1 Adamu alimzaa Sethi, Sethi akamzaa Enoshi, Enoshi akamzaa Kenani,
2 Kenani akamzaa Mahalaleli, Mahalaleli akamzaa Yaredi,
3 Yaredi akamzaa Henoki, Henoki akamzaa Methusela. Methusela alimzaa Lameki,
4 Lameki akamzaa Noa. Noa alikuwa na wana watatu: Shemu, Hamu na Yafethi.
5 Wana wa Yafethi walikuwa Gomeri, Magogu, Madai, Yavani, Tubali, Mesheki na Tirasi.
6 Wana wa Gomeri walikuwa Ashkenazi, Difathi na Togama.
7 Wana wa Yavani walikuwa Elisha, Tarshishi, Kitimu na Rodanimu.
8 Wana wa Hamu walikuwa Kushi, Misri, Puti na Kanaani.
9 Wana wa Kushi walikuwa Seba, Havila, Sabta, Raama na Sabteka. Wana wa Raama walikuwa Sheba na Dedani.
10 Kushi alimzaa Nimrodi, aliyekuwa mtu shujaa wa kwanza duniani.
11 Wazawa wa Misri ni Waludi, Waanamu, Walehabi, Wanaftuhi,
12 Wapathrusi Wakaftori na Wakasluhi (hao ndio asili ya Wafilisti).
13 Wana wa Kanaani walikuwa Sidoni, mzaliwa wake wa kwanza, na Hethi.
14 Kanaani pia ndiye babu yao Wayebusi, Waamori, Wagirgashi,
15 Wahivi, Waarki, Wasini,
16 Waarvadi, Wasemari na Wahamathi.
17 Wana wa Shemu walikuwa Elamu, Ashuri, Arpaksadi, Ludi, Aramu, Usi, Huli, Getheri na Mesheki.
18 Arpaksadi alimzaa Shela, Shela akamzaa Eberi.
19 Eberi alikuwa na wana wawili; mmoja wao aliitwa Pelegi, (kwa maana wakati wake watu walikuwa wametawanyika duniani), na ndugu yake aliitwa Yoktani.
20 Wana wa Yoktani walikuwa Almodadi, Shelefu, Hasarmawethi, Yera,
21 Hadoramu, Uzali, Dikla,
22 Obali, Abimaeli, Sheba,
23 Ofiri, Havila na Yobabu. Hao watu ni wana wa Yoktani.
24 Ukoo wa Abrahamu kutokea Shemu ni kama ifuatavyo: Shemu alimzaa Arpaksadi, naye Arpaksadi akamzaa Shela.
25 Shela akamzaa Eberi, Eberi akamzaa Pelegi, Pelegi akamzaa Reu;
26 Reu akamzaa Serugi, Serugi akamzaa Nahori, Nahori akamzaa Tera,
27 na Tera akamzaa Abramu, ambaye ndiye Abrahamu.
28 Abrahamu alikuwa na watoto wawili wa kiume: Isaka na Ishmaeli.
29 Hivi ndivyo vizazi vyao: Mzaliwa wa kwanza wa Ishmaeli alikuwa Nebayothi na wengine ni Kedari, Adbeeli, Mibsamu,
30 Mishma, Duma, Masa, Hadadi, Tema,
31 Yeturi, Nafishi na Kedema. Hao ndio wana wa Ishmaeli.
32 Abrahamu alikuwa na suria aliyeitwa Ketura. Ketura alimzalia Abrahamu: Zimrani, Yokshani, Medani, Midiani, Ishbaki na Shua. Wana wa Yokshani walikuwa Sheba na Dedani.
33 Wana wa Midiani walikuwa: Efa, Eferi, Henoki, Abida na Eldaa. Wote hao walikuwa wazawa wa Ketura.
34 Isaka, mwana wa Abrahamu, alikuwa na wana wawili: Esau na Israeli.
35 Wana wa Esau walikuwa Elifazi, Reueli, Yeushi, Yalamu na Kora.
36 Wana wa Elifazi walikuwa Temani, Omari, Sefo, Gatamu, Kenazi, Timna na Amaleki.
37 Wana wa Reueli walikuwa Nahathi, Zera, Shama na Miza.
38 Wana wa Seiri walikuwa Lotani, Shobali, Sibeoni, Ana, Dishoni, Eseri na Dishani.
39 Wana wa Lotani walikuwa wawili: Hori na Homamu. Lotani alikuwa na dada yake aliyeitwa Timna.
40 Wana wa Shobali walikuwa Alvani, Manahathi, Ebali, Shefi na Onamu. Wana wa Sibeoni walikuwa Aya na Ana.
41 Mwana wa Ana alikuwa Dishoni; na wana wa Dishoni walikuwa Hamrani, Eshbani, Ithrani na Kerani.
42 Wana wa Eseri walikuwa Bilhani, Zaawani na Akani; na wana wa Dishoni walikuwa Usi na Arani.
43 Wafuatao ndio wafalme waliotawala nchi ya Edomu kabla mfalme yeyote hajatawala Waisraeli: Bela mwana wa Beori alitawala nchi ya Edomu, akiwa na makao yake makuu katika mji wa Dinhaba.
44 Bela alipofariki, Yobabu mwana wa Zera kutoka Bosra alitawala badala yake.
45 Yobabu alipofariki, Hushamu wa nchi ya Watemi alitawala badala yake.
46 Hushamu alipofariki, Hadadi mwana wa Bedadi alitawala badala yake, makao yake makuu yakiwa katika mji wa Avithi. Huyu ndiye aliyewapiga na kuwashinda Wamidiani katika nchi ya Moabu.
47 Hadadi alipofariki, Samla kutoka Masreka alitawala badala yake.
48 Samla alipofariki, Shauli kutoka Rehobothi ulio karibu na mto Eufrate, alitawala badala yake.
49 Shauli alipofariki, Baal-hanani mwana wa Akbori alitawala badala yake.
50 Baal-hanani alipofariki, Hadadi kutoka Pai alitawala badala yake na jina la mkewe Akbori lilikuwa Mehetabeli, binti Matredi, binti Mezahabu.
51 Naye Hadadi akafariki. Wakuu wa makabila ya Edomu walikuwa Timna, Alva, Yethethi,
52 Oholibama, Ela, Pinoni,
53 Kenazi, Temani, Mibsari,
54 Magdieli na Iramu. Hao ndio wakuu wa makabila ya Edomu.
1 Israeli alikuwa na wana wa kiume kumi na wawili: Reubeni, Simeoni, Lawi, Yuda, Isakari, Zebuluni,
2 Dani, Yosefu, Benyamini, Naftali, Gadi na Asheri.
3 Wana wa Yuda waliozaliwa na Bethshua, mkewe Mkanaani, walikuwa Eri, Onani na Shela. Eri, mzaliwa wa kwanza wa Yuda, alikuwa mwovu mbele ya Mwenyezi-Mungu, basi Mwenyezi-Mungu akamuua.
4 Na Tamari, mkwewe, alimzalia wana wawili: Peresi na Zera. Jumla, wana wa Yuda walikuwa watano.
5 Peresi alikuwa na wana wawili: Hesroni na Hamuli.
6 Zera nduguye alikuwa na wana watano: Zimri, Etheni, Hemani, Kalkoli na Dara.
7 Mwana wa Karmi, alikuwa Akari. Huyu aliwaletea Waisraeli taabu kwa sababu alijiwekea nyara zilizokuwa zimewekwa wakfu.
8 Ethani alikuwa na mwana mmoja, jina lake Azaria.
9 Wana wa Hesroni walikuwa Yerameeli, Ramu na Kelubai.
10 Ramu alimzaa Aminadabu, Aminadabu akamzaa Nashoni, mkuu wa kabila la Yuda.
11 Nashoni alimzaa Salma, Salma akamzaa Boazi,
12 Boazi akamzaa Obedi, Obedi akamzaa Yese.
13 Yese aliwazaa Eliabu, mwanawe wa kwanza, wa pili Abinadabu, wa tatu Shimea,
14 wa nne Nethaneli, wa tano Radai,
15 wa sita Osemu na wa saba Daudi.
16 Dada zao walikuwa Seruya na Abigaili. Wana wa Seruya walikuwa watatu: Abishai, Yoabu na Asaheli.
17 Abigaili alimzaa Amasa ambaye baba yake alikuwa Yetheri, Mwishmaeli.
18 Kalebu, mwana wa Hesroni, kutokana na wake zake wawili, Azuba na Yeriothi, aliwazaa Yesheri, Shaobabu na Ardoni.
19 Azuba alipofariki, Kalebu alimwoa Efratha aliyemzalia Huri.
20 Huri alimzaa Uri, naye Uri akamzaa Besaleli.
21 Hesroni alipokuwa na umri wa miaka sitini, alimwoa binti Makiri, dada yake Gileadi. Huyo alimzalia mwana jina lake Segubu.
22 Segubu alimzaa Yairi ambaye alitawala miji mikubwa ishirini na mitatu katika nchi ya Gileadi.
23 Lakini falme za Geshuri na Aramu ziliwashambulia na kuwanyanganya miji ya Haroth-yairi, Kenathi na vijiji vyake, jumla miji sitini. Hao wote walikuwa wazawa wa Makiri, baba yake Gileadi.
24 Baada ya Hesroni kufariki, Kalebu alimwoa Efratha, mjane wa Hesroni, baba yake. Efratha alimzalia Kalebu mwana jina lake Ashuri, aliyekuwa mwanzilishi wa mji wa Tekoa.
25 Yerameeli, mzaliwa wa kwanza wa Hesroni, alikuwa na wana watano: Ramu, mzaliwa wake wa kwanza, Buna, Oreni, Osemu na Ahiya.
26 Yerameeli alikuwa na mke mwingine jina lake Atara. Huyu alimzalia Yerameeli mwana, jina lake Onamu.
27 Wana wa Ramu, mzaliwa wa kwanza wa Yerameeli, walikuwa Maasi, Yamini na Ekeri.
28 Wana wa Onamu walikuwa Shamai na Yada. Nao wana wa Shamai walikuwa Nadabu na Abishuri.
29 Abishuri alioa mke, jina lake Abihaili, naye akamzalia wana wawili: Abani na Molidi.
30 Wana wa Nadabu walikuwa Seledi na Apaimu; lakini Seledi alifariki bila watoto.
31 Apaimu alikuwa na mwana mmoja aliyeitwa Ishi. Ishi alimzaa Sheshani, na Sheshani akamzaa Alai.
32 Yada, nduguye Shamai, alikuwa na wana wawili: Yetheri na Yonathani. Lakini Yetheri alifariki bila watoto.
33 Yonathani alikuwa na wana wawili: Pelethi na Zaza. Wote hao ni wazawa wa Yerameeli.
34 Sheshani hakuwa na watoto wa kiume; alikuwa na binti tu. Hata hivyo, alikuwa na mtumwa wa Kimisri, jina lake Yarha.
35 Hivyo, Sheshani akamwoza Yarha mtumwa wake, mmoja wa binti zake, naye akamzalia mwana jina lake Atai.
36 Atai alimzaa Nathani, Nathani akamzaa Zabadi.
37 Zabadi akamzaa Eflali, Eflali akamzaa Obedi,
38 Obedi akamzaa Yehu, Yehu akamzaa Azaria,
39 Azaria akamzaa Helesi, Helesi akamzaa Eleasa,
40 Eleasa akamzaa Sismai, Sismai akamzaa Shalumu,
41 Shalumu akamzaa Yekamia, na Yekamia akamzaa Elishama.
42 Mzaliwa wa kwanza wa Kalebu, nduguye Yerameeli, aliitwa Mesha. Mesha alimzaa Zifu, Zifu akamzaa Maresha, Maresha akamzaa Hebroni.
43 Hebroni alikuwa na wana wanne: Kora, Tapua, Rekemu na Shema.
44 Shema alikuwa baba yake Rahamu na babu yake Rekemu. Rekemu nduguye Shema alimzaa Shamai,
45 Shamai akamzaa Maoni, na Maoni akamzaa Beth-suri.
46 Kalebu alikuwa na suria, jina lake Efa. Huyu alimzalia wana wengine watatu: Harani, Mosa na Gazezi. Harani alimzaa Gazezi.
47 Yadai alikuwa na wana sita: Regemu, Yothamu, Geshani, Peleti, Efa na Shaafu.
48 Kalebu alikuwa na suria mwingine jina lake Maaka. Huyu alimzalia wana wawili: Sheberi na Tirhana.
49 Maaka alimzalia Kalebu wana; Shaafu mwanzilishi wa mji wa Madmana, na Sheva, mwanzilishi wa mji wa Makbena na Gibea. Kalebu alikuwa pia na binti, jina lake Aksa.
50 Kalebu alikuwa na wazawa wengine pia kwa mkewe Efratha. Huri, mzaliwa wake wa kwanza, alikuwa na wana watatu: Shobali, mwanzilishi wa mji wa Kiriath-yearimu,
51 wa pili Salma, mwanzilishi wa mji wa Bethlehemu, na wa tatu Herefu, mwanzilishi wa mji wa Bethi-gaderi.
52 Shobali, mwanzilishi wa mji wa Kiriath-yearimu, alikuwa pia babu yao watu wa Haroe, na nusu ya wakazi wa mji wa Menuhothi,
53 pamoja na koo zifuatazo zilizoishi Kiriath-yearimu: Waithri, Waputhi, Washumathi na Wamishrai. (Wasorathi na Waeshtaoli walitokana na watu hao).
54 Salma, mwanzilishi wa mji wa Bethlehemu alikuwa babu ya Wanetofathi, Waatroth-beth-yoabu na nusu ya Wamenahathi yaani Wasori.
55 Jamaa zifuatazo za waandishi ziliishi katika mji wa Yabesi: Watirathi, Washimeathi na Wasukathi. Wao ndio Wakeni waliotoka katika uzao wa Hamathi, aliyekuwa babu yao waliokuwa wa ukoo wa Warekabu.
1 Hawa ndio wana wa mfalme Daudi waliozaliwa wakati alipokuwa huko Hebroni: Amnoni, mzaliwa wake wa kwanza; mama yake aliitwa Ahinoamu, Myezreeli; wa pili Danieli ambaye mama yake alikuwa Abigaili, Mkarmeli;
2 wa tatu alikuwa Absalomu, ambaye mama yake alikuwa Maaka, bintiye Talmai mfalme wa Geshuri; wa nne alikuwa Adoniya, ambaye mama yake alikuwa Hagithi;
3 wa tano alikuwa Shefatia, ambaye mama yake alikuwa Abitali; na wa sita alikuwa Ithreamu, ambaye mama yake alikuwa Egla.
4 Wote sita, walizaliwa Hebroni ambako Daudi alitawala kwa muda wa miaka saba na nusu. Huko Yerusalemu, alitawala kwa muda wa miaka thelathini na mitatu.
5 Wafuatao ni wana wa mfalme Daudi alipokuwa Yerusalemu: Mkewe Bathshua, bintiye Amieli, alimzalia wana wanne: Himea, Shobabu, Nathani na Solomoni.
6 Na mbali na hao alikuwa na wana wengine tisa: Ibhari, Elishua, Elifaleti,
7 Noga, Nefegi, Yafia,
8 Elishama, Eliada na Elifeleti.
9 Hao wote walikuwa wana wa Daudi, mbali na wale wengine waliozaliwa na masuria wake. Daudi alikuwa na binti pia, aliyeitwa Tamari.
10 Wazawa wa mfalme Solomoni: Solomoni alimzaa Rehoboamu, aliyemzaa Abiya, aliyemzaa Asa, aliyemzaa Yehoshafati,
11 aliyemzaa Yehoramu, aliyemzaa Ahazia, aliyemzaa Yoashi,
12 aliyemzaa Amazia, aliyemzaa Uzia, aliyemzaa Yothamu,
13 aliyemzaa Ahazi, aliyemzaa Hezekia, aliyemzaa Manase,
14 aliyemzaa Amoni, aliyemzaa Yosia.
15 Yosia alikuwa na wana wanne: Yohanani, mzaliwa wake wa kwanza, wa pili Yehoyakimu, wa tatu Sedekia na wa nne Shalumu.
16 Yehoyakimu alikuwa na wana wawili: Yekonia na Sedekia.
17 Wana wa Yekonia aliyechukuliwa mateka na Wababuloni walikuwa saba: Shealtieli,
18 Malkiramu, Pedaya, Shenazari, Yekamia, Hoshama na Nedabia.
19 Wana wa Pedaya walikuwa Zerubabeli na Shimei. Zerubabeli alikuwa na wana wawili: Meshulamu na Hanania, na binti mmoja, jina lake Shelomithi.
20 Zerubabeli pia alikuwa na wana wengine watano: Hashuba, Oheli, Berekia, Hasadia na Yushab-hesedi.
21 Wana wa Hanania walikuwa Pelatia na Yeshaya. Yeshaya alimzaa Refaya, aliyemzaa Arnani, aliyemzaa Obadia, aliyemzaa Shekania.
22 Shekania alimzaa Shemaya. Wana wa Shemaya walikuwa sita: Hatushi, Igali, Baria, Nearia na Shafati.
23 Nearia alikuwa na wana watatu: Eliehonai, Hizkia na Azrikamu.
24 Eliehonai alikuwa na wana saba: Hodavia, Eliashibu, Pelaya, Akubu, Yohanani, Delaya na Anani.
1 Wana wa Yuda walikuwa Peresi, Hesroni, Karmi, Huri na Shobali.
2 Reaya, mwana wa Shobali, alimzaa Yahathi, aliyekuwa baba yake Ahumai na Lahadi, hizo ndizo jamaa za Wasorathi.
3 Wana wa Etamu walikuwa Yezreeli, Ishma na Idbashi. Walikuwa na dada mmoja aliyeitwa Haselelponi.
4 Penueli aliwazaa Gedori na Ezeri, na Ezeri akamzaa Husha. Hao ndio wazawa wa Huri mzaliwa wa kwanza wa Efratha, baba yake Bethlehemu.
5 Ashuru, mwanzilishi wa mji wa Tekoa, alikuwa na wake wawili: Hela na Naara.
6 Naara alimzalia wana wanne: Ahuzamu, Heferi, Temeni na Haahashtari.
7 Hela alimzalia wana watatu: Serethi, Ishari na Ethnani.
8 Hakosi aliwazaa Anubi na Sobeba, na ndiye aliyekuwa baba wa jamaa za wazawa wa Aharheli, mwana wa Harumu.
9 Kulikuwa na mtu mmoja jina lake Yabesi, aliyeheshimiwa kuliko ndugu zake wote. Mama yake alimpa jina la Yabesi kwa sababu alimzaa kwa maumivu.
10 Lakini Yabesi alimwomba Mungu wa Israeli akisema, “Ee Mungu, nakusihi unibariki na kuipanua mipaka yangu. Mkono wako uwe pamoja nami na unilinde kutokana na jambo lolote ovu, lisiniumize.” Naye Mungu akamjalia yale aliyoomba.
11 Kelubu, nduguye Shuha, alimzaa Mehiri na Mehiri akamzaa Eshtoni.
12 Eshtoni alikuwa na wana watatu: Beth-rafa, Pasea na Tehina. Tehina alikuwa mwanzilishi wa mji wa Ir-nahashi. Wazawa wa watu hawa waliishi Reka.
13 Wana wa Kenazi walikuwa: Othnieli na Seraya; na wana wa Othnieli walikuwa Hathathi na Meonothai.
14 Meonothai alimzaa Ofra. Seraya alimzaa Yoabu, mwanzilishi wa Bonde la Mafundi, lililopewa jina hilo kwa sababu wote waliokuwa humo walikuwa mafundi stadi.
