1 Maneno ya Amosi, mmojawapo wa wachungaji wa mji wa Tekoa. Mungu alimfunulia Amosi mambo haya yote kuhusu Israeli miaka miwili kabla ya lile tetemeko la ardhi, wakati Uzia alipokuwa mfalme wa Yuda, na Yeroboamu mwana wa Yoashi, alipokuwa mfalme wa Israeli.
2 Amosi alisema hivi: Mwenyezi-Mungu ananguruma kutoka mlima Siyoni, anavumisha sauti yake kutoka Yerusalemu, hata malisho ya wachungaji yanakauka, nyasi mlimani Karmeli zinanyauka.
3 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Watu wa Damasko wametenda dhambi tena na tena; kwa hiyo, sitaacha kuwaadhibu; waliwatendea watu wa Gileadi ukatili mbaya.
4 Basi, nitaishushia moto ikulu ya mfalme Hazaeli, nao utaziteketeza kabisa ngome za mfalme Ben-hadadi.
5 Nitayavunjavunja malango ya mji wa Damasko, na kuwang'oa wakazi wa bonde la Aweni, pamoja na mtawala wa Beth-edeni. Watu wa Aramu watapelekwa uhamishoni Kiri. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
6 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Watu wa Gaza wametenda dhambi tena na tena, kwa hiyo sitaacha kuwaadhibu. Walichukua mateka watu kabila zima, wakawauza wawe watumwa kwa Waedomu.
7 Basi, nitazishushia moto kuta za mji wa Gaza, nao utaziteketeza kabisa ngome zake.
8 Nitawang'oa wakazi wa mji wa Ashdodi, pamoja na mtawala wa Ashkeloni. Nitanyosha mkono dhidi ya Ekroni, nao Wafilisti wote waliosalia wataangamia. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
9 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Watu wa Tiro wametenda dhambi tena na tena, kwa hiyo sitaacha kuwaadhibu. Walichukua mateka kabila zima hadi Edomu, wakaukiuka mkataba wa urafiki waliokuwa wamefanya.
10 Basi, nitazishushia moto kuta za mji wa Tiro, na kuziteketeza kabisa ngome zake.”
11 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Watu wa Edomu wametenda dhambi tena na tena, kwa hiyo sitaacha kuwaadhibu. Waliwawinda ndugu zao Waisraeli kwa mapanga, wakaitupilia mbali huruma yao yote ya kindugu. Hasira yao haikuwa na kikomo, waliiacha iwake daima.
12 Basi, nitaushushia moto mji wa Temani, na kuziteketeza kabisa ngome za Bosra.”
13 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Watu wa Amoni wametenda dhambi tena na tena, kwa hiyo sitaacha kuwaadhibu. Katika vita vyao vya kupora nchi zaidi, waliwatumbua wanawake waja wazito nchini Gileadi.
14 Basi, nitazishushia moto kuta za mji wa Raba, na kuziteketeza kabisa ngome zake. Siku hiyo ya vita patakuwa na makelele mengi, nayo mapambano yatakuwa makali kama tufani.
15 Mfalme wao na maofisa wake, wote watakwenda kukaa uhamishoni. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
1 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Watu wa Moabu wametenda dhambi tena na tena, kwa hiyo sitaacha kuwaadhibu. Wamemkosea heshima marehemu mfalme wa Edomu kwa kuichoma moto mifupa yake ili kujitengenezea chokaa!
2 Basi, nitaishushia moto nchi ya Moabu, na kuziteketeza kabisa ngome za mji wa Keriothi. Wanajeshi watakapopaza sauti zao na kupiga tarumbeta, watu wa Moabu watakufa katika makelele hayo ya vita.
3 Isitoshe, nitamuua mtawala wa Moabu, pamoja na viongozi wote wa nchi hiyo. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
4 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Watu wa Yuda wametenda dhambi tena na tena, kwa hiyo sitaacha kuwaadhibu. Wamepuuza sheria zangu, wala hawakufuata amri zangu. Wamepotoshwa na miungu ileile waliyoihudumia wazee wao.
5 Basi, nitaishushia moto nchi ya Yuda, na kuziteketeza kabisa ngome za Yerusalemu.”
6 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Waisraeli wametenda dhambi tena na tena, kwa hiyo sitaacha kuwaadhibu. Wamewauza watu waaminifu kwa kuwa hawakuweza kulipa madeni yao; na kuwauza watu fukara wasioweza kulipa deni la kandambili.
