadhibu, wataangamia. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
13 “Mimi Mwenyezi-Mungu nasema: Nilipotaka kukusanya chochote kutoka kwao, sikupata zabibu hata moja juu ya mzabibu, sikupata tini zozote juu ya mtini; hata majani yao yamekauka. Hata nilichokuwa nimewapa kimetoweka.”
14 “Watu wanauliza: Kwa nini sisi tunakaa tu hapa? Kusanyikeni, tuingie katika miji yenye ngome, tukaangamie huko! Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, ametupangia tuangamie, ametupa maji yenye sumu tunywe, kwa kuwa tumemkosea yeye.
15 Tulitazamia kupata amani, lakini hakuna jema lililotokea. Tulitazamia wakati wa kuponywa, badala yake tukapata vitisho.
16 Sauti za farasi wao zinasikika, kwa mlio wa farasi wao wa vita, nchi nzima inatetemeka. Wanafika na kuiharibu nchi na vyote vilivyomo, kuangamiza mji pamoja na wote waishio humo.
17 “Basi nitawaleteeni nyoka; nyoka wenye sumu wasioweza kurogwa na walozi, nao watawauma nyinyi. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
18 Huzuni yangu haiwezi kutulizwa, moyo wangu wasononeka ndani yangu.
19 Sikiliza kilio cha watu wangu, kutoka kila upande katika nchi. “Je, Mwenyezi-Mungu hayuko Siyoni? Je, mfalme wake hayuko tena huko?” “Mbona wamenikasirisha kwa sanamu zao za miungu, na vinyago vyao vya miungu ya kigeni?”
20 “Mavuno yamepita, kiangazi kimekwisha, nasi bado hatujaokolewa!
21 Jeraha la watu wangu limeniumiza moyoni, ninaomboleza na kufadhaika.
22 Je, hakuna dawa ya kupaka huko Gileadi? Je, hakuna mganga huko? Mbona basi watu wangu hawajaponywa?
1 Laiti kichwa changu kingekuwa kisima cha maji, na macho yangekuwa chemchemi ya machozi ili nipate kulia mchana na usiku, kwa ajili ya watu wangu waliouawa!
2 Laiti ningekuwa na mahali pa kukaa jangwani, ambamo ningewaacha watu wangu na kwenda zangu.” Mwenyezi-Mungu asema: “Wote ni watu wazinzi, ni genge la watu wahaini.
3 Hupinda maneno yao kama pinde; wameimarika kwa uongo na si kwa haki. Huendelea kutoka uovu hata uovu, wala hawanitambui mimi. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
4 Kila mmoja ajihadhari na jirani yake! Hata ndugu yeyote haaminiki, kila ndugu ni mdanganyifu, na kila jirani ni msengenyaji.
5 Kila mmoja humdanganya jirani yake, hakuna hata mmoja asemaye ukweli. Wamezifundisha ndimi zao kusema uongo; hutenda uovu kiasi cha kushindwa kabisa kutubu.
6 Wanarundika dhuluma juu ya dhuluma, na udanganyifu juu ya udanganyifu. Wanakataa kunitambua mimi. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
7 Kwa hiyo mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi nasema: Tazama, nitawayeyusha na kuwajaribu! Au, nifanye nini zaidi na watu wangu waovu?
8 Ndimi zao ni kama mishale yenye sumu, daima haziishi kudanganya; kila mmoja huongea vema na jirani yake, lakini moyoni mwake hupanga kumshambulia.
9 Je, nisiwaadhibu kwa sababu ya mambo haya? Je, nisilipe kisasi kwa taifa kama hili? Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
10 Nitaililia na kuiomboleza milima; nitayaombolezea malisho nyikani, kwa sababu yamekauka kabisa, hakuna mtu apitaye mahali hapo. Hakusikiki tena sauti za ng'ombe; ndege na wanyama wamekimbia na kutoweka.
11 Mwenyezi-Mungu asema: “Nitaifanya Yerusalemu magofu matupu, naam, nitaifanya kuwa pango la mbweha; na miji ya Yuda nitaifanya kuwa jangwa, mahali pasipokaliwa na mtu yeyote.”
12 Nami nikauliza, “Je kuna mtu mwenye hekima kiasi cha kuweza kueleza mambo haya? Mwenyezi-Mungu aliongea na nani hata huyo aweze kutangaza kitu hicho? Kwa nini nchi imeharibiwa na kufanywa tupu kama jangwa hata hakuna mtu apitaye humo?”
13 Mwenyezi-Mungu akajibu: “Kwa kuwa wamekataa kushika sheria yangu niliyowapa, wamekataa kutii sauti yangu na kufuata matakwa yake.
14 Badala yake wamefuata kwa ukaidi fikira za mioyo yao, wakaenda kuyaabudu Mabaali kama walivyofundishwa na wazee wao.
15 Basi, mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, nasema hivi: Tazama nitawalisha watu hawa uchungu na kuwapa maji yenye sumu wanywe.
16 Nitawatawanya kati ya mataifa ambayo wao wenyewe wala wazee wao hawakupata kuyajua; nitawafanya waandamwe na vita mpaka hapo nitakapowaangamiza wote.”
17 Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi: “Fikirini na kuwaita wanawake waomboleze; naam, waiteni wanawake hodari wa kuomboleza.
18 Waambieni: ‘Njoni hima mkaomboleze juu yetu, macho yetu yapate kuchuruzika machozi, na kope zetu zibubujike machozi kama maji.’”
19 Kilio kinasikika Siyoni: “Tumeangamia kabisa! Tumeaibishwa kabisa! Lazima tuiache nchi yetu, maana nyumba zetu zimebomolewa!
20 Enyi wanawake, sikilizeni neno la Mwenyezi-Mungu! Tegeni masikio msikie jambo analosema. Wafundisheni binti zenu kuomboleza, na jirani zenu wimbo wa maziko:
21 ‘Kifo kimepenya madirisha yetu, kimeingia ndani ya majumba yetu; kimewakatilia mbali watoto wetu barabarani, vijana wetu katika viwanja vya mji.
22 Maiti za watu zimetapakaa kila mahali kama marundo ya mavi mashambani, kama masuke yaliyoachwa na mvunaji, wala hakuna atakayeyakusanya.’ Ndivyo alivyoniambia Mwenyezi-Mungu niseme.”
23 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Mwenye hekima asijivunie nguvu zake, wala tajiri asijivunie utajiri wake.
24 Anayetaka kujivuna na ajivunie jambo hili: Kwamba ananifahamu kwamba anajua Mwenyezi-Mungu hutenda mema, hufanya mambo ya haki na uadilifu duniani. Watu wa namna hiyo ndio wanipendezao. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
25 Mwenyezi-Mungu asema: “Siku zaja ambapo nitawaadhibu wote waliotahiriwa mwilini tu:
26 Wamisri, Wayuda, Waedomu, Waamoni, Wamoabu na wakazi wote wa jangwani wanaonyoa denge. Maana watu hawa wote na Waisraeli wote hawakutahiriwa moyoni.”
1 Sikilizeni neno analowaambieni Mwenyezi-Mungu, enyi Waisraeli!
2 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Msijifunze mienendo ya mataifa mengine, wala msishangazwe na ishara za mbinguni; yaacheni mataifa mengine yashangazwe nazo.
3 Maana, mila za dini za watu hawa ni za uongo. Mtu hukata mti msituni fundi akachonga kinyago cha mungu kwa shoka.
4 Kisha watu hukipamba kwa fedha na dhahabu wakakipigilia misumari kwa nyundo ili kisije kikaanguka.
5 Vinyago vyao ni kama vinyago vya kutishia ndege katika shamba la matango, havina uwezo wa kuongea; ni lazima vibebwe maana haviwezi kutembea. Msiviogope vinyago hivyo, maana haviwezi kudhuru, wala haviwezi kutenda lolote jema.”
6 Ee Mwenyezi-Mungu, hakuna aliye kama wewe; wewe ni mkuu na nguvu yako yajulikana.
7 Nani asiyekuogopa wewe, ee mfalme wa mataifa? Wewe wastahili kuheshimiwa. Miongoni mwa wenye hekima wote wa mataifa, na katika falme zao zote, hakuna hata mmoja aliye kama wewe.
8 Wote ni wajinga na wapumbavu mafunzo ya vinyago ni upuuzi mtupu!
9 Vinyago hivyo hupambwa kwa fedha kutoka Tarshishi, na dhahabu kutoka Ofiri; kazi ya mafundi stadi na wafua dhahabu. Zimevishwa nguo za samawati na zambarau, zilizofumwa na wafumaji stadi.
10 Lakini Mwenyezi-Mungu ni Mungu wa kweli; Mungu aliye hai, mfalme wa milele. Akikasirika, dunia hutetemeka, mataifa hayawezi kustahimili hasira yake.
11 Basi, utawaambia hivi: “Miungu ambayo haikuumba mbingu na dunia, itaangamia. Itatoweka kabisa duniani na chini ya mbingu.”
12 Mwenyezi-Mungu aliiumba dunia kwa nguvu zake; kwa hekima yake aliuimarisha ulimwengu, kwa akili yake alizitandaza mbingu.
13 Anapotoa sauti yake, maji hunguruma mbinguni, huzusha ukungu kutoka mipaka ya dunia. Huufanya umeme umulike wakati wa mvua, na kuutoa upepo katika ghala zake.
14 Binadamu ni mjinga na mpumbavu; kila mfua dhahabu huaibishwa na vinyago vyake; maana, vinyago hivyo ni uongo mtupu. Havina uhai wowote ndani yao.
15 Havina thamani, ni udanganyifu mtupu; wakati vitakapoadhibiwa vyote vitaangamia.
16 Lakini Mungu wa Yakobo si kama vinyago hivyo, maana, yeye ndiye aliyeumba vitu vyote, na Israeli ni taifa lililo mali yake; Mwenyezi-Mungu wa majeshi ndilo jina lake.
17 Kusanyeni vitu vyenu enyi watu mliozingirwa.
18 Maana Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Wakati huo nitawatupa nje ya nchi hii, nitawataabisha asibaki mtu yeyote.”
19 Ole wangu mimi Yerusalemu maana nimejeruhiwa! Jeraha langu ni baya sana! Lakini nilisema: “Hakika haya ni mateso, na sina budi kuyavumilia.”
20 Lakini hema langu limebomolewa, kamba zake zote zimekatika; watoto wangu wameniacha, na kwenda zao, wala hawapo tena; hakuna wa kunisimikia tena hema langu, wala wa kunitundikia mapazia yangu.
21 Nami Yeremia nikasema: Wachungaji wamekuwa wajinga, hawakuomba shauri kwa Mwenyezi-Mungu; kwa sababu hiyo, hawakufanikiwa, na kondoo wao wote wametawanyika.
22 Sikilizeni sauti! Habari zinatufikia. Kuna kishindo kutoka kaskazini. Taifa kutoka kaskazini linakuja, kuifanya miji ya Yuda kuwa jangwa ambamo kutakuwa na mapango ya mbweha!
23 Najua, ee Mwenyezi-Mungu, binadamu hana uwezo na maisha yake; hakuna mtu awezaye kuyaongoza maisha yake.
24 Utukosoe, ee Mwenyezi-Mungu, lakini si kwa ghadhabu, wala kwa hasira yako, tusije tukaangamia.
25 Imwage hasira yako juu ya mataifa yasiyokuabudu, na juu ya watu ambao hawakutambui. Maana, wamewaua wazawa wa Yakobo; wamewaua na kuwaangamiza kabisa, na nchi yao wameiacha magofu.
1 Neno lilimjia Yeremia kutoka kwa Mwenyezi-Mungu;
2 “Sikiliza masharti ya agano hili, kisha nenda ukawatangazie watu wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu.
3 Utawaambia hivi: Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, asema hivi: Na alaaniwe mtu yeyote asiyejali masharti ya agano hili.
4 Hili ni agano nililowapa wazee wenu nilipowatoa nchini Misri, kutoka katika tanuri la chuma. Niliwaambia wanitii na kufanya yote niliyowaamuru, na kwamba wakifanya hivyo, watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao.
5 Wakifuata masharti hayo, mimi nitatimiza ahadi niliyowapa wazee wenu, kwamba nitawapa nchi inayotiririka maziwa na asali, kama ilivyo hadi leo.” Nami nikajibu: “Na iwe hivyo, ee Mwenyezi-Mungu.”
6 Mwenyezi-Mungu akaniambia: “Tangaza masharti hayo yote katika miji ya Yuda na katika barabara za Yerusalemu. Waambie watu wayasikilize masharti ya agano hili na wayatekeleze.
7 Maana niliwaonya vikali wazee wao nilipowatoa katika nchi ya Misri, na nimeendelea kuwaonya wanitii mpaka siku hii ya leo.
8 Lakini wao hawakunitii, wala hawakunisikiliza. Badala yake, kila mmoja wao alizidi kuwa mkaidi na mwovu. Basi, niliwaadhibu kulingana na masharti ya agano hili nililowaamuru walishike, lakini hao wakakataa kulishika.”
9 Tena Mwenyezi-Mungu aliniambia: “Watu wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu wanafanya njama za kuniasi.
10 Wameurudia uovu wa wazee wao ambao walikataa kusikiliza maneno yangu; wameiabudu miungu mingine na kuitumikia. Watu wa Israeli na watu wa Yuda wamevunja agano nililofanya na wazee wao.
11 Kwa hiyo, sasa, mimi Mwenyezi-Mungu ninawaonya kwamba nitawaletea maafa ambayo hawataweza kuepukana nayo. Hata kama wakinililia namna gani, sitawasikiliza.
12 Hapo ndipo watu wa Israeli na Yerusalemu watakapoiendea miungu yao ambayo wanaifukizia ubani. Lakini miungu hiyo haitaweza kuwaokoa wakati huo wa taabu zao.
13 Miungu yako, ewe Yuda imekuwa mingi kama ilivyo miji yako; kama zilivyo nyingi barabara za Yerusalemu, ndivyo zilivyo nyingi madhabahu walizomjengea mungu kinyaa Baali, ili kumfukizia ubani.
14 Basi, wewe Yeremia, usiwaombee watu hawa, usinililie kwa ajili yao, wala usiwaombee dua. Maana, hata wakiniomba wanapotaabika, mimi sitawasikiliza.”
15 Mwenyezi-Mungu asema: “Watu niwapendao wana haki gani kuingia hekaluni mwangu wakati wametenda maovu? Je, wanadhani nadhiri na nyama zilizowekwa wakfu zitawaondolea maafa? Je, hayo yatawafurahisha?
16 Wakati fulani, mimi nilisema, wao ni mzeituni wenye majani mabichi, mzeituni mzuri na wenye matunda mema; lakini sasa, kwa ngurumo ya dhoruba kubwa, nitauchoma moto na kuyateketeza matawi yake.
17 Mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi niliuotesha huu mzeituni; lakini natangaza maafa dhidi yake kwa sababu ya maovu ambayo watu wa Israeli na Yuda wameyafanya. Wamenikasirisha kwa kumfukizia ubani mungu Baali.”
18 Mwenyezi-Mungu alinijulisha, nami nikaelewa; Mwenyezi-Mungu alinijulisha njama zao.
19 Nami nilikuwa kama kondoo mpole anayepelekwa machinjoni; sikujua kuwa njama walizofanya zilikuwa dhidi yangu. Walisema: “Na tuuharibu mti pamoja na matunda yake, tumkatilie mbali kutoka nchi ya walio hai, kamwe jina lake lisikumbukwe tena.”
20 Lakini, ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi, wewe unayehukumu kwa haki, unayepima mioyo na akili za watu, unijalie kuona ukiwalipiza kisasi, maana kwako nimekiweka kisa changu.
21 Ndiyo maana Mwenyezi-Mungu wa majeshi anacho cha kusema juu ya watu wa Anathothi ambao wanataka kuniua na kuniambia: “Usitoe unabii kwa jina la Mwenyezi-Mungu, la sivyo tutakuua.”
22 Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi: “Nitawaadhibu watu hao. Vijana wao watauawa vitani; watoto wao wa kiume na wa kike watakufa kwa njaa.
23 Nimepanga muda wa kuleta maangamizi juu ya watu wa Anathothi. Wakati huo utakapofika, hakuna hata mmoja wao atakayebaki hai.”
1 Ee Mwenyezi-Mungu, wewe ni mwadilifu, ingawa nakulalamikia. Lakini ningependa kutoa hoja zangu mbele yako: Kwa nini waovu hufanikiwa katika mambo yao? Mbona wote wenye hila hustawi?
2 Unawaotesha nao wanaota; wanakua na kuzaa matunda. Wanakutaja kwa maneno yao, lakini mioyo yao iko mbali nawe.
3 Lakini wewe ee Mwenyezi-Mungu wanijua; wayathibiti maelekeo yangu kwako. Uwaokote hao kama kondoo wa kuchinjwa, watenge kwa ajili ya wakati wa kuuawa.
4 Mpaka lini nchi itaomboleza kwa ukame, na nyasi za mashamba yote kunyauka? Wanyama na ndege wanakufa kwa uovu wa wakazi wake; wanasema: “Mungu hataona mwisho wetu.”
5 Mwenyezi-Mungu asema, “Ikiwa umeshindana na waendao kwa miguu ukachoka, utawezaje kushindana na farasi? Kama unaanguka katika nchi isiyo na vizuizi, utafanyaje katika msitu wa Yordani?
6 Hata ndugu zako, jamaa yako mwenyewe, nao pia wamekutendea mambo ya hila; wanakukemea waziwazi. Usiwaamini hata kidogo, japo wanakuambia maneno mazuri.”
7 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Nimeiacha nyumba yangu; nimeitupa mali yangu mimi mwenyewe. Israeli, mpenzi wangu wa moyo, nimemtia mikononi mwa maadui zake.
8 Wateule wangu wamenigeuka, wamekuwa kama simba porini, wameningurumia mimi; ndiyo maana nawachukia.
9 Wateule wangu wamekuwa ndege mzuri wanaoshambuliwa na kozi pande zote. Nenda ukawakusanye wanyama wote wakali waje kushiriki katika karamu.
10 Wachungaji wengi wameharibu shamba langu la mizabibu, wamelikanyagakanyaga chini lililo mali yangu; shamba langu zuri wamelifanya jangwa.
11 Wamelifanya kuwa tupu; katika ukiwa wake lanililia. Nchi yote imekuwa jangwa, wala hakuna mtu anayejali.
12 Juu ya milima yote jangwani, watu wamefika kuangamiza. Upanga wangu unapita kuiangamiza nchi, toka upande mmoja hadi mwingine, wala hakuna mtu atakayeishi kwa amani.
13 Walipanda ngano, lakini walivuna magugu; walifanya bidii, lakini hawakupata kitu. Kwa sababu ya hasira yangu kali, mavuno watakayoyapata yatakuwa aibu tupu.”
14 Mwenyezi-Mungu asema hivi juu ya jirani wabaya wa watu wangu: “Wamekigusa kile kilicho changu, kile nilichowapa watu wangu Israeli! Basi nitawangoa kutoka katika nchi yao. Hata watu wa Yuda nitawangoa katika nchi yao.
15 Lakini baada ya kuwangoa, nitawahurumia tena; nitalirudisha kila taifa katika sehemu yake na katika nchi yake.
16 Na kama watajifunza njia za watu wangu kwa moyo wote, kama wataapa kwa jina langu kwa kusema, ‘Kama aishivyo Mwenyezi-Mungu,’ kama vile walivyowafundisha watu wangu kuapa kwa jina la mungu Baali, basi watajengeka miongoni mwa watu wangu.
17 Lakini taifa lolote ambalo halitanitii, nitalingoa kabisa na kuliangamiza. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
1 Mwenyezi-Mungu aliniambia hivi: “Nenda ukajinunulie kikoi cha kitani, ukajifunge kiunoni; lakini usikitie majini.”
2 Basi, nikaenda, nikanunua kikoi kama alivyoniagiza Mwenyezi-Mungu, nikajifunga kiunoni.
3 Kisha, neno la Mwenyezi-Mungu likanijia mara ya pili:
4 “Kichukue kikoi ulichonunua na ambacho umejifunga kiunoni, uende kwenye mto Eufrate na kukificha katika pango mwambani.”
5 Basi, nikaenda na kukificha kikoi hicho karibu na mto Eufrate, kama Mwenyezi-Mungu alivyoniamuru.
6 Ikawa, baada ya siku nyingi, Mwenyezi-Mungu akaniambia, “Nenda kwenye mto Eufrate, ukakichukue kile kikoi nilichokuamuru ukifiche huko.”
7 Basi, nikaenda kwenye mto Eufrate, nikachimbua na kukitoa kile kikoi mahali nilipokuwa nimekificha. Nilipokitoa, nilishangaa kukiona kuwa kilikuwa kimeharibika kabisa; kilikuwa hakifai tena.
8 Ndipo neno la Mwenyezi-Mungu likanijia:
9 “Mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Hivi ndivyo nitakavyokiharibu kiburi cha Yuda na kiburi kikubwa cha Yerusalemu.
10 Watu hawa waovu wanakataa kusikia maneno yangu, na badala yake wanakuwa wakaidi na kufuata mawazo yao wenyewe. Wanaifuata miungu mingine, wanaitumikia na kuiabudu. Hao watakuwa kama kikoi hiki ambacho hakifai kitu.
11 Kama vile kikoi kinavyoshikamana na kiuno cha mtu, ndivyo nilivyowashikamanisha nami watu wa Israeli na watu wa Yuda, ili wajulikane kwa jina langu, wanisifu na kunitukuza. Lakini wao hawakunisikiliza. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
12 Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, aliniambia hivi: “Waambie watu wa Israeli kwamba kila mtungi utajazwa divai. Lakini utakapowaambia hivyo, wao watakujibu hivi: ‘Kwani unadhani sisi hatujui kwamba kila mtungi utajazwa divai?’
13 Nawe utawaambia kuwa mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Nitawalewesha wenyeji wote wa nchi hii; wafalme wanaotawala mahali pa Daudi, makuhani, manabii na wakazi wote wa Yerusalemu.
14 Nitawagonganisha wao kwa wao kina baba na watoto. Sitawahurumia, sitawaachia wala sitawarehemu, bali nitawaangamiza.”
15 Enyi Waisraeli, sikilizeni kwa makini, msiwe na majivuno maana Mwenyezi-Mungu anasema nanyi.
16 Mtukuzeni Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, kabla hajawaletea giza, nanyi mkajikwaa miguu kwenye milima ya giza. Nyinyi mnatazamia mwanga, lakini anaugeuza kuwa utusitusi na kuufanya kuwa giza nene.
17 Lakini kama msiponisikiliza, moyo wangu utalia machozi faraghani, kwa sababu ya kiburi chenu. Nitalia kwa uchungu na kububujika machozi, kwa kuwa watu wa Mwenyezi-Mungu wametekwa.
18 Mwambie mfalme na mama yake hivi: “Shukeni kwenye viti vyenu vya enzi, maana taji zenu nzuri zimeanguka vichwani mwenu.
19 Miji ya Negebu imezingirwa; hakuna awezaye kufungua malango yake. Watu wa Yuda wamechukuliwa mateka, wote kabisa wamepelekwa utumwani.”
20 Inua macho yako, ee Yerusalemu! Tazama! Madui zako waja kutoka kaskazini. Kundi ulilokabidhiwa liko wapi? Kundi lako zuri li wapi?
21 Utasemaje juu ya wale uliodhani ni rafiki, wale ambao wewe mwenyewe uliwafundisha, watakapokushinda na kukutawala? Je, si utakumbwa na uchungu kama wa mama anayejifungua?
22 Nawe utajiuliza moyoni mwako, “Kwa nini mambo haya yamenipata?” Sawa! Kama vazi lako limepandishwa juu, nawe ukatendewa kwa ukatili mno, hayo ni matokeo ya makosa yako mengi mno.
23 Je, Mwethiopia aweza kubadili rangi yake, au chui madoadoa yake? Ikiwezekana, nanyi pia mnaweza kutenda mema, nyinyi mliozoea kutenda maovu!
24 Mwenyezi-Mungu atawatawanya kama makapi yanayopeperushwa na upepo kutoka jangwani.
25 Mwenyezi-Mungu asema: “Hayo ndiyo yatakayokupata, ndivyo nilivyoamua kukutenda mimi Mwenyezi-Mungu, kwa sababu umenisahau mimi, ukaamini miungu ya uongo.
26 Nitalipandisha vazi lako hadi kichwani na aibu yako yote itaonekana wazi.
27 Nimeyaona machukizo yako: Naam, uzinifu wako na uzembe wako, na uasherati wako wa kupindukia, juu ya milima na mashambani. Ole wako ee Yerusalemu! Mpaka lini utakaa bila kutakaswa?”
1 Neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Yeremia kuhusu ule ukame:
2 “Watu wa Yuda wanaomboleza, na malango yao yanalegea. Watu wake wanaomboleza udongoni na kilio cha Yerusalemu kinapanda juu.
3 Wakuu wake wanawatuma watumishi wao maji; watumishi wanakwenda visimani, lakini maji hawapati; wanarudi na vyombo vitupu. Kwa aibu na fadhaa wanafunika vichwa vyao.
4 Wakulima wanahuzunika na kufunika vichwa vyao kwa kuona jinsi ardhi ilivyonyauka.
5 Hata kulungu porini anamwacha mtoto wake mchanga, kwa sababu hakuna nyasi.
6 Pundamwitu wanasimama juu ya vilele vikavu, wanatweta kwa kukosa hewa kama mbweha; macho yao yanafifia kwa kukosa chakula.
7 “Nao watu wanasema: Ingawa dhambi zetu zashuhudia dhidi yetu, utusaidie ee Mwenyezi-Mungu kwa heshima ya jina lako. Maasi yetu ni mengi, tumetenda dhambi dhidi yako.
8 Ewe uliye tumaini la Israeli, mwokozi wetu wakati wa taabu, utakuwaje kama mgeni nchini mwetu, kama msafiri alalaye usiku mmoja?
9 Utakuwaje kama mtu uliyechanganyikiwa, kama shujaa asiyeweza kusaidia mtu? Lakini wewe ee Mwenyezi-Mungu, u pamoja nasi; sisi twaitwa kwa jina lako, usituache.”
10 Mwenyezi-Mungu asema hivi juu ya watu hawa: “Kweli wamependa sana kutangatanga, wala hawakujizuia; kwa hiyo mimi Mwenyezi-Mungu siwapokei. Sasa nitayakumbuka makosa yao, na kuwaadhibu kwa dhambi zao.”
11 Mwenyezi-Mungu aliniambia hivi: “Usiwaombee watu hawa fanaka.
12 Hata wakifunga, sitayasikiliza maombi yao, na hata wakinitolea sadaka za kuteketeza na za nafaka, mimi sitazikubali. Bali nitawaangamiza kwa upanga, njaa na tauni.”
13 Kisha mimi nikasema, “Tazama, ee Bwana Mwenyezi-Mungu! Manabii wanawaambia watu hawa kwamba hapatakuwa na vita wala njaa, kwa sababu umeahidi kuwa patakuwa na amani tu katika nchi yetu.”
14 Naye Mwenyezi-Mungu, akaniambia: “Hao manabii wanatoa unabii wa uongo kwa jina langu. Mimi sikuwatuma, wala sikuwaamuru, wala sikusema nao. Wanawatabiria maono ya uongo, maaguzi yasiyo na maana yoyote, uongo wanaojitungia wenyewe.
15 Kwa hiyo, mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi kuhusu hao manabii wanaotabiri kwa jina langu, ingawa mimi sikuwatuma, na wanaosema kwamba hapatakuwa na vita wala njaa katika nchi hii: Manabii hao wataangamia kwa upanga na kwa njaa.
16 Na hao ambao waliwatabiria mambo hayo, watatupwa nje katika barabara za Yerusalemu wakiwa wamekufa kwa njaa na vita, wala hapatakuwa na mtu wa kuwazika. Hayo yatawapata wao wenyewe, wake zao, watoto wao wa kike na wa kiume; maana mimi nitawamwagia uovu wao wenyewe.
17 Hivi ndivyo utakavyowaambia: Laiti macho yangetoa machozi kutwa kucha, wala yasikome kububujika, maana, watu wangu wamejeruhiwa vibaya, wamepata pigo kubwa sana.
18 Nikienda nje mashambani, naiona miili ya waliouawa vitani; nikiingia ndani ya mji, naona tu waliokufa kwa njaa! Manabii na makuhani wanashughulikia mambo yao nchini, wala hawajui wanalofanya.”
19 Ee Mwenyezi-Mungu, je, umemkataa Yuda kabisa? Je, moyo wako umechukizwa na Siyoni? Kwa nini umetupiga vibaya, hata hatuwezi kupona tena? Tulitazamia amani, lakini hatukupata jema lolote; tulitazamia wakati wa kuponywa, badala yake tukapata vitisho.
20 Tunakiri uovu wetu, ee Mwenyezi-Mungu, tunakiri uovu wa wazee wetu, maana, tumekukosea wewe.
21 Usitutupe, kwa heshima ya jina lako; usikidharau kiti chako cha enzi kitukufu. Ukumbuke agano ulilofanya nasi, wala usilivunje.
22 Je miungu ya uongo ya mataifa yaweza kuleta mvua? Au, je, mbingu zaweza kutoa manyunyu? Je, si wewe ee Mwenyezi-Mungu uliye Mungu wetu? Tunakuwekea wewe tumaini letu, maana wewe unayafanya haya yote.