15 Kalebu mwana wa Yefune alikuwa na wana watatu: Iru, Ela na Naamu. Na mwana wa Ela alikuwa Kenazi.
16 Wana wa Yehaleli walikuwa Zifu, Zifa, Tiria na Asareli.
17 Wana wa Ezra walikuwa Yetheri, Meredi, Eferi na Yaloni. Meredi alimwoa Bithia, bintiye Farao, na hawa ndio wana aliomzalia Meredi: Miriamu, Shamai na Ishba, mwanzilishi wa mji wa Eshtemoa.
18 Meredi alikuwa na mke mwingine Myahudi. Huyu alimzalia Yeredi, mwanzilishi wa Mji wa Gedori, Heberi, mwanzilishi wa mji wa Soko, na Yekuthieli, mwanzilishi wa Mji wa Zanoa.
19 Hodia alimwoa dada yake Nahamu ambaye wazawa wake ndio waanzilishi wa kabila la Garmi, lililoishi katika mji wa Keila, na kabila la Maakathi, lililoishi katika mji wa Eshtemoa.
20 Wana wa Shimoni walikuwa Amnoni, Rina, Ben-hanani na Tiloni. Ishi alikuwa na wana wawili: Zohethi na Ben-zohethi.
21 Wana wa Shela, mwana wa Yuda, walikuwa Eri, mwanzilishi wa mji wa Leka, Laada, mwanzilishi wa mji Maresha; ukoo wa wafuma nguo za kitani waliokuwa wakiishi katika mji wa Beth-ashbea;
22 Yokimu na watu walioishi katika mji wa Kozeba; na Yoashi na Sarafi waliotawala huko Moabu na wakarejea Lehemu. (Taarifa hizi ni za zamani sana.)
23 Hawa ndio wafinyanzi walioishi katika miji ya Netaimu na Gedera, wakimhudumia mfalme.
24 Simeoni alikuwa na wana watano: Nemueli, Yamini, Yaribu, Zera na Shauli.
25 Mwana wa Shauli alikuwa Shalumu; Shalumu alimzaa Mibsamu na Mibsamu akamzaa Mishma.
26 Mishma alimzaa Hamueli, aliyemzaa Zakuri, na Zakuri akamzaa Shimei.
27 Shimei alikuwa na wana kumi na sita na binti sita, lakini ndugu zake hawakuwa na wana wengi, na jamii yake pia haikuongezeka kama kabila la Yuda.
28 Miji walimokuwa wakiishi ilikuwa Beer-sheba, Molada, Hasar-shuali,
29 Bilha, Ezemu, Toladi;
30 Bethueli, Horma, Siklagi,
31 Beth-markabothi, Hazar-susimu, Beth-biri na Shaaraimu. Hiyo ndiyo miji yao mpaka wakati wa utawala wa mfalme Daudi.
32 Pia, waliishi katika miji mingine mitano: Etamu, Aini, Rimoni, Tokeni na Ashani,
33 pamoja na vijiji kandokando ya miji hiyo huko Baali. Hayo ndiyo yaliyokuwa makao yao, nao waliweka kumbukumbu ya nasaba yao.
34 Watu wafuatao walikuwa wakuu wa koo zao: Meshobabu, Yamleki, Yosha mwana wa Amazia,
35 Yoeli, Yehu (mwana wa Yoshibia, mwana wa Seraya, mwana wa Asieli.)
36 Eliehonai, Yaakoba, Yeshohaya, Asaya, Adieli, Yesimieli, Benaya,
37 Ziza (mwana wa Shifi, mwana wa Aloni, mwana wa Yedaya, mwana wa Shimri na mwana wa Shemaya).
38 Jamaa zao waliendelea kuongezeka kwa wingi sana. Hawa waliotajwa majina ni wakuu katika jamaa zao na koo zao ziliongezeka sana.
39 Walienea hadi kwenye lango la mji wa Gedori, upande wa mashariki wa bonde, ili kuwatafutia kondoo wao malisho.
40 Hapo, walipata malisho tele, tena mazuri sana na pia nchi ilikuwa wazi, tulivu na yenye amani, kwani wenyeji wa nchi hiyo wa hapo awali walikuwa Wahamu.
41 Katika siku za mfalme Hezekia wa Yuda, watu hao waliotajwa majina yao walikwenda huko Gedori, wakaharibu hema za Wameuni waliokuwa wakiishi huko na kuwafukuza kabisa mpaka leo. Walifanya makao yao ya kudumu huko kwa sababu kulikuwa na malisho tele kwa ajili ya kondoo wao.
42 Watu wengine wa kabila la Simeoni wapatao 500 walikwenda mpaka kwenye mlima Seiri. Waliongozwa na Pelatia, Nearia, Refaya na Uzieli, wana wa Ishi.
43 Hapo waliwaua Waamaleki waliosalia baada ya kunusurika, na wakaishi huko mpaka leo.
1 Hawa ndio wazawa wa Reubeni, mzaliwa wa kwanza wa Israeli. (Ingawa Reubeni alikuwa mzaliwa wa kwanza haki yake ya mzaliwa wa kwanza ilipewa Yosefu nduguye kwa sababu Reubeni alilala na suria wa baba yake. Hivyo, yeye hakutiwa katika orodha ya ukoo kulingana na haki yake ya mzaliwa wa kwanza.
2 Ingawa kabila la Yuda ndilo lililokuja kuwa lenye nguvu zaidi kuliko mengine, na watawala walitoka humo, haki ya mzaliwa wa kwanza ilikuwa ya Yosefu).
3 Wana wa Reubeni, mzaliwa wa kwanza wa Israeli, walikuwa Henoki, Palu, Hesroni na Karmi.
4 Wazawa wa Yoeli toka kizazi hadi kizazi walikuwa Shemaya, Gogi, Shimei,
5 Mika, Reaya, Baali,
6 na Beera, ambaye mfalme Tiglath-pileseri wa Ashuru, alimchukua mateka ingawa alikuwa kiongozi wa Wareubeni, akampeleka uhamishoni.
7 Wakuu wa koo wafuatao waliandikishwa katika orodha ya kumbukumbu ya kabila la Reubeni, Yeieli, Zekaria,
8 Bela, mwana wa Azazi na mjukuu wa Shema, wa ukoo wa Yoeli, uliokuwa ukiishi Aroeri na katika eneo lote la kaskazini hadi Bela na Baal-meoni.
9 Pia, kwa maana mifugo yao iliongezeka kwa wingi sana, walisambaa upande wa mashariki hadi kwenye maingilio ya jangwa lililoenea hadi mto Eufrate.
10 Katika siku za mfalme Shauli, kabila la Reubeni lilizusha vita dhidi ya Wahajiri, wakawaua vitani na kuitwaa ardhi yao yote mashariki mwa Gileadi, wakaishi humo.
11 Kabila la Gadi lilipakana na kabila la Reubeni upande wa kaskazini, katika nchi ya Bashani iliyoenea mashariki hadi Saleka.
12 Yoeli ndiye aliyekuwa mwanzilishi wa ukoo ulioongoza, wa pili Shafamu. Yanai na Shefati walikuwa waanzilishi wa koo nyingine huko Bashani.
13 Ndugu zao kulingana na koo zao walikuwa saba: Mikaeli, Meshulamu, Sheba, Yorai, Yaakani, Zia na Eberi.
14 Wote hawa walikuwa wana wa Abihaili, aliyekuwa mwana wa Huri, mwana wa Yaroa, mwana wa Yeshishai, mwana wa Yado, mwana wa Buzi.
15 Ahi, aliyekuwa mwana wa Abdieli na mjukuu wa Guni, alikuwa mkuu katika koo hizi.
16 Waliishi katika sehemu ya Gileadi, katika Bashani na miji yake na katika malisho yote ya Sharoni, hadi mipakani.
17 Watu hao wote waliandikishwa katika koo, katika siku za Yothamu, mfalme wa Yuda, na Yeroboamu, mfalme wa Israeli.
18 Makabila ya Reubeni, Gadi na Manase ya mashariki, yalikuwa na wanajeshi shupavu wapatao 44,760, wenye ngao na mapanga, wavuta pinde stadi vitani.
19 Walipigana vita na makabila ya Wahajiri, Yeturi, Nafishi na Nodabu.
20 Waliweka tumaini lao kwa Mungu na wakamwomba awasaidie, naye akaitikia ombi lao na kuwatia mikononi mwao Wahajiri pamoja na marafiki zao.
21 Waliteka nyara ngamia 50,000, kondoo 250,000, punda 2,000 na mateka hai 100,000.
22 Waliua maadui wengi sana kwa sababu vita hivyo vilikuwa ni vita vya Mungu. Nao waliendelea kuishi katika nchi hiyo, mpaka wakati wa uhamisho.
23 Watu wa Manase ya mashariki waliishi katika nchi ya Bashani. Idadi yao iliongezeka kwa wingi sana, wakasambaa upande wa kaskazini hadi Baal-hermoni, Seniri na mlima Hermoni.
24 Wafuatao ndio waliokuwa wakuu wa koo za kabila hilo: Eferi, Ishi, Elieli, Azrieli, Yeremia, Hodavia na Yadieli. Wote walikuwa askari shujaa, watu mashuhuri sana na viongozi katika koo hizo.
25 Lakini watu walimwasi Mungu wa babu zao, wakafanya uzinzi kwa kuabudu miungu ya wakazi wa nchi hizo ambazo Mungu aliziangamiza mbele yao.
26 Basi, Mungu wa Israeli akamfanya Pulu, mfalme wa Ashuru, (ambaye pia alijulikana kama Tiglath-pileseri), aivamie nchi yao na kuwachukua mateka hao Wareubeni, Wagadi na nusu Manase ya mashariki mpaka uhamishoni huko Hala, Habori na Hara, kando ya mto Gozani, ambako wamekaa mpaka leo.
1 Lawi alikuwa na wana watatu: Gershomu, Kohathi na Merari.
2 Kohathi alikuwa na wana wanne: Amramu, Ishari, Hebroni na Uzieli.
3 Amramu alikuwa na wana wawili: Aroni na Mose, na binti mmoja jina lake Miriamu. Aroni alikuwa na wana wanne: Nadabu, Abihu, Eleazari na Ithamari.
4 Eleazari alimzaa Finehasi, Finehasi akamzaa Abishua,
5 Abishua akamzaa Buki, Buki akamzaa Uzi,
6 Uzi akamzaa Zerahia, Zerahia akamzaa Merayothi,
7 Merayothi akamzaa Amaria, Amaria akamzaa Ahitubu,
8 Ahitubu akamzaa Sadoki, Sadoki akamzaa Ahimaasi,
9 Ahimaasi akamzaa Azaria, Azaria akamzaa Yohanani,
10 na Yohanani akamzaa Azaria. (Azaria ndiye aliyefanya kazi ya ukuhani katika hekalu alilojenga mfalme Solomoni huko Yerusalemu).
11 Azaria alimzaa Amaria, Amaria alimzaa Ahitubu,
12 Ahitubu alimzaa Sadoki, Sadoki alimzaa Meshulamu,
13 Meshulamu alimzaa Hilkia, Hilkia alimzaa Azaria,
14 Azaria alimzaa Seraya, Seraya alimzaa Yehosadaki;
15 Yehosadaki alikwenda uhamishoni wakati Mwenyezi-Mungu alipowapeleka uhamishoni watu wa Yuda na Yerusalemu kwa kuutumia mkono wa mfalme Nebukadneza.
16 Lawi alikuwa na wana watatu: Gershomu, Kohathi na Merari.
17 Kila mmoja wao pia alikuwa na wana. Gershomu aliwazaa Libni na Shimei;
18 Kohathi aliwazaa Amramu, Ishari, Hebroni na Uzieli;
19 naye Merari aliwazaa Mahli na Mushi. Hizi ndizo jamaa za Walawi kulingana na koo zao.
20 Wafuatao ndio wazawa wa Gershomu kutoka kizazi hadi kizazi: Gershomu alimzaa Libni, Libni akamzaa Yahathi, Yahathi akamzaa Zima,
21 Zima akamzaa Yoa, Yoa akamzaa Ido, Ido akamzaa Zera, Zera akamzaa Yeatherai.
22 Hawa ndio wazawa wa Kohathi kutoka kizazi hadi kizazi: Kohathi alimzaa Aminadabu, Aminadabu akamzaa Kora, Kora akamzaa Asiri,
23 Asiri akamzaa Elkana, Elkana akamzaa Ebiasafu, Ebiasafu akamzaa Asiri,
24 Asiri akamzaa Tahathi, Tahathi akamzaa Urieli, Urieli akamzaa Usia, Usia akamzaa Shauli.
25 Wana wa Elkana walikuwa wawili: Amasai na Ahimothi.
26 Na hawa ndio wazawa wa Ahimothi: Ahimothi alimzaa Elkana, Elkana akamzaa Sofai, Sofai akamzaa Nahathi,
27 Nahathi akamzaa Eliabu, Eliabu akamzaa Yerohamu, Yerohamu akamzaa Elkana.
28 Wana wa Samueli walikuwa wawili: Yoeli, mzaliwa wake wa kwanza, na Abiya, mdogo wake.
29 Na hawa ndio wazawa wa Merari kutoka kizazi hadi kizazi: Merari alimzaa Mali, Mali akamzaa Libni, Libni akamzaa Shimei, Shimei akamzaa Uza,
30 Uza akamzaa Shimea, Shimea akamzaa Hagia, Hagia akamzaa Asaya.
31 Hawa ndio watu ambao mfalme Daudi aliwaweka wahudumu kama waimbaji katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu, baada ya sanduku la agano kuwekwa ndani.
32 Walifanya kazi yao ya kuimba mbele ya hema takatifu la mkutano hadi wakati mfalme Solomoni alipojenga hekalu la Mwenyezi-Mungu huko Yerusalemu. Waliutekeleza wajibu wao barabara, kwa zamu.
33 Zifuatazo ni koo za wale ambao walitoa huduma hizo: Ukoo wa Kohathi: Hemani, kiongozi wa kundi la kwanza la waimbaji, alikuwa mwana wa Yoeli. Ukoo wake kutokana na Israeli ni kama ifuatavyo: Hemani, mwana wa Yoeli, mwana wa Samueli,
34 mwana wa Elkana, mwana wa Yerohamu, mwana wa Elieli, mwana wa Toa,
35 mwana wa Zufu, mwana wa Elkana, mwana wa Mahathi, mwana wa Amasai,
36 mwana wa Elkana, mwana wa Yoeli, mwana wa Azaria, mwana wa Sefania,
37 mwana wa Tahathi, mwana wa Asiri, mwana wa Ebiasafu, mwana wa Kora,
38 mwana wa Ishari, mwana wa Kohathi, mwana wa Lawi, mwana wa Israeli.
39 Asafu, ndugu yake alikuwa upande wake wa kulia. Ukoo wake kutokana na Lawi: Asafu, mwana wa Berekia, mwana wa Shimea,
40 mwana wa Mikaeli, mwana wa Baaseya, mwana wa Malkiya,
41 mwana wa Ethni, mwana wa Zera, mwana wa Adaya,
42 mwana wa Ethani, mwana wa Zima, mwana wa Shimei,
43 mwana wa Yahathi, mwana wa Gershomu, mwana wa Lawi.
44 Ethani wa ukoo wa Merari, alikuwa kiongozi wa kundi la tatu la waimbaji. Ukoo wake kutokana na Lawi ni kama ifuatavyo: Ethani, mwana wa Kishi, mwana wa Abdi, mwana wa Maluki,
45 mwana wa Hashabia, mwana wa Amazia, mwana wa Hilkia,
46 mwana wa Amsi, mwana wa Bani, mwana wa Shemeri,
47 mwana wa Mahli, mwana wa Mushi, mwana wa Merari, mwana wa Lawi.
48 Ndugu zao wengine walipewa wajibu wa kuhudumia hema takatifu la nyumba ya Mungu.
49 Aroni na wazawa wake ndio waliokuwa wakitoa tambiko juu ya madhabahu ya tambiko za kuteketezwa na pia juu ya madhabahu ya kufukizia ubani. Walifanya kazi zote zilizohusika na mahali patakatifu sana ili kuifanyia Israeli upatanisho. Haya yote waliyafanya kulingana na maagizo aliyotoa Mose, mtumishi wa Mungu.
50 Wafuatao ndio wazawa wa Aroni: Aroni alimzaa Eleazari, Eleazari akamzaa Finehasi, Finehasi akamzaa Abishua,
51 Abishua akamzaa Buki, Buki akamzaa Uzi, Uzi akamzaa Serahia,
52 Serahia akamzaa Merayothi, Merayothi akamzaa Amaria, Amaria akamzaa Ahitubu,
53 Ahitubu akamzaa Sadoki, Sadoki akamzaa Ahimaasi.
54 Yafuatayo ndiyo makazi yao kulingana na mipaka yake: Wazawa wa Aroni katika jamaa ya Wakohathi kulingana na kura yao,
55 hao walipewa mji wa Hebroni katika nchi ya Yuda na malisho kandokando yake.
56 Lakini mashamba ya mjini pamoja na malisho yake alipewa Kalebu mwana wa Yefune.
57 Wazawa wa Aroni walipewa miji ya makimbilio: Hebroni, Libna pamoja na malisho yake, Yatiri na Eshtemoa pamoja na malisho yake,
58 Hileni na Debiri pamoja na malisho yake,
59 Ashani na Beth-shemeshi pamoja na malisho yake.
60 Katika eneo la kabila la Benyamini walipewa miji ya Geba, Alemethi na Anathothi pamoja na malisho ya miji hiyo. Miji yote waliyopewa kulingana na jamaa zao ilikuwa kumi na mitatu.
61 Miji kumi ya eneo la nusu ya kabila la Manase ilitolewa kwa sehemu iliyobaki ya ukoo wa Kohathi kwa kura kulingana na jamaa zao.
62 Ukoo wa Gershomu, kulingana na jamaa zake ulipewa miji kumi na mitatu katika kabila la Isakari, na katika kabila la Naftali na katika kabila la Manase katika Bashani.
63 Vivyo hivyo, miji kumi na miwili katika kabila la Reubeni, na katika kabila la Gadi na katika kabila la Zebuluni ilipewa ukoo wa Merari kulingana na jamaa zao.
64 Kwa njia hii watu wa Israeli waliwapa Walawi miji ili waishi humo pamoja na malisho ya miji hiyo.
65 (Miji iliyotajwa majina hapa juu katika kabila la Yuda, na katika kabila la Simeoni na katika kabila la Benyamini iligawiwa kabila la Lawi kwa kura.)
66 Jamaa nyingine za ukoo wa Kohathi zilipewa miji pamoja na malisho yake katika kabila la Efraimu:
67 Shekemu, mji wa makimbilio katika nchi ya milima ya Efraimu pamoja na malisho yake, Gezeri pamoja na malisho yake,
68 Yokmeamu pamoja na malisho yake, Beth-horoni pamoja na malisho yake;
69 Aiyaloni pamoja na malisho yake, na Gath-rimoni pamoja na malisho yake.
70 Katika nusu ya kabila la Manase walipewa miji ya Aneri pamoja na malisho yake, na Bileamu pamoja na malisho yake. Hii ndiyo miji iliyopewa jamaa za ukoo wa Kohathi.