7 Huwanyanyasa na kuwakandamiza wanyonge, na maskini huwabagua wasipate haki zao. Mtu na baba yake hulala na mjakazi yuleyule, hivyo hulitia unajisi jina langu takatifu.
8 Popote penye madhabahu, watu hulalia nguo walizotwaa kwa maskini kama dhamana ya madeni yao; na katika nyumba ya Mungu wao hunywa divai waliyotwaa kwa wadeni wao.
9 “Hata hivyo, enyi watu wangu, kwa ajili yenu, niliwaangamiza kabisa Waamori ambao walikuwa wakubwa kama mierezi, wenye nguvu kama miti ya mialoni. Naam, niliwaangamiza, matawi na mizizi.
10 Niliwatoeni kutoka nchi ya Misri, nikawaongoza kupitia jangwani miaka arubaini, mpaka mkaichukua nchi ya Waamori kuwa yenu.
11 Niliwateua baadhi ya wana wenu wawe manabii, na baadhi ya vijana wenu wawe wanadhiri. Je, enyi Waisraeli, haya nisemayo si ya kweli? Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
12 Lakini nyinyi mliwafanya wanadhiri wanywe divai, na kuwaamuru manabii wasitoe unabii.
13 “Sasa basi, nitawagandamiza mpaka chini, kama gari lililojaa nafaka.
14 Hata wapiga mbio hodari hawataweza kutoroka; wenye nguvu wataishiwa nguvu zao, na askari watashindwa kuyaokoa maisha yao.
15 Wapiga upinde vitani hawatastahimili; wapiga mbio hodari hawataweza kujiokoa, wala wapandafarasi hawatayanusurisha maisha yao.
16 Siku hiyo, hata askari hodari watatimua mbio bila chochote. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
1 Enyi Waisraeli, sikilizeni neno Mwenyezi-Mungu alilosema dhidi yenu, enyi taifa zima alilolitoa nchini Misri:
2 “Kati ya mataifa yote ulimwenguni, ni nyinyi tu niliowachagua. Kwa hiyo nitawaadhibu nyinyi, kwa sababu ya uovu wenu wote.”
3 Je, watu wawili huanza safari pamoja, bila ya kufanya mpango pamoja kwanza?
4 Je, simba hunguruma porini kama hajapata mawindo? Je, mwanasimba hunguruma pangoni mwake kama hajakamata kitu?
5 Je, mtego bila chambo utamnasa ndege? Je, mtego hufyatuka bila kuguswa na kitu?
6 Je, baragumu ya vita hulia mjini bila kutia watu hofu? Je, mji hupatwa na janga asilolileta Mungu?
7 Hakika, Bwana Mwenyezi-Mungu hafanyi kitu bila kuwafunulia watumishi wake manabii nia yake.
8 Simba akinguruma, ni nani asiyeogopa? Bwana Mwenyezi-Mungu akinena, ni nani atakataa kuutangaza ujumbe wake?
9 Tangazeni katika ikulu za Ashdodi, na katika ikulu za nchi ya Misri: “Kusanyikeni kwenye milima inayoizunguka nchi ya Samaria, mkajionee msukosuko mkubwa na dhuluma zinazofanyika humo.”
10 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Watu hawa wameyajaza majumba yao vitu vya wizi na unyang'anyi. Hawajui kabisa kutenda yaliyo sawa!
11 Kwa hiyo, adui ataizingira nchi yao, atapaharibu mahali pao pa kujihami, na kuziteka nyara ikulu zao.”
12 Mwenyezi-Mungu, asema hivi: “Kama vile mchungaji ampokonyavyo simba kinywani miguu miwili tu au kipande cha sikio la kondoo, ndivyo watakavyonusurika watu wachache tu wa Israeli wakaao Samaria, ambao sasa wanalalia vitanda vizuri na matandiko ya hariri.”
13 Bwana Mungu wa majeshi asema hivi: “Sikilizeni, mkawaonye wazawa wa Yakobo:
14 Siku nitakapowaadhibu Waisraeli kwa sababu ya makosa yao, nitayaharibu pia madhabahu ya mji wa Betheli. Nitazikata pembe za kila madhabahu na kuziangusha chini.