1 Kisha Mwenyezi-Mungu akaniambia: “Hata kama Mose na Samueli wangesimama mbele yangu na kunisihi, nisingewahurumia watu hawa. Waondoe kabisa mbele yangu. Waache waende zao!
2 Na wakikuuliza, ‘Twende wapi?’ wewe utawajibu kuwa mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Waliopangiwa kufa kwa maradhi, watakufa kwa maradhi; waliopangiwa kufa kwa upanga, watakufa kwa upanga; waliopangiwa kufa kwa njaa, watakufa kwa njaa; na waliopangiwa kuwa mateka, watatekwa mateka.
3 Mimi Mwenyezi-Mungu nimeamua kuwaletea aina nne za maangamizi: Vita itakayowaua, mbwa watakaowararua; ndege wa angani watakaowadonoa na wanyama wa porini watakaowatafuna na kuwamaliza.
4 Nitawafanya kuwa kitu cha kutisha kwa falme zote za dunia, kwa sababu ya mambo ambayo Manase mwana wa Hezekia, aliyafanya huko Yerusalemu, alipokuwa mfalme wa Yuda.
5 “Ni nani atakayewahurumia, enyi watu wa Yerusalemu? Ni nani atakayeomboleza juu yenu? Nani atasimama kuuliza habari zenu?
6 Nyinyi mmenikataa mimi, nasema mimi Mwenyezi-Mungu; nyinyi mmeniacha mkarudi nyuma. Hivyo nimenyosha mkono kuwaangamiza, kwa kuwa nimechoka kuwahurumia.
7 Nimewapepeta kwa chombo cha kupuria, katika kila mji nchini; nimewaangamiza watu wangu, kwa kuwaulia mbali watoto wao, lakini hawakuacha njia zao.
8 Wajane wao wamekuwa wengi kuliko mchanga wa bahari. Kina mama wa watoto walio vijana nimewaletea mwangamizi mchana. Nimesababisha uchungu na vitisho viwapate kwa ghafla.
9 Mama aliyesifika kuwa na watoto saba; sasa ghafla hana kitu. Ametoa pumzi yake ya mwisho, jua lake limetua kukiwa bado mchana; ameaibishwa na kufedheheshwa. Na wale waliobaki hai nitawaacha wauawe kwa upanga na maadui zao. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
10 Ole wangu, mama yangu, kwamba ulinizaa! Mimi nimekuwa mtu wa ubishi na ugomvi nchini pote! Sijapata kukopesha mtu wala kukopeshwa na mtu, lakini kila mtu ananiapiza.
11 Haya basi, ee Mwenyezi-Mungu, acha laana hizo nizipate kama sijakutumikia vema na kama sikukusihi kwa ajili ya maadui zangu wakati walipokuwa katika taabu na shida!
12 Je, mtu aweza kuvunja chuma, chuma kitokacho kaskazini, au shaba?
13 Mwenyezi-Mungu asema: “Nitaifanya mali yenu na hazina zenu zichukuliwe nyara tena bila kulipwa fidia yoyote kwa sababu ya dhambi zenu zote mlizotenda kila mahali nchini.
14 Nitawafanya muwatumikie maadui zenu katika nchi msiyoijua kwa sababu hasira yangu imewaka moto ambao hautazimwa milele.”
15 Nami nikasema: “Lakini wewe Mwenyezi-Mungu wajua; unikumbuke na kuja kunisaidia. Nilipizie kisasi watesi wangu. Wewe u mvumilivu, usiniache niangamie; kumbuka kuwa ninatukanwa kwa ajili yako.
16 Mara maneno yako yalipofika, niliyameza; nayo yakanifanya niwe na furaha, yakawa utamu moyoni mwangu, maana mimi najulikana kwa jina lako, ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi.
17 Sikuketi pamoja na wanaostarehe, wala sikufurahi pamoja nao. Niliketi peke yangu nimelemewa nguvu yako; kwa maana ulinijaza hasira yako.
18 Kwa nini mateso yangu hayaishi? Mbona jeraha langu haliponi, wala halitaki kutibiwa? Ama kweli umenidanganya, kama kijito cha maji ya kukaukakauka!”
19 Mwenyezi-Mungu akajibu: “Kama ukinirudia nitakurudishia hali ya kwanza, nawe utanitumikia tena. Kama ukisema maneno ya maana na sio ya upuuzi, basi utakuwa msemaji wangu. Watu watakuja kujumuika nawe, wala sio wewe utakayekwenda kwao.
20 Mbele ya watu hawa, nitakufanya ukuta imara wa shaba. Watapigana nawe, lakini hawataweza kukushinda, maana, mimi niko pamoja nawe, kukuokoa na kukukomboa. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
21 Nitakuokoa mikononi mwa watu waovu, na kukukomboa makuchani mwa wakatili.”
1 Neno la Mwenyezi-Mungu lilinijia na kusema:
2 “Wewe hutaoa wala hutapata watoto mahali hapa.
3 Maana mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi juu ya watoto wa kiume na wa kike watakaozaliwa mahali hapa, na juu ya wazazi wao:
4 Hao watakufa kwa maradhi mabaya, na hakuna atakayewaombolezea wala kuwazika. Maiti zao zitazagaa kama mavi juu ya ardhi. Wataangamia kwa upanga na kwa njaa; na maiti zao zitakuwa chakula cha ndege wa angani na wanyama wakali wa nchi.
5 “Maana mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Usiingie kabisa katika nyumba ya matanga wala usiende kuomboleza wala kuwalilia. Kwa maana nimeondoa amani yangu, fadhili zangu na huruma yangu kutoka kwa watu hawa.
6 Wote, wakubwa kwa wadogo, watakufa katika nchi hii; nao hawatazikwa, wala hakuna atakayewaombolezea. Hakuna atakayejikatakata au kunyoa upara wa matanga.
7 Hakuna atakayemshirikisha aliyefiwa chakula cha kumfariji, wala kumpatia kinywaji cha kumfariji anywe kwa ajili ya kufiwa na mama au baba yake.
8 “Usiingie katika nyumba wanamofanya karamu. Usiketi kula na kunywa pamoja nao.
9 Maana mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, nasema hivi: Nitazikomesha kabisa kutoka mahali hapa sauti za furaha na za shangwe, pamoja na sauti za bwana arusi na bibi arusi. Yote haya nitayafanya wakati wa uhai wenu mkiwa mnaona waziwazi.
10 Nawe utakapowaambia watu hao maneno haya yote, wao watakuuliza, ‘Kwa nini Mwenyezi-Mungu ametamka uovu huu mkubwa dhidi yetu? Tumefanya kosa gani? Tumetenda dhambi gani dhidi ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu?’
11 Nawe utawajibu kuwa mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Wazee wenu waliniacha, wakaifuata miungu mingine, wakaitumikia na kuiabudu. Waliniacha, wala hawakuzitii sheria zangu.
12 Nyinyi mmefanya vibaya zaidi kuliko wazee wenu, maana kila mmoja wenu ni mkaidi na mwenye nia mbaya, wala hamnisikilizi.
13 Kwa hiyo, nitawatupilia mbali kutoka nchi hii mpaka kwenye nchi ambayo nyinyi wenyewe wala wazee wenu hawakuijua. Huko mtaitumikia miungu mingine usiku na mchana, wala sitawafadhili.
14 “Kwa hiyo siku zaja, nasema mimi Mwenyezi-Mungu ambapo watu hawataapa tena kwa kusema, ‘Kama aishivyo Mwenyezi-Mungu aliyewatoa watu wa Israeli kutoka nchini Misri’;
15 bali wataapa kwa kusema, ‘Kama aishivyo Mwenyezi-Mungu aliyewatoa Waisraeli kutoka nchi ya kaskazini na kutoka katika nchi zote alikowafukuzia!’ Maana, nitawarudisha katika nchi yao niliyowapa wazee wao.”
16 Mwenyezi-Mungu asema: “Tazama, nitaita wavuvi wengi waje kuwakamata watu hawa. Kisha, nitaita wawindaji wengi watakaowawinda katika kila mlima, kila kilima na katika mapango ya miambani.
17 Maana, mimi nayaona matendo yao yote. Hakuna chochote kilichofichika kwangu. Makosa yao yote ni wazi mbele yangu.
18 Nitalipiza kisasi maradufu juu ya dhambi zao na makosa yao kwa sababu wameitia unajisi nchi yangu kwa mizoga ya miungu yao ya kuchukiza, wakaijaza hii nchi yangu machukizo yao.”
19 Ee Mwenyezi-Mungu! Wewe ndiwe nguvu yangu na ngome yangu; wewe ni kimbilio langu wakati wa taabu. Mataifa toka pande zote duniani yatakujia na kusema: “Wazee wetu hawakuwa na kitu ila miungu ya uongo, vitu duni visivyo na faida yoyote.
20 Je, binadamu aweza kujitengenezea miungu? Basi, hao si miungu hata kidogo!”
21 “Kwa hiyo,” asema Mwenyezi-Mungu, “wakati huu nitawafundisha watambue waziwazi nguvu zangu na uwezo wangu, nao watajua kwamba jina langu ni Mwenyezi-Mungu.
1 “Dhambi ya watu wa Yuda, imeandikwa kwa kalamu ya chuma; kwa ncha ya almasi imechorwa mioyoni mwao na katika pembe za madhabahu zao,
2 wakati watu wake wanakumbuka madhabahu zao na sanamu za mungu wa kike, Ashera, zilizowekwa kando ya miti mibichi juu ya vilele vya vilima,
3 na juu ya milima katika sehemu tambarare. Mali yenu na hazina zenu zote nitazitoa zitekwe nyara kulipia dhambi zenu mlizotenda kila mahali nchini mwenu.
4 Itawabidi muiachilie hiyo nchi yenu niliyowapeni, nami nitawafanya muwatumikie maadui zenu katika nchi msiyoijua, kwa sababu hasira yangu imewaka moto usiozimika milele.”
5 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Alaaniwe mtu anayemtegemea binadamu, mtu ambaye anategemea nguvu za binadamu, mtu ambaye moyo wake umeniacha mimi Mwenyezi-Mungu.
6 Huyo ni kama kichaka jangwani, hataona chochote chema kikimjia. Ataishi mahali pakavu nyikani, katika nchi ya chumvi isiyokaliwa na watu.
7 “Abarikiwe mtu anayemtegemea Mwenyezi-Mungu, mtu ambaye Mwenyezi-Mungu ndiye tegemeo lake.
8 Huyo ni kama mti uliopandwa kando ya maji, upenyezao mizizi yake karibu na chemchemi. Hauogopi wakati wa joto ufikapo, majani yake hubaki mabichi. Hauhangaiki katika mwaka wa ukame, na hautaacha kuzaa matunda.
9 “Moyo wa mtu ni mdanganyifu kuliko vitu vyote; hauwezi kuponywa, hakuna awezaye kuuelewa!
10 Mimi Mwenyezi-Mungu hupima akili na kuchunguza mpaka ndani ya moyo wa mtu. Na hivyo humtendea kila mmoja, kulingana na mwenendo wake, kadiri ya matendo yake.”
11 Mtu apataye mali isiyo halali ni kama kware akusanyaye makinda ambayo hakuyaangua: Wakati wa kilele cha ujana wake itamchopoka, na mwishoni atakuwa mtu mpumbavu.
12 Kuna kiti cha enzi kitukufu kiti kilichoinuliwa juu; huko ndiko mahali petu patakatifu.
13 Ee Mwenyezi-Mungu tumaini la Israeli, wote wanaokukataa wataaibishwa; wanaokuacha wewe watatoweka, kama majina yaliyoandikwa vumbini, kwa maana wamekuacha wewe Mwenyezi-Mungu, uliye chemchemi ya maji ya uhai.
14 Uniponye, ee Mwenyezi-Mungu, nami nitapona; uniokoe, nami nitaokoka; maana, wewe ndiwe sifa yangu.
15 Tazama watu wanavyoniambia: “Jambo alilotishia Mwenyezi-Mungu liko wapi? Acha basi lije!”
16 Sikuikimbia huduma yako ya kuwa mchungaji wala sikutamani ile siku ya maafa ije. Wewe mwenyewe wajua nilichosema kwa mdomo wangu, nilichotamka wakijua waziwazi.
17 Usiwe tisho kwangu; wewe ndiwe kimbilio langu siku ya maafa.
18 Waaibishwe wale wanaonitesa, lakini mimi usiniache niaibike. Wafedheheshwe watu hao, lakini mimi usiniache nifedheheke. Uwaletee siku ya maafa, waangamize kwa maangamizi maradufu!
19 Mwenyezi-Mungu aliniambia hivi: “Nenda ukasimame penye lango la watu ambapo wafalme wa Yuda huingia na kutoka mjini, na katika malango mengine yote ya Yerusalemu useme:
20 Sikieni neno la Mwenyezi-Mungu enyi wafalme wa Yuda, nanyi watu wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu ambao huingia kwa kupitia malango haya.
21 Waambie kwamba mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Kwa usalama wa maisha yenu, muwe na hadhari msije mkabeba mzigo siku ya Sabato, au kuingiza mzigo mjini kupitia malango ya Yerusalemu.
22 Msibebe mzigo kutoka majumbani mwenu siku ya Sabato wala kufanya kazi. Iadhimisheni siku ya Sabato kama siku takatifu kama nilivyowaamuru wazee wenu.
23 Lakini wazee wenu hawakunisikiliza wala kujali, bali walivifanya vichwa vyao kuwa vigumu, wakakataa kusikia na kufuata maagizo yangu.
24 “Lakini mkinisikiliza mimi Mwenyezi-Mungu, mkaacha kuingiza mzigo wowote kupitia malango ya mji huu siku ya Sabato, wala kufanya kazi siku hiyo,
25 basi, wafalme na wana wa wafalme wanaomfuata mfalme Daudi katika utawala, pamoja na watu wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu, wataingia kwa kupitia malango ya mji huu, wakiwa wamepanda farasi na magari ya farasi. Nao mji huu utakuwa na watu daima.
26 Watu watakuja kutoka miji ya Yuda na maeneo ya kandokando ya Yerusalemu, kutoka nchi ya Benyamini, kutoka Shefela, kutoka nchi ya milima na kutoka Negebu, wakileta sadaka za kuteketezwa na tambiko, sadaka za nafaka na ubani wa harufu nzuri, pamoja na matoleo ya shukrani. Vyote hivyo watavileta katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu.
27 Lakini msiponisikiliza na kuiadhimisha siku ya Sabato kama siku takatifu, msipoacha kubeba mizigo na kuingia nayo kupitia malango ya Yerusalemu siku ya Sabato, basi, nitawasha moto katika malango yake, nao utayateketeza majumba yote ya fahari ya Yerusalemu nao hautazimwa kamwe.”
1 Neno la Mwenyezi-Mungu lilinijia:
2 “Yeremia, inuka uende nyumbani kwa mfinyanzi, na huko nitakupa maneno yangu.”
3 Basi, nikateremka mpaka nyumbani kwa mfinyanzi, nikamkuta mfinyanzi akifanya kazi yake penye gurudumu la kufinyangia.
4 Na ikawa kwamba chombo alichokifinyanga kilipoharibika mikononi mwake, yeye alifinyanga upya chombo kingine kadiri ilivyompendeza.
5 Kisha, neno la Mwenyezi-Mungu likanijia:
6 “Enyi Waisraeli! Je, mimi Mwenyezi-Mungu siwezi kuwafanya nyinyi kama alivyofanya mfinyanzi huyu? Jueni kuwa kama ulivyo udongo mikononi mwa mfinyanzi, ndivyo nyinyi mlivyo mikononi mwangu.
7 Wakati wowote nitakapotoa tamko kuhusu taifa au ufalme kwamba nitalingoa na kulivunja na kuliangamiza,
8 halafu taifa hilo likageuka na kuacha uovu wake, basi, mimi nitaacha kulitendea yale mambo niliyokusudia kulitendea.
9 Hali kadhalika, wakati wowote nikitoa tamko kuhusu taifa au ufalme kwamba nitalijenga na kulistawisha,
10 kisha taifa hilo likafanya uovu mbele yangu na kukataa kunitii, basi, mimi nitaacha kulitendea mema hayo niliyokusudia kulitendea.
11 Sasa, basi, waambie watu wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu kuwa mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Mimi Hufinyanga jambo ovu dhidi yenu na kufanya mpango dhidi yenu. Rudini na kuacha njia zenu mbaya, mkarekebishe mienendo yenu na matendo yenu.
12 Lakini wao watasema, ‘Hiyo ni bure tu! Tutafuata mipango yetu wenyewe na kila mmoja wetu atafanya kwa kiburi kadiri ya moyo wake mwovu.’”
13 Basi, Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Yaulize mataifa yote: Nani amewahi kusikia jambo kama hili. Israeli amefanya jambo la kuchukiza mno.
14 Je, majabali ya Lebanoni hukosa theluji? Je, vijito vya maji vya milima yake hukauka?
15 Lakini watu wangu wamenisahau mimi, wanafukizia ubani miungu ya uongo. Wamejikwaa katika njia zao, katika barabara za zamani. Wanapitia vichochoroni badala ya njia kuu.
16 Wameifanya nchi yao kuwa kitisho, kitu cha kuzomewa daima. Kila mtu apitaye huko hushangaa na kutikisa kichwa chake.
17 Nitawatawanya mbele ya adui, kama upepo utokao mashariki. Nitawapa kisogo badala ya kuwaonesha uso wangu siku hiyo ya kupata maafa yao.”
18 Kisha, watu wakasema: “Njoni tumfanyie Yeremia njama, maana hatukosi makuhani wa kutufundisha, wenye hekima wa kutushauri na manabii wa kututangazia ujumbe wa Mungu! Njoni tumshtaki kwa maneno yake mwenyewe, wala tusiyatilie maanani yote asemayo.”
19 Basi, mimi nikasali: Nitegee sikio ee Mwenyezi-Mungu, usikilize ombi langu.
20 Je, mtu hulipwa mabaya kwa mema? Walakini, wamenichimbia shimo. Kumbuka nilivyosimama mbele yako, nikasema mema kwa ajili yao, ili kuiepusha hasira yako mbali nao.
21 Kwa hiyo waache watoto wao wafe njaa, waache wafe vitani kwa upanga. Wake zao wawe tasa na wajane. Waume zao wafe kwa maradhi mabaya na vijana wao wachinjwe kwa upanga vitani.
22 Kilio na kisikike majumbani mwao, unapowaletea kundi la wanyanganyi ghafla. Maana wamechimba shimo waninase; wameitegea mitego miguu yangu.
23 Lakini wewe, ee Mwenyezi-Mungu, wazijua njama zao zote za kuniua. Usiwasamehe uovu wao, wala kufuta dhambi zao. Waanguke chini mbele yako; uwakabili wakati wa hasira yako.
1 Mwenyezi-Mungu aliniambia: “Nenda ukanunue gudulia la udongo kwa mfinyanzi. Kisha, wachukue baadhi ya wazee wa watu na baadhi ya makuhani viongozi,
2 halafu uende pamoja nao katika bonde la Mwana wa Hinomu, kwa kupitia lango la Vigae. Ukifika huko, tangaza maneno ninayokuambia.
3 Utasema hivi: Sikilizeni neno la Mwenyezi-Mungu enyi wafalme wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu. Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi: Kweli ninaleta maafa mabaya mahali hapa, hata kila mmoja atakayesikia habari zake, atapigwa na bumbuazi.
4 Kwa maana watu wameniacha mimi na kupatia unajisi mahali hapa kwa kufukizia ubani miungu mingine; miungu ambayo wao wenyewe, wazee wao wala wafalme wa Yuda hawajapata kuijua. Pia wamepajaza mahali hapa damu ya watu wasio na hatia,
5 wakamjengea mungu Baali madhabahu, ili kuwachoma wana wao kama sadaka ya kuteketezwa. Mimi sijapata kuamuru wala kuagiza jambo kama hilo lifanywe, wala hata sijapata kulifikiria.
6 Kwa hiyo, jueni kuwa siku zaja ambapo mahali hapa hapataitwa tena Tofethi, wala bonde la Mwana wa Hinomu, bali pataitwa bonde la Mauaji. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
7 Na papa hapa nitaivuruga mipango ya Yuda na Yerusalemu. Nitawafanya watu wao washindwe na kuuawa na maadui zao vitani na kuangamizwa na wale wanaowawinda. Maiti zao nitawaachia ndege wa anga na wanyama wa porini kuwa chakula chao.
8 Nitaufanya mji huu kuwa mahali pa kushangaza; naam, nitaufanya uwe kitu cha kuzomewa. Kila mtu anayepita karibu nao atashangaa na kuuzomea kwa sababu ya maafa yote yatakayoupata.
9 Maadui watauzingira na kujaribu kuwaua watu wake. Watasababisha hali mbaya sana mjini humo hata watu watawala watoto wao wa kike na wa kiume, na kila mtu atamla mwenzake.
10 Kisha wewe utalivunja gudulia hilo mbele ya watu hao watakaokwenda pamoja nawe,
11 na kuwaambia kuwa mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, nasema hivi: Ndivyo nitakavyovunjavunja watu hawa na mji huu kama vile mtu avunjavyo chombo cha mfinyanzi, hata kisiweze kamwe kutengenezwa tena. Watu watazikwa Tofethi, kwa sababu hapatakuwa na mahali pengine pa kuzikia.
12 Hivyo ndivyo nitakavyopatenda mahali hapa na wakazi wake; nitaufanya mji huu kama Tofethi.
13 Nyumba za Yerusalemu na ikulu za wafalme wa Yuda, naam, nyumba zote ambazo juu ya paa zake watu walifukiza ubani kwa sayari za mbinguni, na kumiminia miungu mingine tambiko za divai, zote zitatiwa unajisi kama Tofethi.”
14 Baada ya hayo, Yeremia aliondoka Tofethi, mahali ambako Mwenyezi-Mungu alimtuma aende kutoa unabii, akaenda na kusimama katika ukumbi wa nyumba ya Mwenyezi-Mungu, akawatangazia watu wote akisema:
15 “Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi: Tazama, mimi nitauletea mji huu na vijiji vyote vilivyo jirani maafa yote niliyoutangazia, kwa sababu wakazi wake ni wakaidi na wamekataa kusikia maneno yangu.”
1 Kuhani Pashuri mwana wa Imeri, ambaye alikuwa ofisa mkuu wa nyumba ya Mwenyezi-Mungu, alimsikia Yeremia akitoa unabii huo.
2 Basi, Pashuri akampiga nabii Yeremia na kumtia kifungoni upande wa lango la juu la Benyamini, katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu.
3 Kesho yake asubuhi, Pashuri alipomtoa Yeremia katika mkatale huo, Yeremia alimwambia hivi: “Mwenyezi-Mungu hakuiti tena Pashuri, bali ‘Kitisho Pande Zote’.
4 Maana, Mwenyezi-Mungu asema hivi: ‘Tazama, nitakufanya uwe kitisho kwako wewe mwenyewe na kwa rafiki zako wote. Wao watauawa vitani kwa upanga wa maadui zao huku ukiangalia. Nitawatia watu wote wa Yuda mikononi mwa mfalme wa Babuloni, naye atawachukua mateka hadi Babuloni na kuwaua kwa upanga.
5 Zaidi ya hayo, utajiri wote wa mji, mapato yake yote, vitu vyake vyote vya thamani pamoja na hazina zote za wafalme wa Yuda, nitazitia mikononi mwa maadui zao ambao watazipora na kuchukua kila kitu hadi Babuloni.
6 Na kwa upande wako wewe Pashuri, pamoja na nyumba yako yote, mtapelekwa utumwani; hakika mtakwenda Babuloni. Huko ndiko utakakofia na kuzikwa, kadhalika na rafiki zako wote ambao uliwatabiria uongo.’”
7 Ee Mwenyezi-Mungu, wewe umenidanganya, nami kweli nikadanganyika; wewe una nguvu kuliko mimi, nawe umeshinda. Kutwa nzima nimekuwa mtu wa kuchekwa, kila mtu ananidhihaki.
8 Kila ninaposema kitu, nalalamika, napaza sauti, “Ukatili na uharibifu!” Maana kwangu kutangaza neno la Mwenyezi-Mungu kwanifanya nishutumiwe na kudhihakiwa kutwa nzima.
9 Lakini nikisema, “Sitamtaja Mwenyezi-Mungu, wala sitasema tena kwa jina lake,” moyoni mwangu huwa na kitu kama moto uwakao, uliofungiwa ndani ya mifupa yangu. Najaribu sana kuuzuia humo, lakini ninashindwa.
10 Nasikia wengi wakinongona juu yangu. Wananipanga jina: “Kitisho kila upande!” Wengine wanasema: “Nendeni mkamshtaki! Na tumshtaki!” Hata rafiki zangu wote wapenzi wanangojea tu nianguke! Wanasema “Labda atadanganyika, nasi tutalipiza kisasi.”
11 Lakini wewe Mwenyezi-Mungu u pamoja nami kwangu wewe ni kama shujaa wa kutisha; kwa hiyo watesi wangu watajikwaa, na hawataweza kunishinda. Wataaibika kupindukia, maana hawatafaulu. Fedheha yao itakuwa ya daima; kamwe haitasahaulika.
12 Ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi, wewe humthibiti mtu mwadilifu, huona yaliyo moyoni na akilini mwa watu, unijalie kuona ukiwalipiza kisasi, maana kwako nimekiweka kisa changu.
13 Mwimbieni Mwenyezi-Mungu; msifuni Mwenyezi-Mungu, kwani ameyaokoa maisha ya mhitaji, kutoka mikononi mwa watu waovu.
14 Na ilaaniwe siku niliyozaliwa! Siku hiyo mama aliponizaa, isitakiwe baraka!
15 Na alaaniwe aliyempelekea baba ujumbe: “Umepata mtoto wa kiume”, akamfanya ajae furaha.
16 Mtu huyo na awe kama miji aliyoiangusha Mwenyezi-Mungu bila huruma. Mtu huyo na asikie kilio asubuhi, na mchana kelele za vita,
17 kwani hakuniua tumboni mwa mama yangu; mama yangu angekuwa kaburi langu, tumbo lake lingebaki kubwa daima.
18 Kwa nini nilitoka tumboni mwa mama yangu? Je, nilitoka ili nipate taabu na huzuni na kuishi maisha ya aibu?
1 Hili ni neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Mwenyezi-Mungu, wakati mfalme Sedekia alipowatuma Pashuri mwana wa Malkia, na kuhani Sefania mwana wa Maaseya, wamwambie Yeremia hivi:
2 “Tafadhali, tuombee kwa Mwenyezi-Mungu maana Nebukadneza, mfalme wa Babuloni, anaanza vita dhidi yetu. Labda Mwenyezi-Mungu atatufanyia mwujiza kama afanyavyo mara kwa mara na kumfanya Nebukadneza atuache na kwenda zake.”
3 Yeremia akawaambia:
4 Nendeni mkamwambie Sedekia kwamba hivi ndivyo asemavyo Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli: “Sedekia! Nitakugeuzia wewe mwenyewe silaha unazotumia kupigana na mfalme wa Babuloni na Wakaldayo wanaowazingira nje ya kuta za mji. Nitazikusanya silaha zote katikati ya mji huu.
5 Mimi mwenyewe nitapigana nawe kwa mkono ulionyoka na wenye nguvu, kwa hasira, ukali na ghadhabu kubwa.
6 Nitawaua wakazi wa mji huu: Binadamu na wanyama kadhalika. Watakufa kwa maradhi mabaya sana.
7 Mimi Mwenyezi-Mungu nasema kuwa, baadaye wewe Sedekia mfalme wa Yuda, watumishi wako na watu wa mji huu ambao mtaponea maradhi hayo mabaya pamoja na vita na njaa, nitawatia mikononi mwa Nebukadneza mfalme wa Babuloni na mikononi mwa adui zenu wanaowawinda. Nebukadneza atawaua kwa upanga na wala hatawahurumia au kuwaachilia au kuwasamehe. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
8 “Nawe Yeremia utawaambia watu hawa kwamba mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Sikilizeni! Mimi nawapeni nafasi ya kuchagua njia ya uhai au njia ya kifo.
9 Mtu atakayebaki mjini humu atauawa kwa upanga au kwa njaa au kwa maradhi mabaya. Lakini mtu atakayetoka nje ya mji na kujisalimisha kwa Wakaldayo wanaouzingira mji, ataishi; naam, atayanusurisha maisha yake.
10 Nimeamua kuuletea mji huu maafa na sio mema, nasema mimi Mwenyezi-Mungu. Nitautia mikononi mwa mfalme wa Babuloni, naye atauteketeza kwa moto.
11 “Utaiambia jamaa ya mfalme wa Yuda: Sikilizeni neno la Mwenyezi-Mungu,
12 enyi jamaa ya Daudi! Mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Tekelezeni haki tangu asubuhi, na kuwakomboa mikononi mwa wadhalimu wote walionyanganywa mali zao. La sivyo, hasira yangu itachomoza kama moto, itawaka na wala hakuna atakayeweza kuizima, kwa sababu ya matendo yenu maovu.
13 Tazama, mimi sasa napambana nanyi mnaoishi bondeni, mnaokaa kwenye mwamba wa tambarare, nyinyi mnaosema, ‘Nani atathubutu kutushambulia? Nani awezaye kuingia katika makazi yetu?’