71 Jamaa za ukoo wa Gershomu walipewa miji ifuatayo pamoja na malisho yake: Katika nusu ya kabila la Manase walipewa: Golani katika Bashani pamoja na malisho yake, Ashtarothi pamoja na malisho yake.
72 Katika kabila la Isakari walipewa: Kedeshi pamoja na malisho yake, Deberathi pamoja na malisho yake,
73 Ramothi pamoja na malisho yake na Anemu pamoja na malisho yake.
74 Katika kabila la Asheri walipewa: Mashali pamoja na malisho yake, Abdoni pamoja na malisho yake,
75 Hukoki pamoja na malisho yake, na Rehobu na malisho yake.
76 Katika kabila la Naftali: Kedeshi katika Galilaya pamoja na malisho yake, Hamoni pamoja na malisho yake na Kiriathaimu pamoja na malisho yake.
77 Jamaa za Merari zilizosalia, zilipewa miji ifuatayo pamoja na malisho yake kandokando ya miji hiyo: Katika kabila la Zebuluni walipewa Rimono pamoja na malisho yake na Tabori pamoja na malisho yake.
78 Katika kabila la Reubeni, mashariki ya mto Yordani karibu na mji wa Yeriko walipewa Bezeri ulioko katika nyanda za juu pamoja na malisho yake, Yahasa pamoja na malisho yake,
79 Kedemothi pamoja na malisho yake na Mefaathi pamoja na malisho yake.
80 Katika kabila la Gadi walipewa Ramothi katika Gileadi pamoja na malisho yake, Mahanaimu pamoja na malisho yake,
81 Heshboni pamoja na malisho yake na Yazeri pamoja na malisho yake.
1 Wana wa Isakari walikuwa wanne: Tala, Pua, Yashubu na Shimroni.
2 Wana wa Tola walikuwa: Uzi, Refaya, Yerieli, Yamai, Ibsamu na Shemueli. Hao walikuwa wakuu wa jamaa za koo za Tola na watu mashujaa sana wa vita nyakati zao. Idadi ya wazawa wao siku za mfalme Daudi ilikuwa 22,600.
3 Uzi alikuwa na mwana mmoja, jina lake Izrahia. Na wana wa Izrahia walikuwa Mikaeli, Obadia, Yoeli na Ishia, jumla wanne, na wote walikuwa wakuu wa jamaa.
4 Kwa vile ambavyo wake na watoto wao walikuwa wengi sana, mliweza kupatikana vikosi vya wanajeshi 36,000 kutokana na wazawa wao.
5 Ndugu zao katika jamaa zote za kabila la Isakari walioandikishwa kwa kufuata koo, walikuwa 87,000, na wote walikuwa mashujaa wa vita.
6 Benyamini alikuwa na wana watatu: Bela, Bekeri na Yediaeli.
7 Bela alikuwa na wana watano: Esboni, Uzi, Uzieli, Yeremothi na Iri. Hawa walikuwa viongozi wa jamaa zao, na wanajeshi mashujaa. Walioandikishwa kwa kufuata koo, idadi ya wazawa wao ilikuwa 22,034.
8 Bekeri alikuwa na wana tisa: Zemira, Yoashi, Eliezeri, Eliehonai, Omri, Yeremothi, Abiya, Anathothi na Alemethi. Wote hawa ni wazawa wa Bekeri.
9 Waliandikishwa kwa koo kulingana na vizazi vyao kama viongozi wa jamaa zao, na idadi ya wazawa wao ilikuwa 20,200, wote wakiwa mashujaa wa vita.
10 Yediaeli alikuwa na mwana mmoja, jina lake Bilhani. Bilhani alikuwa na wana: Yeushi, Benyamini, Ehudi, Kenaana, Zethani, Tarshishi na Ahishahari.
11 Wote hawa walikuwa wakuu wa jamaa katika koo zao na askari mashujaa wa vita. Kutokana na wazawa wao, kulipatikana wanaume 178,200, wanajeshi hodari tayari kabisa kwa vita.
12 Shupimu na Hupimu pia walikuwa wa kabila hili. Dani alikuwa na mwana mmoja, jina lake Hushimu.
13 Naftali alikuwa na wana wanne: Yaasieli, Guni, Yereri na Shalumu. Hao walikuwa wazawa wa Bilha.
14 Manase alikuwa na wana wawili kutokana na suria wake Mwaramu: Asrieli na Makiri. Makiri alikuwa baba yake Gileadi.
15 Makiri aliwazaa Hupimu na Shupimu. Jina la dada yake lilikuwa Maaka. Mwana wa pili wa Makiri alikuwa Selofehadi. Selofehadi alikuwa na mabinti peke yake.
16 Maaka mkewe Makiri, alizaa mwana jina lake Pereshi. Jina la nduguye Pereshi lilikuwa Shereshi. Wanawe Shereshi walikuwa Ulamu na Rakemu.
17 Rakemu alimzaa Bedani. Hawa wote ni wazawa wa Gileadi, mwana wa Makiri, mjukuu wa Manase.
18 Hamo-lekethi, dada yake Gileadi, aliwazaa Ishhodi, Abiezeri na Mala.
19 Wana wa Shemida walikuwa Ahiani, Shekemu, Liki na Aniamu.
20 Hawa ndio wazawa wa Efraimu kutoka kizazi hadi kizazi: Shuthela, Beredi, Tahathi, Eleada, Tahathi,
21 Zabadi na Shuthela. Mbali na Shuthela, Efraimu alikuwa na wana wengine wawili, Ezeri, na Eleadi, ambao waliuawa na wenyeji wa asili wa nchi ya Gathi kwa sababu walikwenda huko kuwanyanganya mifugo yao.
22 Efraimu baba yao aliomboleza vifo vyao kwa siku nyingi sana, na ndugu zake wakaja kumfariji.
23 Ndipo Efraimu akalala na mkewe, naye akachukua mimba na kuzaa mwana. Efraimu akampa jina Beria, kwa sababu ya maafa yaliyoipata jamaa yake.
24 Efraimu alikuwa na binti jina lake Sheera. Huyu ndiye aliyeijenga miji ya Beth-horoni ya juu na chini, na Uzen-sheera.
25 Efraimu alimzaa pia Refa ambaye alimzaa Reshefu, Reshefu akamzaa Tela, Tela akamzaa Tahani,
26 Tahani akamzaa Ladani, Ladani akamzaa Amihudi, Amihudi akamzaa Elishama,
27 Elishama akamzaa Nuni, Nuni akamzaa Yoshua.
28 Milki zao na makao yao yalikuwa: Betheli na vitongoji vyake, Naraani uliokuwa upande wa mashariki, Gezeri uliokuwa upande wa magharibi pamoja na vitongoji vyake, Shekemu na vitongoji vyake, na Aya na vitongoji vyake.
29 Na pia mipakani mwa wana wa Manase: Beth-sheani na vitongoji vyake, Taanaki na vitongoji vyake, Megido na vitongoji vyake na Dori na vitongoji vyake. Hiyo ndiyo miji walimoishi wazawa wa Yosefu, mwana wa Israeli.
30 Hawa ndio wazawa wa Asheri. Asheri alikuwa na wana wanne: Imna, Ishva, Ishri na Beria, na binti mmoja jina lake Sera.
31 Beria alikuwa na wana wawili: Heberi na Malkieli, aliyekuwa baba yake Birzaithi.
32 Heberi alikuwa na wana watatu: Yafleti, Shomeri na Hothamu, na binti mmoja jina lake Shua.
33 Yafleti pia alikuwa na wana watatu: Pasaki, Bimhali na Ashvathi.
34 Shemeri, nduguye, alikuwa na wana watatu: Roga, Yehuba na Aramu.
35 Na Helemu, ndugu yake mwingine, alikuwa na wana wanne: Sofa, Imna, Sheleshi na Amali.
36 Wana wa Sofa walikuwa Sua, Harneferi, Shuali, Beri, Imra,
37 Bezeri, Hodu, Shama, Shilsha, Ithrani na Beera.
38 Wana wa Yetheri walikuwa Yefune, Pispa na Ara.
39 Wana wa Ula walikuwa Ara, Hanieli na Risia.
40 Hao wote walikuwa wazawa wa Asheri na walikuwa wakuu wa jamaa zao, watu wateule na hodari wa vita. Idadi ya wale walioandikishwa kwa kufuata koo katika jeshi ilikuwa 26,000.
1 Benyamini alikuwa na wana watano: Bela, mzaliwa wake wa kwanza, Ashbeli wa pili, Ahara wa tatu,
2 Noha wa nne na Rafa wa tano.
3 Bela naye alikuwa na wana: Adari, Gera, Abihudi,
4 Abishua, Naamani, Ahoa,
5 Gera, Shufamu na Huramu.
6 Hawa ndio wazawa wa Ehudi. Hawa walikuwa viongozi wa jamaa za wale waliokuwa wakiishi Geba, lakini wakachukuliwa mateka uhamishoni Manahathi;
7 Naamani, Ahiya na Gera. Gera, baba yake Uza na Ahihudi, ndiye aliyewaongoza kuchukua hatua hiyo.
8 Shaharaimu aliwapa talaka wake zake wawili, Hushimu na Baara na baadaye alipata watoto wa kiume nchini Moabu.
9 Alimwoa Hodeshi, naye akamzalia wana saba: Yoabu, Sibia, Mesha, Malkamu,
10 Yeuzi, Sakia, na Mirma. Hawa wanawe wote walikuja kuwa wakuu wa koo.
11 Shaharaimu na mkewe Hushimu alipata wana wengine wawili: Abitubu na Elpaali.
12 Wana wa Elpaali walikuwa watatu: Eberi, Mishamu na Shemedi ambaye aliijenga miji ya Ono na Lodi, pamoja na vijiji kandokando yake.
13 Beria na Shema walikuwa miongoni mwa jamaa ambazo zilikuwa zinaishi katika mji wa Aiyaloni, na kuwafukuza wenyeji wa Gathi.
14 Nao Ahio, Shashaki, Yeremothi,
15 Zebadia, Aradi, Ederi,
16 Mikaeli, Ishpa na Yoha ni wazawa wengine wa Beria.
17 Zebadia, Meshulamu, Hizki, Heberi,
18 Ishnerai, Izlia na Yobabu walikuwa wazawa wa Epaali.
19 Yakimu, Zikri, Zabdi,
20 Elienai, Zilethai, Elieli,
21 Adaya, Beraya na Shimrathi walikuwa wazawa wa Shimei.
22 Ishpani, Eberi, Elieli,
23 Abdoni, Zikri, Hanani,
24 Hanania, Elamu, Anthothiya,
25 Ifdeya na Penueli walikuwa wazawa wa Shashaki.
26 Shamsherai, Sheharia, Athalia,
27 Yaareshia, Elia na Zikri walikuwa baadhi ya wazawa wa Yerohamu.
28 Hao ndio waliokuwa wakuu wa koo zao kulingana na vizazi vyao. Walikuwa wakuu na waliishi Yerusalemu.
29 Yeieli, alikuwa mwanzilishi wa mji wa Gibeoni. Mkewe alikuwa Maaka.
30 Mzaliwa wake wa kwanza alikuwa Abdoni. Wanawe wengine ni Zuri, Kishi, Baali, Nadabu,
31 Gedori, Ahio, Zekeri,
32 na Miklothi baba yake Shimea. Hawa pia waliishi Yerusalemu karibu na watu wengine wa ukoo wao.
33 Neri alimzaa Kishi, Kishi akamzaa Shauli. Shauli alikuwa na wana wanne: Yonathani, Malki-shua, Abinadabu na Eshbaali.
34 Yonathani alimzaa Merib-baali, na Merib-baali akamzaa Mika.
35 Mika alikuwa na wana wanne: Pithoni, Meleki, Terea na Ahazi.
36 Ahazi alimzaa Yehoada. Naye Yehoada aliwazaa Alemethi, Azmawethi na Zimri. Zimri alimzaa Mosa.
37 Mosa alimzaa Binea, aliyemzaa Rafa, aliyemzaa Eleasa, naye Eleasa akamzaa Aseli.
38 Wana wa Aseli walikuwa sita: Majina yao ni Azrikamu, Bokeru, Ishmaeli, Shearia, Obadia na Hanani. Wote hawa walikuwa wana wa Aseli.
39 Nao wana wa Esheki, nduguye Aseli, walikuwa watatu. Mzaliwa wake wa kwanza alikuwa Ulamu, wa pili Yeushi na wa tatu Elifeleti.
40 Wana wa Ulamu walikuwa watu mashujaa sana wa vita, na wapiga upinde hodari. Alikuwa na wana na wajukuu wengi, jumla150. Hao wote waliotajwa hapo juu walikuwa wa ukoo wa Benyamini.
1 Hivyo, watu wote wa Israeli waliandikishwa katika nasaba, na orodha hiyo imeandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Israeli. Watu wa Yuda walikuwa wamechukuliwa mateka hadi Babuloni kwa sababu ya kutokuwa waaminifu.
2 Watu wa kwanza kuyarudia makazi yao katika miji yao walikuwa raia wa kawaida, makuhani, Walawi na watumishi wa hekaluni.
3 Baadhi ya watu wa makabila ya Yuda, Benyamini, Efraimu na Manase walikwenda kuishi mjini Yerusalemu:
4 Uthai mwana wa Amihudi, mwana wa Omri, mwana wa Imri, mwana wa Bani, wa wana wa Peresi, mwana wa Yuda.
5 Na wazawa wa Shilo, Asaya mzaliwa wa kwanza, kiongozi na wanawe.
6 Na wazawa wa Zera, Yeueli, na ndugu zao; watu 690.
7 Na wa wazawa wa Benyamini: Salu mwana wa Meshulamu, mwana wa Hodavia, mwana wa Hasenua;
8 na Ibneya mwana wa Yerohamu, Ela, mwana wa Uzi, mwana wa Mikri; na Meshulamu, mwana wa Shefatia, mwana wa Reueli, mwana wa Ibniya;
9 na ndugu zao, sawasawa na vizazi vyao; watu956. Watu hao wote ndio waliokuwa wakuu wa koo za baba zao, kwa kadiri ya koo za baba zao.
10 Makuhani wafuatao waliishi Yerusalemu: Yedaya, Yehoyaribu na Yakini,
11 na Azaria mwana wa Hilkia, mwana wa Meshulamu, mwana wa Sadoki, mwana wa Merayothi, mwana wa Ahitubu, mkuu wa nyumba ya Mungu;
12 na Adaya, mwana wa Yerohamu, mwana wa Pashuri, mwana wa Malkiya; na Maasai, mwana wa Adieli, mwana wa Yazera, mwana wa Meshulamu, mwana wa Meshilemithi, mwana wa Imeri;
13 wakuu wa koo za baba zao; pamoja na ndugu zao; jumla watu 1,760. Walikuwa wakuu wenye uwezo mkubwa katika huduma yote ya nyumba ya Mungu.
14 Walawi wafuatao waliishi Yerusalemu: Shemaya, mwana wa Hashubu, mwana wa Azrikamu, mwana wa Hashabia, wa wana wa Merari;
15 na Bakbakari, na Hereshi, na Galali, Matania, mwana wa Mika, mwana wa Zikri, mwana wa Asafu;
16 na Obadia, mwana wa Shemaya, mwana wa Galali, mwana wa Yeduthuni; na Berekia, mwana wa Asa, mwana wa Elkana; waliokuwa wakiishi katika vijiji vya Wanetofathi.
17 Walinzi wa hekalu wafuatao pia waliishi katika Yerusalemu: Shalumu, Akubu, Talmoni na Ahimani na ndugu zao. Shalumu alikuwa mkuu wao.
18 Hadi kufikia wakati huo, walinzi kutoka katika koo zao ndio waliolinda Lango la mfalme la upande wa mashariki. Hapo awali, walikuwa walinzi wa maingilio ya makambi ya Walawi.
19 Shalumu, mwana wa Kore, mwana wa Ebiasafu, pamoja na ndugu zake wa ukoo wa Kora, walikuwa na wajibu wa kuyatunza maingilio ya hema la mkutano, kama vile walivyokuwa babu zake wakati wa ulinzi wa kambi ya Mwenyezi-Mungu.
20 Finehasi, mwana wa Eleazari, alikuwa msimamizi wao, hapo awali, naye Mwenyezi-Mungu alikuwa pamoja naye.
21 Zekaria mwana wa Meshelemia, pia alikuwa mlinzi wa maingilio ya hema la mkutano.
22 Jumla, watu 212 walichaguliwa kuwa walinzi wa maingilio ya hekalu. Waliandikishwa kulingana na vijiji walimoishi. Mfalme Daudi na Samueli mwonaji ndio waliowathibitisha katika wadhifa huu muhimu.
23 Basi, watu hao na wazawa wao, waliendelea kuyalinda malango ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu.
24 Kila upande, yaani mashariki, magharibi, kaskazini na kusini, palikuwa na lango lililokuwa na walinzi.
25 Walinzi hawa walisaidiwa na ndugu zao waliokuwa wakiishi vijijini, ambao walilazimika kushika zamu ya ulinzi kwa muda wa siku saba, mara kwa mara,
26 kwa maana wale walinzi wakuu wanne, ambao walikuwa Walawi, walikuwa na wajibu wa kusimamia vyumba na hazina ya nyumba ya Mungu.
27 Wao waliishi karibu na nyumba ya Mungu kwa sababu ilikuwa ni wajibu wao kuyalinda na kuyafungua malango yake kila siku asubuhi.
28 Baadhi ya Walawi walisimamia vyombo vilivyotumika wakati wa ibada. Walihitajika kuvihesabu wakati vilipotolewa na wakati viliporudishwa.
29 Wengine walichaguliwa kuvisimamia vifaa vya hekalu, na vyombo vyote vitakatifu, na unga safi, divai, mafuta ya zeituni, ubani na manukato.
30 Lakini kazi ya kutayarisha manukato ilifanywa na makuhani.
31 Metithia, mmoja wa Walawi aliyekuwa mzaliwa wa kwanza wa Shalumu, wa ukoo wa Kora, alisimamia utengenezaji wa tambiko ya mikate myembamba.
32 Nao ndugu zao wengine wa ukoo wa Kohathi walikuwa na wajibu wa kutayarisha mikate ya wonyesho kwa ajili ya hekalu kila Sabato.
33 Jamaa nyingine za Walawi zilisimamia huduma ya nyimbo hekaluni. Waliishi katika baadhi ya majengo ya nyumba ya Mungu na hawakuhitajika kufanya kazi nyingine yoyote kwa maana walikuwa kazini usiku na mchana.
34 Watu wote hawa waliotajwa walikuwa viongozi wa kabila la Walawi, kulingana na koo zao. Wao ndio viongozi walioishi Yerusalemu.
35 Yeieli alikuwa mwanzilishi wa mji wa Gibeoni ambamo aliishi yeye pamoja na mkewe, jina lake Maaka.
36 Mzaliwa wake wa kwanza alikuwa Abdoni, naye alifuatiwa na Zuri, Kishi, Baali, Neri, Nadabu,
37 Gedori, Ahio, Zekaria na Miklothi.
38 Miklothi alimzaa Shimeamu. Wazawa wao waliishi Yerusalemu karibu na jamaa nyingine za koo zao.
39 Neri alimzaa Kishi, naye Kishi akamzaa Shauli. Shauli alikuwa na wana wanne: Yonathani, Malki-shua, Abinadabu na Eshbaali.