15 Nitaziharibu nyumba zote mjini na vijijini; nitazibomoa nyumba zilizopambwa kwa pembe, majumba makubwamakubwa hayatasalia hata moja. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
1 Sikilizeni neno hili, enyi wanawake ng'ombe wa Bashani mlioko huko mlimani Samaria; nyinyi mnaowaonea wanyonge, mnaowakandamiza maskini, na kuwaambia waume zenu: “Tuleteeni divai tunywe!” Sikilizeni ujumbe huu:
2 Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu Mtakatifu nimeapa: “Tazama, siku zaja, ambapo watu watawakokoteni kwa kulabu, kila mmoja wenu kama samaki kwenye ndoana.
3 Mtaburutwa hadi ukutani palipobomolewa, na kutupwa nje. Nasema mimi Mwenyezi-Mungu.
4 “Enyi Waisraeli, nendeni basi huko Betheli mkaniasi! Nendeni Gilgali mkalimbikize makosa yenu! Toeni sadaka zenu kila asubuhi, na zaka zenu kila siku ya tatu.
5 Toeni tambiko ya shukrani ya mikate iliyochachushwa. Tangazeni popote kwamba mmetoa kwa hiari; kwani ndivyo mnavyopenda kufanya! Mimi Bwana Mungu nimenena.
6 “Mimi niliwanyima chochote cha kutafuna, nikasababisha ukosefu wa chakula popote. Hata hivyo hamkunirudia. Nasema mimi Mwenyezi-Mungu.
7 “Tena niliwanyima mvua miezi mitatu tu kabla ya mavuno. Niliunyeshea mvua mji mmoja, na mji mwingine nikaunyima. Shamba moja lilipata mvua, na lingine halikupata, likakauka.
8 Watu wa miji miwili, mitatu wakakimbilia mji mwingine, wapate maji, lakini hayakuwatosha. Hata hivyo hamkunirudia. Nasema mimi Mwenyezi-Mungu.
9 “Niliwapiga pigo la ukame na ukungu; nikakausha bustani na mashamba yenu ya mizabibu; nzige wakala mitini na mizeituni yenu. Hata hivyo hamkunirudia. Nasema mimi Mwenyezi-Mungu.
10 “Niliwaleteeni ugonjwa wa tauni kama ule nilioupelekea Misri. Niliwaua vijana wenu vitani, nikawachukua farasi wenu wa vita. Maiti zilijaa katika kambi zenu, uvundo wake ukajaa katika pua zenu. Hata hivyo hamkunirudia. Nasema mimi Mwenyezi-Mungu.
11 “Niliwaangusha baadhi yenu kwa maangamizi kama nilivyoangamiza Sodoma na Gomora. Wale walionusurika miongoni mwenu, walikuwa kama kijiti kilichookolewa motoni. Hata hivyo hamkunirudia. Nasema mimi Mwenyezi-Mungu.
12 “Kwa hiyo, enyi Waisraeli, nitawaadhibu. Na kwa kuwa nitafanya jambo hilo, kaeni tayari kuikabili hukumu yangu!”
13 Mungu ndiye aliyeifanya milima, na kuumba upepo; ndiye amjulishaye mwanadamu mawazo yake; ndiye ageuzaye mchana kuwa usiku, na kukanyaga vilele vya dunia. Mwenyezi-Mungu wa Majeshi ndilo jina lake!
1 Sikilizeni maombolezo yangu juu yenu, enyi Waisraeli:
2 Umeanguka na hutainuka tena ewe binti Israeli! Umeachwa pweke nchini mwako, hamna hata mtu wa kukuinua.
3 Maana Bwana Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Watu 1,000 watatoka mjini kwenda kupigana lakini watarejea 100 tu; wataondoka watu 100 wa kijiji kimoja lakini watanusurika watu kumi tu.”
4 Mwenyezi-Mungu awaambia hivi Waisraeli: “Nitafuteni mimi nanyi mtaishi!
5 Lakini msinitafute huko Betheli wala msiende Gilgali wala msivuke kwenda Beer-sheba. Maana wakazi wa Gilgali, hakika watachukuliwa uhamishoni, na Betheli utaangamizwa!”