14 Nitawaadhibu kadiri ya matendo yenu; mimi Mwenyezi-Mungu nasema. Nitawasha moto katika msitu wenu nao utateketeza kila kitu kinachouzunguka.”
1 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Nenda katika ikulu ya mfalme wa Yuda, uwape watu ujumbe huu:
2 Wewe mfalme wa Yuda unayekikalia kiti cha enzi cha mfalme Daudi, pamoja na watumishi wako na watu wako wanaopita katika malango haya, sikilizeni neno langu mimi Mwenyezi-Mungu.
3 Mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Tendeni mambo ya haki na uadilifu. Mwokoeni mikononi mwa mdhalimu mtu yeyote aliyenyanganywa mali zake. Msiwatendee vibaya au ukatili wageni, yatima na wajane wala msimwage damu ya mtu asiye na hatia mahali hapa.
4 Kama mkishika neno hili nililowaambia basi, wafalme wanaokikalia kiti cha enzi cha Daudi wataendelea kuingia kwa kupitia malango ya ikulu hii. Watapita pamoja na watumishi wao na watu wao, wakiwa wamepanda farasi na magari ya farasi.
5 Lakini kama hamtatii maneno haya, mimi Mwenyezi-Mungu naapa kwa nafsi yangu kwamba mahali hapa patakuwa magofu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
6 Mwenyezi-Mungu asema hivi kuhusu ikulu ya mfalme wa Yuda: “Ingawa waonekana kuwa mzuri kama nchi ya Gileadi kama kilele cha Lebanoni, Lakini naapa kuwa nitakufanya uwe jangwa, uwe mji usiokaliwa na watu.
7 Nitawatayarisha waangamizi dhidi yako, kila mmoja na silaha yake mkononi. Wataikata mierezi yako mizuri, na kuitumbukiza motoni.
8 “Kisha watu wengi wa mataifa watapita karibu na mji huu, na kila mmoja atamwuliza mwenzake: ‘Kwa nini Mwenyezi-Mungu ameutenda hivi mji huu mkubwa?’
9 Wenzao watawajibu, ‘Ni kwa sababu waliliacha agano la Mwenyezi-Mungu, Mungu wao, wakaiabudu miungu mingine na kuitumikia.’”
10 Msimlilie mtu aliyekufa, wala msiombolezee kifo chake. Bali mlilieni kwa uchungu yule aendaye mbali, kwa kuwa hatarudi tena kuiona nchi yake.
11 Maana, Mwenyezi-Mungu asema hivi juu ya Shalumu mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, aliyetawala baada ya Yosia baba yake, na ambaye aliondoka mahali hapa: “Shalumu hatarudi tena mahali hapa,
12 bali atafia hukohuko walikomchukua utumwani. Kamwe hataiona tena nchi hii.
13 “Ole wako Yehoyakimu wewe unayejenga nyumba kwa dhuluma na kuiwekea ghorofa bila kutumia haki. Unawaajiri watu wakutumikie bure wala huwalipi mishahara yao.
14 Wewe wasema: ‘Nitalijenga jumba kubwa, lenye vyumba vikubwa ghorofani.’ Kisha huifanyia madirisha, ukafunika kuta zake kwa mbao za mierezi, na kuipaka rangi nyekundu!
15 Unadhani umekuwa mfalme kwa kushindana kujenga kwa mierezi? Baba yako alikula na kunywa, akatenda mambo ya haki na mema ndipo mambo yake yakamwendea vema.
16 Aliwapatia haki maskini na wahitaji, na mambo yake yakamwendea vema. Hii ndiyo maana ya kunijua mimi Mwenyezi-Mungu.
17 Lakini macho yako wewe na moyo wako, hungangania tu mapato yasiyo halali. Unamwaga damu ya wasio na hatia, na kuwatendea watu dhuluma na ukatili.
18 “Kwa hiyo, mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi juu ya Yehoyakimu mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda: Wakati atakapokufa, hakuna atakayemwombolezea akisema, ‘Ole, kaka yangu!’ ‘Ole, dada yangu!’ Hakuna atakayemlilia akisema, ‘Maskini, bwana wangu!’ ‘Maskini, mfalme wangu!’
19 Atazikwa bila heshima kama punda, ataburutwa na kutupiliwa mbali, nje ya malango ya Yerusalemu.”
20 Enyi watu wa Yerusalemu, pandeni Lebanoni mpige kelele, pazeni sauti zenu huko Bashani; lieni kutoka milima ya Abarimu, maana wapenzi wenu wote wameangamizwa.
21 Mwenyezi-Mungu aliongea nanyi mlipokuwa na fanaka, lakini nyinyi mkasema, “Hatutasikiliza.” Hii ndiyo tabia yenu tangu ujana wenu, hamjapata kuitii sauti ya Mwenyezi-Mungu.
22 Viongozi wenu watapeperushwa na upepo, wapenzi wenu watachukuliwa uhamishoni. Ndipo mtakapoona haya na kufadhaika, kwa sababu ya uovu wenu wote mliotenda.
23 Enyi wakazi wote wa Lebanoni, nyinyi mkaao salama kati ya mierezi; jinsi gani mtakavyopiga kite uchungu utakapowakumba, uchungu kama wa mama anayejifungua!
24 Na kuhusu Konia mfalme wa Yuda, mwanawe Yehoyakimu, Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Naapa kwa nafsi yangu mimi Mwenyezi-Mungu kwamba hata kama wewe Konia mwana wa Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, ungekuwa pete yangu ya mhuri katika mkono wangu wa kulia, ningekuvulia mbali.
25 Nitakutia mikononi mwa wale wanaotaka kuyamaliza maisha yako; naam, mikononi mwa wale unaowaogopa, mikononi mwa Nebukadneza, mfalme wa Babuloni; naam, mikononi mwa Wakaldayo.
26 Nitakufukuzia mbali katika nchi ya kigeni, wewe pamoja na mama yako mzazi. Mtakuwa watumwa katika nchi hiyo ambamo nyote wawili hamkuzaliwa, nanyi mtafia hukohuko.
27 Mtatamani kwa hamu kubwa kurudi katika nchi hii, lakini hamtarudi kamwe.
28 Je, huyu mtu Konia, amekuwa kama chungu kilichovunjika, ambacho hudharauliwa na kutupwa nje? Kwa nini yeye na watoto wake wametupwa mbali wakatupwa katika nchi wasiyoijua?
29 Ee nchi, ee nchi, ee nchi! Sikia neno la Mwenyezi-Mungu!
30 Mwenyezi-Mungu asema hivi: Mwandike mtu huyu kwamba hana watoto, mtu ambaye hatafanikiwa maishani mwake. Maana hakuna hata mmoja wa wazawa wake atakayekikalia kiti cha enzi cha Daudi na kutawala tena katika Yuda.
1 “Ole wao wachungaji wanaowaangamiza na kuwatawanya kondoo wa malisho yangu!”
2 Kwa hiyo, mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli nasema hivi kuhusu wachungaji wanaowachunga watu wangu: Nyinyi mmewatawanya kondoo wangu na kuwafukuza, wala hamkuwatunza. Basi, nami pia nitawaadhibu kwa ajili ya matendo yenu maovu.
3 Kisha, nitawakusanya kondoo wangu waliobaki kutoka nchi zote nilikowatawanya, na kuwarudisha malishoni mwao. Nao watazaa na kuongezeka.
4 Nitawapa wachungaji watakaowatunza vema, nao hawatakuwa na woga tena wala kufadhaika, na hakuna hata mmoja wao atakayepotea, mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
5 “Tazama, siku zaja nitakapomchipushia Daudi chipukizi adili. Huyo atatawala kama mfalme, na atatenda kwa busara, haki na uadilifu katika nchi.
6 Katika siku za utawala wake, Yuda ataokolewa na Israeli ataishi kwa usalama. Naye ataitwa, ‘Mwenyezi-Mungu ni uadilifu wetu.’
7 “Kwa hiyo siku zaja, nasema mimi Mwenyezi-Mungu, ambapo watu hawataapa tena kwa kusema, ‘Kama aishivyo Mwenyezi-Mungu aliyewatoa watu wa Israeli nchini Misri’,
8 bali wataapa kwa kusema, ‘Kama aishivyo Mwenyezi-Mungu aliyewatoa na kuwaongoza Waisraeli kutoka nchi ya kaskazini na kutoka nchi zote ambako aliwatawanya.’ Kisha wataishi katika nchi yao wenyewe.”
9 Kuhusu hao manabii wasiofaa, mimi imevunjika moyo, mifupa yangu yote inatetemeka; nimekuwa kama mlevi, kama mtu aliyelemewa na pombe, kwa sababu yake Mwenyezi-Mungu na maneno yake matakatifu.
10 Maana, nchi imejaa wazinzi; kwa sababu ya laana, nchi inaomboleza, na malisho ya nyanda zake yamekauka. Mienendo ya watu ni miovu, nguvu zao zinatumika isivyo halali.
11 Mwenyezi-Mungu asema: “Manabii na makuhani, wote hawamchi Mungu, uovu wao nimeuona hata nyumbani mwangu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
12 Kwa hiyo njia zao zitakuwa vichochoro vya utelezi gizani ambamo watasukumwa na kuanguka; maana, nitawaletea maafa, ufikapo mwaka wa kuwaadhibu, Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
13 “Miongoni mwa manabii wa Samaria, nimeona jambo la kuchukiza sana: Walitabiri kwa jina la Baali wakawapotosha watu wangu Waisraeli.
14 Lakini miongoni mwa manabii wa Yerusalemu, nimeona kinyaa cha kutisha zaidi: Wanafanya uzinzi na kusema uongo; wanawaunga mkono wanaotenda maovu hata pasiwe na mtu anayeachana na uovu. Kwangu wote wamekuwa kama watu wa Sodoma; wakazi wake wamekuwa wabaya kama watu wa Gomora.
15 “Kwa hiyo, mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi nasema hivi juu ya manabii wa Yerusalemu: Nitawalisha uchungu, na kuwapa maji yenye sumu wanywe. Maana, kutoka kwa manabii wa Yerusalemu kutomcha Mungu kumeenea kila mahali nchini.”
16 Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi: “Msisikilize maneno ya manabii wanaowatabiria; wanawapeni matumaini ya uongo. Wanayowaambia ni maono yao wenyewe, wala hayakutoka kwangu mimi Mwenyezi-Mungu.
17 Wao hawakomi kuwaambia wale wanaodharau neno langu mimi Mwenyezi-Mungu: ‘Mambo yatawaendea vema.’ Na kumwambia kila mtu afuataye kwa ukaidi fikira zake; ‘Hakuna baya lolote litakalokupata!’”
18 Lakini, ni yupi kati ya manabii hao aliyepata kuhudhuria baraza la Mwenyezi-Mungu, hata akasikia na kuelewa neno lake? Au ni nani aliyejali neno lake, hata akapata kulitangaza?
19 Tazama, dhoruba kutoka kwa Mwenyezi-Mungu! Ghadhabu imezuka; kimbunga cha tufani kitamlipukia mtu mwovu kichwani.
20 Hasira ya Mwenyezi-Mungu haitarudi nyuma, mpaka atakapotekeleza na kukamilisha matakwa ya moyo wake. Siku zijazo mtayaelewa vema mambo hayo.
21 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Mimi sikuwatuma hao manabii, lakini wao walikwenda mbio; sikuwaambia kitu chochote, lakini wao walitabiri!
22 Kama wangalihudhuria baraza langu, wangaliwatangazia watu wangu maneno yangu, wakawageuza kutoka katika njia zao mbovu, na kutoka katika matendo yao maovu.
23 “Mimi ni Mungu aliye karibu, si Mungu aliye mbali.
24 Je, mtu aweza kujificha mahali pa siri hata nisiweze kumwona? Hamjui kuwa mimi Mwenyezi-Mungu nipo kila mahali, mbinguni na duniani? Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
25 Mimi nimeyasikia maneno waliyosema hao manabii wanaotabiri uongo kwa jina langu, wakisema, ‘Nimeota ndoto, nimeota ndoto!’
26 Itakuwa hivyo mpaka lini? Hao manabii wataendelea mpaka lini kupotoka moyo; kutabiri uongo na udanganyifu wa mioyo yao wenyewe?
27 Kwa ndoto zao hizo wanapanga kuwafanya watu wangu wanisahau mimi kama baba zao walivyonisahau, wakamwendea Baali!
28 Nabii aliyeota ndoto, na aitangaze ndoto yake, lakini yeye aliye na neno langu, na alitangaze kwa uaminifu. Mimi Mwenyezi-Mungu nasema, makapi si sawa na ngano!
29 Neno langu ni kama moto; ni kama nyundo ipasuayo miamba vipandevipande.
30 Kwa hiyo, mimi Mwenyezi-Mungu nitawashambulia manabii ambao wanaibiana maneno yangu.
31 Kweli mimi Mwenyezi-Mungu nasema, nitawashambulia manabii wanaoropoka maneno yao wenyewe na kusema, ‘Mwenyezi-Mungu asema’.
32 Naam, mimi Mwenyezi-Mungu nasema kuwa nitawashambulia manabii wanaotabiri ndoto zao za uongo kwa watu wangu, na kuwapotosha kwa uongo wao na kuropoka kwao. Mimi sikuwatuma wala kuwaamuru waende; kwa hiyo hawatawafaa watu hao. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
33 Mwenyezi-Mungu aliniambia: “Mtu yeyote, awe nabii au kuhani, akikuuliza: ‘Uko wapi mzigo anaotubebesha Mwenyezi-Mungu?’ Wewe utawaambia: ‘Nyinyi ndio mzigo kwa Mwenyezi-Mungu naye atawatupa mbali.’
34 Tena nabii au kuhani, au mtu yeyote atakayesema ‘Mzigo wa Mwenyezi-Mungu,’ nitamwadhibu pamoja na jamaa yake yote.
35 Kitu mnachopaswa kuulizana nyinyi kwa nyinyi ni ‘Mwenyezi-Mungu amejibu nini?’ au, ‘Mwenyezi-Mungu amesema nini?’
36 Lakini jambo la ‘Mzigo wa Mwenyezi-Mungu,’ msilitaje tena. Kile anachosema binadamu ni mzigo kwake mwenyewe. Watu wanayapotosha maneno ya Mungu aliye hai, Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wao.
37 Basi mtamwuliza nabii hivi: ‘Mwenyezi-Mungu amekujibu nini?’ au, ‘Mwenyezi-Mungu amesema nini?’
38 Lakini wao wakivunja amri yangu na kusema, ‘Mzigo wa Mwenyezi-Mungu,’ wakati ambapo mimi niliwakataza wasiseme, ‘Mzigo wa Mwenyezi-Mungu,’ basi, waambie kuwa
39 mimi nitawanyanyua na kuwatupilia mbali, wao wenyewe pamoja na mji niliowapa wao na wazee wao.
40 Nitawaletea fedheha ya milele na aibu ya kudumu ambayo haitasahaulika.”
1 Baada ya Nebukadneza, mfalme wa Babuloni kuwahamisha Yekonia mwana wa Yehoyakimu mfalme wa Yuda, pamoja na viongozi wa Yuda, mafundi stadi na masonara, kutoka Yerusalemu na kuwapeleka Babuloni, Mwenyezi-Mungu alinionesha ono hili: Niliona vikapu viwili vya tini vimewekwa mbele ya hekalu la Mwenyezi-Mungu.
2 Kikapu cha kwanza kilikuwa na tini nzuri sana, kama tini za mwanzo wa mavuno. Lakini kikapu cha pili kilikuwa na tini mbaya sana, mbaya hata hazifai kuliwa.
3 Basi, Mwenyezi-Mungu akaniuliza: “Yeremia! Unaona nini?” Mimi nikamjibu: “Naona tini. Zile nzuri ni nzuri sana, na zile mbaya ni mbaya sana hata hazifai kuliwa.”
4 Hapo neno la Mwenyezi-Mungu likanijia:
5 “Basi, mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, nasema hivi: Kama tini hizi zilivyo nzuri, ndivyo nitakavyowaona kuwa wema watu wa Yuda ambao niliwatoa mahali hapa na kuwapeleka uhamishoni katika nchi ya Wakaldayo.
6 Nitawalinda daima na kuwarudisha katika nchi hii. Nitawajenga, wala sitawabomoa; nitawapanda, wala sitawangoa.
7 Nitawapa moyo wa kujua kuwa mimi ndimi Mwenyezi-Mungu. Watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao; maana watanirudia kwa moyo wao wote.
8 “Lakini mimi Mwenyezi-Mungu nasema: Kama tini zile mbaya, tini zilizo mbaya hata hazifai kuliwa, ndivyo nitakavyowatenda mfalme Sedekia wa Yuda, maofisa wake pamoja na watu wengine wote wa Yerusalemu waliobaki nchini humo, kadhalika na wale ambao walihamia nchini Misri.
9 Nitawafanya kuwa kitu cha kuchukiza mbele ya falme zote duniani. Watakuwa kitu cha dhihaka, kitu cha kuzomewa, kuchekwa na kulaaniwa kila mahali nitakapowafukuzia.
10 Nao nitawaletea vita, njaa na maradhi mabaya mpaka waangamizwe kabisa kutoka katika nchi niliyowapa wao na wazee wao.”
1 Mnamo mwaka wa nne wa utawala wa mfalme Yehoyakimu mwana wa Yosia, katika Yuda, Mwenyezi-Mungu alinimpa mimi Yeremia ujumbe kuhusu watu wa Yuda. Mwaka huo ulikuwa wa kwanza wa utawala wa Nebukadneza mfalme wa Babuloni.
2 Mimi Yeremia niliwaambia ujumbe huo watu wote wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu:
3 “Kwa muda wa miaka ishirini na mitatu sasa, yaani tangu mwaka wa kumi na tatu wa utawala wa mfalme Yosia mwana wa Amoni, mfalme wa Yuda, mpaka hivi leo, nimekuwa nikipata neno la Mungu na kuwaambieni kila wakati, lakini nyinyi hamkusikiliza.
4 Hamkutaka kusikiliza wala hamkutega sikio msikie, ingawa Mwenyezi-Mungu aliwaleteeni watumishi wake manabii kila wakati,
5 wakawaambieni kwamba kila mmoja wenu aachane na mwenendo wake mwovu na matendo yake mabaya, ili mpate kuishi katika nchi ambayo Mwenyezi-Mungu amewapa nyinyi na wazee wenu tangu zamani, muimiliki milele.
6 Mwenyezi-Mungu aliwaonya Mmsifuate miungu mingine wala kuitumikia na kumkasirisha Mungu kwa kuabudu sanamu ambazo mmejitengenezea wenyewe. Kama Mmkimtii Mwenyezi-Mungu basi, yeye hatawaadhibu.
7 Lakini Mwenyezi-Mungu asema kuwa nyinyi mlikataa kumsikiliza. Badala yake, mlimkasirisha kwa sanamu mlizojitengenezea wenyewe, na hivyo mkajiletea madhara nyinyi wenyewe.
8 “Kwa hiyo, mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi nasema hivi: “Kwa kuwa hamkuyatii maneno yangu,
9 basi, nitayaita makabila yote ya kaskazini, pamoja na mtumishi wangu Nebukadneza, mfalme wa Babuloni. Nitawaleta waishambulie nchi hii na wakazi wake pamoja na mataifa yote ya jirani. Nitawaangamiza kabisa, na kuwafanya kuwa kitu cha kuchukiza, kuzomewa na kudharauliwa milele.
10 Tena, nitakomesha miongoni mwao sauti za furaha, sauti za bwana arusi na bibi arusi. Sauti za kusaga hazitakuwapo, wala mwanga wa taa.
11 Nchi hii yote itakuwa magofu matupu na ukiwa, na mataifa ya jirani yatamtumikia mfalme wa Babuloni kwa muda wa miaka sabini.
12 Kisha baada ya miaka hiyo sabini kukamilika nitamwadhibu mfalme wa Babuloni pamoja na taifa hilo. Nitaiangamiza nchi hiyo ya Wakaldayo kwa sababu ya uovu wao na kuifanya nchi iwe magofu milele.
13 Nitailetea nchi hiyo mambo yote niliyotamka dhidi yake na yote yaliyoandikwa katika kitabu hiki ambayo Yeremia alitabiri dhidi ya mataifa yote.
14 Wababuloni nao itawalazimu kuwa watumwa wa mataifa mengine na wafalme wengine. Nitawaadhibu kadiri ya maovu yao waliyotenda.”
15 Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, aliniambia hivi: “Chukua mkononi mwangu hiki kikombe cha divai ya ghadhabu yangu uyanyweshe mataifa yote ninayokutuma kwao.
16 Mataifa hayo yatakunywa na kupepesuka na kurukwa na akili kwa sababu ya mauaji nitakayosababisha kati yao.”
17 Basi, nikachukua hicho kikombe mkononi mwa Mwenyezi-Mungu, nikayanywesha mataifa yote ambayo Mwenyezi-Mungu alinituma kwao.
18 Kwanza Yerusalemu na miji ya Yuda, wafalme wake na viongozi wake, ili kuifanya iwe jangwa, ukiwa, kitu cha kuzomewa na kulaaniwa, kama ilivyo mpaka leo. Halafu:
19 Farao, mfalme wa Misri, maofisa na viongozi wake, pamoja na watu wake wote;
20 wageni wote walioishi nchini Misri; wafalme wote wa nchi ya Uzi; wafalme wote wa miji ya Wafilisti, Ashkeloni, Gaza, Ekroni na mabaki ya Ashdodi.
21 Watu wote wa Edomu, Moabu na Amoni;
22 wafalme wote wa Tiro na Sidoni; wafalme wa nchi za pwani ya bahari ya Mediteranea;
23 wakazi wa Dedani, Tema, Buzi na watu wote wanyoao denge;
24 wafalme wote wa Arabia; wafalme wote wa makabila yaliyochanganyika jangwani;
25 wafalme wote wa Zimri, Elamu na Media;
26 wafalme wote wa kaskazini, mbali na karibu, mmoja baada ya mwingine. Falme zote ulimwenguni zitakunywa. Na, baada ya hao wote naye mfalme wa Babuloni atakunywa.
27 Mwenyezi-Mungu akaniamuru: “Utawaambia kuwa mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, nasema hivi: Kunyweni, mlewe na kutapika; angukeni wala msiinuke tena, kwa sababu ya mauaji ninayosababisha miongoni mwenu.
28 Kama wakikataa kukipokea kikombe hicho mkononi mwako na kunywa, wewe utawaambia kuwa mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, nasema kwamba ni lazima wanywe!
29 Tazama! Sasa ninaanza kuleta maafa katika mji unaoitwa kwa jina langu; je, mnadhani mnaweza kuepukana na adhabu? Hamtaachwa bila kuadhibiwa, maana ninaleta mauaji dhidi ya wakazi wote wa dunia. Mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi nimesema.
30 “Basi, wewe Yeremia utatabiri maneno haya yote dhidi yao, na kusema hivi: Mwenyezi-Mungu atanguruma kutoka juu, atatoa sauti yake kutoka makao yake matakatifu; atanguruma kwa nguvu dhidi ya watu wake, na kupaza sauti kama wenye kusindika zabibu, dhidi ya wakazi wote wa dunia.
31 Vishindo hivyo vitasikika hadi mwisho wa dunia, maana Mwenyezi-Mungu ana mashtaka dhidi ya mataifa; anawahukumu wanadamu wote, na waovu atawaua kwa upanga! Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
32 Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema: “Tazama, maafa yatalikumba taifa moja baada ya lingine, na tufani itazuka kutoka miisho ya dunia.”
33 Siku hiyo, watakaouawa na Mwenyezi-Mungu watatapakaa kutoka upande mmoja wa dunia hadi mwingine. Hawataombolezewa, hawatakusanywa wala kuzikwa; watabaki kuwa mavi juu ya ardhi.
34 Ombolezeni enyi wachungaji; lieni na kugaagaa majivuni enyi wakuu wa kundi; siku za kuchinjwa kwenu na kutawanywa zimefika; mtauawa kama kondoo madume waliochaguliwa.
35 Wachungaji hawatakuwa na pa kukimbilia, wala wakuu wa kundi hawataweza kutoroka.
36 Sikilizeni kilio cha wachungaji na mayowe ya wakuu wa kundi! Mwenyezi-Mungu anayaharibu malisho yao,
37 na makundi yaliyokuwa matulivu yameharibiwa kwa sababu ya hasira kali ya Mwenyezi-Mungu.
38 Mwenyezi-Mungu amewaacha watu wake, kama vile simba aachavyo pango lake; nchi yao imekuwa jangwa tupu, kwa sababu ya vita vya wadhalimu, na hasira kali ya Mwenyezi-Mungu.
1 Mwanzoni mwa utawala wa Yehoyakimu mwana wa Yosia, katika nchi ya Yuda, Mwenyezi-Mungu alimwambia Yeremia hivi:
2 “Mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Simama katika ukumbi wa nyumba ya Mwenyezi-Mungu, uwatangazie watu wa miji yote ya Yuda wanaofika kuabudu katika nyumba ya Mungu, mambo yote niliyokuamuru uwaambie, bila kuacha hata neno moja.
3 Labda watasikiliza na kuacha njia zao mbaya. Wakifanya hivyo, huenda nikabadili nia yangu kuhusu maafa niliyonuia kuwaletea kwa sababu ya matendo yao maovu.
4 “Utawaambia hivi: Mwenyezi-Mungu asema hivi: Msiponisikiliza na kufuata sheria zangu nilizowawekea,
5 na msipoyajali wanayosema watumishi wangu manabii ambao nimekuwa nikiwatuma kwenu kila mara, ingawa hamkuwajali,
6 basi, nitaiharibu nyumba hii kama nilivyoharibu ile ya Shilo, na nitaufanya mji huu kuwa laana kwa mataifa yote ya dunia.”
7 Makuhani, manabii na watu wote walimsikia Yeremia akisema maneno haya katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu.
8 Basi Yeremia alipomaliza kutangaza mambo yote ambayo Mwenyezi-Mungu alimwamuru ayatangaze kwa watu wote, makuhani, manabii na watu wote walimkamata na kusema, “Utakufa!
9 Kwa nini umetabiri kwa jina la Mwenyezi-Mungu na kusema, nyumba hii itakuwa kama Shilo na mji huu utakuwa ukiwa, bila wakazi?” Watu wote wakamzingira Yeremia katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu.
10 Basi, wakuu wa Yuda waliposikia mambo hayo, walipanda kutoka katika nyumba ya mfalme, wakaenda katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu, wakaketi penye Lango Jipya.
11 Hapo makuhani na manabii wakawaambia wakuu na watu wote: “Mtu huyu anastahili hukumu ya kifo kwa maana amehubiri dhidi ya mji huu, kama nyinyi wenyewe mlivyosikia kwa masikio yenu.”
12 Ndipo Yeremia akawaambia wakuu na watu wote: “Mwenyezi-Mungu alinituma niwatabirie mambo yote mliyosikia nikiyasema dhidi ya hekalu hili na mji huu.
13 Sasa basi, rekebisheni mienendo yenu na matendo yenu na kutii sauti ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu. Mkifanya hivyo, Mwenyezi-Mungu atabadili nia yake na kuacha kuwaletea maafa aliyotamka dhidi yenu.
14 Lakini mimi, tazama nimo mikononi mwenu. Nitendeeni kama mnavyoona vema na haki.
15 Ila jueni kwa hakika kwamba mkiniua, mtakuwa mmejiletea laana nyinyi wenyewe kwa kumwaga damu isiyo na hatia, na kuuletea laana mji huu na wakazi wake. Maana, ni kweli kwamba Mwenyezi-Mungu alinituma niwaambieni mambo hayo muyasikie.”
16 Hapo wakuu na watu wote wakawaambia makuhani na manabii: “Mtu huyu hastahili hukumu ya kifo, kwa kuwa amesema nasi kwa jina la Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu.”
17 Basi, baadhi ya wazee wa nchi wakasimama na kuwaambia watu waliokuwa wamekusanyika:
18 “Wakati Hezekia alipokuwa mfalme wa Yuda, Mika wa Moreshethi, aliwatangazia watu wote kwamba Mwenyezi-Mungu wa majeshi alisema hivi: ‘Mji wa Siyoni utalimwa kama shamba mji wa Yerusalemu utakuwa magofu, nao mlima wa hekalu utakuwa msitu.’
19 Je, Hezekia, mfalme wa Yuda, na watu wote wa Yuda walimuua Mika? La! Badala yake Hezekia alimwogopa Mwenyezi-Mungu na kuomba fadhili zake. Naye Mwenyezi-Mungu akabadili nia yake ya kuwaletea balaa. Lakini sisi tuko mbioni kujiletea wenyewe maafa.”
20 (Kulikuwa na mtu mwingine pia aliyetabiri kwa jina la Mwenyezi-Mungu. Mtu huyo alikuwa anaitwa Uria mwana wa Shemaya, kutoka mji wa Kiriath-yearimu. Yeye alitabiri dhidi ya mji huu na dhidi ya nchi hii kama alivyofanya Yeremia.
21 Naye mfalme Yehoyakimu pamoja na mashujaa wake na wakuu wote waliposikia mambo aliyosema Uria, mfalme alitaka kumuua. Lakini Uria alipopata habari, alishikwa na hofu, akatoroka na kwenda Misri.