40 Yonathani alimzaa Merib-baali, Merib-baali akamzaa Mika.
41 Mika alikuwa na wana wanne: Pithoni, Meleki, Tarea na Ahazi.
42 Ahazi alimzaa Yara, Yara akawazaa Alemethi, Azmawethi na Zimri, naye Zimri akamzaa Mosa,
43 Mosa akamzaa Binea, Binea akamzaa Refaya, Refaya akamzaa Eleasa, naye Eleasa akamzaa Aseli.
44 Aseli alikuwa na wana sita: Azrikamu, Bokeru, Ishmaeli, Shearia, Obadia na Hamani. Hawa wote walikuwa wana wa Aseli.
1 Basi, Wafilisti walipigana vita dhidi ya Waisraeli; nao Waisraeli walikimbia mbele ya Wafilisti na kuuawa katika mlima wa Gilboa.
2 Lakini Wafilisti wakamzingira Shauli na wanawe, kisha wakawaua Yonathani, Abinadabu na Malki-shua wana wa Shauli.
3 Vita vilikuwa vikali sana dhidi ya Shauli. Wapiga mishale walipomwona walimjeruhi.
4 Ndipo Shauli alipomwambia mtu aliyembebea silaha, “Chomoa upanga wako unichome nife, ili watu hawa wasiotahiriwa wasije wakanidhihaki.” Lakini huyo aliyembebea silaha hakuthubutu; kwa sababu aliogopa sana. Hivyo, Shauli alichukua upanga wake mwenyewe akauangukia.
5 Halafu yule aliyembebea silaha alipoona kuwa Shauli amekufa, naye pia akauangukia upanga wake, akafa.
6 Hivyo ndivyo Shauli alivyokufa, yeye na wanawe watatu, na jamaa yake yote.
7 Nao watu wa Israeli walioishi bondeni walipoona jeshi limewakimbia maadui, na ya kuwa Shauli na wanawe wamekufa, waliihama miji yao wakakimbia. Wafilisti wakaenda na kukaa katika miji hiyo.
8 Kesho yake, Wafilisti walipokwenda kuwateka nyara hao waliouawa, waliikuta maiti ya Shauli na wanawe mlimani Gilboa.
9 Walimvua mavazi, wakachukua kichwa chake pamoja na silaha zake, halafu walituma wajumbe katika nchi yote ya Filistia kutangaza habari njema kwa sanamu zao na watu.
10 Waliziweka silaha za Shauli katika hekalu la miungu yao; kisha wakakitundika kichwa chake katika hekalu la Dagoni.
11 Lakini watu wa Yabesh-gileadi waliposikia yote Wafilisti waliyomtendea Shauli,
12 mashujaa wote waliondoka na kuuchukua mwili wa Shauli na miili ya wanawe, wakaileta mpaka Yabeshi. Wakaizika mifupa yao chini ya mwaloni huko Yabeshi, nao wakafunga kwa muda wa siku saba.
13 Shauli alikufa kwa sababu ya kutokuwa mwaminifu; hakuwa mwaminifu kwani hakutii neno la Mwenyezi-Mungu na alikwenda kwa mwaguzi kumtaka shauri,
14 badala ya kumwendea Mwenyezi-Mungu ili kumtaka shauri. Kwa sababu hiyo Mwenyezi-Mungu akamuua, na ufalme wake akampa Daudi mwana wa Yese.
1 Kisha Waisraeli wote walikusanyika pamoja kwa Daudi huko Hebroni, wakamwambia: “Tazama, sisi ni mwili na damu yako.
2 Hapo awali, Shauli alipokuwa mfalme wewe ndiwe uliyewaongoza Waisraeli vitani, na Mwenyezi-Mungu, Mungu wako alikuambia, ‘Utakuwa mchungaji wa watu wangu Israeli, na utakuwa mkuu wa watu wangu Israeli.’
3 Basi, wazee wote wa Israeli wakamwendea mfalme huko Hebroni; naye Daudi akafanya agano nao mbele ya Mwenyezi-Mungu, halafu wakampaka Daudi mafuta awe mfalme wa Waisraeli kulingana na neno la Mwenyezi-Mungu lililotolewa kwa njia ya Samueli.”
4 Baadaye Daudi na Waisraeli wote walikwenda Yerusalemu uliojulikana kama Yebusi, na ambao wenyeji wake walikuwa Wayebusi.
5 Wakazi wa Yebusi walimwambia Daudi, “Hutaingia katika mji huu.” Hata hivyo, Daudi aliiteka ngome ya Siyoni, yaani mji wa Daudi.
6 Ndipo Daudi akasema, “Mtu atakayetangulia kuwapiga Wayebusi, atakuwa mkuu na kamanda jeshini.” Basi Yoabu, mwana wa Seruya, akawa wa kwanza kuwashambulia, hivyo akawa mkuu.
7 Daudi alikaa katika ngome hiyo, na kwa hiyo, mji huo ukaitwa “Mji wa Daudi.”
8 Aliujenga mji huo, akianzia Milo, na kuuzunguka wote, na Yoabu akautengeneza mji huo upya.
9 Naye Daudi akazidi kuwa mkuu kwa sababu Mwenyezi-Mungu wa majeshi alikuwa pamoja naye.
10 Hii ndiyo orodha ya wakuu wa mashujaa wa Daudi, ambao pamoja na watu wengine wote wa Israeli, walimuunga mkono kwa pamoja ili awe mfalme, sawa na neno la Mwenyezi-Mungu alilotoa juu ya Waisraeli.
11 Ifuatayo ni orodha ya mashujaa hao wa Daudi: Yashobeamu, Mhakmoni, aliyekuwa kiongozi wa “Wale thelathini.” Yeye alipigana kwa mkuki wake akaua watu 300 kwa mara moja vitani.
12 Halafu aliyefuata miongoni mwa wale mashujaa watatu alikuwa Eleazari mwana wa Dodo, Mwahohi.
13 Siku moja Eleazari alikuwa pamoja na Daudi huko Pas-damimu, wakati Wafilisti walipokusanyika kupigana vita. Huko kulikuwa na shamba lenye shayiri tele, nao Waisraeli walikuwa wamewakimbia Wafilisti.
14 Lakini Daudi na Eliazari walisimama imara katikati ya shamba hilo ili kulitetea, wakawaua Wafilisti; Mwenyezi-Mungu akawaokoa kwa kuwapa ushindi mkubwa.
15 Kisha mashujaa watatu kati ya wakuu thelathini waliteremka hadi kwenye mwamba, wakamwendea Daudi kwenye pango huko Adulamu. Wakati huo jeshi la Wafilisti lilikuwa limepiga kambi katika bonde la Refaimu.
16 Naye Daudi wakati huo alikuwa katika ngome, nalo jeshi la Wafilisti lilikuwa mjini Bethlehemu.
17 Daudi akasema kwa hamu kubwa, “Laiti kama mtu angeweza kunipa maji ya kunywa kutoka katika kisima cha Bethlehemu kilicho karibu na lango la mji!”
18 Wale mashujaa wake watatu walitoka, wakapenya katikati ya kambi ya jeshi la Wafilisti, wakaenda na kuchota maji katika kisima cha Bethlehemu, karibu na lango la mji, wakamletea Daudi. Lakini Daudi akakataa kuyanywa, na badala yake akayamwaga chini kama tambiko kwa Mwenyezi-Mungu
19 akisema, “Tendo kama hili lipitishie mbali nami; siwezi kulifanya mbele ya Mungu wangu. Je, waweza kunywa damu ya maisha ya watu hawa? Maana kwa kuyahatarisha maisha yao walileta maji haya.” Kwa hiyo Daudi hakuyanywa maji hayo. Hayo ndio mambo waliyotenda wale mashujaa watatu.
20 Abishai, nduguye Yoabu, alikuwa mkuu wa mashujaa thelathini. Yeye alipigana kwa mkuki wake dhidi ya watu 300, akawaua, akajipatia jina miongoni mwa wale mashujaa watatu.
21 Basi, akawa mashuhuri zaidi miongoni mwa mashujaa thelathini, hata akawa kamanda wao, lakini hakuwa shujaa kama wale mashujaa watatu.
22 Naye Benaya, mwana wa Yehoyada, kutoka Kabzeeli, alikuwa askari shujaa ambaye alifanya mambo mengi ya ajabu. Aliwaua mashujaa wawili kutoka Moabu, na siku moja wakati wa barafu, alishuka na kuua simba shimoni.
23 Vilevile, alimuua Mmisri mmoja, mtu mrefu sana, urefu wake kama mita mbili, naye mkononi mwake alikuwa amebeba mkuki mkubwa sana, kama mti wa mfumaji. Lakini Benaya alimwendea akiwa na fimbo tu, akamnyanganya mkuki huo, na kumuua Mmisri huyo kwa mkuki wake mwenyewe.
24 Benaya, mwana wa Yehoyada alifanya mambo haya, akajipatia jina miongoni mwa wale mashujaa watatu.
25 Basi, akawa mashuhuri kati ya wale mashujaa thelathini, ingawa hakuwa shujaa kama wale mashujaa watatu. Na Daudi akampa cheo cha mkuu wa walinzi wake binafsi.
26 Wanajeshi mashujaa wa Daudi walikuwa: Asaheli nduguye Yoabu, Elhanani mwana wa Dodo wa Bethlehemu,
27 Shamothi Mharodi, Helesi Mpeloni,
28 Ira, mwana wa Ikeshi Mtekoa, Abiezeri Mwanathothi;
29 Sibekai Mhushathi; Ilai Mwahohi;
30 Maharai Mnetofathi; Heledi, mwana wa Baana Mnetofathi;
31 Itai, mwana wa Ribai, kutoka Gibea, wa kabila la Benyamini; Benaya Mpirathoni;
32 Hurai kutoka vijito vya Gaashi, Abieli Mwaibathi;
33 Azmawethi Mbaharumu; Eliaba Mshaalboni;
34 wana wa Yasheni Mgiloni; Yonathani, mwana wa Shagee Mharari,
35 Ahiamu, mwana wa Sakari Mharari; Elifali, mwana wa Uri;
36 Heferi Mmekerathi; Ahiya Mpeloni;
37 Hezro Mkarmeli; Naarai, mwana wa Ezbai;
38 Yoeli, nduguye Nathani; Mibhari, mwana wa Hagri;
39 Zeleki Mwamoni; Naharai Mbeerothi, aliyekuwa mbeba silaha wa Yoabu, mwana wa Seruya;
40 Ira na Garebu, waliokuwa Waithri,
41 Uria, Mhiti; Zabadi, mwana wa Ahlai;
42 Adina, mwana wa Shiza Mreubeni, mkuu wa Wareubeni, akiwa pamoja na watu thelathini;
43 Hanani, mwana wa Maaka, Yoshafati Mmithni;
44 Uzia Mwashterathi, Shama na Yeieli, wana wa Hothamu Mwaroeri;
45 Yediaeli na Yoha nduguye, wana wa Shimri Mtizi;
46 Elieli Mmahawi, Yeribai na Yoshavia wana wa Elnaamu; Ithma Mmoabu;
47 Elieli, Obedi, na Yaasieli Mmesobai.
1 Hawa ni wanaume ambao walijiunga na Daudi huko Siklagi, alipokuwa hana uhuru wowote wa kutembea kwa sababu ya mfalme Shauli mwana wa Kishi; walikuwa miongoni mwa askari mashujaa waliomsaidia vitani.
2 Hao walikuwa watu wa kabila la Benyamini kama alivyokuwa Shauli. Walikuwa wapiga upinde hodari, na warusha mawe kwa kombeo kwa kutumia mikono yote, wa kulia na kushoto.
3 Kiongozi wao alikuwa Ahiezeri, aliyesaidiwa na Yoashi, wote wana wa Shemaa kutoka Gibea; wengineo ni: Yezieli na Peleti, wana wa Azmawethi, Beraka, Yehu kutoka Anathothi,
4 Ishmaya kutoka Gibeoni, mtu shujaa miongoni mwa wale thelathini na kiongozi wao pia pamoja na Yeremia, Yahazieli, Yohanani, Yozabadi kutoka Gedera,
5 Eluzai, Yeremothi, Bealia, Shemaria, Shefatia, Mharufi,
6 Elkana, Ishia, Azareli, Yoezeri, Yashobeamu kutoka ukoo wa Kora
7 na Yoela na Zebadia, wana wa Yerohamu, kutoka Gedori.
8 Tena, watu kutoka kabila la Gadi walijiunga na Daudi akiwa ngomeni kule nyikani. Hawa walikuwa askari wenye nguvu na uzoefu, hodari wa kutumia ngao na mkuki; wenye nyuso za kutisha kama simba na wepesi kama swala milimani.
9 Kiongozi wao mkuu alikuwa Ezeri, wa pili Obadia, wa tatu Eliabu,
10 wa nne Mishmana, wa tano Yeremia,
11 wa sita Atai, wa saba Elieli,
12 wa nane Yohanani, wa tisa Elsabadi,
13 wa kumi Yeremia, na wa kumi na moja Makbanai.
14 Wagadi hao, walikuwa maofisa wa jeshi. Kulingana na vyeo vyao, mdogo alisimamia kikosi cha wanajeshi 100, na mkubwa alisimamia kikosi cha wanajeshi 1,000.
15 Hawa ndio watu waliovuka mto Yordani mnamo mwezi wa kwanza, mto ulipokuwa umefurika pande zote na kuwatawanya watu mashariki na magharibi ya mto.
16 Baadhi ya watu kutoka makabila ya Benyamini na Yuda walifika ngomeni alipokuwa Daudi.
17 Daudi akatoka nje kuwalaki, akawaambia, “Ikiwa mmekuja kwangu kama marafiki ili kunisaidia basi nawapokea kwa moyo wote, lakini kama mmekuja ili kunisaliti kwa maadui zangu, ingawa sijatenda ovu lolote, Mungu wa baba zetu awaone na awakemee.”
18 Hapo Roho akamjia Abishai, mkuu wa hao watu thelathini, naye akasema, “Sisi tu watu wako, ee Daudi, tuko upande wako, ee mwana wa Yese! Amani, amani iwe kwako, na amani iwe kwa yeyote akusaidiaye! Maana akusaidiaye ndiye Mungu wako.” Ndipo Daudi akawapokea na kuwafanya maofisa katika jeshi lake.
19 Askari wengine wa kabila la Manase, walitoroka na kujiunga na Daudi, wakati alipoondoka pamoja na Wafilisti kwenda kupigana na mfalme Shauli. (Lakini hata hivyo, hakuwasaidia maana watawala wa Wafilisti walifanya shauri wamfukuze arudi Siklagi wakisema, “Tutayahatarisha maisha yetu kwa sababu atatutoroka arudi kwa bwana wake Shauli.”)
20 Basi, Daudi alipokuwa Siklagi, watu wafuatao wa kabila la Manase walimwendea: Adna, Yozabadi, Yediaeli, Mikaeli, Yozabadi, Elihu na Silethai. Kila mmoja wao alikuwa kiongozi wa kikosi cha watu 1,000 katika kabila la Manase.
21 Walimsaidia Daudi kupigana na magenge ya washambuliaji, kwani wote walikuwa askari mashujaa na makamanda jeshini.
22 Siku hata siku, watu walijiunga na Daudi kumsaidia, hatimaye akawa na jeshi kubwa sana, kama jeshi la Mungu.
23 Hii ndio idadi ya vikosi vya askari wenye silaha waliojiunga na Daudi huko Hebroni ili kumtwalia ufalme kutoka kwa Shauli, kulingana na neno la Mwenyezi-Mungu:
24 Watu wa kabila la Yuda waliokuwa na mikuki na ngao, walikuwa 6,800. Wote walikuwa na silaha zao.
25 Kutoka kabila la Simeoni, watu 7,100 mashujaa na wenye ujuzi mwingi wa vita.
26 Kutoka kabila la Lawi: Watu 4,600.
27 Yehoyada, wa uzao wa Aroni na wenzake: Watu 3,700.
28 Jamaa ya Sadoki, kijana hodari vitani, yeye pamoja na makamanda ishirini na wawili kutoka ukoo wa baba yake mwenyewe.
29 Kutoka kabila la Benyamini, (kabila la Shauli): Watu 3,000. Wengi wao walibaki waaminifu kwa jamaa ya Shauli;
30 Kutoka kabila la Efraimu: Watu 20,800, watu mashujaa sana tena mashuhuri katika koo zao;
31 Kutoka nusu ya kabila la Manase: Watu 18,000, waliotajwa majina ili waje kumtawaza Daudi awe mfalme.
32 Kutoka kabila la Isakari: Wakuu 200 pamoja na ndugu zao wote waliokuwa chini ya amri yao. Wakuu hao walikuwa na elimu ya kujua mambo ya nyakati na walijua kilichowapasa Waisraeli kufanya.
33 Kutoka kabila la Zebuluni: Watu 50,000; waaminifu na wazoefu wa vita. Walijiandaa na zana za vita za kila namna, lengo lao likiwa ni kumsaidia Daudi tu.
34 Kutoka kabila la Naftali: Makamanda 1,000 pamoja na watu 37,000 wenye ngao na mikuki.
35 Kutoka kabila la Dani: Watu 28,600 wenye silaha tayari kwa vita.
36 Kutoka kabila la Asheri: Watu 40,000 wazoefu wa vita, tayari kwa mapigano.
37 Kutoka kabila la Wareubeni, Wagadi na nusu ya kabila la Manase kutoka ngambo ya mto Yordani: Watu 120,000 wenye kila aina ya silaha za vita.
38 Wanajeshi hao wote, waliojiandaa tayari kabisa kwa vita, walikwenda Hebroni na nia yao kubwa ikiwa ni kumtawaza Daudi awe mfalme wa Israeli yote. Nao watu wote wa Israeli, pia waliungana wakiwa na nia moja ya kumtawaza Daudi awe mfalme.
39 Basi, walikaa na Daudi kwa muda wa siku tatu, wakila na kunywa kwani ndugu zao walikuwa wamekwisha waandalia vyakula.
40 Zaidi ya hayo, majirani zao wa karibu na hata wa mbali kama huko Isakari, Zebuluni na Naftali, waliwaletea vyakula walivyobeba kwa punda, ngamia, nyumbu na ng'ombe. Waliwaletea unga, mikate ya tini, vichala vya zabibu kavu, divai na mafuta, ng'ombe na kondoo wengi, kukawa na vyakula tele, kwani kulikuwa na furaha katika Israeli.
1 Daudi alishauriana na makamanda wa vikosi vya maelfu na vikosi vya mamia, pamoja na viongozi wote.
2 Kisha akawaambia Waisraeli wote waliokusanyika, “Ikiwa mtakubaliana nami, na ikiwa ni mapenzi yake Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, na tufanye hivi: Tutume wajumbe waende wakawaite ndugu zetu waliobaki nchini Israeli, pamoja na makuhani na Walawi walioko katika miji yao na malisho yao, waje wajumuike pamoja nasi.
3 Kisha twende tukalichukue sanduku la agano la Mungu wetu, maana hatukulijali wakati wa utawala wa mfalme Shauli.”
4 Watu wote walikubaliana na pendekezo hilo kwani waliliona kuwa jambo jema.
5 Hivyo, Daudi aliwakusanya Waisraeli wote nchini; toka kijito cha Shihori kilichoko Misri, hadi maingilio ya Hamathi ili kulileta sanduku la Mungu toka Kiriath-yearimu.
6 Daudi, akiandamana na Waisraeli wote, akaenda hadi mjini Baala, yaani Kiriath-yearimu, nchini Yudea, ili kulichukua toka huko sanduku la Mungu linaloitwa kwa jina lake Mwenyezi-Mungu akaaye kwenye kiti chake cha enzi juu ya viumbe vyenye mabawa.