6 Mtafuteni Mwenyezi-Mungu, nanyi mtaishi! La sivyo, atawalipukia wazawa wa Yosefu kama moto; moto utawateketeza wakazi wa Betheli na hakuna mtu atakayeweza kuuzima.
7 Tahadhari enyi mnaogeuza haki kuwa uchungu, na kuuona uadilifu kuwa kama takataka!
8 Huyo aliyezifanya Kilimia na sayari Orioni, ambaye huligeuza giza nene kuwa mchana, na mchana kuwa usiku; yeye ambaye ayaitaye pamoja maji ya bahari na kuyamwaga juu ya nchi kavu, Mwenyezi-Mungu ndilo jina lake.
9 Yeye ndiye anayewaangamiza wenye nguvu, na kuziharibu ngome zao.
10 Nyinyi huwachukia watetezi wa haki na wenye kusema ukweli mahakamani.
11 Nyinyi mnawakandamiza fukara na kuwatoza kodi ya ngano kupita kiasi. Mnajijengea nyumba za mawe ya kuchonga, lakini nyinyi hamtaishi humo; mnalima bustani nzuri za mizabibu, lakini hamtakunywa divai yake.
12 Maana mimi najua wingi wa makosa yenu na ukubwa wa dhambi zenu; nyinyi mnawatesa watu wema, mnapokea rushwa na kuzuia fukara wasipate haki mahakamani.
13 Basi, kutakuwa na wakati mbaya ambao hata mwenye busara atanyamaza.
14 Tafuteni kutenda mema na si mabaya, ili nyinyi mpate kuishi naye Mwenyezi-Mungu wa majeshi awe pamoja nanyi kama mnavyosema.
15 Chukieni uovu, pendeni wema, na kudumisha haki mahakamani. Yamkini Mwenyezi-Mungu wa majeshi atawafadhili watu wa Yosefu waliobaki.
16 Basi, Mwenyezi-Mungu, Mungu wa majeshi, naam, Mwenyezi-Mungu asema: “Patakuwa na kilio kila mahali mitaani; watu wataomboleza: ‘Ole! Ole!’ Wakulima wataitwa waje kuomboleza, na mabingwa wa kuomboleza waje kufanya matanga.
17 Patakuwa na kilio katika mashamba yote ya mizabibu; maana nitapita kati yenu kuwaadhibu. Nasema mimi Mwenyezi-Mungu.”
18 Ole wenu nyinyi mnaoingojea kwa hamu siku ya Mwenyezi-Mungu! Kwa nini mnaitaka sana siku hiyo? Siku hiyo, itakuwa siku ya giza na sio ya mwanga!
19 Mambo yatakuwa kama mtu aliyekimbia simba, halafu akakumbana na dubu! Au kama mtu anayerudi nyumbani kwake, akatia mkono ukutani, akaumwa na nyoka.
20 Siku ya Mwenyezi-Mungu itakuwa giza, na sio mwanga; itakuwa huzuni bila uangavu wowote.
21 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Nazichukia na kuzidharau sikukuu zenu; siifurahii mikutano yenu ya kidini.
22 Mjaponitolea sadaka zenu za kuteketezwa na za nafaka, mimi sitakubali kuzipokea; na sadaka zenu za amani za wanyama wanono mimi sitaziangalia kabisa.
23 Ondoeni mbele yangu kelele za nyimbo zenu! Sitaki kusikiliza muziki wa vinubi vyenu!
24 Lakini acheni haki itiririke kama maji, uadilifu uwe kama mto usiokauka.
25 “Enyi Waisraeli, wakati ule mlipokuwa kule jangwani kwa miaka arubaini, je, mliniletea tambiko na sadaka hata mara moja?
26 Je, wakati huo mlibeba kama sasa vinyago vya mungu wenu Sakuthi mfalme wenu na vinyago vya Kaiwani mungu wenu wa nyota, vitu ambavyo mlijitengenezea wenyewe?
27 Kwa hiyo nitawapeleka uhamishoni, mbali kuliko Damasko! Hayo amesema Mwenyezi-Mungu, ambaye jina lake ni Mungu wa Majeshi.
1 Ole wenu nyinyi mnaostarehe huko Siyoni, nanyi mnaojiona salama mlimani Samaria! Nyinyi mwaonekana kuwa viongozi wa taifa maarufu ambao Waisraeli wote huwategemea.