22 Mfalme Yehoyakimu alimpeleka Elnathani mwana wa Akbori, pamoja na watu kadhaa huko Misri.
23 Wao walimrudisha Uria kutoka Misri, wakampeleka kwa mfalme Yehoyakimu. Mfalme akamuua kwa upanga na maiti yake ikazikwa kwenye makaburi ya watu wa kawaida.)
24 Lakini Yeremia alikuwa akilindwa na Ahikamu mwana wa Shefani, ili asitiwe mikononi mwa watu na kuuawa.
1 Mwanzoni mwa utawala wa Sedekia mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, neno hili lilimjia Yeremia kutoka kwa Mwenyezi-Mungu.
2 Mwenyezi-Mungu aliniambia hivi: “Yeremia, jitengenezee kamba na nira ujivike shingoni.
3 Kisha, peleka ujumbe kwa mfalme wa Edomu, mfalme wa Moabu, mfalme wa Amoni, mfalme wa Tiro na mfalme wa Sidoni, kupitia kwa wajumbe waliokuja Yerusalemu kumwona Sedekia mfalme wa Yuda.
4 Waamuru wajumbe hao wawaambie wakuu wao kwamba mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, nasema hivi:
5 Mimi ndimi niliyeiumba dunia, watu na wanyama waliomo kwa uwezo wangu na kwa mkono wangu wenye nguvu, nami humpa mtu yeyote kama nionavyo mimi kuwa sawa.
6 Sasa nimemkabidhi mtumishi wangu Nebukadneza mfalme wa Babuloni, nchi hizi zote; kadhalika nimempa wanyama wa porini wamtumikie.
7 Mataifa yote yatamtumikia yeye, mwanawe na mjukuu wake, mpaka wakati nchi yake itakapoanguka. Kisha mataifa mengi na wafalme wengi watamfanya kuwa mtumwa wao.
8 “Lakini kama taifa lolote au utawala wowote hautajiweka chini ya mamlaka ya Nebukadneza, mfalme wa Babuloni, basi, nitaliadhibu taifa hilo kwa vita, njaa na maradhi mpaka niliangamize kabisa kwa mkono wake. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
9 Basi, nyinyi msiwasikilize manabii wenu, wapiga ramli wenu, watabiri wenu, waaguzi wenu au wachawi wenu, wanaowaambia: ‘Msimtii mfalme wa Babuloni.’
10 Hao wanawatabirieni uongo na hii itasababisha mhamishwe mbali na nchi yenu. Nitawafukuzia mbali, nanyi mtaangamia.
11 Lakini watu wa taifa lolote litakalomtii mfalme wa Babuloni na kumtumikia, nitawaacha wakae nchini mwao, wailime ardhi yao na kuishi humo. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
12 Mimi Yeremia nilikuwa nimemwambia Sedekia mfalme wa Yuda, mambo hayohayo. Nilimwambia: “Mtii mfalme wa Babuloni. Mtumikie yeye na watu wake, nawe utaishi.
13 Ya nini wewe na watu wako kufa kwa vita, njaa na maradhi? Maana, hivyo ndivyo alivyosema Mwenyezi-Mungu kuhusu yatakayolipata taifa lolote litakaloacha kumtumikia mfalme wa Babuloni.
14 Usisikilize maneno ya manabii wanaokuambia: ‘Usimtumikie mfalme wa Babuloni’, kwa sababu wanakutabiria uongo.
15 Mwenyezi-Mungu anasema: ‘Mimi sikuwatuma manabii hao, bali wanatabiri uongo kwa jina langu. Kwa hiyo nitawafukuzia mbali, nanyi mtaangamia, pamoja na hao manabii wanaowatabirieni uongo.’”
16 Kisha, niliwaambia makuhani na watu wote: Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Msiwasikilize manabii wenu wanaowatabiria wakisema: ‘Tazama, vyombo vya nyumba ya Mwenyezi-Mungu vitarudishwa hivi karibuni kutoka Babuloni’, kwa maana wanawadanganyeni.
17 Msiwasikilize. Mtumikieni mfalme wa Babuloni, nanyi mtaishi. Ya nini mji huu ufanywe kuwa magofu?
18 Ikiwa wao ni manabii, na kama wana neno la Mwenyezi-Mungu, basi, na wamsihi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, ili vyombo vilivyobaki katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu na katika nyumba ya mfalme wa Yuda, na katika mji wa Yerusalemu, visichukuliwe na kupelekwa Babuloni.
19 Kwa maana Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi juu ya nguzo, sinia za shaba, vinara na vyombo vingine vilivyoachwa katika mji huu
20 ambavyo Nebukadneza, mfalme wa Babuloni, hakuvichukua wakati alipowachukua Yekonia mwana wa Yehoyakimu, mfalme wa Yuda na waheshimiwa wote wa Yuda na Yerusalemu kutoka Yerusalemu na kuwapeleka uhamishoni.
21 “Sikilizeni mambo ambayo mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, ninasema juu ya vile vyombo vilivyoachwa katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu, katika nyumba ya mfalme wa Yuda na katika mji wa Yerusalemu.
22 Vyombo hivyo vitachukuliwa Babuloni na vitabaki huko mpaka siku nitakapovishughulikia. Hapo ndipo nitakapovirudisha na kuviweka tena mahali hapa. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
1 Mwaka uleule, mnamo mwezi wa tano wa mwaka wa nne wa utawala wa Sedekia mfalme wa Yuda, Hanania mwana wa Azuri, nabii kutoka mji wa Gibeoni, alisema nami katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu. Alisema nami mbele ya makuhani na watu wote, akaniambia,
2 “Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi: Nimeivunja nira ya mfalme wa Babuloni.
3 Mnamo miaka miwili nitavirudisha hapa vyombo vyote vya nyumba ya Mwenyezi-Mungu ambavyo Nebukadneza, mfalme wa Babuloni alivichukua na kuvipeleka Babuloni.
4 Pia nitamrudisha Yekonia mwana wa Yehoyakimu mfalme wa Yuda, pamoja na watu wote wa Yuda waliohamishiwa Babuloni. Naam, nitaivunja nira ya mfalme wa Babuloni. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
5 Kisha, nabii Yeremia akamwambia nabii Hanania mbele ya makuhani na watu wote waliokuwa wamesimama katika hekalu la Mwenyezi-Mungu:
6 “Na iwe hivyo! Mwenyezi-Mungu na afanye hivyo. Mwenyezi-Mungu na ayatimize maneno uliyotabiri, avirudishe hapa vyombo vya nyumba ya Mwenyezi-Mungu kutoka Babuloni pamoja na watu wote waliohamishiwa huko.
7 Lakini sikiliza neno ninalokuambia wewe na watu wote.
8 Manabii waliotutangulia mimi na wewe, tangu zamani za kale, walitabiri kwamba vita, njaa na maradhi vitazikumba nchi nyingi na tawala kubwa.
9 Lakini nabii atabiriye amani, hutambuliwa tu kama nabii aliyetumwa na Mwenyezi-Mungu, ikiwa mambo aliyotabiri hutokea kweli.”
10 Ndipo nabii Hanania akaichukua ile nira shingoni mwa nabii Yeremia, akaivunja.
11 Naye Hanania akasema hivi mbele ya watu wote, “Mwenyezi-Mungu asema: Hivi ndivyo nitakavyovunja nira ambayo mfalme Nebukadneza ameyavisha mataifa yote; nitafanya hivyo mnamo miaka miwili ijayo.” Kisha nabii Yeremia akaenda zake.
12 Baada ya nabii Hanania kuvunja nira kutoka shingoni mwa nabii Yeremia, neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Yeremia:
13 “Nenda ukamwambie Hanania kwamba mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Wewe umevunja nira ya mti, lakini mimi nitatengeneza nyingine ya chuma.
14 Mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, nasema kuwa nimeweka nira ya chuma ya utumwa shingoni mwa mataifa haya yote, nayo yatamtumikia Nebukadneza, mfalme wa Babuloni. Nimempa Nebukadneza hata wanyama wa porini wamtumikie.”
15 Basi, nabii Yeremia akamwambia nabii Hanania, “Sikiliza, Hanania, Mwenyezi-Mungu hakukutuma, nawe unawafanya watu hawa waamini uongo.
16 Kwa hiyo Mwenyezi-Mungu asema kwamba atakuondoa duniani. Mwaka huuhuu utakufa, kwa sababu umewaambia watu wamwasi Mwenyezi-Mungu.”
17 Mwaka huohuo, mnamo mwezi wa saba, nabii Hanania akafa.
1 Ifuatayo ni barua ambayo nabii Yeremia aliwapelekea kutoka Yerusalemu wazee na makuhani, manabii na watu ambao Nebukadneza alikuwa amewachukua kutoka Yerusalemu akawapeleka uhamishoni Babuloni.
2 Yeremia aliiandika barua hiyo baada ya mfalme Yekonia na mama mfalme, matowashi, wakuu wa Yuda na Yerusalemu, mafundi na wahunzi kuondoka Yerusalemu.
3 Barua hii ilipelekwa na Elasa mwana wa Shafani, na Gemaria mwana wa Hilkia, ambao Sedekia, mfalme wa Yuda, aliwatuma kwa Nebukadneza mfalme wa Babuloni. Yeremia aliandika hivi:
4 “Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi kuhusu mateka wote aliowaacha wachukuliwe kutoka Yerusalemu hadi Babuloni:
5 ‘Jengeni nyumba mkae. Limeni mashamba, pandeni mbegu na kula mazao yake.
6 Oeni wake, mpate watoto; waozeni wana wenu na binti zenu nao pia wapate watoto. Ongezekeni na wala msipungue.
7 Shughulikieni ustawi wa mji ambamo nimewahamishia. Niombeni kwa ajili ya mji huo, maana katika ustawi wake nyinyi mtastawi.
8 Mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, nasema hivi: Msikubali kudanganywa na manabii wenu na waaguzi waliomo miongoni mwenu, wala msisikilize ndoto wanazoota.
9 Maana wanawatabiria uongo kwa kutumia jina langu. Mimi sikuwatuma. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.’
10 “Mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Baada ya miaka sabini huko Babuloni, baada ya muda huo, nitawajia na kuitimiza ahadi yangu ya kuwarudisha mahali hapa.
11 Maana, mimi Mwenyezi-Mungu ninajua mambo niliyowapangia. Nimewapangieni mema na si mabaya, ili mpate kuwa na tumaini la baadaye.
12 Hapo ndipo mtakaponiita na kuniomba, nami nitawasikiliza.
13 Mtanitafuta na kunipata. Mtakaponitafuta kwa moyo wote
14 mtanipata. Nami nitawarudishieni fanaka zenu na kuwakusanya kutoka mataifa yote na mahali pote nilipowafukuzia. Nitawarudisheni mahali ambapo niliwatoa, nikawapeleka uhamishoni. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
15 “Nyinyi mnawasadiki manabii ambao mwasema kwamba Mwenyezi-Mungu amewaleteeni huko Babuloni.
16 Sikilizeni nisemavyo mimi Mwenyezi-Mungu kuhusu mfalme anayekalia kiti cha enzi cha Daudi, na kuhusu watu wote wanaokaa katika mji huu, na ndugu zenu ambao hawakuondoka pamoja nanyi kwenda uhamishoni.
17 Mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi nasema hivi: Tazama, ninawapelekea upanga, njaa na maradhi mabaya; nitawafanya kuwa kama tini mbaya sana, hata haziwezi kuliwa.
18 Nitawaandama kwa upanga, njaa na maradhi mabaya. Nitawafanya kuwa kitu cha kuchukiza kwa tawala zote za dunia, naam, kitu cha laana, kioja, dharau na kitu cha kupuuzwa katika mataifa yote nilikowafukuzia.
19 Nitafanya hivyo kwa sababu hamkusikiliza maneno yangu niliyowaambia kila mara kwa njia ya watumishi wangu, manabii, nanyi mkakataa kusikiliza. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
20 Enyi nyote niliowatoa kutoka Yerusalemu, nikawapeleka uhamishoni Babuloni, sikilizeni neno langu mimi Mwenyezi-Mungu.”
21 Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli asema hivi juu ya Ahabu mwana wa Kolaya, na juu ya Sedekia mwana wa Maaseya, ambao wanawatabirieni uongo kwa jina lake: “Nitawatia mikononi mwa Nebukadneza, mfalme wa Babuloni, naye atawaua mkiona kwa macho yenu wenyewe.
22 Kwa sababu jambo hilo litakalowapata, watu wote waliohamishiwa Babuloni kutoka Yerusalemu watatumia msemo huu wa kulaania: Mwenyezi-Mungu akufanye kama Sedekia na Ahabu, ambao mfalme wa Babuloni aliwachoma motoni.
23 Kisa ni kwamba walitenda mambo ya aibu katika Israeli. Walizini na wake za jirani zao, na kusema maneno ya uongo kwa jina langu, jambo ambalo mimi sikuwaamuru walifanye. Mimi nayajua hayo; nimeyashuhudia. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
24 Mwenyezi-Mungu aliniagiza nimwambie hivi Shemaya wa Nehelamu:
25 “Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi: Umepeleka barua kwa jina lako kwa wakazi wote wa Yerusalemu na kwa kuhani Sefania mwana wa Maaseya na kwa makuhani wengine wote. Katika barua hiyo, ulimwambia Sefania hivi:
26 ‘Mwenyezi-Mungu amekufanya wewe Sefania kuwa kuhani badala ya kuhani Yehoyada, uwe mkuu wa nyumba ya Mwenyezi-Mungu. Ni wajibu wako kumtia gerezani na kumfunga minyororo mwendawazimu yeyote anayetabiri.
27 Kwa nini basi, hukumkemea Yeremia kutoka Anathothi anayekutabiria?
28 Maana yeye alituma taarifa huko Babuloni kwamba uhamisho wenu utakuwa wa muda mrefu, na kusema mjenge nyumba, mkae; mlime mashamba, mpande mbegu na kula mazao yake!’”
29 Kuhani Sefania aliisoma barua hiyo mbele ya nabii Yeremia.
30 Ndipo Mwenyezi-Mungu akamwambia Yeremia:
31 “Wapelekee watu wote walioko uhamishoni ujumbe huu: Mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi juu ya Shemaya wa Nehelamu: Shemaya amewatabirieni, hali mimi sikumtuma, akawafanya muuamini uongo.
32 Kwa hiyo mimi Mwenyezi-Mungu nasema kuwa nitamwadhibu Shemaya wa Nehelamu pamoja na wazawa wake. Hakuna hata mmoja wa watu wake atakayebaki hai kuona mema nitakayowafanyia watu wangu, kwa sababu amewachochea watu waniasi mimi Mwenyezi-Mungu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
1 Neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Mwenyezi-Mungu:
2 “Mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, nasema hivi: Yaandike katika kitabu maneno yote niliyokuambia.
3 Maana siku zaja ambapo nitawarudishia fanaka zao watu wangu wa Israeli na Yuda na kuwarudisha katika nchi niliyowapa wazee wao, nao wataimiliki. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
4 Haya ndiyo mambo aliyosema Mwenyezi-Mungu kuhusu watu wa Israeli na Yuda:
5 “Mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Kumesikika kilio cha hofu sauti ya kutisha wala si ya amani.
6 Jiulizeni sasa na kufahamu: Je, mwanamume aweza kujifungua mtoto? Mbona basi, namwona kila mwanamume amejishika kiunoni kama mwanamke mwenye utungu na nyuso zao zimegeuka rangi?
7 Kweli, siku hiyo ni kubwa, hakuna nyingine kama hiyo; ni siku ya huzuni kwa watu wa Yakobo; hata hivyo, wataokolewa humo.
8 “Siku hiyo itakapofika, nasema mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, nitaivunja nira iliyo shingoni mwao na kukata minyororo yao.
9 Nao hawatakuwa tena watumwa wa wageni, bali watanitumikia mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wao, na mfalme wa ukoo wa Daudi ambaye nitawateulia.
10 “Mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Usiogope ee Yakobo mtumishi wangu, wala usifadhaike, ee Israeli; maana nitakuokoa huko mbali uliko, na wazawa wako kutoka uhamishoni. Utarudi na kuishi kwa amani, wala hakuna mtu atakayekuogopesha.
11 Maana mimi niko pamoja nawe, kukuokoa. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema. Nitayaangamiza kabisa mataifa yote, ambayo nilikutawanya kati yao; lakini wewe sitakuangamiza kabisa. Nitakuadhibu kadiri unavyostahili wala sitakuacha uende bila kukuadhibu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
12 “Mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Majeraha yako hayaponyeki, vidonda vyako havitibiki.
13 Hakuna atakayeshughulikia kisa chako, jeraha lako halina dawa, wewe hutaponyeshwa.
14 Wapenzi wako wote wamekusahau; hawajali chochote juu yako, nimekupiga pigo la adui; umeadhibiwa bila huruma, kwa kuwa kosa lako ni kubwa, dhambi zako ni nyingi mno.
15 Mbona unalia juu ya jeraha lako? Maumivu yako hayaponyeki. Nimekutendea hayo yote, kwa sababu kosa lako ni kubwa, dhambi zako ni nyingi mno.
16 Lakini wote wanaokuangamiza, wataangamizwa, na maadui zako wote watachukuliwa uhamishoni; wanaokuteka nyara, watatekwa nyara, wanaokuwinda nitawawinda.
17 “Nitakurudishia afya yako, na madonda yako nitayaponya, japo wamekuita ‘Aliyetupwa’, ‘Mji Siyoni usio na wa kuutunza!’”
18 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Nitazirudisha tena fanaka za maskani ya Yakobo, na kuyaonea huruma makao yake; mji utajengwa upya juu ya magofu yake, na ikulu ya mfalme itasimama pale ilipokuwa.
19 Humo zitatoka nyimbo za shukrani na sauti za wale wanaosherehekea. Nitawaongeza na wala hawatakuwa wachache; nitawafanya waheshimiwe wala hawatadharauliwa.
20 Watoto wao watakuwa kama walivyokuwa zamani, jumuiya yao itaimarika mbele yangu, nami nitawaadhibu wote wanaowakandamiza.
21 Kiongozi wao atakuwa mmoja wao, mtawala wao atatokea miongoni mwao. Nitamleta karibu naye atanikaribia; maana, nani anayethubutu kunikaribia kwa nguvu zake? Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
22 Nanyi mtakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wenu.”
23 Tazama, dhoruba kali kutoka kwa Mwenyezi-Mungu! Ghadhabu imezuka, kimbunga cha tufani kitamlipukia mtu mwovu kichwani.
24 Hasira ya Mwenyezi-Mungu haitarudi nyuma, mpaka atakapotekeleza na kukamilisha matakwa ya moyo wake. Siku zijazo mtayaelewa vema mambo hayo.
1 Mwenyezi-Mungu asema: “Wakati utakuja ambapo nitakuwa Mungu wa jamaa zote za Israeli nao watakuwa watu wangu.
2 Mimi Mwenyezi-Mungu nasema: Watu walionusurika kuuawa niliwaneemesha jangwani. Wakati Israeli alipotafuta kupumzika,
3 mimi Mwenyezi-Mungu nilimtokea kwa mbali. Nami nimekupenda kwa mapendo ya daima, kwa hiyo nimeendelea kuwa mwaminifu kwako.
4 Nitakujenga upya nawe utajengeka, ewe Israeli uliye mzuri! Utazichukua tena ngoma zako ucheze kwa furaha na shangwe.
5 Utapanda tena mizabibu juu ya milima ya Samaria; wakulima watapanda mbegu na kuyafurahia mazao yake!
6 Maana siku yaja ambapo mlinzi atapiga mbiu katika vilima vya Efraimu: ‘Amkeni, twende juu mpaka Siyoni kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu.’”
7 Maana Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Imbeni kwa furaha kwa ajili ya Yakobo, pigeni vigelegele kwa ajili ya taifa kuu, tangazeni, shangilieni na kusema: ‘Mwenyezi-Mungu na awaokoe watu wake, amewaletea ukombozi waliobaki wa Israeli!’
8 Tazama, nitawaleta kutoka nchi ya kaskazini, nitawakusanya kutoka miisho ya dunia. Wote watakuwapo hapo; hata vipofu na vilema, wanawake waja wazito na wanaojifungua; umati mkubwa sana utarudi hapa.
9 Watarudi wakiwa wanatoa machozi, nitawarudisha nikiwafariji; nitawapitisha kando ya vijito vya maji, katika njia iliyonyoka ambamo hawatajikwaa; maana mimi nimekuwa baba wa Israeli, Efraimu ni mzaliwa wangu wa kwanza.
10 Enyi mataifa, sikilizeni neno langu mimi Mwenyezi-Mungu, litangazeni katika nchi za mbali, semeni: ‘Aliyemtawanya Israeli, atamkusanya, atamtunza kama mchungaji atunzavyo kondoo wake.’
11 Maana mimi Mwenyezi-Mungu nimemkomboa Yakobo, nimemwokoa kutoka kwa wenye nguvu kuliko yeye.
12 Watakuja na kuimba kwa sauti juu ya mlima Siyoni, wataona fahari juu ya wema wangu mimi Mwenyezi-Mungu, kwa nafaka, divai na mafuta niwapavyo, kwa kondoo na ng'ombe kadhalika; maisha yao yatakuwa kama bustani iliyotiliwa maji, wala hawatadhoofika tena.
13 Ndipo wasichana wao watafurahi na kucheza, vijana na wazee watashangilia kwa furaha. Nitageuza maombolezo yao kuwa furaha, nitawafariji na kuwapa furaha badala ya huzuni.
14 Nitawashibisha makuhani kwa vinono, nitawaridhisha watu wangu kwa wema wangu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
15 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Sauti imesikika mjini Rama, maombolezo na kilio cha uchungu. Raheli anawalilia watoto wake, wala hataki kufarijiwa kwa ajili yao, maana wote hawako tena.
16 Sasa, acha kulia, futa machozi yako, kwani utapata tuzo kwa kazi yako, mimi Mwenyezi-Mungu nimesema; watoto wenu watarudi kutoka nchi ya maadui zenu.
17 Yapo matumaini kwa siku zenu zijazo, mimi Mwenyezi-Mungu nimesema; kwani watoto wenu watarejea nchini mwao.
18 “Nimesikia Efraimu akilalamika: ‘Umenichapa ukanifunza nidhamu, kwani nilikuwa kama ndama asiyezoea nira. Unigeuze nami nitakugeukia, kwani wewe ndiwe Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu.
19 Maana baada ya kukuasi, nilitubu, na baada ya kufunzwa, nilijilaumu, nikaona haya na kuaibika, maana lawama za ujana wangu ziliniandama.’
20 “Efraimu ni mwanangu mpendwa; yeye ni mtoto wangu nimpendaye sana. Ndio maana kila ninapomtisha, bado naendelea kumkumbuka. Moyo wangu wamwelekea kwa wema; hakika nitamhurumia. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
21 “Weka alama katika njia zako, simika vigingi vya kukuongoza, ikumbuke vema ile njia kuu, barabara uliyopita ukienda. Ewe Israeli rudi, rudi nyumbani katika miji yako.
22 Utasitasita mpaka lini ewe binti usiye mwaminifu? Maana, mimi nimefanya kitu kipya duniani: Mwanamke amtafuta mwanamume.”
23 Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi: “Nitakapowafanikisha tena watu wa Israeli, wao watatangaza tena katika nchi ya Yuda na katika miji yake wakisema: ‘Mwenyezi-Mungu akubariki ewe makao adili, akubariki ee mlima mtakatifu!’
24 “Ndipo watu wa Yuda na miji yake yote, wakulima na wachungaji wanaopitapita na makundi yao, watakaa huko pamoja.
25 Waliochoka nitawachangamsha, na walegevu nitawapa nguvu.
26 Ndio maana mtu ataweza kusema: ‘Niliamka nikatambua kwamba usingizi wangu ulinifaa sana.’”
27 Mwenyezi-Mungu asema: “Tazama, siku zaja ambapo nitaijaza nchi ya Israeli na nchi ya Yuda watu na wanyama kama mkulima asiavyo mbegu.
28 Na kadiri nilivyokuwa mwangalifu kuwangoa, kuwabomoa, kuwaangusha, kuwaharibu na kuwatesa, ndivyo nitakavyokuwa mwangalifu kuwapanda na kuwajenga.
29 Siku hizo watu hawatasema tena: ‘Wazee walikula zabibu chungu, na meno ya watoto yakatiwa ganzi.’
30 La! Kila mmoja atakufa kwa sababu ya dhambi zake mwenyewe; ni yule tu atakayekula zabibu mbivu ndiye meno yake yatatiwa ganzi.”
31 Mwenyezi-Mungu asema: “Siku zaja ambapo nitafanya agano jipya na watu wa Israeli na watu wa Yuda.
32 Agano hili halitakuwa kama lile nililofanya na wazee wao nilipowatoa kwa mkono wangu kutoka Misri; agano hilo walilivunja, ingawa mimi nilikuwa Bwana wao. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
33 Baada ya siku hizo, nitafanya agano lifuatalo na Waisraeli: Nitaiweka sheria yangu ndani yao, na kuiandika katika mioyo yao. Mimi nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
34 Wala haitawabidi kufundishana na kusema: ‘Mjue Mwenyezi-Mungu’, kwa sababu wote, wadogo kwa wakubwa, watanijua mimi Mungu. Maana nitawasamehe makosa yao, wala sitazikumbuka tena dhambi zao.”
35 Hivi ndivyo asemavyo Mwenyezi-Mungu, ambaye jina lake ni Mwenyezi-Mungu wa majeshi, aliyepanga jua liangaze mchana, mwezi na nyota vimulike usiku, na aifanyaye bahari iwe na mawimbi:
36 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Mimi hulifanya jua liangaze mchana, mwezi na nyota vimulike usiku; pia mimi huitikisa bahari, nayo hutoa mawimbi. Jina langu mimi ni Mwenyezi-Mungu wa majeshi. Basi, nami nasema: Kadiri ninavyotegemeza mipango hiyo yote yangu kadiri hiyohiyo Israeli watakavyobaki kuwa watu wangu.
37 Kama mbingu zaweza kupimwa, na misingi ya dunia kuchunguzwa, basi, nitawatupilia mbali wazawa wa Israeli, kwa sababu ya mambo yote waliyotenda. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
38 Mwenyezi-Mungu asema: “Siku zaja ambapo mji huu wa Yerusalemu utajengwa upya kwa ajili ya Mwenyezi-Mungu, kutoka mnara wa Hananeli hadi Lango la Pembeni.
39 Nayo kamba ya kupimia itanyoshwa moja kwa moja hadi mlima Garebu, kisha itazungushwa hadi Goa.
40 Bonde lote walimozikwa wafu na kutupiwa majivu, mashamba yote, mpaka kijito cha Kidroni, mpaka pembe ya lango la Farasi kuelekea mashariki, litakuwa eneo takatifu kwa Mwenyezi-Mungu. Hakuna kitakachoharibiwa humo wala kubomolewa tena milele.”
1 Neno la Mwenyezi-Mungu lililomjia Yeremia mnamo mwaka wa kumi wa utawala wa Sedekia, mfalme wa Yuda, ambao ulikuwa mwaka wa kumi na nane wa utawala wa Nebukadneza.
2 Wakati huo, majeshi ya mfalme wa Babuloni yalikuwa yakiuzingira mji wa Yerusalemu, naye nabii Yeremia alikuwa amezuiliwa katika ukumbi wa walinzi uliokuwa ndani ya ikulu ya mfalme wa Yuda.
3 Maana Sedekia, mfalme wa Yuda, alikuwa amemfunga Yeremia akisema, “Kwa nini unatabiri na kusema: ‘Mwenyezi-Mungu asema hivi: Tazama, mimi nautia mji huu mikononi mwa mfalme wa Babuloni, naye atauteka.
4 Sedekia, mfalme wa Yuda, hataepa kutiwa mikononi mwa Wakaldayo; hakika atatekwa na mfalme wa Babuloni, ataonana naye uso kwa uso na kuongea naye ana kwa ana.
5 Sedekia atachukuliwa hadi Babuloni, naye atakaa huko mpaka nitakapomchukulia hatua. Hata kama Sedekia atapigana na Wakaldayo, hatashinda.’”
6 Yeremia akasema, Mwenyezi-Mungu alinena nami akasema:
7 “Hanameli, mwana wa baba yako mdogo Shalumu, atakujia na kusema: ‘Nunua shamba langu lililoko Anathothi, maana wewe ni ndugu yangu kabisa, na unayo haki ya kulikomboa.’”
8 Kisha binamu yangu Hanameli alinijia katika ukumbi wa walinzi kama alivyonifahamisha Mwenyezi-Mungu, akaniambia, “Nunua shamba langu lililoko Anathothi katika nchi ya Benyamini maana wewe una haki ya kulikomboa. Linunue kwa faida yako.” Ndipo nilipotambua kwamba lilikuwa kweli neno la Mwenyezi-Mungu.
9 Basi, nililinunua shamba hilo lililoko Anathothi, kutoka kwa binamu yangu Hanameli, nikamlipa bei yake shekeli kumi na saba za fedha.
10 Nikaitia sahihi hati ya kumiliki, nikaipiga mhuri, nikawaita mashahidi na kuipima ile fedha katika mizani.
11 Kisha, nilichukua ile hati ya kumiliki niliyoipiga mhuri, ambayo ilikuwa na masharti na kanuni, pamoja na nakala nyingine iliyokuwa wazi.