7 Basi, wakalichukua sanduku la Mungu kutoka katika nyumba ya Abinadabu kwa gari jipya. Uza na Ahio waliliendesha gari hilo.
8 Daudi na Waisraeli wote wakawa wanacheza kwa nguvu zao zote, mbele ya Mungu. Waliimba huku wanapiga ala za muziki zilizotengenezwa kwa mvinje: Vinubi, vinanda, matari, matoazi na tarumbeta.
9 Walipofika kwenye uwanja wa kupuria nafaka wa Kidoni, Uza aliunyosha mkono wake kulishikilia sanduku la agano kwa sababu ng'ombe walijikwaa.
10 Mara Mwenyezi-Mungu akamkasirikia Uza kwa kulishika sanduku, akamuua. Uza akafa papo hapo mbele ya Mungu.
11 Daudi alikasirika kwa sababu Mwenyezi-Mungu alimuua Uza akiwa na hasira. Kwa sababu hiyo, mahali hapo huitwa Peres-uza hadi leo.
12 Siku hiyo Daudi akamwogopa Mungu, akasema, “Sasa, nitawezaje kulichukua sanduku la Mungu nyumbani mwangu?”
13 Basi, Daudi hakulichukua sanduku mpaka mji wa Daudi, bali alilipeleka nyumbani kwa Obed-edomu, Mgiti.
14 Sanduku hilo la Mungu lilikaa huko kwa Obed-edomu kwa muda wa miezi mitatu, naye Mwenyezi-Mungu akaibariki nyumba ya Obed-edomu na mali yake yote.
1 Kisha mfalme Hiramu wa Tiro alituma wajumbe kwa Daudi, pia alimpelekea mierezi, waashi na maseremala, ili wamjengee Daudi ikulu.
2 Hivyo, Daudi akatambua kwamba Mwenyezi-Mungu amemwimarisha awe mfalme wa Israeli, na kwamba ufalme wake umekuzwa kwa ajili ya Israeli, watu wake.
3 Huko Yerusalemu, Daudi alioa wake wengi zaidi, naye akazaa wana na mabinti wengine.
4 Yafuatayo ndio majina ya watoto aliozaa huko Yerusalemu: Shamua, Shobabu, Nathani, Solomoni,
5 Ibhari, Elishua, Elpeleti,
6 Noga, Nefegi, Yafia,
7 Elishama, Beeliada na Elifeleti.
8 Wafilisti waliposikia kwamba Daudi amepakwa mafuta kuwa mfalme wa nchi nzima ya Israeli, wote walitoka kwa wingi kwenda kumtafuta. Daudi alipopata habari, alitoka kwenda kuwakabili.
9 Wafilisti walifika wakaanza mashambulizi katika bonde la Refaimu.
10 Ndipo Daudi alipomwuliza Mungu shauri, “Je, niende kuwashambulia Wafilisti? Je, utawatia mikononi mwangu?” Naye Mwenyezi-Mungu akamwambia, “Nenda, nitawatia mikononi mwako.”
11 Basi, Daudi akaenda huko Baal-perasimu, akawashinda; halafu akasema, “Mungu amepita katikati ya adui zangu kwa mkono wangu, kama mafuriko ya maji yaendayo kasi.” Kwa hiyo mahali hapo panaitwa Baal-perasimu.
12 Wafilisti walipokimbia, waliziacha sanamu za miungu yao huko, naye Daudi akatoa amri zote zichomwe moto.
13 Kisha Wafilisti walifanya mashambulizi katika bonde hilo kwa mara ya pili.
14 Safari hii, Daudi alipoomba shauri kwa Mungu, Mungu akamwambia, “Usiwashambulie kutoka hapa, ila zunguka na kuwashambulia kutoka mkabala na miti ya miforosadi, halafu washambulie kutoka huko.
15 Na mara utakaposikia vishindo vya gwaride kwenye vilele vya hiyo miforosadi, haya, toka uende vitani. Nitakuwa nimekwisha kukutangulia kulipiga jeshi la Wafilisti.”
16 Daudi alifanya kama alivyoamriwa na Mungu. Alilipiga jeshi la Wafilisti kutoka Gibeoni hadi Gezeri.
17 Daudi akawa maarufu kote nchini, naye Mwenyezi-Mungu akayatia hofu mataifa yote, nayo yakamwogopa sana.
1 Daudi alijijengea nyumba katika mji wa Daudi. Tena akalitengenezea sanduku la Mungu mahali, akalipigia hema.
2 Kisha akasema, “Hakuna mtu mwingine yeyote atakayelibeba sanduku la Mungu isipokuwa Walawi, maana Mwenyezi-Mungu aliwachagua wao kulibeba na kumtumikia milele.”
3 Basi, akawakusanya Waisraeli wote waje Yerusalemu, ili kulileta sanduku la Mwenyezi-Mungu mahali alipolitayarishia.
4 Halafu Daudi akawaita wazawa wa Aroni na Walawi:
5 Kutoka katika ukoo wa Kohathi, wakaja Urieli, pamoja na ndugu zake120 chini ya usimamizi wake;
6 kutoka katika ukoo wa Merari wakaja Asaya pamoja na ndugu zake 220 chini ya usimamizi wake;
7 kutoka katika ukoo wa Gershomu, wakaja Yoeli pamoja na ndugu zake 130 chini ya usimamizi wake;
8 kutoka katika ukoo ya Elisafani, wakaja Shemaya pamoja na ndugu zake 200 chini ya usimamizi wake;
9 kutoka katika ukoo wa Hebroni, wakaja Elieli pamoja na ndugu zake 80 chini ya usimamizi wake;
10 na kutoka katika ukoo wa Uzieli, wakaja Aminadabu pamoja na ndugu zake 112 chini ya usimamizi wake.
11 Daudi akawaita makuhani wawili: Sadoki na Abiathari, na Walawi sita: Urieli, Asaya, Yoeli, Shemaya, Elieli na Aminadabu;
12 akawaambia, “Nyinyi ni viongozi wa koo za Walawi. Jitakaseni pamoja na ndugu zenu, ili mkalilete sanduku la Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, hadi mahali ambapo nimelitayarishia.
13 Kwa sababu hamkulibeba safari ya kwanza, Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, alituadhibu kwani hatukulitunza kama alivyoagiza.”
14 Basi, makuhani na Walawi wakajitakasa ili wapate kulileta sanduku la Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli.
15 Walawi wakalibeba mabegani mwao wakitumia mipiko yake kama Mose alivyoamuru, kulingana na neno la Mwenyezi-Mungu.
16 Daudi pia aliwaamuru wakuu wa Walawi wachague baadhi ya ndugu zao wawe wakiimba na kupiga ala za muziki: Vinanda, vinubi na matoazi kwa nguvu, ili kutoa sauti za furaha.
17 Hivyo wakachagua watu wafuatao katika koo za waimbaji: Hemani mwana wa Yoeli, Asafu nduguye aliyekuwa mwana wa Berekia na wana wa Merari, ndugu zao, na Ethani mwana wa Kushaya.
18 Kisha wakawachagua Walawi wafuatao wawe wasaidizi wao kwa kushika nafasi ya pili: Zekaria, Yaasieli, Shemiramothi, Yehieli, Uni, Eliabu, Benaya, Maaseya, Matithia, Elifelehu na Mikneya na walinzi wa lango: Obed-edomu na Yeieli.
19 Hemani, Asafu na Etani wakachaguliwa kupiga matoazi ya Shaba.
20 Zekaria, Azieli, Shemiramothi, Yehieli, Uni, Eliabu, Maaseya na Benaya, walikuwa wapiga vinubi vya sauti ya Alamothi.
21 Lakini Matithia, Elifelehu, Mikneya, Obed-edomu, Yeieli na Azazia waliongoza wakiwa na vinubi vya sauti ya Sheminithi.
22 Naye Kenania kwa sababu ya ujuzi wa muziki aliokuwa nao, aliwekwa kuwa kiongozi wa wote.
23 Berekia na Elkana walikuwa walinzi wa sanduku la agano.
24 Shebania, Yoshafati, Nethaneli, Amasai, Zekaria, Benaya na Eliezeri, waliokuwa makuhani, waliwekwa kupiga tarumbeta mbele ya sanduku la Mungu. Obed-edomu na Yehiya waliwekwa pia kuwa walinzi wa sanduku.
25 Basi, Daudi, wazee wa Waisraeli na makamanda wa maelfu, wakaenda kulichukua sanduku la agano la Mwenyezi-Mungu kutoka nyumbani kwa Obed-edomu kwa shangwe.
26 Wakamtolea tambiko Mungu: Mafahali saba na kondoo madume saba kwa sababu aliwasaidia wale Walawi waliolibeba sanduku la agano la Mwenyezi-Mungu.
27 Daudi alikuwa amevaa joho la kitani safi, hali kadhalika na Walawi wote waliobeba sanduku, waimbaji na Kenania kiongozi wa waimbaji. Mbali na joho hilo, Daudi alikuwa amevaa kizibao cha kitani.
28 Hivyo, Waisraeli wote walijumuika pamoja kwa shangwe kulichukua sanduku la agano la Mwenyezi-Mungu hadi Yerusalemu. Walilisindikiza kwa mlio wa baragumu, tarumbeta, matoazi, na sauti kubwa za vinanda na vinubi.
29 Sanduku la agano la Mwenyezi-Mungu lilipokuwa linaingia katika mji wa Daudi, Mikali, binti Shauli, alichungulia dirishani, akamwona mfalme Daudi akicheza na kushangilia, basi akamdharau moyoni mwake.
1 Kisha waliliingiza sanduku la Mungu, na kuliweka ndani ya hema ambayo Daudi alikuwa ameitayarisha. Halafu wakatoa tambiko za kuteketezwa na za amani mbele ya Mungu.
2 Daudi alipomaliza kutoa tambiko hizo za kuteketezwa na za amani, aliwabariki watu katika jina la Mwenyezi-Mungu,
3 na akawagawia Waisraeli wote, wanaume kwa wanawake, kila mmoja akapewa mkate, kipande cha nyama na mkate wa zabibu.
4 Zaidi ya hayo, Daudi aliwateua baadhi ya Walawi wawe wahudumu wa sanduku la Mwenyezi-Mungu, wamtukuze, wamtolee shukrani na wamsifu Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli.
5 Alimchagua Asafu kuwa kiongozi wao, akisaidiwa na Zekaria. Yeieli, Shemiramothi, Yehieli, Metithia, Eliabu, Benaya, Obed-edomu na Yehieli, aliwachagua wawe wapiga vinanda na vinubi. Asafu alipiga matoazi,
6 nao makuhani Benania na Yaharieli, walichaguliwa wawe wakipiga tarumbeta mfululizo mbele ya sanduku la agano la Mungu.
7 Basi, hiyo ikawa siku ambayo kwa mara ya kwanza, Daudi alimpa Asafu na ndugu zake Walawi wajibu wa kumwimbia Mwenyezi-Mungu nyimbo za shukrani.
8 Mpeni shukrani Mwenyezi-Mungu, tangazeni ukuu wake, yajulisheni mataifa mambo aliyoyatenda!
9 Mshangilieni, mwimbieni Mungu sifa; simulieni matendo yake ya ajabu!
10 Jisifieni jina lake takatifu; wenye kumcha Mwenyezi-Mungu na wafurahi.
11 Mwendeeni Mwenyezi-Mungu mwenye nguvu; mwendeeni Mwenyezi-Mungu daima.
12 Kumbukeni matendo ya ajabu aliyotenda, maajabu yake na hukumu alizotoa,
13 enyi wazawa wa Abrahamu, mtumishi wake, enyi wazawa wa Yakobo, wateule wake.
14 Yeye Mwenyezi-Mungu, ndiye Mungu wetu; hukumu zake zina nguvu duniani kote.
15 Yeye hulishika agano lake milele, hutimiza ahadi zake kwa vizazi elfu.
16 Hushika agano alilofanya na Abrahamu, na ahadi aliyomwapia Isaka.
17 Alimthibitishia Yakobo ahadi yake, akamhakikishia agano hilo la milele.
18 Alisema: “Nitawapeni nchi ya Kanaani, nayo itakuwa mali yenu wenyewe.”
19 Idadi yenu ilikuwa ndogo, mlikuwa wachache na wageni katika nchi ya Kanaani,
20 mkitangatanga toka taifa hadi taifa, kutoka nchi moja hadi nchi nyingine,
21 Mungu hakumruhusu mtu yeyote awadhulumu; kwa ajili yao aliwaonya wafalme:
22 “Msiwaguse wateule wangu; msiwadhuru manabii wangu!”
23 Mwimbieni Mwenyezi-Mungu, ulimwengu wote. Tangazeni kila siku matendo yake ya wokovu.
24 Yatangazieni mataifa utukufu wake, waambieni watu wote matendo yake ya ajabu.
25 Maana Mwenyezi-Mungu ni mkuu, anasifika sana anastahili kuheshimiwa kuliko miungu yote.
26 Miungu yote ya mataifa mengine si kitu; lakini Mwenyezi-Mungu aliziumba mbingu.
27 Utukufu na fahari vyamzunguka, nguvu na furaha vyajaza hekalu lake.
28 Mpeni Mwenyezi-Mungu, heshima enyi jamii zote za watu, naam, kirini utukufu na nguvu yake.
29 Mpeni Mwenyezi-Mungu heshima ya utukufu wa jina lake; leteni tambiko na kuingia nyumbani mwake. Mwabuduni Mwenyezi-Mungu patakatifuni pake.
30 Ee dunia yote; tetemeka mbele yake! Ameuweka ulimwengu imara, hautatikisika.
31 Furahini enyi mbingu na dunia! Yaambieni mataifa, “Mwenyezi-Mungu anatawala!”
32 Bahari na ivume, pamoja na vyote vilivyomo! Furahini enyi mashamba na vyote vilivyomo!
33 Ndipo miti yote msituni itaimba kwa furaha mbele ya Mwenyezi-Mungu anayekuja naam, anayekuja kuihukumu dunia.
34 Mshukuruni Mwenyezi-Mungu kwa kuwa ni mwema, kwa maana fadhili zake zadumu milele!
35 Mwambieni Mwenyezi-Mungu: Utuokoe, ee Mungu wa wokovu wetu, utukusanye pamoja na kutuokoa kutoka kwa mataifa, tupate kulisifu jina lako takatifu, kuona fahari juu ya sifa zako.
36 Asifiwe Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, tangu milele na hata milele! Kisha watu wote wakasema, “Amina!” Pia wakamsifu Mwenyezi-Mungu.
37 Hivyo, mfalme Daudi akawaacha Asafu na nduguze Walawi mahali walipoliweka sanduku la agano la Mwenyezi-Mungu, kwa ajili ya huduma zinazotakiwa mbele ya sanduku kila siku.
38 Obed-edomu, mwana wa Yeduthuni, pamoja na wenzake sitini na wanane waliwasaidia. Obed-edomu mwana wa Yeduthuni na Hosa walikuwa walinzi wa malango.
39 Mfalme Daudi akawaweka kuhani Sadoki na makuhani wenzake kuwa wahudumu wa hema ya Mwenyezi-Mungu iliyokuwa mahali pa kuabudu huko Gibeoni
40 ili kutolea Mwenyezi-Mungu sadaka za kuteketezwa juu ya madhabahu ya sadaka za kuteketezwa daima asubuhi na jioni, kulingana na yote yaliyoandikwa katika sheria ya Mwenyezi-Mungu aliyowaamuru Waisraeli.
41 Pamoja nao walikuwa Hemani na Yeduthuni na wale wote waliochaguliwa, waliotajwa majina yao, ili kumshukuru Mwenyezi-Mungu kwa kuwa fadhili zake ni za milele.
42 Hemani na Yeduthuni walikuwa na tarumbeta na matoazi kwa ajili ya muziki na ala za muziki kwa ajili ya nyimbo takatifu. Wana wa Yeduthuni walichaguliwa kuyalinda malango.
43 Kisha, kila mtu aliondoka kwenda nyumbani kwake; naye Daudi akaenda nyumbani kwake kuibariki jamaa yake.
1 Wakati mfalme Daudi alipokuwa akikaa katika ikulu, siku moja alimwita nabii Nathani, na kumwambia, “Hebu tazama, mimi ninakaa kwenye nyumba nzuri iliyojengwa kwa mwerezi, lakini sanduku la agano la Mwenyezi-Mungu linakaa hemani.”
2 Nathani akamwambia Daudi, “Fanya chochote unachofikiria moyoni mwako, kwa kuwa Mungu yu pamoja nawe.”
3 Lakini usiku uleule, neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Nathani, kusema,
4 “Nenda ukamwambie mtumishi wangu Daudi, ‘Mwenyezi-Mungu anasema hivi: Wewe hutanijengea nyumba ya kukaa.
5 Tangu wakati ule nilipowaongoza watu wa Israeli kutoka Misri mpaka hivi leo, sijaishi kwenye nyumba. Nimekuwa nikihama toka hema hadi hema, na toka makao hadi makao mengine.
6 Je, kila mahali ambako nimekwenda na Waisraeli, nimepata kumwuliza mwamuzi wao yeyote niliyemwamuru awachunge watu wangu, “Kwa nini hukunijengea nyumba ya mierezi?” ’
7 Kwa hiyo basi, mwambie mtumishi wangu Daudi: ‘Mwenyezi-Mungu wa majeshi anasema hivi: Nilikutoa malishoni ulipokuwa unawachunga kondoo, ili uwe mkuu wa watu wangu Israeli.
8 Tangu wakati huo nimekuwa pamoja nawe kokote ulikokwenda na nimewaangamiza maadui zako wote mbele yako. Nitakufanya kuwa maarufu kama wakuu wengine wa dunia.
9 Nami nitawachagulia watu wangu wa Israeli mahali pa kuishi niwapandikize, ili waishi mahali pao wenyewe, wasisumbuliwe tena. Nao watu wakatili wanaotumia nguvu hawatawatesa tena kama hapo awali,
10 tangu wakati nilipowateua waamuzi juu ya watu wangu Israeli; mimi nitawashinda maadui zako wote. Zaidi ya yote, mimi Mwenyezi-Mungu nakutangazia kuwa nitakujengea nyumba.
11 Siku zako zitakapotimia za kujiunga na babu zako, nitamfanya mmoja wa watoto wako, wewe mwenyewe awe mfalme; nami nitauimarisha ufalme wake.
12 Yeye ndiye atakayenijengea nyumba; nami nitahakikisha kwamba ufalme wake unadumu milele.
13 Mimi nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwanangu; lakini sitamwondolea fadhili zangu kama vile nilivyomwondolea Shauli aliyekutangulia.
14 Bali nitamwimarisha katika nyumba yangu na katika ufalme wangu milele, na kiti chake cha enzi kitakuwa imara daima.’”
15 Nathani alimwelezea Daudi mambo yote haya kulingana na maono yote.
16 Kisha mfalme Daudi akaingia ndani ya hema na kuketi mbele ya Mwenyezi-Mungu, halafu akaomba, “Mimi ni nani, ee Mwenyezi-Mungu, na nyumba yangu ni nini hata unitukuze hivi?
17 Isitoshe, umenifanyia mengine zaidi: Umenitolea ahadi juu ya vizazi vyangu vijavyo ee Mwenyezi-Mungu!
18 Nikuambie nini zaidi, mimi Daudi mtumishi wako, kwa kunitukuza hivyo? Wewe unanijua mimi mtumishi wako.
19 Ee Mwenyezi-Mungu, kwa ajili ya mtumishi wako na kwa kufuatana na moyo wako mwenyewe, umeyatenda hayo makuu yote, ili yajulikane hayo matendo makuu yote.