2 Haya! Nendeni Kalne mkaangalie kila mahali, tokeni huko mwende hadi mji ule mkubwa wa Hamathi, kisha teremkeni hadi Gathi kwa Wafilisti. Je, falme zao si bora kuliko zenu na eneo lao si bora kuliko lenu?”
3 Nyinyi mnajaribu kuifukuza siku mbaya. Lakini mnauleta karibu utawala dhalimu.
4 Ole wenu mnaolala juu ya vitanda vya pembe za ndovu na kujinyosha juu ya masofa, mkila nyama za wanakondoo na ndama!
5 Nyinyi mnapenda kuimba ovyo na sauti ya vinubi na kubuni ala mpya za muziki mkimwiga mfalme Daudi.
6 Mnakunywa divai kwa mabakuli, na kujipaka marashi mazuri mno. Lakini hamhuzuniki hata kidogo juu ya kuangamia kwa wazawa wa Yosefu.
7 Kwa hiyo mtakuwa wa kwanza kwenda uhamishoni, na karamu za wenye kustarehe zitatoweka.
8 Bwana Mwenyezi-Mungu ameapa kwa nafsi yake; Mwenyezi-Mungu, Mungu wa majeshi asema: “Nachukizwa mno na kiburi cha wazawa wa Yakobo; tena nayachukia majumba yao ya fahari. Mji wao na vyote vilivyomo nitawapa adui zao.”
9 Kama wakibaki watu kumi katika nyumba moja, wote watakufa.
10 Na atakapokuja mjomba wa aliyekufa kuitoa maiti nje aichome, akamwuliza yeyote atakayekuwako ndani pembeni mwa nyumba, “Je kuna mtu mwingine pamoja nawe?” Naye atamjibu, “La! Hamna!” Naye atamwambia, “Nyamaza kimya! Tusilitaje hata jina la Mwenyezi-Mungu.”
11 Tazama! Mwenyezi-Mungu anatoa amri, nalo jumba kubwa labomoka vipandevipande, na nyumba ndogo kusagikasagika.
12 Je, farasi waweza kupiga mbio miambani? Je, watu huilima bahari kwa ng'ombe? Lakini nyinyi mmeigeuza haki kuwa sumu, na tunda la uadilifu kuwa uchungu.
13 Nyinyi mnashangilia juu ya Lodebari, na kusema mmeuteka Karnaimu kwa nguvu zenu wenyewe.
14 Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi: “Enyi Waisraeli, kweli nitaleta taifa moja lije kuwashambulia, nalo litawatesa nyinyi kuanzia Lebo-hamathi kaskazini, hadi kijito cha Araba, upande wa kusini.”
1 Siku moja, Bwana Mwenyezi-Mungu alinijalia maono: Nilimwona Mungu anaumba nzige kundi zima, mara baada ya watu kumaliza kukata nyasi kwa ajili ya wanyama wa mfalme. Wakati huo, nyasi zilikuwa ndio zinaanza kuchipua tena.
2 Niliwaona nzige hao wakila na kumaliza kila jani katika nchi. Ndipo nikasema: “Ee Bwana Mwenyezi-Mungu, nakusihi utuhurumie! Wazawa wa Yakobo watawezaje kuishi? Wao ni wadogo mno!”
3 Basi, Bwana Mwenyezi-Mungu akabadili nia yake, akasema, “Haitakuwa hivyo!”
4 Bwana Mwenyezi-Mungu alinijalia maono mengine: Nilimwona Bwana Mwenyezi-Mungu akiuita moto wa hukumu ya kuwaadhibu watu. Moto huo uliunguza vilindi vikuu vya bahari, ukaanza kuiteketeza nchi kavu.
5 Ndipo nikasema: “Ee Bwana Mwenyezi-Mungu, nakusihi uache kuadhibu! Wazawa wa Yakobo watawezaje kuishi? Wao ni wadogo mno!”
6 Basi, Mwenyezi-Mungu akabadili nia yake, akasema: “Hili pia halitatukia.”
7 Mwenyezi-Mungu alinijalia tena maono mengine: Nilimwona Mwenyezi-Mungu amesimama karibu na ukuta, ameshika mkononi mwake uzi wenye timazi.