12 Nilimpa hiyo hati ya ununuzi Baruku mwana wa Neria mwana wa Maaseya, mbele ya binamu yangu Hanameli na mashahidi waliokuwa wametia sahihi hati ya ununuzi, na mbele ya Wayahudi wote waliokuwa wameketi katika ukumbi wa walinzi.
13 Mbele ya watu wote hao, nilimpa Baruku maagizo yafuatayo:
14 Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi: “Chukua hati hizi zote mbili, hati hii ya kumiliki shamba iliyotiwa sahihi, na hii nyingine iliyo wazi, uziweke katika chungu ili zipate kuhifadhiwa kwa muda mrefu.”
15 Maana Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi: “Nyumba na mashamba, pamoja na mashamba ya mizabibu katika nchi hii yatanunuliwa tena.”
16 Baada ya kumkabidhi Baruku mwana wa Neria, hati ya kumiliki shamba nilimwomba Mwenyezi-Mungu nikisema:
17 Ee Mwenyezi-Mungu, ni wewe ambaye kwa nguvu zako nyingi na uwezo wako mkuu, umeziumba mbingu na dunia; hakuna kisichowezekana kwako.
18 Wewe unaonesha fadhili zako kwa maelfu ya watu; lakini pia unawaadhibu watu kwa sababu ya dhambi za wazee wao. Wewe ni Mungu mkuu, mwenye nguvu, Mwenyezi-Mungu wa Majeshi ndilo jina lako.
19 Wewe unapanga kwa hekima na unafanya maajabu; njia za watu wote ziko wazi mbele yako, unamlipa kila mmoja kadiri ya njia zake na matendo yake.
20 Katika nchi ya Misri ulifanya maajabu, ukatenda miujiza, na unaendelea kufanya hivyo mpaka leo miongoni mwa Waisraeli na katika mataifa mengine pia, jambo ambalo limekufanya ujulikane kila mahali.
21 Kwa maajabu na miujiza uliyowatisha nayo Wamisri, uliwatoa watu wako Misri kwa nguvu zako nyingi na uwezo wako mkuu.
22 Uliwapa nchi hii ambayo uliahidi kuwapa wazee wao, nchi inayotiririka maziwa na asali.
23 Nao walifika, wakaitwa na kuimiliki. Lakini wao hawakukusikiliza, wala hawakufuata sheria zako. Hawakutenda mambo uliyoamuru. Ndiyo maana utawafanya wapatwe na balaa hii.
24 Tazama, Wakaldayo wamechimba mahandaki kuuzunguka mji; wameuzingira ili wapate kuuteka; wanaushambulia. Vita, njaa na maradhi vitaufanya mji utekwe na watu hao. Kweli mambo uliyotabiri yametokea. Unaona mwenyewe.
25 Lakini, ee Mwenyezi-Mungu, wewe ndiwe uliyeniambia: “Nunua shamba kwa fedha na kuweka mashahidi,” ingawa mji wenyewe umetekwa na Wakaldayo.
26 Ndipo Mwenyezi-Mungu akaniambia,
27 “Tazama, mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wa watu wote. Hakuna lolote linaloweza kunishinda.
28 Kwa hiyo, mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Ninautoa mji huu kwa Wakaldayo na kwa Nebukadneza mfalme wa Babuloni, naye atauteka.
29 Wakaldayo wanaoushambulia mji huu wataingia na kuuchoma moto; watauteketeza pamoja na nyumba ambazo juu ya paa zake ubani ulifukiziwa mungu Baali na tambiko za divai zilimiminiwa miungu mingine, ili kunichokoza.
30 Maana Waisraeli na watu wa Yuda hawakufanya chochote mbele yangu isipokuwa uovu tangu ujana wao; watu wa Israeli hawakufanya chochote isipokuwa kunikasirisha kwa matendo yao. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
31 Mji huu umechochea hasira yangu na kuniudhi tangu siku ulipojengwa mpaka leo hii. Kwa hiyo, nitautoa kabisa mbele yangu,
32 kwa sababu ya uovu wote waliotenda watu wa Israeli na watu wa Yuda, pamoja na wafalme na viongozi wao, makuhani na manabii wao, na wakazi wa Yerusalemu.
33 Wao walinipa kisogo badala ya kunigeuzia nyuso zao; ingawa nimewafundisha tena na tena, wao hawakusikiliza na kuyapokea mafundisho yangu.
34 Waliweka sanamu za miungu yao ya kuchukiza katika nyumba hii inayojulikana kwa jina langu, wakaitia unajisi.
35 Walimjengea mungu Baali madhabahu katika bonde la Mwana wa Hinomu, ili wamtolee mungu Moleki wavulana wao na binti zao, ingawa sikuwaamuru wala sikufikiria kwamba wangefanya hivyo, wakawafanya watu wa Yuda watende dhambi.”
36 Sasa basi, Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, asema hivi: “Yeremia, watu hawa wanasema kwamba, kwa vita, njaa na maradhi, mji huu utatiwa mikononi mwa mfalme wa Babuloni. Lakini nasema:
37 Nitawakusanya watu kutoka nchi zote ambako kwa hasira na ghadhabu na chuki yangu kubwa, niliwatawanya. Nitawarudisha tena mahali hapa, na kuwafanya wakae salama.
38 Nao watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao.
39 Nitawapa moyo mmoja na nia moja, wapate kunicha mimi daima, kwa faida yao wenyewe na kwa faida ya watoto wao watakaofuata.
40 Nitafanya nao agano la milele, kwamba sitaacha kamwe kuwatendea mema; nitaweka mioyoni mwao uchaji wangu ili wasiniache tena.
41 Nitafurahi kuwatendea mema; nitawasimika daima katika nchi hii na kuwatendea kwa uaminifu.
42 “Kama nilivyowaletea maafa watu hawa, ndivyo nitakavyowaletea mema niliyowaahidi.
43 Mashamba yatanunuliwa katika nchi hii ambayo unasema imekuwa ukiwa bila watu wala wanyama, na kwamba imetolewa kwa Wakaldayo.
44 Watu watanunua mashamba kwa fedha, watazitilia sahihi hati zake za kuyamiliki, watazipiga mhuri, na kuweka mashahidi katika nchi ya Benyamini, kandokando ya Yerusalemu, katika miji ya Yuda, katika miji ya nchi ya milima, katika miji ya Shefela, na katika miji ya jangwa la Negebu. Maana nitawastawisha tena. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
1 Neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Yeremia mara nyingine, wakati alipokuwa bado amefungwa katika ukumbi wa walinzi:
2 Mwenyezi-Mungu aliyeiumba dunia, Mwenyezi-Mungu aliyeifanya na kuiimarisha dunia, ambaye jina lake ni Mwenyezi-Mungu, aliniambia,
3 “Niite, nami nitakujibu na kukuambia mambo makubwa yaliyofichika ambayo hujapata kuyajua.
4 Maana, mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, nasema kwamba nyumba za mji wa Yerusalemu na nyumba za wafalme wa Yuda zitabomolewa kwa sababu ya kuzingirwa na kwa sababu ya mashambulizi.
5 Watu watajaribu kuwakabili Wakaldayo lakini hiyo itakuwa bure, maana mahandaki yatajaa maiti za watu ambao nitawaua kwa hasira na ghadhabu yangu. Kwa vile wamefanya uovu huo wote, mimi nitauacha mji huu.
6 “Hata hivyo, mimi nitauponya mji huu na kuwapa watu wake afya; nitawajalia ustawi mwingi na usalama.
7 Nitawastawisha tena watu wa Yuda na watu wa Israeli; nitawaimarisha kama walivyokuwa hapo awali.
8 Nitawatakasa dhambi zao zote na kuwasamehe uovu wao na uasi walionitendea.
9 Nao mji huu utakuwa sababu ya furaha kwangu, mji wa sifa na fahari mbele ya mataifa yote duniani ambayo yatasikia juu ya mema yote ninayowafanyia. Mataifa yataogopa na kutetemeka kwa sababu ya mema na fanaka nitakazouletea mji huu wa Yerusalemu.”
10 Mwenyezi-Mungu asema: “Katika mji huu ambao mnasema umekuwa ukiwa bila watu wala wanyama, naam, katika miji ya Yuda na katika barabara za Yerusalemu ambazo ni tupu, bila watu wala wanyama, humo kutasikika tena sauti za vicheko, sauti za furaha,
11 sauti za harusi na za furaha, sauti za waimbaji wakati wakileta tambiko za shukrani katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu: ‘Mshukuruni Mwenyezi-Mungu wa majeshi kwa kuwa Mwenyezi-Mungu ni mwema, kwa maana fadhili zake zadumu milele.’ Nitairudishia nchi hii fanaka yake ya awali. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
12 Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi: “Mahali hapa ambapo ni jangwa bila watu wala wanyama, na katika miji yake yote, patakuwa na malisho ambayo wachungaji watalisha makundi yao ya kondoo.
13 Katika miji ya nchi yenye milima, katika miji ya Shefela na katika miji ya jangwa la Negebu, katika nchi ya Benyamini, kandokando ya mji wa Yerusalemu na katika miji ya Yuda, watu watahesabu tena kondoo wao. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
14 Mwenyezi-Mungu asema: “Siku zaja ambapo nitatimiza ahadi yangu niliyofanya na watu wa Israeli na watu wa Yuda.
15 Katika siku hizo, naam, wakati huo, nitachipusha chipukizi mwadilifu wa uzao wa Daudi. Chipukizi huyo atatekeleza haki na uadilifu katika nchi.
16 Wakati huo nchi ya Yuda itaokolewa na mji wa Yerusalemu utakuwa salama. Na mji huo utaitwa ‘Mwenyezi-Mungu ni Ukombozi Wetu’.
17 Maana mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Hapatakosekana kamwe mzawa wa Daudi atakayetawala Israeli.
18 Kadhalika nao makuhani wa ukoo wa Lawi watakuwapo daima kunihudumia wakinitolea sadaka za kuteketezwa na sadaka za nafaka na kunitolea tambiko milele.”
19 Neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Yeremia:
20 “Kama vile hamwezi kutangua agano langu nililoweka kuhusu usiku na mchana hivyo kwamba usiku na mchana visiweko kama nilivyopanga,
21 vivyo hivyo hamwezi kutangua agano langu nililofanya na mtumishi wangu Daudi. Nilifanya agano na Daudi kwamba daima atakuwa na mzawa wa kutawala mahali pake; vilevile kutakuwako daima makuhani wa ukoo wa Lawi watakaonitumikia.
22 Kama vile nyota angani na mchanga wa pwani visivyohesabika, ndivyo nitakavyoongeza idadi ya wazawa wa mtumishi wangu Daudi na idadi ya makuhani wa ukoo wa Lawi.”
23 Neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Yeremia:
24 “Je, hujasikia wasemayo watu hawa, kwamba mimi Mwenyezi-Mungu nimewatupilia mbali watu wa Israeli na watu wa Yuda, jamaa mbili nilizoziteua? Wamewadharau watu wangu, hata kuwaona kwamba wao si taifa.
25 Lakini mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Mimi niliweka agano kuhusu mchana na usiku na kuweka sheria za mbingu na dunia.
26 Basi, ndivyo ilivyo pia: Sitawatupa wazawa wa Yakobo na Daudi, mtumishi wangu; nitamteua mmoja wa wazawa wake atawale wazawa wa Abrahamu, Isaka na Yakobo. Kwa maana nitawarudishia fanaka yao na kuwahurumia.”
1 Neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Yeremia wakati Nebukadneza, mfalme wa Babuloni, pamoja na jeshi lake lote na falme zote za dunia zilizokuwa chini yake, kadhalika na watu wote walipokuwa wakiushambulia mji wa Yerusalemu na miji mingine yote ya kandokando yake:
2 “Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli asema hivi: Nenda ukaongee na Sedekia, mfalme wa Yuda. Mwambie kwamba mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Nimeutia mji huu mikononi mwa mfalme wa Babuloni, naye atauteketeza kwa moto.
3 Nawe hutatoroka mikononi mwake, bali kwa hakika utatekwa na kupelekwa kwake; utaonana na mfalme wa Babuloni macho kwa macho, na kuongea naye ana kwa ana; kisha, utakwenda Babuloni.
4 Lakini, ewe Sedekia, mfalme wa Yuda, mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi juu yako: Wewe hutauawa kwa upanga vitani.
5 Utakufa kwa amani. Na, kama vile watu walivyochoma ubani walipowazika wazee wako waliokuwa wafalme, ndivyo watakavyokuchomea ubani na kuomboleza wakisema, ‘Maskini! Mfalme wetu amefariki!’ Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
6 Kisha, nabii Yeremia akamweleza Sedekia, mfalme wa Yuda, maneno hayo yote huko Yerusalemu,
7 wakati jeshi la mfalme wa Babuloni lilipokuwa linaushambulia mji wa Yerusalemu na pia miji ya Lakishi na Azeka, ambayo ilikuwa miji pekee iliyosalia yenye ngome.
8 Hili ndilo neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Mwenyezi-Mungu baada ya mfalme Sedekia kufanya agano na watu wote wa Yerusalemu kuwaachia huru
9 watumwa wao wa Kiebrania wa kiume na wa kike, ili mtu yeyote asimfanye Myahudi mwenzake mtumwa.
10 Viongozi wote na watu wote waliofanya agano hilo walikubaliana wote wawaachie huru watumwa wao wa kiume na wa kike, na mtu yeyote asiwafanye tena kuwa watumwa. Walikubaliana, wakawaacha huru.
11 Lakini baadaye walibadili nia zao, wakawashika tena watumwa hao wa kiume na wa kike ambao walikuwa wamewaacha huru, wakawafanya watumwa.
12 Hapo neno la Mwenyezi-Mungu likamjia Yeremia:
13 “Mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, nasema hivi: Nilifanya agano na wazee wenu nilipowatoa nchini Misri ambako walikuwa watumwa, nikawaambia:
14 ‘Kila mwaka wa saba, kila mmoja wenu atamwacha huru ndugu yake Myahudi aliyeuzwa akawa mtumwa kwa muda wa miaka sita. Mnapaswa kuwaacha huru, wasiwatumikie tena.’ Lakini wazee wenu hawakunisikiliza wala kunitegea sikio.
15 Hivi karibuni nyinyi mlitubu, mkafanya mambo yaliyo sawa mbele yangu, mkawaacha huru Waisraeli wenzenu na kufanya agano mbele yangu katika nyumba yangu.
16 Lakini baadaye mligeuka, mkalitia unajisi jina langu, wakati mlipowachukua tena watumwa walewale wa kiume na wa kike ambao mlikuwa mmewaachia kama walivyotaka, mkawalazimisha kuwa watumwa tena.
17 Kwa hiyo, mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Nyinyi hamkunitii kuhusu kuwapatia uhuru ndugu zenu Waisraeli. Basi, nami pia nitawapatieni uhuru; uhuru wa kuuawa kwa upanga vitani, kuuawa kwa maradhi na kwa njaa. Nitawafanya muwe kioja kwa falme zote duniani.
18 Watu waliovunja agano langu na kukataa kufuata masharti ya agano walilofanya mbele yangu, nitawafanya kama yule ndama waliyemkata sehemu mbili na kupita katikati yake.
19 Watu hao ndio hao maofisa wa Yuda, maofisa wa mji wa Yerusalemu, matowashi, makuhani, pamoja na wananchi wote waliopita katikati ya sehemu mbili za yule ndama.
20 Watatiwa mikononi mwa maadui zao, na mikononi mwa watu wanaotaka kuwaua. Maiti zao zitaliwa na ndege wa angani na wanyama wa porini.
21 Naye Sedekia, mfalme wa Yuda, pamoja na viongozi wake, nitawatia mikononi mwa maadui zao, na mikononi mwa watu wanaotaka kuwaua; yaani mikononi mwa jeshi la mfalme wa Babuloni ambalo limeondoka na kuacha kuwashambulia.
22 Mimi Mwenyezi-Mungu nasema: Nitawaamuru nao wataurudia mji huu. Wataushambulia, watauteka na kuuteketeza kwa moto. Nitaifanya miji ya Yuda kuwa ukiwa bila wakazi.”
1 Neno la Mwenyezi-Mungu lililomjia Yeremia wakati wa utawala wa Yehoyakimu mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda:
2 “Nenda nyumbani kwa Warekabu, ukaongee nao. Kisha, walete katika chumba kimojawapo cha nyumba yangu mimi Mwenyezi-Mungu, uwape divai wanywe.”
3 Basi, nikamchukua Yaazania mwana wa Yeremia, mwana wa Habazinia, na ndugu zake pamoja na wanawe wote na ukoo wote wa Warekabu,
4 nikawaleta kwenye nyumba ya Mwenyezi-Mungu, katika chumba cha wana wa Hanani mwana wa Igdalia, mtu wa Mungu. Chumba hicho kilikuwa karibu na ukumbi wa wakuu, juu ya ukumbi wa Maaseya mwana wa Shalumu, mlinzi wa ukumbi.
5 Kisha nikaleta vikombe na mabakuli yaliyojaa divai mbele ya hao Warekabu, nikawaambia, “Kunyweni divai.”
6 Lakini wao wakajibu, “Sisi hatunywi divai, maana Yonadabu mwana wa Rekabu, mzee wetu, alituamuru hivi: ‘Msinywe divai; msinywe nyinyi wenyewe binafsi wala wana wenu milele.
7 Msijenge nyumba, msilime mashamba, wala msiwe na shamba la mizabibu. Lakini mtaishi katika mahema siku zote za maisha yenu, ili mpate kuishi siku nyingi katika nchi mnamoishi kama wageni.’
8 Sisi tumeitii daima amri hiyo ya mzee wetu Yonadabu mwana wa Rekabu, kuhusu jambo alilotuamuru. Sisi hatunywi kamwe divai; sisi wenyewe hatunywi, wala wake zetu, wala watoto wetu wa kiume au wa kike.
9 Sisi hatujijengei nyumba za kuishi. Hatuna mashamba ya mizabibu wala mashamba ya kulima na kupanda mbegu.
10 Sisi tumeishi katika mahema na kutii mambo yote ambayo Yonadabu, mzee wetu, alituamuru.
11 Lakini Nebukadneza, mfalme wa Babuloni alipofika, kuishambulia nchi hii, tuliamua kuja Yerusalemu ili tuliepe jeshi la Wakaldayo na la Waashuru. Kwa hiyo sasa tunaishi mjini Yerusalemu.”
12 Kisha neno la Mwenyezi-Mungu likamjia Yeremia:
13 “Mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, nasema hivi: Nenda ukawaambie watu wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu hivi: Je, nyinyi hamwezi kupokea mafundisho na kusikia maneno yangu?
14 Ile amri ambayo Yonadabu mwana wa Rekabu, aliwapa wanawe, kwamba wasinywe divai, imefuatwa; nao hawanywi divai mpaka siku hii ya leo, maana wametii amri ya mzee wao. Lakini mimi niliongea nanyi tena na tena, nanyi hamkunisikiliza.
15 Niliwapelekea tena na tena watumishi wangu wote yaani manabii wawaambieni kila mmoja wenu aachane na mwenendo wake mwovu, arekebishe matendo yake na kuacha kuifuata na kuitumikia miungu mingine. Na kwamba mkifanya hivyo mtakaa katika nchi niliyowapa nyinyi na wazee wenu. Lakini nyinyi hamkunitegea sikio wala hamkunisikiliza.
16 Wana wa Yonadabu mwana wa Rekabu, wameshika amri waliyopewa na mzee wao; lakini nyinyi hamkunitii.
17 Kwa hiyo, mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, nasema hivi: Ninawaletea watu wa Yuda na wakazi wote wa Yerusalemu maovu yote niliyotamka dhidi yao, kwa sababu mimi niliongea nao, lakini hawakunisikiliza; niliwaita, lakini hawakuniitikia.”
18 Lakini Yeremia aliwaambia Warekabu hivi: Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi: “Nyinyi Warekabu mmetii amri ya mzee wenu, mkashika maagizo yake yote na kutenda kama alivyowaamuru.
19 Kwa hiyo mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi nasema kwamba Yonadabu mwana wa Rekabu hatakosa hata mara moja mzawa wa kunihudumia daima.”
1 Mnamo mwaka wa nne wa utawala wa Yehoyakimu mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, neno hili la Mwenyezi-Mungu lilimjia Yeremia:
2 “Chukua kitabu uandike humo maneno yote niliyokuambia juu ya Israeli, juu ya Yuda na mataifa yote, tangu siku nilipoanza kuongea nawe, wakati Yosia alipokuwa mfalme mpaka leo.
3 Labda watu wa Yuda watasikia juu ya maovu yote ambayo nimenuia kuwatendea, ili kila mmoja wao auache mwenendo wake mbaya, nami nipate kuwasamehe makosa yao na dhambi yao.”
4 Ndipo Yeremia akamwita Baruku mwana wa Neria. Naye Baruku akaandika katika kitabu maneno yote aliyotamka Yeremia ambayo Mwenyezi-Mungu alikuwa amemwambia.
5 Kisha, Yeremia akampa Baruku maagizo yafuatayo: “Mimi siruhusiwi kwenda katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu.
6 Lakini mnamo siku ya kwanza ya mfungo, wewe utakwenda mbele ya umati wote wa watu, ndani ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu, usome hati ndefu ya maneno ya Mwenyezi-Mungu niliyokuamuru uandike kama nilivyoyasema. Utayasoma maneno hayo pia mbele ya watu wote wa Yuda waliofika kutoka miji yao.
7 Labda maombi yao yatamfikia Mwenyezi-Mungu na kwamba kila mmoja wao ataacha mwenendo wake mwovu kwa maana Mwenyezi-Mungu ametamka adhabu dhidi ya watu hawa kwa hasira na ghadhabu kali.”
8 Basi, Baruku mwana wa Neria, alitimiza yote aliyoamriwa na nabii Yeremia kuhusu kusoma maneno ya Mwenyezi-Mungu ndani ya nyumba yake Mwenyezi-Mungu kutoka katika kitabu hicho.
9 Mnamo mwaka wa tano wa utawala wa Yehoyakimu mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, katika mwezi wa tisa, wakazi wote wa Yerusalemu na watu wote waliofika Yerusalemu kutoka miji ya Yuda, walitangaza siku ya mfungo mbele ya Mwenyezi-Mungu.
10 Basi, Baruku alisoma maneno ya Yeremia kutoka katika kile kitabu mbele ya watu wote, ndani ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu, katika chumba cha Gemaria mwana wa Shafani aliyekuwa katibu. Chumba hicho kilikuwa katika ukumbi wa juu, kwenye lango Jipya la nyumba ya Mwenyezi-Mungu.
11 Mikaia mwana wa Gemaria, mwana wa Shafani, aliposikia maneno yote ya Mwenyezi-Mungu ambayo yalisomwa kutoka kile kitabu,
12 alikwenda ikulu kwa mfalme katika chumba cha katibu walimokuwa wameketi wakuu wote: Katibu Elishama, Delaya mwana wa Shemaya, Elnathani mwana wa Akbori, Gemaria mwana wa Shafani, Sedekia mwana wa Hanania, na wakuu wote.
13 Mikaia aliwaambia maneno yote aliyoyasikia wakati Baruku aliposoma kitabu mbele ya umati wa watu.
14 Kisha, wakuu walimtuma Yehudi mwana wa Nethania, mjukuu wa Shelemia, kitukuu cha Kushi, amwambie Baruku hivi: “Chukua ile hati ya maandishi uliyosoma mbele ya watu uje nayo hapa.” Basi, Baruku mwana wa Neria, akachukua hati mkononi mwake, akawaendea.
15 Nao wakamwambia: “Keti, uisome.” Baruku akawasomea.
16 Waliposikia maneno hayo yote, walitazamana kwa hofu. Wakamwambia Baruku, “Hatuna budi kumweleza mfalme maneno haya yote.”
17 Kisha wakamwuliza Baruku, “Hebu tuambie, umepataje kuandika maneno yote haya? Je, Yeremia alisema, nawe ukayaandika?”
18 Baruku akawajibu: “Yeye alisema, nami nikawa nayaandika kwa wino katika hati hii.”
19 Kisha wakuu hao wakamwambia Baruku, “Wewe nenda ukajifiche pamoja na Yeremia, na pasiwe na mtu yeyote atakayejua mahali mlipo.”
20 Baada ya wakuu kuweka hati ile ndefu katika chumba cha Elishama katibu wa mfalme, walimwendea mfalme ukumbini, wakamjulisha mambo yote.
21 Kisha, mfalme alimtuma Yehudi aende kuleta ile hati. Yehudi aliichukua kutoka chumbani mwa katibu Elishama, akamsomea mfalme na wakuu wote waliokuwa wamesimama karibu na mfalme.
22 Wakati huo ulikuwa mwezi wa tisa, na mfalme alikuwa ndani ya nyumba yake ya majira ya baridi, akiota moto wa makaa.
23 Ikawa, mara baada ya Yehudi kusoma safu tatu au nne hivi za hiyo hati ndefu, mfalme alizikata safu hizo kwa kisu na kuzitupa katika moto wa makaa. Aliendelea kufanya hivyo mpaka hati yote ikateketea.
24 Lakini, ingawa mfalme na watumishi wake wote waliyasikia maneno hayo yote, hawakuogopa wala kuyararua mavazi yao kwa huzuni.
25 Ijapokuwa Elnata, Delaya na Gemaria walimsihi mfalme asiichome hati hiyo, mfalme hakuwasikiliza.
26 Mfalme alimwamuru Yerameeli mwanawe, Seraya mwana wa Azrieli na Shelemia mwana wa Abdeli, wamkamate katibu Baruku na nabii Yeremia. Lakini Mwenyezi-Mungu aliwaficha.
27 Baada ya mfalme kuchoma moto hati ile ya maneno aliyoandika Baruku kwa maagizo ya Yeremia, neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Yeremia:
28 “Chukua hati nyingine ndefu, uandike maneno yote yaliyokuwa katika ile hati ya kwanza ambayo Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, ameichoma moto.
29 Na huyo Yehoyakimu mfalme wa Yuda, wewe utamwambia kuwa mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Yeye ameichoma moto hati hiyo na kuuliza kwa nini Yeremia ameandika kwamba mfalme wa Babuloni atakuja kuiharibu nchi hii na kuwaangamiza watu na wanyama!
30 Basi, mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi juu yake yeye Yehoyakimu mfalme wa Yuda: Yeye hatakuwa na mzawa atakayekalia kiti cha enzi cha Daudi, na maiti yake itatupwa nje kwenye joto mchana na baridi kali usiku.
31 Nami nitamwadhibu yeye na wazawa wake pamoja na watumishi wake kwa sababu ya uovu wao. Nitawaletea wao na wakazi wote wa Yerusalemu pamoja na watu wote wa Yuda maafa yote niliyotamka dhidi yao na ambayo hawakuyajali.”
32 Kisha, Yeremia alichukua hati nyingine ndefu, akampa katibu Baruku mwana wa Neria, ambaye aliandika humo maneno yote aliyoambiwa na Yeremia ambayo yalikuwa katika ile hati ya awali ambayo Yehoyakimu mfalme wa Yuda, aliichoma moto. Maneno mengine ya namna hiyo yaliongezwa.
1 Mfalme Nebukadneza wa Babuloni alimtawaza Sedekia mwana wa Yosia, kuwa mfalme wa Yuda mahali pa Konia mwana wa Yehoyakimu.
2 Lakini Sedekia na maofisa wake pamoja na wananchi wa Yuda hawakusikiliza maonyo ya Mwenyezi-Mungu aliyotoa kwa njia ya nabii Yeremia.
3 Mfalme Sedekia aliwatuma Yehukali mwana wa Shelemia, pamoja na kuhani Sefania mwana wa Maaseya kwa nabii Yeremia, wamwombe awaombee kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wao.
4 Wakati huo, Yeremia alikuwa bado ana uhuru kutembea miongoni mwa watu, maana alikuwa bado hajatiwa gerezani.
5 Tena jeshi la Farao lilikuwa limeondoka Misri, na jeshi la Wakaldayo lililokuwa limeuzingira mji wa Yerusalemu liliposikia habari hizo liliondoka.
6 Ndipo neno la Mwenyezi-Mungu likamjia nabii Yeremia:
7 “Mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, nasema hivi: Utamwambia hivi mfalme wa Yuda ambaye amekutuma uniombe kwa niaba yake: Tazama! Jeshi la Farao lililokuja kukusaidia, liko karibu kurudi makwao Misri.
8 Na Wakaldayo watarudi kuushambulia mji huu. Watauteka mji na kuuteketeza kwa moto.
9 Mimi Mwenyezi-Mungu nasema kwamba msijidanganye wenyewe na kusema kwamba jeshi la Wakaldayo litaondoka; kweli halitaondoka.
10 Hata kama mkilishinda jeshi lote la Wakaldayo wanaopigana nanyi, wakabaki majeruhi tu katika mahema yao, majeruhi hao watainuka na kuuteketeza mji huu kwa moto.”
11 Jeshi la Wakaldayo lilipoondoka Yerusalemu kuliepa jeshi la Farao lililokuwa linakaribia,
12 Yeremia aliondoka Yerusalemu kwenda nchi ya Benyamini ili kupokea sehemu ya urithi wake.
13 Alipokuwa katika lango la Benyamini, mlinzi mmoja aitwaye Iriya mwana wa Shelemia, mwana wa Hanania, alimkamata Yeremia na kumwambia, “Wewe unatoroka uende kujiunga na Wakaldayo!”