20 Hakuna mwingine kama wewe, ee Mwenyezi-Mungu, na yote tunayoyasikia yanathibitisha kwamba hakuna Mungu mwingine ila wewe.
21 Tena ni watu gani duniani ambao wanaweza kulinganishwa na watu wako wa Israeli ambao peke yao Mungu wao alikwenda kuwakomboa ili wawe watu wake? Wewe ulijifanyia jina kwa kutenda mambo makubwa na ya ajabu hapo ulipoyafukuza mataifa mbele ya watu wako ambao uliwakomboa kutoka Misri.
22 Hata umejifanyia watu wako wa Israeli kuwa watu wako milele; nawe ee Mwenyezi-Mungu, umekuwa Mungu wao.
23 “Basi sasa, ewe Mwenyezi-Mungu, liimarishe milele neno lako ulilosema kunihusu mimi mtumishi wako na kuhusu jamaa yangu.
24 Nalo jina lako litatukuzwa milele, nao watu watasema, ‘Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, ndiye Mungu wa Israeli!’ Na jamaa yangu, mimi Daudi mtumishi wako, itaimarika mbele yako.
25 Maana ee Mungu wangu nimepata ujasiri kukuomba kwa sababu wewe, umenifunulia ukisema ya kwamba utanijengea nyumba.
26 Sasa ee Mwenyezi-Mungu, wewe ndiwe Mungu, umeniahidi mimi mtumishi wako jambo hili jema;
27 kwa hiyo nakuomba uibariki nyumba yangu, mimi mtumishi wako, ili idumu milele mbele yako; kwani unachobariki wewe, huwa kimebarikiwa milele.”
1 Baada ya hayo, mfalme Daudi aliwashinda na kuwatiisha Wafilisti. Akauteka mji wa Gathi pamoja na vijiji vyake walivyomiliki Wafilisti.
2 Aliwashinda Wamoabu pia, wakawa watumishi wake na wakawa wanalipa kodi.
3 Daudi pia alimshinda Hadadezeri mfalme wa Soba, nchi iliyokuwa karibu na Hamathi, alifanya hivyo wakati alipokuwa akienda kujisimamishia nguzo ya kumbukumbu kwenye sehemu za mto Eufrate.
4 Daudi akateka magari ya farasi 1,000, askari wapandafarasi 7,000 na wa miguu 20,000. Kisha Daudi alikata mishipa ya miguu ya nyuma ya farasi wote wa magari, ila aliwabakiza 100.
5 Nao Waaramu wa Damasko, walipokwenda kumsaidia Hadadezeri mfalme wa Soba, Daudi aliwashambulia na kuwaua watu 22,000.
6 Halafu Daudi aliweka kambi za kijeshi katika mji wa Shamu ya Damasko. Basi Waaramu wakawa watumishi wake, na wakawa wanalipa kodi. Mwenyezi-Mungu alimpa Daudi ushindi kokote alikokwenda.
7 Daudi alizichukua ngao za dhahabu walizobeba wanajeshi wa Hadadezeri, na kuzipeleka Yerusalemu.
8 Daudi alichukua pia shaba nyingi sana kutoka mji wa Tibhathi na mji wa Kuni; iliyokuwa miji ya Hadadezeri. Solomoni aliitumia shaba hiyo kutengenezea nguzo na vyombo vya shaba.
9 Wakati Tou, mfalme wa Hamathi aliposikia kwamba Daudi amelishinda jeshi lote la Hadadezeri mfalme wa Soba,
10 alituma mwanawe Hadoramu kwa mfalme Daudi, kumpelekea salamu na pongezi kwa sababu alikuwa amepigana na Hadadezeri na kumshinda. Maana Hadadezeri alipigana na Tou mara nyingi. Hadoramu alimpelekea Daudi zawadi za vyombo vya fedha, dhahabu na shaba.
11 Zawadi hizo, mfalme Daudi aliziweka wakfu kwa Mwenyezi-Mungu pamoja na fedha na dhahabu aliyoiteka kutoka mataifa yote kutoka: Edomu, Moabu, Amoni, Filisti na Amaleki.
12 Abishai mwana wa Seruya, aliwaua Waedomu 18,000 katika Bonde la Chumvi.
13 Basi akaweka kambi za kijeshi huko Edomu. Nao Waedomu wote wakawa watumishi wa Daudi. Mwenyezi-Mungu alimpa Daudi ushindi kokote alikokwenda.
14 Hivyo Daudi akatawala juu ya Israeli yote, na akahakikisha ya kwamba watu wake wote wanatendewa haki na usawa.
15 Yoabu, mwana wa Seruya alikuwa mkuu wa majeshi; Yehoshafati mwana wa Ahiludi alikuwa mtunza kumbukumbu;
16 Sadoki, mwana wa Ahitubu na Ahimeleki, mwana wa Abiathari walikuwa makuhani; Shausha alikuwa katibu;
17 na Benaya, mwana wa Yehoyada alisimamia askari walinzi Wakerethi na Wapelethi; wana wa Daudi walikuwa maofisa wakuu katika utawala wake.
1 Ikawa baada ya hayo Nahashi, mfalme wa Waamoni akafariki; naye mwanawe akashika utawala.
2 Basi, Daudi akasema, “Nitamtendea mema Hanuni mwana wa Nahashi, kwani baba yake alinitendea mema pia.” Hivyo Daudi alituma wajumbe na kumpelekea salamu za rambirambi kwa ajili ya kifo cha baba yake. Nao wakaenda kwa Hanuni ili kumfariji, huko katika nchi ya Waamoni.
3 Lakini viongozi wa Waamoni wakamwambia mfalme, “Je! Unadhani ni kwa sababu ya heshima ya baba yako ati Daudi ametuma wajumbe hawa waje kukufariji? Watu hawa si majasusi waliotumwa kuja kuichunguza nchi kuiangamiza na kuipeleleza?”
4 Basi Hanuni aliwachukua wajumbe hao wa Daudi, akawanyoa ndevu na kuzipasua nguo zao katikati hadi matakoni, kisha akawatoa waende zao,
5 nao wakaondoka kurudi makwao. Daudi alipopashwa habari jinsi walivyotendewa wajumbe wake, alituma watu kuwalaki kwani hao wajumbe waliona aibu sana. Naye mfalme aliwaambia, “Kaeni mjini Yeriko, hata mtakapoota ndevu, Kisha mrudi.”
6 Waamoni walipoona wamejifanya wachukizwe na Daudi, Hanuni na hao Waamoni walituma watu wapeleke talanta 4,000 za fedha kukodisha magari na wapandafarasi kutoka Mesopotamia, Aramaaka na Soba.
7 Walikodisha magari 32,000 na mfalme wa Maaka na askari wake, akaja na kupiga kambi karibu na Medeba. Waamoni walikusanyika toka kwenye miji yao yote, wakajiandaa tayari kwa vita.
8 Naye Daudi aliposikia habari hizo alimtuma Yoabu na jeshi lote la mashujaa.
9 Waamoni walitoka wakajipanga kwenye lango la mji, hali wale wafalme waliokuja walikuwa peke yao kwenye tambarare.
10 Yoabu alipoona kuwa vita ni vikali dhidi yake, mbele na nyuma, aliwateua baadhi ya wanajeshi hodari zaidi wa Waisraeli, akawapanga kukabiliana na Waaramu.
11 Wale wanajeshi wengine waliobaki, aliwaweka chini ya uongozi wa Abishai ndugu yake, naye akawapanga ili wakabiliane na Waamoni.
12 Yoabu akamwambia Abishai, “Ikiwa Waaramu wananizidi nguvu, utanisaidia; lakini kama Waamoni wanakuzidi nguvu, nitakuja kukusaidia.
13 Basi jipe moyo! Tupigane kiume kwa ajili ya watu wetu, na kwa ajili ya miji ya Mungu wetu; na Mwenyezi-Mungu atutendee lile analoona ni jema kwake.”
14 Basi, Yoabu na watu wake walisonga mbele kupigana na Wasiria; nao Waaramu walikimbia.
15 Waamoni walipoona Waaramu wamekimbia, nao walimkimbia Abishai, nduguye Yoabu, wakaingia mjini. Ndipo Yoabu akarudi Yerusalemu.
16 Lakini Waaramu walipoona ya kwamba wameshindwa na Waisraeli, walituma wajumbe waende kuwaleta Waaramu wengine waliokuwa ngambo ya mto Eufrate wakiongozwa na Shofaki, kamanda wa jeshi la Hadadezeri.
17 Daudi alipopata habari, aliwakusanya pamoja Waisraeli wote, akavuka mto Yordani, akawaendea, akapanga vikosi vyake dhidi yao. Daudi alipopanga vita dhidi ya Wasiria, basi nao walipigana naye.
18 Lakini Waaramu walikimbia mbele ya Waisraeli. Daudi aliwaua Waaramu waendeshao magari 7,000 na askari wa miguu 40,000. Pia alimuua Shofaki, kamanda wa jeshi lao.
19 Kisha watumishi wa Hadadezeri walipoona kuwa wameshindwa na Waisraeli, walifanya mapatano ya amani na Daudi nao wakawa watumishi wa Daudi. Hivyo Waaramu hawakukubali kuwasaidia Waamoni tena.
1 Hata ikawa katika mwanzo wa mwaka mpya, wakati ambapo wafalme huenda vitani, Yoabu aliliongoza jeshi na kuteka nyara nchi ya Waamoni, pia akaenda na kuuzingira Raba. Lakini Daudi alibaki huko Yerusalemu. Naye Yoabu aliushambulia Raba na kuuharibu;
2 naye Daudi akaichukua taji ya mungu wao Milkomu kichwani pake; naye aligundua ya kwamba taji hiyo ilikuwa na uzito wa kilo thelathini na tano za dhahabu na ndani yake mlikuwemo kito cha thamani. Naye Daudi akakitwaa kupambia taji yake. Pia, aliteka idadi kubwa ya nyara kutoka katika mji huo.
3 Halafu aliwachukua watu wa mji huo, akawaweka wafanye kazi kwa misumeno, sururu za chuma na mashoka ya chuma. Hivyo ndivyo alivyoitenda miji yote ya Waamoni. Hatimaye Daudi na watu wote wakarudi Yerusalemu.
4 Baada ya hayo, kulitokea vita na Wafilisti huko Gezeri. Sibekai, Mhushathi, akamuua Sipai aliyekuwa mmojawapo wa wazawa wa Warefai; hivyo Wafilisti wakawa wameshindwa.
5 Kulitokea tena vita na Wafilisti. Naye Elhanani mwana wa Yairi alimuua Lahmi nduguye Goliathi, Mgiti, ambaye mpini wa mkuki wake, ulikuwa kama mti wa mfumaji.
6 Baadaye kulitokea tena vita huko Gathi ambako kulikuwa na mtu mmoja aliyekuwa na kimo kikubwa, na vidole sita katika kila mkono, na vidole sita katika kila mguu, jumla yake vidole ishirini na vinne. Yeye pia alikuwa mzawa wa majitu.
7 Naye alipowatukana Waisraeli, Yonathani, mwana wa Shimea, nduguye Daudi, alimuua.
8 Hao walikuwa wazawa wa majitu huko Gathi; nao waliuawa na Daudi pamoja na watumishi wake.
1 Shetani akajitokeza kuwataabisha Waisraeli, akamshawishi Daudii awahesabu watu.
2 Hivyo, Daudi akamwambia Yoabu na wale makamanda wengine, “Nendeni mkawahesabu Waisraeli, kutoka Beer-sheba mpaka Dani. Nileteeni ripoti ili nijue idadi yao.”
3 Lakini Yoabu akasema, “Mwenyezi-Mungu na awaongeze Waisraeli mara mia kuliko walivyo sasa! Bwana wangu mfalme, kwani hawa wote si watumishi wako? Kwa nini basi unataka kufanya jambo ambalo litawatia Waisraeli katika hatia?”
4 Lakini tamko la mfalme lilikuwa na nguvu zaidi dhidi ya Yoabu. Hivyo, Yoabu akaenda katika nchi yote ya Israeli, kisha akarejea Yerusalemu.
5 Yoabu akampelekea mfalme Daudi idadi ya watu: Katika Israeli yote, kulikuwamo wanaume 1,100,000, wenye ujuzi wa kutumia upanga; na katika Yuda kulikuwamo watu 470,000, wenye ujuzi wa kutumia upanga.
6 Lakini Yoabu hakuwahesabu Walawi na Wabenyamini, kwa sababu alichukizwa sana na amri ya mfalme.
7 Mungu hakupendezwa na jambo hilo kwa hiyo akaiadhibu Israeli.
8 Daudi akamwambia Mungu, “Nimetenda dhambi kubwa kwa tendo hili nililolifanya! Lakini nakuomba unisamehe mimi mtumishi wako, kwani nimefanya jambo la kipumbavu kabisa.”
9 Basi, Mwenyezi-Mungu alisema na Gadi, mwonaji wa Daudi, akamwambia,
10 “Nenda umwambie Daudi kwamba mimi Mwenyezi-Mungu ninampa mambo matatu. Ajichagulie mojawapo nami nitamtendea.”
11 Hivyo Gadi akamwendea Daudi na kumwambia, “Mwenyezi-Mungu anasema hivi: Jichagulie mojawapo:
12 Njaa ya miaka mitatu, au miezi mitatu ya maangamizi kutokana na maadui zako ambapo upanga wa maadui zako utakushinda; au siku tatu ambapo Mwenyezi-Mungu atawashambulia kwa upanga wake, awaletee maradhi mabaya nchini, na malaika wake apite kuwaangamiza katika nchi nzima ya Israeli. Sasa amua, ni jibu lipi nitakalompa yeye aliyenituma.”
13 Daudi akamjibu Gadi, “Nimeingia katika mashaka makubwa! Lakini afadhali niadhibiwe na Mwenyezi-Mungu kwani yeye ana huruma sana. Ila nisianguke katika mkono wa mwanadamu.”
14 Basi, Mwenyezi-Mungu akawaletea Waisraeli maradhi mabaya, ambayo yalisababisha vifo vya Waisraeli 70,000.
15 Halafu Mungu akatuma malaika aende kuuharibu Yerusalemu; lakini kabla hajafanya hivyo, Mwenyezi-Mungu akageuza nia yake na kumwambia malaika huyo aliyetekeleza maangamizi, “Basi, yatosha!” Malaika alikuwa amesimama karibu na uwanja wa kupuria nafaka wa Ornani, Myebusi.
16 Daudi akainua macho yake, akamwona huyo malaika wa Mwenyezi-Mungu amesimama kati ya mbingu na dunia, naye ameunyosha upanga wake juu ya Yerusalemu tayari kuuangamiza. Hapo Daudi na wazee wote walikuwa wamevaa mavazi ya gunia, wakaanguka kifudifudi.
17 Daudi alimwambia Mungu, “Je, si mimi niliyetoa amri watu wahesabiwe? Ni mimi niliyetenda dhambi na kufanya uovu. Lakini kondoo hawa wamefanya nini? Nakusihi sana, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu, mkono wako uwe dhidi yangu na dhidi ya jamaa ya baba yangu, lakini maradhi haya mabaya yasiwapate watu wako.”
18 Ndipo malaika wa Mwenyezi-Mungu akamwamuru Gadi amwambie Daudi aende amjengee Mwenyezi-Mungu madhabahu, katika kiwanja cha kupuria nafaka cha Ornani Myebusi.
19 Daudi akatii amri ya Mwenyezi-Mungu, akapanda juu kufuatana na neno la Gadi alilosema kwa jina la Mwenyezi-Mungu.
20 Ornani alipogeuka na kumwona yule malaika, ndipo yeye na wanawe wanne waliokuwa pamoja naye wakajificha. Naye Ornani alikuwa akipura ngano.
21 Daudi alipomwendea Ornani, Ornani alitazama na kumwona Daudi; basi huyo Ornani alitoka kwenye uwanja wa kupuria akaenda mbele; kisha akamsujudia akiinamisha kichwa chake mpaka chini ardhini.
22 Daudi akamwambia Ornani, “Nipe nafasi ya uwanja wako wa kupuria nafaka ili nimjengee Mwenyezi-Mungu madhabahu juu yake, ili kwamba tauni ipate kuzuiliwa kwa watu. Niuzie kwa bei yake kamili.”
23 Naye Ornani akamwambia Daudi, “Kichukue kiwanja hiki, bwana wangu mfalme, na ukitumie vile unavyopenda mwenyewe. Tazama, nawatoa fahali kwa ajili ya sadaka za kuteketezwa, na vifaa vya kupuria kwa kuni, pamoja na ngano iwe tambiko ya nafaka. Vyote hivyo ninakupa.”
24 Lakini mfalme Daudi alimwambia Ornani, “La, hasha; nitavinunua kwa thamani yake kamili; sitamchukulia Mwenyezi-Mungu kitu kilicho chako au kumtolea tambiko za kuteketezwa ambazo hazijanigharimu kitu.”
25 Hivyo, Daudi alimlipa Ornani kwa kumpimia shekeli 600 kamili za dhahabu kulipia uwanja huo.
26 Kisha Daudi akamjengea Mwenyezi-Mungu madhabahu mahali hapo na kumtolea sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani. Akamwomba Mwenyezi-Mungu, naye akakubali ombi lake kwa kuleta moto kutoka mbinguni kuiteketeza ile sadaka kwenye madhabahu.
27 Halafu, Mwenyezi-Mungu alimwamuru malaika, naye akaweka upanga wake alani mwake.
28 Wakati huo, Daudi alipoona ya kwamba Mwenyezi-Mungu amekubali ombi lake kwenye uwanja wa kupuria nafaka wa Ornani, Myebusi, akatoa tambiko papo hapo.
29 Hema la Mwenyezi-Mungu ambalo lilitengenezwa na Mose nyikani, na madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa, wakati huo vilikuwa bado pale mahali pa kuabudia huko Gibeoni.
30 Lakini Daudi hakuweza kwenda huko kumwomba Mungu shauri kwa sababu alikuwa anauogopa upanga wa malaika wa Mwenyezi-Mungu.
1 Basi Daudi akasema, “Hapa ndipo mahali ambapo nyumba ya Mwenyezi-Mungu itakuwa, na hii ndiyo madhabahu ambapo watu wa Israeli watatolea sadaka ya kuteketezwa.”
2 Daudi akatoa amri wageni waliokuwa wanaishi katika nchi ya Israeli wakusanyike, naye akawapangia kazi. Akaweka waashi wachonge vizuri mawe ya kujenga nyumba ya Mungu.
3 Daudi pia akaweka akiba tele ya chuma cha kutengenezea misumari na mafungo ya malango ya nyumba, na akiba tele ya shaba isiyopimika.
4 Mbao za mierezi ambazo Daudi aliletewa na Wasidoni na Watiro zilikuwa hazihesabiki.
5 Daudi akajisemea, “Nyumba ambayo mwanangu Solomoni atamjengea Mwenyezi-Mungu itakuwa ya fahari sana, ya kusifika na tukufu duniani kote. Lakini kwa vile yeye bado angali kijana na bado hana uzoefu mwingi, afadhali nimfanyie matayarisho.” Hivyo basi, Daudi akaweka akiba kubwa sana ya vitu vya ujenzi kabla hajafariki.
6 Ndipo Daudi akamwita Solomoni mwanawe, akamwagiza amjengee Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli nyumba.