8 Naye akaniuliza: “Amosi, unaona nini?” Nikamjibu, “Naona timazi.” Kisha Mwenyezi-Mungu akasema: “Tazama! Naweka timazi kati ya watu wangu Waisraeli. Sitavumilia tena maovu yao.
9 Huko vilimani ambako wazawa wa Isaka hutambikia, kutafanywa kuwa uharibifu mtupu na maskani ya Waisraeli yatakuwa magofu. Nitaushambulia kwa vita ukoo wa mfalme Yeroboamu.”
10 Basi, Amazia kuhani wa mji wa Betheli, akampelekea mfalme Yeroboamu wa Israeli habari hizi: “Amosi analeta fitina juu yako katika ufalme wa Israeli. Hotuba zake ni hatari kwa nchi hii.
11 Anachosema ni hiki: ‘Yeroboamu atakufa kwa upanga nao Waisraeli watapelekwa uhamishoni, mbali kabisa na nchi yao.’”
12 Kisha Amazia akamwambia Amosi, “Sasa tumekuchoka, ewe nabii! Nenda zako! Rudi katika nchi ya Yuda, ukatoe unabii huko upate na ujira wako hukohuko.
13 Usitoe tena unabii hapa mjini Betheli, kwa kuwa hapa ni maskani ya ibada ya mfalme; ni hekalu la utawala huu.”
14 Amosi akamjibu Amazia, “Mimi si nabii wa kuajiriwa, wala si mmoja wa kikundi cha manabii. Mimi ni mchungaji na mtunza mikuyu.
15 Mwenyezi-Mungu alinitoa katika kazi yangu hiyo ya uchungaji, akaniamuru nije kuwaambia unabii watu wake wa Israeli.
16 Nawe basi, ewe Amazia, sikiliza neno la Mwenyezi-Mungu: Wewe waniambia nisitoe unabii dhidi ya Israeli, wala nisihubiri dhidi ya wazawa wa Isaka.
17 Kwa hiyo, Mwenyezi-Mungu asema hivi: ‘Mkeo atakuwa malaya mjini, na wanao wa kiume na kike watauawa vitani. Ardhi yako itagawanywa na kupewa wengine, nawe binafsi utafia katika nchi najisi, nao Waisraeli hakika watapelekwa uhamishoni, mbali kabisa na nchi yao.’”
1 Bwana Mwenyezi-Mungu alinijalia maono mengine: Niliona kikapu kilichojaa matunda ya kiangazi.
2 Naye Mwenyezi-Mungu akaniuliza: “Amosi, unaona nini?” Nami nikamjibu, “Naona kikapu cha matunda ya kiangazi.” Kisha Mwenyezi-Mungu akaniambia: “Mwisho umewafikia watu wangu wa Israeli. Sitavumilia tena maovu yao.
3 Siku hiyo, nyimbo za ikulu zitakuwa maombolezo. Kutakuwa na maiti nyingi, nazo zitatupwa nje kimyakimya.”
4 Sikilizeni enyi mnaowakandamiza wanyonge na kuwaletea maangamizi fukara wa nchi.
5 Mnajisemea mioyoni mwenu: “Sikukuu ya mwezi mwandamo itakwisha lini ili tuanze tena kuuza nafaka yetu? Siku ya Sabato itakwisha lini ili tupate kuuza ngano yetu? Tutatumia vipimo hafifu vya wastani na uzito, tutadanganya watu kwa mizani isizo sawa,
6 hata kuuza ngano hafifu kwa bei kubwa. Tutaweza kununua watu fukara kwa fedha, na wahitaji kwa jozi ya kandambili.”
7 Mwenyezi-Mungu, fahari ya Yakobo, ameapa: “Hakika, sitayasahau matendo yao maovu.
8 Kwa hiyo, dunia itatetemeka na kila mtu nchini ataomboleza. Nchi yote itayumbayumba; itapanda na kushuka, kama yanavyojaa na kupwa maji ya mto Nili!”
9 Bwana Mwenyezi-Mungu asema, “Siku hiyo nitalifanya jua litue adhuhuri, na kuijaza nchi giza mchana.
10 Sherehe zenu nitazigeuza kuwa kilio, na nyimbo zenu za furaha kuwa maombolezo. Nitawafanya nyote mvae magunia kwa huzuni na kunyoa vipara vichwa vyenu, kama kuomboleza kifo cha mtoto wa pekee; na siku ya mwisho itakuwa ya uchungu mkubwa.”