14 Yeremia akamwambia, “Huo ni uongo! Mimi sitoroki na kwenda kujiunga na Wakaldayo.” Lakini Iriya hakusadiki maneno ya Yeremia. Basi akamtia nguvuni na kumpeleka kwa maofisa.
15 Maofisa hao walimkasirikia sana Yeremia wakampiga, kisha wakamfunga gerezani katika nyumba ya katibu Yonathani iliyokuwa imegeuzwa kuwa gereza.
16 Yeremia alipokuwa amefungwa gerezani kwa muda wa siku nyingi,
17 mfalme Sedekia alimwita na kumkaribisha kwake. Mfalme akamwuliza kwa faragha wakiwa nyumbani mwake; “Je, kuna neno lolote kutoka kwa Mwenyezi-Mungu?” Yeremia akamjibu, “Naam! Lipo!” Kisha akaendelea kusema, “Wewe utatiwa mikononi mwa mfalme wa Babuloni.”
18 Halafu Yeremia akamwuliza mfalme Sedekia, “Nimekukosea nini, au nimewakosea nini watumishi wako au watu hawa, hata unitie gerezani?
19 Wako wapi manabii waliokutabiria wakisema, ‘Mfalme wa Babuloni hatakushambulia wewe wala nchi hii?’
20 Sasa nakuomba unisikilize, ee bwana wangu mfalme. Nakusihi sana ulikubali ombi langu. Tafadhali usinirudishe tena gerezani katika nyumba ya katibu Yonathani, nisije nikafia humo.”
21 Basi, mfalme Sedekia akatoa amri Yeremia awekwe katika ukumbi wa walinzi akawa anapewa mkate kila siku kutoka kwa waoka mkate mpaka mikate ilipotoweka kabisa huko mjini. Basi, Yeremia alibaki katika ukumbi wa walinzi.
1 Shefatia mwana wa Matani, Gedalia mwana wa Pashuri, mwana wa Malkia, walisikia maneno ambayo Yeremia aliwatangazia watu wote akisema,
2 “Mwenyezi-Mungu asema hivi: Yeyote atakayebaki katika mji huu atakufa kwa vita, njaa na maradhi; lakini yule atakayeondoka na kujisalimisha kwa Wakaldayo, ataishi. Atakuwa ametekwa nyara na kuishi.
3 Mwenyezi-Mungu asema kuwa hakika mji huu utatiwa mikononi mwa jeshi la mfalme wa Babuloni na kutekwa.”
4 Wakuu wakamwambia mfalme, “Yafaa mtu huyu auawe kwa maana anawavunja moyo askari ambao wameachwa katika mji huu na watu wote kwa jumla, kwa kusema maneno kama hayo. Yeye hawatakii watu hawa mema bali mabaya.”
5 Mfalme Sedekia akasema, “Haya! Mtu huyu yumo mikononi mwenu; mimi siwezi kuwapinga.”
6 Basi, wakamchukua Yeremia wakamtumbukiza katika kisima cha Malkia mwana wa mfalme ambacho kilikuwa katika ukumbi wa walinzi. Walimshusha Yeremia ndani kwa kamba. Ndani ya kisima hicho hakukuwa na maji bali tope, naye Yeremia akazama katika tope.
7 Lakini Ebedmeleki, towashi Mwethiopia aliyekuwa akifanya kazi katika ikulu, alipata habari kwamba walikuwa wamemtumbukiza Yeremia kisimani. Wakati huo mfalme alikuwa anabarizi penye lango la Benyamini.
8 Basi, Ebedmeleki akamwendea mfalme, akamwambia,
9 “Bwana wangu mfalme, watu hawa wamefanya kitu kibaya. Wamemtumbukiza yule nabii Yeremia kisimani ambamo kwa kweli atakufa kwa njaa, kwa maana hamna chakula tena mjini.”
10 Hapo mfalme akamwamuru Ebedmeleki, Mwethiopia: “Chukua watu watatu kutoka hapa uende ukamtoe nabii Yeremia kisimani, kabla hajafa.”
11 Basi, Ebedmeleki akawachukua watu hao na kwenda pamoja nao ikulu kwa mfalme, wakaingia katika ghala ya ikulu; Ebedmeleki akatwaa nguo zilizotumika na matambara makuukuu, akamteremshia Yeremia kisimani kwa kamba.
12 Kisha Ebedmeleki, Mwethiopia, akamwambia Yeremia, “Weka hayo matambara kwapani mwako, kisha pitisha kamba hizo chini ya matambara hayo.” Yeremia akafanya hivyo.
13 Kisha wakamvuta Yeremia kwa kamba, wakamtoa kisimani. Baada ya hayo, Yeremia akaendelea kukaa katika ukumbi wa walinzi.
14 Wakati fulani mfalme Sedekia alitaka kumwona nabii Yeremia. Basi, akaagiza Yeremia aletwe kwenye mlango wa tatu wa hekalu la Mwenyezi-Mungu. Huko, mfalme alimwambia Yeremia, “Nataka kukuuliza jambo fulani; usinifiche kitu chochote.”
15 Yeremia akamjibu Sedekia, “Je, nikikuambia ukweli hutaniua? Na kama nikikushauri, hutanisikiliza.”
16 Hapo, mfalme Sedekia alimwapia Yeremia kwa siri akisema, “Kama aishivyo Mwenyezi-Mungu aliyetupa uhai, sitakuua wala sitakutia mikononi mwa hawa wanaotaka kukuua.”
17 Hapo Yeremia akamwambia Sedekia: “Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi: Kama ukijitoa mwenyewe na kujitia mikononi mwa maofisa wa mfalme wa Babuloni, utayaokoa maisha yako na mji hautateketezwa kwa moto; nawe pamoja na jamaa yako mtaendelea kuishi.
18 Lakini usipojitoa mwenyewe na kujitia mikononi mwa maofisa wa mfalme wa Babuloni, basi, mji huu utatekwa na Wakaldayo nao watauteketeza kwa moto, nawe hutaweza kujiepusha mikononi mwao.”
19 Mfalme Sedekia akamwambia Yeremia, “Nawaogopa Wayahudi waliokimbilia kwa Wakaldayo. Huenda nikakabidhiwa kwao, wakanitesa.”
20 Yeremia akamjibu, “Hutakabidhiwa kwao. Wewe sasa tii anachosema Mwenyezi-Mungu, kama ninavyokuambia, na mambo yote yatakuendea vema, na maisha yako yatasalimika.
21 Lakini kama ukikataa kujitoa mwenyewe na kujitia mikononi mwao, haya ndiyo maono ambayo Mwenyezi-Mungu amenionesha.
22 Katika maono hayo, niliona wanawake waliobaki katika ikulu ya mfalme wa Yuda wakipelekwa kwa maofisa wa mfalme wa Babuloni, nao walikuwa wakisema hivi: ‘Marafiki zako uliowaamini wamekudanganya, nao wamekushinda; kwa kuwa miguu yako imezama matopeni, wamekugeuka na kukuacha.’
23 Wake zako wote na watoto wako watapelekwa kwa Wakaldayo, nawe mwenyewe hutanusurika. Utachukuliwa mateka na mfalme wa Babuloni na mji huu utateketezwa kwa moto.”
24 Sedekia akamwambia Yeremia: “Mtu yeyote asijue habari hizi, nawe hutauawa.
25 Kama viongozi wakisikia kuwa nimeongea nawe, kisha wakaja na kukuambia, ‘Hebu tuambie, ulizungumza nini na mfalme. Usitufiche chochote nasi hatutakuua’;
26 wewe utawaambia hivi: ‘Nilikuwa ninamsihi mfalme kwa unyenyekevu asinirudishe gerezani nyumbani kwa Yonathani, nisije nikafia huko.’”
27 Kisha, viongozi walimjia Yeremia wakamwuliza mambo hayo, naye akawajibu kama mfalme alivyomwelekeza. Ndipo walipoacha kuzungumza naye kwa sababu hakuna mtu aliyekuwa amesikia mazungumzo yake na mfalme.
28 Yeremia alibaki katika ukumbi wa walinzi mpaka siku mji wa Yerusalemu ulipotekwa.
1 Mnamo mwezi wa tisa wa mwaka wa tisa wa utawala wa Sedekia mfalme wa Yuda, Nebukadneza mfalme wa Babuloni alifika na jeshi lake lote kuushambulia mji wa Yerusalemu, akauzingira.
2 Na katika siku ya tisa ya mwezi wa nne, mwaka wa kumi na moja wa utawala wa Sedekia, sehemu ya ukuta wa mji ilibomolewa.
3 (Basi maofisa wakuu wafuatao wa mfalme wa Babuloni waliingia na kukaa kwenye lango la katikati: Nergal-shareza, Samgar-nebo, Sar-sekimu mkuu wa matowashi na Nergal-shareza mkuu wa wanajimu, pamoja na maofisa wengine wote wa mfalme wa Babuloni.)
4 Naye Sedekia, mfalme wa Yuda na askari wake wote walipowaona, walitoroka. Walitoka nje ya mji usiku, wakipitia katika bustani ya mfalme, kwenye lango katikati ya kuta mbili, wakaenda upande wa Araba.
5 Lakini jeshi la Wakaldayo liliwafuatia na kumteka Sedekia katika tambarare za Yeriko. Baada ya kumchukua walimfikisha kwa Nebukadneza, mfalme wa Babuloni huko Ribla, katika nchi ya Hamathi, naye akamhukumu.
6 Hukohuko Ribla, mfalme wa Babuloni aliwaua wana wa Sedekia mbele ya baba yao. Aliwaua pia maofisa wote wa Yuda.
7 Kisha alingoa macho yake Sedekia na kumfunga pingu, ili ampeleke Babuloni.
8 Wakaldayo waliichoma moto ikulu na nyumba za watu; pia walizibomoa kuta za Yerusalemu.
9 Kisha, Nebuzaradani, kapteni wa walinzi wa mfalme, aliwapeleka uhamishoni Babuloni watu waliokuwa wamebaki mjini na wale waliokuwa wamejisalimisha kwake pamoja na watu wote waliokuwa wamebaki.
10 Nebuzaradani, kapteni wa walinzi wa mfalme, aliwaacha katika nchi ya Yuda baadhi ya watu maskini ambao hawakuwa na chochote, akawagawia mashamba ya mizabibu na kuwapa maeneo ya kulima wakati huohuo.
11 Nebukadneza mfalme wa Babuloni alikuwa amempa Nebuzaradani kapteni wa walinzi, amri ifuatayo kuhusu Yeremia:
12 “Mchukue Yeremia, umtunze vema wala usimdhuru; mtendee kama anavyokuambia.”
13 Basi, Nebuzaradani kapteni wa walinzi, Nebushani, Nergal-shareza pamoja na maofisa wakuu wote wa mfalme wa Babuloni, wakatuma watu wamtoe Yeremia ukumbini mwa walinzi.
14 Wakamkabidhi Yeremia kwa Gedalia mwana wa Ahikamu, mjukuu wa Shafani, amchukue nyumbani kwake. Basi, Yeremia akaishi pamoja na wananchi wengine.
15 Neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Yeremia wakati alipokuwa amefungwa katika ukumbi wa walinzi:
16 “Nenda ukamwambie hivi Ebedmeleki, Mwethiopia: Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi: Tazama mimi nitatimiza mambo yale niliyotamka dhidi ya mji huo na sio mambo mema. Mambo hayo yatakamilika siku hiyo ukiona wewe mwenyewe.
17 Lakini siku hiyo mimi nitakuokoa wewe, wala hutatiwa mikononi mwa watu unaowaogopa.
18 Maana, kweli nitakuokoa na hutauawa vitani; utapata faida ya kuokoa maisha yako kwa sababu umeniamini mimi. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
1 Neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Mwenyezi-Mungu wakati Nebuzaradani kapteni wa walinzi wa mfalme, alipomruhusu Yeremia aondoke Rama. Huyo kapteni alimchukua Yeremia amefungwa minyororo, akawachukua pia pamoja naye mateka wengine wote wa Yerusalemu na Yuda ambao walikuwa wamepelekwa uhamishoni Babuloni.
2 Kapteni wa walinzi alimchukua Yeremia, akamwambia “Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, alitangaza maafa dhidi ya mahali hapa.
3 Na sasa Mwenyezi-Mungu ametekeleza jambo hilo na kutenda kama alivyosema, kwa sababu nyinyi nyote mlimkosea Mwenyezi-Mungu na kukataa kumtii, jambo hilo limewapata.
4 Haya! Leo nazifungua pingu mikononi mwako. Kama unaona ni vema kwenda pamoja nami mpaka Babuloni, basi twende pamoja; mimi nitakutunza vizuri. Lakini kama unaona si vizuri kwako kwenda pamoja nami mpaka Babuloni, basi, usije. Ujue kwamba waweza kwenda popote katika nchi hii; basi nenda popote unapoamua kuwa pazuri kwenda.
5 Kama ukiamua kubaki, basi rudi kwa Gedalia mwana wa Ahikamu, mjukuu wa Shafani, ambaye mfalme wa Babuloni amemteua kuwa mtawala wa miji yote ya Yuda, ukakae naye miongoni mwa wananchi wengine. La sivyo, nenda popote unapoona ni sawa kwenda.” Basi, kapteni wa walinzi akampa Yeremia masurufu na zawadi, kisha akamwacha aende zake.
6 Kisha Yeremia akaenda Mizpa kwa Gedalia mwana wa Ahikamu, akakaa naye pamoja na wananchi waliobaki nchini.
7 Makapteni wote wa majeshi kutoka bara pamoja na watu wao, waliposikia kwamba mfalme wa Babuloni alikuwa amemtawaza Gedalia mwana wa Ahikamu, kuwa mkuu wa nchi, na kwamba alikuwa amemkabidhi wanaume, wanawake na watoto, yaani watu mafukara kabisa katika nchi ambao hawakuchukuliwa uhamishoni Babuloni,
8 walimwendea Gedalia huko Mizpa. Watu hao walikuwa Ishmaeli mwana wa Nethania, Yohanani na Yonathani wana wa Karea, Seraya mwana wa Tanhumethi, wana wa Efai kutoka Netofa, na Yezania mwana wa Maakathi; wote waliandamana na watu wao.
9 Gedalia aliapa mbele yao na mbele ya majeshi yao akisema: “Msiogope kuwatumikia Wakaldayo. Kaeni nchini mumtumikie mfalme wa Babuloni, na mambo yote yatawaendea vema.
10 Mimi nitakaa Mizpa niwawakilishe nyinyi kwa Wakaldayo watakaofika kwetu; lakini nyinyi kusanyeni na kuhifadhi divai, matunda ya kiangazi na mafuta, mkae katika miji mnayoimiliki.”
11 Pia watu wa Yuda waliokuwa nchini Moabu na miongoni mwa Waamoni na nchini Edomu na nchi nyingine, waliposikia kwamba mfalme wa Babuloni alikuwa amewaruhusu watu wa Yuda wengine kubaki Yuda na kwamba alikuwa amemweka Gedalia mwana wa Ahikamu, mjukuu wa Shafani, kuwa mtawala wao,
12 wote walirudi kutoka mahali pote walipokuwa wametawanyika na kwenda katika nchi ya Yuda kwa Gedalia huko Mizpa. Walichuma zabibu na matunda ya kiangazi kwa wingi sana.
13 Basi, Yohanani mwana wa Karea pamoja na viongozi wote wa majeshi kutoka bara, walifika kwa Gedalia, huko Mizpa, wakamwambia,
14 “Je, una habari kwamba Baali mfalme wa Waamoni, amemtuma Ishmaeli mwana wa Nethania, akuue?” Lakini Gedalia mwana wa Ahikamu, hakuamini maneno yao.
15 Kisha, Yohanani mwana wa Karea, akazungumza na Gedalia kwa faragha huko Mizpa, akamwambia, “Acha niende nikamuue Ishmaeli mwana wa Nethania, na hakuna mtu yeyote atakayejua. Kwa nini yeye akuue na watu wa Yuda wote waliokusanyika hapa watawanyike na Wayahudi waliobaki waangamie?”
16 Lakini Gedalia mwana wa Ahikamu, akamwambia Yohanani mwana wa Karea, “Usifanye jambo hilo! Mambo unayosema juu ya Ishmaeli si ya kweli!”
1 Mnamo mwezi wa saba, Ishmaeli mwana wa Nethania, mjukuu wa Elishama, wa ukoo wa kifalme, mmoja wa maofisa wakuu wa mfalme, alifika Mizpa kwa Gedalia akiandamana na watu kumi. Wakati walipokuwa wanakula chakula huko Mizpa,
2 Ishmaeli mwana wa Nethania pamoja na wale watu kumi, wakainuka na kumshambulia kwa upanga Gedalia mwana wa Ahikamu, mjukuu wa Shafani, wakamuua. Gedalia ndiye aliyekuwa ameteuliwa na mfalme wa Babuloni kuwa mtawala wa nchi.
3 Ishmaeli aliwaua pia Wayahudi wote waliokuwa pamoja na Gedalia huko Mizpa na wanajeshi Wakaldayo waliokuwa mahali hapo.
4 Siku moja baada ya kumwua Gedalia,
5 kabla hata mtu yeyote hajajua habari hizo, walifika watu themanini kutoka Shekemu, Shilo na Samaria. Walikuwa wamenyoa ndevu zao na wamevaa mavazi yaliyotatuka na miili yao imechanjwachanjwa. Walileta tambiko za nafaka na ubani zitolewe hekaluni kwa Mwenyezi-Mungu.
6 Ishmaeli mwana wa Nethania, alitoka nje ya mji kuwalaki watu hao huku analia. Alipokutana nao, akawaambia, “Karibuni nyumbani kwa Gedalia mwana wa Ahikamu.”
7 Walipoingia mjini, Ishmaeli mwana wa Nethania, pamoja na wale watu kumi waliokuwa pamoja naye, waliwaua watu hao na kuzitupa maiti zao kisimani.
8 Lakini palikuwa na watu kumi katika kundi hilo waliomwambia Ishmaeli: “Tafadhali usituue, maana tuna akiba kubwa ya ngano, shayiri, mafuta na asali ambayo tumeificha mashambani.” Basi hao akawaacha hai.
9 Kisima ambamo Ishmaeli alitupa maiti za wale watu aliowaua kilikuwa ni kile kikubwa, ambacho mfalme Asa alikuwa amekichimba ili kujihami dhidi ya Baasha, mfalme wa Waisraeli. Ishmaeli mwana wa Nethania, alikijaza kisima hicho maiti za wale watu aliowaua.
10 Kisha, Ishmaeli aliwateka binti zake mfalme na watu wote waliosalia Mizpa, watu ambao Nebuzaradani, kapteni wa walinzi, alikuwa amemkabidhi Gedalia mwana wa Ahikamu. Ishmaeli mwana wa Nethania, aliwachukua mateka hao, akaondoka, akaenda kwa Waamoni.
11 Lakini Yohanani mwana wa Karea, pamoja na viongozi wote wa majeshi, waliposikia juu ya uovu ambao Ishmaeli mwana wa Nethania, alikuwa ameufanya,
12 waliwakusanya watu wao wote, wakaenda kupigana na Ishmaeli. Walimkuta penye bwawa kuu lililoko Gibeoni.
13 Watu wote waliotekwa na Ishmaeli walipomwona Yohanani mwana wa Karea, pamoja na viongozi wote wa majeshi, walifurahi sana.
14 Basi, watu hao wote ambao Ishmaeli alikuwa amewachukua mateka kutoka Mizpa, waligeuka, wakarudi nyuma, wakamwendea Yohanani mwana wa Karea.
15 Lakini Ishmaeli mwana wa Nethania, pamoja na watu wanane waliponyoka kutoka kwa Yohanani, wakakimbilia kwa Waamoni.
16 Kisha, Yohanani mwana wa Karea pamoja na viongozi wote wa majeshi waliokuwa pamoja naye, waliwachukua watu wote waliosalia, ambao Ishmaeli mwana wa Nethania, alikuwa amewachukua mateka kutoka Mizpa baada ya kumwua Gedalia mwana wa Ahikamu, yaani: Askari, wanawake, watoto na matowashi. Yohanani aliwarudisha wote kutoka Gibeoni.
17 Basi, wakaenda zao, wakakaa huko Geruthi Kimahamu karibu na Bethlehemu, wakikusudia kuingia katika nchi ya Misri, kwa sababu
18 walikuwa wanawaogopa Wakaldayo tangu wakati Ishmaeli mwana wa Nethania, alipomuua Gedalia mwana wa Ahikamu ambaye mfalme wa Babuloni alikuwa amemteua kuwa mtawala wa nchi.
1 Kisha makamanda wote wa majeshi, Yohanani mwana wa Karea, na Azaria mwana wa Heshaia pamoja na watu wote, wadogo kwa wakubwa,
2 wakamwendea Yeremia, wakamwambia, “Tafadhali sikiliza maombi yetu na kutuombea dua kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, sisi sote tuliosalia (kwa maana tulikuwa wengi, lakini sasa tumebaki wachache tu, kama uonavyo).
3 Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, na atuoneshe njia anayotaka tuifuate, na kile anachotaka tukifanye.”
4 Yeremia akawajibu, “Vema; nimesikia. Nitamwomba Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, kama mlivyonisihi; jibu lolote atakalonipa Mwenyezi-Mungu, nitawaambieni; sitawaficha chochote.”
5 Kisha, watu wakamwambia Yeremia, “Mwenyezi-Mungu na awe shahidi wa kweli na mwaminifu dhidi yetu ikiwa hatutafanya jinsi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako atakavyokuagiza utuambie.
6 Iwe ni jambo la kupendeza au la, sisi tutaitii sauti ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu ambaye tunakutuma kwake ili tufanikiwe tutakapomtii Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu.”
7 Baada ya siku kumi, neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Yeremia.
8 Basi, Yeremia akamwita Yohanani mwana wa Karea, na makamanda wote wa majeshi pamoja na watu wote, wadogo kwa wakubwa, akawaambia,
9 “Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli ambaye mlinituma kwake nipeleke maombi yenu, asema hivi:
10 Kama mtabaki katika nchi hii, basi, nitawajenga, wala sitawabomoa; nitawaotesha wala sitawangoa; kwa maana nitabadili nia kwa sababu ya maafa niliyowatenda.
11 Msimwogope mfalme wa Babuloni mnayemwogopa; naam, msimwogope hata kidogo. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema. Mimi niko pamoja nanyi kuwaokoeni na kuwasalimisha kutoka mikononi mwake.
12 Nitawahurumieni na kumfanya mfalme awahurumie na kuwaacha nchini mwenu.
13 “Lakini mkisema: ‘Hatutaki kubaki katika nchi hii,’ na hivyo mkaacha kutii sauti ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu,
14 na kusema kwamba mtakwenda kukaa nchini Misri, ambako hamtaona vita wala kusikia sauti ya tarumbeta wala kukosa chakula,
15 basi, sikilizeni asemavyo Mwenyezi-Mungu enyi mabaki ya Yuda. Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, asema hivi: Kama mmekusudia kuingia nchini Misri na kukaa huko,
16 basi, vita mnavyoviogopa vitawakumba hukohuko Misri, na njaa mnayoihofia itawaandama vikali hadi Misri, na mtafia hukohuko.
17 Watu wote wenye nia ya kwenda kukaa Misri watakufa kwa njaa na maradhi mabaya wala hakuna hata mmoja wao atakayebaki au kunusurika kutokana na maafa nitakayowaletea.
18 “Maana mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, nasema hivi: Kama vile hasira yangu na ghadhabu yangu ilivyowapata wakazi wa Yerusalemu, ndivyo ghadhabu yangu itakavyowapata nyinyi, kama mtakwenda Misri. Mtakuwa kitu cha kutukanwa, kitisho, laana na aibu. Hamtapaona tena mahali hapa.”
19 Yeremia akawaambia watu: “Enyi Wayahudi mliosalia, Mwenyezi-Mungu aliwaambia msiende Misri. Jueni wazi kwamba leo nimewaonya kuwa
20 mmepotoka, mmeyahatarisha maisha yenu. Maana mlinituma kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, mkiniambia, ‘Tuombee dua kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, na chochote Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu atakachosema, utuambie, nasi tutatekeleza.’
21 Leo mimi nimewaambieni lakini hamkutii chochote ambacho Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu amenituma niwaambie.
22 Basi, jueni hakika kwamba mahali mnapotamani kwenda kukaa mtafia hukohuko kwa vita, njaa na maradhi.”
1 Yeremia alipomaliza kuwaambia watu wote maneno yote ambayo Mwenyezi-Mungu, Mungu wao, alimwamuru awatangazie,
2 Azaria mwana wa Hoshaia, Yohanani mwana wa Karea na watu wote mafidhuli, walimwambia Yeremia: “Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, hakukutuma wewe utuambie tusiende Misri, tukaishi huko.
3 Baruku mwana wa Neria, amekuchochea dhidi yetu ili tutiwe mikononi mwa Wakaldayo watuue au watupeleke uhamishoni Babuloni.”
4 Basi, Yohanani mwana wa Karea na makamanda wote wa majeshi pamoja na watu wote hawakutii aliyosema Mwenyezi-Mungu, kwamba wabaki katika nchi ya Yuda.
5 Hapo Yohanani mwana wa Karea na makamanda wote wa majeshi waliwachukua watu wote wa Yuda waliosalia ambao walikuwa wamerudi nchini Yuda kutoka mataifa yote ambako walikuwa wametawanywa;
6 wanaume, wanawake, watoto, binti za mfalme na kila mtu ambaye Nebuzaradani, kapteni wa walinzi, alikuwa amemwachia Gedalia mwana wa Ahikamu, mjukuu wa Shafani, wakamchukua pia nabii Yeremia na Baruku mwana wa Neria,
7 wakaenda nchini Misri, wakawasili mjini Tahpanesi. Ndivyo walivyokataa kutii alichosema Mwenyezi-Mungu
8 Basi neno la Mwenyezi-Mungu likamjia Yeremia huko Tahpanesi:
9 “Chukua mawe makubwa, ukayafiche katika chokaa ya matofali kwenye lango la ikulu ya Farao mjini Tahpanesi, watu wa Yuda wakiwa wanaona.
10 Kisha waambie hivi: Tazameni mimi nitamtuma na kumleta Nebukadneza, mfalme wa Babuloni, mtumishi wangu, naye ataweka kiti chake cha enzi juu ya mawe haya ambayo nimeyaficha hapa, na kutandaza paa la kifalme juu yake.
11 Atakapofika ataiangamiza nchi ya Misri. Hapo waliopangiwa kufa kwa maradhi watakufa kwa maradhi, waliopangiwa kuchukuliwa mateka, watachukuliwa mateka; waliopangiwa kufia vitani watafia vitani.
12 Mimi nitawasha moto katika mahekalu ya miungu ya Misri; naye Nebukadneza ataiteketeza miungu hiyo kwa moto au kuichukua mateka mpaka Babuloni. Ataisafisha nchi ya Misri kama mchungaji atoavyo kupe katika vazi lake na kuondoka Misri akiwa mshindi.
13 Ataivunja minara ya ukumbusho iliyoko huko Heliopoli nchini Misri, na mahekalu ya miungu ya Misri atayateketeza kwa moto.”
1 Neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Yeremia kuhusu Wayahudi waliokuwa wanakaa nchini Misri katika miji ya Migdoli, Tahpanesi, Memfisi na sehemu ya Pathrosi:
2 “Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli asema hivi: Nyinyi mmeona maafa yote niliyouletea mji wa Yerusalemu na miji yote ya Yuda. Miji hii ni magofu mpaka leo wala hakuna mtu aishiye humo.
3 Imekuwa hivyo kwa sababu ya uovu walioufanya, wakanikasirisha kwa kuifukizia ubani na kuitumikia miungu mingine ambayo wao wenyewe hawakuifahamu, wala nyinyi, wala wazee wenu.
4 Hata hivyo, mimi daima niliwatuma kwenu watumishi wangu manabii nikisema: Msifanye jambo hili baya ninalolichukia!
5 Lakini hakuna aliyenisikiliza wala kunitegea sikio. Nyinyi mlikataa kuacha uovu wenu na kuacha kuifukizia ubani miungu mingine.
6 Kwa hiyo, ghadhabu yangu na hasira yangu iliwaka na kumiminika juu ya miji ya Yuda na barabara za Yerusalemu, hata kukawa jangwa na magofu kama ilivyo mpaka leo.
7 “Sasa, mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, nauliza hivi: Mbona mnajiletea madhara makubwa namna hii, na kujiangamiza nyinyi wenyewe, wanaume kwa wanawake, watoto wadogo na wachanga, hata pasibaki mtu katika Yuda?
8 Kwa nini mnanichochea nikasirike kwa kuabudu sanamu mlizojitengenezea wenyewe na kuifukizia ubani miungu mingine katika nchi ya Misri ambamo mmekuja kuishi? Je, mwataka kutokomezwa na kuwa laana na dhihaka mbele ya mataifa yote duniani?
9 Je, mmesahau uovu wa wazee wenu, uovu wa wafalme wa Yuda, uovu wa wake zao na uovu wenu nyinyi wenyewe na wa wake zenu, ambao mliufanya nchini Yuda na kwenye barabara za Yerusalemu?