7 Daudi akamwambia Solomoni, “Mwanangu, nilikusudia moyoni mwangu kumjengea Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu nyumba ili kumtukuza.
8 Lakini Mwenyezi-Mungu aliniambia, ‘Wewe umemwaga damu nyingi kwa kupigana vita vikubwa. Kwa sababu ya damu nyingi ambayo umemwaga mbele yangu hapa duniani, hutanijengea nyumba.
9 Hata hivyo, utapata mwana, ambaye atatawala kwa amani kwa sababu nitampa amani na maadui zake wote wa jirani. Jina lake litakuwa Solomoni, kwa maana katika siku za utawala wake, atailetea Israeli amani na utulivu.
10 Hivyo, yeye ndiye atakayenijengea nyumba. Atakuwa mwanangu nami nitakuwa baba yake, na wazawa wake wataitawala Israeli milele.’
11 Sasa mwanangu, Mwenyezi-Mungu, Mungu wako na awe pamoja nawe ili ufaulu kumjengea nyumba kama alivyosema.
12 Mwenyezi-Mungu akupe busara na akili ili atakapokupa uongozi juu ya Israeli, uzishike sheria zake Mwenyezi-Mungu, Mungu wako.
13 Ukiwa mwangalifu, na ukizitii amri ambazo Mwenyezi-Mungu alimwagiza Mose juu ya Israeli, utastawi. Jipe moyo, uwe imara. Usiogope wala usifadhaike.
14 Kwa juhudi kubwa, nimeiwekea akiba nyumba ya Mwenyezi-Mungu, talanta 100,000 za dhahabu, talanta 1,000,000 za fedha na idadi isiyopimika ya shaba na chuma, kwani ni nyingi sana. Nimeandaa mbao na mawe tayari. Lakini huna budi kuongezea.
15 Unao wafanyakazi wengi: Kuna wachonga mawe, waashi, maseremala na mafundi wa kila aina wenye ujuzi mwingi;
16 wa kufua dhahabu, fedha, shaba na chuma. Haya! Anza kazi! Mwenyezi-Mungu na awe pamoja nawe!”
17 Zaidi ya hayo, Daudi aliwaamuru viongozi wote wa Waisraeli wamsaidie Solomoni mwanawe, akisema,
18 “Je, Mwenyezi-Mungu Mungu wenu hayuko pamoja nanyi? Je, hajawapa amani katika pande zote? Yeye aliwatia wakazi wa nchi hii mikononi mwangu na sasa wako chini ya Mwenyezi-Mungu na watu wake.
19 Sasa, mtumikieni Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, kwa nia na moyo wote. Shime basi! Mjengeeni Mwenyezi-Mungu mahali patakatifu ili sanduku la agano la Mwenyezi-Mungu pamoja na vyombo vyote vitakatifu vitumiwavyo katika ibada, viwekwe ndani ya nyumba iliyojengwa kwa ajili ya Mwenyezi-Mungu.”
1 Daudi alipokuwa mzee wa miaka mingi, alimtawaza Solomoni mwanawe awe mfalme wa Israeli.
2 Mfalme Daudi aliwakusanya wakuu wote wa Israeli, makuhani na Walawi.
3 Walawi wote wanaume wenye umri wa miaka thelathini na zaidi, wakahesabiwa. Jumla yao ilikuwa 38,000.
4 Hao, Daudi aliwagawanya: 24,000 kati yao wawe wasimamizi wa kazi ya nyumbani kwa Mwenyezi-Mungu, 6,000 wawe maofisa na waamuzi,
5 4,000 wawe mabawabu, na 4,000 wawe waimbaji, wakimsifu Mwenyezi-Mungu kwa ala za muziki alizotengeneza mfalme mwenyewe kwa madhumuni hayo.
6 Daudi aliwagawanya Walawi katika makundi matatu kulingana na koo za kabila la Lawi: Ukoo wa Gershoni, ukoo wa Kohathi na ukoo wa Merari.
7 Wana wa Gershoni walikuwa wawili: Ladani na Shimei.
8 Ladani alikuwa na wana watatu: Yehieli mkuu wao, Zethamu na Yoeli.
9 Wana wa Shimei walikuwa watatu: Shelomithi, Hazieli na Harani. Hawa walikuwa viongozi wa ukoo wa Ladani.
10 Wana wa Shimei walikuwa viongozi wanne: Yahathi, Zina, Yeushi na Beria.
11 Yahathi ndiye aliyekuwa mkuu wao, akifuatiwa na Ziza. Lakini Yeushi na Beria, kwa vile hawakuwa na wana wengi, walichukuliwa na ukoo mmoja.
12 Wana wa Kohathi walikuwa wanne: Amramu, Ishari, Hebroni na Uzieli.
13 Wana wa Amramu walikuwa Aroni na Mose. Aroni aliteuliwa awe akiweka wakfu vyombo vitakatifu kabisa, pia wazawa wake daima wafukizie ubani mbele za Mwenyezi-Mungu, wakimtumikia na kuwabariki watu katika jina la Mwenyezi-Mungu milele.
14 Lakini wana wa Mose, mtu wa Mungu, hutajwa miongoni mwa kabila la Lawi.
15 Wana wa Mose walikuwa Gershomu na Eliezeri.
16 Aliyekuwa mkuu miongoni mwa wana wa Gershomu ni Shebueli.
17 Eliezeri alikuwa na mwana mmoja tu; Rehabia, naye alikuwa kiongozi. Lakini Rehabia alikuwa na wana wengi sana.
18 Ishari alimzaa Shelomithi, kiongozi wa kabila zima.
19 Wana wa Hebroni walikuwa wanne: Mkuu wao alikuwa Yeria, wa pili Amaria, wa tatu Yahazieli na wa nne Yekameamu.
20 Wana wa Uzieli walikuwa wawili: Mika mkuu wao, na Ishia wa pili.
21 Merari alikuwa na wana wawili: Mali na Mushi. Wana wa Mali walikuwa wawili: Eleazari na Kishi.
22 Eleazari alifariki bila kupata mtoto wa kiume, ila mabinti tu. Mabinti hao waliolewa na binamu zao, wana wa Kishi.
23 Wana wa Mushi walikuwa watatu: Mali, Ederi na Yeremothi.
24 Hao ndio wana wa Lawi kulingana na koo zao. Kila mmoja wao aliyetimiza umri wa miaka ishirini na zaidi, aliandikishwa kwa jina, na alishiriki katika huduma ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu.
25 Daudi alisema, “Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, amewapa watu wake amani, naye ataishi Yerusalemu milele.
26 Kwa hiyo, Walawi hawatahitaji tena kulibeba hema takatifu au vyombo vyake vya ibada.”
27 Kulingana na maagizo ya mwisho aliyotoa Daudi, Walawi wote waliofikia umri wa miaka ishirini waliandikishwa.
28 Lakini wajibu wao ulikuwa ni kuwasaidia makuhani wa ukoo wa Aroni katika huduma ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu; kuzitunza nyua na vyumba, kuvisafisha vyombo vitakatifu vyote na kufanya kazi zinazohusu huduma ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu.
29 Pamoja na hayo, walisaidia katika kazi ya mikate mitakatifu, unga mwembamba na sadaka ya nafaka, maandazi yasiyotiwa chachu, sadaka iliyookwa; sadaka iliyochanganywa na mafuta; pia sadaka katika kazi ya upimaji wa wingi wa sadaka na ukubwa wake
30 na walisimama kumshukuru na kumsifu Mwenyezi-Mungu kila siku asubuhi na jioni,
31 na wakati wa siku za Sabato, mwezi mwandamo na sikukuu, hapo sadaka za kuteketezwa zilipotolewa kwa Mwenyezi-Mungu. Sheria ziliwekwa kuhusu idadi ya Walawi walioagizwa kufanya kazi hizo daima mbele ya Mwenyezi-Mungu.
32 Kwa hiyo, ulikuwa ni wajibu wao kutunza hema la mkutano na mahali patakatifu, na kuwasaidia ndugu zao makuhani, wazawa wa Aroni, kwenye ibada katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu.
1 Hayo ndiyo makundi ya wazawa wa Aroni. Aroni alikuwa na wana wanne: Nadabu, Abihu, Eleazari na Ithamari.
2 Nadabu na Abihu walikufa kabla ya baba yao, wala hawakuwa na watoto; kwa hiyo ndugu zao Eleazari na Ithamari wakawa makuhani.
3 Mfalme Daudi aliwapanga wazawa wa Aroni katika makundi kufuatana na huduma zao. Alisaidiwa kufanya hivyo na Sadoki, mzawa wa Eleazari, na Ahimeleki, mzawa wa Ithamari.
4 Kwa vile ambavyo kulipatikana viongozi wanaume wengi zaidi miongoni mwa wazawa wa Ithamari, waliwagawanya wazawa wa Eleazari chini ya viongozi kumi na sita, na wazawa wa Ithamari chini ya viongozi wanane.
5 Waligawanywa kwa kura kwani kulikuwa na wakuu wa mahali patakatifu na viongozi wa kidini miongoni mwa koo zote mbili, yaani ukoo wa Eleazari na ukoo wa Ithamari.
6 Naye Shemaya mwana wa Nathaneli, mwandishi, aliyekuwa Mlawi, aliwaandika mbele ya mfalme Daudi, maofisa wake, kuhani Sadoki, Ahimeleki mwana wa Abiathari na viongozi wa jamaa za makuhani na za Walawi. Ukoo wa Eleazari ulipata kura mbili, na ukoo wa Ithamari kura moja.
7 Kura ya 1 ilimwangukia Yoaribu; ya 2 Yedaya;
8 ya 3 Harimu; ya 4 Seorimu;
9 ya 5 Malkia; ya 6 Miyamini;
10 ya 7 Hakosi; ya 8 Abiya;
11 ya 9 Yeshua; ya 10 Shekania;
12 ya 11 Eliashibu; ya 12 Yakimu;
13 ya 13 Hupa; ya 14 Yeshebeabu;
14 ya 15 Bilga; ya 16 Imeri;
15 ya 17 Heziri; ya 18 Hapisesi;
16 ya 19 Pethahia; ya 20 Yehezkeli;
17 ya 21 Yakini; ya 22 Gamuli;
18 ya 23 Delaya; na ya 24 Maazia.
19 Hawa waliandikishwa kulingana na kazi zao kuingia katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu kutoa huduma, kadiri ya utaratibu waliowekewa na Aroni babu yao, kama alivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli.
20 Hawa ndio wazawa wengine wa Lawi: Mmoja wa wazawa wa Amramu alikuwa Shubaeli; wa Shubaeli alikuwa Yedeya.
21 Mmoja wa wazawa wa Rehabia alikuwa Ishio kiongozi wa ukoo.
22 Mmoja wa wazawa wa Ishio alikuwa Shelomithi na wa wazawa wa Shelomithi alikuwa Yahathi.
23 Wana wa Hebroni walikuwa: Yeria wa kwanza, Amaria wa pili, Yahazieli wa tatu, Yakameamu wa nne.
24 Mmoja wa wana wa Uzieli alikuwa Mika. Mmoja wa wazawa wa Mika alikuwa Shamire.
25 Mmoja wa wazawa wa Ishia nduguye Mika alikuwa Zekaria.
26 Wana wa Merari: Mahli, Mushi na Yaazia;
27 wazawa wa Merari kwa mwanawe Yaazia: Shohamu, Zakuri na Ibri.
28 Wana wa Mahli: Eleazari ambaye hakupata mtoto,
29 Kishi ambaye alikuwa na mwana mmoja: Yerameeli.
30 Mushi alikuwa na wana watatu: Mahli, Ederi na Yeremothi. Wao ni wazawa wa Lawi kulingana na koo zao.
31 Pia hao wote walipiga kura kufuatana na ukoo wa kila mkuu na mdogo wake, kama wazawa wa Aroni walivyofanya. Walipiga kura mbele ya mfalme Daudi, Sadoki, Ahimeleki na viongozi wa jamaa za makuhani na za Walawi.
1 Mfalme Daudi na viongozi wa Walawi, waliwateua baadhi ya wana wa Asafu, wa Hemani, na wa Yeduthuni, kuongoza katika huduma ya kutabiri kwa kutumia vinubi, na vinanda na matoazi. Hii ndiyo orodha ya wale waliochaguliwa kuongoza ibada, pamoja na aina ya kazi iliyofanywa na kila kikundi.
2 Wana wanne wa Asafu: Zakuri, Yosefu, Nethania na Asharela. Wao walikuwa chini ya uongozi wa Asafu aliyetabiri wakati wote chini ya uongozi wa mfalme.
3 Wana sita wa Yeduthuni: Gedalia, Seri, Yeshaya, Shimei, Hashabia na Matithia. Wao walikuwa chini ya uongozi wa baba yao; na walitabiri kwa kutumia vinubi, na wakamshukuru na kumtukuza Mwenyezi-Mungu.
4 Wa Hemani: Bukia, Matania, Uzieli, Shebueli, Yeremothi, Hanania, Hanani, Eliatha, Gidalti, Romamti-ezeri, Yoshbekasha, Malothi, Hothiri na Mahaziothi.
5 Mungu alimpa Hemani, mwonaji wa mfalme, hawa watoto wa kiume kumi na wanne, na wa kike watatu, kama alivyoahidi ili kumtukuza.
6 Wanawe wote walipiga muziki kwa matoazi, vinanda na vinubi, kwenye ibada katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu wakiwa chini ya uongozi wa baba yao. Asafu, Yeduthuni na Hemani walikuwa chini ya amri ya mfalme.
7 Idadi yao pamoja na wale ndugu zao Walawi waliofundishwa kumwimbia Mwenyezi-Mungu, wote waliokuwa stadi, ilikuwa 288.
8 Wote, wakubwa kwa wadogo, waalimu kwa wanafunzi, walitumia kura katika kupanga kazi zao.
9 Kura ya 1 ilimwangukia Yosefu wa jamaa ya Asafu; ya 2 Gedalia pamoja na ndugu zake na wanawe kumi na wawili;
10 ya 3 Zakuri pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili;
11 ya 4 ilimwangukia Seri pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili;
12 ya 5 Nethania; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili;
13 ya 6 Bukia; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili;
14 ya 7 Asharela; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili;
15 ya 8 Yeshaya; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili;
16 ya 9 Matania; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili;
17 ya 10 Shimei; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili;
18 ya 11 Azareli; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili;
19 ya 12 Hashabia; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili;
20 ya 13 Shebueli; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili;
21 ya 14 Matithia; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili;
22 ya 15 Yeremothi; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili;
23 ya 16 Hanania; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili;
24 ya 17 Yoshbekasha; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili;
25 ya 18 Hanani; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili;
26 ya 19 Malothi; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili;
27 ya 20 Eliatha; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili;
28 ya 21 Hothiri; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili;
29 ya 22 Gidalti; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili,
30 ya 23 Mahaziothi; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili,
31 ya 24 ilimwangukia Romamti-ezeri; pamoja na wanawe na ndugu zake kumi na wawili.
1 Haya ndiyo makundi ya Walawi waliofanya kazi za ubawabu. Kutoka katika ukoo wa Kora, alikuwa Meshelemia mwana wa Kore wa jamaa ya Asafu.
2 Yeye alikuwa na wana saba: Zekaria mzaliwa wake wa kwanza, Yediaeli wa pili, Zebadia wa tatu, Yathnieli wa nne,
3 Elamu wa tano, Yohanani wa sita na Eliehoenai wa saba.
4 Pia kulikuwa na Obed-edomu, ambaye Mungu alimbariki kwa kumpa wana wanane: Shemaya mzaliwa wake wa kwanza, Yehozabadi wa pili, Yoa wa tatu, Sakari wa nne, Nethaneli wa tano,
5 Amieli wa sita, Isakari wa saba na Peulethai wa nane.
6 Naye mwanawe Shemaya alipata wana waliokuwa na mamlaka juu ya jamaa ya baba yao, kwa sababu walikuwa wanaume wenye uwezo mkubwa.
7 Shemaya, mzaliwa wa kwanza wa Obed-edomu, alikuwa na wana sita: Othni, Refaeli, Obedi, Elizabadi, nduguze walikuwa mashujaa, Elihu na Semakia.
8 Hao wote wana wa Obed-edomu; wao na wana wao na ndugu zao, walikuwa watu hodari wawezao huo utumishi. Wazawa wote wa Obed-edomu walikuwa sitini na wawili.
9 Naye Meshelemia alikuwa na wana na nduguze; watu wenye uwezo kumi na wanne.
10 Hosa mmojawapo wa wana wa Merari alikuwa na wana wanne: Shimri (aliyefanywa kiongozi na baba yake hata ingawa hakuwa mzaliwa wa kwanza),
11 Hilkia wa pili, Tebalia wa tatu na Zekaria wa nne. Wana wote wa Hosa pamoja na nduguze walikuwa kumi na watatu.
12 Mabawabu hao waligawanyika katika makundi kulingana na jamaa zao, nao pia walipangiwa kazi kwenye nyumba ya Mwenyezi-Mungu kama wale Walawi wengine.
13 Kila jamaa, bila kujali wingi, ilipiga kura kuchagua lango watakalosimamia.
14 Kura ya kuchagua wa kulinda lango la mashariki ilimwangukia Shelemia. Walipiga kura pia kwa ajili ya mwanawe Zekaria, aliyekuwa mshauri mwenye busara, ikamwangukia kura ya lango la kaskazini.
15 Obed-edomu aliangukiwa na kura ya lango la kusini, na ya wanawe, ghala.
16 Shupimu na Hosa waliangukiwa na kura ya kulinda lango la magharibi kwenye lango la Shalekethi kwenye barabara ya juu. Ulinzi ulifanywa kwa zamu.
17 Kila siku upande wa mashariki kulikuwa na mabawabu sita, kaskazini wanne, na kusini wanne, pia kwenye ghala kuliwekwa mabawabu wawiliwawili.
18 Kwenye banda zuri lililokuwa upande wa magharibi, kulikuwa na mabawabu wanne barabarani, na wawili kwenye banda lenyewe.
19 Haya ndiyo makundi ya mabawabu miongoni mwa ukoo wa Kora na wazawa wa Merari waliofanya kazi ya ubawabu.
20 Miongoni mwa Walawi, Ahiya alihusika na uangalizi wa hazina ya nyumba ya Mungu, na hazina ya vitu vilivyowekwa wakfu.
21 Ladani, mmoja wa ukoo wa Gershoni, alikuwa babu wa baadhi ya jamaa, miongoni mwao ikiwamo jamaa ya mwanawe Yehieli.
22 Wana wengine wawili wa Ladani, Zethamu na Yoeli, walikuwa watunzaji wa hazina ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu.
23 Pia kazi ziligawanywa kwa watu wa koo za Wasiria, Waishari, Wahebroni na Wauzieli.
24 Shebueli, mwana wa Gershoni, mwana wa Mose, alikuwa ofisa mkuu wa hazina hizo.
25 Na ndugu yake, alikuwa Eliezeri, aliyekuwa baba yake Rehabia, aliyemzaa Yeshaya, aliyemzaa Yoramu, aliyemzaa Zikri, aliyemzaa Shelomithi.
26 Shelomithi na ndugu zake, ndio waliokuwa waangalizi wa hazina zote za vitu vilivyowekwa wakfu na mfalme Daudi, na viongozi wa jamaa, maofisa wa maelfu na mamia na majemadari wa jeshi.
27 Waliweka wakfu sehemu ya nyara walizoteka vitani kwa ajili ya matengenezo ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu.