11 Bwana Mwenyezi-Mungu asema, “Siku zaja ambapo nitaleta njaa nchini. Lakini sio njaa na kiu ya chakula na maji, bali njaa ya kusikia maneno ya Mwenyezi-Mungu.
12 Watu watatangatanga kutoka bahari hata bahari, kutoka upande wa kaskazini mpaka mashariki. Watakimbia huko na huko wakitafuta neno la Mwenyezi-Mungu, lakini hawatalipata.
13 “Siku hiyo, hata vijana wenye afya, wa kiume kwa wa kike, watazimia kwa kiu.
14 Wale wanaoapa kwa mungu wa uongo wa Samaria, na kusema: ‘Kwa nafsi ya mungu wako ee Dani’; na, ‘Kwa nafsi ya mungu wa Beer-sheba’, wote wataanguka na hawatainuka tena kamwe.”
1 Nilimwona Mwenyezi-Mungu amesimama kando ya madhabahu, naye akaniamuru: “Zipige hizo nguzo za hekalu mpaka misingi yake itikisike. Zivunje hizo nguzo ziwaangukie watu vichwani. Wale watakaosalia nitawaua kwa upanga; hakuna hata mmoja wao atakayenusurika, naam, hakuna atakayetoroka.
2 Wajapojichimbia njia ya kwenda kuzimu, huko nitawachukua kwa mkono wangu; wajapopanda mbinguni, nitawaporomosha chini.
3 Wajapojificha juu ya mlima Karmeli, huko nitawasaka na kuwachukua; wajapojificha mbali nami vilindini mwa bahari, humo nitaliamuru joka la baharini liwaume.
4 Wajapochukuliwa mateka na adui zao, huko nitatoa amri wauawe kwa upanga. Nitawachunga kwa makini sana niwatendee mabaya na si mema.”
5 Bwana Mwenyezi-Mungu wa majeshi, anaigusa ardhi nayo inatetemeka na wakazi wake wanaomboleza; dunia nzima inapanda na kushuka kama kujaa na kupwa kwa mto Nili wa Misri.
6 Mwenyezi-Mungu amejenga makao yake mbinguni, nayo dunia akaifunika kwa anga; huyaita maji ya bahari, na kuyamwaga juu ya nchi kavu. Mwenyezi-Mungu, ndilo jina lake!
7 Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Kwangu mimi, nyinyi Waisraeli, hamna tofauti yoyote na watu wa Kushi! Niliwatoa Wafilisti kutoka Krete, na Waashuru kutoka Kiri, kama nilivyowatoa nyinyi kutoka Misri.
8 Mimi, Bwana Mwenyezi-Mungu nautazama ufalme wenye dhambi, na nitauangamiza kabisa kutoka duniani. Lakini sitawaangamiza wazawa wote wa Yakobo.
9 “Tazama, nitatoa amri, na kuwapepeta Waisraeli kati ya mataifa kama mtu achekechavyo nafaka niwakamate wote wasiofaa.
10 Wenye dhambi miongoni mwa watu wangu, watafia vitani kwa upanga; hao ndio wasemao: ‘Maafa hayatatukumba wala kutupata!’
11 “Siku yaja nitakapoisimika nyumba ya Daudi iliyoanguka; nitazitengeneza kuta zake, na kusimika upya magofu yake. Nitaijenga upya kama ilivyokuwa hapo zamani.
12 Nao Waisraeli watamiliki mabaki ya Edomu na mataifa yote yaliyokuwa yangu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema, na nitafanya hivyo.
13 “Wakati waja kwa hakika, ambapo mara baada ya kulima mavuno yatakuwa tayari kuvunwa; mara baada ya kupanda mizabibu utafuata wakati wa kuvuna zabibu. Milima itabubujika divai mpya, navyo vilima vitatiririka divai.
14 Nitarekebisha hali ya watu wangu Waisraeli. Watajenga miji yao iliyoharibiwa na kuishi humo; watapanda mizabibu na kunywa divai yake; watalima mashamba na kula mazao yake.
15 Nitawasimika katika nchi yao, wala hawatang'olewa tena kutoka katika nchi niliyowapa. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”