10 Mpaka hivi leo hamjajinyenyekesha wala kuogopa wala kuzifuata sheria zangu na kanuni zangu nilizowawekea nyinyi na wazee wenu.
11 “Kwa hiyo, mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, nasema hivi: Haya! Nitawageukia niwaleteeni maafa na kuiangamiza Yuda yote.
12 Nitawaondoa watu wa Yuda waliosalia ambao wamepania kwenda kukaa Misri, na kuwaangamiza wote, wakubwa kwa wadogo; watakufa kwa upanga au kwa njaa. Watakuwa takataka, kitisho, laana na dhihaka.
13 Nitawaadhibu wale wanaokaa katika nchi ya Misri kama nilivyouadhibu mji wa Yerusalemu, kwa vita, njaa, na maradhi mabaya.
14 Kwa hiyo hapatakuwa na mtu hata mmoja kati ya watu wa Yuda waliosalia na kwenda kukaa katika nchi ya Misri ambaye atanusurika au kuishi au kurudi katika nchi ya Yuda ambayo wanatamani kurudi na kuishi humo. Hawatarudi, isipokuwa baadhi ya wakimbizi.”
15 Kisha, wanaume wote waliojua kwamba wake zao walikuwa wameifukizia ubani miungu mingine, na wanawake wote waliokuwa hapo, kusanyiko kubwa la watu, pamoja na Waisraeli waliokuwa wanakaa Pathrosi katika nchi ya Misri walimjibu Yeremia:
16 “Jambo hilo ulilotuambia kwa niaba ya Mwenyezi-Mungu hatutalitii.
17 Lakini kila kitu tulichoapa kufanya tutafanya: Tutamfukizia ubani malkia wa mbinguni na kummiminia tambiko ya kinywaji kama tulivyokuwa tunafanya sisi wenyewe na wazee wetu, wafalme wetu na viongozi wetu, katika miji ya Yuda na katika barabara za Yerusalemu. Ama wakati huo tulikuwa na chakula tele, tulistawi na hatukuona janga lolote.
18 Lakini tangu tuache kumfukizia ubani malkia wa mbinguni na kummiminia kinywaji, tumetindikiwa kila kitu, na tumeangamizwa kwa vita na njaa.”
19 Nao wanawake wakasema, “Tulimfukizia ubani na kummiminia kinywaji malkia wa mbinguni. Tulifanya hivyo kwa kibali cha waume zetu. Tena tulimtengenezea mikate yenye sura yake na kummiminia kinywaji!”
20 Ndipo Yeremia akawaambia watu wote, wanaume kwa wanawake, yaani watu wote waliompa jibu hilo:
21 “Kuhusu matambiko ambayo nyinyi na wazee wenu, wafalme wenu na viongozi wenu, pamoja na wananchi wote, mlifanya katika miji ya Yuda na katika barabara za Yerusalemu, je, mnadhani Mwenyezi-Mungu amesahau au hakumbuki?
22 Mwenyezi-Mungu hakuweza kuvumilia tena matendo yenu maovu na mambo ya kuchukiza mliyotenda; ndiyo maana nchi yenu imekuwa ukiwa, jangwa, laana na bila wakazi, kama ilivyo mpaka leo.
23 Maafa haya yamewapata mpaka leo kwa sababu mliitolea sadaka za kuteketezwa miungu mingine na kumkosea Mwenyezi-Mungu, mkakataa kutii sauti yake au kufuata sheria yake, kanuni zake na maagizo yake.”
24 Yeremia aliwaambia watu wote na wanawake wote: “Sikilizeni neno la Mwenyezi-Mungu, enyi watu wa Yuda wote mlioko nchini Misri.
25 Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi: Nyinyi pamoja na wake zenu mmetekeleza kwa vitendo yale mliyotamka kwa vinywa vyenu, mkisema kwamba mmepania kutimiza viapo vyenu mlivyofanya vya kumtolea sadaka na kummiminia kinywaji malkia wa mbinguni. Haya basi! Shikeni viapo vyenu na kutoa sadaka za vinywaji!
26 Lakini sikilizeni neno langu mimi Mwenyezi-Mungu, enyi watu wote wa Yuda mnaokaa nchini Misri. Mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Naapa kwa jina langu kuu kwamba hakuna mtu yeyote wa Yuda katika nchi yote ya Misri atakayelitumia jina langu kuapa nalo akisema: ‘Kama aishivyo Bwana Mwenyezi-Mungu!’
27 Mimi nawachungulia hao sio kwa mema bali kwa mabaya. Watu wote wa Yuda nchini Misri wataangamizwa kwa upanga na njaa, asibaki hata mtu mmoja.
28 Ni wachache watakaonusurika vitani na kurudi kutoka nchi ya Misri na kwenda nchini Yuda. Hapo watu wa Yuda wote waliobaki kati ya wale waliokwenda kukaa Misri watatambua ni tamko la nani lenye nguvu: Langu au lao!
29 Mimi Mwenyezi-Mungu nasema kwamba nitawaadhibu hapahapa mpate kujua kwamba maneno ya maafa niliyotamka dhidi yenu yatatimia. Na hii itakuwa ishara yake:
30 Nitamtia Farao Hofra mfalme wa Misri, mikononi mwa madui zake, mikononi mwa wale wanaotaka kumwua, kama vile nilivyomtia Sedekia mfalme wa Yuda, mikononi mwa adui yake yaani Nebukadneza, mfalme wa Babuloni, ambaye alitaka kumwua. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
1 Haya ndiyo maneno aliyotamka nabii Yeremia mnamo mwaka wa nne wa utawala wa Yehoyakimu mwana wa Yosia naye Baruku mwana wa Neria akawa anayaandika kitabuni. Yeremia alimwambia Baruku:
2 “Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, asema hivi juu yako wewe Baruku:
3 Wewe ulisema, ‘Ole wangu! Mwenyezi-Mungu ameniongezea uchungu juu ya maumivu yangu. Nimechoka kupiga kite, wala sipati pumziko.’
4 Lakini Mwenyezi-Mungu ameniambia nikuambie hivi: Tazama, yale niliyojenga nayabomoa, na yale niliyopanda nayangoa; nitafanya hivyo katika nchi yote.
5 Je, wewe unajitakia mambo makubwamakubwa? Usiyatafute! Achana nayo, maana, ninaleta maangamizi juu ya wanadamu wote. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema. Wewe tuzo lako ni hili: Nitayaokoa maisha yako kila mahali utakapokwenda.”
1 Neno la Mwenyezi-Mungu lililomjia Yeremia kuhusu watu wa mataifa.
2 Kuhusu Misri na jeshi la Farao Neko mfalme wa Misri, lililokuwa huko Karkemishi karibu na mto Eufrate ambalo Nebukadneza mfalme wa Babuloni alilishambulia mnamo mwaka wa nne wa utawala wa Yehoyakimu mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda:
3 Tayarisheni ngao ndogo na kubwa msonge mbele kupigana vita.
4 Tandikeni farasi na kuwapanda, Shikeni nafasi zenu na kofia za chuma mvae. Noeni mikuki yenu, vaeni mavazi yenu ya chuma!
5 Lakini mbona nawaona wametishwa? Wamerudi nyuma. Mashujaa wao wamepigwa, wamekimbia mbio, bila hata kugeuka nyuma. Kitisho kila upande. Mwenyezi-Mungu amesema.
6 Walio wepesi kutoroka hawawezi, mashujaa hawawezi kukwepa; huko kaskazini kwenye mto Eufrate wamejikwaa na kuanguka.
7 Nani huyo aliye kama mto Nili uliofurika kama mito inayoumuka mawimbi?
8 Misri ni kama mto Nili uliofurika kama mito inayoumuka mawimbi Ilisema: “Nitajaa, nitaifunika nchi, nitaiharibu miji na wakazi wake.
9 Songeni mbele, enyi farasi, shambulieni enyi magari ya farasi. Mashujaa wasonge mbele: Watu wa Kushi na Puti washikao ngao, watu wa Ludi, stadi wa kutumia pinde.”
10 Siku hiyo ni siku ya Mwenyezi-Mungu wa majeshi, ni siku ya kulipiza kisasi; naam, siku ya kuwaadhibu maadui zake. Upanga utawamaliza hao na kutosheka, utainywa damu yao na kushiba. Maana Mwenyezi-Mungu wa majeshi anayo kafara huko kaskazini karibu na mto Eufrate.
11 Pandeni Gileadi, enyi watu wa Misri, mkachukue dawa ya marhamu. Mmetumia dawa nyingi bure; hakuna kitakachowaponya nyinyi.
12 Mataifa yamesikia aibu yenu, kilio chenu kimeenea duniani kote; mashujaa wamegongana wenyewe kwa wenyewe, wote pamoja wameanguka.
13 Neno ambalo Mwenyezi-Mungu alimwambia Yeremia wakati alipofika Nebukadneza mfalme wa Babuloni kuishambulia nchi ya Misri:
14 “Tangaza nchini Misri, piga mbiu huko Migdoli, tangaza huko Memfisi na Tahpanesi. Waambie: ‘Kaeni tayari kabisa maana upanga utawaangamiza kila mahali.’
15 Kwa nini shujaa wako amekimbia? Mbona fahali wako hakuweza kustahimili? Kwa sababu mimi Mwenyezi-Mungu nilimwangusha chini!
16 Wengi walijikwaa, wakaanguka, kisha wakaambiana wao kwa wao: ‘Simameni, tuwaendee watu wetu, turudi katika nchi yetu, tuukimbie upanga wa adui.’
17 “Naye Farao, mfalme wa Misri, mpangeni jina hili: ‘Kishindo kitupu!’
18 Mimi naapa kwa uhai wangu nasema mimi mfalme niitwaye Mwenyezi-Mungu wa majeshi, kweli adui anakuja kuwashambulieni: Ni hakika kama Tabori ulivyo mlima kama mlima Karmeli uonekanavyo kutoka baharini.
19 Enyi wakazi wa Misri jitayarisheni na mizigo kwenda uhamishoni! Maana mji wa Memfisi utaharibiwa kabisa, utakuwa magofu yasiyokaliwa na watu.
20 Misri ni kama mtamba mzuri wa ng'ombe, lakini kipanga kutoka kaskazini amemvamia.
21 Hata askari wake wa kukodiwa ni kama ndama wanono; nao pia wamegeuka, wakakimbia pamoja, wala hawakuweza kustahimili, kwa maana siku yao ya kuangamizwa imefika, wakati wao wa kuadhibiwa umewadia.
22 Misri anatoa sauti kama nyoka anayekimbia; maana maadui zake wanamjia kwa nguvu, wanamjia kwa mashoka kama wakata-miti.
23 Wataukata kabisa msitu wake, ingawa haupenyeki, nasema mimi Mwenyezi-Mungu, maana wao ni wengi kuliko nzige wasiohesabika.
24 Watu wa Misri wataaibishwa, watatiwa mikononi mwa watu kutoka kaskazini.”
25 Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, alisema: “Tazama, mimi nitamwadhibu Amoni mungu wa Thebesi, nitaiadhibu Misri na miungu yake na wafalme wake, nitamwadhibu Farao na wote wanaomtegemea.
26 Nitawatia mikononi mwa wale wanaotaka kuyaangamiza maisha yao, yaani Nebukadneza mfalme wa Babuloni na maofisa wake. Baadaye, nchi ya Misri itakaliwa na watu kama ilivyokuwa hapo zamani. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
27 “Lakini wewe usiogope, ee Yakobo mtumishi wangu, usifadhaike, ee Israeli; maana, kutoka mbali nitakuokoa, nitakuja kuwaokoa wazawa wako kutoka nchi walimohamishwa. Yakobo utarudi na kutulia na kustarehe, wala hakuna yeyote atakayekutia hofu.
28 Usiogope, ee Yakobo mtumishi wangu, kwa maana mimi niko pamoja nawe. Nitayaangamiza kabisa mataifa yote ambayo nimekutawanya kati yao, lakini wewe sitakuangamiza. Nitakuchapa kadiri unavyostahili, sitakuacha bila kukuadhibu.”
1 Neno la Mwenyezi-Mungu lililomjia nabii Yeremia kuhusu Wafilisti, kabla Farao hajaushambulia mji wa Gaza:
2 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Tazama! Maji yanapanda kutoka kaskazini, nayo yatakuwa mto uliofurika; yataifunika nchi nzima na vyote vilivyomo, mji na wakazi na wanaoishi humo. Watu watalia, wakazi wote wa nchi wataomboleza.
3 Watasikia mshindo wa kwato za farasi, kelele za magari ya vita, na vishindo vya magurudumu yao. Kina baba watawasahau watoto wao, mikono yao itakuwa imelegea mno.
4 Hiyo ni siku ya kuwaangamiza Wafilisti wote, kukomesha msaada uliobakia kutoka Tiro na Sidoni. Maana Mwenyezi-Mungu anawaangamiza Wafilisti, watu waliosalia wa kisiwa cha Kaftori.
5 Watu wa Gaza wamenyoa upara kuomboleza; mji wa Ashkeloni umeangamia. Enyi watu wa Anakimu mliobaki mpaka lini mtajikatakata kwa huzuni?
6 Ee upanga wa Mwenyezi-Mungu! Utachukua muda gani ndipo utulie? Ingia katika ala yako, ukatulie na kunyamaa!
7 Lakini utawezaje kutulia, hali Mwenyezi-Mungu ameupa kazi? Ameuamuru ushambulie mji wa Ashkeloni na watu wanaoishi pwani.”
1 Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi: “Ole watu wa Nebo, maana mji wake umeharibiwa! Kiriathaimu umeaibishwa, umetekwa, ngome yake imebomolewa mbali;
2 fahari ya Moabu imetoweka. Mpango ulifanywa huko Heshboni dhidi yake: ‘Haya! Tuwaangamize wasiwe tena taifa!’ Nawe Madmeni utanyamazishwa, upanga utakufuatia.
3 Sikiliza! Kilio kutoka Horonaimu: ‘Maangamizi na uharibifu mkubwa!’
4 Moabu tayari imeangamizwa kilio chake chasikika mpaka Soari.
5 Walionusurika wanapanda kwenda Luhithi huku wanalia kwa sauti. Wanapoteremka kwenda Horonaimu, wanasikia kilio cha uharibifu.
6 Kimbieni! Jiokoeni wenyewe! Kimbieni kama pundamwitu jangwani!
7 “Moabu, ulitumainia ngome na hazina zako, lakini sasa wewe pia utatekwa; mungu wako Kemoshi atapelekwa uhamishoni pamoja na makuhani na watumishi wake.
8 Mwangamizi atapita katika kila mji, hakuna mji utakaomwepa; kila kitu mabondeni kitaangamia nyanda za juu zitaharibiwa, kama alivyosema Mwenyezi-Mungu.
9 Mchimbieni Moabu kaburi, maana kuangamia kwake ni hakika; miji yake itakuwa tupu, bila mkazi hata mmoja.
10 Na alaaniwe mtu afanyaye kazi ya Mwenyezi-Mungu kwa ulegevu; alaaniwe anayezuia upanga wake usimwage damu!
11 Moabu amestarehe tangu ujana wake, ametulia kama divai katika gudulia. Hajamiminiwa toka chombo hata chombo, hajapata kuchukuliwa uhamishoni. Kwa hiyo yungali na ladha yake, harufu yake nzuri haijabadilika kamwe.
12 “Kwa hiyo, wakati waja, nasema mimi Mwenyezi-Mungu ambapo nitampelekea wamiminaji ambao wataimimina divai yake. Wataimwaga yote kutoka vyombo vyake na kuvivunja vipandevipande.
13 Hapo Wamoabu watamwonea aibu mungu wao Kemoshi, kama vile watu wa Israeli walivyomwonea aibu Betheli, mungu waliyemtegemea.
14 Mwawezaje kusema: ‘Sisi ni mashujaa, na watu wenye nguvu nyingi za vita?’
15 Mwangamizi wa Moabu na miji yake amewasili vijana wake wazuri wamechinjwa. Nimesema mimi mfalme niitwaye Mwenyezi-Mungu wa Majeshi.
16 Janga la Moabu limekaribia, maangamizi yake yanawasili haraka.
17 Mwomboleezeni Moabu, enyi jirani zake wote, na nyote mnaomjua vizuri semeni: ‘Jinsi gani fimbo ya nguvu ilivyovunjwa, naam fimbo ile ya fahari!’
18 Enyi wenyeji wa Diboni: Shukeni kutoka mahali penu pa fahari, mkaketi katika ardhi isiyo na maji. Maana mwangamizi wa Moabu, amefika kuwashambulia; amekwisha haribu ngome zenu.
19 Enyi wakazi wa Aroeri, simameni kando ya njia mtazame! Mwulizeni anayekimbia na anayetoroka: ‘Kumetokea nini?’
20 Moabu imeaibishwa maana imevunjwa; ombolezeni na kulia. Tangazeni kando ya mto Arnoni, kwamba Moabu imeharibiwa kabisa.
21 “Hukumu imeifikia miji iliyo nyanda za juu: Holoni, Yasa, Mefaathi,
22 Diboni, Nebo, Beth-diblathaimu,
23 Kiriathaimu, Beth-gamuli, Beth-meoni,
24 Keriothi na Bosra. Naam, hukumu imeifikia miji yote ya Moabu mbali na karibu.
25 Nguvu za Moabu zimevunjiliwa mbali na uwezo wake umevunjwa. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
26 “Mlewesheni Moabu kwa sababu alijikuza dhidi yangu mimi Mwenyezi-Mungu. Moabu atagaagaa katika matapishi yake na watu watamcheka.
27 Kumbuka Moabu ulivyomcheka Israeli. Je, alikamatwa pamoja na wezi, hata ukawa unatikisa kichwa chako kila ulipoongea juu yake?
28 “Enyi wenyeji wa Moabu, tokeni mijini, mkakae mapangoni! Mwigeni njiwa ajengaye kiota penye genge.
29 Tumesikia juu ya kiburi cha Moabu; Moabu ana majivuno sana. Tumesikia juu ya kujiona, kiburi na majivuno yake; tumesikia jinsi anavyojigamba moyoni.
30 “Nami Mwenyezi-Mungu nasema: Najua ufidhuli wake; Majivuno yake ni ya bure, na matendo yake si kitu.
31 Kwa hiyo ninaomboleza juu ya Moabu, ninalia kwa ajili ya Wamoabu wote, naomboleza juu ya watu wa Kir-heresi.
32 Nakulilia wewe bustani ya Sibma kuliko hata watu wa Yazeri. Matawi yako yametanda mpaka ngambo ya bahari ya Chumvi yakafika hata mpaka Yazeri. Lakini mwangamizi ameyakumba matunda yako ya kiangazi na zabibu zako.
33 Furaha na shangwe zimeondolewa kutoka nchi ya Moabu yenye rutuba. Nimeikomesha divai kutoka mashinikizo hakuna mtu anayekamua zabibu kwa shangwe; kelele zinazosikika si za shangwe.
34 “Kilio cha watu wa Heshboni chasikika huko Eleale mpaka Yahazi; kinaenea kutoka Soari mpaka Horonaimu na hata Eglath-shelishiya. Hata maji ya kijito Nimrimu yamekauka.
35 Nami nitamfutilia mbali kila mtu katika Moabu ambaye anatambikia vilimani na kumfukizia ubani mungu wake.
36 “Kwa hiyo, moyo wangu unaomboleza juu ya watu wa Moabu na watu wa Kir-heresi, kama mpiga zumari mazishini; maana hata mali yote waliyojipatia imeangamia.
37 Kila mtu amenyoa upara na ndevu zake. Wote wamejikatakata mikononi na viunoni wamevaa mavazi ya gunia.
38 Juu ya nyumba za Moabu na katika viwanja vyao hakuna kinachosikika ila tu maombolezo. Mimi nimemvunja Moabu kama chombo kisichotakiwa na mtu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
39 Tazama alivyovunjika! Tazama wanavyoomboleza! Ajabu jinsi Moabu alivyorudi nyuma kwa aibu! Moabu amekuwa kichekesho na kioja kwa jirani zake wote.”
40 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Tazama, taifa litaruka kasi kuivamia Moabu, kama tai aliyekunjua mabawa yake.
41 Miji yake itatekwa, ngome zitachukuliwa. Siku hiyo mioyo ya wanajeshi wa Moabu, itaogopa kama mwanamke anayejifungua.
42 Wamoabu wataangamizwa, wasiwe tena taifa, kwa sababu walijikweza dhidi ya Mwenyezi-Mungu.
43 Kitisho, mashimo na mtego, vinawasubiri enyi watu wa Moabu. Nasema mimi Mwenyezi-Mungu.
44 Atakayetoroka kitisho atatumbukia shimoni; atakayetoka shimoni atanaswa mtegoni. Kwa maana nitaleta mambo hayo juu ya Moabu, katika mwaka wao wa adhabu. Nasema mimi Mwenyezi-Mungu.
45 Wakimbizi wachovu wanatua Heshboni kutaka usalama, maana moto umezuka huko mjini; mwali wa moto toka ikulu ya mfalme Sihoni; umeteketeza mipaka ya Moabu, umeunguza milima yao hao watukutu.
46 Ole wenu watu wa Moabu! Watu wa Kemoshi sasa mmeangamizwa, wana wenu wamechukuliwa mateka, binti zenu wamepelekwa uhamishoni.
47 Lakini siku zijazo nitamstawisha tena Moabu. Nasema mimi Mwenyezi-Mungu. Hii ndiyo hukumu juu ya Moabu.”
1 Kuhusu Waamoni. Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Je, Israeli hana watoto? Je, hana warithi? Mbona basi mungu Milkomu amemiliki Gadi na watu wake kufanya makao yao mijini mwake?
2 Basi, wakati unakuja kweli, siku zaja, nasema mimi Mwenyezi-Mungu, ambapo nitavumisha sauti ya vita dhidi ya Raba mji wa Waamoni. Raba utakuwa rundo la uharibifu, vijiji vyake vitateketezwa moto; ndipo Israeli atakapowamiliki wale waliomiliki. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
3 “Ombolezeni, enyi watu wa Heshboni, maana mji wa Ai umeharibiwa! Lieni enyi binti za Raba! Jifungeni mavazi ya gunia viunoni ombolezeni na kukimbia huko na huko uani! Maana mungu Milkomu atapelekwa uhamishoni, pamoja na makuhani wake na watumishi wake.
4 Mbona mnajivunia mabonde yenu, enyi msioamini, watu mliotegemea mali zenu, mkisema: ‘Nani atathubutu kupigana nasi?’
5 Basi, mimi nitawaleteeni vitisho kutoka kwa jirani zenu wote, nanyi mtafukuzwa nje kila mtu kivyake, bila mtu wa kuwakusanya wakimbizi. Mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi nimesema.
6 Lakini baadaye nitawarudishia Waamoni fanaka yao. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
7 Kuhusu Edomu. Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi: “Je, hakuna tena hekima mjini Temani? Je, wenye busara wao hawana shauri tena? Hekima imetoweka kabisa?
8 Kimbieni enyi wakazi wa Dedani; geukeni mkaishi mafichoni! Maana nitawaleteeni maangamizi enyi wazawa wa Esau; wakati wa kuwaadhibu umefika.
9 Wachuma zabibu watakapokuja kwenu hawatabakiza hata zabibu moja. Usiku ule wezi watakapofika, wataharibu kila kitu mpaka watosheke.
10 Lakini nimemnyanganya Esau kila kitu, naam, nimeyafunua maficho yake, wala hawezi kujificha tena. Watoto, ndugu na jirani zake wameangamizwa; hakuna hata mmoja aliyebaki.
11 Niachieni watoto wenu yatima nami nitawatunza; waacheni wajane wenu wanitegemee.”
12 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Ikiwa wale ambao hawakustahili kunywa kikombe cha adhabu ni lazima wanywe, je, wewe utaachwa bila kuadhibiwa? La! Hutakosa kuadhibiwa; ni lazima unywe hicho kikombe!
13 Maana nimeapa kwa nafsi yangu kwamba mji wa Bosra utakuwa kioja na kichekesho, utakuwa uharibifu na laana; vijiji vyote vitakuwa magofu daima. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
14 Nimepata habari kutoka kwa Mwenyezi-Mungu, mjumbe ametumwa ayatangazie mataifa: “Jikusanyeni pamoja dhidi ya Edomu; inukeni mwende kuushambulia!
15 Mimi Mwenyezi-Mungu nitakufanya wee Edomu kuwa mdogo kuliko mataifa yote. Ulimwengu wote utakudharau.
16 Vitisho unavyotoa na kiburi chako vimekudanganya, ewe ukaaye katika mapango ya miamba, unayeishi juu ya kilele cha mlima! Ingawa unaweka makao yako juu kama ya tai, mimi nitakuporomosha kutoka huko uliko. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
17 “Edomu itakuwa kitisho na kila mtu atakayepita karibu yake atashangaa, na kuizomea kwa sababu ya maafa yatakayoipata.
18 Kama vile Sodoma na Gomora na miji jirani yake ilivyoangamizwa, mimi Mwenyezi-Mungu nasema, hakutakuwa na mtu yeyote atakayeishi Edomu wala kufanya mashauri humo.
19 Kama vile simba anavyochomoza kutoka msitu wa mto Yordani na kuingia kwenye malisho mazuri, ndivyo nitakavyowafukuza ghafla Waedomu kutoka nchi yao. Nami nitamweka huko kiongozi yeyote nitakayemchagua. Maana, ni nani anayeweza kulinganishwa nami? Nani awezaye kunishtaki? Ni mchungaji gani awezaye kunipinga?
20 Kwa hiyo, sikilizeni mpango ambao mimi Mwenyezi-Mungu nimepanga dhidi ya Edomu pamoja na mambo niliyokusudia kuwafanyia wakazi wa Temani: Hakika, watoto wao wadogo wataburutwa na kuchukuliwa; kweli kutakuwa na mshangao mkubwa katika makao yao!
21 Kwa kishindo cha kuanguka kwao, dunia itatetemeka; sauti ya kilio chao itasikika mpaka bahari ya Shamu.
22 Tazama, adui atapanda juu na kuruka kama tai na kutandaza mabawa yake juu ya Bosra. Siku hiyo moyo wa mashujaa wa Edomu utakumbwa na hofu kama ya mwanamke anayejifungua.”
23 Kuhusu Damasko: “Miji ya Hamathi na Arpadi, imejaa wasiwasi kwa kufikiwa na habari mbaya; mioyo ya watu wake inayeyuka kwa hofu, imefadhaika kama bahari isiyoweza kutulia.
24 Watu wa Damasko wamekufa moyo; wamegeuka wapate kukimbia; hofu kubwa imewakumba, uchungu na huzuni vimewapata, kama mwanamke anayejifungua
25 Ajabu kuachwa kwa mji maarufu, mji uliokuwa umejaa furaha!
26 Basi vijana wake wataanguka viwanjani mwake, askari wake wote wataangamizwa siku hiyo. Mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi nimesema.
27 Nitawasha moto katika kuta za Damasko, nao utateketeza ngome za mfalme Ben-hadadi.”
28 Kuhusu Kedari na falme za Hazori ambazo Nebukadneza mfalme wa Babuloni, alizishambulia na kuzishinda, Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Inuka uende kulishambulia kabila la Kedari! Waangamize watu wa mashariki!
29 Hema zao na kondoo wao vitachukuliwa, kadhalika mapazia yao na mali yao yote; watanyanganywa ngamia wao, na kilio kitasikika: ‘Kitisho kila upande!’
30 Kimbieni, nendeni mbali, kaeni mashimoni. Enyi wakazi wa Haziri, kimbieni mtangetange na kukaa mafichoni! Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema. Maana Nebukadneza mfalme wa Babuloni, amefanya mpango dhidi yenu, amepania kuja kuwashambulia.
31 Inuka uende kulishambulia taifa linalostarehe, taifa linaloishi kwa usalama. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema. Taifa hilo halina malango wala pao za chuma; ni taifa ambalo liko peke yake.
32 “Ngamia wao watatekwa mifugo yao itachukuliwa mateka. Nitawatawanya kila upande, watu wale wanaonyoa denge. Nitawaletea maafa kutoka kila upande. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
33 Mji wa Hazori utakuwa makao ya mbweha, utakuwa jangwa daima; hakuna mtu atakayekaa humo, wala atakayeishi humo.”
34 Neno la Mwenyezi-Mungu lililomjia nabii Yeremia kuhusu Elamu, mwanzoni mwa utawala wa Sedekia, mfalme wa Yuda.
35 Mwenyezi-Mungu wa majeshi, asema hivi: “Nitavunja upinde wa watu wa Elamu ulio msingi wa nguvu zao.
36 Nitaleta upepo kutoka pande zote za mbingu; nitawatawanya kila mahali, wala hapatakuwa na taifa lolote ambalo halitakuwa na wakimbizi wa Elamu.
37 Nitawafadhaisha watu wa Elamu mbele ya maadui zao na mbele ya wale wanaotaka kuyaangamiza maisha yao. Nitawaletea maafa na hasira yangu kali. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema. Nitawaletea upanga kuwafuata mpaka niwaangamize kabisa.