28 Pia, vitu vyote vilivyowekwa wakfu na Samueli, mwonaji, na Shauli mwana wa Kishi, na Abneri, na Yoabu mwana wa Seruya, vilikuwa chini ya uangalizi wa Shelomithi na nduguze.
29 Miongoni mwa Waishari, Kenania na wanawe walipewa kazi za utawala kama maofisa na waamuzi, kwa ajili ya Waisraeli.
30 Miongoni mwa Wahebroni, Hashabia na nduguze 1,700, wote watu mashujaa walipewa wajibu wa kusimamia sehemu za Israeli zilizokuwa upande wa magharibi wa mto Yordani. Walisimamia kazi yote ya Mwenyezi-Mungu na kazi za mfalme Daudi.
31 Miongoni mwa Wahebroni, Yeria alikuwa kiongozi wa koo na jamaa zote, na katika mwaka wa arubaini wa utawala wa mfalme Daudi, uchunguzi ulifanywa, na wanaume wenye uwezo mkubwa walipatikana huko Yezeri katika Gileadi.
32 Mfalme Daudi alimteua Yeriya na ndugu zake 2,700, mashujaa na viongozi wa koo, kusimamia mambo yote yaliyohusu Mungu na mfalme Daudi katika sehemu za Wareubeni, Wagadi na nusu ya kabila la Manase, zilizokuwa mashariki ya mto Yordani.
1 Hii ndiyo orodha ya wakuu wa wazawa wa Israeli waliokuwa viongozi wa jamaa, na makamanda wa maelfu na mamia na maofisa wao waliomtumikia mfalme Daudi kuhusu zamu za kuingia na kutoka. Kila mwezi kila mwaka, kundi tofauti la watu 24,000 walilishika zamu ya kufanya kazi.
2 Yashobeamu mwana wa Zabdieli alikuwa kiongozi wa kikosi cha kwanza mnamo mwezi wa kwanza; kikosi chake kilikuwa na watu 24,000.
3 Yeye alikuwa mzawa wa Peresi, naye akawa mkuu wa makamanda wote wa jeshi katika mwezi wa kwanza.
4 Dodai alikuwa kiongozi wa kundi la pili katika mwezi wa pili. Kikosi chake kikiwa na wanajeshi 24,000.
5 Kamanda wa kundi la tatu likiwa na wanajeshi 24,000 alikuwa Benaya mwana wa Yehoyada, aliyekuwa kuhani mkuu.
6 Huyu ndiye Benaya aliyekuwa mtu shujaa katika kundi la watu 30, na kiongozi wa kundi hilo. Naye Amizabadi mwanawe, alikuwa kamanda.
7 Asaheli, nduguye Yoabu, alikuwa wa nne akiongoza kundi la nne lenye wanajeshi 24,000, na baada yake alimfuata Zebadia mwanawe.
8 Mwezi wa tano: Shamhuthi, Mwizrahi; alikuwa na kundi la wanajeshi 24,000.
9 Mwezi wa sita: Ira, mwana wa Ikeshi, Mtekoa; alikuwa na kundi la wanajeshi 24,000.
10 Mwezi wa saba: Helesi, Mpeloni, wa wana wa Efraimu; alikuwa na kundi la wanajeshi 24,000.
11 Mwezi wa nane: Sibekai, Mhushathi, wa Wazera; alikuwa na kundi la wanajeshi 24,000.
12 Mwezi wa tisa: Abiezeri Mwanathothi, wa Wabenyamini; naye alikuwa na kundi la wanajeshi 24,000.
13 Mwezi wa kumi: Maharai, Mnetofathi wa Wazera; naye alikuwa na kundi la wanajeshi 24,000.
14 Mwezi wa kumi na moja: Benaya, Mpirathoni; wa wana wa Efraimu, naye alikuwa na kundi la wanajeshi 24,000.
15 Mwezi wa kumi na mbili: Heldai, Mnetofathi, wa Othnieli; pia naye alikuwa na kundi la wanajeshi 24,000.
16 Hii ndiyo orodha ya wakuu wa makabila ya Israeli: Wa Wareubeni, Eliezeri mwana wa Zikri; Eliezeri ndiye aliyekuwa ofisa mkuu; wa Wasimeoni, Shefatia mwana wa Maaka;
17 wa Lawi, Hashabia mwana wa Kemueli; wa Aroni, Sadoki;
18 wa Yuda, Elihu, mmoja wa ndugu za mfalme Daudi; wa Isakari, Omri mwana wa Mikaeli;
19 wa Zebuluni, Ishmaya mwana wa Obadia; wa Naftali, Yeremothi mwana wa Azrieli;
20 wa wana wa Efraimu, Hoshea mwana wa Azazia; wa nusu ya kabila la Manase, Yoeli mwana wa Pedaya;
21 wa nusu ya kabila la Manase katika Gileadi, Ido mwana wa Zekaria; na wa Benyamini, Yaasieli mwana wa Abneri;
22 wa Dani, Azareli mwana wa Yerohamu. Hao ndio wakuu wa makabila ya Israeli.
23 Mfalme Daudi hakuwahesabu wale waliokuwa chini ya umri wa miaka ishirini kwa maana Mwenyezi-Mungu aliahidi kuwaongeza Waisraeli wawe wengi kama nyota za mbinguni.
24 Yoabu mwana wa Seruya alianza kuwahesabu lakini hakumaliza; tena ghadhabu iliwapata Waisraeli kwa ajili ya tendo hili, nayo hesabu hiyo haikuingizwa katika kumbukumbu za mfalme Daudi.
25 Aliyesimamia hazina za mfalme Daudi alikuwa Azmawethi mwana wa Adieli. Yonathani mwana wa Uzia alisimamia hazina zilizokuwa mashambani, mijini, vijijini na ngomeni.
26 Aliyewasimamia wakulima alikuwa Ezri mwana wa Kelubu.
27 Aliyesimamia kazi ya mashamba ya mizabibu alikuwa Shimei, Mramathi. Aliyesimamia uzalishaji wa divai alikuwa Zabdi, Mshifmi.
28 Aliyesimamia mizabibu na mikuyu ya Shefela alikuwa Baal-hanani, Mgederi. Aliyesimamia ghala za mafuta alikuwa Yoashi.
29 Aliyesimamia mifugo iliyokuwa Sharoni alikuwa Shitrai, Msharoni; aliyesimamia mifugo iliyokuwa mabondeni alikuwa Shafati mwana wa Adlai.
30 Aliyesimamia ngamia alikuwa Obili Mwishmaeli. Aliyesimamia punda alikuwa Yedeya, Mmeronothi. Aliyesimamia makundi ya kondoo alikuwa Yazizi, Mhagri.
31 Hao wote walikuwa watunzaji wa mali ya mfalme Daudi.
32 Yonathani, mjomba wa mfalme Daudi, alikuwa mshauri na mtu mwenye ufahamu na mwandishi. Yeye na Yehieli mwana wa Hakmoni waliwafunza wana wa mfalme.
33 Ahithofeli, alikuwa mshauri wake mfalme; Hushai Mwarki, alikuwa rafiki yake mfalme.
34 Ahithofeli alipofariki, mahali pake palichukuliwa na Yehoyada mwana wa Benaya na Abiathari. Yoabu alikuwa kamanda wa jeshi la mfalme.
1 Mfalme Daudi akawakusanya huko Yerusalemu wakuu wote wa Israeli: Wa makabila, majemadari na vikosi waliomtumikia mfalme, makamanda wa maelfu, makamanda wa mamia, wasimamizi wa mali zote na ng'ombe wote wa mfalme, na wanawe pamoja na maofisa wa ikulu, mashujaa na askari wote mashuhuri.
2 Ndipo mfalme Daudi akasimama akasemana kusema: “Enyi ndugu zangu na watu wangu, nisikilizeni. Nilikusudia moyoni mwangu kujenga nyumba kwa ajili ya sanduku la agano la Mwenyezi-Mungu, kiti cha kuwekea miguu yake Mungu wetu; na nilifanya maandalizi ya kujenga.
3 Lakini Mungu alinikataza, kwa sababu mimi ni mtu wa vita na nimekwisha mwaga damu nyingi.
4 Lakini Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli alinichagua mimi miongoni mwa jamaa ya baba yangu kuwa mfalme wa Israeli milele. Alilichagua kabila la Yuda liongoze; na kutokana na kabila hilo, aliichagua jamaa ya baba yangu, na miongoni mwa wana wa baba yangu, alipendezwa nami na kuniweka niwe mfalme wa Israeli yote.
5 Mwenyezi-Mungu amenijalia wana wengi, na miongoni mwa hao wote, amemchagua Solomoni mwanangu, aketi juu ya kiti cha enzi cha ufalme wake Mwenyezi-Mungu aitawale Israeli.
6 “Mwenyezi-Mungu aliniambia, ‘Mwanao Solomoni ndiye atakayenijengea nyumba na nyua zangu, kwa maana nimemchagua yeye awe mwanangu, nami nitakuwa baba yake.’
7 Nitauimarisha ufalme wake milele ikiwa ataendelea kuzishika kwa dhati amri na sheria zangu kama anavyofanya leo.
8 “Basi sasa, mbele ya kusanyiko hili la Waisraeli wote, jumuiya ya watu wa Mwenyezi-Mungu, na mbele ya Mungu wetu, angalieni mzishike amri zote za Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, ili mwendelee kuimiliki nchi hii nzuri, na kuwarithisha wazawa wenu baada yenu, hata milele.
9 “Nawe Solomoni mwanangu, umjue Mungu wa baba yako, na umtumikie kwa moyo wako wote na kwa nia thabiti; yeye Mwenyezi-Mungu huchunguza mioyo na anafahamu mipango na fikira za binadamu. Ukimtafuta yeye, utamwona; lakini ukimwacha, atakutupilia mbali milele.
10 Basi, ujihadhari na kukumbuka ya kwamba, Mwenyezi-Mungu amekuchagua wewe umjengee nyumba ya ibada. Uwe hodari ukatende hivyo.”
11 Ndipo Daudi akampa Solomoni mwanawe ramani ya majengo yote ya hekalu, nyumba zake, hazina zake, ghorofa zake, vyumba vyake vya ndani na mahali pa kiti cha rehema.
12 Alimpa ramani ya yote aliyokusudia moyoni kuhusu nyua za nyumba ya Mwenyezi-Mungu, vyumba vya Mungu na ghala za kuwekea vitu vilivyo wakfu.
13 Alimpa pia mfano wa jinsi ya kuwapanga makuhani na Walawi kuzitekeleza huduma zao, kutumikia nyumba ya Mwenyezi-Mungu na kuvitunza vyombo vyote vya Nyumba ya Mwenyezi-Mungu.
14 Alimpa kiasi cha dhahabu iliyohitajika kutengenezea vyombo vyote vya dhahabu vya utumishi wa kila namna, kiasi cha fedha iliyohitajika kwa utumishi wa kila namna,
15 uzani wa vinara vya dhahabu na taa zake, uzani wa dhahabu ya kila kinara na taa zake uzani wa fedha ya kutengenezea kinara na taa zake kulingana na matumizi ya kila kinara;
16 na kiasi cha dhahabu ya kutengenezea meza za dhahabu zilizowekewa mikate iliyotolewa kwa Mungu, hata kiasi cha fedha ya kutengenezea meza za fedha;
17 pia alitoa maagizo kuhusu kiasi cha dhahabu safi iliyohitajika kutengenezea nyuma, mabirika na vikombe, pia kiasi cha dhahabu na fedha iliyohitajika kutengenezea mabakuli ya dhahabu na ya fedha,
18 na kiasi cha dhahabu safi ya kutengenezea madhabahu ya kufukizia ubani. Alimpa pia mfano wake wa gari la dhahabu la viumbe wenye mabawa waliyotandaza mabawa na kulifunika sanduku la agano la Mwenyezi-Mungu.
19 Hayo yote, mfalme Daudi aliyaweka wazi kwa maandishi aliyopewa na Mwenyezi-Mungu. Kazi yote itendeke kulingana na ramani hiyo.
20 Kisha, mfalme Daudi akamwambia Solomoni mwanawe, “Uwe imara na hodari, uifanye kazi hii. Usiogope wala kuwa na wasiwasi. Mungu, Mwenyezi-Mungu ambaye ni Mungu wangu, yu pamoja nawe. Hatakuacha bali atakuwa nawe hata itakapomalizika kazi yote inayohitajika kufanyiwa nyumba ya Mwenyezi-Mungu.
21 Makuhani na Walawi wamekwisha pangiwa kazi watakazofanya katika nyumba ya Mungu. Wafanyakazi wenye ujuzi wa kila aina watakuwa tayari kabisa kukusaidia, na watu wote pamoja na viongozi wao watakuwa chini ya amri yako.”
1 Mfalme Daudi akaumbia ule mkutano wote uliojumuika, “Solomoni, mwanangu, ambaye peke yake amechaguliwa na Mungu, bado yungali mdogo, na hana uzoefu mwingi, na kazi hii ni kubwa. Nyumba atakayoijenga si ya mwanadamu, bali ni ya Mungu, Mwenyezi-Mungu.
2 Basi, nimejitahidi kwa kadiri ya uwezo wangu wote kuiwekea nyumba ya Mungu wangu, akiba ya dhahabu ya kutengenezea vitu vya dhahabu, fedha ya kutengenezea vitu vya fedha, shaba ya kutengenezea vitu vya shaba, chuma cha kutengenezea vitu vya chuma, na miti ya kutengenezea vitu vya miti. Zaidi ya hayo, nimevitayarisha kwa wingi vito vya rangi na mawe ya kujazia vito vya njumu, mawe ya rangi, mawe ya thamani ya kila namna na marumaru.
3 Tena, zaidi ya vyote nilivyotoa kwa ajili ya nyumba takatifu, ninayo hazina yangu binafsi ya dhahabu na fedha, na kwa sababu naipenda nyumba ya Mungu wangu, naitoa kwa ajili ya nyumba ya Mungu wangu:
4 Tani 3,000 za dhahabu kutoka Ofiri, talanta 700 za fedha safi ya kuzifunikia kuta za nyumba,
5 na kwa ajili ya kutengenezea vitu vya kila aina vitakavyotengenezwa na mafundi kwa mikono. Nimeweka dhahabu kwa ajili ya vyombo vya dhahabu, na fedha kwa ajili ya vyombo vya fedha. Ni nani basi atakayemtolea Mwenyezi-Mungu kwa hiari ili ajiweke wakfu hivi leo kwa Mwenyezi-Mungu?”
6 Ndipo wakuu wa koo, viongozi wa makabila ya Israeli, makamanda wa maelfu na wa mamia; pia na maofisa wasimamizi wa kazi za mfalme walipotoa kwa hiari yao.
7 Walitoa kwa ajili ya huduma za nyumba ya Mungu: Tani 170 za dhahabu, tani 340 za fedha, tani 620 za shaba na tani 3,400 za chuma.
8 Wale ambao walikuwa na vito vya thamani walivitoa vitiwe katika hazina ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu, chini ya uangalizi wa Yehieli, Mgershoni.
9 Ndipo watu wakafurahi kwa sababu walitoa kwa hiari, maana kwa moyo wao wote walimtolea Mwenyezi-Mungu kwa hiari, naye mfalme Daudi alifurahi sana.
10 Ndipo Daudi akamtukuza Mwenyezi-Mungu mbele ya mkutano wote, akisema: “Utukuzwe milele na milele, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wa baba yetu Israeli.
11 Ukuu ni wako, ee Mwenyezi-Mungu, una nguvu, utukufu, ushindi na enzi. Vyote vilivyoko mbinguni na duniani ni vyako. Ee Mwenyezi-Mungu, ufalme ni wako, nawe umetukuzwa, u mkuu juu ya vitu vyote.
12 Utajiri na heshima hutoka kwako, vyote wavitawala. Uwezo na nguvu vimo mkononi mwako, nawe wawakuza uwapendao, na huwaimarisha wote.
13 Sasa ee Mungu wetu, tunakushukuru na kulisifu jina lako tukufu.
14 “Lakini, mimi ni nani, na watu wangu ni nani, hata tuweze kukupa kitu? Kwa maana vitu vyote vyatoka kwako, tumekutolea vilivyo vyako wewe mwenyewe.
15 Sisi tu wageni mbele yako, na wasafiri kama walivyokuwa babu zetu wote. Siku zetu duniani ni kama kivuli kipitacho, hapa hakuna tumaini la kukaa.
16 Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, wingi wote huu tuliotoa ili kukujengea nyumba kwa ajili ya utukufu wa jina lako takatifu, watoka mkononi mwako na yote ni yako.
17 Ninajua Mungu wangu, kwamba wewe waujaribu moyo, nawe unapendezwa na unyofu. Nami, katika unyofu wa moyo wangu nimetoa vitu hivi vyote kwa hiari yangu, na sasa ninaona watu wako walioko hapa, wakikutolea kwa hiari na furaha.
18 Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Abrahamu, Isaka na Israeli, babu zetu, dumisha maazimio ya namna hiyo na fikira za namna hiyo mioyoni mwa watu wako, na ielekeze mioyo ya watu wako kwako.
19 Mjalie Solomoni mwanangu ili kwa moyo wote ashike amri zako, maamuzi na maagizo yako, atekeleze yote ili aweze kuijenga nyumba hii ya enzi niliyoifanyia matayarisho.”
20 Kisha, mfalme Daudi aliwaambia wote waliokusanyika, “Msifuni Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.” Na wote waliokusanyika wakamtukuza Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zao, wakamsujudia na kumwabudu Mwenyezi-Mungu na kumtolea mfalme Daudi heshima.
21 Wakamtolea tambiko Mwenyezi-Mungu. Siku ya pili yake wakamtolea sadaka za kuteketezwa: Mafahali 1,000, wanakondoo 1,000, pamoja na sadaka zao za vinywaji na tambiko nyingi kwa ajili ya Waisraeli wote.
22 Basi siku hiyo walikula na kunywa kwa furaha kuu mbele ya Mwenyezi-Mungu. Wakamtawaza Solomoni mwana wa Daudi, mara ya pili. Wakampaka mafuta awe mtawala kwa jina la Mwenyezi-Mungu, na Sadoki awe kuhani.
23 Ndipo Solomoni akaketi katika kiti cha enzi cha Mwenyezi-Mungu, badala ya Daudi baba yake. Naye akafanikiwa, na taifa lote la Israeli likamtii.
24 Viongozi wote, mashujaa na wana wote wa Daudi wakajiweka chini ya mfalme Solomoni.
25 Mwenyezi-Mungu akampa Solomoni sifa nzuri machoni pa Waisraeli wote, akampa fahari ya kifalme ipitayo fahari ya mfalme awaye yote aliyeitawala Israeli kabla yake.
26 Basi Daudi, mwana wa Yese, akawa mfalme juu ya Israeli yote.
27 Na muda aliotawala juu ya Israeli ulikuwa miaka arubaini; miaka saba alitawala huko Hebroni na miaka thelathini na mitatu alitawala huko Yerusalemu.
28 Alikufa akiwa mzee mwenye miaka mingi, ameshiba siku, akiwa na mali na heshima. Solomoni mwanawe, akawa mfalme badala yake.
29 Habari za mfalme Daudi toka mwanzo hadi mwisho, zimeandikwa katika kumbukumbu za Samueli mwonaji, katika kumbukumbu za nabii Nathani na katika kumbukumbu za Gadi mwonaji.
30 Hizo zasema pamoja na mambo ya utawala wake, uwezo wake, na mambo yaliyompata yeye, Waisraeli, na falme zote nchini.