38 Nitaweka kiti changu cha enzi huko Elamu na kumwangamiza mfalme wao pamoja na wakuu wao. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
39 Lakini katika siku za mwisho, nitaurudishia mji wa Elamu fanaka yake. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
1 Neno la Mwenyezi-Mungu alilosema kwa njia ya nabii Yeremia kuhusu nchi ya Babuloni na nchi ya Wakaldayo:
2 “Tangazeni kati ya mataifa, twekeni bendera na kutangaza, Msifiche lolote. Semeni: ‘Babuloni umetekwa, Beli ameaibishwa. Merodaki amefadhaishwa; sanamu zake zimeaibishwa, vinyago vyake vimefadhaishwa.’
3 “Kwa maana, taifa kutoka kaskazini limefika kuushambulia; litaifanya nchi yake kuwa uharibifu. Hakuna atakeyeishi humo; watu na wanyama watakimbia mbali.
4 “Siku hizo na wakati huo, nasema mimi Mwenyezi-Mungu, watu wa Israeli na watu wa Yuda watakusanyika pamoja na kurudi wakilia huku wananitafuta mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wao.
5 Watauliza njia ya kwenda Siyoni, huku nyuso zao zimeelekea huko, wakisema, ‘Njoni!’ Nao watajiunga na Mwenyezi-Mungu katika agano la milele ambalo kamwe halitasahauliwa.
6 “Watu wangu walikuwa kondoo waliopotea; wachungaji wao wamewapotosha, wakawageuza kuelekea milimani; walitembea toka mlima hadi kilima, wakasahau zizi lao.
7 Watu wote waliowakuta waliwaua, na maadui zao wamesema, ‘Hatuna hatia sisi’, maana hao wamemkosea Mwenyezi-Mungu aliye malisho yao ya kweli; Mwenyezi-Mungu ambaye ni tegemeo la wazee wao!
8 “Kimbieni kutoka Babuloni! Tokeni nje ya nchi ya Wakaldayo, muwe kama mabeberu mbele ya kundi.
9 Maana, mimi nitachochea mataifa makubwa kutoka nchi ya kaskazini washambulie Babuloni. Watajiandaa kuishambulia Babuloni na kuiteka. Mishale yao ni kama shujaa hodari asiyerudi mikono mitupu.
10 Nchi ya Wakaldayo itaporwa, na hao watakaoipora wataridhika. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
11 “Enyi waporaji wa mali yangu! Japo mnafurahi na kushangilia, mnarukaruka kama mtamba wa ng'ombe anayepura nafaka, na kulia kama farasi dume,
12 nchi yenu ya kuzaliwa itaaibishwa; hiyo nchi mama yenu itafedheheshwa. Lo! Babuloni itakuwa ya mwisho kati ya mataifa, itakuwa nyika kame na jangwa.
13 Kwa sababu ya ghadhabu yangu Mwenyezi-Mungu, Babuloni haitakaliwa kabisa na watu, bali itakuwa jangwa kabisa; kila atakayepita karibu nayo atashangaa ataizomea kwa sababu ya majeraha yake.
14 “Enyi nyote wapiga mishale stadi, shikeni nafasi zenu kuuzingira mji wa Babuloni; upigeni, msibakize mshale hata mmoja, maana umenikosea mimi Mwenyezi-Mungu.
15 Upigieni kelele za vita pande zote, sasa Babuloni umejitoa ukamatwe. Ngome zake zimeanguka, kuta zake zimebomolewa. Ninalipiza kisasi juu ya Babuloni Basi jilipizeni kisasi, utendeeni kama ulivyowatenda wengine.
16 Zuieni watu wasipande mbegu Babuloni, wala wasivune wakati wa mavuno. Kutokana na upanga wa udhalimu, kila mmoja atawarudia watu wake kila mmoja atakimbilia nchini mwake.
17 “Israeli ni kondoo wanaowindwa na kufukuzwa na simba. Kwanza waliangamizwa na mfalme wa Ashuru, na sasa Nebukadneza mfalme wa Babuloni, amevunjavunja mifupa yake.
18 Kwa hiyo, mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, nasema hivi: Nitamwadhibu mfalme wa Babuloni na nchi yake, kama nilivyomwadhibu mfalme wa Ashuru.
19 Nitawarudisha Waisraeli nchini mwao, nao watakula mavuno yatakayolimwa juu ya mlima Karmeli na Bashani na watatosheka kwa chakula kutoka milima ya Efraimu na Gileadi.
20 Siku hizo na wakati huo, uovu utatafutwa nchini Israeli, lakini hautapatikana; dhambi itatafutwa nchini Yuda, lakini haitapatikana; maana mimi nitawasamehe wale ambao nimewabakiza. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
21 “Pandeni, mwiendee nchi ya Merathaimu, nendeni kuishambulia; washambulieni wakazi wa Pekodi na kuwaangamiza kabisa watu wake. Nasema mimi Mwenyezi-Mungu. Fanyeni kila kitu nilichowaamuru.
22 Kelele za vita zinasikika nchini, kuna uharibifu mkubwa.
23 Jinsi gani huo mji uliokuwa nyundo ya dunia nzima unavyoangushwa chini na kuvunjika! Babuloni umekuwa kinyaa miongoni mwa mataifa!
24 Ewe Babuloni, nilikutegea mtego ukanaswa, wala hukujua juu yake; ulipatikana, ukakamatwa, kwa sababu ulishindana nami Mwenyezi-Mungu.
25 Nimefungua ghala yangu ya silaha, nikatoa humo silaha za ghadhabu yangu, maana mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi nina kazi ya kufanya katika nchi ya Wakaldayo.
26 Njoni mkamshambulie kutoka kila upande; zifungueni ghala zake za chakula; mrundikieni marundo ya nafaka! Iangamizeni kabisa nchi hii; msibakize chochote!
27 Waueni askari wake hodari; waache washukie machinjoni. Ole wao, maana siku yao imewadia, wakati wao wa kuadhibiwa umefika.
28 “Sikiliza! Wakimbizi na watoro kutoka nchi ya Babuloni wanakuja kutangaza huko Siyoni jinsi Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, alivyolipiza kisasi kwa ajili ya hekalu lake.
29 “Waiteni wapiga mishale waishambulie Babuloni. Pelekeni kila mtu ajuaye kuvuta upinde. Uzingireni mji pasiwe na yeyote atakayetoroka. Ulipizeni kadiri ya matendo yake yote; utendeeni kama ulivyowatendea wengine, maana kwa kiburi ulinidharau mimi Mwenyezi-Mungu, Mtakatifu wa Israeli.
30 Kwa hiyo, vijana wake watauawa katika mitaa yake, na majeshi yake yote yataangamizwa siku hiyo. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
31 “Mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, napigana nawe ewe mwenye kiburi, maana siku yako ya adhabu imefika, wakati nitakapokuadhibu umewadia.
32 Mwenye kiburi atajikwaa na kuanguka, wala hapatakuwa na mtu wa kumwinua. Nitawasha moto katika miji yake, nao utateketeza kila kitu kandokando yake.”
33 Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi: “Watu wa Israeli wanakandamizwa; hali kadhalika na watu wa Yuda. Wale waliowachukua mateka wamewabana sana na wanakataa kuwaachia.
34 Lakini mimi, Mkombozi wao ni mwenye nguvu. Mwenyezi-Mungu wa Majeshi ndilo jina langu. Hakika nitatetea kisa chao ili nilete amani katika nchi yao, lakini taabu kwa wakazi wa Babuloni.
35 “Kifo kwa Wakaldayo, kwa wakazi wa Babuloni na maofisa na wenye hekima wake!
36 Kifo kwa waaguzi, wanachotangaza ni upumbavu tu! Kifo kwa mashujaa wake, ili waangamizwe!
37 Kifo kwa farasi wake na uharibifu kwa magari yake, kifo kwa majeshi yake yote ya kukodiwa, ili wawe na woga kama wanawake! Uharibifu kwa hazina zake zote ili zipate kuporwa.
38 Ukame uyapate maji ili yapate kukauka! Maana Babuloni ni nchi ya sanamu za miungu, watu ni wendawazimu juu ya vinyago vyao.
39 “Kwa hiyo wanyama wa porini, mbwamwitu pamoja na mbuni, watakaa Babuloni. Hapatakaliwa kamwe na watu vizazi vyote vijavyo.
40 Kama vile mimi Mwenyezi-Mungu nilivyoiangamiza miji ya Sodoma na Gomora na miji ya jirani, vivyo hivyo hapatakuwa na mtu yeyote atakayeishi humo. Naam, hakuna mtu yeyote atakeyekaa huko. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
41 “Tazama! Watu wanakuja kutoka kaskazini; taifa lenye nguvu na wafalme wengi wanajitayarisha kutoka miisho ya dunia.
42 Wameshika pinde zao na mikuki; ni watu wakatili na wasio na huruma. Vishindo vyao ni kama mvumo wa bahari, wamepanda farasi. Wamejipanga tayari kwa vita, dhidi yako wewe Babuloni!
43 Mfalme wa Babuloni amesikia habari zao, nayo mikono yake ikawa kama kamba. Ameshikwa na dhiki na uchungu kama mama anayejifungua.
44 “Tazama, mimi nitakuwa kama simba anayechomoza kutoka msitu wa mto Yordani na kuingia kwenye malisho mazuri: Mimi Mwenyezi-Mungu nitawafukuza ghafla watu wake kutoka kwake. Nami nitamweka huko kiongozi yeyote nitakayemchagua. Maana, ni nani anayeweza kulinganishwa nami? Nani awezaye kunishtaki? Ni mchungaji gani awezaye kunipinga?
45 Kwa hiyo, sikilizeni mpango ambao mimi Mwenyezi-Mungu nimepanga dhidi ya Babuloni pamoja na mambo niliyokusudia kuitendea nchi ya Wakaldayo: Hakika watoto wao wataburutwa na kuchukuliwa; kweli kutakuwa na mshangao mkubwa katika makao yao.
46 Kwa kishindo cha kutekwa kwa Babuloni dunia itatetemeka, na kilio chake kitasikika miongoni mwa mataifa mengine.”
1 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Nitachochea upepo wa kuangamiza dhidi ya Babuloni, dhidi ya wakazi wa Kaldayo.
2 Nitawapeleka wapepetaji Babuloni, nao watampepeta; watamaliza kila kitu katika nchi yake watakapofika kuishambulia toka kila upande wakati wa maangamizi yake.”
3 Usiwape nafasi wapiga mshale wa Babuloni; usiwaache wavute upinde, wala kuvaa mavazi yao ya vita. Usiwahurumie vijana wake; liangamize kabisa jeshi lake.
4 Wataanguka na kuuawa katika nchi ya Wakaldayo, watajeruhiwa katika barabara zake.
5 Lakini Israeli na Yuda hawakuachwa na Mungu wao Mwenyezi-Mungu wa majeshi, ingawa nchi yao imejaa hatia mbele yake yeye Mtakatifu wa Israeli.
6 Kimbieni kutoka Babuloni, kila mtu na ayaokoe maisha yake! Msiangamizwe katika adhabu yake, maana huu ndio wakati wa Mungu wa kulipa kisasi, anaiadhibu Babuloni kama inavyostahili.
7 Babuloni ilikuwa kikombe cha dhahabu mkononi mwa Mwenyezi-Mungu, ambacho kiliilewesha dunia nzima. Mataifa yalikunywa divai yake, hata yakapatwa wazimu.
8 Ghafla Babuloni imeanguka na kuvunjikavunjika; ombolezeni kwa ajili yake! Leteni dawa kutuliza maumivu yake; labda utaweza kuponywa.
9 Tulijaribu kuuponya Babuloni, lakini hauwezi kuponywa. Uacheni, twendeni zetu, kila mmoja katika nchi yake, maana hukumu yake ni kuu mno imeinuka mpaka mawinguni.
10 Mwenyezi-Mungu amethibitisha kuwa hatuna hatia. Twendeni Siyoni tukatangaze matendo ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu.
11 Mwenyezi-Mungu amezichochea roho za wafalme wa Media, kwa maana amenuia kuiangamiza Babuloni. Naam, hicho ndicho kisasi cha Mwenyezi-Mungu; analipiza kisasi kwa ajili ya hekalu lake. Noeni mishale yenu! Chukueni ngao!
12 Twekeni bendera ya vita kushambulia kuta za Babuloni. Imarisheni ulinzi; wekeni walinzi; tayarisheni mashambulizi. Mwenyezi-Mungu amepanga na kutekeleza mambo aliyosema juu ya wakazi wa Babuloni.
13 Nchi hiyo imejaa mito na hazina tele, lakini mwisho wake umefika, uzi wa uhai wake umekatwa.
14 Mwenyezi-Mungu wa majeshi ameapa kwa nafsi yake: “Hakika nitakujaza majeshi mengi kama nzige, nayo yatapiga vigelegele vya ushindi juu yako”
15 Mwenyezi-Mungu ndiye aliyeumba dunia kwa nguvu yake, aliyeuimarisha ulimwengu kwa hekima yake, na kwa maarifa yake akazitandaza mbingu.
16 Anapotoa sauti yake maji hutitima mbinguni, hufanya ukungu upande kutoka mipaka ya dunia. Hufanya umeme umulike wakati wa mvua huvumisha upepo kutoka ghala zake.
17 Kila mtu ni mpumbavu bila maarifa, kila mhunzi anaaibishwa na vinyago vyake; maana sanamu zake ni udanganyifu mtupu, wala hazina pumzi ndani yake.
18 Hazina thamani, ni udanganyifu mtupu; wakati watakapoadhibiwa, nazo zitaangamia.
19 Mungu aliye hazina ya Yakobo si kama hizo, maana yeye ndiye aliyeviumba vitu vyote, na Israeli ni kabila lililo mali yake; Mwenyezi-Mungu wa Majeshi, ndilo jina lake.
20 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Wewe Babuloni ni rungu na silaha yangu ya vita; nakutumia kuyavunjavunja mataifa, nakutumia kuangamiza falme.
21 Nakutumia kuponda farasi na wapandafarasi, magari ya kukokotwa na waendeshaji wake.
22 Ninakutumia kuwaponda wanaume na wanawake, wazee na vijana, wavulana na wasichana.
23 Ninakutumia kuponda wachungaji na makundi yao, wakulima na wanyama wao wa kulimia, wakuu wa mikoa na madiwani.
24 “Nitaiadhibu Babuloni na wakazi wote wa Kaldayo mkiona kwa macho yenu wenyewe, kwa sababu ya uovu wote walioufanya katika Siyoni. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
25 Mimi ninapingana nawe ewe mlima mharibifu, mlima unaoharibu dunia nzima! Nasema mimi Mwenyezi-Mungu. Nitanyosha mkono wangu dhidi yako, nitakuangusha kutoka miambani juu na kukufanya kuwa mlima uliochomwa moto;
26 hata hamna jiwe lako litakalochukuliwa kujengea, hakuna jiwe litakalochukuliwa kuwekea msingi! Utakuwa kama jangwa milele. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
27 Tweka bendera ya vita duniani, piga tarumbeta kati ya mataifa; yatayarishe mataifa kupigana naye; ziite falme kuishambulia; falme za Ararati, Mini na Ashkenazi. Weka majemadari dhidi yake; walete farasi kama makundi ya nzige.
28 Yatayarishe mataifa kupigana naye vita; watayarishe wafalme wa Medi, watawala na mawakili wao, tayarisheni nchi zote katika himaya yake.
29 Nchi inatetemeka na kugaagaa kwa maumivu, maana nia ya Mwenyezi-Mungu kuhusu Babuloni ni thabiti: Ataifanya nchi ya Babuloni kuwa jangwa, ataifanya iwe bila watu.
30 Askari wa Babuloni wameshindwa kupigana, wamebaki katika ngome zao; nguvu zao zimewaishia, wamekuwa kama wanawake. Nyumba za Babuloni zimechomwa moto, malango yake ya chuma yamevunjwa.
31 Tarishi baada ya tarishi wanapiga mbio, mjumbe mmoja anamfuata mjumbe mwingine, kumpasha habari mfalme wa Babuloni kwamba mji wake umevamiwa kila upande.
32 Vivuko vya mto vimetekwa, ngome zimechomwa moto, askari wamekumbwa na hofu.
33 Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli asema hivi: “Babuloni ni kama uwanja wa kupuria nafaka wakati unapotayarishwa. Lakini bado kidogo tu, wakati wa mavuno utaufikia.”
34 Mfalme Nebukadneza wa Babuloni aliuharibu na kuuponda mji wa Yerusalemu aliuacha kama chungu kitupu; aliumeza kama joka. Alijaza tumbo lake vitu vyake vizurivizuri, akautupilia mbali kama matapishi.
35 Watu wa Yerusalemu na waseme: “Babuloni na ulipizwe ukatili uleule, tuliotendwa sisi pamoja na jamaa zetu! Babuloni ipatilizwe kwa umwagaji wa damu yetu.”
36 Kwa hiyo asema hivi Mwenyezi-Mungu: “Nitawatetea kuhusu kisa chenu, na kulipiza kisasi kwa ajili yenu. Nitaikausha bahari ya Babuloni na kuvifanya visima vyake vikauke.
37 Babuloni itakuwa rundo la magofu, itakuwa makao ya mbweha, itakuwa kinyaa na kitu cha kuzomewa; hakuna mtu atakayekaa huko.
38 Wababuloni watanguruma pamoja kama simba; watakoroma kama wanasimba.
39 Wakiwa na uchu mkubwa nitawaandalia karamu: Nitawalewesha mpaka wapepesuke; nao watalala usingizi wa daima na hawataamka tena. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
40 Nitawashusha chini kama kondoo wa kuchinjwa, kama vile kondoo dume na beberu.
41 Ajabu kutekwa kwa Babuloni; mji uliosifika duniani kote umechukuliwa! Babuloni umekuwa kinyaa kati ya mataifa!
42 Bahari imefurika juu ya Babuloni, Babuloni imefunikwa mawimbi yaliyochafuka.
43 Miji yake imekuwa kinyaa, nchi ya ukavu na jangwa, nchi isiyokaliwa na mtu yeyote, wala kupitika na binadamu yeyote.
44 Nitamwadhibu mungu Beli huko Babuloni, nitamfanya akitoe alichokimeza. Mataifa hayatamiminika tena kumwendea. Ukuta wa Babuloni umebomoka.
45 “Tokeni humo enyi watu wangu! Kila mtu na ayasalimishe maisha yake, kutoka hasira kali ya Mwenyezi-Mungu.
46 Msife moyo wala msiwe na hofu, kwa sababu ya uvumi mnaosikia nchini. Mwaka huu kuna uvumi huu, mwaka mwingine uvumi mwingine; uvumi wa ukatili katika nchi, mtawala mmoja dhidi ya mtawala mwingine.
47 Kweli siku zaja, nitakapoadhibu sanamu za Babuloni; nchi yake yote itatiwa aibu, watu wake wote watauawa humohumo.
48 Kisha mbingu, dunia na vyote vilivyomo vitaimba kwa furaha kuhusu kuanguka kwa Babuloni, waangamizi watakapofika kutoka kaskazini kuushambulia. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
49 Babuloni umesababisha vifo duniani kote; sasa wenyewe utaangamizwa kwa mauaji ya Israeli.
50 “Nyinyi mlinusurika kifo, ondokeni sasa, wala msisitesite! Ingawa mko nchi ya mbali mkumbukeni Mwenyezi-Mungu, ukumbukeni pia mji wa Yerusalemu.
51 Mnasema: ‘Tumeaibishwa na kufadhaishwa; aibu imezifunika nyuso zetu, kwa sababu wageni wameingia katika sehemu takatifu za nyumba ya Mwenyezi-Mungu.’
52 “Kwa hiyo, wakati unakuja, nasema mimi Mwenyezi-Mungu, ambapo nitaviadhibu vinyago vya Babuloni, na majeruhi watapiga kite katika nchi yake yote.
53 Ingawa Babuloni atapanda mpaka mbinguni, na kuziimarisha ngome zake ndefu, waangamizi watakuja kutoka kwangu kumvamia. 2Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
54 “Sikiliza! Kilio kinasikika kutoka Babuloni! Kishindo cha maangamizi makubwa kutoka nchi ya Wakaldayo!
55 Maana mimi Mwenyezi-Mungu naiangamiza Babuloni, na kuikomesha kelele yake kubwa. Adui ananguruma kama mawimbi ya maji mengi, sauti ya kishindo chao inaongezeka.
56 Naam, mwangamizi anaijia Babuloni; askari wake wametekwa, pinde zao zimevunjwavunjwa. Mimi Mwenyezi-Mungu ni Mungu mwenye kuadhibu, hakika mimi nitalipiza kisasi kamili.
57 Nitawalewesha wakuu na wenye hekima wake, watawala wake, madiwani na askari wake; watalala usingizi wa milele wasiinuke tena. Nasema mimi mfalme ambaye jina langu ni Mwenyezi-Mungu wa Majeshi.
58 “Mimi Mwenyezi-Mungu wa Majeshi nasema: Ukuta mpana wa Babuloni utabomolewa mpaka chini, na malango yake marefu yatateketezwa kwa moto. Watu wanafanya juhudi za bure, mataifa yanajichosha maana mwisho wao ni motoni!”
59 Mnamo mwaka wa nne wa utawala wake, mfalme Sedekia alikwenda Babuloni pamoja na ofisa wa askari wake aitwaye Seraya mwana wa Neria na mjukuu wa Maseya. Kutokana na fursa hiyo mimi Yeremia nilimpa Seraya ujumbe.
60 Nilikuwa nimeandika kitabuni maafa yote niliyotangaza juu ya Babuloni na pia maneno mengine kuhusu Babuloni.
61 Nilimwambia Seraya: “Utakapofika Babuloni ni lazima uwasomee wote ujumbe huu.
62 Kisha umalizie na maneno haya: ‘Ee Mwenyezi-Mungu, wewe umesema kwamba utapaharibu mahali hapa hata pasikaliwe na kiumbe chochote, mwanadamu au mnyama, na kwamba nchi hii itakuwa jangwa milele.’
63 Utakapomaliza kusoma kitabu hiki, kifungie jiwe, kisha ukitumbukize katikati ya mto Eufrate, ukisema:
64 ‘Hivi ndivyo mji wa Babuloni utakavyozama, wala hautainuka tena, kwa sababu ya maafa ambayo Mwenyezi-Mungu anauletea.’” Mwisho wa maneno ya Yeremia.
1 Sedekia alikuwa na umri wa miaka ishirini na mmoja alipoanza kutawala. Alitawala kwa muda wa miaka kumi na mmoja huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Hamutali binti Yeremia, mkazi wa mji wa Liba.
2 Alitenda maovu mbele ya Mwenyezi-Mungu kama mabaya yote aliyotenda Yehoyakimu.
3 Mwenyezi-Mungu aliwakasirikia sana watu wa Yerusalemu na Yuda hata akawafukuza mbali naye. Sedekia alimwasi mfalme wa Babuloni.
4 Ikawa katika siku ya kumi ya mwezi wa kumi, mwaka wa tisa wa kutawala kwake Sedekia, Nebukadneza mfalme wa Babuloni, alifika na jeshi lake lote kuushambulia Yerusalemu, wakauzingira kila upande.
5 Mji uliendelea kuzingirwa mpaka mwaka wa kumi na moja wa utawala wa Sedekia.
6 Katika siku ya tisa ya mwezi wa nne, njaa ilikuwa kali sana mjini hata hapakuwa na chakula chochote kwa ajili ya wakazi wake.
7 Basi, sehemu ya ukuta wa mji ilibomolewa, nao askari walikimbia wakatoka nje ya mji wakati wa usiku wakipitia njia ya lango katikati ya kuta mbili, kwenye bustani ya mfalme, wakaenda upande wa Araba, ingawa Wakaldayo walikuwa wameuzunguka mji wote. Waisraeli walikimbia kuelekea bonde la mto Yordani.
8 Lakini jeshi la Wakaldayo lilimfuatia mfalme na kumteka katika tambarare za Yeriko, jeshi lake lote likatawanyika na kumwacha.
9 Basi Wakaldayo walimteka mfalme, wakampeleka kwa mfalme wa Babuloni, huko Ribla, katika nchi ya Hamathi, naye akamhukumu.
10 Hukohuko Ribla, mfalme wa Babuloni aliwaua wana wa Sedekia mbele ya baba yao. Aliwaua pia maofisa wote wa Yuda.
11 Kisha aliyangoa macho ya Sedekia na kumfunga pingu, akamchukua Sedekia Babuloni na kumtia kizuizini mpaka siku alipokufa.
12 Katika siku ya kumi ya mwezi wa tano, mwaka wa kumi na tisa wa utawala wa Nebukadneza, mfalme wa Babuloni, Nebuzaradani kapteni wa walinzi wa mfalme ambaye alimtumikia mfalme wa Babuloni, aliingia Yerusalemu.
13 Alichoma moto nyumba ya Mwenyezi-Mungu, ikulu na nyumba zote za Yerusalemu; kila nyumba kubwa ilichomwa moto.
14 Askari wote wa Wakaldayo waliokuwa pamoja na kapteni wa walinzi, walizibomoa kuta zote zilizouzunguka mji wa Yerusalemu.
15 Nebuzaradani kapteni wa walinzi wa mfalme, aliwachukua uhamishoni watu waliokuwa wamebakia mjini na wale waliokuwa wamejisalimisha kwa mfalme wa Babuloni pamoja na mafundi.
16 Lakini Nebuzaradani kapteni wa walinzi wa mfalme, aliwaacha baadhi ya watu waliokuwa maskini kabisa nchini, wawe watunza mizabibu na wakulima.
17 Wakaldayo walivunja vipandevipande nguzo za shaba nyeusi ambazo zilikuwa katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu pamoja na vikalio na birika kubwa la shaba nyeusi lililokuwamo katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu, wakaichukua shaba nyeusi yote mpaka Babuloni.
18 Kadhalika, walichukua vyungu, sepetu, mikasi, makarai, vijiko vikubwa na vyombo vyote vya shaba nyeusi vilivyotumiwa katika huduma ya hekalu.
19 Pia kapteni wa walinzi wa mfalme alichukua vibakuli, vyetezo, mabirika, vyungu, vinara vya taa, vijiko vikubwa na mabakuli ya sadaka za vinywaji, vyombo hivyo vikiwa vya dhahabu au vya fedha.
20 Kuhusu vitu Solomoni alivyotengeneza: Nguzo mbili, birika kubwa moja na sanamu za fahali kumi na mbili za shaba nyeusi ambazo zilikuwa chini ya hilo birika kubwa pamoja na vikalio, shaba nyeusi ya vitu hivi vyote ilikuwa na uzito mwingi sana.
21 Kila moja ya nguzo hizo mbili ilikuwa na urefu wa mita 8, mzingo wake mita 5.25, na unene wa milimita 75, zote zilikuwa wazi ndani.
22 Juu ya kila nguzo kulikuwa na kichwa cha shaba nyeusi; urefu wa kila kichwa ulikuwa mita 2 na sentimita 20. Kila kichwa kilizungushiwa mapambo ya wavu ya makomamanga, yote ya shaba nyeusi.
23 Kulikuwa na makomamanga tisini na sita ubavuni mwa nguzo hizo; jumla ya makomamanga yote ilikuwa 100 na mapambo kandokando yake.
24 Kisha Nebuzaradani kapteni wa walinzi wa mfalme, alimchukua mateka Seraya kuhani mkuu, na Sefania kuhani wa pili, pamoja na walinda mlango watatu;
25 na kutoka mjini alimchukua ofisa mmoja ambaye alikuwa akiongoza askari vitani, pamoja na watu saba washauri wa mfalme ambao aliwakuta mjini. Kadhalika alimchukua katibu wa kamanda mkuu wa jeshi ambaye alitunza kumbukumbu za jeshi pamoja na watu mashuhuri sitini ambao aliwakuta mjini Yerusalemu.
26 Nebuzaradani kapteni wa walinzi wa mfalme, aliwachukua watu hao na kuwapeleka kwa mfalme wa Babuloni huko Ribla.
27 Mfalme Nebukadneza wa Babuloni aliwapiga na kuwaua watu hao huko Ribla katika nchi ya Hamathi. Basi, watu wa Yuda walikwenda uhamishoni nje ya nchi yao.
28 Ifuatayo ni idadi ya watu ambao Nebukadneza aliwachukua uhamishoni mnamo mwaka wa saba wa utawala wake: Alichukua Wayahudi 3,023;
29 mwaka wa kumi na nane wa utawala wake, alichukua kutoka Yerusalemu mateka 832;
30 mwaka wa ishirini na tatu wa utawala wake Nebukadneza, Nebuzaradani kapteni wa walinzi wa mfalme, alichukua mateka Wayahudi 745. Jumla ya mateka wote ilikuwa watu 4,600.
31 Mnamo mwaka wa thelathini na saba tangu Yehoyakini mfalme wa Yuda alipopelekwa uhamishoni, siku ya ishirini na tano ya mwezi wa kumi na mbili, Evil-merodaki mfalme wa Babuloni, mwaka uleule alipofanywa mfalme, alimsamehe Yehoyakini mfalme wa Yuda, akamtoa gerezani.
32 Aliongea naye vizuri na kumpa nafasi ya heshima kuliko wafalme wengine waliokuwa pamoja naye uhamishoni huko Babuloni.
33 Basi, Yehoyakini alibadili mavazi yake ya kifungoni, akawa anapata chakula chake daima mezani kwa mfalme.
34 Daima alipewa posho na mfalme wa Babuloni kulingana na mahitaji yake ya kila siku, mpaka alipofariki.